Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Eng. Stella Martin Manyanya (221 total)

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri sana yameniridhisha sana, lakini pamoja na hayo nina maswali mawili ya nyongeza. Serikali mwaka juzi ilitangaza kwamba itaweka vyuo vya VETA kwenye Wilaya zote nchi, lakini itaanza na Wilaya 10 ambapo Wilaya ya Chunya ni mojawapo naishukuru sana Serikali kwa kuiweka Chunya katika moja ya Wilaya 10 za kuweka Vyuo vya VETA.
Mheshimiwa Spika, bahati nzuri sana tena Wilaya ya Chunya inagawanyika kuwa Wilaya mbili, Wilaya ya Chunya na Wilaya ya Mkwajuni Wilaya ya Songwe ambako sasa ndiyo kuna heka kumi zimetengwa za kujenga Chuo cha VETA. Sasa swali, kama Serikali ilisema inaipa Chunya Chuo cha VETA, Chunya imegawanyika ziko Wilaya mbili siyo bora tu zote Wilaya zote mbili Chunya na Songwe zipate Chuo cha VETA? Hilo la kwanza na naona Mheshimiwa Mulugo ambaye ni wa Wilaya ya Songwe amefurahi sana. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, la pili, pale kwenye kambi ya ujenzi wa barabara ya Mbeya - Chunya kwa kiwango cha lami Serikali imesema majengo yale ni ya muda siyo ya kudumu. Je, kwa kuwa, eneo lililotengwa ni heka 25 haiwezi ikaanzia kwa majengo hayo ambayo siyo ya kudumu lakini ikajenga Chuo cha VETA kwa eneo kubwa ambalo limebaki?
NAIBU WAZIRI ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimwa Spika, ahsante sana. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mwambalaswa Mbunge wa Lupa kwa jinsi ambavyo amelifuatilia sana jambo hili. Pia niseme tu kwamba, kwa mujibu wa sera tuliyojipangia na mpango tuliojipangia Wizara yetu imedhamiria kuanza kujenga Vyuo vya VETA katika Wilaya zote ambazo hazina kabisa Chuo chochote cha Ufundi au VETA kwa ujumla. Kwa hali hiyo, kwa sababu ya bajeti ambayo kimsingi inahitajika katika maeneo mengi siyo rahisi kuvijenga vyuo vyote kwa siku moja.
Mheshimiwa Spika, nikuombe Mheshimiwa Mbunge kushirikiana Halmashauri yako hilo eneo ambalo umeliangalia ni vema likatengwa na likapimwa na hati zake zikawasilishwa katika Wizara yetu ili liwe katika mpango.
Mheshimiwa Spika, pia nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote, Wizara yangu inapata tatizo kubwa sana inapofikia kuanza mipango ya maandalizi ya ujenzi wa vyuo hivyo kutokana na ardhi hizo kutokupatikana na kupimwa, ni vema Halmashauri zote ambazo ziko katika mpango huu zihakikishe zinatenga maeneo hayo ili isiwe ni kikwazo tunapofikia kufanya hivyo.
Mheshimiwa Spika, pili, nadhani nimejibu yote kwa pamoja kama ambavyo nimeelekeza kwamba ukishapima tutafanya hivyo kwa kuwa sasa Wilaya ya Songwe inajitegemea, lakini itakuwa ni baada ya kumaliza zile ambazo tumeanza nazo. Ahsante sana.
MHE. RASHID ALI ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Baada ya majibu hayo, nitakuwa na swali moja tu la nyongeza

Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na malalamiko makubwa sana hasa kwa baadhi ya wanafunzi wenye familia masikini na wenye sifa za kupata mkopo huo, lakini wameshindwa kupata mikopo hiyo na kuendelea na masomo yao jambo ambalo linawadhoofisha wanafunzi wenyewe, lakini pia, linadhoofisha familia zao na Taifa kwa ujumla. Mheshimiwa Naibu Waziri anawaeleza nini wananchi kuhusiana na madai haya?
NAIBU WAZIRI ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni kweli kabisa mikopo inayotolewa kwa sasa haiwezishi kuwapa wanafunzi wote wakiwemo watoto wa masikini. Hiyo ni kutokana na uhalisia kwamba nchi yetu inayo mahitaji mengi katika sekta mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nachukue nafasi hii pia kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutambua tatizo hilo. Katika mwaka huu wa fedha tulikuwa na bajeti ya shilingi bilioni 306 tu, lakini baada ya kuingia kwake madarakani ameweza kuongeza shilingi 132, 299,067,500/= ambazo zimewezesha sasa kuwapa mikopo wanafunzi ambao walikuwa wanaendelea na wale ambao wanaanza mwaka wa kwanza. Mpaka sasa, jumla ya wanafunzi takribani 121,000 watafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge kwa kutumia nafasi yetu hii ambayo sisi ndio tunaopitisha bajeti, nawaomba wakati wa bajeti ukifika tulipe kipaumbele eneo hili. Ahsante sana.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini ningependa kuuliza swali la nyongeza lenye sehemu (a) na (b).

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa tufahamu wazi kwamba Serikali sasa hivi imeamua kutoa elimu ya bure, lakini hata hivyo haikujipanga nayo. Naweza nikatoa ushahidi katika hili kwa sababu katika Jimbo la Ndanda kuna shule inaitwa Liloya, wamepelekewa pale shilingi 86,000/=. Hii ni shule yenye idadi ya wanafunzi 600, na hiyo ni sawasawa na shilingi 146/= kwa kila mwanafunzi kwa mwezi mmoja. (Makofi)

Je, Serikali haikuona kwamba jambo hili ingeliacha kwanza mpaka pale itakapokaa Bunge la Bajeti na kupitisha bajeti ambayo itakidhi mahitaji ya wakati badala ya kukurupuka kufanya jambo ambalo haijajipanganalo? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili la msingi niliuliza kwamba lini Serikali itakuwa tayari kupeleka ruzuku katika Chuo cha Ufundi Ndanda ili kiweze kudahili wanafunzi wengi zaidi kwa sababu kile ni Chuo kilicho bora kuliko vyuo vyote vya Serikali vinavyotoa elimu ya ufundi vilivyopo katika Mkoa wa Mtwara na Lindi? Naomba kuwasilisha maswali yangu.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, naomba nijibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali haijakurupuka. Haijakurupuka kwa sababu Serikali hii ndiyo inayoishi na wananchi na kufahamu matatizo yao. Ndiyo inayofahamu hali halisi ya mazingira tuliyonayo na ndiyo maana ikajiwekea mpango kupitia Ilani yake ya Uchaguzi wa CCM kwamba itatoa elimu bure kuanzia Chekechea mpaka kidato cha nne. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hali hiyo basi, kama ambavyo tumejionea katika mipango mingine tuliyokuwa tumeianza, ikiwemo na Mipango ya MMEM, Mipango ya MMES na mipango katika sekta nyingine, kila wakati tumekuwa tukianza na tunaboresha kadiri tunavyoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hali hiyo, kama ambavyo nimesema, kimsingi tunafahamu hata baadhi ya shule, tulipowaambia walete idadi ya wanafunzi pamoja na mahitaji kulingana na uhalisia, kuna wengine walileta sawa, kuna wengine hawakuleta vizuri. Pamoja na hayo, tumeshadhamiria kuona ni namna gani tunaendelea kufanya uchambuzi na kuboresha kadiri itakavyowezekana.

Hivyo tunasema kwamba katika majukumu yale yanayoihusu Serikali kwa sababu elimu inaendeshwa kwa ubia baina ya Serikali na wananchi; wazazi kwa ujumla, kwa hali hiyo, katika yale majukumu yote ambayo tumejipangia, tutahakikisha Serikali inatimiza wajibu wake. Huo ndiyo msimamo wa Serikali yangu. Katika swali la pili…
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Najibu swali la nyongeza la pili. Katika swali la nyongeza la pili la Mheshimiwa Cecil, kimsingi swali la mwanzo ulikuwa unahitaji ujenzi wa Chuo na sasa hivi umezungumzia juu ya utoaji wa ruzuku.

Kwa sasa hivi bado hatujafikiria kutoa ruzuku katika Chuo hicho ambacho kipo Ndanda. Hata hivyo, ni suala la kuangalia, kama kuna uwezekano na itaonekana lina faida kufanya hivyo, basi tutazidi kushauriana na kuona suala hilo linaweza likafanyika.

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pia nishukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali wawili ya nyongeza.
La kwanza, nasikitika kwamba swali langu halijajibiwa, suala la Chuo cha VETA Kagera limezungumziwa muda mrefu sana humu ndani na nje ya humu ndani. Mkoa wa Kagera mzima hauna Chuo cha VETA cha hadhi ya Mkoa. Kwa hiyo, vijana wote wanaomaliza kidato cha nne au darasa la saba hawana fursa ya kupata mafunzo ya ufundi kuweza kujisitiri kwenye maisha yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, waliaminishwa kwamba chuo hiki kingejengwa mwaka jana, tukatoa ardhi na mipango mingine ikaendelea na Waziri amefika pale mara mbili, tatu, ameangalia na kusema kwamba ujenzi unaanza, lakini hadi leo kwenye majibu tuliyopewa hapa hakuna matumaini hata kidogo chuo hiki kuanza kujengwa wakati wowote. Kwa hiyo swali langu halijajibiwa, ningependa kujua ni lini hasa kinakwenda kujengwa? Hilo ni la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tupo humu ndani kwa ajili ya Bajeti ya mwaka ujao, ningependa kujua ni kiasi gani kimeombwa kwenye Bajeti hii kwa ajili ya chuo hicho, hayo mambo ya barabara , miundombinu, michoro na chuo chenyewe, ni kiasi gani kimeombwa kwenye Bajeti hii kwa ajili ya Chuo hicho? Asante sana.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niungane na Mheshimiwa Jasson Samson Rweikiza kwa jitihada kubwa ambazo anazifanya juu ya chuo hiki, nami naona umuhimu wa chuo hiki katika Mkoa wa Kagera.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli anaweza kusema kwamba hatujajibu swali lake kwa sababu yeye anataka ni lini, lakini ujenzi wa chuo unaanza baada ya kupitia hatua mbalimbali na baadhi ya hatua zilizopitiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba eneo litakalojengwa chuo hicho limepimwa na ndiyo maana Serikali tayari imeshatoa fedha. Vilevile kushirikisha wadau wengine na baada ya kukamilika jitihada hizo, ndipo sasa tunaweza tukasema tukishakuwa na fedha tuanze kujenga.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu uzito juu ya chuo hicho lakini kimsingi niseme tu kwamba kwa sababu tulishapata hali ya mwelekeo ya baadhi ya wadau kutaka kukisaidia chuo hicho ndiyo tumekuwa tukiendelea nao na mazungumzo yeye mwenyewe ni shahidi, walishawahi kutembelea mpaka huko Kagera. Kwa hiyo naomba tu kwa sababu amekuwa na imani nasi atuamini na ajue kwamba muda wowote tutampa taarifa kadri tunavyoendelea na jitihada za ujenzi wa Chuo hicho.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante, tatizo la watoto au wanachuo wanaohitimu elimu ya diploma au stashahada ni kubwa mno. Haya mambo hayakuanza leo, toka mwaka 2007 wanafunzi wa Vyuo Vikuu kwa Taasisi ya TAHLISO wanadai hili suala halipo vizuri sana.
Kwanza vyuo vyenyewe vinapomaliza muda wake, muda wa kuhitimu masomo unakwepana na muda wa kusajili. Wanafunzi wanapopata ile wanaita supplimentary, kiswahili sijui; lakini na hawa wanachelewa kufanya mitihani yao kujiunga nao chuo. Sasa kama kweli majibu haya yako sahihi, kwanini bado wanapata matatizo haya?
Swali la pili, tatizo hili la kudahili wanafunzi wa diploma, wanapata shida sana kupata mikopo yao kwa maana vyuo vyao vinachelewa sana kupata vile vyeti na wao watu wa Bodi ya Mikopo hawapokei transcript ya mwanafunzi wa diploma. Sasa tunauliza, kwa kutumia hii Taasisi ya Elimu na kwa umaarufu wa Waziri, ndugu yangu Mheshimiwa Ndalichako na kwa kutumia ma-engineer…
NAIBU SPIKA: Naomba uulize swali Mheshimiwa.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Naam!
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la msingi ni kwamba naomba wanafunzi wanaomaliza stashahada wapewe nafasi ya kupata mikopo ya elimu ya juu, nalo ni tatizo. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni kweli kwa siku za nyuma kulikuwa na usumbufu kidogo ambao ulikuwa unajitokeza hususan kwa hawa wanafunzi ambao wanamaliza stashahada. Tatizo ambalo lilikuwa likijitokeza ni kwamba kwa upande wa wale ambao ni wanafunzi kwa mfano form six, wao matokeo yao yanakuwa moja kwa moja yanapitia Baraza la Mitihani ambalo ni moja, lakini kwa upande wa vyuo kumekuwa na utaratibu kati ya chuo na chuo kiasi kwamba baadhi ya vyuo vikuu vimekuwa haviamini kwa uharaka kwamba matokeo tunayoletewa ni sahihi. Kwa hiyo, walikuwa wanatafuta namna ya kufuatilia zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukaa pamoja na kuelezana uhalisia na kwa sababu matokeo hayo ya vyuo vilevile yanaenda kuhifadhiwa katika Hazina data za NACTE, kwa misingi hiyo hakuna huo usumbufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali hiyo, napenda nitoe agizo kwa vyuo vyote kwamba hakuna sababu ya kufanya usumbufu kwa wanafunzi hao ikizingatiwa kwamba matokeo yao yapo na yanaongea moja kwa moja na system ambayo inafanya shughuli ya udahili.
Kwa upande wa suala la udahili wa Stashahada kusababisha wanafunzi kushindwa kuingia katika nafasi za mikopo, kwasababu suala hili linalohusiana na mfumo, ni vyema tulichukue tuendelee kulifanyia kazi na hivyo tutashirikaiana na wewe mwenyewe Mheshimiwa Mbunge kupitia Kamati. Ahsante

