Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu (166 total)

MHE. ZITTO Z. R. KABWE: Mheshimiwa Spika, mwaka 2013 Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali alitoa taarifa ya upotevu wa shilingi bilioni 28 za wakulima wa tumbaku wa Mkoa wa Tabora.
Mheshimiwa Spika, aliyekuwa Rais katika Serikali wa Awamu ya Nne, alikwenda Tabora akaagiza viongozi wa Ushirika wa WETCU na wahusika wote wa ubadhirifu ule wakamatwe mara moja na kufikishwa Mahakamani. Mpaka leo hii hakuna ambaye amekamatwa wala kufikishwa Mahakamani.
Mheshimiwa Spika, wakulima kwa kupitia vyama vyao vya msingi inabidi walipe fedha zile shilingi bilioni 28. Serikali ya Awamu ya Tano inachukua hatua gani dhidi ya watu hawa ambao wamewaibia wakulima wa tumbaku na kuwafanya waendelee kuwa maskini licha ya kwamba wanajitahidi kulima mwaka hadi mwaka? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, hivi tunavyoongea tayari ninayo ile ripoti ya Mkaguzi na naipitia mstari kwa mstari na ninategemea baada ya Bunge hili nitapitia katika maeneo hayo yanayolima tumbaku hasa Mkoa wa Tabora kwa ajili ya kwenda kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Mheshimiwa Rais aliyoyatoa.
Mheshimiwa Spika, siyo tu kwenye tumbaku, tunafuatilia malalamiko ya maeneo mengine yote kwenye mazao mengine yote kuhakikisha wakulima hawaibiwi na watu wasio waaminifu wanaokuwa kwenye vyama hivyo.
Mheshimiwa Spika, ikumbukwe wiki iliyopita tu Mheshimiwa Spika nilikuwa Iringa nikakuta Vyama vya Msingi vimekopa matrekta kutoka CRDB na wamesainiana mikataba na wamekatwa kutokana na michango yao na kutokana na mazao yao, lakini baadhi ya wajanja wameweka utaratibu kwamba baada ya makato kwisha yale matrekta yawe ya kwao.
Mheshimiwa Spika, niliyarudisha kwa Vyama vya Msingi na niliagiza CRDB iandike hati zile kwa Vyama vya Msingi na nikaagiza mamlaka zinazohusika wachukue hatua za kisheria kwa wale ambao wamefanya utapeli.
Kwa hiyo, tutalifanya na wale waliohusika ambao walibainika kupitia Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, hakuna uchunguzi juu ya uchunguzi. Naagiza vyombo vinavyohusika vichukue hatua kwa sababu tayari mtu aliyepewa dhamana ya kukagua alishakagua na kubainisha wale walioiba. Kwa hiyo, nitaenda kufuatilia kujua ni wangapi wameshafikishwa Mahakamani kuhakikisha kwamba sheria inachukua mkondo wake.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa majibu yake na hasa swali langu la (a) amelijibu kikamilifu na kuonyesha ni kwa kiwango gani mradi huu wa MACEMP umeweza kuwasaidia wavuvi hasa hawa wadogo wadogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la (b) bado nina wasiwasi kidogo naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa swali langu la msingi lililenga Ziwa Victoria na hususani Mwibara wavuvi na wao wapate mradi huu wa kuwapa nyavu zinazoruhusiwa halafu wanachukua zile nyavu zisizoruhusiwa ili kuwasaidia wavuvi wadogo badala ya kuendelea kuchoma nyavu zao na wakashindwa kupata nyavu zingine ili waweze kujikimu katika maisha yao. Sasa kwa kuwa amesema Serikali itaanzisha miradi kama hii, naomba Mheshimiwa Waziri awahakikishie Wanamwibara kwamba mradi huu utakapoanza Wanamwibara ndiyo watakao kuwa wa kwanza kunufaika na mradi huu wa kuwapatia wavuvi nyavu badala ya kuwachomea nyavu zao?
Swali la pili, kwa kuwa katika majibu yake ameelezea kwamba manufaa mojwapo ya mradi huu ni kuanzisha kwa BMU hao walinzi wa rasilimali, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Waziri, BMU hizi katika Ziwa Victoria kimekuwa ni kichaka cha kuwasumbua na kuwanyanyasa wavuvi, kimekuwa ni kichaka cha kuwa-harass na kuwasumbua akina Mama kuwanyang‟anya samaki, kumwaga samaki katika mwavuli wa BMU. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na sasa hivi pale Kibara pale kwenye Kijiji cha Mwibara kinamama juzi wamenyang‟anywa samaki na matokeo yake…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Lugola naomba uulize swali tafadhali.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Ndiyo nauliza. Serikali itatoa kauli gani kwa BMU nchi nzima ambao sasa BMU wa Kibara pale wanaitwa Boko Haram ambao wamewanyang‟anya akina mama samaki na kuwatoza faini ya cement mifuko nane na shilingi 5,000/= wakiongozwa na VEO Ndugu Moshi, Azimio Lufunjo, Nyafuru Mgoli, Fredy Moma, Kabezi Chitalo, Mrungu….
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Lugola unavunja Kanuni sasa.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataja watu ambao wanawanyanyasa akina Mama Serikali inatoa kauli gani?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema mafanikio ya mradi huu katika maeneo mbalimbali na nia ama azma ya Serikali ya kutekeleza miradi ya aina hiyo katika maeneo mbalimbali ikiwemo Mwibara, kwa kuwa Mbunge amesema anahitaji niwahakikishie wananchi wake, na mimi niseme kwamba tutakapokuwa tumeshapata uwezo huo nilioutaja na tukaanza kutekeleza kwa kuwa Mbunge ni mdau mkubwa wa kukomesha uvuvi haramu ambao amesema wananchi wake wakipewa zana wataachana na uvuvi haramu, na mimi nimhakikishie kwamba na yeye Jimbo lake na Wilaya yake itakuwa katika maeneo ya vipaumbele vya kuweza kupata mradi huo ili waachane na uvuvi haramu.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumuuliza swali la nyongeza Mheshimiwa Waziri kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, MACEMP Awamu ya Kwanza, ilipeleka nguvu nyingi sana katika udhibiti kwa maana ya ununuaji wa boti, ujenzi wa majengo kwa ajili ya watumishi na kupeleka nguvu ndogo sana kwa wavuvi. Ukiangalia kilimo ni pamoja na uvuvi, lakini upande wa wakulima wanawezesha pembejeo na elimu.
Je, ni lini wavuvi na wenyewe watawezeshwa kwa kupewa zana bora na elimu badala ya kila siku kuwadhibiti, kuwafukuza na kuwatoza faini kama ambavyo tunafanya?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze kwa kazi anayoifanya nzuri ya kufuatilia kazi ya wananchi wake ya uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu inajipanga katika hatua za kuboresha sekta ya uvuvi kuwaangalia na wavuvi wenyewe ikiwemo kuanzia shughuli yenyewe ya uvuvi, ikiwemo adha wanayokutana nayo yakiwemo makato, tozo wanazotozwa lakini pia na uhitaji wa vitendea kazi na kuhakikisha pia kwamba tunawaondolea manyanyaso wanayopewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitoe kauli tu kwa wale ambao wanawanyanyasa wavuvi, wanawanyanyasa akina mama sambamba na yale ambayo tumetoka kuyasikia, ni vema wakazingatia sheria na misingi ya kazi walizotumwa. Kumekuwepo na utaratibu wa baadhi ya watu wanaopewa dhamana, wakipewa mgambo wanatumia kigezo cha sheria, lakini wakiwapokonya maskini wale kama ni chakula wanakula wao wenyewe, wakipewa kazi ya kuzuia sehemu ya kuuzia nguo wakienda pale kuzuia wanapokonya nguo zile wanachukua wanazitumia wao wenyewe. Hivyo hivyo, na kwenye samaki wanawapoka samaki wanachukua wao wenyewe, tabia hiyo waiache na ikitokea katika eneo lolote tupate taarifa ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, mtu anayenyang‟anya wananchi wanaofanya kazi fulani, akawanyang‟anya kwa kigezo cha kutumia sheria na akatumia yeye kwa manufaa yake binafsi ni mwizi kama mwizi mwingine anayenyang‟anya katika kipindi ambacho wananchi hawaoni. Kwa hiyo, tabia hiyo iachwe na kwa wale watakaoendelea watafikishwa katika mkono wa sheria ili kuweza kukomesha tabia hiyo nchi yetu iweze kuendeshwa kwa misingi ya sheria na utawala bora.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuulize swali moja la nyongeza Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, tatizo la pembejeo lililopo kwenye zao la ufuta lipo pia kwenye zao la korosho ambalo ni zao la pili la biashara Mkoa wa Lindi. Changamoto ya pembejeo Mkoa wa Lindi inatokana na utofauti wa maeneo na hali ya hewa. Pembejeo inayoletwa Lindi, Sulpha inaletwa mwezi wa 5 mwezi wa 6 ambao kwa Mchinga wakati huo inakuwa tayari korosho zimeishaanza kuzaa, lakini maeneo mengine ya Tandahimba na Masasi yanakuwa bado.
Je, Serikali ipo tayari sasa, kusambaza pembejeo ya zao la korosho ifikapo mwezi wa tatu ili korosho zinazowahi katika Jimbo la Mchinga ziwahi kupuliziwa na hizo pembejeo.
WAZIRI WA KILIMO MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru sana kwa swali lake la nyongeza ni swali zuri ambalo linahusisha pia pembejeo zinazotolewa kwa mazao mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Wizara yangu, inapanga kuangalia, utaratibu mzima wa utoaji ruzuku, kama nilivyosema jana. Lakini katika kuangalia kwake, nimewaagiza wataamu wangu kila mtaalamu anayesimamia ugawaji wa pembejeo ama mbegu katika eneo husika awe na bango kitita linaloonesha msimu unaanza lini katika eneo gani, na kuhakikisha kwamba Serikali tunasimamia upatikanaji wa ruzuku ama pembejeo husika, kama ni mbegu angalau mwezi mmoja kabla ya msimu kuanza ili kuweza kuwapa fursa wakulima kupata pembejeo hizo kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, niliongea na wataalam wangu ni aibu kwa watu waliosoma wakaaminiwa na Serikali, wakaaminiwa na wananchi wakapewa dhamana kupeleka mbegu ama mbolea ya kupandia, wakati eneo husika watu wako kwenye kupalilia na walishapanda mbegu zao na walishatumia mbolea yao. Kwa hiyo, nimeagiza watu wawe na bango kitita ambalo itasaidia kuwa na uelewa na kuwa na kitu cha kuangalia tunapopeleka pembejeo, tupeleke kwa wakati angalau mwezi mmoja kabla ya msimu kuanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaombe Wabunge, katika maeneo yenu nifikishieni kila mmoja kutoka kwake na mimi nitakuwa na bango kitita langu, anapendekeza mbegu ama pembejeo iwe imeishafika katika eneo lake ifikapo muda gani, na hiyo ndiyo nitakayotumia kusimamia Wizarani kwangu. (Makofi)
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ninaomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, kwa sababu hapa Tanzania tunayo mazao makuu ya biashara, ambayo yalikuwa yanajulikana katika kuongeza uchumi wa nchi yetu ambayo ni pamba, kahawa, korosho pamoja na katani.
Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba mazao haya ambayo yalikuwa yanatoa ajira kubwa, uchumi kwa nchi yetu, kwamba mazao haya sasa yanatafutiwa soko lenye uhakika hasa pamba ambayo zaidi ya Mikoa 14, Wilaya 42 zilikuwa zinategemea zao la pamba, Serikali ina mpango gani hasa? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Ndassa, Mbunge wa Sumve kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana kwa kazi yake nzuri ya Ubunge aliyoifanya na Wabunge wengi wapya tuige kwake, maana yake Mheshimiwa Ndassa ameaminiwa na wananchi wake kwa muda mrefu kwa ajili ya kufanya kazi nzuri namna hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango mzuri sana wa kuendeleza mazao yote ya biashara, mpango wa kwanza ambao Serikali imeweka uzito mkubwa ni kuanzia kwenye ubora wa zao, kwa sababu ubora wa zao una uhusiano wa moja kwa moja na upatikanaji soko lake.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili ambalo Serikali imeweka mkazo mtasikia hata kwenye Mpango utakapowasilishwa na Dkt. Mpango muda siyo mrefu, imeweka mkazo kwenye kuongeza thamani ya mazao, kwa sababu na yenyewe ni hatua nzuri unapoenda kwenye kupata soko la zao husika na baada ya hapo tukishaongeza thamani kwa kupitia viwanda tutakuwa na uhakika wa kuweza kuuza mazao yanayotokana na mazao yetu ya biashara kwa bei ambayo itawaletea manufaa wanachi wetu na kuweza kuwafanikisha kuweza kuchochea watu wengi kujihusisha na uzalishaji wa mazao hayo kwa sababu yatakuwa na tija.
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa katika Halmashauri zetu, hususani Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero kumekuwepo na tatizo kubwa sana la ushuru huu na unaleta matatizo makubwa na kwa kuwa kuna ahadi ya Rais kwamba hizi shughuli ndogondogo zitaangaliwa upya, je, Serikali sasa iko tayari kuziagiaza Halmashauri zote ziangalie upya maeneo ambayo kuna usumbufu mkubwa na ushuru huu, ili marekebisho yafanywe haraka na wananchi wasipate bugudha ikiwemo Wilaya ya Mvomore?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu yake ya ufasaha, na mimpongeze Mheshimiwa Murad kwa ufuatiliaji wake kwa masuala yanayohusu Jimbo lake.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kama ambavyo nilisema wakati nachangia, tunakaa na wenzetu wa TAMISEMI pamoja na Wizara zingine ambazo zinahusiana na sekta ambazo zinahusu mambo ya makato makato na tulishasema tunayafanyia kazi mambo ya makato yote ambayo yanamgusa Mkulima na wafanyabiashara wadogowadogo. Lakini kwa leo nitamke tu kwamba kwa yale makato ambayo hayako kisheria, kwa makato ambayo yanawagusa wakulima ambayo hayako kisheria kuanzia leo hii wale wanaohusika waondoke na tamko hili kwamba wayaache, yale ambayo yako kisheria tunaenda kufuata utaratibu na kuangalia kama yote yabaki ama yabaki kiasi ili kuweza kuhakikisha kwamba tunawapa unafuu wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini yale hayako kisheria na yale ambayo hayahusiani moja kwa moja na uendelezaji wa zao husika hayo yakome moja kwa moja kufuatana na kwamba yamekuwa yakiwapa mzigo wakulima bila kuleta tija katika kuongeza uzalishaji wa zao husika. Na tutachambua moja baada ya lingine na yale ambayo yanaafikiwa kwa kupitia makubaliano ya wadau wahusika, wasikubaliane wao na kuanza kuyatumia mpaka wapate ridhaa ya Wizara kwamba kuna mambo haya wamekubaliana na sisi tuweze kupima umuhimu wa kuwepo makato hayo katika uendelezaji wa zao husika. (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Ndugulile na wa mwisho jirani yako Mheshimiwa Keissy.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Kigamboni lina jamii kubwa sana ya wavuvi lakini sekta hii ina changomoto kubwa sana. Wavuvi wana leseni za chombo, wana leseni za baharia, wana leseni ya aina ya samaki wanayovua lakini wavuvi hawa hawa wakitoka Dar es Salaam wakiingia Mafia kuna leseni nyingine ambayo wanatakiwa kukata. Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mapitio ya mzigo wa leseni ili kuondoa hizi kero kwa ajili ya wavuvi hawa? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Faustine Mbunge wa Kigamboni kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia sana suala la wavuvi, nakumbuka alishakuja ofisini mara kadhaa. Niseme tu kwamba Wizara na Serikali kwa ujumla inayaangalia maeneo yanayolalamikiwa katika kazi zinazowapatia Watanzania kipato hasahasa yanayohusu makato mengi yanayokwenda kwa mtu anapofanya shughuli yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amelisemea hili la leseni nyingi na nilipokutana na Wabunge wanaotokea maeneo ya uvuvi upande wa Kanda ya Ziwa walisema hata mtu akitoka Nyamagana akiingia Ilemela anatakiwa atoe leseni nyingine. Lingine wavuvi ni Watanzania na maji ni ya Tanzania lakini leseni inatolewa kwa dola na lenyewe tumepokea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge kwamba vikao hivi tunavyofanya vya kukutana nao ni kwa ajili ya kuandaa mpango maalum ambao utatoa majawabu ya kudumu ya malalamiko hayo ambayo Wabunge wameyaleta kwa niaba ya wananchi wao. Kwa hiyo, tutalifanyia kazi na tutatoa tamko ambalo litakomesha yale ambayo yanawakwaza wavuvi, wafugaji pamoja na wakulima.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya, lakini zile pembejeo hazifiki kwa wakati. Kwa hiyo, lengo lililokusudiwa haliwanufaishi wakulima. Nataka kujua, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kwamba wakulima wananufaika na pembejeo hizo ikiwa ni kufika kwa wakati?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nampongeza Mheshimiwa Neema Mgaya kwa swali lake zuri na kwa jinsi anavyofuatilia jambo hili la pembejeo ikizingatiwa kwamba Mkoa wa Njombe ni Mkoa wa kilimo na hivyo waliomchagua hawakufanya kosa kumrejesha Bungeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu mfumo huu wa pembejeo umekuwa na upungufu mwingi na Serikali imejitahidi mara kwa mara kuangalia mifumo mipya ili kuhakikisha kwamba kusudi lililokusudiwa linakuwa na ufanisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, nakiri kwamba pembejeo zinapochelewa kusudi la Serikali linakuwa halijafikiwa. Kwa hiyo, kwa sasa hivi tunachoangalia kwenye pembejeo, katika mfumo mpya tunalenga mambo mawili; kwanza ni kuhakikisha kwamba pembejeo zinafika kwa wakati; na pili, tunaangalia namna bora ambayo itafanya pembejeo ziwafikie wakulima wengi kuliko hivi sasa ambavyo tunachukua wachache.
Kwa hiyo, utaratibu ambao tunapanga kama Mheshimiwa Mbunge alivyopendekeza ni kuangalia mfumo ambao utawezesha pembejeo hizi zipatikane madukani kama zinavyopatikana nyingine zile ambazo hazitolewi kwa ruzuku ili wakulima wengi waweze kujinunulia pembejeo zikiwa madukani na zikiwa na bei nafuu. Tunaangalia pembejeo hizi ziweze kupatikana kama coca cola inavyopatikana dukani kwa maskini na tajiri na kila eneo anaipata kwa wakati pale pale anapotaka kuichukua.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Napenda niulize maswali madogo mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa kuna ng‟ombe 320 waliotaifishwa tarehe 08/2/2016 na kwa kuwa haieleweki hao ng‟ombe wameuzwa kwa nani, kiasi cha pesa kilichopatikana na kiko wapi.
Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufuatilia kwa kina ili na mimi niweze kujua hao ng‟ombe wameuzwa kwa nani na hicho kiasi kilichopatikana kimepelekwa wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa kwenye ziara yake Bukombe tarehe 2 mwezi wa nne alipofuatana na Mheshimiwa Waziri wa Mifugo ili kuondoa changamoto hii ya suala la mifugo kuingia kwenye hifadhi alitoa agizo kwamba wafugaji watengewe maeneo kabla ya tarehe 15/06/2016. Je, utaratibu huo na zoezi hilo limefikia wapi?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Elias Kwandikwa kwa kufuatilia kwa ukaribu suala hili na kwa kweli anastahili kuchaguliwa kuwa Mbunge wa eneo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na swali lake la pili la utaratibu ule, tumepanga kukutana na Mheshimiwa Waziri wa Maliasili katika kipindi cha mwisho wa wiki hii kujadiliana utaratibu ambao tutaufuata kuhusu mambo haya ya ardhi. Tunategemea pia kumshirikisha Waziri wa Ardhi kwa sababu utengaji wa maeneo mengine ya malisho unaanzia kwenye Kamati za Vijiji za Matumizi Bora ya Ardhi ambapo jambo hilo halifanywi na Waziri wa Maliasili wala Waziri wa Kilimo. Kwa hiyo, kwenye utaratibu ule wa makundi ya mifugo ambayo yanatokana na vijiji yatatengwa maeneo ya vijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu swali la kwanza, nimekuwa nikifuatilia hata mimi baada ya kuwa nimeambiwa na tuliongea pia na Waziri wa Maliasili, ni kweli sheria inakataza mifugo kuingia kwenye hifadhi na sisi Wabunge tuendelee kutoa elimu hiyo ya kuwaambia wananchi wasiingize mifugo kwenye hifadhi ama kwenye Mapori ya Akiba. Vilevile kumekuwepo na ukiukwaji wa sheria ya baadhi ya watumishi wa Serikali wasio waaminifu kutumia fursa hiyo kama sehemu ya wao kujipatia kipato. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata hizo taarifa kwamba baadhi ya mifugo ambayo imekuwa ikitaifishwa imekuwa ile ambayo wamiliki wake hawakuweza kuwapa fedha wale watu. Kwa hiyo, kwa wale ambao wanamalizana nao, kwa maana ya kutoa fedha wanaachiwa wanaondoka na mifugo. Hilo ni jambo ambalo liko kinyume cha sheria na taasisi zetu za Kiserikali ziendelee kufuatilia na iwachukulie hatua watu ambao wanapindisha sheria kwa manufaa yao binafsi kwa sababu wanaipaka matope Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wengine wamekuwa wakitaifisha mifugo kwa sababu tu wanaenda kuinunua wao wenyewe kwa bei ya kutupa. Hilo na lenyewe liko kinyume cha taratibu za kisheria. Sheria inatakiwa ifuatwe ili kuweza kuendesha nchi kwa utawala bora na wale wananchi wajione hawajaonewa bali wamekiuka sheria na sheria imechukua mkondo wake.
Kwa hiyo, sisi kama Wizara pamoja na Wizara ya Maliasili tutaendelea kutoa elimu lakini na kusimamia sheria ili haki iweze kutendeka.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu yaliyotolewa. Naomba tuweke rekodi vizuri. Hakuna ujenzi wa miundombinu uliokamilika katika Mkoa wa Kigoma hilo la kwanza, Pili, Kampuni ya Kigoma Sugar haifanyi utafiti wa miwa wala BTC hawafanyi utafiti wa chai.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa ruhusa yako naomba swali langu kipengele (a) litafutiwe majibu muafaka kwa sababu hayo siyo majibu yake. Kwa sababu shamba la chai limeachwa limekuwa poro kwa muda mrefu na hakuna utafiti kama huo. Swali la kipengele cha (b) limejibiwa sawasawa. Swali (c)….
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nsanzugwanko kuna nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa hiyo umechagua kusahihisha jibu au utauliza swali la nyongeza? Kwa sababu kama una malalamiko kuhusu jibu umeshayaleta na Kiti kimepokea kitatoa uamuzi. Kama ni hayo tu tumalize au kama unauliza swali la nyongeza uliza swali, suala la kulalamikia jibu tumeshalipata.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nina swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, shamba la Bugaga ambalo Mheshimiwa Waziri anajibu kwamba halikuendelezwa kwa sababu ya ufinyu wa fedha ni kwamba shamba hili hata mwaka huu wa fedha halina fedha. Kwa hiyo ni vizuri tu Wizara waturudishie shamba letu kama wameshindwa kuliendeleza shamba hili la Bugaga tunaomba waturudishie shamba letu ili tulitumie kadri tutakapoona inafaa, kwa sababu inaonekana Serikali haina nia hata kidogo ya kufufu shamba hili la Mbegu.
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri ya swali la Mheshimiwa Nsanzugwanko. Tunaposemea Serikali tunapanga kulifufua shamba hilo hatumaanishi tu kwamba tunategemea bajeti ya Serikali, hata mashamba mengine ambayo tunasemea tunategemea kuyafufua, tumeweka arrangement za tofauti. Kwa mfano, tulisema kwenye shamba la Kitulo tunawategemea ndugu zetu wa Banki ya Kilimo, wiki mbili zijazo wataenda kutembelea shamba hilo waweze kuangalia miundombinu iliyopo na mahitaji ili waweze kuwakopesha nuclear farm pale waweze kuliendeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata kwenye lile shamba la Bugaga, tunategemea kutumia sekta binafsi kama ambavyo tumetumia kwenye lile shamba ambalo liko kule Mbozi na tunategemea pia kutumia ule utaratibu tuliosema kwa wale vijana ambao watakuwa tayari kushiriki kwenye shughuli hizi za kilimo waweze kushiriki kwa arrangement hizo tofauti za kuitumia sekta binafsi na baadae kuuza mbegu zile kwenye taasisi yetu ya mbegu ya Taifa ili iweze kuuza kwa wakulima.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Nsanzugwanko, uridhie tu kwamba tumeshaanza utaratibu wa kuweza kulifufua na kulifanyia kazi na hiyo itaenda sambamba na utaratibu wa kuwarejesha vijana kwenye shughuli za kilimo, sawa na kuwafanikisha vijana kuyafikia masoko kama swali lile lililoulizwa na Mheshimiwa Esther Mmasi ambalo linatupatia masoko mengine ambayo vijana wanaweza wakafikia wakafanya kazi hiyo. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge kuwa limeisha, natarajia kuzungukia kwenye shamba hilo na yeye atakuwepo na tutakuwa pia na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mbegu ikiwa ni mikakati ya kwenda kwenye utekelezaji wa jambo hili ambalo tunalisema.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, lakini kwa upande wa kahawa, Jimbo la Karagwe tunalima kahawa sana na zao la kahawa bado lina fursa kubwa sana kuwainua kiuchumi wakulima wa kahawa na uchumi wa nchi kwa ujumla lakini mikopo ya TIB imekuwa ni kidogo mno kwenda kwenye kukopesha walimaji wa kahawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yangu ni kama ifuatavyo: Kwa vile miche ya kahawa ni ya zamani sana, imepandwa toka enzi za wakoloni na mababu zetu, je, Benki ya Kilimo ina mpango gani wa kuwakopesha wakulima wa kahawa pesa ile waweze kununua miche wakiwemo vijana ambao wana tatizo la ajira na kama miche ikipatikana wanaweza wakajikita kwenye kilimo cha kahawa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa vile kabla ya kuanzishwa kwa Benki ya Kilimo, TIB ilikuwa ikitoa mikopo kwenye sekta ya kilimo kupitia Dirisha la Kilimo, kwa nini hii portfolio isitoke TIB ikaenda Benki ya Kilimo ili hii fedha shilingi bilioni 58.8 itumiwe na Benki ya Kilimo kukopesha wakulima wa Tanzania?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge Innocent Bashungwa kwa kufuatilia suala la miche ya kahawa na kusema kuwa imechakaa na kwenye hotuba yangu nilisema katika Wilaya na Mikoa inayolima miche ya kahawa wajitahidi kupanda miche 5,000 kwa kila hekari ili kuweza kurejesha heshima ya zao hilo la kahawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ombi lake hili la kuangalia uwezekano wa vijana kukopeshwa fedha kwa ajili ya kupanda miche mipya, niseme tu nitaielekeza Benki ya Kilimo wawasiliane na Mheshimiwa Mbunge na wapangilie safari ya kuweza kufika huko ili wakaangalie mazingira sambamba na vile ambavyo tulishakubaliana watafika pia Kitulo kwa ajili ya kuangalia uwezekano wa kukopesha uzalishaji wa mitamba ili wananchi waweze kupata mbegu za mazao haya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Mbunge na naelekeza uwasiliane na Benki ya Kilimo ili waweze kuwakopesha vijana wapande miche mipya ili kurejesha heshima ya zao hilo la kahawa. Zao la kahawa litaendelea tu kama tutalipokea kutoka kwa wazee wetu na sisi vijana tukaona ni zao la fursa kwa ajira na kwa ajili ya biashara.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa shamba hili ni kubwa sana takribani ekari 12,000; na wazalishaji wa mbegu hata ekari 1000 hazijafika katika kuzalisha mbegu kwenye shamba hili. Wananchi wamehangaika kwa muda mrefu wanaharibu mazingira wanatafuta maeneo mapya ya kulima.
Je, Waziri sasa yuko tayari kwenda kuyapitia upya yale maeneo angalau kuwarudishia wananchi eneo angalau hata kidogo ili waendelee kulima kwa maana wanaharibu mazingira hawana maeneo ya kulima?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, NFRA walipokuwa wananunua mahindi msimu wa mwaka 2015; Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi inawadai ushuru wa shilingi milioni 420, hawajalipa fedha hizo.
Je, Serikali ipo tayari kupeleka fedha hizo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, shilingi milioni 420 ambazo hazijapelekwa?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze Wabunge wa Mbeya kwa kufuatilia suala hili, nakumbuka tuliambatana na Mbunge wa Mbozi pamoja na pacha wake Mheshimiwa Hasunga, Mbunge wa Vwawa. Niseme tu maeneo ya aina hii yapo, ambayo yamekuwa yakivutia wananchi kutaka wagawiwe. Nakumbuka hata suala la Bugaga ambalo Mheshimiwa Nsanzugwanko amekuwa akilihangaikia, naelewa concern ya Wabunge kutaka wananchi wapate maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wabunge tukubaliane kwamba zoezi la kuwagawia wananchi mashamba ya Serikali siyo endelevu kwa sababu uhitaji wao ni mkubwa kuliko ukubwa wa maeneo yanayopatikana. Kwa hiyo leo hii hata tungesema tunatoa ekari 2000, kwa sababu hatutoi kwenye shamba la ujamaa, ni dhahiri kwamba wale vijana hawataweza kupata wote eneo hilo ambalo litakuwa tunaligawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, utaratibu endelevu ni kuwaweka vijana kwenye vikundi, halafu washirikiane na taasisi na Serikali, kutimiza lengo lile la kupata mbegu kutoka katika eneo hilo, huku wakisimamiwa na kutimiza vigezo ambavyo vinatakiwa katika suala hilo la mbegu. Nimeelekeza wataalam wangu wanipe mashamba yote ambayo yalishageuka kama mapori ambayo yanatamanisha wananchi kuona hayatumiki ili tuweze kutengeneza ushirika wa vijana wanaotaka kwenda kwenye kilimo waweze kuyatumia na Serikali itimize lengo lake la kupata mbegu kutoka katika mashamba hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kulipa fedha zile ambazo hazikuwa zimelipwa, nimelipokea na nitawaelekeza wataalam wangu wa NFRA waweze kutimiza jambo hili, kwa kulipa deni hilo ili Halmashauri iweze kutekeleza miradi yake ya maendeleo.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. Haya mashamba ya NAFCO hata kwa Babati yapo, yaka-transform kwenda RIVACU. Hivi karibuni mwaka jana, Waziri wa Ardhi alitaka Ofisi ya DC katika Wilaya ya Babati, shamba la RIVACU - Dareda lirudishwe kwa wananchi ambalo wanalihitaji kwa kilimo. Lakini hadi leo jambo hilo halifanyiki ilihali wananchi hao wamekuwa wakihangaika sana. Naomba nifahamu kupitia kwa Waziri wa Kilimo, je, uko tayari sasa kushirikiana na Waziri wa Ardhi, kuhakikisha mashamba ya RIVACU Babati yanarudi kwa wakulima wa Babati?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya ardhi katika Mkoa wa Manyara yamekuwa yakipigiwa kelele sana na Waheshimiwa Wabunge akiwepo Mama Mary Nagu upande wa Hanang na Mheshimiwa Jitu Soni.
Kwa hiyo, kwa jambo hili alilolisema schoolmate wangu, Mheshimiwa Gekul, Serikali tunafanya kazi kwa pamoja, na ndugu zangu wa Manyara ni majirani zangu, nitazungukia kuona maeneo hayo kama ratiba itaweza kwenda sambamba tutaweza kupata fursa hata ya kuwa na wenzentu wa Ardhi ili tuweze kuamua kama Serikali tukiwa wote tuko na taarifa sahihi ambalo zinahusu eneo hilo ili tuweze kuwa na jawabu la kudumu la maeneo hayo. Kwa hiyo, kwa sababu si mbali sana Manyara, tutapangilia utaratibu tuweze kufika katika maeneo hayo, na mimi sioni taabu kwenda kuwasalamia watani zangu japo tu sitaenda na nyama ya punda.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa kutoka Benki Kuu inaonesha kwamba kuanzia mwaka 2006 mpaka 2015 takribani miaka kumi kila mwaka nchi imekuwa ikitumia gharama ya takribani wastani wa dola milioni 900 ambayo ni sawa sawa na shilingi trilioni mbili katika fedha hizi zinatumika kwa ajili ya kununulia bidhaa kutoka nje. Katika fedha hizi, fedha dola milioni 120…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Jesca uliza swali.
MHE. JESCA D. KISHOA: Nauliza swali Mheshimiwa Mwenyekiti, dola milioni 120 zinatumika kununulia mafuta ambayo ni sawa na takribani shilingi bilioni 250.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini Serikali iliyoko madarakani itawakumbuka wananchi wa Singida ambao wamepuuzwa wametelekezwa, lakini wamesahaulika hata katika hili la mafuta? Ninaomba Waziri aje anipe majibu.
MHE. JESCA D. KISHOA: Ni lini bodi itaundwa kwa ajili ya mafuta?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitambue umuhimu wa maswali haya kwa logic, kwa maana ya kwamba Wizara na Serikali, tukishirikiana na Wizara ya Viwanda, tumedhamiria kwa dhati kabisa kuhakikisha kwamba tunajitegemea kwenye sekta hii ya mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Mheshimiwa Mwijage, ameshazindua mkakati ambao utatuondoa katika tatizo hilo. Mheshimiwa Jesca mdogo wangu ambaye tuligombea naye Jimbo moja, wananchi wa Mkoa wa Singida hawajapuuzwa, isipokuwa tunalotaka kufanya kama Serikali na Wabunge wote wanaotokea mikoa hii tuwahamasishe na sisi tulisema kwenye hotuba yetu kila familia iwe angalau na ekari moja ya alizeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Kigoma na Mheshimiwa Jesca amewagusa watu wake wote, kaanzia Singida kwa wazazi wake halafu kaenda swali la michikichi kwa wakwe zake alipoolewa kule na Mheshimiwa Kafulila. Tuwahamasishe, hamasa hii ambayo inatoka kwenye alizeti ambayo Mheshimiwa Allan Kiula, Mheshimiwa Kingu na Mheshimiwa Mlata na Aisharose wanafanya pamoja na akina Mheshimiwa Nkamia na Mheshimiwa Ashatu, tuhamasishe walime alizeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kule Kigoma, kama Mheshimiwa Naibu Waziri alivyojibu ya michikichi 137 kwa kila ekari tuwahamasishe walime, baada ya hapo hatua zitakazofuata za Serikali zitakuwa zile za kisera za kuhakikisha kwamba tuna-discourage mafuta kutoka nje na yatumike yale yanayotoka ndani. Tukianza kwanza kwa ku-discourage mafuta ya nje kabla hatujahamasisha watu kulima kitakachofuata bei zitapanda na watu watakosa hiyo bidhaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili linalohusu bodi na lenyewe sasa hivi alizeti itakuwepo kwenye Bodi ya Mazao Mchanganyiko kwa sababu uzalishaji wake haujawa mkubwa, wananchi hawa tusije tukawawekea mzigo ambao wamekuwa wakibeba wengine kwa ajili ya kuhudumia bodi hizi ile hali wao hawajajitosheleza na kuvutiwa zaidi kwa ajili ya zao hilo.
MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Namuomba sasa Mheshimiwa Mwiguli na Naibu wake Mawaziri hawa shapu wanaofanya mambo kwa ushapu watumie neema hiyo kwa kutengeneza mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji wa mazao ambayo yatawakomboa wana Kishapu.
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalipokea wazo la Mbunge shapu wa Jimbo shapu la Kishapu, ambaye kwa kweli kwa ushapu wake ndiyo maana amekuwa akichaguliwa. Tayari tumeshaandika barua kwa Waziri pacha ambaye kwa leo yupo na heshima kubwa.
Kwa hiyo tutatengeneza hilo ili tuweze kutumia mabwawa hayo.
MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii.
Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali napenda tu nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba katika vile vijiji 73 ambavyo vimeshaandaa Mpango Shirikishi wa Matumizi Bora ya Ardhi, ni vijiji vingapi vipo katika Wilaya ya Bariadi. Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mtemi Andrew Chenge, kama ifuatavyo:-
Kwanza kabisa vijiji vilivyoulizwa kwenye swali la msingi baadhi yake mimi nilishafika akiwa amenipeleka Mheshimiwa Njalu enzi zile nimeenda na helicopter wakati wa kampeni na nikapokea kile kilio cha wananchi wake, nilipanga kwamba nitafika katika eneo hilo baada ya bajeti kwa ajili ya kujionea hali hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tukirudi kwenye swali hili alilolisemea Mheshimiwa Mtemi Andrew Chenge linalohitaji idadi ya vijiji, suala hili la migogoro limekuwa endelevu kutokana na kupanuka kwa idadi ya mifugo pamoja na ongezeko la wanadamu na mahitaji ya matumizi ya ardhi, kwa hiyo, kila wakati panapokuwa pamepimwa, panakuwa pana uhitaji zaidi.
Mheshimiwa Spika, hivi tunavyoongea tayari zaidi ya vijiji 23 vilishafanya upimaji huo lakini mahitaji ni makubwa kuliko idadi hiyo ya vijiji na nitawaomba Wabunge wanaotoka maeneo ya wafugaji waungane na viongozi wa wafugaji ambao tumewaomba watuorodheshee mapendekezo ya maeneo yanayoweza kutatua matatizo haya, lakini pia na maeneo ambayo yana migogoro ili Serikali tuweze kupitia mgogoro mmoja baada ya mwingine ili tuweze kupata majibu ya kudumu kwa ajili ya watu wetu wanaogombana katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, jambo hili tumelipanga kati ya Ijumaa na Jumatatu tutakuwa tumeshapata taarifa hiyo na Waheshimiwa Wabunge wote mnaotoka maeneo ya aina hiyo mtatangaziwa ili tuweze kukaa pamoja. Jambo hili linahitaji ushirikiano wa pamoja na uamuzi wa pamoja katika kupata majawabu ya kudumu na kuondokana na tatizo hili.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba, nakumbuka ulifanya ziara mkoani Mwanza na ulizungumza na wadau wa pamba. Msimu wa pamba umeanza Jumatatu, bei elekezi tunaambiwa ni shilingi 1,000, lakini wapo wanunuzi wengine wanasema hawawezi kununua pamba kwa bei ya shilingi 1,000.
Je, nini msimamo wa Serikali kuhusu bei ya pamba, kwa sababu viwanda vyote hivyo Manonga, MWATEX, vinahitaji pamba ya kutosha; na ili wakulima wa zao la pamba waweze kulima zaidi lazima bei iwe nzuri, nini msimamo wa Serikali kuhusu bei ya pamba?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UFUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, sheria ya zao la pamba inataka bei elekezi itajwe na Bodi ya Pamba kwa kushauriana na wakulima, wanunuzi na wadau wengine wa zao lenyewe. Hiyo processes ilifanyika na hatimaye Bodi ya Pamba ikatangaza bei elekezi ya shilingi 1,000 kwa kilo moja pamba mbegu. Sasa wanunuzi wanayo hiari ya kupima wenyewe, kama hiyo bei wakinunua kwa bei hiyo elekezi au zaidi ya pale, watakuwa na faida katika biashara yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimuarifu Mheshimiwa Mbunge, kwamba hadi hapa ninapozungumza makampuni nane, yamekwisha pewa license ya kununua pamba, na ununuzi wa pamba umeanza. Utaratibu wa msimu wa pamba ni mrefu kidogo, kwa hivyo kwa miaka ya nyuma msimu unapoanza kampuni hizi huwa zinaendelea kupata leseni na kuongezeka kadri msimu unavyokwenda mbele. Kwa hivyo, bei ya pamba ya sasa ni nzuri kwa wakulima, pia baada ya bodi kupitia vizuri ile mjengeko wenyewe wa bei, wana hakika pia itakuwa na manufaa hata kwa wanunuzi wa pamba.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Spika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Vyama vya Upinzani vimekuwa vikileta vurugu, kutotii amri ya halali za Serikali na Jeshi la Polisi na wakati mwingine kuleta vurugu, kwa mfano, katika Jimbo langu la Ulanga kwenye kijiji cha Iputi - Nambuga walichoma nyumba sita za wananchi. Je, Serikali ina kauli gani kuhusiana na suala hili, ili kutokomeza kabisa tabia hii.
Pili, kumekuwa na Wabunge, wakileta uchochezi wa kisiasa katika maeneo yetu ya makazi. Je, Serikali ina kauli gani kuhusiana na Wabunge kama hawa?(
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Jeshi la Polisi limekuwa likitekeleza kazi zake kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni kama ambavyo nimeeleza katika jibu la msingi. Kwa maana hiyo basi, katika kutekeleza wajibu wake huo Jeshi la Polisi halibagui mtu yoyote na lina thamini vilevile maisha ya Watanzania wote kwa mujibu wa Ibara ya 14 ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na limekuwa likichukua hatua stahiki mbalimbali kwa uhalifu wa aina yoyote iwe kutoka katika Vyama Vya Siasa ama raia wa kawaida.
Kwa hiyo, nilitaka nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mlinga kwamba kuna hatua mbalimbali ambazo zimechukuliwa na viongozi ambao wamekuwa wakitoka katika vyama vya siasa wakishiriki katika vitendo vya uhalifu. Mfano halisi ni katika matukio ambayo yanajitokeza sasa hivi Pemba, miongoni mwa watu ambao wameshikiliwa na polisi kwa tuhuma za kuchochea vurugu Kisiwani Pemba wapo ambao walikuwa na nafasi kubwa za uongozi katika vyama vya siasa na katika chombo cha kutunga sheria.
Kwa hiyo, hiyo inadhihirisha kwamba Jeshi la Polisi halibagui mtu na atashughulikiwa mtu kwa mujibu wa matendo yake na siyo kwa mujibu wa affiliation yake ya siasa ama rangi, dini, kabila la mtu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana na Wabunge kushiriki katika vitendo vya kihalifu ni kama nilivyozungumza katika swali la nyongeza la mwanzo kwamba iwe Mbunge, mwanachama wa kawaida, kiongozi wa chama cha kisiasa kitakachoamua hatua za kuchukuliwa ni matendo yake na niseme tu kwamba kwa kuwa umegusia suala la Wabunge wao wana haki zao kwa mujibu wa Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge yanamlinda Mbunge kwa kila ambacho anakisema Bungeni lakini haimlindi Mbunge kwauhalifu wa aina yoyote wa jinai iwe ndani ya Bunge ama iwe nje ya Bunge.
Kwa hiyo, naomba nichukue nafasi hii kuwasihi sana wanasiasa hasa viongozi ikiwemo Wabunge kuwa makini sana na kauli zao na matendo yao kwani yanaweza kuchochea uvunjifu wa amani katika nchi yetu.
Lakini pia nichukue fursa hii kuwanasihi wananchi kuwa makini sana na kauli za wanasiasa ikiwemo viongozi wa siasa katika kuhakikisha kwamba wanafuata misingi ya sheria ya nchi yetu ili waweze kuepuka madhara yanayoweza kuwatokea katika maisha yao.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu sahihi na majibu yanayokidhi. Niongezee tu kipengele kile alichosemea kuhusu Wabunge na viongozi wa vyama vya kisiasa kuwa vyanzo vya vurugu na nieleweke wazi kwamba utaratibu ambao tutautumia kuanzia sasa kwa kupima kwamba kila kiongozi anawajibu wa kuhimiza amani katika Taifa hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, ikitokea uchochezi wa aina yoyote ambao na kiongozi yupo tutashughulika na kiongozi aliyewapeleka watu wengine kwenda kwenye matatizo hayo. Kwa sababu mara nyingi viongozi wamekuwa wakiwatanguliza watu wengine na kupata madhara kwa sababu wao hawaguswi na madhara yale. Kwa hiyo, tutakachofanya na nitaaambia vijana wangu kwamba kunapotokea na uchochezi hangaikeni na mzizi wa tatizo ambaye ni kiongozi aliyesababisha watu waende katika matatizo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nisema kwamba watanzania pamoja na hao ambao hawajasoma vitabu vya historia vinavyoelezea udikteta ni nini wasichanganye udikteta na msimamo wa kusimamia sheria. Mimi niwape taarifa tu kama hawawajui madikteta niwape kwa taarifa zao dikteta huwa hatoi fursa hata ya kuambiwa wewe ni dikteta, huwezi ukamsema mtu wewe ni dikteta na ukaendelea kutembea kwenye disco upo, kwenye unywaji upo, kwenye sherehe upo, yaani kile kitendo kwanza cha kupewa fursa za aina zote zile zinaonyesha kwamba nchi yetu inafuata utawala wa sheria na demokrasia. Wale waliozoea maisha ya deal deal wanatakiwa tu waachane na mambo ya deal deal na wafuate sheria na wataishi kwa usalama.

