Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Yussuf Kaiza Makame (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyenzi Mungu, lakini pili niendelee kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Chake Chake kwa kuniamini, lakini tatu nikishukuru chama changu na niwashukuru pia wananchi wa Chake Chake kwa kuendelea kuyaheshimu maazimio na maagizo ya chama chao. (Makofi)
Baada shukrani hizo naomba sasa nianze kuchangia hoja, na nianze kwa kumnukuu Rais wa mwanzo wa Afrika ya Kusini Iliyohuru, Hayati Nelson Mandela aliwahi kusema; “education is the most powerful weapon which you can use to change the world.” Elimu ndio silaha pekee, taaluma ndio silaha pekee inayoweza ikatumika kuubadili ulimwengu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie kiriri hiki, nitumie nyumba hii kusema kwamba elimu ndio silaha pekee ya kuibadili Tanzania, si jambo linginge. Si Jeshi, si Polisi wala si kingine kitakachoweza kuibadili Tanzania isipokuwa tutumie elimu yetu, tu-invest kwenye elimu ndio itakayoweza kututoa hapa tulipo tukaenda tunapotaka. The best way ni kutumia elimu kwenda kwenye uchumi tunaoutaka wa viwanda, the best way ni kutumia elimu kwenda kwenye demokrasia halisi na mambo mengine yenye faida kwa Taifa hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la mikopo limezungumzwa na wazungumzaji wengi, wachangiaji wengi wamelizungumza suala hili kwa kina. Ila kwa sababu na mimi ni mdau katika suala hili la mikopo naomba nizungumze kwa mantiki ifuatayo; kwanza niwashukuru kama Serikali niwashukuru kwamba mmeianzishia sheria maalum, sheria mlitunga, Namba 9 ya mwaka 2004 ya kwamba isimamie Bodi ya Mikopo ambayo itawezesha kuwapa mikopo vijana wetu wa elimu ya juu, lakini sheria hii ikaeleza kwamba wanaopaswa kupewa mikopo ni wale tu wenye mahitaji ya kupewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, si kila Mtanzania kwamba anapaswa kupewa mikopo kwa mujibu wa sheria hii, ila practically ni vinginevyo. Wale watu waliosoma katika shule za kayumba wanakoseshwa mikopo na wanapewa watoto wa Mawaziri na watoto wengine wa vigogo. Kwa hiyo, niseme suala hili lina changamoto kubwa, kwanza ucheleweshaji wa mikopo ya wanafunzi, ni changamoto kubwa kwa Serikali na hii ndio inayosababisha migogoro baina ya Bodi ya Mikopo na wanafunzi na Wizara ya Elimu, ucheleweshaji wa mikopo ya wanafunzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, , lakini pili wanafunzi wasio na sifa, kupewa mikopo hii, lakini lingine Ofisi za Kanda zimefunguliwa kwenye suala la mikopo. Kuna Ofisi za Kanda katika Miji Mikubwa kama Mbeya, Arusha, Zanzibar, lakini ofisi hizi pengine kuna mtumishi mmoja tu ambaye hawezi kutimiza majukumu ya kikanda, Zanzibar akuna mtumishi na kuna Ofisi ya Kanda. Lakini wanafunzi wanaopata mikopo kutoka Bodi ya Bara au Bodi ya Muungano ya Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu wanalazimika kusafiri kutoka Zanzibar kuja Bodi ya Mikopo Dar es salaam.