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu wangu wa Elimu, ningependa kuchangia kidogo tu katika suala hili.
Kwanza napenda kutoa ufafanuzi kwamba mwanafunzi ambaye ana supplementary bado hajamaliza chuo. Mwanafunzi anakuwa amemaliza chuo pale ambapo anakuwa ame-clear mitihani yake. Kwa hiyo, mwanafunzi ambaye ana supplementary hawezi akadahiliwa kwenda katika chuo kwa sababu bado hajakamilisha masharti ya kumaliza elimu yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia kuhusiana na mikopo kwa wanafunzi wenye stashahada ya ualimu. Mwanafunzi anapata mkopo kulingana na vigezo vinavyowekwa na hivyo basi, kama mwanafunzi wa stashahada amekidhi matakwa ya kujiunga na elimu ya juu na anakidhi matakwa ya mikopo, hakuna usumbufu wowote unaotokea katika upatikanaji wa mkopo.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na jiografia ya Wilaya ya Nkansi, naomba hilo swali labda angesaidia kujibu Mheshimiwa Stella Manyanya, Naibu Waziri wa Elimu, Teknolojia na Elimu ya Juu. Inaonekana hilo swali halikujibiwa jinsi inavyotakiwa na aliyeandika hilo jibu, hajui Wilaya ya Nkasi ilivyo; Kipili iko wapi, Namanyere iko wapi, Kala iko wapi, Itindi iko wapi, Kabwe iko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na majambazi katika mwambao wa Ziwa Tanganyika, hilo gari haliwezi kuhudumia vijiji vya mwambao wa Ziwa Tanganyika. Kwa hiyo, lini Serikali, itawapatia mgawo wa mafuta wa kutosha Wilaya ya Nkasi?
Mheshimiwa Naibu Spika, gari lenyewe liko Wilaya ya Nkasi, hata mafuta halina! Lini itaongeza mgao wa mafuta katika Wilaya ya Nkasi? Lini itawapatia pikipiki vijana wa Marine Kipili, ili kuondoa tatizo la usafiri ambako unatokea ujambazi katika vijiji vilivyopo jirani jirani na mwambao wa Ziwa Tanganyika ili kupunguza uharamia katika mwambao wa Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni kweli kwamba Wilaya ya Nkasi kijiografia imekaa na changamoto nyingi sana hasa ikizingatiwa kwamba baadhi ya vijiji vyake kama Kipili, Kala, Wampembe na vijiji vingine kama Samazi, vimekaa mbali kidogo, vinahitaji mwendo mrefu kuvifuata. Kwa hiyo, vinahitaji mafuta ya ziada. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali imefanya jitihada kubwa sana katika Mkoa wa Rukwa na Nkasi kwa ujumla. Kwanza kuna maboti ya kutosha ambayo yalipelekwa kwa ajili ya Jeshi la Wananchi ambao wamekuwa wakishirikiana kwa karibu sana na Jeshi la Polisi.
Vilevile kuna vituo ambavyo vimeanzishwa katika maeneo hayo na hivyo, kuwezesha kuwa na urahisi wa kuwafikia wananchi wanapokuwa na tatizo, hususan katika kijiji cha Kipili. Kwa hali hiyo, naamini kwamba pamoja na jitihada ambazo zimekuwa zikiendelea kufanyika hali ya Nkasi kwa sasa ni bora kuliko ilivyokuwa hapo awali. Ahsante sana.
MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi, lakini lazima ni-admit kwamba nimefedheheshwa sana na majibu ya Wizara.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba elimu imeporomoka kama ambavyo amekiri lakini hajatupa mikakati. Katika majibu yake ya msingi anasema kwamba Walimu wamekuwa na morali, ni wazi kwamba Serikali labda haijui maana ya motivation theories na hawa Walimu wanapata motive gani. Ni wazi hilo suala la umeme miaka ya 60, 70 hapakuwa na umeme lakini nyumba za Walimu zilionekana. Sasa hivi mtoto anaona aibu kusema yeye ni mtoto wa Mwalimu, anaona afadhali hata aseme ni mtoto wa Mmachinga.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunavyoongea Walimu...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Susan, naomba uende kwenye swali tafadhali.
MHE. SUSAN A. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naenda kwenye swali, nataka kujua kama tuna tatizo kubwa la Walimu, Walimu wame-graduate toka mwaka jana mwezi wa tano mpaka leo tunapoongea hawajaajiriwa, hiyo ndiyo motisha? Kwa hiyo, naomba kujua ni lini Walimu waliomaliza masomo yao wanapata ajira zao?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, moja ya mikakati ni kuhakikisha kwamba Walimu wanapata mafunzo, lakini ukisoma ripoti ya CAG inaonesha Walimu hawajakwenda mafunzo, ni asilimia 11 ya Walimu wa sekondari ndiyo tu wanapata in-service program na Walimu wa primary ni asilimia 30. Ni lini Walimu hawa watapata in service training ili waweze kuendana na mazingira halisi ya ualimu na hasa kuhakikisha kwamba elimu yetu haiporomoki?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni kweli tulivyoeleza kwamba Walimu wameanza kupata motisha kwa sura mbalimbali hasa za mazingira wezeshi na ni jambo endelevu. Hata hivyo, katika suala la ajira huwezi kuajiri mtu kabla hujamwekea bajeti yake. Katika mwezi huu unaoanza mpaka mwishoni kuna mpango wa kuajiri Walimu. Kwa misingi hiyo, mimi nafahamu kwamba kumaliza ni namba moja na kuajiriwa ni namba mbili, lakini kwa taratibu ambapo lazima uwe umeshamwandalia stahiki zake zote ili kupunguza malalamiko yasiyo ya lazima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kuhusu Walimu kutopewa mafunzo ya ziada kama ambavyo imeelezwa katika taarifa ya Mkaguzi Mkuu, niseme tu kwamba, hili suala ni endelevu, hata hivi tunavyoongea sasa hivi kuna mafunzo yanayoendelea huko Mwanza na wiki iliyopita kuna mafunzo yalikuwa Iringa. Kwa hiyo, suala hilo haliwezi kukamilika kwa siku moja lakini kimsingi Wizara imedhamiria.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunachosema ni kwamba, fedha inayotengwa kwenye bajeti haendi katika Wizara ya Elimu peke yake, inaenda katika Wizara mbalimbali na kila Wizara kama tulivyojionea ina umuhimu wake. Kwa hiyo, tutakwenda hivyo hivyo kutokana na kiasi kile kinachopatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. MASHIMBA M.NDAKI: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu aliyotoa Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina swali moja tu la nyongeza. Kwa kuwa wananchi walionufaika na fedha hizi za mikopo wanakatwa kupitia waajiri wao, lakini hawapati taarifa kwamba ni lini deni lao hilo litaisha. Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza kutoa taarifa hizo kwa wanufaika hao wanaokatwa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza napenda kuwashukuru na kuwapongeza sana hao ambao tayari wameshatambua wajibu wao wa kurudisha mikopo, kwani heshima ya mtu ni kukopa kwa staha, lakini pia dawa ya deni ni kulipa.
Mheshimiwa Spika, kwa misingi hiyo, napenda kusema kwamba katika mfumo wetu wa kulipa kupitia sheria zilizopo, tumegundua pia kulikuwa na upungufu wa aina mbalimbali ikiwemo na baadhi ya maeneo mengine, badala ya kukata kwa kutumia 8% ya mshahara, wamekuwa wakikata aidha kwa kusema ni shilingi nane au vinginevyo. Pia hizo taarifa zimekuwa hazipatikani siyo kwa wale ambao wanakatwa, lakini pia hata kwa bodi katika kuhakikisha kwamba watu wote wanalipa.
Mheshimiwa Spika, kwa misingi hiyo, tunashukuru kwa ushauri, lakini pia na sisi wenyewe tumekuwa tukifanyia kazi ili kuona kwamba wanufaika wanaolipa na sisi Serikali, wote tunakuwa na taarifa zinazostahili.
Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nadhani kuna shida ya mawasiliano, wakati nilipoletewa nifanye marekebisho niliandika ni kifungu namba 20 na nikazungushia na sheria ninayo.
Mheshimiwa Spika, jambo la pili, naomba niseme tu kwamba nasikitika sana kwa majibu niliyopewa. Haya majibu, nimeuliza kuhusiana na mitaala utamsikiliza katika majibu Mheshimiwa Naibu Waziri hakugusa kabisa mitaala. Nimeuliza juu ya maswali ya kuchagua ya masomo ya hesabu, hakugusia. Nimeuliza kipengele cha tatu cha Waziri kutoa maelekezo, Sheria inasema The Minister may give the Council directions of a general or specific character and the Council shall give effect to every such direction, hakuna kushauriana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitaomba niulize maswali mawili ya nyongeza wakati anajiandaa kunipa majibu sahihi kwenye swali hili.
Swali la kwanza, kwa nini Waziri wanang‟ang‟ania na kipengele cha kutunga mambo yao wao yaani kusema leo watu watumie GPA au watumie division, yaani leo waseme tufanye sayansi, hesabu na physics pamoja, biology na kemia. Haya wanakubali yawepo lakini hii ya ushauri na wataalam hawataki kwa nini naomba tujibu?
Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kwa nini Wizara hii inakataa kushirikisha Wataalam katika maamuzi ya kupima wanafunzi wetu, atueleza hapa wale watoto ambao walipimwa kwa kiwango cha kutumia GPA na wakapewa vyeti, sasa hivi Waziri ametoa tamko lake hapa anasema sasa ni division, hivi vyeti anavi-compromise namna gani katika elimu? Naomba atusaidie mambo hayo.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa amelalamika kwamba hatujazungumzia masuala ya kuchagua majibu ya hesabu na mambo mengine. Kimsingi najibu kadri ya swali lilivyowekwa, kule uliweka utangulizi lakini swali lako ulisema kwa nini kifungu hiki kisiondolewe na ndicho nilichokujibu.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo kimsingi lazima ieleweke Mheshimiwa Waziri hafanyi maamuzi kwa kukurupuka bila kupata taarifa mbalimbali zinazomwezesha kufanya maamuzi hayo. Hata hivyo si kwamba kila jambo linalofanyika kwenye Wizara linakuwa limetangazwa, lakini hatua mbalimbali zinakuwa zimechukuliwa, ikizingatiwa kwamba Wizara hii inazingatia sana masuala ya kitaalam.
Mheshimiwa Spika, katika maswali ya kuchagua majibu ya hesabu, siku za nyuma wanafunzi walikuwa hivyo hivyo wanachagua, lakini walikuwa na sehemu ya kufanyia kazi halafu wanachagua. Hata sasa hivi wanapewa karatasi wanazofanyia kazi, lakini wanachagua kwa ku-shade kwa misingi kwamba kwa siku za nyuma kwa sababu walikuwa wanasahihisha karatasi kwa mikono, sasa hivi inasahihisha mashine, ndiyo maana baada ya kuchagua lile jibu lake sahihi anakwenda ku-shade na kuweka ili mashine iweze kusahihisha.
Hiyo imepunguza kazi iliyokuwa inatakiwa kufanyika na watu 3000, sasa inafanyika na watu 300. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali lingine Mheshimiwa amezungumzia kwamba kwa nini tumeking‟ang‟ania hicho kifungu. Siyo suala la kuking‟ang‟ania, kifungu hiki kikitumika vibaya ndipo kina kasoro, lakini kama kinatumika vizuri kinaharakisha utendaji na maamuzi ya Wizara.
Kwa hiyo, nasimamia katika sura hiyo kusema kwamba, Waziri aliyeaminiwa na Serikali kutekeleza majukumu yake ipasavyo, naamini atakitumia kifungu hiki inavyostahili. Hata hivyo, baada ya kubadilisha GPA kuweka katika division, kimsingi hakuna athari zilizopatikana kwa sababu bado kuna uwiano katika hizo alama na wanafunzi hawa bado wanaendelea kupata haki zao kama kawaida.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ili niulize swali moja dogo la nyongeza. Ukiangalia katika majibu amesema kwamba, mabadiliko haya yanafanywa baada ya utafiti, baada ya wataalam kuleta taarifa mbalimbali. Naomba kujua GPA imetumika kuanzia mwaka 2013 na sasa 2015 tayari imebadilika imekuwa madaraja, yaani ilikuwa madaraja ikaja GPA within a year, sasa naomba kujua huo utafiti ulifanywa lini hasa ikizingatiwa wataalam walioko Baraza la Mitihani ni wale wale kuanzia Mtendaji Mkuu? Kwa hiyo, naomba kujua huo utafiti umefanywa wapi na mazingira ya jamii ni watu gani walitaka hasa wabadilishwe kutoka madaraja kwenda GPA na kurudi tena kwenye madaraja?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kimsingi wakati huu mfumo wa GPA unaanza kutumika ulikuwa pia uanze katika misingi ya majaribio. Lengo lilikuwa ni kufanya kwamba, toka mwanafunzi anapokuwa katika hatua za awali yaani katika sekondari na kuendelea aweze kuwa na mfumo mmoja unaokwenda mpaka vyuo vikuu. Kwa sababu unakuta vyuo vikuu tunatumia GPA, lakini huku chini tulikuwa tunatumia division na kwa kweli lilikuwa ni jambo jema tu, lakini kukawa na maneno tena ya malalamiko mbalimbali kupitia vyombo, kama jana ulivyoona Mheshimiwa Susan Lyimo ulisema kwamba hata magazeti na yenyewe pia ni nyaraka sahihi kutumika katika Bunge letu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, maneno haya yamekuwa yakitoka katika pressure mbalimbali na hata hivyo baada ya kupitisha huu mfumo wa division hii juzi, nafahamu kuna magazeti mengi hata Waheshimiwa Wabunge walipongeza. Sasa mjue tu kwamba ni hayo mawazo yetu tunayoyatoa na Serikali ni wajibu wake kufanyia kazi. Ahsante sana.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri ametoa ufafanuzi mzuri, ningependa tu kuongezea pale alipojibu Mheshimiwa Naibu Waziri, kwamba kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri hata huu mfumo wa GPA ulitokana na maoni ya wadau. Hata hivyo, baada ya Serikali kutekeleza, wadau tena wakawa wameleta malalamiko, kwa hiyo, lazima Serikali tuweze kuyafanyia kazi kadri mahitaji yanavyojitokeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwasihi Watanzania tunapopewa nafasi ya kutoa maoni, tuitumie nafasi hiyo kutoa maoni ya dhati kabisa. Kwa sababu tunatoa maoni, Serikali inapotekeleza halafu tena kuna kuwa na malalamiko kama ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri amesema. Vilevile ningependa pia kuchukua nafasi hii kumwambia Mheshimiwa Ndugu yangu Mwita Waitara kwamba hii Sheria ya Baraza la Mitihani akisoma kifungu cha nne, kinatoa fursa kwa wananchi kutoa maoni kwa Baraza la Mitihani kuhusiana na masuala ya uendeshaji mitihani na maoni yao yanazingatiwa. (Makofi)
Kwa hiyo, siyo kwamba tu imempa mamlaka Waziri wa Elimu, lakini vilevile imetoa fursa kwa maoni kutolewa na naomba kama kuna maoni yoyote ambayo yana tija, basi wahakikishe na yatafanyiwa kazi.
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na kwa kuitikia wito wetu wa kusaidia kupokea hiki chuo kiwe cha Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo letu kubwa Ileje na maeneo mengi ya pembezoni ni upimaji wa ardhi kwa ajili ya kuweka taasisi muhimu kama hizi za vyuo na masuala mengine. Naomba Serikali kwa ujumla itusaidie kwa sababu kupima viwanja muhimu kama hivi kwanza ni gharama lakini vilevile hatuna wataalam katika maeneo yetu wa kutupimia kwa haraka ambayo tungeitegemea. Je, Serikali ipo tayari kupitia Wizara nyingine yoyote ambayo inahusika na mambo haya kusaidia Wilaya ya Ileje tuweze kupima viwanja vyote muhimu tulivyoviainisha kwa ajili ya taasisi kwa mfano viwanda, elimu kama hivyo, vyuo vya unesi na vyuo vingine mbalimbali vya ualimu ili tuweze kupata maendeleo haraka zaidi? La sivyo tukiendelea kungojea tu mpaka sisi wenyewe tuwe na uwezo wa kupima tutachelewa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine, kwa kuwa sasa hivi tumeshaanzisha mkakati wa kuwa na chuo cha ufundi, tungeomba sasa tunapoendelea na mipango basi hiki chuo kiwe na mitaala ambayo itatusaidia kuzalisha vijana watakaokuja kufanya kazi katika viwanda kwa sababu sasa hivi tunalenga kwenda kwenye uchumi wa viwanda. Ahsante
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA MAFUNZO YA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni kweli kama ambavyo amezungumza Mheshimiwa Mbunge Janet Zebedayo Mbene kwamba kuna tatizo kubwa katika baadhi ya halmashauri kushindwa kumudu kupima viwanja hususani vile vinavyohitajika katika maendeleo ya vyuo na taasisi mbalimbali za kiuchumi. Suala hilo linatokana na hali halisi ya uchumi katika halmashauri hizo. Sisi pia kwa upande wetu Wizara kwa kupitia VETA imekuwa ikicheleweshwa sana katika upatikanaji wa viwanja kutokana na halmashauri husika kushindwa kuleta hati za viwanja au maeneo ambayo yameshapimwa kwa ajili ya shughuli hizo. Hilo suala tumeliona na nadhani linahitaji pia kuangaliwa kwa mapana zaidi.
Katika hili nachukua nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha alivyozungumzia kuangalia mapato katika halmashauri kwa upana zaidi na kuweza pia kuangalia namna ya hizi halmashauri nyingine ambazo zipo katika hali ngumu ya kiuchumi nazo ziweze kupata mitaji hasa katika upimaji kadiri itakavyowezekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika suala la kuangalia mitaala inayoendana na shughuli za viwanda, ni kweli kwamba kabla Chuo cha VETA hakijajengwa mahali popote, kitu kinachofanyika ni kuangalia mitaala na kozi ambazo zitaweza kutolewa katika maeneo hayo tukiwa na lengo la kuwanufaisha hata wananchi wengi wa maeneo hayo kutegemeana na shughuli mbalimbali zinazofanyika katika maeneo hayo. Kwa hali hiyo ni kwamba kabla hiki chuo hatujaweza kukichukua na kuanza kukiendesha, suala hilo la kuangalia mitaala litakuwa ni mojawapo ya shughuli zitakazozingatiwa. Nachoomba Mheshimiwa Mbene jitahidi kadiri inavyowezekana kumalizia angalau hasa zile taratibu za awali za makabidhiano rasmi kupitia vikao vya kisheria wakati masuala mengine yakiendelea.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Vilevile, naipongeza Serikali kwa jitihada za kutatua matatizo hasa changamoto zinazowakabili watoto wenye ulemavu. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Lugha ya alama ni changamoto kwa watoto viziwi ambao wengi wao huishia elimu ya sekondari na kushindwa kuendelea na elimu ya juu kutokana na Wahadhiri wengi kutokujua lugha ya alama. Je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa wa kuingiza lugha ya alama katika shule za msingi, sekondari na katika Vyuo vya Ualimu hapa nchini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, ni Vyuo vingi hasa vyuo binafsi, mazingira yake sio rafiki kwa wanafunzi wenye ulemavu. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwepo mwongozo utakaoviongoza vyuo vyote kuzingatia mahitaji na hasa miundombinu kuwa rafiki kuwatimizia majukumu yao hasa watoto hawa wenye ulemavu ili waweze kusoma vizuri? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni kweli kabisa lipo hilo tatizo, kutokana na kwamba kama inavyojulikana kwa muda hawa watu wenye ulemavu wamejikuta hawapati elimu za aina mbalimbali kutokana na mahitaji yao. Sasa hivi Wizara inachofanya, kwanza imetambua hayo mahitaji maalum ya aina mbalimbali na kupitia bajeti hii, tumeshatenga fedha kwa ajili ya kuandaa mitaala kwa ajili ya kutoa mafunzo maalum kwa ajili ya Walimu pamoja na wanafunzi wenyewe katika shule husika, vile vile, kwa ajili ya kununua vifaa ambavyo vitatumika katika kufundishia.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili, juu ya miundombinu rafiki, niseme tu kwamba, hilo suala limekuwa likijitokeza. Ninayo mifano mingi ambayo nimeishuhudia mwenyewe kwamba, watu wanapojenga shule au taasisi maalum, wanasahau kabisa kwamba kuna siku wanaweza wakawa na mwanafunzi ambaye ni mlemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unakuta hata mtu anapojenga iwe ni ghorofa, iwe ni choo, haangalii kama atakuja mwanafunzi mwenye wheel chair, atafika vipi huko au angalau kuwashusha wale wanafunzi badala ya kusoma ghorofani waweze kusoma katika madarasa ya chini ili nao waweze kupata hiyo fursa. Kwa hiyo nitoe wito, tujue kwamba, ulemavu siyo jambo la kujitakia bali ni mapenzi ya Mwenyezi Mungu katika kuonesha kazi za uumbaji wake. Ni vyema tuwafikirie na kuwajali watu wenye ulemavu.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa elimu ndiyo ufunguo wa maisha, je, Wizara imechukua hatua gani kuwahamasisha wazazi wenye watoto walemavu kutoa kipaumbele kwa watoto hao kupata elimu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kweli Wizara yetu imekuwa ikizungumza katika nyakati mbalimbali kupitia vyombo vya habari, lakini pia kupitia Wizara nyeti sana hii ya Sera, Bunge, Watu wenye Ulemavu na mambo yote yaliyoko kule, kwamba tumekuwa tukishirikiana pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wenzangu kuhakikisha kwamba tunahamasisha jamii kwa kupitia makongamano, mikutano na kupitia Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hivi tunavyoona, kwamba tuna Waheshimiwa Wabunge wenye ulemavu, mtu anaanza kuona kwamba kumbe mwanangu nikimsomesha, kumbe nikimsaidia, kuna siku ataweza kuwa Mbunge, Waziri au kiongozi yeyote yule. Kwa hiyo, kwa hali hiyo niwaambie sana Waheshimiwa wazazi mlio huko, naomba muwatoe watoto wenu wenye ulemavu barabarani, msiwape kazi ya kuomba, hiyo sio kazi yao. Ninyi ndiyo kazi yenu mfanye kazi na hatimaye iweze kuwasaidia watoto hawa wenye ulemavu.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu ina shule ya viziwi kule Dongobesh na pia ina Kitengo cha Elimu ya Watoto Walemavu katika Shule ya Msingi Endakkot na kwa kuwa kundi hili ni kubwa katika jamii; je, Serikali haioni umuhimu mkubwa wa kuweka Kitengo cha Elimu kwa Walemavu katika kila halmashauri kwa shule mojawapo ili kundi hili lililokosa nafasi wapate huduma stahiki?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni kweli kuna umuhimu mkubwa sana kwa kila halmashauri kuwa na shule yenye kitengo cha watu wenye ulemavu. Hata hivyo, niseme tu kwamba, kuwa na kitengo ni kitu kimojawapo, lakini kuangalia hivyo vitengo vikafanya kazi iliyokusudiwa ni hatua ya pili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningetamani kuona kwamba, kwanza kila halmashauri iwatambue hawa watoto wenye ulemavu pamoja na mahitaji yao yanayohusika. Baada ya hapo, katika hizo shule zinazotengwa, naomba ziwasilishwe kwenye Wizara yetu pamoja na Wizara ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kuona kwamba vinawekwa vifaa vinavyohusika na kukidhi mahitaji yanayostahili, tukifanya hivyo tutakuwa tumetatua matatizo makubwa ya watu wenye ulemavu.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Kwanza, nilitaka nifahamu kwa wale waandishi na wachapishaji ambao wamechapisha vitabu vyenye maadili mabovu au wametoa taarifa za uongo kupitia vitabu hivyo wamepewa adhabu gani?
Pili, ninataka kujua kwa kuwa wananfunzi wanaotoka Visiwa vya Unguja huwa wanafanya mitihani ya Kitaifa sambamba na wenzao wa Tanzania Bara; je, Wizara inafanya utaratibu gani kuhakikisha kwanza mihtasari na vitabu kwa maana ya mitaala na vitabu inawafikia wanafunzi wa Zanzibar mapema ili na wao waweze kujisomea na kufanya vizuri katika mitihani ya Taifa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi vitabu vyote kabla ya kupitishwa vinatathminiwa na baada ya kutathminiwa, vinaangaliwa katika suala la maadili inayoendana katika misingi ya kwamba huyu mwanafunzi atafundishwa vipi. Lakini vilevile siyo maadili tu hata uchapishaji wake kitabu kilivyochapishwa kinaleta uhalisia wa yale yanayokusudiwa kufundishwa au laa! Kwa mfano, kama tuna lengo la kumfundisha mtoto kwamba haya ni mayai, basi tunategemea kwamba na kitabu hicho hata picha itaonyesha mayai ambayo ni meupe na itaonyesha kweli yale ni mayai, hayataonyeshwa mayai wakati hapo imechorwa embe. Kwa wanaokuwa hawajatekelza wajibu wao ipasavyo vitabu hivyo vinakuwa haviruhusiwi kupelekwa au kusambazwa au kuchapishwa kwa maana hiyo wanatakiwa kurekebisha hayo makosa. Hayo yalishafanyika hata katika vitabu ambavyo sisi wenyewe tulikuwa tukivishughulikia na tulivizuia visiweze kuendelea.
Pili; kwa upande wa Zanzibar kimsingi Zanzibar wao wanayo mamlaka yao ya elimu ambayo inashugulikia masuala yote hayo ya mitaala pamoja na vitabu. Lakini kwa kuwa sisi wote ni ndugu na tuna masuala ya ushirikiano wa kielimu huwa pia tunaweza kusaidiana katika masuala ya kitaalam lakini pia hata kuchukua best practice katika kutoka upande wowote wa nchi kwa faida ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, ningependa kuongezea kidogo majibu mazuri aliyoyatoa Naibu Waziri wa Elimu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka nitoe tu ufafanuzi kuhusiana na mitaala ya elimu ya sekondari kwa upande wa Zanzibar. Kama alivyoelezea Mheshimiwa Naibu Waziri kwa upande wa elimu ya msingi mitaala inatengenezwa na upande wa Zanzibar, lakini kwenye upande wa sekondari mitaala inatengenezwa na Taasisi ya Elimu Tanzania ambayo utaratibu ni shirikishi wakati wa mitaala inapotengenezwa tunawashirikisha upande wa Zanzibar na vilevile hata katika Bodi ya Taasisi ya Elimu Tanzania kunakuwa na uwakilishi wa Wajumbe wa kutoka Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na utaratibu wa usambazaji wa vitabu ili vifike Zanzibar kwa wakati, utaratibu ni kama unavyotumika Bara kwamba kwanza zoezi ni shirikishi la vinapokuwa tayari Wizarra ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar huwa inafanya hilo jukumu.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa shule zetu nyingi bado zinaendelea na utaratibu wa matumizi ya vitabu vingi vya kiada; na kwa kuwa vitabu hivi vimekuwa vikitofautiana kwenye baadhi ya maudhui yaliyomo kwenye vitabu hivi na kuleta mkanganyiko kwa wanafunzi. Je, lini sasa Serikali itaanza kutekeleza utaratibu wa kutumia kitabu kimoja nchi nzima ili kuleta usawa na kuondoa mkanganyiko wa wananfunzi hao?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa baada ya Serikali pamoja na wananchi kugundua kwamba kuna vitabu vingi ambavyo vinatumika mashuleni kiasi cha kushindwa kutoa mwelekeo halisi hasa katika usimamiaji wa maarifa yanayopatikana, Serikali iliamua kwamba kuwe na vitabu vya kiada na ziada, mpaka sasa imekuwa inasimamia katika zoezi hilo la upatikanaji wa hivyo vitabu kadri ya fedha tunavyozipata. Hivyo naamini tukishakuwa tumekamilisha hali hiyo ya kuwa na vitabu ambavyo ni vya aina tofauti tofauti itaondoka.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.
NAKALA YA MTANDAO (ONLINE DOCUMENT)
16
Kwa kuwa hapo awali Serikali ilikuwa na chombo ambacho kinadhibiti education materials yaani EMAC na kwa kuwa ilivunjwa rasmi huko nyuma na kutamka kwamba wataunda chombo kingine kwa ajili ya kudhibiti vifaa vinavyoingia katika mfumo wa elimu pamoja na vitabu.
Je, Serikali inaukakasi gani wa kuunda chombo hicho maana mpaka leo hakijaundwa bado?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli hapo mwanzo Wizara yenyewe ilikuwa inahusika katika kudhibiti kwa kutumia Kitengo hiko cha EMAC, lakini baadaye kupitia Waraka Na. 4 ambao niliutaja kulikuwa kumeundwa Taasisi ya Elimu Tanzania ambayo kwa sasa ndiyo inashughulikia masuala hayo.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mwenyekiti ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza swali moja fupi la nyongeza. Malalamiko haya ni ya muda mrefu sana na kila siku yanazidi kwa wananchi. Je, Wizara imewahi angalau kuwaonya wamiliki wangapi angalau kwa barua mpaka kufikia mwaka uliopita?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu imeshawahi kuwaonya wamiliki IMTU na mwenzao KIU kwa kukiuka masharti hayo na hivyo tunazidi kusisitiza wamiliki wote wachukue fedha ambayo ni ada kwa kutumia fedha za Kitanza ni ana pale inapobidi iwe tu kwa wananfunzi ambao wanatoka nchi za nje
MHE. SALUM MWINYI REHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba nimuulize swali moja la nyongeza.
Kwa Zanzibar suala hili limekuwa na manung‟uniko sana na hasa kwa kutokuweko watendaji katika hizi taasisi na hili limetokana kwamba wanafunzi wengi wanaopata huduma kupitia TCU, NACTE na NECTA wamekuwa wanahisi hakuna uwiano na hakuna haki inayotendeka kwa vile hakuna watu ambao wanaohusiana wanaotoka upande ule kule. Je, Waziri au Wizara ina mpango gani wa kuweza kupata angalau maana yake watu wawili, watatu kuweza kuingia katika taasisi hizi ili kuepusha manung‟uniko ya kila siku hasa yanayohusiana na masuala ya vyeti na mengineyo ambao wanataka kujiunga katika vyuo mbalimbali vya huku Tanzania Bara?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwaombe Watanzania tusifanye mambo kwa masuala ya hisia. Lazima twende katika misingi na misingi iliyopo ni hiyo ya kufuata sifa stahiki kwa nafasi zinazohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kusema kwamba pamoja na kwamba hakuna hivi vigezo vilivyowekwa, kimsingi ukiangalia katika hizo taasisi zote wapo Wazanzibari ambao wanafanya hizo kazi na isitoshe kwa mfano kwa Baraza la Mitihani nafahamu hata Mkuu wa Kitengo kile kule Zanzibar anatoka Zanzibar. Lakini ukiacha hiyo nataka tu niseme kwamba sisi tumekuwa na mahusiano ya karibu sana na Serikali ambayo iko kwa upande wa Zanzibar na tunawasiliana katika masuala yote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tarehe 11 Agosti, huu tulitembelewa na Mheshimiwa Waziri wa Elimu pamoja na Naibu wake na Katibu Mkuu na tuliweza kujadili mambo mablimbali ikiwemo ya kushirikiana na kusaidiana pale tunapoona upande mmoja haujakaa vizuri na kila jambo linalofanyika huwa tunashirikishana. Kwa hiyo, ninachoomba ni kwamba Mheshimiwa Mbunge tusiende kwa hisia. Kama nafasi zitaonekana kwamba Watu walioomba wenye uwezo wengi wanatoka Zanzibar basi itabidi wapewe kwa sababu tunachohitaji ni uwezo na siyo tu kuangalia upande wanakotoka.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa mwenyekiti, napenda kuongezea katika majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Elimu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa taaisis za Muungano kuwakilishwa kwa uwiano sahihi na muafaka kwa watu wa pande zote mbili, Serikali iliamua kwamba kuwe na quota kwa watumishi kwenye taasisi za Muungano na quota iliyokubalika ni asilimia 79 kwa asilimia 21 na sisi ofisi yetu tuliwaandikia taasisi na viongozi wote ambao wanahusika na masuala ya Muungano kwanza watuletee idadi ya watumishi waliopo, lakini pili watuletee mpango kazi wa kufikia quota iliyokubalika ya taasisi za Muungano ziwe na uwiano sahihi wa kimuungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu na mwisho ni kwamba Serikali ilishafanya uamuzi wa kufungua Ofisi ya Tume ya Ajira Zanzibar kwa sababu moja ya changamoto ilikuwa ni kwamba Tume ya Ajira ambayo inaajiri hawa watendaji na watumishi wengineo ipo Bara peke yaake na hizi nafasi wakati mwingine hazifahamiki au hazifikiwi na watu wa upande wa Zanzibar, kwa hiyo, ofisi hii sasa imefungua ofisi yake Zanzibar na nafasi zitatangazwa kwa upana wake kwa watu wa Zanzibar na wenyewe wataziomba ili waweze kupata fursa za kushiriki katika taasisi za Muungano.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza ni kwamba zipo shule za ufundi ambazo zipo katika majengo ya shule za msingi na shule za sekondari ambazo zilikuwa zikijulikana kama shule za ufundi na sekondari. Shule hizi katika miaka ya nyuma zilikuwa maarufu sana, lakini katika miaka ya hivi karibuni shule hizi umaarufu wake umepungua. Je, Serikali haioni kuwa ni wakati sasa wa kuboresha shule hizi na vyuo vya ufundi hapa nchini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Tanzania inaelekea kwenye uchumi wa viwanda na ili kuwapata vijana wenye ujuzi kukabiliana na ajira zitakazokuwepo katika viwanda hivyo tunavyovitarajia na kwa kuwa vyuo vingi vya watu wenye ulemavu vilisaidia kwa kiasi kikubwa kuwapa mafunzo watu wenye ulemavu na katika makundi hayo ya ajira tunatarajia pia kwamba kundi la watu wenye ulemavu nao pia watakuwemo katika uchumi huu wa viwanda na biashara. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha vyuo vya ufundi mfano kama Chuo cha Yombo Dovya na vyuo vingine ili watu wenye ulemavu waweze kujiandaa kukabiliana na ajira tunapoelekea kwenye uchumi wa viwanda? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. La kwanza, ni kweli kwamba kumekuwa na upungufu kidogo katika baadhi ya shule zetu hasa shule za ufundi zikiwemo zile ambazo zimekuwa ni za ufundi primary pamoja na ufundi sekondari. Sisi kama Wizara suala hilo tulishaliona na kupitia bajeti yetu ya mwaka 2016/2017, Wizara imetenga fedha kwa ajili ya kuboresha shule zote za ufundi zile za zamani ambazo ni pamoja na Mtwara, Iyunga, Ifunda, Moshi, Bwiru na Musoma, nadhani nimezitaja zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo tunategemea kwamba baada ya hapo na ukarabati utakaoendelea pamoja na kuweka vifaa itasaidia kuboresha. Pia tunazipitia hata zile shule za msingi ambazo zimekuwa zikitoa mafunzo ya ufundi hasa kwa vijana wanaomaliza darasa la saba ili pia waweze kupata stadi ambazo zitawasaidia katika kumudu maisha yao. Kwa hiyo, naamini kwa bajeti ya mwaka huu, kuna marekebisho mengi ambayo yatafanyika katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili katika suala linalohusu watu wenye ulemavu, ni kweli ulemavu siyo maana yake kushindwa kufanya kila kitu. Mimi binafsi nilishawahi kutembelea Shule ya Yombo na nikajionea matatizo wakati huo bado sijawa Naibu Waziri. Kimsingi Waziri wangu pia yuko katika msukumo mkubwa sana kuhusiana na shule za ufundi hasa zinazowahusu watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tulichoamua kukifanya katika Wizara kupitia bajeti yetu ni kuona kwanza mitaala inaboreshwa kuona inakidhi kufundisha watu wenye ulemavu na kuweza kuelewa yale wanayofundishwa kwa kutumia lugha inayoendana na hali yao, lakini vilevile vifaa saidizi vinavyoendana na hali yao. Pia kuhakikisha kwamba tunaweka vifaa ambavyo vitahusika katika mafunzo. Kwa hiyo, kwa kuwa sisi wenyewe pia ni wadau wa watu wenye ulemavu naamini kuna mambo mengi yataboreshwa katika eneo hilo.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu maswali vizuri, lakini tunajua kabisa kwamba kuna tatizo kubwa sana la walimu wa sayansi katika Wilaya zote. Sasa je, Serikali ina mkakati gani wa kuchagua chuo kimoja kuweza kusomesha walimu wa sayansi tu? Kwa mfano, Chuo Kikuu cha Mkwawa pale, tungeamua kitoe masomo ya sayansi ili tuweze kupata walimu wengi?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kwa nini Serikali sasa isitoe mkopo kwa asilimia mia moja kwa wale wanafunzi ambao wanasomea masomo ya sayansi ili kuwavutia wanafunzi waweze kujiunga na ualimu wa sayansi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la mkakati wa kuwapata walimu wa sayansi, kama unavyofahamu kwamba tayari Serikali ilishachukua hatua na kama mnavyokumbuka kwamba tulikuwa na wanafunzi zaidi ya 7,800 ambao walikuwa katika Chuo cha UDOM ambao kwa sasa tumewatawanya katika vyuo mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale ambao wana vigezo sasa hivi kwa kufundisha shule za sekondari ni zaidi ya walimu 6,305 wakishamaliza masomo yao wataweza kwenda kwenye hizo shule. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kuweka mikakati ya kufundisha walimu wa sayansi na wakati huo huo kuhakikisha kwamba maabara kwa ajili ya shule za sekondari ili kupata wanafunzi wengi zaidi katika maeneo ya sayansi yaweze pia kukamilika na kupewa vifaa vinavyostahili.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na nitambue kazi kubwa inayofanywa na Wizara hii katika utekelezaji wa majukumu yake, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti mfumo wa uhakiki wa vigezo vinavyotumika kutoa mikopo kwa wanafunzi, ili kuhakikisha wanaopata mikopo ni wenye sifa na uhitaji na sio wale ambao wanafanya udanganyifu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha mfumo huu wa utoaji mikopo utaendelea kuwa himilivu na endapo idadi ya wanafunzi itaendelea kuongezeka?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Bodi inatakiwa kuhakikisha kuwa kumbukumbu za wote wanaoomba mikopo zinakuwa kamilifu kwa kushirikiana na vyuo ambavyo vina wanafunzi wanaopewa mikopo hiyo. Kila chuo kinatakiwakuwa na dawati maalum ambalo linashughulikia mikopo, lakini pia katika kutoa mikopo ni lazima kuzingatia vigezo na sifa ambazo zimewekwa. Hivi karibuni Wizara imepitia vigezo hivyo na vigezo vinazingatia hasa uhitaji, uraia, lakini pia uombaji lazima upitie kwenye mtandao na vilevile kwa kuzingatia mahitaji ya nchi, yaani kipaumbele katika taaluma ambazo zinahitajika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kuona kwamba, mikopo hiyo inakuwa endelevu ni kwamba, Wizara baada ya kuangalia matatizo yaliyokuwa yakijitokeza katika ulipaji wa mikopo, imeangalia upya Sheria ya Bodi ya Mikopo na hivyo tuko katika kutaka kuileta Bungeni, ili kuona kwamba, inarekebishwa kuweka mikopo kuwa ni deni la kipaumbele kwa mwombaji ambaye ameshamaliza chuo. Lakini vilevile kuhakikisha kuwa waajiri wanahusika nao moja kwa moja katika kuhakikisha mikopo hiyo inalipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika sambamba na hiyo tunaangalia namna ya kuboresha upya mifumo mizima ili kuona mfumo huo unaweza kuongea na taasisi nyingine zinazohudumia raia, ikiwemo ya Vitambulisho vya Taifa. Ahsante.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante ka kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa zipo tafiti nyingi muhimu zilizokwishafanyika, ikiwemo tafiti ya uyoga pori kwa matumizi ya chakula, je, Wizara imejipanga vipi kufikisha matokeo ya tafiti hizo kwa wananchi walio wengi, hasa ambao wako vijijini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Waziri anaweza kuahidi nini kwa vyuo vikuu vilivyoko mkoani Iringa kuhusiana na ongezeko la bajeti yao ya tafiti katika mwaka ujao wa fedha?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru sana Mheshimiwa Mwamwindi kwa kuweka kipaumbele katika maeneo haya ya utafiti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa tafiti inapofikia katika nafasi ya uendelezaji (commercialization) inakutana na changamoto kubwa ya kuendeleza kutokana na kutokuwa na fedha zinazoweza kuondoa utafiti huo katika awamu ya awali na kufikisha katika hatua ambayo sasa inaenda kwenye matumizi. Vilevile Wizara imeliona hilo, lakini pia, hata wanasayansi wengine wa nchi za SADC wameliona hilo na hivi jitihada iliyopo ni kuona kwamba katika kila nchi, fedha za utafiti angalau ziwe ni asilimia moja ya bajeti ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande wa Chuo cha Iringa kwanza niwapongeze kwa hatua mbalimbali wanazozifanya, lakini niwasisitize kuwa wanachotakiwa ni kuandika hayo maandiko mazuri, ili sasa Wizara iweze kutoa kipaumbele katika ku-support bajeti za utafiti za chuo hicho.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo cha Ulebwe ni chuo ambacho kina eneo linalozidi hekta 94 na kwa sasa hivi ninavyoongea, kina wanafunzi 64 tu.
Je, Serikali haioni kwamba sasa kutokana na mazingira mazuri ya Ulebwe kuna ulazima wa kubadilisha mifumo katika chuo kile na kuimarisha fani za kilimo na mifugo ili kusudi vijana wa Njombe waweze kunufaika na chuo kile? (Makofi)
Swali la pili, vijana wengi wamekuwa hawasomi hivi vyuo kwa sababu ya mfumo wanautumia kufundishia ambao ni wa VETA ambao sasa unatumia zaidi lugha ya Kiingereza katika mitaala pamoja na mafunzo yote na vijana wengi hawana uwezo wa lugha hiyo ya Kiingereza; je, Serikali iko tayari kuandaa mitaala ya Kiswahili ili iweze kuwasaidia vijana wadogo wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari waweze kunufaika na haya mafunzo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia kubadilisha mafunzo katika chuo hicho, napenda tu kumfahamisha Mheshimiwa Mwalongo kwamba kwa mujibu wa Katiba yetu kifungu cha 9(i) kinazungumzia kwamba utajiri wa nchi na rasilimali utaelekezwa zaidi katika kuhakikisha kwamba unatoa umaskini, maradhi na ujinga katika maeneo yetu yote. Vilevile inaendelea kwa kusema kwamba haki ya kupata mafunzo au elimu ni ya Watanzania wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, vyuo hivi vya FDC vilianzishwa kwa lengo la kuhakikisha kwamba wananchi wote hata wale ambao hawajafika kidato cha nne au darasa la saba wanapata mafunzo na kuweza kuwasaidia kukimu katika maisha yao ya kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni mtazamo wangu kuona kwamba vyuo hivyo viimarishwe ili kuweza kutoa mafunzo kwa wananchi wengi zaidi ambao bado tunao katika maeneo yote. Sio wote kwamba wamefika darasa la saba au kidato cha nne.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile suala la kufanya mafunzo haya lazima yafanane na VETA, Wizara inaona kwamba iko haja ya kuona kwamba mafunzo yanayotolewa katika vyuo hivi vya FDC yanakidhi uwezo wa wananchi hao kuweza kuyatumia kikamilifu kwenye kazi zao na hivyo siyo lazima yafundishwe kama ilivyo Vyuo vya VETA.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali hiyo, naona kwamba kwa siku za nyuma kulitokea na mkanganyiko kidogo wa kuona kwamba Vyuo vya VETA ni bora kuliko FDCs, lakini tungependa kuona kwamba FDCs zifanye kazi kwa malengo yake na VETA zifanye kazi kwa malengo yake, lakini vyuo vyote viimarishwe na kuweza kutoa mafunzo stahiki kwa walengwa wanaohusika.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa suala la elimu ya juu ni suala la Muungano, je, wanafunzi wangapi katika idadi ya hao aliowataja wametokea Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, wanafunzi hawa wanaporudi masomoni hukuta ajira tayari au wanaachwa wanazurura mitaani?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kimsingi nafasi hizi za kusoma nje mara nyingi zinapotolewa zinatangazwa kupitia Balozi husika ambazo zimepanga kutoa masomo hayo, lakini wakati mwingine pia kupitia vyuo vyetu vikuu. Wakati wa uombaji suala linalozingatiwa zaidi ni sifa ikizingatiwa kwamba masuala ya elimu ya juu ni masuala ya Muungano.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wakati mwingine inawezekana kabisa Ubalozi ukaamua kama umependa watu wa Zanzibar, basi utaelekeza moja kwa moja kupitia masuala ya kimahusiano kwa upande wa Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kimsingi kwa sasa sitaweza kukupa taarifa kamili na ikizingatiwa kwamba linahitaji data. Kwa upande wa ajira, hawa wanafunzi wakirudi, kwa sababu wengi wanakuwa wamepelekwa kwa ajili ya jambo mahsusi, kwa mfano, upande wa gesi, kwa hiyo wanapofika yale maeneo ambayo yanawahitaji ndiyo ambayo yanakuwa yametangaza kazi na wakati huo huo wenye sifa wanakuwa wanachukuliwa kupitia taratibu zetu za kiutumishi.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Suala la idadi ya wanafunzi ambao wametokana na bajeti linaendana na sifa za wanafunzi wanaotakiwa kujiunga na vyuo vikuu. Ningependa kuuliza swali dogo tu, kwamba, sasa hivi Serikali imetoa kauli mbili tofauti, mwezi Julai iliweka vigezo vya wanafunzi kujiunga na Chuo Kikuu vya GPA ya 3.5 kwa watu wa diploma, si zaidi ya hapo. Hata hivyo, juzi wametoa tena tamko lingine la GPA ya 3.0 kwa watu wa ordinary diploma. Je, Serikali itueleze hapa, ni kwa nini inawasumbua wanafunzi katika kipindi hiki ambacho wanafunzi wengi walikuwa wameshakata tamaa na hawaku-apply katika Vyuo Vikuu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, kama ambavyo siku Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania analihutubia Bunge; alisisitiza kwamba Awamu hii ya Tano, jukumu lake kubwa litakuwa ni kuongeza ubora. Vile vile lazima ikumbukwe kwamba, Serikali kwa kushirikiana na wananchi imefanya kazi kubwa ya kuwezesha wanafunzi wengi kusoma na kiasi kwamba tunao wengi wenye sifa za ufaulu wa juu. Hiyo imejidhihirisha wazi hata katika udahili wa mwaka huu wa Vyuo Vikuu, waombaji ni wengi na waliofaulu ni wengi sana kiasi cha kupandisha zile points ili tuweze kuendana na haki katika kuwachukua.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika suala hilo katika maeneo hayo pia kuna ushindani mkubwa, lakini Wizara kila wakati inaangalia kama hao watu wenye sifa hizo itaonekana kwamba hawapatikani hapo ndipo tunaweza tukafikiria zaidi namna ya kusema tushuke chini, lakini kama wanapatikana basi hamna haja ya kumchukua mtu ambaye ana ufaulu wa chini ukamuacha mtu ambaye ana ufaulu wa kiwango cha juu.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri naomba niulize swali moja la nyongeza.
Pamoja na kufanya kazi nzuri ya kupatikana kwa wafanyakazi hewa ambao takribani wataokoa zaidi ya shilingi bilioni kumi na Serikali inapaswa ijazie hizo nafasi kutokana na watumishi wengine. Lakini walio wengi ni wale wanavyuo ambao sasa wanakwenda kuanza vyuo, lakini mpaka leo tunavyozungumza hawajapata mikopo wanahangaika. Je, kuendelea kutokuwapa mikopo hatuoni kwamba tunaweza tukazalisha hewa nyingine zaidi? Sasa Serikali iseme mpango mzima kwa nini mpaka leo mikopo ya wanafunzi baadhi hawajapata?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo imekuwa ikisisitizwa katika nyakati tofauti tofauti ni kwamba kimsingi fedha kwa ajili ya mikopo kwa awamu hii zilishatolewa jumla ya shilingi bilioni 80 na tayari bajeti yake ipo sawa. Suala lililokuwa limetuchelewesha lilikuwa ni suala la uhakiki kwa misingi kwamba watu wanaohitaji mikopo sio wote watakaoweza kupata kwa sababu fedha ambayo inatolewa ni kwa ajili ya watu wale ambao hasa wana uhitaji wa kupita wenzao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema hivyo nina maana kwamba tumeangalia mikopo tu, lakini Serikali kupitia Wizara ina majukumu mengine makubwa sana ya kuangalia mfano tumeona vijana wetu wengi walikuwa wanakaa katika maeneo ambayo walikuwa wakijipangia wenyewe, mabweni yalikuwa yanakuwa hayapo, vitendea kazi vingine vilikuwa viepungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunavyoangalia katika utoaji wa elimu tunaangalia Nyanja zote na haswa katika kuona kwamba elimu inatolewa kwa kiwango kinachostahili na kwa haki inayostahili mwanafunzi kuipata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa misingi hiyo wale wote ambao wanastahili kupata mikopo kutokana na uhitaji uliopimwa, mikopo yao itapatikana, lakini hata hivyo lazima tuzingatie kwamba mikopo hiyo inamfikia mlengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naamini ndani ya wiki hii tutakuwa tumefikia mahali pazuri zaidi. Ahsante
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa mara ya kwanza Serikali kutoa jibu zuri la kuridhisha kwa wananchi wa Nkasi.
Kwa kuwa aliyekuwa Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa John Pombe Magufuli aliniahidi mimi humu Bungeni kwamba mara baada ya kukamilika ile barabara yuko tayari kutoa yale majengo kwa Chuo cha Ufundi VETA. Na sasa barabara yetu inakwenda speed ya ajabu, imebaki kilometa 10 au 12 na wakandarasi wameniahidi Januari au Disemba kipande cha barabara hiyo kitakamilika.
Je, lini sasa mazungumzo kati ya Wizara ya Elimu na Wizara ya Ujenzi yataanza haraka iwezekanavyo wananchi wapate kile chuo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wake tumeupokea, na mara baada ya kumaliza Bunge hili, tutawasiliana na wenzetu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili tuweze kuona suala hili kabla hata barabara hazijaisha.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, kuna majengo ambayo yalikua yanatumika na Halmashauri ya Karatu, na sasa Halmashauri imehamia kwenye majengo mapya na huku nyuma kulishakuwa na azimio la Baraza la Madiwani kwamba majengo yale yatumike kama Chuo cha VETA.
Je, Serikali iko tayari sasa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Karatu kutumia yale majengo ya zamani ili kuweza kufungua chuo cha ufundi VETA?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi, nilipokuwa najibu swali la Mheshimiwa Keissy nilijibu kwa confidence kwa sababu majengo hayo ninayafahamu, nikiwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa na mimi mwenyewe pia nilishiriki kuona kwamba yangefaa kutumika hivyo. Sasa katika hili ambalo umenifahamisha kuhusu majengo ya Karatu, naomba tuweze kuyaangalia kwanza kabla sijatoa majibu. Kwa hiyo, tutafanya utaratibu wa kuja kuyaona.
MHE. OMARY A. BADWEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa yalikuwepo makubaliano kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Bahi na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi miaka minne iliyopita ya kufungua Chuo cha VETA katika Wilaya ya Bahi, katika kijiji cha Kigwe na yako majengo yaliyokuwa ya Chuo cha Kilimo ya Halmashauri na Wizara iliomba ipewe majengo yale ili iweze kufungua chuo cha VETA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Bahi kupitia kikao cha Madiwani miaka mnne iliyopia iliyakabidhi majengo yale kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, na Naibu Waziri wakati huo Mheshimiwa Mulugo alikwenda kutembelea majengo yale na akayakubali kwamba yanafaa kufunguliwa Chuo cha VETA. Lakini hadi sasa miaka mnne imepita majengo yale yamekaa bure, Wizara haijarudi tena.
Je, ni lini sasa Wizara itarudi pale kuendelea na mchakato wake wa kufungua chuo cha VETA katika Halmashauri ya Bahi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu kwa pamoja kwa Waheshimiwa Wabunge wote ambao wanaona kuna majengo yanayostahili kuweza kutumika kama sehemu za kuweza kutolea mafunzo ya ufundi, wanipe taarifa hizo ili tuweze kuyatathimini kwa pamoja na hivyo kuwezesha sisi kupanua wigo wa kuongeza vyuo vya kutolea mafunzo ya ufundi katika nchi yetu, ikizingatiwa kwamba hata hivyo uhitaji ni mkubwa lakini imekuwani ngumu kwetu kuweza kujenga VETA kwa Wilaya zote kwa wakati mmoja.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nianze kushukuru kwa ajili ya majibu, vilevile maandalizi ya ujenzi wa hiki Chuo cha VETA, Mkoa wa Geita ni wa muda mrefu, ni tangu awamu iliyopita, lakini mpaka sasa ujenzi haujaanza. Ningependa kujua Mheshimiwa Waziri amesema utaanza hivi mapema, ni lini? Je, ni katika mpango wa mwaka huu wa 2016/2017?
Swali la pili, kwa kuwa tunaelekea kwenye viwanda, Awamu ya Tano ni awamu ya viwanda na vijana wetu hasa katika Mkoa wa Geita na Wilaya ya Geita hawana ujuzi kabisa, Serikali inasemaje kuanzisha program maalum kupitia SIDO, kwamba vijana wetu sasa waanze kuelimishwa ili viwanda vikianza waweze kuajiriwa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumshukuru kwa shukrani alizotupa. Pili, nikubaliane naye kwamba mchakato huu umeanza muda mrefu, hata hivyo tunapozungumzia kuanza kwa ujenzi, nina maana ni hatua zote zinazohusika ili kuwezesha ujenzi huu. Kama ambavyo tumekuwa tukizungumza hapo awali, chuo hiki kinategemewa kujenga kwa fedha za mkopo kutoka ADB, kwa hiyo, kuna taratibu ambazo lazima zifuatwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza la muhimu ilikuwa ni kupata hati na kiwanja ambacho kiko mahali pazuri ambapo wanachuo wengi watapenda kwenda hapa na pia itakuwa rahisi kufikika kazi hiyo imekamilika, sasa hivi tunaendelea na hatua za kumpata mshauri elekezi, tunaamini hatua hizi hazitakuwa na utata mkubwa kwa sababu ziko wazi na zinakwenda kwa taratibu zilizopo tukishakamilisha ndipo tukakapoanza ujenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuhusiana na tatizo la upungufu wa wataalam hasa katika azma ya kwenda uchumi wa viwanda. Ni kweli kabisa vijana wetu wengi wanamaliza darasa la saba, form four na vyuo, wanahitaji ujuzi. Kupitia ziara hiyo niliweza kutembelea maeneo mbalimbali vikiwemo Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi ambavyo navyo vinaonekana kuwa na mchango mkubwa katika kutoa mafunzo haya ya ufundi. Wizara tumeshajipanga kuona kwamba vyuo hivyo vinakarabatiwa na kuongezewa vifaa ili vijana wengi zaidi waweze kunufaika.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Matatizo yaliyopo kwenye hii Wilaya ya Busanda yanafanana kabisa na yale yaliyoko katika Wilaya ya Liwale. Wilaya ya Liwale hatuna Chuo cha Ufundi, je, ni lini Serikali itatujengea Chuo cha Ufundi Wilayani Liwale?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Liwale wanahitaji chuo, lakini kwa bajeti ya mwaka huu Liwale haimo katika vyuo vitakavyojengwa. Ninachoshauri kwa sasa ,wale wanafunzi wote wanaohitaji kupata mafunzo haya ya ufundi waende pale katika vyuo vyetu ambavyo viko tayari na chuo ambacho kina uwezo wa kuchukua wanafunzi wengi pale Mtwara na watapata mafunzo yanayostahili.
MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa, tatizo la ukosefu wa Chuo cha Ufundi katika Wilaya ya Geita inafanana kabisa na Wilaya yangu ya Pangani. Je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba inatujengea Chuo cha Ufundi kwa sababu vijana wa Pangani wanashindwa kunufaika na rasilimali zilizopo katika Wilaya yangu ya Pangani?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo kwa Wilaya nyingi, ambazo zina uhitaji mkubwa wa kuhitaji kupata vyuo hivi vya VETA, niseme tu kwamba, tayari bajeti ya mwaka huu Waheshimiwa Wabunge wote mnayo na vyuo vitakavyotekelezwa vimo. Kwa hiyo, kama Wilaya yoyote ile imo katika orodha ya vyuo vinavyoanza kutekelezwa, basi ajue kwamba tupo katika kutekeleza mpango huo na kama haipo basi tunaendelea na michakato ya kupata ardhi ili na vyenyewe viweze kuwa katika mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumegundua kwamba kwa muda mrefu fedha ambazo zimekuwa zikitengwa kwa ajili ya vyuo imekuwa ni kidogo, mwaka huu baada ya kutembelea na kuona huu uhitaji mkubwa tulichojifunza ni kuongeza maeneo hayo ya bajeti katika vyuo vyetu hasa hivi vyuo vya ufundi vya Wilaya.
MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na swali langu ni hivi, wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne, darasa la saba kwenye nchi hii na hata wanaomaliza kidato cha sita na wakashindwa kuendelea ni wengi mno na Serikali yenu hii imesema inataka kujenga viwanda, japo ni viwanda vya akina Bhakresa na tunajua tunahitaji ma-technician wengi sana kwenda kufanya kazi kwenye viwanda, makampuni na hata migodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri hebu atuambie ni lini kwa mipango yenu nchi nzima hii kutakuwepo na vyuo kwenye Wilaya, kwa sababu siyo kila siku tunasimama hapa tunauliza kwamba swali hili linafanana na la kwangu, lini mnataka muwe mmefikisha vyuo angalau kwenye Wilaya au tuvipeleke kwenye Kata kama shule za sekondari?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo amezungumzia katika suala lake, maudhui yake ya msingi kwamba kuna tatizo kubwa la mahitaji ya vijana kubakisha ujuzi. Ujuzi unapatikana katika staili za aina mbalimbali, mojawapo ni hiyo ya kuwa na vyuo maalum ikiwemo Vyuo vya Ufundi pamoja na Vyuo hivi vya Maendeleo ya Wananchi, pia tunavyo Vyuo Vikuu, ambavyo vyote vinatoa mafunzo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa kutambua mahitaji haya yalivyo mengi, kuna vijana wengine pamoja na watu wazima ambao siku zote wamekuwa wakifanya shughuli za ufundi, lakini wamekuwa hawatambuliwi. Tayari kwa kutambua hilo tunao mpango wa kutambua wale ambao wana ujuzi ambao hawakupitia katika maeneo rasmi na hiyo tukishawatambua wanapewa mafunzo ya ziada ya ujasiriamali na kuwawezesha kutambulika.
Vilevile kupitia mpango ambao ni wa kuwezesha vijana katika mafunzo mbalimbali ya ufundi, hivi juzi tarehe 28 nimezindua tena mpango wa pili wa kuwezesha vijana mbalimbali ambao wataweza kupata mafunzo, yakawezesha kujiajiri na kuwezesha kuhudumia hivi viwanda vidogovidogo kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wa Viwanda jana alivyoeleza ili waweze kufanya shughuli zao. Mpango huo utanufaisha vijana zaidi ya 22,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwa staili mbalimbali ambazo tunatumia tutaweza kuwafikia vijana wengi zaidi na kwa muda mfupi zaidi.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa, kuna uhusiano chanya kati ya elimu na maendeleo katika sekta za kijamii na kiuchumi; je, ni lini Serikali au Wizara itaona umuhimu wa ku-link elimu na maendeleo ya Taifa letu au katika mipango ya maendeleo ya Taifa letu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kuwa, tayari Serikali imeshachelewa kutathmini; je, tuna upungufu wa aina gani au tunahitaji watu wenye elimu ya aina gani ili kuleta maendeleo katika sekta fulani? Wameji-commit kwamba mpaka mwisho wa mwaka huu wa fedha watakuwa tayari wamekamilisha huo mkakati.
Je, huu mkakati watau-link vipi na Mpango wa Maendeleo wa Taifa hili?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kimsingi Serikali inatambua mahusiano kati ya elimu inayotolewa na ustawi wa jamii au katika kuleta maendeleo. Ndiyo maana msisitizo uliopo sasa hivi ni kuhakikisha kuwa, course zote zinazoanzishwa hasa katika vyuo vyetu, ni zile zinazojitahidi kujibu changamoto zilizopo katika jamii zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo basi, baada ya kukamilisha mpango huu ambao umeandaliwa, unaoangalia kwa kina sasa kwa jinsi ambavyo Mpango wetu wa Maendeleo wa Miaka Mitano lakini pia Dira yetu ya Taifa ya mwaka 2020 - 2025, kwamba tunataka kwenda wapi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, sasa hivi tunataka kwenda kwenye uchumi wa viwanda. Katika uchumi wa viwanda tutahitaji wataalam mbalimbali watakaoendesha viwanda vyetu, vilevile katika hao watakaoendesha viwanda tunategemea humo kutakuwa na mambo ya aina mbalimbali. Kwa mfano, afya zetu ili hao watumishi waweze kufanya kazi zao vizuri. Pia tunategemea kupunguza madhara kwa akinamama waweze kujifungua salama. Kwa hiyo, kutokana na matatizo kama hayo, ndiyo maana hata sisi sasa mitaala yetu lazima ijibu changamoto ambazo zipo katika jamii.
MHE. ESTER M. MMASI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo kimsingi yamejikita kwenye suala la msingi.
Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ni dhahiri kwamba kupitia miongozo ya Serikali juu ya mishahara na posho za waendeshaji na hata walimu wa vyuo vikuu Tanzania, ni kwamba iko mikondo mathalani PGSS 13, PGSS 14, PGSS 15, hizi ni kada ambazo zinapaswa kuongozwa na waendeshaji kwa maana ya kwamba siyo academicians. Practice iliyopo sasa hivi ni kwamba viwango hivi vya mishahara havitumiki kwenye kada husika kwa kuwa nafasi hizi za uongozi wa juu ni kwamba unaongozwa na academicians.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kutafsiri kiwango cha mshahara PGSS 13 ambayo inashikiliwa na Wakurugenzi ambao ni wanataaluma PGSS 14 na PGSS 15 ili viwango hivi viweze kutumika kwa waendeshaji wa vyuo vikuu au taasisi za elimu ya juu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Kama ambavyo nimejibu katika swali la msingi niende tu katika ufafanuzi wa ziada kwamba baada kuona kwamba kuna malalamiko aina hiyo na mengine kwa kweli katika vyuo vyetu mbalimbali hasa vyuo vikuu, Wizara kwa kuzingatia hilo, mwezi huu wa kumi ulioisha tumeunda vikundi kazi (team) kwa ajili ya kufuatilia hayo mambo yote katika vyuo vyetu vyote vikuu vikiwemo vyuo binafsi ili kuona kwamba kwanza vinaendeshwa kwa mujibu wa sheria, lakini pili uongozi unapangwa kutokana na taratibu na sifa zinazostahili, vilevile kuangalia miundombinu na maslahi kwa ujumla yanayohusu viongozi wa ngazi hizo kama yapo sahihi au hayapo sahihi. Bila kusahau hata watumishi wengine ambao hawaonekani kama ni watumishi muhimu (supporting staffs), kama wapishi, kuona kwamba je, chuo kinaweza kujiendesha kiuhalali au laa!
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nizidi tu kusema haya mapendekezo yako, unayozungumza nayo yatazingatiwa katika kutafakari masuala hayo.
MHE. DKT. ELLY M. MACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kusema tu kwamba sikuridhika kabisa na nina hakika watu wenye ulemavu hawakuridhika kabisa na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ambayo ameyatoa. Ina maana kwamba kwa kutokuwa na miundombinu au kutokuwa na watumishi ni sababu ya kutosha ya kusababisha vyuo vifungwe kwa miaka mingi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza. Naomba Mheshimiwa Naibu Waziri atupe concrete sababu kwa nini vyuo vimefungwa na vitafunguliwa lini, atupatie time frame.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, hawa watumishi ambao anasema wanatayarishwa, tunahitaji muda gani kuwatayarisha hawa watumishi kwa sababu watu wenye ulemavu wamekuwepo na vyuo vimekuwepo miaka mingi lakini vimefungwa kwa miaka mingi na inaonekana kama ni business as usual but it is not business as usual. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kimsingi, pamoja na kufungwa kwa vyuo hivyo jambo ambalo tayari limeshatolewa ufafanuzi namna gani litafanyika, kupitia mfumo wa elimu jumuishi sasa hivi vyuo vyote vya ufundi ikiwemo VETA, FDC lakini hata shule zinazotoa mafunzo ya ufundi tunahakikisha kwamba tunazingatia namna tunavyoweka miundombinu na namna ya kufundisha kwamba watu wenye ulemavu wanazingatiwa. Hao nawazungumzia hasa wale vijana wenye umri wa kuweza kuingia katika vyuo hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niseme tu kwamba, kwa hali ya sasa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia lakini pia kupitia ngazi zetu za juu kama tulivyoona Ofisi ya Waziri Mkuu, tunahakikisha kwamba walemavu wanapewa kipaumbele cha hali ya juu na yeye atakuwa shahidi hata sasa tunapotoa kwa mfano karatasi zetu humu Bungeni au taarifa zozote lazima tuzi-print kwa nukta nundu na mambo mengine. Kwa hiyo, walemavu wanapewa fursa nyingi na tunawajali kupita kiasi katika kila ngazi. Naomba atuvumilie aone namna ambavyo tutaweza kuendelea katika kuhakikisha tunarekebisha hali ambazo zipo.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa changamoto katika suala zima la elimu na hasa elimu jumuishi kwa watu wenye ulemavu ni kutokana na uhaba wa walimu katika vyuo mbalimbali hasa vyuo vikuu hapa nchini. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba katika vyuo vyote vikuu hapa nchini vinakuwa na programu mahsusi kabisa kwa ajili ya kuwafundisha walimu watakaokwenda kuwafundisha wanafunzi wenye ulemavu hapa nchini ili tuondokane na tatizo hili la uhaba wa walimu pamoja na kuhakikisha kwamba ajira zinakuwepo kwa watu wenye ulemavu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza ili kufanikisha hilo, kwa mfano ukiangalia katika utoaji wa mikopo safari hii watu wenye ulemavu wote kwa ujumla wake bila kujali fani anayochukua wamepewa mikopo. Pili, tunacho chuo maalum, Chuo cha Patandi - Arusha ambacho ni kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa walimu ambao wanaenda kuwafundisha wanafunzi wenye ulemavu. Hali kadhalika, kwa upande wa vyuo vikuu tunayo maeneo ambayo yanahusika katika kuzingatia ufundishaji wa walimu kwa ajili ya watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla wake niseme tu kwamba eneo hili ni pana sana kwa sababu linahitaji walimu wa aina tofauti tofauti kwa ajili ya kufundisha watu wenye ulemavu wa aina tofauti tofauti. Kwa hiyo, ukiwachukua kwa ujumla wake useme kwamba walimu wenye ulemavu labda 200 ukafikiria ni wengi, hawatakuwa wengi kwa sababu mahitaji ya wale wanaoenda kuwafundisha inakuwa wanafunzi ni wachache katika eneo fulani lakini yale maeneo ni mengi sana. Kwa hiyo, juzi tu mimi mwenyewe nimefuatilia pale Patandi na kuona ni jinsi gani tutaweza kurekebisha hasa miundombinu na kuwawezesha walimu wengi zaidi. Ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mawaziri, kuna hivi vyuo viwili Chuo cha Yombo na Chuo cha Singida, pamoja na uwepo wa vyuo hivi viwili lakini bado kuna changamoto nyingi sana ambazo zinavikabili vyuo hivi. Naomba niongelee specific Chuo cha Yombo kwa sababu ni chuo ambacho nimekitembelea. Chuo hiki kina changamoto ya deni kubwa la umeme, miundombinu chakavu pamoja na vifaa vya kujifunzia na kufundishia. Naomba nisikie kauli ya Serikali ni hatua gani za haraka na za makusudi za kunusuru vyuo hivi ili visije vikafungwa kama ambavyo vimefungwa hivi vyuo vingine? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa upande wa chuo hicho nikiri pia hata mimi nimewahi kukitembelea kilikuwa na upungufu fulani lakini kama ilivyozungumzwa na Ofisi ya Waziri Mkuu ni kwamba kimewekwa kwenye bajeti. Hata hivyo, kwa mwaka huu wa fedha tayari Wizara ya Elimu tulikuwa tumeagiza vifaa kwa ajili ya watu wenye ulemavu vya gharama ya shilingi takribani bilioni tatu na tayari vimeshawasili. Kwa hiyo, tutaangalia katika ugawaji na wao waweze kufikiriwa. Ahsante.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na kutotaka kuniona naomba niulize maswali madogo sana mawili ya nyongeza na niombe Waziri wa Fedha awe tayari kumsaidia Naibu Waziri. Ninachozungumza ni Kiswahili wala si Kihindi. Waziri wa Fedha ningeomba akainuka yeye maana hili swali linamhusu yeye. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge ni chombo kizito cha Tanzania na Watanzania wametutuma ili tuyasemee matatizo yao. Mheshimiwa Naibu Waziri au Waziri atakuwa yuko tayari kujiuzulu pindi nikimletea ushahidi wa kutosha juu ya suala hili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena, Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari kujiuzulu pindi nikimletea ushahidi wa kutosha juu ya kadhia hii kwa vijana wa Tanzania kutozwa fedha za kigeni katika vyuo hivyo na anajibu hapa hamna? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, je, amefanya utafiti kwenye vyuo gani mpaka akatueleza hakuna utaratibu wa kutoza fedha za kigeni ili Bunge lako liweze kuridhia tatizo hili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, swali la tatu, hakuna sheria…
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu yeyote anayekuwa hatendewi haki kwa mujibu wa sheria anayo fursa ya kuchukua hatua. Hatua mojawapo ni pamoja na kutoa taarifa kwa ngazi zinazohusika. Ndiyo maana nimesema kwamba kwa kipindi chote hiki Wizara yetu haijaweza kupata taarifa na hata wewe ulivyoendelea kuuliza umeshindwa hata kutuambia mfano wa chuo ambacho kinafanya hivyo. Kwa misingi hiyo, mimi nachukulia hilo suala halipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuhusiana na kufanya utafiti, ni sawa, ni jambo jema, hilo nalichukua kuendelea kulifanyia kazi.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili limekuwa likijirudia mara nyingi na naomba nitoe maelezo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Kigeni ya mwaka 1992 inamruhusu mtu yeyote kupokea na kumiliki na kutumia fedha za kigeni kwa shughuli za kiuchumi. Kwa hiyo, hao wenye shule siyo kwamba hawaruhusiwi, hilo la kwanza tuelewane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Sheria ya Benki Kuu ya mwaka 2006 inaweka bayana kabisa kwamba legal tender ya nchi yetu ni Shilingi ya Kitanzania. Nilikwishalieleza Bunge lako Tukufu kwamba ni makosa kwa mtu yeyote kukataa Shilingi ya Tanzania kwa malipo hapa nchini. Kwa hiyo, narudia tena, pale ambapo kuna Mtanzania yeyote anakwenda kulipa ada au malipo mengine akadaiwa kwa dola lakini yeye akatoa Shilingi za Kitanzania akakataliwa, atoe taarifa mara moja ili tuchukue hatua za kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine Benki Kuu tumeshafanya utafiti na nilikwishalitolea taarifa hapa ni 3% tu ya shughuli mbalimbali ambazo wana-quote bei zao kwa dola. Kwa hiyo, kosa ni kukataa shilingi kosa sio ku-quote bei zao kwa dola.
MHE. ALLY SALEH ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Zama hizi si rahisi kukataa kuja kwa wawekezaji kuwekeza katika shule za kigeni na vyuo vikuu mfano ni Shule za Sekondari kama Feza na nyinginezo. Serikali haioni kuna haja kwa utata huu unaotokezea, kwa mfano Chuo cha KIU, Chuo Kikuu cha Zanzibar kiliwahi kutoza kwa dola na Serikali inasema haijui kuwa na sera ya vyuo au shule zinazokuja hapa ili waelewe nini wafanye na nini wasifanye ikiwa ni pamoja na kutolazimishwa na nchi za kigeni kufunga shule kwa sababu ya maslahi yao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi vyuo vyote vimeshaelekezwa na vimejua nini wajibu wao kufuatana na kanuni na taratibu na sheria hizi. Labda jambo ambalo naweza nikalichukua ni kuendelea kuvikumbusha vyuo kama ambavyo tumekuwa tukifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutumia nafasi hii niombe tu kuvisisitiza vyuo pamoja na kwamba wanao uhuru huo wa kuweza kutumia fedha za kigeni lakini suala liwe ni kwamba mwananchi wa Tanzania sarafu yake ni Shilingi ya Kitanzania. Kwa hiyo, hiyo ipewe kipaumbele badala ya kutoa kipaumbele kwa fedha za kigeni.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukarabati unahitaji fedha za kutosha na Chuo Kikuu cha Mzumbe kwa muda mrefu kina madai halali sana kutoka Serikalini ambapo chuo kinaidai Serikali kama vile fedha za ada kutoka Bodi ya Mikopo. Fedha hizi zingeletwa mapema zingeweza kusaidia kufanya ukarabati. Je, ni lini sasa Serikali itaweza kulipa madeni haya ili Chuo Kikuu cha Mzumbe kiweze kufanya marekebisho haya madogo madogo na kukifanya chuo hiki kiweze kuwa na muonekano mzuri kuliko ilivyo sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kama ambavyo amezungumza Mheshimiwa Mbunge Dkt. Jasmine ni kweli kuna umuhimu mkubwa sana wa kufanya marekebisho katika chuo hiki, lakini pia katika suala la ada kuna wakati tulikuwa tumeagiza vyuo vyote kufanya uhakiki hasa kwa wale wanafunzi ambao walikuwa hawastahili kupata mikopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako, alishatoa maagizo kwamba Bodi ya Mikopo ipeleke fedha hizo wakati uhakiki ukiwa unaendelea ili wasikwamishe shughuli zinazoendelea. Kwa hiyo, naamini muda wowote ule hizo fedha watakuwa wamezipata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali imedhamiria kuona kwamba vyuo vyote vikuu vinaongezewa fedha ili kuongeza udahili unaostahili kwa wanafunzi ili kwenda kusoma kwenye chuo binafsi iwe ni hiyari zaidi ya mwanafunzi kuliko kuwa ni sababu ya kukosa nafasi katika vyuo vyetu vya Serikali. Kwa hiyo, naamini mpango huu ukikamilika hali itazidi kuwa nzuri zaidi kwa vyuo vyote ikiwepo Mzumbe.
MHE. SUSAN J. A. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Katika siku hizi za karibuni, Tanzania tumepata sifa kubwa sana ya kuwa na chuo kikubwa sana Afrika Mashariki na Kati, Chuo Kikuu cha Dodoma; na chuo hiki kinaweza kuchukua takribani wanafunzi 40,000. Kwa mshangao mkubwa sana, leo Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeamua kufanya Chuo Kikuu cha Dodoma kuwa sehemu ya majengo ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua, Serikali kwa kuleta utaratibu wa kubadili au wa kuchanganya wanafunzi na majengo ya Serikali (Wizara), maana yake ni kwamba tunachukua wanafunzi wetu kuwapekeleka kwenye simba. Nataka kujua huu ndiyo utaratibu wa kuhamia Dodoma kwa maana ya kubadilisha miundombinu ya elimu kuwa Ofisi za Serikali? Naomba majibu.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumfahamisha Mheshimiwa Suzan Lyimo kwamba pamoja na hayo aliyoyazungumza, ukweli ni kwamba chuo maana yake siyo majengo peke yake. Chuo maana yake ni majengo, Walimu pamoja na vitendea kazi vingine vya kufundisha na kufundishia. Kwa hali hiyo Chuo cha UDOM kilipojengwa kilijiwekea utaratibu wa namna gani kitakuwa kinakua sambamba na majengo. Kwa hiyo, kwa taasisi au Wizara kuhamia katika majengo haya ni kwa vile ni suala la muda mfupi na kwa sababu majengo hayo yalitokana na…
Kulingana na utaratibu na mipango yake ya kukua yalikuwa kwa sasa hayatumiki. Wizara zinatafutiwa maeneo yake ya kujenga, CDA wakishakamilisha kuleta viwanja hivyo, kila Wizara itakuwa na majengo yake katika eneo lake.
Kwa hiyo, niwaombe tu kwamba suala la kuhamia Dodoma, sisi kwetu tunaona ni suala lenye tija na litaongeza ufanisi mkubwa hasa kwa wananchi wetu kwa sababu sasa watakuwa wanapata huduma kiurahisi zaidi, ikizingatiwa kwamba Dodoma hata foleni hakuna na ni Makao Makuu ya nchi. Kwa hiyo, sisi Wizara tumejipanga na tutahakikisha kwamba tutahamia kwenye maeneo yetu muda ukifika.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa hapa ndani ya Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, naomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba nia ya Serikali katika kukiendeleza Chuo cha Dodoma ilijidhihirisha kutokana na nia njema ya Chama cha Mapinduzi kutoa ukumbi wake na kubadilisha matumizi kutoka kwenye matumizi ya Chama kuwa Chuo Kikuu cha Watanzania wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hatua hiyo hiyo ya nia njema ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi, tunaendelea na mpango wa Taifa wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya kuhamishia Serikali Dodoma. Naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge Majengo yatakayotumika na Serikali ni majengo ambayo Serikali ya Chama cha Mapinduzi ilishayajenga na yakawa mengi. Kwa sababu majengo yale ni mengi na yamejengwa na Serikali hii, badala ya kuyaacha yaharibike bila kutumika, yatatumika na baadhi ya Wizara za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, majengo yale hayaingiliani na shughuli zozote za elimu pale UDOM. Nawahakikishia Watanzania wote, nazipongeza Wizara hizo kwa kuyalinda kwa kuyatumia majengo hayo.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Kwanza, naishukuru Wizara ya Elimu iliweza kutoa fedha kwa ajili ya ukarabati wa Chuo cha Ualimu pale Korogwe ambapo kilileta wanachuo karibu 800 na kitu kwa ajili ya mafunzo pale. Hata hivyo, naiomba Serikali, kwa kuwa chuo kile kina maktaba ndogo na sisi wananchi tumeweza kujenga maktaba kubwa ambayo ingeweza kuwasaidia wanachuo ambao ni wengi sasa pale chuoni, pamoja na wananchi wa Korogwe kwa ujumla: Je, Serikali itakuwa tayari kutupa fedha ili tuweze kukamilisha lile jengo la maktaba?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Chatanda kwa kufuatilia masuala ya kielimu na Mheshimiwa Mbunge anapofanya jitihada kama hizo sisi Serikali tunao wajibu wa kusaidia. Kwa hiyo, tutachukua hilo jukumu la kusaidiana nao kuhakikisha maktaba hiyo inakamilika vizuri.
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi, nami naomba niulize swali dogo la nyongeza kuhusu Chuo Kikuu cha Mzumbe. Kwa kuwa Serikali inaongeza wanafunzi kila mwaka; na kwa kuwa kuna ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alipokuja Mzumbe kwamba Serikali itatoa fedha kwa ajili ya Ofisi za Walimu na nyumba za wafanyakazi; na kwa kuwa ahadi hiyo hadi leo haijatekelezwa.
Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne pamoja na kuongeza nyumba za watumishi pale main campus Mzumbe?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo ilielezwa hapo awali, niseme tu kwamba katika Vyuo Vikuu ambavyo vina kipaumbele katika uongezaji wa miundombinu kwa mwaka huu unaokuja wa fedha 2017/2018 ni pamoja na Chuo Kikuu cha Mzumbe. Kwa hiyo, naomba ajue hilo.
MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri.
Kwa kuwa kuna malalamiko makubwa yanayohusiana na kubainika kwamba kuna rushwa ya ngono katika vyuo vyetu, jambo ambalo linapelekea wasichana wengi kupata ufaulu mdogo, lakini vilevile wasichana wengine kutoroka shule, lakini kama haitoshi kuna wasichana ambao wamefanya maamuzi ya kujiua na ushahidi upo. Sasa je, Serikali ina mkakati gani wa kufanya utafiti ni kiasi gani wasichana wameathirika na rushwa ya ngono?(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wasichana wetu wanapatiwa elimu kuhusiana na rushwa ya ngono?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli taarifa hizo za rushwa za ngono zimekuwa zikisikika na hata hivi karibuni ilijitokeza taarifa ya aina hiyo kwa mwalimu mmoja ambaye ameendelea kuchukuliwa hatua na niseme tu kwamba suala la kufanya utafiti ni suala jema, mimi nichukulie kwamba ntalichukua ili kujifunza tatizo hilo kwa undani zaidi. Lakini niwaombe pia wanafunzi wa kike kutoa ushirikiano, lakini pia hata wanafunzi wa kiume wanaweza kusaidia kutoa ushirikiano kwa mambo ambayo yanajitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili katika suala la elimu, sisi wenyewe tumekuwa tukiongea na wanafunzi kupitia wakati tofauti tofauti tunapowatembelea, lakini pia nafahamu kuna taasisi mbalimbali zinazoshughulika na masuala ya kijinsia zimekuwa zikiendelea kuelimisha. Niwaombe pia hata Waheshimiwa Wabunge mnapopata nafasi muweze pia kuongea na wasichana hao ili kuweza kusaidiana kwa pamoja kuona kwamba wote tunakuwa pamoja katika kupigana na kupambana kwamba rushwa za ngono zisipatikane katika shule na hata katika maeneo ya kazi.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Suala la ufaulu wa watoto wa kike elimu ya juu inategemea na ufaulu wa watoto haohao wa kike kwenye shule za chini (O-Level na A-level), sasa kumekuwa na tatizo la watoto wa kike wanaobeba mimba wakiwa shuleni kuachishwa masomo, na hili tumekuwa tukilizungumza muda mrefu; ni lini Serikai italeta utaratibu hapa Bungeni, sheria itungwe ili watoto wa kike wanaobeba mimba shuleni wakishajifungua waruhusiwe kuendelea na shule?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hilo limezungumziwa katika nyakati tofauti tofauti, hivi karibuni pia tulipitisha mpango wa kushughulikia masuala yoyote yanayohusika na unyanyasaji kwa watoto wa kike na suala hilo limekuwa likishughulikiwa mia na Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na tayari rasimu ya mwanzo ya mwongozo imeshatoka namna gani tufanye na pia niliweza kwenda kutembelea Zanzibar kuongea na Mheshimiwa Waziri kule kuweza kujua wenzetu wamekuwa wakifanya vipi katika eneo hilo, tukajifunza changamoto ambazo zilikuwa zinajitokeza kwa upande wao kwa mfano mwingine anaweza akasema anapata mimba na aliyempa mimba akasema anataka kumuoa katika mazingira kama hayo. Lakini mwisho wa yote tunaamini kwamba tutaweza kutekeleza kuona kwamba fursa zinatolewa kwa mtoto wa kike aliyepata mimba kuweza kurudi shuleni.
Changamoto tu ni namna gani, je arudi kwenye shule ileile, je unyanyapaaji utakuwepo au apewe shule maalum, ndiyo hayo ambayo wadau mbalimbali wanaendelea kutoa mawazo lakini mwisho wa yote tutatekeleza mapema iwezekanavyo.
MHE. AMINA S. MOLELL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Katika vyuo vikuu suala la miundombinu kwa watu wenye ulemavu ni tatizo, na mfano katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni moja ya changamoto inayochangia wanafunzi wengi hasa watoto wa kike katika kwenda madarasani na hata katika suala zima la mitihani ni tatizo kwao kutokana na changamoto mbalimbali zilizopo. Je, Serikali inatoa kauli gani na hasa kwa kuzingatia chuo hiki ni kikongwe, lakini mpaka leo miundombinu bado ni tatizo na ni kikwazo kwa watu wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa mujibu wa sera kwa ajili ya watu wenye ulemavu, inazungumzia kuwawekea mazingira bora ya kujifunzia na kufundishiwa. Kwa hali ya sasa ni kwamba tunayo majengo ambayo yamejengwa zamani na unakuta kweli yana changamoto ya miundombinu, lakini tunachofanya ni kwamba tunashauri madarasa yale yenye wanafunzi wenye ulemavu wahakikishe yanakuwa ni yale yanayofikika, kwa mfano kama darasa lina mwanafunzi mwenye ulemavu ni vyema likachaguliwa lile ambalo liko katika ground floor ili mwanafunzi yule aweze kufika darasani bila usumbufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa majengo yote mapya yanayojengwa tumeagiza kwamba lazima kila jengo liwekewe miundombinu inayomuwezesha mtu mwenye ulemavu kufikia katika eneo lolote analohitaji kuishi au kujifunzia na hivyo imekuwa ikifanyika na ni rai yangu kusema kwamba hata hiyo miundombinu inayowekwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu iwe ni ile inayozingatia viwango vinavyohusika, kwa sabau sasa hivi unakuta kwamba kuna shule zinapokaguliwa ili zionyeshe miundombinu yenye ulemavu zinaweza zikaonesha tu kwamba kuna lile tuta (rump) limewekwa pale lakini unakuta jinsi ambavyo limewekwa lina msimamo mkubwa kiasi kwamba hata huyo mtu mwenye ulemavu anapata shida, kwa hiyo lazima kuzingatia viwango vinavyohusika katika kuweka miundombinu ya watu wenye ulemavu ikiwemo kuweka lifti. ahsante.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupewa
nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Pamoja na majibu
mazuri ya Serikali nina maswali mawili.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja, kwa kuwa lengo la Serikali ilikuwa ni
kujenga VETA kila Wilaya ili vijana wetu waweze kupata mafunzo, vijana ambao
wanakuwa wameshindwa kuendelea na vyuo vikuu na kadhalika. Je, sasa
Serikali imejipangaje kuhakikisha inakamilisha azma yake iliyopanga ya kujenga
chuo cha VETA kila Wilaya?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, pamoja na majibu mazuri kama
nilivyosema ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Serikali kwa majibu yake imesema kule
Njombe tuna Chuo cha Ulembwe pale ambacho kinamilikiwa na Wilaya yetu ya
Njombe. Je, Serikali sasa kwa majibu haya imejipangaje kuhakikisha chuo hiki
kinaboreshwa kama walivyosema ili wananchi wa Wilaya ya Njombe hususan
pamoja na Jimbo la Makambako, vijana hawa waweze kwenda kusoma chuo
hiki cha VETA ambacho kiko pale Ulembwe?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika,
ahsante sana. Serikali imeendelea na hiyo mikakati, lakini niseme tu kwamba
kujenga chuo kimoja cha VETA ni gharama. Kwa hiyo, kwa kutumia fursa hii
kwamba Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDC’s) navyo sasa hivi
vimerudishwa katika Wizara yetu. Tunaangalia katika Wilaya ile ambayo ina chuo
cha aina hiyo basi kiweze kuboreshwa na kiweze kuchukua nafasi ya mafunzo
ambayo yatakuwa yanatolewa yanayowahusu wale wananchi wote bila kujali
sifa zao ili mradi wana akili timamu lakini hali kadhalika kwa wale ambao
wanahitaji mafunzo yale yanayofanana na yanayotolewa katika VETA yaweze
kupatikana, tayari tumeshaanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika Mkoa wa Kagera, chuo cha
Gera tayari sasa hivi kimeshafanyiwa ukarabati, lakini pia Rubondo tumeshaanza
kufanya ukarabati, kuna Kibondo, Kasulu na maeneo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwa upande wa Ulembwe tutahakikisha
kwamba chuo hicho kinaboreshwa. Niwafahamishe tu kwamba ili tusifanye kazi
ambazo hazina tija, tayari Wizara imeshapanga kukutana na Wakuu wa Vyuo
vyote vya FDC’s ili kuweza kukaa pamoja na kufahamu kwa undani changamoto
zilizowakabili kabla hatujatoa fedha za kwenda kukamilisha au kuanza uboreshaji
wa vyuo hivyo.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana
kwa kunipa fursa hii ili niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa Serikali iliwahi
kutoa orodha ya Wilaya za kipaumbele za ujenzi wa vyuo vya VETA na katika
orodha ile Wilaya ya Mkinga ilikuwa ni miongoni mwa Wilaya hizo. Je, ni lini sasa
Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga chuo kile kule Mkinga?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu
Spika, ni kweli Serikali inatambua hilo na hata tunapojibu maswali ya VETA
tunajua tutapambana nna swali la Mkinga. Nimfahamishe tu kwamba katika
vipaumbele vya Serikali bado Mkinga iko pale pale. Tukipata fedha tunaamini
kwamba tutatekeleza.
MHE. ANTHONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Kwa kuwa, wananchi wa Moshi Vijijini kule Tarafa ya Kibosho katika Kata sita,
Kata ya Kirima, Kibosho Kati, Okaoni, Kibosho Magharibi na Kibosho Mashariki
wameshaitikia huu wito na kujenga chuo ambacho kwa kweli kina hadhi kubwa
sana na kinaweza hata kubeba Wilaya kama mbili, tatu. Waziri atakuwa tayari
kwenda na mimi kule kwenda kuona hiki chuo na kukiwekea utaratibu mzuri,
maana naamini akienda kule ataweza kukiwekea utaratibu mzuri wa kukipa
ruzuku kama Walimu na kadhalika?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu
Spika, kwanza nawapongeza wananchi kwa kutambua umuhimu wa stadi za
kazi kwa wanafunzi wa vyuo hivyo.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa
kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo la uhaba wa vyuo vya ufundi
na ahadi imekuwa ni ya muda mrefu na tatizo ni la muda mrefu. Katika
Halmashauri ya Wilaya ya Msalala tumekwishaanza juhudi za kufanya au
kutekeleza jambo hili. Kwa bahati nzuri kwa mazingira yetu tuna mgodi wa
Bulyanhulu ambao vijana wengi sana wanakosa fursa za kufanya kazi pale kwa
sababu ya kukosa elimu fulani ya ufundi na mgodi umeonesha nia ya kushirikiana
na Serikali kuutekeleza mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumwomba au kumuuliza swali
Mheshimiwa Waziri kwamba anaonaje akitusaidia katika kutia chachu
mazungumzo kati ya Halmashauri ya mgodi ili kuweza kutekeleza mradi huu kwa
yeye mwenyewe kufika na kukaa na watu wa mgodi ili kuona namna gani
tunaweza tukatekeleza mradi ambao tayari eneo lilishapatikana muda mrefu
kwenye Kijiji cha Bugarama?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu
Spika, ahsante. Niseme tu kwamba kwanza nawapongeza hao wadau wa
madini kwenye migodi wanavyotu- support katika masuala ya elimu kwa Mkoa
wa Shinyanga na Msalala nadhani ikiwa ni wanufaika wamojawapo. Kwa hiyo,
kama kuna jitihada za aina hiyo Wizara pia tuko tayari. Hata hivyo, niseme tu
kwamba Msalala mtakuwa hamjapungukiwa sana kwa sababu tayari kuna chuo
cha VETA kiko Shinyanga ambacho pia kinajihusisha na masuala ya madini.
Vilevile tunategemea kujenga chuo ambacho kitakuwa ni cha Mkoa katika
Mkoa wa Geita ambapo pia ni jirani zenu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hizo jitihada nitakuwa tayari kushirikiana
nanyi kuweza kuomba kama kuna huo uwezekano.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, nashukuru kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kama ambavyo Naibu Waziri amesema kwamba chuo kile kina uwezo wa kudahili wanachuo 1,200 na ameeleza mwenyewe kwamba 2015/2016 kilidahili wanachuo 234. Kutokana na miundombinu na rasilimali iliyopo pale, kuwa na wanafunzi 234 kati ya 1,200 hatuoni kwamba hatukitendei haki chuo hiki?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kuna utaratibu ule wa kuwadahili kupitia mtandao na huko vijijini hakuna mitandao kwa nini isirejee utaratibu wa kuandika barua pamoja na kutumia hizo internet kwa wenzetu walioko mijini ili watoto wa wanavijiji na wenyewe waweze kupata hizi nafasi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, zamani utaratibu ulikuwepo wanafunzi ambao wako shuleni walikuwa wakiomba nafasi za ualimu wakiwa shuleni. Je, kwa nini wasirudishe utaratibu huo mtu aweze kuomba akiwa shuleni ili tuweze kupata wanachuo wa kutosha kuliko kuwa na chuo ambacho kinataka wanafunzi 1,200 halafu wanadahili wanachuo 234?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli baada ya kuboreka kwa miundombinu hiyo, Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba chuo hicho kinachukua wanafunzi wanaostahili kuwepo. Ieleweke kwamba baada ya kubadilisha hizo sifa kwanza hali ya ufaulu wa wanafunzi katika shule zetu ulikuwa uko chini lakini pia kutokana na mambo ambayo yalikuwa yanachangiwa humu Bungeni juu ya sifa za Mwalimu, kwa sababu ilikuwa inaonekana kwamba ualimu anapelekwa mtu mwenye sifa hafifu, kwa hiyo, Wizara ilifanya marekebisho na kuona kwamba sasa sifa ziwe mwisho ni daraja la III.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali hiyo, kwa mwaka wa kwanza tulikuwa na wachache lakini kwa sasa hali ya ufaulu imeboreka kutoka katika shule zetu za Serikali na zisizo za Serikali kwa hiyo, tunao wanafunzi wengi ambao wanaweza kupelekwa huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika niseme tu kwamba katika suala la udahili tunaliangalia na Kamati yetu ya Huduma ya Jamii imelizungumza sana. Tunaangalia namna bora ya kudahili bila kupoteza dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kuwa ubora unalindwa. Kwa hiyo, tutafikia maamuzi baada ya tafiti zinazoendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kuwapeleka wanafunzi moja kwa moja kutoka shuleni ni kwamba wanafunzi hao ni mpaka wawe wameshafanya mitihani na wengine wanachukuliwa kutoka katika ngazi mbalimbali za uombaji, kwa hiyo, matokeo yao ndiyo yanayowapeleka huko siyo tu ilimradi yuko pale shuleni na aanze kujaza. Kwa hiyo, suala ni kuhakikisha kwamba wanafunzi wanaopelekwa katika Chuo cha Korogwe na vyuo vingine vyote ni wale wenye vigezo vya ubora unaohitajika.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nitaongea kwa kifupi. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na napenda tu kuongezea jambo dogo kwamba, suala hili la vyuo vya ualimu kuwa na wanafunzi wachache kuliko uwezo wake lilitokana na uamuzi wa kuwapeleka wanafunzi UDOM ambapo ilisababisha mlundikano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kulihakikishia Bunge lako Tukufu yale mambo yaliyokuwa yanasemwa kwamba Serikali iliwaondoa wanafunzi UDOM ili ipate nafasi siyo kweli kwa sababu iliona ni vizuri, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba Vyuo vya Ualimu vichukue wanafunzi kulingana na uwezo wake. Nashukuru.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nataka kuuliza swali la nyongeza kuhusiana na elimu Mkoa wa Katavi. Ukosefu wa Chuo Kikuu cha Kilimo Mkoa wa Katavi umeleta usumbufu kwa wananchi wa Katavi. Serikali ilitenga pesa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Kilimo lakini chuo hicho kimeyeyuka. Ni nini mkakati wa Serikali kufuatilia zile pesa zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Kilimo Mkoa wa Katavi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Chuo kikuu kilichokuwa kinategemewa cha Mkoa wa Katavi kilikuwa kinadhamiriwa kujengwa kwa ushirikiano wa Halmashauri ya Mpanda pamoja na wawekezaji ambao walikuwa ameingia nao ubia. Kwanza katika taratibu zilizokuwa zinaendelea kulikuwa na suala la mbia kutaka kupewa dhamana ya Serikali katika kujenga chuo hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo tuliona kwamba, kama mtu anahitaji kujenga chuo, wakati yeye tunategemea kwamba ni mwekezaji kwa maana kwamba atakuja kuwekeza katika kile chuo, dhamana ya Serikali inaweza ikasababisha mtu kuchukua deni mahali na kukimbia na kazi isiwe imefanyika. Ni vema mwekezaji awe ni mwekezaji wa kweli na awekeze kadri inavyotakiwa. Hata hivyo, kwa fedha zilizotolewa Halmashauri ya Mpanda inafahamu juu ya mambo yake na hivyo kwa kutumia Baraza lao wafuatilie na kuona kwamba fedha zao hazipotei.
MHE. ZAYNAB M. VULLU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwanza niseme nilitarajia angeniambia Mwongozo huo utaanza lini ukizingatia Wizara inaongozwa na Waziri mwanamke, Naibu Waziri mwanamke na Katibu Mkuu mwanamke. Je, Sheria ile ya SOSPA haoni kwamba inakinzana na sera ambayo wanaleta na vipi mtawasaidia hao watoto waweze kuendelea na utaratibu ambao mmeuweka? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa mtoto wa kike na wanawake wote kibaiolojia kuna siku ambazo lazima tuzitumikie. Watoto wa shule wengi wanaacha kwenda shule kati ya siku sita mpaka saba, ukipiga kwa mwaka mmoja mtoto wa kike anapoteza zaidi ya siku 60 au 70. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kuweza kupeleka mataulo ya kuweza kuwasaidia na kutenga chumba maalum kwa ajili ya wao kuweza kujihifadhi wakati wanapohitaji?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nikiri kwamba ni heshima kubwa sana Wizara yetu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupewa sisi wanawake kuiongoza ambao tuko jirani sana na mahitaji au matatizo ya wanawake na ndiyo maana tunasema kwamba mwongozo tayari umeshaandaliwa. Kama mazungumzo yote tunayoendelea kuyafuatilia yatakuwa yamekamilika, tunatarajia tarehe Mosi, Machi, 2017 mwongozo huo uwe umekamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wanawake ni mtambuka. Tunapozungumzia kuwawezesha vijana katika demokrasia na katika kushiriki shughuli mbalimbali za kiuongozi, tunachozungumzia ni kwamba lazima watoto wa kike wasiachwe nyuma. Kutokuwa na sehemu za kujihifadhia wanapokuwa shuleni ni tatizo. Mwongozo ulishatolewa kwamba kila shule lazima itenge chumba maalum kwa ajili ya wanafunzi hao kujihifadhia wakati maalum lakini hali kadhalika tunasema kwamba hata hizi fedha za elimu bure zinazotolewa ni vema ikatengwa sehemu ndogo kwa ajili ya kuwasaidia hawa watoto wa kike pale inapotokea mambo yametokea kwa dharura.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema bila kuficha wapate pedi zao kwa sababu tumekuwa tukificha mambo haya ya wanawake, matokeo yake hata kwenye bajeti hayawekwi. Tuseme wazi kwamba mahitaji ya mwanamke ikiwemo pedi ziwekwe kwenye bajeti ili hawa watoto wa kike waweze kusaidiwa.

WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee jibu zuri la Naibu Waziri. Napenda nitoe taarifa kwa Bunge lako Tukufu kwamba imekuja teknolojia ambapo taulo nzuri za bei nafuu zitatengenezwa. Zaidi nitoe taarifa kwamba kuna Wabunge wawili wamejasiria, tunawaongoza kusudi watengeneze viwanda hivyo.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Nami niulize swali la nyongeza kutokana na swali la msingi la Mheshimiwa Zaynab Vullu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imalize tatizo la watoto wanaopata mimba kuendelea na masomo. Tunajisikia vibaya sisi Watanzania wanawake, kwa mfano, chukua Zanzibar, Zanzibar mtoto wa kike akipata ujauzito wanaruhusu anaendelea na masomo. Zambia, Kenya, sisi ndiyo tumebaki peke yetu wa mwisho kwa nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashangaa, kwa kifupi tu, taarifa zinatolewa kila siku watoto 30 wamepata mimba, watoto 20 wamepata mimba, hivi mnaona ninyi raha kutangaza kila siku na wasababishaji mnawajua ninyi wenyewe? Iliyobaki hawa watoto waruhusiwe wakasome, hakuna mjadala hapa.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lolote lile linapotekelezwa ili litekelezwe kikamilifu ni vema wadau wote wakawa pamoja. Sisi wanawake pamoja na hao wanafunzi wa kike hatuishi kwenye jamii peke yetu. Katika utekelezaji wa suala hili si tu kwamba maadam tukisema wanafunzi warudi shuleni basi unakuwa unasema umesema wakati hujui utekelezaji utakuwaje. Ndiyo maana tumewashirikisha…

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Tulieni. Kama majibu ninayo mimi basi sikilizeni. Nasema hivi suala hili linahitaji Wabunge wote kuwa on board kwa misingi kwamba…

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Na msisahau sisi wenyewe tulitunga sheria ya kuhakikisha kwamba yule anayetoa ujauzito kwa mtoto wa shule achukuliwe hatua.

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Sasa kama ndivyo tumetunga hiyo sheria bila kuwa na ushirikishwaji na utaratibu maalum wa kuwapata hao wanaoendelea kutoa ujauzito kwa watoto wa shule, utaratibu vipi? Ndiyo maana tunataka sekta zetu zote, wadau wote, tuwe na uratibu wa kuweza kukabiliana na mambo yote mawili.

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Kwa hali hiyo, wanafunzi watarudi shuleni lakini wakati huo huo lazima taratibu zetu za msingi za kufanya uratibu katika maeneo yote ikiwemo utoaji wa adhabu hasa wale akinababa ambao wanawanyemelea watoto wa shule uweze kuendelea.
MHE. SOPHIA M. SIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi alivyojibu kwa umakini sana na hususani pale alipozungumzia kwamba walimu wanapata mafunzo zaidi, refresher course ambazo kwa kweli wengi wanazihitaji. Lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiuliza Serikali je, haioni kwamba kuanza kutumia kiingereza kama lugha ya kufundishia kuanzia masomo ya sekondari inasababisha kuleta ugumu sana kwa wanafunzi na matokeo yake wanakuwa wanakariri hasa katika masomo ya sayansi na teknolojia, kitu ambacho kinapelekea wasifanye vizuri sana katika masomo hayo wakati wa mitihani yao, na wale ambao wapo kwenye shule za private wanafanya vizuri zaidi? Sisemi shule zote, lakini hii ni sababu mojawapo ya shule za sekondari za private kufanya vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali haioni kwamba upo umuhimu wa kipekee kabisa kuhakikisha kiingereza kinatiliwa mkazo kwa sababu kwenye soko la ajira mara nyingi unaona inatokea kwamba interview zinafanywa kwa kiingereza. Hata mashirika mengine ya umma wakienda vijana interview unawauliza mmefanyiwaje anasema ni kwa kiingereza. Isitoshe sisi tunawakaribisha wawekezaji lakini wale wawekezaji wanahitaji wale ambao wana lugha ya pili ambayo ni kiingereza ili ku-communicate. Je, Serikali haioni kwamba tunapoteza ajira nyingi kutokana na ukosefu wa kujiamini wa kuongea lugha ya kiingereza na matokeo yake uakuta hata kwenye EPZ wako Wakenya, Waganda na Wazimbabwe wameajiriwa na mashirika haya ya uwekezaji. Naomba anijibu hilo tunafanya nini, ajira zinapotea. Ahsante sana
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda ifahamike lugha ya kiswahili ni lugha ambayo ni lugha ya taifa, na ni lugha ambayo inafahamika na wananchi wengi toka wakiwa wadogo. Mwanafunzi anapofundishwa lugha ambayo ameiozoea na amezaliwa nayo ni rahisi zaidi kupokea mitaala anayowekewa kuliko pale ambapo unamfundishia lugha mpya kabisa. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa misingi hiyo tunasema kwamba, sisi kwa kuzingatia kwamba kiswahili ndiyo lugha yetu ya msingi tunasema kwamba mtoto aanze kufundishwa kwa lugha hiyo, lakini mara anapofika darasa la tatu dozi ya kiingereza inaanza kuongezeka kama nilivyosema mpaka kufikia vyuo vikuu. Kwa siku za nyuma kulikuwa na upungufu zaidi kwa sababu unakuta kwamba walimu walikuwa wanaweza kufundisha somo la Kiingereza hata kama alikuwa hana ufaulu wa kutosha. Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile unakuta mwalimu mmoja alikuwa anafundisha masomo mengi. Kadiri tunavyoenda na kuimarisha sifa za walimu na kuongeza idadi ya walimu kutakuwa na specialization kiasi kwamba sasa mwalimu atakuwa anafundisha somo husika na somo alilofaulu na hivyo kiingereza kitazidi kuimarika. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa upande wa suala la kukosa ajira nipende tu kusema ukweli kwamba kiingereza kimekuwa kikiendelea kuzingatiwa; na niseme tu kwamba kwetu Watanzania yawezekana pengine unyanyapaaji wetu nao unachangia katika kuwafanya watoto waogope somo la kiingereza; na kila wakati kutokujiamini na kutokuzungumza kiingereza kwa hofu kwamba nitaambiwa sijui kiingereza. Mimi nasema kwamba kiingereza ni lugha sawa na lugha nyingine, mtu zungumza bila uoga sawa na ambavyo wengine wanaweza kujaribu kuzungumza kiswahili bila uoga na watu tunaelewana. Mheshimiwa Mwenyekiti, serikali itaendelea kuweka mikakati ya kuboresha somo la kiingereza katika shule na kuongeza mijadala katika shule au midahalo, lakini vilevile kupata hata wataalam mbalimbali wanaopenda kuja kujitolea katika nchi yetu kutoka nchi mbalimbali. Kwa hiyo, niwaombe wote tushikamane kuona kwamba lugha hii ya pili ambayo itatusaidia zaidi katika masuala ya mawasiliano hasa ya kibiashara ili nayo iweze kupata nguvu sawa na ambavyo tunasisitiza katika lugha yetu nzuri lugha ya kiswahili, lugha ambayo ni ya upendo na upole. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hali kadhalika tunasema kwamba bado lazima tuongeze jitihada hata katika lugha za alama kwa sababu huyu mwanafunzi si kiingereza peke yake, ni pamoja na lugha ya alama…
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika,
nashukuru. Pamoja na majibu ya Serikali, lakini naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza:-
Mheshimiwa Spika, kwa mfano tu Wilaya ya Same mwaka 2016, wasichana wadogo waliopata mimba na kufukuzwa shule ni 64 ambao hawa ni wa O-Level ikiwa ina maana mimba hizi ni za utotoni. Mwaka huu 2017 mwezi wa Kwanza, wa Pili na wa Tatu, miezi mitatu tu wamefukuzwa wanafunzi wa shule kwa mimba za utotoni 42 na kati ya hao akiwepo mtoto wa darasa la sita ikiwa ina maana ni kati ya miaka 12 mpaka 14.
Mheshimiwa Spika, hivi Serikali haioni kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kuwa na mitaala ambayo itawafundisha watoto hawa kuanzia shule ya msingi mpaka sekondari, ambayo itawafanya waelewe athari za kupata mimba utotoni ambazo ni muhimu sana? Mitaala hii itaweza kuwasaidia watoto hawa kujitambua na kufahamu umuhimu wa kutokukubali kupata mimba utotoni.
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali
inafanya jitihada kubwa sana kupambana na madawa ya kulevya sasa hivi na naiunga mkono, nai-support na tunashukuru sana. Jitihada hii ni kwa sababu Serikali imeona athari hasa inayowapata vijana wa kiume na wa kike kwa
kutumia madawa ya kulevya, lakini watoto wa kike
wanapata athari mara mbili, kwanza athari ya madawa ya kulevya na mimba za utotoni.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuleta mkakati
mkubwa kama ule wa madawa ya kulevya ili tupunguze athari za mimba za utotoni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali linalohusiana na masuala ya mitaala kama ifuatavyo:-
Kimsingi katika elimu ya Msingi na elimu ya Sekondari wanafunzi wanapewa maarifa kuhusiana na masuala ya Kibaiolojia na sayansi yanayohusisha hata masuala ya maumbile ya miili yao, kwa hiyo kimsingi suala hilo linafanyika labda tunaloweza kuahidi hapa ni kutoa msisitizo wa kuona kwamba wanafunzi hao wanapewa dozi zaidi hasa kwa kuwachukua hawa watoto wa kike na kuwapa elimu ya ziada kwa ajili ya kuwanusuru katika mazingira hayo.

