Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Oliver Daniel Semuguruka (17 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuwa mahali hapa katika Bunge lako Tukufu. Pia napenda kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayozidi kuifanya. Mimi binafsi namwombea kwa Mwenyezi Mungu aendelee kumpa nguvu tele aendelee kutumbua majipu. Ewe Mwenyezi Mungu msaidie Rais wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri wanazozifanya kwa kulitumikia Taifa letu kwa moyo wa dhati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuwashukuru akinamama wa Mkoa wa Kagera kwa kunipigia kura nyingi za kutosha ili niweze kuwawakilisha katika Bunge lako Tukufu. Nawaahidi kwa moyo wangu wa dhati sitowaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze moja kwa moja katika mchango wangu katika Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambayo ni Wizara nyeti inayotegemewa na watu wengi. Mkoa wa Kagera tumebarikiwa kuwa na ardhi nzuri yenye rutuba na hali ya hewa nzuri yenye mvua za kutosha. Mkoa wa Kagera kilimo kimekuwa cha kusuasua kwa sababu ya teknolojia duni pamoja na pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera pembejeo hazifiki kwa wakati, unakuta mkulima ameshaandaa shamba lake kwa muda mrefu lakini kupata mbolea au mbegu bora kwa muda unaotakiwa imekuwa ni changamoto kwani mbolea haifiki wala mbegu. Kwa hiyo, naomba Serikali yako Tukufu iweze kuliangalia hilo. Pia kuna miundombinu mibovu ya usafiri wa mazao kutoka shambani hadi kwenye masoko, hilo pia naomba liangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera tuna zao kuu ambalo ni mgomba (ndizi). Zao hilo limevamiwa na ugonjwa unaitwa mnyauko hasa kwa Wilaya za Ngara, Karagwe, Muleba na Bukoba Vijijini. Ugonjwa huo wa mnyauko umeshambulia sana migomba. Tunaomba Wizara husika iweze kuangalia jinsi itakavyoweza kutusaidia kutibu ugonjwa huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wangu wa Kagera umebarikiwa kuwa na mazao makuu mawili ya biashara nayo ni kahawa na miwa. Kuhusu kahawa masoko yamekuwa ya kusuasua, imefika hatua wakulima wanapata shida, wanaanza kukata tamaa ya kulima zao la kahawa kwa kukosa soko. Unakuta wanaanza kufanya magendo ya kwenda kuuzia nchi jirani ili wapate unafuu wa bei. Tunaomba Wizara husika iangalie zao letu la kahawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu zao la miwa, Mkoa wa Kagera pia umebarikiwa kuwa na Kiwanda kikubwa cha Sukari. Hata hivyo, nashauri wale wakulima wadogo wadogo waweze kusaidiwa kuwapa mashamba darasa ili waweze kuungana na wale wenye mashamba makubwa ili tuweze kupata viwanda vya kutosha vya sukari.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niongelee kuhusu mifugo. Mkoa wa Kagera una mgogoro kati ya Ranchi ya Kitengule na wananchi. Wananchi hawana sehemu ya kufugia mifugo yao, tunaiomba Serikali kushughulikia mgogoro huo haraka iwezekanavyo. Kagera tuna mifugo ya kutosha, inakadiriwa kuwa na ng‟ombe wanaofugwa wapatao 550,070, ng‟ombe wa asili wanakadiriwa kuwa 528,632 na ng‟ombe wa maziwa 21,438, mbuzi wafugwao wanakadiriwa kuwa 593, 607, mbuzi wa asili wanakadiriwa kuwa 583,202 na mbuzi wa maziwa 10,405. Wanyama wengine ni kondoo 53,061 na nguruwe 44,402. Ikitumiwa vizuri na Serikali itasaidia sana ukuaji wa uchumi Mkoa wa Kagera na Taifa kwa ujumla. Kwani itachochea ujenzi wa viwanda vya mazao ya mifugo na kutoa fursa za ajira kwa wananchi walio wengi hususani vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia kuongelea upande wa uvuvi. Usalama wa wavuvi siyo mzuri katika Mkoa wetu wa Kagera. Maharamia wanavamia sana wavuvi wanaokuwa ziwani wakivua samaki. Tunaomba Serikali iweke doria ili wavuvi wetu waweze kuwa katika security. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu leseni, nashauri wasitoze zaidi ya mara moja. Unakuta mvuvi yupo Bukoba Mjini akiamua kwenda Muleba akifika pale kuna leseni tena anatakiwa alipie. Tunaomba leseni iwe moja ili waweze kuzunguka kwa unafuu zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali yako iangalie kuhusu nyavu. Wavuvi wadogo hawana makosa kununua hizo nyavu, washughulikiwe wale wanaoziingiza ili wapate zinazokubalika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba Serikali yako kwa hiyo shilingi milioni hamsini ambayo inatarajiwa kutolewa iangalie na wavuvi. Hiyo shilingi milioni hamsini imezungumziwa sana upande wa akinamama na vijana lakini kwa wavuvi sijasikia. Naomba pia wavuvi wakumbukwe, wana vikundi vyao nao wagawiwe hela hiyo ili waweze kujiongeza katika uchumi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya machache naunga mkono kwa asilimia mia moja bajeti ya Wizara ya Kilimo iweze kupita.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na pia kuwa mchangiaji wa kwanza katika Bunge lako Tukufu jioni hii. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anazozifanya katika Taifa letu. Pia nazipongeza Kamati zote mbili pamoja na Mawaziri na Wizara husika kwa ushirikiano wanaoutoa kwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze moja kwa moja kuchangia hoja zote mbili zilipo mbele yetu. Kwanza kabisa nianze na ripoti ya Nishati na Madini. Nianze kumshukuru Waziri wa Nishati kwa kuwezesha kupata umeme katika Wilaya yetu ya Ngara, lakini kuna vijiji ambavyo havijapata umeme, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini, nasikitika kwa kuwa simuoni humu ndani, lakini Naibu Waziri yupo, naomba alisikize hili. Kuna kaya ambazo hazijapa umeme katika Wilaya yetu ya Ngara, naomba wajitahidi wamalizie ili waweze kupata umeme. Kwa mfano, unaweza ukakuta kuna kaya mimi nina umeme, Mheshimiwa Matembe hana umema, Mheshimiwa Kangi ana umeme, ndiyo ilivyo. Kwa hiyo naomba kila Kaya wapate umeme, kwa kweli wanafanya kazi nzuri na nampongeza sana Mheshimiwa Rais, bila yeye hata tusingeweza hata kupata umeme huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze moja kwa moja katika mradi wa Kabanga nickel, ambao uko Wilaya ya Ngara. Mradi wa Kabanga nickel umesemwa muda mrefu sana, pindi niko shule ya msingi, mpaka sasa hivi nazeeka unaitwa ni mradi tu wa Kabanga nickel, lakini hakuna kitu ambacho tunakiona. Kwa hiyo, ninaomba, naishukuru sana Serikali kwa kurudisha leseni ya Kabanga nickel Serikalini, lakini naomba Mwekezaji wanayemtafuta Serikali awe ni mwekezaji kweli, kwa sababu kuna wawekezaji ambao ni makanjanja. Nimesema tangu niko primary wanakuja wawekezaji wanatafuta research kwamba kuna madini ya Kabanga nickel wakifika wanaondoka, hamna kinachoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati niko shule ya msingi nilikuwa naona ndege zinapita, unaambiwa zinaenda Kabanga nickel kuangalia madini yanavyoendelea. Baada ya muda wale watu wana disappear, hiyo research gani inayofanyika? Kweli mimi mpaka nafika umri huu, hiyo ni research kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishukuru kwamba Mheshimiwa Rais ameweza kuliona hili na kurudisha leseni Serikalini. Naomba iwe kweli kweli, sababu wananchi wa Wilaya ya Ngara wanahitaji kunufaika na mgodi ule, kwa sababu bila kunufaika na mgodi ule, wanaishia tu kuona majengo, kuna majengo yamejengwa na pale na Kabanga nickel, ukienda pale ni Kabanga nickel. Kwa hiyo ni vema zaidi tuweze kupata ushirikiano na Serikali walete Mwekezaji wa kweli, asiwe Mwekezaji wa uongo uongo ili tuweze kunufaika na hayo madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, madini haya yanapatikana Ngara mpaka Congo, Congo yapo nafikiri kwa asilimia 65, pia yaani huo mkondo unaanzia Ngara mpaka Congo. Sasa kwa nini Congo waendelee kunufaika sisi Tanzania tusinufaike au ni kwa sababu tuko mpakani. Kwa hiyo, naomba Waziri wa Madini na Naibu wake wanisikilize kwa makini, kuna ujenzi wa reli ya kati, tunapenda ikitokea tuweze kunufaika na hii reli ya kati, tupate kusafirisha haya madini yetu ili yaweze kununuliwa huko nje, lakini sasa hakuna hakuna kinachoendelea.(Makofi)

Naomba niongelee pia Jimbo la Kyerwa; madini ya tin, naiomba Serikali ifanye haraka kukamilisha taratibu za kuruhusu kusafirisha tin kwenda kwenye masoko ya nje. Wananchi wa Kyerwa wanasubiri kwa hamu sana ili waweze kunufaika na hayo madini ya Kyerwa. Pia naomba wananchi wapate mafunzo ili wanufaike katika mgodi ule kwa sababu kuna ambao wanaenda kuchimbia vijembe, akifika kule mara unaporomoka udongo umemuua, kuna vifo vingi vimetokea. Jamani hivi kweli hatuwezi kuangalia hili kwa jicho la huruma?

