Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Fakharia Shomar Khamis (33 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Sina budi kuishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka amani na utulivu kwa muda wa miaka 52 hivi sasa Tanzania ipo katika utulivu. Lazima nitoe shukrani kwa Serikali zote mbili kuweza kukaa kwa utulivu na amani na Muungano utaendelea kudumu tena wa Serikali mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi kutoa shukrani za pekee kwa Jemadari Mkuu wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuweza kuweka amani na utulivu kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na tukaweza kurejea uchaguzi kwa amani na utulivu na Wazanzibari chaguo lao likawa CCM wakamchagua Mheshimiwa Ali Mohamed Shein kuwa Rais wa Zanzibar.
Nawaambia Wazanzibari hongereni kwa uchaguzi wenu, haya maneno ya kutupatupa yasiwashtue humu ndani ya Bunge, dua la kuku halimpati mwewe, sasa wanaokaa wakaapiza, wakasema hovyo, wakajilabu hovyo ni sawa na kujishusha tu, lakini hakuna kitakachokuwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwaka 2000 wakati wa Mheshimiwa Salmini walikuwa wanawadanganya wenzi wao hawa uchaguzi utarejewa! Uchaguzi utarejewa! Iko wapi? Tukawaambia hapa Katiba inasema mpaka mwaka 2005, hayakuwa, yamekuwa mwaka 2005! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kazi kuwatia wenzenu drip mkawachoma asubuhi na jioni, wameshachoka kudanganywa! Anasimama mtu anajinasibu eti tutapeleka Mahakamani, hamkwenda Mahakamani hapo mwanzo Mheshimiwa Shein hajakamata nchi, leo mtakwenda Mahakamani nchi imeshakamatwa, siyo mnajidanganya tu? Huko ni kujidanganya, msidanganye wenzenu uchaguzi hapa mpaka mwaka 2020 kama ulivyokuwa nyuma 2000 mpaka 2005 na hii ni mwaka 2015 mpaka na mwaka 2020. Hayo mnayozungumza kama mtakwenda Mahakamani mtakwenda wapi, hiyo danganya toto, ukweli ndiyo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia masuala ya Muungano lakini lazima hawa wenzangu watani wangu niwaambie ukweli waulewe, wasidanganye wenzi wao! Uchaguzi mwaka 2015, msijisumbue tutakwenda Mahakamani! Mwaka huu mtakiona! Kitakuwa nini! Tukione nini na kuna Katiba! Kuna Katiba inazungumza na Jemadari Mkuu namshukuru, Zanzibar imetulia, ndiyo maana mnatuona tuko hapa tunapendeza! Walioweka makoti, walioweka vitenge tumekaa hapa, hakuna anayekwambia anataka kuondoka, miezi mitatu mtatuona humu tunamangamanga na shughuli zetu za Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 51, Kifungu cha 92, Gawio. Nakubaliana na maelezo yote aliyosema Mheshimiwa Waziri, sina matatizo nayo na ile aliyosema 9.9 billion ya gawio sina matatizo nayo, lakini nina ushauri kwamba 4.5 imekaa muda mrefu naona wangekaa tena Serikali hizi mbili wakakokotoa kwamba, hii 4.5 itakwenda mpaka lini? Au ndiyo makubaliano ya Serikali mbili, au ndiyo maamuzi? Naomba hili waliangalie kisha watutolee uamuzi, maana hakuna mtu anayekataa nyongeza na nyongeza huwa inakwenda kwenye fungu! Sasa na hili kama mtalikokotoa mkaliangalia na mkaona hakuna uwezekano wa kutuongezea itakuwa maa-salam, Muungano unazidi kudumu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira ya Muungano, ajira ya Muungano kwa maelezo yaliyoelezwa nayakubali sina matatizo. Mgawanyo wa ajira ulivyo sina matatizo, lakini tatizo langu kwa nini Zanzibar hamuweki ofisi ikawa inashughulikia ajira za Muungano? Kama tatizo lilikuwa ni jengo au ofisi, Ofisi ya Makamu wa Rais Zanzibar ni kubwa na ofisi zipo! Mlituahidi mwaka jana kwamba mtachukua ofisi pale! Je, nini tatizo? Kumetokea nini? Au kuna jambo gani hata hadi leo jengo lipo, ofisi haijafunguliwa pale Zanzibar? Mnawafanya akina kaka na akina dada asubuhi kaenda Bara, jioni karudi kufanya interview na siku nyingine asifanikiwe na hela yake imekwenda! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni jengo la Ofisi ya Makamu wa Rais, Zanzibar. Jengo ni zuri lakini linahitaji ukarabati. Ukarabati tulikubaliana mwaka jana, Kamati ya Katiba na Sheria ilivyokwenda iliuona uozo uliokuwepo pale mkasema kwamba, tayari mtalitengeneza. Nimefuatilia halijatengenezwa, mlikwenda mkaligusagusa, lakini mmeliacha liko vile vile na usipoziba ufa utajenga ukuta! Sasa ningewaomba hii kazi na tunataka Makamu wetu wa Rais akae mahali pazuri penye usalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile pale tulikubaliana kwamba sehemu ya nyuma ambapo kuna jengo refu, tukasema Serikali mbili zikae zizungumze ili lile jengo lipate kuondoka au lichukuliwe au mtakavyoamua, lakini tusimpe tabu yule mwenye jengo.
Kutokana na jengo kuweko pale refu, usalama wa Ofisi ya Makamu, usalama wa nyumba anayokaa Makamu haupo, kwa sababu jengo refu, yule akikaa juu anaona wote mle ndani! Sasa usalama uko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hamjatuambia kwenye hiki kitabu mmefikia hatua gani? Kama kweli hii kazi mliifanya na vikao vilikaa, lazima mngeleta mrejesho! Ningeomba na hili kujua kipi kinachoendelea? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na njia ya dharura ambayo kuna njia main road ya kuingilia ambayo ndiyo mnayotokea, lakini tukasema nyuma kuna geti lingine, kujengwe barabara ya dharura ambayo anaweza Mheshimiwa Makamu akaitumia. Tulikubaliana mkasema itakuweko njia ya dharura kwa usalama wa Mheshimiwa Makamu! Hiyo njia hadi leo haijajengwa na sitegemei kama mtaijenga kwa sababu hata kwenye hiki kitabu hamjaelezea! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia nizungumzie vitu ambavyo vitaweza kudumisha Muungano. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliahirisha sherehe za Muungano siyo kwamba kaziahirisha, aliboresha maendeleo akasema zile fedha zipelekwe Mwanza kwa ajili ya maendeleo, sasa kwa ajili zile fedha zilikuwa ni za Muungano na Muungano ni wa nchi mbili, hili gawio ilibidi tulipate na sisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai. Tunataka kumtua mama ndoo kichwani. Naomba tozo ya mafuta ile ya sh.50/= bado ni ndogo na inahitajika kuongezwa ili tuweze kuingiza katika mfuko na maji tumsaidie kumtua mama ndoo kichwani. Ombi langu ni kwamba asilimia 70 iende vijijini na 30 iende mijini ili kumtua mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. FAKHARIA S. KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa na imetoa mwelekeo kwa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nasema mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Nimezungumza kwa kusema fumbo hilo; tunalizungumzia Jeshi. Jeshi wajibu wake ni kwenda Zanzibar na kuwepo Bara. Sasa kupelekwa Jeshi Zanzibar imekuwa hoja kubwa hapa ndani, kwa nini Jeshi limekwenda Zanzibar?
Mheshimiwa Waziri ukurasa wake wa 20 alizungumza hivi, nanukuu: “Kukamatwa kwa mabomu ya kutengenezwa kwa mkono katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar.” Sasa kwanini majeshi yasiende? Atakayeyategua mabomu haya ni nani kama siyo Jeshi? Sasa haya mabomu kayatengeneza nani? Wakasema ni wananchi wa Zanzibar. Sasa ikiwa ni kweli jambo hilo limefanyika Zanzibar, wa kufanya shughuli hiyo ni majeshi; wa kuangalia ulinzi huo ni majeshi na mabomu yamelipuliwa Zanzibar. Tatizo liko wapi? Anayetaka kusema na aseme tu ili afurahishe roho yake na maamuzi yake, lakini ukweli ndiyo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia kuhusu mgao wa nafasi za ajira Zanzibar. Nakubali wanajeshi wanaajiriwa Zanzibar, lakini utaratibu unaotumiwa Mheshimiwa Waziri angalieni. Mnapeleka nafasi katika Mikoa, watu wanatafutwa katika mikoa, wanaajiriwa. Kwa nini msiende JKU kama mnavyokwenda JKT? Kwanza kule mtapata vijana tayari wameshapata elimu ya jeshi, wakakamavu, wameshajua nini wanakwenda kutenda; lakini kuchukua Mkoani, hamumjui mtu yupo vipi, lakini kwa sababu vipi aajiriwe! Nafikiri hilo mliangalie tena na mlipange tena. Bora vijana wetu wakimaliza, waende JKU wapate elimu ya ukakamavu na inakuwa rahisi kwenu kujua wapo vipi, afya yake ni vipi na uwezo wake uko vipi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuja katika ukarabati wa ujenzi wa majengo ya jeshi Zanzibar. Kambi za Zanzibar zipo kwenye hali mbaya. Ukiangalia Mtoni, Mwanyanya, Mazizini na nyingine zote hazipo kwenye hali nzuri na sielewi toka zilipojengwa lini zimekarabatiwa. Nimeona katika kitabu chako ukurasa wa 37 umeelezea kwamba kuna nyumba kama 4,744; siyo mbaya hiyo kazi mtakayoifanya; na mmesema tayari kwa Pemba. Kama zipo nyumba 320 siyo mbaya; lakini kwa Unguja hali ndiyo mbaya. Kwa Unguja majeshi yetu pale ndiyo Zanzibar City. Sasa tunataka kama mlivyojenga nyumba 320 na Zanzibar tujue nyumba zetu mtazijenga lini? (Makofi)
Mheshimiwa Waziri, malipo ya wanajeshi wastaafu yanakuwa yana matatizo; matatizo yake ni nini? Inabidi lazima mwanajeshi aende Bara kutoka Zanzibar kufuatilia. Kwani Zanzibar hamwezi kuweka kituo kukawa na kituo kama Bara? Mwanajeshi kastaafu Zanzibar, anakwenda pale anahudumiwa, anapata malipo yake Zanzibar baada ya kuondoka. Maana akifika Bara kwanza humjui mtu, wala humwelewi mtu, hujui unaanzia wapi! Wakati mwingine huyo mwanajeshi hajapata nafasi hata ya kwenda huko. Mwenyewe yupo Zanzibar tu! Sasa mnampeleka Bara akafuate kiinua mgongo, akahangaike! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, asaidie Wizara kama inaweza kujigawa na Zanzibar wakawepo wafanyakazi na wakaweza kufanya kazi hiyo vizuri na kwa wepesi bila matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni kuhusu uvamizi wa ujenzi wa nyumba karibu na kambi za Zanzibar. Kambi za Zanzibar zimevamiwa, zipo katikati ya mji. Kambi hizo kwa kweli ukiangalia Mtoni, Mazizini, Mwanyanya na nyingine kadhalika, pale linalofanywa ndani ya kambi wananchi wa pale wanajua, kinachotokea wananchi wa pale wanajua na inatakiwa ndani ya kambi kuwe kuna siri. Huwezi kuyajua mambo ya kambini.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine inawezekana ikatokea madhara itakuwa rahisi kwa wale wananchi kupigwa. Itabidi wananchi wanaokaa karibu na kambi wapate elimu wajue jinsi ya kujihami, maana ukishakaa kambini na wewe ni sawa sawa na mwanajeshi, litakalotokea na wewe umo. Sasa mngechukua wakati wenu mkatoa elimu kwa watu waliokuwepo pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika uchaguzi wake 2010-2015 ilisema ujenzi wa zahanati katika vijiji na kata ili kuokoa vifo vya akina mama. Sera ya afya ni ya Wizara ingawa mtekelezaji ni TAMISEMI, lakini wananchi wanaitazama Wizara ndiyo inaona haitekelezi ili kumuokoa mama na watoto katika vifo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majengo ya zahanati hizo yapo katika vijiji na kata lakini yapo magofu bila ya Serikali kuyamaliza. Je, Serikali hilo mmeliona maana tulitegemea mwaka 2015 -2020 yawe tayari yanafanyakazi ili kuokoa maisha ya mama na mtoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi ya Saratani inashindwa kufanya kazi zake kwani kipimo cha upimaji wa saratani ya matiti kimeharibika toka mwaka 2008 na akina mama wanapata taabu, inabidi kwenda vituo vya nje kwa matibabu. Hivi sasa Tanzania imekumbwa na kansa mbalimbali; kuna saratani ya matiti, ya shingo ya kizazi kwa wanawake. Pia kuna saratani ya tezi dume kwa wanaume limekuwa tatizo kwa Watanzania.

