Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ali Hassan Omar King (57 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Kwanza sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu, ambaye ametujaalia uhai na kutupa afya tukahudhuria hapa kutekeleza wajibu wetu huu ambao tumeuomba kwa
wananchi.
Pili nawashukuru wananchi wa Jimbo langu la Jang‟ombe kwa kunichagua kwa kura nyingi na kwa kumchagua Rais Dkt. Magufuli kwa kura nyingi na hatimaye leo tumepata fursa hii ya kusimama hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu ni kwako, kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia hotuba ya Rais aliyoitoa wakati akilihutubia Bunge siku ya ufunguzi wake.
Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kufanya baadhi ya maeneo ambayo tayari ameshayafanyia kazi baada ya kuahidi kwa kipindi kifupi sana. Hii tayari tumeona jinsi alivyokuwa na nia ya dhati ya kuifikisha Tanzania hapa ilipo. Hii imeonyesha kwamba nia yake ataipeleka Tanzania pale tunapotaka.
Maana tukichukulia hotuba tutapata ushahidi wa kutosha kwamba hivi sasa maeneo mengi yameshafanyiwa kazi na tumeyaona. Ni kweli hapa kazi tu, maneno na fitina baadaye. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa nimsifu Rais wangu, huyu ni muungwana. Kuna usemi wa Kiswahili unasema kwamba ada ya mja hunena, muungwana ni vitendo, tenda watu wataona, majisifu weka kando. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais baada ya kuapishwa aliahidi katika ukurasa wa 10 wa kitabu cha hotuba, kwamba atashughulikia ule mgogoro watu wanaouita wa Zanzibar. Kwa hiyo, alifanya hivyo, tumeshuhudia sote, alimwita Makamu wa Pili wa Rais, Rais wa Zanzibar,
Makamu wa Kwanza wa Rais ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha CUF, akaenda akazungumza nao na hatimaye matokeo tumeyaona kwamba Tume ya Uchaguzi imeshatangaza tarehe ya uchaguzi, nayo ni tarehe 20 Machi, 2016. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda kulizungumza hili kwa sababu inawezekana kuna watu wakawa wanakosa njia za kuzungumza, wakafikiria kwamba Zanzibar kuna mzozo kiasi ambacho kwamba hakuna amani na usalama, kitu hicho siyo kweli. Ndugu zangu tufahamishane kabisa hapa, Zanzibar kuna amani na Tume ya Uchaguzi wa Zanzibar ndiyo yenye mamlaka ya kufanya uchaguzi na kutoa matangazo ya uchaguzi. Hao waliosema kwamba aliyeshinda atangazwe, atangazwe nani? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, matangazo yako mengi, kuna matangazo ya vifo yatatangazwa yote, lakini suala la kutangaza matokeo ya uchaguzi liko chini ya Tume, kifungu cha 42(1) mpaka (5), hakuna mwingine. Sasa katika suala hili la amani na mgogoro wa Zanzibar, Mheshimiwa Rais amelishughulikia vizuri sana na kwa sababu anafahamu yale mamlaka yaliyokuwepo ndani ya Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu walikuwa wakijinadi kwamba wanataka mamlaka kamili, leo wanakimbilia Marekani, wanakwenda Uingereza, wanakwenda kwa Papa, sasa hapo mamlaka hayo kamili ya ndani unayakataa mwenyewe. Wewe umetaka upate mamlaka
kamili, basi tumia Tume yako ambayo imepewa mamlaka kamili. Kwa hiyo, Tume ya Uchaguzi wa Zanzibar ina mamlaka kamili kwa mujibu wa Ibara ya 104 ya Katiba ya Tanzania na pia kwa mujibu wa Ibara ya 119 ya Katiba ya Zanzibar, hilo limeelezwa wazi na halina utata wowote.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuhusiana na habari hiyo ya matangazo nani anagombea Urais, Mwenyezi Mungu ndiyo anaamua nani awe Rais, hatuwezi kuamua hapa.
“Qul-allahumma maalika‟lmulki tuuti-lmulka mantashaa‟u watanzi‟u-lmulka mimman tashaa‟u.” Mungu yeye ndiye anayetoa ufalme, hakukupa Mungu huwezi kuupata kokote; sema, toka mapovu, zunguka, hutoweza kupata chochote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mshairi mmoja anasema, kutapatapa haachi mfa maji baharini, ashika kila mahali aokoke maskini, kafa angali mbichi, mfa maji buriani. (Kicheko)
Sasa ndiyo maana watu wanashika kule na huku wapate hayo mambo. Watu labda hawaelewi, kwa nini Tume ya Uchaguzi ilifuta matokeo ya uchaguzi au ilifuta uchaguzi na matokeo yake hawajui. Kwanza yale ni mamlaka ya Tume, hakuna yeyote wa kuingilia Tume, ile ni Tume Huru, mambo yametangazwa wazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, natoa mfano mmoja, mnaweza mkalia nyinyi. Kura ambazo zimepigwa Zanzibar, nyingine zimepigwa za watu waliokufa. Watu wote wanaelewa kwamba ilitokea ajali ya MV. Spice, watu zaidi ya 6,000 lakini baadhi ya waliokufa mle wamepigiwa kura
zao, sasa huu ni ukiukwaji kwa mujibu wa Tume na Tume ndiyo imetoa takwimu hizo. Sasa wako watu hata vitambulisho hawana…
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Hata vitambulisho hawajachukua, lakini kura zao zimepigwa, katazameni katika taarifa ya Tume.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Hapo hapo ndipo aliposema Rais mzozo na ndipo hapo hapo walipojadili watu na sisi tunajadili hapo hapo. Kwa hiyo, Tume ndiyo yenye mamlaka kamili, watu ambao…
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza muda wangu uulinde. Sasa wamepigishwa kura maiti, sasa hawa wanakaa wapi? Leo mnasema kama uchaguzi ule halali, hawa watu mnaweza kuturejeshea, tukawaona? Kule kwetu kuna kitu kinaitwa giningi au wamewekwa giningi? (Makofi/Vigelegele)
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, hiki ndicho kilichotokea, kama hamjui, mnashabikia mnacheza ngoma si yenu, huo ndio ukweli.
Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, napenda kuipongeza Hotuba hii ya Rais na napenda Rais aendelee kutufanyia mambo mazuri. Miongoni mwa mambo mazuri katika Mfuko wa Jimbo, Rais ameahidi kwamba atautoa mapema na haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo, tunasubiri
ili tuweze kwenda kufanya maendeleo yetu. Ombi letu katika Mfuko huu wa Jimbo uwe unawiana kwa thamani ya sasa hivi kwa sababu ulifanyiwa thamani muda wa nyuma kidogo, kwa hiyo, uende na wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo tunamsisitiza Mheshimiwa Rais, kwa sababu tunafahamu yeye ni mzee wa hapa kazi tu, ni kwamba katika mchakato huu wa Katiba Mpya, amesema amepokea kiporo, kwa kuwa ni kiporo kipashwe moto tu, halafu tuendelee,
kwa sababu mchakato wa Katiba ulikuwa umeshafikia mahali pake, tuanzie pale mahali ambapo tuliachia ili tumalize.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine katika ukusanyaji wa mapato. Tumeona jitihada zake Mheshimiwa Rais, lakini pia, tunapenda ashirikiane na taasisi au zile Professional Bodies ambazo wamo wadau wa ukusanyaji wa mapato. Mle mna Wahasibu, mna na ma-auditors wa Kampuni, ili kusifanyike udanganyifu katika ukusanyaji wa mapato na mapato yasivuje. Kwa hiyo, hii tunasisitiza sana aweze kutumia Sheria, hebu wapewe hizi Professional Bodies zipewe meno.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote haya, tunapenda Rais awe na mashirikiano mazuri na wafanyabiashara au Serikali iwe na mashirikiano mazuri, lakini siyo kwa ajili ya kufanya kodi isikusanywe. Kwa hiyo, wakiwa na mashirikiano hayo, Serikali itaweza kukusanya kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika suala la ulinzi na usalama; katika suala la ulinzi na usalama, nafikiri najilipalipa dakika zangu hapa! Katika suala la ulinzi na usalama hili ni jambo…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kingi, muda wako uliingiliwa hapo katikati, dakika moja ukae!
MHE. ALI HASSAN KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Bado dakika moja!
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Vyombo vya Ulinzi na Usalama hili suala liangaliwe, kwa sababu katika baadhi ya maeneo, watu wanavikebehi vyombo vya ulinzi na usalama. Yako maeneo ambayo vyombo vya ulinzi na usalama havifanyi kazi vizuri kwa sababu ya nature ya
maeneo yale.
Kwa hiyo, hili Mheshimiwa Rais alichukulie hatua, alisema ataboresha makazi kwa wana ulinzi wetu, watu wa ulinzi na usalama. Kwa hiyo, afanye makazi yapatikane ili waepukane na kukaa kwenye nyumba za kupanga katika maeneo ya watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sehemu moja siitaji, alikatwa kichwa Askari akitoka kweke kwenda kazini. Kama watakuwa wanapewa makazi, basi Askari hawataweza kufanyiwa mambo haya ambayo yako kinyume na Sheria. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara hii ya Katiba na Sheria ili kuweza kuboresha mambo yetu ya kisheria katika nchi yetu ya Tanzania kwa maslahi ya wananchi wetu wa Tanzania.
Mheshimiwa Spika, awali namshukuru Mwenyezi Mungu kwa mara nyingine kutujaalia kufika hapa kuja kuchangia mambo ya Watanzania. Watanzania hawa wana matumaini na sisi sana, kwa hiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuchangie kwa mujibu wa mahitaji ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tumesikiliza hotuba tofauti hapa, tumemsikia Mhesimiwa Waziri, tumesikia Kamati, tumewasikia na Wapinzani, siku zote sitegemei kwamba kutatoka jambo zuri upande wa Upinzani hata siku moja! Mheshimiwa Waziri angesema hapa kwamba jamani kuna Mungu aliyetuumba mimi naamini wangesema hakuna Mungu aliyetuumba, hicho ndicho kitu ambacho kwao wao ni cha msingi.
Katika hoja ambazo zinajadiliwa hapa, wengi wamejikita katika kuzungumza mahusiano haya katika Muungano, wako wanaosema kwamba Zanzibar ni koloni la Tanganyika, nilikuwa najiuliza huyu aliyesimama akasema yeye ni nyapara? Maana yake na yeye katokea Tanganyika sasa ikiwa kwamba Zanzibar ni koloni la Tanganyika ina maana kwamba yeye huyu ni nyapara. Ametumwa aseme hivyo. (Makofi/kicheko)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo huyu nyapara tunamwambia kwamba huu ni Muungano halali na Muungano unaojulikana, lakini kuna msema husema kwamba nyapara huwa ana nguvu kuliko bwana na hao wanazungumza hivi maksudi kwa sababu nafikiri hawaelewi. Humu ndani tutatofautiana kwa mengi sana, hata tukiulizana uhuru umepatikana lini basi pia tutatofautiana humu kwa sababu tu ya kusema kwamba labda kuna upinzani na utawala, lakini tunachojadili hapa ni maslahi ya wananchi, kwa hiyo tujikite katika kuchangia vitu ambavyo vitafanya maslahi kwa wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna msemi mmoja pale kwetu Jang‘ombe alisema hivi alitumia lugha moja; ―kuendesha siyo lazima kupitia kwenye haja kubwa, inawezekana kuna wengine wanaendesha kwa mdomoni.‖ Kwa hiyo tumewaona hao, kwa sababu leo tukitazama maneno ambayo yamezungumzwa, hiyo ni kuendesha kupitia mdomo au kwa jina la haraka haraka kuharisha. Kwa hiyo, tumepokea na tutamsafisha na atasafishika. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la haki za binadamu. Suala hili la haki za binadamu na utawala bora kule kwetu iko Tume ingawa mwanzo ilikuwa Zanzibar, kuna tatizo kidogo lakini ikaja pakarekebishwa. Kwa hiyo, tunachoomba kwa sasa hivi ile Tume ya kule kwetu ifanye kazi vizuri sana, kwa sababu yako mambo ya kuzingatiwa na ni muhimu yafanyiwe kazi kwa haraka kwa sababu tunataka kuimarisha masuala ya haki za binadamu.
Mheshimiwa Spika, Tanzania tujue kwamba tumesaini Mikataba ya Kimataifa, hizo nazo zinahitajika kulindwa, hususan haki za watu ambao wanaishi katika Magereza, zimetajwa, kwa hiyo zifuatiliwe na zifanyiwe uchambuzi watu waweze kupewa haki zao. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kingine ambacho ni cha muhimu sana kukizungumza hapa ni suala la Katiba Mpya. Mheshimiwa Waziri aligusia, amezungumzia katika kurasa za mwanzo kuhusiana na Katiba Mpya na ameeleza kwamba taratibu zimegusa sekta tofauti ikiwemo Tume zetu za Uchaguzi, tunaomba jambo hili lifanywe haraka ili liweze kukamilika.
Mheshimiwa Rais alivyokuja kulihutubia Bunge hapa alizungumza kwamba atamalizia kiporo, kwa hiyo maana ya kiporo ni pale kilipofikia, kinapashwa moto tunamaliza. Nafikiri mchakato ulikwenda vizuri, palipobakia tuje tumalize kwa kuzihusisha Tume zetu hizo ili tuwe na Katiba Mpya.
Mheshimiwa Spika, nizungumzie jambo lingine ambalo limezungumzwa hapa kuhusu vibaraka. Mimi nilishangaa sana kwamba kuna vibaraka kule Zanzibar ambao wameweka Serikali...
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.
SPIKA: Mheshimiwa, Taarifa
TAARIFA....
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika siipokei, hata ningesema kuna Mungu, yule angesema hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naendelea. Alizungumzia habari ya vibaraka na akataja pande mbili kana kwamba hazina mahusiano kwamba je, tungewauliza na wao hawa ambao wamekuwa wana ndoa hii ya mkeka hii ambayo siyo rasmi watu wote wanaijua je, yeye anakuwa kama nani wakati anayasemea haya? Kwa sababu hata na yeye huyu mimi simkumbuki kama labda ametokea katika Majimbo ya kule kwetu sijui atakuwa ni nani, lakini ndiyo wale niliosema kwamba nyapara siku zote huwa ana nguvu kuliko bwana. Amejaribu kulinganisha uhusiano, anakubali Mwafrika wa Tanzania kwamba ukoloni ulikuwa bora kuliko uhuru, huyu mtu sijui tumuite mtu wa aina gani? Lakini siku zote ukitaka kumjua mtu ambaye amezoea kulamba makombo ya sahani ya bwana siku zote atakuwa yuko chini yake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hawa ni watu ambao wamezoea kulamba makombo ya sahani ya bwana, watakumbuka tu kwamba wao wanahitaji kulamba. Hakubali uhuru, mimi nashangaa sana tunamwita mtu kwamba utakuja kuwawakilisha wapinzani, unakuja kutoa hoja kama hizi, kwamba uhuru siyo bora kuliko ukoloni. Unauponda uhuru ambao umepatikana umerudi kwa watu wengi, Waafrika wenyewe una-support kwamba bora usingepatikana wewe ni mtu wa aina gani, kwa kutaja nukuu nyingi, kutaja nukuu nyingi siyo kujua, ni kwenda kusoma hata magazeti ukaja ukanukuu hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hicho tunajaribu kusema kwamba wajaribu kukiangalia na wakitathmini, upinzani siyo wa aina hiyo hapa tupo kwa ajili ya wananchi, tumeingia humu kwa sababu ya uhuru na tumo humu tunajadili kwa sababu ya uhuru. Uhuru na Muungano ndiyo uliotuleta hapa, utakapozungumza kinyume na hivi Watanzania watakushangaa, hawahitaji haya, ndiyo maana mnapokosa televisheni huumwa ninyi. Product kama hii ingerushwa kule kwenye televisheni watu wangeonaje kitu kama hicho? tujaribuni kufanya kwa ajili ya Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningelipenda kuchangia, tunajua kwamba zipo Tume, Haki za Binadamu, Tanzania tuna mahusiano ya Kimataifa, pia kuna masuala mengine ya kupata fedha pengine za kutoka nje katika kuhuisha masuala haya ya haki za binadamu. Tujaribu katika fedha zetu za maendeleo tuwe japo kidogo tunazipata ziwe zinatokana na sisi wenyewe, kuliko zaidi kutegemea kutoka kwa wafadhili. Bila ya hivyo tutakuja kujikuta kwamba wakati mwingine tunaweza tukaja tukakwama katika utekelezaji wa masuala ambayo tumejipangia wenyewe.
Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu, tumo humu katika Bunge kama chombo cha kutunga sheria, basi tujaribu tukubali ukweli kwamba Watanzania wanatutegemea na wanatukubali na ndiyo maana wametuchagua kwa hiyo tusiendeleze mambo ambayo yanaweza yakatuletea mfarakano ambao utakuwa hauna maana...
SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALI HASSAN. OMARI KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante, nashukuru sana kupata nafasi hii na la kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uhai tumekuwa wazima, tumekuja humu kwa pumzi ambayo ametupa yeye watu wanaongea kwa sauti kali kwa pumzi ya Mwenyezi Mungu, tunamshukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Mpango ambaye amekuja na mpango huu mimi naweza kusema kwamba ni madhubuti, kwa yule ambaye alikuwa hana sikio alilopewa na Mungu la kusikia hawezi kusikia, aliyekuwa hakupewa jicho la kuona hawezi kuona. Kwa hiyo, haya mengine yatazungumzwa lakini sisi Dkt. Mpango tunampongeza, mpango ni mzuri na mwaka jana tumeona jinsi ya utekelezaji wake unavyokwenda mwenye macho haambiwi tazama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine nimpongeze Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa speed anayoenda. Hii kasi hii haiwezi kuzuilika kwa vitendo vile ambavyo Wapinzani wanaweza wakafanya ni kasi ambayo wao wanajaribu kupuliza kwa maneno kwamba izimike lakini haiwezi kuzimika, haiwezi kuzimika kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mfano mmoja kuna kidege kidogo kilitua juu ya mgongo wa kobe, kilivyotua juu ya mgongo wa kobe kile kidege kikawa kinamwambia kobe, kobe jiandae mimi nataka kuruka sasa. Eeh, kidege wewe? Juu ya mgongo wa kobe ulipotua kobe hajawa na habari! Leo sasa hivi unataka kuruka ndio utakuwa na nguvu za kumshtua kobe? Gamba lote lile la kobe? Kwa hiyo, haya maneno yatasemwa kutaka kuzima nuru ya Serikali hii inavyokwenda, lakini tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini haya maneno ya kupotosha kusema data za uongo watu kuzungumza vitu ambavyo labda vya kupingapinga tu vinajulikana. Kuna msemo wa Kiarabu unasema khalif tawrab, wewe ukitaka kujulikana nenda kinyume, ukienda kinyume utajulikana, wewe ukiambiwa uchumi unakuwa kwa 7% wewe sema unakuwa kwa 4% utajulikana kwasababu utaandikwa zile 4% unazozisema wewe, lakini hata siku moja hajatokezea mke mwenza akasifu kaburi la mke mwenziwe, umeshapata kuona hiyo na yule tayari ameshakufa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilitokea kisa kmoja kwamba mke mwenza kapita katika kaburi la mke mwenziwe akaliona kwamba liko vizuri, alivyoliona lipo vizuri akalisifu, akaambiwa kazikwa nani hapa, aah! Alozikwa hapa ni yule mke mwenzio aaa! Kumbe kaburi baya, kaburi linanuka, hayo ni yale majibu ya maneno yenu ambayo mnaongea, mimi ninachozungumza mtoto akinyea kiganja hakikatwi, lakini tunaongeza mbele kidogo, mtoto akinyea kiganja kwanza unakosha kiganja, unamwosha na yeye na nyie ni watoto mmenyea kiganja, sasa tunakuosheni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huohuo katika hotuba ya Upinzani mlizungumza kwamba katika utawala bora, mkazungumza nyie nyote, kila aliyetoa makelele humu alizungumza hivyo kwamba mkasema polisi hawajafuatilia mpaka leo kesi ile ya Mheshimiwa Tundu Lissu lakini mnajisahau, ukiwa mwongo usiwe msahaulifu kwani si ndio nyie manaotaka polisi wa Kimataifa au sio? Sio nyie mlioambiwa mumlete dereva shahidi wa mwanzo mkasema ana msongo wa mawazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni sawasawa na mtu mwenye busha, mtu mwenye busha, busha linamtatiza na daktari kamwita amfanyie operation, yeye akakataa. Halafu akasema mmeona akasema nitafanyiwa operation na madaktari wa nje, halafu anasema mnaona busha hilo madaktari wenu hawajanitibu, ndio nyie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumzia deni la Taifa ambalo limesemwa humu sisi tunakuwa kwa 32% ya deni la Taifa, lakini ilitakiwa tuwe na asilimia zaidi 55% kwa hiyo, kiwango hicho kinakidhi tusome na ripoti za sehemu nyingine. Deni la Taifa linapimwa kwa uhimilivu wake kwa hiyo tusipotoshe watu katika masuala hayo. (Makofi)