Mheshimwia Mwenyekiti, tulitengemea sisi ile ofisi ya Kanda iliyopo Zanzibar isaidie kutatua kero za wanafunzi wanaopata mikopo pale Zanzibar. Kwa hiyo, hii ni tatizo nini result ya changamoto hizi za wanafunzi, nini result yake, matokeo yake wanafunzi wanaandamana hovyo hovyo, baadaye mnaweka ma-red block kila mahali. Mfano leo tu, hatuhitaji hata kutoa historia leo tu wanafunzi wa natural science wa Chuo Kikuu cha Dodoma walitaka kuandamana kuja kudai fedha na hawajawahi kuingia darasani toka tarehe Mosi Aprili. Leo wanakuja kudai fedha, kutumia njia za kidemokrasia kwa sababu maandamano ni haki, mnawanyanyasa, mnaweka magari humo, tension barabarani, vitambaa vyekundu wanakuja hapa kuomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la mikopo mnawapelekea baada ya maandamano, kingine ni kuwafukuza wanafunzi. Wanaandamana mnawabandikizia kesi, huyu CHADEMA, huyu nani, huyu CUF jambo ambalo si la msingi kabisa, watu wanadai haki ya msingi kabisa. Lakini changamoto nyingine wanafunzi wanaenda wakijiuza, kwa sababu ya kukosa mikopo hii kwa wakati. Baadae mnaanza kudili watu wanaojiuza sijui huko Dar es Salaam wasiwepo na nini, ninyi hamjatimiza wajibu wenu Serikali ya CCM, tafadhalini timizeni wajibu wenu kwa wanafunzi hawa, tujenge Taifa letu kwa pamoja.
Mheshimwa Mwenyekiti, ushauri wangu, Serikali kupitia Wizara ya Elimu kwanza itimize wajibu wake wa kupeleka fedha kwa wakati, mpeleke fedha ili kuepuka changamoto hizi, lakini pia wanafunzi wanapoandamana kwa kudai haki na ninyi mkijua kwamba fedha hizi hamjawapa kwa wakati muwaache wadai haki zao kwa sababu wanaeleza hisia zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni kwamba hili suala la Dkt. Suleiman alilolieleza Baraza la Mitihani. Kuna Baraza la Mitihani (NECTA), mimi nataka kulizungumzia kivingine kabisa, ni kwamba Baraza la Mitihani ndio linalopanga division au GPA. Miaka mingi tumekuwa tumekuwa tukitumia division, mwaka 2012 kukafeli wanafunzi wengi hasa kutoka Zanzibar ikaundwa tume na Waziri Mkuu iliyoongozwa na Profesa Sifuni Mchome na Wabunge humu akina Mwenyekiti Mbatia walikuwemo, Mkaja na mapendekezo waliyopendekeza kwenda kwenye GPA lakini sasa siku saba tarehe Mosi mlienda Waziri....
Kengele ya kwanza…
Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Chakechake kwa kuniamini kuja kuwawakilisha katika nyumba hii muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba niseme maneno ya utangulizi yafuatayo. Kwa muda mfupi niliokaa katika Bunge hili, nimegundua kwamba kuna dhambi kubwa inayofanywa ndani ya nyumba hii muhimu. Dhambi kubwa ni kwamba kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, jukumu kubwa la Bunge ni kusimamia, kuishauri na kuielekeza Serikali. Bahati mbaya sana ni kwamba, walioko upande wa Chama Tawala wao wamekuwa Serikali na Wapinzani ndio wamekuwa washauri na waelekezi. Hii ni sawasawa na mkubali tu; ni sawasawa na wale wanaotoka Usukumani kusema wote ni Marais kwa sababu Rais ni Msukuma. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie; historia mara zote inatufunza, hatujifunzi historia. Isiwe shida, kila tunachowaeleza mkawa ninyi ni watu wa ku-argue tu. Yako mengi tuliyo-argue, yako mengi tuliyowaeleza mka-argue, leo mmeyafanya na kwa ufanisi mkubwa. Hiyo faida mmeipata ninyi!