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Waziri napenda kuongezea kama Waziri ninayesimamia utawala wa sheria (rule of law) nchi hii kwamba kimsingi swali hili halikutakiwa hata kuwemo kwenye Order Paper kwa kuwa linakiuka masharti ya Kanuni ya 40 ya Kanuni zetu za Kudumu.
Kanuni ya 40 inasema; “Swali lolote la Bunge halitaruhusiwa kuulizwa Bungeni kama (d), limekusudiwa kupata maoni ya kisheria ya kinadharia au kutoa mapendekezo juu ya jambo la kubahatisha tu.”
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ukilisoma hili swali la msingi ni nadharia tupu na hoja zakubahatisha, linasema kumekuwepo na vifo vyenye utata wa kisiasa, vifo vipi hivyo vilivyothibitishwa kitaalamu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilieleze Bunge lako Tukufu kifo kikitokea, vijana wetu wa polisi wakishirikiana na mamlaka nyingine kama Mkurugenzi wa Mashtaka wanatumia muda mrefu kufikiri hiki kifo kimetokana na nini, wanatafuta ile blameworthy state of mind au unavyopeleka mahakamani kinachotafutwa ni malice aforethought sio tu unakaa kwenye jukwaa unasema hii ni siasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, (b) inasema; linatokana na habari za kubahatisha tu, linasema inapotokea mpinzani kupoteza maisha suala halipewi kipaumbele. Ushahidi upo wapi tuletee huo ushahidi hapa sisi kama Serikali tutajibu, lakini sio maswali generalized, yanaleta tu hisia mbovu katika jamii ya Watanzania.
(f) inasema linaulizwa kwa njia inayoonyesha jibu lake au kutambulisha mkondo fulani wa maoni na hapa unaona bayana mkondo fulani wa maoni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kusisitiza tu kwamba Watanzania siasa zisitufikishe huko; kibaka anakamatwa tunaanza kukimbilia kwenda mfukoni ana kitambulisho cha CHADEMA au cha CCM, hatutajenga Taifa hili kwa njia hiyo, ahsante.
MHE. KHAMIS M. ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza je. La kwanza, je Serikali haioni utaratibu huu wa askari au wakuu wa vituo kujaza fomu na kupeleka risiti unaonesha urasimu, na inapelekea hadi askari anastaafu kutokulipwa pesa zake hizi za kulipa umeme?
Lakini la pili kwa upande wa askari wadogo ambao si maafisa kwa nini wasiwekewe pesa zao za posho za umeme na maji katika mishahara yao kama wanavyofanya JWTZ? Nashukuru.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khamis Mtumwa, Mbunge wa Kiwengwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali lake la pili, ukweli ni kwamba sio askari wote ambao wanalipwa posho kuna askari ambao hawalipwi posho, kuna askari ambao wanaishi katika nyumba binafsi ambao ndio wengi. Kama unavyofahamu Waheshimiwa Wabunge sasa hivi tuna changamoto ya makazi kwa askari, ambao hawa kiutaratibu wanalipwa posho ya pango ni asilimia 15 ya mshahara. Kwa hiyo hawa hawana shida. Tatizo lilipo ni kwa wale askari ambao wanaishi kwenye nyumba za askari ambapo wakati mwingine kuna tatizo la kuchelewa kwa posho zao. Hata hivyo Serikali Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusiana na swali lake la kwanza ambapo alizungumzia kuchelewa kwa malipo hayo hadi kufikia wakati askari wanastaafu.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge kuna sababu nyingi ambazo zinasababisha ucheleweshwaji wa malipo ya madeni haya. Moja kama ambavyo mnafahamu wakati mwingine kunakuwa na ucheleweshaji wa kupata fedha za bajeti ama wakati mwingine zinakuja kidogo. Lakini pia wakati mwingine hata ambapo zinapokuja kuna matukio ambayo mara nyingi hatuyatarajii, ambayo yanajitokeza yanafanya matumizi yale yaweze kuhamishiwa na kutekeleza yale matumizi ya dharura, ikiwemo ya ujambazi, migogoro ya kijamii, hata operesheni za baadhi ya wanasiasa zisizokuwa na tija. Haya mambo na mambo mengine yanachangia wakati mwingine kufanya fedha hizi zitumike kwa matumizi mengine ya dharura na kuchelewesha malipo yale.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza, nitoe shukrani kwa Serikali kwa jitihada ambazo imeendelea kuzichukua kwa ajili ya kunusuru uchumi wa Lupembe. Kwa namna ya pekee, nimpongeze Waziri wa kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa kufanya ziara Lupembe na ni Waziri pekee aliyekuja Lupembe kwenye Jimbo langu kwa kutembelea hivi viwanda vyote viwili. Pamoja na shukrani hizo, nina swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mgogoro huu umedumu kwa muda mrefu sana na umekuwa ukienda mahakamani bila mafanikio au suluhu ya kudumu. Ni kwa nini sasa Serikali isichukue hatua ya kuwakutanisha wakulima pamoja na mwekezaji ili kuweza kupata suluhu ya kudumu?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa jitihada anazofanya kurekebisha mgogoro ulioko pale Lupembe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utatuzi wa mzozo ule wa Lupembe nadhani unakaribia mwisho kwa maana kwamba mwekezaji yule sasa yuko tayari kulegeza masharti aliyokuwa ameyaweka kwa kile chama cha MUVYULU na tumekwishazungumza naye. Kwa hiyo, nitoe wito tu pia kwa MUVYULU na wao kutong‟ang‟ania mambo ambayo mahakama imeamua siyo kwa kuwapa wao ushindi. Kwa hivyo, wakikubali kwamba watoe na kupokea (give and take) hili jambo litapata muafaka mara moja kwa sababu kimsingi wananchi hawana nia na huo mgogoro isipokuwa ni mmiliki na wale MUVYULU ndiyo wanaendesha mvutano na hivyo kuwafanya wananchi wapate hasara ya kutokuwa na viwanda viwili vinavyofanya kazi kwa mara moja.
MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika,Serikali inatoa kauli gani kwa Jeshi la Polisi kupitia askari wasio waadilifu wanaokamata watu hasa viongozi na wafuasi wa UKAWA na kuwaweka mahabusu kwa zaidi ya saa 24 bila kuwapeleka mahakamani wakijua kwamba wanavunja sheria kwa kuwabambikizia kesi za uchochezi na CyberCrime? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi linapokamata watu huwa haliangalii itikadi zao na linapowafikisha watu mahakamani haliwaulizi kadi ya chama alichonacho, bali Jeshi la Polisi hukamata watu kufuatana na kosa alilofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kwa Watanzania wengine, akishakamatwa, kuna hatua ambazo zinafanyika na baada ya hapo anafikishwa mahakamani. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini nitake tu kumhakikishia kuwa eneo hilo la ekari 10,760 na hizo ekari 5,760 ambazo yeye amezitolea majibu kwamba zinatumika kwa ajili ya mifugo na kilimo, nimhakikishie tu kwamba eneo kubwa halijaendelezwa kwa miaka mingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna zadi ya ekari 4,500 hazijaendelezwa kwenye kitu chochote. Gereza hawajalima wala hawana mifugo. Wananchi wa vijiji vitatu, kijiji cha Kabeba, Ilagala na Sambala hawana maeneo ya kulima na historia inaonesha walichukua zaidi ya ekari 4,000 bila makubaliano na vijiji hivi vitatu.
Swali langu je, ni kwanini Mheshimiwa Waziri asielekeze gereza litoe angalau ekari 1,500 ili na hawa wananchi wa Jijiji vitatu wapate maeneo ya kulima? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kumekuwa na tabia ya baadhi ya Maafisa Magereza kuwakamata wananchi wa vijiji hivi vitatu kuwapiga, kuwanyang‟anya zana zao za kilimo, lakini pia kuwafungulia kesi na kuwapeleka mahakamani. Je, Mheshimiwa Waziri, kama Serikali anatoa tamko gani kwa wananchi wa vijiji hivyo vitatu ambao wamekuwa harassed na Maafisa wa Gereza la Ilagala? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Hasna Mwilima kwa jinsi anavyofuatilia mambo ambayo wananchi wake wamemtuma na kwa kweli yeye ni Mbunge makini, hata juzi nilipita kule wakasema hata uchaguzi ungefanyika leo, angeshinda kwa kiwango kikubwa kuliko kilichopita. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwenye suala hili alilolisemea, ni kweli kuna ekari ambazo hazijaendelezwa, lakini kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, zile zilizoachwa ni zile ambazo zimewekwa kwa sababu ziko kwenye chanzo cha maji ambayo yanatumika siyo tu kwa gereza, yanatumika hata kwa wananchi wengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utaratibu wa malengo mapana ya taasisi zetu hizi za magereza ni hasara kuwa na wafungwa wanaolishwa kwa kodi za walipakodi halafu wakawa hawana kazi ya kufanya. Kwa hiyo, hicho tunachosema hata eneo lile lililopo halijatosheleza tunamaanisha malengo marefu ya kuweza kuwatumia wafungwa wanaoweza kufanya kazi ikiwa ni sehemu ya kuwarekebisha ili magereza yetu yaweze kujiendesha.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu tamko la Serikali kwa wale wananchi ambao wananyang‟anywa vifaa; moja niseme Serikali ya Wilaya ambako ndiko na Jimbo lilipo ni vizuri wakapanga matumizi bora ya ardhi na wanaweza hata wakawasiliana na Wizara ya Ardhi ili kuwatafutia wananchi maeneo mbadala ya kufanya kazi hizo ili wasiingie bila ruhusa katika maeneo ya Magereza na hivyo kusababisha mgongano huu ambao unasababisha wao kukamatwa. Lakini maeneo yote ambayo yana Magereza, tunaendelea kuhimiza mahusiano bora kati ya Taasisi hizo za Serikali pamoja na wananchi wanaozunguka maeneo husika.
MHE. HAMADI SALIM MAALIM: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri lakini pia naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Wizara imekubali kwamba kumekuwa na ucheleweshaji wa mishahara kwa askari hawa wanaopandishwa vyeo, ni kwa nini basi askari hawa wacheleweshwe mishahara yao wakati kila bajeti inapopitishwa tayari nyongeza ya mishahara inakuwa tayari imeshaingizwa katika bajeti ile? swali namba moja.
Pamoja na kwamba Wizara pia imekubali kucheleweshwa kwa mishahara kwa askari hawa, kwa nini basi wanaporekebishiwa mishahara yao washindwe kulipa zile arreas za ile miezi ya nyuma au miaka ya nyuma ambayo imepita kabla ya kurekebishiwa mishahara yao?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mbunge kwa kufuatilia na kuwasemea vizuri vijana wazalendo hawa wanaojitolea kwa ajili ya Taifa letu. Mwenyewe nimezunguka katika mikoa mbalimbali na nimepata fursa ya kuwasikiliza. Matatizo ya aina hiyo si hilo tu, lakini kama Wizara tunaandaa utaratibu wa kila mkoa kuwa na watu wanaofuatilia masuala ya askari ili askari yeye kazi yake iwe ni kulitumikia Taifa na kuondokana na ucheleweshwaji wa marekebisho haya ambayo kimsingi yanatokana na taarifa kamili zinazokusanywa zinazohusu mabadiliko hayo kuchelewa kupatikana na kufikia Utumishi ambao wanahusika kwa ujumla wake kutambua nani anatakiwa alipwe kiasi gani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunapanga si hilo tu la mishahara pamoja na stahili zingine zingine ambazo wanazipata zikiwemo wanapokwenda kufanya kazi nje ya kituo chake, anapokwenda kwenye operation maalum, anapopata haki yake anayo stahili, kuwa na malalamiko mengine hata ya posho anayostahili ambayo inatakiwa kimsingi iendane kwa asilimia ya mshahara wake, mshahara unapopanda posho ile inabaki constant licha ya kwamba ilitakiwa iwe kwenye uwiano wa asilimia.
MHE. UPENDO F. PENEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii. Pamoja na Serikali kufanya jitihada za kuwapa maslahi watu wa Jeshi la Polisi, lakini askari hawa wamekuwa wakitumia nafasi zao vibaya kwa masuala binafsi, kwa kuwaonea wananchi. Serikali ina mkakati gani sasa wa kutoa elimu kwa wananchi ili kutambua ofisi hizo za malalamiko ili askari hawa waweze kuchukuliwa hatua kwa kuwa wananchi wa Mkoa wa Geita, vijana wa boda boda na watu wengine wamekuwa wakionewa na Polisi kwa masuala binafsi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, moja, Taasisi ya Jeshi la Polisi ina utaratibu wake mahususi wa kuchukua hatua kwa kila askari anapokuwa amefanya makosa na wanafanya hatua hizo hata licha ya kuwa pamekuwepo na mlalamikaji, kwa sababu suala la nidhamu kwenye Jeshi la Polisi ni jambo la kipaumbele hata bila kulalamikiwa, ndiyo maana utaona Askari wetu wana nidhamu kubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, inapotokea matatizo ya aina hiyo, Jeshi la Polisi linachukua hatua. Hata hivyo, niseme tu kwa Waheshimiwa Wabunge na kwa Watanzania kwa ujumla, tunapodai haki ni vyema sana tukatambua kwamba tuna wajibu wa kutimiza na hivyo itaondoa taratibu za kuwepo malalamiko ya mara kwa mara. Kwa sababu katika maeneo mengine unaweza ukamnyooshea kidole askari, lakini ukifuatilia undani wake unakuja kutambua kwamba pana mtu ambaye hakutimiza wajibu wake vizuri ndiyo maana Askari akachukua hatua. (Makofi)
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika nashukuru sana kwa kuniona, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Askari wetu wanafanya kazi kwenye mazingira magumu sana na wanafanaya kazi kwa muda mrefu bila kupanda vyeo mpaka kustaafu. Je, Serikali haioni haja sasa ya kutathmini upya vigezo vya kuwapandisha vyeo ili kuongeza ufanisi wa kazi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana kwa kutumia weledi wake kama mtumishi wa umma na kutambua umuhimu wa motisha inayoambatana na upandaji wa vyeo kwa askari kama ilivyo kwa Mtumishi mwingine ili kuweza kuongeza ufanisi. Wazo lake ni zuri, tumelipokea na Mheshimiwa Rais alishaongelea kuhusu kuongeza motisha kwa watumishi wa umma wote hapa nchini mara baada ya kuwa ameshamaliza marekebisho na kutoa dira ya Serikali yake. Sisi wasaidizi wake tunatembea kwenye miguu yake, tunatembea kwenye maneno yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimwahidi Mheshimiwa Mussa Sima taratibu hizo zitakapoanza kufanyika tutatoa kipaumbele kwa vijana wetu wazalendo wanaolitumikia Taifa kwa uzalendo na kwa moyo wao kwa ajili ya kuhakikisha raia wa Tanzania na mali zao wako salama.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, katika jibu lake la msingi amesema kwamba, pindi biashara hii itakapoendelea, Serikali itachukua hatua zinazostahili. Sasa biashara hii ipo inaendelea na hasa katika Majiji makubwa kama Dar es Salaam na ni hatarishi kwa sababu mtu anakuja anajifanya kama anakuuzia kisu, mimi mwenyewe ni muathirika, pindi akikuona umeshika kitu anajifanya kama anakuuzia kisu lakini anakuamuru utoe kile kitu ulichokishika. Sasa naomba tamko la Serikali kwa habari ya biashara hii. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuliona hilo. Kama ilivyo kwa uhalifu mwingine, Serikali inapiga vita uhalifu wa aina yoyote na nitoe rai kwa mtu yeyote ambaye atakutana na mambo ya aina hiyo na yeyote aliye karibu na mtu anayepatwa na jambo hilo, tushirikiane kuhakikisha kwamba tunakomesha uhalifu wa aina hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi litakuwa bega kwa bega na litakuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba wale wote wanaotumia vibaya mazingira hayo watafikishwa katika mkono wa sheria ili kuweza kukomesha uhalifu wa aina hiyo.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona ili niulize swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa askari hawa ambao wanatekeleza kufanya nchi hii iwe na amani kuhakikisha wahalifu wanakuwa hawafanyi vizuri wako katika Jimbo langu la Itigi na wanakaa katika nyumba ya railway ambayo ni mbovu sana. Kituo kile kiko katika nyumba za railway; Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwaboreshea Kituo cha Polisi na Mheshimiwa Waziri anajua kabisa kituo kile ni kibovu na hakifai na wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Itigi wamejitahidi kwa nguvu zao wameshindwa. Nini kauli ya Serikali na je, itawasaidia wananchi wa Halmashauri ya Itigi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, natambua mazingira ya kituo kilichopo Itigi na Mheshimiwa Mbunge amekuja mara kadhaa kulielezea jambo hilo na ameandika na barua ya kiofisi na nimemwahidi kwamba kwa hatua ambazo wameshazifanya wao, akiongoza yeye mwenyewe jitihada hizo na sisi kama Wizara tutawaunga mkono na binafsi nitafika katika Jimbo lake kuweza kuongeza nguvu kwa kuona mazingira yaliyopo na hatua ambazo zimeshachukuliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge, nimhakikishie, awahakikishie na vijana wetu kwamba jambo hilo ameshalifikisha na sisi tutalichukulia hatua zinazostahili kwa kulipa uzito unaostahili.
MHE. USSI SALUM PONDEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, ni wangapi ambao walipandishwa vyeo ambao waliweza kujiendeleza kielimu toka mwaka 1999 na 2000 mpaka sasa na ni utaratibu upi ambao unatumika kupandisha vyeo kwa vijana wa uhamiaji? Kwa sababu mpaka sasa kuna vijana ambao wana vigezo na viwango vya elimu sawa na waliopandishwa vyeo miaka sita nyuma. Kutoka miaka sita mpaka sasa hivi hakuna hata kijana mmoja kwa upande wa Zanzibar ambaye amepandishwa cheo. Je, Mheshimiwa Waziri anaweza akatupa sababu ambazo zimepelekea miaka sita mpaka sasa hivi kuwe hakuna mtu ambaye ameweza kupandishwa cheo? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, si kwamba hakuna ambaye amepandishwa cheo. Wamepandishwa vyeo katika nafasi tofauti tofauti, kumbukumbu zinaonesha zaidi ya vijana 137 kwa gap lile alilolisemea la mwaka 1999 – 2000 walipandishwa vyeo katika nafasi tofauti tofauti.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wale ambao amesema wa upande wa Zanzibar na lenyewe nitalifuatilia kwa undani wake ili niweze kuwasiliana na Mheshimiwa Mbunge. Kama alichosema ndicho, basi katika hatua zinazofuata tunakokwenda tutazingatia ushauri wa Mheshimiwa Mbunge ili kuhakikisha kwamba jambo linapoletwa na watetezi wa wananchi, Waheshimiwa Wabunge, wawakilishi wa wananchi; sisi Serikali tunalifanyia kazi kuhakikisha kwamba panakuwepo na haki ya watu wetu hao wanaofanya kazi vizuri. (Makofi)
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na matatizo ya askari ambayo yameelezwa, lakini kuna matatizo yaliyoko kwa Askari wetu wa Kikosi cha Reli ambao huwa wanasindikiza hizi treni katika maeneo mbalimbali kama vile Mpanda, Kigoma na Mwanza. Sasa kuna utaratibu wa wao kulipwa allowance katika hizo kazi wanazofanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Askari wa Kikosi cha upande wa Kata ya Katumba na Ugala wana madai yao tangu mwaka 2013 mpaka sasa hawajalipwa. Sasa je, Waziri yuko tayari kuhakikisha kwamba Shirika la Reli linalipa mafao yao ili waondokane na tatizo la usumbufu kwa sababu imepelekea mpaka wamefungua kesi Mahakamani?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yapo malalamiko ya madai mbalimbali ya askari yakiwemo hayo ya askari wale wanaofanya kazi upande wa TAZARA. Kilichokuwa kinafanyika ilikuwa ni uhakiki wa madai hayo na Wizara yangu tayari imeshawasiliana na Wizara ya Fedha ili punde ambapo uhakiki huo utakuwa umekamilika wa madai mbalimbali yakiwemo ya askari hao aliowataja Mheshimiwa Mbunge, malipo hayo yaweze kufanyika na kuweza kuondoa kero hiyo ambayo imekuwa ikijitokeza kwa askari wetu wanaofanya kazi nzuri.
MHE. FAKHARIA SHOMARI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru kwamba swali langu limejibiwa vizuri, lakini naona kajibu kwa kifupi sana, hivyo nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza; je, ni lini Serikali itaanzisha mfumo wa CCTV camera katika maeneo ya vituo vya polisi ili kusaidia kubaini matendo ya uvamizi huo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali inasema nini kuhusu huduma za wanafamilia hususan watoto wa askari hao waliovamiwa na kuuawa; watuambie kwamba watoto wao watawapa huduma gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante!
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa concern yake ya usalama wa askari pamoja na huduma kwa wanafamilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu CCTV cameras tunaliangalia kwa ukubwa wake ambapo tunalenga kuangalia majiji kwa ajili ya usalama wa majiji, vituo vya polisi lakini pia katika maeneo ambayo askari wetu wanalinda yakiwemo mabenki pamoja na maeneo mengine ambako huduma hizo zinahitajika. Kwa hiyo jambo hilo tumelipokea na tunalifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu huduma kwa wanafamilia, kwa sasa upo utaratibu ambao fidia huwa inatolewa, lakini tunaongea na wenzetu wa bima tuweze kuangalia upande wa bima ya afya, lakini na upande wa bima ya maisha ambao utalenga utaratibu mzima wa familia zinazoachwa na askari ambao wanapata dharura za aina hiyo. Pia kwa kuwa sasa hivi Wizara ya Mambo ya Ndani inaangalia upya Police Force Act ambayo itakuja Bungeni, ambayo inafanyiwa kazi tunategemea tutapata michango mingi ya Wabunge kupitia Kamati, lakini pia na wote ambao watahusika katika kutengeneza Act hiyo mpya.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza niseme kwamba, natambua kazi nzuri inayofanywa na baadhi ya askari polisi, lakini kuna baadhi ya askari polisi ambao katika utekelezaji wa majukumu…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema, natambua kazi nzuri ambayo inafanywa na baadhi ya askari polisi, lakini kuna baadhi ya askari polisi ambao katika utekelezaji wa majukumu yao wanatumia nguvu kupita kiasi, wanatoa adhabu za kutweza wakati wa kukamata watuhumiwa, kuwasababishia vilema na wengine kuwasababishia maumivu ambayo ni ya muda mrefu.
Sasa Waziri atuambie ni hatua gani ambazo zinachukuliwa ili kuhakikisha kwamba baadhi ya askari hawa wanachukuliwa hatua au kuondolewa kwenye jeshi ili kuondoa chuki ambazo zinaweza zikajengwa na baadhi ya raia kwa jeshi zima la polisi kutokana na vitendo ambavyo vinafanywa na baadhi ya askari polisi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Selasini kwa kutambua kazi nzuri inayofanywa na askari polisi. Nimezunguka nchi nzima nimewaelezea maaskari polisi kuchukua hatua kufuatana na makosa na kufuatana na rika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano vijana walio chini ya miaka 18 wanapokuwa na makosa madogomadogo waangalie namna ya kuyashughulikia, lakini pia na watu wanapokuwa na makosa ya aina hiyo na ni vijana wadogo wasiwekwe sana mahabusu yaliyo na watu waliokithiri kwenye vitendo vya uovu, mfano, kumweka kijana wa miaka 12 ambaye labda alikuwa yuko kwenye magwangala akakaa sehemu moja na watu ambao wameshazoea kwenye uuaji ni kumwandaa kisaikolijia baadaye kuwa mhalifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matumizi ya nguvu; jambo hili lina dhana tofauti. Nimewaambia maaskari wanapopambana na wahalifu watumie nguvu zote kuhakikisha kwamba tunadhibiti uhalifu. Kwa mfano, watu wamekuja wamevamia na wana silaha, wakavamia kituo; ama watu wamevamia eneo kama maeneo ambayo tumeyaona, nimewaelekeza maaskari watumie nguvu zote walizonazo kuhakikisha kwamba tunadhibiti uhalifu. Kwa hiyo, kwenye hilo la uhalifu, kwa wale wanaokuja kihalifu kwa kweli jeshi la polisi tutatumia nguvu zote kwa sababu hatutaruhusu wahalifu waweze kutamalaki katika eneo la nchi yetu.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa wavamizi ama majambazi hao, baadhi yao inasemekana wanatoka nje ya nchi yetu ambao wanaingia kwa njia za panya ama njia nyingine zozote na hawa wanakuja kufanya uhalifu na hata kuwaua askari wetu. Je, Serikali ina mkakati gani mahususi wa kulinda mipaka yetu?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru na nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa hoja aliyoitoa. Tunatambua kweli katika matukio ya uhalifu ambayo yamejitokeza tumebaini wahalifu wakiwa wanatoka nje ya nchi, kwa mfano, silaha zile tulizokamata pale Mbezi na watuhumiwa kati ya wale watu sita baadhi yao walikuwa sio Watanzania. Pia kati ya silaha zilizokamatwa Tabora, Mkoa wa Kigoma kwenye operesheni mbalimbali tulipoziangalia hazikuwa na usajili wa hapa ndani, ni silaha za kutoka nje ya nchi, kwa hiyo tumeendelea kuimarisha operesheni za aina hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunatoa rai kwa wananchi pale wanapotambua kwamba, katika nyumba ya jirani ama katika mtaa wao kuna watu wasiofahamika ama watu wasiotambulika au watu wasioeleweka kama ni Watanzania na kazi zao hazieleweki watoe taarifa katika vituo vya jirani ili hatua ziweze kuchukuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaimarisha taratibu zote za mipakani, lakini wengi wanaoingia hawaingii katika njia rasmi, wanatumia njia za panya. Kwa hiyo, ni muhimu sana kila Mtanzania aweze kutambua kwamba ana wajibu wa usalama wake pamoja na mali zake kwa ujumla wake.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali, nina maswali madogo ya nyongeza. Nashukuru Serikali inatambua kwamba kuna msongamano hasa katika gereza la Manispaa ya Tabora. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kupanua mahabusu ya Kwa Zuberi ili kuweza kupunguza msongamano wa mahabusu walioko katika gereza la Tabora?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kuwasaidia mahabusu ambao wamepelekwa magereza bila kuwa na hatia na kusababisha msongamano usiokuwa na sababu eti kwa sababu upelelezi haujakamilika; wanaendelea kuwekwa tu katika mahabusu hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuleta jambo hili na bahati nzuri na mimi nilishazungukia Mkoa wa Tabora. Tunachokifanya tunakubaliana naye kwamba kuna msongamano katika gereza la Tabora na mapendekezo yake ya kufanya upanuzi katika gereza la Kwa Zuberi ni jambo la msingi tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara tunapokea maoni yote haya, lakini tunachofanya tunaweka vipaumbele katika kuongeza ukubwa wa magereza katika maeneo ambayo magereza yale yana kazi za kufanya ili wafungwa wanapokuwepo waweze kuwa na kazi za kufanya ili waweze kulisaidia Taifa katika kurekebishwa kwao kuliko kuwa na wafungwa wengi, tunatumia kodi za walipa kodi kuwatunza, halafu wakawa hawana kazi za kufanya na wala hawana namna ambayo wanarekebishwa. Kwa hiyo tumepokea na tutaweka vipaumbele kulingana na jambo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kuwasaidia mahabusu ambao wamerundikana na wapate msaada wa kisheria. Serikali tumekuwa tukifanya hivyo na katika kipindi cha tangu Julai, binafsi nimezunguka, Waziri wa Katiba na Sheria amezunguka na katika vipindi tofauti aliambatana na Mkurugenzi wa Mashtaka pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na zoezi hilo limekuwa endelevu na kuna wakati maafisa wenyewe wa ngazi ya juu kutoka katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka wamekuwa wakipita katika mikoa mbalimbali kwa ajili ya kutoa huduma hiyo na kushughulikia kesi zile ambazo si za msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nilipopita Rukwa nilikuta kwenye gereza moja kulikuwepo na vijana kama 11 hivi, nilipowahoji kwamba kwa nini wapo pale, waliniambia makosa yao. Kumi walikuwa wana makosa ya kunywa supu. Walikunywa supu wakashindwa kulipa, walishakaa karibu mwezi hivi na mmoja alikuwa amekunywa soda ya kopo. Sasa nikawambia muda waliokaa umeshazidi gharama ya soda ile ya kopo na ile supu. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tumewaelezea na wenzetu kule waweze kuchukua hatua za kurekebisha kulingana na makosa watu waliyofanya na wale ambao wanastahili kurekebishwa na kuondoka, wasirundikwe mle, wapate dhamana waweze kuondoka na kuendelea kufanyiwa hatua zingine.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Tatizo lililopo la msongamano wa mahabusu kwenye Gereza la Tabora linafanana kabisa na tatizo lililopo kwenye Gereza la Keko lililopo Jimbo la Temeke katika Halmashauri ya Manispaa ya Temeke. Mbaya zaidi ni kwamba, miundombinu ya majitaka ndani ya gereza imekufa na hivyo sasa vinyesi kutoka gerezani vinatiririka mpaka mtaani na kuhatarisha afya za mahabusu na wakazi wa maeneo ya jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye maelezo Mheshimiwa Waziri amesema bilioni tatu iliyotengwa kwa ajili ya kukarabati magereza haijalitaja Gereza hili la Keko. Sasa nataka kujua, Mheshimiwa Waziri anawaambia nini wakazi wa maeneo ya Keko wanaolizunguka gereza lakini na mahabusu waliopo ndani ya Gereza la Keko, waendelee kukaa katika mazingira hayo mpaka lini?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshapokea concern ya Mheshimiwa Mbunge na kwa kuwa katika ratiba ya ziara zangu natarajia kuzungukia na magereza yaliyopo Mkoa wa Dar es Salaam, nitafika na Gereza la Keko na baada ya hapo kama Wizara tutakaa kuangalia hali hiyo na namna ya kulifanyia kazi.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kutokana na msongamano huo wa magereza na mahabusu ambao hata Mheshimiwa Waziri ameukiri hapa, kunasababisha magonjwa mengi hasa ya mlipuko; nimewahi kutembelea Gereza la Uyui pale Tabora, kulikuwa na wagonjwa wengi wa upele; na sasa hivi kuna tatizo kubwa sana la upatikanaji wa madawa sijui Serikali ina mkakati gani wa kufanya upendeleo kuhakikisha wale mahabusu na wale ambao ni wafungwa wanapata dawa za kutosha?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge Mwakasaka amefuatilia mara nyingi sana jambo hili na hata kuna kipindi tumekaa, yeye pamoja na wenzangu wa Wizara ya Afya. Jambo lake tulishalipokea, kadri mtiririko wa fedha unavyokuja tutalifanyia kazi kwa sababu ni jambo ambalo alishalifuatilia hata kwa ngazi ya Wizara na tulimuahidi kwamba tunalifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, naomba uendelee kuvuta subira na niwapongeze wana Tabora kwa kukuamini kwa sababu kwa kweli umeendelea kulifuatilia hilo pamoja na mambo ya uhalifu ambao mara nyingi mmekuwa mkiusemea na sisi tunachukua hatua.
MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ningependa kuuliza swali dogo la nyongeza. Mheshimiwa Waziri tulikuwa naye Tarime na alifika kwenye Gereza la Tarime. Gereza hili linatumika kama gereza linalotumiwa na wilaya mbili, Wilaya ya Rorya na Wilaya ya Tarime na bahati mbaya hata makazi ya askari Waziri mwenyewe aliona. Gereza limejengwa mwaka 1941 likiwa na uwezo wa kubeba watu 245. Sasa hivi gereza lina wafungwa 600 na mahabusu, watu hawana hata pa kulala, Serikali inasema nini kuhusu kurekebisha hali ile ili isije ikaleta matatizo makubwa pale?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishafika kwenye gereza analolisema Mheshimiwa Mbunge, nimejionea hali yake na kumbukumbu zangu zinanionesha kesho nina swali la Gereza la Tarime na nitalifafanua kwa urefu zaidi. Hata hivyo, niseme nimeshapokea jambo hilo na kesho nitalifafanua na sisi kama Wizara tunayafanyia kazi mambo haya ambayo Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakiyaleta.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize swali dogo la nyongeza. Kwa sababu suala hili limekuwa ni kero ya muda mrefu toka naingia Bungeni humu 2010, watu wanaongelea kuhusu kujazwa kwa magereza na Serikali imekuwa ikitujibu kwamba itafanya upanuzi na itapeleka pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kutuletea sheria humu Bungeni ili tubadilishe makosa madogomadogo yalipiwe faini polisi; kama yale aliyosema Mheshimiwa Waziri, mtu kanywa soda anawekwa ndani mwezi mmoja, dada amekutwa barabarani akaambiwa anajiuza anawekwa ndani miezi mitatu, mtu amegombana kisimani na mwenzake anawekwa ndani miezi mitatu. Je, Mheshimiwa Waziri, anaweza kuleta sheria sasa tukabadilisha humu Bungeni makosa mengine yakalipiwa faini polisi kama yalivyo ya trafiki?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Munde kwa hoja aliyoitoa na kwa jinsi alivyoleta mapendekezo kwa umakini. Sisi kama Wizara tumepokea na tutaliangalia kwa ujumla wake hili alilolisema na kabla ya hapa, njiani alinishauri tulifanyie kazi na suala la parole kwa kupanua wigo kwa wanaonufaika na parole, wale ambao wamesharekebika waweze kufanya kazi wakiwa nje. Kwa hiyo, tumelipokea na tutakapokuwa tuna fursa ya mabadiliko ya sheria tutazingatia mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge ili kuweza kupunguza msongamano kwa njia hiyo na kuendelea kuwarekebisha watu kwa kadri sheria inavyosema.
MHE. TWAHIR AWESU MOHAMMED: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Naibu Waziri, naomba nimuulize maswali madogo mawili. Je, Serikali iko tayari kwa sasa kupokea majina ya wananchi walionyanyaswa na kupigwa chini ya mikono ya Jeshi la Polisi?
Swali la pili; je, Serikali imewahi kuwatia hatiani Askari Polisi waliotajwa kuwanyanyasa raia kulingana na ukubwa wa makosa?
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara tuko tayari kupokea majina ya aina hiyo na tuna kitengo rasmi ambacho kinashughulikia malalamiko ya wananchi na mara wanapopokea wakijiridhisha huwa wanachukua hatua.
Kuhusu swali la pili kama Serikali ama Wizara iliwahi kuchukua hatua kwa watu ambao wamelalamikiwa kunyanyasa wananchi. Wanachukua mara kwa mara na jana tu tulisema zaidi ya Askari 154 tayari waliwahi kuchukuliwa hatua hizo na hivi tunavyoongea Waheshimiwa Wabunge hata leo kwenye magazeti mmesikia kuna Askari wamefukuzwa kazi jana tu kwa kuwanyanyasa wanafunzi kinyume na taratibu za sheria za utendaji wa kazi.
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa, tatizo ambalo linaonekana la kuwanyanyasa wananchi ambalo linafanywa na Polisi linafanana sana na malalamiko mbalimbali ambayo yanatoka katika Idara ya Uhamiaji kwamba Idara ya Uhamiaji nao wanafanya unyanyasaji mkubwa kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningeomba kujua kwa sababu katika Idara hii kuna watumishi ambao hawajalipwa mishahara yao kwa kipindi kirefu sana. Serikali inasema nini au ina tamko gani kuhusu watumishi hawa wa ajira mpya ambao hawajalipwa mishahara yao ili Serikali iweze kutoa majibu yanayoeleweka, kwamba watalipwa lini mishahara yao watumishi hao wa ajira mpya?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza suala la watu kunyanyaswa lina pande mbili. Sisi tumesema yale ambayo tunajiridhisha nayo tunachukua hatua, lakini suala la kutimiza wajibu ni suala la Watanzania wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Askari wapya ambao hawakuwa wamelipwa mishahara yao, nimhakikishie Mbunge kwamba tatizo hilo kweli lilikuwa kubwa na niwaombe radhi wale askari wetu ambao wamefanya kazi kwa muda bila kupata haki yao, kwa sababu mshahara na posho siyo hisani ni haki yao. Serikali imeshafanya kazi kubwa. Mwanzoni kulikuwa na idadi kubwa waliokuwa wanadai zaidi ya 297, lakini Askari 181 tayari walishapewa mishahara yao na watapewa na yale ambayo yalikuwa malimbikizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na tatizo ndani ya Wizara na nilishatoa maelekezo. Kuna watu bado wanafanya kazi kwa mazoea wakidhani labda Askari anatakiwa aishi kimsoto msoto hivi. Hakukuwa na sababu ya kutokupeleka majina yale Utumishi na kuyaingiza kwenye mfumo ili waweze kulipwa. Kuna watu kwa sababu zao wenyewe na nilielekeza wachukuliwe hatua, wamekaa na majina hayo kwa muda mrefu bila kupeleka Utumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naelekeza kwa wale wachache ambao walikuwa bado wanafanyiwa uhakiki waharakishe haraka, wale wanaostahili waweze kulipwa na walipwe na malimbikizo yao ili waweze kufanya kazi bila manung’uniko.
MHE. CATHERINE C. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa, malalamiko juu ya Polisi yamekuwa mengi sana. Wamekuwa wakinyanyasa raia kila siku, kila mkoa. Hivi tu majuzi wiki iliyopita nimeshuhudia Polisi anaejulikana kwa jina la Msafiri akimpiga raia hapa Dodoma kwa amri ya bosi wake. Je, nataka kujua hivi hawa Polisi wako juu ya sheria kwa sababu wanapopiga raia wanapokwenda Polisi wenyewe ndiyo wamekuwa wakiandika kesi. Je, haki itatendeka kweli?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, linapotokea tukio la Askari mmoja ama wawili kufanya jambo hilo si jambo la Jeshi la Polisi linakuwa la Askari mhusika, mtu mmoja na sio utaratibu wa Kiutumishi wa Kipolisi. Polisi kama Jeshi la Polisi Waheshimiwa Wabunge wote tunakubaliana kwamba wanafanya kazi nzuri kwa Taifa letu na ndiyo maana usalama upo. Kwa maana hiyo, inapotokea jambo mahsusi kama hilo tuendelee kuwasiliana na Mheshimiwa Mbunge ni mmoja wa pioneers wa mambo ya haki kutendeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utaratibu wetu inapotokea jambo la aina hiyo tuna vitengo ambavyo vinasimamia malalamiko hayo ili haki iweze kutendeka na uzoefu unaonesha haki imekuwa ikitendeka na hata hatua zinachukuliwa katika baadhi ya maeneo na ninyi ni mashahidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Catherine aendelee kusukuma hivyo utaratibu wa haki kutendeka na kwa hilo ambalo amelitaja tutalifuatilia ili haki iweze kutendeka.
MHE. ALLY SALEH ALLY: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kweli hii ni standard answer, hata tungefumba macho tu tungejua kwamba jawabu lingekuwa hili. Ni kawaida swali hili limeulizwa hii mara ya tano tangu mimi kuingia Bungeni na Serikali yenye macho, masikio, yenye pumzi, inasema haijui chochote kinachotokea kule Zanzibar. Hili ni jambo la aibu kwa Serikali.
Mheshimiwa Spika, sasa je, kwa sababu hapa mimi mwenyewe nimeleta ripoti za haki za binadamu na nikawapa baadhi ya Mawaziri hapa kuonesha matendo yanayoonekana Zanzibar. Je, Bunge hili kwanza halioni wakati sasa umefika wa kuunda Tume ya Kibunge kuchunguza mambo yanayotokea Zanzibar? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa sababu wananchi wa Zanzibar sasa hawana imani na vituo vya polisi ambako wamekuwa wakiripoti. Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari kutoa commitment humu ndani Bungeni leo kwamba tukutane Uwanja wa Amani tarehe ambayo yeye anataka, tumletee wananchi ambao wameonewa, wamenyanyaswa, wamepigwa, wamedhalilishwa, tumuoneshe kwamba watu wapo na ushahidi wa hili Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani akiri, mara ngapi nimemwandikia na hata siku moja hajaja Unguja wala Pemba tukafanya naye kazi kuhusu suala hili? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa Mbunge ameshatoa hoja hizo na ameandika, lakini sehemu moja tu anasema Waziri wa Mambo ya Ndani hajaja Unguja ama Pemba. Mimi nimeshafika Unguja na Pemba na…
Mheshimiwa Spika, taratibu za utendaji wa kazi zinafanyika kwa kutumia vikao na baadhi ya Wabunge nilikutana nao, tena Wabunge wa Majimbo mpaka Pemba na Mheshimiwa Khatib ni Mbunge mmojawapo na nilionana naye.
Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba utaratibu wa upokeaji wa malalamiko upo kwa njia zilizo rasmi na hakuna utaratibu wa kuweka parade uwanjani kupokea malalamiko. Kwa sababu vitendo vya aina hiyo ikiwa vimetokea tunapokea malalamiko na kuna taasisi nyingine ambazo zinatakiwa ku-verify kwamba vile vilifanyika.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa sababu Mheshimiwa Mbunge ndiyo tunaanza tu Bunge leo, waelekeze watu wako na mimi nitawaelekeza watu wangu wafike na wafikishe hayo malalamiko, halafu verification zifanyike kujua ukweli wa hicho kinachofanyika.
MHE FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mbali na kujitokeza watu ambao wanawanyanyasa binadamu wenzao kwa kuwapiga lakini kuna baadhi ya watu hususani kule Pemba wanachoma mashamba ya mikarafuu, wanawapiga watu na kuwachomea nyumba. Je, Serikali imechukua hatua gani ya kuwalipa fidia watu waliodhalilishwa kwa matukio kama hayo? Vilevile imewachukulia hatua gani wahalifu hao?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwepo na matatizo ya wananchi kujichukulia sheria mkononi na hili si tu kwenye mikarafuu lakini tumeshuhudia hata kwenye upande wa wakulima na wafugaji. Tamko letu kama Wizara na kama Serikali tunasema hakuna sababu yoyote ile inayotosha kuhalalisha mwananchi kuchukua sheria mkononi dhidi ya mwenzake iwe kwa kudhuru maisha yake ama kwa kudhuru mali zake. Yeyote atakayefanya hivyo tumesema atafika kwenye mkono wa sheria na wale ambao walishafanya hivyo tumesema wachukuliwe hatua ili iwe mfano na kwa wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeelekeza na Waheshimiwa Wabunge nawaomba kwenye hili tukubaliane, ili Serikali ionekane ipo na inatetea wale wanaoonewa tutachukua hatua kali kwa wale wanaofanya vitendo hivi vya kihalifu dhidi ya wenzao. Hii ndiyo itakuwa njia pekee ya kuweza kuhakikisha kwamba wananchi hawajichukulii sheria mkononi kwa sababu duniani kote sheria isipochukua mkondo wake ndipo wananchi huchukua sheria mkononi.
MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Mambo ya Ndani inakabiliwa na upungufu mkubwa wa magari na ninamshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kukiri kwamba wanapungukiwa sana magari, vitendea kazi pamoja na ofisi. Vilevile wana upungufu mkubwa wa rasilimali watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu, siku za karibuni, kwenye upande wa Jeshi la Polisi ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani pamejitiokeza utaratibu ambapo Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wanalitumia Jeshi la Polisi kuwalinda wao binafsi wakati kuna matatizo makubwa ya kiulinzi katika Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu ni hili, nikitoa mifano halisi, katika Mkoa wa Arusha, Mkuu wa Mkoa wa Arusha analindwa na section nzima ya Jeshi la Polisi, ana motorcade, ana ving‟ora asubuhi mpaka usiku. Sasa magari kama mawili au matatu yanamhudumia Mkuu wa Mkoa na section nzima ya Jeshi la Polisi ambayo ina askari tisa na ving‟ora na hata Wakuu wa Wilaya wamejipa utamaduni huo sasa.
Je, ni nini itifaki ya Kitaifa kuhusu ulinzi wa Viongozi kama hata hawa Mawaziri wenyewe hawalindwi na Askari, lakini Wakuu wa Mikoa leo wanajilundikia Askari badala ya Askari kwenda kwenye lindo, ma-OCD wote siku hizi hawafanyi kazi ya ulinzi wanafanya kazi ya kulindana na kufuatana na Wakuu wa Wilaya. Tunaomba Wizara watueleze leo, ni nini sera ya Serikali kuhusu itifaki hii na matumizi mabaya ya Jeshi la Polisi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwenye utendaji wa kazi kwenye ngazi za Mikoa na Wilaya, Mkuu wa Mkoa ni Mwenyekiti wa Ulinzi na Usalama wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya ni Mwenyekiti wa Ulinzi na Usalama wa Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, panapokuwepo na jukumu hasa ambalo linapohusisha shughuli za kiulinzi na nje ya ofisi, ni sahihi Mkuu wa Mkoa ama Mkuu wa Wilaya kuambatana na timu yake kwenda katika eneo husika. Inapotokea Mkuu wa Mkoa anakwenda ofisini kwake ama Mkuu wa Wilaya anakwenda ofisini kwake, maana yake OCD ama RPC ama wengine na wenyewe watakuwa kwenye ofisi zao. (Makofi)
Kwa hiyo, mimi kwa mazingira ambayo nimekuwa nikipewa ni pale ambapo hawa viongozi wanakwenda katika eneo la tukio ambalo linahusisha ulinzi na usalama. Huo ndiyo muogozo kwamba kama wanaelekea katika eneo ambalo linahusisha ulinzi na usalama ni sahihi viongozi hawa kwenda na timu zao kwa sababu ni mambo ya kiusalama na sehemu ya kutolea maelekezo, lakini siyo wakati wa kwenda ofisini on daily routine, unless kama wanafanya hivyo itakuwa maeneo ambayo kila mmoja anaenda kwenye ofisi na ofisi hizo ziko katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, kwa maelekezo haya, ni kwamba viongozi hawa wanapokwenda kwenye majukumu ambayo yanahitaji maelekezo na ni ya kiulinzi na usalama na wao ndio Wenyeviti wa Ulinzi na Usalama itifaki inataka hawa watu wawe na hao viongozi kwa ajili ya maelekezo ya site, lakini wanapoenda kazini na hawa viongozi wengine nao wanaendelea na majukumu yao.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali moja dogo la nyongeza. Kule Musoma nako tumekuwa na tatizo kubwa sana la nyumba za askari na kwa bahati nzuri Serikali iilisikia kilio chetu. Hivi ninavyozungumza ni zaidi ya miaka mitatu sasa kuna jengo kubwa la ghorofa ambalo limejengwa pale Musoma Mjini. Cha kushangaza mpaka leo askari wetu hawajakabidhiwa. Nataka kujua Serikali inasubiri nini kukabidhi jengo hilo ili liweze kusaidia kuondoa ile adha kubwa wanayopata maaskari wetu?
Waheshimiwa Wabunge linapofika suala la maslahi ya askari, robo ya tatu ya Bunge huwa wanasimama kutaka askari wetu wapewe maslahi hayo. Nitakapokuwa nakutana nao nitawaambia kwamba Wabunge huwa wanawasemea ili mnapopita majimboni wawape ushirikiano. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu jengo la Mara, kuna hatua za ukamilishwaji ambazo ndiyo zilikuwa zinafanyika kutoka kwa mkandarasi wetu. Ni moja ya majengo ambayo yapo kwenye hatua za ukamilishwaji na yatakapokuwa yamekamilika yatakabidhiwa ili askari wetu wasipate shida hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwa sababu wengi mlikuwa bado mnafuatilia, nimeshazunguka mikoa yote kasoro mikoa minne na kwa Mheshimiwa Sikudhani nitafika, bado Ruvuma, Njombe, Songwe, Geita pamoja na Singida. Nimetambua ukubwa wa tatizo hili na sisi ndani ya Serikali tunaendelea kuwasiliana kuweza kuhakikisha kwamba tunalibeba kwa ukubwa wake na hivyo tutalifanyia kazi ili kuweza kupatikana jawabu la kudumu linalohusu makazi ya askari wetu ili waweze kuendana na hadhi ya kazi wanazozifanya.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ni miaka saba sasa nikiwa hapa Bungeni swali hili linapoulizwa majibu ni haya haya, hayajawahi kubadilika hata siku moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna changamoto kubwa zaidi kwa hao wenzetu polisi kwa sababu kuwalaza polisi uraiani wakati huohuo ukawatuma kwenda kufanya operesheni ambazo zitapelekea kuwapiga wananchi, ni hatari kwao na kwa familia zao. Ni lini Serikali itafanya mkakati wa makusudi kabisa kuhakikisha kwamba imeleta majibu tofauti na haya ili wananchi wa Rombo waone nyumba za polisi zinajengwa, waone nyumba za askari magereza zinajengwa, badala ya majibu haya ya kisiasa yanatolewa kila mwaka?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niliweke sawa swali la shemeji yangu Mheshimiwa Selasini. Suala la majibu kuwa yanafanana ni kwa sababu kila mwaka pia tunaajiri, kwa hiyo tutatarajia upungufu uendelee kuwepo, hiyo ni mathematically. Suala la jibu kuwa lilelile si kwamba Serikali haifanyi kitu, hivi tunavyoongea ukiangalia Dar es Salaam tu kuna nyumba zaidi ya 300 zinajengwa lakini hazitatosha kwa sababu mwaka jana pia tumeendelea kuajiri na kwa kuwa tunaendelea kuajiri maana yake mahitaji yale yataendelea kuongezeka kadri tunavyoajiri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu iliyopita mmeona imejenga majengo mengi tu tena ya ghorofa, ndiyo mengine kama haya ya Mara ambayo Mheshimiwa Vedastus ameyaongelea. Mwezi uliopita, Mheshimiwa Rais ametoa shilingi bilioni 10 kwa upande wa magereza na ujenzi unaendelea. Kwa maana hiyo ujenzi utaendelea lakini na mahitaji yataendelea kwa sababu tunaendelea kuajiri, hata mwaka huu tunategemea tuendelee kuajiri kwa sababu bado idadi ya askari ambao wanatakiwa haijatosheleza. Kwa maana hiyo tumelipa uzito unaostahili suala hili lakini hatuwezi kuacha kuongeza vijana kwa sababu hakuna nyumba, tutaendelea kuongeza vijana lakini tutaendelea kujenga nyumba ili vijana waweze kupata nyumba hizo.
MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kumuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa idadi ya watu ambao wanapoteza maisha kutokana na ajali za bodaboda basi hata tungekuwa vitani tungekuwa tunapigwa! Kwa hivyo, namuuliza Mheshimiwa Waziri, tuna mikakati gani ya ziada ya kutoa elimu juu ya waendesha pikipiki ili tuzipunguze ajali hizi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; barabara wanayokatisha Wabunge kuingia ndani na kutoka nje ya Bunge sio salama. Tarehe 5 juzi kagongwa Mbunge mwenzetu na kapata majeraha makubwa sana. Je, Serikali inawahakikishiaje Wabunge usalama wa eneo hilo? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kupata concern hiyo. Ni kweli watu karibu 7,000 ni wengi na ajali zaidi ya 31,000 ni nyingi sana. Tunalolifanya, kwanza