Mheshimiwa Waziri ninaomba utoe elimu ya kinga badala ya tiba na pia elimu ya kutumia chakula gani ili kujinusuru na saratani, elimu ndiyo itamsaidia Mtanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iendelee kuhamasisha kufanya mazoezi Watanzania kwani Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan anahimiza mazoezi kwa kila Mkoa katika wiki ya mwisho ya mwezi kwa siku ya Jumamosi, maana mazoezi ni afya. Ingawa Mheshimiwa Waziri Ummy anajitahidi kuhamasisha Watanzania lakini binadamu ni mzito. Hata sisi baadhi yetu Wabunge endeleeni kutuhamasisha kwa kufanya mazoezi kwa baadhi yetu tayari tunasumbuliwa na pressure pamoja na sukari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la watoto njiti. Nursing ya watoto njiti ni mtihani kwani hakuna uangalifu na watoto wanafariki kwa kukosa matunzo. Vifo vya akina mama, vifo vya watoto hivi sasa kati ya akina mama 100,000 basi kuna akina mama 430 hadi 556 hufa kwa uzazi kwa kukosa huduma. Ninajua Waziri wa Afya ni mwanamke na ninajua atachukua hatua za haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kukosa theatre kwa ajili ya akina mama kujifungulia kwani mama anatakiwa kuwa karibu na sehemu ya kujifungulia. Ingawa Wizara yako ilitakiwa kutekeleza; je, suala hilo limefikia wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwanza sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, na viongozi wote wa Wizara hii, kwanza kwa hotuba nzuri waliotusomea imeifunika hotuba ya Kambi ya Upinzani, ndio maana mkawaona wamekuja na jazba kubwa mpaka mwisho mtu anakunywa maji, ili kutafuta sauti akwamue, aifunike speech ya Mheshimiwa Waziri, lakini ameshindwa na vilevile nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi ya Upinzani wamezungumza kwamba Mheshimiwa Rais anajifungia Ikulu, anashindwa kutoka nje. Nawaambia Mheshimiwa Dkt. Magufuli ndiye Rais bora duniani na ambaye ameweza kutekeleza sera zake, kwa Watanzania na hivi sasa ana sifika Tanzania nzima na nje ya nchi kwa sababu ya uwezo wake, na hapo anapokuwepo Ikulu si kwamba anakaa anafanya kazi, anatafakari nini cha kuwafanyia Watanzania kuwaondoshea madhila, lakini mimi ninajua wenzetu ninyi kazi yenu ni kupinga tu kila kilichokuwa kizuri kazi yenu ninyi kupinga, kila kinachotendeka kikiwa kimekaa sawa imekuwa sawasawa na mke mwenza, amelisifia kaburi la mke mwenzie, hili kaburi la nani zuri limependeza, alipambwa na mke mwenzie, ndio maana nikaona limekaa upande, ndio upinzani huo, wakati ameshalisifia anakuja analiponda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mabalozi. Mabalozi wetu wanafanya kazi nzuri, hata wao wanapokwenda nchi za nje, wanahemea kwa Mabalozi. Sasa leo imekuwaje maana yake baniani mbaya kiatu chake dawa, jamani hebu tuwe makini katika masuala yetu tunapozungumza. Maana yake wakati mwingine mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni, tusiwe kwa sababu kuna upinzani, ndio upinge kila kitu mengine mshukuru kwa sababu yanawafaeni na ninyi wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na suala lingine, kuna siku alisimama Mbunge akazungumza kwamba Zanzibar utalii wao kama hauna uendelezo wala hauna faida nao upo upo tu. Namwambia huyo Mheshimiwa kwamba Zanzibar hivi sasa bajeti yake anatumia pesa za ndani, hategemei za nje na kinachofanya hivyo ni kwa sababu utalii unaenda vizuri, karafuu anauza vizuri na ndio maana ikaweza kujitosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa utamkuta mtu anakurupuka anakuambia, Seif ndio atakuwa Rais atauweza uchumi, unajidanganya. Seif alitia mpira kwapani na Bwana Jecha alimpa uhuru mkubwa tu wa kugombea na alimuambia tarehe 20 Machi, 2016 uchaguzi kashindwa. Katia mpira kwapani, ninawaambieni msilolijua ni sawa na usiku wa kiza, tulieni Mheshimiwa Shein akamate madaraka aendelee nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa uchaguzi mwaka 2020, mwaka 2020 kama hamkuja basi tena tunaendelea, tunapiga more waliyojionea vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi nitajikita katika diplomasia ya kiuchumi. Ninajua Wizara imejipanga katika kukuza diplomasia ya kiuchumi na kwenye kitabu chenu nimeona kwamba tayari mmejikita na mnakwenda vizuri. Nilikuwa nataka kusema hivi, kwa sababu Tanzania hivi sasa inataka kujikita katika viwanda, je, Wizara imejipanga vipi kutafutia masoko ya biashara ambapo kwa sababu tutakapojiingiza kwenye viwanda, lazima tuwe na masoko nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namtaka Mheshimiwa Waziri utakapokuja kujumuisha, uniambie masoko ya nje tumejikita vipi ili kwa bidhaa zetu tuweze kuuza. Kwa kweli Tanzania inajikita katika mambo ya utalii, kwa sababu tunavyo vitu vinavyotufanya ili tuweze kuvutia watalii wetu. Kuna Mlima Kilimanjaro, kuna fukwe za Bahari za Zanzibar, kuna bustani ndani ya Bahari ya Hindi na hiyo wanakuja wanapoenda kuangalia, vilevile tuna mbuga za wanyama. Sasa ningekuomba na haya sasa myafanyie kazi ya kuyatangaza, msiwaachie Kenya ambao wakitoka wao ndio Tanzania wakatutangazia, wakati sisi tuna uwezo na uwezo huo najua Mheshimiwa Waziri unao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia ambalo sikuliona kwenye kitabu chake, mwaka jana tulizungumza kwamba kuna vijana Wazanzibari 13 mliwasomesha, ili baadae muwaajiri katika Wizara zenu au vitengo vyenu. Lakini kwenye kitabu chako sijaona hao vijana ambao wameajiriwa au hawakuajiriwa, umetuambia kwamba kuna watu wamestaafu, kuna watu wamemaliza muda wao, lakini hujasema vijana gani ambao tayari umewaajiri kama kutoka Tanzania Bara au Tanzania Visiwani. Sasa hivyo Mheshimiwa Waziri ningependa pia ukija unijulishe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kuhusu kitabu chako cha mwaka jana ukurasa wa 61; mlisema Wizara mnajikita katika kuweka vitega uchumi, kufanya wafanyakazi watakaokuwa nje ya taasisi yenu ambao watakua Ubalozi kupata sehemu zao za kukaa na ofisi zao za kukaa. Lakini sijaona kwenye kitabu chako maendeleo yake yamekuwaje kama kweli, maana ulisema mpaka mtakuwa na mapato katika sehemu za vitega uchumi, kwa kupata viwanja na majengo ambayo mengine mtaweza kukodisha. Sasa na hilo ningependa utakapokuja Mheshimiwa Waziri nipate kujua maendeleo yake yakoje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa sababu Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki makao makuu yake yako Zanzibar. Sasa hili lazima nitoe pongezi kwamba Zanzibar ambayo mmeipa kitengo kama mlivyosema kwamba Kamisheni ya Kiswahili Makao Makuu yake yatakuwa Zanzibar, ni katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ilianzia kuanzia mwaka 2014. Sasa hili kwangu ni pongezi na ninashukuru, na tutaendelea kuilinda, na tutaendelea kuilea kama tunavyoilinda na kuilea CCM, kwa maelezo hayo naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nashukuru kwa kupata nafasi hii adhimu katika Bunge lako Tukufu ya kuweza kuchangia hoja ya PAC na LAAC kama hivi nitakavyoelezea.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Kamati na CAG wote fedha za kufanyia kazi zilikuwa ndogo, lakini tumshukuru Mwenyezi Mungu kila mmoja ilibidi atekeleze wajibu wake ili suala hili liweze kufanikiwa. Ukweli ni kwamba kulikuwa na uhaba wa fedha za kufanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF). Kulikuwa na hoja hapa ilizungumzwa kuhusu ujenzi wa Kigamboni ambapo NSSF waliingia mkataba na Azimio Housing Estate. Azimio House Estate ilikuwa watoe ekari 20,000 za ujenzi huo kulingana na makubaliano ya mkataba. Kiukweli ekari walizotoa ni 300. Makubaliano yao ilikuwa kama wangetoa ekari 20,000 ilikuwa na sawasawa na 20% ya hisa na 35% ya hisa ilikuwa ni kuchangia fedha, lakini hayo hayakuweza kutendeka na ndiyo maana ujenzi wa Kigamboni ukasuasua na kusimama kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ya Kamati aliyoeleza Mwenyekiti nakubaliana nayo kwamba kuundwe Kamati Ndogo iweze kusimamia na kufuatilia nini kilichokwamisha, nini ilikuwa tatizo hata makubaliano hayo hayakufikiwa na mradi huo ukawa haukuendelea. Taarifa hiyo baadaye iletwe Serikalini kuangaliwa na kujadiliwa hadi suala hilo liweze kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kuongelea Mfuko wa Pensheni ya Watumishi wa Umma. Mfuko wa Pensheni wa Watumishi wa Umma una matatizo, baadhi ya wastaafu wetu wanahangaika, hawalipwi na kutokana na upungufu uliojitokeza katika tathmini ya kitaalam kwa muda mrefu mfuko huo umekuwa unasuasua haufanyi kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naona mfuko huu unakwamishwa na Serikali, inatakiwa Serikali ikikopa kwenye mifuko hii iweze kulipa. Serikali imechukua fedha za mfuko huu na tumefanya kazi zetu, lakini hatulipi tutegemee hawa wastaafu wetu watapata fedha wapi na wanategemea walipwe na mfuko? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa tathmini iliyofanyika inaonesha kuanzia mwaka 1999 hadi leo wazee wetu wanahangaika. Wengine hawana watoto, wengine hawajiwezi, tunategemea hawa watapata wapi matumizi yao? Ingawa wamezungumzia kwamba wanategemea Februari watamaliza tathmini yao na waweze kuwalipa, hivi kweli mtu ataweza kukaa bila kutumia, bila kula mpaka ifike Februari? Naiomba na Serikali iweze kulipa madeni ya mashirika yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala lingine la Bandari. Udhibiti wa mapato ya bandari kidogo uko hafifu, na kwanini nasema hivyo? Kuna meli nne zilikuja bandarini lakini hakuna mapato yaliyokusanywa kutokana na meli hizo kuwepo pale. Meli ziliondoka na baada ya kuondoka, baada ya muda wa miezi 18; CAG katika kuangalia taarifa kwenye vitabu vya hesabu za bandari ile anakuta kwamba meli nne zimeingia na zimetoka, makusanyo hayakupatikana kiusahihi na meli zimeshaondoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie ni meli ngapi zimeingia. Hizi nne CAG ameziona, je, hizo za nyuma ambapo siku nyingine hata kwenye vitabu hazikuingizwa? Inamaana wao wenyewe Bandari wanajikosesha mapato yao kutokana na kutokuwa udhibiti katika makusanyo yake.
Mimi ninampongeza Mheshimiwa Rais kwa kufanya ziara bandarini, kaujua udhaifu wa bandari yetu na ndiyo maana Mheshimiwa Rais ikabidi aende akaangalie hali halisi na sote tulisikia kwenye vyombo vya habari nini Mheshimiwa Rais alichogundua na matokeo yake yalikuwa nini. Ushauri wangu, naiomba bandari iweze kudhibiti mapato yao maana tunaitegemea kimapato. Wakiweza kudhibiti mapato yao ndipo Serikali yetu itakapoweza kufanyakazi na wananchi tutafaidika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba kuzungumzia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Taarifa ya CAG inayoishia Juni 30, 2015 ilionesha kwamba misamaha ya kodi imepungua kufikia jumla ya bilioni 1.6, sawa na asilimia 15.1 kwenye makusanyo ya TRA. Ingawa tunasema misamaha ya kodi imepungua lakini Serikali bado inapoteza mapato yake kutokana na misamaha hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninao mfano naweza kutoa. Kuna misamaha ya kodi iliyotolewa kwenye mafuta yenye thamani ya shilingi bilioni 22.3 ya Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Geita na Resolute. Mafuta hayo badala ya kutumiwa na Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Geita na Resolute wao wakawapelekea wakandarasi wengine kuyatumia. Sasa msamaha umepewa wewe kisha wewe unampelekea mwenzio, hilo si tatizo? Tena tatizo sugu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningeiomba Serikali, masuala kama haya CAG akishayaona lazima tuwe tunayafuatilia. Lakini wakati mwingine ufuatiliaji unashindikana kwa sababu fedha ambayo ndiyo nyenzo hakuna.
Kamati imetaka kufuatilia ili ipate uhakika, inashindwa kwenda kutokana na nyenzo ziko hafifu. Sasa nafikiri kwa haya machache niliyoyazungumza na yote ambayo yanakwamishwa na nyenzo za kifedha naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru au kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa umahiri wake anaouonesha Tanzania kuimarisha uchumi, uwajibikaji na maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile sina budi kumshukuru Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, mama chapa kazi na tunakuona umevaa viatu vya Marehemu Dkt. Omar Ali Juma, umevaa viatu vya Dkt. Mohamed Shein,

tunakuona unavyoenda mbio na Muungano na Muungano utadumu. Mama unapofika Dodoma mwezi wa Ramadhani, usitusahau katika ufalme wako, Inshallah. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie Ziwani Zanzibar katika Jimbo la Jang’ombe. Ziwani marehemu bibi zetu tulikuwa tunasikia wanaita Bomani. Mimi nazaliwa nimeliona Ziwani boma liko vilevile na mpaka leo liko vilevile, kama linatengenezwa matengenezo yake siyo makubwa. Isitoshe unapotaka kuingia bomani njia za panya zimejaa tele, ukaingia ndani na utatoka hakuna atakayekuona ingawa wao wenyewewanatumia milango, kuna milango mizuri na kuna ulinzi, lakini imekuwa ni bure wakati milango iko ya kuingilia na kutoka na humu kuna milango ya panya imekuwa haina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivyo kwa sababu ya uzio, uzio uliojengwa toka ukoloni mpaka leo haujatengenezwa, Ziwa liko karibu na mitaa wanayokaa watu, wametengeneza njia za panya. Sasa naomba Mheshimiwa Waziri aende akaangalie na aweze kutuwekea imara ya boma letu ambalo tunaliamini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia vijana wetu hawa ambao katika ukurasa wako wa 11, Mheshimiwa Waziri alizungumza udhibiti wa dawa za kulevya. Najua dawa za kulevya nikizungumzia ‘unga’ haliko kwenu, kuna kitengo kimeundwa, lakini nalileta kwenu kwa sababu mnao askari wa kutosha wa kusaidia kitengo kilichoundwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, marehemu bibi yangu niliwahi kumsikia akizungumza kuna Askari Kanzu ambao niCID. Hawa askari kama mtawatumia wataweza kukisaidia hiki kitengo, kwa sababu hiki kitengo kinahitaji kipate watu na ninyi ndiyo mtakaoweza kuyapangua haya mafiga matatu, kwa sababu kuna mletaji, kuna msambazaji na kuna mlaji. Sasa hawa wote, hili figa hili kama hamkuweza ninyi kuliangalia mkalipangua kwa sababu CID anaweza kupenya sehemu zote akampata mletaji, akampata msambazaji, walaji tunawaona kwa sababu picha yao inaonekana, ili muweze kukisaidia hiki kitengo tuweze kusaidia nguvu kazi ambayo inapotea katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu suala la NIDA. Unajua katika bajeti yenu ya mwaka jana, mlizungumza kwamba hiki kitengo mtakiboresha baada ya kupata vifaa kutoka Tume ya Uchaguzi. Vifaa mmevipata, lakini hakuna kinachotendeka. Hatuoni tena NIDA kazi inayoifanya, hatuoni kuangalia kuboresha maslahi ya watu, wafanyakazi waNIDA mmewatoa/mmewapunguza, sasa kweli hivi vifaa mlivyopewa vikae ndani ni mapambo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa vilivyopo mle ndani viweze kufanya kazi na wafanyakazi ni hawa vijana ambao tayari mmewatoa. Maana mmesema mtafanya utambuzi wa Watanzania, mtafanya usajili wa Watanzania, usajili hauko, upembuzi hauko, watu wanajiingilia na kutoka. Nataka Waziri utakapokuja uniambie, kwa nini mlipunguza wafanyakazi na wakati ulikuwa hujaimaliza kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ujenzi wa ofisi ya Mambo ya Nje Zanzibar, hii itasaidia kuwa na jengo la ofisi ambalo lipo chini ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uraia wa nchi mbili (diaspora) ni jambo la siku nyigi lakini bado halijafanikiwa. Ofisi yako ukurasa wa 112 na113 ndiyo kwanza inasimamia usajili, ina maana fursa hii ya kuinua uchumi wetu wa Tanzania bado?

Kuhusu diplomasia ya kiuchumi hususan kwenda katika uchumi wa viwanda, hii vita ni kubwa na bado nchi yetu hatujajipanga, sababu elimu bado kutolewa kwa mabalozi wetu, Balozi anakwenda nchi za nje lakini haielewi Sera ya Diplomasia ya Uchumi. Tunaomba elimu itolewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. FAKHARIA SHOMARI KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sina budi kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu na kukushukuru wewe pia na kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi pamoja na UWT kwa kuniwezesha leo miye kuwa bado niko Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nitazungumzia ujio wa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipokuja Zanzibar wakati wa kampeni. Amekuja Zanzibar kwa kweli tulimpokea kwa shangwe kubwa na tukakuweko pale Mnazi Mmoja tuliujaza uwanja na kwa kweli wananchi wa Zanzibar walifurahi na tunzo yao waliyoitoa kwamba majimbo yote ya Ugunja wamechukua na ngome ya Pemba tumeivunja na hadi hii leo tunakwenda kifua mbele Zanzibar, haya yote yalikuwa ni matunda ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, baada ya kufika na kutuhamasisha na kutupa busara katika hotuba zake alizokuwa akituelezea pale Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wa 15 Mheshimiwa Rais alisema tunu ya Taifa, tunu ya Taifa kuna vitu alivitaja na hivyo na ndivyo vilivyotupa moyo sisi kule Zanzibar, ambapo alisema amani, umoja na mshikamano, uhuru wa nchi yetu, Muungano baina ya Tanzania Bara na Zanzibar na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli atakuwa karibu na atashirikiana sana na Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi, Rais wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hilo la kwa Zanzibar tumelipokea na lilikuwa jambo la tunu kwetu na tumekubali katika tunu zake alizozisema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Bunge la Kumi na Mbili, wakati anakuja kutuhubia Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, alizungumza kwamba atashirikiana na akinamama kwa karibu na kwa kweli Mama Samia anafanya kazi nzuri na Mheshimiwa wetu na yeye ndiye aliyetupelekea akatuona kwamba wanawake tunafaa na akasema wanawake ukiwakabidhi dhamana ni watendaji wazuri na hii lazima tumpongeze kwa sababu yeye katuweka karibu, baadhi ya Mawaziri wanawake wapo na wanafanya kazi nzuri, Makatibu Wakuu wako wanafanya kazi nzuri ili kwetu sisi lazima tumlipe wema wanawake wote wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa nini tumeingia? Mheshimiwa alijitoa alitembea mikoa yote, na akatuletea kura za kishindo, leo humu ndani wengi wetu UWT tunatamba na tusingeweza kutamba kama sisi yeye Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kutupatia kura nyingi tukaweza kuingia humu Bungeni, hatuna la kumshukuru isipokuwa tufanye kazi nzuri akinamama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna lingine katika ukurasa wake wa 15 Mheshimiwa Rais alisema kwamba anampongeza Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuimarisha utawala bora hususan kwa kusimamia nidhamu kwenye utumishi wa umma na kuzidisha mapambano dhidi ya ubadhirifu, rushwa, wizi, ufisadi na hili kwa Zanzibar ambapo yeye ameweza kuonesha njia kwa Bara na Zanzibar alivyokuwa amelizungumza hili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. FAKHARIA SHOMARI KHAMIS: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kwa kazi nzuri mnayoifanya humu ndani ya Bunge, kwa uweledi mliokuwa nao na kazi nzuri iliyotukuka, lazima mpongezwe.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Watendaji wake kwa kazi aliyotuletea hapa ametufahamisha, tumeelewa, lakini wenzetu wa upande wa pili walikuja na kashfa hawakuja na maelezo ya kuujulisha umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa sababu Zanzibar iko kwenye hali ya amani na utulivu, kuanzia uchaguzi uliofanywa wa marudio walikuwepo Wanajeshi wakaweza kuiweka hali ya salama na utulivu na hadi leo hali hiyo inaendelea ya usalama na utulivu, tunashukuru.

Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante. Taarifa yake siipokei kwa sababu ilikuwa ishara tayari walishaonesha upande wa pili na walioweza kutuliza ni Jeshi waliofanya kazi na tukaenda kwa amani na utulivu. Polisi walikuwepo wakifanya shughuli zao na wao walikuwa wakiangalia amani na utulivu wa nchi yetu na hadi hii leo tunaendelea kuwa na amani na utulivu katika nchi yetu.

Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante, nilindie muda wangu. Naomba kuzungumzia habari ya viwango vidogo vya pensheni wanavyolipwa askari wastaafu wa zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku tunavyokwenda hali ya maisha inapanda na siku zinavyokwenda mishahara inapanda, lakini wale wastaafu wa zamani kiwango kinakuwa kiko kile kile, ambapo hakiongezeki. Sasa ningemwomba Mheshimiwa Waziri awe anaangalia, baada ya muda na wale askari wastaafu wa zamani viangaliwe viwango vyao. Kama kuna Koplo/Sajenti/Luteni Kanali wa sasa kastaafu basi na wale kiwango kile kile kwa mwaka ule waweze kuwapa wasiwaachie kile kiwango duni ambacho wanacho na kinaweza kuwapa maradhi, labda akapata sukari, pressure matumizi yake yatakuwa madogo wakati matumizi yako juu na yamepanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja na suala lingine la JKT. JKT Mheshimiwa Waziri kaizungumza katika ukurasa wa
26 na amezungumza vizuri, tunakupongeza. Lakini ningekuomba Mheshimiwa Waziri idadi ya vijana wa Zanzibar wanaokwenda JKT utuongezee. Kwa sababu umesema kule wanapata elimu ya ukakamavu, elimu ya kujiajiri na elimu ya kuajiri wenzi wao. Sasa ukituongezea idadi ya vijana wetu wakaenda kule wakarejea tena kufanya kazi hiyo ya kwenda kujiajiri, wakawa wakakamavu watapata ajira nyingi za ukakamavu, watapata kujiajiri wao na wenzi wao. Naomba Mheshimiwa Waziri ulipokee ili uweze kutusaidia kwa upande wa Zanzibar. (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia eneo la mambo ya kuingiliana baina ya majeshi na raia mitaani. Kuna maeneo kimazingira ni magumu, kuna maeneo ambayo wanayo jeshi lakini maeneo yale yalikuwa ya raia hapo wakati wa mabibi na mababu zetu, lakini jeshi sasa hivi imehodhi. Watu wa pale ilikuwa inabidi walipwe kwa kutoa viwanja vyao lakini huwa hawalipwi hivyo kunakuwa na mvutano baina ya raia na Jeshi. Sasa liangalie hili na kwa upande wenyewe tuangalie, kama upande wa Unguja Ukuu, Kisakasaka matatizo hayo yapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna mengine, wanajeshi wanawalipa raia, lakini baada ya kuwalipa raia hawaondoki sehemu ile na ninyi mnakuwa hamna uthibiti wa kuyazuia yale maeneo yenu; sasa kunakuwa mvutano mwingine mpya. Utayakuta haya kama kule Dunga, Mgeni Haji, sasa na hayo myaangalie. Kama mtu mmeshamlipa aondoke, kama hamjawalipa na wamekubali kuondoka itabadi muwalipe ili kuweka amani na utulivu uliokuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya Jeshi lazima mfanye utafiti kwa sababu hivi sasa maeneo ya Jeshi yameshaingiliana na ya raia. Bila kufanya utafiti mkaweza kujua sehemu zenu ziko wapi na za raia ziko wapi hapo mwisho kutazuka mtafaruku baina ya Jeshi na raia. Mimi ninajua Ninyi Wanajeshi ni wasikivu, walinzi na pia mnawapenda raia wenu. Sasa naomba Mheshimiwa Waziri na hili mliangalie ili kuondoa mtafaruku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naunga mkono hoja, sina matatizo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante, sina budi kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuipongeza na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa pamoja na Waziri wao na watendaji wote ambao leo wamewasili hapa ili kuangalia mwenendo wa bajeti yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nilikuwa nataka nizungumzie ukosefu wa hati miliki katika kambi zetu. Ukosefu wa hati miliki katika kambi zetu ndiyo unaoleta migogoro baina ya jeshi na wananchi. Utawakuta wananchi wanakwenda kuvamia sehemu za jeshi, wakati sehemu zile hazina hati miliki sehemu ni za jeshi lakini hati miliki hawana na hawafuatilii kuzitafuta matokeo yake watu wanalima, wanajenga, migogoro inaanza wanaanza kuvutana baina ya Jeshi na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano; ukija Kambi ya Ubago iliyopo Zanzibar, Unguja Ukuu iliyoko Zanzibar na baadhi ya kambi nyingi hukuhuku Tanzania Bara. Pia nina wasiwasi kama kambi yangu ya Mtoni au Mazizini zimezungukwa na raia/wananchi na bado wanapenya wanaingia. Utakuta hakuna uzio, kuna msitu na ule msitu mtu anaweza akapenya, sasa na hilo waliangalie, watafute mbinu kupatikane hati miliki waweze kudhibiti sehemu zao kuondoa mgogoro baina ya jeshi na wananchi wakaiingize na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka kuzungumzia suala la Sera ya Ulinzi wa Taifa. Toka Bunge la Tisa, la Kumi, la Kumi na Moja na la Kumi na mbili kelele ndiyo hizo hizo. Lakini tushukuru hili Bunge la Kumi na Mbili taarifa iliyokuwepo tayari kwa sababu walikuwa wanazungumza kwamba bado kwamba Serikali ya Zanzibar haijatoa maoni yao, wadau hawajatoa maoni yao na sasa hivi tayari wadau wameshatoa, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshatoa. Je, itaanza kutekelezwa lini? Maana yake sera ikifanyakazi ndipo jeshi litakapozidi kuimarika, kwa wafanyakazi na jeshi lenyewe. Lakini bila kuwa sera kufanyakazi inamaana ipo ndani vitabu au ndani ya mafaili itakuwa bado utekelezaji wake haujaonekana, bado elimu haijatolewa na bado wananchi watakuwa hawajafahamu nini kinachoendelea. Hatutaki kwamba mambo yao ya siri yatoke, tunataka yale yaliyokuwa ni wajibu ambao kila mmoja ayatambue aweze kuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija na hili la mashirika haya, Shirika la NYUMBU na MZINGA. Haya mashirika ni mazuri, yanazalisha lakini kwanza wana upungufu wa wafanyakazi na hao wafanyakazi waliopo pale wawe na utaalam kwa sababu sehemu ile inafanyakazi ya kitaalam; bila ya kuwa na wataalam haitaweza kuzalisha kama anavyofikiria. Ina uhaba wa rasilimali watu na hao watakaoajiriwa wawe wataalam waweze kufanyakazi za kuweza kutambulika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la umwagiliaji maji; wanacho kilimo cha umwagiliaji maji, tulikwenda tukaona Chita, wapo vizuri wanalima, kuna samaki wazuri, watamu maana tulipewa tukala. Lakini tatizo lililopo pale hawana vitendea kazi vya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri iliyotoa matumaini na iliyomfanya kila Mtanzania aende kifua mbele kutokana na hotuba ilivyopangika. Hata wasomi kwenye redio, kwenye mitandao, kwenye television wanaizungumza speech yake jinsi ilivyokuwa zaidi ya kusomeka imetekelezeka na bado inaendelea kupendwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitazungumzia zaidi tena kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ujio wake Zanzibar wakati ule wa Sherehe za Mapinduzi na alipangiwa kwenye ratiba kwenye mabanda ya maonyesho pale Maisara, watu walifurahi jinsi alivyohudhuria na jinsi alivyotekeleza wajibu wale aliopangiwa. Zaidi ningependa kumuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni Waziri wa Muungano na Zanzibar ni sehemu ya Muungano ningependa apange ziara yake kama Waziri Mkuu aje Zanzibar kuimarisha Muungano. Taasisi za Muungano Zanzibar zipo, wafanyakazi wa Muungano Zanzibar wapo kama anavyofanya huku Bara akazitembelea taasisi, akanong’ona na Watanzania waliokuwepo huku, basi tunaomba na Zanzibar afanye ziara kama hiyo. Tunampenda na tunamuomba aje Zanzibar.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najielekeza katika ukurasa wa 12 ambapo Mheshimiwa Waziri Mkuu amezengumza kuhusu mafanikio ya Watanzania na takwimu siyo mbaya katika ajira, lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu ningesema ajira kweli zinafanywa na zinatekelezwa vizuri, lakini kuna ajira nyingine tunaziacha. Kwa mfano, Mabalozi wetu wako nje tumewapa kazi wanashughulikia diplomasia ya uchumi lakini Watanzania wako wenye Masters, wako waliokuwa na degree, wana Ph.D wamebobea kiswahili, kiswahili sasa hivi kina mantiki kubwa nje ya Tanzania. Watu wengi wanazungumza kiswahili na kinataka walimu wa kiswahili na Tanzania tunao walimu, sasa ajira ni hizi tunaziacha.

Baadhi ya walimu wetu tuwapeleke, tuwaambie Mabalozi watafute hizi ajira kwa upande wa nchi walizokuwepo baadae walimu waende wakasomeshe, ajira itapatikana na Kiswahili kitazidi kuendelea katika kila nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu kazungumzia kwamba tayari tumeshahamia Dodoma, baadhi ya wafanyakazi, baadhi ya taasisi na alifika hadi akasema wafanyakazi 3,829 wamehamia kwa awamu na bado wataendelea na ataimarisha miundombinu. Miundombinu aliyokusudia ni miundombinu mikubwa lakini ya ndani hapa Dodoma tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda barabara ya Sengia, Site Two kule, nenda maeneo ya Area D karibu mtasikia kumetokea ajali maana mashimo yaliyopo ni makubwa, kila mmoja anabidi ayakwepe, huku bajaji, huku pikipiki, huku gari sasa kila mmoja anakimbia shimo anamfuata mwenzie. Sasa kama kweli amekusudia tuiimarishe Dodoma iwe nzuri basi na barabara za ndani pia zitengenezwe ili tuweze kujisikia walipa kodi kwamba tayari Dodoma iko ya kileo na ya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia kuhusu sekta ya uzalishaji ambayo iko ukurasa wa 27. Nakubaliana na maelezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu lakini unapotaka kuzalisha kufungua viwanda ujitahidi kuwa na malighafi na malighafi zetu nyingi ni kilimo.

Sasa tuwahamasishe watu wetu kulima ili waweze kupata malighafi kama ni pamba, kama ni nyanya ama kitu chochote ili wakati tukiwa tunafanyakazi zetu za viwanda tutakapotoa mazao yetu yawe bei rahisi. Ikiwa malighafi tutanunua, tunaimarisha viwanda, itabidi mazao yatakayotoka yawe ghali, sasa lazima tutoe elimu kwa wakulima wetu, tutoe elimu kwa watu wetu wenye viwanda tuwaambie kwamba lazima tutekeleze wajibu wetu ili malighafi iweze kupatikana na tuweze kujitosheleza na kazi zetu ziwe kuimarika kwa mujibu wa shughuli zetu za viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi pia nimpongeze Mheshimiwa Jenista Mhagama alipofanya ziara yake Zanzibar, akatembelea Mikoa ya Zanzibar kuangalia mambo ya TASAF, kwa kweli ameimarisha Muungano, watu waliridhika na akaona kuanzia awamu ya kwanza, ya pili na ya tatu vipi inavyokwenda na vipi Zanzibar imejikita katika kupokea mradi huu wa TASAF.

Sasa na yeye pia namwomba kuja kule Zanzibar isiwe ni mara yake ya kwanza tu, aendelee kuja kwa sababu miradi ya Muungano ipo ambayo inamhusu aje kuingalia na Wabunge wenzie tutakuwa pamoja bega kwa bega kuwa nae. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina budi kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Mama Ummy Mwalimu, Waziri, Naibu Waziri wake pamoja na watendaji wake wote, Katibu Mkuu na Wakurugenzi kwa kitabu kizuri walichotuletea ambapo wameelezea utekelezaji wa nyuma na utekelezaji kwa mwaka 2018/2019 sasa unalinganisha na unaiona faraja katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie na pia kutoa pongezi nyingine juu ya kinga ya saratani. Kwa kweli, hii kinga ya vijana wetu wale wa miaka tisa mpaka 14 ni nzuri, lakini hii kinga inayotolewa je, vijana wetu wamepewa elimu? Unakwenda kumpeleka kwenye kinga anapata kinga yeye anajua ana kinga, lakini hizo kinga unazompa umpe na elimu namna ya kuweza kujikinga na ile kinga aliyokuwa nayo na elimu hii bado sijaiona na hata kwenye hiki kitabu chako sijaiona, ningeomba hili mliangalie.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine ni la ugonjwa wa fistula. Fistula anapata wa mjini, anapata wa vijijini na ukiangalia utakuta hospitali inayoshughulikia siyo hospitali ya Serikali, ni hospitali ambayo imekubali kujitolea na kutoa huduma za bure kwa anayetibiwa hata kama yuko kijijini, nauli mpaka anaweza kufika akatibiwa. Sasa mimi ninashangaa kwa nini Serikali na ninyi msingeingia hamu mkaona hili jambo muweze kulitekeleza kama Serikali, mkapeleka vituo katika Mikoa. Kumtoa mtu kijijini kuja mjini kutibiwa ndiyo mtakuta baadhi ya wananchi hawawezi kuja hawezi kuiacha familia yake akaja huku wakati anajua anakuja kupata matibabu, lakini kama na Mikoani mngeweka vituo ambavyo vikaweza kutibu fistula ambayo inatibika, ingekuwa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja kwenye suala lingine ambalo lilikuwa linazungumzwa mara nyingi na kwenye hiki kitabu sijaona. Walikuwa wanazungumza kuna kit bag ina vifaa au zana mama anapokwenda kuzaa anakuwa navyo. Hata Dar es Salaam wakati wa pasaka Mheshimiwa Makonda alivitumia kama yeye alitoa msaada kwa akina mama na ambapo ilisemekana vinauzwa, sikumbuki kama ile kit bag moja ni shilingi 20,000 au kiasi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini msingefanya vikawa bure mkaviweka hospitali kwa anayekwenda kujifungua akifika ana uhakika kwamba atapata zana za kutosha ambazo zimetolewa na Serikali.

Kwa hiyo, inavyoonesha hizi kit bags syo mbaya, mimi naona hata mtakapokuwa katika ushirikiano baina ya Bara na Visiwani ingawa Visiwani kule inatolewa matibabu ni bure, ni Sera ya Zanzibar, lakini na ninyi pia mngeipeleka hii elimu wa kuwa na kit bags kama zile wakaweza kuwawekea akina mama wakati wanakwenda kujifungua wakapata wepesi na kuwa na uhakika kuna kitu kinaweza kunisaidia.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa 21, namba 23 ilikuwa inaelezea ujenzi wa vituo vya afya ambapo ilikuwa TAMISEMI ishirikiane na Wizara ya Afya muweze kujenga vituo vya afya vya vijiji, Wilaya na Kata, lakini hadi hii leo mnazungumzia tu mnaboresha vya zamani vya zamani tunajua vipo, tunataka vipya vijengwe na ni muda mrefu havijajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na haya mengine yaliyobakia nitayaleta kwa maandishi. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwanza sina budi kuwasifu Wizara, Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wao wote kwa kazi nzuri na hasa Kamishna wangu Bwana Mohamed Hassan ambaye anafanya kazi nzuri na uteuzi wake ameupata hivi karibuni na tunamwona jinsi anavyojitahidi kwa utendaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi tumelipa majukumu makubwa, majukumu ya kutulinda sisi raia na mali zetu lakini kwa kweli utendaji wao wa kazi na vitendea kazi walivyokuwa navyo siyo rafiki. Kwanza anapokuwa anaenda kazini, baadhi ya sehemu anazofanyia kazi yake siyo nzuri, anaporudi kazini kachoka, sehemu anapoishi au anapokaa sio rafiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sisi Kamati yetu tulikwenda kutembelea Mtwara, Lindi pamoja na Kilwa, jamani nyumba tumezikuta huwezi kuamini kwamba kweli nyumba hizi wanaweza kukaa binadamu na wakafanya kazi na wakaweza kutulinda na kuwa wako kwenye nafasi ya kufanya kazi kwa weledi ambao tunauona hivi sasa majeshi kwa kazi zake nzuri wanazotufanyia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli utasikitika na utawaona hawa watu wana shida katika utendaji kazi wao lakini wanajitahidi kuweza kutufanyia kazi na kuweza kuturidhisha. Wanapokuwa katika doria wana matatizo ya mafuta, bajeti yake inakuwa ndogo. Wao wenyewe kimafao pia malimbikizo yao wanakuwa hawayapati kwa wakati. Sasa haya yote yanakuwa ni mtihani kwao ina maana lazima Mheshimiwa Waziri awatazame hawa watendaji wetu kwa jicho la ziada ili waendelee kufanya kazi zao nzuri wanazotufanyia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitembelea majengo ya Uhamiaji yaliyokuwepo Lindi na Mtwara. Majengo hayo kwa kweli yanasikitisha na kama ulifika kule, maana kipindi kile ulikuwa kwenye majukumu mengine hatukuwa na wewe lakini sisi Kamati tumeona na hatukupendezwa nayo na kwa sababu tumekuta kikwazo ni pesa za maendeleo haziendi kwa wakati na badala ya kupata kitu kizuri mtapata hasara.

