Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Capt. Abbas Ali Mwinyi (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. KAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ununuzi wa ndege mpya kutoka Bombardier umefikia hatua gani? Ni lini hasa ndege hizo zitawasili tayari kwa kutumika (time frame)? Ndege ngapi zinategemea kununuliwa kwa hatua hii ya awali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Tanzania Airport Authority (TAA) mamlaka yake yanagusa pande zote mbili za Muungano (Unguja na Pemba)?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takribani miaka sita sasa cheo cha Ukurugenzi Mkuu wa Shirika la ATCL kimekuwa kikikaimiwa (acting), lini hasa utakuwa mwisho wa kukaimu? Je, unatambua kuwa ndege pekee inayomilikiwa na ATCL, Dash 8-300 imeacha kuruka toka tarehe 11/5/2016 na hakuna taarifa, kipi hasa kimesababisha hali hiyo? Naomba maelezo kuhusiana na hilo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu kwa Taifa letu ambayo imeendelea kudumisha amani na utulivu kwa Taifa letu pamoja na kulinda Muungano dhidi ya maadui wa ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ufinyu wa bajeti kumekuwa na upungufu mkubwa wa makazi ya wanajeshi wetu na wale waliobahatika kupata makazi, hayapo katika hali ya kuridhisha. Upungufu huo wa makazi unapelekea baadhi ya wanajeshi kuishi nje ya Kambi za Jeshi, jambo ambalo ni hatari kwa askari wetu. Suala la askari kuchanganyika na raia kunawashushia hadhi yao kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto kubwa ya ajira kwa vijana wanaomaliza JKT Bara na Visiwani. Nashauri Wizara ya Ulinzi zishirikiane na Wizara nyingine kutoa vipaumbele vya ajira kwa vijana wanaomaliza JKT. Hii itasaidia kwa kiwango kikubwa kurudisha nidhamu ya utumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri, atakapokuja kuhitimisha (kufanya majumuisho) ananiambie nafasi za ajira zinazopelekwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ziko kwa uwiano gani ukilinganisha na Tanzania Bara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na uwiano mdogo kati ya wanawake na wanaume kwa maafisa wa ngazi za juu wa uongozi wa JWTZ. Naomba kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, anapokuja kuhitimisha, ni kwa nini hali hii inajitokeza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, hali ya ulinzi na usalama wa mipaka ya nchi yetu ni shwari kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Napenda kujua mgogoro wa mpaka wa Malawi na Tanzania kupitia Ziwa Nyasa ambao umechukua muda mrefu, ambao unaweza kuleta athari za uwekezaji katika nchi yetu, na hivyo kupelekea hasa Ukanda wa Nyasa kudorora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka wa jana 2016 tulipata taarifa kuwa kuna fedha zilizopelekwa kwenda Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutoka Serikali ya Muungano (Fedha hizo zinatoka Serikali ya India) kwa lengo la kufanya utatuzi wa kero za maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kero hiyo inazidi kuwa kubwa na kutishia vibarua vyetu kama Wabunge. Je, fedha hizo kweli zilipelekwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Muungano ilipata mrejesho wowote juu ya suala hili? Serikali ya Muungano ina nini cha kusema kuhusiana na kadhia hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa kuwa Serikali ya India ina makusudio ya kuikopesha Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dola za Kimarekani 500 milioni na hatimaye Zanzibar kufaidika na fedha hizo, Zanzibar mgao wake ni kiasi gani kati ya hizo? Je, nini kinachokwamisha mkopo tajwa usitolewe mpaka sasa na hasa ukitilia maanani kuwa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi inatuelekeza utatuzi wa kero hiyo?