Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Mussa Ramadhani Sima (20 total)

MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI (K.n.y. MHE. GIMBI DOTTO MASABA) aliuliza:-
Tanzania inakabiliwa na tishio la mabadiliko ya tabianchi linalosababishwa na uchafuzi wa mazingira, hasa wa viwandani:-
Je, Serikali inatoa kauli gani kwa wamiliki wa viwanda wanaokiuka Sheria za Mazingira?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Doto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mhesimiwa Mwenyekiti, tatizo la mabadiliko ya tabianchi kwa kiwango kikubwa linasababishwa na uzalishaji wa gesi joto unaotokana na matumizi ya nishati kwa 47%, uzalishaji wa viwanda kwa 30% na usafirishaji 11% kwa shughuli za maendeleo katika nchi zinazoendelea kiviwanda hususan Ulaya, Marekani, Asia na Australia. Bara la Afrika kwa ujumla linachangia gesi joto kiasi kisichozidi 3%. Tanzania huzalisha kiasi cha tani 0.09 za hewa ukaa (Per Capital Emission) kwa mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, Tanzania inachangia kiasi kidogo sana katika tatizo la uzalishaji wa gesi joto ambazo ndiyo chanzo cha mabadiliko ya tabianchi. Hata hivyo, pamoja na kuchangia kidogo kiasi hicho Tanzania imeendelea kuathirika kutokana na athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, kama vile kupungua kwa barafu ya Mlima Kilimanjaro, kuongezeka kwa usawa wa bahari, ukame, mafuriko ya mara kwa mara na mlipuko wa magonjwa. Tatizo kubwa linatokana na uchafuzi wa mazingira unaofanywa na baadhi ya viwanda nchini kwa kutiririsha majitaka yenye sumu na kemikali ambazo huathiri sana viumbe hai pamoja na mazingira kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inayo Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya Mwaka 2004. Sheria hii imeweka misingi ya usimamizi, tathmini na kuchukua tahadhari kuhusu madhara kwa mazingira, yakiwemo ya viwandani. Kwa kuzingatia sheria hii, Serikali imekuwa ikielimisha na kuwatoza faini wamiliki wa viwanda wanaokiuka sheria hii. Aidha, wamiliki wanaoendelea kukaidi maelekezo na masharti wanayopewa hufungiwa kufanya shughuli na hupewa masharti kabla ya kuruhusiwa kuendelea na shughuli zao tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa wito kwa wamiliki wa viwanda kuzingatia utekelezaji wa sheria na mikakati mbalimbali iliyopo kwa ajili ya kuwezesha usimamizi endelevu wa hifadhi ya mazingira kwa faida yetu na vizazi vijavyo. Wamiliki wa viwanda wanatakiwa kuhakikisha Tathmini ya AAthari kwa Mazingira na Ukaguzi wa Mazingira (Environmental Audit) vinafanyika na kuzingatiwa. Aidha, wamiliki wa viwanda wanapaswa kutumia nishati rafiki kwa mazingira na kutumia teknolojia banifu katika uzalishaji wa bidhaa zao ili kusaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-
Upo uharibifu mkubwa wa mazingira katika Ukanda wa Ziwa Rukwa unaotokana na ukataji miti ovyo, wingi wa mifugo na kilimo kisichozingatia utaalamu; shughuli hizi zinahatarisha kukauka kwa ziwa hilo kwa miaka ijayo:-
Je, Serikali ina mpango gani madhubuti na wa haraka kunusuru ziwa hilo, hasa ikizingatiwa kuwa imegundulika gesi ya helium katika ziwa hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ignas Malocha, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo Oktoba, 2016 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) alifanya ziara ya kutembelea Mkoa wa Rukwa na moja ya maeneo aliyotembelea ni Bonde la Ziwa Rukwa ambapo alitoa maelekezo ya kuanza mchakato wa kulitangaza Ziwa Rukwa kama eneo nyeti la mazingira kwenye Gazeti la Serikali kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa kutangaza eneo hilo kuwa eneo nyeti unaendelea na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa kwa 2018. Eneo hilo litakapotangazwa rasmi kuwa eneo nyeti litakuwa chini ya usimamizi wa Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mzingira (NEMC) ambalo kwa kushirikiana na wadau litaandaa mpango wa matumizi ya eneo husika hivyo kuongeza nguvu ya usimamizi wa eneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Mheshimiwa Waziri alielekeza Halmashauri zote ambazo zina eneo katika Bonde la Ziwa Rukwa kuweka alama za kuonesha mwisho wa umbali wa mita 60 kutoka kwenye kingo za Ziwa Rukwa kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 pamoja na kuweka mabango ya kukataza shughuli zinazoharibu mazingira ndani ya umbali huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa eneo la Bonde la Ziwa Rukwa limebainika kuwepo kwa dalili ya gesi ya helium. Tathimini ya Athari ya Mazingira imefanyika katika hatua hii ya utafiti ili kuweza kubaini athari na madhara yoyote yanayoweza kutokea wakati wa zoezi hilo.
MHE. SAADA SALUM MKUYA aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto mbalimbali katika Muungano ambazo zinaendelea kutatuliwa mojawapo ikiwa ni ajira za Muungano ziwe asilimia 21 kwa upande wa Zanzibar.

(a) Je, ni kwa kiasi gani makubaliano hayo yametekelezwa hadi sasa?