Maana yake majumba yanavyopata mvua na miti ishaoza ina maana itafika wakati patabakia kiwanja badala ya kumalizia zile nyumba. Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni ajira za Jeshi la Polisi ambapo tayari hivi sasa zimeshatangazwa na tayari vijana wetu wameshaanza kuomba kwa mujibu wa utaratibu. Kwa upande wa Zanzibar hizi nafasi hatujui zitagawiwa vipi lakini najua utaratibu wanao na wakija hapa watatueleza jinsi wenyewe taratibu zao walivyozipanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasisitiza vijana walioko JKU Zanzibar tayari ni wakakamavu, wameshakaa chuoni kule, washasomeshwa na baadhi yao elimu zao zinafika degree, vijana hawa wasiwasahau waweze kuwachukua. Wengine wamewekwa kama wakufunzi ili wawepo pale JKU waweze kujitolea pia waweze kuwasaidia waweze kupata kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kulizungumza ni malipo ya askari wastaafu. Kwa kweli askari wastaafu wanapata shida Zanzibar na shida wanazozipata kwamba kule Zanzibar hakuna ofisi inayoshughulikia mambo ya pensheni, inabidi waende Tanzania Bara. Mtu unapokuwa tayari umeshaastafu hata ile haiba yako kwa wenzio inapungua, sasa wanahangaika kupata pesa kwa wakati hawapati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungeomba ofisi kama hiyo iwepo na Zanzibar kwa wale wanaomaliza Zanzibar walau waweze kuhangaikiwa palepale na mambo yao yaweze kuwa pale pale. Kwa kipindi hiki wanakuwa hata pesa za kupanda boti kwenda na kurudi hawana tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia kuhusu Makao Makuu ya Polisi Ziwani, wazee wetu walikuwa wanaita bomani. Mimi nimefunua macho boma lile nimeliona liko vilevile na hadi hivi sasa ni bovu, ukiangalia senyenge iliyozunguka boma ni mbovu, ukiangalia majumba yenyewe ni mabovu ambayo yapo kabla ya 1964 toka ukoloni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar pana historia na maboma yale na kuna nyimbo inaimbwa tarehe 12 bomani tuliiingia. Sasa kwa nini hatulipi hadhi yake ya boma hilo tuliloingia ili likaweza kuonekana? Kwa sababu kila anayekuja historia pale anaiona. Ukiingia ndani majengo mabovu, njia za kupitia usafiri wa ndani mbovu, unachokiangalia hata kama mtu anataka kwenda toilet pia atafute vipi apenye aingie ili akajisaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ningeomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuelezee katika bajeti yake ya maendeleo kwa upande wa Zanzibar na boma lile lililokuwepo Ziwani watalisaidia vipi ili historia iweze kujiendeleza? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nashauri kwamba hawa wastaafu wetu ambao niliowazungumzia jamani wanateseka, wazidi kuwaangalia. Kama hawatowaangalia baadaye watakuja kujuta waje kuwasifu au wasikie wamefanya vitu vingine havistahili kumbe njaa mtu imemkabili mtu na njaa kwa kweli ni mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. FAKHARIA SHOMARI KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza, sina budi kuipongeza Wizara kwa hatua nzuri wanayofikia katika majukumu yao Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Kurugenzi yake yote kwa utendaji wao mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, sina budi kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwasamehe wafungwa na kuwa huru kwa mujibu wa Katiba na ndani yake ndiyo Mheshimiwa Mbilinyi na yeye kapata msamaha leo tunaye hapa Bungeni na tunaweza kuwa naye na kuchangia naye katika Bunge letu hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia diplomasia ya uchumi; diplomasia ya uchumi inasaidia kwa Wizara na nchi nzima kuweza kujua jinsi Mabalozi wetu wanavyokwenda nje nini majukumu yao ya kufanya. Hata hivyo, ilivyo Wizara bado haijajipanga kuweza kupatikana sera mpya yao ya Wizara ikaungana na hii ya diplomasia ya uchumi ikaenda pamoja, vikawa vitu viwili sambamba tukaweza kufanikiwa katika majukumu ya utendaji wetu wa kazi na Wizara mpaka leo sijui inasubiri nini na kushindwa kutoa sera mpya ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje. Mheshimiwa Waziri naomba atakapokuja atuambie wanakwama nini hata wanashindwa kutoa sera mpya itakayoendana na sera ya uchumi ya diplomasia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sera hiyo ya diplomasia ya uchumi itasaidia kutupatia masoko, kutuletea watalii tena siyo wale wa makundi tunataka waliokuwa na hadhi za juu, itaweza kutuletea wawekezaji maana tuna sera ya viwanda, tunataka kuanzisha viwanda Tanzania ili tuweze kutanua uchumi wa Watanzania. Zanzibar kuna fukwe nzuri za watalii, Bara kuna Kilimanjaro nzuri kwa watalii, tuna mbuga za wanyama, kuna bahari au bustani ndani ya bahari ambavyo hivyo vyote ni vivutio kwa utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwa Mheshimiwa Waziri, kama inavyozungumzwa, anavyopeleka watendaji katika Balozi zetu, apeleke watendaji ambao wanaendana na diplomasia ya uchumi ili waweze kutusaidia katika majukumu yetu tunayotaka kuyaanzisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukija kwa upande wa Zanzibar, Zanzibar tunataka au tungependa tuwe na jengo letu kama Ofisi ya Wizara ya Muungano, kama walivyo Mambo ya Ndani, kama walivyo Wizara nyingi za Muungano zina Ofisi zao wenyewe wamejenga. Sasa tunashangaa Mambo ya Nje mpaka leo kuanzia 1964 hadi leo hamna jengo, wana jengo lile ambapo wanasema wapo kwenye mazungumzo na mazungumzo hayo haijulikani yatamalizika lini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawaomba viwanja Zanzibar kwa kujenga Ofisi vipo. Waache mazungumzo, waombe viwanja waweze kujenga lakini wakisubiri wanazungumza hii kama inabidi wanavuta muda na wakati, wakati muda wa kujenga hawajakuwa nao na wala hawajakuwa na tamaa ya kujenga. Mheshimiwa Waziri naona Kamati imemwambia kwamba tunataka Kurugenzi za Zanzibar na wao wafanye kazi katika jengo linaloridhisha na linaloitwa kwamba ni jengo la Ofisi siyo nyumba imegeuzwa jengo wanasema ni Ofisi, hiyo haitowezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, makazi ya Ofisi za Ubalozi wetu wa nje pamoja na Ofisi zao hayaridhishi na kwa nini hayaridhishi? Kwa sababu kuanzia sasa pesa nyingi tunapoteza kulipa katika majengo. Ikifika mwaka lazima tutenge bajeti ili tulipe pesa za Ofisi. Kwa mwaka huu tayari Wizara imeshatenga bilioni 21.6. Pesa hizi ni za kodi za walalahoi tunazokwenda kulipa, kwa nini tunashindwa kujenga? Tungejenga ili kunusuru pesa za walipa kodi wetu tena maskini wa Tanzania walalahoi.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, hili wazidi kuliangalia maana hizi pesa zitatoka nyingi na pesa hizi kama wangekuwa wanatoa kidogo kidogo huku wanaanza kujenga Ofisi zetu za Ubalozi tungekuwa tayari tuko mbali na tungeweza kupata mafanikio.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, Ubalozi wa Oman umetoa kiwanja Muscat. Tayari Mheshimiwa Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete amekwenda kuweka jiwe la msingi. Hata hivyo, toka mwaka 2012 hadi hii leo hakuna kinachoendelea na wako tayari wenyewe kuchukua sehemu yao kwa sababu wameshatuona hatuna maendeleo ya kuyafanya. Ingawa aliomba 1.8 billion lakini mpaka leo hajapewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naiomba Wizara ya Fedha wangefanya kila mbinu, hizi pesa zikatoka angalau tukaonekana na sisi tunajihangaisha kuleta maendeleo. Ikiwa watu wamesema ukibebwa na wewe jikaze, wametupa kiwanja, wako tayari kutusaidia ina maana sisi kujiendeleza tunashindwa? Mheshimiwa Waziri akishirikiana na Wizara ya Fedha, naomba hili waliangalie na liweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, unyanyasaji wa wafanyakazi wa majumbani nje. Unyanyasaji huu umekuwa mkubwa na vijana wetu wengi wanaondoka kinyemela, Wizara au Serikali inakuwa haijuii, Balozi kule za nje hawajui kama vijana wetu wapo. Sasa hili walitilie mkazo na waweze kujua mbinu wanazopita na waweze kujua Ma-agent wanaosimamia ili hili jukumu liweze kumalizika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtoto yeyote anauma, lakini akiwa wa mwenziwe, mtu anajifanya punguani anamwuona haumi, lakini mtoto anauma na hasa akiwa katika nchi yako akaondoka, akaenda nchi nyingine na nchi yenyewe ina ubalozi na akafika akateseka bila Wizara kujua au ubalozi kujua na hiyo yote inaelekea kwamba wanaondoka hawajui, watafute mbinu wanapita vipi, inakuwaje mpaka wanafika waweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba bado Wizara ya Fedha kwa bajeti hii ingawa safari hii imepanda kidogo kwa 17 percent basi waweze kusimamia hii bajeti itoke kwani ikitoka ndiyo manufaa kwa Tanzania. Tunamwona Mheshimwia Waziri anavyohangaika, anavyokwenda safari zote ndani na nje ili kuisaidia Tanzania na hali tunaiona Tanzania tunavyopiga hatua. Naomba Mheshimiwa Waziri hizi pesa zitoke, Balozi zetu zipate pesa, waweze kufanya kazi na tufaidike. Haitofaidika Balozi itafaidika Tanzania nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya machache, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kupata nafasi hii na mimi kuchangia hoja ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza lazima nifurahie kwamba sasa hivi Tanzania inaelekea katika viwanda, ina maana Tanzania ya Viwanda. Bajeti aliyoileta Mheshimiwa Waziri imepangika, ina vionjo vya kutendea kazi na inatekelezeka. Hongera Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu na watendaji wote wa Serikali katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kujielekeza katika viwanda lazima tuwaangalie wakulima. Bila ya kuwa na wakulima hodari wakaweza kutupatia malighafi viwanda vitakosa malighafi na amesema kwamba viwanda vya ndani vitapata malighafi hapa hapa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa wakulima, kama kweli watajielekeza kwenye kulima ina maana sasa ni mwaka wao nao wa kufarijika katika maisha. Kwa sababu wataweza kuongeza mashamba, watakuwa na ushindani katika bidhaa zao watakazokuwa wanalima, watakuwa na masoko kwamba watapeleka mazao yao katika viwanda vyetu. Naomba wakulima waangaliwe ili kupata malighafi ili viwanda vyetu viweze kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija kwa upande wa pili, tukumbuke kwamba Wizara ya Fedha wanatumia cash budget kwa maana makusanyo mnayoyapata ndiyo mnayoyatumia. Sasa inabidi lazima wajitahidi kupata kodi ili kupata pesa za kutosha, bila ya kukusanya haitawezekana kutumia. Baadhi ya watendaji wetu wanaweza wakazembea katika kukusanya huruma isiwepo, mtu anazembea kwenye kazi unamuondoa kwenye nafasi yake kwa sababu akizembea yeye ameifanya Serikali yote mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuchukulie mfano, siku za hivi karibuni zile mashine zetu za kukusanya mapato EFD zimeharibika, Wabunge wanapiga kelele, jawabu tunalolipata halitoshi kwa sababu mpaka leo ukweli hasa hatujaupata. Sasa tuangalie, tatizo lilikuwa kwa wenye mashine au uzembe wa wafanyakazi au kuna kitu gani kilichojitokeza mpaka leo hakuna suluhisho? Kuna Mbunge mmoja pia hapa kalizungumza hili kwa sababu sasa hivi watu wanatumia risiti na kama tunatumia risiti tayari tunapigwa. Mheshimiwa Waziri akija na hilo lazima alizungumzie ili tuweze kufarijika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, malalamiko mengi yanatokea hapa kuhusu malipo ya kodi mara mbili katika bandari zetu kwa vitu vinavyotoka Zanzibar. Suala hili limezungumzwa, nakumbuka Naibu Waziri wa Fedha alilitolea ufafanuzi kwamba wanakaa sasa hivi wanalizungumza na wakati wowote watafikia muafaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi nina ushauri, kwa sababu jambo lolote linataka elimu, Wizara ya Muungano iko inashughulikia Bara na Visiwani, ipeni majukumu pia Wizara hii kutoa elimu. Taasisi za Zanzibar na na Bara zinazoshughulika na mambo ya fedha wapewe elimu ili waelewe kwa nini huu mvutano unatokea, kwa sababu sheria mnajua ziko vipi na mwelekeo uko vipi ili huu mvutano uzidi kupungua. Nendeni kwenye media mtoe maelezo kuna nini na baadaye mkubali watu wapige simu nao watoe taarifa au malalamiko yao, myapokee na myajibu. Haya ni mambo madogo tu yanazungumzika. Jambo hili linachukua muda mrefu ilhali si refu. Tunalifanya liwe refu ili tuweke mvutano hapa usio na maana ilhali jambo hili linazungumzika na ni rahisi kumalizika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja na suala lingine ambalo liko katika ukurasa wa 46(v), kuhusu kusamehe Kodi ya Ongezeko la Thamani kwenye taulo za kike ili isaidie vijana wetu wa kike na akina mama katika matatizo yao ya kawaida. Nakubali Mheshimiwa Waziri alivyosema kwamba wamepunguza kodi, ni sawa lakini kupunguza huko kusiwe kwa mwaka huu na mwakani upunguze tena ili iwe wanapunguza kidogo kidogo mpaka ifikie sawasawa kama mtu anakwenda kununua karanga haoni shida tena bei yake itakuwa rahisi tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vya ndani vinazalisha, itakuwa kila wakiteremsha bei na bei ya dukani itakuwa inashuka na itakuwa rahisi kila mmoja kununua hata mtoto wa chini atanunua. Inaweza ikafika mpaka Sh.500; inategemea jinsi Wizara itakavyokuwa inashusha na malighafi hiyo itakavyokuwa inauzwa madukani ili vijana na akina mama wetu wamudu kununua bidhaa hiyo. Baadaye itafikia mpaka kupata bure, maana unaenda kununua kitu unaambiwa Sh.200 au Sh.500, si bure hiyo? Naomba Mheshimiwa hili aliangalie kila akija anapunguza bei mpaka tufikie katika malengo tuliyoyakusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kuhusu halmashauri, ukurasa wa 54. Marekebisho ya Sheria ya Fedha Serikali za Mitaa, Sura Namba 290 kwa kuongeza kifungu cha 37A. Nakubaliana na maelezo ya Mheshimiwa Waziri, ni sahihi kwa sababu hii asilimia 10 inayokwenda kwa vijana na wanawake ilikuwa haina sheria lakini mtakapotungia sheria itakuwa ni lazima itendeke. Kwa hiyo, nawaomba TAMISEMI watengeneze kanuni haraka ili ziweze kutengenezewa sheria ije Bungeni ili tuwe na uhakika kwamba 10% ya vijana na wanawake ipo kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shida tunayoipa mkaona halmashauri hawatoi ni kwa sababu wanaona hawana panapombana ni maelezo tu ya maandishi. Isitoshe halmashauri zinajipangia miradi ambayo haina priority nyingi… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, mengine nitachangia kwa maandishi. Naunga mkono hoja na Mheshimiwa hapa kazi tu, endelea na majukumu yako kama yalivyo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FAKHARIA SHOMARI KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri aliyotoa na ambayo imetoa mwanga kwa Watanzania na wengi walioisikia hotuba yake wanaiunga mkono kama tunavyounga mkono sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua ameweza kufanya hivi kwa sababu ana Mawaziri walio mahiri, ana Manaibu Waziri walio mahiri na watendaji wake katika Wizara yake pia ni watendaji walio bora na waliotukukuka na ndio maana akaweza kufanya kitu kizuri kama hiki. Vilevile sina budi kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wake wa Rais kwa maelekezo yao mema wanayoyatoa na kwa shughuli zao njema za kazi wanazozifanya, inakuwa dira kwa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia huu ukurasa wa 56 unaozungumzia mambo ya afya. Kwa kweli nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pale alipoeleza kwamba vituo vya afya vilikuwepo 7,678 na sana vimefika 8,119. Hili ni jambo jema kwa sababu tunaongeza vituo ili kuwasaidia Watanzania kupata afya bora. Hata hivyo, tukae tukijua kuna vituo vinavyotoa dawa hovyo mitaani pharmacy. Vituo hivi unakwenda unasema unataka dawa au unamwambia nini shida yako unayoumwa na unapewa dawa bila kuangalia una cheti ya Daktari au hauna. Unajua kuna dawa nyingine kama akina panadol unaweza ukapewa, hasa hizi za maumivu, ukaeenda kule kwenye hospital pharmacy zao na unaweza ukapewa bila hata kuwa na cheti, lakini kuna zingine lazima uwe na cheti cha Daktari, sio unakwenda unamwambia naumwa kitu fulani na baadaye anakupa dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapa panataka elimu itolewe, watupe elimu sisi wananchi, wawape elimu na wale wenye vituo, maana wao wanajali fedha kuliko afya ya mtu. Sasa na hivyo tutawapa matatizo Watanzania ambao wengine hawajui, yeye anajua nikienda hospitali itabidi Daktari nimlipe na nani nimlipe, lakini nikienda pharmacy nitanunua dawa tu, wakati dawa atakayonunua siku nyingine haitamtibu, itampa madhara. Sasa hapa kitu kikubwa ni elimu kutolewa kwetu zote na vilevile kufanya ziara mara kwa mara kuvamia hivi vituo ili wapate uhakika wa hao wanayoyatenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna msemo unatumiwa sana, tunaweza au naweza. Huu unamtaka mama mjamzito na baba mwenye mjamzito nyumbani awe anamsaidia mama mjamzito kwenda kliniki na hii lazima pia iwe inapigiwa debe. Mama mjamzito anapokwenda kliniki kupima akienda na baba toka kuanzia mwanzo mpaka atakapojifungua, itasaidia sana baba kujua upungufu wa mama yule. Sasa unaambiwa utumie neno naweza, sasa mnaweza mkikaa baba anasema na mama anasema ili kumfanya kiumbe aliyeko tumboni kupata uhai uliokuwa mwema. Hivyo, hili linataka elimu ili kwa mama inambidi lazima aende lakini kwa baba inakuwa kidogo mbinde kumsindikiza mama, hata handbag yake baba inabidi ambebee maana imeshakuwa mama ana mzigo. Sasa na yeye akienda naye na kambebea ki-handbag chake mapenzi yanazidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija ukurasa wa 29 uzalishaji wa mazoa ya biashara, suala hili nampongeza Mheshimwa Rais kwa ziara yake aliyoifanya juzi Mtwara, kaupata ukweli kuondosha upotoshwaji, maana vyombo vya habari vilikuwa vinasema kwamba watu hawajalipwa, Serikali haijawalipa watu inawasumbua kumbe katikati kuna watu walipita njia za mkato wakazinunua korosho wakajifanya wao ndiyo wenye korosho wakauze Serikali ili wao wapate faida. Baada ya kujulikana Mheshimiwa kawasemehe, kawaambia wapite kwenye sheria, wawaone, wawalipe lakini lisiendee. Namshukuru Rais wangu mweledi, ana ufahamu mpana na anatizama tatizo na akalipatia ufumbuzi ili kuwasaidia Watanzania kuondokana na matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuongelea ukurasa wa 81 kuhusu Muungano. Kwanza niipongeze Serikali ya Muungano na lazima nipongeze kwa kufuta malimbikizo ya deni ya kodi ya VAT yaliyofikia shilingi bilioni 2.8, hili ni jambo jema, hapa ndiyo Muungano tunapouona. Muungano unazungumza pande zote mbili msaidiane, hii ilikuwa si kusaidia ni wajibu wake umefanya kwa sababu ilikuwa kelele ikipigwa muda mrefu, wameliangalia, wakaona tatizo hakuna, ni haki yao na kuweza kulitekeleza. Kwa hili natoa pongezi kwa Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana hili suala likamalizika kwa amani na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sikitiko langu liko mwisho hapa, baadhi ya Ofisi za Muungano Zanzibar zina majengo ya Muungano lakini Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje kuanzia mwaka 1964 hadi leo mwaka 2019 halina jengo lake officially walilojenga, jengo wanalotumia ni nyumba iliyokuwa ya Kiongozi wa Upinzani kabla ya Mapinduzi. Jengo la nyumba ukaligeuza ofisi unatupa pesa zako bure kwa sababu halitokubali. Suala hili nimeshalizungumza mara nyingi, naomba Mheshimiwa Waziri alichukue, tunataka jengo la Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje Zanzibar kama ilivyojenga Muungano, Polisi, Jeshi, Uhamiaji na Wizara nyingine na wao ni Wizara kubwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Fakharia, kengele ya pili.