tumesemea iwepo elimu kwa kila mkoa na kila wilaya ambazo zinafanywa na department yetu inayoshughulika na masuala ya usafiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili nitoe rai hata kwa Wabunge tunapokuwa na vijana wetu, watambue kwamba vyombo hivyo pamoja na kuwa na matairi mawili lakini ni vyombo vya moto. Wazingatie masharti ya uendeshaji wake kwa sababu kwa kiwango kikubwa kwenye upande wa magari huwa kuna sababu zingine ambazo
zinasababisha ikiwepo na uchakavu wa vyombo, lakini kwa bodaboda ajali nyingi zinasababishwa na kutokuzingatia utaratibu wa uendeshaji ikiwepo kwenda mwendokasi na kuendesha vyombo hivyo kabla ya kuwa wamejifunza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili hapa alilosemea la pili kuhusu kuzingatia masuala ya usalama, tumeshaongea kuweza kuweka utaratibu mahsusi ambao utakuwa unadhibiti. Siku ile walikuwa wamesimamisha magari lakini
yule wa bodaboda akaja akapita moja kwa moja kama ambavyo nimesema wamekuwa na utaratibu huo wa kwenda kasi lakini tumeendelea kutoa elimu na tumesema ianzie hata ngazi za familia waweze kutambua kwamba kwenda kasi kwa vyombo hivyo vya moto pamoja na kuwa
na matairi mawili lakini vinasababisha ajali.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri kwa kuwa wananchi wengi
wamekuwa waoga kwenda kwenye kituo cha polisi hususan wanawake na kwa kuwa maeneo mengi hayana vituo vya polisi hususan vijijini. Je, Serikali iko tayari sasa kugatua madaraka kwa Wenyeviti wa Mitaa, Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji ili waweze kupata matibabu pale wanapopata ajali?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuona uhalisia unaotokea kwenye grass root. Niseme tu tumepokea wazo hilo, itabidi tuongee na wenzetu wa TAMISEMI kwa sababu likiamuliwa kufanyika katika msingi huo kuna vitu ambavyo lazima tujiridhishe navyo na aina ya maumivu ambayo yanaweza yakatumika kwenye ngazi ya viongozi wetu wa Serikali za Vijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kitu ambacho huwa tunakiepusha na kulazimisha ipitie polisi hasa ni kwa wale ambao wanaweza wakafanya makosa makubwa kwa mfano, mtu aliyeenda kuiba akawa amejeruhiwa angetamani sana asipitie polisi aende moja kwa moja hospitalini. Kwa hiyo, huwa tunaona apitie polisi na wale
wengi wanaokwepa kupitia polisi tunakuwa tunajua watakuwa wana vitu wanavyovihofia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa vitu ambavyo
vimefanyika katika ngazi ya familia labda mtu amepata ajali ya kawaida katika ngazi ya familia ama katika eneo na anafahamika, ana kumbukumbu nzuri za kutokuwa na vitendo vya kihalifu ni maeneo ambayo tunaweza tukaongelea tukaenda katika taswira hiyo aliyoisemea Mheshimiwa Mbunge.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali nilikuwa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Kitengo cha Zimamoto kikiwa kipo kwenye Mamlaka za Halmashauri za
Miji na Manispaa, Manispaa ya Moshi ilikuwa ina uwezo wa kuhudumia magari makubwa mawili na gari moja dogo ambalo tuliazima kutoka Japan. Tangu magari yale yachukuliwe na Kitengo cha Zimamoto Mkoa wa Kilimanjaro, leo tunahudumia gari moja tena tunahudumia kwa taabu na hicho kigari kimoja tulichokiomba Japan ndicho kinachofanywa kama ndiyo gari wanalotembelea Maafisa wa Zimamoto.
Je, Serikali imetumia kigezo gani kuonesha kwamba ufanisi umeongezeka baada ya kuhamisha kitengo hiki
kwenye Wizara ya Mambo ya Ndani tofauti na kilivyokuwa Halmashauri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naomba kama Serikali haioni kwamba kuna haja sasa ya kusaidia Mkoa wa
Kilimanjaro kwa kuazima gari moja ya zimamoto kutoka KIA kwa sababu KIA wanaonekana wana magari ya ziada ili iweze kusaidiana na gari lililopo sasa hivi Mkoa wa Kilimanjaro ili kutoa huduma ya zimamoto kwa watu wa Mkoa wa Kilimanjaro? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wa jambo hili. Niseme tu kwamba vigezo vilivyotumika kwa sasa, moja tofauti na ilivyokuwa katika ngazi za Halmashauri, sasa hivi vipo dedicated kwa ajili ya masuala haya ya zimamoto na kutokuhudumia gari mbili ni kwa sababu tu gari yenyewe imeenda kwenye uchakavu. Ukipima kwa ujumla wake, ni kwamba ufanisi umeongezeka na utaona kwamba sasa kikosi kipo dedicated kwenye masuala ya zimamoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hili la kuazima gari; gari za zimamoto zipo kwa ajili ya matukio na mara zote
katika maeneo yote panapotokea tukio la moto, gari zilizo karibu za kuzimia moto huwa zinaenda kutumika. Kwa hiyo, hilo hatuna tatizo nalo, lakini tunapanga kuimarisha hasa katika Miji ikiwemo hiyo ya Moshi kwa ajili ya ukubwa wa miji pamoja na uwepo wa uwanja wa ndege.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Kwa kuzingatia umuhimu wa magari ya zimamoto katika Mikoa yetu, lakini mikoa mingi mipya hususan Mkoa wa Songwe unakabiliwa na ukosefu wa magari ya zimamoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kupata kauli ya Serikali kwamba je, Serikali ina mpango gani wa kutuletea
magari ya zimamoto katika Mkoa mpya wa Songwe? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa
ufuatiliaji wake na siyo tu jambo la zimamoto, bali masuala mazima yanayohusu idara zilizopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ikiwemo Makao Makuu ya Polisi katika Mkoa mpya wa Songwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu Songwe ni moja ya mikoa mipya, lakini una bahati ya kuwa karibu na uwanja
wa ndege. Tutaupa kipaumbele kama Mkoa mpya lakini pia kama mahitaji ya Mji ambao upo karibu na Mji wa Tunduma ambao unakua kwa kasi, ambao mara nyingi sana Mheshimiwa Juliana Shonza amekuwa akitetea masuala ya maendeleo ya mkoa huo na miji hiyo.
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi naomba niulize swali moja dogo la nyongeza.
Mkoa wa Kilimanjaro matatizo yake yanafanana kabisa na Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Morogoro unakua
sana na viwanda vipo vingi na vingine vinaendelea kujengwa, lakini Kikosi cha Zimamoto katika Manispaa ya
Morogoro kinafanya kazi nzuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, kutokana na uchakavu wa magari katika Manispaa ya Morogoro, je,
Serikali iko tayari kushirikiana na Manispaa ya Morogoro kupata magari mapya katika Manispaa ya Morogoro?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli alichosema Mheshimiwa Murald na
nimpongeze sana kwamba maeneo ambayo yana viwanda gharama za bima huwa zinakuwa juu sana kama magari ya zimamoto ama huduma za zimamoto zisipokuwa karibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nature ya Mkoa wa Morogoro Serikali iko tayari kushirikiana na Mkoa na Mji wa
Morogoro kuweza kupata magari mapya. Kwenye taratibu hizi tunazoendelea nazo za upatikanaji wa magari mapya,
tutazingatia maombi na ushauri wa Mheshimiwa Mbunge.
MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Issue siyo kujenga ukuta kuzuia mwingiliano kati ya wananchi wanaokwenda hospitali na magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vikao vya RCC Mkoa wa Iringa, makubaliano na Wizara ya Mambo ya Ndani ilikuwa kupatiwa eneo mbadala ili Hospitali ya Mkoa wa Iringa ambayo sasa ni Hospitali ya Rufaa iweze kupanuliwa. Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ilitekeleza agizo la vikao vya RCC, Magereza walipewa eneo mbadala ambalo liko katika eneo la Mlolo na Serikali kuanzia mwaka 1998 na 2000 imelipa fidia kwa wananchi wote waliokuwa wanamiliki eneo lile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali, kama Serikali imeshawalipa wananchi fidia na eneo liko pale kubwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuhamishia matumizi ya Gereza pale, eneo lile ni dogo, Hospitali ya Rufaa inatakiwa iendelezwe na TANROADS waliokuwepo pale wameshaondoka, wamepisha eneo hilo kwa ajili ya eneo la Hospitali. Ni lini Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaondoa Jeshi la Mageraza pale ambapo ni eneo linalowatunza wafungwa pale?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, akubaliane na mimi kwamba Mheshimiwa Mwigulu amekuja Iringa ameona hali halisi…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua, ni lini sasa magereza wataondoa matumizi yao pale na kuachia Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokisema Mheshimiwa Mbunge ni kweli, na sisi kama Wizara tunakubaliana naye kwa asilimia 100 ya mapendekezo yake aliyoyasema. Niweke sawa sawa hivyo, maana yake nilikuwa naona Mheshimiwa Ritta Kabati hapa anajiandaa kusimama; sasa ili alielewe ni kwamba Wizara inaelewa kwamba kati ya hospitali na gereza kinachotakiwa kuondoka pale mjini ni gereza na siyo hospitali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hospitali ile inahitaji upanuzi, Wizara inakubaliana na gereza kuhama pale na kwenda kwenye eneo lingine ambalo na lenyewe liko ndani ya mji lakini pembeni kidogo kilometa kama saba kutoka pale mjini ili kuweza kuwa na nafasi ambayo hata kiusalama itaruhusu mazingira yale kuwa salama zaidi ya kutunza wafungwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, alichojibu Mheshimiwa Naibu Waziri ni kwamba wakati jambo hilo halijafanyika, kuna hatua za mpito ambazo tunazifanya zikiwemo hizo za barabara ile kupitika kwa dharura pamoja na masuala ya ukuta aliyoyasemea. Kadri bajeti inavyoruhusu na taratibu nyingine za ndani ya Wizara ya kutumia nguvu kazi inayoendelea, mpango ni huo huo kuhamisha gereza na kuacha fursa kwa Hospitali ya Mkoa kuweza kuwa na nafasi ya kutosha.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwa ajili ya matatizo ya migogoro ya wafugaji na wakulima, maeneo mengi yanahitaji sasa hivi kuwe na vituo vidogo vya Polisi. Je, Serikali au Wizara inatupa commitment gani kuwa kutakuwa na vituo vya Polisi katika maeneo hayo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa wananchi wamekuwa wakijitolea kujenga vituo vya Polisi kama ilivyokuwa kwa kituo cha Polisi cha Wilaya ya Mbeya ambao wamejenga kwa asilimia karibu zaidi ya 50. Je, Serikali inawaahidi nini wale wananchi wa Mbalizi kuwaunga mkono kuwamalizia kile kituo chao cha Polisi? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpe pole Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete kwa kupatwa na msiba na ndiyo maana hajaweza kuwepo kuuliza swali. Mungu ampe moyo wa ustahimilivu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la nyongeza alilouliza Mheshimiwa Oran; moja kituo cha Mbeya ambacho wameshafanya kazi kubwa sana nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amefanya hamasa kubwa sana na najivunia kwamba nilikwenda kumuunga mkono wakati wa kampeni. Kwa kuwa amefanya kazi kubwa sana na sisi kama Wizara tuna bajeti ambayo tumetenga kwa ajili ya umaliziaji wa majengo ambayo yameshafikia hatua kubwa. Hivyo, tutafanya ziara, tutajionea na tutaweka wataalam ili waweze kukadiria na kwenda kwenye utekelezaji wa umaliziaji ili nguvu ya wananchi isiweze kupotea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi wa vituo karibu na maeneo ambayo yanakuwa na migogoro ya mara kwa mara, Serikali inaendelea kufanya utaratibu wa kuweza kuwepo vituo hivyo lakini pale ambapo vituo hivyo havipo tutaendelea kufanya doria ili kuweza kuhakikisha kwamba tunawahakikishia wananchi usalama wao punde panapokuwepo na migongano ya aina hiyo hata kama bado hatujaweka vituo vya Polisi.
MHE. HAMAD SALIM MAALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya…
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa askari wengi hufanya kazi mbali na walikozaliwa na hulazimika kuwa pamoja na familia zao, je, askari hawa wanapohamishwa na wanachotegemea ni mshahara tu, pamoja na familia zao na mizigo yao, watahamaje kufika maeneo waliyohamishiwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa kila mwaka Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani hupitishwa ikiwa na stahiki zote za askari polisi na sasa hivi askari wengi wamehamishwa, zaidi ya miaka mitatu hawajapata stahiki zao, ni lini Jeshi la Polisi litawalipa askari hao wanaodai stahiki zao za uhamisho?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kuwa na concern na maisha ya askari wetu. Hata hivyo, niseme tu kwamba askari anapohama kuna taratibu za Kijeshi pale alipokuwa anakaa ama pale ilipokuwa familia ipo huruhusiwa kukaa mpaka pale atakapokuwa amepewa fedha za kuhama na kuweza kuhamisha vifaa vyake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uwepo wa madai; katika mwaka wa fedha huu uliokwisha tumetumia zaidi ya bilioni tano kulipa madeni yaliyokuwa ya askari polisi wetu na tumetumia zaidi ya bilioni saba kulipa zilizokuwa stahili za askari wetu wa Magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotokea na kwa nini anaendelea kuona bado wapo wanaodai, ni kwa sababu uhitaji wa kuhama wa askari ni mkubwa kufuatana na mazingira na maeneo ambako anaweza akahitajika tofauti na watumishi wengine wa umma.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali, lakini ni wazi kwamba siku za nyuma kulikuwa na mgogoro kati ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na Bwana Siro kuhusiana na suala hili. Naomba kujua wakati ambapo Polisi walisema hakuna, lakini Mkuu wa Mkoa alikuwa anasema zipo. Je, huu mgogoro umeishia wapi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba hakukuwa na mgogoro wowote kati ya Kamanda wa Kanda Maalum na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa ni viongozi wanaofanya kazi kwa pamoja na mara zote maelekezo ya Kamati ya Ulinzi na Usalama imekuwa ikielekezwa kwenye utekelezaji na shughuli hiyo imeendelea kufanyika na kama nilivyosema Mheshimiwa Waziri Mkuu alishaelekeza na Mikoa yote imeitikia na sisi kama Wizara tunawaelekeza wote wanaokuwa field kuhakikisha kwamba maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu yanafanyiwa kazi bila kupunguza hata nukta.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante nami nataka kujua hapo kwamba kwa kuwa wakati shisha linapigwa marufuku, huku nyuma kuna watu walikuwa wamepewa leseni ya kufanya hiyo biashara kwa sababu ilikuwa inaonekana ni biashara halali. Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu hilo? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala yote yanayohusu afya za Watanzania ni kipaumbele cha Serikali na kwa kuwa ni kipaumbele cha Serikali, jambo la kwanza tunalofanya ni kuokoa maisha ya Watanzania. Wakati tunafanya hivyo, ndiyo maana tunasema tunaliwekea utaratibu mzuri wa Kisheria na hivi tunavyoongea, ukienda kwenye ukurasa wa 15 wa kitabu cha hotuba ya Waziri wa Afya, ameongelea utaratibu ambao utachukuliwa na tayari alishatungia kanuni. Kwa hiyo, inasubiria mashauriano ya mwisho ndani ya Serikali ambayo yanazingatia concern aliyoitoa Mheshimiwa Shangazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Shangazi, n kwa kutambua kwamba hilo jambo lilikuwepo lakini ni lazima tuzingatie afya za Watanzania na tuzingatie utaratibu ambao utaweka utaratibu wa kisheria wa kudumu ili kuweza kuhakikisha kwamba afya za Watanzania zinalindwa. (Makofi)
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi. Swali langu, je, kwa tafiti ambazo zimefanywa nchi nyingi sana, ikiwemo kwa nafasi kubwa nchi za Kiarabu, sigara ina madhara makubwa, mara dufu kuliko hii Shisha na kila siku tunasema ajira, ajira. Biashara ya Shisha ilikuwa inaajiri vijana wengi sana na kweli wamepata matatizo tangu hili zuio.
Swali langu kwa Serikali; je, mlifanya utafiti wa kutosha wa kuona kwamba hii Shisha ina madhara makubwa kuliko sigara? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mariam kwa kutaka kujua kuhusu utafiti wa jambo hili. Nimhakikishie tu kwamba jambo hili lilifanyiwa utafiti na Wizara ya Afya na hivi vitu ambavyo vina vilevi, ubaya wake ni kwamba vijana wetu hawavitumii peke yake, wanachanganya na vitu vingine, kwa hiyo, wanaongeza makali zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira, nimhakikishie Mheshimiwa Mariam kwamba vijana bado wana fursa nyingi sana na nitolee mfano wa kwake yeye mwenyewe, ni mmoja wa vijana wanaofanya vizuri sana kwenye kilimo na yeye ni shahidi na amefanikiwa sana; ni mmoja wa Waheshimiwa Wabunge vijana waliofanikiwa sana kwenye kilimo. Kwa maana hiyo, vijana wengine wanaweza wakaiga mfano ule, wakalima mazao ya biashara. Mheshimiwa Mariam analima ufuta, wao nawakaribisha walime alizeti ama mazao mengine yanayostawi katika mikoa yao ili waweze kufanya biashara iliyo halali isidhuru maisha ya watu wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira ya kudumu, ndiyo maana Mheshimiwa Rais ana mpango wa muda mrefu wa kukuza uchumi kwa kuhakikisha kwamba fedha zote zinatumika vizuri ili kuweza kutengeneza uchumi wa viwanda, uchumi unaojitegemea, uchumi unaotengeneza ajira nyingi ambazo zitakuwa zinaingiza kipato halali kwa vijana na afya za Watanzania.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini majibu aliyonijibu ni too general. Mimi niliulizia suala la Kingulungundwa lakini ametoa takwimu nyingi za Magereza ya Ukonga na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza la nyongeza; nahitaji kufahamu hizi nyumba 320 ambazo Mheshimiwa Waziri amezisema zinajengwa huko Ukonga na maeneo mengine; je, kati ya hizo, Kingulungundwa zinapelekwa nyumba ngapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Gereza lile, kuna shida kubwa ya maji ambayo inasababisha wakati mwingine wafungwa na Askari watumie muda mwingi kabisa kutafuta maji. Kama inavyofahamika, hili ni Gereza maalum kwa Mkoa wa Lindi, limewekwa mbali kidogo na makazi ya wananchi kwa kazi maalum ambayo nadhani Mheshimiwa Waziri anaijua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kupata commitment ya Mheshimiwa Waziri ni lini Serikali itawapatia maji Gereza la Kingulungundwa na jirani zao wa Mjimwema ili kuondoa adha ambayo wanaipata wafungwa na Maafisa wa Gereza lile? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Bobali, Goal Keeper wa Timu ya Bunge ya Wabunge wa Yanga, kama ifuatavyo:- (Makofi)
Moja, suala la nyumba za Ukonga; tulikuwa tunaelezea tu commitment ya Serikali kuhusu nyumba za Askari Magereza kwa maana ya kwamba zinajengwa kule, tunaendeleza ili kutatua tatizo hilo na tunakamilisha nyumba nyingine ambazo ziko katika hatua za mwisho ili Askari waweze kuhamia, hatuzihamishi zile za Ukonga kwenda Gereza lile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upande wa maji,
hata wakati napitisha bajeti, Mheshimiwa Salma Kikwete aliniambia hatashika shilingi, lakini anaomba siku nikipita Lindi niende kwenye Gereza hilo kujionea tatizo hilo la maji. Mheshimiwa Mbunge amelitaja jambo hili, naweka uzito, nitakapozungukia kule, nitahakikisha napita kujionea lakini hoja hiyo tumeshaipokea kama Serikali kuhakikisha kwamba tunaweka kipaumbele kuweza kuhakikisha kwamba suala la maji linaenda sambamba na hilo la barabara ambalo lilikuwepo kwenye swali la msingi. (Makofi)
MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Gereza kuu la Wilaya ya Kibondo pamoja na kuhudumia Watanzania na mahabusu kwa wafungwa, linahudumia vile vile mahabusu na wafungwa kutoka nchi jirani ya Burundi kwa maana ya Wakimbizi kwa wingi sana. Lina upungufu mkubwa sana wa maji na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la UNHCR liliahidi kwamba litasaidia kuleta mradi wa maji kwa Gereza lile na taarifa tulishazitoa mpaka kwa Waziri wa Mambo ya Ndani. Je, Srikali imefikia hatua gani kuwalazimisha sasa wale watu wa UNHCR walete maji katika Gereza hilo la Kibondo? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nampongeza Mheshimiwa Nditiye kwa kufuatilia jambo hili na mara kwa mara tukionana, amekuwa akinikumbushia jambo hili hili. Nimwambie tu kwamba, kati ya wiki hii mpaka wiki ijayo, timu ya Wawakilishi wa Shirika la Wakimbizi Duniani hapa kwetu nchini, pamoja na wadau wanaoshughulikia masuala ya wakimbizi, watazungukia Mkoa wa Kigoma, watazungukia makazi likiwemo Gereza hilo na moja ya ajenda kubwa wanayokwenda kufanya ni kuangalia miundombinu jinsi inavyoweza kusaidia uwepo wa watu wengi katika Makambi pamoja na Magareza kama hilo ambalo amelitaja.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Magereza mengi nchini yanaendeshwa kinyume kabisa na Kanuni Namba 10 ya Umoja wa Mataifa ambayo inazungumzia namna ya kuwahifadhi wafungwa kwamba ni lazima wakidhi vigezo ikiwemo afya, hali ya hewa, joto na nafasi ya kutosha. Magereza mengi nchini likiwemo Gereza la Songea ni mojawapo ya magereza kongwe nchini ambalo lilijengwa tangu mwaka 1948. Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba gereza hili nalo linakidhi vigezo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tangu Rais aseme maneno ka-ta yameleta athari kwa magereza mengi nchini ikiwemo magereza 14 ya Mkoa wa Morogoro ambayo hivi sasa yako kwenye giza tororo. Serikali haioni kama magereza haya kuendelea kuwa na giza ni kinyume kabisa na haki za Umoja wa Kimataifa na pia inasababisha Askari Magereza kushindwa kufanya kazi zao vizuri? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, moja, nimpongeze kwa kuonyesha concern ya msongamano wa wafungwa kwenye magereza na ameuliza Serikali tuna mkakati gani. Moja ya mkakati wa muda mrefu tunaofanya ni wa kuhahakisha kwamba tunajenga magereza hasa kwenye maeneo ambayo ni ya kilimo yawe na ukubwa wa kutosha na magereza ya mijini yawe kwa ajili ya mahabusu ambao wanahitajika kuwa karibu na mahakama kwa ajili ya usikilizaji wa kesi zao. Kwa hawa ambao walishahukumiwa wawe katika magereza ambako kazi ya kuwarekebisha inaweza ikafanyika huku kukiwa na kazi ya uzalishaji inayoendelea katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la umeme kukatwa, jambo hilo lilishashughulikiwa kwa sababu tayari Hazina ilishatoa fedha kwa ajili ya mafungu yetu ya Polisi, Magereza pamoja na maeneo mengine. Mimi niwasisitizie Waheshimiwa Wabunge, nia na maelekezo aliyoyatoa Mheshimiwa Rais yanarekebisha kwa kiwango kikubwa Maafisa Masuuli wanapopewa fedha zilizokuwa zimeelekezwa kwa ajili ya utilities waweze kutumia katika maeneo yale ambayo yalikusudiwa fedha hizo ziweze kutumika. Kwa maana hiyo, badiliko hili linaweza likaathiri katika kipindi ambacho tu madeni yalikuwa yamelimbikizwa lakini itajenga nidhamu ya kudumu ya Maafisa Masuuli kuweza kuelekeza fedha zilipokuwa zimeelekezwa ili kupata jawabu la kudumu la matumizi bora ya fedha zinazotolewa na Serikali. (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafasi ya kuuliza swali fupi la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa magereza mengi nchini yamekuwa chakavu likiwemo Gereza la Kalilamkurukuru lililopo Wilaya ya Tanganyika. Nini mkakati wa Serikali kuimarisha magereza haya kwa kuyafanyia ukarabati sambasamba na nyumba za askari?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Kakoso kwa swali lake zuri la nyongeza. Niseme tu kwamba tuna mikakati ya aina mbili, kwa upande wa nyumba za askari kama nilivyoelezea wakati wa bajeti tunaenda hatua kwa hatua, tuna miradi midogo na mikubwa ambayo tunaitekeleza. Kwenye ukarabati sambasamba na upande wa ujenzi wa nyumba tumekubaliana kutumia bajeti inayotengwa lakini pamoja na nguvukazi tunayoipata kutokana na wajuzi tulionao kwa upande wa askari, lakini wajuzi tulionao kwa wale walioko magerezani ili tuunganishe nguvu zote hizo na bajeti inayopatikana tuweze kufanya marekebisho pamoja na ujenzi wa makazi mapya pamoja na mabweni kwa ajili ya wafungwa.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa kumekuwa na tabia mbaya kwa baadhi ya askari kudhalilisha raia na hata kuwatolea kauli mbaya ikiwemo hata sisi Wabunge tumekuwa tukikutana na kauli mbaya kutoka kwa baadhi ya askari lakini inapokuja kwenye kutetea maslahi yao sisi ndiyo tumekuwa wa kwanza kuwatetea. Je, Serikali inatoa kauli gani? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, moja, askari wetu wa Jeshi la Polisi pamoja na askari wengine ni Watanzania na wanafanya kazi kwa gharama za maisha yao. Kwa hiyo, tuna wajibu wa kutimiza kama Taifa kwa kutambua kwamba askari wanafanya kazi kwa mujibu wa sheria na hakuna haki isiyo na wajibu. Sisi kama Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na taasisi zingine tuna utaratibu wa kuchukua hatua punde inapotokea askari amefanya kazi kinyume na taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna wajibu ambao Watanzania, wananchi kwa ujumla wanatakiwa watimize wanapokuwa wamekutana na askari wetu. Kwa mfano, afadhali sisi ni viongozi, wengi wetu tunatoa uongozi tunapokutana na askari lakini kuna watu wengine ambao hawatoi heshima inayostahili kwa vyombo vyetu vya dola. Sasa vyombo vyetu vya dola vimepitia mafunzo na mimi kama kiongozi wao nisingependa kuona Jeshi la Polisi linafanana na green guard, blue guard au red brigade.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima Watanzania watambue kwamba vyombo vyetu vya dola vina heshima, vinafanya kazi kubwa na vinastahili kupewa heshima kama vyombo vya dola. Ukitaka kupambana na vyombo vya dola wana sehemu ambayo wanaruhusiwa kutumia nguvu wanapoona kile kinachofanywa na raia kinaweza kikahatarisha ama kikaleta athari iliyo kubwa zaidi. Kwa kuwa Waheshimiwa Wabunge tunakutana na watu wetu, tuendelee kuitoa elimu hiyo ili vyombo vya dola katika nchi yetu kama ilivyo katika nchi zingine viweze kupewa heshima vinavyostahili.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya haki za wafungwa zinazovunjwa ni pamoja na makazi duni sambamba na kukosekana kabisa kwa rufaa za hukumu jambo ambalo linafanywa kwa makusudi na baadhi ya maafisa husika na Case Flow Management Committees haziendi kwa wakati. Swali, Serikali ina mkakati gani wa ziada kukamilisha taratibu hizi ili wafungwa wapate haki zao inavyostahili? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Masoud kwa swali hilo. Niseme tu kama nilivyotaja baadhi ya haki, zile nilizotaja ni baadhi tu, lakini kwa upana wake kuna vitu vingine vingi zaidi na kama Serikali tumejipanga na hivi vinahusisha zaidi ya Wizara moja. Utaona Mheshimiwa Rais anapoweka nguvu upande wa mahakama anamaanisha kesi zisikae sana kwa sababu haki ikicheleweshwa inakuwa haki iliyokataliwa, unaona jambo hilo linavyofanyika. Anavyoiwezesha magereza kupata magari ya kubebea mahabusu waweze kupelekwa kusikilizwa kesi zao anawezesha connection kati ya mahakama, magereza pamoja na polisi waweze kufanya kazi hizo ambazo zote hizo zikipunguza mahabusu waliokuwa magerezani automatically inakuwa zimepunguza msongamano kwenye magereza hayo na kuwafanya wapate haki hiyo mojawapo aliyoitaja.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme tu maswali yenu yote mliyouliza yale ambayo yana mlengo wa kiushauri kama Serikali tumepokea na tutaenda kuyafanyia kazi ili kuweza kuleta ustawi katika maeneo haya mliyoyataja.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita Mkoani Dar es Salaam lilitokea tukio la kusikitisha dhidi ya watu wenye ulemavu ambao ni waendesha bajaji ambapo walifanyiwa vitendo vya udhalilishaji pamoja na vitendo vya kinyama, walipigwa sana na baadae kuburuzwa chini. Pamoja na makosa ambayo walidaiwa kuwa nayo lakini approach ambayo ilitumika na askari wetu haikuwa nzuri kabisa. Je, nini kauli ya Serikali kwa hili? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Ikupa kwa kuleta swali hilo na yeye ni Mbunge anayewakilisha kundi hilo, kwa sababu yupo ni-apologize kwa niaba yake awafikishie salamu hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyosema kwamba pamoja na utaratibu kuwepo ama ukiukwaji wa utaratibu, kwa kuzingatia hali yao ni nguvu kubwa imetumika. Serikali tumeshajadiliana na wenzetu wa TAMISEMI, watakutana na Wizara ya TAMISEMI pamoja na wenzao wa ngazi ya Mkoa ili kuweka utaratibu ambao utakuwa una taswira nzuri na kufanya jambo hilo ili lisiweze kujirudia kuweka utaratibu ulio wa kudumu ili liweze kufanya utaratibu huo wa kudumu. Kwa hiyo, tumepokea concern hiyo na linafanyiwa kazi ili jambo la aina hiyo lisijirudie.(Makofi)
MHE. WILFRED M. LWAKATARE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri na kwa niaba ya Serikali, kwamba matukio ya moto ambayo yanatokea katika shule, yamekuwa pia yakitokea katika maeneo mbalimbali yakisababisha maafa makubwa. Lakini tatizo kubwa ambalo limeonekana kuchangia maafa kuwa makubwa ni pale ambapo vikosi vyetu vya Zimamoto vinapofika kwenye eneo la tukio na vikishafika pale magari yanaonekana yanakuja tu, labda kuja kutembea yanakuwa hayana maji na wala hawana vifaa, matokeo yake wakati mwingine wamekuwa wakiambulia kipigo au matusi kutoka kwa wananchi wenye hasira kali.
Je, Serikali inasemaje juu ya hili na wamejipangaje kuliondoa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kunachangamoto nyingi ambazo panatokea maendeleo na zenyewe zinajitokeza. Kwa mfano, miji inapokua majengo yanapojengwa, kuna maeneo mengine yanakuwa hayajatoa provision za magari ya kisasa kuweza kufanya kazi ile ya zimamoto.
Kwa hiyo, sasa hivi tunashirikiana na Wizara zingine zinazohusika ili tuweke provison hizo ambazo zitawezesha wenzetu wa zimamoto waweze kufanya hivyo. Lakini pia hilo jambo alilolisema lilishajitokeza maeneo mengi tumechukua hatua kuweza kuhakikisha kwamba, magari yanakuwa yako standby na vitendea kazi vyote vinavyotakiwa kwa ajili ya kwenda kuzima moto ili wasije wakafika kwanza halafu wakajikuta kwamba walikuwa na upungufu wa vitendeakazi vinavyotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumelizingatia na hata tulivyopitisha kwenye bajeti tulilielezea jinsi ambavyo tunakiunda upya kikosi kile kiweze kuwa na vitendeakazi vinavyostahili kwa ajili ya kukabiliana na matukio ya aina hiyo aliyoyasema. (Makofi)
MHE. USSI SALUM PONDEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri japo hayakidhi ukweli halisi wa mahabusu.
Je, Waziri yuko tayari apewe ushahidi wa raia ambao wanawapelekea chakula raia ambao wanakuwa mahabusu Zanzibar? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili kuhusu haki za binadamu, kila mara kumekuwa na taarifa ya Tume ya Haki za Binadamu juu ya ukosefu wa hali ya amani katika vyuo vya mafunzo Zanzibar. Je, Serikali imeshatolea ufafanuzi kuhusu chombo hicho? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake lakini niseme tu kitu kimoja amekichanganya kwamba, sijakataa watu kupeleka chakula kwa mahabusu na hiyo ni hospitality ya Kitanzania. Mtu kama ana mtu wake yuko mahabusu akaamua kumpelekea chakula, Magereza ama Polisi hawazuii ndugu kuwapelekea ndugu zao chakula wanapokuwa wako mahabusu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, ndugu zao kuwapelekea chakula mahabusu haimaanishi kwamba Serikali haikupeleka chakula. Wakati mwingine hata mahabusu wenyewe wanakuwa na chaguo lao la chakula anachokula, wengine wana diet zao wanazotaka kula, kwa maana hiyo haingekuwa vyema sana kwa Serikali kusema lazima mtu akiwa mahabusu ale chakula cha Serikali na nadhani hata ninyi msingekubaliana na utaratibu wa aina hiyo. Sisi tunachosisitiza ni kwamba Serikali inaweka bajeti na huo ndiyo umekuwa utaratibu lakini haizuii watu kupelekewa chakula kufuatana na mahitaji yao ama ndugu wanapokuwa wamepeleka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu lile la pili la uvunjifu wa amani, tumelisisitiza na tumeendelea kulisisitiza kwamba vyombo vya dola vinafanya kazi kwa mujibu wa sheria na inapotokea kesi moja moja tunazishughulikia kama kesi moja moja na hatua huchukuliwa inapotokea makosa yamejitokeza.
MHE. MOHAMMED JUMA KHATIB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.
Swali la kwanza naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, yeye mwenyewe amekiri hapo kwamba ajali hizi zinasababishwa na uzembe na wahusika kutofuata sheria. Lakini pamoja na kuelewa hivyo bado ajali zinaendelea kutokea na bahati mbaya sana ni kwamba ajali hizi zinawahusu nguvu kazi vijana wadogo sana wa Taifa letu.
Je, Serikali inafikiria njia gani nyingine ya kuwabana hawa kuhakikisha kwamba suala hili halitokei?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali lingine, Mheshimiwa Waziri hamuoni kwamba inawezekana hawa vijana mbali na uzembe wanapata hizi leseni kwa njia ya rushwa? Kwamba wanafanya kazi hii bila ya ujuzi lakini ukiwafuata unakuta kwamba leseni wanazo. Je, Serikali itahakikisha vipi kwamba hawa vijana wote wanapata leseni kwa njia inayostahili?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa concern yake kwa sababu ni kweli jambo hili linagharimu maisha ya vijana wenzetu. Lakini niseme tu njia mbadala ambayo tumekuwa tukisisitiza ni kila familia na kila rika na kila vijiwe vya bodaboda kuchukulia kwamba jambo hili wana wajibu nalo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili si la Serikali peke yake kwa sababu Serikali imeweka taratibu zote hizi. Lakini ambacho huwa kinatokea kwa vijana wenzetu hawa anaweza akawepo mmoja anayemiliki leseni au anayemiliki pikipiki kwa taratibu zote, lakini anavyotoka na anavyokuwa kituoni, wanatokea wengine kirafiki wanapeana unakuta yeye hata mafunzo ya kuendesha bodaboda hiyo amejifunza ziku hiyo hiyo mpaka saa 4 asubuhi na inapofika mchana anabeba abiria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa sababu abiria anayepanda hamuulizi kwanza leseni yako iko wapi yeye anaona tu yuko na chombo mambo haya yanajitokeza. Na ndio maana tunapoona hayo yamejitokeza tunachukua hatua kali. Lakini msisitizo tunaofanya na tunapotoa mafunzo, tunaelekeza kila mmoja atambue kwamba hiki ni chombo cha moto na ukikiuka utaratibu wa matumizi yake una hatari ya kupata majeraha ama kupoteza maisha wewe mwenyewe pamoja na wale uliowabeba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuhusu taratibu za leseni, kwa kiwango kikubwa tunafanya hivo. Sasa hivi kwenye kila Mikoa tumeelekeza taratibu za namna ya kuweza kupunguza hata athari za ajali zinapokuwa zimetokea kwa vijana wetu hawa kwa kuzingatia mahitaji yanayotakiwa katika matumizi ya vyombo hivyo vya moto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nimewaelekeza hata wale viongozi wa vijiwe hivi vya bodaboda kuchukua wajibu wa kiuongozi kuelekezana kwamba hili jambo ni jambo linaloua, lakini vilevile wazingatie matumizi bora ya mahitaji ambayo yanatolewa katika uendeshaji wa vifaa hivo vya moto.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ajali hizi za wanaoendesha vyombo vya moto ni nyingi sana hapa nchini, je, Serikali iko tayari sasa kuhakikisha kila anayehitaji leseni anakuwa na bima ya afya ili waweze kurahisisha matibabu?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa swali la Mheshimiwa Mchemba kwa concern hiyo ya vijana wetu, tumelipokea kama Serikali na tunaendelea kuongea na wenzetu wa Wizara ya Afya. Lakini kubwa si kwa anayehitaji leseni, tunaongelea kwa wale ambao wanafanya ile shughuli yenyewe. Kwa sababu kwenye leseni kuna kuwepo na vitu vya aina mbili, kuna yule anayemiliki na kuna wale wanaoendesha ambao ndio wamekuwa wakipata zaidi ajali kuliko wale wanaomiliki bodaboda zenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na viongozi wa vijiwe hivi tumeendelea kuwaelekeza kwamba wahakikishe katika makundi yale wanatambuana wale wanaohusika na akiongezeka ambaye hayuko kwenye kijiwe chao na hawajui kuhusu leseni zao, nao wachukue wajibu huo kwa sababu kwa kweli ni jambo ambalo linatoa ajira, lakini limekuwa likitugharimu sana maisha ya vijana wetu hawa wanapofanya kazi hizo.
MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, ikiwa Serikali inayaamini haya majibu waliyonipa, swali la kwanza, je, haioni kwamba kuwahamisha Masheikh ambao mnawatuhumu kwa ugaidi kutoka Zanzibar kuja kushitakiwa Bara, ni kuinyang’anya Mahakama ya Zanzibar mamlaka yake? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, ukisoma Tanzania Law Reports ya mwaka 1998, ukurasa wa 48 inayohusu kesi ya Maalim Seif Shariff Hamad akipingana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inasema wazi kwamba iwapo mtu atafanya kosa Zanzibar kwanza anapaswa kushtakiwa Zanzibar, pili anapaswa kushtakiwa na Mahakama ya Zanzibar. Swali linakuja hapa ni sheria ipi iliyotumika kuwahamisha Mashekhe kutoka Zanzibar ambao ni Wazanzibar kuja kushtakiwa katika Mahakama za Bara? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, sipingani na muuliza swali kwenye upande wa vipengele vya kisheria lakini naomba tu nimwambie kwamba kuna makosa ambayo specifically siyo ya kijiografia. Kwa mfano, kama watu watafanya makosa ya kung’oa michikichi Kigoma hilo unaweza ukalitaja kama ni kosa la Kigoma. Kama watu watang’oa mikarafuu Pemba unaweza ukasema kwamba hilo ni kosa lililofanyika Pemba na ni karafuu ya Pemba, lakini yanapofanyika makosa ambayo ni ya nchi nzima, Mtanzania ama raia yeyote awe wa Tanzania ama nje ya Tanzania atachukuliwa na taratibu za kufuata haki/sheria zitafanyika pale ambapo mamlaka inayochukua hatua hizo inaona ndipo panapofaa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, haya ambayo muuliza swali ameuliza yanaendelea kubakia kwa maeneo na makosa ambayo yamefanyika na ni mahsusi katika eneo husika na hicho ndicho kinachofanyika. Hatua zote zitaendelea kujulikana kadiri hatua zinavyochukuliwa na upelelezi unavyofanyika. (Makofi)
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu yenye kutia moyo ya Mheshimiwa Waziri, hivi anafahamu kituo hiki sasa hivi kimefunga huduma zake na wanatoa huduma kwenye jengo la kuazima? Je, ni lini tathmini hii itafanyika ili gharama ijulikane na umuhimu wa kukijenga pia uonekane? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini pia anawahakikishia vipi wananchi wanaotumia kituo hiki umuhimu wa kujengwa na kuweza kukitumia kama walivyozoea? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, mama yangu Asha, kwa kweli kwa kufuatilia sana suala la kituo hiki. Mbali na swali la hapa amekuwa pia akiulizia mara zote anapopata fursa ya kutembelea ofisini ama kwenye shughuli za Kamati.
Mheshimiwa Spika, niseme tu, kwa umuhimu huo na kwa ufuatiliaji wake, jambo hili tumesema lifanyiwe tathmini kwa upekee kwa maana ya Kituo cha Dunga kama kituo peke yake mbali ya vituo vingine kwenye maeneo mengine ambavyo vinafanana kama kituo hicho.
Mheshimiwa Spika, mara tathmini hiyo itakapokuwa imekamilika ambapo tunaamini ni katika kipindi hikihiki, basi utaratibu wa upatikanaji wa fedha utaanza na hapo ndipo tunaposema tunatoa rai hata kwa wadau mbalimbali ili tuweze kufanya kama ni jambo mahsusi kufuatana na mazingira ya pale.
Mheshimiwa Spika, mara ukarabati wake utakapokamilika basi niwahakikishie wananchi kwamba matumizi yake yatarejea katika hali ya kawaida na wataendelea kumpongeza na kumpigia kura Mheshimiwa Mbunge ambaye amelitetea sana jambo hili. (Makofi)
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nina swali moja tu dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, ni muda mrefu hapa Bungeni Serikali imekuwa ikiahidi kukitengeneza Kituo cha Polisi cha Kengeja ambacho ni kibovu, chakavu na cha zamani ambacho mnasema mlirithi kutoka kwa wakoloni lakini mara nyingi hamkitengenezi na kimekuwa kikihatarisha maisha ya askari na baadhi ya wale wanaowekwa pale kwa muda.
Je, ni lini Serikali hasa itaandaa mazingira ya ziada kuhakikisha mnakikarabati kituo hiki ili kuepusha madhara yanayoweza kutokea? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa swali la nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Mjumbe makini wa Kamati inayosimamia Wizara ya Mambo ya Ndani, naye nimhakikishie tu kwamba kikosi chetu kinachosimamia masuala ya ukarabati kitafanyia tathmini pamoja na kituo anachokiongelea.
Mheshimiwa Spika, ni kipaumbele cha Wizara kufanya ukarabati na kukamilisha majengo ya vituo ambavyo vimeshafikia hatua za kuweza kutumika ili vianze kutumika na cha kwake tutaweka umuhimu huo kama alivyohitaji kwenye swali.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.
Kwanza napenda kuishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kusikia kilio cha askari wetu wa Tanzania, wakiwemo askari wa kule Pemba kwa kuwatengea bajeti kwa mwaka 2018/2019 ya kuwajengea nyumba. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imekiri na kukubali na kuweka ahadi kwamba itatenga bajeti hiyo ya kuwajengea askari wa Zanzibar nyumba. Je, Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba bajeti hiyo ikitengwa na nyumba hizo zitakapoanza kujengwa kipaumbele kipewe kwa askari wetu wa Mkoa wa Kusini Pemba? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Faida Bakar, kwa kweli ni balozi wa askari wote hapa nchini kwa kuwasemea vizuri sana kuhusu mahitaji yanayowahusu kwenye mahitaji yao na Waheshimiwa wengine wanaokuwepo kwenye Kamati inayosimamia mambo ya ndani akiwemo Mheshimiwa Masoud.
Mheshimiwa Spika, nakubaliana tutaweka kipaumbele hicho cha askari walioko Pemba na mimi nilishafika kwa kweli mazingira yao ni magumu ya kufanyia kazi kwa kukosa nyumba. (Makofi)
MHE. ZUBEDA H. SAKURU: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, la kwanza, Januari mwaka 2016 Wizara ilitangaza kufanya msako mkali kwa ajili ya kukabiliana na wahamiaji haramu. Jambo la kusikitisha ni kwamba, wimbi la ongezeko la wahamiaji haramu limeendelea na mwezi Mei mwaka huu wa 2017 Mkoani Ruvuma, Wilaya ya Mbinga katika Kata ya Kigonsera, takriban wahamiaji haramu nane walikutwa miili yao imetupwa katika kijiji hicho. Nataka kujua kauli ya Serikali msako huu umeishia wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pili, kumekuwa na changamoto kubwa ya vitendea kazi hasa katika mikoa na ofisi ambazo ziko mipakani. Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba mikoa hii ambayo iko mipakani inapewa vitendea kazi? (Makofi). Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuileta hoja hiyo. Kwa kupitia swali hili niwaelezee tu Waheshimiwa Wabunge kwamba hapa kuna mambo mawili; kwanza, kuna wapitaji haramu na wahamiaji haramu.
Mheshimiwa Spika, hili la wapitaji haramu ndiyo ambalo tumekuwa tukikutana na adha kama hii aliyoisema kwa sababu wanabebwa kwenye malori. Wakishabebwa kwenye malori wana-suffocate, wanakosa hewa, wanakosa chakula na hata wanafikia hatua hiyo wengine kupoteza maisha na kutupwa.
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi pamoja na Magereza wamehangaika sana kwa vigezo tu vya kiubinadamu, mara kwa mara wanawakuta wakiwa wameshatupwa wakiwa hawana nguvu, hata wanawatafutia huduma za kwanza ikiwepo hospitali na kuwapikia chakula.
Mheshimiwa Spika, kubwa tunalofanya, kama tulivyopitisha jana kwenye itifaki ile, tunahangaika namna ya kuanza kukabiliana na hawa watu kuanzia kwenye mipaka wanakotoka, hasa kwa hawa wa upande wa wapitaji haramu, lakini pia na kuwa na sheria zinazowiana.
Mheshimiwa Spika, jambo linalotusumbua kwa sasa ni kwamba sisi tunahangaika kukabiliana nao kwenye nchi yetu, lakini unakuta wameshasaidiwa kupita kuanzia wanakotoka katika hizo nchi nyingine walizopita ikiwemo majirani zetu wa Kenya.
Mheshimiwa Spika, pia baada ya kuwa wamemaliza Tanzania, kwingine wanakokwenda wanakuwa wanapita katika mazingira ambayo katika nchi hizo wanaruhusu. Kwa hiyo, hilo ni moja ya jambo ambalo tunapambana kuhakikisha tunaziba mianya hiyo kwa utaratibu wa kushirikiana, lakini pia na kisheria; sheria zinazowiana.
Mheshimiwa Spika, hili la wahamiaji haramu ambao wamekusudia kuja kwenye nchi yetu, tumetoa rai kwa wananchi wote pamoja na viongozi wa kuanzia ngazi za matawi na vijiji kuhakikisha kwamba wanatoa ushirikiano na wanafichua pale wahamiaji haramu walipo na muda wowote, siyo tu pale ambapo wanaona kuna maslahi yao yameguswa.
Mheshimiwa Spika, tunaongea na wenzetu wa TAMISEMI, tunataka kuangalia uwezekano, ule mfumo uliokuwa unatumika na Chama cha Mapinduzi wa kuwa na Balozi anayeshughulikia nyumba 10, ndiyo uwe utaratibu ambao viongozi wetu wa mitaa, wale wa Serikali za Vijiji wanaounda Serikali za Vijiji, wapatikane kwa kuwakilisha mitaa badala ya sasa hivi ambavyo wanachaguliwa, wanaweza wakatoka mtaa mmoja na wakawakilisha kijiji kizima.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Watanzania wengi ni wakulima, wafugaji na wavuvi. Kwa mantiki hiyo, kisu na panga ni kitendea kazi muhimu na adhimu kwa kukamilisha kazi zao. Kama ni misuse, hata tai inaweza kutoa maisha ya mtu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nini tafsiri sahihi ya neno silaha? Naomba majibu.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, tafsiri ya silaha tunaitafsiri kufuatana na mazingira inapotumika. Kama mtu amebeba fimbo na anachunga, tunaelewa kwamba mazingira ya anakochunga anastahili kuwa na fimbo hiyo. Leo hii kama mtu anaingia Bungeni na amebeba kisu, ile inageuka kuwa silaha ambayo iko katika matumizi ambapo haitakiwi kuwa na huyo mtu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo, kama mtu anaenda kuangalia mpira (Ndondo Cup), hata kama kwenye utamaduni wake anatakiwa kuwa na mkuki, hatutarajii aende nao kwenye uwanja wa michezo, tunatarajia aende nao anakochunga ambako anaweza akakutana labda na wanyama wakali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, hata uholela tunaoungelea kama ambavyo silaha zote zina utaratibu wa maeneo ambapo zinatakiwa kuuzwa, tunatarajia pia hata kwenye matumizi ziwe katika mazingira yanapotakiwa kutumika. Hatuwezi tukaruhusu Watanzania kila mmoja akawa anatembea na silaha popote anapojisikia kuwa nayo kwa sababu udhibiti wake utakuwa ni hatari kwa namna ya kuweza kuhakikisha wale wasiopenda au wasio na silaha wanaweza wakapata athari popote pale ambapo mwenye silaha anaweza akaamua kuitumia. (Makofi)
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa umakini wake, ufuatiliaji wake na utendaji wake na hasa kwa wapiga kura wake vilevile Jimboni kwake ingawa majukumu ni mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza kwa kukiri na hii ni mara ya pili kukiri, katika wakati wa bajeti na leo hii. Nafikira baada ya kupitisha bajeti yake ataniambia labda kesho au kesho kutwa tufuatane. Naomba kumwuliza maswali mawili madogo sana ya nyongeza.
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, zabuni zinafunguliwa na Serikali, iweje leo hii uhakiki ufanyike wakati mradi umeshafanyika na kukamilika karibu miaka mitano? That is (a).