Kwa hiyo, sasa hivi labda nizungumze kitu kimoja kuna kitu kinazungumzwa kinapotoshwa ambacho kipo katika mpango huu. Hususani kwamba kuna watu wanasema kwamba tunategemea maendeleo ya nchi hii kwa fedha za nje wakati kwamba trilioni 12.2 ndio zinatakiwa lakini trilioni
9.5 ni za ndani. Sasa wanaozungumza hivyo wanapotosha hawataki kusema ukweli, ndio hao wa kaburi la mke mwenza. Asilimia 77% ya mpango huu fedha zinatoka ndani, kwa hilo asiyejua nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie vipaumbele vya Serikali, katika vipaumbele vya Serikali cha kwanza ni viwanda vya kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda. Naipongeza Serikali viko viwanda vimeanzishwa na sisi wenyewe tunaona viwanda chungu mzima vinaendelea sasa hivi. Tumepita katika ziara tumeviona viwanda, watu waliokuwemo katika Kamati tofauti tofauti wamekwenda wameona hiyo tofauti, lakini bado watu wanazungumzia kwamba hakuna maendeleo yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa hapa, wanabeza juhudi hizi lakini mwenye macho haambiwi tazama, tumeenda, tumeona. Wewe umeshaona mkia wa ng’ombe halafu unauliza ananyea wapi na wakati wewe mwenyewe umeenda ukakagua viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili natoa ushauri kwa Mheshimiwa Waziri; kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi inavyotaka, hivi viwanda vyetu tunavyovitaka ni lazima vitumie malighafi inayotoka hapa nchini kwetu ili viweze kukuza ajira, viweze kuleta multiplier effect katika wananchi wetu. Pia kupunguza kuuza malighafi nje tukaletewa bidhaa tukauziwa kwa bei kubwa, nayo pia ni tatizo kwa hiyo sisi wenyewe tuongeze thamani, tujaribu kuongeza fursa hizo katika maeneo hayo.