MHE. FAKHARIA SHOMARI KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza sina budi kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, IGP na Makamishna na hasa Kamishna wangu Mohamed Hassan wa Zanzibar, ambaye hivi karibuni kulitokea tokeo la vikosi kuingiliana katika majukumu ya kazi na wakaweza kulidhibiti na kukaa salama na shwari. Lazima niwapongeze kwa kazi yao nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna msemo watu wanapenda kusema ambao nitausema hapa leo, “domo, nyumba ya maneno.” Sisi watu wa Pwani tunapenda sana kuzungumza. Kuna baadhi ya watu wanapenda kusema mambo mengi wakailaumu Serikali, wakasema ovyo, baadaye wakamtafuta mchawi, kumbe mchawi anakuwa yeye mwenyewe ambaye amejidhuru kwa kauli zake alizozisema na hilo linatendeka humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna msemo mwingine unasema hivi, “kwa shujaa huenda kilio, kwa mwoga huenda kicheko.” Sasa baadhi yetu humu yakija yakiwakuta, wanapiga kelele kumbe amejifanya shujaa, yamemkuta, akina siye tuliokuwa waoga, tunamwangalia tunacheka. Sasa jamani tunapokuwa tunataka kusema mambo, lazima ufikirie kwanza nini athari yake ya mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia kuhusu ujenzi wa nyumba za Askari. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa majeshi hapa Tanzania kwa huruma zake kwa Wizara hii ambapo aliweza kuwapatia shilingi bilioni 6.3 kwa ujenzi wa nyumba 400 za askari, pia mkachagua mikoa minane katika mikoa minane na Zanzibar wakapata Unguja na Kaskazini Pemba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo ni jambo la fahari, la kujivunia, kwa uwezo iliyokuwanao Tanzania na kujali wapiganaji wake. Naomba Wizara pia mjiongeze. Mjipongeze vipi? Kwa sababu tunayo mifuko yetu ya jamii, mngekuwa mnazungumza nayo wakaweza kuwapatieni mkopo wa riba nafuu, mkaweza kujiongeza kwa kuwawezesha kujenga nyumba na katika mikoa mingine pia nao wakapata nyumba, Askari wetu wakajisitiri katika makazi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia Jeshi la Magereza, Mheshimiwa Waziri alizungumzia katika ukurasa 28 na 29, Jeshi la Magereza kubuni ili kuweza kuzalisha chakula na pia kuzalisha mazao ya biashara. Sasa nasema wangejiongeza na wakatafuta na mifugo kwa sababu tayari wanao vijana, wanaingia kwenye magereza yetu hodari, wana nguvu, wana uwezo, ni shabab kabisa, takribani wengi wanakuwa vijana sio wazee. Sasa hawa isiwe kazi yao ni kula na kulala, wawatumie waweze kufanya kazi ili waweze kuzalisha na kuipunguzia mzigo magereza au kuipunguzia mzigo Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija katika mwaka 2017/2018, zilitengwa bilioni 5.8 kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa Ofisi ya Uhamiaji Mikoani, Wilayani vituo na kadhalika. Hata hivyo, hizi pesa hazikutoka, ujenzi haujakamilika, mfano tukienda Lindi na Mtwara, yale majengo hali yake ni mbaya, hayajamalizwa, ile ni hasara kwa pesa za wananchi na ni kodi zao. Kwa sababu ukienda ukiyaona hali ni mbaya na humjui umkamate nani uchawi? Tuwakamate Wizara ya Fedha, tuwakamate Wizara ya Mambo ya Ndani au tuwakamate Magereza, lakini hali ni mbaya na hili jambo lazima walingalie kwa upeo mrefu na liweze kufanyiwa kazi hiyo ya matengenezo ila majengo hayo watu wakae na kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitanzungumzia dawa za kulevya kwa upande wa Zanzibar. Hivi karibu Mheshimiwa Naibu Waziri alikwenda Zanzibar akazungumza na Wanahabari. Nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, kazi aliyoifanya ni nzuri na akagundua udhaifu uliokuwepo na akasema udhaifu ulikuwa kwa viongozi wetu watendaji na kuna maneno alizungumza akasema na itakuwa si mbaya baadaye hili jambo akalizungumza kwa mapana tukaelewa sote kwa sababu wanaopata tabu ni watoto wetu na wanatajirika ambao wanaiharibu nchi kwa kutaka manufaa yao ya kupata hela. Sasa hilo jambo azidi kulisimamia ili huu udhaifu uondoke, kama amegundua kiongozi, basi huyo kiongozi ashughulikiwe au amegundua taasisi, hiyo taasisi ishughulikiwe, lakini hili jambo liweze kuangaliwa kwa mapana na tuweze kupata nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia kuhusu jengo letu au pale Mkoa wa Mjini Magharibi kuna sehemu panaitwa bomani, hilo boma ambalo ndio kambi kubwa ya mwanzo tulikuwa tunaitegemea pale Zanzibar maana ipo kwenye historia, maana hata wakizungumza hayo Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964 lazima boma lile lina historia. Hata limetungiwa nyimbo katika historia, lakini wanaliacha, boma lile majumba ndani hayapo sawa halishughulikiwi, njia zilipo ndani haziko sawa hazishughulikiwi. Utakuta mlango mkubwa kuna askari kasimama analinda. Sasa analinda nini wakati ule uzio wote mbovu, utaingia utatoka askari hana habari, utafanya unalotaka, askari hana habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, naomba safari hii katika bajeti ya maendeleo watakayoomba, kama mwaka huu hawakuomba, wataomba mwakani wangefanya uzio na huo uzio usiwe wa waya, uwe wa matofali. Nasema hivyo kwa sababu pale pamezungukwa na majumba, zamani palikuwa nje ya mji, lakini sasa katikati ya mji, majumba yote yamezunguka, wanalofanya mle ndani mtu wa nje anawaona, sasa hiyo siri hapo iko wapi? Sasa naomba wakapaangalia, ile historia iliyokuwepo mle wakaiweka sawa na wanaijua ili watu waliokuwepo mtaani, au waliokuwa nje au mtu akidhamiria kufanya jambo kidogo apate shida ya kuingia mle ndani, asiingie kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, sina budi kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na taasisi yote ya Wizara yake kwa bajeti nzuri waliyotuletea ambayo inaeleweka na pia Mheshimiwa Waziri jinsi alivyo-present hapa pia unataka kumsikiliza vilevile sina budi kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchagua majembe akayaweka Wizara ya afya yanatufanyia kazi nzuri na tunaridhika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitakuja kwenye ile kinga ya kansa ya kizazi. nakumbuka mwaka jana kulikuwa na kampeni ya watoto wetu wa miaka tisa mpaka miaka kumi na nne ambao hawa wafanyiwe chanjo ile ya kinga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna baadhi mikoa nasikia kuna vijana hawakwenda wazazi wao wamewazuia sijui kama taarifa hiyo mnayo. Na kama mnayo kwanini waliwazuia wakati Serikali ilishagharimika ilishatafuta pesa na hii ni kinga kwa wao wenyewe itakayo wasaidia huko mbele watakapo endelea na maisha yao lakini wakawa hawakuwapeleka ingawa mlitumia shule mkaenda mkafanya hiyo lakini bahati mbaya baadhi ya wazazi waliwazua watoto wao. Sasa tunataka kujua kwa nini ilitokea Hivyo na kama ni kweli nyinyi mnajua na mmechukua hatua gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja nyingine kwenye fistula kwa kina mama suala hili hata mwaka jana lilizungumzwa. Kwa sababu CCBRT wao ndio wanashughulika na suala fistula lakini utakuta kuna watu wapo mikoa tofauti na fistula wanapata. Fistula hachagui ni bahati mbaya tu unaweza ukapata, sasa kwanini hamsomeshi watu wenye fani hii mkawasambaza katika hospitali za mkoa, hospitali za kanda ili wakaweza kuwa mabingwa wa ainai ile mtu likimtokea jambo hili asiweze kuhangaika anajua mimi hiki kimenitokea na madaktari hapa wapo wenyewe wataona na wanaweza wakamtibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Waziri nataka hili mliangalie kama madaktari wa fani hiyo hawana msomeshe ili muweze kupata madaktari waweze kuwatibu wananchi bila matatizo maana kuwa na fistula wakati haja inatoka bila kawaida ni tatizo kwa binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja suala la watoto njiti, mama anapobeba mimba sijui kwa uzoefu anajua kuwa mimi nitazaa njiti au nitazaa mtoto aliyekamika. Sasa ninataka nijue wakati wanapokwenda kliniki mnatoa elimu au na wale madaktari wanakuwa hawajui kama atazaa mtoto njiti? Kwa sababu unapomzaa na baadhi ya hospitali haina vifaa utaambiwa umuweke kufuani, umuwekee tumboni apate joto hilo tatizo. Unajua kama mama wakati mwingine ana joto la kutosha? Mama wengine wapo baridi tu. Sasa kama mkiwa hamjaangalia mkawa mnatoa elimu toka watu wapo kliniki kwamba mtoto njiti yuko hivi mzazi unatakiwa kuwa hivi au unahisi kabla hujazaa uko hivi ili mama anakwenda kuzaa tayari anakuwa na elimu ya kutosha anakuwa hana wasiwasi na hata atakapo mzaa yule mtoto anajua huyu mtoto anajua huyu mtoto nimemzaa wa aina fulani na nitakiwa nimuhudumie vipi ili makuzi yake yawee vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye suala lingine la sober house. Unajua kila siku tunahangaika na vijana wetu wanaokula unga, na hili ni tatizo sugu. Nashukuru Wizara ya Mambo ya Ndani wanavyohangaika nalo, lakini je Wizara ya Afya wamechukua hatua gani? Kwa sababu wanatakiwa lazima kuwa na dawa za kutosha zakuweza kuwatibu hawa vijana wetu. Mambo ya Ndani kazi yake yeye ni kutafuta na kupembua na kukamata lakini wa kutibu ni Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilikuwa naomba Wizara ya Afya mshirikiane na Mambo ya Ndani ili muweze hili jambo kulimaliza, mlimalize kabisa. Kwa sababu watoto wetu wanaumia na wao ndio nguvu kazi bila ya wao wakiwa hawataweza kufanya kazi taifa letu litadolola. Sasa nakuombeni Wizara ya Afya wakati Mambo ya Ndani tayari wanalishughulikia mshirikiane nao kwa kuwaweza kuwatibu wale vijana wetu ambao tayari wameathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, lingine bima ya afya bila ya afya kwa upande wa Zanzibar naomba iboreshwe. Kwa sababu unapokuwa na bima ya afya Zanzibar inabidi uende Vialeni, Globaly, Arhma au Hospitali zilizokuwa chini ya vyombo vya ulinzi kama jeshini au polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwetu kwa upande wa pili ni tatizo kwa sababu tunazo Cortege hospitali kama moja ipo Makunduchi, nyingine ipo Mkwajuni sasa wa Kaskazini watakwenda zoa kule. Wapo watu wanafanya kazi za muungano kuna Wabunge wana familia zoa wanazo bima za afya na wengine kuna polisi kuna wanajeshi wataweza kutumia. Na wa Kusini watakuwa wanakwenda Makunduchi. Lakini sote tunakimbilia mijini huko mjini napo kuna matatizo yake kwa sababu utaambiwa dawa hakuna, hiki hakuna, Na itabidi matatizo. Sasa namuomba Mheshimiwa Waziri najua bima ya afya ipo kwenu mtuboreshee na Zanzibar iweze kuwa na uwezo wa kufanya kazi na uwezo wa kutibu na kila mmoja alidhike na fedha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kama Mbunge nakwenda hospitali naambiwa dawa hakuna nikiitizama bima yangu natakiwa kila kitu niifanyiwe. Lakini hakuna kwa sababu hamjaboresha kule. Wanakwambia hakuna, sasa Naomba muwe mnalingalia suala hili kwa jicho la rehema ili liweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja suala la mwisho, Usambazaji wa dawa za baridi na moto katika Pharmacy zetu. Najua kuna kanuni zinazongumza dawa aina gani ziende zikauzwe mitaani. Lakini naona hizo kanuni hazifuatwi naweza jirani yangu kaenda hospitali katibiwa nami maradhi yale nikaja nikayapata akaniambia nenda dawa fulani mimi nilipewa wakati mie cheti sina nitakwenda pharmacy na pharmacy atanipa ile dawa na siku nyingine dawa ya moto lakini anayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama mtafanya ziara ya kushtukiza mkawa mna kwenda mara kwa mara mnaangalia kwa sababu hii mnasaidia tiba ya raia wenu ambao ndio raia wa Tanzania watakao weza kufanya majukumu yao na kuwaondoshea matatizo katika miili yao na afya zao. Nafikiri hayo naunga mkono hoja mia kwa mia nawapongeza kwa kazi yao nzuri nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na Amiri Jeshi Mkuu wa Jeshi hili na pia sitomsahau Mkuu wa Jeshi la Nyuki Zanzibar ambaye kwa umahiri wa kazi zake anavyozifanya pamoja na viongozi wote wa Jeshi mliokuja hapa Bungeni leo, hongereni kwa Waziri wenu alivyotoa hotuba yake vizuri, hotuba yake ndogo lakini imeeleweka na imefahamika na tumeielewa vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa nataka kuzungumzia nyumba za makazi za wanajeshi Zanzibar. Nyumba ziko chakavu za muda mrefu ukiangalia tuliokuweko Brigedi ya Nyuki pale Zanzibar, tayari ni chakavu za zamani toka Mapinduzi walivyozijenga, ukija Mtoni unakuta hivyo hivyo, ukienda Mwanyanya na kwingine kote, angalau mngezifanyia ukarabati zikaridhisha angalau na wanajeshi wakaweza kukaa pahala wakatulia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiendelea utaangalia kwamba hizo Kambi zenyewe tayari ziko uraiani, ukija Brigedi ya Nyuki imezungukwa mpaka nyuma yake kuna soko, ukija Mwanyanya imezungukwa na raia, ukija Mtoni tena pale ndio imekuwa mashaka maana kuna mtu amejenga ameingia ndani ya Kambi ambaye ni mtu maarufu ambaye tuna wasiwasi mtu maarufu akikaa pahali kama penye Jeshi ni tatizo kwa kweli. Sasa ningeona lazima muweze kujipanga. Sikwambieni muhame kwa sababu nikisema muhame kwa Zanzibar ile mnakwenda wapi, lakini inabidi muweze kutoa elimu ya kutosha kwa wale wanaokaa pale na tuchukulie isije ikatokea kama yale yaliyotokea Mbagala inatakiwa mtoe elimu, muwaeleweshe, muwape mipaka yao wanatakiwa wanafika wapi na wapi ili kuimarisha ulinzi wa Kambi zenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja lingine kuhusu malipo ya fidia ya maeneo yaliyotwaliwa au yaliyochukuliwa na Jeshi, ukurasa wa 30 umeelezea na nimeshukuru kwamba umesema Kigoma kule tayari mmelipa, na kule Lindi tayari mmelipa ambapo hili ni mwanzo mzuri na hayo mengine waliobakia wanadai fidia zao mjitayarishe nao muwalipe kwa sababu mtu akianza uzuri amalizie uzuri na kwa wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali walituarifu kwamba JKT na JKU wataweza kupata ajira ya Jeshi na ninajua hivi karibuni kama nilimsikia Mheshimiwa Rais akilizungumza hilo. Sasa nilikuwa nataka kujua hatua aliyofikia katika ajira hiyo wamefikia hatua gani, tunataka kujua pia na fedha hizo za kuajiri hao vijana wetu wanazo, kwa sababu ukiwaajiri vijana kutoka JKT na JKU unapata vijana wazalendo. Kwa sababu kule Jeshini wanafundishwa somo la uzalendo, ukakamavu na heshima, sasa ukipitia kwenye misingi ya kuwachukua wao unapata watu waliobora na watoweza kuliheshimu Jeshi na kuwaheshimu raia wao na kuheshimu utendaji wao wa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija suala la haki za wastaafu wanaomaliza muda wao wa kazi wanajeshi. Unajua kwa wale waliokuweko Zanzibar wakati wanapomaliza wakistaafu wanapata shida kwenda Bara kufuatilia mafao yao na nilishazungumzia mara nyingi. Kwanza inapendeza unapostaafu unapewa chako kabisa, ki-cheque chako mkononi, unaondoka. Maana hii kumpeleka mara kaenda Bara kufuatilia mara karudi unamtia umaskini, kwa sababu pesa yenyewe hana na kwenda na kurudi unamuongezea umaskini.

Sasa Mheshimiwa Waziri nataka akija aniambie ile Ofisi ya Zanzibar itashughulikia pensheni kwa waliokuweko Zanzibar vipi ipo au itaanzishwa au mnachukua hatua gani au bado waendelee kupata usumbufu na kuhangaika kwenda huku na huku? Ningeomba na hilo nilijue Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja la mwisho mambo ya michezo, michezo ajira, michezo ni afya, michezo maingiliano baina ya upande huu na upande huu na tuna michezo yetu ya aina mbalimbali na ninyi mnao vijana wenu mahiri wa JKT na JKU, kwa nini hao hamuwafanyi ndio vijana wa Taifa? Kwa sababu tayari wana umahiri, mnawafundisha michezo, wana uwezo ili watakapokuwa mkiwapeleka kwenye Kambi zetu za michezo mpira kitaifa, riadha kwenda mbio, hebu liangalieni na hili badala ya kuokota vijana hatukatai vijana mitaani kuwa mnakuwa nao lakini ingekuwa jicho lenu kubwa mnalenga hawa vijana ambao mmewasomesha JKT na JKU. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa hii nafasi adhimu ili nami niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Wakuu. Wizara hii viongozi wa juu wamo Wazanzibari, kwa hiyo, naiangalia kama ni sehemu ya Muungano, naipongeza Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa jinsi alivyowajali Watanzania katika bajeti yake kwa kuwaondolea tozo, ushuru wa forodha na VAT. Hapa tunaiona Serikali inavyowajali raia wake na kuwapunguzia ukali wa maisha katika utendaji na ufanyaji kazi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kutoa misamaha kwa viwanda vyetu vya ndani. Hili ni jambo adhimu na kubwa la kuvisaidia viwanda vyetu vya ndani kupata mapato na kuwezesha Serikali kupata mapato lakini kuwanufaisha Watanzania kwa kuyatumia mapato yao wanayochangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ushuru wa forodha naomba uwakilishi uwe wa pande zote za Tanzania Bara na Tanzania Visiwani. Pia kinachopatikana kiwe ni kwa faida ya pande zote mbili. Kwa kufanya hivyo itasaidia kuonesha jambo hili linafanya kazi kwa mujibu wa makubaliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia taulo za kina mama. Sipingi maelezo yaliyotolewa kwenye kitabu hiki na Mheshimiwa Waziri, yapo sahihi na tunayakubali lakini bado Wizara izidi kuliangalia tena suala hili kwa sababu vijana wetu hawana uwezo. Wizara itafute mbinu ili taulo za watoto ifikie Sh.300 mwisho Sh.500 kwa box ili mtoto aweze kulinunua au hata mzazi maskini aweze kumnunulia mtoto wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, kuna matangazo ya dawa ya mswaki Colgate, wanaambiana vijana/watoto wadogo Sh.300 tu unaweza ukanunua na meno yako yakakaa sawa. Sasa vitu kama hivyo ukiviangalia na ukivisaidia itapendeza na itawasaidia vijana wetu waweze kujikimu lakini maelezo uliyoyatoa nayakubali na hayana matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kulizungumzia suala la Bandari ya Mpiga Duri. Zanzibar inategemea bandari iliyopo Malindi na bandari ile tayari imeshazidiwa maana ni ya toka ukoloni. Sasa hivi tumeamua kuanzisha Bandari ya Mpiga Duri lakini nguvu zetu sisi bado zipo chini ya dhamana na mikono yako Waziri. Naomba hili Waziri uliangalie tena kwa jicho la huruma na imani maana hivi sasa baadhi ya makontena tumeyatoa Malindi kule tumeweka Darajani lakini kwa mazingira haijapendeza na hayajakaa sawa na ile sehemu si nzuri ukiweka makontena maana kuna vijana wanayavamia, wanakwenda kufanya ufuska pale, haipendezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikiwa kwa huruma na busara zako Waziri utaweka mkono na kutufanikisha bandari ile ikaweza kujengwa utakuwa umeisaidia Zanzibar katika uchumi wake. Uchumi wa Zanzibar ukikua tayari Tanzania itafaidika, itakuwa tayari Zanzibar inaweza kujitegemea na Zanzibar ikaweza kutekeleza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenykiti, ahsante. Sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwenye kuumba mbingu na ardhi, vilevile kukushukuru na wewe Mwenyekiti ambaye ndio Naibu Spika na Mheshimiwa Spika na uongozi wote wa Bunge pamoja na Waziri Dkt. Mpango kwa huu Mpango wake uliokuwa mzuri, bora na uliotukuka, pamoja na Chama changu Cha Mapinduzi kilichoniwezesha kufika hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia kidogo ukuaji wa pato la Taifa ambalo limeendelea hadi kufikia 6.9 na vile kufika katika kundi la uchumi wa kati. Kwa kweli ni jambo jema na jambo kama hili linataka kupigiwa upatu kila leo ili wale waliokuwa hawasikii wasikie na wale waliojifanya hawaoni, waone na wajue kwamba tuko vingine sisi Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuelezea pia mkakati uliokuwa umewekwa na Taifa ambao ni mkakati mkubwa, kwa mfano, ujenzi wa reli ya kati kiwango cha standard gauge; mradi wa kufua umeme wa maji; uboreshaji wa mashirika ya ndege; ujenzi wa barabara na madaraja, ni jambo la faraja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna deni kubwa hapa, tuko Dodoma ambapo ndio Makao Makuu ya Nchi, lakini hatuna uwanja wa ndege wa kuridhisha na uwanja wa ndege ndio unaoleta maendeleo ya nchi, Kiwanja kipo miaka 15 nyuma, lakini bado tunang’ang’ana na kiwanja kidogo, kiko katikati ya mitaa ya watu, sasa hili Mheshimiwa Dkt. Mpango aliangalie, nini tatizo wakati hapa ni Makao Makuu ya Mji na mikoa mingi imepakana? Kuna mikoa mingine haina viwanja vya ndege itakuwa rahisi wakitua Dodoma wakaweza kufika katika mikoa yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hilo nataka katika mipango yetu tunayopanga, mpango ni mzuri lakini unakuwa na upungufu mdogo mdogo ambao tuukumbuke ili tuweze kuushughulikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ambaye katika ukurasa wake wa 31 alielezea elimu stadi kazi za ufundi wa vijana wakimaliza elimu waweze kujiajiri; hili nimelikubali mia kwa mia. Elimu yetu kwa kweli tunaosomeshwa school ni ya kukariri ili upate shahada, ukimaliza kama umepata degree umepata Master ndio umemaliza, lakini kama utampa elimu stadi ya ufundi, akimaliza anajua anakwenda kufanya nini. Kijana huyu hata kama atakuwa ni fundi cherehani, lakini anajua nikiondoka nakwenda kufanya kazi fulani, kama nitakwenda kutengeneza baiskeli au kutengeneza magari. Hayo yote tunayafanya mtu aende ajibagize bagize kwenye magari mabovu afundishwe, lakini kama atapata toka school itamsaidia na ajira zitakuwepo, hatutoweza kutegemea ajira ya Serikali kwa sote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale vijana watakaobahatika, watabahatika na tutakaobakia tutafanya kazi zetu wenyewe za kuzalisha mali kwa kufanya kazi nyingine hata kama kutakuwa na viwanda, wakati mtu unampeleka kiwandani, hana stadi ya elimu anaenda kufanya nini? Ina maana itakuwa umempeleka mahali akaanze kufundishwa, ambapo kile atakachofundishwa atakuwa shambaganga tu lakini sio uwezo wa kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye uchumi wa blue, uchumi wa blue ambao tunaiongelea bahari na bahari ina mazao mengi na bahari kuna wazee wetu wanafanya kazi kwa kutumia urithi wa babu, baba na mjomba, lakini haijui vipi bahari ilivyo. Sasa ningeshauri elimu ya bahari ingeanza kufundishwa kuanzia elimu ya msingi mpaka tunamaliza vyuo, unamjua mtoto ushampanga, anaijua bahari ikoje na anajua mazao ya bahari yanapatikana wapi. Sasa Serikali wakati itakapojitahidi kutafuta vifaa na watoto wameshasomeshwa, wanajua nini wanachokifanya, litakuwa ni jambo jema, ina maana tutaitendea haki blue economy na kila mmoja atajua anachokifanya. Ushauri wangu napenda masomo ya uchumi wa bluu wasomeshwe vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na pia kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia na kuipongeza Wizara; Waziri, Naibu Waziri na watendaji wao wote waliokuwepo Bara na Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia magari ya doria ya Polisi pamoja na Magereza na magari yanayochukua mahabusu. Magari ya doria ya Polisi ndiyo kiini kikuu kwa Polisi kuweza kuwakamata au kufuatilia majambazi na aina zote za tatizo litakalotokea katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati Viongozi Wakuu wanapokwenda ziara, magari ya doria ndiyo yanayoshughulikia, lakini Mheshimiwa Waziri alipokuja kuzungumzia hapa ukurasa wake wa 37, kasema anatoa magari tisa na hayo anawapa Magereza kwa ajili ya utawala. Hiyo kweli sikatai, lakini kwanza tutizame katika utendaji. Kamati yetu ilikwenda ziara, tukapewa gari ya doria, kila mkoa tulikuwa tunabadilishiwa na ndiyo utaratibu. Ilikuwa likifika kwenye kilima, gari inatoa moshi utafikiri chetezo. Haliwezi kwenda, halina nguvu. Sasa ina maana hizi gari ni mbovu na haziwezi kukidhi mahitaji. Unamfukuza jambazi kwa gari kama hiyo utampata? Humpati. Sasa kwa vyovyote mjitahidi baada ya gari kutumia ninyi utawala au viongozi, mtafute gari za doria kwa ajili ya maskari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukichukua Magereza wakati mahabusu wako Magereza, tatizo linakuwepo hapo, hawapelekwi Mahakamani kwa wakati, maana hakuna gari na Magereza yapo mbali na Mahakama. Ina maana tunawapa tatizo wafungwa wale walioko ndani au mahabusu kuweza kufika kwa wakati Mahakamani. Namwomba Mheshimiwa Waziri aangalie, magari ndiyo uti wa mgongo katika kazi zao, maana bila hayo magari hao Polisi hawataweza kufanya kazi zao kwa ufasaha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija na ajenda ya pili, nataka kuzungumzia kwa upande wa Zanzibar kidogo. Zanzibar kuna kituo kinaitwa Ng’ambo Police Station. Nakumbuka wakati mimi mdogo ndiyo kwanza nazaliwa, bibi yangu nilimsikia anakiita kibiriti ngoma, ambalo ndilo jina la awali, baadaye likabadilishwa, likawa Ng’ambo. Kituo kile kiko katikati ya mji pale Mkoa wa Mjini Wilaya ya Mjini, ambapo kipo katika katika Jimbo la Mheshimiwa Abdulwakil. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la kushangaza, kituo kile hakina uzio na kituo cha mwanzo kikubwa kile; hicho Madema kimefuatia baadaye, lakini kituo kile ndiyo kilikuwa kituo mama na kimezungukwa na barabara. Unaweza kupita ukakuta ndani kuna kuku anaranda, mara ndani kaingia mbuzi anaranda. Sasa Polisi na hivyo vitu vinaendaje? Unaweza ukapita ukaona kinachofanyika ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale pale pana kituo kingine tu cha Serikali wamejengea uzio wa matofali. Sasa na nyie naomba kile kituo kwa sehemu kilipokuwepo kipate uzio wa matofali ili kiweze kujisitiri, baadaye na kile kituo mtaweza kukikarabati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiendelea, kuna tatizo hili la Magereza. Magereza wanapokea mahabusu, lakini mahabusu wanaopokea wengine na kwa wale wakimbizi ambao wamechukuliwa kama 100 au 50. Sasa baada ya kupelekwa Mahakamani inabidi warejeshwe mahabusu. Wanaporudi mahabusu kwa kweli tunawaonea wale Jeshi la Magereza. Mnawapeleka, wale hawako kwenye bajeti, hawana chakula na wale wako wengi, mnategemea kule Magereza watakula nini? Ina maana sasa wajibane.