(b) Je, ni ajira ngapi zimepatikana kwa utaratibu huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira naomba nichukue fursa hii sasa kujibu swali la Mheshimiwa Saada Mkuya Salum, Mbunge wa Welezo lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Utaratibu uliokubalika ni kwamba ajira katika taasisi za Muungano zinatakiwa kuwa kwenye uwiano wa asilimia 79 kwa watumishi wa Tanzania Bara na asilimia 21 kwa watumishi wa Zanzibar kwa utumishi wa ngazi ya utaalamu. Katika kutekeleza utaratibu wa muda wa mgao wa nafasi za ajira (quota) katika taasisi za Muungano kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Ofisi ya Makamu wa Rais ilipewa kibali cha nafasi tatu, mtumishi mmoja alipangwa Zanzibar ikiwa ni asilimia 33 na watumishi wawili walipangiwa Tanzania Bara sawa na asilimia 67.

Aidha, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ilipewa kibali cha nafasi 28 za Maafisa Mambo ya Nje na kati ya nafasi hizo saba zilijazwa na Watumishi kutoka Zanzibar ikiwa ni asilimia 25 na nafasi 21 zilijazwa na watumishi kutoka Tanzania Bara ikiwa ni asilimia 75.

(b) Tangu kufikiwa kwa makubaliano ya uratatibu wa muda wa mgao wa ajira katika Taasisi za Muungano mwaka 2013/2014 na kuanza kwa utekelezaji wa utaratibu huo mpaka sasa jumla ya wazanzibari 8 kati ya 31 wameajiriwa katika taasisi za Muungano ambao ni sawa na asilimia 25 ya waajiriwa hao. Taasisi za Muungano zina mwongozo wa utekelezaji wa makubaliano hayo na zinaendelea kuzingatia utaratibu huo wanaopata fursa ya kuajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwongozo huu ulianza kutekelezwa mwaka 2013/2014 lakini utekelezaji wake umekumbwa na changamoto ikiwa ni kusitishwa kwa ajira Serikalini kuanzia mwaka 2016 hadi 2017 kutokana na kupisha zoezi la uhakiki wa Watumishi hewa na watumishi wenye vyeti feki. Hivyo, napenda kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa taasisi zote za Muungano zilipewa utaratibu huo na zitaajiri watumishi kama ilivyoelekezwa.
MHE. ABDALLAH HAJI ALI aliuliza:-

Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo (CDCF) hutolewa kila mwaka kwa Majimbo yote ya Uchaguzi Tanzania lakini fedha hizi zimekuwa zikichelewa sana kutolewa kwa upande wa Zanzibar tofauti na Tanzania Bara:-

Je, ni sababu zipi za msingi zinazofanya fedha za mfuko huo kuchelewa kupelekwa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba nichukue fursa hii kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Haji Ali, Mbunge wa Kiwani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo ulianzishwa kwa lengo la kuchochea maendeleo ya Majimbo ya Uchaguzi ya Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kutokana na makubaliano hayo, Sheria Na.16 ya mwaka 2009 ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo katika kifungu cha 3 inamtaja Waziri anayehusika na Mfuko huo kuwa ni Waziri anayehusika na masuala ya Serikali za Mitaa.

Aidha, kifungu cha 4(2) cha Sheria kinasema kwamba, kwa upande wa Tanzania Bara ni Waziri anayehusika na Serikali za Mitaa na kwa upande wa Zanzibar ni Waziri anayehusika na masuala ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia mwaka 2010, Ofisi ya Makamu wa Rais ameratibu na kufuatilia miradi ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo kwa upande wa Zanzibar. Mchanganuo wa mgawanyo wa fedha kwa kila Jimbo kulingana na vigezo vilivyoainishwa vya idadi ya watu katika Jimbo, ukubwa wa eneo na kiwango cha umaskini hufanywa na Ofisi ya Makamu wa Rais na kuwasilishwa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi zinatakiwa kufuata utaratibu wa mgawanyo kama nilivyoeleza. Utaratibu huo ni kama ifuatavyo: Fedha zinatolewa na Wizara ya Fedha na Mipango (SMT), baada ya kutolewa, Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hufanya mchanganuo wa kila Jimbo, mchanganuo huo huwasilishwa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambapo huwasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango ya SMZ. Wizara ya Fedha na Mipango ya SMZ ndiyo inayoingiza fedha kwenye akaunti za majimbo ya Zanzibar. Hivyo, ni dhahiri kuwa hatua hizo zinaweza kusababisha ucheleweshaji wa fedha ikilinganishwa na fedha zinazotolewa katika majimbo ya Tanzania Bara. Hata hivyo, jitihada za makusudi zinafanyika ili kuhakikisha fedha hizo zinaingia kwenye akaunti za majimbo ya Zanzibar kwa wakati.
MHE. HAWA A. GHASIA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakarabati mifereji ya maji ya mvua na kuta za mito inayoingiza maji ya bahari katika Mji wa Mikindani ili kuirejesha katika hali yake ya awali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 kifungu cha 129(1) kinaeleza wajibu wa kila mamlaka ya Serikali za Mitaa kwenye eneo lake itajenga au kuandaa mifereji ya maji ya mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kumekuwepo na changamoto ya kujaa kwa maji katika maeneo mengi nchini yanayopakana na bahari kunakosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi na hivyo kufanya baadhi ya mifereji kushindwa kumudu athari zake. Kufuatia hali hii, Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira imeanza kuchukua hatua zinazolenga kuzuia na kupunguza madhara yaliyojitokeza katika maeneo yaliyoathirika nchini ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ya jumla ya maeneo haya ikiwemo Mikindani ili kuwezesha kuandaa Mpango wa Taifa wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali ipo katika hatua za kuandaa Mpango Endelevu wa Kitaifa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi (National Adaptation Plans) wenye malengo ya muda wa kati na muda mrefu ili kuboresha usimamizi wa mabadiliko nchini kwa kushirikiana na halmashauri zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kujenga uwezo wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabia nchi, tunashauri halmashauri za maeneo husika kuingiza gharama za ukarabati wa mifereji kwenye bajeti zao ili kupunguza athari zilizozidi kuongezeka kwa kuiga mfano wa Jiji la Dar es Salaam.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-