Pia kuna fursa za masoko ya Tanzania sisi wenyewe tunaweza kununua pia Afrika Mashariki, SADC, AGOA endapo tutazalisha, hivyo, tukizalisha tutapata kitu kizuri kabisa. Kwa hiyo, naunga mkono suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale ambao waliokuwa wanasema kwamba hili jambo la viwanda haliko vizuri kama ilivyozungumzwa katika hotuba ya Wapinzani kwamba hawa wafanyabiashara na wenye viwanda wananyanyaswa siyo kweli. Wafanyabiashara na wenye viwanda hawanyanyaswi kwa sababu kituo cha wawekezaji sasa hivi, Mkurugenzi Mkuu wa TPSF yumo mle ni Mjumbe na wanapanga kwa ushahidi wao wenyewe wamesema kwamba vile vikwazo vya biashara sasa hamna na vimeondolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, isitoshe, Baraza la Biashara ambalo Rais mwenyewe ndiye Mwenyekiti katika baraza hili, wao wanakaa na wanapanga na wao wenyewe wametoa ushahidi, wafanyabiashara na wawekezaji binafsi. Llingine, Rais mwenyewe amewaita wafanyabiashara katika siku zake za mwanzo kabisa akawaeleza. Kingine ambacho kwamba maneno yenu mnayosema ni ya uongo, kila mgeni katika viongozi wa nchi za nje wanaokuja hapa wanakutanishwa na wafanyabiashara, sasa wananyanyaswa vipi hawa watu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, Rais kila akizindua mradi wa kiwanda Mheshimiwa Rais naye pia huwa anawapa nafasi na anatoa changamoto kwa watu wanaotaka kuanzisha viwanda na yeye yuko tayari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo katika vipaumbele ni ujenzi wa mazingira wezeshi kwa uendeshaji wa biashara na uwekezaji; kwanza hapa niipongeze Serikali, mazingira ya uwekezaji sasa hivi yanajengwa:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kwa hizo Taasisi ambazo zipo zinafanya kazi ikiwemo Baraza la Biashara, ikiwemo Tanzania Investment Center (TIC). Kwa hiyo, hivi vinafanya kazi vizuri; Pili, pia kuanza kwa reli hii ya standarg gauge itakuza; na tatu ndege ambazo tumewekeza, ujenzi wa viwanja vya ndege na vitu vingine hivi vyote vinakuza mazingira ya biashara. Kwa hiyo hapa naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naipongeza kwa mpango wa kuja kuendeleza katika mpango huu. Wataendeleza Stiegler’s Gorge, wataendeleza reli ya kati, viwanja vya ndege, Shirika la Ndege litaendelea kuimarishwa na mengine ambayo yanazungumzwa, kwa hiyo haya yatatengeneza mazingira ya biashara na uwekezaji. Kwa hiyo, wakati yamo humu na mwanzo yameshaendelea kufanyika katika kipindi kilichopita ina maana kwamba tunajua kwamba, haya mazingira yatakuwa. Hivyo, ukilinganisha haya mazingira ya biashara na ukuaji wa kipato chetu. Sasa naomba tulinganishe na ukuaji wa kipato chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wa kipato chetu sasa hivi per capita ni dola 979, tumetoka hapo tumekuwa kwa 2017 kwa dola 1,025 na sisi tunataka kufikia katika lengo mwaka 2020 - 2025 kwa dola 3,000. Kwa hiyo ili tuweze kwenda speed kama hiyo, sekta binafsi hapa ishirikishwe na ikishirikishwa sekta binafsi tutakwenda vizuri na pia Serikali iweke mazingira katika sekta ya miundombinu. Wakiweka mazingira mazuri hayo pia yatatusaidia katika kufikia mambo ambayo tunaweza tukayafikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengine ni ushauri mbalimbali katika sehemu ya mapato; Mashirika ya Umma yale ambayo yanajiendesha kwa hasara tunaiomba Serikali kwanza ifanye utafiti ikihisi kwamba wanaweza wakaendelea nayo yanaweza yakageuka, sawa, lakini ikiona hayawezi kugeuka, yabinafsishwe ili yatakapobinafsishwa Serikali itakuwa inakusanya kodi na Serikali itakapofanya study itajua nini ifanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mfumo wa tozo za wharfage katika Bandari; Bandari yetu inazalisha mapato zaidi ya asilimia 40, lakini mfumo wa wharfage unaweza ukaturudisha nyuma. Sasa mfumo wa wharfage urekebishwe lakini kwa kufanya utafiti. Tufuate njia ipi? Tutakapofanya utafiti tukaona njia tutakayoweza kufuata, hiyo njia inaweza ikatusaidia, inaweza ikawa ni mwarobaini katika kuzidisha mapato. Tunashukuru kwamba bandari itaongezeka na itajengwa. Tulipita Mtwara kule tumeona Bandari inaendelea, Dar es Salaam sasa hivi tumeona. Kwa hiyo, kwa mazingira ya kujenga Bandari tuweke na mazingira mengine katika mambo ya wharfage ili tuweze kupata kipato kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni katika urasimishaji wa sekta binafsi na urasimishaji wa biashara ndogo ndogo. Kwenye urasimishaji huu tunaomba ufanyike katika ngazi za mikoa kwa sababu utakaposema unafanya katika ngazi ya Taifa kwamba ni lazima TRA ndiyo awe anashughulika na suala hili kidogo itakuwa tabu na ndiyo maana sasa hivi katika huo urasimishaji imefanyika kwa Dar es Salaam peke yake, mikoani bado haijaweza kufika. Kwa hiyo zoezi hili lifanyike mpaka mikoani ili tuweze kuona ile convenience na economy ya kukusanya kodi na wale ndiyo wanaowajua, mkaa na mgonjwa ndiyo anamjua mihemo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali yangu Tukufu ifanye haya, vinginevyo nawapongeza sana na Mwenyezi Mungu atatusogeza mbele ili jambo lingine ambalo watu wanazungumza haya maneno kwa ajili ya kupata umaarufu, tuyasikilize tu. Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru kunipa nafasi hii kuchangia bajeti hii ambayo ina mwelekeo mzuri sana katika nchi yetu hii, hususani katika miundombinu ambayo itatuondoa hapa tulipo na kusogea mbele zaidi. Pia napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na uzima kuweza kusimama hapa kuzungumzia juu ya suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani kule ilikuwa mtu akitaka kubebesa ikiwa ile mistari ya kubebesea imemshinda basi huwa anatafuta maandiko matakatifu aidha aya za Quran au anaweza akatumia hata mistari ya Biblia ili kubebesea. Wakati mwingine ujue mtu kama huyu anakuwa ameshaishiwa. Kwa hiyo, wakati mwingine watu wanaotumia hizi aya inakuwa sivyo wanazitoa katika mantiki yake kwa sababu tu ya kutaka kuhalalisha neno analotaka kulisema, naomba hili tujaribu kuliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali hasa kwa marekebisho ya bandari, ikiwemo Bandari za Dar es Salam, Mtwara lakini pia na mipango iliyopo kwa ajili ya Bandari ya Tanga. Bandari inachangia zaidi ya asilimia 70 ya pato letu au ya kodi zinazokusanywa, bidhaa nyingi sana zinapitia bandarini, kwa hiyo naipongeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa kuwa tunazifanya hizi bandari zifanye kazi vizuri na tunazirekebisha, tuzidi kufanya kazi katika miundombinu iliyobakia kama reli na barabara ili huo mzigo unaopokelewa ufikie vizuri. Huo ni ushauri wangu baada ya pongezi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi nyingine ni katika kuimarisha Shirika la Ndege. Sawa ndege zetu zitakuja na zitakuwepo, lakini pia naipongeza Serikali kwa kuimarisha viwanja vya ndege, kuna viwanja vya ndege14 ukisoma katika hotuba ya miundombinu vitafanyiwa marekebisho na zaidi vitawekewa taa za kuongozea ndege. Hapa naishukuru Serikali lakini ilifanye hili kwa haraka kwa sababu wasipolifanya kwa haraka ina maana tutapoteza vitu vingi sana au mapato mengi sana kutokana na ndege zetu kulala jioni, ikifika jioni zinalala. Kwa hiyo, viwanja vya ndege tukiviimarisha ina maana hapa ndege zetu zitafanya kazi vizuri hata wakati wa usiku na itapunguza muda wa kulala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni hili ambalo limezungumzwa katika Wizara tano, suala la VAT ya bidhaa zinazokuwa manufactured Tanzania Mainland ambazo zitapelekwa Zanzibar. Tulifanya marekebisha mwaka 2016/ 2017 katika Finance Act tukaweka zero rate. Tumeweka zero rate lakini kwa mtu ambaye atanunua kwa manufacturer na zero rate kwa mtu ambaye ni VAT registered. Mheshimiwa Waziri hili suala analifahamu sana, tumelizungumza hapa siku ya Wizara ya Muungano ilikuwa kama ni changamoto, kama changamoto hii haijapatiwa ufumbuzi inageuka inakuwa kero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Finance Bill ya safari hii hatujaona hili suala. Zanzibar kule watu wanatozwa VAT asilimia 36; asilimia 18 anatozwa original na asilimia 18 anatozwa kule kwenye destination. Tatizo hili lipo katika ile sheria, kwa nini tusiondoe utaratibu huu tukarudia ule utaratibu wa marejesho kama ilivyokuwa zamani? Kwa sababu tukisema tunataka tutumie destination principle ina maana kwamba tuendane na vitu vinafuatana navyo. Mheshimiwa Waziri ni mtaalam zaidi katika masuala haya, hili suala linawaudhi wananchi wetu wa Zanzibar. Zanzibar hakuna mashamba, Zanzibar kuna wafanyabiashara. Kwa hiyo, wafanyabiashara hawa ukawawekea kikwazo ina maana kwamba maisha ya watu yanakua mabaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala linakosesha mapato Zanzibar na Bara, pia linasababisha magendo yawe makubwa zaidi na wafanyabiashara na mitaji yao itakufa. Kwa hiyo, naomba hili suala lifuatiliwe na litolewe ufafanuzi. Mimi nimeuliza Zanzibar wamesema hawajatoa ushauri kabisa katika suala hili na lilishazungumzwa kama kero mpaka mbele ya Rais wetu Mtukufu na hapa tumelizungumza sana lakini halijafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni Electronic Tax Stamp. Suala hili kidogo naona kwangu liko kinyume zaidi. Kwanza siyo economy, fedha za kukusanyia ni kubwa zaidi kuliko kodi inayoenda kukusanywa kwa lita. Yaani lita Excise Duty yake ni ndogo kuliko gharama za kukusanyia hizo fedha zenyewe, kwa hiyo siyo economy.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, nimejaribuni kulinganisha jedwali tumeweka Excise Duty kwa bidhaa ambazo zitatoka nje za vinywaji, ukija ukapima moja kwa moja ukihesabu ile gharama itakayoongezeka ya hii Electronic Tax Stamp ni kubwa kuliko gharama ambayo tumemtoza yule ambaye atatoa hicho kinywaji nje. Tukitazama katika majedwali haya tutaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala hilo pia tumesema kwamba kuna mkataba, huu mkataba haiwezekani ikawa ni kikwazo cha kutoondoa maamuzi haya. Kwa sababu mtu unaweza ukaozesha mtoto ikawa siyo wako. Kwa hiyo, ukiozesha mtoto siyo wako ina maana kwamba lazima mkataba huo ufe au cheti hicho cha ndoa hakikubaliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitolee mfano mwingine hata sumu mtu anapokunywa huwa anapewa maziwa. Kwa hiyo, kama tumeshaingia katika mkataba huu naomba tungejiondoa kwa sababu hauna maslahi kwa wananchi, walaji ndiyo watakaolipa gharama hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia huyu vendor ambaye tunataka kumtumia Kenya tayari amekuwa suspended, kwa nini tunataka kumtumia? Kingine, kuna regulation tayari zilishatengenezwa. Kwa hiyo, ni sawasawa na kwamba tuko katika hatua ya kuvalishana pete halafu mtoto anazaliwa ina maana mtoto alizaliwa kabla ya ndoa, sasa hiki kitu naomba kiangaliwe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni tax amnesty ambayo Mheshimwa Waziri amepewa uwezo katika Tax Administration Act, section 70. Naomba mngeshauriana na mngeshauriana na Zanzibar, kwa sababu Zanzibar wanakusanya kodi income tax zinabakia kule kule. Ukisema Waziri wa huku unazisamehe na katika sheria Minister siyo Minister responsible for Finance wa Zanzibar inakuwa ni yule wa Tanzania. Kwa hiyo, naomba mngeshauriana nao kwa sababu mnaweza mkasamehe kitu huku lakini kule kikaleta impact katika mapato ambayo yanatakiwa yakusanywe katika penalties, interest na mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu tozo ya maji ya Sh.50. Tumeona ugumu wake, tutumie ile bird in the hand fallacy, mwenzetu Waziri ni Mchumi, ndege mmoja aliye mkononi ana thamani zaidi kuliko mia ambao wanaoruka katika mbuga au katika msitu au sehemu nyingine yoyote. Waswahili wanasema moja shika, siyo kumi nenda uje. Kweli Serikali imesaini mikopo hata juzi tumeona katika TV kutoka Ufaransa, lakini sasa hii ni ya kwetu, tukikusanya tutapata pesa yetu, hii ndiyo ile moja ya kwetu, moja shika siyo kumi nenda uje. Ndege huyu yuko mkononi ana thamani zaidi. Naomba hilo tulijali na tuweze kulisisitiza liwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe hongera kwa Serikali kuhusu taulo za kike. Ni sawa tunaipa hongera Serikali lakini taulo hizi za kike pia kuna baadhi ya bidhaa zinafungamana nazo navyo vingeweza kusamehewa. Kuna equipment’s na materials pengine yanakuwa imported,hivi navyo pia tungejaribu kutizama ili tukapata uwanja mpana ili hili jambo likawa zuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni kupunguza Income Tax kwa kampuni za wazalishaji wapya wa madawa. Naomba pia ingekuwa ni busara mkawashauri na wale wa Zanzibar kwa sababu makusanyo ya Zanzibar yanakusanywa Zanzibar na yanabakia Zanzibar. Kwa hiyo, ukisema huku ushasamehe hivyo watu wanatafuta loophole na anaweza akapenya na pengine inaweza ikaja ikaathiri. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ajaribu kutueleza, je, makubaliano yapi yalifikiwa katika suala hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni makusanyo ambayo Serikali Kuu itakuwa inakusanya kila kitu. Kusema kweli hapa kidogo inaweza ikatupelekea katika nafasi mbaya sana ya kiuchumi. Ina maana kwamba ukifeli upande mmoja kila kitu kinaharibika. Kila kitu kikiharibika ina maana lawama zote zitakwenda Serikali Kuu. Tujaribu kutazama hii diversification inasaidia, tukiwa na portfolio ya kukusanya mahali na kutumia katika maeneo mengine atleast inapunguza zile risk za kukwamakwama. Kuna vitu vingine utendaji wake utakuwa unakwama kwa sababu mapato yote yanakusanywa upande mmoja. Kwa mujibu wa sheria hii inayotaka kutumika sasa hivi, imewekwa baada ya siku moja kama fedha hazijatumika fedha zitarudi. Je, zitarudishwa tena kwa muda gani au ziombwe tena vipi? Kwa hiyo, hili naomba Serikali ijaribu kulitazama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu korosho, asilimia 65 ya korosho katika export levy. Hili at least lingekuwa linafanyika kama lilivyopangwa, kwamba zirudi kwa wakati vinginevyo, jamaa zangu wa Kimakonde wana msemo mmoja wanasema kwamba, ‘Channumbile Nnungu Cha Kumemena’, ina maana kwamba kila kilichoumbwa na Mungu kinaliwa tu. Hizi asilimia 65 ikiwa haturudishi tukamemena hukuhuku tutawapa taabu na hili zao halitakuja kustawi tena. Tumetanua wigo wa zao, tumeongeza mikoa, sasa hivi hatuko Kusini peke yake tunakuja Kanda ya Kati, tunakwenda na Magharibi, kwa hiyo, tutazame kwamba hili jambo linaendaje katika huu ushuru wa korosho ambao unakusanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na Serikali ijaribu kuangalia ushauri ambao tunaipa. Nashukuru.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na uzima na salama kwa leo kukutana hapa kujadiliana kuhusu bajeti ya ulinzi na usalama katika nchi yetu hii ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa neno moja; kule kwetu kuna ndege kwa kiarabu anaitwa bull bull, kwa Kiswahili anaitwa kasuku. Kasuku ukisema hodi, basi naye anasema vilevile hodi! Sasa kasuku yule ile hodi hajui kama maana yake ni nifungulie mlango. Kwa hiyo, imekuwa yeye ame-copy tu kwamba ndiyo amesema hodi. Nafikiri mmeshuhudia, watu wanazungumza ekari, halafu baadaye wanageuza maneno kwa sababu ni maneno ya bull bull. Anaondoka bull bull! (Kicheko/Makofi)
Mimi najikita zaidi katika kuongelea masuala ya maslahi ya wanajeshi wanapokuwa kazini na wale wanaostaafu. Nachelea kupoteza muda mwingi, nitakuwa consistency na wale waliochangia suala hili. Nitajaribu kuongelea kuhusu wastaafu wa Jeshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mambo mawili; kuna watu waliingia kwenye mikataba huko katika majeshi tunafahamu, pengine watachukua kwa mkupuo au watakuwa wanapata pensheni. Badala yake wakaja wakataka ku-reverse, kuja kujirejesha tena upya. Kwa hiyo, hawa ilikuwa wazingatiwe jambo lao hili kwa sababu lengo ni kulinda usalama na amani ya nchi yetu na lengo ni kuwa na wanajeshi wa akiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wote hawa walioingia kwenye mambo hayo mawili whether ya kuchukua kwa mkupuo au kupata pensheni, lengo letu kama Taifa sasa hivi ni kuwaweka kama askari wa akiba na tusiwe na wapinzani katika ulinzi na usalama.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine la kushukuru, watu wengi sana wameunga mkono hii bajeti. Hii bajeti imeungwa mkono kwa vitendo na watu wote, kwa hiyo, na mimi naiunga mkono bajeti hii na hoja hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napata mashaka kidogo; inakuaje mtu umekaa ukimwona mwanajeshi unaanza kutetemeka, una nini wewe? Una kitu gani ulichoficha? Kuna ajenda gani? Kwa nini wewe uwe unaona taabu kukutana na majeshi ya ulinzi na usalama? Kwanza anza kujiangalia kutokea hapo, una mashaka gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, niongee kitu kimoja; Jeshi la Ulinzi na Usalama kazi yake moja ni kulinda mipaka yetu nje na ndani. Mimi ni shahidi, bomu la mwanzo kulipuka baada ya uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba pale Zanzibar lililipuka mbele ya Kanisa Anglikana Mkunazini, lililipuliwa na majeshi, tulitarajia aende nani?
Mheshimiwa Naibu Spika, bomu la pili lililipuka round about ya Michenzani upande wa njia ya kutokea Bwawani. Likalipuka la kwanza pale, baada ya dakika 10 likalipuka bomu la pili; na mimi mwenyewe nilikuwa niko maeneo ya pale pale kwa sababu ni maeneo yangu ya kujidai. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, haya mabomu ikiwa tunao maadui wa ndani, kwa nini Jeshi letu la ulinzi lisifanye kazi ndani? Mabomu mengine mawili yalienda kuteguliwa katika Kambi ya JKU Zanzibar Saateni. Yametegwa na haya mabomu, tunafikiri jukumu hili ya kutegua hayo mabomu akafanye nani? Jeshi la Wananchi wa Tanzania liendelee kufanya kazi zake ndani na nje ya mipaka yetu, kwa sababu bado tunao maadui wa ndani na nje. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, halafu waliokuwa wanazungumza kwamba jeshi lilienda kuwatisha watu wasishiriki uchaguzi wa tarehe 20 Machi, wamemsahau aliyewatisha! Hivi dakika ile ile kiukweli wamesahau? Basi akili hizi zitakuwa za kuku, maana kuku ukimwinga, anaondoka. Baada ya dakika chache kuku anarudi pale pale. Itakuwa wana akili za kuku hawa, wameshahau aliyewaambia wasiingie kwenye uchaguzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kweli Jeshi la Wananchi ndiyo limeenda kusimamia kwamba watu wasiingie kwenye uchaguzi wa marudio? Mtu anazungumza maneno hayo hapa wakati anafahamu kwamba kiongozi wake ndiye aliyesema hayo maneno. Sasa leo wanakuja kuyaleta hapa, nashangaa sana! (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo moja ambalo lilizungumzwa hapa na wengi kila mtu akikaa anasema kwamba anaunga mkono. Maneno yaliyozungumzwa na Kambi ya Upinzani, mimi namheshimu sana mzee wangu. Maneno aliyozungumza kwamba, demokrasia ya Zanzibar iliharibiwa na majeshi, nashangaa sana. Naweza nikasema, kuna mshairi mmoja anasema; “masikini roho yake, kioo kimemcheza.” (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kweli alijipima na akajiangalia kwamba yeye aje azungumze maneno hayo hapa, amewahi kuwa kiongozi wa ngazi za juu kabisa, maskini roho yake kioo kimemcheza!
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine unapoambiwa ufanye jambo, ujaribu kutazama, wenzako wanakutoea hao! Usiwe zumbukuku ulimwengu uko huku! Ni lazima ujiangalie huko katika hali gani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niunge mkono hoja lakini kingine cha umuhimu kabisa katika kuangalia masuala haya ni hali ya uwiano katika ajira na utawala wa Jeshi la Wananchi, hili ni Jeshi la Wananchi wa Muungano wa Tanzania, ikiwemo Zanzibar na Tanzania Bara.
Kwa hiyo, hata katika utawala, leo wametajwa pale Majenerali nikasema na mimi nitasikia jina la kwetu sikulisikia, tuwe na uwiano katika masuala haya na kwenye ajira pia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ni la msingi na kubwa zaidi, Jeshi letu litahusika na ulinzi wa mipaka katika bahari kuu. Hili liangaliwe kwa sababu ni jambo la kiuchumi na linahitaji zana za kijeshi, lakini pia kuzingatia uharamia unaofanyika katika nchi jirani ikiwemo Somalia lakini uchujaji uwe mzuri kwa sababu pia na wavuvi wetu nao huwa wanakwenda kuvua. Nilimsikia Mbunge wa Bumbwini aliuliza swali katika kipindi cha maswali na majibu kuhusiana na suala hili. Kwa hiyo, naomba masuala hayo yazingatiwe na yafanyike vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo ni muhimu, nimejaribu kupima hapa na nime-synthesis hoja nyingi sana…
(NAIBU SPIKA: Kengele ya pili hiyo, Mheshimiwa muda wako umekwisha.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante, nashukuru sana kupata nafasi hii. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia uhai kufika hapa leo kuchangia bajeti hii ya Taifa. Pia nakushukuru na wewe kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze na pongezi na shukrani kwa Wizara ya Mambo ya Ndani. Shukrani zangu, mwaka 2018 nilikuja hapa nikasikitika kwamba kuna familia 120 ambazo zina wakazi au zina watu ambao wanafikia 480 walikuwa wakitumia choo kimoja. Hivi sasa Jeshi la Polisi kule Ziwani, Jimboni kwangu Jang’ombe tayari kuna choo kinajengwa na sasa hivi kipo katika hatua za mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali ni kwamba kuna choo pale cha zamani cha tokea Mkoloni mimi nimeanza kukikarabati pale, tumeshaingiza fedha kadhaa, lakini tumekwama katikati. Hata kama tukipata shilingi milioni mbili hivi au tatu, basi tunaweza tukatengeneza kile choo kikachangia pale kikaweza kuondoa matatizo. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, hili nalitupa kwake, nikipata fedha hizo kile choo kitamalizika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, nizungumze kwa Wabunge wenzangu kwamba kuna msemo unasema, “asiyelijua chozi, amtazame aliaye.” Kuna msanii mmoja Marehemu John Komba alisema kwamba, “amani duniani imetoweka na pia Afrika imetoweka”; lakini kumbe Tanzania imejichimbia na kama hujui hayo, kaangalie Kongo. Kama hujui kufa, kaangalie Somalia.