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Kyerwa wanapenda sana wanufaike na haya madini ya tin, lakini hakuna mafunzo yanayotolewa kwa wananchi. Pia wachimbaji hawana vitendea kazi, ndiyo kama huo mfano nilioutoa, vitendea kazi anaenda na kajembe kake amekaweka begani, kajembe ka kawaida, hawezi kuambiwa kwamba kuna kitu hiki kinatakiwa kifanyike uchimbe hivi uende urefu fulani hivi, hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwona pale Naibu Waziri wa Madini, naomba mtusaidie ili tuweze wale wachimbaji wadogo wadogo wa Kyerwa waweze kupata elimu ya kuweza kujua hapa nikienda kuchimba na haka kajembe hakatanisaidia au mwisho wa siku atafariki, ataacha familia yake inateseka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naiomba sana sana Wizara ya Madini iangalie kwa jicho la huruma mradi, mgodi wa Kabanga nickel na mgodi wa Kyerwa, kwa kweli nawaomba sana sana. Mheshimiwa Rais wetu mpenzi anasaidia wanyonge, sasa hawa wachimbaji wadogo wadogo na wale watu wa hali ya chini, tulisipowasaidia inaleta ukakasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuna ripoti mbili za Kamati ziko mbele yetu. Naomba nijielekeze katika ulinzi na usalama. Wilaya yetu ya Ngara, mimi ni mzaliwa wa Ngara japo ni Mbunge wa Mkoa Kagera Viti Maalum, lakini wahamiaji haramu wako wengi. Hao wahamiaji haramu wanatokea Burundi, wanapita njia za panya, njia za chocho, kwa hiyo wakipita njia za panya wanakuja kutudhuru sisi Watanzania ambao tuko mpakani. Kwa hiyo, naomba Serikali itusaidie kupata magari mapya na mafuta ya kutosha ambayo yatafanya doria, masaa 24.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika kusema ilikuwa ni mwaka juzi, 2017, kuna Afisa wa Uhamiaji alipata ajali na akafariki kwa sababu ya gari bovu na alikuwa anaenda kwenye doria katika hizo njia za panya za uhamiaji. Sasa naomba tuweze kupata magari ya kutosha mapya na tuweze kupata mafuta ya kutosha ili hata wale Maaskari wa Uhamiaji waweze kufanya kazi zao bila kipingamizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikirudi Karagwe, ni mpakani pia tunapakana na Uganda, Rwanda na Burundi yaani kuna Ziwa linazunguka. Naomba upande wa Karagwe barabara siyo rafiki kabisa, barabara ni za shida sana. Naomba Wizara hii ya Usalama na Mheshimiwa Kangi, babu yangu ananisikia, watuwekee barabara rafiki ili hata mtu akienda kufanya doria aweze kufika. Katika hilo naomba sana sana kwa Mheshimiwa Kangi, Waziri wa Mambo ya Ndani atusikilize na atuangalie kwa jicho la huruma; kule Karagwe kuna maziwa mfano Ziwa Ngoma, Buligi, Kavunjo, Nyamlebe, tunaomba kupatiwa boti ili doria ziweze kufanya kazi kwa urahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaomba kuwepo kwa boti kutasaidia kupambana na biashara haramu zinazofanyika majini kwa sababu ile Karagwe imezungukwa na ziwa. Kwa hiyo, tusipopata boti ndiyo hivyo wahamiaji haramu wanatusumbua wanatoka, Uganda, Rwanda na Burundi hakuna tunachofaidika. Kwa hiyo Mheshimiwa Kangi, babu yangu Waziri wa Mambo ya ndani, naomba ulifanyie kazi tupate boti kwa ajili ya kusadia wananchi ambao wako Karagwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda Misenyi, Wilaya ya Misenyi kwenye Kituo cha Ushuru wa Pamoja na Uganda yaani tulijiunga Kituo cha Ushuru Uganda na Tanzania. Kile kituo kazi kinafanya kazi twenty four hours, lakini Maaskari wa Uhamiaji ni wachache, hawatoshi, yaani mtu anaweza aka-overnight, akaja akashinda, hivyo. Kwa hiyo hatafanya kazi kwa ufanisi, naomba tuongezewe Maaskari wa Uhamiaji, pale ni mpakani, ukitoka tu pale Mutukula unaingia Uganda. Kwa hiyo wanaotoka Uganda kuja Tanzania wengi ni wahamiaji, sasa tutawajuaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto tuliyonayo Maaskari wa Uhamiaji ni wachache, mtu mwingine anaweza akachoka hata asiweze kufuatilia aanze kuangalia pasipoti imetoka wapi na inaenda wapi. Kwa hiyo, tukipata Maaskari wa kutosha wa kuwa wanapeana shift itatusaidia hata sisi. Kwa hiyo naomba sana sana Mheshimiwa Kangi babu yangu atusaidie katika hilo. Tangu mwaka jana 2018 ndiyo huo muungano ulifanyika Uganda na Tanzania, lakini ndugu zetu wa kule Uganda wana Maaskari wa kutosha wa Uhamiaji why kwetu tusipate wale Maaskari wa uhamiaji wa kutosha? Ni kwamba hawapo au ni ile kutokupanga kwamba ukiambiwa uende Kagera ni mpakani huko, kama changamoto tunazozipata kwamba ukienda huko kuna Wanyarwanda, kuna Wahutu, utauawa no siyo hivyo, mimi nimezaliwa Ngara lakini kuna shida hizo za wahamiaji, lakini wakitusaidia katika kuleta Maaskari yanaisha. Kwa hiyo naomba hilo lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, gari la uhamiaji la Misenyi ni chakavu chakavu yaani halifai katika kufanya doria, hivi kweli tuko Tanzania na tuko mpakani mwa Uganda? Yaani Maaskari wa Uganda ndiyo wanasaidia kwamba huyu ni mhamiaji kutoka Uganda, huyu ni Mganda amekujaje Tanzania yaani ni aibu, kwa hiyo naomba sana sana, waweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna tishio la usalama mpakani, kama madawa ya kulevya ni ngumu sana kubainika sababu mbwa aliyepo pale Misenyi amezeeka, hata akifundishwa hawezi kufundishika. Sasa tunafanya kitu gani? Kwa hiyo naomba wahusika watulee mbwa ambaye bado ni kijana sijui niseme yaani ambaye anaweza kufundishika akaelewa. Kwa hiyo naomba sana sana, Wizara ya Mambo ya Ndani muweze kutuangalia kwa jicho la huruma.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, naona dakika zimeisha nilikuwa nayo mengi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipatia nafasi. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii na kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa najikita katika Sheria ya Mtandao iliyopitishwa na Bunge lako Tukufu mwaka jana. Naona hii sheria haijafahamika vizuri kwa wananchi, nilikuwa naomba Serikali iweze kufuatilia kwa undani zaidi utumiaji wa hii Sheria ya Mitandao. Je, ni lini Wizara yako itatoa elimu ili watu waielewe hii Sheria ya Mitandao, maana mitandao inatumika ndivyo sivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba pia kuhusu simu. Ni lini simu zitakuwa na rate moja? Kwa mfano, mtandao wa Vodacom au Airtel na Tigo kuwa na rate moja? Nilikuwa naomba pia Serikali iweze kulingalia hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mkongo wa Taifa umeenea nchi nzima, lakini internet inasumbua sana, baadhi ya maeneo ni shida. Unaweza uka-download kitu kwa muda wa masaa mawili, document. Labda una haraka sana ya kwenda sehemu unataka document uwasilishe sehemu, lakini inakuwa ni shida, nini maana ya kuweka Mkongo wa Taifa zima?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia network kwa vijijini imekuwa shida sana. Mtu unaenda vijijini unabeba simu tatu, atleast, upate communication. Unabeba labda simu ya Vodacom, Airtel na TTCL, hapo pote unatafuta communication. Nilikuwa naomba pia, hili iweze kuliangalia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najikita moja kwa moja katika SUMATRA. Mara nyingi tunasikia SUMATRA ikidhibiti nauli za mabasi na treni, lakini kwenye nauli za ndege hakuna kudhibiti, ukiuliza unaambiwa inategemea soko kwa kuwa ni huria. Mbona basi ni huria na inazidhibitiwa? Unakuta ndege, kila ndege ina nauli yake, unakuta FastJet ina nauli yake, ATCL ina nauli yake, kila ndege ina nauli yake. Tulikuwa tunaomba na hili nalo muweze kuangalia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa Kagera Airport. Kagera tuna Kagera Airport, lakini pia Ngara tuna uwanja wa ndege unaitwa Luganzo Airport. Huo uwanja wa Luganzo ulishasahaulika kabisa, hata hauongelewi katika Ilani ya CCM sijawahi kuona. Ule uwanja ulitumika sana kipindi cha wakimbizi, ndege zote za UN tulikuwa tunatumia pale. Na mimi ni mmoja wapo nilikuwa nafanya kazi UN, ndio tulikuwa tunatumia hata kuleta mizigo, cargo zote za wakimbizi zilikuwa zinatumia huo uwanja, lakini uwanja umesahaulika kabisa. Tunaomba Wizara hii iweze kuangalia ule uwanja wa Luganzo kama Serikali inaweza ikaanza kuutumia ili hata wawekezaji wa ndege waweze kutumia ule uwanja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najikita pia katika ujenzi wa nyumba za watumishi wa umma. Watumishi wa umma wana tatizo la makazi kutokana na uhaba wa nyumba za Serikali. Unakuta mtumishi wa Serikali amehamishwa kutoka kituo kimoja kwenda kingine, anakaa hotelini muda mrefu sana, hapa hela za Serikali zinazidi kutumika. Kabla ya kuhamishwa kwa nini asitafutiwe nyumba ili Serikali kuweza kuangalia hizo hela zisiende bure. Nyumba hazina hadhi bora kwa…