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ABBAS ALI HASSAN MWINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na kutuwezesha kukutana asubuhi ya leo kwa lengo la kujadili maendeleo ya sekta ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii ya adhimu na adimu ya kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mheshimiwa Ali Mohamed Shein kwa kutekeleza kwa umahiri mkubwa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano imefanya kazi kubwa ndani ya kipindi cha muda mfupi sana na baadhi ya mambo waliyofanya yaliyoleta tija kubwa ni pamoja na kupata mafanikio katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya afya, bajeti imeongezeka kwa kiasi kikubwa sana na sasa hivi hata hospitali zetu za rufaa msongamano wa wagonjwa umepungua kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inatokana na kuimarisha hospitali zetu za wilaya na vituo vyetu vya afya. Sio hayo tu bali hata wale wagonjwa waliokuwa na matatizo ya kuwekewa figo (kidney transplant) na wale ambao walikuwa na matatizo ya moyo hali kadhalika sasa huduma tunazo hapa hapa nchini na kwa hali hiyo basi Serikali imeweza ku- save pesa nyingi za kuwapeleka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue fursa hii ya kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na Naibu Mawaziri wake wawili, Mheshimiwa Nditiye na Mheshimiwa Kwandikwa kwa kazi nzuri sana ambayo wanaifanya na kutekeleza wajibu wao ipasavyo, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi ya leo mchango wangu utajielekeza katika maeneo matatu: usafiri wa anga ambapo mimi ni mdau mkubwa; Mamlaka ya Viwanja vya Ndege - TAA (Tanzania Airport Authority) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti - TCAA (Tanzania Civil Aviation Authority). Kama muda utabakia basi nitazungumzia ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa cha standard gauge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuanze na usafiri wa anga. Nichukue tu fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la ATCL na timu yake kwa kazi nzuri sana wanayoifanya na kuandaa mpango mkakati wa muda mrefu wa kujiendesha. Naamini ukitekelezwa vizuri basi kutakuwepo na matunda mazuri ambayo yatazaliwa kutokana na mpango huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina shauku kubwa sasa kuelewa, je, shirika hili lini hasa litaanza kujiendesha lenyewe? Narudia tena swali hilo kwa Mheshimiwa Waziri, lini shirika hili litapata uwezo wa kujiendesha lenyewe? Sio hilo tu, muda gani sasa itatuchukua kurudisha gharama za uwekezaji ambao umewekezwa na Serikali? Nalo hilo ni swali la pili ambalo napenda kujua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshawahi kufanya kazi katika shirika hilo kwa muda wa miaka nane. Kwa kweli kipindi ambacho nilikuwa nafanya kazi, shirika hilo lilikuwa limegubikwa na ukata mkali, hata fedha ambazo ilikuwa tunapaswa sisi wafanyakazi kupelekewa katika Mifuko ya Hifadhi kama PPF zilikuwa haziendi kutokana na ukata huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuarifu kwamba sasa ukata huo na mwaka mmoja tu baada ya uwekezaji mambo yamekuwa mazuri zaidi. Sasa fedha zinapelekwa katika mifuko hiyo kwa wakati, shirika linaendesha mipango yake vizuri kabisa kwa maana ya kwamba linalipa kodi za Serikali na baadhi ya madeni ya shirika yamelipwa, kwa hiyo, hilo ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna faida nyingi sana za kuboresha shirika hili la ndege. Faida ambazo zimepatikana ni pamoja na gharama nafuu za usafirishaji kwa kutumia anga na safari hivi sasa ni za uhakika kuliko ilivyokuwepo siku za nyuma. Kubwa zaidi ni kutengeneza ajira, tunategemea baada ya mwaka huu kumalizika shirika litakuwa limeajiri wafanyakazi takribani 600 ambapo hii ni utekelezaji wa moja kwa moja wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2015. Kwa hiyo, hili ni jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo kidogo pale la kulipwa marubani. Marubani sasa hivi katika shirika letu wanapokea mishahara ambayo ipo chini kidogo na soko la ajira la ndani lilivyo, hili linashusha kidogo morali yao. Kwa hiyo basi, ningemwomba Mheshimiwa Waziri angalau basi awaongezee mishahara marubani