Mheshimiwa Spika, katika nchi yetu hii, ukiona vyaelea, basi ujue vimeundwa, amani iliyokuwepo ni kwa sababu ya mifumo ya kazi ya majeshi yetu ambayo yanafanya kazi ndani ya nchi hii. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuyapongeza majeshi yetu yote ambapo sasa hivi sisi tuko katika amani na usalama.

Kwa hiyo, kama kuna watu ambao waliwahi kubeza, wasifanye hicho kitu kwa sababu siyo kitu kizuri na wale ambao wanataka kutulizia ndege mbaya, washindwe na walegee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vote 28 - Jeshi la Polisi huwa mara nyingi linafanya kazi zake kwa kutegemea taarifa na mara nyingi mawasiliano ndiyo kitu muhimu kinachowezesha Jeshi la Polisi kufanya kazi. Sasa nilivyoangalia randama na kitabu hiki cha bajeti, pamoja na maelezo ya Mheshimiwa Waziri, nikagundua sub-vote 2036 ambayo iko katika mkoa wangu wa mjini kuna kifungu 22012 ambacho kinaelezea communication and information. Kifungu hiki kinahusiana na mambo ya mawasiliano ya simu pengine na mambo ya masunduku ya barua.

Mheshimiwa Spika, kwenye sub-vote hii ya Mjini Magharibi, kule hakuna hata senti tano: Je, kule Jeshi litafanya kazi vipi? Nikadhani labda zimewekwa Makao Makuu, nikaenda katika sub-vote 2005 ambayo ni Polisi Zanzibar. Kuangalia pale nikakuta zimewekwa shilingi 180,000/
= na hizi ni kwa ajili ya kulipia masunduku ya posta. Sasa nilikuwa najiuliza: Je, Jeshi la Polisi katika Mkoa wa Mjini tunakoishi sisi pale, litafanya kazi zake vipi bila kuwa na vitu hivi vya mawasiliano? Watafanya kazi vipi?

Mheshimiwa Spika, nilipoangalia maeneo mengine kwenye mikoa mingine kama Kusini, Kaskazini, nimegundua kila sehemu kumewekwa shilingi 15,600,000/=, huku kwetu Mjini Magharibi, hakuna kitu. Nataka Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa, aniambie sisi tutafanya kazi vipi pale Mjini Magharibi? Aje anipe ufafanuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nililiomba katika bajeti iliyopita, nilisema kuna jengo la Kilimanjaro, Ziwani Polisi. Jengo lile liko katika hali mbaya na wakati wowote linaweza likaleta madhara kwa wakazi wa jengo lile. Familia zinazokaa pale zinaweza zikaadhirika. Serikali jambo hili hawajalichukua.

Mheshimiwa Spika, nimeenda kuangalia katika kifungu cha repairs and maintenance of buildings, nimetazama, hakuna fedha iliyotengwa pale kwa ajili ya Mkoa wa Mjini Magharibi. Nimetazama katika kifungu hicho chicho kwa Polisi Zanzibar 2005, hakuna fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya jengo hili kulikarabati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwulize Mheshimiwa Waziri: Je, pale Jeshi la Polisi amewahi kufika katika lile jengo akaona ile hali pale? Usipoziba ufa, utajenga ukuta. Kwa nini tusikarabati? Nimetazama katika fedha za ukarabati, kuna fedha zimewekwa chache sana lakini ziko katika mkoa mwingine. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuangalia hiki kitu. Nasi tulikizungumza hiki, lakini sasa hakuna ambacho kimetengwa.