Mheshimiwa Spika, Magereza itafute mbinu wewe Polisi umekamata, kazi yako imekwisha; Mahakama kuhukumu, kazi yake imekwisha; lakini wakati mwingine hukumu inatoka inabidi watolewe wale na wakitolewa inatoka faini ili watoke, lakini ile faini haiendi Magereza, inakwenda Serikalini. Sasa yeye ile bajeti yake ya chakula aliyoitumia akiwalisha wale itakuwaje? Mngefanya basi wakati wao wanapita njia za panya nanyi mkawakamata, basi wajilishe, japo ni mahabusu wajilishe wenyewe, lakini uzito huo msiwape Jeshi la Magereza ambao wanapata usumbufu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukija kwenye zimamoto, nawapongeza. Wana club ambayo wanafundisha katika katika school za sekondari jinsi ya kuzima moto ili ukitokea moto waweze kujihami wenyewe, lakini wanakwenda kidogo kidogo. Maana toka wameanza, ndiyo kwanza sekondari 10. Nawaomba wajitahidi wafanye kila mkoa angalau sekondari tatu, nne na siku hizi majanga ya moto kwa mashule yako mengi, halafu tena kama wao watakuwa hawafanyi hii club, siyo vibaya kuwa na club, lakini wafanye haraka ili zisambae kwa Tanzania nzima, vijana wetu wawe na weledi wa kuweza kuhami moto kabla haujawaathiri.

Mheshimiwa Spika, nikija kwa Polisi wastaafu, hawa kila siku wanaongeza ingawa suala hili mama kaligusia jana, lakini kwa nini hawafanyi wakati mtu unamjua tarehe fulani anastaafu. Kwa nini hawamfanyii ili akiondoka pale, aende na cheque yake, unajua umemtumia toka kijana, ujana wake kamalizia pale mpaka anakuwa mtu mzima, leo unamtoa haki yake humpi na nina hakika kwa viongozi wa juu, wakiondoka wanaondoka na cheque zao au wanaondoka pesa imeshaingia kwenye akaunti, lakini hawa wanyonge ndio wanaowahangaisha.

Mheshimiwa Spika, sasa hawa wanyonge wajaribu kuwapa, ikiwa wanatoa cheki au cash, tena wanawapingia tunajua tarehe fulani mwaka fulani, fulani atastaafu, anajijua mimi naondoka pale naagwa na changu tayari, la sivyo tutakuta wanapata malazi ya pressure, wanakufa mapema, ameshazoea kutumia, ana familia wanawaangaliaje, ina maana kila siku wawafuate, bora wampe chake. Nalishukuru Bunge, unaondoka, unaondoka na chako, tena mwenyewe utajijua. Kwa hilo Bunge halina mjadala. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Fakharia.

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, Ahsante naunga mkono hoja.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwanza sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa alivyowasilisha vizuri taarifa yake, vilevile kuwapongeza walinzi wetu wote waliokuwepo hapa jinsi walivyokuja na tulivyowaona na jinsi wanavyohamasisha wanapokuwepo kwenye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kidogo nilikuwa nataka kuzungumza makazi ya wanajeshi wetu waliokuwepo pale Mererani wanaolinda Tanzanite. Kwa kweli Kamati ilipokwenda hali tuliyoikuta pale ilikuwa siyo nzuri, maana kwa maneno ya mjini utasema hali ya full suit, makazi yao juu bati, kuta bati, sasa kwenye joto, kwenye baridi wanapata shida. (Makofi)

Sasa tungeomba wawaboreshewe yale makazi kwa sababu askari wetu wasikivu wakakamavu wanatufanyia kazi nzuri basi na makazi yao japo nyumba mbili, tatu pale zijengwe za za kudumu waweze kufanya kazi zao kwa uweledi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia tena JKT; kuhusu ujuzi, kazi ya JKT kumfanya kijana awe mkakamavu, kijana awe mzalendo, lakini vilevile kuwafanya vijana wetu wakiondoka wawe na ujuzi, mnaweza kumfanya fundi cherehani, fundi makenika, fundi ujenzi, fundi mchundo, lakini akiondoka pale tayari anakwenda mitaani ana ufundi wake mwenyewe wa kwenda kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ningependa kuwaongezea lingine, mngekuwa mnatoa elimu ya Muungano, vijana wetu akitoka pale tayari anakuwa anajua nini chimbuko la Muungano. Akifika pale anatoka anajua nini faida ya Muungano, sasa hilo mkilifundisha ninyi kule na vijana wetu wengi mnawachukua litasaidia. Hii kuzungumza nitaienzi, nitaitukuza itakuwa rahisi kule ameshapata elimu ya kutosha. Sasa ningewaomba katika masomo yenu mnayotoa chimbuko la Muungano lazima liwemo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie lingine kuhusu Ofisi ya Wizara ya Ulinzi - Zanzibar. Ofisi za Muungano ipo ni moja tu, Ofisi ya Makamu wa Rais na ipo nyingine Mambo ya Nje, lakini zote haziridhishi, kwa sababu ya Makamu wa Rais imo ndani ya makazi yake, kule haipendezi kuwekwa ofisi. Kule kuna makazi ya Makamu, ofisi lingejengwa jengo moja kama la ghorofa au jengo la chini, ikawepo Wizara ya Ulinzi, Mambo ya Ndani, Muungano, Mambo ya Nje na taasisi zote za Muungano zikawepo pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu kama anashida ya jambo la Muungano anajua nakwenda sehemu fulani nitaikuta ofisi na nitamaliza mambo yangu. Mtu anastaafu aende Bara, mtu ana matatizo yake katika Wizara ya Muungano aende Bara, kwa kweli haipendezi, na hata ninyi mkija Zanzibar mtafikia rest house, hotelini au kambini, pia haipendezi. (Makofi)

Sasa ningeomba mkashirikiana na mkajenga jengo moja tukasema hili jengo la Muungano, mtu anashida anakwenda pale Wizara zote atazikuta pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka sehemu nyingine stahili za likizo za wanajeshi. Toka mwaka 2011 mpaka 2020 wanajeshi hawajapata stahili zao za likizo na hasa wale wanyonge, wanadai shilingi bilioni 114 kama sikosei. (Makofi)

Sasa na hili mliangalie, mwanajeshi hawezi kusema hana wa kumsemea, atanung’unika pembeni na hastahiki kunung’unika. Sasa kama hatukuwasemea mtu haki yake apewe. Hata mama mwenyewe analipigia kelele hili watu wenye stahili zao walipwe, sasa ningekuona na hili ukaliangalia kwa jicho la huruma na kwa jicho la imani vipi mtawasaidia wanajeshi wetu waendelee kufanya vizuri ingawa wanafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja la mwisho, Hospitali ya Jeshi iliyokuwepo Zanzibar Bububu, hospitali nzuri inafanyakazi vizuri, lakini tungeomba kizuri lazima na kingine uongeze. Mngetuongezea nyingine kama Mkoa wa Kusini mkatufanyia kama ile iliyokuwepo Bububu au moja mkapeleka Pemba kama iliyokuwepo ili tunajua kwa sababu unapotaka upate matibabu mazuri ukikimbilia jeshini, jeshini hambagui, hambagui kitu, yoyote atakayekuja mnamtibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hasa ningeona hili mliangalie kwa sababu pale pana vifaa vya kileo, pana madaktari wazuri, kuna kila sifa mnayo, mtu uzuri wake aambiwe, lakini tunataka kama itakupendeza au itawezekana mtutafutie na nyingine ikiwa mtaweka Mkoa wa Kaskazini maana hii ipo Mkoa wa Mjini Magharibi. Kama mtatuwekea Kaskazini au Kusini na nyingine Pemba kama mtaweka Kaskazini au Kusini ili kila zikiwa zipo nyingi na mambo yetu yanakuwa mazuri na ninyi kama mnapata thawabu kwa Allah. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kwa haya machache naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza sina budi kukushuru wewe kwa kunipatia hii nafasi, pia na kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wao wote wa Bara na Zanzibar kwa kazi nzuri wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nataka kuzungumzia hii diplomasia ya uchumi. Diplomasia ya uchumi ni wazo zuri walilotoa Wizara ya Mambo ya Nje ili kuisaidia nchi kukua kiuchumi. Lakini lengo walilolifanya bado halijafikia. Kwa sabababu lengo lilikuwa kutafuta masoko, masoko bado kitendawili, hamna masoko na hayo masoko, ilikuwa sisi kama Watanzania, tuweze kusarifu bidhaa zetu ziweze kwenda kuuzwa nje, ina maana bidhaa ziwe value added na hayo hatujayaweza kwa sababu hatuna viwanda. Sasa utakuta bado sera ya diplomasia haijakamata kasi.

Vilevile hii sera ilikuwa ihamasishe watalii ambao wana uwezo wa kuja Tanzania. Tanzania ni nchi nzuri, Tanzania Bara kuna Mlima Kilimanjaro, mbuga za wanyama nzuri. Ukija Zanzibar kuna fukwe mwanana, kuna bustani ndani ya bahari ambavyo hivyo ni vitu vya maajabu. Lakini kwa sababu hii sera bado haijafanya kazi kikamilifu haya yote hayajaweza kufanyiwa au kutendeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli ukiangalia ilikuwa Wizara itoe sera mpya ya mambo ya nchi za nje na ilikuwa hii Juni, 2021 wawe nayo mkononi. Haijapatikana hadi leo na hatukui itapatikana lini. Sasa hii sera mpya ya mambo ya nje ingeshirikiana na diplomasia ya uchumi ina maana tayari tungekuwa tumejua nini tunachokifanya kwa sababu sera ilikuwa idhibiti diasporas wafanyiwe kanzidata ili tujue kila nchi tuna nani na nani wako vipi, lakini tumeshindwa. Balozi zetu kuwadhibiti wanashindwa na ilikuwa hawa diasporas ambao ilikuwa wao washirikiane na Mabalozi wetu, wawe muda mwingi kwa mazingira ya raha na shida wanakua nazo, lakini halitendeki.

Mheshimiwa Spika, utakuta tunawafanyakazi raia wa Tanzania nchi za nje wanapata manyanyaso, wanaharibikiwa, lakini wanashindwa kwenda ubalozi kutokana na sera hakuna inayowafanya wafike ofisi zetu za ubalozi. Sasa hili itabidi wazidi kuliangalia kwa mapana ili waweze kujua kwamba hawa vijana wetu wa Tanzania waliokuwepo nje ya Tanzania nao pia wanataka kusaidiwa. Tazama vijana wetu wale wanaofanya kazi majumbani nchi za nje wanavyonyanyaswa. Mtu anafika ananyang’anywa passport yake, mtu anafika halipwi, aende wapi? Hana pa kwenda, lakini kama hiyo sera mtakapokuwa mmeifanya na mkampa nguvu, atakuwa anakwenda kifua mbele hana matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuja uhaba wa wafanyakazi; Wizara ina uhaba wa wafanyakazi kutoka Makao Makuu, Kurugenzi ya Zanzibar na Balozi zetu. Hata wewe mwenyewe umelizungumza hilo ingawa unalifanyia kazi. Lakini kwa nini mkawa na uhaba wa wafanyakazi ndiyo unaosababisha majukumu yenu yote mshindwe kuyatekeleza kwa sababu mna desk zina majukumu, lakini hazina wafanyakazi. Makaimu ndiyo mmekuwa nao wengi, sasa ina maana hayo mnayoyapanga yatakuwa? Hayawezi kuwa, tatizo lenu ni uhaba wa wafanyakazi, uhaba wa vitendeakazi, hivi sasa hivi magari hakuna ya kutosha na kazi zenu zinahitaji gari, maana mnafuatilia.

Mheshimiwa Spika, ukija Zanzibar hawana gari, ukija Bara Makao Makuu hakuna gari, Balozi zetu hazina gari, sasa hilo pia tatizo. Najua kwa bajeti hii ndiyo mmeshachelewa, hakuna kitakacho. Lakini bajeti ya mwakani mkija haya angalau mawili/matatu mtuletee tuyapitishe angalau tuone yanafanya kazi na hayo ndiyo yatakayowasaidia na ninyi wakati mkishakuwa na sera mpya, ita-guide mambo yenu yote na mtajua ninyi mnafanya na mtafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuja na suala dogo la mwisho; najua mimi nikizungumzia Zanzibar na Muungano tu, tuna miaka 57, lazima nilizungumze na nyumbani. Zanzibar mnayo ofisi, lakini ile sio ofisi ni nyumba, ile imekaa kama rest house. Lakini pale kwenye ofisi yenu mliyosema ofisi, nafasi mnayo ya kutosha. Pale mngejenga kiofisi chenu ambapo mtaa mliokuweko mzuri Maisara, nyumba kuna ofisi za SMZ nzuri, ubavuni nzuri, pembeni nzuri na ninyi mngeteremsha kiofisi chenu pale na nafasi mnayo. Mkawa na rest house ambayo mmeifanya ofisi.