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mhusika amemaliza kazi, kwa nini Serikali isimlipe fedha yake na uhakiki huo ufanyike kwa watendaji waliosimamia tender hizo ili kuwawajibisha? Hii ni sawa sawa na kumchukua kuku aliyechinjwa kisha akaliwa, ushahidi huwezi kuupata. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Jaku kwa kufuatilia masuala yanayohusu wananchi wake. Hili siyo jambo moja ambalo Mheshimiwa Jaku amefanya hivyo, nawaomba na Wabunge wengine tuige mwenendo wake. Panapotokea jambo linalohusu wapiga kura wake, Mheshimiwa Jaku huwa anafuatilia Ofisini, Wizarani na hapa Bungeni. Nampongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba suala la uhakiki ni utaratibu ambao tulijiwekea Serikalini kwa ajili ya; moja, kuwa na uhakika wa madeni ambayo yanatakiwa kulipwa; pili, kuweka kumbukumbu sawa ili kuondokana na ulipaji wa madeni mara mbili. Hii ina faida pia hata kwa anayedai kuweza kuhakikisha kwamba haki yake haipotei. Kwa maana hiyo, kwa sababu ni utaratibu ambao una-cut across kwa wazabuni wote kwa madeni yote ya Serikali na suppliers wengine wote, ni lazima na sisi kama Wizara, ni lazima tufuate taratibu hizo kwa wazabuni wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa taratibu hizo zilishafanyika kama nilivyokwambia, sasa hivi ni suala tu la upatikanaji wa fedha. Sehemu kubwa ilikuwa ni kukubalika kwa deni hilo, kukubalika kwa kazi ambavyo hivyo vyote vimeshafanyika na tunampongeza kwamba amefanya kazi nzuri.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kumekuwa na upungufu wa vituo vya polisi nchini. Pamoja na changamoto hizo, lakini polisi hao wamekuwa na changamoto za kukosa magari na mafuta kwa ajili ya kulinda wananchi wetu kwenye maeneo yetu. Vilevile hivi karibuni polisi wamekuwa wakilalamika kwamba magari hayana mafuta, kwa hiyo, wanashindwa kufanya doria kuzunguka kwenye maeneo korofi kwa ajili ya kuwalinda wananchi wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha sasa polisi hao wanapatiwa mafuta, lakini pia kuongezewa magari kwa ajili ya usalama wa Watanzania? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia jambo la sskari wetu. Niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba katika bajeti hii tuliyopitisha, fedha zilizotengwa kwa ajili ya mafuta, doria pamoja na shughuli nyingine imeongezeka tofauti na iliyokuwa inatoka katika Awamu ya Kwanza ya mwaka wa fedha uliopita. Kwa maana hiyo, tutakuwa tumepunguza kwa kiwango kikubwa ukosefu wa mafuta katika shughuli zetu hizo za doria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 tulipokea magari 77 kwa ajili ya askari wetu na kati ya mwezi huu mpaka mwezi wa saba tunatarajia kupokea magari mengine zaidi ya 200 na tutayagawa katika maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa wa magari kwa ajili ya shughuli za doria ikiwemo Mikoa kama ya Kagera, Kigoma, Katavi pamoja na maeneo mengine ambayo yanahitaji doria na yanahitaji magari yawepo katika maeneo yale ikiwemo kwa ndugu yangu Mheshimiwa Nsanzugwanko na Mheshimiwa Bilago.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo la kutolipa wakandarasi au wazabuni katika sehemu mbalimbali za nchi hasa wale ambao wanatoa huduma kwenye vituo vya polisi limekuwa ni kubwa kwa muda mrefu. Kwa mfano, mkoani Tabora kuna wazabuni wengi ambao wanaidai polisi malimbikizo ya muda mrefu ya huduma wanazotoa na hasa utengenezaji wa magari.
Kwa mfano Tabora yapo malalamiko ya muda mrefu ya mzabuni ambaye anatengeneza magari ya polisi hajalipwa sasa hivi ni zaidi ya miaka mitatu, anadai zaidi ya shilingi milioni 222. Sijui Mheshimiwa Waziri anazo taarifa hizi na kama hana, atasaidiaje mkandarasi huyu ambaye ndiye anatengeneza magari ya polisi pale Tabora Mjini alipwe fedha zake?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazo taarifa anazozisemea Mheshimiwa Mbunge. Nakumbuka nilivyotembelea Mkoa wa Tabora nililetewa jambo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi, ni utaratibu wa Serikali tulioweka wa kuhakiki kwanza madeni yote. Baada ya kuwa tumeshafanya uhakiki, yale madeni ambayo yamehakikiwa ndiyo yanalipwa kukiwa na kumbukumbu sawa za kazi iliyofanyika na fedha zinazodaiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, kwa jambo hili ulilolileta Mheshimiwa Mbunge, mhakikishie mtoa huduma huyo kwamba baada ya uhakiki huo ambao ulishafanyika nitawaelekeza watu wangu waweke kipaumbele katika kulipa madeni hayo ili kutokuwakwamisha wazabuni wetu kuweza kuendelea na shughuli zao na kutoa huduma hizo ambazo wametoa hata huko kwetu.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Serikali ilitoa ahadi ya kujenga Kituo cha Polisi katika bonde la Yaeda Chini na muda umepita sasa na wananchi wanaibiwa mifugo na kutokea mauaji katika lile bonde.
Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi ya kutengeneza Kituo cha Polisi ya Yaeda Chini? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Flatei jambo hili amelileta mara nyingi sana nami nampongeza kwa hamasa ambayo ameifanya Jimboni kwake kuhusu masuala haya ya ulinzi na usalama. Nilimhakikishia kwamba baada ya Bunge hili la Bajeti kuisha nitazungukia maeneo hayo ambayo kuna uhalifu umekuwa ukijitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuahidi kwamba punde tutakapoanza utaratibu wa ujenzi wa vituo hivyo, eneo lake ni moja ya eneo la kipaumbele kufuatana na uhalifu ambao umekuwa ukijitokeza katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kwenye jibu nililojibu la masuala ya magari, Mheshimiwa Flatei pamoja na ndugu yake (pacha yake) Mheshimiwa Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, alikuja jana tu kusemea mambo ya aina hiyo yakihusisha pia na mambo ya magari.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Flatei pamoja na Mheshimiwa Issaay, niwahakikishie kwamba tutawapa kipaumbele kwenye vituo pamoja na upatikanaji wa magari kufuatana na jiografia ya Majimbo yao na Wilaya yao.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, suala la ajali hizi kutokana na jibu la msingi imekuwa ni hatari kubwa na ukiangalia idadi ya watu waliopoteza maisha, waliopata ulemavu na majeruhi ni wengi. Vilevile ajali hizi zinasababisha kuwepo kwa walemavu, wategemezi, wajane na wagane wengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hatua ambazo zinachukuliwa na Wizara na Serikali kuona kwamba ajali zinapungua lakini bado ajali zinaongezeka.
Je, Serikali haioni sababu kubwa ya ajali hizi ni kwamba madereva wa bodaboda hawafuati sheria za barabarani ikiwepo ku-overtake kushoto badala ya kulia? Serikali haioni sababu ya kuendesha masomo au mafunzo maalum kila Wilaya kwa bodaboda wote waweze kuelewa kanuni na sheria za barabarani na hivyo kuweza kupunguza ajali za barabarani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, baadhi ya maaskari barabarani badala ya kuwaelimisha bodaboda wamefanya bodaboda ni vyanzo vya mapato, kila wakiwaona wanakimbizana nao barabarani matokeo yake wao wanakuwa ni kisababishi cha ajali badala ya kupunguza ajali. Serikali inafanya nini na inachukua hatua gani kwa wale maaskari wote ambao wanakimbizana na bodaboda barabarani hajali amebeba abiria au hajabeba abiria ili kupunguza ajali hizi na kuokoa maisha ya Watanzania wanaopoteza maisha? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mbunge kwamba jambo hili linamgusa na ameongea kwa hisia kama mama na kama mwakilishi wa vijana wetu hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu Serikali imefanya jitihada kubwa kama ambavyo nimeelezea, jambo ambalo limesalia ni familia zetu kuanzia ngazi za familia na ngazi za vijiwe, kuliongea jambo hili kama moja ya jambo linalomaliza maisha ya vijana wetu. Kila tunapokaa tuambizane kwamba ukienda mwendo kasi, usipofuata taratibu za uendeshaji wa vifaa hivi vya moto, madhara yake ni kupoteza maisha ya mwendeshaji mwenyewe ama yule aliyebebwa. Kwa hiyo, hili jambo likienea elimu yake itakuwa kubwa kuliko hii tu ambayo mpaka sasa tunaendelea kuifanya ya kutoa semina Wilaya kwa Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu vijana hawa kukimbizwa na askari, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge ukichukulia kwenye sura moja unaweza ukaona kama vijana wanaonewa sana lakini niseme kuna utaratibu ambao unakuwa unakosewa. Moja, vijana wanakuwa wameshapewa leseni lakini inatokea wanapokuwa kule vijiweni wanakabidhiana bodaboda hizi kwa mtu ambaye hana leseni, mtu ambaye hana mafunzo yaani amejaribisha tu akaona pikipiki inatembea naye anabeba abiria, hili ni kosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimewaelekeza viongozi wa vijiwe vile vya bodaboda kwamba na wenyewe watimize majukumu ya kiuongozi kwamba akitokea mwenzao aliyekosea na wenyewe wawe tayari kumwambia unatakiwa uripoti kistaarabu polisi ili uweze kumaliza jambo lako la kisheria. Kama hawatafanya hivyo, polisi itakuwa haina njia nyingine zaidi ya kumtafuta kwa nguvu na kuweza kumkimbiza popote pale ambapo yupo aweze kufikishwa katika mkono wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge tunawapenda sana vijana wetu lakini mapenzi yetu kwa vijana wetu ni kuhakikisha tunaokoa maisha yao. Kwa hiyo, huruma tunayoweza kufanya ni kuhakikisha tunadhibiti jambo hili na hamna njia mbadala zaidi ya kuweza kuhakikisha tunachukua hatua za kisheria kwa yule ambaye anaonekana anakiuka sheria. Kwa wale ambao kwenye vijiwe vyao watatimiza maelekezo haya, tumeelekeza askari wasikimbizane nao bali wamalize kistaarabu mambo ambayo yanahusu sheria.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, napenda niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mashaka, matatizo, huzuni na gharama kubwa za matibabu zinaendelea kuwakabili vijana wetu hawa kutokana na hizi ajali za bodaboda. Je, ni lini Serikali itaongeza usimamizi na udhibiti wa kuhakikisha kwamba helmet na reflector zinavaliwa na vilevile kudhibiti upakianaji wa kimishikaki ambao unasababisha watu wengi zaidi kuumia kwa wakati mmoja? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu maelekezo tulishatoa na tunachukua hatua kwa maswali yote mawili aliyoyauliza. Moja likiwepo hili la kuvaa kofia ngumu, tumeweka hiyo ni sheria na tumeenda mbali zaidi tunataka si tu mwendesha bodaboda tunataka hata abiria naye atimize wajibu huo wa kuvaa kofia ngumu. Pamoja na hilo, hili lingine la ubebaji wa mishikaki kama alivyoita, abiria zaidi ya moja na lenyewe tumeelekeza popote pale yanapotokea lichukuliwe kuwa ni kosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema mwanzo kwamba jambo hili ni vema likaongelewa kwa ngazi ya kijamii na familia kwamba tuendelee kuwaelekeza vijana wetu. Mara nyingi vijana wetu wakielekezwa kwa mkono wa Serikali wanaona kama wanaonewa lakini wakielekezwa kuanzia ngazi ya familia, tunapokaa tuwaambie vijana wetu tunawapenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe niliwahi kuwapa vijana bodaboda kule Jimboni, niliwahi kuwapa wadogo zangu, watoto wa dada zangu lakini jambo la kwanza nililowaambia, niliwaambia nawapa chombo hiki cha moto lakini chombo hiki kinauwa. Wakiambiwa mkono ambao usio wa kisheria ambao ni wa kifamilia linawakaa zaidi kutambua kwamba ukikosea masharti ya uendeshaji ukaenda kasi, ukakosea sheria za uendeshaji barabarani, gharama yake ni kupoteza maisha ya mwendeshaji mwenyewe na abiria aliyebebwa kutoka kwenye hicho chombo.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Jimbo la Ukonga lina kata 13 na kata zote zina bodaboda karibu vijiwe zaidi ya kumi kila kata moja. Ukonga tumechangishana fedha tukajenga Kituo cha Polisi kule Chanika na kingine kinataka kujengwa pale Kata ya Kivule, lakini kwa hali ilivyo sasa, wananchi wa Ukonga na hasa bodaboda nikiwaambia wachangie fedha hawatachangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyozungumza usiku wa kuamkia leo, wanakuja askari zaidi ya 20 wana bodaboda, walikuwa wanakuja na gari wanaificha, halafu wanapiga watu mpaka na marungu, wana-search kwenye wallet, kwenye pochi kila mahali wanaomba fedha. Sasa wanaenda wanakusanya bodaboda zile wanaomba shilingi 10,000 kwa lazima, kama huna zinapakiwa kwenye gari zinapelekwa central.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natakiwa nijue, ili kuleta mahusiano mazuri kati ya vijana wa bodaboda na polisi, Waziri anatoa kauli gani kuhusiana na jambo hili? Hata haya mambo ya mauaji kama watu wana uhasama hawatoi taarifa. Wanawakimbia kwa sababu ukikamatwa na polisi wala hakuulizi leseni, wala hakuelekezi, kama huna pesa unatembea. Naomba Waziri atoe kauli hapa kusaidia vijana wa bodaboda Mkoa wa Dar es Salaam na hasa Jimbo la Ukonga. Ahsante Mwenyekiti.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba maelekezo ya Wizara tuliyotoa ni kwamba kuwa na bodaboda sio kosa na tumeelekeza watu wanaofanya makosa ndiyo wakamatwe. Kuwa tu na bodaboda haitoshi kuwa kosa kwa sababu hilo ni jambo ambalo lipo kisheria. Kwa maana hiyo nimepokea tu hiyo ya nyongeza aliyoisema ambayo yenyewe imekaa kituhuma zaidi nitalifanyia kazi, kama kweli lipo tutachukua hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini maelekezo yetu tumesema kama vijana wamekosea wafikishwe kwenye mkono wa sheria lakini kama hawajakosea waachwe wafanye kazi zao za kujitafutia maisha kwa uhuru na usalama na wala wasikimbie. Nilielekeza nikasema kuna wakati mwingine hata wanaweza wakawamata kwa bahati mbaya na ikafika mpaka vituoni, niliwaambia wasione aibu kumuachia yule ambaye walimkamata kimakosa ambaye alikuwa hausiki.
Nilisema hata wamuombe radhi kwamba wewe si tuliyekuwa tunakutafuta nenda kaendelee na shughuli lakini isiwe kosa kwamba yeyote ambaye ameshakamatwa akifika kituoni basi inakuwa kazi kutoka, tuwatendee haki kufuatana na kosa kama amefanya ama hajafanya.
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii.
Mheshimiwa Spika, kabla sijauliza maswali yangu mawili ya nyongeza naomba nichukue nafasi hii, nilishukuru sana Jeshi la Polisi Wilayani Bukombe kwa kudhibiti uhalifu ambao umekuwa wa mara kwa mara na kwa kutumia kikosi cha Anti-Robbery cha Mkoa kwa kweli wametusaidia kudhibiti uhalifu huu ambao ulikuwa unasumbua sana wananchi.
Mheshimiwa Spika, sasa naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. La kwanza ukweli ni kwamba sisi wa Wilaya ya Bukombe tuna eneo tayari kwa ajili ya kuwapatia polisi waweze kujenga nyumba kwa ajili ya makazi ya askari wetu. Nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri anithibitishie sasa ni lini wataweza kujenga kwa kuwa eneo lipo?
Mheshimiwa Spika, la pili; kwenye Kata ya Namonge pamoja na Bulega wananchi wenyewe wameamua kujenga vituo vidogo vya polisi na wamefika mahali vinahitaji finishing kwa ajili ya kuweka askari. Nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri awaambie wananchi wa Bukombe, je yuko tayari kuwasaidia wananchi ambao wamejotolea kwa kiasi kikubwa sana, aweze kukamilisha vituo vidogo hivyo vya polisi? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii.
Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Doto Biteko kwa jinsi anavyofanya vizuri kazi za kibunge. Amesemea sekta zote ambazo ziko jimboni kwake kwa ufanisi mkubwa sana, na nadhani wananchi wa Bukombe watakuwa wameiona tofauti kati ya Ubunge wa Doto pamoja na ule mwingine ambao ulikuwa ni wa mvua hadi mvua. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nimhakikishie Mheshimiwa Doto Biteko kwamba kwa kuwa kiwanja kimeshapatikana, basi mimi naelekeza wataalam wangu watengeneze ramani zinazoendana na viwango ambavyo tumevisema kama Wizara na kama Makao Makuu ya Jeshi la Polisi ili baada ya fedha kuwa zimepatikana tuweze kuanza utekelezaji wa mradi huo ambao Mheshimwia Mbunge ameuleta.
Mheshimiwa Spika, kuhusu la pili ambalo amelisemea, wadau pamoja na vijana wangu walishafanya kazi hiyo ya kujenga nyumba na zinahitaji ukamilishwaji, nielekeze watuletee makadirio yanayohitajika kwa ajili ya ukamilishwaji ili niweze kuwakabidhi wataalam wangu na watendaji wangu waweze kutafuta kwenye akiba ya bajeti yetu tuliyonayo ili tuweze kukamilisha ili vijana wangu waweze kuhamia. Na nikupongeze Mheshimiwa Doto kwa kuwasemea vijana wangu Jeshi la Polisi kwani polisi wanapofanya kazi vizuri na mimi nakuwa Waziri wa Mambo ya Ndani mzuri na naendelea kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani. (Makofi)
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru. Kwanza awali ya yote niishukuru Serikali sasa hivi amani Kibiti inazidi kuimarika. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu, wananchi wa Kibiti wametenga takribani ekari 15 kwa ajili ya ujenzi wa Polisi Kanda Maalum. Je, ni lini watajenga kituo hicho?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya na kwa kweli amekuwa bega kwa bega kuzileta hoja za wananchi wa Kibiti pamoja na ukanda ule. Nimhakikishie tu, kwa sababu kanda tayari ilishaanza tayari tumeshateua uongozi na uongozi uko kazini kwa hiyo hatua inayofuata ni ujenzi wa jambo hilo na tunalielewa, tunategemea tu kulitekeleza kufuatana na mtiririko wa fedha kwa tutakapokuwa tunapata. (Makofi)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona na ningependa kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, Kahama nyumba za Polisi zina hali mbaya kweli, na nimewahi kuuliza hapa na kumuomba Mheshimiwa Waziri akaniahidi kwamba watatusaidia kukarabatai zile nyumba. Kwanza hazitoshi na zina hali mbaya.
Je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakuja kutusaidia kuweza kukarabati nyumba zile ili anglau polisi nao waweze kuishi katika mazingira mazuri? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Salome kwa kuleta jambo hili. Nilishazungukia Wilaya ya Kahama. Kama tunavyojua Kahama ni moja ya eneo potential sana katika nchi yetu, hata kimakusanyo; kwa hiyo hata vijana wetu wanaokaa kule na wanapokabiliana na changamoto za eneo husika wanatakiwa wawe katika mazingira mazuri. Tunalitambua jambo hilo na kwa sababu limekuwa likiletwa mara kwa mara. Niseme tu kwamba tutalipa kipaumbele, tutalipa uzito ili hadhi za nyumba za askari wetu ziweze kulingana na eneo husika.
MHE. SILAFU J. MAUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninashukuru hayo majibu niliyopewa na Mheshimiwa Waziri, lakini niliuliza swali kwamba kufufuliwa Kambi ya JKT, sikuuliza swali la kwamba mabadiliko ya matumizi ya Kambi ya JKT, la hasha. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa tunajua wazi kwamba kujiunga kwa vijana wetu kwenye JKT ndiko ambako kuna chachu ya kuwawezesha wao kujiunga na Polisi, kujiunga na JWTZ na kadhalika. Sasa je, ni sababu zipi zilizopelekea kutoka JKT na kuwa Kikosi cha Jeshi na kusababisha Mkoa wetu wa Rukwa kukosa Kambi ya Jeshi?
Swali la pili, je, vijana wetu ambao wanauhitaji wa kujiunga na JKT wa Mkoa wa Rukwa kutokana na wingi wao wa kila mwaka kuongezeka ndani ya jamii, je, hawa vijana watanufaika vipi na vikosi hivyo ambavyo vimebadilishwa makambi yao kuwa ni vikosi vya Jeshi au watajengewa Kambi ya Jeshi upande gani? Naomba uniambie katika Mkoa wetu wa Rukwa. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mbunge kwa kuguswa kwake na vijana hasa hasa wa Mkoa wa Rukwa na hoja yake ya kutaka vijana wapate fursa hiyo, lakini nimhakikishie tu ninapojibu maswali yake yote mawili kwa pamoja ni kwamba Kambi la Jeshi kubwa hasa linaloangaliwa ni suala la kibajeti.
Natambua katika nchi nzima vijana wengi hata maeneo ambako kuna Kambi wengi sana wanajitokeza kuomba nafasi hizo, unaweza ukakuta Wilaya ambako wamejitokeza vijana kama 500, idadi inayotakiwa kupatikana labda ni 50 mpaka 60 kwa maana hiyo sisi kama Serikali tunapokea tu hoja ya Mbunge na uhitaji mkubwa huo wa kuona vijana wanataka kujitolea kwenda kujenga Taifa ili tuliangalie kwenye upande wa bajeti kwasababu kwenye upande wa makambi hilo ni jambo rahisi tu ambalo wanaweza wakakaa tu katika Kambi yoyote ile na mafunzo haya yakaendelea kama ambavyo inafanyika katika mikoa mingine.
MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Naibu Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, miundombinu ya vyoo hususan katika Kambi ya Polisi wanaoishi katika eneo la Msambweni Madina ni mibaya sana kiasi ambacho wenyewe wanaita ni SACCOS.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwatengenezea vyoo vyao wakati wanasubiri utaratibu wa kujengewa hizo nyumba?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa askari wale wanatumia maji ambayo Serikali ndio inawalipia, lakini maji hayo hayo utakuta wenyewe hawayatunzi vizuri, utakuta maji yanamwagika na wanayaachia.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawekea mita kama walivyoweza kuwawekea LUKU?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa maswali mawili madogo ya nyongeza. Nikianza na lile la uchakavu, la vyoo, niseme tu kwamba naelekeza wafanye tathmini na nitawaambia watu wangu Wizarani ili tuweze kuangalia namna ambavyo tunaweza kusaidia kwa sababu hilo ni jambo ambalo linahitaji uharaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili la kuhusu maji kumwagika ni suala la miundombinu na ni suala la umakini katika utumiaji wa maji. Tutayaangalia yote pamoja, lakini la msingi sana ambalo linafaa kwa askari wetu ni upatikanaji wa maji wa kila wakati. Tumejaribu kwenye LUKU, maeneo mengi sana tumepata shida sana kwa sababu ya wakati fulani fedha ambazo zinatakiwa zilipie kuchelewa na hivyo kuwafanya askari walipe kwa fedha zao na baadae kuanza kuhangaika kupata fedha za kufidia. Kwa hiyo, tutayaangalia yote kwa pamoja, ili tuweze kuhakikisha kwamba, tunatunza maji ili askari wapate maji kwa kila wakati. (Makofi)
MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, askari wanaoishi uraiani huwa wanapewa shilingi 40,000 kwa ajili ya pango. Shilingi 40,000 hii ni kwa ajili ya room moja, maji, umeme na familia hizi wana watoto.
Je, Serikali haioni umuhimu a kuongeza kiasi hiki cha fedha, ili askari wetu wanaporudi kupumzika nyumbani waweze kupumzika vizuri bila kelele za watoto?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Grace kwa swali alilolileta. Niseme tu jambo alilolisemea ni kilio cha askari na hata nilipozunguka maeneoe mengi nimekutananacho na Mheshimiwa Rais tayari alishatuelekeza tufanye upya uchambuzi wa masuala mengi yanayohusu stahiki za askari pamoja na sheria zinazo-govern utaratibu mzima wa taasisi hizi za majeshi yaliyoko ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani na hiyo ni moja ya kitu ambacho tutakiangalia yakiwepo na mengine ambayo yanashusha morali ya kazi ya askari wetu. (Makofi)
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa pale kwenye Mji wetu wa Musoma tatizo la nyumba za polisi limekuwa ni tatizo kubwa na kwa muda mrefu. Na ninakumbuka kuanzia mwaka 2006 nimekuwa nikipiga kelele hapa Bungeni na bahati nzuri Serikali yetu sikivu ikakubali na ikaanza kujenga pale jengo na kufikia mwaka 2014 likawa limekamilika zaidi ya asilimia 85, lakini cha ajabu Serikali imeshindwa kutoa fedha za kulimalizia, matokeo yake wameanza kuiba milango, masinki na vitu vingine.
Je, Serikali sasa ni lini itatoa fedha ili ujenzi huu uweze kumalizika na wale askari waweze kuihsi vizuri?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru babu yangu Mheshimiwa Veda Mathayo kwa swali lake alilolileta. Nilishafika kwenye jengo hilo analoliongelea na kwa kweli limeshakamilika kwa kiwango kikubwa. Na sisi kama Wizara tunajipanga kuhakikisha kwamba, katika mwaka wa fedha huu fedha zitakazopatikana na ambazo zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya ukamilishaji wa majengo ambayo yameshafikia hatua nzuri, likiwepo hilo pamoja na maeneo mengine yanakamilishwa.
Kwa hiyo, punde fedha zitakapopatikana tutatoa kipaumbele kwa majengo haya ambayo yameshafikia hatua nzuri, ili yaweze kukamilishwa na askari waweze kuhamia. (Makofi)
MHE. MUNIRA MUSTAFA KHATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, asante. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri swali moja dogo tu. Mheshimiwa Waziri nyumba zilizopo ndani ya Mkoa wa Kusini Pemba, hasa Wilaya ya Mkoani ni chakavu sana. Je, Serikali ina mkakati gani kukarabati nyumba hizo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuleta swali hili. Ni kweli, hata mazingira ya kazi tu katika Mkoa wa Pemba ni magumu sana kufuatana na uchache wa nyumba za askari. Jambo hili Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakilipigia sana akiwemo Balozi wa Askari, Mheshimiwa Faida Bakar.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba, kama ambavyo nimesemea katika maeneo mengine ambayo yana hali tete za makazi ya askari, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ambaye nay eye amekuwa akifuatilia sana masuala ya askari, yakiwemo nyumba pamoja na haki zao nyingine yakiwemo madai kwamba, tutatoa kipaumbele kwa ajili ya nyumba hizo kwa sababu, mazingira ya kazi yanakuwa magumu pale askari wanapokosa makazi bora ya kukaa.
MHE. GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa matatizo ya Tarime Mjini yanafanana kabisa na Gereza la Bariadi Mjini, msongamano wa wafungwa. Naomba niulize kuwa Mheshimiwa Waziri alifika katika Gereza la Bariadi Mjini, hali halisi aliiona jinsi ambavyo wamesongamana hawa watu na Gereza hili linatumika kwa Wilaya zote tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba inajenga Gereza ambalo lina hadhi ya Kimkoa? Kwa sababu kesi nyingine zinasababishwa na Jeshi la Polisi kuwabambikizia watu kesi, wakiwemo Madiwani wa Wilaya ya Itilima, Wenyeviti wa Vijiji, Kiongozi Naibu Katibu Mkuu CHADEMA ambaye alishikiliwa takriban siku 12 bila sababu za msingi akiwa na vijana…
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimepokea pendekezo ama ombi la Serikali kuangalia upya mazingira ya Gereza la Bariadi, nami nilifika, kuna mambo ya kufanyia kazi pale na sisi kama Wizara tume-earmark kwamba kuna jambo la kufanyika ukianzia na nafasi yenyewe ya Gereza, lakini pia na ngome/kuta kwa ajili ya Gereza. Kwa hiyo, hilo tumelipokea.
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, sisi ni viongozi. Mimi nimetembelea Magereza, nimeongea na wafungwa na mahabusu. Wale watu ukifika katika mikoa yote nilikotembelea ni mmoja tu ambaye nilipomwuliza kama umefanya kosa ama hukufanya akasema nimefanya. Wengine wote ukiwasikiliza, kama una fursa ya kuwatoa, unaweza ukawatoa dakika hiyo hiyo, wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, nami nimekuja kupeleleza baada ya hapo, napeleleza mmoja mmoja; ukipeleleza mmoja mmoja utakuta makosa aliyofanya ni ya kupindukia. Kwa maana hiyo, tunapokuwa tunasemea kwa ujumla wake kwamba Polisi wanabambika kesi, nadhani tuwaamini kwamba wale ni Watanzania ambao wanafanya kazi kwa kiapo. Kama kuna jambo la mtu mmoja mmoja, hayo ndiyo kama viongozi tuyafanyie kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishie kule Magerezani, chukueni muda Waheshimiwa Wabunge; ninyi ni viongozi, nendeni mkawasikilize. Ukiwasikiliza wote unaweza ukadhania Gereza hilo limeshika malaika, lakini ukifuatilia undani wake utaona mambo mabaya waliyoyafanya katika familia nyingine ambayo wanastahili kwa kweli kuwa katika maeneo hayo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kiukweli majibu ya Mheshimiwa Waziri yapo kiujumla zaidi na inasikitisha kwa sababu tunapokuwa tunatoa maswali yetu tunatarajia mwende sehemu husika kujua uhalisia wa sehemu husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mahabusu waliopo Gereza la Tarime, zaidi ya asilimia 65 ni kesi au makosa ambayo yanatakiwa yapewe dhamana; na kwa kuwa kesi nyingi ni kesi za kisiasa za kubambikwa na nyingine ni kesi za watoto chini ya miaka 15; na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri alikuja Tarime na hakupata muda wa kuingia Gerezani, ningependa sasa leo mtuambie ni lini Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Katiba na Sheria, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mkurugenzi wa Mashtaka watakuja Tarime kuangalia hali halisi ya mahabusu walioko Gereza la Tarime ili waweze kuondoa zile kesi ambazo jana Mheshimiwa Waziri alikiri kwamba nyingine ni za juice, ili Watanzania warudi uraiani na wafanye kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa kuna msongamano mkubwa sana kwenye Gereza la Tarime, capacity yake ilikuwa ni watu 260 wakiwa wamezidi sana. Sasa hivi ni zaidi ya watu 600; na kwa kuwa ukitokea mlipuko wa magonjwa tutapoteza Watanzania wengi waliopo kwenye lile Gereza; na kwa kuwa gereza lile linahudumia Wilaya ya Rorya na Tarime: ni lini sasa Serikali ya Chama cha Mapinduzi mtajenga gereza katika Wilaya ya Rorya, mtajenga Mahakama ya Wilaya kule Rorya ili wale Watanzania wa Rorya waweze kushtakiwa kule na kuhudhuria kesi zao kule ili kuondoa msongamano ambao upo katika Gereza la Tarime?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwape pole timu yangu ya Magereza (Tanzania Prisons) kwa kushindwa jana kwa figisu za Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda zilipocheza na Ndanda. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wizara ya Mambo ya Ndani, Mwanasheria Mkuu na Wizara ya Katiba na Sheria tutalifanyia kazi jambo hilo; huo ni wajibu wetu na tumekuwa tukifanya hivyo. Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria ameshafika Mkoa wa Geita, ameshafika Mkoa wa Mwanza, Mkoa wa Kagera na anakuwa na Ofisi ya DPP na anakuwa pamoja na Wizara ya Mambo ya Ndani. Nikubaliane nalo, hilo tutafanya, ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba wale ambao kwa kweli wanaweza wakapata namna ya kwenda nje waende nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitofautiane na Mheshimiwa Mbunge kwenye takwimu, anasema asilimia 75 ya kesi ni za Wanasiasa. Natofautiana naye kwa sababu amesema asilimia 75 ni za wanasiasa na wakati ule ule ni za watoto. Huwezi ukawa na asilimia 75 ya wanasiasa na watoto. Kwa hiyo, kwenye hilo siyo kweli na kama kuna issue specific ya kesi ya mtu mmoja mmoja, Waheshimiwa Wabunge ninyi ni Viongozi, tusaidiane kupeana taarifa ili tuweze kufanya intervention inayostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kujenga gereza Rorya hata Mheshimiwa Mbunge wa Rorya amelisema mara nyingi na ameongelea matatizo wanayopata wananchi wake. Ni kweli wanapata shida kwa sababu mashahidi wanatakiwa kutoka Rorya na ni gharama hata kwa Serikali kuwatoa watu Wilaya nyingine kwenda kutoa ushahidi katika Wilaya nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo tumelipokea na kama Serikali tunachukua hatua kwa Wilaya zote mpya ambazo zimeanzishwa, ambazo bado hazina huduma hizo za Mahakama pamoja na Magereza, kuhakikisha kwamba tunawapunguzia usumbufu wananchi na sheria iweze kuchukua mkondo wake kwa wakati.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo itakuwa ni mara ya pili nipende tu kusikitika kwamba swali hili tena halijajibiwa na Bunge lililopita mwezi Novemba, swali langu nalo halikujibiwa vizuri sasa sijui nina mkosi gani. Kwa sababu swali la msingi haliendani kabisa na majibu ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na swali langu la kwanza liwe hivi. Naomba Serikali iniambie inatumia mfumo gani wa kuwajibu maswali Wabunge humu ndani, kwa sababu Wabunge wengi wamekuwa wakilalamika maswali hayo hayajibiwi vizuri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, bado niseme namuomba Waziri tena Waziri mwenye dhamana aje Jimbo la Songwe afanye ziara aangalie jinsi ambavyo vijiji vyangu na kata vilivyo scattered ili aone umbali wa kutoka kijiji kimoja kwenda kijiji kingine, karibuni kilometa 20 hapa, ndipo wanaweza kujenga vituo vya polisi. Lakini kunijibu kwamba kipaumbele ni RPC na OCD wala haviingi akilini naomba Mheshimiwa Waziri mwenyewe anijibu.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mulugo; ni kweli anafuatilia sana masuala ya Jimbo lake na hasa haya yanayohusu askari kufuatana na aina ya Wilaya yake na aina ya Jimbo lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwa sababu la msingi na ushauri alioutoa ni kufika kule, nimuahidi baada ya Bunge hili kabla ya Bunge la Bajeti nitazungukia Wilaya yake kule ili nijionee mwenyewe haya anayoyasemea ili tuweze kutengeneza utaratibu ulio mzuri wa kushughulika na jambo hilo alilolielezea.
MHE. USSI SALUM PONDEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Vile vile nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini nina swali moja la nyongeza. Tatizo la samani katika vituo vya Zanzibar, zaidi katika Majimbo ya Chwaka, lakini yako katika Wilaya nyingi za Zanzibar yote. Jimboni kwangu kuna Kituo cha Chumbuni ambacho kinahudumia wilaya mbili, Wilaya ya Magharibi na Wilaya ya Mjini, lakini kituo hiki hakina samani, hakina gari, kinahudumia watu zaidi ya 70,000 na kinavuja.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshalisemea sana suala hili na nimeshaliuliza zaidi ya mara tatu, mara nne na nikaahidiwa kitatengenezwa na huduma zitapatikana, lakini mpaka leo hali iko vile vile. Je, Mheshimiwa Waziri anatuambia nini wananchi wa Chumbuni kuhusu suala letu hili?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa mfuatiliaji sana wa masuala ya jimbo lake na masuala yanayohusu Vituo vya Polisi vilivyoko katika Jimbo lake. Amekuja Mara kadhaa akisemea jambo hilo na tulishatuma wataalam wetu wafanye tathmini ili tuweze kujua namna tunavyoweza kulishughulikia. Kwa kuwa tunaelekea kwenye bajeti niendelee tu kumhakikishia kwamba, punde bajeti inavyoruhusu tutaweka kipaumbele kwenye jambo hilo ambalo amekuwa akilisemea mara kwa mara. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi. Kwa kuwa mwaka 2015 nilipokuwa Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki nilitoa ufadhili wa gari la golisi kwenye Kituo cha Kata ya Maore kwa ajili ya Jimbo la Same Mashariki; nina uhakika Serikali inalifahamu hilo. Kwa kuwa, lile gari sasa halina matairi, linahitaji kufanyiwa maintainance kubwa. Je, Serikali mnatoa ahadi gani leo hapa ili wananchi wa Same Mashariki wasikie?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mhesimiwa Mbunge Anne Kilango Malecela kwa kusaidia kazi za Ofisi ya Polisi katika Jimbo la Same Mashariki kuweza kufanya kazi na wanakukumbuka sana. Nimefika mwenyewe Same nimeona wakikukumbuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Serikali inatambua jitihada alizofanya Mheshimiwa Mbunge na tutaongea na Kamanda wa Polisi wa Mkoa ili tuweze kuona namna ambavyo tunaweza tukaunga mkono jitihada hizo ambazo Mheshimiwa Mbunge ulizifanya. Hata hivyo niendelee kukuomba uendelee kuwakumbuka wananchi wa Same kwani wanakukumbuka sana ili vitu kama vile matairi wasiendelee kuvikosa, waendelee kupata kama ulivyokuwa unafanya.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kituo cha Polisi cha Kingeja, Jimbo la Mtambire ni kibovu, chakavu na kimekaliwa tangu enzi ya ukoloni. Kumekuwa na ahadi ya Serikali karibu miaka 13 kwamba watakijenga kituo kile, lakini dalili hazioneshi kwamba kuna nia njema ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ituambie ina mkakati gani wa ziada kuhakikisha kwamba, Kituo cha Polisi cha Kingeja kinajengwa sambamba na Kituo cha Polisi cha Mkoani hasa ukizingatia kuna vifaa vya Polisi ambavyo tayari vimewekwa katika eneo la Wilaya ya Mkoani ambavyo vinatakiwa viweze kusambazwa. Je, Kituo cha Polisi cha Kingeja…
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nia ya Serikali ni njema na utaona kwamba, wiki moja iliyopita Mheshimiwa Makamu wa Rais alikuwa ziarani kule pamoja na Naibu Waziri. Pia utaona kwamba, wamefanya shughuli kubwa ambayo inahusu ujenzi wa vituo na kazi inaendelea. Kwa hiyo kazi ile inayoendelea itafika pia mpaka Jimboni kwako pamoja na kituo kile ulichokitaja na vituo vingine ambavyo vinahitaji huduma kama hiyo.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa, Kituo cha Polisi Makambako ni kituo cha kiwilaya na kwa sababu Makambako ndipo katikati ya kwenda Songea, Mbeya na Iringa; na kwa sababu, Waziri alituahidi kutupatia kitendea kazi cha gari. Je, ahadi yake ya kutupatia gari iko pale pale ili shughuli za kipolisi pale ziweze kufanyika kwa ufanisi mzuri?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli pana uhitaji mkubwa wa gari katika Kituo cha Makambako. Niendelee kusema tu kwamba, Serikali inaendelea kuweka umuhimu mkubwa wa kukipatia gari kituo kilichopo hapo na punde magari yatakapopatikana tutaweka kipaumbele kile kama ambavyo tuliahidi.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mheshimiwa Waziri mimi nilikuwa very specific kwenye swali langu la msingi, niliuliza ni watu wangapi waliomba fidia na wangapi wamelipwa mpaka sasa hivi. Kwa maelezo yako Mheshimiwa Waziri inaonesha jumla ya vifo na majeruhi ni zaidi ya elfu 14, hiyo ni kwa mwaka 2016 mpaka 2018 na ambao wamelipwa fidia mpaka sasa hivi ni watu 1,583, ni kama asilimia zaidi ya 10 kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kuwa mwaka 2009 Bunge lilipitisha Sheria namba 10 ili kuwalinda waathirika wa ajali hizo. Sasa Mheshimiwa Waziri hawa wenzetu ambao wanaoshughulikia hili suala la bima hawa wenzetu wa TIRA (Tanzania Insurance Regulatory Authority) inaonesha kabisa kuna upungufu. Ambao wamekuwa beneficiary wakubwa wa hii issue ya bima ni hizi kampuni ambazo yanakatisha bima, lakini ajali inapotokea inaonesha kabisa Watanzania wamekuwa ni waathirika wakubwa ambao wameachiwa mzigo mkubwa. Sasa Mheshimiwa Waziri huoni ni wakati muafaka sasa tuanzishe idara maalum ambayo itakuwa inatoa elimu kwa Watanzania pale ajali inapotokea ili wajue hatua stahiki ambazo wanatakiwa kuchukua ili walipwe fidia zao? Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rose Tweve kwa ku-take serious concern ya Watanzania wanaopata matatizo hayo na kutokupata fidia ama kuchelewa kupata fidia. Niseme tu kama Serikali tunapokea wazo lake na kwa sababu tuna wataalam wazo hilo litachambuliwa kitaalam.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe rai kwa Watanzania kuchukua hatua haraka za kufuata taratibu zinazotakiwa badala ya utaratibu ambao maeneo mengi wamekuwa wakifanya panapotokea matatizo ya aina hiyo; kuamua kuchukua sheria mikononi ama kuamua kufanya taratibu za njia za mkato ambazo zinasababisha wao kukosa kile ambacho walitakiwa wapate.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa kuweza kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa hizi ajali za barabarani zinatokana na uzembe wa baadhi ya madereva na baadhi ya madereva kutumia simu wakati wakiwa wanatumia vyombo ya moto. Je, Serikali ina mkakati gani wa kurekebisha Sheria ya Usalama Barabarani ili kuwachukulia hatua kali zaidi hawa madereva ambao wamekuwa wakitumia simu wakati wakitumia vyombo vya moto? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kweli kuna kiwango kikubwa cha ajali zinatokea kutokana na uzembe. Ukiangalia hata kwenye kumbukumbu zaidi takribani ya matukio zaidi ya 1,500 yanatokana na uzembe.
Mheshimiwa Naibu Spika, kile alichokisema cha kurekebisha sheria na kuchukua hatua tunaendelea na utaratibu huo na tunasema tunakokwenda tutaanza hata kutumia taratibu ambazo nchi zingine wanatumia kwa ku- count down dereva ambaye anapatikana sana na makosa aweze kukosa sifa za kuendelea kumiliki leseni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunalifanyia kazi wazo lake na nimpongeze sana kwa kuguswa na jambo hili kwa sababu limekuwa likisababisha hasara sana kwa familia na kwa Taifa. (Makofi)
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo anaifanya. Swali langu ni hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, ajali zinaendelea kutokea kwa wingi, hata hivi sasa hivi ninavyoongea ukipita barabara ya Morogoro – Dodoma kuna ajali nyingi sana, lakini traffic wamegeuka agent wa TRA kazi yao ni kusimamisha magari na kutoza faini. Sasa Mheshimiwa Waziri naomba atoe tamko kuanzia leo hii matrafiki waache kutoza faini wakazane na kutoa elimu kwa kutoa elimu kwa watumia vyombo vya moto na wasafiri ili wajue ni haki gani watapata pindi ajali zinapotokea. (Makofi) Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, moja, sisi kama Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Polisi, kutoza faini ama kukusanya faini si kipaumbele chetu; sisi kipaumbele chetu ni maisha ya Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuwa imepita miaka mingi sana ya kutoa elimu na tunaendelea kuona kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge alisema uzembe bado uko mwingi sana ndipo tunapokwenda kwenye hatua hiyo ya kutoza faini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama Watanzania watazingatia kwamba wamebeba dhamana kubwa ya maisha ya Watanzania na maisha yao wao wenyewe, wakawa waangalifu hili suala la faini litakuwa limeisha, lakini kwa kuwa tunawapenda zaidi na tunapenda zaidi maisha yao ndiyo maana tunakuwa hatuna njia nyingi zaidi ya kuchukua sheria kali ili kuweza kuokoa maisha yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nitoe rai kwa Jeshi la Polisi kuendelea kuwa strictly, kuendelea kuwa wakali punde watu wanapofanya mzaha na huku wakiwa wamebeba abiria ili kuweza kuokoa maisha yanayopotea kutokana na ajali nyingi zinazotokea barabarani. Jambo hili ninalolisemea ni kwa vyombo vya moto vyote, ukianzia magari ambayo si ya abiria pamoja na bodaboda.
Mheshimiwa Naibu Spika, nalisisitiza sana hili kwa sababu tumeshuhudia vifo vikiwa vimetokea na pale tunapokwenda kwenye kuokoa miili tunakuta watu walikuwa tayari walishaandikiwa faini ikiwa ni kwamba wameambiwa kwamba wanakwenda mwendo kasi. Hata hivyo, pamoja na faini wanaendelea na mwendo kasi ama na uzembe na baadaye inagharimu maisha ya Watanzania.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuuliza swali. Kwa kuwa kuna upungufu mkubwa wa askari katika baadhi ya sehemu na askari wengi sana kwa maana ya traffic wako barabaran, je, Serikali sasa haioni imefikia wakati wa kuweza kupata kamera au teknolojia nyingine badala ya kutumia askari ambao kwa kweli utendaji wao hauna tija. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Mwamoto kwa jambo hilo alilolitoa. Ni kweli kuna uhitaji mkubwa sana wa kuhamia kwenye teknolojia, nchi nyingi zilizoendelea ndio utaratibu unaotumika. Sisi kama Serikali wataalam wanaendelea kufanyia kazi jambo hilo ikiwepo na kufanya upembuzi yakinifu ili kuweza kujua mahitaji pamoja na maeneo ambayo tunaweza tukaanza nayo ili kuweza kupunguza adha inayojitokeza; kwa sababu kwanza tu kukaa kwenye jua kukaa kwenye mvua pamoja na uchache wa askari inasababisha ufanisi kupungua.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, jambo lake hilo tunalifanyia kazi na nimpongeze sana kwa kuleta hoja hiyo makini, lakini nimpe pole tu kwa yeye ni ndugu yangu kwa yale yaliyotokea Jumamosi, yaliyotokea tarehe moja. (Makofi) Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF: Mheshimiwa Naibu wa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Katika jawabu la msingi la Mheshimiwa Waziri amesema Jeshi la Polisi limepewa mamlaka kisheria kutuhumu, kukamata, kuhoji na kuweka watuhumiwa mahabusu kwa muda ulioruhusiwa kisheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, wako watu wengi ambao wanawekwa mahabusu ya polisi kwa zaidi ya siku 15, akiwemo mwanafunzi Abdul Nondo, ambao wanawekwa mahabusu ya polisi kwa zaidi ya siku 15 bila ya kupelekwa mahakamani. Nataka nijue ni sheria gani ambayo inatumika au inatumiwa na polisi kuwaweka watu mahabusu ya polisi kwa muda huo mrefu bila ya kuwapeleka mahakamani? Nataka kujua sheria ni sheria gani. Swali la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ni hatua gani ambayo Mheshimiwa Waziri ataichukua iwapo tutamletea orodha ya watu ambao wamebambikiziwa kesi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama nilivyosema jeshi la polisi linafanya kazi kwa mujibu wa sheria na katika ufanyaji kazi wake kuna hatua mbalimbali za kuchukua ikiwemo kufanya upelelezi, kufanya mahojiano na baadaye mambo yote yale yakikamilika hatua nyingine ndipo huwa zinafuatia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa jambo la usalama ni kipaumbele, usalama wa mtuhumiwa lakini na usalama wa raia wengine wanaosalia, Jeshi la Polisi hutumia wajibu wake lililopewa wa kulinda usalama wa raia kuweza kuhakikisha kwamba linatimiza majukumu yake na huku watu wakiwa salama pamoja na mali zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu jambo la pili, kwa kuwa ni suala la takwimu nitamwomba Mheshimiwa Mbunge niweze kuwasiliana naye kuweza kumpa masuala yale ya takwimu na yeye kama ana orodha kuweza kubadilishana orodha hizo. Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri, ni muda gani kisheria jeshi la polisi linaposhindwa kupeleka ushahidi wa kesi unaopeleka mahakamani naweza kupeleka maombi ya kuondoa mashitaka hayo mahakamani?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu ndugu yangu Khatib wa kutoka kwetu kule kwa mama, kwamba makosa ya jinai hayana ukomo kwa hiyo, inategemea kosa analolisemea ambalo anaweza akasubiria na akaenda kuomba liondolewe ni aina gani ya makosa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo kama makosa ni yale ambayo shitaka lake halina ukomo, basi ni vyema kuacha vyombo vingine ambavyo vinatoa hukumu vikatoa hukumu ndipo yeye akatambua kwamba jambo hilo limeshafika ukomo. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada nzuri zinazofanywa na Jeshi la Polisi pamoja na wadau mbalimbali kuhusu kutoa elimu kuacha imani potofu na mila dhidi ya ukatili unaofanywa kwa watu wenye ualbino.
Je, ni lini Serikali itaanzisha database ili kuwepo na takwimu kwa jinsia na umri ambazo zitasaidia kuhakiki mauaji na ukatili ambao haukuripotiwa? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Leah kwa kulileta swali hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali tunazo taarifa za masuala ya sensa ya watu aliowaongelea, ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi, kwa sababu tuna taratibu za kupata taarifa kufuatana na mfumo wa Kiserikali. Kwa ajili ya mambo ya kiusalama huwa hatupendi kuziweka wazi kwamba huyu yuko wapi na anafanya nini, lakini tunachofanya ni kuimarisha ulinzi kwa ajili ya kuwahakikishia usalama wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitangazie tu Bunge lako Tukufu kwamba katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita hakukuwepo na tukio lolote lililojitokeza linalohusisha kitendo cha kikatili kwa ndugu zetu wenye ulemavu. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kupambana na vitendo vyote vya kikatili likiwemo jambo hili alilolisemea Mheshimiwa Mbunge. Kanzidata hiyo ipo na ilishazinduliwa tayari kama nilivyotangulia kusema. (Makofi)
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Spika, katika majibu ya Mheshimiwa Waziri kuhusu demokrasia, hivi tunavyozungumza wanafunzi wa CHASO wanaohusiana na Chama cha Demokrasia na Maendeleo wanazuiwa kufanya mahafali yao wakati wanafunzi wa Chama cha Mapinduzi wanaruhusiwa na kuna barua za polisi zinazuia mikutano hiyo. Unawezaje kusema tunafanya demokrasia kwa kiwango kikubwa wakati kuna upendeleo wa wazi kabisa? Ni sawa na kwenye ndondi, mmoja amefungwa mikono halafu unasema upigane.
Je, Waziri atakuwa tayari kuliagiza Jeshi la Polisi liache kufanya upendeleo katika kutekeleza majukumu ya ku- practise demokrasia? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, niseme tu mambo mawili, moja, alilosema Mheshimiwa Masoud la mikutano ya hadhara, mikutano hii haijazuiwa ila imewekewa utaratibu na duniani kote standard ya mikutano ya hadhara ni kama hivi tunavyofanya sisi hapa sasa. Tusifanye vitu kimazoea, duniani kote standard ya mikutano ya hadhara ni hivi tunavyofanya sisi, nendeni hata kule tulikojifunza demokrasia ya siasa ya vyama vingi huu ndiyo utaratibu wanaoutumia. Mwaka jana Marekani imefanya uchaguzi, mmemuona Hillary akishukuru? Aliyeshinda ndiye anaendesha Serikali kwa utaratibu wa Kiserikali wa kuendesha taratibu, hili liko wazi duniani kote wala si la kuuliza, ndiyo utaratibu unaotumika. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu mikutano aliyoisemea Mheshimiwa Mchungaji Msigwa, niseme tu taratibu ziko wazi. Kama CCM wamefuata taratibu wakapewa mikutano, chama kingine chochote wanachotakiwa ni kufuata taratibu zilezile waweze kupewa mikutano…