Moja kati ya majukumu ya kuimarisha Muungano ni pamoja na kuhakikisha kuwa kero zote za Muungano zinatatuliwa; na vikao vingi vimekaa na kujadili kero hizo:-

Je, ni kero ngapi tayari zimetatuliwa na zipi ambazo hadi sasa zimeshindikana kupatiwa ufumbuzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ambazo zimekwishapatiwa ufumbuzi ni 11 kati ya 15 zilizowasilishwa na kutafutiwa ufumbuzi. Changamoto nne zilizobaki zinaendelea kutafutiwa ufumbuzi na hakuna changamoto iliyoshindikana kupatiwa ufumbuzi. Dhamira ya Serikali zetu zote mbili ni kumaliza changamoto zote zinazoukabili Muungano wetu ili uendelee kuwa nguzo pekee ya kuimarisha amani, umoja na mshikamano wa nchi yetu.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-

Matumizi ya mifuko ya plastiki hapa nchini yamekuwa na athari kubwa kwenye uharibifu wa mazingira na uchafuzi wa miji yetu:-

Je, Serikali ina mikakati gani ya kuondoa matumizi ya plastiki hapa nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa matumizi ya mifuko ya plastiki yameongezeka hasa kutokana na mifuko hii kutolewa bure kwenye maduka, masoko, migahawa na maeneo mbalimbali. Aidha, kutokana na baadhi ya nchi jirani kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki na kuruhusu uzalishaji kwa ajili ya soko la nje ya nchi, kumekuwa na wimbi kubwa la uingizaji wa mifuko ya plastiki nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia hali hii na mwelekeo wa Jumuiya ya Kimataifa wa kudhibiti uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka za plastiki, Serikali inadhamiria kusitisha uzalishaji na matumizi ya mifuko ya plastiki katika siku zijazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, imeanza kuchukua hatua zifuatazo katika kuelekea kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki:-

(a) Kuhamasisha wajasiriamali, vikundi vya akinamama na vijana, sekta binafsi na viwanda kuwekeza katika uzalishaji wa mifuko mbadala ikiwemo vikapu vya asilia, mifuko ya karatasi na vitambaa;

(b) Ofisi imeendesha mikutano miwili ya wadau katika Mikoa ya Dar es Salaam tarehe 6 Novemba, 2018 na Mwanza tarehe 18 Novemba, 2018, kuelimisha umma kuhusu changamoto na athari za mifuko ya plastiki na kuhamasisha uwekezaji katika uzalishaji wa mifuko mbadala kutokana na dhamira ya Serikali kusitisha matumizi ya mifuko ya plastiki katika siku zijazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mikutano hii, wadau na wananchi waliishauri Serikali kuchukua hatua za haraka kudhibiti matumizi ya mifuko ya plastiki na kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji katika uzalishaji wa mifuko mbadala.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, napenda kuchukua fursa hii, kwa mara nyingine tena kuhimiza viwanda vinavyozalisha mifuko ya plastiki na wadau wengine kujitayarisha kwa kubadili teknolojia na kutathmini fursa zinazojitokeza katika kuzalisha mifuko mbadala hasa katika kipindi hiki cha mpito wakati taratibu za maamuzi ya Serikali zikikamilishwa.
MHE. KHADIJA HASSAN ABOUD (K.n.y. MHE. ABBAS A. H. MWINYI) aliuliza:-

Changamoto za Muungano wetu bado zipo licha ya vikao vya Kamati za pamoja kati ya SMT na SMZ kukutana mara kwa mara:-

(a) Je, ni changamoto zipi zilizopata ufumbuzi tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani?