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naunga mkono hoja asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna matatizo mengi kwa wananchi hasa wakazi wa maeneo ya karibu na hifadhi. Wananchi wanataka kulima na kufuga, maeneo wanayoishi yamejaa, hayawatoshi. Wanaona kuna eneo jirani miaka yote lipo wazi na lina rutuba nzuri ya kilimo, wanaingia kulima na kufuga, wanakamatwa na kufunguliwa mashtaka ya uvamizi wa Hifadhi ya Taifa. Nini maana ya neno hifadhi ya Taifa maana isijekuwa inatumika sivyo. Hifadhi haina zuio lolote la mipaka inayojulikana kwa kijiji ikiwamo vibao vya kutambulisha hifadhi au fence.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi haina hata wanayamapori; kama ni hifadhi ya ardhi kwa wananchi kuitumia baadae basi ijulikane ni kwa matumizi yapi na hiyo baadae labda ndio imefika sasa kwa maana hifadhi nyingi za aina hiyo zimetengwa tokea ukoloni na zingine ni zaidi ya miaka 40. Je, Serikali ina mipango gani ya kutambulisha maeneo ya uhalisia wa leo na mwaka ulioanza kuwa hifadhi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utalii; utalii unajulikana kwa matangazo. Tanzania ni nchi ya pili duniani kwa vivutio vya utalii ya kwanza ikiwa ni Brazil, lakini ni nchi inayopata watalii wachache sana kulinganisha na nchi zenye vivutio vichache. Watalii milioni moja tu wakati vivutio kibao, amani na utulivu inakuwaje nchi kama Misri yenye tatizo la usalama inapata watalii zaidi ya milioni ishirini kwa mwaka? Nchi kama Mauritania yenye vivutio vichache mno nayo inatushinda? Je, Wizara kweli inafanya matangazo? Makampuni ya utalii yanajihusishaje na kuuza utalii? Tunayo kweli makampuni ya utali maarufu ya kimataifa? Tunahitaji kuona utalii ukitangazwa kila kona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Ndege ni zao kubwa la utalii. ATCL haipo Kimataifa; ni nini mipango ya Serikali kufanya biashara ya utalii na ATCL kwa makampuni ya utalii kuwa na hisa ATCL? Ushauri wangu kwa Wizara ni kuhamasisha bidhaa za Tanzania hasa kazi za mikono kuuzwa kwenye maduka ya airports kubwa kama London - Heathrow, Schiphol - Amsterdam, Frankfurt - German na kadhalika. Jina Tanzania lionekane kila sehemu, linakuza hamu ya watu kuja kufanya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia unaweza kufanya mikakati ya kuandaa vijana 100 kwenye miji mikubwa yenye watalii na kumvalisha nguo zenye maandishi ya Tanzania huku wakishikilia mabango na kuzunguka mitaani. Vijana hao wanalipwa ujira mdogo tu. Wizara ihakikishe jina Tanzania linasikika kila kona ya dunia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi zinazotozwa kwenye hotels za kitalii ni kubwa au ni hotels zenyewe maana hotels ni ghali sana ikiwemo chakula. Watalii wengi wanaokuja nchini ni wale ambao wamejibana kwa muda mrefu hivyo kutokuwa na pesa nyingi kutosheleza matumizi makubwa. Tuweke bei nafuu kuvutia watalii kuja nchini kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera ni mojawapo ya Mkoa wenye upungufu mkubwa wa Madaktari. Katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, wanahitajika Madaktari (MD) 30; waliopo ni 12, pungufu ni 19. Madaktari Bingwa wanaohitajika ni 24 ila wapo watatu. Daktari Bingwa wa magojwa ya akinamama, Daktari Bingwa wa meno na Daktari Bingwa wa magonjwa ya watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia upungufu huo, Mkoa uliamua kuajiri Madaktari (MD) na kuwalipa kwa kutumia fedha za uchangiaji wa huduma za afya (cost sharing). Hadi wiki iliyopita, walikuwepo Madaktari (MD) saba ambao wanalipwa kwa fedha za cost sharing. Madaktari hao ni Dkt. Yunus H. Ibrahim; Dkt. Nathaniel Ngeta, ambaye kwa sasa amepelekwa kwa DED Kyrerwa; Dkt. Paschal Peter; Dkt. Goodluck Chenga, kwa sasa amepangiwa Hospitali ya Mkoa Bukoba; Dkt. Bartazar W. Benedicto, amepangiwa Wizara ya Afya; Dkt. Lunyonga R. Shija ambaye kwa sasa amepangiwa Hospitali ya Mkoa Bukoba; na Dkt. Felix T. Otieno ambaye kwa sasa amepangiwa Hospitali ya Mkoa Bukoba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Madaktari hao wawili waliobaki wapewe kipaumbele cha ajira na wapangiwe kufanya kazi kwa RAS Kagera. Pia tunaomba Madaktari Bingwa zaidi ili kupunguza upungufu uliopo katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi ya vifaa vya uchunguzi hasa CT-Scan na MRI pamoja na wataalam wa kuvitumia vifaa hivi vya uchunguzi ni muhimu kwa Hospitali ya Mkoa, kwa sababu huduma hii ya uchunguzi inapatikana Mwanza. Hivyo tunaomba sana muweze kutukumbuka Mkoa wa Kagera. Pamoja na maombi hayo, tunaomba pia Halmashauri zetu zipewe kipaumbele katika mgawo wa Medical Doctors (MD) hasa ikizingatiwa kuwa baadhi ya Halmashauri tayari zimeanza kutoa huduma ya upasuaji CEMONC katika vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vinavyotoa huduma ya upasuaji, licha ya upungufu wa Madaktari ni Nyakachura na Nyakanazi katika Halmashauri ya Wilaya Biharamulo; pia kwenda katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa na Kayanga katika Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe. Vituo vinne vya afya vinavyotarajiwa kuanza kutoa huduma za upasuaji kupitia Mpango wa Strengthening Primary Health Care for Results Programme ni Mabame (Ngara), Kimaya (Muleba), Kishanje (Bukoba) na Morongo (Kyerwa). Vituo vingine vilivyokamilisha ujenzi wa theatre ili kuanza kutoa huduma za CEMONC ni Kaigara (Muleba), Bunazi (Missenyi), pamoja na Kabyaile (Missenyi) kilichojengwa na Kamati ya Maafa kufuatia tetemeko la ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ijikite katika kufanya tafiti mbalimbali kwa kushirikiana na Taasisi za Utafiti za Idara za Vyuo Vikuu na taasisi zingine zinazojihusisha na utafiti wa malikale au maliasili. Mpaka sasa bado Wizara haijajikita kiundani kuweza kuzigundua maliasili zetu nyingi tulizonazo hapa nchini hali inayopelekea Watanzania wengi kutokuwa na uelevu juu ya vivutio vya kale tulivyonavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ihakikishe inayatambua maeneo yote ya urithi wa kihistoria tuliyonayo hapa nchini na maeneo mengine yote yenye maliasili kwa kushirikiana na watendaji wa vijiji na vitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara kwa kushirikiana na Serikali kwa ujumla wahakikishe wanajenga miundombinu ya kufikia kirahisi maeneo yenye malikale na vivutio vingine vya asili ili paweze kufikika kirahisi na kujenga au kuweka karibu nyumba za kulala wageni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ikishirikiana na Serikali katika kuanzisha utaratibu maalum wa kuwa na somo la ziada mashuleni ambalo litawafunza wanafunzi wote wa shule za msingi na sekondari pamoja na vyuo vikuu juu ya umuhimu na faida za malikale zetu na utalii tulionao hapa nchini.