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, hili na lenyewe liko wazi. Kama wengine hawajafuata utaratibu hawatapewa tu kwa sababu CCM walipewa, watapewa kwa kufuata utaratibu. Mheshimiwa Mchungaji Msigwa tumekuwa tukifanya hivyo kote na si sehemu yako tu, mbona kuna sehemu nyingine CHASO haohao wamepewa mikutano? Kwa hiyo kinachotakiwa ni kufuata taratibu za kupewa mikutano hiyo. (Makofi)
Sasa Mheshimiwa Esther, Waziri wa Mambo ya Ndani akiongea unatakiwa unyamaze, nimeshajua kwa nini babu zangu kule Mara wanapiga wake zao. Mtu anapoongea, hasa Waziri ambaye ana Jeshi la Polisi unatakiwa unyamaze kimya umsikilize. (Makofi/Kicheko)
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa niseme kwamba majibu ya Waziri yanaonesha kana kwamba suala la bodaboda limeanza juzi ama jana.
Suala la bodaboda ni la muda mrefu na kero za watu wenye bodaboda zimekuwa ni kubwa kwa wananchi lakini bado Serikali inasema inajipanga kufanya haya na yale wakati bodaboda ni suala la muda mrefu. Ni dhahiri traffic police wameelemewa na usimamizi wa kudhibiti uvunjifu wa Sheria Barabarani kwa waendesha bodaboda. Kwa mfano; bodaboda zina…