(b) Je, changamoto hizo ni ngapi?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abbas Ali Hassan Mwinyi, Mbunge wa Fuoni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2015 mpaka 2019 Serikali ya Awamu ya Tano iliyoingia madarakani, changamoto mbili zimepatiwa ufumbuzi. Hoja zilizopatiwa ufumbuzi katika kipindi cha Serikali Awamu ya Tano ni utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia na kutoa VAT kwa asilimia sifuri kwa umeme unaouzwa na TANESCO kwa ZECO ikiwa ni pamoja na kufuta deni la kodi ya VAT lililofikia shilingi bilioni 22.9 kwa umeme uliouzwa kwa ZECO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi hizo, Ofisi ya Makamu wa Rais imeendelea kuitisha vikao vya kisekta, kutafuta ufumbuzi wa changamoto zilizobakia na zinazoendelea kujitokeza. Sekta hizo ni Sekta ya Fedha, Uchukuzi, Biashara, Mifugo, Uvuvi na Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja zilizojadiliwa ni pamoja na Taarifa ya Mapendekezo ya Tume ya Pamoja ya Fedha, hisa za SMZ zilizokuwa katika Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki na mgawanyo wa mapato yanayotokana na faida ya Benki Kuu, usajili wa vyombo vya moto, upatikanaji wa fursa za masoko Tanzania Bara, ushirikiano kati ya Taasisi ya Viwango na Zanzibar (ZBS) na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) na Mamlaka ya Chakula na Dawa ya Zanzibar (ZFDA), ZBS kupatiwa nakala ya usaili kiwango cha Afrika Mashariki ili kurahisisha usaili wa kiwango hicho kwa wakati; Leseni za viwanda, Zanzibar kuwa designated member country wa mashirika ya African Regional Intellectual Property Organization (ARIPO) na World na World Intellectual Property Organisation (WIPO) na upatikanaji wa fursa za miradi inayohusisha maendeleo ya viwango na ubora wa bidhaa kwa maendelo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo miradi inayohusu maendeleo ya wajasiriamali na kuzuiwa kwa bidhaa ya maji ya kunywa inayozalishwa Zanzibar kuingia Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali zote mbili za SMZ na SMT zimeendelea kuhakikisha kuwa makubaliano yaliyofikiwa na pande mbili yanatekelezwa na kuhakikisha kuwa changamoto zinazojitokeza zinashughulikiwa ipasavyo.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD (K.n.y. MHE. MBAROUK SALIM ALI) aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwa Watanzania hususan kizazi kipya, kuhusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ili kutoa uelewa wa pamoja na dhamira njema za Muungano huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbarouk Salum Ali, Mbunge wa Wete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua kwamba, karibu asilimia 80 ya kizazi cha sasa kimezaliwa baada ya Muungano na hivyo kuna haja ya kutoa elimu ya Muungano kwa wananchi wote, hususan vijana wa Kitanzania. Elimu hii ni muhimu kwa mustakabali wa Muungano kwani inaongeza ari ya uraia, uzalendo na kujenga undugu wa Kitaifa kati ya wananchi wa pande mbili za Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2018/2019, ofisi imetoa elimu ya Muungano kupitia vipindi vya redio na television, ili kuhakikisha makundi mbalimbali yanapata elimu ya Muungano, hususan vijana. Katika Mwaka wa Fedha 2017/ 2018, shughuli za elimu ya Muungano, hususan kwa vijana, zilitolewa kupitia kongamanko la vijana, hususan fursa zilizopo katika Muungano ambapo ilifanyika Zanzibar tarehe 22 Oktoba, 2017. Wanafunzi wa shule za msingi zilizopo Dodoma ilifanyika tarehe 18 Aprili, 2018 na Kongamano la Vyuo vya Elimu ya Juu vilivyopo Dodoma, itafanyika tarehe 21 Aprili, 2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, ofisi ilishiriki katika maonesho ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani iliyofanyika viwanja vya Mnazi Mmoja kuanzia tarehe 31 hadi tarehe 6 Juni, 2018, ambapo wananchi walipata fursa za kujulishwa kuhusu masuala ya Muungano. Pamoja na kazi hizo, ofisi ilishiriki katika vipindi vya redio, television na magazeti katika kutoa elimu ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua faida zitakazopatikana kwa kutoa elimu ya Muungano, Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, itaendelea kutoa vipaumbele katika Mwaka wa Fedha 2019/2020 na imetenga fedha kwa ajili ya kutoa elimu ya Muungano kwa vijana kupitia makongamano na warsha, ambayo yamelenga wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo vya elimu ya juu Tanzania Bara na Zanzibar.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN (K.n.y. MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF) aliuliza:-

Zanzibar kwa namna ilivyo inahitaji uchumi wa Visiwa ambapo Bandari ni kitu cha lazima:-

Je, Serikali ya Muungano inaungaje mkono nia ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kujenga Bandari kubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Suleiman Ally Yussuf, Mbunge wa Mgogoni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Bandari Na. 17 ya mwaka 2004 (The Ports Act No. 17), majukumu ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) ni kuendeleza bandari, kuendesha shughuli za bandari, kutangaza huduma za bandari na kushirikisha na kusimamia sekta binafsi katika uendelezaji na uendeshaji wa bandari.

Aidha, Shirika la Bandari Zanzibar (ZPC) lilianzishwa kwa Sheria ya Bandari ya mwaka 1997, Sheria hii ilifanyiwa marekebisho mwaka 2013. Kwa mujibu wa Sheria hiyo, ZPC ina majukumu ya kuendeleza bandari, kuendesha shughuli za bandari na kutangaza huduma za bandari ndani na nje ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Nyongeza ya Kwanza imeorodhesha Mambo ya Muungano ambapo kipengele cha 11 katika orodha ya Mambo ya Muungano kinahusu Bandari, mambo yanayohusika na usafirishaji wa anga na posta na simu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia maelekezo hayo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimeendelea kushirikiana katika masuala mbalimbali ya uendelezaji wa bandari nchini. Ushirikiano huo umedhihirika zaidi katika kupanga miradi ya kipaumbele na kutafuta fedha za uendeshaji wa miradi hiyo kutoka vyanzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Washirika wa Maendeleo. TPA na ZPC zimeendelea kushirikiana kwa utaalam na kushirikiana katika kutoa huduma za bandari nchini hususan katika uongozi wa meli kutoka nje ya nchi. Aidha, tunaendelea kuboresha ushirikiano kupitia vikao vya mara kwa mara vya Sekta za Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia maelezo hayo, Serikali ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikiunga mkono nia ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kujenga bandari kubwa ili kuimarisha miundombinu na huduma ya bandari nchini.
MHE. RITTA E. KABATI (K.n.y. MHE. MARTHA M. MLATA) aliuliza:-

Je, ni kwa nini Sherehe za Muungano zimekuwa zikifanyika na kupewa nafasi kubwa Kitaifa tu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Moses Mlata, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Singida, kama ifuatavyo-