Pia naiomba Wizara kuanzisha utaratibu maalum wa kuwapatia elimu wanavijiji na wananchi kupitia mikutano ya hadhara na mikutano mingine ya maendeleo ya vitongoji, vijiji na mitaa mijini. Ifikie mahali wananchi na wasomi wengi waone umuhimu wa kutembelea mali kale zetu mbalimbali walau kwa mwaka mara mbili, hii itapelekea kuongezeka kwa pato la ndani kupitia utalii wetu wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ihakikishe inayatambua maeneo yote ya urithi wa kihistoria tuliyonayo hapa nchini na maeneo yote yenye maliasili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali/Wizara ihakikishe kila panapofanyika ujenzi wa barabara itakayopita sehemu ndefu kuna mtaalam wa malikale na vivutio vingine vya asili ambavyo atavigundua na kushauri mradi huo usipite maeneo hayo upitie njia nyingine ili kuvilinda vivutio hivyo na kuvifanya kuwa hifadhi kwa manufaa ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwneyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naunga mkono hoja. Changamoto tuliyonayo kubwa inayokabili viwanda nchini ni pamoja na ukosefu wa mitaji na teknolojia ya uzalishaji kupitwa na wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine kubwa ni kutokuwa na uhakika wa umeme na maji ambayo inafanya viwanda vyetu kutoimarika, hivyo nashauri kuwa ili viwanda viimarike nchini, Serikali ihakikishe umeme na maji vimepatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa na mwenendo usioridhisha kutoa fedha za miradi ya maendeleo, hivyo kuchelewesha utekelezaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali iangalie namna bora ya kuiwezesha Benki ya Rasilimali Tanzania (Tanzania Investment Bank) ili ifungue matawi mikoani hasa Mkoa wa Kagera, hatua ambavyo itasaidia mikopo kuwafikia Watanzania walio wengi. Kuna changamoto ya kukosekana kwa soko kwa baadhi ya bidhaa zinazotengenezwa nchini kwa sababu ya kukosa ubora unaotokana na gharama za uzalishaji kuwa juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Ongezeko la Thamani (VAT), hususan kwa wawekezaji wa viwanda vya madawa ya kilimo na mifugo kutozwa kodi ya ongezeko la thamani (VAT), unapunguza ushindani wa bidhaa zinazoingia nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iboreshe Kiwanda cha Kagera Sugar ili kiweze kutoa sukari kwa wingi ili kukidhi mahitaji ya Watanzania hasa waliopo Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Kagera Sugar kipo Mkoani Kagera, lakini wananchi hawanufaiki na kiwanda hicho kwa sababu sukari inakuwa ni ya bei ya juu sana. Hivyo, naiomba Serikali iweze kutusaidia wananchi wa Kagera kupata sukari kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeongeza ugumu katika hatua ya kuanzisha biashara kwa kuongeza tozo za usajili. Jambo hili linaathiri juhudi za kuongeza ajira kwa vijana. Pia inafanya wajasiriamali wasifanye shughuli rasmi za kuingiza mapato ya Serikali na kupunguza ajira zitokanazo na biashara rasmi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kuwapongeza Mawaziri wa Wizara hii, Dkt. Charles Tizeba pamoja na Mheshimiwa William Olenasha pamoja na Makatibu wa Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze moja kwa moja kutoa mchango wangu katika Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambayo ni Wizara nyeti inayotegemewa na Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera tumebarikiwa kwa kuwa na ardhi nzuri yenye rutuba na hali ya hewa nzuri yenye mvua za kutosha. Mkoa wa Kagera kilimo kimekuwa cha kusuasua kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo teknolojia duni pamoja na pembejeo kutokufika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkoani kumekuwa na miundombinu mibovu ya kusafirisha mazao kutoka shambani hadi kwenye masoko. Naomba Wizara husika iweze kuwasiliana na Wizara ya Uchukuzi ili waweze kutuwekea miundombinu mizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, magonjwa ya mimea kwa mazao ya chakula yamekuwa yakiongezeka sana. Katika mkoa wa Kagera zao la mgomba linalolimwa na kutegemewa na wananchi wa Mkoa huo linashambuliwa na ugonjwa wa mnyauko ambao unatutesa sana kwa sababu ndizi ndicho chakula kikuu kwa mkoa wetu. Hivyo naomba Serikali itusaidie kutokomeza ugonjwa huo ili wananchi wa Mkoa wa Kagera waweze kunufaika na zao hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkoa wangu wa Kagera umebarikiwa kwa kuwa na mazao ya biashara kama vile kahawa na miwa. Kwenye zao la kahawa tuna changamoto ya masoko kiasi kwamba inasababisha wananchi kwenda kutafuta soko nchi jirani. Naiomba Serikali iweze kutatua changamoto hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa miwa napenda kuishauri Serikali kuweka mashamba darasa kwa wakulima wadogo wadogo ili waweze kuungana na wakulima wakubwa na hivyo waweze kupata utaalamu wa kulima kisasa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani kama Serikali na Wizara ya Kilimo wakiweza kuutumia Mkoa wa Kagera nina uhakika unaweza kuzalisha sukari ya kutosha nchini kwetu na kuuza nje ya nchi. Mawakala wa pembejeo za kilimo mpaka sasa wameendelea kupigwa dana dana kwa kutolipwa fedha zao. Tukumbuke mawakala wengi walichukua fedha za mikopo kwenye benki na sehemu nyingine kama dhamana hali iliyosababisha wengine kupigiwa minada nyumba zao na hivyo kusababisha wengine kupoteza maisha kwa ajili ya pressure (blood pressure).