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza tunao mpango wa kudhibiti ukatili dhidi ya wanawake na watoto ambao ni jumuishi kwa sekta takribani tisa za Serikali yetu na mpango huu umezinduliwa mwaka jana mwezi Desemba na Mawaziri tisa wa Serikali hii ya Awamu ya Tano na Mawaziri wameonesha comittment kubwa sana ya kuweka utaratibu
wa kumlinda mtoto wa kike dhidi ya ndoa za utotoni lakini pia mimba za utotoni na vitendo vyote vinavyohusu ukatili dhidi ya wanawake na watoto wa kike.
Mheshimiwa Spika, tunachokihitaji kwa sasa ni
kupewa fedha kwa ajili ya kutekeleza mpango huo na kwenye mpango huu tunalenga kupunguza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto kwa kiwango cha asilimia isiyopungua 50 kufikia mwaka 2022. Kwa hivyo, mpango huu kama tutapangiwa fedha, tunapanga kuanza kuutekeleza mwezi Julai mwaka 2017. Kwa hivyo, mpango tunao pia tuna mikakati mbalimbali inayoendelea kama ya elimu ya malezi chanya (Positive Parenting Education) kwa watoto ambao umefanyika kwenye Wilaya 72 za Nchi yetu
na tunawalenga zaidi viongozi wa kimila, wazazi pamoja na watu mashuhuri wenye kufanya maamuzi kwenye jamii.
MHE. MATTAR ALI SALUM: Mheshimiwa Mweyekiti, ahsante sana kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nisawazishe jina langu, mimi naitwa Mattar Ali Salum, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri akilijibu alijibu vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake ambayo ameyatoa.
Mheshimiwa Waziri, wapo wanafunzi wanaendelea kupata mikopo ya Serikali kwa kima kidogo hadi sasa, husababisha kukosa kukidhi mahitaji ya vyuo husika ambavyo wamepangiwa. Je, Serikali ni kwa nini isiwaongezee fedha wanafunzi hawa ili waweze kukidhi mahitaji ya vyuo husika?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wako wanafunzi walikuwa wakipata mikopo kwa kipindi kirefu, ghafla Serikali imewafutia mikopo yao, sijui ni kwa nini. Je, Mheshimiwa Waziri, Serikali ina mpango gani wa kuwarejeshea mikopo hawa wanafunzi ili waweze kukidhi na kuendelea na masomo yao vizuri? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama alivyorekebisha jina lake, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba kiuhalisiatulingependa kutoa mikopo kwa wanafunzi wengi zaidi, lakini vilevile ingewezekana hata kila mwanafunzi akapata mkopo kwa kadiri ya mahitaji ya chuo anachosoma; lakini kwa sababu fedha hazitoshi inakuwa ni vigumu kufanya hivyo na tunaangalia zaidi ni uhitaji wa kiasi gani upo.
Kwa hiyo, kwa misingi hiyo niseme tu kwamba, Serikali itaendelea kutenga fedha ya kuona kwamba, inawasaidia wanafunzi wengi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuhusu kufuta mikopo. Ni kweli kuna baadhi ya wanafunzi walifutiwa mikopo kutokana na kutokuwa na vigezo vinavyostahili. Hata hivyo Serikali imeendelea kulifanyia kazi suala hilo ili kuona kwamba, anayefutiwa mkopo iwe kweli ni mtu ambaye hana uhitaji. Kwa yule mwenye uhitaji na kwamba vigezo vyote vimetimia basi, baadhi yao tumeweza pia kuwarejeshea.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza na nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, nini commitment ya Serikali juu ya kuwapandisha madaraja watumishi hawa kwa wakati?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, katika bajeti ya mwaka huu, Serikali imetenga kiasi gani cha fedha ili kuondoa adha hii wanayoipata walimu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, kimsingi ni kwamba kama ambavyo tumekuwa tukizungumza kila wakati ni kwamba madaraja ya watumishi husika ikiwemo walimu yatakuwa yanapandishwa mara baada ya zoezi la uhakiki ambalo pengine wengine hawapendi kulisikia lakini ni zoezi muhimu sana litakapokamilika. Kwa hiyo, nikuhakikishie tu kwamba mara zoezi hilo likishakamilika tutafanya hivyo.
Mheshimiwa Spika, lakini la pili kuhusiana na kiasi gani cha bajeti kimetengwa, naomba tusiiwahishe
shughuli, siku yetu ya bajeti mtapata majibu mazuri zaidi. Ahsante sana.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika majibu yake ya msingi amesema kwamba ziko fedha ambazo zimelipwa kwa madai ya walimu lakini ni kidogo sana kuendana na madai halisi ya walimu wa Tanzania kwa miaka karibu mitatu iliyopita. Kwa Wilaya ya Kaliua tu walimu wa sekondari wanadai shilingi 221,347,561 kwa mwaka 2015/2016 tu. Ni lini sasa madai haya ya walimu kwa Wilaya ya Kaliua yatalipwa kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, kimsingi tunatambua kwamba kuna madeni ya walimu lakini naomba pia mnikubalie kwamba kweli kuna baadhi ya madeni sio madeni halali. Uzoefu unaonesha kwamba baada ya uhakiki kuna baadhi ya madeni yanashuka mpaka kufikia moja ya tatu kitu ambacho kinasikitisha na kimekuwa kikichelewesha kuwalipa walimu kwa wakati pamoja na watumishi wengine.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni rai yangu kwa watumishi wote waone jambo la kulipwa ni haki yao lakini vilevile ni vyema madai yakawa halali ili kuepusha usumbufu usio wa lazima. Haipendezi sana mtu umedai halafu baadaye unaambiwa hayo madai hayastahili kwa sababu taratibu na kanuni zetu tunazijua na hivyo unaweza ukajua ni kipi unastahili na kipi hustahili.
Kwa hiyo, niseme tu kwamba kwa maneno ya Mheshimiwa Mbunge tutajitahidi kufuatilia katika Wilaya au Jimbo lako kuona kwamba hawa watumishi wanaostahili kulipwa waweze kulipwa kwa wakati baada ya uhakiki.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa swali la msingi linaulizia vitendea kazi vya elimu, ubora wa elimu, pamoja na mazingira yake yote ambayo ni elimu kwa wote, shirikishi na yenye ubora; mwaka 2013 tarehe 2 Machi siku ya Jumamosi, Mheshimiwa Rais aliunda Tume ya Sifuni Mchome ya kuangalia vigezo vyote hivi. Tarehe 31 hoja binafsi ilikuwa Bungeni kuhusu vigezo vyote hivi. Je, ni lini Serikali italeta ile ripoti ya Tume ya Sifuni Mchome hapa Bungeni ili Wabunge tuweze tukaishauri vizuri Serikali kuhusu ubora wa elimu Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni kweli nafahamu kuna hiyo Tume ilikuwa imeundwa na kuna baadhi ya mambo ambayo yalikuwa yameelezwa kwenye ile Tume; lakini baada ya hapo kuna team mbalimbali ziliundwa ambazo pia nyingine zilikuja kuona hata baadhi ya mapendekezo pengine hayako sawa; yaani hayaendani sawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wizara tumekuwa tukiendelea kufanya marekebisho kulingana na mahitaji, kwa mfano katika suala la utoaji wa tuzo. Mwanzo zilikuwa zinatumia GPA, sasa hivi tumerudi tena kwenye division. Kwa hiyo, kuna mambo mengi tu ambayo yamekuwa yakifanyiwa kazi kila wakati. Hata hivyo, siyo tatizo kuweza kuwaonesha Waheshimiwa Wabunge nini kilikuwa kimezungumzwa kwenye Tume, lakini pia mabadiliko yanayoendana na uhalisia wa sasa yaliyofanyika.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza nampongeza Waziri wa Elimu na Naibu wake na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa basi, Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari kufuatana nami ili aweze kuangalia lile jengo ili kusudi waweze kutoa kitu ambacho kinalingana na kazi ambayo inakusudiwa kumaliziwa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jibu ni ndiyooo! (Makofi)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Kwa kuwa takwimu za mwaka 2016 zinaonyesha kwamba Watanzania ambao ni zaidi ya miaka 15 na ambao hawazidi miaka 54 wako takribani milioni 25 na kuendelea; na kwa kuwa asilimia 22.4 ni kubwa sana, maana yake ni kwamba karibu takribani watu 5,813,066 hawajui kusoma na kuandika.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kurudisha sasa vituo vya kufundishia kama ilivyokuwa zamani katika kila kijiji, kwa sababu tatizo hili ni kubwa sana na hasa katika Jimbo la Vwawa na maeneo mengine nchini?
Swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri umesema kwamba mmeziagiza Halimashauri kutenga fedha ili wahakikishe kwamba huo mfumo wa KKK unatekelezwa.
Je, mmeweka mkakati gani wa kuhakikisha kwamba kutakuwa na uwajibikaji na ufuatiliaji wa utekelezaji wa agizo hili?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Hasunga kwa kuridhika na majibu yetu ya awali, pia kwa majibu yanayofuata ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi ni kwamba kila mahali kwenye taasisi ya elimu, iwe ni shule ya msingi, iwe ni sekondari, iwe ni chuo ni kituo halali cha watu wasiojua kusoma na kuandika kuweza kupata elimu au mahali pa kujifunza.
Vilevile Wizara baada ya kutembea na kuona kwamba eneo hilo bado lina uhitaji mkubwa, tumeshaweka mikakati ya kuona kwamba elimu ya watu wazima inapewa kipaumbele na kuona kwamba wananchi wetu wa Tanzania tupungue ikiwezekana angalau tufikie asilimia tano mwaka 2025.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na ufuatiliaji katika Halmashauri ili kuhakikisha kwamba wanatimiza wajibu wao, niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge kwa kuwa sisi sote ni Madiwani kwenye Halmashauri zetu, basi tuone umuhimu wa kutenga fedha kwa ajili ya shughuli hiyo ya kuhakikisha wenzetu wote wanajua kusoma, kuandika na kuhesabu.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swlai dogo la nyongeza. Kwa kuwa kukua kwa soko huria katika utoaji wa huduma ya anga nchini, hivyohivyo naweza nikaambatanisha na kukua kwa elimu yetu kuwa huria na nilikuwa nataka tu kupata maelekezo ya Wizara juu ya huria hii ya kutokana na elimu yetu ya Tanzania kuwa huria, hali iliyosababisha baada ya kutoka kwa uhakiki wa vyeti feki imepelekea baadhi ya Madaktari, Walimu, Watumishi, taarifa zao kuonekana ni incomplete. Hii ni kwa sababu ya elimu yetu kuwa huria. Sasa naiomba Serikali itoe maelekezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninapozungumza,
kuna watumishi sasa wanaelekea Dar es Salaam kwenda kuhakiki incomplete zao…
Mheshimiwa Mwenyekiti,
swali langu ni kwamba nakata kujua: Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya wafanyakazi ambao taarifa iliyotoka juzi ya uhakiki wa vyeti vyao, hasa wale wote walioandikiwa incomplete? Serikali hasa Wizara hii ya Elimu ituelekeze, maana leo hii watu wanasafiri wengi kwenda kuhakiki vyeti vyao vya Form Four. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni hilo nalielekeza kwa Mheshimiwa Waziri kwa sababu hapa ni mada huria na elimu yetu ni huria, naomba Wizara ya Elimu itoe tamko juu ya kadhia hii ya elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ni kweli kwamba tumekuwa tukitoa elimu huria ili kuwezesha maeneo mbalimbali ya ajira kuweza kupata wataalam wanaohitajika. Katika suala hili la watu kusafiri kuhusiana na kuhakiki vyeti vyao, napenda tu kutoa ufafanuzi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna makundi makuu matatu ambayo yameendana na uhakiki uliofanyika. Kuna kundi la kwanza la vyeti feki au vyeti vya kugushi, kundi hili kama kuna yeyote anayeona kwamba hajaridhika, anachotakiwa kufanya siyo kusafiri, bali ni kukusanya vyeti vyake halali na kumwona mwajiri wake ambaye ni DED (Mkurugenzi wa Halmashauri) au Katibu Tawala wa Mkoa ili apeleke huo ushahidi wake na viweze kuwasilishwa. Vitawasilishwa kwa Katibu Mkuu, Utumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna kundi lingine,
hili analolizungumza la incomplete (vyeti visivyokamilika). Yawezekana wakati wa kuwasilisha, mtu aliwasilisha labda vyeti vya Chuoni, vyeti vya Kidato cha nne au cha sita hakuwasilisha; au vyeti vingine vinavyohusiana. Kwa hiyo, anachotakiwa kufanya ni vilevile, kupeleka vile vyeti ambavyo vilikuwa havijawasilishwa kwa hao waajiri wake ambao ni Mkurugenzi wa Halmashauri au RAS (Katibu Tawala wa Mkoa).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kundi la tatu la vyeti vyenye utata. Vyeti vyenye utata unakuta kwamba cheti kimoja kimetumika na watu zaidi ya mmoja. Kwa hali hiyo inabidi lazima kumfahamu ni yupi mwenye cheti halisi. Wanachotakiwa kufanya ni kila mtu anayeamini ndiye mwenye cheti hicho, hao ndio wanaotakiwa kusafiri, waende NECTA ili sasa wakahakikiwe na kujulikana mwenye cheti chake ni yupi kwa sababu haiwezekani cheti kimoja kikatumika na mtu zaidi ya mmoja. Huo ndiyo ufafanuzi wangu. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ambayo hayaridhishi kabisa, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; Mheshimiwa Waziri haoni Serikali kushindwa kumalizia majengo haya na kutoa majibu haya ni kuwavunja moyo wafadhili tuliowabembeleza na kuwaomba watujengee majengo haya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; wafadhili kujenga majengo na kuyamalizia au kutoyamalizia ni jambo la kawaida kabisa kwenye nchi yetu; na kwa kuwa Serikali imesema kwamba haiukufuata sheria wakati majengo yale yamesimamiwa na Engineer wa Halmashauri ya Wilaya ya Igunga. Je, Mheshimiwa Waziri haoni anawanyima haki wananchi wa Igunga kwa kukosa kuwa na VETA yao ambayo wameihangaikia kutafuta wafadhili, bado tu kumalizia lakini wanasema kwamba sheria haikufuatwa wakati Engineer wa halmashauri ndiye aliyesimamia majengo haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, nadhani hakunisikia vizuri katika jibu langu. Nimesema kwamba shirika linaweza likajenga chuo na kuikabidhi Serikali, lakini kwa sababu katika swali la msingi haikuzungumzwa kwamba chuo hicho kimeshakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachosisitiza ni kwamba, kwa sababu mwisho wa yote hicho chuo itabidi kiendeshwe kwa mujibu wa taratibu na sheria zilizopo, ndiyo maana tunasisitiza kabla ya wadau wetu wa maendeleo kuanza kufanya shughuli ya ujenzi, ni vema kuwasiliana na taasisi husika ili kile wanachokifanya kiendane na viwango na kiweze kuwa na tija kwa maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, sijasema kwamba wao wamejenga bila kufuata sheria. Katika jibu langu la msingi nilisema kwamba ni vema kabla ya kujenga yawe yanafanyika mawasialiano kupitia halmashauri na VETA ili kwa pamoja kuweza kuzingatia masuala ya kisheria. Kwa misingi hiyo, ninachosema ni kwamba, kwanza hicho chuo hatujakitembelea na hatuwezi kukiamuru kama ilivyo, lakini niseme tu kwamba nazidi kuwaomba wadau wa maendeleo, wanapofanya shughuli yoyote ya kimaendeleo kuhusiana na Wizara fulani, ni vema kushirikisha Wizara husika ili kile kinachofanyika kiwe na tija ili fedha zao zisipotee bila utaratibu ambao pengine usingekuwa wa lazima.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa hitaji la vyuo vya ufundi kwenye nchi yetu liko juu sana na uwezo wa Serikali unaonekana kwamba ni mdogo kuwezesha kujenga vyuo vya VETA nchi nzima kwa wakati mmoja. Je, Serikali iko tayari kutumia fursa tulizonazo kwenye shule zetu za sekondari kujenga karakana ya fani angalau moja kila shule ya sekondari ili kuwezesha vijana wengi kupata elimu ya ufundi na kurejesha elimu hiyo katika shule za sekondari?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba kupitia Sera yetu ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ya Mwaka 2014, Wizara inaangalia kwa umakini uwezekano wa kuongeza nafasi za udahili kwa wanafunzi wa vyuo vya ufundi ili kuwezesha wanafunzi wengi zaidi kupata fursa hizo. Kisera ni kwamba tungehitaji kuona mwanafunzi akisoma moja kwa moja mpaka kidato cha nne na kwa misingi hiyo kuna mambo mbalimbali ambayo yanaangaliwa ili kwa pamoja tuone kwamba ni jinsi gani tutaweza kuangalia mafunzo ya kawaida na vilevile mafunzo ya ufundi ili kuwezesha fursa hizo kupatikana.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Kwa kuwa tatizo lililopo Manonga linafanana kwa ukaribu kabisa na tatizo lililopo katika Mkoa wa Songwe na kwa kuzingatia kwamba Mkoa wa Songwe ni mpya, lakini mpaka sasa Wilaya za Mbozi, Ileje, Momba pamoja na Songwe hazina vyuo vya ufundi. Je, ni lini Serikali itajenga vyuo vya ufundi katika wilaya hizo ili kuwasaidia vijana wa Mkoa wa Songwe kuweza kuondokana na tatizo la ukosefu wa ajira? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninavyofahamu ni kwamba Wilaya ya Songwe ni miongoni mwa maeneo ambayo yamo kwenye mpango, nafahamu kuna kiwanja kilishatengwa eneo la Makutano, kwa hiyo, muda ukifika tutafanya hiyo shughuli ya ujenzi.
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nami kwa kifupi tu ni kwamba, mwezi wa kwanza mwaka huu nilikuwa nchini Uswisi na kuna wadau nilizungumza nao na wakaonesha nia kwamba wako tayari kutujengea chuo cha ufundi pale kwenye Jimbo letu la Arumeru. Swali langu kwa Wizara; naomba commitment ya Serikali, kwamba wadau watakapokuja na watakapokuwa tayari kutujengea ninyi mtakuwa tayari kutusaidia utaalam na vifaa pale ambapo chuo kitakamilika?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Nassari na naomba niunganishe na maeneo yote ambayo wamejenga Vyuo vya VETA kwa kutumia taasisi binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, katika kujenga vyuo vya ufundi kuna njia mbili za kuviendesha; kuna njia ya kwanza, watu wanajenga wenyewe na wanaendesha wenyewe katika sura zote za vifaa na Walimu. Njia ya pili, kujenga na kuikabidhi Serikali ili iweze kuviendesha. Sasa tatizo ninaloliona ni kwamba halmashauri zinashirikiana na wadau kujenga hivyo vyuo lakini baadaye wanakuwa hawawezi kufikia muafaka katika kupeleka Walimu pamoja na vifaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe tu
toka mwanzo, ni vema ushirikiano uanzie toka mwanzo ili tujue wadau watakaokuja kusaidia ujenzi wa chuo hicho wajibu wao utakuwa ni nini na upande wa Serikali wajibu wetu utakuwa ni nini ili suala hilo litekelezwe kwa ukamilifu kama inavyostahili.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa ruhusa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto nyingi za ukaguzi kwenye shule zetu za sekondari, msingi na vyuo vya ualimu, je, Serikali haioni sasa imeshafika wakati wa kuunda mamlaka au taasisi itakayosimamia ubora wa elimu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Idara zetu za Ukaguzi wa Elimu, shule za sekondari na msingi zimekuwa zikipata changamoto nyingi hasa za vyombo vya usafiri na watendaji. Je, Serikali ina mpango gani wa kuiwezesha Idara hiyo ya Ukaguzi ili iweze kufanya kazi yake katika ubora unaotakiwa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimesema awali ni kweli Idara yetu ya Ukaguzi inakabiliwa na changamoto mbalimbali hususan katika ukuaji wa sekta ya elimu kama ilivyo sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyemiti, mwanzo idara hii ilikuwa inakaguliwa kupitia kwenye kanda zetu, lakini kwa sasa ni kanda pamoja na Wilaya, hata hivyo tunaona kwamba kuna mapungufu kidogo katika mfumo mzima, na ndio maana kupitia mabadiliko haya ya sheria tutaangalia namna bora zaidi ya kuendesha shughuli ya ukaguzi katika shule zetu za primary, sekondari na vyuo. Hali kadhalika kwa upande wa uwezo wa Idara za Ukaguzi, ni kweli kuna mapungufu hasa yanayotokana na vifaa kama vitendea kazi kama magari, ofisi na Wizara imeshaona hilo na tayari tumeshaanza kufanyia kazi, tayari kuna magari yamekuwa yakipelekwa kwenye Wilaya na mwaka huu tumeagiza magari mengine kwa ajili ya kupeleka kwenye Wilaya nyingine na wakati huo huo tunatarajia pia kwa mwaka huu kuanza kujenga angalau ofisi 100 kwa ajili ya wakaguzi katika Wilaya zetu.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa suala la udhibiti wa elimu huwezi kutofautisha na udhibiti wa vitabu vinavyoingia kwenye mfumo wa elimu na kwa kuwa imeonekana wazi kwamba taasisi ya elimu ambayo imepewa jukumu la kuthibiti ubora wa vitabu vinavyoingia kwenye mfumo wa elimu imeonekana kuna dosari kubwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kurudisha chombo cha ithibati kama ilivyokuwa EMAC huko nyuma ili kudhibiti vitabu vinavyoingia katika mifumo yetu ya elimu na kuacha madudu yanayoendelea sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kurudisha mamlaka zilizokuwa zinafanya juu ya utungaji wa vitabu za wakati huo ni suala ambalo linabidi kuangaliwa zaidi. Kimsingi mapungufu yaliyojitokeza kwa mwaka huu Wizara ya Elimu imeanza kutunga vitabu kwa mara ya kwanza. Kwa hiyo, chombo kama hicho inabidi lazima kijengewe uwezo na ndio maana katika kufanya tathmini ya matatizo yaliyojitokeza, moja ya mambo yatakayoangaliwa ni uwezo wa chombo chenyewe, vilevile hata ushirikishwaji mpana wa wadau mbalimbali ikiwemo watu binafsi na wataalam kutoka katika maeneo mbalimbali.
Kwa hiyo, mimi nadhani kiujasiriamali tunasema kwamba kujifunza ni pamoja na kufanya makosa, lakini yasiwe ya kudhamiria yawe ni ya bahati mbaya. Kwa hiyo, tutaendela kuboresha na kushirikisha wadau wengi zaidi ili kuona kwamba tunapata vitabu vilivyo sahihi.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata hii nafasi. Kwa kuwa Mheshimiwa waziri amesema kwamba wana mpango wa kupeleka vitendea kazi na magari katika Ofisi za Ukaguzi wa Elimu, lakini kwa muda mrefu kumekuwa na matatizo makubwa ya ukosefu wa fedha za uendeshaji, unaweza ukapeleka magari kama hakuna fedha za uendeshaji bado hawataweza kufanya kazi; na kwa kwa muda mrefu wakaguzi wamekuwa wakifanya ukaguzi katika shule ambazo ziko jirani tu kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapelekea OC ofisi hizo zote za kanda ili ziweze kufanya kazi yao sawasawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimesema awali ni kwamba kimsingi Wizara imedhamiria kuboresha eneo hili la ukaguzi. Suala la OC limekuwa likiimarishwa kila wakati na ndio maana tunataka kuangalia mfumo mzima, hata ikiwezekana mafungu yao ya upatikanaji wa OC yaende moja kwa moja bila kupitia katika ngazi nyingine.
Vilevile ukaguzi tunaotaka kuuzingatia si tu ule wa kuangalia masomo peke yake, mpaka miundombinu, shule iko wapi? Inafundisha vipi na imesajiliwa katika sura ipi? Kwa hiyo, tunataka kwenda kwenye ukaguzi kwa njia ambazo ni pana zaidi ili kuwezesha kuona kwamba mambo ambayo tunaagiza kupitia sera zetu na miongozo yanatekelezwa pia katika shule zetu za Serikali.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Serikali yetu ya awamu ya tano imedhamiria kuifanya Tanzania kuwa Taifa la viwanda je, Serikali haioni muda muafaka sasa wa kuandaa mitaala ya stadi za kazi na ufundi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa kuwa mahitaji ya dunia sasa yamebadilika, je, Serikali haioni umuhimu wa kufanya marekebisho makubwa ya sera yetu ya elimu ya juu na elimu ya kati ili wahitimu waweze kushindana kimataifa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sera zetu mpaka sasa zimekuwa zikizingatia masuala ya kuwezesha stadi za kazi. Suala linalojitokeza katika ugawaji wa rasilimali na kuboresha ili ziendane na uhalisia hiyo ndio inakuwa ni changamoto. Kwa mfano suala la kujifunza kwa vitendo ni jambo muhimu sana, lakini wakati mwingine unakuta kwamba bajeti inapokuwa finyu ule muda wa vitendo unapunguzwa.
Kwa hiyo, Serikali itaendelea kuongeza jitihada katika maeneo hayo ikiwemo kuboresha vyuo vya ufundi kama vile vyuo vya wananchi ambavyo tumeshavichukua kwenye Wizara yetu pamoja na VETA, lakini pia kufungua vituo mbalimbali vya kujifunzia ukiacha katika mfumo rasmi hata mfumo usio rasmi ili baadaye hata wale wanaokuwa wanajifunza kupitia mifumo isiyo rasmi waweze kupata hizo stadi za kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa elimu ya
juu hivyo hivyo, wanafunzi wamekuwa wakifundishwa, lakini pia tumekuwa tukiangalia nchi mbalimbali zinaenda vipi kupitia workshops ambazo tunabadilishana mawazo, vilevile hata kupitia mitaala yetu. Kwa mfano siku nyuma elimu ya ujasiriamali ilikuwa haipo vyuoni, ilikuwa haifundishwi lakini sasa hivi tunazo degree, masters mpaka Ph.D za ujasiriamali. Kwa hiyo, tumekuwa tukifanya hivi na naamini tutaendelea kuzingatia kadiri tunavyopata mawazo mbalimbali ikiwemo ya kwenu Waheshimiwa Wabunge.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
Kwa kuwa mitaala ya elimu Tanzania inazingatia misingi na mahitaji ya kijamii hususan masuala ya utandawazi. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka somo la computer katika shule za sekondari na msingi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi tayari Serikali ilishaanza kuweka masomo ya computer au TEHAMA kwa ujumla katika shule zetu, isipokuwasiyo shule zote ambazo tayari zimeshapata hizo fursa kutokana na miundombinu halisi. Lakini kupitia hii miradi ya REA ambayo sasa karibu kila kijiji kinakuwa na umeme, vilevile karibu taasisi zote za umma ikiwemo shule zitakuwa na umeme. Kwa hiyo, tunaamini kwamba eneo la TEHAMA litaweza kupata nguvu zaidi na tayari wizara inafanyia kazi kuhakikisha kwamba wanafunzi wengi wanapata fursa ya kupata mafunzo hayo.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa takribani miaka miwili iliyopita kumekuwa kuna uhitaji mkubwa sana wa mafunzo ya ujasiriamali, lakini kumekuwa kuna walimu wanaofundisha chini ya kiwango. Serikali inasema nini kuwadhibiti walimu hao kwa kupunguza bei lakini pia kufundisha katika viwango ambavyo vinaweza kusaidia walaji ambao wengi ni wanawake?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, somo la ujasiriamali ni somo ambalo linaweza likafundishwa katika ngazi mbalimbali kama ambavyo wengi tunafahamu, ujasiriamali upo katika sura mbalimbali. Kuna ule ambao unakuwa informal ndio wajasiriamali hawa wadogo wadogo wanaanza, lakini kuna ule ambao unakuwa katika ngazi kubwa zaidi. Kwa hiyo kunaile kupata mafunzo ya awali na kupata mafunzo makubwa zaidi. Jambo kubwa ambalo ningependa leo Waheshimiwa Wabunge mlifahamu ni kwamba katika suala zima la ujasiriamali wengi tunafikiria ni ile kufanya biashara, kuuzauza labda vitu au maduka na vitu kama hivyo. Lakini ujasiriamali tunachotamani hasa watu wakifahamu, ni ile namna gani mtu anafanya shughuli zake kwa njia tofauti ili kuongeza thamani, kiasi kwamba hata Waheshimiwa Wabunge kufanya Ubunge pia ni ujasiriamali wa aina yake. Kwa hiyo, naomba tulizingatie katika sura hiyo.
MHE. RIZIKI S. MNGWALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na nishukuru kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri ameweka vizuri swali ambalo nilitaka kuuliza, ni hiyo hiyo kwamba kuja na misamiati ambayo mwisho wake tunaona kama tunakwama na pale mwanzo akazungumzia mpaka suala la bajeti. Lakini ni vipi Serikali sasa itarudisha katika shule za msingi na sekondari yale mafunzo au taratibu za elimu ya kujitegemea ambapo watoto walikuwa wanajifundisha kupika maandazi, kufuga kuku, kutengeneza mifuko na kazi kama hizo, hizo hazihitaji bajeti wala hazihitaji misamiati lakini watoto wakitoka pale wana ujuzi. Ni lini Serikali itafanya hivyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba kupitia stadi za kazi wanafunzi wamekuwa wakipata muda wa kujifunza masomo kama hayo. Lakini kuna wakati sera zetu huwa zinakuwa kama zina mgongano kidogo. Kwa mfano kuna wakati tulisema kwamba wanafunzi wasipewe kazi, watoto wasipewe kazi, watu wakachukulia hiyo ni kufuta mpaka hizo stadi za kazi. Lakini kwa kuacha kufanya hivyo, tumejikuta tumerudi nyuma. Kwa mfano, katika shule tunazosema kwamba wazazi wachangie chakula, kwa kweli kupitia mashamba hasa kwa shule zile ambazo zina maeneo huko vijijini wangeweza kulima mashamba yao na wakapata chakula, watoto huku wakiwa wanajifunza na wakati huo wanapata chakula.
Kwa hiyo, mimi nitoe rai yangu kwa shule zote kuona kwamba stadi za kazi hasa kulingana na mazingira yetu ni ya muhimu sana nawapongeza sana shule kama sekondari ya Rugambwa, wao wanafanya vizuri sana.(Makofi)
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Ni lini Serikali itarudisha mitaala ya shule za upili ili iweze kuzalisha mafundi mchundo na mafundi sadifu kama ilivyokuwa zamani watu hawa walizewa kujitegemea? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi binafsi nikiwa ni mnufaika katika eneo hilo niliweza kutembelea katika shule nyingi ambazo zinatoa mafunzo ya ufundi, ikiwemo Ifunda, Mtwara, Bwiru na kadhalika. Lakini kitu nilichojifunza ni kwamba zile shule baada ya kuzichanganya na wanafunzi ambao wanasoma kidato cha tano na cha sita imejikutwa kwamba kwa upande wa ufundi ni kama vile ufundi haupo. Vilevile baada ya kuwa VETA ina uwezo wa kuingiza wanafunzi moja kwa moja katika masomo ya ufundi sanifu.
Kwa hiyo, ilionekana lile eneo kama linakuwa reduntant, sasa baada ya hapo tuliita timu kutafakari namna gani tunaweza tukaendelea na shule hizo. Jambo tuliloliona ni kwamba kwa hali ya sasa ambayo elimu imeongezeka na shule nyingi zinatoa wanafunzi wanaofaulu vizuri mpaka kidato cha nne, tunafikiria kwamba hizo shule zirejeshwe katika kutoa mafunzo ya ufundi sanifu, lakini baada ya kujenga shule ambazo zitawachukuwa wale waliokuwa wanasoma kidato cha tano na sita ili kusiwe na upungufu katika eneo hilo, kwa hiyo hali halisi ndio hiyo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo cha FDC Sikonge kinatakiwa kutoa mafunzo katika fani za useremala, uashi, uchomeleaji, ushonaji na ufundi umeme. Kutokana na upungufu wa walimu uliopo na uchakavu wa majengo, chuo kwa sasa kinatoa mafunzo kwenye fani ya umeme peke yake. Maswali yangu mawili, je, Serikali aione kuwa chuo hiki kinahitaji jicho la kimkakati ili kukiokoa?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, katika jibu la msingi ameahidi kwamba Chuo hiki kitatembelewa, kitatembelewa lini na nani? Ahsante sana.
NAIBU WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inatambua umuhimu wa kuviimarisha vyuo hivi ili kuweza kuchukua wanafunzi wengi zaidi na kutoa mafunzo yaliyo bora zaidi kulingana na uhitaji wa soko, lakini vilevile kuhakikisha kwamba wananchi wengi zaidi wanaweza kujiajiri wenyewe. Kwa upungufu alioainisha Mheshimiwa Mbunge tutatembelea chuo hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla wake Waheshimiwa Wabunge ili tu-save muda, kimsingi mkakati ni kutembelea vyuo vyote vya FDCs ili kuona namna bora zaidi ya kuviendesha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la kwenda Sikonge nitakufahamisha Mheshimiwa, kimsingi tutaenda na kwa sababu Mheshimiwa Mbunge ni muhimu kuwepo, tutakujulisha twende wote ikiwezekana katika kipindi hiki cha bajeti katika weekend mojawapo.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Ahsante Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la nyongeza ninalo. Je, Serikali ina mpango gani ya kuwasaidia vijana wanaohitimu mafunzo ya ufundi kama hao wa Makete kupata angalau vifaa tu vya kuanzia kazi?
Swali la pili, Halmashauri ya Mji Njombe ina shule za sekondari 22 na zoezi hili la kujenga Vyuo vya Ufundi linaonekana sasa kwa Serikali limekuwa gumu sana na linakwenda pole pole sana.
Je, Serikali ipo tayari kupokea ushauri, sasa ianze kuzibadilisha baadhi ya shule za sekondari kuwa shule za ufundi ili kusudi vijana wetu walio wengi watakaokuwa wanahitimu Kidato cha Nne waweze kuwa mafundi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Kimsingi ni kwamba VETA imekuwa ikifanya hivyo baada ya kumaliza mafunzo ya ufundi kwa baadhi ya wanafunzi wanaohitimu wamekuwa wakipewa vifaa kwa ajili ya kuanzia shughuli zao za kiufundi, pia kusaidia kutengeneza clusters za hao wanaokuwa wamehitimu pamoja na wengine ambao wamekuwa wamehitimu mafunzo ya ufundi siyo tu kupitia VETA hata kupitia kwa wananchi wa kawaida, tunawatambua na kuweza kuwapa vifaa, vilevile kuwatambua rasmi na kuweza kuwapa vyeti.
Swali la pili la kuweza kubadilisha shule ziwe za ufundi, Wizara tayari tumeshaliona hilo na tunafikiria kubadilisha baadhi ya shule za sekondari hasa zilizokuwa shule za ufundi kama Ifunda, Mtwara, Tanga, Bwiru na shule ya Musoma ili ziweze kuwa vyuo vitakavyoweza kutoa mafunzo kwa ajili ya technicians.
Kwa hiyo, muda ukikamilika tutafanya hivyo na kwa mwaka huu tunategemea tuanze kujenga shule mbadala kwa sababu shule hizi zinachukua wanafunzi wa sayansi kwa kidato cha tano na sita na form one mpaka form four tunawajengea shule yao ili hayo majengo ambayo ni muhimu sana kama workshops yaweze kutumika kwa Vyuo vya Ufundi.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ninaomba niendelee kutambua juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali kupitia Wizara hii na hasa pale ilipotamka wazi kwenye hotuba yake kwamba imetoa kipaumbele cha elimu kwa watoto wenye ulemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoongelea elimu jumuishi tunamaanisha kwamba watoto wenye ulemavu wasome na wasio na ulemavu. Sasa Serikali inaonaje hii elimu maalum ikafundishwa kwenye vyuo vyote vya ualimu nchini tofauti na ilivyo sasa hivi kwamba ni walimu wachache wanaopata ujuzi huu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili katika hii mitaala mipya inayoandaliwa Serikali inaonaje ikaingiza lugha ya alama kuwa miongoni mwa masomo ambayo yatafundishwa ili kizazi kijacho kiweze kuwasiliana na viziwi kwa urahisi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stella Ikupa kama ifuatavyo; ni kweli ili wanafunzi hawa waweze kupata haki yao ya msingi ya kuweza kujifunza vizuri popote walipo ni pale tutakapokuwa na walimu wa kutosha ambao wana uwezo wa kuwasiliana na kutoa elimu husika kwa watoto hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, hali hii ni muhimu sana, lakini kwa sasa tunachoangalia ni kuona kwamba ni namna gani tunafanya hivyo, kwa mfano katika suala la lugha ya alama, Wizara tayari inaliangalia jambo hili ili kuwezesha walimu wote angalau wawe na msingi wa lugha ya alama ili kuweza kuwasaidia wanafunzi hao. Kwa hiyo, jambo hilo mimi naona tulichukue tuone ni namna gani tutalifanyia kazi. Kwa msingi huo nimejibu maswali yote mawili kwa pamoja, ahsante.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa Waziri kunijibu majibu mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza, nitoe pole kwa wananchi wa Jimbo la Lushoto na Wilaya ya Lushoto kwa ujumla kwa mvua zinazoendelea kunyesha maana mpaka sasa hakuna mawasiliano kati ya Dar es Salaam - Lushoto, Arusha – Lushoto na Tanga - Lushoto. Nimeongea na Meneja wa TANROADS Mkoa akaniambia kwamba atashughulikia suala hilo. Hata hivyo, nikiangalia tatizo lile ni kubwa sana, madaraja yamekatika zaidi ya kilometa 32. Kwa hiyo, nipaze sauti Serikali ipeleke msaada maeneo yale haraka iwezekanavyo ili kunusuru maisha ya wananchi wa Lushoto na uchumi unaotegemea barabara ile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa pole hiyo kwa wananchi wangu wa Wilaya ya Lushoto na mkoa mzima kwa ujumla basi niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri amenijibu kwamba kwa kuwa Serikali itaanza ujenzi katika Wilaya ya Lushoto mara baada ya kukamilisha miradi ya Vyuo vya VETA vilivyoanza. Je, Serikali haioni kwamba itaendelea kulimbikiza vijana wengi wa Wilaya ya Lushoto bila kupata elimu ya VETA?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tayari kuna majengo ya kuanzisha Vyuo vya VETA je, Waziri yupo tayari kuongozana nami ili kwenda kuona majengo yale kama yanafaa na kutoa tamko la kuanzisha Chuo cha VETA? Hata kama VETA hiyo itaanzishwa chini ya mti, lakini naomba wananchi wangu hususani vijana wangu waweze kupata elimu hiyo ya VETA, hiyo ndio shida kubwa. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, si lengo la Serikali kudidimiza Jimbo la Lushoto na kimsingi Serikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha kuwa vyuo vilivyopo vinaweza kudahili wanafunzi wengi zaidi na ndiyo maana kwa sasa badala ya kusubiri tu kujenga chuo kipya, tunaona kuna haja pia ya kuongeza idadi ya mabweni katika vyuo vilivyopo ili kuchukua hata wanafunzi wa mbali. Kwa hiyo, lengo ni kuweza kujenga Chuo cha Lushoto muda muafaka utakapofika na fedha zitakavyopatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kuongozana naye kwenda kuona majengo yaliyopo, kwa moyo mkunjufu kabisa niko tayari na endapo majengo haya yataweza kufaa aidha kwa kutumiwa kama VETA au Chuo cha Maendeleo ya Jamii tutafanya hivyo.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali pamoja na mikakati mizuri ambayo Serikali inaiweka lakini ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa nina imani kwamba Waziri na Maprofesa wote mlioko ndani humu mmesoma bure A-Level na kwa sababu watoto hawa wanachaguliwa, wengine wanashindwa kuendelea na masomo haya kwa kukosa fedha, kwa sababu bado ni watoto wa maskini na wengine wamefaulu vizuri masomo ya sayansi pamoja na hesabu, je, Serikali haioni kwamba inapoteza vijana wazuri ambao wanaweza kusaidia Taifa?(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hawa watoto wanaochaguliwa kuendelea na A-level ni wachache kuliko wale ambao wanahudumiwa na Serikali kwa maana ya O-Level, je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka sasa wa kuleta bajeti ili tuweze kuwasaidia watoto hawa wa maskini ili waweze nao kusoma bure wafaidi matunda ya Serikali hii? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Serikali ingependa kusomesha wanafunzi katika ngazi zote za elimu bure endapo uwezo ungekuwa wa aina hiyo. Kama nilivyosema ni kwamba awamu ya mwanzo tuliongeza shule za msingi lakini tukaja tukaongeza shule za sekondari kila kata na sasa hivi tunaendelea kuongeza shule za kidato cha tano na sita (A-level) kwa sababu ni chache ukilinganisha na wanafunzi wanaofaulu na hasa baada ya Serikali kuchukua jitihada za makusudi za kuongeza ubora wa elimu, imekuwa sasa wanafunzi wanaofaulu ni wengi na hivyo hatuwezi kuwaacha bila kupata elimu hiyo. Kwa hiyo, kabla hatujaweza kutoa fedha kwa kuwalipia hiyo ada, ina maana kama hawana sehemu ya kusomea itakuwa bado hatujafanya jambo la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili la kuongeza bajeti, hilo ni suala letu sote kama Wabunge. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais lakini pia Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye tukonaye humu, Wizara yetu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ni kati ya Wizara ambazo zinapewa kipaumbele cha hali ya juu kwa kupewa bajeti kubwa kuliko Wizara nyingine. Kwa hiyo, naamini Serikali itaendelea kufanya hivyo.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Mheshimiwa Waziri, mimi kama mtaalam wa misitu, naomba hili swali lijibiwe tena, halikujibiwa, la kwanza hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na majibu haya ambayo wataalam wa Mheshimiwa Waziri wamejaribu kuzunguka, unaposema FITI ni Chuo Cha Misitu, Chuo cha Nyuki kwa nini umekiacha? FITI ni consumers siyo misitu. Tukisema foresters ni yule ambaye unampa mbegu anakupa product ama ya timber ama ya log, huyo ndiyo mwanamisitu, sio unayempa ubao akafanya processing. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo, hivi kweli Watanzania tunajiangalia kwamba misitu ina umuhimu kwa maisha yetu na vizazi vyetu na viumbe vingine vilivyomo katika ardhi? Hekta 5,000 kuhudumiwa na mtu mmoja, tuko serious kweli? Hilo swali la kwanza.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, unaposema katika kipindi cha miaka 10…
Mheshimiwa Naibu Spika, sawa. Swali la pili, unaposema una wanataaluma 3,500 katika kipindi cha miaka 10, ni wastani wa 350 kwa mwaka. Hebu tupe mchanganuo kwa sababu katika vyuo vyote darasa halizidi watu 40 na ni madarasa mawili tena ya certificate, wanaochukua degree hawazidi watu 50 kwa siku. Kwa hiyo, mnatoaje watu 350 kwa mwaka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la kwanza, pamoja na maelezo mengi ya utangulizi aliyotoa, nililoweza kulinukuu kama swali mahsusi ni kwamba, inawezekanaje hekta 5,000 zikahudumiwa na mtaalam mmoja wa misitu. Dunia inaendeshwa kwa sayansi na teknolojia, wataalam na miongozo mbalimbali. Mawazo na maoni ya mtu mmoja-mmoja yanaheshimiwa lakini yanatakiwa yakae ndani ya utalaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati nasoma jibu langu nimenukuu kwamba takwimu hizi au viwango hivi vimewekwa kimataifa na vimewekwa na Shirika la Chakula Duniani la FAO. Sasa inawezekana Mheshimiwa Mbunge ana maoni mazuri zaidi kuliko yale ya Shirika la Kimataifa la Dunia, basi nafikiri maoni yake hayo afuate channels zinazofaa ili kuweza kwenda kuboresha hali hiyo kwa namna ambavyo ataona inafaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, nalo pia ni la takwimu. Anasema inampa mashaka kidogo kuona kama kweli tuna wataalam hao 3,500 kwa kuwa, kwa mujibu wa taarifa alizonazo yeye watalaam wanaozalishwa kwa mwaka kwa vyuo vyote ni 350, sasa ni muda gani utakuwa umepita huo kuweza kupata idadi ya watalaam hawa 3,500. Kwa sababu, hili ni swali linalohusiana na takwimu, swali lake hilo ili niweze kuwa kwenye nafasi nzuri zaidi ya kuweza kumwambia namna gani tumefikia hapo, basi anione kwa wakati muafaka, hata mchana huu nitaweza kumpa mchanganuo mzuri. (Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikitishwa sana na majibu ya Wizara. Suala kwamba tuna wataalam wachache wa sayansi, sikubaliani nalo kwa sababu hivi karibuni tu Mheshimiwa Rais alikuwa ameishatoa kibali madaktari wetu 500 kwenda kufanya kazi nchini Kenya. Vilevile tunatumbua kwamba kuna manesi wengi wako mitaani hawajaajiriwa kwa sababu ya kukosa vibali.
Mheshimiwa Naib Spika, kwa hiyo, swali langu la msingi ninataka kuuliza ni kwamba ni kweli kwamba Mheshimiwa Waziri alitoa tamko na mimi nashukuru kwamba umesema waraka bado haujatoa na ninajua kwamba government moves with papers. Kwa kuwa masomo ya sayansi najua ni muhimu sana na kwa kuwa kwa bajeti ya mwaka huu ukiangalia tuna upungufu wa maabara nyingi sana, vilevile ili kumfanya mtoto asome sayansi inabidi kuwe na madarasa mazuri. Kwa mwaka huu tuna upungufu wa madarasa 158,000 na Serikali imesema inaweza ikajenga madarasa 2,000, hii ina maana itachukua miaka 79 kuweza kukamilisha hayo madarasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama lengo la Serikali ni kufanya watoto wetu wasome sayansi, nini mpango mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba wanajenga mazingira mazuri na sio tu kutoa matamko wanafunzi wasome sayansi?
Swali la pili, kwa kuwa tunatambua kwamba nchi hii haihitaji tu wanasayansi bali pia inahitaji wengine, kwa mfano mameneja wanahitajika watu waliosoma, lawyers kama Mheshimiwa Naibu Spika na wengine, ni kwa nini sasa Serikali isihamasishe pia wanafunzi wasome masomo mengine kwa bidii?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba nijibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Waziri Kivuli wa Wizara yetu Mheshimiwa Susan Lyimo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ieleweke bajeti zote za Wizara zinapitishwa na Bunge lako Tukufu na Bunge hili linao uwezo mkubwa sana wa kusema jambo hili lipewe kipaumbele au jambo hili lisubiri kidogo, kama ambavyo tumeona kwenye Wizara ya Maji wote kwa pamoja tumesema iongezewe fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imekuwa ikijitahidi sana kuhakikisha inatafuta wafadhili kila kona ya dunia kuhakikisha kwamba tunapunguza tatizo hilo. Mfano ni madarasa ambayo yamejengwa mwaka huu zaidi ya madarasa 2,000, vyoo tulivyojenga na hali hiyo itaendelea kufanyika hivyo. Pamoja na kwamba kwa upande wako Mheshinimwa Waziri Kivuli unaona hakuna upungufu wa wanasayansi, nataka nikuhakikishie kutokana na mikakati ya Serikali ya kutaka uchumi uwe uchumi wa viwanda, uchumi wa viwanda unaendeshwa na sekta tofauti tofauti, kwenye kiwanda utahitaji watu wa afya, kwenye kiwanda utahitaji watu wa ujuzi wa ufundi, kwenye kiwanda utahitaji mambo mengi, lakini hali kadhalika kwenye sehemu zetu za kuhudumia afya zinahitaji wataalam wa aina hiyo. Kwa hiyo, ukiangalia kwa mapana yake huwezi ku-plan kwa kuangalia leo unaangalia kwa mapana, sisi tunaona iko haja kubwa sana ya wanafunzi wetu kuchukua masomo ya sayansi kwa wingi zaidi ili kukidhi maeneo ambayo bado yana upungufu.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni pamoja na hiyo ya kusema kwamba tunatamka tamka, niseme tu kwamba suala siyo kutamka, unapohamasisha lugha unayotumia ni yoyote inayowezeshwa kutoa hamasa kwa wale vijana na wakafanya maamuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, samahani swali la pili la nyongeza yako naomba limenitoka kidogo, kama unaweza ukarudia.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba labda awe pia anaandika wakati mtu anauliza ili isimletee shida. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili niliuliza kwamba kwa sababu nchi hii nadhani pia ameshalijibu amechanganya kwamba kwa sababu tunahitaji wataalamu mbalimbali ni kwa nini pia Serikali isihamasishe masomo mengine, kwa sababu hatuhitaji tu wanasayansi tunahitaji variety ya watu.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi mbali ya hayo niliyomjibu ninayo ya kumuongezea na nilikuwa nataka nijue kama na wewe bado unakumbuka swali lako vizuri. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la wanafunzi katika maeneo mengine Wizara yetu haijajikita kwenye sayansi peke yake. Kwa mfano sasa hivi tunaendelea kuona namna ambavyo tunaweza hata tukaingiza somo la kuwezesha wanafunzi katika masuala ya moyo (mindset). Unakuta mtu anao uwezo wa kufanya jambo lakini kwa sababu tu kimoyo hajawa tayari anashindwa hata kusoma. Kwa hiyo, kuna masomo mengi pamoja na hilo, lakini haya ya sayansi tumeyapa kipaumbele kutokana na uhaba wake mkubwa.(Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, napata taabu kidogo maana yake na mimi ni mwalimu, iwapo Serikali tutaacha kwenda kwenye specialization na tukafanya watoto wote wakasoma sayansi. Mimi nina wasiwasi kwamba tutapata wanasayansi wabovu zaidi.
Je, Serikali haioni kwamba specialization ni important kuliko ambavyo sasa tunakwenda kumfanya kila mtoto asome sayansi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, specialization inaanza na msingi na niseme tu kwamba tunawahitaji wataalam wa aina tofauti tofauti. Kuna hao specialization ambao wanakuwa wamekuwa vertical yaani anajikita katika eneo moja pia tunawahitaji wale ambao wanakua kimapana (wide knowledgeable people) ambao wanaweza wakaoanisha upande huu na upande huu. Kwa hiyo, katika ku-specialize kupo lakini lazima kuwe na msingi ni wa eneo gani ambalo huyu mtu atafanya specialization. (Makofi)
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona.
Swali langu lilitaka kufanana kidogo na Mama Anne Kilango na nikichukulia mwenyewe kuwa mfano, lakini kwa sababu Mheshimiwa Naibu Waziri amekwishajibu labda nilisogeze mbele kidogo kwamba kama kweli lengo letu ni kuongeza idadi ya wanasayansi kwenye nchi hii na hususan walimu wa masomo ya sayansi kwenye shule zetu, ni kwa nini basi ile Programu ya Serikali ya Awamu ya Nne, Serikali ya Chama hiki cha Mapinduzi ambayo ilianzisha program maalum kwa ajili ya watoto, Chuo Kikuu cha Dodoma kwa ajili ya kutengeneza walimu wengi wa sayansi kwenye nchi hii, ni kwa nini basi watoto wale walifukuzwa mwaka jana tena kwa polisi na mbwa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TAKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, wanafunzi wale hawakufukuzwa kwa sababu wako kwenye vyuo kumi ambavyo wanaendelea na masomo yao na bado Serikali inaendelea kuwalipia. (Makofi)
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Elimu imerithi Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na Vyuo vya Maendeleo ya Jamii kutoka Wizaraya Afya. Je, kwa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi cha Msaginya kilichoko Jimbo la Nsimbo, Mkoa wa Katavi, kuna mkandarasi miaka miwili amesimama kazi anaidai Serikali. Je, Serikali ina mpango gani wa kumlipa ili kukamilisha ukarabati wa majengo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mkandarasi anadai, kimsingi kama ambavyo mnafahamu vyuo hivi vimeletwa kwenye Wizara yetu katika kipindi cha mwaka huu wa fedha unaoishia. Tunachofanya ni kwanza kuvitembelea na kuweza kuviangalia viko katika hali gani, kama kuna Mkandarasi alikuwa anafanya kazi eneo hilo na hakulipwa, Wizara tunao wajibu wa kumlipa lakini baada ya kufanya uhakiki na kujua kwamba kazi aliyoifanya inafanana na uhalisia na aweze kulipwa kwa kadri ya kazi yake.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Elimu, hoja ya swali la Mheshimiwa Kishimba ni kwamba kumekuwa na utaratibu wa kumtahini mwanafunzi kwa mtihani wa mwisho na wakati mwingine unakuta mwanafunzi pengine zile siku za mwisho anakuwa na matatizo ambayo yanamfanya ashindwe kufaulu vizuri.
Je, Serikali haioni kwamba kuna haja ya kuangalia maendeleo ya mwanafunzi huyu ili kusudi maendeleo yake yawe ni sehemu ya mtihani wake wa mwisho ili kuondoa mchanganyiko huu?
Swali la pili, kwa vile kumekuwa na wizi wa mitihani mara kwa mara na hii inachangiwa kwa sababu wanafunzi wanajiandaa kwenda kushinda mtihani badala ya kujua namna ya kujibu mtihani.
Je, Serikali inatafuta mbinu gani mbadala za kuwasaidia vijana badala ya kukariri kufanya mtihani, wafanye mtihani kwa kuelewa namna ya kushinda mtihani?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza kwenye jibu la msingi, Serikali imekuwa ikifanya hivyo kwa kutumia matokeo endelevu yaani mwanafunzi amekuwa akipimwa katika muda wake anaokuwa darasani, vilevile hata wale wanaofanya shughuli za vitendo, kwa mfano wale wanaosoma masomo ya ufundi wamekuwa wakienda kwenye mazoezi wanafuatiliwa na pia shughuli za vitendo zimekuwa zikichangia asilimia 30 niliyosema katika mitihani ya mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mtihani wa mwisho ni kweli ndiyo unakuwa na nafasi kubwa zaidi kwa ajili ya hiyo asilimia 70; endapo mwanafunzi amepata tatizo siku ya mwisho ya mtihani, taarifa huwa zinatolewa na kuweza kuangalia kwamba alikuwa kwenye mazingira gani. Wakati mwingine mwanafunzi anashauriwa asifanye mtihani kama hali yake kwa mfano itakuwa ni ya ugonjwa ili aweze kurudia na kufanya mtihani wakati mwingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa wizi kwa kiwango kikubwa Serikali imeweza kudhibiti tatizo hilo, nanyi mtakuwa mashahidi katika kipindi hiki, hasa toka tumeingia halijawahi kutokea tatizo la wizi wa mitihani. (Makofi)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante sana. Namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na ningependa kuweka msisitizo kwenye suala la wizi wa mitihani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kulihakikishia Bunge lako kwamba Serikali imedhibiti suala la wizi wa mitihani na kinachotokea ni udanganyifu katika mitihani, ambapo baadhi ya Walimu ama huwa baada ya kufungua zile karatasi za mitihani wanaenda pembeni wanawaandalia wanafunzi majibu na kuyapeleka katika chumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo Serikali imekuwa pia makini katika kuhakikisha kwamba inaangalia kwa karibu usimamizi wa mitihani na wote ambao wanakuwa wanajihusisha na udanganyifu katika mitihani hatua zimekuwa zikichukuliwa na zitaendelea kuwa zinachukuliwa.(Makofi)
MHE. ESTER M. MMASI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa swali la Mheshimiwa Kishimba linafanana kabisa na changamoto ya udanganyifu wa mitihani yaani thesis and dissertation kwa wanafunzi wa shule ya Uzamili na Uzamivu elimu ya juu.
Je, Serikali imejipangaje kuwa na mfumo mahsusi katika kudhibiti ubadhilifu wa mitihani kwa maana ya kuwa na mfumo mathalani central system plagiarism test? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika masuala haya ya kuhakikisha kwamba wanafunzi wanafanya mtihani na wanapimwa kwa kiwango wanachostahili kwa kadri ya kuwapima uelewa wao, Serikali tumeendelea kufanya hivyo. Kwa upande wa vyuo vikuu hasa kwa upande wa wanapofanya maandishi yao, niseme thesis kwa mfano, kweli kumekuwa kunajitokeza udanganyifu wa watu kuomba ama kufanyiwa na watu, wakati mwingine kunakili maandiko ya watu wengine waliopita kiasi kwamba mtu anakuwa hajafanya kazi yake na kupimwa kwa haki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali imeshaliona hilo na tumeshaandaa mfumo kiasi kwamba kila mtu akishamaliza andiko lake litakuwa linapitishwa humo kiasi kwamba likioanishwa litajulikana kwamba huyu ameiba kutoka kwa andiko la mtu mwingine. Ikizingatiwa katika mfumo huu wa digital watu ni rahisi kuiba. Kwa hiyo tumeshaona namna ya kudhibiti eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa elimu ya sekondari ngazi mbalimbali tunafanya uhakiki. Kwa mfano, mara hii ya mwisho hata sisi wenyewe Mawaziri tumekuwa tukitembelea baadhi ya shule za kidato cha sita kuona kwamba taratibu na sheria zinazingatiwa katika sehemu za mitihani. Mfano, safari hii nimeenda shule ya Ifunda na shule ya Iringa Girls. Hivyo tunasimamia kikamilifu.
MHE. ANNA J. GIDARYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Pamoja na kuwa lugha yetu ya Taifa ni kiswahili lakini kumekuwa na mkanganyiko katika mfumo wetu wa ufundishaji wanafunzi. Shule nyingi za Serikali kuanzia darasa la kwanza mpaka la saba wanafundisha kwa kiswahili lakini wakifika sekondari wanaambiwa wazungumze lugha ya kiingereza. Sambamba na hilo, tatizo hili liko kwenye vyuo vyetu vya Serikali ya Mitaa hususan Hombolo. Masomo yote yanafundishwa kwa kiingereza ilhali watu hawa wanaenda kusimamia watu ambao hawajasoma.
Je, Serikali haioni ni muhimu kubadilisha mitaala hii kuondoa mkanganyiko huu katika sera ya ufundishaji?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza tunamshukuru kwa kuwa ni mdau wa kiswahili na kwa namna ya pekee nimpongeze Mheshimiwa Mama Salma Kikwete kuwa Balozi wa Kiswahili Afrika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika elimu ya msingi kiswahili imekuwa ndiyo lugha ya kufundishia na kiingereza inakuwa kama somo. Tunafanya hivyo kwa sababu tunaamini Watanzania wengi lugha ya kiswahili japokuwa ni lugha ya pili, lakini wana uelewa zaidi na hivyo kuwawezesha kuelewa vizuri elimu yao ya msingi katika lugha ambayo wamekuwa nayo. Hali kadhalika tunapokwenda kwenye sekondari ndipo sasa wanapotumia lugha ya kiingereza kama lugha ya kufundishia na kiswahili kama somo na hiyo sasa inaenda vilevile kwa upande wa zile shule zinazotumia lugha za kiingereza toka awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwalimu hakatazwi kuweka msisitizo katika lugha ile ambayo anafahamu inaeleweka na wanafunzi kwa uzuri zaidi ili kumfanya yule mwanafunzi kile kilichofundishwa aweze kukitafsiri katika lugha yake iliyo rahisi na kukielewa vizuri zaidi. Ieleweke kwamba lugha pekee siyo maarifa. Lugha pamoja na yale maarifa unayofundishwa ndiyo yanayomfanya mwanafunzi kuwa imara na kuweza kutumika katika nyanja mbalimbali zinazohitajika. (Makofi)
MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nazungumzia shule hizi ambazo tunazijenga kutokana na umbali wa shule mama. Kuna maeneo ni zaidi ya kilometa 20 watoto wanatembea, hata hawa kuanzia darasa la nne mpaka darasa la saba wanatembea zaidi ya kilometa 20 kwenda na kilometa 20 kurudi, tunasababisha wasichana kukatisha masomo yao kutokana na kupata mimba, lakini pia tunasababisha wavulana kuona hakuna umuhimu wa kwenda kusoma kwa sababu ya umbali wa shule hizi.
Je, kwa nini sasa Serikali haioni umuhimu wa kutumia kigezo hicho kuzisajili shule hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili Mheshimiwa Waziri amesema moja ya sababu ya vigezo vinavyoweza kufanya shule hizo zisisajiliwe ni kutokuwa na ofisi za Walimu Wakuu na kadhalika kama alivyovitaja. Baadhi ya shule zetu nyingi hizo tunazoziita za satellite zimeshajengwa kwa asilimia zaidi ya 80 zimekamilika lakini bado hazisajiliwi. Wakaguzi wakija wanatoa kila siku sababu mpya. Kwa nini shule hizi ambazo zimetimiza zaidi ya 80% ya vigezo zisijaliwe? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni lengo la Serikali kuhakikisha kuwa wanafunzi wote wanaotakiwa kusoma wanasoma, kwa hiyo shule hizi zinapoanzishwa ni vema kukawa na ushirikishwaji vizuri. Kwa mfano kuanzisha shule katika maeneo ambayo yanatambulika rasmi, kama ni vijiji ni vijiji rasmi isiwe ni yale maeneo ambayo watu wanaenda labda pengine kwa shughuli za kilimo za msimu tu halafu wakasema kwamba wanaanzisha shule kwa sababu shule inatakiwa iwe endelevu.
Sasa kama kuna shule ambazo zimeanzishwa kwa mujibu wa kamati za shule zinatambua na kwa jinsi ambavyo wananchi walioko huko ni wengi wa kutosha na kuna hiyo miundombinu ya kutosha na bado haijasajiliwa, basi mimi nashauri wafuate tataribu na mimi nitakuwa tayari kusaidia kama hizo shule zinakidhi vigezo husika.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Pamoja na jitihada za Serikali kudhibiti taasisi ambazo zinatoa elimu na mafunzo ambazo hazijakidhi vigezo kwa maana ya kusajiliwa bado kuna taasisi ambazo zinaendelea kufanya hivyo, kwa mfano ni Chuo kimoja ambacho kinaitwa Dodoma College of Business Management ambacho kiko hapa Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niombe au niseme Mheshimiwa Waziri anaweza kufuatilia na kujiridhisha kuona kwamba Chuo hiki cha Dodoma College of Business Management hakijasajiliwa? Kwa sababu kinasababisha hasara kwa watoto, kwa miaka minne mfululizo chuo hiki kimekuwa kikitoa vyeti ambavyo havitambuliwi na NACTE wala VETA yuko tayari kufuatilia na kujiridhisha?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kusema kwamba ni marufuku Chuo ambacho hakijasajiliwa rasmi kuanza kutoa mafunzo na kuanza kukusanya ada kwa wazazi kiasi cha kusababisha usumbufu baadaye. Vilevile kwa hicho chuo ambacho unakizungumzia nitaomba nipate taarifa ili tuweze kukifuatilia.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Kwa sababu katika Wilaya ya Mkalama ziko shule shikizi ndio hizo satellite schools za Ilangida, Songambele, Ilama pamoja na Mkola ambazo zinafanya kazi lakini hazijasajiliwa. Na TAMISEMI tuliona udahili au uandikishaji unakuwa ni wa kiasi kidogo kwa sababu wanafunzi wengine wadogo wanashindwa kwenda mbali.
Je, Waziri yuko tayari kuingilia suala hili na kuhakikisha shule hizo nne zimesajiliwa, ambapo zimeshajengwa na miundombinu ipo kwa asilimia 80 kama alivyosema muuliza swali?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi kama nilivyosema hapo awali kama shule inakidhi vigezo na inastahili kupata usajili basi ni suala la kuwasiliana tuweze kufanya hivyo.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, wakati Waziri anaendelea kufanya utafiti juu ya Grafo Gemu, je, Serikali ina mpango mkakati gani wa haraka wa kuweza kuwapatia baadhi ya vifaa ili wataalam wetu hao waendelee kuwasaidia watoto wetu pamoja na kwamba suala hili litakuwa ni suala la Kitaifa?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ni ya hapa kazi tu; je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kuongozana na mimi wakati Bunge likiahirishwa ili akaone juhudi za wataalam hawa watokao SEKOMU wanaofanya kazi kubwa kuwasaidia watoto wetu hasa mama yangu mtaalam anaitwa mama Gorosho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimezungumza kwamba Wizara ingependa kujiridhisha namna gani teknolojia hiyo inavyofanya kazi na namna gani inavyoweza kuwanufaisha wanafunzi wengi zaidi na wananchi kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kawaida yetu sisi Waheshimiwa Mawaziri wengi tumekuwa tukiambiwa kutembelea maeneo na tunafanya hivyo. Kwa hiyo, nimwambie tu kwamba nitakuwa tayari kutembelea katika eneo la Mheshimiwa Mbunge ili kujiridhisha lakini vile vile kuona uwezekano wa kutoa vifaa ambavyo vitahitajika kama ambavyo ameomba. Namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake. (Makofi)
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwanza ni vizuri Serikali ikakiri kwamba imeshindwa katika Sera hii ya Elimu Bure na nitatoa mfano. Fedha wanazopeleka katika shule zetu asilimia 35 ni fedha kwa ajili ya utawala na chini ya utawala kuna mambo matano yafuatayo: Kuna stationery, maji, walinzi, umeme na dharura. Nitoe mfano katika sekondari moja ya Babati, sekondari ya Bagara – wanapeleka milioni moja na laki saba asilimia 35 ni 302, 4716.55. Katika 324,000 mlinzi analipwa 150,000, maji 200,000 acha stationery, acha dharura, kwa hali ya kawaida walinzi wameshaondoka katika shule zetu. Maji yamekatwa katika shule zetu za msingi na sekondari. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini hawataki kueleza ukweli kwamba wameshindwa kutekeleza sera hii kwa sababu shule zetu zimeachwa sasa na hakuna maji. Naomba majibu ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa wamefanya uchambuzi huu tangu Februari, 2017 mpaka sasa hawajarekebisha haya, ni kwa nini sasa wasiruhusu wazazi wachangie maji na walinzi katika shule zao kwa sababu sasa ukitaka kuchangia tu wanasema Serikali inapeleka fedha wakati Serikali haipeleki. Watoe mwongozo tuchangie kuliko watoto wetu wakose maji na walinzi waache shule zetu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; Serikali haijashindwa! Narudia tena kusema, Serikali haijashindwa! Kwa nini nasema Serikali haijashindwa? Nimeshatembelea mikoa mingi sasa hivi, nimeshatembelea shule nyingi sasa hivi, kimsingi wanashukuru sana kwamba sasa kuna utaratibu wa wazi wa kupeleka fedha hizo kwenye shule. Wao wenyewe wanapanga, isipokuwa, lazima nikiri bado yapo matatizo machache yanayohitaji kurekebishwa. Tatizo mojawapo lilikuwa ni kutokuwa na ubora wa takwimu. Kuna baadhi ya shule zilikuwa hazijaweza kuleta takwimu zilizo sahihi na hapo ndipo tulipoweza kubaini hata wanafunzi hewa na hivyo tukaweza hata ku-save baadhi ya fedha takriban shilingi milioni 720 zilizokuwa zinaenda zikiwa hewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa Rais na sisi kupitia Wizara hizi mbili tumekuwa tukisema kila wakati kwamba, wazazi wasijitoe katika kuendelea kusaidia elimu nchini. Pale panapoonekana kuna mahitaji ya msingi zipo taratibu zimeshatolewa mwongozo, Kamati za Shule kushirikiana na wazazi kuweza kuendelea kushirikiana na Serikali katika kutatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nadhani nimejibu yote kwa ujumla. Kwa hiyo, ninachomwomba tu Mheshimiwa kule kwenye jimbo lake aendelee kuhakikisha anashirikiana na Kamati za Shule lakini pia na uongozi kuona kwamba elimu hii tunaishughulikia wote kwa pamoja na hili sio suala la kusema nani afanye, nani asifanye! Mzazi anao wajibu wa kwanza katika kuhakikisha mwanafunzi wake anasoma vizuri. (Makofi)
MHE. GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Waziri alivyosema kwamba usanifu wa majengo utakamilika mwezi Novemba 2017, swali langu linauliza, ni maeneo gani yaliyobainishwa kujengwa chuo hicho? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, wakati Serikali inaendelea na mpango wa kujenga Chuo cha VETA Mkoa wa Simiyu, Serikali ina mpango gani kuwasaidia vijana wanaomaliza kidato cha nne wanaokosa sifa ya kuendelea na kidato cha tano? (Makof)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, Chuo cha Mkoa cha Simiyu kinategemewa kujengwa eneo ambalo lipo umbali wa takribani kilometa tisa mpaka kumi ambapo kilikuwa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (FDC), eneo linalojulikana kama Kinamhala, nashindwa kidogo kutamka jina hilo, lakini ni eneo hilo.
Mheshimiwa Spika, vilevile katika swali lake la pili juu ya Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne na hawajafanikiwa kidato cha tano. Kwanza ni kwamba tunavyo vyuo mbalimbali vinavyoweza kuchukua wanafunzi wa aina hiyo lakini vilevile Serikali kupitia mpango mpya wa ESPJ, mpango ambao unajipanga katika kuzalisha ajira nyingi kwa vijana wetu wale waliomaliza darasa la saba, kidato cha nne na ngazi nyingine zote ili waweze kupata ujuzi kamili wa kuweza kujiajiri. Kwa hiyo, kuna fedha tumeshapata nyingi kabisa, niwafahamishe tu Waheshimiwa Wabunge, Waziri wangu ameshatoa maelekezo kuwa kutakuwa na semina kwenu ya kuwapitisha juu ya mpango huo ambao utakuwa na manufaa makubwa sana katika nchi yetu.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa majibu ya Serikali, kwa kuwa wananchi wa Bukene wamepata fursa nzuri ya kupata umeme na wananchi wa Bukene wamejipanga katika shughuli nzima ya ujasiriamali na tatizo kubwa wao wana ukosefu wa mitaji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wananchi wa Bukene ili waweze kupata mitaji na waweze kuanza shughuli za ujasiriamali?
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Katavi una fursa nyingi za uwekezaji na vivutio vya kutosha hasa kwenye sekta ya kilimo, uvuvi na eneo la maliasili. Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara wana mpango upi wa kusaidia Mkoa huu ili kuweza kupatiwa wawekezaji waje kuwekeza katika maeneo hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, la kwanza katika suala la mitaji, nipende tu kuwahamasisha wananchi wote wakiwemo wananchi wa Bukene kwamba mtaji wa kwanza ni mtu kuamua kufanya shughuli ya uzalishaji, mtaji wa pili ni huo wa kupata taarifa na mafunzo, lakini vilevile kufuatilia taasisi kama za benki na kwa upande wetu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kupitia SIDO kama nilivyosema awali, tunao mfuko ambao unawezesha wajasiriamali pale ambapo wapo serious katika kufanya shughuli zao.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Katavi niwaombe kupitia Serikali ya Mkoa na Halmashauri na wananchi kwa ujumla kuendelea kuhamasisha fursa zilizopo katika Mkoa wa Katavi ili wawekezaji wengi wa ndani na wan je waweze kupenda kuwekeza katika Mkoa huo. Kwa siku za nyuma mmekuwa mkifanya makongamano mbalimbali ya kukaribisha wawekezaji, nashauri muendelee kufanya hivyo.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa SIDO ndio wanaohusika kutoa elimu kwa wajasiriamali wadogo lakini imeonekana wanachaji pesa kubwa sana hasa mafunzo ya vifungashio. Ninaomba Mheshimiwa Waziri atusaidie ni jinsi gani SIDO itapunguza bei na kusaidia hao wajasiriamali wadogo waweze kufanikiwa katika biashara zao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kimsingi bei iliyokuwa inakuwa-charged ilikuwa inategemeana na gharama halisi za upatikanaji wa vifungashio hivyo. Jambo ambalo tunaweza tukafanya ni kuendelea kuangalia uwezekano wa kuipatia SIDO ruzuku ya kutosha lakini pia kuwakaribisha watu binafsi katika kutengeneza vifungashio hivyo kwa kadri itakavyowezekana.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu lakini ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.
Kwa kuwa Kenya iliruhusiwa kuuza bidhaa zake zinazozalishwa EPZ asilimia 20 bila kodi jambo ambalo alitakiwi, lakini kwa nini wakati huo huo baada ya muda mfupi Kenya hiyo hiyo ikaruhusiwa mitumba inayotaka nje badala ya kutozwa senti 40 kwa kilo watoze senti 20 kwa kilo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa nchi za Ethiopia, Afrika ya Kusini, India, Morocco na nyinginezo zinatoa mkakati maalum wa kusaidia viwanda vya nguo na ngozi ili watu waweze kuwekeza kwenye sekta hizo kwa kutoa garantees walau ya miezi ya sita na baadaye Serikali inajiondoa na wazalishaji wanaendelea na kwa kufanya hivyo Ethiopia na nchi nyingine zimefanya vizuri Je, Tanzania tuko tayari walau kujifunza kidogo kutoka katika nchi hizo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza suala la nguo pamoja na mitumba ni suala ambalo ni nyeti na suala ambalo linahusu viwanda vyetu vya Afrika Mashariki kwa ujumla. Kimsingi ni kwamba kufuatia maombi hayo kumekuwa na mambo mengine ambayo yameendelea ambayo yameendelea kujadiliwa na nchi. Lakini kubwa zaidi ni kama nilivyosema awali kwamba swala hilo lilikuwa limejadiliwa na Wakuu wetu wananchi.
Kwa hiyo, mabadiliko mengine yoyote yale ni muhimu lazima yarudi tena kwa wakuu wetu wa nchi na misingi hiyo naamini kwamba Serikali kwa kushirikiana na nchi ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki kwa ujumla wake tutapata ufumbuzi wa mambo ambayo yanayoonekana labda pengine yanakuja kuwa ni kikwazo hasa katika kuhakikisha kwamba bidhaa zinazotoka kwenye nchi zetu zinalindwa vilevile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusiana na kujifunza kutoka nchi nyingine za Morocco na kadhalika. Kimsingi wajasiriamali hawa wawekezaji wanapokuja kwenye nchi wanakuja na mitaji lakini wanakutana na sheria mbalimbali ambazo kwa upande mmoja zinakuwa zinasaidia kuwezesha uwekezaji huo, lakini upande mwingine inaweza ikatokea kwamba kuna vikwazo na sisi tumekuwa tukiendelea kujifunza na kuona namna bora zaidi ya kuwasaidia wawekezaji wetu ili waweze kukua na kuendeleza viwanda vinavyowekezwa na ajira kwa ujumla.
Kwa hiyo, ni wazo jema tutaendelea kujifunza na vilevile kuona namna bora kadri inavyoonekana kila siku ya kuweza kuwasaidia wawekezaji wetu.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Pamoja majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda napenda kuuliza maswali kama ifuatavyo.
Swali la kwanza; kiwanda cha Nyuzi cha Tabora kinazalisha vifa tiba ambavyo vinatangenezwa na pamba yetu inayolimwa hapa hapa nchini. Inazalisha vifaa kama pamba, bandage na nyuzi. Je, kwa nini Serikali kupitia MSD isimuunge mkono Mheshimiwa Rais maneno yake aliyotamka Mwanza na kununua vifaa tiba kwenye viwanda vyetu vya ndani hususan Tabora badala ya kuagiza nje ya nchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kiwanda hicho kina uwezo wa kutengeneza sare za wanafunzi (uniform). Kwa nini sasa Serikali isitoe agizo, badala ya kununua sare za shule sehemu tofauti, sare za shule zinunuliwe kwenye viwanda vilivyopo nchini? Kwanza, ili kuchochea uchumi pia kupanua ajira hususan katika Mkoa wetu wa Tabora ambao kwa kweli hauna viwanda vya kutosha. Naamini vijana wetu wa Tabora watapa ajira za kutosha kama sare zitanunuliwa katika kiwanda hicho cha nyuzi cha Tabora.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni kweli kabisa iko haja ya kuunga mkono jitihada zinazofanywa na viwanda vyetu nchini ikiwemo vifaa tiba. Kimsingi viwanda hivi wakati vinaanzishwa vilikuwa na lengo la kusaidia kutoa malighafi katika viwanda vingine, lakini baada ya kuanza biashara huria na mikataba mbalimbali tuliyosaini Kimataifa, tumejikuta kwamba baadhi ya viwanda vyetu vinashindwa kuzalisha kutokana na wadau waliokuwa wanunue vifaa hivyo kutoka kwetu wanaamua kuagiza kutoka nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo ni suala ambalo Wizara tayari tumeshaliona na tunalifanyia kazi. Vilevile kuimarisha masoko ya ndani na nje kwa hiyo kitengo chetu kitaendelea kufanyia kazi eneo hilo na hivyo niwaombe MSD waweze pia kufuatilia na kuweza kununua pamba na bandage zinazozalishwa katika kiwanda hiki nasi tutafutilia.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusu uniform; naomba vilevile kuwashawishi wadau mbalimbali ambao wanatumia uniform zinazofanana na zile zinazozalishwa katika kiwanda hiki waweze kukipatia kipaumbele pamoja na viwanda vingine ambavyo viko humu nchini. Niwaombe pia Watanzania wote kupenda bidhaa zetu kwanza. Tufahamu kwamba viwanda hivi vinapokufa vinakosesha ajira kwa watu wetu na kwa kweli uzalendo ni kutumia mali zetu za ndani. (Makofi)

WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nichukue fursa hii kumshukuru na kumkaribisha Naibu wangu mpya. Napenda nitoe jibu la nyongeza kuhusu bidhaa tiba za Tabora Textile.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Mbunge Munde Tambwe kwa jinsi alivyopigana kufufua kiwanda hiki, watu wa Tabora watamkumbuka. Nataka nisisitize tamko la Mheshimiwa Rais, Wawekezaji wa Tabora Textile na wote mnaozalisha vifaa tiba nendeni sasa hivi MSD, msisubiri MSD iwafuate. Ni agizo la Rais kwamba MSD kwanza inunue vifaa vinavyotengenezwa hapa ndiyo maana ya kutenga bilioni 269 kwa ajili ya tiba. Kwa hiyo wote nendeni mkanunuae vifaa pale, mkauze vifaa vyenu pale kwa kufuata taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili la uniform, hili wazo la uniform namshukuru Mheshimiwa Tambwe, maamuzi yetu sasa tutaleta mapendekezo kwenu na watu wasituletee mambo ya WTO. Tukiweza kununua uniform kutoka kwenye viwanda vyetu vya nguo, tutaweza kuchochea viwanda vyetu kufanya kazi na kutumia pamba yetu badala ya kununua nguo zisizofaa zinazotoka nje ya nchi. Hiyo italeta kelele tunategemea ninyi Wabunge mtusaidie kutetea viwanda vyenu vya ndani. Ahsante. (Makofi)
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na nashukuru kwa majibu hayo yanayoonesha jitihada za Serikali katika kusaidia watu wenye ulemavu. Pamoja na hayo nina maswali mawili ya nyongeza. Kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri, ningependa kujua sasa (time frame) ni lini mchakato wa kukusanya maoni ya wadau utakamilika na kwa kuwa ni miaka minne sasa na wenzetu wa Kenya tayari wameshasaini mkataba huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kutokusainiwa kwa mkataba huu wa Marrakesh kumesababisha watu wenye ulemavu wasioona kushindwa kwenda na wakati na kuendelea kuwa maskini na hasa kutokana na kukosa fursa mbalimbali za kujiongezea kipato, fursa hizo ambazo zinapatikana kwenye maandishi zinazohusu maendeleo ya nchi lakini pia ulimwengu kwa jumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba majibu hayo.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mollel kwa jitihada kubwa anayoifanya lakini pia yeye mwenyewe atakuwa shahidi, Mheshimiwa Rais wetu amekuwa ni mdau mkuu namba moja katika masuala yanayohusu watu wenye ulemavu na ndiyo maana unaona hata kwenye Baraza tayari kuna watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo jambo hili tunalichukua kwa uzito mkubwa na tutahakikisha kwamba mapema iwezekanavyo baada tu ya kumaliza hili zoezi wanaloendelea nalo lipelekwe kwenye vikao vya wataalam na kikao cha Makatibu Wakuu na hatimaye liende kwenye Baraza la Mawaziri. Mheshimiwa Waziri wangu amekuwa akilifuatilia sana suala hili na najua nadhani umeona hata anakuja kusisitiza kwamba tutafanyia kazi haraka iwezekanavyo ili watu wenye ulemavu wapate haki zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nikijibu swali la pili ni kwamba, tunatambua watakapoweza kupata machapisho ya aina mbalimbali bila vikwazo itawasaidia pia hata wao kuona namna ya kuweza kuondokana na umaskini. Kwa hiyo, naomba sana ajue kwamba suala hili tumelichukua kwa uzito mkubwa ikizingatiwa kwamba wote sisi ni walemavu watarajiwa. (Makofi)
MHE. CECILIA DANIEL PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kumekuwa na Mamlaka nyingi za usimamizi na uwezeshaji katika mipango ya Serikali hasa katika suala hili la la viwanda.
(a) Je, Serikali kupitia SIDO ina mkakati gani wa kuunganisha mipango hii na hiyo mipango ikaunganishwa na rasilimali watu wanaozalishwa katika vyuo vyetu vya Ufundi hapa nchini?
(b) Sera na usimamizi wa kodi ni mambo muhimu sana katika kufanikisha suala la viwanda. Je, ulipwaji na utozwaji wa kodi unaofanywa na mamlaka husika hapa nchini, umezingatia vipi suala hili ili kutokuhathiri sekta hii changa ambayo inakua?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, niseme tu kwamba katika ujenzi wa uchumi wa viwanda ni kwamba suala hili ni mtambuka na linafanywa na wadau mbalimbali na sekta nyingi na hivyo hata usimamizi ulikuwa umepangwa zaidi kulingana na uhalisia wa eneo ambao usimamizi wake unahitajika ufanyike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano kwenye suala la madawa na vyakula, tunazungumzia masuala ya kiafya. Kwa hiyo, unaangalia kwamba kulikuwa na kuangalia mamlaka hiyo ya usimamizi itakuwa imeweza kufanya kazi zake vizuri na kuondoa vikwazo kwa kiasi gani kama itakuwa imekaa katika eneo hilo. Hata hivyo, Serikali imekuwa ikiendelea kufanyia kazi suala hilo ili kuona namna bora zaidi ya hizi mamlaka za usimamizi zinavyoweza kuunganishwa ili kuweza kuleta tija zaidi katika uchumi huu wa maendeleo ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika, kwa suala ambalo ni la SIDO kuwa yeye sasa kama muunganishaji. Kimsingi SIDO haifanyi kazi peke yake, mfano tu kwamba kwa mfano katika Mkoa wako wa Manyara ukiangalia katika suala la uendelezaji wa zao la vitunguu swaumu, pale tayari kuna wadau wengi ambao wamehusika MIVAP ambao kulikuwa na jengo pale lakini pia katika chain ya kuongeza thamani, ukienda Magugu kuna SNV wanaoshirikiana na SIDO katika uongezaji thamani katika eneo la mpunga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika na katika eneo la Hanang, vilevile kuna suala la kuangalia menejimenti ya kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvuna. Kwa hiyo, kimsingi ni kwamba lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba wadau wote wanaunganika pamoja na kila mtu kuweka intervention katika eneo linalohusika ili kuweza kupata tija katika uendelezaji wa wajasiriamali na viwanda kwa ujumla.
MHE. RASHID M. CHUACHUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusiana na swali langu. Lakini ukweli kwamba kuna shida ya kupatikana kwa malighafi ya korosho kwa viwanda vyetu vidogo vidogo vya ndani uko pale pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi ili kuweza kuingia kwenye mnada wa korosho unahitaji kuweka bond ya zaidi ya shilingi milioni 100 ili kuweza kupata kupata korosho, jambo ambalo wajasiriamali wetu wadogo wadogo ambao wana viwanda vidogo vidogo wanashindwa kulimudu.
Sasa ni lini Serikali itaona haja ya kuhakikisha kwamba utaratibu mzuri tulionao unaendelea, lakini pia inatangeneza utaratibu wa kuhakikisha kwamba wajasiriamali wenye viwanda vidogo vidogo nao wanapata fursa ya kununua korosho kwa ajili ya kuzichakata? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kuona kwamba na yeye anaunga mkono mfumo unaoendelea sasa, ni lengo la Serikali kuona kwamba wadau wote ambao wanashiriki katika mnyororo mzima wa thamani ya korosho wananufaika. Na kwa hali hiyo basi, niseme tu kwamba baada ya kuona manufaa makubwa ya mfumo huu, lakini pia baada ya kupata changamoto kwa wadau wengine kama ambavyo unavyoeleza. Serikali itakaa pamoja na wadau kuangalia namna bora zaidi ya kuhakikisha kwamba hivi viwanda vidogo navyo vinafanya shughuli zake bila kuathirika. (Makofi)
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Katika moja ya masharti ya mkataba uliosainiwa kati ya Kampuni ya Sunshine na wamiliki wa ghala la Lindi Pharmacy ambayo kilikuwa Kiwanda cha Korosho Wilayani Nachingwea ilikuwa ni kuanza kufanya kazi Septemba, 2017. Lakini mpaka sasa ninapozungumza kiwanda kile hakijaanza kufanya kazi, naomba kupata majibu ya Serikali juu hatma ya kiwanda cha korosho Nachingwea.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia na niseme tu kwamba lengo letu ni kuhakikisha kwamba Mikataba inayokuwa imeingiwa inafanya kazi yake inavyostahili. Lakini kwa sababu suala hili limekuwa ni very specific kwa Kiwanda cha Sunshine na mimi maishani mwangu sipendi kutoa majibu ya kukurupuka au ya uongo, nitalifanyia kazi na nitakuletea taarifa inayostahili.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru sana kwa nafasi na nasikitika sana kwa majibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi (CCM) iliyoruhusu kufanya elimu kuwa commodity, kuwa biashara. Pia ni Serikali hii hii inayoleta ada elekezi na kwamba utafiti umefanyika na wamebaini kwamba shule zinatofautiana. Hapakuwa na haja ya utafiti kwa sababu inajulikana shule hizi zinatofautiana. Sasa swali langu ni kwamba wanipe sababu ni kwa nini wanataka shule hizi za binafsi ziwe na ada elekezi huku wakijua kabisa kwamba shule hizi zinatofautiana ubora na ni wazi hata katika matokeo ya mitihani kwa muda wa miaka 10 mfululizo shule hizi zinaongoza? Watupe sababu.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, nataka kujua Serikali haioni kwamba shule hizi ada inakuwa kubwa kwa sababu kubwa moja tu, kwamba kuna tozo nyingi, kwa mfano wanalipa property tax, lakini vilevile kwenye suala la ukaguzi, wakati shule za Serikali wanalipa chini ya shilingi 3,000, hawa kila mwanafunzi anapaswa kulipa shilingi 5,000 ya ukaguzi. Je, ni lini Serikali itaondoa tozo kwenye shule hizi ili ada yao iweze kuwa kidogo na ili wazazi waweze lakini pia kwa nini msiboreshe shule zenu za Serikali ili wazazi waweze kuwapeleka kwenye shule za Serikali kwa sababu hakuna mwananchi yeyote asiyependa bure?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza napenda kusema, pamoja na kwamba elimu imekuwa ikitolewa kwa kushirikiana na taasisi binafsi na pamoja na kwamba kumekuwa na element ya biashara, lakini lazima tuzingatie kwamba elimu siyo biashara per se, elimu ni haki ya kila Mtanzania na si mwenye uwezo tu wa fedha ndiyo anayestahili kupata elimu bora. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na dhana hiyo, kumekuwa na wazazi wengi ambao wangetamani kupeleka watoto wao katika shule mbalimbali, lakini wakati huo huo kumekuwa na ada za aina tofauti tofauti wakati mwingine si halisia kulinganisha na uwekezaji uliofanyika.
Hata hivyo, dhana kubwa ya uwekezaji ni pamoja na mwekezaji kuja na mtaji na si tu kuwekeza kwa kutegemea mtaji ule unaokusanywa kutokana na ada za wanafunzi kwa wakati huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hali hiyo, kutokana pia na kilio kutoka kwa wananchi wengi na hilo si tu kwamba litakuwa linafanyika kwa mara ya kwanza kwa Wizara yetu ya Elimu, bali pia limekuwa likifanyika katika maeneo mbalimbali ikiwemo mafuta kwa mfano EWURA, wamekuwa wakipanga bei kutegemeana na uhalisia ili bei zinazotozwa zilingane na uhalisia. Kwa misingi hiyo ndiyo maana tumeona kuna umuhimu wa kushirikisha wadau wengi ili kupata bei ambayo haitaathiri utoaji wa huduma, lakini wakati huo kuwawezesha wananchi wengi zaidi kufaidika na sera hii nzuri ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, pamoja na jitihada kubwa inayofanywa na Serikali ya kuhakikisha kwamba shule zake za Serikali zinaboreshwa, ikiwemo shukrani kubwa kwa Bunge kupeleka Shilingi bilioni sita kwa ajili ya Madawati, hiyo ni sehemu ya kuboresha elimu katika shule za msingi, napenda tu niseme kwamba, sehemu za tozo ambazo zimekuwa zikitozwa zinaendana na uhalisia. Kwa misingi hiyo, niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge kukaa katika viatu vya wananchi ambao wapo na tunawawakilisha kuona kwamba kila jambo tunalolifanya, kila biashara inayofanyika, inaendana na uhalisia na si kuwa ni sehemu ya unyonyaji.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Kwanza na-declare interest, mimi ni mmiliki wa shule.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyoongea, kuna vikao kadhaa vinaendelea kati ya Wamiliki, Mameneja na Serikali, Ofisi ya Kamishna Wizara ya Elimu, lakini mpaka sasa hatujafikia muafaka kwa sababu ya hiki ambacho amekiongea Mheshimiwa Naibu Waziri. Tunaonekana kama vile tunafanya mchezo, lakini jambo hili ni gumu sana. Shule zimetofautiana, wapo wamiliki wamewekeza na wamekopa fedha benki. Zipo shule zina utofauti wa vijijini na mjini. Menu ya chakula huwezi kulinganisha menu ya chakula shule za Dar es Salaam na shule za Rukwa, Mbeya ama Mwanza. Hata hivyo, mpaka wiki iliyopita, tumekutana na Serikali kwamba hata hawajafanya utafiti kwenye shule za msingi lakini ada elekezi inataka kutolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize swali, ni lini Serikali itaita tena kikao cha mwisho TAMONGSCO pamoja na Serikali wakae pamoja waweze kufanya utafiti wa pamoja? Serikali ifanye utafiti na shule binafsi zifanye utafiti ili wakae pamoja waweze kufanya negotiation ili ada elekezi itolewe si kwa upande mmoja tu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama ambavyo ameeleza Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeshawahi kukaa na wadau hao, lakini niseme tu kwamba ni msingi huo huo ambao Serikali haitaki kuwanyanyasa wawekezaji wake ambao ni Washirika wakubwa wa elimu na ndiyo maana tumefanya tafiti katika maeneo mbalimbali. Mfano, tumeshakwenda katika maeneo hata ya vijijini, kuna shule za Sekondari kama Fingwa kule Rukwa, Idigima-Mbozi na Kitunda kule Kalambo, hizo zinatoza laki moja kule vijijini kabisa kwa Sekondari lakini ukienda kwenye shule nyingine, kama Feza yenyewe inatoza shilingi milioni 9.4, ukichukua St. Joseph shilingi milioni 5.9, ukichukua Mwanza Alliance shilingi milioni 4.8 na ndiyo maana tunafanya utafiti ili kuona kwamba bei zitakazotolewa kwanza zitapangwa kutegemeana na madaraja na shule mahali ilipo na uhalisia wa utoaji wa hiyo elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo siyo lengo la Serikali kuwatesa au kuwanyanyasa wawekezaji, bali ni kutoa bei inayofanana na uhalisia na hiyo itachochea utoaji wa elimu bora, lakini vilevile uwekezaji ulio sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kikao napenda niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge, si kwamba Wamiliki tu wa shule ndiyo wanaostahili kukaa vikao, vikao hivi vitawashirikisha hata walezi pamoja na wazazi, pamoja na wananchi wengine ikiwemo Wabunge ili tupate bei zenye uhalisia.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu suala la elimu na TAMISEMI tunaguswa sana na bahati nzuri Naibu Waziri wa Elimu ametoa maelezo ya kutosha, kulikuwa na suala lini litafanyika hili, maana yake hili ndiyo suala la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba Naibu Waziri ameshazungumza kwamba, hicho kikao kitaitwa na hili naomba nikiri wazi, kwa sababu nchi yetu ni pana sana, lengo kubwa la Serikali ni kui-support private sector, lakini pia kuangalia na watu hao wanaopata huduma hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni kwamba, mchakato huu ni mpana kwa kushirikiana na wadau wote, imani yangu ni kwamba, tutakapofika mwisho wa siku hasa wamiliki wa shule na ndugu yangu Mulugo akiwa mmojawapo, tutafika maeneo ambayo Mtanzania wa kawaida wa kila level ataweza kuguswa kwa maslahi mapana ya nchi yetu.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli mbiu ya Serikali sasa ni viwanda, lakini viwanda havitakuwepo katika nchi hii kama hatutoweza kuzalisha mafundi mchundo wengi ili waweze kutekeleza majukumu mbalimbali ndani ya viwanda hivyo. Je, Serikali haioni kwamba inapoteza muda wa kutamka kwamba itakuwa ni Serikali ya viwanda wakati haitaki kuzalisha mafundi mchundo wengi ili waweze kutekeleza wajibu wao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika hali halisi
ya majibu ya Mheshimiwa Waziri jana wakati anajibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge alisema kwamba Serikali imejipanga kujenga Vyuo vya VETA nchi nzima na maeneo mbalimbali katika Taifa hili. Leo katika majibu yake anatuambia kwamba Serikali haina mpango wa kujenga Chuo cha VETA katika Mji wa Tunduma. Je, jana alikuwa akiwadanganya Wabunge katika majibu yake ya msingi aliyokuwa akiyatoa ndani ya Bunge hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi Serikali inatambua juu ya umuhimu huo wa kuendelea kuzalisha mafundi sanifu na mafundi mchundo pamoja na wahandisi, lakini njia za kuzalisha mafundi hao haziko tu kupitia VETA, zipo pia kupitia vyuo binafsi lakini pia kupitia mafunzo ya muda mfupi ambayo wanafundishwa na kuweza hata kujitegemea katika viwanda vidogo vidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huo upo, kwa mfano mwaka huu, kuna mafunzo ya vijana wapatao 23,000 ambayo yanaendeshwa na VETA ambayo ipo chini ya Wizara yetu lakini pia kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Ajira, Vijana na watu Wenye Ulemavu kuhakikisha kwamba vijana wengi wanapata fursa hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusiana na majibu yangu kwamba jana nimesema tutajenga vyuo nchi nzima. Kwanza naomba nipende kuliomba Bunge lako Tukufu, naona kuanzia jana hiyo kama ulivyosema na pengine siku zote Waheshimiwa Wabunge pengine huwa hawanisikilizi vizuri ninapotoa majibu yangu kiasi kwamba wameanza kuniwekea maneno ambayo sijazungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ni hivi Serikali ina dhamira ya kujenga Vyuo vya VETA katika kila Wilaya lakini vilevile kuhakikisha kwamba inaimarisha Vyuo vya Wananchi kila mahali vilipo ambapo vipo 55. Hata hivyo, kwa sasa kutokana na hali halisi ya kibajeti tumesema tutaimarisha kwanza vyuo vilivyopo na vile ambavyo vilishakuwa vimeanza mchakato wa kuanza kuvijenga. Kwa hiyo, sio kwamba tutajenga tu kila mahali bila utaratibu au bila fedha, naomba nieleweke hivyo tafadhali. (Makofi)
MHE. RASHID M. CHUACHUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa hali iliyoelezwa Tunduma inafanana sana na hali iliyopo katika Wilaya ya Masasi. Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha kwamba kutakuwa na Chuo cha VETA ambacho kitahudumia karibu asilimia 54 ya watu wa Mkoa wa Mtwara pamoja na wale wanaotokea katika Wilaya ya Nanyumbu? Majibu ya Naibu Waziri hayaoneshi ni lini sasa mpango huo utaanza. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachohitajika ni wananchi kupata mafunzo na mafunzo sio majengo peke yake. Kwa hiyo, kwa upande wa Masasi au Nanyumbu tunacho Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Masasi ambacho tayari kimo katika mpango wa kukiboresha kwa kukifanyia ukarabati wa zaidi na kukiongezea uwezo ili kiweze kutoa mafunzo ambayo yanafanana pia na yale yanayotolewa VETA. Vilevile kuna Chuo cha Ndanda, naomba pia wananchi waweze kutumia chuo hicho ili kuweza kupata mafunzo yanayostahili.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali la msingi linaulizia kupata ujuzi na kujiajiri na ifikapo mwaka 2030 kwenye Maendeleo Endelevu ya Dunia, Lengo la Nne ni elimu bora sawa kwa wote. Je, Serikali imejipangaje kuwa na uendelevu wa kutoa masomo kwenye sekondari zetu yaani kwenye mitaala ya sayansi, biashara na kilimo badala ya kulazimisha watoto kuchukua sayansi tu ili iweze ikawa ni endelevu watoto wakaweza kujikita kwenye uelewa wao na stadi ambazo wanazipenda zaidi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru pia kwa swali zuri. Kimsingi hata sasa hivi kwenye baadhi ya maeneo tunazo shule hata za msingi ambazo zinatoa pia mafunzo ya ufundi, lakini vilevile tunaona kwamba kuna haja ya kuwapandikiza watoto wetu ujuzi kuanzia katika ngazi za elimu za msingi, sekondari na kuendelea ikiwemo masuala yanayohusiana na sayansi na mazingira au kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachokiona tu ni kwamba, kuna ugumu wa kusema kwamba kila jambo tunalolihitaji litawekwa kwenye mtaala kwa ajili ya huyo mwanafunzi. Kupitia vipindi vyetu vya elimu ya kujitegemea na mafunzo nje ya vipindi vya kawaida bado hawa wanafunzi wanaweza wakapata pia mafunzo kama hayo.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ilani ya Chama cha Mapinduzi moja ya ahadi kubwa iliyotolewa ilikuwa ni kujenga VETA katika kila Wilaya Tanzania nzima. Kwa kuwa Mkoa wa Kagera unaongoza kwa idadi kubwa ya wanafunzi wanaomaliza darasa la saba na kidato cha nne lakini wanashindwa kujiendeleza kutokana na ukosefu wa vyuo hivyo. Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha vijana hawa wanajengewa vyuo hivyo angalau hata katika Wilaya tatu za Mkoa wao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa Mkoa wa Kagera ni kweli kuna uhitaji wa fursa hizo, lakini tayari kuna Chuo cha VETA pale Makao Makuu ya Mkoa. Vilevile kuna Chuo cha Wananchi Karagwe (KVTC) ambacho tunaendelea kukifanyia ukarabati na sasa hivi tayari tupo kwenye hatua za mwisho ili kiweze kuchukua wanafunzi wengi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna Chuo cha Maendeleo ya Wananchi cha Gera ambacho nacho kilikuwa katika hali mbaya sasa hivi kimeshafanyiwa ukarabati na tutaendelea kukiboresha ili kiweze kuchukua wanafunzi wengi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa niseme kwamba, kwa Mkoa wa Kagera kuna fursa kubwa ambapo tuna chuo tunategemea kukijenga kule Muhengele ambacho kitakuwa kinatoa mafunzo ya ujuzi wa juu zaidi kidogo kulingana na mahitaji ya soko kwa kushirikiana na ndugu zetu wa China.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Chuo Cha Maendeleo ya Wananchi Tarime miundombinu yake ni mibovu sana na haina hadhi ya kuwa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi. Kwa bajeti ya mwaka jana 2016/2017, Serikali iliahidi hapa kwamba Vyuo vyote vya Wananchi vitapandishwa hadhi na kuwa VETA. Napenda kujua sasa ni lini Serikali itaenda kutimiza azma yake ya kupandisha Vyuo hivi vya Wananchi kuwa VETA kwa kuanzia na Chuo cha Wananchi cha Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba kuna dhana ya kufikiria kwamba labda mafunzo yanayotolewa na VETA ni bora zaidi kuliko yale yanayotolewa na Chuo cha Wananchi. Nitake tu kusema kwamba Vyuo vya Wananchi vina uwezo mzuri na mkubwa sana katika kutoa mafunzo isipokuwa kwa muda mrefu vilikuwa havijapewa haki yake ya kuendelezwa na kufanyiwa ukarabati unaostahili pamoja na kuwekewa miundombinu na vitendea kazi vya kufundishia kama inavyostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu Wizara imetenga jumla ya shilingi bilioni 12 kwa ajili ya kufuatilia vyuo hivyo na kuvirekebisha. Kwa hali hiyo, tutafuatilia pia Chuo cha Tarime kama alivyoeleza Mheshimiwa Mbunge ili kiweze kusaidiwa.
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kweli nasikitika hili jibu ni la juu juu mno. Hii Wizara imeshafanya mambo mengi tunayoyajua, ningetegemea hapa ingekuwa ndio wakati Serikali ingetueleza ambayo wameshafanya na yale ambayo bado. Hata hivyo, tumeletewa taarifa ambayo mwananchi wa kawaida anayesikiliza sasa hivi wala haelewi kama Serikali imefanya chochote katika masuala ya viwanda katika maeneo maalum wakati nafahamu kuwa yameshafanyika mengi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, basi baada ya kusema hivyo nina maswali mawili ya nyongeza. Sasa katika hayo maeneo ambayo yametengwa ambayo nayafahamu kuna industrial parks, stand alones na kuna maeneo mengine ambayo ni ya Wilayani; ni mangapi ambayo mpaka sasa hivi yameshawekewa hiyo miundombinu saidizi na miundombinu wezeshi na kiasi gani ambacho tayari kinazalishwa na mapato kiasi gani nchi inapata na ajira kiasi gani kimeshazalishwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuzingatia kuwa katika changamoto ambazo zinakwamisha na ambazo zimekuwa zikikwamisha kuendelezwa maeneo haya nyingi ziko katika uwezo wetu kuzitekeleza. Hiyo miundombinu inayozungumzwa ni kitu ambacho kiko kwenye uwezo wetu tukiamua. Haya masuala ya utata kati ya special economic zones na economic processing zones yanaweza kutatuliwa. Sasa ni kwa nini basi hatujakamilisha japo tuwe tuna maeneo mawili kila mwaka yanayofanyiwa kazi? Maana yameshatengwa na wananchi wamezuiwa kuyaendeleza lakini sisi hatujayafanyia chochote zaidi ya miaka 10 sasa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nashukuru pia kwa majibu na maelezo ya Mheshimiwa Mbene. Kimsingi majibu yaliyoletwa ni majibu sahihi isipokuwa kwa maswali yake ya nyongeza naomba nimjibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza; katika suala la uendelezaji wa maeneo hayo, ninavyofahamu ni kwamba katika uendelezaji wa miundombinu kuna miundombinu ambayo ni direct inayotokana na uwekezaji wa moja kwa moja katika eneo la economic processing zone au (SEZ); lakini pia kuna maeneo wezeshi yanayofanywa na sekta nyingine kama nishati pamoja na maji na miundombinu mingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa misingi hiyo, kwa mfano, ukisikiliza katika michango ya jana kuna uwezeshaji mkubwa uliofanyika na Serikali kwa ajili ya bomba la gesi ambalo mpaka sasa limezunguzwa kwamba itatumika takribani asilimia sita; lakini bomba hilo itakuwa tayari kuwekeza viwanda 190 vinavyotarajiwa katika Bagamoyo Economic Zone na maeneo mengine. Kwa hiyo, ni tayari Serikali imeshawekeza fedha nyingi katika miundombinu ya aina hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukirudi pia Benjamini Mkapa pale kuna miundombinu ambayo imewekezwa na Serikali lakini pia na wadau binafsi jumla yake ni takribani bilioni thelathini na saba na ina uwezo kuajiri watu moja kwa moja 5,000 ambao wanazalisha ajira zisizo rasmi zaidi ya 12,500. Hiyo yote ni uwekezaji ambao umefanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwa upande wa Kigoma economic processing zone, pale tumepata mwekezaji binafsi ambaye yeye amewekeza umeme wa sola wa takribani mega watt 5 ambao uko tayari inangojewa tu kuunganishwa kwa upande wa TANESCO. Kwa hiyo kimsingi Serikali imekuwa ikiwekeza na inaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande maeneo ambayo yalitengwa katika mikoa Serikali imelipa fidia maeneo mbalimbali ikiwemo Kurasini ambayo tumelipa takribani shilingi bilioni mia moja na tatu na maeneo mengine kama Songea na Mara na mengine. Kimsingi tunachozungumza sasa hivi ni kwamba badala ya kuchukua fedha yoyote ya Serikali kuifungia katika kuilipia maeneo na wakati mwingine hao wawekezaji wanakuwa hawajajitokeza. Kwa hiyo tunachofanya sasa ni kuwashirikisha wawekezaji wenyewe ili yule anayehitaji eneo maalum basi aweze kusaidia katika kulipa fidia na kulitumia kwa malengo ambayo yanakuwa yamekusudiwa kwa win win stuation kwa upande wa Tanzania na huyo mwekezaji wetu.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa sababu miradi hii ni ya muda mrefu na miundombinu yake inazidi kuharibika kama vile vifaa ambayo viko pale kuna kama nondo na vifaa vingine vinazidi kuharibika, kwa sababu Serikali imeshatenga pesa kwenye bajeti ya 2017/2018, kwa nini Serikali isichukue hatua za dharura kupeleka pesa hii ili iweze kukamilisha miradi hii kwa sababu ya umuhimu wake?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, pale kwenye miradi ile kuna walinzi ambao walikuwa wamewekwa pale, walinzi hao wametelekezwa muda mrefu na imefikia wakati hao walinzi wameondoka, pale hakuna walinzi. Serikali haioni pasipokuwa na walinzi inaweza ikasababisha vifaa vingine kuibiwa na kuharibu miundombinu ya mahali pale?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo amezungumza kwamba miradi hii ni ya muda mrefu, lakini ni muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya wananchi, nimuahidi tu kwamba nitafuatilia kuona kwamba kama tunaweza tukapata fedha hizo zilizotengwa kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusiana na walinzi, niiombe Halmashauri ya Kyerwa kuhakikisha kwamba hata kwa kutumia wananchi wanaoishi katika maeneo hayo ni vema kuendelea kulinda miundombinu hii ambayo tayari ipo wakati tukiendelea kupata fedha kwa ajli ya kukamilisha miradi hiyo.
MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza yenye seheu (a) na (b).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ubora wa tumbaku unategemea sana upatikanaji wa mbegu, mbolea, madawa kwa wakati muafaka. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha pembejeo zinawafikia wakulima kwa wakati unaotakiwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni nini faida na hasara ya kumruhusu mnunuzi kupeleka mbolea kwa wakulima?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kama inavyofahamika kwamba zao hili la tumbaku limekuwa na mchango mkubwa sana katika uchumi wa nchi yetu. Kwa misingi hiyo, Serikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha kwamba pembejeo zinapatikana na zinawafikia walengwa kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nini tatizo la kumfanya mnunuzi aweze yeye kupeleka mbolea. Mnunuzi mzuri anapopeleka mbolea kwa tija ili mwananchi huyu apate hiyo mbolea kwa tija huwa hakuna tatizo lakini kuna wanunuzi ambao ni wanyonyaji ambao wanapeleka mbolea na kumwambia mwananchi kwamba ukishapata hii mbolea yangu na mazao yako yote lazima uniuzie mimi kwa bei anayoitaka yeye, huo ni unyonyaji na mnunuzi wa aina hiyo huwa tunakuwa hatumtaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndiyo maana sasa hivi kupitia maagizo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa, katika mazao makuu matano ya nchi hii yanawekewa utaratibu maalum ili kuhakikisha kwamba vyama vya ushirika viwe na nguvu na kusaidia kuwawezesha wananchi ili wasiendelee kunyonywa.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kila Wilaya nchi nzima vijana wametenga maeneo kwa ajili ya shughuli za kiuchumi. Je, Serikali lini itaona umuhimu wa kutumia maeneo haya kwa ajili ya uzalishaji wa malighafi hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, tumekuwa tukiona Serikali ikihamasisha wakulima wetu kulima mazao mbalimbali ya kibiashara bila ya kuwa na mikakati mizuri ya masoko na matumizi. Je, ni nini kauli ya Serikali juu ya hili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ni kweli Serikali imesisitiza na imeendelea kutenga maeneo kwa ajili ya vijana pamoja na wajasiriamali wengine. Serikali katika kusaidia hilo, kwa mfano katika bajeti ya mwaka 2017/2018 tayari kupitia SIDO imetenga shilingi bilioni saba kwa ajili ya kujenga sheds yaani sehemu za kufanyia kazi ikiwa ni pamoja na kuweka viwanda. Maeneo hayo yapo katika Mikoa ya Kagera, Geita, Simiyu, Mtwara, Manyara na Katavi, hiyo ni kwa kuanzia. Kwa hiyo, niseme tu kwamba itakapotokea sheds hizo zimekamilika, tutawahamasisha vijana pia kutumia fursa hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa masoko, tumekuwa tukiendelea kuhakikisha kwamba tunalinda wazalishaji wa mafuta walioko nchini lakini vilevile kwa kushirikiana na nchi zinazotuzunguka kuona kwamba mazingira ya biashara ya mafuta ya kula ushindani wake ni ule ambao hauiathiri nchi yetu. Kwa misingi hiyo, kwa kuangalia mafuta ya kula ambayo yanaagizwa kutoka nje na uhalisia wa kodi ambazo zinatolewa tayari kuna timu inafanya utafiti ili kuhakikisha kwamba masoko yanakuwa ya uhakika na watu wanazalisha kwa faida.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipende kuipongeza Serikali kwa kuanza na miundombinu wezeshi ili miradi hii ya Makaa ya Mawe Mchuchuma na Chuma Liganga iweze kuanza. Mfano ni ile barabara ya kutoka Mchuchuma kupitia Kijiji cha Ibumi - Amani mpaka Mundindi ambako Liganga ipo. Sasa maadam kuna timu ya wataalam ambayo imeundwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wanaongea na mwekezaji.
Je, timu hii ya wataalam itachukua muda gani kumaliza mazungumzo yao na kufanya miradi hii ya Mchunchuma na Liganga ianze ikiwa ni pamoja na kulipwa na fidia?
Pili, kwa nini Serikali isichukue jukumu la kulipa fidia ili kuwafanya hawa waliopisha huu mradi wa Liganga na Mchuchuma waendelee na shughuli zao huku yenyewe ikiendelea na mazungumzo na mwekezaji?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianzie kumshukuru sana Mheshimiwa Deogratias Ngalawa kwa pongezi alizotumpa Serikali, lakini pia tumshukuru na kumpongeza yeye mwenyewe kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee kabisa nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wanachi wa Ludewa hususani katika maeneo ya Mchuchuma na Liganga kwa uvumilivu wa kuona kwamba mradi huu unaendelea kushughulikiwa kwa manufaa ya nchi wakati wakisubiri fidia zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Mchuchuma na Liganga ni mradi ambao ni wa kimkakati, kuna maliasili kubwa sana ambayo ipo pale. Mlima wa Liganga ambao ni chuma tupu, mimi mwenyewe nimeshafika pale, lakini pia na makaa ya mawe ambayo yapo Mchuchuma ni kiasi kikubwa sana cha rasilimali ya nchi ambayo majadiliano yake lazima yafanyike kwa kina na tuweze kuona kwamba tunapata haki kwa ajili ya manufaa ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo nikijibu kwa pamoja, niseme tu kwamba Serikali imekuwa ikitoa fidia katika baadhi ya maeneo, lakini sasa tunaona fedha nyingi ya Serikali imekuwa ikikaa mahali wakati mwekezaji anakuwa bado hajapatikana, kiasi kwamba ingeweza kutumika pia katika kutengeneza miundombinu wezeshi maeneo mengine.
Hivyo mkakati wa Serikali sasa hivi ni kuona kwamba tunamshawishi mwekezaji achukue pia na dhamana ya kulipa fidia kwa wananchi katika maeneo ya uwekezaji. Kwa misingi hiyo nikupe tu uhakika kwamba tutajitahidi kwa kila hali kuhakikisha kwamba majadiliano yanaenda kwa kasi, lakini sio kasi tu kuwa yenye tija kwa faida ya wananchi wa Tanzania.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatumia fedha nyingi sana za kigeni kuagiza chuma kutoka nje kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa reli ya kati.
Je, Serikali haioni haja ya kutumia fedha hizo kununua chuma kutoka Liganga na Mchuchuma badala ya kuendelea kupoteza fedha za kigeni kutoka nje? Na kama alivyoelezea…
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa reli unaoendelea sasa ni kwamba upo katika kuanza, lakini hatua za kujenga kiwanda kwa ajili ya kutegemea chuma cha Liganga ni kazi ambayo inahitaji hatua katika vipindi mbalimbali na chuma kile ni tofauti na vyuma vingine, pale tuna tinanium, tuna vanadium zote ni madini ambazo ni aghali sana na muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika ni upembuzi yakinifu katika kuwapata wataalam watakaoweza kuifanya kazi hiyo kwa utaalam wa hali ya juu unaowezekana na hivyo lazima tufate taratibu zote. Kwa hiyo, hatuwezi kusimamisha miradi mingine wakati tukisubiri mradi wa Liganga na Mchuchuma.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Tumekuwa tukiona wawekezaji wetu wa ndani wakijitahidi kuzalisha bidhaa mbalimbali zenye ubora wa hali ya juu.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kibiashara wa kuzipa kipaumbele bidhaa zetu zinazozalishwa nchini ili kuweza kuendana na ushindani wa soko hili ambalo lipo huru na lenye ushindani mkubwa ili sasa kuweza kufanana na nchi nyingine zinavyofanya? Ahsante nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kimsingi kupitia itifaki mbalimbali ambazo tunakuwa tumezisaini tunajitahidi kuwa na ushindani wa haki. Hata hivyo kwa bidhaa ambazo zinazalishwa ndani zinapewa kipaumbele na tunahamasisha wadau kupenda kununua zaidi bidhaa zetu za ndani kuliko hata hizo za nje. Vilevile wakati mwingine pia kuna tozo ambayo inatolewa katika baadhi ya bidhaa zinazotoka nje ili kufanya bidhaa za ndani ziweze kuwa na nafasi nzuri zaidi katika ushindani. (Makofi)
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Shule hii iliyotajwa na Mheshimiwa Gimbi na ninapenda nimshukuru kwa swali lake, lengo lake ni kwamba kuipandisha kuwa high school, lakini kwa mpangilio wa Wilaya ya Busega tumeipanga kuwa ni Chuo cha VETA. Je, ni lini Serikali kupitia Wizara ya Elimu itatusaidia kuwa na shule ya VETA katika majengo haya Sogesca?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi ipo tayari kwa kila fursa inayojitokeza, kwa hiyo tutaenda kuangalia kuona kama inafaa, basi tutafanya hivyo.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa bado hali ya upatikanaji maji katika baadhi ya mabweni hasa vyooni haujarekebishwa pamoja na kutengewa hizo shilingi bilioni mbili na kupatikana hizo zilizopatikana. Je, ni lini Serikali itafanya zoezi la dharura kuhakikisha maji yanapatikana hasa hizi sehemu za vyooni wakati ukarabati mkubwa ukiendelea?
Swali la pili, nilitaka kufahamu katika ukarabati huo, je, Serikali ina huo mpango wa kuyabomoa kabisa yale majengo yaliyochoka na kuyaweka mengine yenye sifa na haiba ya Chuo hiki Kikuu cha Mzumbe na lini jambo hili litatekelezwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. la kwanza; katika kufanya marekebisho ya dharura tayari tumeshawaelekeza na hatua zinachukuliwa kuhakikisha kwa kutumia fedha zao za ndani Chuo cha Mzumbe kitaanza mara moja katika ukarabati wa miundombinu hiyo ya maji.
Lakini vilevile katika mpango wa kudumu kuhusiana pia na majengo ambayo yana hali mbaya, kwa mwaka huu wa fedha unaoanza Wizara yetu imejipanga vizuri sana na kwamba tuna fedha taslimu takribani shilingi bilioni 56 hizo tunazo mkononi kwa ajili ya kuboresha vyuo vyetu mbalimbali ikiwemo Mzumbe ambayo itapatiwa mabweni ya kutosha wanafunzi 3,000 pamoja na kumbi za mihadhara na majengo mengine ya utawala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vyuo vingine ni pamoja na Chuo Kikuu Huria ambacho kitapata jengo hapa Dodoma, Chuo cha Ushirika-Moshi lakini pia mabweni ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na pale DUCE.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.
Wakati Serikali inajibu swali mwezi Januari mwaka huu iliahidi kutenga fedha kwa mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya ukarabati na kuvifufua vyuo vya watu wenye ulemevu; na kwa kuwa fedha hii haijatengwa, je, Serikali ina kauli gani kwa hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wizara inazo fedha kwa ajili ya kufufua baadhi ya vyuo vya watu wenye ulemavu kupitia mradi wake wa P4R. Kwa hiyo naomba uwe na amani ni kwamba zoezi hilo litafanyika kama ambavyo tumeanza katika shule nyingine ikiwemo shule ya Luwila pale Songea, shule ya Kipera pale Iringa na nyinginezo.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kuwa Mkoa wa Tabora ni Mkoa ambao uko katikati ya Mikoa ya Singida, Shinyanga, Kigoma na Katavi; na kwa kuwa Mikoa hii haina Vyuo Vikuu vya Serikali ambavyo mwanafunzi anaweza akapata mkopo wa Serikali tofauti na Open aliyoisema Mheshimiwa Waziri, ni lini sasa Serikali itaweka mkakati wa kukipandisha hadhi Chuo cha Uhazili Tabora ambacho ni kikubwa na ni kizuri kama ilivyofanya katika Chuo cha Chang’ombe cha Dar es Salaam na katika Chuo cha Ushirika Moshi, walivipandisha hadhi, sasa wana mpango gani wa kupandisha hadhi Chuo cha Utumishi wa Umma cha Uhazili cha Tabora? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiwe Chuo Kikuu cha Serikali ambacho kitaweza kutoa degree ambayo sasa hivi haitoki.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, ahsante na nashukuru kwa maswali yake ya nyongeza; nikianzia na umuhimu wa Mikoa ya Tabora pamoja na jirani zake kuwa na Chuo eneo hili, kimsingi Vyuo Vikuu ni Vyuo vya Kitaifa na kwa sasa hivi tuna Vyuo ambavyo bado havijaweza kudahili kwa idadi ambayo ni ya kutosha kwa mfano Chuo Kikuu cha UDOM bado kina nafasi nyingi na hata vyuo vingine, kwa hiyo tutakuwa tunaanzisha Vyuo kulingana na uhitaji.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Chuo cha Uhazili Tabora ambacho kimsingi kipo chini ya Wizara ya Utumishi, naomba tu niseme kwamba hiyo sasa itategemeana na hali halisi ya Mazingira na uainishwaji wa kozi husika kulingana na mitaala iliyoboreshwa, ikitokea hivyo nadhani Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba wataona namna gani kinavyoweza kufanyika.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na namshukuru pia Mheshimiwa Naibu Waziri wa Elimu kwa majibu mazuri nipende tu kusema yafuatayo:-
Mheshimiwa Spika, Chuo hiki ni mahususi kabisa kwa kuwaendeleza watumishi wa umma na kitaendelea kubaki hivyo na kama alivyoeleza kwa masuala ya Vyuo Vikuu kwa kuwa yako chini ya Wizara ya Elimu endapo wataona kuna haja ya kufungua Vyuo Vikuu vingine hayo yako chini yao, lakini kwa Chuo hicho cha Uhazili ni Chuo cha Watumishi wa Umma na tuna mipango ya kuviendeleza zaidi ili kuhakikisha kwamba wanatoa kozi nyingi kuwahudumia Watumishi wa Umma. Ni mafunzo maalum kwa watumishi wa umma.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na pia namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri katika majibu yake amekiri kuwa mitaala na vitabu vya elimu ya awali na msingi vinavyotumika upande wa Zanzibar ni tofauti na vya Bara.
Je, haoni kuwa kitendo hicho kinafifisha na kudhoofisha uwezo wa wanafunzi ambao wanaanza mitaala mipya badala ya kuendeleza ile waliyokuwa nayo na kusababisha wanafunzi kutoka Zanzibar kutofaulu vizuri mitihani yao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; kwa kuwa Naibu Waziri amekiri kuwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar huendesha mitihani ya elimu ya awali na msingi Zanzibar, na kwa kuwa Baraza la Mitihani Zanzibar lipo, Serikali haioni kuwa ni wakati muhimu sasa iruhusu mitihani ya kidato cha nne na cha sita ikatungwa na kusahihishwa na Baraza la Mitihani la Zanzibar na kupewa hadhi sawa ya Kitaifa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema awali, kwa kuwa vitabu katika eneo hili la mafunzo katika elimu ya awali na msingi vimekuwa vikitungwa upande wa Zanzibar, basi kwa kushirikiana imeonekana kwamba ni vyema wao wenyewe kuendelea kutunga hiyo mitihani. Hata hivyo tuelewe kwamba suala la Baraza la Mitihani ni suala ambalo lipo katika mambo ya Muungano katika jedwali la kwanza namba 16.
Kwa hiyo, kwa misingi hiyo pale inapotokea kwamba kuna haja ya kufanya marekebisho ina maana ni suala la Kikatiba ambalo inabidi kufuata taratibu za Kikatiba katika kupata marekebisho kama hayo. (Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa swali la msingi linahusiana na kutokuwa na usawa katika suala la mitihani naomba niulize swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa na huku Bara kuna tatizo kubwa sana kwamba kuna wanafunzi wa sayansi wana maabara nzuri sana lakini wengine hawana maabara lakini mitihani inakuja sawa. Je, Serikali haioni kuna haja sasa ya kuhakikisha kwamba shule zote zinakuwa na maabara ili wanapotungiwa mtihani wawe sasa wana usawa katika mitihani hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli pale inapokuwa kwamba wengine wana fursa za kujifunzia zilizo kamili tofauti na wenzao na wakapata mtihani unaofanana si jambo jema ndiyo maana marekebisho yanafanyika. Jambo hilo kwa kweli haliko katika elimu tu, na hata katika masuala ya maji nimesikia Waheshimiwa Wabunge wakisema kwamba vijijini hakuna maji, mjini kuna maji na vitu kama hivyo. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba inatoa fursa na usawa katika maeneo yote kulingana na mahitaji ya wananchi wake. (Makofi)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ambayo yametolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Elimu ningependa pia kutoa ufafanuzi kwamba utaratibu ulioko kwa sasa kwa shule ambazo hazina maabara lakini kuna wanafunzi wanafanya masomo ya sayansi, wanakuwa na mtihani tofauti na hawalazimishwi kufanya practical. Kwa hiyo kuna kitu ambacho kinaitwa alternative to practical.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mpango wa Serikali kama ambavyo tumekwisha eleza katika swali ambalo lilikuwa limeulizwa hapo awali ni kwamba tunataka kuhakikisha kwamba shule zote zina maabara na zinakuwa na vifaa ili hatimaye hii alternative to practical ambayo imekuwa ikitolewa isiendelee kuwepo. Ahsante.
MHE. SAADA MKUYA SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwakatika jibu la msingi Mheshimiwa Naibu Waziri alisema kwamba hii Bodi ya Baraza la Mitihani ni suala la Muungano katika Katiba imo katika nyongeza. Sasa nataka tu kumuuliza, hivi kuna wawakilishi wangapi kutoka Zanzibar katika Bodi ya Baraza la Mitihani na kwamba kama tunaona idadi hiyo inakidhi matakwa na haja ya wanafunzi kutoka Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyofahamu ni kwamba shughuli zote zinazofanyika zinazohusu masuala ya Muungano yanashirikishwa kikamilifu kwa pande zote mbili kwa idadi ni ngapi, kwa mujibu wa taratibu za Kibunge nadhani sitaweza kumpa hiyo namba kwa sasa hivi. Ahsante.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Ahsante Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la nyongeza ninalo. Je, Serikali ina mpango gani ya kuwasaidia vijana wanaohitimu mafunzo ya ufundi kama hao wa Makete kupata angalau vifaa tu vya kuanzia kazi?
Swali la pili, Halmashauri ya Mji Njombe ina shule za sekondari 22 na zoezi hili la kujenga Vyuo vya Ufundi linaonekana sasa kwa Serikali limekuwa gumu sana na linakwenda pole pole sana.
Je, Serikali ipo tayari kupokea ushauri, sasa ianze kuzibadilisha baadhi ya shule za sekondari kuwa shule za ufundi ili kusudi vijana wetu walio wengi watakaokuwa wanahitimu Kidato cha Nne waweze kuwa mafundi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Kimsingi ni kwamba VETA imekuwa ikifanya hivyo baada ya kumaliza mafunzo ya ufundi kwa baadhi ya wanafunzi wanaohitimu wamekuwa wakipewa vifaa kwa ajili ya kuanzia shughuli zao za kiufundi, pia kusaidia kutengeneza clusters za hao wanaokuwa wamehitimu pamoja na wengine ambao wamekuwa wamehitimu mafunzo ya ufundi siyo tu kupitia VETA hata kupitia kwa wananchi wa kawaida, tunawatambua na kuweza kuwapa vifaa, vilevile kuwatambua rasmi na kuweza kuwapa vyeti.
Swali la pili la kuweza kubadilisha shule ziwe za ufundi, Wizara tayari tumeshaliona hilo na tunafikiria kubadilisha baadhi ya shule za sekondari hasa zilizokuwa shule za ufundi kama Ifunda, Mtwara, Tanga, Bwiru na shule ya Musoma ili ziweze kuwa vyuo vitakavyoweza kutoa mafunzo kwa ajili ya technicians.
Kwa hiyo, muda ukikamilika tutafanya hivyo na kwa mwaka huu tunategemea tuanze kujenga shule mbadala kwa sababu shule hizi zinachukua wanafunzi wa sayansi kwa kidato cha tano na sita na form one mpaka form four tunawajengea shule yao ili hayo majengo ambayo ni muhimu sana kama workshops yaweze kutumika kwa Vyuo vya Ufundi.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Kampasi ya DIT iliyoko Myunga anayoizungumzia Mheshimiwa Naibu Waziri yalikuwa ni majengo ya TANROADS ambayo kwa sasa ni takribani mwaka mmoja umepita tangu Serikali ipeleke Walimu wanne, lakini hakuna maandalizi mengine yoyote yanayoendelea pale kuonyesha kwamba hicho chuo kitafunguliwa hivi karibuni. Kwenye jibu la msingi Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba hicho chuo kitafunguliwa hivi karibuni.
Mheshimiwa Naibu Waziri anatuhakikishia vipi wananchi wa Wilaya ya Momba pamoja na Mkoa wa Songwe kwa ujumla kwamba hicho chuo kitakuwa bora kwa sababu mpaka sasa maandalizi yake ya ufunguzi ni hafifu sana?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; katika Wilaya ya Ileje kuna chuo cha VETA ambacho kimejengwa kwa jitihada kubwa za Halmashauri pamoja na JICA, mpaka sasa chuo hicho hakijafunguliwa kwa sababu ya ukosefu wa vifaa. Je, Serikali sasa haioni kwamba kuna umuhimu wa kukiongezea nguvu chuo hicho ili kiweze kufunguliwa na hatimaye kiweze kutumika kama chuo cha VETA kwa Mkoa wa Songwe ukizingatia kwamba mpaka sasa Mkoa wa Songwe hakuna chuo cha VETA? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Chuo cha Myunga, kwanza nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wenzetu TANRODS kwa kukubali kambi hiyo itumike kwa ajili ya kutoa mafunzo kupitia Chuo cha DIT. Kimsingi ni kweli kwamba ile kambi haikuandaliwa kama Chuo cha Ufundi, kwa hali hiyo ilibidi kuanza kufanya taratibu zinazostahili ikiwa ni pamoja na kuangalia ni course zipi zinaweza zikafanyika kwa kuanzia katika eneo lile. Vvilevile kupata mahitaji muhimu kama umeme, pamoja na miundombinu ambayo itakuwa sahihi katika ufundishaji na ujifunzaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shughuli hiyo imekamilika lakini tumekwama hasa katika suala la umeme na tumeona tutaanza na umeme wa Solar mna generator lakini baadaye tunategemea kupitia umeme vijiji mahali hapa patakuwa pameshapata umeme na kuweza sasa kutoa mafunzo makubwa zaidi kwa mujibu wa fursa zinazotolewa katika kampasi za vyuo vyenye uwezo wa kutoa mafunzo kuanzia ya ufundi wa sanifu mpaka degree.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika swali la pili kuhusiana na Chuo cha Ileje. Suala hili limekuwa pia likifuatiliwa na Mheshimiwa Janeth Mbene na tulikuwa tumetoa maelekezo baada ya Mkuu wa Wilaya kuja ofisini kwetu. Tulilokuwa tunaliomba kwao ni wao kuongeza eneo lile ukubwa kidogo lakini wakati huo kutupa sisi hati baada ya kupitia mikutano yao ya Halmashauri za Wilaya na RCC ili sasa kuhamisha ile ardhi kuwa katika mikono ya VETA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo sisi tutaendelea na hayo tumeshayafanya maeneo mengi ikiwemo Busekelo. Kwa hiyo, ninachoomba tu kwamba wao wenyewe wajitahidi katika kuongeza jitihada katika hilo. (Makofi)
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa, swali lilivyoulizwa na majibu ni kwamba Chuo hicho ambacho kinataka kuanzishwa kipo katika Jimbo la Momba ambalo mimi naongoza. Sasa nataka tu nimuulize pamoja na ahadi hii ambayo imetolewa na tunaamini kwamba kitaanza hivi karibuni na nina uhakika ni mwaka huu wa fedha. Je, endapo hicho anachokizungumza kisipotekelezwa ni hatua gani tumchukulie yeye kama Waziri kuwadanganya wananchi wa Momba? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi ninavyojibu lengo langu sio kusherehesha, ni lengo la kueleza Serikali ni mikakati gani inachukua. Kwa hiyo huu ni mkakati ambao hatujalazimishwa bali tunaona ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma inayostahili. Ndiyo maana tunataka kuanza na mafunzo hayo ya kawaida wakati mikakati mingine inaendelea. (Makofi)
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali moja la nyongeza kuhusiana na VETA ya Ileje. VETA ya Ileje mimi ndiyo nilienda kuomba fedha kwa wafadhili zikapelekwa pale na VETA imejengwa kwa kiasi kikubwa. Hata hivyo, hayo masharti kuwa lazima tuwe na hati ndiyo yametukwamisha mpaka sasa hivi. Kupima na kupata hati pia ni suala la Serikali vilevile. Sasa kwa nini hicho Chuo kisianze wakati suala la upimaji linaendelea? Kwa sababu ni miaka miwili sasa Chuo kimesimama na kile Chuo kingekuwa tayari kinasaidia vijana wetu wengi sana wakati suala la hati likiendelea maana nalo ni sehemu ya Serikali vilevile.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sioni kama kuna ugumu kama watu wameamua, kwa sababu kimsingi utoaji wa hati au hatua za kuweza kuchukua eneo na kupeleka eneo lingine linaanzia huko kwenye Halmashauri. Hata hivyo, toka kipindi hicho tulichoongea mpaka leo sijaona kama kuna jitihada yoyote iliyofanyika, kwa sababu maeneo mengine wameshafanya hivyo na wakafanikiwa na wao hawajafanya chochote kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tukikubaliana si lazima ipatikane hati kabisa, lakini basi hata yale makubaliano ya kwamba Chuo hiki sasa wanakikabidhi kwa VETA basi itakuwa ni jambo jema lakini hatuwezi kwenda tu kuvamia mali ambayo sio mali ya VETA. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru kwa swali na kwa niaba ya Waziri wa Elimu naomba nijibu swali la nyongeza kama ambavyo limeulizwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokupatikana kwa hati inaweza kuwa ni kigezo kweli cha wafadhili kushindwa kuwasaidia. Hata hivyo, ningeomba pengine baadaye tuonane na Mheshimiwa Mbene tujue wamekwama wapi, kwa sababu kama ni suala la taasisi ambayo ni ya Kiserikali na imepitia katika process zote sasa kuna mahali watakuwa wamekwama wao wenyewe katika kufuatilia hati ama kwenye malipo au kitu kingine. Kwa hiyo, nitawasiliana nae ili nijue wamekwama wapi na tuone tunawasaidiaje ili waweze kupata huo ufadhili.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, umekuwa ni utaratibu wakati wa mtihani wa kidato cha nne Serikali inapeleka askari tena askari wenye silaha kwenda kuwasimamia watoto wakati wanafanya mtihani. Kitendo hiki kinawatia uoga wanafunzi kwa sababu hawajazoea kusimamiwa na askari wakati wakifanya mitihani au wakati wanajisomea, hivyo wanapoteza concentration katika mitihani na hii inawapeleka wengine kufeli.
Je, Serikali haina njia mbadala ya kuhakikisha kunakuwa na ulinzi lakini usiotisha kama vile kuweka askari ambao hawana uniform na hawana silaha ili waweze kuwasimamia watoto hawa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, tunaaminishwa kwamba mtihani wa mwisho sio pekee ndiyo unaomfanya mtoto afaulu katika mitihani yake ya kumaliza kidato cha nne, kwamba continuous assessment inachukua asilimia 50 na mitihani ya mwisho inachukua asilimia 50, kama hili ni kweli kuna sababu gani ya kuweka ulinzi mkubwa wakati wa mtihani wa mwisho wakati ule unachangia tu asilimia 50? Je, ulinzi huo pia unawekwa kwenye zile continuous assessment ili kufanya usawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kimsingi tunapoweka ulinzi lengo si kuwatisha watahiniwa bali kuhakikisha kwamba mazingira hayo yanakuwa salama kabisa. Kama ambavyo imeshuhudiwa katika siku za karibuni, hali ya uhatarishi imekuwa ikijitokeza katika aina tofauti tofauti. Kwa kweli siamini kama wanafunzi wa Kitanzania wanaweza wakamuogopa askari kwa sababu ni maisha yao ya siku zote, hawezi akawa hamuoni kabisa askari, karibu kila mahali nchi hii imeimarisha ulinzi na askari kama polisi tuko nao siku zote tena kuna ulinzi jumuishi na shirikishi.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa misingi hiyo mimi nadhani kwamba lengo la muhimu lieleweke kwamba ni kuhakikisha kwamba tunaweka mazingira salama kabisa ambayo wanafunzi wale badala ya kuogopa askari kwao ni suala la usalama ili wafanye mitihani yao bila kupata uhatarishi wa aina yoyote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa kupimwa kwa kufuata matokeo endelevu (continuous assessment), ni kweli tumekuwa tukifanya hivyo na hiyo haiwezi kuwa ndio sababu ya kusema kwamba kwa sababu marks tunazozitegemea mwishoni ni asilimia 50 tu, basi tusiwawekee mazingira ya usalama. Tutaendelea kufanya hivyo, na kwa sababu umetoa hoja hiyo, tutafanyia kazi kama tukiona kweli mwanafunzi anaogopa sana askari tutajua namna bora zaidi ya kufanya.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naomba niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, mitihani ya kidato cha nne tunajua inatumika kwa lugha gani lakini kuna mitihani ya darasa la saba ambapo mitihani hii inatungwa maswali ya kuchagua yote. Sasa nilikuwa naomba niiulize Serikali ni lini mtaanza kutunga mitihani ambayo si ya kuchagua, hasa katika masomo ya hesabu ili watoto wetu wapimwe uelewa badala ya kuchagua na wengine wanabahatisha kufaulu kwenda sekondari? Swali langu ni hilo.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na mtazamo wa wadau tofauti tofauti katika maswali ya kuchagua hasa katika mitihani ya hisabati. Serikali nasi pia tumekuwa tunaliangalia hilo japo katika utafiti uliofanyika ilionesha kwamba kuchagua peke yake hakumwezeshi mtu kufaulu isipokuwa lazima kwanza awe ana msingi wa kujua swali analolifanyia uchaguzi.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kwa siku za nyuma hasa kipindi chetu sisi, ni kwamba hata kama unakuwa na mtihani wa kuchagua ilikuwa bado unakuwa na sehemu ya kufanyia kazi ambayo na yenyewe inakuwa ni sehemu ya kuiangalia. Kwa hiyo, tutaona namna gani tuweze kufanya hivyo ili yule anayekuwa amechagua tuweze pia kupata uthibitisho isiwe tu kwamba swali la mwisho ndio jibu la kuliangalia, lakini ni suala ambalo linafanyiwa kazi. (Makofi)
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Mheshimiwa Spika, lengo la nne la maendeleo endelevu ya dunia ni elimu bora, sawa, shirikishi kwa wote. Suala la mitihani na udanganyifu ni mchakato mdogo to end product. Sasa Serikali ina weka lini au itaanzisha lini chombo cha kudumu cha kuangalia mchakato mzima wa elimu yaani ubora wa elimu, kuwekeza kwenye miundombinu ya elimu kwa walimu, ukaguzi, vyote yaani quality assurance itaanzishwa lini chombo hiki ili elimu yetu, mitihani iwe ni sehemu ndogo tu kama ilivyo nchi ya Finland ambapo asilimia kumi tu ndiyo ile mitihani lakini mchakato mwingine wote wa kumuandaa mtoto unakuwa umeandaliwa na umesiamamiwa na chombo chenye mamlaka na kinachojitegemea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, wizara imeliona hilo. Ni kwamba kwa sasa hivi kwanza tunaiangalia upya Sheria yetu ya Elimu kwa sababu ni ya muda mrefu na kuna mambo mengi yamejitokeza na hiyo tungependa iendane na uhalisia. Vilevile tunataka kuangalia mfumo mzima wa namna ya ukaguzi. Kwa mfano mwanzo tulikuwa na ukaguzi katika sehemu za kanda na kwenye Halmashauri/kwenye Wilaya zetu lakini sasa hivi baada ya kuongeza shule nyingi, inaonesha kwamba sasa kanda peke yake si sehemu sahihi badala yake tungeweza kuangalia mfumo mzima na tukauboresha zaidi. Hii ni kwa sababu sasa shule za Serikali kwa mfano za sekondari zimeshaongezeka sana.
Mheshimiwa Spika, vilevile tunaona kwamba haitoshi tu kuangalia shule ina walimu wangapi, madarasa mangapi na vyoo vingapi, tunataka tuangalie mfumo mzima, na hivyo wizara sasa hivi inaandaa Mfumo wa Uthibiti na Tathmini kwa ujumla (National Schools Assurance Framework) ambayo itawezesha sasa hata kama unafanyika ukaguzi unakuwa tayari una mwongozo unaokwambia ni nini unatakiwa ufuatilie. Vilevile hata kushirikisha kamati za shule pamoja na walimu na wananchi wenyewe kwa ujumla katika kudhibiti ubora wa elimu Tanzania. (Makofi)
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hiki kilinunuliwa kwa shilingi milioni 100 mwaka 2013 na mwaka huo huo Waziri Mkuu, Mheshimiwa Pinda ambaye ni Waziri Mkuu Mstaafu alifungua hiki kiwanda na tangu alipofungua mpaka leo hii hakijazalisha hata tani moja. Je, ni lini Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Bisahara na Uwekezaji atakaa na Mheshimiwa Waziri wa Nishati, ili waweze kupeleka umeme haraka kwa kuwa, tatizo ni nishati?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili pia ni lini sasa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji ataongozana na mimi kwenda Madeke kujionea mwenyewe jinsi wananchi wale wanavyopoteza fedha nyingi/mabilioni ya fedha, kutokana na kukosa soko la kuuza haya mananasi na matunda mengine? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Hongoli kwa jitihada kubwa anayoifanya katika kufuatilia kiwanda hiki na tija kwa wakulima wa matunda ya eneo hilo, lakini vilevile nichukue nafasi hii ya pekee kabisa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Nishati kwa jitihada kubwa ambayo anaifanya katika kuhakikisha kwamba, umeme unapelekwa hasa katika maeneo ambayo tunatarajia kuwa na uzalishaji mkubwa na kuongea thamani katika matunda na eneo hili tayari tumeshafanya hayo mazungumzo.
Kwa hiyo, niseme tu kwamba, ni rai yangu kwa wadau wengi kuona kwamba, umeme wa REA unaoombwa katika vijiji kweli uwe na tija na hivi tufanye uzalishaji kwa sababu gharama za kupeleka umeme katika maeneo hayo ni kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, suala la kuongozana hiyo itakuwa ni bahati ya pili kwa sababu, bahati ya kwanza tayari Mheshimiwa Waziri wangu mwezi huu ulioisha wa tatu alishaenda mpaka Njombe na amejionea hali halisi na vilevile tunategemea kujenga shades kwa ajili ya viwanda vidogo pale Njombe.
Kwa hiyo, mimi sina taabu nitaenda, nakubali kwenda huko. Ahsante.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipatia nafasi, ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Tatizo lililopo Lupembe linafanana kabisa na tatizo lililopo Mtwara Mjini, viwanda vingi vimekufa ikiwemo Kiwanda cha Kubangulia Korosho cha Oram ambacho kilikuwa kinatoa ajira kwa wananchi wengi wa Mkoa wa Mtwara. Je, Serikali ina mpango gani wa kufufua viwanda hivyo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge, kupitia Sera yetu ya Uendelezaji wa Viwanda endelevu, sisi wenyewe kama nchi tuliona kwamba, masuala yote yanayohusiana na uzalishaji yaondoke sasa kwenye mikono ya Serikali iende katika mikono ya sekta binafsi. Jambo ambalo tunafanya sisi ni kuhakikisha kuwa tunaweka mazingira wezeshi kwa kuhakikisha kuwa ile miundombinu inayohitajika pamoja na uunganishaji wa taarifa na vikwazo vyote ambavyo vinawakabili hao wawekezaji viweze kutatuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa korosho, kwanza tunashukuru kwamba kwa sasa hali ya korosho/bei ya korosho imekuwa ni nzuri, lakini sisi kama Taifa tusingependa tu kuuza korosho zikiwa ghafi. Kwa misingi hiyo, tunaendelea kufanya jitihada ya kuhakikisha kuwa viwanda mbalimbali vya korosho vinaimarishwa ili kuhakikisha kuwa tunapata tija katika zao hili.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Ukerewe ni wazalishaji wakubwa wa matunda hasa machungwa na nanasi. Lakini wananchi wa Ukerewe wamekuwa hawafaidiki sana na matunda haya kwa sababu sehemu kubwa ya matunda imekuwa ikiharibika kwa sababu ya kukosa soko.
Je, Serikali iko tayari kusaidia upatikanaji wa kiwanda cha kusindika matunda haya ili wananchi wa Ukerewe wapate soko la uhakika wa matunda yao?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba bado tunayo changamoto katika usindikaji wa matunda. Na katika mtazamo wetu Tanzania tunajipanga zaidi katika huu ukuzaji wa viwanda hasa katika eneo la kilimo na manasi pamoja na machungwa ni mazao mojawapo ambayo yana changamoto. Jambo ambalo tunaliona sasa hivi ni kwamba iko haja ya kuunganisha taasisi zetu hasa katika kukuza teknolojia zitakazowezesha matunda yanapokuwa yamezalishwa, yasiharibike kiurahisi na kuyaongezea thamani.
Lakini vilevile nikuombe Mheshimiwa Mbunge ukiwa ni sehemu ya uhamasishaji pamoja na Serikali kuendelea kuwahamasisha wadau binafsi kwa ajili ya kuwekeza viwanda katika eneo hilo.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikijinasibu kuwa ina mpango wa kujenga viwanda 100 kwa kila mkoa...
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikieleza kuwa ina mpango wa kujenga viwanda 100 kila mkoa na mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa mikoa ambayo ilikuwa na viwanda vingi tangu enzi za Mwalimu. Lakini hivi sana viwanda vingi vimekufa na vimegeuka kuwa ma-godown, mfano wa viwanda hivyo ni Kiwanda cha Komoa, Kiwanda cha Tanzania Leather Shoes, Kiwanda cha CERAMIC, Kiwanda cha U-nuts, sasa Serikali haioni kama kuna umuhimu wa kufufua viwanda vilivyokuwa ndipo ije na wazo la kujenga viwanda vipya. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza tunamshukuru kwa ufuatiliaji. Ni kweli Serikali iko serious kuona kwamba viwanda vingi vinajengwa Tanzania hasa katika kuongeza thamani mazao ya wananchi tulio nao jirani na viwanda hivyo kama ambavyo nimekuwa nikisistiza kila wakati viko katika ngazi za aina mbalimbali. Kuna viwanda vidogo sana, viwanda vidogo, viwanda vya kati na viwanda vikubwa. Kwa hiyo, wananchi wenye mitaji midogo wanao uwezo pia wa kuanzisha viwanda kulingana na hali inayowezekana.
Sasa suala la viwanda vya zamani ambavyo havifanyi kazi, kwanza tufahamu kwamba kiwanda kina tabia sawa sawa na binadamu. Kiwanda kinapokosa mazingira mazuri na wezeshi kinaweza kufa sawa na binadamu anavyokufa. Kwa hiyo, ni wajibu wetu sasa hivi kuhakikisha kuwa tunajenga mazingira wezeshi ikiwemo kupunguza au kuondoa kabisa vifo vya viwanda na hiyo ndiyo kauli mbiu na hiyo ndiyo jitihada inayofanyika ndiyo maana unakuta jitihada mbalimbali zinaendelea.
Kwa hiyo, Morogoro ni sehemu mojawapo ambayo tayari tumeshaitembelea na hivyo viwanda ambavyo unasema vimekuwa havifanyi kazi vizuri kama Leather Industries tayari tuko katika mchakato wa kuhakikisha kwamba makongano mbalimbali ya leather yanafanyika ili kuhakikisha viwanda hivyo vinakuwa vizuri na kuleta tija kwa Taifa. Na nizidi kuwaomba watanzania wengi msitishike, nimetembelea viwanda. Zaidi ya viwanda nilivyotembelea asilimia 90 vingi vinaendeshwa na sisi Watanzania wenyewe. Kwa hiyo, tujitoe hata sisi Wabunge tuanzishe viwanda kadiri inavyowezekana kulingana na mahitaji ya maeneo yetu.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Tabora ni miongoni mwa mikoa inayoongoza katika uzalishaji wa maembe. Mpaka jina la Unyanyembe likapatikana ni kutokana na uzalishaji wa hizo embe, lakini cha ajabu mkoa huo wa Tabora mpaka leo hauna kiwanda cha usindikaji wa maembe, hali inayopelekea maembe yanazagaa kila mahali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niiulize Serikali ni kwanini haitaki kujenga Kiwanda cha Usindikaji wa Maembe Tabora?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba nirejee tena nazidi kuhamasisha Watanzania pamoja na Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuwahamasisha wawekezaji katika maeneo hayo. Kwa mfano hapa Dodoma kuna Kiwanda kizuri cha Matobolo wanasindika maembe wanakausha na maembe hayo yanaweza kutumika kwa muda mrefu. Kwa hiyo, sisi tusisubiri kiwanda kije chenyewe ni lazima tuwahamasishe wadau mbalimbali hata sisi wenyewe tuweze kuwekeza ili kuhakikisha kuwa maembe hayo yanakaa muda mrefu.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ambayo yamenitosheleza, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Kwanza, kwa kuwa Serikali imekiri wazi kuwa kuna baadhi ya viwanda viliuzwa na kubadilishwa matumizi; na kwa kuwa sera ya Tanzania ni kutaka tupate Tanzania ya viwanda; je, Serikali inatoa tamko gani sasa kwa hao wanunuzi na wafilisi wa hivyo viwanda wasibadilishe matumizi na badala yake waendeleze viwanda kama Serikali yetu inavyotaka?
Swali la pili, kwa kuwa wanawake wa Dar es Salaam, Lindi na Mtwara walikuwa wanapata ajira kubwa sana katika viwanda vya kubangua korosho vya TANITA, leo hii viwanda hivyo vimewekwa kuwa maghala na maeneo ya kuweka matakataka tu mengine; hususan wanawake wa Mbagala, Kongowe, Temeke, Kurasini, Tandika, wote walio wengi walikuwa wanapata ajira katika kiwanda cha TANITA cha Mbagala; je, Serikali ina mpango gani wa kuvifufua viwanda vya TANITA vya kubangua korosho ili wanawake walio wengi waweze kupata ajira katika viwanda hivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, kwanza kuhusiana na viwanda ambayo vimebadilisha matumizi, niseme tu kama ambavyo nimesema awali. Lengo la Taifa ni kuhakikisha kwamba viwanda vinatoa ajira. Kwa hiyo, tusingependa kusema moja kwa moja kwamba ni marufuku kubadilisha matumizi kwa sababu inawezekana biashara iliyokuwepo wakati huo, kulingana na mtaji na mashine zilizopo yawezekana haiendani na wakati wa sasa. Tunachotaka ni kwamba viwanda hivyo viendelee kufanya kazi hata kwa kuangalia bidhaa nyingine ambazo zinaweza zikazalishwa hapo na kuendelea kutoa ajira.
Mheshimiwa Spika, lakini kuna wale ambao wakati viwanda vinabinafsishwa, waliandika maandika na wakapewa masharti maalum ya kuendeleza viwanda hivyo. Wengine hawajatekeleza kabisa masharti hayo na matokeo yake, viwanda hivyo vimehujumiwa na vingine vimekuwa hata mashine zake hazipo. Tunawaambia ole wao, tutapitia kimoja hadi kimoja na wale ambao wataonekana kwamba hawajakidhi matakwa ya mikataba, naamini Serikali itachukua hatua kali inayostahili.
Mheshimiwa Spika, kuhusu kiwanda ambacho ni cha TANITA, niseme tu kwamba sambamba na maelezo uliyoeleza Mheshimiwa Mbunge pia sisi tutatembelea lakini la msingi kama ambavyo nimesema awali tungehitaji kuona kwamba viwanda vyetu vinafanya kazi yenye tija na kuweza kutoa ajira kwa watu wengi zaidi ikiwemo akina mama.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, vifungashio vya mazao haya ya vitunguu katika Tarafa ya Eyasi hufanyika kwa aina mbili. Kuna kifungashio cha Mkenya maarufu wanaita net ambapo net hii ikijazwa net tatu inakuwa sawa na debe kumi; na kuna kifungashio kingine kinaitwa kifungashio cha Mganda ambapo kifungashio hiki cha Mganda kinachukua kati ya debe nane mpaka tisa jambo ambalo kwa kweli linawaumiza wakulima.
Je, ni kwanini Serikali isihakikishe kunakuwa kuna standard ya vifungashio kwa wakulima hawa ili tusiweze kuwaumiza?
Swali la pili, tatizo la ujazo kupita kiasi maarufu kama lumbesa bado ni changamoto kwa wakulima hawa katika maeneo mbalimbali na zao hili linapofika sokoni wanunuzi wanachukua yale ambayo yamejazwa kwa maana ya lumbesa kuliko yale ambayo yana ujazo wa kawaida. Mfano, labda ujazo huu unatokea Singida, unatokea Kilimanjaro, unatokea Mang’ola wale ambao wana ujazo zaidi ndiyo itanunuliwa zaidi na wale ambao wana ujazo wa kawaida ambao ni standard inakuwa hainunuliwi.
Je, ni kwa nini sasa Serikali isiendelee kutia msisitizo ili jambo hili lisimamiwe katika maeneo yote kwa ukamilifu wake ili kuwepo na ujazo ambao unafanana?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Kwanza, nisisitize tu kama ambavyo swali limejibiwa kwamba kipimo sahihi cha uzito wa aina ya bidhaa kama vitunguu ni kilogram, kwa hiyo tunachosema ni kwamba whether hicho kifurishi kitawekwa kwenye net, kitawekwa kwenye debe, kitawekwa kwenye kitu chochote kile ilimradi baada ya kuwekwa humo basi kipimwe kwenye uzito sahihi ambao ni kilogram ndivyo inavyostahili.
Pili, ulivyouliza kuhusu suala la lumbesa ni hivyo hivyo kwamba kwa mfano, unavyofungasha kwenye gunia likaitwa hili ni gunia la kilo 50 wakati ndani yake kumbe kuna kilogramu zaidi ya 50 inasababisha kwamba kwanza mkulima mwenyewe ananyonywa, lakini vilevile hata Halmashauri inaweza ikakosa mapato kutokana na kuwa na uzito ambao haustahili kutokana na kwenye kile kitu ambacho kimefungashiwa. Ijulikane kwamba siyo kwamba bidhaa zote zinakuwa na ujazo unaofanana. Kwa mfano, ujazo wa pamba kwenye kiroba ni tofauti na ujazo huo huo ukiwa ni wa viazi na ndiyo maana tunasisitiza kilogramu ambayo ndiyo kipimo sahihi ambacho kinastahili katika kupimia.
Mheshimiwa Spika, hivyo ninawaomba sana wananchi wote pamoja na wafanyabiashara kuhakikisha kwamba tunakuwa na mizani katika maeneo yetu ya kibiashara na hilo ndiyo linalosisitizwa sasa kuwa na masoko ya pamoja ili kuweza kuwafanya hawa wananchi wanaolima mazao kama hayo, kuweza kuwa na ushirikiano katika kudhibiti hali kama hiyo ya kuwa na vipimo ambavyo haviruhusiwi kisheria.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru ka kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:
Mheshimiwa Spika, itakumbukwa msimu uliopita soko la mbaazi lilisababisha kuanguka kwa bei ya mbaazi kutoka shilingi 2,000 kwenda mpaka shilingi 150, Serikali ilihaidi hapa Bungeni kwamba itahakikisha inahangaika kupata soko la kuaminika la zao hili. Sasa ni msimu wa kilimo hicho, Serikali imefikia wapi kupata soko hili na kama hali bado haileweki tuwashauri wananchi wetu waachane na mbaazi badala yake wajikite kwenye mazao mengine ambayo yana soko la uhakika?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante, ni kweli kabisa katika msimu huu ulioisha kulikuwa na hali isiyopendeza katika soko la mbaazi, hiyo ni kutokana na kwamba wadau ambao tulikuwa tunawategemea sana katika biashara hiyo ilikuwa ni wenzetu kutoka India. Niseme tu kwamba mbaazi ni chakula kizuri, mbaazi ni chakula ambacho kina protini na hata sisi wenyewe tunaweza tukala siyo kuwategemea tu watu wa maeneo mengine. Kama tunaavyosema kwamba biashara ni ushindani na kila watu wanajitahidi kuhakikisha kwamba wanakidhi soko lao la ndani, upande wa Tanzania tunaendelea kutafuta soko wakati huo tunaendelea kusisitiza kwamba hata wenyewe tupende kutumia mbaazi.
Mheshimiwa Spika, nimepita hapa katika masoko yetu kwa mfano soko la hapa Dodoma, nilipofuatilia nilikuta kwamba mbaazi zinauzwa mpaka shilingi 1,800 kwa kilo. Soko la pale Dar es Salaam kwenye supermarket mbaazi inauzwa mpaka shilingi 2,400 kwa kilo. Kwa hiyo, tusitegemee tu soko kutoka nje hata ndani ya nchi bado kuna watu ambao wananweza kula mbaazi na mimi mwenyewe ni mtumiaji wa mbaazi, vilevile tunategemea kwamba hata kupitia shule zetu tutaweza pia kuhamasisha na kuweza kupeleka chakula cha aina hiyo wakati masoko mengine ya nje yakiendelea kutafutwa.
MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza, nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza; kwa kuwa kiwanda cha mbolea hakiwezi kujengwa Njombe kutokana na kutopatikana kwa malighafi; na kwa kuwa wananchi wa Mkoa wa Njombe wanalima mwaka mzima, je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha mbolea inapatikana katika Mkoa wa Njombe kila wakati?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa wananchi wa Mkoa wa Njombe mwaka jana wamelima kwa wingi mahindi ambayo yamekosa soko na hata mwaka huu bado wamelima mahindi kwa wingi yatakosa soko vile vile. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha inawatafutia soko la uhakika hawa wananchi wa Mkoa wa Njombe?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi Serikali imekuwa ikifanya hivyo kuhakikisha kwamba mbolea inapatikana na si mara moja Waziri wa kilimo amekuwa akitoa taarifa juu ya upelekaji wa mbolea katika maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili kuhusu suala la masoko ya mahindi; kimsingi nizidi tu kuwakumbusha, ni kwamba Serikali imekuwa ikiendelea kutafuta masoko. Pamoja na kutafuta masoko tunazidi kusisitiza kuhakikisha kwamba mbali ya kuuza mahindi yakiwa ghafi ni vyema kuhakikisha kwamba mahindi hayo kwanza yanatengenezwa kama unga au chakula cha mifugo au kuhakikisha kwamba yameongezwa thamani badala ya kuyasafirisha mahindi ghafi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ambayo inapenda kusafirisha mali zake zikiwa ghafi kwa kweli si nchi ambayo itaweza kupiga hatua kubwa katika uchumi hususani katika malengo ya nchi, haya ya uchumi huu wa viwanda.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa. Niombe tu kuliarifu Bunge kwamba katika muda wa wiki moja ijayo tutafanya semina ya Bunge zima kuwaeleza mchakato mzima wa upatikanaji wa mbolea nchini. Tunatumaini kwamba katika semina hiyo Wabunge sasa tutakuwa tumekuwa na uelewa wa pamoja wa nini Serikali inafanya na kama zipo changamoto, basi hiyo itakuwa fursa nzuri ya kuzijadili ili tuweze kwenda kwa pamoja sawasawa.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Sisi Wabunge wa Mkoa wa Njombe kwa ujumla wetu tumekuwa tukilalamika sana juu ya upatikanaji wa mbolea katika mkoa wetu; na wananchi wetu ni wakulima ambao hawatumwi na mtu kwenda kufanya kazi ya kilimo. Je, ni lini sasa TFC watakuwa na godowns za kutosha ili ku-supply mbolea katika Mkoa wa Njombe?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wa Njombe kwa jitihada kubwa wanayoifanya katika kuhakikisha kwamba Tanzania inakuwa na kilimo kinachotosheleza katika ulishaji wa Taifa na kuweza kuuza nje. TFC imekuwa na maghala karibu katika kila Mkoa na hata sasa bado kuna mazungumzo yanayoendelea ya kuona kwamba pengine iweze kuwa moja kwa moja chini ya Wizara ya Kilimo ili sasa masuala hayo yaende vizuri zaidi.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa ujenzi wa Kiwanda cha Mbolea Kilwa ni suala la Ilani ya Uchanguzi wa Chama cha Mapinduzi lakini pia ni ukombozi mkubwa kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara na mapinduzi kwa kilimo chetu. Mwaka jana Serikali ilitoa ahadi kwamba mchakato unaendelea vizuri, nataka kujua mchakato huo umefikia wapi kwa sasa.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wakati najibu swali la msingi kama Mheshimiwa Nape hakunisikiliza vizuri; ni kwamba nilisema tayari kuna wawekezaji ambao wameshaonesha nia wa Makampuni ya HELM na FERROSTAAL wa Ujerumani, kwa hiyo mchakato unaendelea katika mazingira hayo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kilichokuwa Kiwanda cha Mbolea cha Tanga kimebinafsishwa na sasa zinaendelea shughuli nyingine pale ambazo hazihusiani na mbolea. Kwa mahitaji haya ambapo bado mbolea inahitajika nchini, je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa wa kukirejesha kiwanda kile ili kiweze kuzalisha mbolea?
NAIBU WAZIRI VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimshukuru kwa jinsi ambavyo anafuatilia shughuli zetu za viwanda na kulifanya swali letu kuwa makini katika eneo husika. Niseme tu kwamba ni kweli eneo hilo ambalo lilikuwa Kiwanda cha Mbolea Tanga kimebadilishwa na sasa kinashughulika na shughuli za mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba lengo la kubinafsisha ilikuwa si tu kwamba lazima kuendeleza kiwanda kile kilichopo hata kama mashine zilizopo zilikuwa hazifai. Kimsingi mashine zile zilikuwa zimezeeka sana na mwekezaji alitoa mapendekezo akaandika umuhimu wa kuwekeza katika mafuta kwa misingi ya kupokea mafuta, kuhifadhi na kusambaza na sasa hivi ana uwezo wa kusambaza mafuta kufikia lita za ujazo milioni 126.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli imekuwa ni mkombozi kwa wananchi na wafanyabiashara wote wa maeneo ya Tanga, Arusha na maeneo ya Kaskazini hata Kigoma. Kwa hiyo, binafsi nampongeza kwa uwekezaji huo kwa sababu lengo letu sisi ni kuongeza tija katika shughuli zote za kiuwekezaji.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa mikoa inayolima zao la korosho na yapo maeneo mengi ambayo ni rafiki kwa ujenzi wa viwanda vya korosho ikiwemo Wilaya ya Tunduru na Namtumbo ambapo zao la korosho linalimwa katika Wilaya hizo.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha tunajenga viwanda katika maeneo hayo ili wakulima sasa waweze kubangua korosho zao katika Wilaya hizo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi kwanza nampongeza Mheshimiwa Chikambo, lakini pia nawapongeza wote wanaofuatilia suala hili la korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa rai kwa sisi sote ambao tuko hapa na Watanzania wengine ambao watafanikiwa kuwafahamu wanaohitaji kuwekeza katika viwanda vya korosho; tafadhalini Tanzania ni katika nchi ambayo inatoa korosho bora sana. Hali kadhalika kupitia SIDO tunatengeneza viwanda vidogo vidogo vya kuweza kuendeleza ubanguaji au viwanda vya korosho. (Makofi)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ya viwanda Tanzania ni gharama kubwa za uzalishaji katika viwanda hivi. Serikali ina mpango gani wa kuweka mazingira wezeshi ili kupunguza gharama kama kuboresha miundombinu na kutengeneza mazingira mazuri ya kilimo cha malighafi kama pamba kwa ajili ya uzalishaji wa viwanda hivi? Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira hayo ili wawekezaji hasa kwenye viwanda vya nguo waweze kupata gharama nafuu za uzalishaji zitakazopelekea wao kupata faida?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, viwanda vingi vimekuwa vikikwama kwa sababu ya kukosa mitaji. Je, Wizara ina mkakati gani wa kuzungumza na mabenki ambayo yanatoa mikopo kuweka riba nafuu kwenye viwanda ili waweze kupata pesa kwa ajili ya kufanya biashara? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimeeleza hapo awali, Serikali kwa kutambua changamoto zilizopo ndiyo maana ilikuwa imeitisha kikao na wadau ili kujadili na kuweza kubaini changamoto hizo na hivyo ipo mbioni katika kuzifanyia kazi ikiwemo kuangalia mazingira ambayo yanafanya bidhaa hizo zisiwe na ushindani wa kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mitaji, ni kweli kwamba kuna baadhi ambao wanahitaji kuwekeza lakini suala la mitaji hasa katika uwekezaji binafsi ni jukumu la mwekezaji mwenyewe. Kwa upande wa Serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi wanaweza kulima pamba iliyo bora zaidi, lakini pia wanastahili wapate faida inayostahili kutokana na kilimo chao.
MHE. BONIFACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Wilaya ya Bunda ni moja ya wilaya zinazolima pamba sana kwa Mkoa wa Mara. Ginnery ya Buramba na Ushashi baada ya kilichokuwa Chama cha Ushirika cha Mkoa wa Mara kufa au kufilisika, zilikabidhiwa mufilisi. Ni lini sasa Waziri atafika kuangalia zile ginnery mbili ambazo zimekabidhiwa mufilisi muda mrefu na ziko taarifa kwamba mufilisi ameuza kila kitu na vile viwanda vimetelekezwa? Ni lini Waziri atafika pale kuangalia makabidhiano yaliyokuwepo ya Mara Corp na hali ilivyo kwa sasa kwa ginnery hizo mbili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya kumaliza Bunge. (Kicheko/Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali kwamba wawekezaji binafsi wafanye jitihada wenyewe za ku-access mikopo, naomba kuuliza ni lini Waziri atatembelea viwanda vya Mafinga ambavyo vimeitikia kwa wingi sana katika suala la uchumi wa viwanda ili kuzungumza na wenye viwanda kuhusu changamoto na fursa mbalimbali za mikopo ya riba nafuu inayopatikana kutoka Benki ya Uwekezaji Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kwenda Mara nitaelekea Mufindi. (Kicheko/Makofi)
MHE. MUNIRA M. KHATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kiwanda cha Urafiki hakizalishi kwa kiwango kinachotakiwa na kiwanda hiki kinamilikiwa na Wachina. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kiwanda hiki kinamilikiwa na Serikali ili kuongeza uzalishaji na kupata ajira kwa vijana?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Urafiki kimsingi kinamilikiwa na Wachina na kuna hisa ambazo ni za Serikali. Tumekuwa tukiwasiliana juu ya uboreshaji wa kiwanda hiki na kuhakikisha kwamba tunazalisha kwa kiwango kikubwa zaidi, hata hivyo, bado uzalishaji hauridhishi. Kwa hiyo, Serikali bado inaendelea kulifanyia kazi.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, masharti ya mauzo hayo yaliruhusu ukodishwaji?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kutokana na kwamba malengo ya Serikali ilikuwa ni kuweza kubangua tani 200,000 za korosho na hii ikapelekea kwamba hata Bodi ya Korosho pamoja na mfuko wa kuendeleza zao hili la korosho ulitenga pesa kwa ajili ya kujenga viwanda katika Mkoa wa Pwani, Ruvuma pamoja na Mtwara. Sasa wakati tunasubiria hivyo viwanda viweze kujengwa kwa nini Serikali isifufue viwanda vilivyoko ili kuweza kutimiza hayo malengo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kimsingi Serikali ina taarifa juu ya huo ukodishaji kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi.
Katika swali lake la pili nipende tu kuzidi kumuhakikishia ni kwamba kama amekuwa akifuatilia hata kupitia bajeti yetu, lakini pia ziara mbalimbali tunazofanya, Serikali imeamua kuona kwamba viwanda vyote vilivyobinafsishwa vinafanya kazi yake kama iliyokusudiwa, lakini pia kuhamasisha viwanda vingine viweze kufanya kazi hiyo ikizingatiwa kwamba korosho ni zao kubwa na ni zao ambalo linapendwa duniani na hivyo si vyema tu kusafirisha ikiwa ghafi ni bora kuiongezea thamani ili faida yake iwe ni kubwa zaidi na kuleta tija zaidi katika nchi.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kuwa viwanda ni muhimu sana kwa ustawi wa Taifa letu, lengo la viwanda ni kuleta tija kwa Taifa na wananchi wake kwa ujumla ili waweze kunufaika.
Je, Serikali haioni kuwa sasa hivi ni wakati muafaka wa kwenda kutembelea kiwanda hicho kule Mtama?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa viwanda ni muhimu sana na viwanda hivi vitakapofanya kazi vizuri vitaweza kuwa na tija kubwa katika Taifa letu. Swali lake, je, hatuoni sababu ya kwenda kutembelea huko.
Mheshimiwa Spika, kama utakumbuka kwamba mwezi wa kwanza nilikuwa pia kwenye mzunguko katika Mkoa wa Lindi kufuatilia Kiwanda cha Wanga ambacho kinajengwa katika Jimbo hili la Mtama na kuweza kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zinakabili na hivi sasa hivi wanafanya vizuri. Kwa hiyo, vilevile katika masuala haya ya viwanda vya korosho tutafanya hivyo ili kuona kwamba viwanda hivyo vinaleta tija kwa ajili ya nchi yetu.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kutoka kwenye swali namba 273 la msingi ambalo liliulizwa na Mheshimiwa Lathifah Chande.
Mheshimiwa Spika, tunafahamu kabisa nia ya Serikali ya kutaka kuwa na viwanda kwenye maeneo mengi na kwamba mikoa ya Kusini Mtwara na Lindi kimkakati kabisa miaka ya 1970 tayari tulikuwa na viwanda vingi tu vya korosho Masasi ukienda Lindi, ukienda Nachingwea na maeneo mengi tu.
Sasa swali, mara nyingi tumekuwa tukiwasiliana na Waziri anatueleza kwamba kuna kesi mbalimbali mahakamani ambazo zinasababisha viwanda vile visiendelezwe, lakini wamiliki waliouziwa vile viwanda sasa hivi wanavitumia kama maghala. Wakati Serikali inasubiri hizi kesi ziishe Mahakamani wengine wanapata faida kwenye maeneo hayo hayo.
Sasa swali langu, kwa nini wasiwasimamishe watu wale kutumia viwanda hivi kama maghala kwa sababu wanajipatia pesa na Serikali haipati faida yoyote?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kimsingi nchi yetu inatekeleza shughuli zake kwa mujibu wa sheria lakini vilevile tusingependa kuona sheria zikatumike kama kichaka cha kuwanufaisha watu wachache. Tumeshafanya hivyo katika mashamba ya mpira Kihui ambapo mtu alikuwa na kesi, akasingizia kesi yeye akawa anaendelea kuvuna, tukafanya jitihada ameondoka. Kwa hiyo, hata hayo tutayafuatilia na ushauri wako tutauzingatia.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, asante sana. Kwanza nampa pole ndugu Jaku jana kwa kutolewa nje ya Baraza la Wawakilishi na Naibu Spika.
Mheshimiwa Spika, lini sasa utafanyika utafiti maalum wa uagizaji sukari upande wa Zanzibar ili kulinda Kiwanda cha Mahonda?
Mheshimiwa Spika, lini sasa Zanzibar itajiunga na Mfumo wa Kodi wa TANSIS? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kimsingi Wizara yetu imekuwa ikifanya kazi kwa karibu sana na Mheshimiwa Waziri upande wa Zanzibar, kwa hiyo, katika suala hili la kufanyia utafiti juu ya sukari Zanzibar ni suala muhimu sana ili kuona kwamba kunakuwa na sukari ambayo itawezesha hata kukifanya hata Kiwanda cha Mahonda kifanye kazi yake vizuri zaidi na kuwe na ile bei ambayo ni shindani. (Makofi)
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Tabora na Kanda ambazo tunalima tumbaku kwa miaka zaidi ya 10 tumekuwa tunaomba kiwanda cha tumbaku kijengwe Mkoa wa Tabora na ikithibitika kabisa kwamba asilimia 60 ya tumbaku ya Tanzania inalimwa Mkoa wa Tabora, lakini mwaka jana tu Serikali imeruhusu kiwanda cha pili kujengwa Mkoa wa Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokuwepo kwa kiwanda cha Tumbaku Mkoa wa Tabora kwanza kumewanyima ajira vijana wetu wa Tabora, lakini kubwa zaidi ni kwamba wakulima wa tumbaku wanachajiwa gharama za kusafirisha tumbaku kutoka Tabora kupeleka Morogoro, kwa hiyo wanaongezewa maumivu. Swali la kwanza, kwa kuwa Serikali iliruhusu sasa mwaka jana kiwanda kipya kujengwa Mkoa wa Morogoro ambako hakulimwi tumbaku, iko tayari sasa kushawishi kile kiwanda kimoja kihamishiwe Mkoa wa Tabora ili wakulima wa Tabora nao pia waweze kunufaika na zao lao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwenye jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kawmba uzalishaji umepungua, ni kweli umepungua lakini umepungua kutokana na wakulima hawapewi makisio na kampuni. Wana lengo la kulima, wanakopa hata msimu huu wenyewe tu Kaliua peke yake zaidi ya Vyama vya Msingi sita vimekosa makisio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa zao hili ni zao la uchumi wa Taifa na Mkoa wa Tabora, je, Serikali iko tayari sasa kuhakikisha kwamba Vyama vya Msingi ambavyo vimekosa makisio mwaka huu vinapatiwa makisio? Kwa sababu uchumi wa Tabora unategemea tumbaku na uchumi wa familia unategemea tumbaku? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na dhamira nzuri ya Serikali na wananchi wa Tabora kupenda kujenga Kiwanda cha Kuchakata Tumbaku Tabora lakini pia Muwekezaji huwa anaangalia mazingira ya yanayoweza kumuwezesha kupata faida zaidi na kufanya shughuli zake vizuri zaidi. Kwa hiyo kama tulivyosema awali tutaendelea kuhamasisha lakini pia kuwakatisha tamaa wale ambao wameamua kuwekeza Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu kutoa makisio; kwa kweli kama kuna zao ambalo linapambana na changamoto ni pamoja na hili la tumbaku. Fikiria mteja anaanza kwanza kuhamasishwa “uvutaji wa sigara ni hatari kwa maisha yako” lakini pia uweze kufanya biashara. Kwa hiyo kwa misingi hii unakuta hata kampuni wakati mwingine zinashindwa kufikia malengo kutokana na mazingira kama hayo. Hata hivyo, nizidi kuwaomba wananchi wa Tabora, wote kwa pamoja tutaendelea kufuatilia na kuona kwamba hali ya bei yanzuri kwa upande wa wakulima inapatikana. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Serikali ya Awamu ya Tano imejinasibu kwamba ni Serikali ya viwanda na tunataka kuhakikisha tutakapofikia mwaka 2025 tuwe kwenye nchi ya kipato cha kati. Sasa nataka kufahamu kutoka kwa Waziri; tulipofanya vikao vya Kamati alikuwa anatueleza kwamba maghala ya korosho yaliyopo Masasi yamegeuzwa, tunafahamu, kufanywa maghala badala ya viwanda na kwamba kuna kesi zilizoko mahakamani kwa sababu ya kutanzua migogoro iliyoko pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba, mpaka sasa hivi wamefikia hatua gani ya kesi hizi zilizoko mahakamani ili kuhakikisha viwanda vile vinafufuliwa badala ya kuendelea kutumika kama maghala na wale watu waliovinunua wakati huo? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza katika majibu yangu ya hapo awali niliahidi kutembelea eneo hilo, nasikitika kuliarifu Bunge kwamba sikuweza kutembelea. Hata hivyo, kama ambavyo nimekuwa nikizungumza siku zote, Wizara kwa kushirikiana pia na Kamati yetu ya Viwanda, Biashara na Mazingira tupo katika kuendelea kuhakikisha kuona kwamba wawekezaji wanatimiza wajibu wao, lakini pia kuhakikisha maeneo yote ambayo yanalima korosho basi korosho hiyo iweze kubanguliwa au kuongezwa thamani kabla ya kusafirishwa. Kwa hiyo tupo katika mchakato na mchakato wa kisheria kawaida huwa hatuuingilii.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa tumbaku nyingi inayolimwa Mkoa wa Tabora inatoka Wilaya ya Urambo, Kaliua, Uyui na kwingineko. Je, Serikali iko tayari kuja kuona eneo ambalo lilishatengwa kwa ajili ya kiwanda Wilayani Urambo? Kwa kuwa wakulima wanapoteza kilo nyingi sana kusafirisha tumbaku kutoka Tabora kupeleka Morogoro.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tutakapopata nafasi tutaweza kuja kuona na kushauri kadri itakavyowezekana japo kama ambavyo hapo awali nimeeleza changamoto zinazojitokeza.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni muunganiko wa nchi mbili na unapotaja viwanda vya Tanzania huwezi kuvitenga viwanda vilivyoko Zanzibar. Nataka kujua ni sababu ipi ya msingi inayoifanya Kiwanda cha Sukari cha Mahonda – Zanzibar kisiruhusiwe kuingiza sukari yake katika soko la Tanzania Bara, sababu ya msingi hasa ni ipi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili swali limekuwa likijirudia mara kwa mara, lakini niseme tu kwamba pamoja na kwamba Tanzania ni moja, suala la ulinzi wa viwanda lipo kila mahali na kama ulivyoona hata Tanzania Bara imerundikana sukari ya kutosha. Kwa hiyo, pengine badala ya kutaka nyingine iingie tushughulikie kwanza hii hali mbaya ya kuingiza sukari ya magendo inayoendelea.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Nashukuru kwa majibu ya Wizara kwa maswali yote yaliyopita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapata miaka kadhaa sasa bidhaa hii ya sukari nchini inapanda bei kila inapofika mwezi wa tatu na inampa wakati mgumu mlaji katika gharama kulingana na hali ya uchumi ya Mtanzania wa chini.
Je, ni kwa nini Serikali isitazame namna ya kuzalisha sukari hii ikamudu katika ule muda wa sukari kupanda kila mwaka kuanzia mwezi wa tatu ili kila Mtanzania kwa wakati mmoja aweze kupata bidhaa hii kwa bei nafuu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba wawekezaji au wazalishaji wa sukari ni wafanyabiashara binafsi na Serikali imekuwa haiwaingilii sana katika upangaji wa bei, lakini tunawaomba fursa hii wanayoipata ya kulindwa wasiitumie vibaya. Tumefanya hivyo kwa viwnada vya saruji, tumeelewana vizuri na ninatoa rai kwao iwe ni mwiko kupandisha sukari kiholela.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya uchumi ya nchi yoyote inatakiwa kuwa na mahusiano ya moja kwa moja na sekta wezeshi kama sekta ya elimu ili kuweza kuleta matokeo chanya. Sasa Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kubadilisha mitaala yetu ya elimu ili kuweza kuendana na sera ya uchumi wa viwanda?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Khadija kwa kufungamanisha sera hii ya uchumi na namna ya kuwezeshwa kupitia elimu; na ndiyo maana hata kwenye majibu ya msingi tunazungumza hayo. Ni kwamba tunapozungumzia kufanya uwezeshi katika ujenzi wa uchumi ni lazima huyu mtu awe ameandaliwa kielimu lakini vile vile kimafunzo ya ujuzi.
Kwa misingi hiyo sera zetu zote sasa hivi zimekuwa zikifanya kazi kwa pamoja kuangalia maeneo gani yanaweza yakaongezewa nguvu na pia kuangalia kwamba sera zetu zinazungumza na kuweza kuleta matokeo chanya. Kwa hiyo, kupitia Wizara ya elimu vilevile kuna mafunzo ambayo yamekuwa yakitolewa katika vyuo vyetu vikuu, lakini vilevile katika vyuo vya ufundi ili kuwezesha kuona kwamba hawa wahitimu wanatekeleza majukumu yao vizuri katika ujenzi wa uchumi.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya nchi yetu ya Tanzania imekuwa kama ni laana kwa mwanafunzi kufeli darasa la saba au form four, lakini India, mainjinia leo wanaoendesha mitambo ya gas and petroleum ni wale waliofeli darasa la saba.
Je, Serikali yetu lini itaona umuhimu wa kuwaendeleza vijana waliofeli darasa la saba na form four ili na wao waje kuwa mainjinia katika viwanda vyetu na mitambo yetu Nchini?