Mheshimiwa Spika, zimetengwa pesa katika kifungu cha Polisi Zanzibar cha 2005 ambapo fedha zilizotengwa, zimetengwa katika kifungu cha 22019 ambayo ni kwa ajili ya ukarabati mdogo wa Vituo vya Polisi. Kwa hiyo, hakuna ukarabati unaolenga nyumba za Polisi. Mheshimiwa Waziri hili mimi ni ombi langu tokea nimeingia katika Bunge hili. Moja nimepata, lakini hili sijapata. Kwa hiyo, hili nalitupia kwa Mheshimiwa Waziri tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine kwenye bajeti ya maendeleo; sisi pale Zanzibar Polisi viwanja vya kujenga majengo vimo, lakini Mkoa wa Mjini hatujatengewa fedha. Nimetazama kwa Zanzibar nzima kwenye bajeti hii, ukienda katika bajeti ya maendeleo, utakuta kuna shilingi milioni 500 kwa ajili ya Kituo cha Mkokotoni Kaskazini Unguja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale Zanzibar ukija ni aibu. Nyumba ya IGP wamewekwa maofisa wane. Watu wanaohamishwa wakazungushwa vituo, huwa wanakuja pale Mkoa wa Mjini Magharibi na wanafikia Ziwani Polisi. Kwa hiyo, hali ya makazi mle haiko vizuri. Nilipotazama katika kifungu cha 6303 construction of offices and quarters cha Zanzibar, ndiyo nimegundua kwamba kuna hiyo shilingi milioni
500. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, ajaribu kuangalia hivi vitu kwamba vitafanyika vipi ili nasi mjini pale tuweze kupata majengo.

Mheshimiwa Spika, kingine, nakwenda katika vote ya vitambulisho, hapa kwenye vote ya vitambulisho nizungumzie kitambulisho kule kwetu tunachokiita kitambulisho cha Mzanzibar. Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar iliingia gharama na mpaka sasa hivi inaendelea kuingia gharama kutoa vile vitambulisho ili viweze kufanya kazi; na kweli vikatoka. Vilitoka mwanzo kabla ya Kitambulisho cha Taifa. Vitambulisho hivi vimetoka, sasa hivi eti hata benki unapokwenda wanakwambia lete namba yako ya leseni ya gari wanakidharau hiki kitambulisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, hapa sasa hivi kuna usajili wa simu kwamba mtu anaweza akasajiliwa hata na leseni ya gari au kadi ya kupigia kura, lakini kitambulisho kilichomtambulisha kwa taarifa zake zote kinakataliwa. Kwa nini kitambulisho hiki kisiende sambamba na kitambulisho hiki cha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? Kwa nini tunakidharau hiki kitambulisho wakati tayari Serikali moja imeshaingia gharama na bado Ofisi ya Vitambulisho ipo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikwenda benki moja nikasema kwamba kadi yangu ya Uraia ya Utanzania sijachukua, nikawatolea kadi ya Zanzibar wakasema, aah bora ulete leseni ya gari. Hivyo kweli kitambuilisho cha Mzanzibar Mkaazi kikadharaulike ikapate hadhi leseni ya gari katika kupita huduma!

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri kupitia Idara hii ya Vitambulisho vya Taifa ajaribu kuliweka sawa au kutupa ufafanuzi, kwa nini watu wasiweze hata kusajili simu kwa kutumia Vitambulisho vya Uzanzibar? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa nami naweza nikajiandikisha kukamata shilingi, kwa sababu kule Ofisi ya Vitambulisho ipo na bado inafanya kazi na gharama kubwa zimetumika.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nizungumzie katika masuala ya ufanisi kwenye Jeshi la Polisi hususan nazungumzia utendaji kazi katika mikoa yote. Natoa mfano tu, mikoa yote ina Askari tofauti. Mkoa wa kwangu mimi wa Mjini Magharibi, takribani sitaji namba, ukienda kwenye randama ipo, lakini ina Askari wengi zaidi ya mara nne au mara tano ukilinganisha na mikoa mingine.

Mheshimiwa Spika, ukiacha tofauti ya mshahara, ukienda kwenye kifungu cha fuel, ukienda kwenye kifungu cha utilities, military services, travel in country, communication and information, ukiangalia vifungu hivi vyote vimepewa idadi sawa. Amount ya fedha sawa. Hivi kweli hii bajeti ni realistic?

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mjini tumewazidi watu mara nne. Watu wanaoishi pale Mkoa wa Mjini ni wengi, Mkoa wa Mjini Magharibi ni sehemu kubwa, kuna population kubwa, matukio ni mengi. Kwa nini katika kulihudumia Jeshi la Polisi tupewe sawa na Mkoa ambao uko chini mara nne?

Mheshimiwa Spika, naomba ufafanuzi kwa Mheshimiwa Waziri kwa sababu pale tunapokaa wakati mwingine Askari hutumia pesa zao kupiga simu kwa ajili ya kazi, kwa ajili ya kujaza gari mafuta na kufuatilia matukio mengine. Kwa hiyo, aje anipe ufafanuzi, kwa nini viko hivi? Is it realistic?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. (Makofi)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kupata pumzi zake na leo kusimama hapa, lakini pia namshukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia katika Mpango wa Maendeleo. Kabla ya yote, napenda niipongese Serikali kwa hatua kubwa sana za maendeleo ambazo imechukua na sasa tunaona kwamba hatua tunazokwenda, tunakwenda vizuri. Kwa hiyo, naishukuru sana Wizara ya Fedha pamoja na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli. Tunamwombea Mungu aendelee kuchapa kazi na aendelee kufanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna msemo unasema kwamba penye nia pana njia. Kwa nini nikasema hayo? Ukiwa una nia ya kitu, basi njia ya kulitekeleza kile kitu itatokea. Sasa naishauri Serikali, tumeweka shilingi trilioni 107 katika Mpango ule wa Miaka Mitano kwenye ugharamiaji, lakini tukaweka shilingi trilioni 59 kwa ajili ya Serikali kwamba ndio itagharamia huo Mpango; lakini shilingi trilioni 48 ndizo ambazo zitatumika na Sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nije katika sekta binafsi, je, kuna jitihada za kutosha kuhamasisha sekta hii kugharamia huu Mpango? Kwa sababu cha Serikali tunakijua, tutakuja kwenye bajeti hapa, tutapitiasha mipango kwenye bajeti, itakapopita tutajua kwamba hii ni kasma ya Serikali katika kugharamia Mpango, tumeiona. Isipokuwa hatuioni wazi wazi sekta binafsi inavyotumika kugharamia Mpango huu. Kwa maana hiyo, hata hizi figures ambazo tumeziweka, ina maana labda tuje tujumuishe mwisho baada ya miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali iwe na umakini na ichukue hatua za kutosha katika kuhamasisha sekta binafsi. Sekta binafsi hazijahamasishwa vya kusha na huu Mpango ni mipango yetu, imewekwa kwa ajili ya Serikali na sekta binafsi. Kwa hiyo, hilo nilikuwa naliomba. Kwa mwaka ukichukua average, sekta binafsi ilipaswa ichangie kwenye Mpango huu shilingi trilioni 9.6. Sasa je, tunazipata hizi? Kama tunazipata, sasa tumeshakwenda miaka mitatu, tumebakia na miaka miwili, hizo shilingi trilioni 48 za sekta binafsi zitapatikana? Kwa hiyo, naishauri na naiomba Serikali itumie kasi kubwa zaidi katika kuhamasisha miradi ambayo imepangwa kufanywa na sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, kuna msemo unaitwa nia na azma. Azma, unaweza ukaazimia tu, lakini nia unatia nia wakati kile kitendo kiko njiani kwenye kukitekeleza. Nimesema hivi kwa sababu kuna mambo humu yanaonesha kama ni azma siyo ya nia. Huu Mpango umeandikwa kwa ajili ya mwaka unaokuja. Sasa kuna mambo yameandikwa lakini utekelezaji wake huwezi kuja kuyaona, kwa sababu yatafanywa na sekta binafsi. Sasa naiomba Serikali ijaribu kuangalia kitu ambacho wana nia nacho, kile cha azma tukiache kule kwenye Mpango Mkuu, yale mambo ni mengi, sasa mengine yameazimiwa, lakini hayajatiliwa nia kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niongelee kitu kimoja katika msemo huu, kuna kitu kwa Kiingereza wanaita scope. Umetajwa mradi hapa wa bandari ya uvuvi wa bahari kuu, ununuzi wa meli; najiuliza, hii scope itakuwemo ndani ya mwaka unaokuja yote?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia ukurasa wa 66 umetajwa uvuvi wa bahari kuu katika kitabu cha Mpango. Sasa kama kitu tuna nia nacho, basi tukiandike kile ambacho tuna nia nacho kuliko tukiweka scope kubwa halafu baadaye tukaja kushindwa kuifikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote hayo, naishukuru Serikali kwa kuleta Mpango huu na kuyaona hayo mengine na kuyaweka, lakini tunahitaji tuboreshe. Tuweke kitu ambacho kitafanyika kwa karibu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuzungumzia ni mambo mawili, bandari zetu na reli. Tunajenga reli, ni sawa, ni kitu kizuri, lakini mapato ambayo tulitarajia tuyapate kule yalikuwa ni makubwa. Speed ambayo tunaenda nayo au tuliyoanza nayo nahisi bado ni ndogo. Kwa sababu tulisema itakapofika mwaka 2025, tuwe tuna kipato cha kati. Mwaka 2025 kwa mujibu wa Mpango huu, iwe tuna ukuaji wa asilimia 10. Itatoka vipi hiyo asilimia 10? Ni kama tutaziweka bandari zetu vizuri pamoja na reli. Angalau hii mipango imepangwa humu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inaweza ikaja ikatufungua katika kufikia hiyo asilimia 10, lakini Mpango huu wa miaka mitano ambao tumeenda nao tuliolenga hiyo asilimia 10, sasa tumebakia na miaka miwili: Je, tunaweza tukaifikia hii asilimia 10? Kama tunataka kuifikia, hata kama kwa kuchelewa kidogo, basi tujaribu kuangalia bandari zetu pamoja na reli ambazo zitachukua mzigo kupeleka nje. Tanzania ni nchi ambayo imebarikiwa, iko katika eneo zuri, tuna majirani ambao wanatutumia vizuri. Kwa hiyo, nasi ili tuweze kupata uchumi wa nchi hizo, ina maana ni lazima bandari zetu na reli ziwe zinakwenda sambamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, niongelee viwanja vya ndege na ununuzi wa ndege. Tunaishukuru Serikali, ni kweli tumenunua ndege, tunapongeza, lakini bado zile ndege haziko busy vya kutosha. Ili ndege ziwe zinaleta faida na ufanisi, ina maana kwamba ziwe angani, zisiwe kwenye zimepaki. Sasa ndege zetu zinapaki sana. Tatizo ni kitu gani? Ni viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru viwanja vya ndege vya kanda vimejengwa vikubwa ambapo ndege zetu zinakwenda, lakini tujaribu kuwa na viwanja vya ndege vikubwa vya mikoa ili hizi ndege nazo zitumike vizuri ziweze kusaidia uchumi katika nchi hii. Kwa hiyo, Serikali imesema kwamba itasimika taa za kuongezea ndege, ndio; lakini tujaribua kuangalia kwa mikoa sasa. Kanda ya Kusini tumeona, Kaskazini kuna kiwanja kikubwa, tumekiona; Kanda ya Kati, kitakuwepo kiwanja hapa na hiki kingine kimeboreshwa; lakini tujaribu kutizama kwa mikoa, kwa sababu huu uchumi wetu tunaotaka uende, kama tutakuwa na hizi ndege na viwanja vya ndege vikikaa sawa, tutakuwa tunao uwezo mkubwa sana wa kukuza mapato katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nimekusudia niliongelee ni uvuvi wa bahari kuu. Uvuvi wa bahari kuu ni sehemu ambayo hatujaenda na mkakati mzuri wa kuweza kusema kwamba tutakwenda kuukamata uvuvi huo wa bahari kuu au uchumi huo unaopatikana kutokana na uvuvi wa bahari kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, page ya 66 amesema Mheshimiwa Dkt. Mpango kwamba wao watajenga bandari au Serikali itajenga bandari, itanunua meli za uvuvi. Tulikuwa tunaomba ingeshirikishwa na sekta binafsi. Acha Serikali ijenge bandari, lakini ununuzi wa meli kwa nini tusiachie sekta binafsi? Kwa sababu kujenga bandari peke yake ni shughuli; na kama nilivyosema kwamba hata hapa scope yake mimi kidogo naona haikukaa vizuri sana, kwa sababu limesemwa jambo moja pana sana na kutekelezeka kwake katika Mpango na bajeti hii nahisi itakuwa siyo rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali ijaribu kubinafsisha baadhi ya mambo, siyo lazima kwamba Serikali inunue meli, inaweza ikaweka hayo mazingira mazuri kwa ajili ya upatikanaji wa huo uvuvi wa bahari Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine katika uvuvi wa bahari kuu, naiomba sana Serikali itoe tamko au iseme wazi, ule mrahaba wa 0.4; mrahaba ule unavunja shughuli zote za uvuvi wa bahari kuu. Tulikuwa tunapokea meli 81 ambapo kila meli inalipa dola 36,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi baada ya kuweka huo mrahaba, hakuna meli zinazokuja. Hiyo imeweka kwa Kanuni. Sasa tulikuwa tunaomba Serikali hebu iwe wazi, iondoe hicho kitu, at least tuwe tuweze kupata mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amezungumza katika hotuba yake aliyoitoa ukurasa wa sita, alizungumzia...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ali King, malizia sasa hapo.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono...