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi tu; nilikuwa chuoni mara moja, wanafunzi wakawa wanaandamana kuhusu masuala ya mikopo. Huyu Makonda alikuwa Mwenyekiti wangu mimi nikiwa Katibu Mkuu wa TAHIRISO, wanafunzi walikuwa wakiandamana sana, tulipokwenda kuzungumza na Serikali tukawaambia shida siyo wanafunzi kuandamana, shida ni Serikali ya CCM kutowapa mikopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa nijielekeze kwenye hotuba. Nina mambo matatu tu ya kuelekeza na naomba niyaseme kwa ufupi kwa sababu dakika zangu ni tano. Moja, ni ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na Jeshi la Polisi; na hii nita-cite zaidi Tumbatu Zanzibar; Mpendae ambapo Jeshi la Polisi limekwenda likanyang’anya vifaa, simu na baadaye wakawakanyaga wanawake katika vifua vyao na hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, wakati anapokuja kuhitimisha hotuba yake aje atuambie kabisa ni lini ataileta ripoti ya matukio yaliyotokea Zanzibar? Kwa sababu kuna matukio makubwa ambayo ni ya ulinzi, ni ya kuweka amani na usalama wa nchi yetu. Kuna ulipuaji wa bomu katika nyumba ya Kamishna Mukadam na mengine mengi. Tunaomba Waziri akija hapa atuambie, ni lini ataleta ripoti ya matukio yote yaliyotokea Zanzibar na nani waliofanya? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, utendaji kazi wa Polisi kinyume na PGO yao inavyowaelekeza. Kwa mujibu wa Police General Order, kazi ya Polisi ni kulinda raia na mali zao, lakini si vinginevyo. Sasa hivi Polisi ni watu wa kudhalilisha raia wa Tanzania, zaidi Wapinzani. Kuna vitu vimetokea; kuna matukio kadhaa yametokea; kuuawa kwa Diwani wa Muleba, Mkoani Bukoba, kuuawa kwa Alphonce Mawazo, mtuletee ripoti na mtuletee taarifa; lakini pia kuteswa na kuwekwa watu zaidi ya saa 24 ndani ya Polisi bila kupelekwa Mahakamani, mtuambie mnatumia sheria gani? Kwa mujibu wa PGO yenu inaonesha kabisa kwamba Polisi anatakiwa kuweka…
MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, siungi mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2017/2018
MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina ajenda tatu tu za kuzungumza, ajenda ya kwanza ni huu mchanga wa dhahabu ambao kila mmoja anauzungumza. Ajenda ya pili ni ile sheria ambayo ilipitishwa na Bunge hili mwaka 2015 inayohusu mafuta na gesi na ajenda ya tatu ni hili deni la ZECO kwa TANESCO.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mchanga; hapa hatuhitaji kunyoosheana vidole tena kama Bunge, hatuhitaji kunyoosheana vidole, hatuhitaji kuonesheana mchanga ulichukuliwa vipi au dhahabu iliibiwa vipi. Kinachohitajika sasa ni kuwa wamoja, hatuhitaji tena kukaa tofauti, kinachotakiwa tumeona kwamba tunaibiwa ni lazima Bunge liwe kitu kimoja, hatuhitaji kitu kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu Mheshimiwa Profesa Muhongo kabeba wizi wote au uhanga wa miaka au nusu karne, miaka 50 tumekuwa tukiibiwa mhanga leo katolewa Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo, kaondoka. Mbuzi wa kafara kashaondoka na tulishajua nini tulichoibiwa, tujitahidi tukae pamoja kwa ajili ya Taifa na manufaa ya watoto wetu wanaofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri kwa Serikali; kwangu mimi na muono wangu, hii ni sehemu nzuri kabisa ya kuanzia. Haiwezekani unakuwa unaibiwa baadaye ukasema kwanza usizuie mali iliyoibiwa utafute namna ulivyotayarisha kuibiwa. Kwanza ukamate mali, baadaye u…, haya, ila mkubali makofi haya myakubali kwamba ninyi ndio mliotuingiza katika wizi wa miaka 50 na hili mpige makofi. Kama mlivyoleta ndege, mkubali kwamba ninyi CCM au Serikali ya CCM ndio mliotupeleka kwenye wizi huu wa miaka 50; na mkisimama mjisifu na mkubali udhaifu wenu, hilo ni moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, nashauri mikataba, sheria na zile sera zote tuzilete Bungeni na zile zinazotakiwa kwenda kwenye mamlaka ya utendaji zifanyiwe marekebisho ili mambo haya yasijitokeze tena. Hata hivyo, tujenge refinery zetu wenyewe, kwa nini