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Kwa mfano; Bodaboda zimekuwa zikipita kwenye traffic lights wakati wowote bila kufuata taa. Je, Serikali haioni ni wakati sasa wa kubadili ama kuboresha mikakati yake ili kuimarisha usalama barabarani hususani jinsi ya kusimamia hawa wenye bodaboda?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, nchini Rwanda wenzetu wana utaratibu mzuri wa kusajili madereva wa bodaboda na kusajili vituo ambavyo wanafanyia kazi. Je, ni lini Serikali itasajili hawa vijana wenye bodaboda na maeneo wanayofanyia kazi ili kuweza kubaini watu wanaofanya uhalifu kwa kutumia bodaboda?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali haya yaliyoulizwa nilishayajibu kwenye jibu la msingi. Ninachosema siyo kwamba Serikali inajipanga, ni Serikali imeshachukua hatua hizi na mambo haya yamefanyika kwa mfano, swali la msingi linauliza Dar es Salaam. Pale Dar es Salaam hatua kubwa sana imeshafanywa ya kusajili waendesha pikipiki na haikuishia hivyo tu wamewapa mpaka jezi za kuwatofautisha na mtu mwingine ambaye hakupangiwa katika vituo hivyo. Lakini siyo hilo tu, ukisema tunajipanga ni kama vile pikipiki ni zile zile ambazo zilishasajiliwa. Kama tulishasajili wakija wapya inabidi pia tuendelee kuwasajili ndiyo maana utaona kwamba zoezi hilo linaendelea kuwa endelevu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hii ya waendesha bodaboda kupita kwenye taa, hilo ni jambo la tabia ambalo tumeendelea kuchukua hatua, lakini elimu imeshatolewa na utaratibu ambao wanatakiwa wafuate ulishatolewa, kwa hiyo, tunaendelea kuchukua hatua kwa wale wanaovunja sheria hizo.
MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri yenye kuleta matumaini ya ujenzi wa Vituo vya Polisi na Magereza, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Gereza hili la Kigongoni lina changamoto kubwa ya tatizo la mgogoro wa mpaka wa ardhi kati yake na wananchi wa Sanzare na Matibwa, mgogoro huu umepelekea uvunjifu wa amani mara kadhaa. Je, ni lini Serikali itashirikiana na uongozi wa Wilaya ya Bagamoyo katika utatuzi wa mgogoro huu?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Mkoa wa Pwani ukiachia Wilaya ya Mafia una tatizo kubwa la kutokuwepo kwa Vituo vya Polisi na kwa kuwa kuna hali tete ya usalama katika maeneo hayo ya Wilaya za Mkoa wa Pwani ukiacha Mkuranga, Kibiti na Rufiji. Pia kwa kuwa Wilaya ya Mkuranga imeanza ujenzi wa Kituo cha Polisi kwa ushirikiano wa Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo na wananchi wa Wilaya ile ya Mkuranga. Je, ni lini Serikali itakubali kuisaidia Wilaya hii ya Mkuranga kukamilisha kituo hicho cha Polisi ili kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Mbunge na wananchi wake? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri. Nikianza na la kwanza la mgogoro uliopo kati ya Gereza pamoja na wananchi wa kule Bagamoyo, nikiri ni kweli mgogoro huo upo na Mheshimiwa Mbunge Dkt. Shukuru Kawambwa amekuja mara kadhaa Ofisini na mara nyingine aliongozana na baadhi ya viongozi.
Mheshimiwa Spika, kitu tulichomuahidi ni kwamba baada ya Bunge, ama tukipata fursa baada ya kupigia kura bajeti, tutatembelea eneo husika tukiwa na Timu ya Mkoa ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ili tuweze kujionea wapi na nini chanzo cha mgogoro huo na njia nzuri ya kulimaliza tatizo hilo ili wananchi wake wasipate shida na uwepo wa Gereza hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu kuunga mkono jitihada za Mbunge wa Mkuranga, ni kweli na Mbunge anafanya kazi nzuri sana na sisi kama Serikali ukanda ule tumeupa Mkoa Maalum wa Kipolisi, kwa hiyo Wilaya zote ambazo zinakaa ukanda ule ikiwemo Mkuranga tutazipa umuhimu na upendeleo unaostahili ili tuweze kupata makazi ya Askari, Ofisi za Polisi pamoja na Ofisi za Kanda na kwa pamoja na wingi wa Askari ili kuweza kusaidia shughuli za usalama katika eneo hilo ili wananchi waweze kufanya kazi bila kuwa na hofu yoyote. (Makofi)
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita Mkoani Dar es Salaam lilitokea tukio la kusikitisha dhidi ya watu wenye ulemavu ambao ni waendesha bajaji ambapo walifanyiwa vitendo vya udhalilishaji pamoja na vitendo vya kinyama, walipigwa sana na baadae kuburuzwa chini. Pamoja na makosa ambayo walidaiwa kuwa nayo lakini approach ambayo ilitumika na askari wetu haikuwa nzuri kabisa. Je, nini kauli ya Serikali kwa hili? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Ikupa kwa kuleta swali hilo na yeye ni Mbunge anayewakilisha kundi hilo, kwa sababu yupo ni-apologize kwa niaba yake awafikishie salamu hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyosema kwamba pamoja na utaratibu kuwepo ama ukiukwaji wa utaratibu, kwa kuzingatia hali yao ni nguvu kubwa imetumika. Serikali tumeshajadiliana na wenzetu wa TAMISEMI, watakutana na Wizara ya TAMISEMI pamoja na wenzao wa ngazi ya Mkoa ili kuweka utaratibu ambao utakuwa una taswira nzuri na kufanya jambo hilo ili lisiweze kujirudia kuweka utaratibu ulio wa kudumu ili liweze kufanya utaratibu huo wa kudumu. Kwa hiyo, tumepokea concern hiyo na linafanyiwa kazi ili jambo la aina hiyo lisijirudie. (Makofi)
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Jibu la Serikali limeeleza kwamba kwa muda huu Wilaya ya Malinyi inapata huduma za Kibenki kupitia mawakala wa fahari ambayo ni Malinyi SACCOS na Zidua Shop. Huduma hizi hazitoshelezi kabisa, kwa sababu mawakala hawa wawili wana changamoto kubwa ya mtaji. Je, Serikali kupitia hiyo benki CRDB wanawawezeshaje kwa mikopo isiyokuwa na masharti magumu kuongeza mitaji kwa mawakala hawa wawili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani yupo na maeneo haya ya Malinyi ndio wazalishaji wakubwa wa Mpunga wa Brand inayojulikana ya Kilombero au Ifakara. Wananchi hawa kwa kukosa huduma za kibenki wanalazimika kwenda Mahenge au Ifakara kupata huduma hizi za kuweka na kutoa fedha. Sasa matokeo yake kutembea na fedha nyingi wanahatarisha maisha yao na usalama wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na matukio kwa muda wa miaka mitatu iliyopita zaidi ya matukio kama kumi hivi, ni kwamba kati ya Lupilo, Ilagua na Itete kuna matukio ya ujambazi yanayotokea mara kwa mara wananchi wanapora fedha na kuhatarisha maisha yao. Je, Wizara ya Mambo ya Ndani wanawasaidiaje Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro hususani Wilaya ya Malinyi kukabiliana na ujambazi huo? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Mponda kwa swali lake zuri na anaonekana analielewa vizuri Jimbo lake na ndio maana wananchi wameendelea kumchagua. Niseme tu Wizara ya Mambo ya Ndani kwanza tumejipanga kuwasaidia usafiri watu walioko maeneo yale ambayo yanahitaji doria zinazohitaji kuzunguka mwendo mrefu kama ilivyo kwenye Jimbo lake na Majimbo mengine ya aina hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapokuwa tumeimarisha usalama, tutakuwa tumeweka ushawishi pia kwa taasisi za kifedha kuweza kuweka benki zao huku wakijua kwamba kutakuwepo na usalama wa kuweka benki hizo na fedha zao zitakuwa salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Wilaya hiyo pamoja na Majimbo hayo ni wazalishaji wakubwa, sina mashaka kuhusu upatikanaji wa wateja ambao unaweza ukavutia benki hizo kuweza kuweka matawi yao kwa namna hiyo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutalifanya hilo na mimi binafsi nitatembelea huko ili kuweza kutekeleza haya tunayoyasema. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Waziri, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Katika nchi yetu raia wengi hawana vyeti vya kuzaliwa. Katika Mkoa wa Mara lipo kabila la jamii ya Waluo kwa maana ya Wajaluo. Kwa kuwa wao ni wengi, wengi wao wanaishi Kenya na inaonekana kwamba, zipo hisia tu kila Mjaluo anayeonekana Tanzania hapa anakuwa kama mhamiaji. Ni lini sasa hawa Wajaluo ambao ni raia wa Tanzania wanaoishi mpakani na hasa kwenye vijiji nilivyovitaja, ni lini watapewa haki yao ya msingi kama raia kuliko kusumbuliwa kila siku kuonekana kama wahamiaji wakati wao ni wa karibu hapa wanaishi maeneo ya Rorya?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; hivi mtu akiwa mlowezi, ni lini ulowezi wake unakoma? (Kicheko)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana babu yangu, Mheshimiwa Getere, kwa maswali mawili mazuri sana. Moja, hili alilosema la Wajaluo, si Wajaluo tu watu ambao wana makabila yanayoingiliana na nchi za jirani kupata misukosuko ya aina hiyo, yapo matatizo haya Mikoa yote ya pembezoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimwambie tu kuhusu lini hilo litakwisha ni kwamba, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani, kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa wako katika hatua za mwisho za kufanya utambuzi na badaye kuwapatia vitambulisho wananchi wote wa Tanzania. Kwa hiyo, pale watakapokuwa wameshapata vitambulisho hapatakuwepo na mtu tena kuhisiwa hisiwa kwa ajili ya makabila kuwa yana mwingiliano katika nchi za jirani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu walowezi na lenyewe liko karibu sana na hili nililolisema. Kuna taratibu za walowezi, watu waliolowea hapa kupewa uraia wao. Kwa hiyo, kwa wale ambao watakidhi vigezo na wakapewa uraia watapewa vitambulisho na hilo litakuwa limekoma la kuwa walowezi na watakuwa Raia wa Tanzania. (Makofi)
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la Bunda la Mheshimiwa Getere, halina tofauti sana katika Jimbo langu la Serengeti katika Vijiji vya Rwamchanga, Masinki, Ring One na maeneo mengine, ambapo kuna jamii ya Wakisii, Wanandi, ambao wamekuwepo kabla ya uhuru. Je, ni lini Serikali itawafanya kuwa raia wa Tanzania? Maana tumeona maeneo mengine wakimbizi…
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimjibu babu yangu Mbunge wa Serengeti kwamba, kwa wale wote ambao wameshakaa tangu enzi ya uhuru na wako Tanzania na wangependa kuwa raia wa Tanzania, pana taratibu. Wafike kwenye Ofisi za Uhamiaji watapewa taratibu za kuhalalisha uraia wao kwa sababu, uraia hatuwapi tu kwa kutamka, lazima wapite kwenye taratibu zile ili kuweza kuweka kumbukumbu sawa kwamba, wameshakuwa raia.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kabla sijauliza swali la nyongeza ningependa nitumie fursa hii kuishukuru sana Serikali ya Zambia kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya ya kuhakikisha kwamba wanatuazima gari yao ya Zimamoto kwa ajili ya kuzima moto kwenye mji wa Tunduma, ninasema mwasalifya sana mwe wantu wa Kuzambia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza; najua kabisa kwamba Tunduma iko mpakani mwa Zambia na Tanzania na shehena kubwa sana ya mizigo inayoshuka kwenye bandari ya Dar es Salaam inapita Tunduma na Tunduma hatuna gari ya Zimamoto. Je, Serikali haioni kwamba inahatarisha maisha ya wana Tunduma lakini pia na mizigo inayopita kwenye mpaka wa Tunduma?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, wananchi wa Tunduma wanaendelea kutoa ada za zimamoto wakati huduma ya zimamoto kwenye Mji wa Tunduma haipo, hatuoni kama huu ni uzulumaji wa wazi kabisa wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa wananchi wa Tunduma kuendelea kutozwa fedha hizi bila kupata huduma ambayo ni muhimu katika maisha yao? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Spika, kwanza alivyotoa shukurani hizi nikapata mashaka sana, maana mipakani kule kuna mwingiliano sana wa uraia na nilipoona sifa nyingi sana zinaenda Zambia nikataka kujua sana babu zake wake wako wapi. (Makofi/Vicheko)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Spika, lakini yote kwa yote ni kheri. Niseme tu kwamba yale aliyoyasema Mheshimiwa Mwakajoka kwa utaratibu wetu, tungekuwa hatuna gari kabisa katika eneo husika ingekuwa ni hatari sana, lakini vitu hivi vya moto huwa vinaharibika, na kama nilivyosema kimeenda matengenezo na baada ya hapo kitarudi.
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu kuwatoza hii ni kwa mujibu wa sheria na sheria za kodi za nchi yetu, si kila kodi inakwenda specific huduma kwa mtu aliyechangia kodi hiyo, na tukifanya hivyo tutakuwa tumekosea kwa sababu kuna maeneo mengine makusanyo ni kidogo.
Kwa hiyo, mimi nitoe rai kwa wananchi wetu waendelee kutoa kodi hizo na hivi tunavyoongea kwenye bajeti iliyopita tumepitisha bajeti ya magari mengine, tunategemea kupata magari mengine kwa ajili ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na huduma hiyo itasambaa katika maeneo mengi zaidi kama ambavyo tumepanga katika malengo yetu. (Makofi)
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa fungu la mafuta katika magari hayo linakuwa ni kidogo, je, ni lini Serikali itaongeza mafuta hayo? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la pili katika Mkoa wangu wa Magharibi ‘A’ mafuta wanapokea kwa siku lita saba au hawapokei kabisa, je, ni lini Serikali itawaongeza mafuta hayo? Ahsante (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia kwa ukaribu sana mazingira ya kazi ya askari wetu na kwa kweli watu wa Bububu hawakukosea na mimi mwenyewe nilishafika Bububu nikaona hali ya uhitaji wa usalama unavyohitajika.
Mheshimiwa Spika, niseme tu katika muhula kwanza, katika mwaka wa fedha uliopita nusu mwaka ya kwanza ukilinganisha na nusu mwaka ya pili utaona kwamba bajeti ya mafuta iliongezeka. Katika bajeti tuliyoipitisha fedha ambazo tulitenga kwa ajili ya mafuta ziliongezeka. Nashukuru wenzetu wa Wizara ya Fedha wamekuwa wakizitoa fedha hizo ambazo zinaenda kwa ajili ya mafuta ili kuweze kuwezesha vijana wetu waweze kufanya doria kikamilifu. Kwa hiyo jambo hilo litafanyiwa kazi tunavyomaliza bajeti ili waweze kupata fedha hizo waweze kufanya doria kikamilifu. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Wakati Mheshimiwa Naibu Waziri anajibu alitueleza kwamba kuna Madawati ya Jinsia 117. Hii inaonesha dhahiri kwamba kuna Wilaya nyingine hazina haya Madawati ya Jinsia. Ni ukweli kabisa kwamba kiwango cha ubakaji kwa maana ya watoto wa kike lakini na ulawiti wa watoto wa kiume kimekuwa kikiongezeka sana na tunajua sheria zipo. Ni kwa nini hawa watu wanaendelea kufanya hivi labda ni kutokana na mianya ambayo ipo kuanzia kwenye Jeshi la Polisi na kwingineko.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua kwa sababu sheria zipo lakini bado vitendo hivi vinaendelea, ni kwa nini sasa Serikali isije na njia mbadala kama tiba kabla ya hili tukio kutokea, kuwafanyia kama counseling hao wanaotenda kwa maana kwenye maeneo husika wazazi au jamii husika ili tuwe na tiba mbadala kabla ya tukio kutokea kwa sababu tunaona haya mambo yanatokea na sheria zipo ni kwa nini msibuni …
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali inafanya njia mbadala nyingi tu na niweke tu kumbukumbu sawa kwamba Madawati ni zaidi ya 417 na kwenye Vituo vya Polisi vyote tumeweka Madawati ya aina hiyo ili kuongeza idadi iwe kubwa zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu njia mbadala, kama Serikali tumeendelea kuongeza jitihada za kutoa elimu licha ya hatua kali tunazozichukua. Ndiyo maana tunaendelea kuwasihi hata viongozi wa kiroho kwenye nyumba za ibada kuendelea kutoa elimu hiyo kwa sababu matukio haya maeneo mengi yanaambatana na imani za kishirikina. Wengine wanaamini wakifanya hivi watapata utajiri, wengine wanakuwa na kesi wanaamini wakifanya hivyo watakuwa wamesafishika kwenye kesi hizo na wengine wanaamini watapona magonjwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, jamii kwa ujumla wake katika maeneo tofauti tofauti tumeona tupanue elimu hasa hasa zikiwepo nyumba hizo za ibada kwa sababu maeneo ambapo nyumba za ibada watu wameshika sana mienendo ya Kimungu matukio haya ya kikatili yamekuwa pungufu zaidi. Kule ambapo kuna imani nyingi za kishirikina ndiko ambapo matukio haya ya ajabu ajabu yamekuwa yakiendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, licha ya kazi hiyo kuwapa viongozi wa kiimani tunaendelea kutoa rai kwa wananchi kutoa taarifa ili sisi kwa upande wa Serikali tuweze kuchukua hatua kali kwa wale watakaobainika wamefanya hivyo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante kwa kuwa hili tatizo la uwepo wa ofisi mmbovu na ambazo hazina hadhi katika maeneo yetu ya Tanzania na zinatutia aibu limekuwepo kwa muda mrefu sasa nini commitment ya Serikali kwamba sasa hizi aibu tunaziondoa lini katika maeneo hayo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa mambo haya pia yanahusu mambo ya uhamiaji na kwa kuwa katika Jimbo la Rorya na Jimbo la Bunda kwenye vijiji vya Tlinati, Jabuzume na Nyaburundu kumekuwepo na hisia za kuwaita watu jamii ya Wanandi, Wakisii na Wajaruo kwamba ni wahamiaji na hasa wakati wa uchaguzi, je, ni lini sasa Serikali katika upande wa uhamiaji watamaliza hii kero ili wananchi waishi huru? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana na nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwani amekuwa mstari wa mbele sana kwenye kufuatilia mambo yanayohusu wananchi wake na mpaka kuna siku aliwahi kunipeleka kufanya mkutano saa mbili usiku, na kwa kweli wananchi wake hawakufanya makosa kumchagua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali hili analolisema kwamba lini Serikali itamaliza tatizo hili; sasa hivi Serikali iko kwenye uandikishaji wa Watanzania kupewa vitambulisho vya uraia na zoezi hili linaendelea mikoa yote, na Mkoa wa Mara ni moja ya mkoa ambao zoezi hilo limefanyaka vizuri sana. Pale ambapo zoezi la upatikanaji wa vitambulisho vya uraia vitakuwa vimepewa kwa kila Mtanzania tutakuwa tumemaliza tatizo la watu kuhisiana kuwa si raia kwa maslahi ya kiuchaguzi kama alivyosema ama kwa kutazamana kwenye sura ama lugha mtu anapoongea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo punde ambapo kila mmoja atakuwa na kitambulisho cha uraia tutakuwa tumelimaliza tatizo hilo na wananchi wake wataendela kukaa kwa usalama. (Makofi)
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nasafi. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Waziri na pamoja na bajeti ambayo wameipanga, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali ambalo limeulizwa la polisi Mazizini linafafana kabisa na suala la Mvomero katika Kituo cha Polisi Turiani. Kituo cha Polisi Turiani kipo katika jengo la mabati na jengo lile lilijengwa tokea enzi ya mkoloni na hadi leo kituo kinatumika. Hata hivyo, wananchi na wadau mbalimbali tumeamua kujenga kituo cha polisi na sasa hivi kimefikia hatua ya lenter na ujenzi huo umefanyika zaidi ya miaka kumi iliyopita. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutembelea Turiani na kuonesha nia yake kuweza kumalizia kituo cha polisi Turiani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba Turiani ni sehemu ya Wilaya ya Mvomero migogoro ya wakulima na wafugaji ni mingi na jitihada kubwa zimefanyika. Je, yuko tayari kutusaidia gari kwa ajili ya Kituo cha Polisi Turiani?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Murad kwa jinsi ambavyo anafuatilia kwa karibu sana masuala ya wananchi wake wa Jimbo la Mvomero. Natambua Jimbo la Mvomero jiografia yake ni ya tofauti sana kwa sababu kuna baadhi ya tarafa ziko ukanda mwingine huku kama unaelekea barabara hii ya kwenda Mikumi na upande mwingine ndiko huko Turiani anakokusemea. Kwa hiyo nianze tu kwa kusema kwamba niko tayari na si mbali kutembea kituo hicho anachokisemea ili kuweza kujionea kazi nzuri ambayo wananchi wameshafanya kwa muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tutaweka kipaumbele kwenye upande wa kuipatia wilaya yake vitendea kazi ikiwemo gari kwa kuzingatia hali halisi ya migogoro ambayo imekuwa ikijitokeza katika Wilaya ya Mvomero pamoja na Kilosa ambayo inahitaji sana vitendea kazi kama hivyo. Kwa hiyo tunazingatia punde tutakapokuwa tumepata magari kwa ajili ya kusaidia vituo vya polisi. (Makofi)
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi. Waswahili wanasema usipoziba ufa utajenga ukuta na usipotibu utazika, swali langu dogo tu, namuuliza Mheshimiwa Waziri. Ni lini Serikali itakusanya mchango wa maafa kwa jengo bovu la Ziwani Polisi la Kilimanjaro pindi maafa hayo au jengo litakapoanguka. Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili limeletwa mara kadhaa. Niseme tu, kwa sababu tuna siku chache kabla hatujakwenda kwenye bajeti yetu tutapa fursa tuongee na Mheshimiwa Mbunge ili tukubaliane kuhusu ni lini kwa sababu swali lake ametaka tumtajie ni lini tutachukua hatua hiyo aliyoisema yeye.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kuniona. Nina swali dogo sana la nyongeza. Swali la msingi linahusu vituo na nilikuwa nikipigia kelele huu mwaka wa tatu au wa nne kuna mjenzi wa kampuni ya Albatina na Mheshimiwa Waziri amekuwa akiahidi sana ndani ya jengo hili muhimu kwa wananchi. Kesho kutwa tarehe mosi mwezi wa Tano Mungu akijalia tunapitisha bajeti; na nilimwambia huyu mzee mpaka leo asubuhi tumezungumza, huyu mzee bado anaumwa anadai ng’ombe kama 30; na amekiri si mara ya kwanza si mara mbili, si mara tatu, kesho kutwa sitakuja kuizuia shilingi Mungu akinijalia. Je, lini atalipwa mjenzi huyu karatasi zake na lini nimlete?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikiri kwamba Mheshimiwa Jaku amelifuatilia sana jambo hili Ofisi na hata kwenye masuala ya anapopata fursa ya kusemea hapa kwenye bajeti. Kama nilivyosema, tutaonana naye ili tuweze kukubaliana, kwa sababu kitu ambacho kimetuchelewesha hapa katikati ilikuwa ni kwamba lazima madeni yote yafanyiwe uhakiki kabla hayajalipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa yalikuwa yanafanyiwa uhakiki, nitaomba Mheshimiwa Jaku aridhie tuwe na kikao mimi pamoja na yeye na watendaji wangu ili tuweze kupata kwanza status ya upande wa uhakiki umefikia hatua gani. Tukishajua kwamba limeshahakikiwa liko tu kwenye hatua za kulipwa tutaweza kulifanyia uharaka kwa sababu kama anavyosema Meshimiwa Jaku mhusika anahitaji sana fedha kwa ajili ya matibabu.
MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa Mkoa wa Ruvuma unapakana na nchi za Msumbiji na Malawi. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza idadi ya magari pamoja na boti kwa polisi ili kudhibiti uhalifu katika sehemu za mipakani?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, hata nilipotembelea Songea Mheshimiwa Mbunge pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma walileta hoja hiyo ya magari. Niseme tu kwamba Serikali tutazingatia maombi hayo punde tutakapopata magari. (Makofi)
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante, good to see you again. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, pamoja na matatizo waliyokuwa nayo polisi kwenye masuala ya vyombo vya usafiri lakini nikuhakikishie Jeshi la Magereza lina hali mbaya sana, siyo tu magari mabovu ni kwamba hawana magari kiasi kwamba wanafikia kupeleka wafungwa ambao wana kesi au rufaa wanawafunga pingu wanawapeleka Mahakamani kwa miguu. Sasa hii ni mbaya sana kwa usalama wao Askari Magereza, lakini pia kwa usalama wa wale watuhumiwa ambao wamefungwa pingu na kutembezwa kwa miguu kwa sababu mathalani mtu anatuhumiwa kwa ujambazi halafu anapita mitaani wale wanaomtuhumu wanamuona, wanaweza wakamvamia na kumshambulia na kuhatarisha maisha ya yule mfungwa. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Sugu kwa kuuliza swali kwa experience na niseme tu kwamba yeye ni mshauri mzuri tutazingatia hilo ili tuweze kuweka mgao upande Jeshi la Magereza ili kuweza kuepuka tahadhari hiyo aliyoisema. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika Mkoa wetu wa Iringa kuna magari ambayo huwa yanaharibika tu kidogo yanawekwa katika vituo lakini tumekuta kuna mlundikano mkubwa sana wa magari mabovu. Ni kwa nini Serikali sasa aidha itengeneze au iyauze haraka sana ili yaweze kusaidia upungufu mkubwa ulipo katika Mkoa wetu wa Iringa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Ritta kwa wazo alilotoa. Niseme tu kama Serikali tunapokea ushauri huo, tutayatengeneza yale yanayotengenezeka na tutafanya utaratibu wa kuyauza yale yasiyoweza kutengenezeka.
Mheshimiwa Spika, kuhusu maoni yako upande wa pikipiki nilishatoa maelekezo kwamba vijana wa bodaboda wanaokamatwa kwa makosa madogo madogo wafanyanyiwe utaratibu wa kuandikisha na kuruhusiwa waendelee na kazi zao ili waweze kulipia kama kuna faini ambazo walitakiwa kulipa kuliko kuzirundika pikipiki hizo na zingine kuweza kuharibika wakati wangeweza kulipia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la mwisho, juzi sikukuona pale Uwanja wa Taifa, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kwenda pale kwa sababu kwa kweli kwa matokeo yale kama Rais asingekuwepo viti visingebaki salama. (Makofi/ Kicheko)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa hawa baadhi ya maaskari wetu ambao wamekuwa wakiwakamata hawa bodaboda wakiwa kwenye mwendo na kuwasababishia ajali ambapo wengine wamepata ulemavu mkubwa na hata kusababisha kifo. Sijui Serikali pale inapokuwa imethibitisha kwamba uzembe ulikuwa ni wa askari na yakatokea madhara kwa muendesha bodaboda, sijui huwa wanakuwa na mpango gani wa kuwapa fidia hawa waendesha bodaboda? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini swali langu la pili, kuna malalamiko mengi ya waendesha bodaboda kwamba mara nyingi wanapokuwa wamekamatwa huwa wanabadilishiwa mashtaka wanapofika kituoni. Sasa kwa kuwa hatuna CCTV camera za kuangalia hasa yule wa bodaboda alikamatwa kwa kosa gani, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba kosa lile alilokamatiwa yule mhusika ndilo analoshtakiwa nalo? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuleta swali hili kwa sababu ni kweli ni jambo ambalo linajitokeza katika baadhi ya maeneo na linaleta malalamiko.
Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba maisha ya vijana wetu yakipotea hayana fidia ya kusema umeweza kufidia maisha. Kwa hiyo, jambo ambalo tunafanya kama Wizara kwa kweli sisi kiutawala tunaelekeza utaratibu wa kiustaarabu wa ukamataji wa vijana hawa ili isisababishe ajali ambazo zinapoteza maisha kwa vijana wetu. Pia, tumeendelea kuwaelezea vijana wetu kwa sababu wamekuwa na uongozi kwenye vituo vyao kuhakikisha kwamba nao wanatoa ushirikiano, kwa wale ambao wamefanya makosa ni haki yao kufika kwenye adhabu ili kuweza kupunguza makosa hayo yanayojitokeza.
Mheshimiwa Spika, kuhusu yale ya kubambika kesi hilo ni kosa la kimaadili na sisi kama Wizara wale wote wanaofanya haya kwa wananchi wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa utaratibu wa ufanyaji kazi wa Jeshi la Polisi.
MHE. ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali moja kuhusiana na bodaboda hapa nchini.
Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mapendekezo ya kuleta mabadiliko ya baadhi ya sheria za usalama barabarani, ikiwepo bodaboda. Kwa sababu, takwimu zinaonesha kwamba vifo vinavyosababishwa na ajali barabarani bodaboda zinaongoza. Chama cha Wabunge kimetoa mapendekezo ya kuleta hapa Bungeni mabadiliko ya sheria hiyo. Ni lini Wizara au Serikali italeta mabadiliko hayo ili yaweze kufanyiwa kazi ili kupunguza hizi ajali za barabarani, hususan, bodaboda?
WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Adadi Rajab kwa swali zuri la nyongeza na yeye ni dictionary yetu kwenye Wizara kwa sababu ana kumbukumbu nzuri ya masuala ya Wizara hii.
Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba jambo hilo analolisemea limeshapita ngazi ya Wizara na liko ngazi ya vikao vya Makatibu Wakuu na baada ya hapo litapitia Baraza na tutaleta Bungeni kwa ajili ya ukamilishwaji wa hatua hiyo anayoiomba Mheshimiwa Mbunge.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mheshimiwa Waziri wakati akijibu hoja zangu za kuhusu fine kwa madereva wa bodaboda alikiri kweli haiwezekani bodaboda anabeba abiria mmoja, anatozwa fine Sh.30,000 wakati basi linalobeba abiria 60 fine ni ile ile Sh.30,000. Tunaomba atuhakikishie katika hayo mabadiliko ya sheria, je, hii sheria ya fine kwa ajili ya madereva bodaboda itakuwepo? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nimempata vizuri mwakilishi na msemaji/mtetezi wa vijana, Mheshimiwa Mlinga. Niseme tu suala la fine sheria yake inapitishwa na Bunge kupitia Finance Bill ambayo itakuja kwenye mapendekezo ya Wizara ya Fedha. Sisi kama Wizara tumependekeza hivyo hivyo kwamba kwa kweli, ni vyema fine ya bodaboda itofautishwe na fine ya mabasi na coaster kwa sababu fine ya bodaboda kuwa sawasawa na ya magari makubwa yanayobeba abiria wengi ndiyo inayosababisha bodaboda nyingi zinarundikana kwenye vituo vya polisi kwa kushindwa kulipia fine zile. Kwa hiyo, tuliona ni vyema ikawa fine inayoweza kulipika ili kuweza kuwa na mantiki ile ya kutoa onyo badala ya kuwa chanzo cha fedha.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ni kweli kwamba kuna tatizo kubwa sana la ajira katika nchi hii hasa kwa vijana na vijana wengi wamejiajiri kupitia njia ya bodaboda na nyingi wamekopeshwa kwa mikataba mbalimbali na watu wenye fedha zao. Ukizunguka katika vituo vya polisi nchi hii, hata hapa Dodoma, bodaboda zimejaa kila mahali.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anakiri kwamba fine ni kubwa kweli kweli, kwa hiyo, kuna kesi nyingi za vijana hawa na wenye bodaboda zao wanawadai fedha. Ni nini kauli ya Serikali na hasa Mheshimiwa Waziri, kuondoa bodaboda katika vituo vya polisi, kwa maana ya kupunguza gharama, ili vijana hawa waendelee kujiajiri na wapunguze kesi ambazo wameshtakiwa na watu wenye bodaboda zao ambao wamefunga nao mikataba? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, sikumpata vizuri babu yangu, Mheshimiwa Mwita, Wanyiramba tulishaondoka siku nyingi Mara, kwa hiyo, lafudhi kidogo imenishinda.
Mheshimiwa Spika, lakini ambacho tunafanya, moja, tunatoa elimu kuweza kuhakikisha kwamba wanafuata taratibu, kwa sababu kwa kweli maisha ya vijana wetu wengi sana yanakatika kutokana na wao kutokuzingatia taratibu za kujifunza maana bodaboda ni vyombo vya moto kama vyombo vingine na vimekuwa vikisababisha sana ajali. Kwa hiyo, tumeweka mkazo sana kwenye kutoa elimu lakini hata wao tumewaelekeza sana kuhakikisha kwamba nao wanaliongelea jambo hili kama moja ya jambo la hatari ambalo linasababisha madhara haya.
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu kupunguza mishtuko hiyo pamoja na bodaboda nyingi kwenye vituo vya polisi, hilo tumeelekeza moja kwenye hili la upande wa fine, lakini la pili tumeelekeza hata kiutawala tu kwamba, kuwe na utaratibu wa kuwaandikisha na kuwaruhusu wawe na hivyo vifaa vyao ili waweze kulipa baada ya muda ambao wataweza kupewa. Nchi nyingine ambazo zimeendelea taratibu zote za mambo ya fine za usalama barabarani wanafanya kuandikisha na kumpa muda mtu aliyekutwa na kosa wa kufanya malipo hayo punde atakapokuwa ameshaanza kufanya kazi na hicho chombo chake.
Mheshimiwa Spika, utaratibu ambao umekuwa unatumika muda huu ni wa kushikilia bodaboda hiyo na kusema mpaka atakapokuwa amelipa ndipo atakapewa. Tumeelekeza tu zile bodaboda ambazo zinatakiwa kutumika kama sehemu ya ushahidi, kwa mfano, kwenye makosa makubwa kama ya madawa ya kulevya, mambo ya uhalifu wa kutumia silaha, hivyo ndivyo ambavyo tunaweza tukashikilia kwa sababu makosa yake kwa kweli haturuhusu yaendelee kufanyika kwa kutumia bodaboda hizo.
MHE. MARTH M. MLATA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa hivi karibuni Serikali imewaondoa madereva wengi ambao ni wazoefu kwa sababu wao ni darasa la saba na kuwaajiri vijana wadogo kwa sababu wao wana-qualify ama kidato cha nne na kuendelea, lakini bila uzoefu na tumeshuhudia sasa ajali zimeanza kuwamaliza viongozi wetu. Serikali haioni sasa hilo ni bomu kubwa sana inatengeneza kwa ajira za vijana ambao hawana uzoefu kwa kuwamaliza watu? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana dada yangu Mheshimiwa Martha Mlata kwa swali nzuri na swali lenye mantiki. Nachoweza kusema tu ni kwamba Idara yetu ya Usalama Barabarani itaendelea kufuatilia masuala ya uzoefu kuhusu uendeshaji wa vyombo hivi vya moto. Hata kwenye swali la msingi tulipotoka kwenye upande wa bodaboda ndivyo vitu ambavyo tumeendelea kuwasisitizia kwamba mtu anajifunza ndani ya robo saa na baada ya hapo anabeba watu watatu kwenye pikipiki yake. Kwa maana hiyo hata upande wa magari tutaendelea kuongea na wenzetu kwa upande wa magari haya ya Serikali ambayo ameyaongelea, waweze kuzingatia suala la uzoefu wa anayeendesha gari hiyo pamoja na mwendo ambao anatakiwa kuendesha gari hiyo.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la wahamiaji haramu kutoka Ethiopia linaongezeka, je, Serikali haioni imefikia wakati wa kulizungumza suala hili kidiplomasia kati ya Tanzania na Ethiopia ili kuweka utaratibu maalum kuepuka kuwaweka magerezani ambapo huligharimu Taifa? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu sahihi aliyoyatoa tangu mwanzo na niwapongeze Waheshimiwa Wabunge kwa kulileta swali hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ijumaa na Jumamosi tulikuwa na vikao vya Jumuiya ya Afrika Mashariki vinavyoshughulikia masuala ya kiusalama ya kisekta na kwenye maazimio tuliyoyapitisha ni pamoja jambo hili kuwa jambo la mipaka yote ya Jumuiya ya Afrika Mashariki tofauti na ilivyo sasa ambako nchi zingine zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwepo Kenya wanapopitia zaidi kwao wao hili jambo halikuwa kama tatizo walikuwa wanapita tu kama mtembeaji mwingine yeyote aliyeko ndani ya nchi husika. Kwa hiyo, kwa sasa tumesema hili ni jambo ambalo tutalioanisha na mambo mengine ambayo yanazuiwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ili hawa watu waweze kuanza kuzuiwa kwenye mipaka ya Kenya na Sudan Kusini tofauti na ilivyo sasa ambapo huwa wanapata kipingamizi wanapofika Tanzania na nchi zingine zote wanakuwa wameshapita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tunalipokea na hilo jambo ambalo amelisemea la kuongea nanchi husika ambao wahamiaji hawa wanatoka ambapo ni Ethiopia, Eritrea pamoja na Somalia. Hiyo tutaifanya kwa kuanzia na Balozi zao zilizopo hapa ili jambo hilo liweze kuongewa pia katika nchi zao.
MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, mwezi wa Kwanza mwaka huu wakati Serikali ikijibu swali langu kuhusu wachimbaji hawa wadogo ilisema kwamba inatambua vikundi ambavyo nilikuwa nimewahamasisha wachimbaji hawa kuviunda na itawapatia maeneo ya kuchimba. Hata hivyo, baada ya mwezi mmoja Serikali hii hii ilienda kuwazuia wasichimbe na sasa Waziri ananiambia kwamba tena nihamasishe kwamba waunde vikundi vingine, ni vikundi gani tena hivyo? Je, Serikali ina mkakati gani wa kuweza kutatua hii migogoro kwa sababu naona kama wanakwepa kwepa na wamekuwa na ndimi mbili mbili kuhusu huu mgogoro?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, malalamiko ya wananchi ni kuhusu huyu mwekezaji ambaye anamiliki eneo kubwa ambalo lina ukubwa wa ekari 2,250, lakini ameshindwa kuliendeleza na wananchi hawa wana nia njema kabisa ya kuliendeleza na Serikali ilikiri mbele ya wananchi kwamba mwekezaji huyu ameshindwa kuliendeleza eneo hili. Je, Serikali itatekeleza lini hii ahadi yake ambapo ilisema kwamba ingemnyang’anya huyu mwekezaji hiyo leseni na kuwapatia wananchi na si kutumia nguvu kwa ajili ya kutatua migogoro? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikiri kwamba maswali ya Mheshimiwa Mbunge yana logic, lakini niseme tu kitu kimoja kwamba kuunda kikundi ni hatua moja lakini kumiliki kihalali ni hatua nyingine. Kwa hiyo kile ambacho Mheshimiwa Mbunge alishauriwa na ambacho ndicho msimamo wa Serikali ni kwamba hao vijana wakishakaa kwenye vikundi wanatakiwa pia wafanye zile taratibu za kuweza kumilikishwa kihalali na wakishamilikishwa ndio watakuwa wamekamilisha utaratibu wa kuweza kuchimba kihalali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusu mwekezaji anayesema anamiliki eneo kubwa, nalo hilo lina taratibu zake naamini Wizara husika watakapokuwa wamejiridhisha na taratibu zile kukamilika kwenye maelekezo waliyokuwa wameyatoa basi wanaweza wakachukua hizo hatua.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwa majibu mazuri. Nimwombe tu ndugu yangu Mheshimiwa Susanne Maselle tuweze kuonana ili kuweza kulipata suala hili kwa kina na kuona namna gani tunaweza tukalitatua. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, kwanza nianze kabisa kuipongeza Serikali pamoja na changamoto zote hizi za miundombinu na idadi ndogo ya askari lakini bado wameimarisha ulinzi katika Wilaya ya Mbeya na hususani Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi.
Swali la kwanza, je, ni lini Serikali itapeleka shilingi milioni 120 ambazo zitaunga mkono shilingi milioni 200 walizotumia wananchi kukamilisha Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi?
Swali la pili; je, ni lini Serikali itajenga Vituo vya Polisi katika miji inayochipukia ya Mjele, Ilembo pamoja na Igoma? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika umaliziaji pamoja na majengo mapya aliyoyasemea tutaweka kipaumbele katika mwaka huu wa fedha pamoja na bajeti zitakazofuatia kulingana na upatikanaji wa rasilimali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze tu Mheshimiwa Mbunge, amefanya jitihada kubwa sana katika jengo hili ambalo tunalisemea na aendelee na moyo huo huo na ndiyo maana wananchi wa Mbalizi pamoja na Mbeya Vijijini wanaendelea kumuamini na kuchangua.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona.
Wilaya ya Igunga ina Kata 35 na ina Vituo vya Polisi saba, Kituo cha Igunga, Nanga, Ziba, Simbo, Sungwizi na Choma na Igurubi lakini ina magari mawili tu ya polisi. Nauliza ni lini Serikali itasaidia Wilaya ya Igunga ikapata magari mengi ili kuhudumia wananchi wetu?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Kafumu kwa kulileta swali ambalo linaungwa mkono na jiografia ya Wilaya ya Igunga na naitambua Wilaya ya Igunga na natambua umuhimu wa swali alilouliza Mheshimiwa Kafumu, niseme tu tutaweka uzito pale tutakapokuwa tunagawa vitendea kazi kulingana na upatikanaji wake.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mwaka jana Mheshimiwa Waziri Mkuu alipotembelea Jimbo la Mtama alikuta tunajenga Kituo cha Polisi pale Mtama na akaahidi kwamba tukimaliza ujenzi wa kile kituo atatupatia gari kwa ajili ya kusaidia huduma za usalama katika lile eneo. Ni lini sasa ahadi hii ya Waziri Mkuu itatekelezwa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Nape kwa ufuatiliaji wake wa masuala ya jimboni kwake. Niseme tu kwamba ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ni maelekezo na sisi tutafanyia kazi maelekezo hayo.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni kumezuka tabia mbaya ya Jeshi la Polisi, wanapokwenda kumkamata mtuhumiwa wakimkosa wanakamata mtu mbadala akiwa mke au watoto.
Naomba kufahamu Jeshi la Polisi linatoa wapi mamlaka haya ambapo wanashindwa kutumia mbinu zao za kiintelijensia kukamata mtuhumiwa badala yake wanarahisisha na kukamata mke au watoto na kuwatesa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Devotha Minja, shemeji yangu na niseme tu kwa Jeshi la Polisi linafanya kazi kwa mujibu wa sheria na niseme hakuna mtu anayeruhusiwa kufanya adhabu kwa mbadala. Kosa linabaki kuwa la mkosaji. Kwa hiyo, nielekeze tu popote pale ambapo pana mtu amefanya kosa atafutwe yule yule aliyekosa na kama wengine wanaweza wakasaidia basi wasaidie katika namna ya kuelezea jinsi wanavyoweza kufahamu, lakini siyo kuchukua adhabu ya mtu mwingine aliyekosa.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa kipaumbele cha watu wa Kinole ni ujenzi wa Kituo cha Polisi ambacho tumeshajenga ambacho kimefikia mtambaa wa panya kinasubiri kuezekwa pamoja na ujenzi wa kituo cha afya; na kwa kuwa katika Kata ya Kinole kuna SACCOSS ya mfano yenye mtaji wa zaidi ya shilingi bilioni mbili na wakulima wakubwa wa matunda na viungo lakini kuna mzunguko mkubwa sana wa pesa lakini usalama ni mdogo na Serikali imepeleka pesa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Kituo cha Kisimbi.
Je, Serikali iko tayari kuhamisha pesa hizi ilizopeleka katika ujenzi wa Kisimbi ambao ni ujenzi wa kituo cha utalii ambao siyo kipaumbele cha wananchi na kuna tatizo la mgogoro wa fidia na kupeleka kwenye umaliziaji wa Kituo cha Polisi kwenye mapato ya ndani?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo alilolisema Mheshimiwa Mbunge ni pendekezo. Niseme tu kama Serikali tunapokea pendekezo, lakini nimuombe Mheshimiwa Mbunge tupate fursa tuongee kwa undani zaidi ili tuweze kuhusisha na wadau wengine na Wizara zingine ambazo zinahusika.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa, matatizo yanayotokea Masasi ni sawa kabisa na matatizo ya ndani ya Jimbo la Mlimba lenye kata 16, halina Kituo cha Polisi wala halina gari la Askari, hivyo kusababisha mahabusu kukaa muda mrefu kwenye kituo kidogo cha Polisi kilichopo pale TAZARA. Je, ni lini sasa na Waziri Mwigulu alishatembelea, Halmashauri tumeshatenga kiwanja na tuna baadhi ya matofali. Je, ni lini sasa Serikali itafikiria kuweka kituo cha Polisi Mlimba na kupata Askari wa kutosha ili kuwatawanya kwenye vituo ambavyo wananchi wamejitolea na tunakosa Askari kwa sababu hatuna mahali pa kuwaweka Askari kwa wingi pale Jimbo la Mlimba na hatuna kabisa usafiri na anajua? Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli mazingira yale aliyoyasema Mheshimiwa Mbunge nimeyashuhudia. Nilifika mazingira yale yanafanana kabisa na mazingira ya Jimbo la Mheshimiwa Joram Ismail Hongoli.
Mheshimiwa Spika, niseme tu Serikali inatoa uzito mkubwa kwenye maeneo kama hayo ambayo jiografia yake inalazimisha tuwe na usafiri wa kujitegemea ili kuweza kuwatengenezea mazingira mazuri Askari wetu ya kufanya kazi. Kwa hiyo, tunaweka uzito kwenye jambo hilo la usafiri pamoja na kituo hicho kikubwa anachokisemea. Punde tutakapoanza kutekeleza bajeti yetu na balance itakapokuwa imeruhusu tutatengeneza hili la kituo, lakini na hilo la gari tutakapokuwa tumeanza kugawa magari tutaweka uzito mkubwa katika Jimbo hilo.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Jeshi la Wananchi liliweka kambi katika Vijiji vya Wenje na Makande kwa ajili ya kuimarisha ulinzi katika mipaka yetu na kama inavyofahamika kwamba Wilaya ya Tunduru ni miongoni mwa Wilaya zilizoko mpakani mwa Msumbiji. Je, Serikali haioni sasa wakati umefika wa kurudisha kambi katika maeneo yale ili kuendeleza ulinzi kama ilivyokusudiwa awali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, hivi karibuni Serikali imetangaza halmashauri ya mji katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; kutangaza halmashauri ya mji ni wazi kwamba tunaongeza maeneo ya utawala. Kuongeza maeneo ya utawala ni wazi pia kwamba idadi ya watu inaongezeka. Je, nini sasa kauli ya Serikali katika kuandaa mpango huo rasmi wa kukabidhi maeneo yale ya Kitanda katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ili wananchi sasa wapate kuyaendeleza maeneo yale? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa anafuatilia sana jambo hili. Niseme tu Mikoa ya Kusini ikiwemo Mtwara na Ruvuma, Kamati za Ulinzi na Usalama zilishafanya maombi ya uimarishwaji wa masuala ya kiulinzi mpakani. Kwa kuwa wamefanya maombi hayo, mawasiliano yanaendelea kufanyika kuona namna bora ya kuimarisha ulinzi huko mipakani. Jambo litakalokuwa limeamuliwa Kamati za Ulinzi na Usalama pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwa kuwa wanafuatilia wataweza kujulishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili aliloliuliza, nisema tu kama ambavyo nimejibu kwenye jibu la msingi kwamba Jeshi la Kujenga Taifa pamoja na Jeshi la Wananchi watatuma timu ya wataalam. Wakishamaliza kufanyia vipimo kwa kushirikiana na halmashauri wataweka matumizi bora ya ardhi na kuweza kukidhi kile alichokisemea kuhusu ongezeko la watu pamoja na uwepo wa halmashauri ya mji.
MHE. ALHAJ ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kutokana na swali la msingi naomba kuuliza Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, wananchi wa Makoko katika mji wa Musoma waliachia eneo wananchi 95 mwaka 1982 mpaka leo ni miaka 36 hawajalipwa haki yao ya bilioni 1.4 Serikali inatoa tamko gani kwa wananchi hao? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bulembo kwa sababu amelisemea jambo mahususi ambalo linahusu fidia, niseme tu nimelipokea na nitalishughulikia kujua status yake kwa maana ya jambo ambalo linahusisha fidia ili kuweza kujua kama tathmini na masuala yote ya uhakiki yalishafanyika na kama inastahili kutakiwa kulipwa.
MHE. SUSAN A. LYMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa mwaka 1994 Serikali ilifuta ile kwenda jeshini watoto wanaomaliza kidato cha sita kwa lazima na moja ya sababu hiyo ilikuwa ni pamoja na ukosefu wa fedha. Sasa hivi nchi yetu ina fedha na nikikukumbuka maneno ya Mheshimiwa Profesa Kabudi alisema nyumba yenye fedha ndio inaingiliwa na wezi. Sasa je, Serikali haioni kwa kuwa sasa tuna fedha nyingi, fedha hizo zitumike kupeleka wanafunzi wote wanaomaliza kidato cha sita kwenda jeshini ili kuwajengea ujasiri, ukakamavu na uzalendo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo aliloliuliza Mheshimiwa Mbunge hata sasa linafanyika mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sharia yalisharejeshwa na hivi ambavyo yanafanyika kufuatana na utaratibu wa kwenye makambi ambayo yanaendesha mafunzo hayo. Kutokana na bajeti zilivyotengwa idadi ya wanafunzi na wale wanaoenda kwa mujibu pamoja na wale wanaoenda kujitolea itaendelea kuongezea mwaka hadi mwaka. (Makofi)
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza. Bajeti inayomalizika hivi sasa ya 2017/2018, kulikuwa na tathmini ya fidia juu ya maeneo ambayo ya jeshi yalichukuliwa kwa wananchi, bilioni 27 na eneo mahususi Jimbo la kilwa masoko la Mheshimiwa Bwege na linaloitwa Rasi Mshindo, Mtaa wa Mpala ni eneo muhimu nyeti ambalo Jeshi wanataka kufanyia kazi kwa ajili ya shughuli zao. Je, nini mkakati wa Serikali kuweza kulipa kwa dharura eneo la Rasi Mshindo, Mtaa wa Mpala, Kilwa Masoko? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Masoud ni mjumbe Veterani kwenye Kamati inayosimamia Wizara hizi. Mapendekezo yaliyoletwa na Mheshimiwa Waziri yalikubaliwa na Bunge hili bila hata shilingi moja kushikwa. Niseme tu kwa sababu ndio tunamaliza bajeti tumpe tu Mheshimiwa Waziri muda wa kwenda kuyatekeleza hayo na haya yote ambayo ya kipaumbele kama ambavyo Mjumbe wa Kamati amesema yatapewa uzito unaostahili.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Diwani wa Kata ya Mihingo Mheshimiwa Nyambula Nyamhanga yuko lockup miezi sita sasa kwa kosa la uchochezi. Naomba kupata ufafanuzi wa Serikali, ni njia gani tuitumie huyu Diwani apate dhamana, kwa hiyo kesi ya uchochezi kwa sababu ana miezi sita yuko gerezani bila kupata dhamana? (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu jambo alilolisemea Mheshimiwa Mbunge ni mahsusi na kwa mujibu wa sheria kuna makosa yenye dhamana na kuna makosa yasiyo na dhamana; nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge tuje tuliongee. Pia nimpongeze kwa kufuatilia sana masuala ya wapiga kura wake. Kama ni jambo ambalo lina dhamana maana yake taratibu tu za dhamana zitafuata ili ziweze kukamilika na Mheshimiwa Diwani aweze kupata dhamana. Mara zote yale makosa yasiyo na … (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.
Kwanza kabisa naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri alipokuwa anakwenda Mbeya alipitia katika hospitali yetu ya Iringa na akajionea changamoto kubwa kabisa ambazo ziko katika mkoa wetu. Kwanza kabisa ni udogo wa eneo la hospitali ambayo iko katika mkoa wetu ambayo kwa kweli pia kuna muingiliano wa Magereza. Tatizo kubwa Madaktari Bingwa hawana kabisa maeneo ya kuishi kwenye lile eneo na wagonjwa wanapata shida sana wanapokuja kutibiwa usiku na vilevile alielezwa kuhusiana na eneo ambalo mkoa umeutafuta ili kuwepo na alternative mbili aidha magereza itoke au walipie lile eneo ili madaktari wetu waweze kuwasaidia wagonjwa usiku.
Je, sasa Serikali inatuambiaje maana yake hili ni tatizo la muda mrefu ili wananchi wa Mkoa wa Iringa waweze kutatua hiyo changamoto? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Ritta Kabati kwa sababu jambo hili amekuwa akilifuatilia sana na hii inaonyesha ni jinsi gani anavyojali masuala ya ustawi wa wananchi wa Iringa Mjini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani imelitafakari sana jambo hili na kuona kwamba kilicho rahisi kuhama ni Magereza kwa sababu kwanza eneo lipo na lipo ndani ya Manispaa na kiusalama liko vizuri zaidi kuliko pale ambapo wagonjwa au ndugu wanaoenda kuwaona wagonjwa hulazimika kupita mbele ya geti kubwa la gereza ambacho kiulinzi inaleta matatizo. Kwa maana hiyo sisi kama Wizara tunaendelea tu kuangalia logistic za kibajeti ili tuweze kuanza utaratibu huo wa kuhamisha gereza ili kutoa fursa nzuri ya wananchi kuweza kupata matibabu na expansion ya Hospitali ya Mkoa kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa ajali za barabarani zimekuwa zikisababisha vifo na kuacha baadhi ya familia katika mazingira magumu kwa kupoteza wategemezi na pia wengine kupata ulemavu wa kudumu. Je, wahanga hao hulipwa bima au fidia yoyote ili kuwapunguzia machungu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ajali za barabarani ziwe zimesababishwa na bodaboda, bajaji, baiskeli au magari zimekuwa zikisababisha vilema kwa wananchi au hata vifo na inapotokea yule aliyeathirika kama ni kifo ama majeruhi anatakiwa kupitia Shirika la Bima ambalo ile gari imekingwa katika ajali aweze kufuatilia na mpaka aweze kulipwa mafao yake ya bima. Kwa hiyo, hili ni suala la kisheria na ninaomba Watanzania wote wafuatilie bima zao pale ambapo ajali zinatokea na pia niwaelekeze Jeshi la Polisi wamekuwa wakiwasumbua baadhi ya wananchi katika kuwapatia document muhimu ikiwemo michoro ya ajali pamoja na document zingine ambazo Mashirika ya Bima yanazihitaji ili waweze kupata bima zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia bado Tanzania hapa Watanzania bado wanalalamika na hususani hawa bodaboda. Bodaboda hawa nilishatoa maelekezo kwa mujibu wa Ilani hii ya CCM, ibara ya nne kwamba Ilani hii ya CCM kwa makusudi kabisa CCM imeamua kupambana na umasikini, kwa makusudi kabisa CCM imeamua kutengeneza ajira na ikatamka hasa kwa vijana. Ni nia ya Serikali kuwalinda vijana hawa wanaopambana na umaskini na wanaotengeneza ajira. Nikaelekeza kuanzia siku ile ya bajeti hakuna bodaboda itakayokamatwa na askari wa usalama barabarani na kupelekwa kituoni kama bodaboda hiyo haipo kwenye makundi matatu yafuatayo narudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kundi la kwanza ni bodaboda ambayo imehusika kwenye uhalifu itapelekwa kituoni; bodaboda kundi la pili ni ile ambayo haina mwenyewe imeokotwa, imetekelezwa itapatikana na kupelekwa kituoni; na kundi la tatu ni bodaboda ambayo yenyewe imehusika kwenye ajali ama ilikuwa imeibiwa imepatikana itakuwa kama kielelezo lakini makosa ya amebeba mshikaki, hana element, side mirror sijui imekuaje, wataendelea kupigwa adhabu zao na siku saba watatafuta faini bila bodaboda zao kupelekwa kituoni na nimesema tarehe 15 kama ambavyo imeandikwa kwenye Biblia kwamba siku ya kuja kwa mwana wa adamu mwana wa Mungu aliye hai hakuna ajuaye siku wala saa nitaanza kutembelea Vituo vya Polisi na ole wao nikute bodaboda hizi nilizokataza kwa nia njema ya CCM kwa watu wake zimewekwa kituoni, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la ubakaji katika Mkoa wetu wa Iringa limekithiri sana; na kwa kuwa, tunaona kwamba, wanaobaka mara nyingi wamekuwa wakiweka Mawakili tena wasomi kwa ajili ya kutetea hizo kesi, matokeo yake wanashinda; na wale wanaobakwa kwa sababu, hawana uwezo walio wengi tumeona mara nyingi hata kesi zikienda wanashindwa. Je, Serikali inasaidiaje kuhakikisha wale watu wanapata haki zao, na hasa watoto wetu wanaobakwa?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri amejibu maswali ya kwanza kwa ufasaha sana. Jambo kubwa ambalo Serikali tumeendelea kusisitiza ni watu wetu kutokuyamaliza haya masuala kwa namna ya kindugu ama kirafiki na kuficha ushahidi, lakini kwa kile kipengele alichosema kwa wale watu ambao hawana uwezo wa kutafuta Mawakili tumetengeneza ule utaratibu wa msaada wa kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuko kwenye hatua za mwisho za kuzungumza kati ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ili kuweza kuanza kuwatumia Wanasheria popote pale walipo hapa nchini, wale walioko chini ya halmashauri, wale walioko chini ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, waweze kuwasaidia wananchi wale wasioweza kupata Mawakili kuwapatia msaada wa kisheria kama ambavyo viongozi wetu wakuu wamekuwa wakionesha mfano punde wanapofika katika eneo ambako kuna wananchi wana kilio, wamekuwa wakiingilia kati kuweza kuwasaidia, ili waweze kupata msaada huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshajaribisha sehemu mojawapo tulipokuwa na suala moja la mwananchi mmoja ambaye hakuweza kupata suala la wakili, lakini pia hakuweza kujua masuala ya kisheria, kuweza kusaidiwa na Wanasheria waliopo Ofisi za Mkuu wa Wilaya ama Ofisi za Mkurugenzi kwa maelekezo ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye Wanasheria wote Mawakili wako chini yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la muuliza swali ni la msingi kwa sababu kwa wakati mwingine hata mwananchi akiwa na Wakili kumekuwa na utaratibu wakati mwingine Mawakili wanazungukwa na wale watenda maovu, I mean wale Wanasheria, kama mlalamikaji hana fedha wanaweza wakazungukwa na wale wenye fedha ikatokea wakashindwa kupata haki yao. Kwa hiyo, tutakapokamilisha hili, tangazo rasmi litatoka ili wananchi waweze kupata haki zao.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Pamoja na maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri na mikakati mingi ambayo wameweka kuhakikisha tunapambana na hali hii, bado kuna mianya mingi hasa kwenye sheria yetu ambayo inaenda kuchochea hii changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, niruhusu nitoe mfano, kuna binti Iringa wa miaka 13, alibakwa na kijana wa miaka 18, akakiri kuwa amembaka binti huyu na adhabu yake ilikuwa ni viboko na akaachiwa. Huyu kijana anaruhusiwa kupiga kura, lakini sheria inapokuja kwenye kumbaka mtoto inamlinda kuwa bado ni minor. Kwa hiyo, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na mikakati hiyo inabidi waangalie upungufu mkubwa wa kisheria ambao unakwenda kuchochea changamoto hii ya watoto kubakwa na kulawitiwa katika mikoa yetu. Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, tumepokea na tuko kwenye hatua tunaziangalia hizo sheria, Sheria ya Ndoa, Sheria ya Mtoto pamoja na Sheria za Mirathi ambazo kimsingi ni sheria zinazogusa jamii moja kwa moja ili tuone pale ambapo patakuwa na upungufu tuweze kurekebisha, ili kuweza kulinda jamii yetu na ustawi wa jamii wa nchi yetu.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi ya swali la nyongeza na nitauliza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Shirika la Huduma za Mawasiliano Nchini, yaani TTCL inadai Taasisi za Serikali zaidi ya bilioni 82 za Kitanzania na Shirika la Posta linadai zaidi ya bilioni 1.5 kwa Taasisi za Serikali nchini.