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawakala wote nchi nzima wanaidai Wizara ya Kilimo shilingi bilioni 64.4 ambapo Wizara inawapiga dana dana na hawajui hatima ya deni lao, japo Wizara ya Kilimo inasema bado ina hakiki uhalali wa deni hilo. Basi ni vyema Serikali ikaanza kuwalipa wale iliyojiridhisha kuwa wanastahili kulipwa na wale ambao bado hawajajiridhisha Wizara iangalie namna ya kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usalama kwa wavuvi haupo vizuri wakiwa ziwani au baharini, wanatekwa na majambazi, wananyang’anywa samaki na wengine kupoteza maisha. Ninaomba Wizara waweke doria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wasitozwe leseni zaidi ya mara mbili na kwa kweli ninaomba Wizara iwaangalie kwa jicho la huruma hawa wavuvi wanaoingiza nyavu ambazo hazifai. Itawasaidia wavuvi kupata nyavu zinazokubalika, za kiwango kuliko kuchukua mbovu ambazo zinawaletea hasara zikishachomwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona na kunipati nafasi niweze kuchangia katika Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayozidi kufanya katika Taifa letu. Mimi binafsi namuombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kumtia nguvu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri wanazozidi kuzifanya kwa kulitumikia Taifa letu kwa moyo wa dhati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze moja kwa moja kutoa mchango wangu katika Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambayo ni Wizara nyeti inayotegemewa na Taifa letu. Mkoa wa Kagera tumebarikiwa kuwa na ardhi nzuri yenye rutuba na hali ya hewa nzuri yenye mvua nyingi za kutosha. Mkoa wa Kagera kilimo kimekuwa cha kusuasua kutokana na changamoto mbalimbali. Kwanza kabisa kuwa na teknolojia duni na pembejeo kutokufika kwa wakati. Mkoa wa Kagera tuna ardhi nzuri sana na tunapata mazao ya kila aina lakini pembejeo zimekuwa za shida sana kutufikia kwa wakati na pia teknolojia duni, bado hatujapata teknolojia za kisasa kuweza kulima kwa kutumia teknolojia hizo. (Makofi)

Katika Mkoa wa Kagera kuna miundombinu mibovu ya kusafirisha mazao toka shambani hadi kwenye masoko. Wakulima wanapata shida sana kutoka shambani hadi kufikia masoko, miundombinu ni mibovu, barabara ni mbovu. Namwomba Mheshimiwa Waziri aweze kuwasiliana na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili waweze kutengeneza barabara wakulima wetu waweze kufika kwenye masoko bila tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Kagera magonjwa ya mimea na mazao ya chakula kama zao la migomba linalolimwa na kutegemewa na wakazi wa Kagera linashambuliwa na ugonjwa wa mnyauko. Ugonjwa wa mnyauko umetushambulia sana katika Mkoa wetu wa Kagera ambapo migomba ndiyo tunayoitegemea kama chakula chetu kikuu. Naiomba Wizara ya Kilimo pamoja na Waziri waweze kutusaidia ili kuweza kupata tiba ya huu ugonjwa wa mnyauko kwa sababu ndilo zao kuu tunalolitegemea kwa Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wangu wa Kagera umebarikiwa kuwa na mazao ya biashara ya kahawa na miwa lakini kahawa imekuwa haipati soko zuri sana yaani hatupati bei nzuri hadi inapelekea wakulima kwenda nje ya nchi, kwa mfano, wanapeleka Uganda ili waweze kupata bei nzuri. Naomba Serikali na Wizara husika waweze kuangalia zao letu la kahawa (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna zao la miwa, kwa upande wa zao hili napenda kuishauri Serikali kuweka mashamba darasa kwa wakulima wadogo wadogo ili waweze kuungana na wakulima wakubwa waweze kupata utaalamu wa kulima kwa kisasa zaidi. Naishauri Wizara ya Kilimo waweze kutuletea Maafisa Ugani, ikiwezekana kila kijiji, ili wakulima waweze kujifunza zaidi katika zao letu hili la miwa. Miwa ni zao kubwa sana ambalo linatupatia sukari, kwa mfano kwa sasa hivi sukari imekuwa tatizo katika nchi yetu, lakini tungekuwa na wakulima ambao wanaelewa vizuri hili tatizo lisingekuwepo, tungeweza ku-supply katika mikoa yote kutoka Mkoa wa Kagera. Kwa hiyo, naomba sana Wizara ya Kilimo iweze kufikiria kuweka mashamba darasa ili wakulima waweze kupata elimu ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongelea kuhusu mawakala wa pembejeo za kilimo, mpaka sasa wameendelea kupigwa danadana kwa kutokulipwa fedha zao. Tukumbuke mawakala wengi walichukua fedha za mikopo katika benki, wengi wamepoteza hadi maisha yaani mtu akiwaza nyumba yake inapigwa mnada, hakuna mtu ambaye anaweza kumsaidia ili aweze kulipa lile deni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameshasema kwamba wanafanya uhakiki wa mawakala wanaodai Wizara, mawakala wote nchi nzima wanadai Wizara ya Kilimo shilingi bilioni 64.4 ambapo Wizara inawapiga danadana na hawajui hatma ya deni lao, japo Wizara ya Kilimo inasema bado inafanya uhakiki wa deni hilo. Sasa itafanywa uhakiki mpaka lini na watu wanazidi kupoteza maisha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hebu fikiria hivi tunavyokuja Bungeni, mtu usipopata posho yako, tunalalamika kutokupata posho, sasa endapo umechukua mkopo wa benki na ume-supply hizo mbegu sehemu yako na bado hujaweza kulipwa, kweli hii inaumiza sana kwa sababu watu wanapoteza maisha, wanaacha familia zao zikihangaika. Naiomba sana Serikali na Wizara husika iweze kuwafikiria hawa watu ambao wali-supply hizi mbegu kwa wakulima. Basi ni vyema ikaanza kuwalipa wale iliyojiridhisha kuwa wanastahili kulipwa na wale ambao bado hawajiridhisha Wizara iangalie namna ya kuwasaidia watu hawa hata kwa mawazo. Kwa sababu mtu kama ameshatoa hela yake, inatakiwa kwa kweli apate counseling ili vifo visiendelee kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwenye uvuvi. Wavuvi hawako salama, kuna wavuvi wanakwenda kuvua usiku, wanatekwa na majambazi na wananyang’anywa samaki wao. Kwa hiyo, naomba angalau kuwepo na doria mle ziwani au baharini wanapokwenda kuvua samaki. Naomba Serikali waangalie kwa jicho la huruma suala hili. Pia leseni wasitoze zaidi ya mara moja, unaweza ukakuta mvuvi anatozwa leseni zaidi ya mara mbili, tunaomba Serikali iliangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongelea pia nyavu wanazotumia zinazosemekana kwamba ni mbovu. Hivi, hizo nyavu ambazo hazitakiwi mpaka zinaingia nchini Serikali inakuwa inaangalia wapi mpaka waweze kumuonea huyu anayekwenda kuvua samaki au hawa wavuvi wanawachomea nyavu zao. Kabla hawajafika hiyo hatua, naomba Serikali ifanye uchunguzi wa hizo nyavu zisiweze kuuzwa hata madukani kwa sababu wanawapa hasara wananchi wetu. Kwa kweli inatia uchungu sana katika upande wa uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee sekta ya mifugo. Mkoa wa Kagera wafugaji wamenyanyasika sana, wamehamishwa kupelekwa huku na huku na wengine wamepoteza ng’ombe wao wengi. Huku wanasema kwamba hakuna sehemu ya kufugia na wakulima vilevile wanasema hakuna sehemu ya kulima, lakini naomba Serikali iwaangalie kwa jicho la huruma hawa wafugaji na wakulima pia, itenge sehemu ya kwamba hawa wafugaji wanatakiwa wafugie sehemu fulani na hawa wakulima wapate sehemu ya kulima lakini imekuwa ni tatizo kubwa. Wafugaji wa Mkoa wa Kagera wanalia, wamenyang’anywa ng’ombe wao, wamepotea na kwa upande wa wakulima ng’ombe wanaenda kula mazao ya wakulima vilevile, yaani kote kote ni shida. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Dkt. Tizeba uliangalie hili kwa uso wa huruma. Mimi mwenyewe ni mfugaji, hata wewe najua ni mfugaji, kwa hiyo, naomba uangalie jinsi ya kusaidia hawa wafugaji waweze kupata sehemu ya kufugia ng’ombe wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishie hapa, naunga mkono hoja ya Wizara yetu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia katika Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniweza kusimama katika Bunge lako Tukufu, siyo kwa uwezo wangu bali ni kwa uwezo wake. Nampongeza Rais wetu mpendwa wa Jamhuri ya Muungano Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anazofanya za kujenga Taifa letu, binafsi namuombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kumtia nguvu ili aendelee kulijenga Taifa letu na sisi tuko nyuma yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Makamu wa Rais Mama Samia Hassan Suluhu na Waziri Mkuu Kasim Majaliwa na Mawaziri wote, Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri wanazozifanya kwa moyo wa dhati wa kujenga Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze dada yangu mpenzi Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Mheshimiwa Dkt. Ndungulile kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kitengo cha afya. Sasa naomba nijielekeze moja kwa moja katika mchango wangu katika Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naishukuru Serikali kwa mwaka wa fedha 2017/2018 kwa kutenga bilioni 3.5 kwa ajili ya ukarabati wa vituo vya afya vya Mkoa wa