tunashindwa? Wameamua kuhamia Dodoma bila bajeti wameweza, kwa nini wanashindwa kujenga viwanda vya kuchakatia dhahabu yetu hapa? Kwa nini wanashindwa hili? Wamewalipa wafanyakazi wa Wizara ya Fedha milioni 10, 15, 20 wengine kuhamia Dodoma, wanashindwa ku-maintain hii mali yetu tuliyonayo? Hii ni natural resources, ikiondoka hakuna tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, nashauri, kwa nchi za wenzetu wenye maono ya mbali wanajenga, kwa sababu hizi zikiondoka hazirudi tena, baada ya miaka 50, 55 hatuna tena hiki kitu. Kwa hiyo, tusije tukawaonesha wenzetu historia ya mashimo, tuwaoneshe kwamba tulikuwa na dhahabu, tulikuwa na tanzanite, tulikuwa na whatever, kwa hiyo hivi vyote vinatakiwa vifanyike.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie pia Sheria ya Gesi; Waheshimiwa Wabunge, Sheria ile ya Mafuta waliiingiza mkenge Zanzibar na lazima wakubali na walivunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 102(1), Ibara ya 105(2), Ibara ya 106(3), zote walizivunja…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu, pili nakushukuru wewe kwa kunipa fursa na mimi ya kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu. Kabla ya kusema chochote naomba kwanza niunge mkono Hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani kuhusiana na Ofisi hii ya Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda kwenye maeneo matatu mpaka manne. Suala la kwanza nitazungumzia masuala ya general ya Bunge, nitazungumzia unit ya Bunge Sports, nitazungumzia masuala ya misaada ya Wahisani kwa Serikali ya Tanzania, nitazungumzia Ofisi ya Msajili kwa sababu hii haiwezekani kutokuizungumza kwa yeyote anayesimama upande huu kwa sasa inavyotekeleza majukumu yake, lakini na nne kama nitapata muda nitazungumza suala la uanzishwaji wa Baraza la Vijana la Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwenye issue ya Bunge. Mimi ni Mbunge wa awamu ya kwanza hii 2015/2020, wakati tunakuja hapa kwenye briefing ya kuapishwa mwezi wa Novemba, 2015 nilidhani kwamba Bunge linaloyasema linayasimamia. Tuliambiwa kwamba issue ya vitabu itakuwa mwisho kwenye meza zetu Mkutano ujao kwenye Bunge hili tuliloanza. Mwezi Novemba, tuliambiwa maneno hayo na Spika wa Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matarajio yangu ni kwamba, sasa hivi sisi tungekuwa tunatumia zile computer mpakato. Hizi siyo kwa mantiki ya kujionesha sisi tunatumia ni kwa usiri wa siri za Serikali, nyaraka hizi ni muhimu na kila kitu, lakini mpaka leo tunaenda mwaka wa pili, lile neno
baada ya kulisikia kwenye Briefing ya Bunge halijawahi kuzungumzwa tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu atakapokuja kuhitimisha haya makabrasha yanajaa humu, hebu tujitahidi basi, kwenye hili atakapokuja kuhitimisha atuambie Bunge letu linaenda electronically technological whatever! Atambie tunaenda kwenye computer mpakato au tunaendelea na hili mpaka tumalize Bunge hili la 11? Hilo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nataka kuzungumza kwenye maslahi ya Wabunge. Wabunge kituo chao cha kazi ni Dodoma na ndiyo mmeamua kwamba, kituo cha kazi kiwe Dodoma. Wabunge wanapotoka Majimboni wanakuja Dodoma asilimia kubwa ya Wabunge ni watu wanaoishi katika hoteli ama Guest hapa Dodoma. Tunapotoka kuja hapa tunapanga kwenye vyumba vyetu vya hoteli, sasa tukitoka kwenda kukagua miradi ya maendeleo ya Serikali tunakuwa tayari tumepanga kwenye vyumba vya hoteli, lakini bajeti tunayotengewa ni ile ya kukaa