Je, nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wadaiwa wote sugu wanalipa madeni yao haraka ili mashirika haya yaweze kujiendesha kiushindani? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kushukuru sana kwa kunipa fursa hii nikiunganisha na kadondoo ulikokasema nakushukuru sana kwa mwongozo huo, na ni washukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa jinsi ambavyo wamesimama na Serikali pamoja na Wizara ya Fedha katika kutoa elimu ya sheria tulizozipitisha na tumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuzisaini.

Mheshimiwa Spika, nikirejea kwenye jambo alilokuwa ameliuliza Mheshimiwa Mbunge ni kweli tumeshapokea deni la TTCL na tuna hata baadhi ya wengine wanaoidai na wenyewe TTCL wamelazimika kufika hata Wizarani kwetu kusema tunaidai TTCL, lakini TTCL wanasema na wenyewe wanazidai Taasisi za Serikali, mnatusaidiaje.

Mheshimiwa Spika, nikiri mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba jambo hili tumelipokea na jambo ambalo ameleta Mheshimiwa Mbunge tumelipokea tunaendelea kufanyia kazi na uchambuzi na namna ya kushughulika na madeni haya madogo pamoja na haya makubwa na tutaziangalia hizi taasisi ambazo tutaongea ndani ya Serikali kuziangalia hizi taasisi za Serikali kwa sababu Serikali ni moja tuweze kuona ni namna gani tunalisaidia shirika letu hili ili na lenyewe liweze kufanya hizo commitment ambazo zimefanya katika hizo taasisi zingine.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha uhalali wa magawio ambayo tunapewa kutoka kwenye makampuni haya Serikali haioni kama kuna haja ya ku-list share zake kwenye stock market ambako kule wanafanya scrutiny ya hali ya juu pamoja na kuweka hesabu wazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa maslahi mapana ya umma ni lini Serikali itaona ipo haja ya CAG kupewa mamlaka kisheria ya kuweza kufanya ukaguzi kwenye mashirika na makampuni hayo? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa maswali mazuri ambayo yanaelezea mpango mbadala wa kuona namna gani CAG anaweza akakagua mashirika haya ambayo Serikali ina hisa chache.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na la kwanza la listing of shares nadhani kuna taratibu tu ambazo huwa tunafanya uchambuzi hata kwa mashirika haya ambayo Serikali ina hisa kubwa tunaangalia namna ambavyo yanaweza yakastahimili kwenye ushindani ule punde watakapokuwa wameshaweka hesabu zao zote zikiwa sawa, kwa sababu kuna implication zingine za viashiria vya performance za mashirika ambavyo vinatumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili la pili la CAG kuweza kukagua hata kwenye maeneo ambayo Serikali ina hisa chache nikiri tu kwamba hilo ni wazo jema na sisi kama Serikali tunaona tunapokwenda huenda kukawa na uhitaji huo kwa sababu utakubaliana na mimi kwamba hata juzi juzi tulibadilisha sheria kuweza kuiruhusu Serikali kuweka guarantee hata katika maeneo ambayo Serikali ina hisa chache, tukiwa tumeenda kwenye uchumi wa kisasa ama kwenye uwekezaji wa kisasa wa maeneo ambayo ni miradi mikubwa kama ilivyo kwenye bomba la mafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo kwenye bomba la mafuta hata kama Serikali ina hisa chache lakini uwekezaji wake ambao Serikali inaweka unaweza ukawa mkubwa kuliko eneo ambalo Serikali ina hisa chache kwa maana hiyo kutakuwepo na justification ya kuona kwamba CAG anaenda kufanya ukaguzi kwenye maeneo ambayo Serikali imeweka uwekezaji na ni uwekezaji mkubwa licha ya kwamba inaweza ikawa na hisa chache.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru, nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Sekta ta kilimo ni sekta ambayo inaajiri kati ya asilimia 65 hadi 70 ya Watanzania, hii ni robo tatu ya Watanzania wanategemea hii sekta moja kwa moja, directly ama indirectly. Lakini sasa ukiangalia mikopo iliyotolewa kwa sekta binafsi kwa mwaka huu uliopita eneo la kilimo ambalo linategemewa na asilimia 65 mpaka 70 ya Watanzania limepata asilimia 8.7 tu ya mikopo yote iliyotolewa kwa sekta binafsi. Sasa na hii inajumuisha Benki ya Kilimo yenyewe pamoja na hizi benki nyingine. Sasa hiki ni kiashiria kwamba, mazingira ya kibenki sio rafiki kwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu, kwa kuzingatia haya, Serikali ina mikakati gani, mosi kuiongezea mtaji benki ya kilimo, lakini pili kuzungumza sasa na mabenki haya mengine ya biashara ili kuwe kuna riba rafiki ili wakulima waweze kukopa mikopo? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, Benki ya Kilimo ni miongoni mwa benki ambayo ina mikopo chechefu sana, na taarifa ya CAG iliyopita imeonesha kwamba, kati ya mikopo chechefu ya shilingi bilioni 129 iliyorekodiwa ni mikopo chechefu ya shilingi bilioni 2.1 tu iliyoweza kukusanywa. Sasa Serikali ina mkakati gani basi, kuhakikisha kwamba, hii mikopo inakusanywa ili kutoa nafasi kwa wakulima wengine kuweza kukopa na benki kuendelea kama kwaida? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa maswali maswali aliyoyasema. Na kipengele cha pili cha swali lake ndio kinatoa majibu ya kipengele cha kwanza kwamba, ni kwa nini inaonekana mikopo inayokwenda kwenye sekta hiyo ni kidogo:-

Mheshimiwa Spika, sababu yake ni hiyo ambayo umeweza kuona kwamba, hata Mdhibiti, CAG, aliweza kuonesha kwamba, sekta hiyo inaongoza kwa mikopo chechefu.

Mheshimiwa Spika, na sababu kubwa na ameuliza mkakati ni nini wa Serikali:-

Mheshimiwa Spika, utasikiliza mara kwa mara Waziri wa Kilimo amelisemea ni kuibadilisha sekta nzima, ili itoke kwenye ubahatinasibu kwenda kwenye uhakika. Na sehemu ya kwanza ambayo Mheshimiwa Waziri wa kilimo ameweka mkazo, kama ambavyo Mheshimiwa Rais ameelekeza nguvu ielekezwe, ni kuanzia na mbegu bora zenyewe. Kwamba, mtu anapokopa halafu akaenda kuwekeza kwenye kilimo, halafu akatumia mbegu bora ana uhakika wa kupata kutokana na kile kilichowekezwa. Kwa maana hiyo sekta nzima ikibadilishwa ikawa sekta ya uhakika, mbegu bora, kilimo cha umwagiliaji, matumizi bora ya zana za kilimo pamoja na uhifadhi pamoja na masoko, ukiukamilisha ule mnyumburisho wote maana yake unamfanya yule aliyekopa akawekeza kwenye kilimo awe na uhakika wa kurejesha.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo utaratibu ule utakapokuwa umekamilika kwa kuanzia na hilo la mbegu bora pamoja na vingine ambavyo viko kwenye mpango wa sekta ya kilimo vitawezesha sekta hiyo iwe ya kutabirika na ya uhakika na hivyo, itawezesha mtu aweze kukopa. Na ikishakuwa ya uhakika hata benki zitakuwa na uhakika wa kukusanya kutokana na hiyo kwa hiyo, riba zitakuwa rafiki.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali kuiwezesha, kuiwekea nguvu; tutaendelea kuliangalia kwa sababu ni moja ya kipaumbele ambacho tunalenga ili kuweza kuwezesha uchumi wa viwanda, lakini pia kukuza kipato cha kila Mtanzania, ili tuweze kusonga mbele kiuchumi.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, iliyokuwa benki ya FDME, sasa ni zaidi ya miaka minne tangu BOT waifunge. Wananchi wa Arusha na sehemu mbalimbali waliokuwa na akaunti katika benki hiyo hadi leo hawajui hatima ya pesa zao. Nini kauli ya Serikali?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa swali zuri. Na mara zote amekuwa kinara wa kuwatetea wananchi wa Tanzania, hasa wa Arusha, nadhani ndio maana huwa wanamchagua mara kwa mara:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kulikuwepo na zoezi hilo la kuichukua iliyokuwa benki ya FDME na kilichochelewesha ni ule utaratibu ambao ni wa kawaida unapoikabiodhi kwa mufilisi kwa hatua zile. Kwamba, unatoa kile cha kwanza ambacho kiko kisheria kwa wale ambao walikuwa na akiba zisizozidi kiwango kilichowekwa kisheria, lakini kwa wale ambao viwango vyao vilikuwa zaidi ya kiwango kinachogawanywa kwa awamu ya kwanza huwa ni lazima zoezi la mufilisi likamilike kwanza.

Mheshimiwa Spika, na zoezi hilo linahusu uhakiki wa mali zote zilizopo zikusanywe, ziuzwe, halafu zikishauzwa zikageuzwa kuwa fedha ndio watu wale waweze kugawanywa, wale ambao akiba zao zilikuwa zinazidi kiwango cha kwanza ambacho kilikuwa kimegawanywa. Sasa kwa kuwa zoezi hilo kukamilika linachukua muda, kuhakiki mali uzipate zote, lakini pia uzibadilishe ziwe fedha linachukua muda, hicho ndicho ambacho kimechelewesha.

Mheshimiwa Spika, sasa ni lini itakamilika?

Mheshimiwa Spika, nakumbuka utaratibu huu ulikuwa bado unaendelea na ulikuwa hatuia nzuri. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge tutakapokuwa tumemaliza zoezi lako la hapa Bungeni nitapata taarifa ambapo imeshafikia hatua gani ili niweze kujua ni lini watakuwa wameshakamilisha kwasababu, zoezi lilikuwa linaendelea.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri na nampongeza Waziri kwa kutoa majibu haya ambayo yanatoa faraja sana kwa hawa wanaoendesha shughuli hizo. Hata hivyo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je, Serikali itakuwa tayari kurejesha kodi iliyokusanywa kutoka kwenye taasisi hizo kwa shinikizo na hatimaye kuzidhoofisha sana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali iko tayari kuchukua hatua za kinidhamu kwa hawa maafisa wa TRA wanaokiuka sheria? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, Serikali ina utaratibu wa kurejesha fedha ambazo zilichukuliwa na kwa mujibu wa sheria zinatakiwa kurejeshwa kwa utaratibu ulio wa kawaida wa kufanya refund na refunds hizo huwa zinafanyika kwa mujibu wa sheria. Kwa maeneo ambako kuna makosa ya ukiukwaji wa kisheria, taratibu za kisheria huwa zinafuatwa na hatua stahiki za kinidhamu kuchukuliwa kwa wale wanaokiuka sheria.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama kuna maeneo ambako maafisa wetu wamekiuka sheria, taratibu za kisheria zitafuatwa na hatua za kisheria kuweza kuchukuliwa.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ukweli ni kwamba bado bei ya bidhaa sokoni ni kubwa na haijashuka hasa kwenye vifaa vya ujenzi. Je, Serikali inasema nini juu ya suala hili?

Mheshimiwa Spika, ni takribani miaka kama mitano au kumi hatujawahi kupata utulivu wa uhakika wa bei ya mafuta ya kula, sukari na unga wa ngano ambayo ni mahitaji muhimu kwa wananchi kila siku. Serikali inasema nini juu ya suala hili? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Cecilia ni mfuatiliaji sana wa masuala haya ya mfumuko wa bei, nakumbuka hata kwenye michango yake ya hotuba mbalimbali nimewahi kujibu swali linalohusiana na mfumuko.

Mheshimiwa Spika, mfumuko wa bei (inflation) sio bei kama ambavyo amesema bei za bidhaa fulani bado zipo juu. Mfumuko wa bei ni ile kasi ya bei kubadilika, tofauti na bei zenyewe kama bidhaa ipo katika bei hii hauwezi ukai-judge hapa Bungeni kama ipo juu au chini kwa sababu itategemeana tu na bidhaa zenyewe zimepatikana kwa kiwango gani.

Mheshimiwa Spika, sisi tunachoongelea na tunachoshughulika nacho ni ile kasi ya bei zenyewe kubadilika na katika Tanzania utakumbuka kwa takribani karibu miaka zaidi ya 10 tumefanikiwa kushusha mfumuko wa bei na tumefanikiwa kuuweka ucheze kati ya asilimia 3.0 hadi 5.0 ambacho ni viwango vya Afrika Mashariki. Na hilo ndio lengo kubwa la kuweza kuhakikisha kwamba bei zetu hazibadilikibadiliki kwa kiwango ambacho kinasababisha vitu visitabirike katika uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ambalo ametaja bidhaa mahususi, kuna mikakati ambayo ni mahususi kwenye mazao hayo aliyoyataja ikiwemo mafuta ya kula pamoja na masuala kama ya sukari. Utakumbuka hotuba ya Waziri wa Viwanda ilielezea vizuri jinsi Serikali ambavyo imejikita kwenye kuongeza uzalishaji wa sukari ambapo kutakuwepo na upanuzi wa mashamba pamoja na uzalishaji wa sukari ambao sasa utaenda kutoa jibu la uhakika na la kudumu kuhusu hizo bei zinazokuwa zinapandapanda na kubadilikabadilika kwenye masuala ya sukari.

Mheshimiwa Spika, na hii ilikuwa inatokea kwa sababu, kwenye masuala ya sukari kuna vipindi ambavyo viwanda vinakuwa havizalishi. Tulikuwa tunalazimika kutafuta sukari kutoka maeneo mengine kuziba pengo la aina hiyo, lakini kwa mkakati ambao umewekwa wa kuziba pengo hilo la sukari kwa uzal;ishaji wa ndani, utaenda kutoa jibu la kudumu la mabadiliko ya harakaharaka ya bei za sukari.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye mafuta ya chakula utaona jinsi ambavyo Waziri Mkuu kila wakati utamuona yuko katika maeneo mahususi ambayo yanashughulika na masuala ya uzalishaji, kuhamasisha uzalishaji wa mazao haya ambayo yatatupatia mafuta ya chakula, ili kupata jawabu la kudumu la upungufu wa mafuta ya chakula ambao ndio unasababisha kupanda kwa bei. Umeona jinsi anavyofanya kazi Kigoma, anavyofanya kazi Singida pamoja na maeneo mengine ambayo anashughulikia masuala ya aina hiyo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu haya ya Serikali ambayo kwa kweli yanaonyesha bado tuko nyuma sana, maana kati ya 140,000 kwa Afrika sisi tuna 5,000 sawa na asilimia 4.2: Sasa ni upi mkakati wa Serikali katika kuhuisha sera na sheria ambazo wakati mwingine ndiyo zinazokuwa kikwako katika ukuaji wa mitaji wa kibiashara na uwekezaji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Mheshimiwa Waziri ametaja sekta mbalimbali ambazo mabilionea hawa aliowataja wanatoka, lakini kwa masikitiko makubwa hakuna hata mmoja anayetokana na Sekta ya Kilimo na Mifugo na Uvuvi. Haoni kwamba kwa stahili hiyo wakulima, wafugaji na wavuvi wataendelea kuwa wasindikizaji katika eneo zima hili la kiuwekezaji wa mitaji? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Shangazi kwa swali lake nzuri. Nampongeza kwa jana niliambiwa alikuwa anashabikia moja ya timu iliyoshinda kwa mbinde sana. Taarifa alizonipa Mkuchika anasema, basi timu yake isingeshinda, mpaka sasa mpira ule ungekuwa bado unaendelea kuchezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mabilionea hawa tuliotaja, tumewataja tu kwa mfano. Tumetoa tu mifano ya baadhi ya sekta ambazo tumeweza kuziainisha, lakini haina maana kwamba kwenye Sekta ya Kilimo na Mifugo hakuna mabilionea. Hata Sekta ya Mifugo na Sekta ya Kilimo wapo mabilionea na takribani kila mkoa kwenye sekta hiyo ya kilimo mabilionea wapo kuanzia ngazi zote; kuanzia kwenye kulima kwenyewe wapo ambao wako ngazi ya processing ambazo ziko ngazi ya viwanda, lakini wapo pia wa ngazi ya export. Kwa hiyo, hii tulitolea tu mifano ya baadhi ya maeneo ambayo yapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta nyingine zipo ambazo hatujazitaja kwa kiwango kikubwa na zenyewe zina mabilionea ambao wako. Kwa mfano, King Musukuma pamoja na wengine ambao na wenyewe wapo katika makundi yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kwamba tuna sera gani? Serikali ina sera na moja ya maeneo ambayo tumeyapa uzito mkubwa ni kutengeneza mazingira bora kabisa ya ufanyaji biashara ambapo tunahamisha watu kutoka kundi moja la kipato kwenda kipato kingine na mkakati huo unaanza na biashara kuanzia zile zilizo ndogo kwenda biashara zilizo kubwa na zilizo kubwa kwenda kwenye ngazi ya mabilionea ili Tanzania iweze kuwa na mabilionea wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tamko lilitolewa siku siyo nyingi sana, hata Wabunge wanakaribishwa waungane na King Musukuma kwenye kundi lile la mabilionea ili waendelee kuongozwa kwa mfano kwa wananchi hao wanaowaongoza. (Kicheko/Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, ili mtu aweze kuwa bilionea, wengi wanaanza katika biashara ndogo ndogo. Kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema, unaanza na biashara ndogo ndogo, unafika kati na hatimaye unakuwa mkubwa ukiacha wale ambao wanarithi. Sasa imekuwa ni utamaduni wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi kuwafukuza Wamachinga ambao wanatumia kipato chao kidogo kwenye maeneo yao ya biashara na kuwapeleka pembezoni na maeneo ambayo hayajaandaliwa na mazingira ambayo siyo wezeshi kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuthibitisha kwamba Serikali haijali kundi hili la wafanyabiashara wadogo wadogo, hapa kwenye mpango ambao Waziri ameusoma jana, hakuna maeneo ambayo anazungumza atawapanga vipi hawa vijana wetu? (Makofi)

Sasa nataka Waziri aniambie, kwa kuwa anatambua ili uweze kuwa milionea na hatimaye bilionea, lazima uanzie chini; na kwa kuwa anatambua...

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Halima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakuja, ninakuja. Serikali...

