Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Lazaro Samuel Nyalandu (1 total)

MHE. LAZARO S. NYALANDU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na kwa kweli Serikali nzima, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa wanavyoshughulikia suala zima la maji katika maeneo ya vijiji tunavyotoka. Nawashukuru sana kwa niaba ya wananchi wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la pili, naomba nitoe ombi la pekee, wananchi wa Tarafa ya Mtinko na Mji Mdogo wa Mtinko ambao ni mji unaokuwa kwa kasi sana na una watu wengi. Mfumo wao wa maji ulitegemea kuwepo na pampu iliyoharibika na hapa tunavyozungumza kuna dharura kubwa sana ya maji katika Mji huu Mdogo wa Mtinko. Naomba kwa kadri inavyowezekana Serikali iangalie uwezekano wa haraka wa kuweza kusaidia tatizo hili la Mtinko. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, ameipongeza Serikali kwa kutekeleza miradi ya maji hapa nchini, Mheshimiwa Nyalandu nakushukuru sana lakini pia na mimi nakupongeza wewe kwa sababu juhudi kubwa umeifanya katika Jimbo lako. Pamoja na Serikali kuwa na Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji lakini wewe mwenyewe binafsi umekuwa unawasiliana na wafadhili ndiyo maana jimbo lako limefikia katika hatua hii. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu ombi lako la pumpu tunalichukua na nakuomba Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane leo leo, tushirikiane pamoja na Mkurugenzi hili ni tatizo dogo ili tuhakikishe pumpu hii inapatikana kwa haraka ili wananchi wa Mtinko wapate maji.