Siku moja mimi nilialikwa kwenye mkutano pale Mambo ya Nje, nimeenda sijui hata niingilie mlango gani. Nimeingia pale nimejikuta niko juu. Mkutano kumbe, daah naambiwa jamani mkutano naambiwa uko chini. Nipenye wapi nitoke huko chini kwenye mkutano kwa sababu ile nyumba mtu alijenga mwenyewe anavyotaka, haikujengwa kiofisi. Sasa inabidi hata utakapokuwa unakwenda kwa shughuli za Kiserikali, inabidi uhangaike. Nafasi tunayo na tutaweza. Ninajua Waziri akiwa mwanamke anakuwa msikivu na ninajua hili japo ofisi ndogo pale kaweke, unaweka alama alikaa Waziri mwanamke kafanya kitu fulani, hiki hapa kinaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafikiri kwa hayo machache naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mama Samia ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Alhaj Hussein Mwinyi - Rais wa Zanzibar, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu ambaye tayari ameweka hotuba yake ya bajeti mezani na Watendaji wake, pamoja na Mheshimiwa Spika na Naibu Spika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na TASAF. TASAF imefanyakazi nzuri kwa Zanzibar, kwanza nitaizungumzia Unguja kwa sababu mimi ndiyo niliko TASAF kuna Shehia 126 zote zimefanya kazi nzuri wameweza kutoa ruzuku vizuri, wametoa ruzuku za vijana au watoto waliokuwa chini ya umri wa miaka 18 ambao wazee wao hawajiwezi, wametoa ruzuku kwa watoto wa chini ya miaka mitano kwenda kliniki, wametoa ruzuku kwa watoto wa kimaskini ambao wanaosoma Sekondari na Primary, wamewasaidia walemavu kwa ruzuku, wamewasaidia hata wajasiriamali, TASAF kwa Zanzibar tunaishukuru Serikali ya Muungano imesaidia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile imechukua vijana wanaofanyakazi ofisi ya Makamu wa Rais Zanzibar ambao ndiyo wanasimamia TASAF wamewapeleka masomoni ili kwenda kuongeza ujuzi waweze kusimamia mazingira ya TASAF. Jambo likiwa nzuri likinafanywa na Serikali ya Muungano ikishirikiana na Serikali ya Zanzibar inabidi kulishukuru na kuliangalia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba itakapokuja TASAF nyingine ya nne ifanyekazi vizuri zaidi ya hii iliyofanya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja na changamoto za Muungano ambazo Mheshimiwa Waziri Mkuu ziko kwenye ukurasa wake wa 72. Kwanza Muungano ni tunu kwa Tanzania na Muungano wetu unaendelea vizuri, lakini kwenye changamoto walituambia kwamba 11 tayari zimefanyiwa kazi na zishamalizika kabisa na Serikali zote mbili hoja hizo Tisa tayari wamekubaliana kwa kuandikiana na tayari zimeisha. Mbili ziko katika utendaji lakini mimi bado naona hakuna tunalolifanya kwanini niulize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hizi Wabunge tuliopo humu ndani msimamishe mmoja tumuulize hakuna hata atakayeelezea nini na nini kimetendeka na kwa sababu gani, baada ya kuisha kuzifanya au kutanzuliwa zimo katika makaratasi au mafaili, hazijasambazwa kama kutengenezewa vipeperushi au kutengenezewa vitabu au kwenda ofisini kwa viongozi wakati unamsubiri kiongozi ukakuta juu ya meza yake pale vipo ukawa unasoma au mashuleni mwetu, kwa sababu kuna vijana humu siyo wazalendo hizi changamoto kila siku wanazirejea hizo hizo kwa sababu hawazijui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakuta kila siku bandarini gari yangu imekamatwa kwa sababu hatuelewi nini kinachoendelea, sasa ninaomba Ofisi ya Waziri Mkuu changamoto zote ambazo mlikubaliana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ziweze kuwekwa bayana kila mmoja azijue, vijana waliopo vijiweni, vijana waliopo shuleni, na vijana ambao watatumia hizi changamoto wakati wakitaka manufaa yao kuzorotesha au kufarakisha nchi anatumia hizi changamoto. Mheshimiwa Waziri Mkuu tuwe waungwana kwa kuweza kuzisambaza kila mmoja azipate. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la ukurasa wa 44 na 45 unazungumzia viwanja vya ndege na usafiri wa anga. Suala hili ni zuri na amesema ndege zetu zitatimia 16 ni jambo jema lakini kuna kitu kidogo ningeomba kiangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua hizi ndege zina route na route zake mpaka Zanzibar zinafika lakini mkae mkijua Zanzibar kuna Wabunge, wafanyabiashara, wafanyakazi wa Serikali na Wafanyakazi wa Chama wanakuja direct Dodoma. Sasa wakati mtu unataka kuja Dodoma kwa ndege lazima ukasubiri ndege Dar es Salaam ndiyo ufike Dodoma. Kwa nini route moja tusiifanye kwenye wiki direct Zanzibar to Dodoma unaitoa Dar, Dar inakuja Zanzibar, Zanzibar to Dodoma au unaitoa Mkoa wowote…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Fakharia Shomari. Ahsante muda wako umekwisha.

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Ahsante naunga mkono hoja na mimi nilikuwa nishamaliza.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante. Kwanza sina budi kuzipongeza Kamati zote zilivyowasilishwa hapo, zimewasilisha vizuri. Vilevile nipongeze na Vikosi vyetu vya Ulinzi ambavyo vinafanya kazi nzuri ya kulinda raia wake waliyokuwepo nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongelee Magereza kuhusiana na parole. Parole ilikuwa nia yake kupunguza msongamano uliokuwepo Magerezani. Sheria ni nzuri, lakini wanashindwa kufikia mwisho na kwa nini wanashindwa kufikia mwisho na magereza yetu yanakuwa na msongamano wa wafungwa? Ni kwa sababu Bodi inakaa inaangalia, inafanya tathmini inamwona huyu raia alivyo anastahiki kuwa huru, lakini raia yule hawezi kuwa huru kwa sababu sheria inazungumza kwamba lazima mhusika wa kesi ile aliyomshtaki yule mtu aridhike na yeye, kwa sababu yeye ndiye aliyemshtaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa pili wa ubinadamu mtu ameshakaa Gerezani muda mrefu, Bodi wameunda kisheria na huyu mtu ameshaangaliwa anafaa kutoka, anachukuliwa mtu wa mtaani kwa sababu ndiye aliyemshtaki anakuwa mtu yule ana roho mbaya, siku nyingine anaichukia familia ya yule mtu anakataa, akikataa hawezi kutoka. Sasa hii sheria inafanya kazi gani? Hii sheria wailete tuibadishe au mhusika anayekuwa na ile kesi Bodi wanapokaa wamwalike, ili kama kuna hoja zitoke kule, hawawezi kumfanya yule mtu anakubali mwenzie atoke kutokana na hoja zilizokuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama hii sheria haijaletwa, ikafanyiwa marekebisho kipengele baada ya kipengele, msongamano wawafungwa Magerezani utakuwa unaendelea. Hili lingine nataka nilizungumze kwamba hivi sasa Bodi ya Parole haina Mwenyekiti na pia si mbaya mkaliangalia na hilo ikapata Mwenyekiti, Bodi ikaweza kutimia na ikafanya kazi kihalali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja na hii diplomasia ya kiuchumi. Diplomasia ya Kiuchumi kwa Tanzania itatusaidia sana, lakini tuishinikize Wizara ile Sera ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje itoke, kwa sababu ile sera ndiyo itazidi kuiboresha hii diplomasia ya kiuchumi kwa sababu kuna mambo mengi humo yanataka kuangaliwa. Tunataka kuangalia the diaspora, tunataka kuangalia Wawekezaji wetu watafanya kazi vipi? Tunataka kuona Wizara za Kisekta ambazo nazo zinataka kuchangia ingawa Wizara inasema wanashirikiana na Wizara za Kisekta, lakini mwamko hatuoni. Watakapotoa sera kutakuwa na kanuni, wataweza kuzibana hata hizi Wizara za Kisekta ziweze kufanya kazi na zikiweza kufanya kazi tutajua kwamba hii Sheria itaweza kufanya kazi na diplomasia ya kiuchumi itaweza kunyanyuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile bila kuwepo sera na kanuni na elimu mikoa yetu haitoweza kufanya kazi kwa sababu jambo lolote literemke chini kwenye mikoa na wilaya lakini hawajui kinachoendelea na hawajui kinachoendelea kwa sababu sera bado haijajipanua, ingawa Wizara wanasema kwamba iko njiani wakati wowote itatolewa. Tungeomba itoke tupate na kanuni ili iweze kufanya kazi na hizi shughuli za kidiplomasia za kiuchumi, tuweze kufanya wafanyabiashara, wawekezaji, wakulima wajue mipaka yao vipi watafanya kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja katika hili la wahamiaji haramu nchini. Hili kweli suala zito, hili suala pia tunaongeza msongamano Magereza kwa sababu watu wanatoka nchi nje anaingia ndani Tanzania, anazamia, anakuja tuseme kaja kisheria au kaja kinyume na kisheria, anazamia humu, wanawakamata wanawapeleka Magerezani Serikali ndiyo inaingia gharama, lakini kuna mtazamo Wizara ya Mambo ya Ndani ambao wanauangalia kwamba wanataka wafanye sasa hivi wanaingia kama wameingia kisheria, wanawagongea wapite waende zao itakuwa nzuri au hawakuja kisheria wanaambiwa arejee tena kwao lakini hapa Tanzania asikae kutuongezea msongamano Magerezani, kuwalisha Magerezani, mtu kakaa akiondoka kama alikuja na lilishe duni anaondoka ametengemaa hapa Tanzania. Sasa hata na hilo tunaona liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naweza kuzungumzia kidogo tu fedha za maendeleo. Jamani Wizara ya Fedha vioneni vikosi, fedha ya maendeleo hamuwatilii na barua za kuomba wanakuleteeni na barua wakileta, hii tunaingia quarter ya mwisho, kesho kutwa quarter ya mwisho, unampa pesa mwisho aifanye nini? Wakati ilikuwa kuna quarter ya kwanza, ya pili, ya tatu, hata yale malengo yalikuwa kayapangia hayawezi kufanikiwa. Sasa hebu watazameni jamani, kwani Vikosi vimekosa nini Hata hamuwapi? Naomba hili suala jamani tuliangalie, Vikosi wanatusaidia, wanatulinda na ndiyo watu wetu wa karibu katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, sina budi kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wake wote. Nashukuru mama hakufanya kosa kwa kumchagua Waziri Masauni katika nafasi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka kuzungumizia fire hydrants. Unajua hata kipindi kile nilizungumza kuhusu fire hydrant, kwa sababu zimamoto na uokozi huwa tunawalaumu kwamba wanakwenda na maji yanakuwa madogo, maji yanakwisha wakati wa kuzima moto, lakini wanapokuwa na fire hydrants watakuwa wanajua mimi nakwenda kufanya kazi yangu pale na nikiimaliza maji yamekwisha sehemu fulani mimi naweza kupata maji nikamaliza majukumu yangu. lakini hali halisi haipo hivyo, kwanza kwenye fire hydrants zote mamlaka anayemiliki ni Mamlaka ya Maji siyo Zimamoto. Sasa kwa vyovyote kitu ambacho hakipo kwenye mamlaka yako kwa kukitegemea inakuwa ni shida.

Mheshimiwa Spika, naomba Mamlaka ya Maji ikazifanyia ukarabati na ikazitafuta fire hydrants popote zilipo wakaweza kushirikiana na Zimamoto ili wawakabidhi Zimamoto kwani wao ndiyo watendaji wa shughuli ya kuzima moto. Wao wenyewe watazishughulikia na zitakuwa chini ya mamlaka yao na watajua mipaka yao wanafanya kazi nazo vipi, lakini zikibaki kwenye Mamlaka ya Maji wao kule hawana habari nazo, hawazijali, ina maana tutapiga kelele siku zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka kuzungumzia na Bodi ya Parole. Bodi ya Parole kweli ni nzuri inafanya kazi na mikoa. Katika mwaka 2021/2022 walipewa shilingi 134,000,000 wakafanyia kazi lakini ni ndogo. Katika mwaka huo 2022/2023 wamepewa shilingi 324,000,000 pia ni ndogo kwa kufanyia kazi, maana yake ina-combine mikoa yote waliyokuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, la msingi ni elimu. Parole hawajatoa elimu kwa jamii. Kwa sababu, wale wafungwa wa Parole, baadaye wanapokuwa wametumikia kule na Bodi ikakaa ikasema sasa hivi hawa watu tayari wamejitathmini, wako vizuri, wame-behave kule ndani tuwatoe, tatizo linalotokea hapo, lazima wakaulize kwenye mitaa walipokuwa, kwenye familia au kwenye jamii na ile jamii ikifuatwa haikubali. Isipokubali, haki za binadamu ziko wapi hapo? Kwa sababu mtu ameshaonekana tayari anastahiki, aweze kutoka na pia ni kuwapunguzia Magereza kuwa na msongamano wa watu Magerezani wakati tayari wale watu muda wao kwa mujibu wa Parole umemalizika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawaomba Bodi ya Parole kutoa elimu kwa jamii na isitoshe kama Sheria ina upungufu ndani yake na watuletee hapa tuje tuirekebishe, lakini hawa wafungwa waweze kupata amani.

Mheshimiwa Spika, niseme kidogo kuhusu wimbi la wahamiaji haramu. Wahamiaji haramu kwa kweli ni matatizo, wanapita kila mikoa kwa njia za panya kuingia, inawezekana wakapita njia, inawezekana wakaja wakahamia. Ni tatizo kwa sababu, tunapowaona tunawakamata tunawapeleka Mahakamani, wanakwenda Magereza. Tunampa mzigo Magereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi sasa anao wahamiaji haramu kama 5,679 katika hao, wako mafungu matatu; wako bado wanaotumikia vifungo, wako ambao ni mahabusu na wako ambao tayari wameshamaliza vifungo vyao, lakini hawatoki. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu pamoja na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa Hotuba yake nzuri, ilikuwa ndefu lakini tumemwelewa dhima na dhamira yake aliyoikusudia kwa Tanzania na kwa Bunge zima. Vile vile sina budi kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Mama Samia, kwa kazi nzuri anayoifanya kwa kuiletea maendeleo Tanzania pamoja na Mheshimiwa Hussein Mwinyi Rais wa Zanzibar, kwa kazi nzuri kwa kushirikiana bega kwa bega na Mama Samia, kwa kuifanyia kazi Tanzania na Zanzibar kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 27, Serikali ilizungumzia jinsi Mahakama zetu zilivyoongeza watendaji ambao Majaji wa Mahakama ya Rufaa, Mahakimu na baadhi ya viongozi wengine kwa kuweza kufanya kazi kwa weledi katika Mahakama zetu, lakini kwa kweli utendaji bado uko chini, siyo wa kiwango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameongezwa lakini kazi iko vile vile as usual, kwa sababu umewekwa pale kama Hakimu, wamewekwa pale kama Majaji Wakuu lakini kazi wanazozifanya na watendaji wao haziridhishi raia, raia bado wanapiga kelele, Mahakama hazitendi haki, mahakama zinakawia kufanya shughuli zake na mwisho hata hayo magereza yetu pia yameambukizwa kwamba nayo yanafanya kazi chini ya kiwango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija ukurasa wa 86, hii ambayo inazungumzia shughuli za Muungano, imesema kwamba kulinda, kuenzi na kudumisha Muungano wetu. Hili ni kusudio kubwa kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikishirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Nasema hivyo kwa sababu nilimwona Mama, Mheshimiwa Dkt. Samia kipindi kile alichopewa pesa za UVIKO, alikasimu akaleta Zanzibar na huu ndiyo mtazamo mwema wa Muuungano kwa sababu zilikuja Zanzibar zimetenda kazi katika Sekta za Jamii, Sekta za Afya, Sekta za Elimu na Sekta za Maji. Sasa hapa moja kwa moja unaona kwamba Muungano wetu unafanya kazi pande zote mbili. Kinachopatikana huku na huku kinapelekwa, Mwenyezi Mungu ambariki Mheshimiwa Rais, wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri ya jinsi anavyotuangalia raia yake kwa pande zote mbili za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja katika ukurasa wa 84, unaozungumzia ukatili wa watoto. Mheshimiwa Waziri Mkuu, alisema kwamba kuna mikoa nane ambayo imeunda Madawati ya Ulinzi na Usalama ambayo madawati hayo yako 1,993. Nasema hivi, haya madawati ni kidogo kwa mikoa nane madawati yawe kwa Tanzania nzima, hali imebadilika sasa hivi Tanzania, tunasikia mambo yanavyokwenda, tunasikia watoto wetu wanavyodhalilika, tunasikia watu wanavyopenyapenya wa kutaka jinsia moja, sasa hii dawati ikiwepo itatoa elimu nzuri na watoto watakuwa rahisi kwenda kuwa–face kule na kuweza kuzungumza. Nasema hivi kwa sababu tatizo lililopo sasa hivi ulezi tumeuachia Serikali, wenyewe wazazi kila mmoja yuko busy anatafuta maisha na kwa vyovyote Serikali haiwezi kulea mtoto, mtoto alelewe na wazazi wake kwa kushirikiana na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar na Tanzania Bara zote zinahitaji kuangaliwa kwa jicho pana, kwa sababu hili jambo lipo sehemu zote za Tanzania na tunatakiwa tuungane ili kulipiga vita. Unajua ushoga si jambo zuri, bora akuharibikie mtoto mwanamke unajua ataolewa, atastirika, lakini akikuharibikia mtoto mwanaume kwishinei, kaisha, hawezi kitu. Taifa litakuwa limeharibikiwa, mzazi kaharibikiwa na yeye mwenyewe kaharibikiwa, ina maana hawa madada poa na makaka poa Tanzania wawe hawana nafasi. Maana kama hatukukazana hii aibu haitokuwa kwa yule mtendwa na mtenda, itakuwa aibu kwa Taifa letu. Tupige kelele, tupaze sauti, twende na sheria, tuwe na uwajibikaji kwa vitendo Serikali tuwajibike kwa vitendo siyo kupiga kelele, tukipiga kelele hili jambo mtu anaona ahaa si wanasema tu, lakini kama tutakuja kwa vitendo hili jambo litakoma. Tanzania bila ya ushoga inawezekana, tujikaze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija ukurasa wa 83 haya ya 199, hili linazungumzia kuhusu sheria ziwe za Kiswahili, tuzitafsiri, siyo mbaya kwa sababu hii itatatua migogoro kwa wananchi. Baadhi ya wananchi hawazifahamu hizi sheria kwa Kiingereza na hili si gumu kwa sababu wenzetu Baraza la Wawakilishi Zanzibar wanalifanya. Ya Kiingereza iwepo na ya Kiswahili iwepo na nashukuru Dkt. Samia Hassan Suhuhu, kalibariki hili lifanyike na katika maelezo ya Waziri Mkuu kalisema, sasa naomba hili jambo lifanyike ili nasi ile dhamira iliyokuwa imekusudiwa itekelezwe na mambo yetu yote waweze kukaa sawa na tuweze kufanikiwa. (MakofI)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya na uzima kusimama mbele ya Bunge lako tukufu. Vilevile nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa usomaji wake mzuri pamoja na Mheshimiwa Zahor pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Ulinzi na viongozi waliokuja wastaafu wa ulinzi na viongozi wanaoendelea na majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sina budi kwanza kuishukuru Wizara na SUMA - JKT kwa ujenzi wa Ikulu yetu nzuri, ya kileo ya kufahari, kwa pesa za kodi za Watanzania. Jengo linapendeza na wamelijenga kizalendo, lazima tuwapongeze. Mtu akifanya kitu kizuri ana haki ya kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia ujenzi wa hanga la kuegesha ndege za jeshi. Kwa kweli walipewa Shilingi bilioni 11 na walitakiwa wajenge Dar es Salaam, Dodoma, pamoja na Chato Mkoa wa Geita. Wamejitahidi na kampuni iliyopewa M/S Simba Limited imefanya kazi nzuri. Tumekwenda kulitembelea la Dodoma liko katika hali nzuri na hata Kamati imeeleza hapo mbele kwamba wamejitahidi na lazima na wao pia kampuni ipongezwe na Wizara tuipongeze kwa kusimamia. Ingawa walianza mwaka 2021 wakatakiwa kumaliza mwanzoni mwa 2023, lakini hawajachelewa, kazi imekamilika, hongereni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuja kwenye suala la ukusanyaji wa maduhuli. Ukusanyaji wa maduhuli kwa kweli kidogo wameshuka, lakini siyo sana na ilikuwa Ngome - Fungu 38, JKT - Fungu 39 pamoja na Wizara - Fungu 57 kwa pamoja zipatikane Shilingi bilioni 87.6, lakini kwa kweli hawakufikia lengo. Wamefikia Shilingi bilioni 85.1. Siyo mbaya, lakini hawakufika lengo.