MWENYEKITI: Nasema malizia dakika zimeisha.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ingeweza kukusanya mapato mazuri sana kutokana na hiko kitu. Kwa hiyo Serikali iwe wazi, hiyo Kanuni kama ipo ieondolewe kwa sababu tunakosa uchumi kutokana na uvuvi wa bahari kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu na nikushukuru kwa kupata hii nafasi ili niweze kuongea mambo ya kitaifa ambayo yanahusiana na asilimia 38 ya Watanzania ambao ni milioni 23 ya population yetu ya milioni 61 ambao ni labor force ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nataka niongelee kitu kimoja, kuna msemo wa Kiswahili unasema kwamba; chanda chema huvishwa pete, kabla sijaenda huko. Nazipongeza taasisi za NSSF, PSSSF, WCF, OSHA, CMA na taasisi zote ambazo ziko chini ya Wizara hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme na msemo mwingine; ada ya mja hunena, muungwana ni vitendo. Muungwana ukinena unatakiwa utende. Katika Mpango wetu wa Taifa umezungumzia kwamba utazidi kuhamasisha kukuza ajira na ujuzi, hii iko katika paragraph ya mwanzo katika mpango mpya. Pia kuna makubaliano ya Association of Tanzania Employers (ATE), waajiri wa Tanzania walikubaliana na Serikali kwamba zikusanywe skills development levy na one third ipelekwe kama ni investment katika kukuza ujuzi kwa vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa agenda yangu ni moja tu, ni Mradi Na. 6581 ambayo ni Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi. Hii programu walikubaliana, Serikali na Waajiri kwamba, itatoka one third ya skills development levy ili kutazama gap of skills ambayo inakosekana katika viwanda vyetu, katika maeneo yetu ya kazi na ndio maana hawa wamechangia, badala yake sasa muungwana amenena lakini hajatenda kwa sababu mpaka sasa hivi hiki kitu bado hakijafanyika na tumezoea kupeleka shilingi bilioni tisa katika bilioni 300 zinazokusanywa za skill development levy. Tunapata gap of skills kwa sababu hatufuati haya makubaliano yaliyopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nazungumzia investment katika ujuzi, investment katika ujuzi kwa Tanzania, mwaka jana kwa Watanzania milioni 61 tuliwekeza bilioni tisa. Mwaka huu tumeshuka tumewekeza bilioni 7.8 katika nchi ambayo sasa tunakwenda katika kipato cha kati, nchi ambayo ukiitazama tuko nyuma kiujuzi, halafu katika mipango yetu tunasema kwamba hiki ni kipaumbele. Naomba tutende yale tunayoyasema. Kipaumbele hiki kweli katika hawa vijana milioni 23 tunaweza tukakuza ujuzi kwa bilioni saba? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Mpango Mkuu wa Miaka Mitano umezungumzia kwamba tutakuza ujuzi kwa vijana 681,000. Hapa ina maana kwamba kila mwaka tungekuza ujuzi kwa vijana 136,200, lakini kwa bahati mbaya msimu uliopita tulikwenda na vijana 10,000 tu ambao ni sawasawa na asilimia saba ya hii 136,000 ya mwaka. Mwaka huu plan yetu kukuza ujuzi kwa ajili ya kupata ajira kwa vijana 12,280, ni sawasawa na asilimia tisa ya mwaka. Kwa maana hiyo hii asilimia tisa ndio itakayokwenda kukuza ujuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nimemsikiliza vizuri Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye paragraph ya 163 na 164 ya hotuba yake ukurasa wa 81 na 82 alielezea kwamba tutatengeneza fursa za ajira 470,257, lakini Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi imetaka tutengeneze fursa za ajira 8,000,000 na hii itakuwa ni sawasawa na asilimia 29 kwa mwaka. Milioni nane kwa mwaka maana yake ni sawasawa na kupata fursa za ajira 1,600,000, badala yake tunapata 470,000, ina maana hapo bado tunaenda kuanguka.