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi Serikali na nchi kwa ujumla inathamini kila rasilimali ya mwananchi iliyopo nchini na ndiyo maana kupitia vyuo vyetu vya VETA, kupitia FDC, kupitia mafunzo yasiyo rasmi imekuwa ikiendelea kutoa mafunzo ili kuhakikisha kwamba vijana hao wanaendelea kuajirika na kujiajiri wao wenyewe.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkazo uliwekwa vizuri sana katika elimu ya msingi na elimu ya sekondari tulipojenga shule nyingi sana za kata. Mkazo pia umewekwa kwa elimu ya juu kwa maana ya vyuo vikuu. Hata hivyo vijana wengi sana baada ya kumaliza form four na form six wana-hang hapa katikati hawana pa kwenda na viwandani wanahitajika sana…
… kama mafundi mchundo na kadhalika. Sasa, je, Serikali ina mkakati gani na vijana hawa kuwapa elimu ambayo baadae itawasaidia kuwa mafundi mchundo na kazi nyingine za viwandani badala ile elimu ya chuo kikuu ambayo inatengeneza mameneja zaidi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba katika ngazi za kati hatuna mafundi wa kutosha kama ambavyo ameeleza Mheshimiwa Selasini, lakini niseme tu kwamba jitihada zimeendelea na kama tutakumbuka mara ya mwisho kupitia Bunge lako tukufu tuliweza hata kupitisha uwezekano wa makundi hayo kupewa mkopo ili kuweza kuziba hayo mapengo. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kufanyiakazi ili kuweza kuona kwamba maeneo hayo yanaimarishwa na vijana wengi zaidi wanapatikana kutoka katika makundi hayo.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji wa soko ni kitu muhimu sana hasa ukizingatia eneo hili vijiji vinavyozunguka Miganga, Mwanga na Nkalakala vinalima sana vitunguu na kilimo ni uti wa mgongo, na tunakwenda kwenye uchumi wa kati na uchumi huo lazima uwe supported (to be supported) na kilimo. Je, Serikali lini itatoa uwekezaji wa kutosha kuweza kujenga soko kubwa na la kisasa maana hapa tumeanza tu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; upangaji wa madaraja na ufungashaji wa vitunguu unakwenda sambamba na utangazaji wa bidhaa hiyo ambayo ni vitunguu. Serikali inachukua hatua gani kutangaza bidhaa hii ambayo tunatambua kwamba inakwenda katika nchi jirani za Kenya, Mauritius na Sudan Kusini. Ni lini Serikali itachukua hatua za kutangaza bidhaa hii?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Allan Kiula ambavyo tumekuwa tukishrikiana katika suala hili. Niseme tu kwamba naishauri Halmashauri wakati wa bajeti itakapokuja tutenge fedha za kutosha na sisi kwa upande wetu Wizara tutaangalia kila uwezekano unapojitikeza kuweza kusaidia soko hili liweze kupata fedha za kutosha na kulifikisha katika kiwango cha kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuhusu kutangaza vitunguu vya maeneo hayo, niseme tu kwamba ni kweli vitunguu vinavyotoka kwa ujumla wake katika Mkoa wa Singida ni vizuri sana. Niwaombe Watanzania wote kutumia vitunguu hivyo, lakini pia tutaendelea kutangaza kimataifa na wakati wa shughuli za Sabasaba zinapojitokeza waje pia katika maonesho ili kutangaza vitunguu hivyo.
MHE. MGENI JADI KADIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa swali la nyongeza.
Kwa kuwa viwanda vingi vimejengwa Nchini ili kuleta uchumi wa viwanda lakini viwanda vingi havifanyikazi kwa ukosefu wa malighafi.
Je, ni viwanda vingapi vilivyojengwa vya kuchakata ili kuondoa tatizo hili na kuipa Serikali mzigo kuagizia malighafi kutoka nje?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kimsingi ni swali la kitakwimu, lakini vilevile niseme tu kwamba kwa hali ya sasa, katika usindikaji wa mazao wananchi wenyewe wamekuwa msitari wa mbele katika kujifunza na kisindika mazao na kwa kutumia taasisi zetu kama SIDO wamekuwa wakipewa mafunzo ili kusindika mazao hayo.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Vijana na wanawake wengi wa Kitanzania wamekuwa na jitihada kubwa sana katika kilimo hususani cha mbogamboga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali imefanya jitihada zipi za kuhakikisha kwamba bidhaa za shamba zinasindikwa nchini?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi kama ambavyo nimezungumza hapo awali, kwa kupitia miradi ambayo SIDO imekuwa ikiendeleza pamoja na wadau mbalimbali, kwa kweli usindikaji wa mazao sasa hivi umekuwa ni mzuri zaidi. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, inapotokea katika maonesho ya saba saba tafadhalini hebu mpitie muone bidhaa ambazo sasa hivi hawa Watanzania wanazifanya. Ziko katika viwango vya hali ya juu na tutaendelea kuwezesha kuona kwamba wajasiriamali hao wanapata ubora zaidi katika bidhaa zao.
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Waziri ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza kwa kuwa wapo watoto ambao wanamaliza elimu ya msingi hawajui kuandika wala kusoma. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba kila mtoto wa Tanzania anapomaliza elimu ya msingi ambayo ni darasa la saba anajua kusoma na kuandika?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa kuwa wapo watu wazima wenye umri na wazee labda umri kama wangu pia hawajui kusoma kutokana na mazingira labda waliyokuwa labda maeneo yao yalikuwa hayana shule. Je, Serikali ina mpango gani wa kurudisha elimu ya watu wazima iliyokuwepo hapo zamani miaka 1973 ili watu hawa waweze kusoma na kuandika?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI (K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbogo kwa maswali yake mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nisisitize tu kwamba Serikali imeendelea kutoa hamasa na kuwafuatilia walimu, lakini vilevile kuhakikisha kuwa watoto waweze kusoma na kuandika pale wanapokuwa hasa elimu ya msingi na hivyo kwa sasa mtoto inapofikia darasa la tatu ikigundulika hajui kusoma na kuandika imekuwa akipewa mpango maalum wa kumsaidia na kumuwezesha kuweza kumudu masomo yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa elimu ya watu wazima nikubaliane naye kwamba kweli Tanzania bado tunalo kundi kubwa takribani 20% ambao hawajui kusoma na kuandika. Kuna programu mbalimbali ambazo zimekuwa zikiendelea kupitia elimu ya watu wazima ambapo wanapewa baadhi ya mafunzo ya kujitegemea, lakini vilevile nipende kusisitiza kwamba kila Mtanzania ambaye hajui kusoma na kuandika awe na kiu ya kuweza kujifunza kusoma na kuandika kwa sababu sasa elimu imeshakuwa karibu kila mahali hasa katika maeneo yetu tunayoishi.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, hata hivyo nina maswali mawili madogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa kilimo cha bustani kinamtoa mkulima na hasa akinamama na vijana kwenye umaskini kwa uharaka na kupata ajira, lakini licha ya kuwaunganisha na pamoja na TAHA na SAGCOT kuwasaidia wakulima hawa, tatizo kubwa wanalolipata ni mitaji. Je, kuna mkakati gani wa kuwasaidia kupata mikopo nafuu ili akinamama hawa na vijana wanaoshughulika na kilimo cha bustani waweze kupata mikopo hiyo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, licha ya kuwaunganisha na kuanzisha viwanda kwenye mikoa mbalimbali, Mkoa wa Morogoro ni Mkoa unaolima sana mbogamboga na matunda. Je, kuna mkakati gani wa kuweka wawekezaji katika Mkoa wa Morogoro kuanzisha kiwanda cha matunda na mbogamboga? (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tatizo la mitaji limekuwa ni moja ya changamoto zinazowafanya wakulima hao hasa ambao wanajihusisha na shughuli za mbogamboga na bustani washindwe kufanya vizuri zaidi. Hata hivyo, kwa kuwa halmashauri zetu zinayo asilimia 10 ambayo inawasaidia akinamama, vijana na watu wenye ulemavu katika kupata mitaji, ni vema Halmashauri basi zielekeze nguvu katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kupitia Mfuko wetu wa NEDF ambao uko katika Shirika la SIDO, tutahakikisha kwamba hawa wananchi wanafikiriwa zaidi katika kuhakikisha kwamba wanapata mikopo ya aina hiyo pamoja na taasisi nyingine za kifedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili kuhusu kuhamasisha viwanda, Wizara imekuwa ikiendelea kuhamasisha viwanda mbalimbali viweze kuwekeza katika nchi yetu na Mkoa wa Morogoro ambao umeonesha kuwa na fursa kubwa za mbogamboga na matunda. Vilevile, sasa hivi nchi ipo katika majadiliano ya mkataba ambao utawezesha kuwa na soko huru la Afrika litakayowezesha mitaji ya aina mbalimbali kuweza kuingia katika nchi ikiwepo na Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo tunaamini kwamba, wawekezaji wengi watakuwa na ari ya kuja hasa baada ya kuona kwamba sasa fursa hizo zinafunguliwa na baadhi ya kodi zisizo za lazima au vikwazo vinapunguzwa ili waweze kuwekeza zaidi. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, katika maeneo ya Mkoa wa Dar es Salaam na hasa katika Bonde la Mzinga Mbagala, maeneo ya Chanika, Msongola, Kitunda, Mwanagati, Boko, Kibamba, Bunju, Yombo, Kimbiji, Pembamnazi, na Kisarawe II; akinamama na vijana wa maeneo haya wanashughulika sana na biashara ya mbogamboga na matunda. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia akinamama wajasiriamali wa Mkoa wa Dar es Salaam waweze kupeleka bidhaa zao za mboga na matunda nje ya nchi ukizingatia tuna fursa kubwa ya uwanja wa ndege mpya mkubwa wa Kimataifa katika Mkoa wa Dar es Salaam.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kutoa mafunzo ya namna bora ya kusindika matunda hayo kwa kupitia SIDO vilevile kuona kwamba hata uuzaji wa mboga hizo unakaa katika viwango na tija. Jambo ambalo linahuzunisha kidogo ni kwamba katika Halmashauri zetu au Serikali za Vijiji tumekuwa hatutengi maeneo mazuri mahsusi kwa ajili ya hawa wakulima ili sasa hizo bidhaa zao za mashambani ziweze kukaa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwamba, mkulima aweze kusaidiwa kuanzia shambani mpaka sokoni na pia kupewa mafunzo ya aina hiyo na hivyo kuweza kufanikisha hata inapokuja fursa ya kuweza kuuza nje ya nchi.
MHE. ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ukitoka Dodoma hapa kama unaelekea Dar es Salaam, ukianza Wilaya ya Gairo kabla ya kufika Jimbo Mvomero, hapa katika maeneo ya Magole wapi kila sehemu unakuta vijana wamebeba nyanya, karoti, na kadhalika huko Morogoro na ukifika pale kituo cha mizani. Ni mkakati gani Serikali wanafanya maalum kwa ajili ya Morogoro kuwasaidia hawa vijana wadogo wadogo ili kukuza uchumi wao, kwa sababu wanashinda barabarani, mwisho watagongwa na magari. Naomba Serikali iseme ni mkakati gani kuhusu Morogoro mnawasaidia hawa vijana wanaoshinda barabarani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi kama ambavyo nimesema hapo awali, jukumu letu ni kuhamasisha kwanza kuwatambua hawa wafanyabiashara wadogowadogo sana yaani (Micro Entrepreneurs). Ninalosisitaza ni kwamba mara nyingi hata tunapozungumzia maeneo ya uwekezaji au katika shughuli za kuwezesha tumekuwa tunawaangalia zaidi hawa wakubwa kuliko hawa wadogowadogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kwa sasa imeshajipanga kuona kwamba hawa wajasiriamali wadogo wadogo wawe wa matunda, wawe wa biashara nyingine, wanasaidiwa ili kuweza kupata maeneo ambayo yatawawezesha kufanya shughuli zao vizuri na tunasema kwamba uchumi uanzie shambani hadi sokoni na maeneo mengine kama viwandani.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika msimu wa kilimo wa mwaka jana na hata mwaka juzi, mazao ya mbaazi na kilimo yalipata anguko kubwa kwenye masoko. Hivi sasa msimu wa mavuno wa mazao hayo umeanza katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Je, Serikali ina habari yoyote njema kwa wakulima kuhusu masoko ya mazao ya mbaazi na mahindi? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo mara ya mwisho nilijibu suala la soko la mbaazi, kwanza tumekuwa tukitegemea sana soko hilo kutoka nchi za nje hasa India lakini nao wakawa wamelima kiasi kwamba hawakuweza kununua mbaazi kutoka kwetu. Kupitia TanTrade tumewaagiza kuendelea kufuatilia masoko kwa ajili ya mbaazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huu kwa kutambua umuhimu wa zao hili la mbaazi na umuhimu wake katika afya naendelea kusisitiza kwamba Watanzania tupende pia kutumia mbaazi kwa sababu ni chakula bora na kina lishe nzuri. (Makofi)
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Vijana wote nchini wameamka na kuungana na Serikali yao katika kutekeleza kwa vitendo Sera ya Uchumi wa Viwanda, japokuwa katika majibu ya Serikali, Serikali imeshindwa ku-acknowledge jitihada za vijana katika kukuza uchumi wa nchi. Sasa Serikali ni lini itatambua na kuthamini jitihada za vijana katika kukuza uchumi wa nchi? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, naomba tu tufahamu kwamba, suala la kuwezesha vijana kiuchumi ni suala mtambuka. Sekta zote inabidi tushirikiane kwa pamoja ikiwemo Waheshimiwa Wabunge. Wizara kama ambavyo nimesema awali tumeshajipanga kuhakikisha kwamba tunakuwa na mkakati maalum wa kuwezesha makundi hayo ya kibiashara kuanzia katika maeneo yao ya kufanyia biashara na tunazidi kuhamasisha Halmashauri zetu, kwa mfano zitenge maeneo ambayo vijana wanaweza kufanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, si jambo jema kuwaona vijana wakiwa wanazunguka zunguka tu mitaani, halafu yanajengwa majengo makubwa yanaachwa vijana hawaingii humo kufanyia kazi. Kwa misingi hiyo, tumejipanga na tunataka kuona kwamba vijana wanasaidiwa ili iwe ni rahisi kuwatambua na vilevile kuweza kupata huduma zote za msingi zinazohusiana na uwezeshaji. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri na Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuwatambua vijana na kuwasaidia ili waweze kuingia kwenye sekta ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kulithibitishia Bunge lako Tukufu kwamba, Serikali imekuwa ikiwasaidia sana vijana na kuwawezesha katika sekta mbalimbali. Wizara ya Habari ya Michezo na Utamaduni wameshafanya kazi kubwa sana katika kutambua vipaji vya vijana na kuwajengea uwezo. Ofisi ya Waziri Mkuu tumeshasema tumetambua vijana waliokwishafanya vizuri kwa mfano, wale vijana wa kutoka Chuo cha SUA, wamefanya vizuri sana kwenye sekta ya kilimo, sasa tunawatumia hao kuendesha mafunzo ya kilimo cha kitalu nyumba katika nchi nzima ya Tanzania, huko ni kutambua juhudi zao na kuwawezesha zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaendelea kutoa mafunzo yenye ujuzi wa namna mbalimbali ili vijana wajiajiri na waajiriwe katika maeneo mbalimbali ya sekta za viwanda na sekta za biashara. Serikali inatambua sana na tutaendelea kutambua juhudi hizo kila siku na kuwawezesha vijana wa Tanzania. (Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa. Moja ya jukumu kubwa walilopewa Benki ya Maendeleo ya Kilimo ni pamoja na kuhakikisha usalama wa chakula lakini kubwa zaidi ni kuchangamkia fursa za upatikanaji wa masoko ya bidhaa za kilimo nje ya nchi. Nataka kujua benki hii imeshafanya juhudi hizo kwa kiasi gani?
NAIBU WAZIRI, VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani anaendelea kumuunga mkono Mheshimiwa Rais katika hotuba yake ya hivi karibuni siku anazindua mradi wa ASDP kwamba benki hii imefanya kazi lakini ifanye kazi zaidi. Kwa sasa tunachosema ni kwamba isaidie zaidi katika suala la kuhakikisha kwamba pembejeo na nyenzo za kilimo zinawafikia wakulima wengi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo Wizara yetu tayari katika tractors ambazo tayari tumeshaziunganisha zaidi ya 148, Benki ya Kilimo (TAB) tayari tupo nao pamoja katika kuhakikisha kwamba tunawawezesha wakulima na wale ambao watahitaji kukopa trekta hizo. Kwa hiyo, niseme tu kwamba Mheshimiwa Mbunge ameunga mkono kwa kuuliza swali lakini tunataka Benki hiyo ifanye zaidi na zaidi.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini pamoja na majibu hayo naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, nilitaka nijue Serikali imejipanga vipi au imejiandaa vipi? Kwa sababu wakati Kiwanda hiki cha Mafuta Ilulu kinabinafsishwa, kilikuwa na majengo pamoja na mitambo yake, lakini ukaguzi nilioufanya kwa awamu ya mwisho mpaka sasa hivi huyu mwekezaji anatangaza kukirudisha, kiwanda kile hakina mashine hata moja na amesema kwamba anakirudisha. Nini kauli ya Serikali juu ya mashine ambazo zilifungwa katika Kiwanda kile cha Mafuta cha Ilulu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, nilikuwa nataka nijue; kwa sababu Serikali imetoa hisa asilimia 100 kwa wawekezaji kwa ajili ya Kiwanda cha Korosho, ambapo wawekezaji waliopewa ni Sunshine na mashine walizozifunga pale hazioneshi kama zinaweza zikafanya kazi ambayo tunaikusudia. Kwa nini Serikali isichukue angalau asilimia 51 ya hisa zile ili Serikali iweze kupata gawio lake la moja kwa moja badala ya kutegemea mwekezaji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa upande wa Kiwanda cha Mafuta cha Ilulu ambacho anadai kwamba mashine zake zimeshaondolewa na kiko katika hali mbaya na kinarejeshwa, ndiyo maana tumesema kwamba tutakipokea kufuatana na taratibu za kisheria. Kwa hiyo, tutaangalia masuala yote ya kisheria pale tutakapoona kwamba mwekezaji huyu anabanwa na masharti hayo, basi hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kiwanda cha korosho, niseme tu kwamba Serikali ilikuwa imeshajitoa katika kufanya shughuli za uwekezaji na hiyo ndiyo sera yetu. Tunachofanya zaidi ni kuwahamasisha wawekezaji, wao ndio wawekeze na mitaji mingi zaidi iweze kufika na kuwekeza katika nchi. Ila tu katika maeneo yale ambayo tunaamini kwamba pengine kwa mwekezaji binafsi ataona hakuna tija, lakini wakati huo kwa upande wa Serikali tunaona kwamba suala hilo lina manufaa makubwa kwa Watanzania au jamii kwa ujumla, ndipo Serikali inapoingilia na kuweza kuona umuhimu wa kuwekeza.
MHE. AIDA J. KHENAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kulikuwa na kiwanda kinachozalisha zana za kilimo kwenye Mkoa wa Mbeya mpaka sasa hatujui nini kinaendelea. Tunaomba kujua kwenye Wizara ya Kilimo nini mkakati wa Wizara kuweza kufufua kiwanda hicho ili kuendeleza zana za kilimo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya mwisho nilitembelea Kiwanda hiki cha Zana za Kilimo pale Mbeya, ni kweli bado kinaendelea kutengeneza zana za kilimo, lakini pia kimejikita kuanza kutengeneza nguzo za cement za umeme. Kwa hiyo, kimsingi mwekezaji bado anaendelea na kazi na tunazidi kumshauri aendelee kuongeza jitihada.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru namshukuru pia Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake. Nina maswali mawili ya nyongeza. Taarifa ya Mkaguzi Mkuu inaeleza kwamba kati ya lita 92,000 ya dawa hizo zilizosambazwa kwenye mikoa 26 ya Tanzania Bara ni lita 25,000 tu ndiyo ambazo zimeweza kutumika mpaka sasa. Ukizingatia dawa hizi zina life span, inawezekana kama hazijaharibika, sasa zinakaribia kuharibika. Serikali inatoa maelezo gani juu ya upungufu huo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa kuwa dawa hizi zilisambazwa kwa mkopo wenye thamani ya shilingi bilioni 3.1 na makubaliano yalikuwa kwamba Halmashauri husika ziweze kulipa fedha hizi, Serikali ina
mkakati gani kusimamia fedha hizi ili ziweze kulipwa? Ahsante?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni kwamba kimsingi dawa hizi ni muhimu sana na zinaua hasa katika maeneo yale ya mazalia. Sasa kama kuna Halmashauri zimechukua dawa hizo na zikaacha kupeleka kwenye maeneo hayo ya mazalia ya mbu kwa kweli wanatenda kosa kubwa kwa sababu wanawanyima wananchi haki yao ya kupona kutokana na kutokomeza viluwiluwi vya Malaria. Nawaomba wafanye hivyo mapema iwezekanavyo na wajue kwamba kufanya hivyo ni kurudisha nyuma jitihada za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuhusiana na madeni, ni kweli kabisa Halmashauri nyingi hazijaweza kulipa madeni waliyochukua dawa hizo. Kwa hiyo, nizitake pia Halmashauri kuhakikisha kwamba wanalipa madeni yao na kuyapa kipaumbele iwezekanavyo kuhakikisha kwamba wanalipa ili kutelekeza azma ya Serikali ya kukifanya kiwanda hicho kuwa endelevu.
MHE. OSCAR R. MUKASA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nina swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa Biharamulo kijiografia inafursa ya kufanya biashara na nchi na Congo, Rwanda na Burundi na inafanya hivyo lakini kwa namna ambayo haina tija ya kutosha na kwa kuwa Halmashauri ya Biharamulo imetenga eneo la hekari 61 kwa ajili ya kuanzisha eneo la Agro Processing Zone.