Dodoma. Kwa hiyo, kimsingi kwenye hili tuache itikadi zetu za vyama na mambo mengine, Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunahitaji stahiki za mtu anayetoka kituo chake cha kazi kwenda sehemu nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa utaratibu tu kwa sababu tukienda Geita, huku tuna chumba, kule tuna chumba, cost zinaongezeka, otherwise mliangalie kwa namna nyingine suala hili kwa ajili ya Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Bunge Sports Club, limeongelewa sana. Tutaliongelea kwa umuhimu wake, hasa mwaka huu ambao tutapokea ugeni. Ninayeongea ni mchezaji wa Bunge Sports Club wa kutegemewa tena. Sasa tuliyoyapata hatutarajii tuyaone tena. Tunakushukuru Waziri Mkuu kwamba mambo yetu yamekua vizuri Kurwa ametoka kama Doto alivyotoka, lakini ilikuwa ni kusuguana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni stahiki zetu kama Wabunge hatuombi. Tunapotoka nje ya nchi ni stahiki zetu tunazopaswa kulipwa siyo kwamba ni maombi au ni huruma ya Bunge kutufanyia hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoomba sasa tunapanga bajeti hapa, mara nyingi tukiongea na Spika anasema bajeti mliipitisha ninyi na nini. Tuliangalie kwa kina suala la Bunge Sports Club hasa tukitilia umuhimu kwamba mwaka huu tutakuwa na ugeni wa East Africa kwenye
mashindano hayo ya East Africa, pia Rais wa Jamhuri ya Muungano ndiye Mwenyekiti wa East Africa. Kwa hiyo, itakuwa aibu kuja kuyapata yale tuliyoyakuta Mombasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine, walisema akina Mheshimiwa Cosato Chumi hapa kwamba tulikuwa tunaingia kwenye magari ya Askari! Wabunge! Wanatushangaa Wakenya, eeh! Wewe Mbunge kweli? Kwa hiyo, tunatarajia mambo haya myarekebishe yakae vizuri, kwa sababu tukipata aibu Wabunge wa michezo linapata aibu Bunge na linapata aibu Taifa kimsingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilisema nitazungumzia ni suala la misaada. Wakati Serikali hii inaingia madarakani mlikuwa mnazungumza kwa kina kwamba tutaenda kwenye kujitegemea na suala la misaada halitakuwa muhimu sana kwa Serikali hii. Tumemaliza mwaka huu wa bajeti asilimia 30 ya bajeti ya maendeleo ndio iliyopatikana na sababu zilizoandikwa kwenye mpango ni mbili tu; kubwa kwamba kuchelewa kwa mazungumzo ya wahisani ambayo kwa kumwambia Mbunge mwenye akili kama mimi hiyo haiingii akilini ndio iliyoandikwa kwenye mpango wa bajeti 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwamba miradi ya maendeleo iliyoandikwa haikukidhi vigezo. Kwa hiyo, ilikuwa haina maana kwangu, sio hoja za kimantiki zinazoingia kwa Mbunge; tuangalie kwa kina kwa nini Serikali yetu ilikosa misaada na fedha za bure kama za MCC, za bure kabisa.
Tuangalie kwa kina tusitoe hoja dhaifu kama hizi kwenye vitabu vyetu vya maandishi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Msajili; suala la Msajili limezungumzwa vizuri kwenye hiki kitabu cha Bunge cha Kamati ya Katiba na Sheria. Hii ni taarifa ya Bunge imeiagiza Ofisi ya Msajili ukurasa wa 30 imeiagiza Ofisi ya Msajili kwamba ifuate sheria, taratibu na kanuni. Kwa maana ya kwamba Bunge limeona kwamba Ofisi ya Msajili inakiuka sheria na taratibu hasa kwenye mgogoro wa Chama cha Wananchi CUF na suala la kutolewa kwa ruzuku isiyofuata utaratibu wa kiserikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa suala hili limeleta mjadala; msidhani kwamba hapa tukijadili tunafurahishana, Watanzania wanaona what is going on kwenye CUF. Huu mgogoro wanaujua what is going on, nini kilichopandikizwa na nini kinachofanywa. Lipumba humu ana genge lake la watu wawili tu and we are forty MPs from CUF. Hatuungi mkono kwa Lipumba, why tunafanya hivi vitu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili suala ni la kuangaliwa kwa kina na Ofisi ya Msajili siyo Ofisi ya kutoa haki kama mtu amefukuzwa anaenda mahakamani na huko ndio kwenye kutoa haki wala hawezi ku…