Mheshimiwa Naibu Spika, isitoshe uwekezaji katika program hii ni mdogo tena ni mdogo mno, ni sawasawa na kusema kwamba hakuna kitu. Waarabu wana kitu wanasema kwamba kuna kitu kinaitwa Mudahala, Mudahala ni kumpaka mtu mafuta kwa mgongo wa chupa. Maana yake anaona anapakwa mafuta, lakini kumbe mafuta yako ndani ya chupa, kwa maana hiyo tunakuwa tunamdanganya na kwa kuwa tunajidanganya wenyewe ni sawasawa na kujitekenya halafu tunacheka. Sasa hapa hatufikii malengo ambayo tumeyaweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninazo statistics hapa, nchi yetu ina watu milioni 61, labor force yetu ni milioni 23, lakini pia skilled labor ni asilimia 3.6 peke yake, lakini inatakiwa tufikie asilimia 12. Ni sawasawa tunafikia labor force ya watu 828,000 ambao ndio waliosoma katika milioni 61, ndio skilled labor, hapa tuko chini sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija ukatazama katika hotuba ya Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati yetu amesisitiza kwamba itolewe one third kama tulivyokubaliana na tusipofanya hivyo ina maana kwamba hii program inaweza ikafanyika lakini isilete tija. Tumebaini katika ziara yetu ya Kamati watu wanasomeshwa lakini inakuwa kama anakwenda na kurudi shule, hana kifaa chochote, anarudi mtaani anasahau kila kitu. Ina maana bado elimu hiyo ya ufundi huo tunayowapa inakuwa haileti tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wa Kamati pia umesema kwamba, ni lazima ipelekwe hii, lakini kuna Sheria ya Mafunzo Mheshimiwa Mwigulu alikuja nayo hapa kwenye Finance Act katika Finance Bill, alikubali kuweka one third kama iwe ring fenced, lakini tunashangaa mwisho Serikali haikupitisha. Hapa ninayo Hansard ya tarehe 26 Juni, Mheshimiwa Mwigulu alisema hili jambo litaletwa mwaka huu kwa sababu mwaka jana halikuweza kufanikishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kuzungumza hivi hivi isipokuwa bora labda tujilinganishe na wenzetu ambao na wao wako katika hizi nchi za Afrika, wao wanawekeza vipi na wamefanikiwa vipi? Tutazame Botswana, Botswana imewekeza dola milioni 11.35 ambayo inakuwa ni sawasawa inakaribia kwenye shilingi kama bilioni 25 za Tanzania, lakini Mauritius imewekeza karibu ya bilioni 70. Sisi Tanzania tunawekeza shilingi bilioni 9.0, Mauritius population yao ni 1,301,636, lakini vijana ambao ni labor force, ni sawasawa na watu 532,000, sisi ukitutazama tuko wengi milioni 23 tunawekeza fedha kidogo kuliko ya wao. Botswana labor force yao ni 1,145,000 lakini fedha walizowekeza ni nyingi kuliko sisi na ukitazama population yao ni ndogo kuliko sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa labda tutazame katika skilled labor au labor force ambao ipo. Wenzetu, watu ambao wamekuwa employed ni 400,000 katika labor force ya 500,000, vijana 400,000 wamekuwa employed, vijana 100,000 ndio wako nje ya ajira, lakini bado wamewekeza vizuri. Hiyo ni Mauritius.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukija Botswana katika 970,000 waliokuwa wamekuwa employed ni 732,000 na 232,000 pekee ndio ambao wamekuwa unskilled. Hii inatokana na maamuzi ya makusudi na utashi wa kisiasa. Sisi tuna vijana wengi lakini hatutaki kuheshimu makubaliano. Sasa tatizo linakuja wapi? Tatizo linakuja kwamba bado hatujakubali kubadilika na kama hatutakubali kubadilika ina maana kwamba hatutoweza kufikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huu ni wakati wa kufanya mageuzi katika kutazama ufundi unaohitajika katika soko. Hawa employers wanatoa hizi fedha ili tuangalie required force inayotakiwa pale. Kwa hiyo zile skills zinazotakiwa na hawa waajiri ni lazima sisi tuweze kuzi-produce lakini hatuwezi kutoa zile skills kwa sababu tunaangalia vitu vingine. Hizi fedha zimekosa clarity, hazina uwazi na uwazi wenyewe kwamba hatujui kiasi gani kimekadiriwa kwenda kule, sisi tunasema iende one third kwa makubaliano, lakini inakwenda bilioni tisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwigulu alituahidi kwamba atafanya liwezekanalo ili aweze kukidhi haja ya kupeleka hizi fedha kule ili ziwe nyingi, lakini mpaka leo hatujaona mid-year review. Kwenye hii mid-year review ingeonesha kwamba kuna fedha zimekwenda kwa ajili ya ku-train watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yote yanachangiwa kutokana na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa King, ahsante.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: …msimamo katika kutazama vijana. Naweza nikasema neno moja ambalo niliwahi kulisema…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa King muda wako umekwisha.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: …Mungu anasema; famaa amalali Mussa ila dhuriya, waliomuamini Musa ndio maana akashinda walikuwa ni vijana, lakini sisi vijana tunawatelekeza, hatutaki kufanya kama Musa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwanza nashukuru sana kupata hii nafasi ili tuweze kuchangia mawazo katika upatikanaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na shairi moja ambalo labda litafupisha maudhui wa hii sheria yetu ya fedha. Kuna mshairi mmoja anasema limelia baragumu wameanza kuuliza mlio wake mtamu wengi limewaliwaza wamepayuka kwa hamu wamo wanacheza cheza lakini wapo wasiofahamu bado linawatatiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii bajeti na sheria yetu hii ambayo tunataka kuipitisha ya fedha ni sawasawa na baragumu ambalo limelia na wengi kweli limewaliwaza hakuna mtu ambaye hajasifia kwenye hii bajeti wala hajasifia hii sheria ya fedha. Kwa hiyo, hii ni sawasawa na baragumu lakini kwa wasiofahamu litawachanganya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme kitu kimoja ambacho ni muhimu sana tunaishukuru sana Serikali kwa kupokea mawazo mengi ya Wabunge na kuchukua mengi mazuri kuyafanyia kazi tumeona kwamba mapendekezo yaliyotolewa mengi yameshatengenezewa schedule of amendments na tumeyaona humu. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa kutusikiliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na yote hayo tuna mawazo au nina mawazo ambayo yamesemwa kutokana na hizo sheria ambazo tunataka kuzipitisha hapa. Mawazo yangu ya kwanza katika sheria ya posta na Mawasiliano ya kielektronic sura 306, katika sheria hii Mheshimiwa Waziri ameisema vizuri na jana alitaja mpaka figure ambazo zitakazopatikana kutokana na fedha hizi na akatoa na mgao kabisa mle, kwamba huku kitakwenda hiki, hapa kitakwenda hiki, kwenye maji kitakwenda hiki tunashukuru sana. Lakini hii sheria ni sheria ya Muungano utakaposema unawakata watanzania hizi tozo wanakatwa watanzania wote wale wa Bara na wa Visiwani wa Zanzibar wote watakuwa wanakatwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo watakapochajiwa na hizi fedha tayari Mheshimiwa Waziri umeshazitangaza zinaenda wapi na wapi kuna pahala pamoja hatujasikia kwamba zitaenda ngapi kwa sababu hatosalimika mpaka yule wa Zanzibar kwamba kama atakuwa hachajiwi wala hawezi kukwepeka na sisi tunajua regulator wa haya ni TCRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo Mheshimiwa Waziri utakapokuja kufunga utuambie kuna utaratibu gani wa fedha hizi kwenda Zanzibar kwa sababu hujalisema, sasa tunakukumbusha au kama lilikwisha kuwepo basi uje utuambie Mheshimiwa kwa sababu hatosalimika kule kuna tigo, kuna Zantel, kuna Halotel, kuna Airtel mitandao yote kule ipo. Kwa hiyo, uje utuambie na pia jambo kama hili tunapenda Zaidi likifanyika lifanyike kwa mashirikiano kwa sababu kama kutakuwa hakuna mashirikiano hata hiyo formular ya kusema mnazigawa vipi hizi fedha itakuwa haipo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri utakaposimama utakuja na wewe ni wa jangwani mwenzangu nafikiri utanipa jawabu zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende katika sura ya 148 ambayo inazungumzia masuala ya VAT naipongeza kwanza Serikali kwa VAT refund na tunaipongeza tena Serikali tulipoishauri kwamba warejesheane TRA na ZRB wazo letu amelichukua na wamelifanyia kazi na tumeliona katika schedule of amendment. Pia katika sura hiyo hiyo ya 148 kuna jedwali namba 7 ambalo linazungumzia VAT exemptions tunaishukuru Serikali imepokea kusamehe vifungashio vya madawa na kufuta lile neno kwamba lazima viwe printed tunashukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna jambo moja ambalo niliseme hapa ambalo ni muhimu sana jambo lenyewe kuna raw materials ambazo zinatengeneza vifungashio hizi raw materials zinazotengeneza vifungashio bado hizi hazijasamehewa na raw materials hizo kwa majina ni polypoprene grainews na petgrainews.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chembechembe hizi zinatengeneza hivi vifungashio vinatumika sasa hivi hizi hazijasamehewa kodi ilikuwa tunamuomba Mheshimiwa Waziri kupitia jedwali hilo hilo namba 7 hebu waweke basi na hizi raw material za kutengeneza vifungashio ili tukisema kwamba tumeimarisha sekta ya madawa ionekana kwamba tumeimarisha. Wasiwasi wa Serikali kwamba labda raw materials hizi zitakuwa misused labda zitatumika vingine kutengenezea bidhaa nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme ndani ya hiyo schedule kumetoka control mechanism kwamba lazima Waziri wa Afya approved kwa kuwa Waziri wa Afya aki-approve na hawa kabla hivi vifungashio hawajaviingiza nchini kwanza wanapeleka maombi yao. Wakipeleka maombi yakiwa approved wakati bado materials ziko nje itakuwa tayari ni control moja lakini watakapoingia hapa kuna TMDA wanahusika lakini zitakapopelekwa viwandani nako zinaenda kukaguliwa lakini pia zinafanyiwa uhakiki baada ya kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo tukisema kwamba zitakuwa misused hii control mechanism tuliyoweka ina maana kwamba itakuwa haiwezi kufanyakazi. Lakini kwamba hii control mechanism iliyokuwepo inao uwezo wa kufanyakazi, kwa hiyo niiombe Serikali iruhusu na raw materials kwa sababu utaratibu wa kukaguliwa upo kwa hiyo hivi havitokuwa misuse na tutoe huo uhakika kwa sababu taratibu zote zitafanywa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo jingine ambalo nilizungumzie linahusiana na masuala la takwimu ambalo hili mara nyingi sana huwa tunalizungumza. Hatuna takwimu sahihi tunapotaka kufanya maamuzi ya kikodi mara nyingi tunakuwa tuna importers pengine wa raw materials lakini pia tunakuwa tuna viwanda vyetu vya ndani kwa hiyo tuna base na takwimu zao pengine mfano labda nitoe kwenye mafuta ya kula wako watu ambao ni manufacture na wako wengine ni importers ni suppliers tu ambao wao wanachukua kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa takwimu zinatupeleka wrong wakati mwingine, sasa hivi hakuna mbegu za kuzalisha mafuta na tunajua kwamba huku tumepandisha kodi kwa mafuta ghafi tayari mafuta ya kula ghafi tushapandisha kodi lakini huku mbegu hatuna ina maana kwamba takwimu zimetucheza. Zimetucheza pia kwenye sukari, wazalishaji wa ndani wanaweza wakasema kwamba tunaouwezo wa kulisha sukari katika nchi yetu lakini kumbe tukaweka kodi kubwa kwa sukari ya kutoka nje matokeo yake mzigo wanakuja kuubeba wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali ijaribu kuwa na takwimu sahihi ili kufanya maamuzi haya ya sera za kodi yawe sahihi tusiweke maamuzi haya ya sera za kodi halafu baadaye haya maamuzi hayaji kuwa sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo Mheshimiwa Waziri alilizungumza ambalo alisema katika hotuba yake ya mwanzo na leo napenda nilizungumze kuhusiana na kupunguza miaka kwa Jeshi la Polisi miaka ya awali 12 kufikia hadi miaka 6. Hapa kwanza niipongeze Serikali lakini kingine Serikali ijaribu kuangalia hawa watumishi wetu kwani haiwezekani kwamba tokea mwaka wa kwanza ameajiriwa huyo askari akaanza kupelekewa pesa zake katika mfuko wa pensheni kwa sababu unapokaa uaskarini kwa miaka 12 halafu baadaye hii pensheni fund sheria zao kama hujachangia kwa miaka 15 wewe huwezi kupewa pensheni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuwa huwezi kupewa pensheni ina maana kwamba miaka yako kama ikiwa haijamalizika na taratibu za ajira za askari tunazielewa. Askari kama hujapewa cheo ukiwa una miaka 48 unatakiwa ustaafu na ukiwa cheo chako kidogo pengine huwezi kufika umri ule mkubwa na huku miaka 12 ambayo ulikuwa umekaa bure bila kuchangia kule inawezekana ukapata kiinua mgongo siyo kikubwa na ukakosa pensheni ya maana na ndiyo maana tunaweza tukaja tukawatesa askari wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niishauri Serikali wakati tumeamua kwamba askari watakapokuwa wanaajiriwa basi wapelekewe fedha zao katika mfuko wao tokea mwaka wa kwanza ili kuepusha kuja kupata pensheni ambayo pengine askari wengi wanaweza wakaja wakalalamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuwa na tatizo hili, jimbo langu ni jimbo ambalo lina askari wengi ndiko kwenye kambi kubwa ya polisi kwa pale Zanzibar ziwani kwa hiyo hili tatizo nimeshughulikia kesi nyingi sana za askari malalamiko yao kutokana na viinua mgongo na pensheni ambazo wanazopewa kutokana na tatizo hilo. Kwa hiyo, niipongeze Serikali lakini wafikirie Zaidi kuwapa pensheni tokea mwaka wa mwanzo ambapo anapoanza.
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kuwa hai na kuwa salama tukahudhuria kikao hiki kujadili Mpango wa miaka Mitano wa Maendeleo wa Taifa. Pili, ninashukuru kupata nafasi hii ili na mimi kutoa maoni yangu kuishauri Serikali juu ya Mpango huu wa Maendeleo ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, uongo usiokanushwa hugeuka kuwa ukweli. Maelezo ambayo yametolewa hapa kwamba hawatotambua, hawatofanya nini, hayo yanazungumzwa na wengi, lakini kutotambua Serikali wamefanya kama watu ambao wamekula soro ya kizamani, maana soro ya kizamani inavyoliwa huwa yule mlaji hufunikwa kanga haonekani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu wanasema hawatambui lakini sasa kinachotoka Serikalini wanasema ni haki yao, sasa ni wajibu wa nani? Ikiwa wewe kwako haki ina maana kwamba ni wajibu wa mwingine, sasa hapo tayari umeshatambua Serikali ukitaka usitake. Kama wewe kweli hutambui kama Mungu yupo kwa nini unavuta hewa yake, imetengenezwa na nani? Wewe unasema hiki kitu hakipo kwa nini wewe unatumia na unasema hakipo, sasa hayo ni maneno tu ya mtu ambaye tuseme ni maneno ya mfa maji. (Makofi)