NAIBU SPIKA: Aah, uliza swali, kwa sababu umepewa nyongeza.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina uwezo wa kuajiri asilimia mbili tu: Je, sasa ana mpango gani rasmi wa kuingiza eneo hili muhimu katika Mpango wetu ambao tutakuja kuufanyia kazi Januari, kwa kundi hili kubwa la vijana ambalo sasa hivi wanahangaika mtaani?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Halima kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali inayowajali sana wafanyabiashara wadogo. Mfano na uthibitisho mmoja ni kwamba mabilionea wote walioko katika nchi hii, ni zao la Chama cha Mapinduzi kwa sababu hakuna chama kingine kimewahi kuongoza. Kwa hiyo, mabilionea wote unaowaona katika nchi hii na wengine wame-spill over mpaka nchi za SADC na nchi nyingine kwa ukombozi wa Chama cha Mapinduzi. Ni zao la Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hawa ambao wako hapa, amesema Mpango haujasema watapangwa vipi? Mpango wa nani akae wapi, ni suala la kisekta ambalo litafanywa na Serikali za Mitaa. Kwa upande wa Wizara ya Fedha, Mheshimiwa Rais ana mpango mzuri sana na kundi hili ambalo Mheshimiwa Halima amelisema la wafanyabiashara wadogo wadogo. Kwa sababu ndiyo kwanza bado tunaendelea kuchambua huu Mpango, tutawapa undani wake Waheshimiwa Wabunge, ni kwa sababu tu hatukusema kwa kuwa bado tuko kwenye mazungumzo ya awali. Hata hivi tunavyoongea, tunaendelea kuongea na wenzetu wa Benki ya Dunia, lakini pia tunaendelea kuongea ndani ya Serikali kutengeneza utaratibu ambalo lengo lake kubwa hasa ni kuwafanya hawa ambao tumewataja kwa jina la Wamachinga waweze ku- graduate, wapige hatua kwenda kwenye hatua nyingine inayofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, habari njema hii mtaiona katika Mpango huu na mtaona katika bajeti hii inayokuja na wenyewe Wamachinga watakuwa mashahidi kwamba kumbe kweli huu Mpango ulikuwa ni mwema ambapo umetufanya tu-graduate. Kwa sababu katika hali ya kawaida, hakuna Mmachinga anayetaka aendelee kuwa Machinga katika maisha yake yote. Hata wao wanataka siku moja wawe kama GSM wafanye mambo ya kweli na yanayoonekana katika nchi hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa shauri hili lilizungumzwa toka mwaka 2018 na Ofisi ya Msajili Hazina wakapewa jukumu la kulisimamia tuna miaka zaidi ya mitatu sasa hivi imeshapita: Je, ni lini tutaelezwa kwamba shughuli hii itakuwa imemalizika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Wananchi wa Mtwara ambao wanadai zaidi ya shilingi milioni 250: Ni lini Mheshimiwa Waziri atakuja kuzungumza na wananchi wa Mtwara ili waelewe mustakabali mzima wa fedha zao ambazo zimepotea mpaka sasa hivi haijulikani watalipwaje? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Mtenga kwa kufuatilia sana masuala ya wananchi wake wa Jimbo la Mtwara. Mara kwa mara akija ofisini anafuatilia masuala yanayohusu wananchi wa Mtwara katika sekta mbalimbali na anatumia vizuri uzoefu wake wa kuwa Katibu wa Mkoa wa Chama na maeneo tofauti tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kwanza kwamba jambo hili limechukua muda, ni kweli lilichukua muda kwenye hatua za awali kwa sababu lilipokuwa kwenye ngazi za kimahakama, hatua nyingine hizi zisingeweza kufanyika, lakini baada ya kuwa shauri hilo limeshaamuliwa na Mahakama, kwenye hizi hatua nyingine, zinaweza zikafanyika kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba wananchi wake watapata uhakika haraka tu. Naamini nami nitapata uhakika kutoka kwa Msajili wa Hazina ili niweze kumuarifu makadirio hasa ya muda aliyokuwa anataka aujue kuwa ni lini?

Mheshimiwa Spika, hili la pili kwa ridhaa yako, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tukishamaliza Bunge tutapanga utaratibu ili tuweze kuwaandaa wahusika hao, nami niweze kufanya ziara kuweza kuwaelimisha nikiwa tayari na majibu ya uhakika kutoka kwa Msajili wa Hazina kuhusu kipindi ambacho kitatumika kuweza kuhakikisha kwamba hatua hizo za kiutawala zitakuwa zimekamilika.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba tu Serikali inieleze, inakuwa wapi mpaka matatizo haya yanatokea? Ukizingatia kwamba watu wengi wanaoweka na kukopa kwenye hizo taasisi ni watu wa kipato cha chini; Serikali inakuwepo inaona jambo linaendelea mpaka linakua, wanakuja kunyang’anya ama kuchukua, watu wanaathirika. Kumbuka mambo ya DECI, ilikuwa hivi hivi. Leo PRIDE iko hivi hivi. Nataka nijue, Serikali inakuwa wapi mpaka inaacha mambo haya yanafikia hapo wananchi wanaathirika ambapo wengi wao ni wakipato cha chini? Nakushukuru. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kazi ya Serikali kutoa miongozo na kusimamia hizi taasisi. Kwa upande mmoja Serikali ni pamoja na wananchi inapofika masuala ya kifedha kwa sababu taasisi zote za kifedha zinakuwa na mikutano yao ya kila mwaka, lakini mara nyingi sana wananchi wetu wakishaweka fedha kwenye maeneo haya ya kibenki, hawafuatilii sana mienendo ya kifedha kwenye maeneo walikoweka. Wakati Serikali inafanya yale mambo ya kiutawala, ni wajibu wao pia kuangalia mwenendo wa taasisi yao ambako wameingia mkataba na taasisi husika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, rai yangu, kwanza wananchi watumie taasisi za kifedha ambazo hazina mashaka mashaka. Tuna mabenki yanaendelea kuenea katika maeneo mengi, watumie mabenki ambayo yako accredited na Serikali, wasitumie taasisi zile ambazo zina mashaka mashaka, lakini hata taasisi zile ambazo ziko accredited kama ambavyo masharti ya kifedha yanasema, wanapokuwa na mikutano ya mwaka ya taasisi hizo, wachukulie umuhimu kufuatilia mienendo ya taasisi hizo ambazo wameingia mkataba nazo.
MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya CAG ya mwaka 2019/2020 na mwaka 2020/2021 kesi hizo nilizozitaja zimesajiliwa katika Mabaraza yetu; Baraza la Rufani za Kodi (TRAT) na Bodi ya Rufani za Kodi (TRAB) zilisajiliwa kesi hizi zenye thamani ya trilioni 360 na hivyo kama majibu ya Serikali kwamba hakuna kesi ya trilioni 360 wakati kwa mujibu wa Taarifa ya CAG hizi kesi zilikuwa zimesajiliwa na Mabaraza haya; hizi kesi zipo wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, zipo taarifa za uhakika kwamba katika mwaka huu wa fedha Serikali iliamua kupokea shilingi bilioni 700 kupitia katika hizo kesi za shilingi trilioni 360 na katika kipindi cha Disemba, 2021 na Februari, 2022 Serikali ilipokea fedha hizo na kuzifuta kesi zenye thamani ya shilingi trilioni 360. Kwa nini Serikai iliamua kupokea fedha bilioni 700 badala ya shilingi trilioni 360 kama madai halali ya nchi? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake aliyoyaleta, lakini naomba niweke kumbukumbu sawa; jambo hili hata jana nimeona limejadiliwa kwa kirefu sana na nitakuomba unipe dakika ili niweze kuliweka sawa.

Mheshimiwa Spika, jambo hili liko namna hii, ni kweli anachosema Taarifa ya CAG ya mwaka 2019 ilisema hivyo na Taarifa ya CAG ya mwaka 2019 maana yake ni ukaguzi wa vitabu vya mwaka 2018 (mwaka unaofuatia nyuma yake) lakini kilichofanyika ni kipi?

Mheshimiwa Spika, baada ya mzozo kujitokeza kati ya kesi ya Acacia pamoja na Serikali, Acacia aliuza jambo lile kwa Barrick na Rais wa wakati ule, Rais Magufuli aliunda timu ya kufanya makubaliano na hawa watu mwaka 2017/2018 na makubaliano hayo yaliendelea kwenye mjadala, yakaisha tarehe 24 Januari, 2020 na sherehe hizi zilifanyika Ikulu mbele ya Rais Magufuli na shamrashamra kubwa na Tanzania tukakubali kuachilia shilingi trilioni 360 tumalize shauri lile na tukaunda Kampuni ya Twiga na nchi nzima tunasheherekea kampuni ile kwamba ina ubia wa asilimia 16 kwa Serikali na asilimia 84 kwa Barrick.

Mheshimiwa Spika, na mambo mengine yaliyokubaliwa kwenye makubaliano hayo la kwanza ni lile la ubia kwamba Serikali tutakuwa na asilimia 16 na wao watabakiza asilimia 84.

La pili, wao walikuwa na kesi na sisi ya dola bilioni 2.7 wakafuta kesi hiyo; la tatu, tukakubaliana kwamba watatoa dola milioni 40 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ambayo hata kwenye briefing ndio Mbunge wa Kahama aliyekuwa anaiulizia, tukakubaliana hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, si hilo tu, tukakubaliana kwamba watakuwa wanatoa dola sita kwenye kila wakia ya dhahabu na tukakubaliana kwamba watatoa dola milioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa maabara ya madini.

Kwa hiyo, haya yalikuwa sehemu ya frame work agreement ile ambayo ilikubalika na baada ya hapo tukawa tumeshamaliza yale mashauri yakiwemo na mengine ambayo yaliyokuwa yanahusisha mjadala kwenye makubaliano yale yaliyokuwa yanafanyika.

Mheshimiwa Spika, sasa baada ya kuwa imeshafanyika hivyo, kilichofanyika kingine ilikuwa ni kuanza kupokea gawio baada ya kuwa jambo lile limeshafungwa tangu mwaka 2020, kama lilishafungwa tangu mwaka 2020 kilichofuatia mwaka 2021 tulipokea gawio, mwaka 2022 tumepokea gawio na dola milioni 300 ambazo ndio kama bilioni 700 ilikuwa sehemu ya makubaliano kwenye mjadala uliofanyika na sherehe ile ilifanyika Ikulu, mbele ya Rais Magufuli. (Makofi)
MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, kwanza nasikitika kwamba swali limeuliza shilingi trilioni 360 lakini limejibiwa shilingi trilioni 4.21. Hata hivyo, ninayo maswali mawili ya nyongeza: -

La kwanza, kwa nini Serikali iliamua kukubali kupokea shilingi bilioni 700 kutoka katika kesi za malimbikizo ya makampuni ya madini maarufu “makinikia” badala ya shilingi trilioni 360 ambayo ni madai halali katika nchi yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nini kilichowafanya TRA washindwe kukusanya malimbikizo ya kodi yasiyo na kesi ya shilingi trilioni 7.54 na kusababisha ongezeko hili la malimbikizo ya kodi kufikia asilimia 94.6 lakini wakati huo huo uwezo wa TRA wa kukusanya malimbikizo hayo umekuwa ukishuka kila wakati na kufikia asilimia 10 tu na wakati huo TRA ikijivuna kwamba inaongeza makusanyo ya kodi?

SPIKA: Mheshimiwa Mpina kwanza nipate ufafanuzi; swali linazungumzia kesi 1,097; shilingi trilioni 360 na hizo Dola za Kimarekani milioni 181.4.

Mheshimiwa Naibu Waziri jibu linazungumzia mashauri kuwa 854 ambayo thamani yake ni shilingi trilioni 4.21 na dola za Kimarekani milioni 3.48. Haya ndiyo mashauri yaliyopo ambayo Serikali inayajua ambayo ni tofauti na ya Mbunge au mmechagua kati ya yale ambayo yapo, mmeamua kuyajibia haya ambayo mmeleta majibu? Nataka kuelewa kwanza hapa. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Hayo ni mashauri ambayo yapo na Serikali tunayatambua.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, naona umesimama. Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, ufafanuzi wa hiyo sehemu ya kwanza, halafu nimpe fursa ya kujibu yale maswali mawili.
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwenye suala la msingi lile la shilingi trilioni 360; moja, Serikali haijakubali tu kimya kimya, haijakubali kupokea fedha hizo kwa maana ya kuacha shilingi trilioni 360, isipokuwa kilichofanyika, utakumbuka Serikali ilipeleka complain against makampuni hayo ya madini na baada ya complains zile kupelekwa…

SPIKA: Ngoja Mheshimiwa, twende kwa mtiririko mzuri. Ninachotaka kuelewa, swali la Mheshimiwa Mpina linazungumzia kesi 1,097; jibu linazungumzia kesi 854 na thamani ambayo Mheshimiwa Mpina anazungumzia ni shilingi trilioni 360, serikali inasema ni shilingi trilioni 4.21. Mimi nataka kuelewa ili nitoe mwongozo vizuri wa majibu hapa, namna Serikali ijibu. Haya majibu ambayo Serikali mmetoa, ni kwamba ndiyo kesi zilizopo ama idadi ni hii aliyotaja Mheshimiwa Mpina na kiasi cha fedha ni hiki alichotaja Mheshimiwa Mpina?

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, pana utofauti. Ile kesi kubwa aliyoiongelea ya Shilingi trilioni 360 ni ya upande wa makinikia. Hii ya mashauri ambayo yanaenda kwenye shilingi trilioni nne, ni ya mashauri ya kesi nyingine ambazo ziko TRAB na TRAT ambazo ndiyo Serikali inaendelea kuyafanyia kazi moja baada ya nyingine.

Kwa hiyo, pana mambo ya aina mbili na lingine limeongezeka ya yale yasiyo ya kesi na lile linakuwa la tatu. Kwa hiyo yameunganishwa pamoja.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali ilitenga shilingi trilioni 1.5 kwenye Wizara ya Ujenzi na Bunge likapitisha. Mpaka Machi, mwaka huu 2022, imepewa asilimia 68 ambayo ni shilingi trilioni 1.09, hakuna barabara mpya hata moja iliyojengwa katika kipindi hiki cha mwaka fedha, sana sana wamelipa madeni: -

Mheshimiwa Spika, swali langu kwa Serikali, kwanini msiwe wakweli kwa Wabunge hawa, mkawaeleza kwamba mwaka huu tunalipa madeni, na mwaka ujao tunajenga barabara, kuliko kuwapa majibu mazuri ya matumaini wakati fedha hazipo? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa; na niwahakikishie Wabunge pamoja na Watanzania kwamba fedha za kutekeleza hii miradi zipo; na Serikali inajenga barabara mpya na inalipa madeni. Ujenzi ule unavyofanyika, utaratibu wake ni kwamba kazi inapokamilika ndipo mtu analipwa. Tunalipa kwa certificate, hatugawi tu fedha zikasubiri mtu aanze kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, kinachofanyika, tunatekeleza mradi, ukishakamilika tunalipa; na tunaendelea na miradi mipya, na yenyewe kadri certificate zinavyokuja tunalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo anayosema ya madeni inawezekana kwenye hatua nyingine madeni yakawepo, kwa sababu ni lazima tufanye uhakiki; na miradi mingine ilishafanyika katika vipindi tofauti tofauti, kwa hiyo tuna uhakiki na tunalipa.

Mheshimiwa Spika, hivi ni kweli kwamba tungeweza kujenga reli inayokwenda mpaka Pacific, inayokwenda mpaka Bara lingine, inayokwenda mpaka upande mwingine wa bahari, halafu tushindwe kujenga barabara? (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote, tunajenga barabara mpya, tunalipa kwa certificate zinapokuwa tayari, lakini pia tunalipa na madeni ambayo kazi hizo zilishafanyika.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi tukaacha kutengeneza barabara mpya wala kutekeleza miradi mipya tukafanya kazi moja ya kulipa madeni. Tutalipa madeni na tutatekeleza miradi mipya ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, haya ndiyo maelekezo ya Mheshimiwa Rais na hii ndiyo dira ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na hasa fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya kuhudumia vituo vya afya vilivyobaki. Kwa Kituo cha Nemba nashukuru kwa ajili ya vifaa vilivyopokelewa. Hata hivyo, nina swali moja la nyongeza; Kituo cha Afya cha Rukaragata ndicho kinachohudumia Wilaya ya Biharamulo Mjini, kwa sababu hatuna hospitali ya wilaya, kwa sababu hospitali iliyojengwa iko Kata jirani ya Lubungo. Sasa swali, kwa sababu tuna akinamama ambao wanajifungua pale na wanapata shida na hamna jengo la upasuaji na wametuambia tutapata pesa katika mwaka 2023/2024, ni mbali sana kwa sababu akinamama wanaendelea kuzaa na wanahitaji huduma. Sasa kwa sababu Waziri wa Fedha yuko hapa na Waziri ametuambia twende huko mbele, naamini Serikali inaweza ikapata fedha katika vyanzo vingine tukapata hii fedha katika mwaka huu wa fedha. Je, Waziri haoni haja ya kumpa nafasi Waziri wa Fedha aweze kutusaidia kwenye hili ili tuweze kupata fedha hii na akinamama wa Biharamulo waweze kunufaika na hili? Nashukuru.
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge wa Biharamulo kwa swali lake na kwa kweli amekuwa akifuatilia sana wizarani fedha ya hospitali ya wilaya ambayo ni takribani milioni 204, pamoja na hili suala ambalo anasema hospitali yake ya wilaya, I mean kituo hiki cha mjini kinafanyika kama hospitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe na nimwombe Mheshimiwa Mbunge aridhie tulichukue jambo hili Wizara ya Fedha ili tuwasiliane na wenzetu wa TAMISEMI, pamoja na yeye na Mkurugenzi wake, tuweze kuona namna ya kuliharakisha kwa ajili ya maisha ya Wanabiharamulo kama ambavyo amesema. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha mpaka sasa inaonekana ni shilingi bilioni 100 ndizo ambazo wananchi wameweza kukopeshwa na kuwafikia walengwa hao wa kilimo.

Je, Serikali haioni kwamba kama ulivyosema jibu la msingi, Serikali inakopesha taasisi na asasi za fedha kwa asilimia tatu lakini wakulima hawa wanakopeshwa kwa asilimia 10 ambazo ni kubwa sana na hatuwezi kuwasaidia wananchi wetu wa kawaida. Kwa nini Serikali isishushe na wananchi hawa wakapata kwenye asilimia Tano ili iweze kuwa na tija kwa wakulima wa Tanzania?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, tunafahamu asilimia zaidi ya 70 ni wakulima hapa Tanzania, hatuoni kuna haja sasa ya kuhakikisha kutoka shilingi trilioni moja zimetoka tu, wewe unatamka hapo shilingi bilioni 160 ni ndogo, zaidi ya shilingi bilioni 800 bado hazijafika.

Je, hauoni sasa kuna haja, Serikali ihakikishe ahadi iliyosema kwenye shilingi trilioni moja angalau shilingi bilioni 900 tuweze kuwasaidia wakulima wa Tanzania?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii na nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake ya nyongeza lakini naomba niweke kumbukumbu sawa.

Mheshimiwa Spika, mikopo hii hawakopeshwi kwa asilimia 10, nilichosema wanatakiwa wakopeshwe kwa kiwango kisichozidi asilimia 10, kwa hiyo tulichokiweka ni asilimia Tisa kushuka chini. Tulichosema atakayepata fursa hiyo kutoka Benki Kuu anatakiwa awakopeshe wakulima kwa single digit, kwa riba ya asilimia isiyozidi kumi, kwa hiyo ni tisa kushuka chini na hicho ndicho ambacho kimekuwa kikifanyika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kiwango, tofauti na fedha zingine ambazo tuna-finance project, hii hapa inatoka kufuatana na uhitaji, kwa hiyo kadri benki zinavyochukua na kadri wahitaji wanavyochukua, ndivyo kiwango hiki kinavyoendelea kuwa kikubwa. Kwa hiyo, kwa kuwa Bunge ni sehemu ya viongozi tunaoongoza wananchi tuendelee kuweka hamasa. Hili linaendana sambamba kabisa na jinsi ambavyo hii sekta ya kilimo imekuwa na uamsho kuhusu masuala ya kutumia benki.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kiuhalisia, ongezeko la Mawakala wa Bima linatokana na vijana wengi waliomaliza elimu ya fani ya bima nchini kuamua kujiajiri wenyewe baada ya kukosa kazi Serikalini: -

Mheshimiwa Spika, je, ni utafiti gani wa kina ambao umefanyika na Serikali hadi kujua kwamba ongezeko hilo linatokana na mfumo wa biashara ya bima kukua?

Mheshimiwa Spika, je, ni utafiti gani ambao mmeufanya katika kujua mawakala vijana ambao wamefunga biashara baada ya kushindwa biashara kutokana na ushindani mkubwa wa biashara ya bima ambao umevamiwa na benki pamoja na kampuni za simu? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa maswali mazuri. Moja, hivi tunavyoongea mpaka sasa, upande wa masuala haya ya bima hapa nchini ziko takribani asilimia 16 tu, ndiyo tunapata ushiriki wa vijana ambao wako chini ya umri wa miaka 18 na utafiti huo uliofanywa na Finscope ulionesha hivyo. Sasa katika nchi ambazo zimeendelea na kule tunakoelekea tunatamani angalau tufike asilimia 84 au zaidi ya hapo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu utafiti wa mawakala, taarifa ambazo zilikusanywa kwa miaka kadhaa kama nilivyotoa pale mwanzo, zinaonesha kwa mwaka 2020 walikuwa zaidi ya 700, lakini kwa sasa tumeshazidi 930. Kama tumeshazidi 930 hii inaonesha kwamba bado pana fursa ambapo vijana wote wanaweza wakashiriki na bado mafanikio yakapatikana bila wao kuzuiliwa kwa sababu ya uwepo wa BenkiWakala.

Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo, TIRA ilishatoa mwongozo ambao unaweka mipaka ambayo inaonesha ni namna gani italinda BenkiWakala zisilete athari kwa Mawakala hawa wa kawaida ambao wanaendesha shughuli hizo. Tunaamini kwamba biashara hiyo itaendelea kusambaa zaidi kwa wananchi walio wengi zaidi. (Makofi)
MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, wale waliokutwa na ubadhirifu wamechukuliwa hatua gani?

Swali la pili, je, Serikali itakuwa tayari kuweka utaratibu wa kuutangazia umma wale waliochukuliwa hatua pamoja na hatua zilizochukuliwa ili kuwafanya Watanzania waweze kuiamini Taasisi hii ya CAG? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, tunalipokea wazo la Mheshimiwa Mbunge na hivi ndivyo ambavyo tumekuwa tukifanya kwamba wale ambao wanabainika kuwa na makosa wanachukuliwa hatua. Mpaka sasa kuna hatua mbalimbali ambazo zinaendelea baada ya taarifa ya CAG kukamilika. Baada ya majibu ya Serikali kutolewa yale maeneo yanayoonekana kuwa na hatia ndani yake yanakwenda kwenye uchunguzi na sasa hivi tuna majalada ambayo yako ngazi ya uchunguzi na tuna yale ambayo yalishafika ngazi za kimahakama. Pia kuna maeneo ambayo kesi zilishahukumiwa ambazo zinahusisha upotevu ambao taarifa zake zimepatikana kupitia taarifa ya CAG.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kutangaza tumepokea hilo, tutaboresha vitengo vya mawasiliano ili vianze kutoa matamko kwenye maeneo ambayo hatua zimechukuliwa pale ambapo kulikuwa na ubadhirifu umebainika kupitia taarifa ya CAG.
MHE. NICODEMAS HENRY MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, anafahamu usumbufu wanaoupata wafanyabiashara kwenye mipaka yetu, kwa maana ya mipaka ya Kenya na Rwanda, kwa vile kule kila wakati faranga inapanda bei na kushuka lakini shilingi nakumbuka mwaka 1995 enzi za Mkapa ndiyo shilingi ilipanda bei na hii ndiyo inachangia ugumu wa maisha.

Sasa kuna mkakati gani wa kuifanya shilingi yetu iwe na thamani ili wananchi waweze kupata bidhaa kwa bei nafuu kulingana na upandishaji wa thamani?

Swali la pili, Serikali ina mpango gani wa kudhibiti mfumuko wa dola, kwa sababu kumekuwa na kupanda sana kwa dola bila utaratibu. Leo unakuta dola inabadilishwa kwa shilingi 2,550 lakini jioni ukienda tena unakuta inabadilishwa kwa shilingi 2,800 na hii inafanya Taifa kuwa na maisha magumu, ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii ya kumjibu Mheshimiwa Mbunge maswali yake mawili ya nyongeza. Moja, Serikali imejitahidi kusimamia kuhakikisha la kwanza, thamani ya shilingi haishuki; la pili, ambalo tunalifanya katika mikakati yote hii ambayo unaiona Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu aliyoielekeza ya kuwekeza kwenye sekta za uzalishaji, malengo ya muda mrefu kwenye hilo ni kwenda kuimarisha, kuongeza thamani ya shilingi yetu. Tutaongeza thamani ya shilingi yetu kwa namna nyingi zikiwemo hizo mbili za kuongeza mauzo nje ili tuwe na dola nyingi. Pili, kwa kuzalisha bidhaa ambazo tunaweza tukajitegemea na tukatumia ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kudhibiti mabadiliko ya haraka haraka ya bei ya dola, Mheshimiwa Mbunge, katika kipindi cha muda mfupi, tunalishughulikia jambo hili ili kuweza kukabiliana na tatizo ambalo limejitokeza la dunia nzima la upungufu wa dola, ambapo hicho ndicho kinachosababisha mahitaji ya dola yanakuwa makubwa kuliko upatikanaji wa dola na hivyo kufanya bei ya dola kuanza kubadilikabadilika.

Mheshimiwa Spika, hata sasa tuna hatua ambazo tumeendelea kuzichukua ambazo tunaamini zitaweza kusaidia dola ziwepo nyingi sokoni, na zikiwa nyingi sokoni zitasababisha tatizo la bei kubadilikabadilika kuweza kupungua.

Mheshimiwa Spika, tunatoa rai kwa wadau wote wanaoshiriki katika soko la kubadilisha fedha, waendelee kushiriki kikamilifu ili kuweza kuhakikisha kuwa Dola haiadimiki sokoni na hivyo kusababisha bei kubadilikabadilika.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Mkoa wa Iringa una potential kubwa ya madini ya chuma pamoja na madini ya viwandani, je, Wizara ya Fedha iko tayari kutuunganisha na wadau ili tuweze kutumia potential hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mkoa wa Iringa pia umekuwa ukikusanya maduhuli kila mwaka takribani bilioni moja kutokana na madini. Sasa Wizara ya Fedha ipo tayari kuwa na mpango mahususi kuisaidia GST na STAMICO kufanya utafiti wa kijiolojia ili tuongeze mapato hayo na yenyewe inufaike? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la kwanza, Wizara ya Fedha tuko tayari na Mheshimiwa Mbunge kabla ya kurudi Jimboni tufanye kikao ili tuweze kumuunganisha na Idara inayosimamia hiyo ili aweze kuwaunganisha na wadau aliowataja kwa ajili ya kufanikisha hilo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu lile la pili, GST pamoja na taasisi zingine kuhusu kuongeza utafiti zaidi, tulishaongea na Wizara ya Kisekta na tuko tayari kuongeza fedha ili utafiti zaidi uweze kufanyika, kwa sababu potential ya kugundua maeneo mengine ya uchimbaji bado ipo na inaweza ikatuletea tija zaidi. (Makofi)
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana pamoja na majibu mazuri ya Serikali ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa kuna Wakandarasi wengi wamesaini mikataba na Serikali hasa mikataba ya ujenzi; na kwa kuwa Mikataba hiyo imeathiriwa sana na mabadiliko makubwa ya viwango vya kubadilisha fedha za kigeni hasa dola za Kimarekani. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia Wakandarasi hawa ili wasishindwe kutekeleza miradi hiyo hasa miradi ya ujenzi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa mabadiliko ya viwango vya kubadilishia fedha za kigeni kabla hatujapitisha bajeti ya nchi ilikuwa shilingi 2,350, hiyo ni dola ya Kimarekani na sasa ni shilingi 2,500 hadi shilingi 2,600 na mabadiliko haya yameathiri bajeti ya nchi tuliyoipitisha hapa Bungeni hasa kwenye maeneo ambapo Serikali inahitaji kununua bidhaa nje ya nchi.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuinusuru bajeti yetu tuliyoipitisha hapa Bungeni ili iweze kutekelezeka vizuri? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa maswali mazuri aliyouliza Mheshimiwa Ndaisaba; kuhusu swali la kwanza ambalo linahusisha Wakandarasi ambao watakuwa wameathirika na mabadiliko ya bei za kubadilishia fedha huku Mikataba yao ikiwa imeshasainiwa, nimwombe Mheshimiwa Mbunge na niwaombe Wakandarasi wa aina hiyo kufanya engagement, kufanya mashauriano na sekta zinazohusika kwa sababu masuala ya kimkataba ni ya sekta kwa sekta ili jambo hili liweze kusogelewa kwa umahususi wake katika eneo husika.

Mheshimiwa Spika, tunazo taarifa katika baadhi ya miradi ambako tayari walishafanya mashauriano ya aina hiyo kutokana na mabadiliko haya ambayo yalikuwa yanajitokeza ya kiuchumi. Kwa hiyo hata hawa ambao watakuwa wamekumbwa na jambo hilo, ni vizuri kufanya majadiliano katika maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu jambo la pili la kunusuru bajeti, Serikali inachukua hatua ambapo mpaka hivi sasa tumefanya utaratibu wa kuona namna ambavyo tunaweza tukabana matumizi ya ndani ya Serikali hasa katika maeneo ya matumizi ya kawaida ili kuweza kutoa fursa miradi ya wananchi isiathirike. Hilo ndiyo lilikuwa agizo la Mheshimiwa Rais kuhakikisha kwamba, tunafanya utaratibu wa kuangalia matumizi ambayo siyo ya lazima ili fedha ambayo inapatikana iweze kutekeleza miradi ya maendeleo ili bajeti ya miradi ya maendeleo isiathirike.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameendelea kutuongoza katika baadhi ya maeneo kuweza kuhakikisha kwamba tunapata fedha nyingi za kigeni ili ziweze kupunguza tatizo la uhaba wa dola ndani ya nchi na kuruhusu uhimilivu ama ustahimilivu, uimara wa bei ya kubadilishia fedha na uimara wa shilingi yetu ya Tanzania. (Makofi)
MHE. ESTHER E. MALEKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nina maswali mawili ya nyongeza; mwaka jana wakati wa Waziri wa Fedha akihitimisha hotuba ya bajeti ya mwaka 2021/2022 alisema kwamba wale wote ambao wana haki ya kupata msamaha huo watapata msamaha wa kodi hiyo, lakini mpaka sasa wanaendelea kutozwa.

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka TRA na TANESCO kuweza kubadilisha mifumo hiyo ili watu hawa waendelee kupata msamaha wa kodi hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali ina mpango gani wa kurudisha fedha hizo ambazo wamekuwa wakiwakata watu hawa ambao tayari walikuwa wamewaahidi kwamba fedha hizo hazitaendelea kukatwa? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Esther Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Kilimanjaro, shemeji yangu huyu kwa kuwatetea sana Watanzania hasa wanyonge.

Mheshimiwa Spika, nakumbuka wiki moja iliyopita alisimama kidete kuhusu ruzuku ya kahawa na Serikali tumechukua jambo hilo. Hata hili alilolileta, ni kweli tulipoanza tulianza tukiwa tuna ujaribisha mfumo huku tukiwa tunatekeleza sheria ya Bunge, kwa maana hiyo ni kweli kulitokea baadhi ya watu waliendelea kukatwa huku wakiwa wanastahili kusamehewa. Lakini tulirekebisha kwa kiwango kikubwa mifumo hiyo, kwa hiyo kama bado wapo ambao wamebakia wachache ambao wameendelea kukatwa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo tutalifanyia kazi na nielekeze Mamlaka ya Mapato kufanya haraka kumalizia wale ambao bado hawajanufaika na msamaha huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mwaka wa fedha unakwenda kuanza tutafanyia kazi na hilo la kimfumo ili kuweza kufanya sorting zote ili tunapoanza mwaka mpya tuwe tumekamilisha jambo hilo kikamilifu, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, kwanza nachelea kusema kiendacho kwa mganga hakirudi kwa sababu Kilimanjaro hata waganga walishakwisha, ninachoweza kusema tu ni kwamba kwa wale ambao kumbukumbu zao zinaonesha wamekatwa na walitakiwa wasilipe wawasiliane na Mamlaka ya Mapato kwa sababu kwenye kodi huwa kuna utaratibu wa kufanya offsetting kile ambacho ulishakilipa in advance ili kiweze kuwa offsetted wakati unalipa kinachofuata. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwamba mpaka wa Sirari ni mkubwa sana kutoka Sirari mpaka kule Nyanungu ambako ukimtaka mwananchi atoke aje apishe Sirari pale alipe kodi ya Serikali ni ngumu kidogo. Kwa nini kusiwe na kituo kidogo cha Forodha pale Witembe Itirio ili wananchi walipe mapato halali ya Serikali badala ya kufanya magendo kugombana na polisi? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nimpongeze babu yangu Mheshimiwa Mwita kwa kuleta swali hilo. Nilishapokea swali la aina hiyo pia kutoka kule Kakonko kwa ndugu yangu Aloyce, niunganishe tu kwamba baada ya Bunge wale Waheshimiwa Wabunge ambao kwenye maeneo yao wangehitaji kuwa na mpaka mpya nizungukie mimi pamoja na Naibu wangu ama wataalam wetu ili tujiridhishe na zile sifa ambazo zinatakiwa kwa ajili ya kuanzisha mpaka mpya wa Tanzania na nchi jirani kwa upande wa ofisi ya Mamlaka ya Mapato ili tuweze kuwarahisishia wananchi wanapotaka kupata huduma ya Mamlaka ya Mapato.
MHE. ESTHER E. MALEKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nina maswali mawili ya nyongeza; mwaka jana wakati wa Waziri wa Fedha akihitimisha hotuba ya bajeti ya mwaka 2021/2022 alisema kwamba wale wote ambao wana haki ya kupata msamaha huo watapata msamaha wa kodi hiyo, lakini mpaka sasa wanaendelea kutozwa.

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka TRA na TANESCO kuweza kubadilisha mifumo hiyo ili watu hawa waendelee kupata msamaha wa kodi hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali ina mpango gani wa kurudisha fedha hizo ambazo wamekuwa wakiwakata watu hawa ambao tayari walikuwa wamewaahidi kwamba fedha hizo hazitaendelea kukatwa? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Esther Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Kilimanjaro, shemeji yangu huyu kwa kuwatetea sana Watanzania hasa wanyonge.

Mheshimiwa Spika, nakumbuka wiki moja iliyopita alisimama kidete kuhusu ruzuku ya kahawa na Serikali tumechukua jambo hilo. Hata hili alilolileta, ni kweli tulipoanza tulianza tukiwa tuna ujaribisha mfumo huku tukiwa tunatekeleza sheria ya Bunge, kwa maana hiyo ni kweli kulitokea baadhi ya watu waliendelea kukatwa huku wakiwa wanastahili kusamehewa. Lakini tulirekebisha kwa kiwango kikubwa mifumo hiyo, kwa hiyo kama bado wapo ambao wamebakia wachache ambao wameendelea kukatwa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo tutalifanyia kazi na nielekeze Mamlaka ya Mapato kufanya haraka kumalizia wale ambao bado hawajanufaika na msamaha huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mwaka wa fedha unakwenda kuanza tutafanyia kazi na hilo la kimfumo ili kuweza kufanya sorting zote ili tunapoanza mwaka mpya tuwe tumekamilisha jambo hilo kikamilifu, nakushukuru.

SPIKA: Swali lake la pili lilikuwa linataka kujua kama wale ambao sasa baada ya msamaha wameendelea kukatwa fedha, je, watarejeshewa zile fedha zao? (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nachelea kusema kiendacho kwa mganga hakirudi kwa sababu Kilimanjaro hata waganga walishakwisha, ninachoweza kusema tu ni kwamba kwa wale ambao kumbukumbu zao zinaonesha wamekatwa na walitakiwa wasilipe wawasiliane na Mamlaka ya Mapato kwa sababu kwenye kodi huwa kuna utaratibu wa kufanya offsetting kile ambacho ulishakilipa in advance ili kiweze kuwa offsetted wakati unalipa kinachofuata. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwamba mpaka wa Sirari ni mkubwa sana kutoka Sirari mpaka kule Nyanungu ambako ukimtaka mwananchi atoke aje apishe Sirari pale alipe kodi ya Serikali ni ngumu kidogo. Kwa nini kusiwe na kituo kidogo cha Forodha pale Witembe Itirio ili wananchi walipe mapato halali ya Serikali badala ya kufanya magendo kugombana na polisi? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nimpongeze babu yangu Mheshimiwa Mwita kwa kuleta swali hilo. Nilishapokea swali la aina hiyo pia kutoka kule Kakonko kwa ndugu yangu Aloyce, niunganishe tu kwamba baada ya Bunge wale Waheshimiwa Wabunge ambao kwenye maeneo yao wangehitaji kuwa na mpaka mpya nizungukie mimi pamoja na Naibu wangu ama wataalam wetu ili tujiridhishe na zile sifa ambazo zinatakiwa kwa ajili ya kuanzisha mpaka mpya wa Tanzania na nchi jirani kwa upande wa ofisi ya Mamlaka ya Mapato ili tuweze kuwarahisishia wananchi wanapotaka kupata huduma ya Mamlaka ya Mapato.
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini bado kuna hela nyingi ziko pale kwenye hizi TRAT na TRAB. Kuna shilingi bilioni 600 zipo TRAB na shilingi trilioni 2.29 bado zipo TRAT.

(a) Je, Serikali mnatupa muda gani wa kuwa mmemaliza hizi hela zirudi kwenye Mfuko wa Serikali zikafanye kazi za maendeleo? (Makofi)

(b) Katika kuchelewesha huku na kusuasua, hamuoni kwamba tunaharibu mahusiano mema ya Serikali na wafanyabiashara ambao ndiyo tegemeo letu la mapato? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia jambo hili ambalo ni muhimu sana na amejenga hoja za Kibunge. Niliyaepuka haya maneno ya TRAT na TRAB lakini kwa kuwa ameshayasema ngoja niyasema tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja; fedha zile ambazo zipo zinabishaniwa kabla hazijaamuliwa haziwi fedha za Serikali ni fedha zinazobishaniwa, na katika kubishaniwa kwake na hivi sasa tumeanzisha Ofisi hiyo ya Msuluhishi, kimsingi Serikali inataka kujenga mahusiano mazuri na walipakodi, kwa sababu Serikali ingenyoosha mkono tu kwamba hapa tunachokadiria sisi ndiyo tunataka ulipe, hiyo ndiyo ingeharibu mahusiano na walipakodi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo zitakuwa fedha za Serikali mpaka pale ambapo mkono mwingine whether TRAB ama TRAT itakaposema kwamba hii sasa ni fedha ya Serikali, lakini ikiwa bado inabishaniwa Serikali inatoa fursa ya haki kutendeka na vyombo hivyo vinaongozwa na watu ambao ni maarufu katika tasnia ya sheria. Kwa hiyo, tunaamini haki itaendelea kutendeka.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuharakisha ndiyo tumetengeneza utaratibu wa kuanzisha hizi sessions maalum ili haya mambo yasiwe yanakaa sana, kwa sababu yanaondoa utulivu katika ufanyaji wa biashara.

Mheshimiwa Spika, lingine kama ambavyo nimeweka kwenye jibu la msingi, uwepo wa ofisi hii ambayo wafanyabiashara wameitamani siku nyingi ya Msuluhishi wa Masuala ya Kikodi, tunaamini na yenyewe itaenda kupunguza mrundikano wa masuala yanayobishaniwa kwa sababu sasa maeneo ambako makadirio hawakuridhiana yataenda kwa mtu mwingine ambaye hayuko kwenye mfumo ule wa kukadiria.