wetu angalau ikubaliane na soko la ajira ya ndani. Kwa hiyo, hilo litakuwa ni jambo zuri sana na wenzetu wale watapata motisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ilivyo sasa ni kwamba shirika au nchi kwa ujumla wake imepungukiwa na kada hii ya wafanyakazi (marubani) kwa sababu hakuna succession plan nzuri kati ya wale marubani ambao wanamaliza muda wao na wale ambao wanaajiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina taarifa kwamba kila shirika la ndege kwa maana ya waajiri kuna tozo la asilimia nne ambalo linakwenda kwenye programu ya SDL (Scheme Development Levy) ambapo sijui fedha hizi zinatumikaje au zimenufaisha marubani na ma-engineer wangapi. Kwa hiyo, napenda kujua manufaa ya hii SDL ambayo inatolewa na waajiri wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la viwanja vya ndege, Tanzania Airport Authority inasimamia viwanja 58. Kati ya hivyo vitatu tu ndiyo ambavyo vina manufaa kwa maana vinaweza kujiendesha vyenyewe, vilivyobakia vyote 55 haviwezi kujiendesha vyenyewe vinategemea faida ambayo inazalishwa na hivi viwanja vitatu ambavyo ni cha Mwanza, Arusha na Kilimanjaro nafikiri. Kwa hiyo, hii inapelekea mamlaka hiyo kupata fedha chache sana ya kuweza kutekeleza majukumu yake. Kwa hiyo… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ABBAS ALI HASSAN MWINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema. Pia nichukue fursa hii kumpongeza Waziri Eng. Kamwelwe na Naibu wake wawili kwa kazi nzuri sana wanayoifanya ya kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu kwa asubuhi ya leo nitajikita katika taasisi mbalimbali ambazo ziko chini ya Wizara hii. Nitaanza na Chuo cha Taifa cha Usafirishaji ambacho kwa siku za karibuni tulipata fursa kwenda kukitembelea na Kamati. Tumeona hatua ya maendeleo iliyofikiwa na chuo hicho lakini tatizo kubwa ni kwamba kitendea kazi kikuu hakijapatikana ambacho ni ndege. Kwa heshima na taadhima naomba Waziri atakapokuja kufanya wind-up, aje kutueleza lini hasa fedha ambazo zimeahidiwa na Serikali za shilingi bilioni 4.2 zitatolewa kwa chuo hicho kwa lengo la kununua ndege single engine aina Cessna 172 ambapo mpaka dakika ndege hizo hazijapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, tuna taarifa ya kwamba chuo hiki kitapata fedha kutoka Benki ya Dunia kiasi cha dola milioni 21.5. Fedha hizi pia zitatumika katika ununuzi wa ndege tatu, kwa hiyo, pamoja na zile mbili ambazo zimeahidiwa na Serikali zitafanya jumla kuwa tano. Mpaka ninavyozungumza hawana hata ndege moja katika kitengo hicho jambo ambalo kwa kweli linakifanya Kitengo hicho cha Usafiri wa Anga kudumaa, naomba Mheshimiwa Waziri aje kutueleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli wa hali halisi ilivyo sasa kuhusiana na uwiano wa marubani ambao wamepata leseni uko 60:40 yaani wageni wana asilimia 60 na wazawa wana asilimia 40 ya idadi ya marubani. Kwa hali hiyo basi, iwapo tutakisaidia chuo hiki, nafikiri uwiano huu utapungua kwa kiasi kikubwa. Itafika wakati sasa sisi kwa maana ya wazawa tutakuwa wengi zaidi kuliko idadi ya foreigners kama ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine nilikuwa nataka kugusia kuhusiana na Shirika letu pendwa la Air Tanzania ambapo kwa hali ilivyo hivi sasa linaendelea vizuri. Mengi ambayo nilikuwa nayakusudia kuyazungumza kwa siku ya leo wenzangu walionitangualia kama Mheshimiwa Kitwanga ameyazungumzia, kwa hiyo, sasa hivi nitazungumzia vile vipande ambavyo yeye hakuvigusia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli biashara ya ndege ni ngumu sana na gharama zake za uendeshaji hali hadhalika ni kubwa kupita kiasi. Napenda kukufahamisha tu kwamba, Rubani yeyote validity ya leseni yake ni miezi sita, ukimaliza miezi sita ina maana aidha ufanye revalidation course ambayo haifanyiki nchini bali ni nje ya nchi katika nchi za Canada, Uingereza au Ethiopia na watu gani wana-incur cost hizo ni shirika lenyewe. Kwa hiyo, wameelemewa na