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Yussuf.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza naunga mkono hoja ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kuhusiana na hili jambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nataka niweke sawa record au Hansard kwamba wakati jana Mheshimiwa Ali Salim akichangia, alipewa taarifa na Mbunge mmoja kwamba kwenye Taifa hili haikumbukwi Tanganyika. Hili ni jambo la upotoshaji na tunajua kwamba Muungano wetu huu ni wa Watanganyika na Wazanzibari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Tanganyika ipo. Hapa pia tukiwa Bungeni tunasema kuna mambo ambayo siyo ya Muungano. Hayo siyo mambo ya sehemu nyingine, ni mambo ya Tanganyika na hakuna jambo ambalo ni la Tanzania Bara. Hakuna Taifa lililozaliwa Tanzania Bara na hakuna uhuru tunaousherehekea ukawa wa Tanzania Bara, ni uhuru wa Tanganyika. Kwa hiyo, naomba tuweke record sawa katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo nilitaka niliseme leo hii ni hili suala la mchanga. Suala la mchanga kidogo limetutoa kwenye ajenda kuu ya bajeti kwa Bunge zima. Sizungumzii Wapinzani wala sizungumzii watawala; nasema kwamba limetutoa na pengine ni mkakati maalum, uliotengenezwa ututoe katika ajenda ya msingi ya bajeti. Watu wengi kwa asilimia 70 bajeti hii, wanazungumzia makinikia ya mchanga, hawazungumzii bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema kwenye kuchangia hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini na nasema tena. Katika jambo ambalo linahitaji mshikamano na umoja wa Kitaifa ni hili, lakini mshikamano huo hauwezi kupatikana kwa maneno tu, tunahitaji kubadilisha sheria zetu na ikibidi twende juu zaidi kwenye Katiba yetu ya nchi kufanyia yale mapendekezo yaliyoletwa na Tume ya Jaji Warioba, yaletwe tena basi tuyapitie na tupitishe Katiba mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili mnadhani kana kwamba linaongelewa kijuujuu. Kama neno alilolitumia Mheshimiwa Bilago, kama kuna watu wanaoenda na maandamano ya mioyo ni Wazanzibari. Suala la Muungano siyo suala la mchezo mchezo la kuangaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumzia mikataba ya madini na tunazungumzia tume zilizoundwa. Leo tumempongeza Mheshimiwa Rais lakini tume zilizoundwa kuangalia masuala ya madini ni nyingi na findings zake zilisomwa, lakini utekelezaji wake haukufanyika. Leo Mheshimiwa Rais kaja, kazungumza aliyoyazungumza, kawa na ujasiri kafanya alichokifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mungu katika Taifa hili kwamba aje Mheshimiwa Rais azione tume zilizopitia masuala ya Muungano au jambo hili la Muungano na mapendekezo yao, aje aseme kwamba sasa ipo haja ya kuunda Serikali tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu jambo hili lipo na tume zote zaidi ya nane zilizoundwa kwenye nchi hii toka kipindi cha Mwalimu Nyerere mpaka leo zote zimependekeza Serikali tatu. Leo tukizungumzia suala la Muungano humu ndani ni kana kwamba unazungumzia kitu cha ajabu. Wapo waliozungumzia madini tunayoibiwa mkawaona wa ajabu; leo ndiyo mnaona hili jambo ni jema zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utawala wa sheria, haki na demokrasia; hatuwezi kuendesha bajeti zetu hizi kama hakuna haki, hakuna demokrasia ya kweli katika nchi yetu. Hili jambo mnaweza mkaliona nila mchezo mchezo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamekosa maji, wamekosa umeme, wamekosa na huduma nyingine muhimu kutoka misaada ya nje ……(Kicheko)

TAARIFA . . .