Mheshimiwa Spika, Sherehe za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar huazimishwa kwa kuzingatia Mwongozo wa Maadhimisho na Sherehe za Kitaifa wa mwaka 2011 uliotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo ndiyo ina dhamana ya kuratibu sherehe zote za Kitaifa. Aidha, katika Mwongozo huo, Sura ya Tano katika maelezo ya Utangulizi imeelezwa kuwa “Sherehe za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar zitafanyika tarehe 26 Aprili ya kila mwaka katika uwanja wa Uhuru, Dar es Salam mahali ambapo udongo wa Tanganyika na Zanzibar ulichanganywa. Sherehe hizo zinaweza kufanyika nje ya Dar es Salam kama Kamati ya Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa itakavyoelekeza”

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuzingatia Mwongozo huo wa Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa hadi hapo kutakapokuwa na sababu za msingi zitakazofanya Mwongozo huo kufanyiwa marekebisho kwa nia ya kuuboresha. Hata hivyo, Serikali inahimiza wananchi kuadhimisha sherehe hizo kwa kufanya shughuli mbalmbali za maendeleo ikiwemo usafi, michezo, makongamano na shughuli mbalimbali za kijamii.
MHE. HALIMA J. MDEE aliuliza:-

Jiji la Dar es Salaam linakabiliwa na tatizo sugu la uchimbaji mchanga na uchafu uliokithiri;

Je, Serikali ina mikakati gani ya muda mfupi na muda mrefu kukabiliana na kero hiyo sugu na hatarishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ridhaa yako naomba kwanza nichukue fursa hii kuwapongeza Mheshimiwa George Simbachawene kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, lakini pia Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Maziringira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Kawe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna changamoto kubwa ya uchimbaji wa mchanga Dar es Salaam. Aidha, yapo machimbo ya mchanga yaliyoruhusiwa kisheria na kupata vibali kutoka mamlaka husika kama Serikali za Mitaa (Halmashauri za Jiji na Manispaa), Ofisi za Mamlaka ya Mabonde na Wizara ya Madini. Hata hivyo, upo uchimbaji holela hususan katika maeneo ya mito na machimbo mengine ya mchanga ambayo si rasmi yanayoanzishwa na wananchi katika maeneo mbalimbali. Uchimbaji wa madini ya mchanga usio rasmi ni kosa kwa mujibu wa Kifungu 6 (1) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji huu huleta athari ikiwa ni pamoja na mmomonyoko wa kingo za mito, uharibifu wa maji na miundombinu, mwingiliano wa maji ya bahari katika nchi kavu (sea water intrusion), kubadilika kwa mkondo wa mto kutoka uelekeo wa asili, kuharibika kwa uimara wa mto (channel instability), uharibifu wa mimea ya asili ambayo husaidia kupunguza mmomonyoko na uharibifu wa mazalia ya viumbe hasa wakati kina cha maji kinapoongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na hili hatua zifuatazo zinachukuliwa:

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, kuelimisha wananchi kuhusu athari za uchimbaji holela wa mchanga na kuzuia uchimbaji holela. Aidha, mamlaka mbalimbali zikiwemo Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Dar es Salaam, Mamlaka za Mabonde na Tume ya Madini kupitia Ofisi ya Madini Mkoa wa Dar es Salaam zimekuwa zikifanya ukaguzi wa mara kwa mara na hatua stahiki kwa mujibu wa sheria
huchukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili, Serikali inaandaa mkakati wa muda mrefu utakaotokana na Mapendekeo ya Kamati Maalum ya Wadau iliyoundwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kupendekeza hatua za kuchukuliwa ili kuwa na uchimbaji endelevu wa mchanga usiokiuka sheria za nchi; na kufanya tafiti na kuendeleza teknolojia za ujenzi zinazoweza kutumia mchanga kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uchafuzi wa mazingira uliokithiri, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya Mwaka 2004 Kifungu 139(1) imetoa mamlaka kwa Serikali za Mitaa kuzuia au kupunguza taka ngumu, taka vimiminika, gesi taka na taka zenye madhara. Serikali itaendelea kuelimisha wananchi na kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria. Aidha, Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia programu ya Elimu kwa Umma inatoa elimu kuhusu usimamizi na udhibiti wa taka kuanzia ngazi ya jamii, viongozi na wadau hasa katika eneo la urejelezaji wa taka ngumu. Natoa wito kwa Serikali za Mitaa kuwajibika kwa kuweka mipango endelevu na usimamizi wa taka kama ilivyobainishwa katika Kifungu 139(1) cha Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya Mwaka 2004.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWAKO aliuliza:-

Katika nchi yetu na hasa Mkoa wa Kigoma kuna vyanzo vingi vya maji (Water sources) Jimbo la Kasulu peke yake kuna vyanzo vya uhakika zaidi ya 150.

(a) Je, kwa nini Serikali haiji na Mkakati wa kina wa uhifadhi wa vyanzo vya maji katika Wilaya ya Kasulu:-

(b) ambo hili haliwezi kuachiwa Halmashauri zetu peke yake. Je, ni lini Serikali itakuja na mpango "A Comprehensive Water Sources Protection Program‟ ili vyanzo vya maji vilindwe na vitunzwe ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira na kukabiliana na madhara ya tabianchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwako, Mbunge wa Kasulu Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inayo mikakati mbalimbali ya kuhifadhi vyanzo vya maji nchini ikiwemo Wilaya ya Kasulu. Mikakati hiyo ni pamoja na:-

(i) Mkakati wa hatua za haraka za kuhifadhi mazingira ya ardhi, vyanzo vya maji nchini ulioandaliwa mwaka 2006 wenye hatua za muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu; na

(ii) Mkakati wa hatua za haraka za kuhifadhi mazingira ya bahari, maziwa, mabwawa na mito uliandaliwa mwaka 2008 kwa lengo la kuboresha mazingira ya bahari, maziwa, mabwawa na mito ili kuongeza kasi ya kulinda vyanzo vya maji kama vile mito ikiwa ni pamoja na kulinda na kuhifadhi bioanuai na rasilimali zake.