mambo mengi sana, cost ya vipuri halikadhalika iko juu sana. Tairi tu lile la Dreamliner linaweza kufika hata dola 10,000, tairi tu moja. Kwa hiyo, mnaweza kuona gharama za vipuri zilivyokuwa juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda nishauri Serikali ni kwamba hatuwezi tukaendesha Shirika la Ndege kwa kutegemea fedha ambazo zinapatikana kutoka katika mauzo ya tiketi peke yake, haiwezekani lazima kuwe na mambo mengine, vyanzo vingine vya kupata mapato. Na vyanzo hivyo kwa upande wa Serikali wanaweza kutoa msahada hii Air Tanzania ikawa na Ground Handling Company yake yenyewe hiyo itafanya wapate fedha mbadala inaweza alikadhalika ikapate ile inflight catering service zile na hiyo ni chanzo kingine cha fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuwapatia sehemu ambayo kama godauni wale abiria ambao wanatoka nje ya nchi kuja kwetu wakija na mizigo yao na ile hasa ile ambayo iko sensitive kwa temperature inaweza ikahifadhiwa katika sehemu zile na baadaye sasa shirika likipata nafasi za kwenda kuzipeleka mizigo hiyo katika nchi za jirani kama Malawi na kadhalika na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jana Mheshimiwa Shangazi alizungumza ya kwamba kuna haja ya kupata Cargo Plane nakubaliana naye kwa hundred per cent, isipokuwa ushauri wangu si lazima iwe cargo plane hundred per cent per serve lakini kuna ndege ambayo inaitwa Comb Q4100 ambayo inachukua mizigo na abiria kwa wakati mmoja nafikiri aina hii ya ndege itakuwa inafaa zaidi kuliko kupata ile ambayo Mheshimiwa Shangazi ame-suggest. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nichukue tu fursa hii kumpongeza Mkurugenzi Mkuu na pamoja na Mwenyekiti wa Bodi kwa kazi nzuri sana ambayo wanaifanya na ninaomba nahisihi kwa kuwa shirika letu hili Air Tanzania halijaweza kusimama katika miguu yake miwili yenyewe limefufuliwa tu majuzi bado lina mahitaji mengi tungeweza kusamehe baadhi ya tozo na hilo si geni Ethiopia Airliner kwa mfano hawalipi landing fees, hawalipi parking fees, wala hawalipi navigation fees na sisi tungewasamahe hawa kwa fees kama hizo kwa sababu kwa mwezi tu kwa aina hiyo kwa calculation zangu ina maana fees hiyo ni zaidi ya milioni 400.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni mzigo sana hili shirika bado halijakua kiasi cha kutosha cha sisi kuanza sasa kuwanyonya. Kwa hiyo, kwa maana hiyo basi naomba Serikali iweze kufikiria jambo hili la kuweza kuwasamehe kodi za aina hiyo itapendeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitaka kulizungumzia leo ni kuhusiana na hifadhi ambayo ya Serengeti, asilimia yaani asilimia 90 ya hifadhi hii iko nchini kwetu Tanzania na asilimia 10 iko upande wa Kenya ambao wao wanaitwa Masai Mara. Sasa kwa ufupi katika sehemu Masai Mara peke yake wao wana airfields tatu za lami ambazo zina urefu zaidi wa kilometa 1.8, ambayo zinakuwa na uwezo sasa wa ndege aina ya Bombardier Q4100, kuweza kutua katika uwanja ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanachokifanya watalii wanapofika katika uwanja wa kimataifa wa Nairobi ambao wanachukuliwa nchi tofauti huko nje ya nchi. Sasa Kenya Airways wanakuwa na kampuni tanzu, nafikiri subsidiary company ambayo inaitwa Jambo Jet, inachukua watalii inawapeleka moja kwa moja Masai Mara. Sasa pale wale watalii hawawi inconvenient hata kidogo, wanakuwa wanafurahia safari yao kwa sababu ni rahisi. Lakini kwa mazingira hapa ya kwetu sehemu ambazo watalii wanaingia nchini ni Dar es Salaam, Kilimanjaro na Zanzibar, halafu wanakuja kwa makundi makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa maana hiyo basi tungeweza kutengeza uwanja wetu wa ambao uko katika sehemu ya Tanzania unaitwa Sereneira ambao uwanja wenyewe una kilometa 2.2 ni mrefu kiasi cha kutosha, lakini unataka maboresho ili wale watalii ambao wanatelemkia Kilimanjaro au Zanzibar wapate fursa au waweze kuchukuliwa moja kwa moja na Bombardier ya Air Tanzania na kupeleka katika uwanja huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo tutakuwa tumeusaidia uwanja wenyewe kupata mapato, lakini kwa Taifa kwa ujumla siyo watalii wote ambao wanapenda kutelemka uwanja wa Kilimanjaro halafu wakachukua magari kuelekea katika sehemu husika, unakuwa unawasumbua kwa hali ya kutosha. Na hii ndiyo namna ambayo Air Tanzania ingeweza kushiriki moja kwa moja katika kukuza utalii kwa sababu unachukua watu unapeleka kule na wakimaliza shughuli zao wanapanda katika huo uwanja wa Sereneira wanarudi katika sehemu ya Airport kubwa ili waweze kuendelee na safari zao nchi ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ningeliomba hili sana upande wa Serikali uboreshwe uwanja ule na hautaki kazi kubwa, ni kuuweka tu control tower pale kwa sababu uwanja tayari upo mrefu ikiwa kama hali ya uchumi hairuhusu pengine si lazima lami kwa kipindi hichi unaweza ukaweka lami baadaYe ukauchonga katika namna ambayo ndege zinaweza kuteremka na kupaki kiurahisi. Hilo linawezekana kabisa nikuhakikishieni pato la Taifa litakuwa kabisa kwa kufanya hili jambo ambalo nail-suggest, halafu kingine… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa ahsante sana, Mheshimiwa Abbas umeongezea dakika tatu za Mheshimiwa Mwita Getere, kwa hiyo, malizia hoja yako.(Makofi)

MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa la mwisho kuhusiana na hali ya Air Tanzania ambayo nilikuwa nataka kuizungumzia ni kwamba kwa ndege zetu, hazitumiki yani kuna underutilization na hizo hizo ndege hazitumiki ipasavyo naweza kusema kama vinatumika kama asilimia 60 underutilization ndiyo inavyofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii inasababishwa na factors zingine kwa mfano viwanja vyetu vingi havina taa na kwa hali ya kawaida ndege haitakiwi kabisa isimame, wanaobadilishana ni Ma-crew lakini ndege inatakiwa ifanye wakati wote masaa 24 ikiwezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kutokana ukweli kwamba viwanja vyetu vichache tu vyenye huduma ya taa ndiyo maana sasa hatufikii ile kiwango cha matumizi ya ndege zilizokuwepo ya kutosha, lakini hii ni sababu moja. Nyingine ni sababu ya kibiashara ya kwanza unapowachukua watalii au watu wa nchi mbalimbali kwa maana ya wa hapa karibuni Malawi, au Lubumbashi kwa mfano ili kuwaleta Dar es Salaam lazima pengine wale wanasubiriwa sasa ndege nyingine ili waende nje, sasa kama hakuna ndege nyingine ambayo inawasubiri wale abiria ambao wanatoka katika nchi jirani inakuwa ni ngumu, hizo ndiyo sababu za kibiashara ndiyo maana ya kwanza tukawa asilimia 60 tu ya matumizi ya ile ndege ambayo tunayafanya ndiyo ambayo yanatokeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ni muda mchache sana yaani si rahisi kumaliza hoja ambazo ninazo kwenye meza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie katika hoja iliyopo usoni kwetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujaalia afya na uzima na kwa wale ambao wana changamoto ya maradhi, basi Mwenyezi Mungu awaponye. Amina.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu kwa siku ya leo nitajielekeza katika taasisi ambazo ziko chini ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Zipo nyingi sana na Taasisi zote hizo nina jambo la kusema juu yake, lakini kwa kuwa muda ni mfupi sana nitafikia pale ambapo…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Abbas maelekezo ya kiti yameletwa kwa wote ni kumi kumi. (Makofi)

MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Basi kwa kuwa ni dakika 10 nami nichukue fursa hii adhimu na adimu kabisa ya kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza vyema yote yale ambayo mtangulizi wake aliishia. Vile vile niwashukuru viongozi wote wengine wa kitaifa Makamu, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Waziri Mkuu na wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa usafiri wa majini na baharini siyo jambo la Muungano, kwa hiyo hapa kwetu Tanzania kuna mamlaka mbili ambazo zimepewa majukumu za kuendesha mamlaka hizo. Kuna mamlaka ya ZMA (Zanzibar Maritime Authority) ambayo iko Zanzibar, lakini vile vile kuna TASAC ambayo iko Tanzania Bara. Kwa hiyo maeneo haya mawili, Mashirika haya mawili au mamlaka haya mawili yanafuata sheria tofauti, kwa upande wa Tanzania Bara kuna Match & Shipping Act. lakini kwa Zanzibar kuna Maritime Transport Act. Sasa katika maeneo haya au mashirika haya mawili au wadhibiti hawa kila mmojawapo amepewa majukumu maalum na yameainishwa katika sheria. Kwa hiyo mipaka inajulikana na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika suala zima la uendeshaji wa mamlaka hizi, masuala haya yote ya baharini yanapaswa kuendeshwa na mamlaka kama nilivyosema awali. Kuna wakaguzi ambao wamekuja kutoka Shirika la Bahari la Ulimwengu ambao wamekuja kufanya utafiti na kutukagua katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo Shirika la Umoja wa Kimataifa la Mabaharia walitupa majukumu ya kwenda kukagua flag state obligation (majukumu ya nchi yaliyopewa usajili wa meli ambayo ndiyo ZMA) lakini na vile vile kulikuwa na Flag State Obligation ambayo majukumu haya yalipaswa kufanywa na nchi ambayo imesajili meli zenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna coastal voyage obligation ambayo anapewa nchi ambayo ina maeneo ya mwambao. Kwa hiyo majukumu haya yamekuwa haya ya mwambao walikuwa wamepewa hawa watu wetu wa upande wa Tanzania Bara kwa maana ya TASAC. Sasa kinachoelekea ni kwamba hii IMO (Umoja wa Ukaguzi wa hayo Mashirika) umetuelekeza ya kwamba lazima ukaguzi uendane na matakwa ambayo wao wanayataka.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kulikuwa na mapungufu yafuatayo na mapungufu hayo ambayo tumeelekezwa tuyafanye na hiyo Kamati ya IMO – International Maritime Organization ni mengi na tunatakiwa kwamba tuyatafutie suluhu. Yapo maeneo ambayo inabidi tuyatekeleze kwa pamoja yaani kati ya TASAC na ZMA lakini yako ambayo ZMA inatakiwa ifanye kivyake, na TASAC inaweza kufanya kivyake kwa hiyo hayo ndiyo maeneo ambayo yanatakiwa kuzingatiwa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Abbas wewe ni Captain wa Boeing, Captain wa Dreamliner, Captain wa Air Bus, tusaidie mengine viwanja vilivyo, matatizo ya ILS, matatizo ya vertical approach, slope indicators…

MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, hapana! Katika kutekeleza hayo ambayo nimeyasema nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri yafuatayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Je, ameunda Kamati ya Kitaifa ambayo inatakiwa ilete majibu kwa yale yote ambayo tumeelekezwa na IMO waweze kuyatekeleza? Tunataka kujua hayo kwa sababu Kamati hiyo ya kitaifa ndiyo ambayo ina majukumu ya kuweza kutusaidia kwa pande hizi mbili za Muungano. Hali kadhalika, Tanzania Bara katika yale mambo ambayo tumeambiwa tuyafanyie marekebisho na IMO - Shirika la Bahari Duniani, kuna maeneo ambayo tumeambiwa lazima tuyafanyie marekebisho, lazima tuwe na pande mbili za Bara na Visiwani ambavyo wafanye hayo mambo kwa umoja wao. Sasa Je, kuna Kamati ya Kitaifa ambayo imeundwa na Mheshimiwa Waziri katika kuhakikisha yanatatuliwa hayo?

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kusema ni kwamba kwa upande wa Zanzibar mamlaka zote hizo imekuwaje na kwamba zinasaidiana vipi, hilo tunataka kujua kwamba je, kuna action plan yoyote ambayo Mheshimiwa Waziri ameunda kwa lengo la kuhakikisha kwamba yale mapungufu tuliyokutana nayo yamepata suluhisho, kwa sababu findings kwa maana ya kwamba mapungufu yameonekana 20 na maangalizo matatu, kuna utaratibu gani wa kuhakikisha ya kwamba tunapata majibu ya hayo ambayo tumeambiwa tuyafanye kwa sababu tumepewa miaka minne ya kuyarekebisha hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa Wakaguzi watarudi mwaka 2023.

NAIBU SPIKA: Ahsante Captain Mheshimiwa Dkt. Abbas kwa mchango mzuri.

MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naunga mkono hoja ahsante.