Je, Wizara iko tayari kuja kuzungumza nasi wakisindikizana na TAN-TRADE kwa ajili ya kuchukua hizo fursa za nchi ambazo zimetuzunguka?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kwanza tunamshukuru na kumpongeza sana kwa jitihada kubwa anazofanya za kusaidia Wizara yetu kuhakikisha kwamba anasaidia kuonesha fursa zilizopo nimuhakikishie kwamba ningependa sana kuambatana naye na kuweza kufanya hivyo.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwanza nipende kupongeza majibu mazuri ya Mheshimiwa Stella Manyanya, Naibu Waziri wa Viwanda, lakini kipekee sana kupongeza Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo kwa namna ambavyo wanatekeleza muongozo wa kuanzisha viwanda katika ngazi ya Serikali ya Mtaa na kwa maeneo zaidi ya matatu ambayo wameyatenga katika eneo la Usahunga pamoja na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, lakini niendelee kutoa rai kwa halmashauri zingine kuhakikisha kwamba wanaweka kipaumbele katika kutenga maeneo ya uwekezaji lakini zaidi kuhakikisha kwamba wanaweka miundombinu muhimu ili kuweza kuvutia wawekezaji wengi zaidi na niwahakikishie kwamba tutaendelea kuvutia wawekezaji ikiwemo Biharamulo na sehemu zingine muhimu tu tuendelee kupeana ushirikiano. Nashukuru sana.
MHE. AJALI R. AKBAR: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna taarifa kwamba kiwanda hiki anataka kutarajia kuchakata yeye mwenyewe, mchakato wa muhogo pale Lindi. Je sisi ambao tunalima muhogo sana katika Wilaya ya Newala na Mtwara kwa ujumla, huu muhogo wetu tutauza wapi na jitihada gani Serikali imefanya kututafutia soko lingine nje kwa kuwa hili yeye mwenyewe anasema kwamba already hilo soko linamtosha kwa ajili ya kiwanda tu?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa kuanzia kiwanda hiki kimepata mashamba katika maeneo ya Nankauka (a) na (b) na maeneo mengine ili kuweza kuzalisha muhogo kwa kiwango ambacho kinatakiwa. Pia kwa kufuata taratibu zinazotakiwa, lakini katika majadiliano tuliyofanya ni pamoja na kuwawezesha wakulima wanaozunguka maeneo hayo, nao waweze kuuza muhogo wao katika eneo hilo na vilevile waweze kufaidika kwa sababu kiwanda hiki kitauza, unga lakini vilevile kitauza wanga.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kama ilivyo kwa wananchi wa Newala, Wilaya ya Kyela ina zao la kokoa. Je, ni lini Serikali itatusaidia kupata wafanyabiashara wengi zaidi kuweza kusaidia kununua zao la kokoa kwa wananchi wa Wilaya ya Kyela? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kama ilivyo kwa mazao mengine, Wizara yetu inalo jukumu kupia TANTRADE, kuhakikisha kwamba tunashirikiana na Wizara ya Kilimo kutafuta masoko ya uhakika na wawekezaji ili kuweza kuendeleza mazao yote. Kwa hiyo zao la kokoa ni mojawapo ya mazao ya kimkakati na linapendwa duniani na hivyo nalo ni sehemu mojawapo ambayo linashughulikiwa.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami naomba kuuliza swali la nyongeza. Ni kwa kiasi gani Serikali imefikisha taarifa ya uwepo wa soko la muhogo huko China katika mikoa yetu, kwa sababu katika RCC iliyopo Mkoa wetu wa Mtwara ajenda ambayo ilikosa majibu ya uhakika ni ajenda hii. Je hizo taarifa walizonazo za uhakika wa masoko wamezifikisha mikoani?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kimsingi kama nilivyosema kwamba kwanza kuliundwa Kamati ya Wataalam kwa ajili ya kutathmini changamoto mbalimbali juu ya zao hilo. Vilevile TANTRADE iliwaita wadau ambao nilikaa nao katika mkutano na kuwaelimisha juu ya upatikanaji wa masoko hayo. Kwa misingi hiyo kwa sababu Mheshimiwa Hawa Ghasia amezungumzia katika eneo maalum la Mtwara; nimwahidi tu kwamba, watumia fursa hiyo kwenda kuelimishwa ili waweze kushiriki kikamilifu.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Naibu Waziri wa Viwanda kwa majibu mazuri aliyoyatoa kwa niaba ya Serikali. Katika nyongeza ya swali hilo kwamba, ni kweli kama Serikali tarehe 1 mwezi huu tumekaa na mnunuzi mkubwa wa mhogo kampuni ya Epoch Tanzania Limited ambaye tumeshampa kibali kama uthibitisho ili kwenda kukionesha kwenye Serikali ya China. Tumefanya hivyo, kwa sababu mnunuzi yoyote anatakiwa kwanza athibitishwe na Serikali wazalishaji wa zao hilo na tumempa jana na hiyo taarifa imeshafika Ubalozi wa China maana Serikali ya China kuthibitisha hilo. Kwa hiyo, baada ya mkataba huo sasa tunakuja maana yake tumepata soko la uhakika na linalotambulika kisheria. Kwa hiyo mwaka huu 2019 tutakuja kuwatangazia rasmi ni lini sasa tutaanza usafirishaji.

Mheshimiwa Spika, sambamba na kampuni hiyo ya Epoch Limited, kuna kampuni zingine tatu tumeshawapa
vibali, zote zimeshapata idhini ya kuuza mhogo katika soko la China, kwamba siyo kazi rahisi kwa utaratibu waliojiwekea wenzetu China, kwamba mtu yeyote tu ukiwa na mhogo sehemu unauingiza, hapana ni lazima upate uthibitisho kwenye Serikali ya uzalishaji ili kupata uhalali kama mzigo huo ni salama kwa matumizi ya nchi yao.
MHE. USSI S. PONDEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza ningependa Hansard isomeke vizuri, mimi sio Mbunge wa Chumbageni, ni Mbunge wa Chumbuni, Zanzibar, Chumbageni ipo Tanga, kwa hiyo ningependa hansard isomeke vizuri.

Mheshimiwa Mwneyekiti, nina maswali mawili ya nyongeza ambayo ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri. Kwanza angetupatia tafsiri ya viwanda, katika majibu yake mazuri ametuambia kuna viwanda vidogo na viwanda vidogo sana; kwa hiyo tungependa tupate tafsiri nini tofauti ya viwanda vidogo na viwanda vidogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ningependa kumuuliza, kwa kuwa Wizara yake haihusiki na uwekezaji wa viwanda katika Serikali ya Zanzibar; hadi sasa wawekezaji wakitaka kuwekeza Zanzibar wanatakiwa wachukue leseni zitoke BRELA. Je, Serikali haioni sasa umefika wakati wa kuiachia Wizara ya Viwanda ya Serikali ya Zanzibar kuweza kusimamia kazi hii ya utoaji wa leseni?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimuombe radhi kwa kukosea Jimbo lake na nashukuru amesahihisha. Pili, napenda kusema kwamba viwanda vidogo sana ni vile ambavyo mtaji wake hauzidi milioni tano na wafanyakazi wake hawazidi wane. Viwanda ni vidogo vile ambavyo mtaji wake ni ule ambao hauzidi milioni 200 na wafanyakazi wake hawazidi 49.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa suala la leseni; suala hilo umelizungumza lakini kimsingi ni kwamba Wizara ya Viwanda na Biashara inashirikiana kwa karibu sana na Wizara ya Viwanda Zanzibar kiasi kwamba shughuli nyingi tunafanya pamoja. Hata hivyo maboresho yoyote yanayolenga kurekebisha na kuleta urahisi wa kuwekeza yatafanyiwa kazi ili kuwawezesha wananchi wetu na wadau mbalimbali wanaopenda kuwekeza wafanye shughuli zao bila shida na kwa uharaka iwezekanavyo.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Sera ya Viwanda Tanzania imetamalaki. Sasa nipende kumuuliza Mheshimiwa Waziri Kiwanda cha Kufua Chuma pale Liganga kitaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ngalawa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi chuma cha Liganga kinahitaji uwekezaji mkubwa sana na pale tunazungumzia kuwekeza katika suala la ufuaji wa chuma, ambacho kimechanganyika na madini ya aina nyingine ikiwemo Titanium, Vanadium na Aluminium; wakati huo huo kuna suala la kufua umeme. Hayo yote yanafanyiwa kazi na ikizingatiwa kwamba hivi karibuni tulipitisha sheria zetu ya kutunza rasilimali zetu na kuwawezesha Watanzania kunufaika zaidi, hayo yote yanaangaliwa kwa umakini na tutakapo kuwa tayari, shughuli hiyo itaanza mara moja.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuongeza swali la nyongeza. Kwa kuwa miongoni mwa viwanda ambavyo vimebinafsishwa na Serikali, ni Kiwanda cha Nguo cha Urafiki. Katika Kiwanda cha Nguo cha Urafiki mwekezaji hakuja na mtaji, badala yake Serikali ndiyo ilikwenda kukopa katika Benki ya Exim ya China na ikampa mwekezaji mtaji wa kuendesha Kiwanda cha Urafiki. Je, ni lini Serikali itakirejesha Kiwanda cha Urafiki mikononi mwa wananchi wa Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kubenea kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo umezungumza, Kiwanda cha Urafiki kinatokana na urafiki kati ya nchi ya China na Tanzania. Ni Kiwanda ambacho msingi wake ulijengwa katika mahusiano hayo ya nchi mbili ya Kidiplomasia. Kwa hiyo, tunatamani kuona kiwanda hicho kikifanya kazi vizuri zaidi na wote tumekifuatilia na kujua kwamba kuna maeneo yanayohitajika kufanyiwa marekebisho. Hivyo, Serikali hizi mbili zinashughulika kwa pamoja kuona ni namna gani kiwanda hicho kitaendelezwa vizuri zaidi. (Makofi)
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali dogo tu la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aomba niiulize Serikali, kwa kuwa Kiwanda cha Nyuzi cha Tabora hakifanyi kazi; na kwa kuwa mpaka sasa kimeiondolea Tabora kupata mapato ya uhakika na vijana kupata ajira: Je, Serikali iko tayari sasa kukinyang’anya na kukirejesha kiwanda hicho Serikalini? Hakifai kabisa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kimsingi Kiwanda hicho kimezungumzwa siku nyingi na mmekuwa mkikifuatilia. Niseme tu kwamba kabla ya kukirejesha kiwanda Serikalini, hatua ya kwanza ni sisi kukitembelea na kujiridhisha, kwa nini hakiwezi kufanya kazi zake inavyopaswa, ikizingatiwa kwamba Tanzania ni nchi ambayo inalima pamba kwa wingi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapomaliza Bunge, nitatembelea kiwanda hicho ili kujiridhisha na niweze kutoa ushauri Serikalini juu ya utekelezaji utakaofuata. (Makofi)
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, lengo la Serikali kubinafsisha viwanda ilikuwa ni kuongeza ufanisi. Kuendelea kuwepo na viwanda ambavyo havifanyi kazi, Serikali haioni kama imeshindwa kutimiza wajibu wake?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hivi kulikuwa kuna uharaka gani wa Serikali kuvitwaa viwanda hivi bila kuwaandaa wawekezaji badala yake hivi sasa viwanda vya Morogoro vimegeuka kuwa ma-godown, mahali pa kuhifadhi mbuzi na kuishi popo?

Mheshimiwa Spika, naomba kupata majibu ya maswali haya.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, Serikali haijashindwa kwa sababu kubinafsishwa kwa viwanda ni process na kuvitwaa vilevile ni process na tunapovitwaa ni lazima kuzingatia sheria, taratibu na kanuni tulizojiwekea. Kwa hiyo, tunafanya hivyo kwa kufuata taratibu zote.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili la uharaka gani, huwezi ukaanza kumtangazia mtu kwamba kuna kiwanda sasa kimepatikana ukichukue kabla hujakamilisha taratibu za awali za kukirejesha Serikalini.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii, wote tunatambua jambo kubwa linalotuweka Watanzania pamoja ni kutokuwa na ubaguzi, lakini mikopo ya wanafunzi wa Chuo Kikuu imekuwa ikitolewa kwa ubaguzi. Mfano, mimi nimepata division one nasoma Feza, mwenzangu kapata division one anasoma Msalato, atakayepewa mkopo ni yule anayetoka Msalato kwa maana ya kwamba wa Feza ni wa kishua, wa Msalato ni maskini, huu ni ubaguzi wa hali juu, tunajua hustles zinazotumiwa na wazazi kuwapeleka watoto wao shule nzuri tu na si kwamba wana pesa nyingi sana. Je, Wizara itakubaliana na mimi umefika wakati sasa wa kubadilisha kigezo cha kupata mikopo na kigezo kikuu kiwe ni ufaulu wa mwanafunzi badala ya kwamba huyu ana mahitaji zaidi ya mwenzie? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI (K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Halima kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi vigezo vilivyowekwa ni hasa vinazingatia hali halisi ya uhitaji wa mwanafunzi kwamba mwanafunzi mwingine hana uwezo. Kwa hiyo kama hana uwezo ndiyo atakayesaidiwa kwanza.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Mradi wa Mchuchuma na Linganga umekuwa ukizungumzwa kwa muda mrefu sana kipindi ambacho sasa mpaka wananchi na Watanzania kwa ujumla wanakata tamaa. Sasa je, Serikali haioni kwamba sasa hivi hii hela ya fidia ingeichukua yenyewe badala ya kumwachia mwekezaji na watu wetu wakapata fidia hiyo mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili tumeona jitihada za Serikali kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara ya kutoka Mkiu - Liganga mpaka Madaba na ya kutoka Mchuchuma mpaka Liganga kilometa 70. Je, ujenzi hasa wa lami na kuhakikisha kwamba maeneo hayo yanaweza kupitika yataanza lini?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kabla sijaendelea na maswali ya nyongeza kwa umuhimu wake kwa niaba ya wanaviwanda pamoja na Wizara yetu ya Viwanda kwa ujumla napenda kutoa pole kwa msiba mkubwa uliotupata kupitia kifo cha mwanakiwanda au mfanyabiashara wetu Mkuu ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Tanzania Private Sector Foundation, Dkt. Reginald Mengi. Mwenyezi Mungu amrehemu na roho yake aiweke mahali pema peponi. Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianzia swali la kwanza kuhusu Serikali uwezekano wa kulipa fidia, tunapotathmini mradi huu kuna njia mbili; ya kwanza ni kwa kumtumia mwekezaji aweze kulipa fidia, lakini Serikali inapokuwa na uwezo inaweza ikalipa yenyewe. Kwa hiyo, katika kuangalia mradi huu ambao una umuhimu sana kwa Taifa letu kutokana na rasilimali zilizoko pale, Serikali inaangalia uwezekano pia wa yenyewe kuweza kulipa fidia endapo itawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuhusiana na barabara kujengwa kwa kiwango cha lami, hayo yote yapo katika mchakato huo wa Serikali kujipanga ili kuwezesha mradi huu ufanyike kwa tija na kwa manufaa mapana ya Taifa.

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda tu niongezee kwamba Serikali inayo mpango wa kujenga kiwango cha lami kuzingatia kama Mheshimiwa Mbunge anavyozungumza katika maeneo ambayo tumeya-alert kwa ajili ya uchimbaji wa makaa ya mawe na chuma. Tumemaliza usanifu wa barabara kutoka Madaba kwenda Mkiu kilomita mia moja kumi na mbili, lakini pia eneo la barabara ya kutoka Mchuchuma kwenda Liganga, ziko kilometa 72 tumesanifu, Serikali ikipata fedha maeneo hayo muhimu tutajenga kwa kiwango cha lami.
MHE. SILAFU J. MAUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini bado napenda kufahamu kwamba, ikiwa mikoa na wilaya zimeweza kutanganza fursa ambazo zimo ndani ya mikoa husika, lakini bado mikoa ile ama wilaya zile zinasuasua katika kupata wawekezaji; Je, Serikali haioni umuhimu wa wao wenyewe kwenda kusukuma katika mikoa ile na wilaya zile kuweza kupata viwanda hivyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili la nyongeza, napenda kufahamu kwamba wanapewa muda upi wa utangazaji wa fursa na kama fursa haina majibu Serikali inachukuwa mkakati gani katika mkoa huo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Maufi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kuupongeza sana Mkoa wa Rukwa umekuwa ukifanya makongamano mbalimbali ya kuhamasisha uwekezaji na makongamano hayo kwa kweli yamekuwa yakiza matunda. Kwa mfano, wameweza kuhamasisha na kupata kiwanda cha kusindika unga wa mahindi, Kiwanda cha Energy, vilevile wameweza kuhamasisha na mpaka kuwezesha mradi wa makaa ya mawe kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu kwamba Serikali hatuiachi mikoa peke yao isipokuwa mikoa yenyewe kwa sababu inazo fursa hizo kwa karibu zaidi inapohamasisha inaungana na Serikali Kuu kuona kwamba hawa wenye viwanda waweze kwenda kuwekeza huko. Sisi kwa kutumia Tantrade, TIC na Wizara kwa ujumla kwa kushirikiana na Wizara ya Uwekezaji tumekuwa tukiendelea kuhamasisha wenye viwanda au wawekezaji mbalimbali kwenda kwenye maeneo hayo.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa mikoa ambayo ilikuwa vinara wa kuwa na viwanda vingi na imekuwa ikitoa ajira nyingi sana kwa wananchi wa Mkoa wa Morogoro enzi hizo za ujana wetu.

MWENYEKITI: Uliza swali.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, vilikuwepo viwanda vya maturubai, magunia, ngozi, mafuta ya kupikia, vipuli vya mashine, mazulia hata Ulanga tulikuwa na kiwanda cha pamba lakini baada ya ubinafsishaji viwanda vyote vikawa kushne, vikawa magofu ya kufugia mbuzi na Serikali imekuwa ikipiga mikwara mara kwa mara…

MWENYEKITI: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Je, Serikali inatoa kauli gani sasa kwa magofu hayo ambayo yamegeuzwa na wawekezaji badala ya kufanywa kuwa viwanda?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Goodluck, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli ya Serikali ni kwamba wale wote waliokuwa wamebinafsishiwa viwanda na hawajaweza kuviendeleza kama ambavyo mkataba wao ulikuwa na ambavyo Serikali ilitarajia, tunatarajia viwanda hivyo vitarejeshwa. Mpaka sasa Serikali imesharejesha viwanda 15 na tunaendelea na zoezi hilo ili hivi viwanda viweze kufanya kazi kwa tija iliyokusudiwa.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili nami niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Korogwe Mji tulikuwa na kiwanda cha matunda na kama tunavyofahamu Mkoa wa Tanga una kilimo sana cha matunda. Kiwanda kile baada ya kubinafsishwa, yule mwekezaji ni miaka karibu 20 sasa kiwanda kile alishang’oa mashine zote na mabati yote yameshatolewa. Je, mtakuwa tayari sasa kutukabidhi eneo lile ili kusudi tuweze kuwawekea vijana shughuli za kufanya katika eneo lile?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mary Chatanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi kiwanda hicho kinachozungumzwa nimekitembelea na kwa kweli hatuwezi kuendelea kukiita kiwanda na Mheshimiwa Waziri alishakitolea kauli ya kukifuta katika orodha ya viwanda. Kwa hiyo, kama ni eneo, naamini linaweza likatumika kwa Halmashauri inayohusika.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Msingi wa swali langu uko kwenye swali namba 170, kipengele (b) kuhusiana na suala la bei ya mazao kwamba imekuwa ni holela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara itueleze, kwa sababu watu wa Wizara ya Kilimo wanasema wao walishamaliza kazi ya kukusanya, je, korosho ghafi na korosho iliyobanguliwa mnaiuza kwa shilingi ngapi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwambe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi baada ya Serikali kufanya uamuzi wenye hekima kabisa wa kununua korosho kwa hawa wananchi ili kuwapunguzia maumivu ya kuuza kwa bei mbaya, korosho iliyopo sasa hivi tunaendelea kuiuza na hatujapanga bei maalum, inategemeana na mteja anavyokuja na pale itapofikia sisi kuwa imelipa gharama zetu zile ambazo tulitumia. Kwa misingi hiyo, nikuombe Mheshimiwa Mwambe ukiwa pia ni mdau na mwananchi mwingine yeyote anayenisikia hata watu wa nje korosho ghafi zipo na zilizobanguliwa zaidi ya tani 391 zipo na ziko katika hali nzuri basi yeyote anayetaka kununua karibu sana aweze kuuziwa.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika miaka ya 70 na 80 Serikali ilikopa kutoka Japan na Italia dola milioni 20 kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya korosho katika Mikoa ya Lindi na Mtwara. Wakati wa ubinafsishaji viwanda hivyo vilibinafsishwa lakini hadi leo viwanda hivyo havifanyi kazi. Mara nyingi Serikali imesema hapa Bungeni itakaa na wawekezaji kuona kwamba…

MWENYEKITI: Hebu uliza swali Mheshimiwa.

MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali linakuja, ni kwa nini Serikali imelidanganya Bunge mara kadhaa kwamba itakaa na wawekezaji ili waweze kusaidia viwanda hivi na wananchi wapate manufaa yanayohitajika?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masoud, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi katika viwanda hivyo vipo ambavyo vinafanya kazi vizuri na vimeajiri zaidi ya watu 750 kwa kimoja. Kwa mfano, kiwanda cha Tunduru, cha Korosho Afrika lakini pia Kiwanda cha Newala Micronics, hivyo vimeajiri watu 750 kila kimoja lakini pia Micronics pale Mtwara kimeajiri kama watu 350. Vilevile kuna Kiwanda cha Mtwara kinachohusika na korosho pia ambacho sasa hivi ndicho kinachosaidia kufungasha hizo korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kuna baadhi ya viwanda havikufanya vizuri, kwa mfano, Kiwanda cha Mtama na Kiwanda cha Nachingwea, hivyo tumeshavinyang’anya. Pia kuna Kiwanda cha Lindi Buko, nacho tumeshakinyang’anya na tumeshaanza kukifufua. Hiyo ndiyo hali halisi.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na jitihada za Serikali kama ilivyoeleza kwenye swali langu la msingi, lakini wafanyabiashara WENGI wanashindwa kufanikisha kutokana na utitiri wa kodi na vikwazo mbalimbali na kuwa siyo rafiki na TRA kutokana na ukusanyaji wa kodi. Je, ni lini sasa Serikali itaweka mikakati kuondoa vikwazo hivi? Maana wanapata vikwazo vingi sana, watu wa TRA wanawasumbua sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa kuwa masoko hasa ya nje bado ni kikwazo kwa wajasiriamali na wazalishaji wa ndani, ni mkakati gani endelevu wa Serikali kutafuta na kuwaunganisha wazalishaji ambao ni wajasiriamali wetu na masoko ya nje?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza hapo awali ni kwamba Serikali baada ya kutambua changamoto zinazowakabili wafanyabiashara, ndiyo maana tulikuja na suala linaloitwa blue print. Katika mpango huu ambao sasa tuko katika hatua za mwisho za kuandaa mpango wa utekelezaji, ni kwamba taasisi zote za udhitibi ikiwemo TRA, tutaangalia vile vikwazo ambavyo tayari vimeshaainishwa, aidha viweze kuunganishwa na kutozwa na mamlaka moja badala ya kutozwa na mamlaka nyingi nyingi pamoja na kuondoa vikwazo vingine vinavyohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa TRA, hivi juzi tu nimemsikia Mheshimiwa Waziri wa Fedha akitangaza kwamba iwe ni marufuku kwa mtu wa TRA kufungia biashara kwa kuweka makufuli, badala yake wazungumze na wafanyabiashara na kuona namna bora ya kulipa kodi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, katika kutafuta masoko ya nje, napenda tu kuwaambia kwamba kimsingi kupitia taasisi yetu ya TANTRADE, tumekuwa tukifanya maonyesho na kuwashirikisha wafanyabiashara kuwaonesha masoko mbalimbali yaliyopo. Pia na sisi wenyewe tunasaidia kutafuta hayo masoko na kuhakikisha kwamba bidhaa zinazozalishwa zinakuwa na kiwango na zinafungashwa vizuri ili kuweza kutumika kwa ajili ya soko la nje.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kampuni hii ya East Usambara Tea Company Limited (EUTCO)ni kampuni kubwa sana pale Muheza ambayo inalima chai na inasindika chai, sasa kampuni hii imekuwa inapeleka chai hii baada ya kuisindika kwenye mnada kule Mombasa na kule Mombasa baada ya kununua wanafanya packaging na kurudisha tena hapa nchini kuanza kuuza na hii wanaifanya kwa sababu ya kuzuiwa kupata kibali cha kuanzisha kampuni hiyo ya packaging na blending.

Mheshimiwa Spika, sasa Mheshimiwa Naibu Waziri unaweza kutoa ukaamuru sasa hivi kampuni hiyo iache kupeleka chai hiyo ambayo imesindikwa hapa nchini kwenye mnada Mombasa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa sababu umesema, hakuna kampuni ambayo imekatazwa kufanya blending na packaging, ningependa uwaandikie barua kampuni hii ili waanze kutengeneza, waandae kiwanda cha kufanya kazi hiyo ya blending na packaging. Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwanza nikubaliane na mtazamo wake Mheshimiwa Balozi Adadi na nilipotembelea Muheza pia tuliweza kutembelea eneo hili na nikaona kwamba ni kweli ni kampuni kubwa ambayo inafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, lakini kama ambavyo nimeeleza hapo awali, kama ni masuala ya kanuni, inabidi lazima yapitiwe na kufanyiwa marekebisho, lakini wakati huo huo, napenda pia kumsisitiza mwenye kiwanda kwamba anao uwezo wa kuanzisha hii kampuni tanzu ambayo itawezesha kuongeza thamani mpaka hatua za mwisho kupitia uzalishaji wa mashamba yake na hatua za awali ambazo anazifanya kwa sasa.

Kwa hiyo, nipende tu kuwataka wenye mashamba wote wa chai, sisi Tanzania tunahamasisha viwanda, na tungependa ajira zipatikane kupitia mlolongo mzima wa thamani katika nchi yetu. Kwa hiyo, wachukue hizo hatua lakini wakati huo tunaendelea kufanyia marekebisho ya kanuni na sheria ili kuwezesha wadau hawa kushiriki vizuri katika shughuli hii ya uongezaji thamani chai.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi. Sera tunayoenda nayo sasa tunaelekea katika uchumi wa viwanda, ili tuweze kuwa na uchumi wa viwanda lazima tuhakikishe viwanda vinapata malighafi ipasavyo. Katika Mji wa Mafinga kuna Kiwanda cha Pareto hata hivyo kumekuwa na walanguzi ambao wananunua maua ya pareto na kuyasafirisha kwenda nje ya nchi hivyo kusababisha kiwanda kukosa malighafi.

Serikali inatuambia nini katika kudhibiti walanguzi ambao wanasabisha Kiwanda cha Pareto Mafinga kukosa maua?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo ameeleza changamoto inayopatikana katika Kiwanda cha Pareto cha Mafinga, changamoto hizo pia zipo katika maeneo mengine ya kuhitaji malighafi nchini kama kwenye maeneo ya ngozi na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo ni kwamba unakuta kiwanda kinahitaji kipate hizo malighafi lakini baadhi ya viwanda utakuta kwamba vinanunua malighafi kwa bei ndogo sana kiasi kwamba mkulima anakuwa ahapendi kupeleka hiyo malighafi katika kiwanda kama hicho. Lakini wakati huo hivyo viwanda vinahitaji malighafi hiyo kwa bei ndogo labda kutokana na uwezo wake mdogo wa kifedha hasa katika hatua za awali za ujenzi wa kiwanda.

Kwa hiyo, sisi tunafikiria kama Serikali tunaowajibu sasa wakuingilia kati kuona kwamba viwanda viweze kupata malighafi hizo kwa kusaidiwa na Serikali lakini wakati huo mkulima na yeye aweze kupata bei inayostahili kutokana na kazi aliyoifanya. Kwa hiyo, tumeanza kufanyia kazi masuala hayo katika baadhi ya viwanda na tunaamini kwamba kuna hatua stahiki zitachukuliwa kwa viwanda maalum ambavyo vinatumia malighafi zinazozalishwa hapa nchini.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante, sisi watu wa Mkoa wa Njombe ni wakulima wazuri wa kilimo cha chai tangu enzi ya ukoloni, nilitaka kujua.

Ni lini Serikali itawasaidia wakulima wadogo wadogo wa kilimo cha chai ndani ya Mkoa wa Njombe na Mikoa mingine kuanzishia viwanda vidogo vidogo vya kuchakata chai ili kukuza thamani ya chai ile na kuweza kuuliza kwa bei nzuri kwenye kiwanda vikubwa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mgaya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kwamba wakulima wa Njombe, kwanza nipongeze jitihada ambazo zimeshafanyika na vilevile nipongeze kiwanda cha Unilever ambacho tayari kimeshaanza kuchukua chai ya wakulima wanjombe pamoja na inayozalishwa na hao wenyewe. Lakini wakati huo nimepata barua kutoka kwa chama cha Ushirika cha Muvyulu cha Njombe kule Lumbembe ambao nao wanaona kuna changamoto ziko pale kuhusiana na kiwanda ambacho kilianzishwa toka mwaka 1969 na kimekuwa hakijaweza kuendelea na uzalishaji kama ilivyokusudiwa.

Kwa hiyo, tutakapotembelea maeneo hayo kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo naamini tutapata hatua nzuri zaidi za kuwasaidia wananchi wa Njombe.
MHE. DKT. SAADA MKUYA SALUM: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza na nashukuru sana majibu ya Serikali kwa swali langu hilo.

Mheshimiwa Spika, biashara ni nyenzo muhimu sana katika uchumi wa mtu binafsi, lakini vilevile uchumi wa Taifa kwa ujumla. Sasa ucheleweshaji wa kutatua changamoto kama hizi ambazo zinapitia katika mfumo ambapo kama Waziri alivyoeleza wa vikao na taratibu, unaathiri moja kwa moja maisha ya watu na uchumi wa nchi kwa ujumla.

Je, ni lini Serikali itaangalia utaratibu mahsusi wa kutatua changamoto hizi za kibiashara hususan kwa biashara ambazo zinatoka Zanzibar zinakuja katika soko la Tanzania Bara kwa sababu hiyo ndio changamoto kubwa ambayo inajitokeza na sio otherwise? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili Zanzibar kwa sasa kuna Taasisi ya Viwango (Zanzibar Bureau of Standards - ZBS), lakini mara nyingi bidhaa ambazo zinapimwa na ZBS zikiingia katika soko la Tanzania Bara, wafanyabiashara wanalazimika biashara zile kupimwa tena na TBS.

Je, mfumo wa uthibitishaji wa bidhaa wa ZBS hauaminiki au hauko sambamba na mfumo huu wa TBS mpaka inafanya bidhaa ambazo zinakuja zilizopimwa na ZBS zinapimwa tena na TBS?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Saada Mkuya Salum, Mbunge wa Welezo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusiana ni lini kutakuwa na utaratibu au mfumo maalum. Kwanza niseme tu kwamba kama ambavyo nilieleza hapo awali mfumo upo kulingana na ngazi zetu za kimashirikiano na hasa kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais ambayo inashughulikia pia masuala ya Muungano. Kwa bahati mbaya katika maswali yake hajasema hasa bidhaa zipi, amesema kwa ujumla wake, ingekuwa ni bidhaa ipi pengine ingenisaidia zaidi kujua ni kitu gani hasa kishughulikiwe.

Mheshimiwa Spika, lakini niseme tu kwamba kama ambavyo hata juzi tumeshuhudia ni kwamba changamoto muhimu au jambo muhimu linalotakiwa wakati tunapohitaji kujadili juu ya changamoto zinazowakabili wafanyabiashara hao, ni vyema kuwa na umakini, lakini pia kuwa na maelezo ya kina yanayozungumzia hilo suala baada ya kulifanyia utafiti na tafakari ya kutosha. Kwa mfano katika kipindi cha nyuma nimejibu zaidi ya maswali manne yakizungumzia suala la sukari kuingia Tanzania Bara, lakini hivi karibuni tumeshuhudia kuona kwamba kumbe sukari hata inayozalishwa katika Kiwanda cha Mahonda ilikuwa hata haitoshelezi kwa upande wa Zanzibar endapo hakuna sukari nyingine itakayoagizwa kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni mambo ambayo wote inabidi tuyaangalie kwa pamoja. Vilevile Mheshimiwa Makamu wa Rais juzi amesisitiza juu ya umuhimu wa sisi kufanya kazi kwa pamoja kwa mashirikiano na bila kubaguana na hiyo ndio iwe spirit yetu katika kujenga umoja wetu na mashirikiano.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili TBS na ZBS, niseme tu kwamba kupitia hii blueprint katika mambo ambayo yataangaliwa ni pamoja na taasisi ambazo zimekuwa zikifanya kazi kwa pamoja za Kimuungano na hata za Kimataifa ili kuwapunguzia vikwazo wafanyabiashara wetu.