Aidha, Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na UNEP inaandaa Mradi wa urejeshaji wa mifumo ya ikolojia pamoja na hifadhi ya bioanuai katika Bonde la Mto Malagarasi, Ruaha na Ziwa Rukwa. Mradi huu utatekelezwa katika ngazi za Mgazi, Uvinza, Buhoro, Msambala na Basunzu zilizopo katika Wilaya ya Uvinza, Kasulu na Kibondo Mkoani Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iko kazini na inashirikiana na wadau wengine katika suala la kulinda vyanzo vya maji, hii ikiwa ni pamoja na kuvitambua vyanzo vya maji na kuweka mipaka na kulinda eneo hilo kwa mujibu wa Sheria. Kazi hii inafanywa na Wizara ya Maji na Umwagiliaji. Aidha, hatua mbalimbali za kisheria zinaendelea kuchukuliwa kwa waharibifu wa mazingira. (Makofi)
MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-

Dalili za maji safi na salama kuchanganyika na maji chumvi (bahari) zinatishia ustawi. Je, nini utatuzi wa tishio hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa maji safi na salama kuchanganyika na maji chumvi bahari yanatishia ustawi wa jamii na kilimo. Hali hiyo inasababishwa na athari ya mabadiliko ya tabianchi, kutokana na kuongezeka kwa joto la dunia linalosababisha na kuyeyuka kwa barafu kwenye ncha za dunia na kwenye vilele vya milima mirefu. Kuyeyuka huko kwa barafu kunasababisha maji kutiririka kwenda baharini na kuongeza ujazo wa maji ya bahari na kusambaa katika maeneo ya mwambao ambayo yana shughuli muhimu za kijamii kama vile visima vya maji, kilimo na miundombinu muhimu ambayo huingiliwa na maji chumvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti ya sita ya jopo la watalaam inaonesha kuwa ujazo wa bahari umeongezeka kwa sentimita 19 katika miaka ya hivi karibuni na kusababisha mmomonyoko wa kingo za bahari na baadhi ya maeneo ya Pwani yameingiliwa na maji chumvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utatuzi wa kudumu wa suala hili unahitaji ushirikiano wa Kimataifa hususani katika kupunguza gesi joto ambazo huchangia ongezeko la joto duniani ambalo husababisha mabadiliko ya tabia nchi. Kwa kuwa suala la kupunguza gesi joto sio rahisi kufikiwa katika kipindi kifupi nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania zinahimiza kujenga uwezo wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi ikiwemo kuchimba visima vipya, kupanda miti ya mikoko katika maeneo ya kandokando ya bahari, kujenga kuta na makinga maji pale panapowezekana na kuhamasisha shughuli za kilimo kufanya katika maeneo mengine ambayo hayajaathirika. Sambamba na suala la kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi, nchi zinazozalisha gesi joto kwa wingi zinahimizwa kupunguza gesi joto ili kuzuia athari zaidi za mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA (K.n.y. MHE. JANET Z. MBENE) aliuliza:-

Uchomaji wa mkaa kwa kiasi kikubwa unatumia miti ya asili pamoja na mapori ya akiba, ukataji wa miti hauendi sambamba na upandaji wa miti na hii ina athari kubwa sana kwenye mazingira yetu ikiwemo kupungua kwa mvua na kukauka kwa vyanzo vya maji:-

Je, ni lini Serikali itaanza kutoza ada kwa mkaa unaosafirishwa nchi za nje ili iweze kurejesha mazingira katika hali yake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira naomba kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene Mbunge Ileje kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uchomaji wa mkaa hutokanao na miti kwa kiasi kikubwa unatumiamiti ya asili pamoja na mapori ya Akiba na nidhahiti ukatajia wa miti hauendi sambamba na upandaji wa miti na hii ina athari kubwa sana katika mazingira yetu. Ikiwemo kuendelea kupotea kwa Bionuai, kupungua kwa mvua na kukauka kwa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya mkaa inafanyika katika kwa mujibu wa sheria ya misitu ya mwaka 2002 kanuni za mwaka 2004 ni miongozo mbalimbali. Aidha, usafirishaji wa mkaa nje ya nchi umezuiliwa kwa mujibu wa kifungu Na. 16 cha sheria inayozuia usafirishaji wa baadhi ya bidhaa nje ya nchi yaani The export control Act cape 381RE 200 pamoja na makatazo mengine. Vilevile tangazo la Serikali Na. 417 la tarehe 24 Mei, 2019 kifungu Na. 21(1) limetoa zuio kwa mtu yoyote kusafirisha mkaa kwenda nje ya nchi isipokuwa mkaa mbadala yaani charcoal briquettes na kwa kibali maalum kutoka kwa Waziri mwenye dhamana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa kwa sasa Serikali haisafirishi mkaa unaotokana na miti kwenda nje ya nchi kama ilivyotoa ufafanuzi hapo juu gharama za kurejeleza au kung‟oa kuondoa maeneo yaliyoharibika kutokana na shughuli za kibinadamu ikiwemo mkaa zitatokana na mapato yanayopatikana kupitia tozo mbalimbali zilizoainishwa kwenye sheria ya misitu ya mwaka 2002 ikiwepo asilimia tano ya ushuru wa halmashauri inayotozwa kwa wafanyabiashara kwa mazao ya misitu. Aidha, tozo nyingine zinazotokana na tozo za ukaguzi wa biashara ya mkaa unaotokana na mabaki ya miti au mimea kwa maana ya briquettes ambao unaruhusiwa kwenda nje ya nchi.
MHE. MWANTUM DAU HAJI aliuliza:-