Kagera. Pamoja na kazi nzuri zinazofanywa kwa upande wa afya, napenda kusemea wafanyakazi wa Murugwanza Wilaya ya Ngara, wafanyakazi 17 ambao hawajaingizwa kwenye payroll licha ya kuombewa kibali Wizarani na hupelekea kupata mishahara yao kwa shida. Naomba sana Wizara ya Afya pamoja na Serikali iweze kuwaona hawa watu ambao wanafanya kazi kwa moyo wao wote lakini hawajaingiziwa majina yao kwenye payroll mpaka muda huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanapata shida sana na ikumbuke kwamba wanazo familia, wana watoto wanaowasomesha na mambo yao binafsi kwa ajili ya kupata fedha ili waweze kujikimu, lakini mpaka muda huu hawajaweza kupata mishahara wanadai zaidi ya muda mrefu sana hata wakipata mshahara wanaweza kupata mshahara wa mwezi mmoja miezi miwili, ambayo haikidhi mahitaji yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna wafanyakazi 49 walitolewa kwenye payroll na baadaye wakarudishwa wako chini ya Dayosisi ambao wanalipwa na Wizara, walivyorudishwa kwenye payroll hadi leo kuna arrears zao wanadai, ambapo kuna mtumishi anadai miezi kumi miezi sita, miezi mitano, hiyo pia inaleta shida sana katika kufanya kazi. Watu hawa wako kwenye kitengo ambacho ni mahsusi lakini mtu unakuta ameshindwa hajapata mshahara zaidi ya miezi kumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli naomba Wizara iweze kuwaangalia hasa dada yangu mpenzi Mheshimiwa Ummy Mwalimu, najua ana moyo sana wa upendo hebu naomba aangalie Wilaya yangu ya Ngara jamani, hawa watu waweze kusaidiwa. Mheshimiwa Dkt. Ndungulile nilishamlilia sana nilishamwona uso kwa uso nikamwelezea kuhusu hawa watu lakini bado hawajapata mishahara yao, naomba sana waangalie kwa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vya afya katika Wilaya ya Ngara tuna upungufu wa watumishi kwa asilimia 67, jambo linalotatiza huduma za afya. Hebu imagine asilimia 67 vituo vya afya hamna watumishi. Unaweza ukaenda kituoni ukakuta kuna Mganga mmoja huyu ndiyo receptionist, huyo ndiyo aangalie wazazi, huyo ndiyo angalie watoto na kila kitu. Jamani Wizara ya afya naomba watuangalie sana Wilaya ya Ngara, tuko mpakani mwa Rwanda na Burundi lakini tuko Tanzania, tunaomba watuangalie inawezekana wameshatusahau lakini tunaomba watuangalie kwa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuongelea Watumishi wa Afya kutolipwa stahiki zao kwa muda mrefu kama vile on call allowance na malimbikizo ya mishahara, likizo na matibabu. Unakuta wafanyakazi wanafanya kazi kwa muda mrefu bado hawajapata stahiki zao, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee na Watoto yaani mimi nakufa na yeye kwa sababu najua ni dada wa upendo nina imani ataweza kunisaidia huko ili tuweze kuwasaidia hawa ndugu zetu waweze kupata mishahara yao kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Nyamiaga inayomilikiwa na Serikali kwa asilimia 100, hiyo hospitali wodi ya wajawazito kuna vitanda vichache, unakuta wajawazito wanalala watatu hadi watano katika kitanda kimoja. Imagine, dada yangu Ummy ni mzazi kama mimi, wakati mwingine uchungu unakushika, unaenda kushika tumbo kumbe unashika la mwenzako, unaenda kushika mgongo unashika wa mwenzako, mmelala kitanda watu mko watatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri aangalie hili, tupate angalau vitanda vya kutosheleza katika hospitali yetu ya Nyamiaga ambayo iko chini ya Serikali asilimia 100. Tunaweza tukasemea Murugwanza lakini Murugwanza iko chini ya Dayosisi na tuna watumishi wetu wa Serikali lakini Nyamiaga ni ya Serikali asilimia 100, lakini wagonjwa wanapata shida sana hasa akinamama wajawazito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mama nawawakilisha akinamama inaniuma sana, ninapokwenda nakuta akinamama wamelala watatu, watano kitanda kimoja na ile habari dada Ummy unaifahamu jinsi inavyouma, yaani sijui nisemeje, Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndungulile naweza nikamwacha pembeni kwa sababu hajui uchungu wa akinamama tunaoupata wakati wa kujifungua. Kwa hiyo, naomba kwa kweli watuangalie kwa jicho la huruma sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo zahanati ya Kijiji cha Ishozi, Wilaya ya Misenyi iliangushwa wakati wa tetemeko la ardhi mpaka leo ukarabati wa zahanati hiyo haujaweza kufanyika ipasavyo. Naomba Serikali iweze kufanya ukarabati wa kutosha ili wale wananchi wa Ishozi kule Misenyi waweze kupata matibabu ya kutosha especially wazee, kuna watoto kuna akinamama, lakini hawapati huduma ile kutokana na kutokukarabatiwa kwa yale majengo yaliyoanguka kwa tetemeko. Sisi wa Mkoa wa Kagera hatukuliita tetemeko, lilikuja tu kwa bahati mbaya. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri na Wizara husika iweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa haina hospitali ya Wilaya. Ile hospitali ina watu wengi sana pale Kyerwa kuna zaidi ya wananchi laki tatu, wote tunatuma kituo cha Kyerwa, naomba Serikali ituangalie kwa jicho la huruma tuweze kupata hospitali ya Wilaya katika Wilaya ya Kyerwa ili wananchi waweze kupata matibabu pasipo shida. Mheshimiwa dada yangu Ummy Mwalimu naomba anisikilize kwa makini sana na Mheshimiwa Dkt. Ndungulile nisije nikashika shilingi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali zote za Wilaya za Mkoa wa Kagera zina upungufu wa watumishi, kwa kweli tuna shida sana, kila Wilaya, kila zahanati kuna shida ya upungufu wa watumishi. Kipindi wanafanya uhakiki wa vyeti watu waliondoka wengi. Mheshimiwa baba yangu Mzee Mkuchika alishasema uhakiki ulishapita, sasa kwa nini wasiajiri watu wa kutosha katika hospitali zetu ili wazee, mama zangu, watoto, baba zangu waweze kupata huduma. Naomba sana watuangalie sana kwa jicho la huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri za Manispaa za ya Bukoba na Muleba tayari zimeanza kujenga vituo vya afya. Je, ni lini Serikali au ina mpango gani wa kutenga pesa ili kuweza kusaidia hizi Halmashauri zikamilishe ujenzi wa vituo vile vya afya? Kwa sababu wananchi walishajitolea kwa moyo wao, tumejitolea kama wananchi kujenga vituo vya afya lakini havijakamilika, wanatusaidiaje ili tuweze kukamilisha vituo vile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Kagera tuna visiwa 25 ambavyo vinakaliwa na wananchi, lakini visiwa vyote hivyo vina zahanati tano tu, katika zile zahanati...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE.OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii niweze kuchangia katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama katika Bunge lako Tukufu. Pia nampongeza Rais wangu, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anazozifanya za kujenga Taifa. Nawapongeza pia Mawaziri, Mheshimiwa Profesa Mbarawa na Manaibu wake kwa kazi nzuri wanazozifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nielekee moja kwa moja katika mchango wangu. Kwa kuwa ukarabati unaoendelea wa Barabara ya Nyakanazi – Rusahunga - Rusumo haukidhi viwango kutokana na magari mazito yanayopita pale ya mizigo yanayoelekea nchi jirani za Rwanda, Burundi, Kongo na Uganda. Naomba sana Mheshimiwa Waziri husika na Wizara waweze kuangalia hii barabara itengenezwe kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba waikarabati kwa kiwango kinachokidhi, kwa sababu kila siku kuna viraka vinavyowekwa pale. Mara leo kuna kiraka, mara kesho kuna kiraka, barabara inaendelea kuwa vilevile, bado kuna magari mazito yanayopita pale. Hii ni barabara ambayo ni muhimu sana katika uchumi wa Taifa. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri naomba waliangalie hili kwa jicho la huruma na kwa kusaidia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano kuna watu wana madaladala, wana teksi zinazotoka Ngara mpaka Kahama, kila baada ya mwezi wanabadilisha shock up na hali ilivyokuwa ngumu, kwa kweli inasikitisha sana. Naomba sana Serikali iweze kutuangalia kwa jicho la huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuongelea huduma za ndege za Dar es Salaam to Bukoba, huduma za Dar es Salaam ni nzuri, abiria wameongezeka sana kutoka Dar es Salaam mpaka Bukoba, lakini trip ya Dar es Salaam to Bukoba ni moja tu. Naomba trips ziongezeke, sisi watu wa Kagera tumezoea sana kutumia ndege kuliko magari, kwa hiyo naomba mtuongezee trips angalau ziwe mbili au tatu, kwa kweli naomba watuangalie sana. Naomba sana sana iwepo trip ya mchana, tuna trip ya alfajiri tu, mtu unaamka saa kumi, saa tisa kuelekea airport, kwa kweli naomba Mheshimiwa Waziri hili waliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili naomba kama inawezekana kuwepo na trip ya Dar es Salaam – Dodoma - Mwanza kwa sababu Kanda ya Ziwa kuna abiria wengi sana na Dodoma ndiyo Makao Makuu ya Nchi, kwa nini wasituwekee ndege ya kutoka Dar es Salaam – Dodoma - Mwanza? Kama tuko hapa tunahitaji kwenda Mwanza na moja kwa moja inaenda Kagera bila shida, kwa kweli namwomba Mheshimiwa Waziri waweze kutuangalia sana watu wa Kanda ya Ziwa kwa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakandarasi walio-supply vifaa vya kujenga miundombinu katika Shule za Sekondari Ihungo na Nyakato wakati wa kipindi cha tetemeko bado wanadai pesa zao nyingi. Je, ni lini watalipwa pesa zao? Kwa sababu wame-supply majengo yamekuwa mazuri lakini hawajalipwa pesa zao. Kwa kweli naomba Wizara husika, Mheshimiwa kaka yangu Profesa Mbarawa, naamini ni mtu mzuri sana, hebu atuangalie kwa jicho la huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo ya usikivu wa simu yaliyopo Wilaya ya Ngara, Kata za Nyakisasa, Keza, Kabanga na Rusumo yanaingiliana na Nchi za jirani za Rwanda na Burundi. Nimeshaongelea hili suala zaidi ya mara tatu ndani ya hili Bunge lako Tukufu, lakini sioni kinachoendelea. Wananchi wa Ngara tunapata shida, mtu unapiga simu uko Ngara inaingiliana na mtambo wa Rwanda, inaingiliana na mtambo wa Burundi. Kwa nini wasituangalie waongeze minara, waongeze mitambo ili tuweze kupata communication ambayo ni within Tanzania, kwa nini wasituangalie sana? Nimeshamwomba sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuongelea kuna uwanja ambao uko Ngara unaitwa Ruganza Airstrip, ule uwanja umesahaulika kabisa. Tumeutumia sana kipindi cha wakimbizi wakati nafanya kazi UNHCR ndiyo ulikuwa uwanja mkubwa sana na bado kuna madini ya Kabanga nickel, kule Kabanga nickel ndege zinatoka kule zinatumia ule uwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, juzi kuna wakimbizi wamepata ajali wakati wanatoka Kigoma wanaelekea Burundi, wanapitia Kigoma – Kasulu – Kibondo – Ngara. Wamefika Ngara wakapata ajali, ule uwanja ndiyo ulitumika na watu wa UN, UN ni shirika kubwa la kimataifa lakini wametua…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kuwapongeza Mawaziri husika. Mheshimiwa Luhaga Mpina na Mheshimiwa Ulega, pamoja na Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa Hotuba yao nzuri ya bajeti iliyowasilishwa hapa Bungeni. Sasa naomba kutoa maoni yangu katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya malisho kutokana na kutokuwa na Mpango wa Matumizi bora ya Ardhi, hivyo kusababisha migogoro kati ya Wakulima na Wafugaji.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya Wilaya katika Mkoa wetu wa Kagera wana maeneo maalum ya malisho hasa yale yaliyokuwa Ranch za Taifa lakini kwa Jimbo la Ngara hakuna maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine tuliyonayo ni ya masoko ya mazao ya mifugo, mfano ngozi, maziwa, nyama pamoja na mayai ya kuku.