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefuta hayo maneno. Nasema kwamba utawala wa sheria ambao unafuata haki na demokrasia, sawa sawa! Hapa tunachokizungumza hasa ni uchaguzi ule wa Zanzibar; na hapa mimi sizungumzii nini kinachoendelea Zanzibar, nazungumzia impact ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kutokana na uchaguzi wa Zanzibar kwa kulazimisha viongozi ambao hawakuchaguliwa na wananchi kukaa katika madaraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania sasa hivi ni karibu milioni 50. Sisi Wazanzibari hatufaidiki na REA, lakini wanaoathirika ni Majimbo yenu hayo mnayopigia kelele. Kwa hiyo, ili utekelezaji wa bajeti uende vizuri, ni lazima Serikali ikubali utawala wa sheria, haki na demokrasia katika nchi yetu kwa sababu tumekubali mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mfuko wa UKIMWI; ninachotaka kuzungumza hapa kuna Watanzania wenzetu wanaoishi na virusi vya UKIMWI, wengi sana. Donors wamejitoa au wengi wamejitoa kutoa misaada katika masuala haya ya UKIMWI. Pengine huko tunakoenda hali itakuwa mbaya zaidi. Sasa ninachotaka kushauri kwa Serikali hii, tuwa-serve Watanzania wenzetu kwa pesa zetu za ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetengeneza percent ya kuingia kwenye REA, basi tutengeneze percent ya kuingia kwenye mfuko wa UKIMWI kwa ajili ya kuwa-serve Watanzania wenzetu wanaoishi na virusi vya UKIMWI. Mfano, tumeweka tozo ya Sh.40/= kwa kila lita ya mafuta, tunaweza aidha, kupandisha ikawa Sh.42/= ama kwa hiyo hiyo iliyowekwa tukaweka Sh.2/= kwa kila lita ikaingia kwenye Mfuko wa UKIMWI ili waweze kujiendesha wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Zimbabwe tumeambiwa hawategemei misaada kwenye suala hili. Kwenye suala la UKIMWI Wazimbabwe pamoja na kasoro zao walizonazo, suala la UKIMWI wanategemea fedha zao za ndani. Kwa hiyo, nasi tujitathmini katika hili, linapoteza nguvu kazi kubwa ya Taifa. Kwa hiyo, tuweke tozo japo ya Sh.2/= kwenye lita ya mafuta ama kwenye bia. Kwenye bia tumeongeza Sh.765/= kutoka Sh.729/=. Sasa hapa kwenye Sh.765/= tunaweza tukatoa Sh.5/= tukaingiza moja kwa moja kwenye Mfuko wa UKIMWI kwa ajili ya kwenda ku-serve Watanzania wenzetu. Hii itaenda na yale malengo ya kwamba 2030 UKIMWI uwe haupo tena Tanzania au katika dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la ajira kwa vijana, bajeti hii haikuzungumza kabisa suala la ajira na Serikali hii haijazungumza kabisa toka iingie madarakani suala la ajira. Wanafunzi wanaomaliza vyuo ni numbers...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kusema kwamba miaka mitatu inatosha kujitathmini kile tulichopanga na tulichofanya na sasa tukaja na mpango mpya. Kwa miaka mitatu tulipanga kutumia trilioni kadhaa, mwaka 2015/2016 tulipanga shilingi trilioni 29, mwaka 2016/ 2017 tukapanga shilingi trilioni 31 na mwaka 2017/2018 tukapanga shilingi trilioni 32 hizo tulizoziandika. Hii inatosha kujitathmini kwamba mipango yetu tuliyopanga na kile tunachokifanya ni realistic? Kwa hiyo, ni lazima tujiulize are we realistic kwa tunachokipanga na tunachokifanya kama Serikali? Hilo ni la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili nililisema kwenye Mpango wa 2016/2017 na jana kalisema Mheshimiwa Silinde, mimi naona hakuna succession plan kwamba awamu hii na awamu hii wanapeana vipi mambo yao. Ilivyo sasa awamu hii anatoka na kitabu chake na awamu ijayo anakuja na kitabu chake kipya kabisa which is quite different. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na suala la Katiba Mpya. Katiba Mpya imetumia mamilioni ya pesa za Watanzania. Sasa hivi watu humu wanapita wanasema aah, ilikuwa mambo ya kisiasa, eeh! Katika legacy ambayo ataiacha Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli, katika legacy muhimu kuliko zote mnazoziona leo, basi ni kuandika Katiba Mpya ya Watanzania. Kama leo mnaona Standard Gauge Railway na Stieglers’ Gorge leo ni ya msingi, basi Katiba Mpya ni ya msingi zaidi kwa vizazi na miaka 100 ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimelisema hili kwa sababu, Rais wa awamu iliyopita, Mheshimiwa Kikwete alileta Katiba Mpya, imefikia katika hatua za mwisho kumalizika tumeiacha tunasema kwamba hatuna mpango nayo. Sasa hivi awamu hii ya Rais John Pombe Magufuli imekuja na Stieglers’ Gorge, imekuja na Standard Gauge Railway, imekuja na ATCL, atakuja Rais mwingine, tumefika Makutupora tunataka twende Mwanza - Isaka kwenye Standard Gauge Railway asipokubali…

T A A R I F A . . .

MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachozungumza ni mambo ya msingi, kwa sababu mimi Mheshimiwa Vuma ni rafiki yangu, acha tu aseme alichotaka kusema hakina shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, the issue is tunatumia rasilimali pesa ya Watanzania, tume-invest kwenye Katiba Mpya mabilioni ya pesa lakini sasa suala la Katiba Mpya tumeacha tumeanzisha Standard Gauge Railway, awamu itakayokuja 2025/2035 akisema kwamba mimi kipaumbele changu siyo Standard Gauge Railway, tunafanyaje? Atakapokuja mwingine akasema kwamba mimi kipaumbele changu siyo ATCL, tunafanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachoshauri kuwe na Kamati au Tume Maalum ambayo inaratibu hii miradi ya kimkakati kwa nchi ili rasilimali zisipotee burebure, tumepoteza mabilioni ya pesa. Kila mtu akija na kitabu chake, Tanzania maisha yote tutalaumiana, humu tutakuja kuchekeshana, lakini hatutafika pale tunapotaka, ni lazima kuwe na succession plan, ni lazima kuwe na Tume itakayoratibu masuala ya Kitaifa ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimemsikia Rais mara mbili, mara ya kwanza alisema ataendelea pale alipomalizia Rais wa awamu iliyopita, lakini mara ya pili amesema hana mpango wa kutenga pesa ya Katiba Mpya. Mimi naomba nimshauri Waziri Mkuu, yeye ni msimamizi wa Serikali katika Bunge hili, Rais ni mtu, inawezekana ameteleza, inawezekana amekosea, Mheshimiwa Waziri Mkuu nenda kamshauri Rais juu ya Katiba Mpya, ni lazima irudi kwa Watanzania amalize mchakato huu na legacy yake itakuwa kubwa zaidi kuliko kitu kingine chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia, Mheshimiwa Waziri Mkuu rudi kwa Mheshimiwa Rais, mimi ni mdogo sana, rudi kwa Mheshimiwa Rais kamshauri, mwambie yeye ni binadamu kama sisi as long as amepewa tu mamlaka ya kuongoza nchi hii, ni binadamu anaweza akakosea. Nenda kwa Rais mshauri tena kuhusu suala la Katiba Mpya amalize hapa palipobaki, ataacha legacy kubwa kuliko vitu vyote atakavyoviacha kwa muda mwingi utakaokuja au vizazi vyote vinavyokuja Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni mahusiano. Nataka nizungumze kidogo kuhusu mahusiano ya washirika wa Muungano baina ya Tanganyika na Zanzibar na nitazungumza kwenye vitu viwili tu, kwanza suala la VAT kwenye umeme. Suala hili pengine halitakiwi kuzungumzwa lakini tumelizungumza kwenye mipango yote kwamba Zanzibar ni nchi ndani ya Tanzania si nchi nje ya Tanzania. Sisi tunauza umeme, sisi tunanunua umeme VAT hiyo haipo. Kwa hiyo, sasa imefika muda Mheshimiwa Waziri wa Fedha alichukue na alilete kwenye mpango na kwenye bajeti liishe.

T A A R I F A . . .

MHE. YUSSUF KAIZA MAKAME: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea tarifa hiyo ya Mheshimiwa Jaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nachotaka kusema ni kwamba miaka mitatu tunaenda mwaka wa nne tunazungimzia suala hili. Mara tunaambiwa kaeni na Wizara ya Nishati na Madini ya wakati ule mta-solve, mwaka wa pili inaenda hivyo hivyo, mwaka wa tatu hivyo hivyo, huu ni mwaka wa nne, sasa ni muda wa Serikali kutekeleza jukumu lenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni nchi washirika. Zanzibar siyo Rwanda au Burundi, Zanzibar ni nchi ndani ya Muungano huu, ni washirika, hatuwezi kuuziwa umeme tofauti. Mnawauzia umeme Zambia lakini hakuna VAT hii, Kenya mnanunua Kenya mnanunua hakuna VAT hii, kwa nini Zanzibar?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.