Kasi ya mmomonyoko wa ardhi na uhaba wa udongo katika Visiwa vya Unguja na Pemba inatishia uhai wa Visiwa hivyo:-

Je, ni hatua zipi za makusudi zimechukuliwa katika kuvinusuru Visiwa hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), naomba nichukue fursa hii sasa kujibu swali la Mheshimiwa Mwantum Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Visiwa vya Unguja na Pemba vina maeneo takribani 148 yaliyoathirika na mabadiliko ya tabianchi (Pemba 125 na Unguja 23). Athari hizi ni pamoja na mmomonyoko wa fukwe na kuingia kwa maji ya bahari katika mashamba na makazi ya watu. Ili kuvinusuru visiwa hivi dhidi ya athari ya mabadiliko ya tabianchi, Serikali imechukua hatua mbalimbali kupitia miradi inayofadhiliwa na Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Mradi wa kujenga uwezo wa jamii kuhimili athari ya mabadiliko ya tabianchi (LDCF) ambao umetekelezwa mwaka 2012 - 2018, shughuli zifuatazo zimefanyika: Ujenzi wa kuta mbili za mita 25 kila moja katika eneo la Kisiwa Panza - Pemba na ujenzi wa makinga bahari (gloynes) matano ya wastani wa urefu wa mita 100 kila moja katika eneo la urefu wa mita 538 Kilimani
– Unguja; upandaji mikoko Pemba maeneo ya Kisiwa Panza hekta 200, Tumbe hekta 10, Ukele hekta 7 na Tovuni hekta 1; na upandaji mikoko Unguja maeneo ya Kisakasaka hekta 8 na Kilimani hekta 1.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kupitia Mradi wa Kupunguza Uhalibifu wa Ardhi na Kuongeza Uzalishaji wa Chakula katika Maeneo Kame nchini mwaka (2017 - 2022), shughuli zifuatazo zinategemewa kufanyika katika maeneo ya Micheweni, Kata ya Micheweni na Kiuyu Maziwang’ombe ambazo ni: Kujenga makinga maji katika mashamba (dykes) ili kuzuia maji ya bahari kuingia katika mashamba; kutoa elimu kuhusu kilimo kinachokabiliana na mabadiliko ya tabianchi kupitia mashamba darasa; upandaji wa miti ili kuhifadhi udongo na kutunza mazingira; na uanzishaji wa biashara ndogo ndogo ili kuwezesha jamii kuwa na shughuli mbadala za kujiongezea kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi; kudhibiti mmomonyoko wa udongo; na kukabiliana na uhaba wa udongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-

Kwa mujibu wa taarifa ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ya mwaka 2014, Kisiwa cha Latham ni mali ya Zanzibar tangu kilipofunguliwa rasmi mwaka 1898. Hata hivyo, zipo taarifa zilizothibitishwa kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu iliiandikia Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuwaarifu kuwa Kisiwa hicho ni cha Tanzania Bara.

(a) Je, ni lini Serikali hizi mbili ambazo ni ndugu wa damu watakaa kutatua kero hii ya muda mrefu?

(b) Je, Serikali haioni kuwa umefika muda muafaka kulifanyia kazi suala hilo?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashim Ayoub lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83, Ibara ya 2(1) inatamka wazi kuwa eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni eneo lote la Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar pamoja na sehemu ya bahari ambayo inapakana na nchi za Kenya, Shelisheli, Comoro na Msumbiji. Hivyo basi, kwa mujibu wa tafsiri ya mipaka hiyo, Kisiwa cha Latham (Fungu Baraka) kiko ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mgogoro wa umiliki wa eneo la kisiwa hicho kwa vile kimo ndani ya mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:-

Kwa kuwa Muungano wetu ni Tunu na tunahitaji kuwatunza hata wazee wetu wanne walioshiriki kuchanganya mchanga wa Muungano wetu baina ya Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar:-

(a) Je, Serikali inawaangalia vipi wazee wetu hao wanne kwa kuwapa ahsante baada ya utu uzima kuwafikia?

(b) Wakati wa sherehe za Muungano, wazee hao hufikishwa kwenye sherehe; je, huko ndiko kuonesha Serikali inawatunza?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua michango ya watu mbalimbali walioshiriki katika ukombozi na Nchi yetu na ujenzi wa Taifa ikiwa ni pamoja wazee wetu walioshiriki katika tukio la kuchanganya udongo tarehe 26 Aprili, 1964. Kundi hili ni moja kati ya makundi mengi yaliyotoa mchango wa hali na mali katika kulijenga Taifa hili ikiwemo wastaafu na walioshiriki katika vita vya Kagera. Hata hivyo, kwa sasa hakuna sheria mahsusi ya ahsante au malipo kwa watu waliofanya mambo makubwa yanayojenga historia ya nchi.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwashirikisha wazee hawa katika maadhimisho ya sherehe za Muungano ni sehemu ya kutambua mchango wao na kukumbuka tukio muhimu la uchanganyaji wa udongo wa Tanganyika na Zanzibar. Ushiriki wao huwezeshwa na Ofisi ya Makamu wa Rais. Aidha, pamoja na wazee hawa, yapo makundi mengine ya wazee ambao kwa namna moja au nyingine walitoa mchango wao katika ujenzi wa Taifa ambao pia hualikwa kushiriki katika maadhimisho hayo mfano Viongozi Wastaafu na Wanasiasa Wakongwe.