Mheshimiwa Spika, sababu zinazofanya ngozi nyingi kuwa na ubora wa chini ni pamoja na upigaji wa chapa ovyo hususan katika maeneo muhimu ya ngozi, hali mbaya ya miundombinu ya machinjio, makaro, mabanda ya kukaushia na kuhifadhia ngozi.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina utajiri mkubwa wa mifugo ambayo ingezalisha ngozi kama malighafi za viwandani na kuongeza pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, shughuli za ufugaji wa samaki nchini unafanywa na wafugaji wadogo wadogo kwa asilimia kubwa. Ufugaji wa samaki hukabiliwa na matatizo na changamoto nyingi, kama ukosefu wa teknolojia bora, upungufu wa vifaranga bora na miundombinu ya usafiri kuwa duni.

Mheshimiwa Spika, changamoto katika sekta ya uvuvi inakabiliwa na upungufu katika sera na sheria, elimu duni juu ya shughuli za uvuvi katika jamii, uvuvi uliopitiliza na hivyo kuathiri rasilimali za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mwendelezo wa wavuvi kuchomewa nyavu zao za kuvulia kila mara na kumekuwa na matamko kutoka Wizara husika juu ya matumizi ya nyavu sahihi za kuvulia.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama tena katika Bunge lako Tukufu. Pili, niwashukuru wa kina mama wa Mkoa wa Kagera kwa kunipigia kura nyingi za kishindo. Tatu, nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa kunipitisha tena kuingia tena Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Rais wetu wa Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri anazozidi kuzifanya katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Pia nampongeza Waziri wa Fedha na Mpango kwa kutuwasilishia Mpango ili tuweze kuujadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze moja kwa moja katika mchango wangu. Nitachangia kuhusu vituo vya afya na elimu kidogo. Vituo vyetu vya afya vilivyojengwa sasa hivi ni vya kisasa kabisa, vina maternity ward, theatre, maabara, mortuary na nyumba ya daktarin. Hata hivyo, changamoto iliyopo hakuna wodi ya wanaume wala wanawake. Kwa hiyo, naiomba Serikali Tukufu waweze kujenga wodi za kina baba na kina mama kwa ajili ya kusaidia wale wananchi wa hali ya chini ili wakifika pale waweze kupata first aid, labda wanaweza kupata drip wakapumzishwa pale kabla hawajaenda kwenye vituo vikubwa vya afya. Kwa hiyo, naomba Serikali yangu Tukufu iweke mpango mzuri wa kujenga hizo wodi za kina baba na kina mama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja nijielekeze katika suala zima la elimu. Nashukuru Serikali yangu Tukufu imetelekeza vizuri Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa suala la elimu, kuanzia darasa la kwanza hadi form four elimu ni bure. Hata hivyo, mwanafunzi wa hali ya chini akimaliza form four, form five na six kama amefaulu vizuri hawezi kwenda shule. Kwa hiyo, naomba Serikali yetu Tukufu kwa sababu imeshajitoa yaani hapo imekula ng’ombe mzima bado mkia, iweze kuangalia watoto wetu waweze kufika mpaka form six kwa elimu bure kwa sababu akishaingia chuo kikuu anapata mkopo. Kwa hiyo, naomba Serikali yangu Tukufu iliangalie hilo kwa kwa ajili ya kuokoa kizazi chetu na watoto maskini kama Rais wetu wa wanyonge anavyosaidia. Kwa hiyo, naomba aendelee kusaidia hawa watoto waweze kusoma vizuri mpaka form six ili waweze kuingia chuo kikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze pia kwenye miundombinu ya barabara. Kule kijijini kwetu miundombinu siyo mizuri, unakuta hakuna barabara, mkulima ameshalima mazao yake ili aweze kuyafikisha kwenye soko barabara ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo, naomba Serikali yangu Tukufu isiangalie barabara kuu tu iangalie na Kisingimbi kwetu kule vijijini waweze kuweka barabara Rafiki, mkulima akimaliza mazao yake mazuri aweze kufika katika masoko kuuza mazao yake ili kujikwamua kiuchumi aweze kusaidia na familia yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu yalikuwa ni hayo, nashukuru san ana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. OLIVER D. SUMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuanza kwa kukushukuru kwa namna ambavyo umekuwa kiungo muhimu katika kuhakikisha Bunge letu tukufu linatimiza wajibu wake wa kuisimamia Serikali ili iweze kutimiza wajibu wake kwa manufaa ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kupoteza muda ninaomba nianze moja kwa moja kutoa mchango wangu kwa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na mchango wangu unaanza kwa kuishauri Serikali kuwekeza nguvu kubwa katika kuboresha mazingira ya utendaji kazi wa Maafisa Ardhi katika Wilaya zote na mikoa yote nchini ili waweze kupata ari na ubunifu wa kuweza kutimiza majukumu yao kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipindi kirefu tumekuwa tukishuhudia migogoro mingi ya ardhi ambayo mara nyingi imetokana na Idara ya Ardhi na Mipango Miji katika maeneo mengi ya nchi hii kushindwa kutimiza majukumu yao kwa ufanisi kutokana na ufinyu wa bajeti na vitendea kazi katika Idara ya Ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mengi ningependa kuiomba Wizara ya Ardhi kuweka mpango wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yote yanayozunguka Hifadhi za Taifa nchini pamoja na maeneo yenye miradi ya kimkakati. Kwa kufanya hivyo itapunguza kwa kiasi kikubwa migogoro ya ardhi ambayo tumekuwa tukiishuhudia mara kwa mara pale wananchi wanapoamua kuvamia maeneo ya mapori ama Hifadhi za Taifa kwa ajili ya kuendesha shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Wilaya ya Ngara ambayo imepakana na Mapori ya Akiba ya Kimisi na Burigi kunahitajika kuwekwa mpango wa matumizi bora ya ardhi ili kuweza kuwanufaisha moja kwa moja wananchi wa Wilaya ya Ngara hususani wakazi wa vijiji vya Rusumo, Mshikamano, Kasulo, Rwakalebela, Keza na Kazingati.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo naiomba Wizara ya Ardhi kukaa pamoja na Tume ya Taifa ya Matumizi ya Ardhi kuandaa mpango huo wa matumizi bora ya ardhi ambao utahusisha kutenga baadhi ya maeneo kwa matumizi ya kilimo, ufugaji, uwekezaji viwanda pamoja na utunzaji wa mazingira kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ningependa kuishauri Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo na Makazi kuandaa mpango bora wa matumizi ya ardhi hususani kwa Wilaya ya Ngara eneo la Mgodi wa Tembo Nickel. Kutenga maeneo matatu maalum kwa ajili ya shughuli za kiuchumi kama kilimo, ufagaji pamoja kuanzisha mpango wa kuinua hadhi ya Kijiji cha Bugarama kilicho eneo jirani ya mgodi huu ili kiweze kuwa na hadhi ya kibiashara.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi kwa jioni ya leo na kuwa mchangiaji wa kwanza. Nampongeza Waziri wa Ardhi na Naibu wake dada yangu Mheshimiwa Angelina kwa kazi nzuri wanazozidi kuzifanya pamoja na watendaji wote wa Wizara na Katibu Mkuu dada yangu Mary Makondo. Nawapongeza sana kwa ajili ya kazi zote wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze moja kwa moja katika changamoto zilizopo katika ardhi. Migogoro ya ardhi imekuwepo mingi na haiishi. Sababu mojawapo ni hawa wazee wa Mabaraza ya Ardhi. Wananchi wanyonge wamekuwa ndiyo victim wakubwa. Hawa wazee wa Baraza la Ardhi hawapati posho yao kwa wakati. Unaweza ukakuta wamepata posho baada ya miezi mitatu, minne au mitano. Sasa hapo tunawawekea wananchi ambao ni wa hali ya chini kupata shida. Kwa sababu, ambao wanapata haki katika haya Mabaraza ya Ardhi ni wale ambao wana kitu ambao ni matajiri lakini wanyonge wanapata shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, mtu anaenda pale ana kesi yake, lakini yule Mzee wa Baraza la Ardhi atazungusha nenda rudi, atakayepata haki ni huyu ambaye amempa kitu kidogo na hiyo inatokana na wale wazee kutokupata posho yao kwa wakati. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali yangu, kaka yangu Lukuvi naomba awaangalie kwa umakini hawa wazee wa Baraza la Ardhi, awalipe posho yao kwa wakati, ili hii migogoro ya kupata rushwa iweze kutoka. Rushwa haiwezi kukoma kwa style hiyo. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Ardhi aweze kuliangalia hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee pia vijana. Vijana wengi hawana ajira. Wanazunguka na karatasi na vyeti vyao kila kukicha. Ningeshauri ardhi ya akiba inayotengwa na vijiji wangepewa hawa vijana wakalima, wangepewa hawa vijana wakapata hati, hatimiliki itakayowawezesha kupata mkopo wa pembejeo. Wakishapata ile mikopo watalima, watapata mazao. Mfano mzuri ni mimi mwenyewe nalima mpunga, nina heka na heka, naweza kupata tofauti na hii hapa ambayo ajira yangu niliyonayo ya wananchi, naweza nikapata hela kutoka huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tukiwaangalia hawa vijana au nikimtolea pia mfano Mariam Ditopile. Naye ni mkulima na anapata hela kutokana na huo ukulima. Kwa hiyo wakiwapa vijana hatimiliki wakamiliki kutoka katika hizi ardhi za vijiji vya akiba, wakafanya hata biashara ya kilimo. Wanaweza wakapata hela wakaondokana na hali duni ya maisha. Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri aangalie hali za vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ardhi ya akiba inayotengwa mara nyingi hupewa wawekezaji wenye hela zao na matajiri. Hawa watu ambao hawana uwezo wanakosa. Naomba Serikali iangalie kama kuna mwekezaji ambaye sio tajiri sana, wasiangalie wawekezaji wanaotoka nje, waweze kuwasaidia hawa wawekezaji wa ndani ya nchi ambao wanaweza wakalima vitu na wakasaidia ndugu zetu wakatoka katika hali duni ya Maisha na kuwaondolea umaskini. Kwa hiyo, naomba huu upande wa wawekezaji wasiangaliwe sana matajiri, waangaliwe pia wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Ardhi naomba ijikite sana kusafisha Maafisa Ardhi na Wapima ambao wamekuwa ni chanzo cha migogoro. Unaweza ukaenda ukakuta mpima anakuja mpima sijui binafsi, anakuja mpima wa Serikali, anakuja sijui mpima gani. Sasa inakuja kutokea unakuta kila mtu ana hati, shida inayokuja kutokea huyu ana hati na huyu ana hati. Mwingine anasema Serikali ilikuja ikapima, huyu mwingine anasema nilileta mtu binafsi alikuja kupima, huyu ana Sekta Binafsi ya kupima. Kwa hiyo, naomba Serikali ijikite kuangalia mpima ambaye anatambulika na Serikali kuliko kuzidi kuchanganya wananchi katika ule upimaji wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, licha ya uwepo wa Mabaraza ya Ardhi ya Kijiji, Kata na Wilaya bado lipo ongezeko la migogoro ya ardhi. Migogoro ya mipaka kati ya kijiji na kijiji kingine, migogoro kati ya wakulima na wafugaji, hapa ndiyo balaa kabisa. Mkulima analima mazao yake, mfugaji anaenda anapeleka ng’ombe au mbuzi au whatever, wale wanyama anaowafuga wanaenda wanaharibu mazao ya yule mkulima. Ukiangalia, mfugaji ndiyo ana hela kuliko mkulima. Kwa hiyo anaweza kufanya chochote kile. Kwa hiyo naomba Serikali yangu iangalie haki ya hawa watu. Huu mgogoro wa mkulima na mfugaji wauangalie kwa undani sana. Waache kunyanyasa, hakuna mtu anayependa kutokuwa na kitu. Kila mtu anapenda awe na kitu lakini ukimnyanyasa yule ambaye hana kwa kweli inatia huzuni na simanzi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna migogoro kati ya vijiji na taasisi za Serikali, wenzangu wameshaongea. Unakuta kuna beacon, huyu anakuja anasema beacon yangu iko hapa, beacon yangu iko pale, lakini hiyo yote inatokana na wale Wapima. Ndiyo maana nilianza kumwambia Waziri wangu wa Ardhi angalia hawa Wapima kwa umakini. Sio kuangalia tu mtu huyu anapewa, wewe nenda ukapime, mara sijui nina taasisi fulani napima, wawe ni watu wanaoeleweka ili kuondoa hiyo migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee pia migogoro hii msingi wake inasababishwa na tamaa. Rushwa kwa baadhi ya watendaji katika Mabaraza, waliopewa kusimamia migogoro ya ardhi kwa njia ya usuluhishi. Narudi kule kule kwa wale wazee wa Mabaraza. Hawa hawa ndiyo wanakuwa chanzo cha migogoro lakini migogoro yao ni kutokulipwa posho. Unakuta huyu mzee wa Baraza anadai posho yake miezi mitano, miezi minne na kuendelea. Sasa kweli, akutane na pedeshee amwambie sasa huyu hapa, lazima ummalize mimi nakupa hela. Atashindwa kweli kama mwanadamu? Ili kumaliza rushwa, naomba tuwalipe hawa wazee kila anapodai posho yake mwezi au siku ikiisha, nafikiri wanalipwa kwa siku, wawalipe posho yao kuondoa huo mkanganyiko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua Wizara ina mpango gani mahsusi wa kuhakikisha inasimamia na kuwajibisha watendaji hawa. Endapo mtu amejulikana kabisa huyu mtu ametoa rushwa, je, Serikali inamchukulia hatua gani. Naomba Mheshimiwa Waziri na Naibu Wake waangalie kuanzia kwenye Kata, wasiangalie wilayani wala mkoani. Huku chini ndiyo chanzo cha yote, huku vijijini. Kwa hiyo, wakitaka kupata information iliyo sahihi, waanziae huku chini ndiyo kuna shida. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Ardhi afuatilie kwa undani sana. Tusipofuatilia, hii rushwa haitakaa iishe katika mambo ya ardhi kutokana na huo mpango unaoendelea kuwepo, ambapo hatuwasaidii hawa ambao wanatakiwa kusuluhisha ili kila mtu apate haki yake, zaidi tunazidi kuwaumiza hawa wanyonge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kuna hawa ma-secretary ambao wanawasaidia hawa Wazee wa Mabaraza, unaweza kukuta wamelipwa miezi mitatu na miezi mingine hawalipi. Au wanalipwa kwa miezi mitatu mitatu. Hawana ajira, namwomba Mheshimiwa Waziri Lukuvi awasiliane na Waziri wa Utumishi ili tuweze kujua hawa watu watalipwa kwa wakati au…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii ya TAMISEMI. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazozifanya katika Taifa letu. Pia nampongeza sana Waziri wa TAMISEMI, wifi yangu Kairuki na Manaibu wake pamoja na watendaji wote wakiongozwa na Katibu Mkuu. Nawapongeza sana. Pia nampongeza Mkuu wangu wa Mkoa, Albert Chalamila, anatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika Mkoa wetu wa Kagera, anafanya kazi asubuhi, mchana na jioni. Nampongeza sana Mkuu wangu wa Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwenye mchango wangu. Ujenzi wa madarasa ya msingi na sekondari, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa ujenzi huo. Hata hivyo, kuna changamoto ambayo ipo kwenye shule hizo ambayo ni matundu ya vyoo. Kwa kweli shule nyingi zimejengwa lakini matundu ya vyoo ni machache sana, nilikuwa naomba sana Serikali iweze…

MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Oliver, kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mchangiaji anayechangia kuwa, kazi kubwa sana imefanywa kujenga madarasa na miradi mingi, na Mkoa wetu wa Arusha ni mfano wa Mkoa mmoja, na yote hayo yamefanywa chini ya Mkuu wa Mkoa John Mongella. Tunampongeza sana na tunakushukuru Mheshimiwa Rais kwa kutuletea John Mongella. (Makofi)

MWNEYEKITI: Mheshimiwa Oliver, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili na John Mongella alikuwa ni Mkuu wetu wa Mkoa wa Kagera kabla hajaenda huko. Namjua ni jembe sana, kwa hiyo, naipokea sana taarifa yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoka kwenye matundu ya vyoo, naomba nijielekeze kwenye nyumba za watumishi. Kwa kweli waalimu wanapata shida sana. Tumejenga madarasa ya kutosha katika shule za sekondari na shule za msingi, lakini waalimu hawana nyumba za kuishi. Unakuta mwalimu anatoka kilomita kama 10 au 20 kutoka sehemu A Kwenda B, anafika shuleni ameshachoka, atafundishaje wadogo zetu na watoto wetu kwa weledi sana? Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali ijielekeze kwa nguvu zote kwenye ujenzi wa nyumba za watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile walimu wanatakiwa wawe na mazingira mazuri, wakitoka shuleni kuna jinsi ya kuandaa andalio la kesho yake, na kuandaa notes. Anatoka shuleni ametembea kilomita saba au kilomita 10, anakuwa ameshachoka chakari. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali yangu sikivu iweze kujenga hata nyumba za watumishi hasa za walimu wa shule za msingi, kwa kweli wanapata shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa watumishi. Mheshimiwa Waziri naomba kipaumbele kwenye ajira hizi wanazoajiri wapewe wale ambao wanajitolea. Unakuta mtu amejitolea zaidi ya miaka mitatu, lakini ajira zikitokea hayupo.

MBUNGE FULANI: Kweli!

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mmoja, kuna shule moja ya Ngara; Shule ya Msingi Nyamiaga, kuna mwalimu ameshajitolea zaidi ya miaka mitatu, lakini huyo mwalimu kila akiomba nafasi zikija jina lake halipo. Kwa bahati nzuri, hakati tamaa. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Serikali yetu sikivu iwaone kwa jicho la pekee, hawa walimu wanaojitolea, kwa upande wa afya pia, waweze kuwapa kipaumbele kwa ajira hizi ambazo zimetokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu pia nilikuwa naomba katika hizi ajira, nilikuwa namsikiliza Mheshimiwa Kairuki wakati anasoma hotuba, kwamba wakishaajiri hawawezi kukuhamisha kabla ya miaka mitano. Nilikuwa naomba iwe hivi, kwa mfano kama Kagera waajiri kikanda. Wakiajiri kama ni mwalimu, wameshaona kwenye database ni wa Kagera, basi wamwajiri Mwanza au Geita au Kahama ili iwe rahisi hata kwenda kuona familia yake, wasianze kusumbua kwamba naomba uhamisho. Kwa mfano, umemtoa Kagera, umemepeleka Mtwara. Umemtoa Kagera, umempeleka Songwe, kwa kweli inakuwa ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo, naomba katika hizo ajira wazingatie sana Kanda ili kupunguza kusumbuliwa katika mambo ya uhamisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri waangalie katika ajira hizi, pembezoni huku, kwenye Halmashauri za vijijini unakuta hakuna waalimu, hakuna watu wanaoenda huko; kila mmoja anakataa. Kwa mfano, ukimwajiri mtu ambaye yuko Kagera ukampeleka Wilayani kule pembezoni, ataenda tu, lakini umtoe Kagera, umpeleke Songwe huko karibu na Zambia, kwa kweli inakuwa ni changamoto. Ndiyo hii inaanza kuleta usumbufu kwa ajili ya kuomba uhamisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najielekeza TARURA. Kwa kweli TARURA wanafanya kazi nzuri sana. Wana muda mfupi lakini kazi zinaonekana. Changamoto kwa TARURA ni bajeti. Mfano kwa Mkoa wangu wa Kagera, nilikuwa naomba, kuna Kivuko cha Nyabasa kiko Wilaya ya Bukoba Vijijini. Hicho ni kivuko ambacho tunategemea tujenge daraja. Nilikuwa naiomba Serikali yangu Sikivu, na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, huko ndio nyumbani kwenu pia. Naomba sana kuharakisha usanifu na ujenzi wa Daraja la Chanyabisa la Halmashauri ya Bukoba. Mwaka jana 2022 kuna gari ilitumbukia kwenye hicho kivuko, likakaa almost one-week mle, bila kutolewa.

MBUNGE FULANI: Uuh!

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Kwa kweli ni shida. Ukitupatia bajeti ya kutosha, daraja likajengwa, italeta tija pia kwa wananchi na maendeleo kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuongeza bajeti kwa ajili ya ujenzi pia wa barabara za ulinzi na usalama katika Wilaya za mipakani hasa kule kwetu Ngara, Kyerwa na Missenyi, tujenge barabara ambazo zitakuwa ni za usalama zaidi. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iweze kutupatia bajeti ya kutosha katika hii TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Missenyi na Bukoba vijijini naomba zipatiwe fedha maalum (special fund) kwa sababu kule barabara zake hutengenezwa kwa bajeti ambayo ndiyo hiyo ya special fund. Barabara ni tambarare, mvua zikinyesha maji yanajaa, wananchi hawawezi kwenda upande A na upande B, yaani inakuwa ni changamoto kubwa sana. Tukipata bajeti ya kutosha, watatengeneza barabara ziinuke ili mvua zikinyesha sana maji yasituame na kusababisha wananchi kushindwa kwenda kwenye shughuli zao katika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda umeisha! Eh, mh!

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili hiyo.

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani! Naunga mkono hoja. Mengine nitaandika kwa maandishi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama katika Bunge lako tukufu na pia nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuichangia katika Wizara hii ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na kumpongeza Rais wetu kipenzi, Daktari Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea pesa nyingi katika Mkoa wetu wa Kagera na ndoto yake ya kupunguza vifo vya akinamama na watoto Tanzania inawezekana, hongera sana Mama yetu, tunazidi kukuombea afya kila iitwapo leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze Waziri wa Afya, dada yangu Ummy pamoja na Naibu wake Dkt. Mollel na Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Afya kwa kazi nzuri wanazozifanya, hakika wanatutendea haki. Sasa naomba nijielekeze kwenye mchango wangu, Mkoa wetu wa Kagera halmashauri sita, zimekamilisha ujenzi wa hospitali, Katoke Biharamulo, Bujinangoma Bukoba DC, Bulembo Misenyi, Karagwe, Kyerwa, Ngara Rusumo. Pia kuna vituo vya afya na zahanati zilizokamilika zinahitaji vifaa tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizi hospitali zimekamilika, lakini vifaa tiba imekuwa ni changamoto kubwa sana, pamoja na wataalam wa afya ili ziweze kuanza kutoa huduma. Kwa hiyo, naomba Serikali yangu Tukufu iweze kuleta vifaa tiba vya kutosha katika hospitali hizi pamoja na wataalam ili kuweza kuwasaidia wananchi.

Mheshimiwa Spika, katika hospitali na vituo vilivyokamilika, tunahitaji ujenzi wa nyumba za watumishi wa afya ili kuwezesha kutoa huduma Madaktari Bingwa kwa muda wa saa 24. Kwa mfano, mgonjwa pale anaweza akaja mama mjamzito anakuja kujifungua anafika pale kituoni daktari yuko mbali, lakini tukiwa tumejenga pale nyumba ina maana Daktari atakuwa pale masaa 24. Kwa hiyo vifo vitapungua havitakuwepo kabisa kwa mama wajawazito pia na watoto na wazee. Nilikuwa naomba hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wetu wa Kagera katika mipaka yetu kuna mapungufu makubwa ya namna ya kudhibiti magonjwa hatarishi. Tunaomba kujengewa majengo ya medical department, insulation na kadhalika ili huduma za afya katika mipaka yetu ya Mtukula, Chamchusi, Bugango, Msagamba, Igoma, Rusumo na Kabanga ili kudhibiti magonjwa hatarishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wetu wa Kagera uko katika mlipuko wa majanga mengi. Kwa hiyo tunahitaji kujengewa kituo cha ufuatiliaji wa matukio ya mlipuko, kwa mfano ebola, marburg, surua, polio na yellow fever pamoja Covid, kwa sababu tumepakana na mipaka na nchi zetu jirani. Kwa hiyo, tunaomba sana Serikali yetu iweze kutuangalia kwa jicho la huruma katika Mkoa wetu wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wetu wa Kagera tuna visiwa 38, visiwa vitano tu ndio vina zahanati. Mama wajawazito visiwani hawana pa kujifungulia ili kunusuru uhai wao, tunaomba Serikali yetu itununulie ambulance boat ili kuwezesha dharura za matibabu kutoka kwenda visiwa vingine. Kwa mfano mgonjwa mwingine yuko mahututi ili kumtoa katika visiwa vile aje katika hospitali ya rufaa. Kwa hiyo, naomba sana kwa Waziri, dada yangu Ummy tupate hiyo ambulance boat ili kuweza kunusuru uhai wa wananchi wetu wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wetu wa Kagera umeanza upanuzi wa hospitali ya rufaa ya mkoa kwa kubomoa majengo chakavu. Sasa hivi tumeanza kujenga maghorofa, tuliahidiwa kuletewa bilioni tatu ili kuweza kumalizia. Kwa hiyo, tunaomba hela ije kipindi hiki ili tuendelee na ujenzi wa OPD, wodi za watoto na wodi za wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yangu ni hayo machache, naunga mkono hoja. (Makofi)