Mheshimiwa Spika, kimsingi labda tuangalie pesa walizokuwa wakilipwa na Wizara ya Fedha zilikuwa chache tuseme ikawa ndiyo sababu, kwa sababu na Wizara ya Fedha safari hii imewabinya. Maombi ya fedha walizokuwa wakiwapa siyo waliyoomba. Wanasahau kama hiki ni chombo cha ulinzi, kinahitaji pesa. Usalama wetu na ulinzi wa mipaka yetu iko chini ya dhamana yao, na mtu hawezi kufanya kazi kama hana pesa. Sasa Waziri wa Fedha hili awe analiangalia. Makisio ya ulinzi yawe hayapungui, yanapelekwa kama wanavyoomba na matokeo yake tunayaona kwa sababu wanajeshi wetu ni wazalendo, wanafanya kazi zinavyopangwa kwa mujibu wa taarifa wanazozileta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu sera ya ulinzi wa Taifa (defense policy). Hii sera bado haijafanya kazi kwa sababu hatuoni hizo missions na visions zao walizozipanga na wanashindwa kutokana na kwamba hii sera haijatolewa tukajua. Unajua tu kwamba wameambiwa wafanye siku nyingi toka Bunge la Tisa. Wanasema hivi, Serikali ya Zanzibar bado haijatoa maoni yake, wadau; lakini Serikali ya Mapinduzi Zanzibar tayari ilishatoa maoni na wadau tayari walishatoa maoni. Sasa kinachochelewesha nini hii sera haifanyi kazi? Bila ya sera huwezi kufanya kazi. Sera ndiyo itakayokupa mwongozo ukaweza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri atuambie amekwama wapi? Kuna tatizo gani? Hii sera hadi hii leo mambo yote umeshapata, majukumu itakuwa yote umeshapata, kwa nini mpaka hii leo haijafanya kazi? Tunaomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja utuambie umekwama wapi? Kama utataka upate msaada kwenye Kamati au kwenye Serikali tutajua vipi tunakuisaidia Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazungumzia kwamba Wizara iongeze kasi ya utekelezaji wa mkakati na kupata hatimiliki za maeneo. Unajua maeneo ya jeshi kwa sasa na tunakoelekea siyo makubwa ya hivyo, yanahitaji kuongezwa, na nafasi hamna kwa sababu mshabanwa na wananchi wamejenga mpaka karibu na kambi. Mliambiwa mkae na Wizara ya ardhi ili mweze kuelewana, vipi mtaondoa, vipi mtapima, kwa sababu kuna kambi nyingine mpaka hii leo hazina hatimiliki.

Mheshimiwa Spika, ingawa leo wamezungumza hapa kwamba Kambi ya Chukwani tumeshalipwa, lakini ziko nyingi tu. Kuna Mtoni, kuna Ubago, zipo nyingi tu ambapo bado nina hakika hazina hatimiliki. Hiyo ni kwa upande wa Zanzibar. Sikwambii kwa upande wa Pemba, sikwambii kwa upande wa Mikoani. Naomba hili Mheshimiwa Waziri mliangalie mweze kujua kwamba ni vipi mtaweza kuvuka ili tusigombane na wananchi, tusigombane na Taifa na mweze kuwa na makambi yenu ambayo mnayamiliki na yawe hayana matatizo.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kweli, sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha leo kusimama mbele ya Bunge hili na kuweza kuichangia Wizara hii. Sina budi kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri aliyoifanya pamoja na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu na wote wa Wizara yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu, kwa kazi zake nzuri. Ameiweka Tanzania katika ramani iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi pia, kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Zanzibar, Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kazi yake nzuri anayoifanya Zanzibar na tunajiringia Wazanzibari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka niipongeze Wizara kwa pesa walizozipata safari hii, Shilingi bilioni 17.8 ambazo ni fedha za maendeleo. Wizara hii inakwama, kwani kwa miaka mitatu mfululizo pesa za maendeleo wanazopatiwa ni ndogo; na hiyo ndogo wanayopewa, pia haifanyi kazi. Wanaweza wakapewa robo yake, hata nusu haifiki. Sasa tunalaumu kwamba balozi zetu hazijengwi, vitega uchumi havijengwi, na mambo mengi tu kwamba Wizara hii haiwezi kutekeleza. Tatizo siyo Wizara, tatizo pesa za kutekeleza miradi ambayo wanajipangia, hawapewi kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naiomba Wizara ya Fedha itupie jicho Wizara hii ya kimataifa. Wizara hii ni jicho, Wizara hii inafika mbali, Wizara hii ina mambo mengi. Sasa hii Wizara tuiangalie, pesa wanazotengewa wapewe kwa mujibu wa taratibu, waweze kujenga vitega uchumi katika balozi zetu ambapo tunakwenda kwenye Sera ya Uchumi wa Diplomasia. Bila mtu kumpa pesa, hataweza kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija na suala la Makao Makuu ya Mahakama ya Afrika, ya Haki za Binadamu, ambayo ilikuwa ijengwe kipindi kirefu; ina maana kuna miaka 16 mfululizo toka tumeridhia hatujafanya chochote. Tumeridhia, tumekubali, lakini hakuna kilichokuwa. Sasa tunajiuliza, tunakwenda kwenye diplomasia ya kiuchumi, ni ambayo ni ya kubana matumizi! Kwa sababu, hatuwapi pesa. Mtu haumpi pesa, hawezi kutekeleza. Tanzania tunaiweka katika picha gani au ramani gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeahidi nyie kujenga. Miaka 16 hatujajenga, tunailaumu Wizara! Hatuilaumu Wizara, tunalaumu hawapewi fedha kulifanya hili tukio walilotakiwa wafanye. Nashukuru safari hii angalau wametengewa Shilingi bilioni 5.4, naiomba Wizara iweke alama, ifanye kitu na kazi iendelee na waweze kujenga. Isiwe sababu hampati pesa. Pesa mmeshapewa, mnatakiwa muanze jukumu la kujenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija na hii Royal Tour. Mheshimiwa Dkt. Samia aliondoka ofisini kwake, akatembea kwenye mbuga na nyika; kwenye vielelezo vyote vya utalii; na akafanya kuipaisha Tanzania katika ramani ya utalii, lakini watalii wanakuja kwa wingi Zanzibar, wanakuja kwa wingi Tanzania Bara, na wanaotakiwa wafanye kazi kubwa ya kuhamasisha ni Wizara hii. Sasa na mtu hawezi kuhamasisha kitu kama hana pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narejea pale pale. Kazi ya mama haikuwa ya bure, kazi ya mama kajituma, inatakiwa ienziwe. Tumuenzi Mheshimiwa Dkt. Samia kwa kazi yake nzuri aliyoifanya ambayo inatuletea mapato Tanzania. Sasa ili Wizara iweze kutekeleza majukumu yake, lazima iwe na pesa za kutosha za kufanya kazi zake. Nampa pongezi Mheshimiwa Dkt. Samia Hassan Suluhu kwa ari yake, kwa kubuni hii ziara akaweza kuipaisha Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sera ya Mambo ya Nchi za Nje, kwanza naiomba Wizara, muda ulikuwa mrefu na ninategemea hii 2023/2024 inawezekana sera hii ikatoka maana iko katika hatua za mwisho za utendaji kutokana na maelezo yako Mheshimiwa Waziri. Nami naunga mkono itoke, aweke alama kwamba kile kitu umekisimamia na kimekuwa na kimetoka. Kwa sababu hii pia ndiyo itakayotusaidia katika diplomaisa ya uchumi, au diaspora, hii ndiyo itakayoleta ari na mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu hili suala la uraia pacha kwa Tanzania bado mapema. Tuikamate hii hii hadhi maalum. Hadhi maalum unapata kila kitu; tatizo liko wapi? Kwa sababu unatambulika, familia inakujua, Taifa linakujua, nyumbani wanakujua; tunataka nini tena? Kwanza hata ukisema unataka uraia pacha itakusiadia nini? Muhimu ujulikane kwenu na ufanye mambo ya kisheria ya kwenu, na sheria inakutambua kwenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri aendelee na mchakato wake. Sera inatoka na hadhi maalum inatoka zinakwenda sambamba, Tanzania oyee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, diplomasia ya uchumi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa, maana yake kengele imelia, malizia hiyo moja.

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika diplomasia ya uchumi – nazungumza dogo tu – kwamba sekta mtambuka za Tanzania zishirikiane na mambo ya nje zitoe elimu kwa wananchi, kama biashara, sehemu za masoko, investment, kwa sababu kuna watu hawaielewi, wanakosa kujua maadili ya hilo jambo linavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza sina budin kumshukuru Mwenyezi Mungu aza wajaalah kwa kunijalia uhai na uzima na leo kuwa mbele ya Bunge hili. Vilevile kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu pamoja na watendaji wao wote wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa nataka nizungumzie kidogo kuhusu hii Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ishirikiane na Wizara ya Utalii wakati sisi tuna Balozi ambao Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje waweze kufanikisha kuleta watalii kwa wingi Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi aliyoifanya Mheshimiwa Mama Samia, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutembelea vivutio vyote vya kiutalii vya Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar hii kazi iwe sio ya bure, ametengeneza filamu ya royal tour na ile filamu inatakiwa itekelezwe na watekelezaji wetu ni mabalozi wetu kwa kuweza kutuletea watalii kwa wingi, kazi ya mama isiwe ya bure iwe kazi ya mama inafaa, yeye kaona maono kutuanzisha sisi nini tufanye. Sasa suala hili Wizara mlikamate, mshirikiane na mabalozi kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia suala la Sera ya Mambo ya Nchi za Nje. Mheshimiwa Waziri ameeleza uzuri katika ukurasa wake wa saba na tunashukuru kwamba, ilikuwa siku nyingi imekaa kwa sababu, hii sera ndio itazidi kuwa chachu ya diplomasia ya kiuchumi. Kwa sababu sera ikifanya kazi sambamba na diplomasia ya kiuchumi ikaenda pamoja ina maana wakulima, wafanyabiashara, bidhaa zetu zinatoka mashambani, usafirishaji wa bidhaa pamoja na masoko ya nje yataweza kupatikana na tutanufaika na tutaondokana na umasikini. Nafikiri na hilo mliangalie, lakini kuliangalia vipi, mtoe elimu kwa wafanyabiashara, mtoe elimu kwa wakulima maana maparachichi yanalimwa, tunalima vitu vingi Tanzania na vina soko nje, lakini bila kumpa mtu elimu atalima na kisha yatajaa Kariakoo tele yamerundikwa pale chini, bila ya kufanya kazi hataweza kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni ukarabati wa Balozi zetu. Balozi zetu kwa kweli kuzikarabati kama Wizara si rahisi maana yake nyingi chakavu, kwingine hakuna, kwingine hazikaliki, nyumba za mabalozi, nyumba za wafanyakazi na ofisi za ubalozi, lakini jambo lililokuwepo tunaweza tukafanya awamu kwa awamu na tukazishirikisha taasisi za kiuchumi na wanakubali. Kama kuna sheria inapinga leteni Bungeni, tuleteeni ushauri ili hizi ofisi, itakuwa kila siku tunaimba, tunasema, tunapiga kelele, utekelezaji hauonekani. Sasa tubuni mbinu, mbuni mbinu, ili hizi balozi ziweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu mfano mimi nilikwenda ziara Congo, Kinshasa, tumeona nyumba ya Balozi haina hadhi ya kibalozi. Ofisi yao haina hadhi, ingawa zimekarabatiwa, lakini itakuwa ndio hapo kwa hapo tu, lakini wamejiongeza kwa sababu ule mtaa waliokuwepo Mtaa wa Gombe, prime area na nafasi wanayo kubwa ambayo plot yao nafikiri namba 912 tatizo lililokuwepo walivyojiongeza, makisio wamefanya tayari, lakini hata wakifanya makisio wakati Wizara hamjawapelekea pesa wafanye nini? Hawawezi kufika kokote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na wametuonesha hilo jumba wanalotaka, maana yake la kiuchumi, mtakuwa na ofisi, nyumba, watakodisha watapata wao na itanufaika Tanzania na sifa itakuja Tanzania. Sasa hizi hii awamu kwa awamu lazima hizi ofisi muwe mnaziangalia ili Tanzania nayo iwe katika maajabu katika mabalozi yao. Sio niwe Tanzania Balozi inaonekana ya kizamani, hilo halipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi jumuiya ya kikanda na masoko; hii Mheshimiwa tulipewa semina sisi hivi juzi tukaelezewa kwa kweli, mafanikio tumeyaona, lakini nawaomba hii semina wapewe na Wabunge wote kwa sababu kila mmoja akipata kwa sababu sasa hivi uzalishaji mzuri tu, masoko yako na isitoshe njia zi wazi, Tanzania tunauza sana, lakini watu hawajui. Elimu itolewe na Wabunge pia wafanyiwe semina ili na wao wawe ni mabalozi watakaotoka nje ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
The Fire and Rescue Force (Amendment) Bill, 2021
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri, kuipongeza Kamati ya NUU kwa ushirikiano wao mzuri wakaweza kuufanya Muswada huu wa Sheria wa Jeshi la Zimamoto na Uokozi leo kuingia ukumbini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia Ibara ya 6(3)(b), kinazungumzia fire hydrants. Kwa kweli, jeshi limejipanga na mitaani tayari fire hydrants zipo, lakini haziwezi kuonekana na kwa bahati mbaya ziko katika mitaa ambayo wanaishi watu au wananchi wetu, lakini na ndimo mnamopatikana na majanga ya moto. Sasa kuwepo sehemu hizo siyo tatizo.

Mheshimiwa Spika, tatizo lililokuwepo hapa kuna sheria inaweza ikaja ikawazonga wakazi wa pale wakati watakapoharibu miundombinu hiyo. Wakati miundombinu ile ipo wao hawaijui wala hawaifahamu ina maana uharibifu utatokea.

Mheshimiwa Spika, sasa nilikuwa naliomba Jeshi la Zimamoto waanze kutoa elimu waweze kutembelea kila sehemu zilizokuwa na Fire Hydrant zao ili watoe mwongozo na maelekezo na waambiwe kwamba Sheria tayari ipo na adhabu itatolewa wao waliokuwepo kwenye mitaa waweze kulinda kwa sababu wakati ninapokwenda pale linapotokea janga la Moto fire zinapokwenda wanapoanza kuushambulia ule moto maji yakiisha ndio wanatumia maji yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa na pale ikiwa yale maji au mtu katoka na kioski chake kajenga pale kwenye Fire Hydrant wao watafika pale hawaoni kitu. Na kama pale hawaioni wanajua ipo mtu kaweka kioski chake watampa adhabu kumbe yule mtu kwa bahati mbaya hajui, hajapata elimu hajaelezwa. Kwa upande wangu ningependa hilo watoe elimu ili watu wazingatia elimu na wajue kwamba nitakapokwenda kinyume na hili adhabu itaniandama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazungumzia Ibara ya 5 kifungu cha 11(a) Ibara ya 5 ambayo inazungumzia kwamba Jeshi la zimamoto sasa hivi inatakiwa wawe na Silaha wawe na Amari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa vyovyote ni haki yao kwa sasa kwa hali ya nchi inavyokwenda na upanuzi wa mitaa na miji. Wakati wanapokwenda kuzima moto, majanga ya moto yanapotokea kila mtu pale anakuwa na utashi wake wengine wanakwenda kuangalia, wengine wanakwenda kusaidia, wengine wanakwenda kwa kuiba na pale tuseme wao wanashughulikia kuzima moto huku watu wanashughulikia kuiba au wakati mwingine maji yamewaishia wanakwenda kwenye fire hydrant huku watu tayari wanaanza kuwashambulia. Sasa kwa vyovyote lazima wawe na kitu cha kuwalinda na pale hawalindwi wao tu kuna miundombinu yao wanawalinda na raia na mali zao kwa sababu nao watakuwepo.

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine polisi wanawahi, wakati mwingine polisi wanakawia kufika lakini wao watakuwa tayari wapo wanaushambulia ule moto pamoja na kulinda mali za Serikali pamoja na kulinda na mali za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hii kujihami inawezekana hata wanapokuwa maofisini, unajua siku hizi anaweza akatokea mtu akaja akawaingilia tu ofisini kwao bila ya kutegemea anajua humu ndani kazi yao kulinda maji tu lakini anajua hapa nikiingia kwenye kikosi nikifanya fujo naweza kushughulikiwa wakati wowote kwa sababu wao tayari ni jeshi kamili wanastahili kuwa na silaha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia Ibara ya 9, Ibara ya 9 inayopendekeza marekebisho ya kifungu cha 22 nakubaliana nao na maelezo yao kwamba lazima nyumba zinazoanzia ghorofa ya tatu kwenda na kuendelea ziwe tayari na sehemu ya zima moto, ziweze kujiwekea kinga yao na hata hizi nyumba nyingine za chini vile vile zitakuwa na utaratibu lazima lakini elimu ipite, waelekezwe wafahamishwe ili wajue kwamba hii ukiwa nayo itakusaidia wewe mwenyewe kama kinga yako ya kuweza kujikinga na madhara ya moto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nilikuwa nataka kuzungumzia kwamba kuna nyumba kuanzia ghorofa ya tatu mpaka kwenda juu kuendelea ambazo zilijengwa zamani hawa watakuwa vitu hivyo wengine hawana sasa wasiwachukulie kwenye sheria haraka haraka lazima wafanya utafiti wayapitia yale majengo wakawape elimu ili na wao hata kama wao walijenga zamani kwenye hii Sheria na wao itawagusa kama watakuwa vifaa hivyo hawana lakini wasiwachukuliwa sasa hivi Sheria imeshapita wao majengo yao hayana wakaweza kuwapa adhabu hilo litakuwa halipo sahihi kwa upande wao.

Mheshimwa Spika, na isitoshe kuna nyumba nyingine za ghorofa zipo sehemu za mitaani miundombinu yake ya tabu hata kama litatokea janga la moto kufika tabu tena isiwe kuwa ndio sababu kwanini nyumba yako umeharibu na nyumba nyingine, wakati yeye alijenga zamani na yeye alipojenga hakuelewa nini kitafanyika halafu ikawa limetokea lililotokea kwa bahati mbaya mkamtia adhabu, lazima haya yaangaliwe na tuweze tuyafuatilia sisi kama Jeshi la Zimamoto na tuweze kulitekeleza kabla ya kumpa mtu adhabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafikiria kwa haya machache ahsante sana. (Makofi)