Hata hivyo, Serikali yetu ni sikivu sana na moja ya vipaumbele vyake ni kuhakikisha inawaenzi watu wake wote ambao wamechangia kwa namna moja au nyingine kuifanya Tanzania ya leo na pia kuendelea kulinda historia kwa ajili ya faida ya kizazi kilichopo na kijacho.
MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-

Athari za mabadiliko ya tabianchi zimesababisha uharibifu mkubwa katika Bandari ya Tanga eneo la deep sea lango kuu la kuingia na kutokea katika bandari hiyo:-

Je, Serikali inachukua hatua gani za dharura kudhibiti uhalibifu huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa niaba ya Waziri Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said haji Mbunge wa Konde kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, athari za mabadiliko ya tabianchi zinatofautiana katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo maeneo ya Ukanda wa Pwani ambapo ni muhimu kwa shughuli za uchumi. Ofisi ya Makamu wa Rais imeendelea kuchukua hatua za makusudi katika kukabiliana na athari hizo ikiwa ni pamoja na kuandaa na kutekeleza Mkakati wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi wa Mwaka 2007 na Mkakati wa Mabadiliko ya Tabianchi wa Mwaka 2012. Mipango hii imeelekeza hatua za haraka za kuhimili mabadiliko ya tabianchi katika sekta muhimu ikiwemo maji, maliasili, miundombinu, afya, nishati, Ukanda wa Pwani na maeneo ya bahari.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la ufukwe lijulikanalo kama deep sea lililopo katika Jiji la Tanga linakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo athari za kimazingira kama vile utupaji holela wa taka hasa za plastiki na taka zingine ambazo huletwa na mifereji ya maji ya mvua inayoingia baharini kuto katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Tanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hatua zilizochukuliwa na Serikali na Halmashauri ya Jiji la Tanga katika kuhifadhi na kulinda eneo hili dhidi ya uchafuzi wa mazingira ni pamoja na kufanya kampeni za usafi wa mazingira zikihusisha wavuvi, wafanyabiashara na vikundi vya mazingira. Pia kutoa elimu kwa wavuvi na wadau wengine katika eneo hili kuhusu usafi wa mazingira na kuhifadhi miti na uoto wa asili kuzunguka fukwe hizo.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:-

Je, Serikali inafaidikaje na rasilimali ya miti ya mikoko iliyoanzia katika Ukanda wa Pwani ya Tanga mpaka Mtwara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, umuhimu wa misitu ya mikoko ni pamoja na kuwa mazalia na makazi ya viumbe wa baharini; nan i moja ya vivutio vya utalii nchini; na ni mfumo ikolojia unaosaidia kuondoa kiwango kikubwa cha hewa ukaa (carbon sequestration) ambayo ingeweza kuongeza kiwango cha joto la dunia na kusababisha mabadiliko ya tabia nchi. Aidha, misitu hii huhifadhi fukwe na mazingira ya bahari kwa kuzuia uharibifu utokanao na mmomonyoko wa fukwe na kingo za bahari, hivyo kuokoa mali na maisha ya makazi ya wakazi wa Pwani kutokana na vimbunga, dhoruba na mawimbi ya bahari.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile misitu hii husaidia kuchuja udongo, uchafu na sumu zinazoweza kutiririshwa na maji yanayoingia baharini ambayo huchangia kuharibu matumbawe ambapo ni makazi ya mazalia ya samaki wa aina mbalimbali. Kwa hiyo, miti ya mikoko ina umuhimu kwa Taifa kama sehemu muhimu ya hifadhi ya ikolojia, huipatia jamii chakula na kipato kupitia shughuli za ujenzi, ufugaji nyuki na kuongeza pato la kaya pia ni chanzo cha mapato kwa Serikali kupitia vibali vya kuvuna miti ya mikoko na biashara ya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu wa misitu ya mikoko nchini, misitu hii imekuwa ikihifadhiwa tangu kabla ya uhuru kwa kuchukua hatua ikiwemo kutunga sheria ijulikanayo kama The Tanganyika Forest Laws and Rules Handbook ya mwaka 1947. Baada ya uhuru Serikali imeendelea na jitihada za kuhakikisha mikoko inalindwa. Mwaka 1987 Serikali ilipiga marufuku ukataji wa miti ya mikoko hadi mwaka 1991 ulipoandaliwa mpango wa usimamizi wa mikoko. Chini ya mpango huu, misitu ya mikoko imeendelea kuhifadhiwa na ukataji wake hufanyika kwa kibali maalum kutoka Wakala wa Misitu Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuhifadhi misitu hii, Tanzania inachangia katika malengo ya kidunia ya kupunguza hewa ukaa na kupunguza athari zinazotokana na mabadiliko ya tabia nchi. Kwa kuzingatia umuhimu wa rasilimali hii, nawasihi wadau wote wakiwemo wananchi wa maeneo ya Pwani na Serikali zote za Mitaa kushirikiana katika kuitunza na kuihifadhi kwa manufaa ya Taifa.