Kwa hiyo, naamini na hilo pia litashughulikiwa kuweza kuona ni jinsi gani mamlaka zetu zote mbili zinajengewa uwezo na kuwa na uelewa wa pamoja ili bidhaa ikikaguliwa upande mmoja isiwe lazima kukaguliwa upande wa pili.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali madogo mawili ya nyongeza, kwa kuwa hivi karibuni kumekuwa na malalamiko ya Viwanda vya ndani kukosa masoko kikiwemo na Kiwanda cha marumaru. Je, nini Mkakati wa Serikali kuhakikisha Viwanda vya ndani vinapata masoko ya uhakika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa kumekuwa na malalamiko ya bidhaa nyingi zisizo na ubora kuingizwa katika Nchi yetu. Je, ni nini Mkakati wa Serikali kuhakikisha bidhaa ambazo hazina ubora yaani bidhaa feki hazingii katika nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kwamba Viwanda vya ndani vinapata masoko ya uhakika ikiwemo hivi vya marumaru kama ambavyo umesema ni kweli kabisa kama ambavyo nimejibu kwenye jibu la msingi ni kwamba marumaru zinazozalishwa nchini sasa hivi ni takribani mita za mraba 32.4 milioni na matumizi yetu ni takribani mita za mraba 30 milioni lakini unakuta bado ni kwamba bidhaa kama hizo zimeendelea kuingia toka nchi za nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kutokana na kwamba Viwanda hivi vinatumia malighafi takribani asilimia 95 ambazo zinapatikana hapa nchini kimsingi tunastahili kuvilinda ili viweze kuhakikisha kwamba vinapata masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni kama ambavyo nimesema kwamba tutaongeza Kodi kwa hizo bidhaa zinazotoka nje ili kuhakikisha kwamba hizi za ndani zinakuwa na bei yenye ushindani. Hata hivyo, napenda kutoa angalizo kwa wenye Viwanda hivyo pamoja na wenye Viwanda wengine, si tu kwamba kwa sababu Serikali imeamua kuongeza Kodi kwenye hizo bidhaa wao sasa wakae tu bila kufanya majukumu yao ya msingi ikiwemo kuandaa business strategies nzuri na marketing strategies ili kuweza kuwafahamisha watumiaji juu ya ubora wa bidhaa zao ili hayo hatuyaendekeza sana kwa sababu tungependa pia walaji wapate bidhaa zilizo nzuri na wanazozitaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuhusu bidhaa feki kupitia TBS, TBS imeendelea kufanya ukaguzi kwa bidhaa zote zinazotoka nje ya nchi na hata zile za ndani kwa mfano kuanzia mwaka 2015 mpaka sasa ni kwamba jumla ya sampuli sabini na nne elfu mia sita tisini na saba zimefanyika na kuzitambua bidhaa ambazo zimefikia viwango vinavyotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kwa bidhaa zinazotoka nje zinakaguliwa kutoka huko nje kabla hazijaingizwa na hata zikitokea kwamba hazikukaguliwa nje tunakagua hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe watanzania kuzingatia Viwango ambavyo vinastahili. Ahsante sana.

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Catherine Magige kwa swali zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, mkakati wa Serikali sio tu kulinda viwanda vya ndani, lakini pia mkakati wa Serikali ni kusaidia viwanda vya ndani na wafanyabishara waweze kufanya biashara nje ya nchi, ndani ya SADC, Jumuiya ya Afrika na hivi sasa tunafanya uchambuzi wa kuhakikisha nchi yetu inajiandaa vizuri na Soko la Pamoja la Afrika yaani Africa Continental Free Trade Area.

Kwa hiyo mpango wa Blue Print, hivi sasa Serikali tumeanda Muswada kwa ajili ya kuja hapa Bungeni, Muswada ambao utasaidia kuweka mazingira ya kirafiki kwa Watanzania kufanya biashara si tu ndani lakini kwenye bara la Afrika na maeneo mengine ya dunia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mkakati wetu ni kulinda viwanda vya ndani lakini pia kuvipa fursa ya kufanya biashara za kimataifa. Nashukuru sana.
MHE. DKT. RASHID M. CHUACHUA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza kwa kuwa mpango ulikuwa ni kupeleka umeme katika vijiji saba na mkandarasi kwa sasa hayuko site isipokuwa kwenye kijiji kimoja ambacho amepeleka umeme kwenye kaya saba peke yake.

Mheshimiwa Spika, kwa nini Serikali haioni haja ya kumfukuza mkandarasi huyu ambaye hafanyi kazi kwa kasi inayohitajika kwa kuwa site hayupo na kwa sababu ni vijiji vichache sana ambavyo vimewekewa umeme na pia alipewa vijiji vichache?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tumeambiwa Mji wa Masasi umeungwa na Grid ya Taifa kutokea Mkoa wa Ruvuma lakini hali ya kukatikakatika kwa umeme ni mbaya zaidi kuliko hata kabla haijaungwa. Ni juhudi gani sasa zinatakiwa zifanywe na Serikali kuhakikisha kwamba inawaondoa wananchi wa Masasi katika adha hii kubwa nay a muda mrefu ya kukatikakatika kwa umeme? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Chuachua, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mkandarasi ambaye yuko site, kwanza tunataka atimize wajibu wake kwa mujibu wa mkataba aliousaini. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, suala hilo litafuatiliwa ili kujua tatizo lake ni uwezo au ni jambo gani ili aweze kuchukuliwa hatua zinazostahili.

Mheshimiwa Spika, kwa sehemu ya pili, niseme tu kwamba kwa ufahamu nilionao ni kwamba kwa sasa bado Masasi haijaungwa kutoka kwenye Gridi ya Taifa kutoka Mkoa wa Ruvuma kwa sababu hata hiyo line haijajengwa isipokuwa kuna mpango wa kufanya hivyo. Naamini endapo utekelezaji huo utafanyika, hali ya Mji wa Masasi itakuwa ni bora zaidi ikizingatiwa kwamba umeme ambao umekuja mpaka Songea Mjini Ruvuma ni wa KV 220 na capacity ya megawatt 60 ni mwingi na unatosheleza kupeleka mpaka maeneo hayo.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami napenda kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri yangu ya Mtwara Vijijini ninazo kata mbili za Moma na Muungano ambazo mpaka sasa hivi mkandarasi hajaweka umeme hata kijiji kimoja. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba anawapelekea wananchi hao umeme kwa haraka?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Ghasia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika masuala ya kuweka umeme kuna hatua. Hatua ya kwanza ni mipango kama kawaida na ku-plan network kama itakavyokuwa. Hatua ya pili ni ya kujenga kwa mfano kujenga line kubwa au line ndogondogo na baada ya hapo kuweka transforma na kuwasha. Katika misingi hiyo niseme tu kwamba nalichukua kama ambavyo umeeleza kumfuatilia huyo mkandarasi tuone kwamba hajafanya kitu kabisa au yuko kwenye hatua ambazo zimebakiza kuweka transforma tu na kuwasha.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa wakandarasi wote nchini kwamba suala la umeme katika vijiji kama ambavyo Serikali inategemea kusambaza umeme katika vijiji vyote Tanzania ni la muhimu hasa ikizingatiwa katika kipindi hiki ambacho Watanzania wanahitaji kuwekeza katika viwanda na shughuli mbalimbali za kibiashara na maisha yao.

Kwa hiyo, niwaombe wakandarasi, Serikali imewapa heshima, hasa wakandarasi wa ndani kuwapa nafasi ya kufanya kazi hizo badala ya kuwategemea wakandarasi wakubwa kutoka nje, watumie wakati huo mzuri na watumie nafasi hiyo kuhakikisha kwamba hawaiudhi Serikali na kusababisha kuwanyang‟anya kazi na kuwapa kazi wakandarasi kutoka nje jambo ambalo walikuwa wakililalamikia siku zote.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa niishukuru Wizara kwa majibu yao mazuri lakini kiukweli mabadiliko hayajaanza kufundishwa vyuoni wala shuleni na TANESCO wamekuwa wakitumia nyaya za zamani. Kwa hiyo basi, kuna mkanganyiko mkubwa zaidi na ukizingatia sasa hivi tuko katika uchumi wa viwanda. Hivyo basi, naiomba Serikali yangu itafute namna sahihi ya kutatua mkanganyiko huu ili kuepusha athari zinazoweza kujitokeza katika kuchanganya nyaya za umeme. Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, pamoja na kupokea ushauri kwa sababu jambo hili ni la muhimu, naomba nitoe maelezo kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kimsingi hizi rangi hazina athari kwa ujumla wake isipokuwa chimbuko la mabadiliko haya ya rangi ilikuwa ni kwa ajili ya kuweka mazingira wezeshi kwa upande wa wenzetu ambao tumekuwa tukichukua standard zao (Commonwealth) walipokuwa wameungana na hawa nchi za Ulaya. Kwa hiyo, unakuta watu wa AU walikuwa na standard zao na watu wa British walikuwa na standard zao ilibidi wawianishe na ndiyo zikatokea hizi rangi nyingine ambazo zimejitokeza.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa mazoea, watu wetu walikuwa wamezoea mtindo huu wa red yellow, blue. Sasa kinachofanyika ni kwamba kupitia TBS, kuanzia mwaka 2010 tulianza kufanya huo uwianisho na tayari tumeshafikia hatua nzuri. Vilevile ili kuondoa hizi changamoto ambazo zinaweza kusababisha madhara kutokana na watu kuchanganya hizo rangi japo pia tunasisitiza na sheria inasema kwamba mtu anayefanya wiring installation iwe kwenye high voltage au low voltage lazima awe na uwezo wa kutosha na awe amethibitishwa au kama akifanya mtu mwingine asiyethibitishwa lazima apeleke kwa aliyethibitishwa.

Kwa hiyo, tunategemea kwamba TBS itakuja na huo mwongozo maalum unaoelekeza hizi standards ili sasa ziweze kutumika kwa mkazo zaidi. Hata hivyo, suala la mpito hilo hata kwenye nchi nyingine lilifanyika.

Mheshimiwa Spika, pia nawaomba wakandarasi wanapokuwa wamefanya kazi inayochanganya mfumo wa zamani na mfumo wa sasa, waweke maelekezo pale kwenye main switch ili mtu yeyote anayefika aweze kujua kwamba mfumo huu umechanganywa.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara na pamoja na jitihada nzuri za Serikali ya Awamu ya Tano ya kufufua viwanda, tayari kuna mpango ambao Serikali kupitia Mifuko ya Jamii inataka kufufua viwanda vya Ngasamo, na Nasa. Viwanda hivi viko katika Wilaya ya Busega na ni viwanda ambavyo vinatoa huduma nzuri sana kwa wakulima wa pamba. Nilitaka kujua tu ni lini Serikali sasa maana wanasema wanategemea, ni lini tutarajie kwamba kiwanda kama cha Ngasamo na kiwanda Nasa vitaanza kufanya kazi kuwahudumia wakulima wa pamba katika Wilaya ya Busega. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, sijui kama nitakuwa na majibu mazuri zaidi sana ya yale ambayo amesema Mheshimiwa Waziri wangu. Kimsingi niseme tu zao la pamba ni kati ya mazao ya kimkakati na ni zao ambalo linategemewa sana ikizingatiwa kwamba pale ambapo kunakuwa na uchakataji wa pamba katika hatua yoyote ile iwe ni kwenye pamba mwanzoni au kwenye utengenezaji wa nguo, ajira zinazotokea hapo ni nyingi sana. Kwa mfano kwenye kiwanda kama cha A to Z nilichokitembelea juzi unakuta kwamba ni watu zaidi ya 8,000 wameajiriwa pale kwa hiyo Serikali inaona umuhimu wa kuhakikisha kwamba viwanda hivi vinafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hatua tulizonazo pamoja na ambazo amezieleza vizuri sana Mheshimiwa Waziri, tumekuwa tukikutana na wataalam wa aina mbalimbali lakini pia wataalam wetu kama TILDO wamekuwa wakienda kushirikiana katika kufuatilia wadau ambao tunaweza tukashirikiana nao. Hivi juzi tu tulikuwa na wataalam kutoka Korea na tunafikiria kwamba katika maeneo yote ambayo yanalima pamba, hizo ginneries pamoja na viwanda vya pamba katika kipindi hiki tunachoendelea nacho tuweze kuhakikisha kwamba angalau tunapata kiwanda kimoja kikubwa. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa masoko haya ya vitunguu yamekuwa tatizo karibu maeneo mengi, je, kuna mpango gani sasa kama Serikali kusaidia eneo hilo la msitu wa tembo na maeneo hayo ili wachuuzi wanapokuja basi waweze kuuza vitunguu vyao katika hali ya biashara.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa eneo la Simanjiro ni kubwa sana na walima vitunguu kwa maeneo hayo. Je, unaonaje, uko tayari kushirikiana na Mbunge wa Simanjiro ili kusaidia ujenzi wa soko la vitunguu katika Jimbo la Simanjiro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme tu kwamba katika mikakati ya Tanzania kwa ujumla wake na hasa katika kuwezesha biashara kufanyika katika mazingira mazuri, suala la ujenzi wa masoko pamoja na kuweka muunganiko kati ya wafanyabiashara na wazalishaji ni jambo muhimu sana. Kwa hiyo, kwa ujumla wake niseme tu kwamba kwa kushirikiana na ofisi ya Rais TAMISEMI Wizara ya Viwanda na Biashara lakini pia pamoja na uwekezaji kwa pamoja tunaangalia kwanza kusaidia katika suala la kuongeza thamani mazao hayo kwa kuwezesha kuwepo kwa viwanda vidogo vidogo na viwanda vikubwa. Vilevile kuhakikisha kwamba bei zinazotumika zinakuwa ni nzuri na sio zile za kuwanyonya wakulima ikizingatiwa pia suala la vipimo.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanzaa, suala la kuanza Miradi ya Liganga na Mchuchuma nimekuwa nikiliuliza mara nyingi katika Bunge lako na nimekuwa nikiuliza mfulizo miaka yote. Kwa hiyo, kuhusu fidia imekuwa ni sintofahamu kubwa kwa wananchi wa maeneo ambayo miradi hii inatakiwa kufanyika. Je, kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa wananchi hao kuendelea kuyatumia maeneo hayo mpaka hapo itakapokuwa tayari kulipa fidia hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, imekuwa ikiwekwa bajeti miaka miwili mfululizo sasa juu ya ulipaji wa fidia. Kwa nini Serikali isilipe fidia wakati inaweka kwenye bajeti zake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Deogratias Ngalawa, kama ifuatavyo:-

Katika suala la wananchi kuendelea kutumia maeneo hayo mimi kwa mtazamo wangu naweza nikasema kwamba wanaweza kuendelea kutumia katika misingi ya kilimo na shughuli zile ambazo hazitakuwa na uwekezaji mkubwa ili kuhakikisha kwamba wanaweza kupata tija inayotokana na matumizi hayo lakini masuala ya ujenzi au kuwekeza kwa gharama kubwa zaidi na kwa sababu tayari tathmini imeshafanyika ni vema wasifanye hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili kuhusu bajeti imekuwa ikitengwa lakini haipatikani, kama nilivyosema hapo awali kwamba kutenga bajeti ni namba moja lakini upatikanaji wa fedha unategemeana na makusanyo yetu lakini pia matumizi kutegemeana na mahitaji na vipaumbele tunavyojiwekea. Sasa tumeona badala ya kulipa fidia wakati mradi huu hauendelezwi kwa sasa ni vema hela zikaelekezwa kwenye yale maeneo ambayo tayari miradi inatekelezwa ili sasa miradi hiyo iendelee kuwezesha kuzalisha fedha nyingi zaidi zitakazowezesha kukamilisha hata hiyo miradi mingine ya kimkakati.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, ili tusipate wakati mgumu, wananchi wanaruhusiwa kufanya shughuli zao kwenye maeneo hayo? Kwenye jibu lako la swali la nyongeza la swali la kwanza, je, wanaruhusiwa sasa kwenda kulima na kufanya shughuli nyingine ukiacha hizo za ujenzi?

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, imekuwa ni kawaida kwa masuala ya kilimo hata maeneo ambayo yana uwekezaji ulimaji wa kawaida huwa upo tu.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, subira ina mipaka yake, nisubiri hadi lini maana hata kuna wimbo umeimbwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, je, ni lini mtairuhusu Zanzibar kujiunga moja kwa moja katika soko la Jumuiya la Afrika Mashariki kwa nchi zile za Uganda, Burundi na Rwanda kwa vile soko la Tanzania Bara limefungwa kabisa, Zanzibar hairuhusiwi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa vile Jamhuri ya Muungano ndiyo yenye nguvu katika sekta ya fedha, sera za kodi na ndiyo mhimili mkubwa wa uendesha wa biashara na nchi. Je, hamuoni mnaendelea kuikandamiza Zanzibar kiuchumi kwa vile bidhaa za Tanzania Bara zinaingia Zanzibar bila vikwazo kwa maana kwamba saa 24 milango iko wazi na zinapokelewa na kupigiwa salute? Je, lini mtaondosha pingamizi hilo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza hapo awali masuala yanayohusu Muungano wa nchi yetu hii ni muhimu na sensitive na ndiyo maana yamewekewa utaratibu maalumu wa namna ya kujadiliana. Kwa hiyo, niseme tu kwamba hayo yote ambayo yanaonekana yanahitaji kufanyiwa maboresho mbalimbali ni vema yakajadiliwa kupitia vikao hivyo ambavyo tumeona ni muhimu sana na vimekuwa vikifanya kazi nzuri sana katika kutatua changamoto za Muungano.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba niseme, taarifa za soko kukamilika kwa asilimia 50 siyo kweli, labda tuambiwe 20 mpaka 30, lakini pia soko hilo limesimama kuendelezwa tangu mwaka 2013. Swali la hivyo lilijitokeza Bungeni mwaka 2016 na taarifa iliyotoka ni kwamba, Nkwenda ilitengewa shilingi milioni 385….

MWENYEKITI: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, najenga hoja, lakini pointi yangu ni kwamba, kumekuwepo na taarifa za kutenga fedha tangu mwaka 2016/2017 ambazo hazijaenda. Sasa swali, hizo bilioni 2.5 kama tumeahidiwa muda mrefu na hazijaenda, zitakwenda kweli?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Wilaya ya Kyerwa iko mpakani, inapata faida ya kuwa na Rwanda na Uganda, hakukuwa na juhudi zozote za kujenga viwanda na kuifanya wilaya kuwa damping place ya bidhaa kutoka Uganda. Nini mkakati wa Wizara kujenga viwanda katika wilaya hii ili kuifungua?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli kama alivyokiri kwamba swali hili lilishawahi pia kuulizwa na Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mbunge wa Jimbo hilo na msisitizo wetu ni uleule, kwamba Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Kilimo na Serikali kwa ujumla, pamoja na Waheshimiwa Wabunge, ni kwamba tunayo dhamira ya dhati, kuhakikisha kwamba, masoko haya ya mpakani yanaimarishwa, ikizingatiwa kwamba hiyo ni sehemu ya kuondoa vikwazo kwa wafanyabiashara wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakumbuka kwamba tarehe 6 Septemba, 2019 Marais wetu, kutoka Uganda pamoja na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, walifanya mkutano kupitia Baraza la Biashara wa kuimarisha biashara za mipakani. Kwa hiyo, suala hilo ni la kipaumbele na litafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusiana na kujenda viwanda, hiyo ni moja ya fursa ambazo ziliibuliwa katika kongamano hilo la wafanyabiashara na nimhakikishie tu kwamba, kadri muda unavyoenda, hayo yote yatashughulikiwa kwa nia ya kuongeza tija ya bidhaa zetu na kuhakikisha kwamba wananchi wetu wa Afrika Mashariki na Tanzania wanafaidika kwa pamoja.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake ambayo ameyatoa. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza eneo ambalo amelizungumzia zaidi siyo eneo la Msanga Mkuu, ni eneo la Mtwara Mjini. Kwa upande wa Msanga Mkuu hakuna kazi yoyote ambayo mpaka sasa hivi imefanyika ambayo inaweza kubeba ujenzi wa viwanda ambavyo amezungumzia. Je, ni lini majadiliano ya bei ya gesi asilia yatakamilika ili hivyo viwanda vianze kujengwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, inapotokea kwamba mchakato wa majadiliano unachukua muda mrefu sana kama ambavyo Helm na TPDC wamechukua tangu mwaka 2011 mpaka leo 2019 majadiliano hayajakamilika. Nini nafasi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kuwasaidia wawekezaji ili waweze kutoka katika huyo mkwamo ambao wameupata. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwanza ninashukuru kwa niaba ya Wizara kwa pongezi alizotupa kwa majibu, pili niseme tu kwamba Serikali imekuwa ikiendeleza juhudi ya kukamilisha mazungumzo hayo, suala la gesi ni utajiri wa Tanzania ambao unapaswa kutumika kwa uangalifu mkubwa. Kwa hiyo, kabla ya kuingia mkataba, ni muhimu sana kwa Serikali kuangalia kwamba inampa mwekezaji gesi hiyo kwa bei ambayo kwanza itakuwa ni bei inayokubalika lakini vilevile kumhakikishia upatikanaji wa malighafi hiyo kwa wakati wote.

Mheshimiwa Spika, nikiendelea na swali lake la pili la kuchukua muda mrefu niseme tu kwamba Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Uwekezaji pamoja na Wizara ya Nishati na Madini tutahakikisha kwamba hilo zoezi la kukamilisha kwa bei inayotakiwa ili aweze kupewa mwekezaji linafanyika mapema iwezekanavyo. Kwa hiyo, nalichukua hili kama commitment ya kushirikiana na Wizara nilizozitaja kuhakikisha kwamba tunafanyia kazi mapema ili nchi iweze kunufaika na gesi ambayo inapatikana Mtwara.(Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti ukiangalia hiyo takwimu utajua wazi kwamba bado kiwango chetu cha ubanguaji ni kidogo kwa sababu msimu wa 2017/2018 Tanzania tulifikisha mavuno ya korosho Tani 312,000, kwa hiyo kinachobanguliwa ni kiasi kidogo sana. Sasa kwa kuwa Mkoa wa Mtwara na Lindi wameshatenga maeneo ya uwekezaji hususani viwanda vya korosho, je, Serikali itatoa vivutio maalum ikiwemo kufuta baadhi ya kodi ili wawekezaji hawa waje Mikoa ya Mtwara na Lindi kuwekeza Viwanda hivyo vya Korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mavuno ya korosho hutegemea sana upatikanaji wa pembejeo na niipongeze Bodi ya Korosho kwa sababu wale wakulima ambao hawajalipa fedha zao za korosho inatoa mkopo, lakini kuna urasimu mkubwa sana wa kupata hiyo pembejeo. Je, Serikali haioni ni muda muafaka sasa badala ya mkulima kuzaminiwa na AMCOS na Serikali ya Kijiji na Mkurugenzi waondoe huo mlolongo mrefu ili wakulima wadhaminiwe na AMCOS na kupewa hiyo sulfur (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota Mbunge wa Nanyamba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana kwa jitihada kubwa anayofanya katika kufatilia juu ya maendeleo mazuri ya zao hili la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusiana na kuweka vivutio kwa ajili ya uwekezaji kimsingi Serikali imekuwa ikifanya hivyo hasa kwa viwanda vyote ambavyo vinatumia malighafi inayozalishwa hapa nchini; na hivi karibuni tumeshuhudia kwamba kodi zimeondolewa kwa ajili ya kuwezesha viwanda hivyo viweze kufanya kazi. Hali kadhalika tunajaribu kuendelea kuona kwamba vile Viwanda ambavyo vilikuwa kwa siku za nyuma vinabangua korosho lakini kwa sasa vimekuwa havibangui na vitaendelea kuwa kama maghala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunajaribu kuwaunganisha sasa na Wawekezaji wengine ili waweze kutumia viwanda hivyo katika kuwekeza mashine na waweze kubangua korosho pasipo kulazimika kuanza kujenga upya pamoja na maeneo hayo ambayo yametengwa. Niupongeze sana Mkoa wa Lindi wa Mtwara kwa jitihada ambazo zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la pili, kuhusu pembejeo suala lake alivyolizungumza nimelisikia. Niseme tu kwamba tungependa zaidi kuona kwamba pembejeo hizo kwa wale wanaoagiza na kuzileta waweze wao wenyewe kuziuza kwa kulingana na uhalisia wa maeneo kuliko tu kutegemea kwamba Serikali yenyewe iwe inaingilia halafu badala yake pengine kutokuwa na usimamizi unaotakiwa. Hata hivyo mawazo yake tunayachukua na yataendelea kufanyiwa kazi.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimimiwa Spika, nakushuru sana na pia naishukuru Serikali kwa majibu mazuri sana ambayo yanawapa matumaini wananchi wa Wilaya ya Chunya. Halmashauri ya Wilaya Chunya imetenga eneo la eka 10 kwenye Kata ya Mbugani kwa ajili ya chuo hicho.

Je, Mheshimiwa Waziri sasa kwa pamoja na majibu mazuri aliyoniambia Serikali iko tayari kupeleka pesa hiyo bilioni 1.5 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Chunya ili ujenzi uanze katika mwaka huu wa fedha ambao tunaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kuipongeza Halmashauri ya Chunya kwa kutenga eneo hilo, vilevile niipongeze Serikali kwa jinsi ambavyo imendelea kuimarisha, miundombinu ya barabara na maji ambayo sasa itawezesha eneo hilo kuzidi kulifanya kuwa rafiki kwa ujenzi wa chuo hicho. Niseme tu kwamba kama ambavyo nimesema katika jibu la msingi ni kwamba kwa sababu fedha hizo zimeshatengwa muda utakapofikia zitapelekwa mara moja ili ujenzi uweze kuanza.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimimiwa Spika, ahsante, kwanza nipongeze nchi za Scandinavia zilikuwa zikisaidia sana Serikali yetu kupeleka Walimu wa mahitaji maalum kwa muda wa miaka mingi, swali langu la kwanza.

Je, ni lini Serikali itaongeza nguvu ya kipesa kuweza kuwadahili wanafunzi wengi zaidi watakaosomea mafunzo ya alama?

Mheshimimiwa Spika, swali la pili katika Wilaya ya Rungwe kuna shule ya watu wenye ulemavu ya Katumba ambayo ina miundombinu iliyochakaa kwa muda mrefu na ina Walimu wachache wa lugha za alama pamoja na lugha za watu wenye ulemavu, Serikali itatia jitihada gani kuweza kusaidia shule hii ya Katumba kupata mahitaji hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimimiwa Spika, ni kwamba suala la watu Wenye Ulemavu ni muhimu sana na Serikali inatambua na kulipa
kipaumbele. Katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na wanafunzi wengi wanaoweza kujifunza lugha ya alama kwa sababu haitoshi tu kila mtu kuongea anavyoelewa ni vizuri kukawa na lugha ambayo kwa yoyote utakayemkuta anaongea lugha ya alama itakuwa ni hiyo hiyo. Wizara tayari ilishashughulikia na kuna vitabu ambavyo vimeshatayarishwa ambavyo vinaweza kuwafundisha watu wengi tukiacha wanafunzi hawa wazazi waweze kuifahamu lugha ya alama.

Mheshimimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuwezeshwa suala hilo. Na kwa upande wa shule ambayo imezungumzwa ya Katumba niseme tu kwamba kwa suala la Watu Wenye Ulemavu hilo ni suala muhimu kwa sababu Tanzania inahitaji kuona kwamba wananchi wote wanafaidika na elimu, iwe mlemavu, iwe asiye mlemavu. Kwa misingi hiyo nikuombe tu Mheshimiwa nitaona kwamba kuna umuhimu wa kutembelea shule hiyo ili iweze kusaidiwa inavyotakiwa.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wanaozalisha umeme ni TANESCO na wanaopanga bei ya kuuza umeme ni EWURA. Kwa muda mrefu TANESCO imekuwa haipati faida, katika kipindi cha miaka kumi iliyopita ni mwaka 2008 na mwaka 2014 waliweza kuzalisha bila hasara.

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka kuwa inatoa ruzuku ya upungufu wa gharama katika uzalishaji wa umeme pale ambapo TANESCO wanakuwa hawapati faida kutokana na mauzo yao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; wanunuzi wa umeme wanaoomba kuunganishiwa umeme wakati mwingine hulazimika kununua nguzo na pale maeneo ambako mpango wa Serikali haujaanza, wamekuwa wakitumia kuanzia 500,000 mpaka milioni kununua nguzo lakini nguzo zinabaki kuwa mali ya TANESCO.

Kwa nini wale wanaojinunulia nguzo na kuunganishwa wasiwe wanapewa units za umeme sambamba na ile gharama waliyotumia kununua nguzo ambazo ni mali ya TANESCO? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. kimsingi Shirika la Umeme TANESCO ni Shirika la Serikali na kwa kweli kwa mara nyingi sana ingekuwa limeachiwa lijiendeshe lenyewe bila kusaidiwa kabisa na Serikali labda sasa hivi lingekuwa limefungwa. Lakini kwa kutambua kwamba hilo ni shirika pekee ambalo pia linachochea uchumi katika nchi yetu kwa maendeleo ya Watanzania kwa ujumla, Serikali yenyewe imekuwa pia ikitoa fedha kwa ajili ya kulisaidia shirika hili pamoja na misaada mbalimbali ikiwemo ya kuanzisha vituo vya kuzalishia umeme, kurekebisha mifumo kwa mfano kujenga line ya msongo wa kv 400 ambao unatoa Iringa mpaka kwenda Mwanza, na sasa hivi unategemea tena kujengwa mwingine wa kv 400 kutoka Iringa mpaka Mbeya, Tunduma, Sumbawanga, Mpanda, Kigoma ambayo ni 400 na kutoka pale kv 220 kwenda mpaka Nyakanazi.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuanzisha uzalishaji katika maporomoko ya maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, Serikali imekuwa ikitoa ruzuku ya aina mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili kuhusiana na kwa nini mwananchi anapokuwa amelipishwa nguzo hiyo nguzo inatakiwa iwe ni mali ya TANESCO; sio nguzo tu, hata transfoma, akifungiwa transfoma ambalo amelinunua mwenyewe bado anashauriwa kuwa ni mali ya TANESCO. Kuna faida kubwa sana kwa kufanya hivyo kwa sababu nguzo ikishakuwa imejengwa pale utatumia lakini ikitokea imeoza kama umeshairejesha kuwa ni mali ya TANESCO inakusaidia kwamba hata wewe usiweze tena kununua nguzo, ile kazi ya ukarabati inafanyika na TANESCO.

Mheshimiwa Spika, lakini siyo hivyo tu, pale nguzo inapokuwa imefika maeneo hayo inawezesha pia kumfanya mwananchi mwingine aweze kuunganishiwa ikizingatiwa kwamba hatuwezi kuweka nguzo nyingi katika mtaa mmoja. Ileile line moja inayokuwa imenda inasaidia na hata hivyo hizo bei zinakuwa siyo bei kamili, zinakuwa zimezingatia sana kumfanya mwananchi aweze kununua kwa bei anayoimudu.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, alipopita pale Mafinga tuli-raise hii concern ya suala la umeme na Mheshimiwa Waziri akaahidi kutupatia transfoma tano ambazozitakwenda kwenye vijiji vya Itimbo, Isalavanu, Matanana na Ndolezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa vijiji hivyo wanasubiri hizo transfoma kwa hamu sana nimeambiwa wanashughulikia. Sasa maswali yangu mawili ya nyongeza kama nilivyosema kwenye swali langu la msingi Mji wa Mafinga unakua kwa kasi kiviwanda na kimakazi kiasi kwamba uhitaji wa umeme ni mkubwa na hata TANESCO hivi sasa inakusanya mapato makubwa kushinda hata baadhi ya mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ninalouliza, je, Serikali iko tayari kujenga kituo cha kupoozea umeme ili wananchi hawa wa Mafinga ambao wanapoteza asilimia 30 ya muda wao wa kuzalisha mali, wapate umeme wa uhakika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ninaomba kuthubutu kusema kwamba, mtu aliyepewa kazi ya ku-survey maeneo ya kupeleka umeme REA Awamu ya III, hakufanya kazi yake kwa weledi na kwa ufanisi. Kwa sababu scope coverage ya maeneo mengi ya vijiji iko chini ya nusu, kiasi kwamba maeneo kama Zanzibar, Bandabichi, Dubai, Ndolezi, Rumwago, Ihongele na Matanana, ambako surveyor alisema kuna kaya 33, lakini kuna kaya 700, Serikali iko tayari kuhakikisha kwamba ile scope coverage katika maeneo yale REA Awamu ya III inatekelezwa, inakwenda kuongezeka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, ni kwamba, Mkoa wa Iringa kwa kubahatika kupitiwa na huu msongo mkuu, yaani backbone ya umeme ya umeme wa KV 400, tunatarajia kuimarisha sana ili uweze kutoa support katika maeneo mengine, hasa inapotokea kuna changamoto ya umeme. Kwa hiyo, tunategemea kwanza kuboresha kwa kuongeza hiki kituo cha umeme ambacho kitakuwa cha msongo wa 220 mpaka 33 kwa kuweka transformer mbili zenye ukubwa wa 60 MVA, kwa hiyo, mara mbili ni 120 pale Mafinga, ili uweze pia kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika katika eneo la Kisada, tunategemea pale kwa ajili ya kupitiwa na hii backbone tuweke pia vituo, kituo ambacho kitakuwa ni cha msongo wa 400 KV kitakachokuwa mpaka 220 na mpaka 33 KV na kitakuwa na transformer mbili zenye saizi ya MVA 200 kila moja. Kwa misingi hiyo tunategemea kwamba eneo hilo litakuwa ni kitovu cha uimarishaji wa umeme katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa upande wa kusambaza umeme, ni kweli katika baadhi ya maeneo ambayo yanazunguka miji, siyo tu kwa Mkoa wa Iringa, yaani Mafinga, lakini pia hata maeneo mengine katika nchi. Tunao mradi wa kuendeleza, kusambaza umeme katika maeneo ya pembezoni mwa miji ambao unafadhiliwa na Benki yetu ya Afrika. Kwa hiyo, tunategemea kwamba kwa Mkoa wetu wa Iringa na maagizo haya ambayo alikuwa ameyatoa Mheshimiwa Rais utafanyiwa kazi na utakuwa mnufaika moja wapo.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Jimbo la Mufindi Kusini tuka kata 16, tuna vijiji 80, tuna vitongoji 365, lakini hatuna Ofisi Za TANESCO, na bahati nzuri tumeanza kujenga Hospitali kubwa sana pale Igohole na Halamshauri ya Mufindi itajengwa pale, Makao Mkuu. Je, Serikali ina mkakati gani sasa kujenga ofisi ya TANESCO kubwa kwa ajili ya kuhudumia vijiji nilivyotaja?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Umeme TANESCO limekuwa likiweka ofisi kulingana na mahitaji na uhalisia wa upatikanaji wa fedha. Kwa sasa taratibu zinazotumika ni kwamba, sehemu ambayo ina wateja zaidi ya 10,000 na laini ya umeme kutoka inapochukuliwa mpaka kufikia huko, umbali wa kilomita 500, mara nyingi imekuwa ikiwekwa ofisi. Lakini vilevile tumekuwa tukiangalia mazingira halisi ya umbali kutoka katika makao makuu ya Serikali kwa maana ya mkoa au wilaya na vilevile pale ambapo inaonekana kwamba mazingira yake ni magumu kiasi kwamba upatikanaji wa huduma ni mgumu zaidi, tumekuwa tukiweka ofisi za TANESCO na kwa kuanzia tunaweka hata zile ofisi ndogo za kuhudumia wananchi.

Kwa hiyo, niseme tu kwamba, eneo hilo litapewa umuhimu baada ya kutathmini hayo ambayo nimeyazungumza.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa katika Jimbo la Mpwapwa, ni vijiji nane tu ambavyo havijapatiwa huduma ya umeme, na Vijiji hivyo ni Kiyegea, Kazania, Tumaligo, Mkanana, Ngaramiro, Nana, Mafuto, Kiboriani, Majani na Namba 30.

Je, Mheshimiwa Waziri ni lini vijiji hivi vitapatiwa huduma ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi katika mzunguko wa tatu, katika REA phase lll, mzunguko wa kwanza, ni kwamba tunatarajia kufikia mwezi wa sita, vijiji vilivyokuwa katika mzunguko huo viwe vimekamilika kupewa umeme na vijiji vingine vyote vinavyofuata tunatarajia kwamba vitaingia katika mzunguko wa pili ambao unategemewa kukamilika ndani ya miaka hii kufikia mwaka 2021. Kwa hiyo, vijiji hivyo kama havikuwemo katika mzunguko huo wa kwanza, basi naamini kwamba vitaingia katika huu mzunguko wa pili.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Naomba kufahamu, kwa sababu tumebakiza takribani mwezi mmoja ili tuweze kuvuna mbaazi na kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri anakiri kwamba ziko jitihada zimefanyika ikiwemo watu wa Malawi kuwashawishi waje wachukue mbaazi hizi; hebu atuambie mpaka sasa ndani ya mwezi huu mmoja ni maandalizi gani ambayo yamefanyika ili kuwahakikishia wakulima kupata uhakika wa masoko ya mbaazi ambazo wanakwenda kuvuna?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili ambalo nilikuwa naomba kuuliza, hebu watu wa Wizara watuambie pia, watu wa SUA sasa hivi wameanzisha project moja inaitwa Vegi- Leg. Hii project kuna baadhi ya maeneo wanaanza kufanya kazi ikiwemo ndani ya Wilaya ya Nachingwea, kuna Kijiji kinaitwa Mitumbati na Ruangwa wamechukua kijiji kimoja kinaitwa Mibure. Kazi kubwa wanayokwenda kuiandaa ni kuweka utaratibu wa kusindika zao la mbaazi au mazao ya jamii ya mikunde. Hebu watuambie, wao kama Wizara wanashirikiana vipi na watu wa SUA kuhakikisha kazi hii inafanyika kwa wingi katika maeneo yote ambayo yanalima zao la mbaazi?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, maandalizi yaliyofanyika kama ambavyo nimezungumza hapo awali, kwanza kwa kushirikiana na TANTRADE lakini na Wizara yenyewe tulifanya ziara ya kutafuta hayo masoko ili kuona kwamba mbaazi zinapokuwa tayari tuweze kujua ni wapi tunapeleka kwenda kuuza.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema ni kwamba sisi wajibu wetu mwingine ni kuwahamasisha wadau mbalimbali na kuwafahamisha wapi wakulima wa mbaazi wapo na waeze kununua, lakini pia kulinda bei ya mkulima ili asionewe wakati wa kuuza mbaazi zake.

Mheshimiwa Spika, kwa kupitia huu mpango ambao umeungumza unaotekelezwa na SUA, kimsingi Wizara yetu kama mratibu inashirikiana na Taasisi zote pamoja na Wizara nyingine katika masuala hayo yanayohisiana na lishe, lakini pia uongezaji thamani wa mazao hayo ya mbaazi pamoja na mazao mengine ili kuweka mazingira wezeshi ya wadau hao kuweza kushiriki kikamilifu na kuweza kuchakata au kuongeza thamani inayostahili.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili name niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika sana kwa majibu ya Serikali namna yalivyo. Ilikuwa tarehe 7 Februari, 2018 kwenye swali langu namba 93, niliuliza swali kuhusiana na kiwanda hiki hiki cha SONAMCU, majibu ya Serikali niliambiwa kwamba ikifika mwezi wa nane mwaka jana, kiwanda hiki kitakuwa kimeanza kufanya kazi, lakini mpaka leo hii ni takribani mwaka mmoja na miezi minne, kiwanda hakijaanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niulize swali moja dogo la nyongeza, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Ni kwa nini Serikali inawadanganya wananchi wa Mkoa wa Ruvuma hususan Songea na Namtumbo?

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kutokufanya kazi kwa kiwanda hiki, Serikali haioni kama inapoteza ajira kwa wananchi 2500, lakini pia Serikali haioni kama inakosesha Serikali mapato? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika,naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kadri ambavyo nitachagua kama ifuatavyo, kwa sababu nimeulizwa mengi kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimfahamishe Mheshimiwa Msongozi, uwekezaji katika kiwanda hicho unafanywa na sekta binafsi. Wajibu wa Serikali ni kuwezesha na kazi ambayo imefanyika. Kuhusiana na mazingira yaliyoko sasa, kwanza kabisa mwekezaji alikuwa anadai VAT Refund na wakati huo huo kabla ya kulipwa anastahili kuchunguzwa hapo ambapo itaonekana alichodai ndicho kiachostahili atarejeshewa na ndipo atakapowezeshwa sasa kuendelea na shughuli zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo hatuna nia ya kuwakatisha tamaa wananchi wa Songea wala Namtumbo. Kwa hiyo, kwa misingi hiyo, kiwanda hiki kitaendelea kuhamasishwa na kuwezeshwa ili kuweza kufikia malengo ambayo yamekusudiwa. Niwaombe sana wananchi wa Mkoa wa Ruvuma ambao mimi pia ni mwananchi wa Mkoa wa Ruvuma, tunayo dhamira ya dhati ya kuona kwamba, ajira zilizokuwa zinapatikana kupitia kiwanda hiki zinarejea na wananchi wananufaika.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kama ilivyo kwa Kiwanda cha SONAMCU kilichopo Songea Mjini. Je, ni lini Serikali itatusaidia sisi wananchi wa Wilaya ya Rungwe kwa Kiwanda cha Chai cha Katumba ili kuongeza kiwanda kingine na kuleta ufanisi wa utengenezaji wa chai na kuleta bei bora kwa wakulima kwa sababu kutakuwa kuna ushindani?

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba kujua Serikali itaruhusu lini kiwanda kingine kijengwe kuweza kusaidia wakulima wa chai? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi sisi tungetamani kuona viwanda vingi vinajengwa na vinaweza kuchakata mazao ya wananchi na kwa tija. Kwa hiyo, kadri viwanda vinavyojengwa, sisi ndiyo tunavyofurahi, kwa hiyo, hatujazuia kiwanda kingine kujengwa Katumba na kilichopo tungependa kiweze kufanya kaz vizuri zaidi. Kwa hiyo, kama kuna kikwazo chochote ambacho kinawakabili hawa Wana Katumba, ni vema tufahamishwe ili tuweze kushirikiana nao katika kuondoa vikwazo hivyo.
MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona, naomba nirudi tena pale kwenye Kiwanda cha SONAMCU, nashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri anafahamu kwamba changamoto iliyopo kwa kutotekeleza ule mkataba, ni kwa Serikali kutowarudishia wale wanunuzi haki yao ambayo ni VAT return na kama mnakumbuka Mheshimiwa Rais aliliongelea hilo juzi kwamba inaonekana Wizara ya Viwanda haifanyi jitihada yoyote ya kuwasaidia wawekezaji kuondokana na changamoto zao.

Je, sasa Wizara ya Viwanda na Biashara imejifunza na iweze kutatua changamoto hiyo ya VAT return kwa kampuni inayonunua tumbaku Songea ili iweze kujenga kile kiwanda?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kama nilivyosema hapo awali, hizi VAT return haidaiwi na kiwanda cha SONAMCU peke yake, kuna wadau wengi ambao walidai, wengine wamerejeshewa, wengine bado wapo katika mchakato wa uhakiki.

Nipende tu kusema kwamba, kimsingi Serikali ina dhamira njema ya kurejesha VAT returns lakini, baadhi ya waliodai, wengine hawakutoa taarifa ambazo ni sahihi, na hiyo imepelekea kufanya zoezi hili kuwa kubwa kwa kuhakiki wale wote ambao walikuwa wanadai VAT returns zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Wizara inao wajibu wa kuendelea kujifunza lakini kuendelea kutatua changamoto ambazo wote tunaona kwamba ni za msingi. Tunayo dhamira njema na niseme tu kwamba katika maeneo ambayo tutafuatilia ni pamoja na Kiwanda hiki cha SONAMCU Songea.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA:Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Pamoja na majibu ya Serikali ya kuonesha masoko mbalimbali nje ya nchi, lakini ukweli tu ni kwamba Serikali hii imekuwa ikizuia sana wafanyabiashara wanaopata masoko nje kwa kisingizio kwamba kuna njaa na haijawahi hata siku moja kuweka mpango wa kufidia hasara ambazo zinatokana na zuio hilo la Serikali.

Sasa Je, Serikali imejiandaa namna gani kuhakikisha kwamba inawapa taarifa wakulima hawa na wafanyabiashara kwamba haya masoko yapo kwasbaabu Bunge sasa hivi haliko live?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili; Mheshimiwa Waziri amesema kwamba kuna mpango wa stakabadhi ghalani lakini katika mazao haya ambayo ni ya mpunga pamoja na mahindi hasa katika Nyanda za Juu Kusini mpango huu haujaanza kufanyakazi. Serikali ina mpango gani wa kuweka utaratibu huu wa stakabadhi ghalani katika mazoa ya mahindi na mpunga kwenye Nyanda za Juu Kusini?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kimsingi ufanyaji wa biashara katika nchi yoyote ile ni lazima uende sambamba na kuzingatia mahitaji halisi ya wananchi wake kwa faida ya wananchi wake. Lakini niseme tu kwamba kwa hali iliopo sasa tunacho chakula cha kutosha na nipende kuwajulisha Watanzania wote na wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi kwamba fursa ya kuuza mazao hayo nje ipo na pale ambapo mfanyabiashara atakwama basi aweze kuwasiliana na sisi kupitia simu zetu, kupitia mitandao ya Wizara ya Viwanda na Biashara, lakini pia Wizara ya Kilimo ambayo tunashirikiana ili kuondoa vikwazo ambavyo vinaweza kuwa vinamzuia mfanyabiashara kufanya shughuli zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili kuhusu Stakabadhi Ghalani; kimsingi ni kwmaba mfumo huo umeshaanza. Nimeshawahi kutembelea baadhi ya maeneo, kwa mfano, pale Tunduru tayari mfumo unatumika kwa masoko ya mpunga, soya pale Namtumbo na maeneo mengine, kwa hiyo niseme tu kwamba huu mfumo ni mzuri kwa sababu unamuwezesha mkulima kwanza kupeleka mazao yao kwa pamoja sehemu moja na kupata soko la uhakika lakini vilevile kuzingatia ubora unaohitajika.
MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na mimi nilitaka kumuuliza Waziri kuhusu mazao, sisi kule Tarime tuko mpakani, kwa mfano, upande wa Kenya, tumbaku wananunua kwa bei juu na soko lipo, kahawa wananunua bei juu soko lipo, mahindi wananunua bei juu kuliko Tanzania na soko lipo na watu wa Tarime wanalima wenyewe, wanaweka mbolea wenyewe. Kwa nini mnawazuia kupeleka mazao yao kwenye soko na bei ya uhakika na wanapolipwa kwa muda?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza ni kwamba kuna mazao ya kimkakati na mazo ya chakula ya kawaida na Serikali kimsingi haijazuia kuuza tunatafuta masoko, kinachohitajika ni kufuata taratibu zinazotakiwa ili pia tuweze kuwa na uratibu mzuri wa kusema kwamba katika mwaka huu, kwa mfano, katika zao fulani tumeuza nini, kwa sababu kama hakuna uratibu maalum itakuwa hata tukiulizwa swali hatuwezi kujibu kwasababu mtu anakuwa ameuza kwa njia za panya na Serikali pia inakuwa imekosa mapato mengine ambayo yanahitajika pale inapotakiwa kutozwa katika mazao hayo.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Waziri ametoa maelezo mazuri sana kuhusu utafutaji wa masoko ambao unafanywa na TanTrade, lakini inaonesha kwamba hizo taarifa TanTrade wanakaa nazo. Na nafikiri kwamba TanTrade wanatakiwa wazipeleke hizo taarifa kwa wahusika, kwa maana watu wetu wa vijijini ambao ndio wakulima.

Je, TanTrade wana mkakati gani wa taarifa hizo kufika zinakohitajika badala ya Wizara kujibu hapa kwa sababu hii ni Wizara sasa tunataka TanTrade ifikishe taarifa kwa wakulima?
NAIBU WAZIRI VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwanza nimpongeze yeye pamoja na waliouliza maswali ya awali kwa jinsi ambavyo wanafuatilia suala la mazao haya na kwa manufaa ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba TanTrade kama Taasisi tunawataka kutoa elimu mara kwa mara, na sasa hivi pia kupitia maonesho ambayo yanategema kufanyika katika viwanja vya Sabasaba pale Temeke ni fursa nzuri na kubwa kwa wakulima kuweza kujifunza na kupata taarifa mbalimbali kuhusiana na uongezaji wa thamani mazao, lakini pia kupata masoko yanayotakiwa. Kwa hiyo, nimuombe tu kwamba Mheshimiwa Mbunge na yeye mwenyewe akiwa ni sehemu yetu basi anapofanya mikutano yake aweze kuwafikishia wananchi taarifa hizi.
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuongeza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na mazao ya chakula sisi Mkoa wa Kagera tunalima mazao ya matunda, mazao ya maparachichi. Ni Majimbo mengi ambayo wanalima mazao ya parachichi kutokana na mvua zinapatikana kwa wingi, lakini maparachichi hayo yanaozea kwenye mashamba, hawana soko la kuuza hayo maparachichi yao.

Ni lini Serikali itawatafutia soko la uhakika la kuuza maparachichi hayo? Kwa sababu nchi ya Uganda wanalima maparachichi kama sisi, lakini wanayasifirisha kuyapeleka nchi za nje. Ninaomba uwasaidie na wenyewe wananchi wa Kagera kutafutiwa masoko. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mazao ya maparachichi na matunda kwa ujumla yanafursa kubwa sana ya kuweza kupata soko ndani na nje ye nchi na habari njema ni kwambakuanzia leo na hata kesho pale Mbeya wadau wa mazao ya matunda ikiwemo matunda na mbogamboga tupo katika kujadili namna gani ya kuweza kuongeza tija katika mazao haya na niseme tu kwamba kwa upande wa wenzetu Mkoa wa Mbeya pia wamefanya vizuri sana kuwekeza katika viwanda vya matunda hususani kwenye maparachichi.

Lakini changamoto zilizokuwa zinawakabili mojawapo ni namna ya usafirishaji wa mazao hayo mpaka nje kwa sababu imekuwa ni lazima wapeleke kwanza mpaka Kenya halafu baada ya hapo ndio yaweze kwenda nje, lakini kwa hatua tuliyonayo sasa kwa uwepo wa viwanja vya ndege ambavyo vimeimarishwa na ndege zetu katika mambo ambayo tunaenda kuyaangalia ni namna gani kunawekezwa fursa za uhifadhi ya mazao hayo ili yasiharibike mapema, lakini pia kuwa na taasisi za kitafiti ambazo zitaweza kutoa ripoti rasmi yaani accredited labs (maabara maalum) ambazo zitakuwa zimeanza kuhakiki na kuwezesha mazao yetu kuuzwa moja kwa moja nje ya nchi naamini kwamba na Mkoa wa Kagera utakuwa ni miongoni mwa wanufaika.