Kuna maneno hapa yanazungumzwa kwamba labda CCM wangetuachia sisi, sasa ninyi mnataka kushindanisha nazi na machicha katika kutoa tui? Hata mkimsimamisha 2020 na 2025 yale ni machicha, machicha ni machicha tu, yamebakia kuanikwa sasa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo langu ni kuchangia Mpango huu na nimelenga kuchangia katika suala la financing strategy ambayo imeelezwa kama ni mpango wa upatikanaji wa fedha katika kugharamia huu Mpango. Wazungumzaji wengi wameeleza katika kuchangia kuinua maendeleo ya nchi hii lazima tukope, hata nchi zingine nazo zinakopa katika kufanya mipango yao, Marekani wanakopa China, Japan wanakopa China na wote hawa wanakopa ili ku-finance mipango ambayo ipo wameiweka ili kuendeleza mataifa yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikizungumzia suala ya deni la Taifa ambalo limewahi kuzungumziwa na wachangiaji, kuna msemo mmoja wanasema mcheza ngoma isiyo yake daima ataharibu, hawi sawa na wenzake kutwa huwa kwenye taabu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika,una mtu anazungumza deni la Taifa kwamba kutokana na ile percent ambayo ameizungumza Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ni asilimia 36.8 ya Pato la Taifa, anasema ni kubwa na halitofaa, wame-comment mengi. Lakini niwafahamishe tu vile ni vigezo vya Kimataifa siyo vigezo ambavyo labda vimezaliwa hapa Tanzania peke yake, ni vigezo vya Kimataifa na kila nchi inatumia vile vigezo, hilo ni jambo moja kwanza lifahamike.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili watu wafahamu kwamba Deni la Taifa kuwa himilivu vile ndiyo vigezo vyake, watu wafahamu kwamba Japan ni nchi ambayo inaongoza hata hapa Tanzania kwa kutupa misaada, lakini deni lake la Taifa kwa Pato la Taifa ni asilimia 246. Marekani asilimia 105 mwaka jana, mwaka huu asilimia 104, sisi ni asilimia 36.8. Kwa hiyo, ili kuweza kufanikisha malengo ambayo yapo katika mpango huu ni lazima tukope, wanaita leverage, ukitaka kubeba kitu kizito ni lazima uweke lever. Kwa hiyo, lever ni huu mkopo ambao utatusaidia kubeba mzigo wa maendeleo ambao tumejipangia wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kitu kimoja katika kukopa. Tumepanga kukopa ndani pia tumepanga kukopa nje, ninatoa ushauri kwa Serikali katika kukopa ndani bora zaidi tukope nje kuliko kukopa ndani, kwa sababu tutakapo kopa ndani mwenendo wa riba unaweza ukaongezeka, tulichopanga kwamba tuna sekta binafsi tunazitarajia nazo zishamirishe ukuaji wa uchumi. Kwa hiyo, mwenendo wa riba ukiwa juu ambao utasababishwa na kukopa ndani utainua riba ikiwa Serikali inakopa ina maana kutakuwa free risk, ile free risk kila mmoja atapenda aikopeshe Serikali, hatopenda kukopesha watu binafsi, hapa riba zitapanda juu kwa maana hiyo watu binafsi ama sekta binafsi zinaweza zikaanguka, hivyo nashauri tukope nje zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili tukope nje zaidi tujaribu kutizama mikopo nafuu, mikopo nafuu ipo lakini pia Serikali inaweza ikaingia katika International Financial Market ikakopa, hiyo ipo, lakini tunasahauri pia tena kuwa jambo hili kwamba ile sovereign credit rating ifanyiwe haraka ya Tanzania imalizike ili riba tutakayokopa kutoka nje iwe chini. Hili jambo tunaishauri Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, utakapokopa mwaka huu, utakapofanya maendeleo kama umekopa ni muhimu kwetu kuonekana kile tulichokopea kimefanyika. Kikiwa kimefanyika lile deni litakuwa halina shida kulipwa kwa sababu tayari kilichokopewa kimefanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika aina za financing strategies ambazo zimeelezwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha, moja ni kufanya FDI (Foreign Direct Investment). Katika hili watu wa nje kuja kuwekeza mitaji yao moja kwa moja tujaribu kuchambua, tuchambue mapema ili tusije tukaja tukapata hasara kama inayowakuta watu wengine. Kwa sababu kuweka moja kwa moja Foreign Direct Investment bila ya kuchungulia chungulia au kaungalia tunaweza tukaja tukajitwisha mzigo ambao baadaye unaweza ukaja ukatugharimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi Foreign Direct Investment zinafanyika lakini tuangalie mazingira yatakayotupa nafuu katika kufanyika kwake. Kwa mfano, hivi sasa tunaweza tukawaita watu kuja kufanya hiyo Foreign Direct Investment kwetu, lakini baadaye ikaja ikawa mzigo wakataka kuweka mishahara wanayotaka wao, wakaweka mazingira magumu ya kazi, wanaweza wakawa wanabeba faida wanaenda nazo kwao, lakini jambo baya zaidi wanaweza wakaja wakafanya transfer pricing waka-quote bei kubwa kwa kupeleka kule kwao halafu sisi tukaja tukaathirika zaidi. Kwa hiyo, hili tujaribu kuliangalia ili tuweze kufaidika na hii Foreign Direct Investment tuchuje, kwa sababu wanaweza wakaja kutokana na hamu kubwa tuliyonayo tukawapokea haraka bila ya kuwachuja.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa niongelee ni kuhusiana na viwanda ambavyo Tanzania tumelenga kuviweka. Nchi yetu ya Tanzania siyo kisiwa, tuna ushirikiano wa Kimataifa, tuna ushirikiano wa Kikanda na kuna makubaliano mengine ambayo yamefanyika ya Tanzania na nchi nyingine, kupanga ni kuchagua.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokusudia kufanya viwanda hapa kwetu tujaribu kufanya comparative advantage analysis, kwamba ni jambo gani tunaweza sisi katika kuzalisha kwetu likatunufaisha zaidi kuliko kitu kingine, ni viwanda gani ambavyo ni vya kuweka hapa kwetu kuliko kuweka viwanda vya aina zote, tusije tukaja tukakurupuka. Kwa mfano, alizeti inazalishwa Tanzania, wafanyabiashara wa mafuta ya alizeti au wazalishaji wa mafuta hayo hapa Tanzania wanahitaji nafuu fulani. Tunaweza tukasema kwamba tuna-block pengine bidhaa za kutoka nje, lakini ku-block kwetu bidhaa za kutoka nje tuna ushirikiano wa Kikanda, tuna ushirikiano wa Kimataifa, tujaribu kupima ile comparative advantage yetu na wenginge, tuzalishe kitu gani zaidi hapa ndani ili tuweze kutunufaisha zaidi, tujaribu kutazama kitu ambacho technology yake tunaiweza. Tujaribu kutazama kitu ambacho rasilimali zake zinapatikana hapa kwetu, pia kuangalia masuala mengine kama vile demand, kitu ambacho pengine kinahitajika sana na mambo mengine ya sera za kibiashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala hili la viwanda linahitaji sera. Watu wa viwanda wanasema wanahitaji sera, kwa hiyo, tuwawekee sera ambayo itaweza kuwapelekea wafanyabiashara wetu wa hapa waweze kuzalisha, watakapoweza kuzalisha basi itakuwa ni nafuu kwetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mtu alizungumza kwamba uchaguzi uliofanyika Zanzibar ni uchaguzi haramu. Mimi napata taabu sana kwa kitabu kipi? Wamesema hakuna kitabu kilichozungumza CUF na CCM ama CHADEMA hakuna! Sasa ni kitabu kipi kilichotaja habari za uchagzi huu haramu na huu halali?
Mimi ninavyofahamu uchaguzi uhalali wake na uharamu wake ni kwa Katiba na Sheria. Tuliwafundisha hawa ndugu zetu hapa wakatulia, wakajua kwamba uchaguzi unakwenda kwa Katiba na Sheria, leo unakuja kusema uchaguzi ni haramu! Ni haramu kwa sababu ya kukosa kwako wewe! (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, hayo yote umeyataka mwenyewe, iliyobaki shauri yako. Kwa sababu kama kuna kitu ambacho kimefanyika nje ya utawala bora ni mtu kuwazuia watu haki yao ya kwenda kupiga kura. Hili ndilo kubwa ambalo limefanyika. Sasa mtu aina kama hii atachukuliwa kama nani wakati jambo la vyama vya siasa ni jambo la Muungano, unazungumza wewe kama kiongozi, unawazua watu wasiende kupiga kura, matokeo yake unawakataza na wenzako wasishiriki, unawakataza wasigombee, matokeo yake watu wanalia huko! Hili ndilo ambalo wenzetu liliwasibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mtaka nyingi nasaba hupata mwingi msiba. Sasa huu msiba waache tu waende nao waomboleze, kwa nasaba kubwa walioitaka waache wapate msiba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuzungumzia suala moja ambalo ni muhimu, ulinzi na usalama ni kitu muhimu sana katika nchi yetu. Utakapokuwa unatega mabomu sasa unataka watu wasifuatiliwe? Mabomu yanalipuka nchi nzima usifuatiliwe, usiguswe, wewe ni nani? Mimi ninaomba iwe hivyo hivyo. Mheshimiwa Mawe Matatu nenda nao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia kukutana leo hapa, bila yeye tusingekutana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii adhimu kuweza kuchangia masuala ya Muungano wetu wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia kuna mfano mmoja kule kwetu visiwani huwa tunautumia sana. Mfano huo ni wa ndege kurumbizi. Kurumbizi anapotoka kwenye kichaka chake kile anachokaa husema kichaka hiki kichaka mavi, kichaka hiki kinanuka, lakini ikifika jioni kurumbizi huyo chwii anajiingiza tena mle mle.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wasemaji wa Kambi ya Upinzani tuliwasikia waliyoyasema lakini mengine tena tunaweza tukatumia huu mfano wa kurumbizi kwa sababu naona hawana ajenda zao. Wanasema kwamba huu Muungano umeshindwa, hauwezi kufanya kitu, lakini pamoja na kwamba Muungano umeshindwa suala la Zanzibar wanalileta kwenye Muungano huu. Sasa sijui wanakusudia wasaidiwe nini hapa ikiwa hakuna maana ya kuwepo kitu hiki, mimi sijafahamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna mfano mwingine, nitasomesha sana mwaka huu. Kuna mfano mwingine, kule kwetu ikifika siku za kuandama mwezi ikiwa hujauona basi wewe ukilala unakujia mwezi tu, mwezi tu, mwezi tu. Wao walishindwa kushirika uchaguzi ule kutokana u-dictator wa kiongozi wao, kwa hiyo kila wakikaa hapa uchaguzi, uchaguzi. Mwezi kama hujauona utaendelea kuuota tu na huo uchaguzi mtauota tu mambo yameshakwisha na tayari tumepata Rais. Nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kuchaguliwa tena na Wazanzibar kuendelea kuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vitu vingine hivi ni lazima tuvitazame. Kuna watu inawezekana ikawa mapungufu yao ndiyo wanataka kuja kuyatatulia humu. Jana nilikuwa nikiangalia televisheni kuna mkoa mmoja ulimuita aliyekuwa Mwenyekiti wa chama fulani kwamba arudi mambo yanaharibika. Aliitwa akaambiwa kwamba mambo yanaharibika, kwa hiyo kweli mambo yanaharibika arudi akatengeneze, hakuna viongozi kule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze tu wachangiaji wenzangu ambao wamechangia, wamechangia vizuri. Namshukuru sana kaka yangu, mimi leo nimpe jina la Daktari, Dkt. Shamsi Vuai Nahodha, kwa kuwang‟oa watu jino huku anacheka, unajua ni kazi. Kumng‟oa mtu jino huku anacheka ujue kwamba una falsafa kubwa sana halafu mtu hajijui kama anang‟olewa jino. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba huko Zanzibar kama miafaka ilipita na vyeo watu wakapeana lakini watu shida yao sio vyeo wana lao. Wamepewa watu nafasi, Makamu wa Rais, uchaguzi umepita watu wakafikiri labda watatulizana hawa lakini tumeona wamefanya nini?
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kilichobakia na anachoshauri Mheshimiwa Shamsi kwamba uchumi mkubwa usaidie uchumi mdogo ndio jambo la kulifanya hapa, hayo mengine hamna sera. Kwa hiyo, hayo mimi ndiyo nayozungumza…
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia masuala ya muungano, tunaushukuru sana muungano wetu. Muungano umetusaidia sana katika ulinzi na usalama wa nchi yetu. Labda kwa kuzungumzia historia ndogo katika Muungano, baada ya Mapinduzi ya Zanzibar yalifanyika majaribio mengi sana ya kutaka kupindua nchi. Majaribio yale baada ya kuungana hayakuweza kufanikiwa tena kwa sababu ya Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nitasema sababu za kutaka kufanya majaribio ya mapinduzi hayo, kuna watu hawajaridhika na yale Mapinduzi matukufu ya mwaka 1964 na watu hao bado wapo.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Uwepo wa watu hao ndiyo tatizo wala hakuna tatizo lingine. Kwa hiyo, tunashukuru kwa ulinzi na usalama katika Muungano wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Muungano wetu ni wa watu na jamii, tumechangamana na tunafanya kazi sehemu zote za Muungano. Wafanyabiashara wanakwenda huku na kule kufanya mambo yao ya kibiashara ndani ya Jamhuri ya Muungano. Hakuna mipaka ambayo amewekewa huyu labda ni Mzanzibari huyu ni Mtanganyika kutembea katika Tanzania yetu. Watu wanafaidika na uwekezaji, wanafaidika na kupata mambo ya financing, kuna mabenki yamo ndani ya Muungano yanakopesha kwa mtu yeyote yule ambaye yuko na wengine wamekopa wanajua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la kuipongeza Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni katika ile misaada ya GBS. Siyo hiyo peke yake hata kwenye busket fund na direct project ambayo gawiwo lake linakwenda vizuri, tunaishukuru Serikali. Tunashauri kitu kimoja, katika GBS (General Budget Support) sasa inaanza kupungua na tunawashukuru wafadhili. Kwa hiyo, tujaribu kuangalia mitazamo mengine ya kuweza kusaidiana katika suala hili la GBS.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Kwanza nimpongeze mzungumzaji aliyemaliza kwa shairi lake kilichochema ni chema hakibadili tabia. Tabia ya Maalim Seif ni kushindwa uchaguzi na nashangaa kwa nini mnamwachia aendelee na tabia hiyo hiyo na ataendelea kushindwa tu. Kwa hiyo, kwa kuwa hakibadili tabia siku zote atashindwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichangie katika nyumba zitakazojengwa kwa Jeshi la Polisi kwa Zanzibar. Tuweke proportion ambayo ni nzuri, lakini cha pili mawasiliano ya redio kwa Zanzibar askari wanaongoza kwa simu kule, kwa hiyo, hili nalo pia ni muhimu tulitazame. Kingine masuala ya umeme wanalipa Wakuu wa Vituo wakati mwingine, kwa hiyo na hili liangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumzie jambo moja, amesimama hapa kuna mtu alijiita mchungaji, lakini nikimnukuu ndugu yangu mmoja alisema sijui kanisa hilo hawa wafuasi watakuwa wakoje, mimi sisemi. Anasema kwamba, Wabunge 250 wanashindwa labda kuzijibu hoja, upinzani hauna hoja, hapa hawana hoja, hawana ajenda za kuzungumza sasa hivi wamekuwa ni virukia, kuna miti inaitwa virukia haina mizizi. Ikitajwa Lugumi wanajipaka damu za simba kama wao ndio waliomuua simba, ninyi sio, wako wenyewe waliofanya hiyo kazi, mnajipaka damu halafu mnajisingizia ninyi ndiyo mlioua simba, hamna hoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Toka wauvae ulitima kwa kulamba joka la ufisadi sasa wanadandiadandia, kwa hiyo hawana hoja ya msingi. Lakini Mheshimiwa Lwakatare kule amesema amethibitisha kwamba, wanatangwa maji kwenye kinu na hayabadiliki kwenye kinu hayawezi kupita smoothly kwa sababu ya kuyatwanga kwenu. Watu wanawashuhudia hata mngeletewa hiyo TV katika hoja zenu za kurukiarukia basi pia msingefanya kitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa wale waliokuja na habari za matukio jamani mnasahau? Hamtajwi matokeo ya mabomu nyie? kuwamwagia watu acid, kuwaua ma-padre mbona hamtaji kama huu ni uvunjifu wa amani, mnazungumza hoja gani katika hili? Zungumzeni kitu ambacho kitaleta amani na utulivu katika nchi hii, wadau wa amani na utulivu wanajulikana na wanaochafua wanajulikana mahali popote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe unalalamika kupelekewa askari Zanzibar, unalalamika nini, wewe ndiyo mhalifu kama unalalamika, kwanini unakataa kupelekewa askari kama sio mhalifu. Sasa hili ni lazima liangaliwe, nikija kuchangia katika hoja nyingine amezungumzia Mheshimiwa Waziri katika utekelezaji wa bajeti iliyopita kwamba, wamejaribu kuzuia biashara haramu ya kuuzwa watu, hili jambo bado lipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ndugu zetu wanapelekwa Oman, Dubai, wanapelekwa Bara Arab wanakwenda kutumikishwa bila ya hiari zao, mikataba inaondoka hapa mingine na wakifika kule wanafanyiwa mambo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuunga mkono hoja hii mimi labda hapa nizungumzie kitu kimoja, kuna wenzetu wanajaribu kulipaka matope jeshi letu la polisi, amani na utulivu wa nchi yetu ya Tanzania basi Jeshi la Polisi ndiyo mchango wake mkubwa na waharibifu wa amani hiyo na utulivu ndiyo hawa, nashangaa. Kuna msemo unasema homa mpe paka, maana yake homa mpe paka kwamba wewe kwa kuwa unaumwa ikutoke homa ile kwa kuwa paka haitomdhuru. Sasa hicho sio kitu sahihi wanachokifanya, tunapozungumzia amani na utulivu, majeshi yetu yanakwenda vizuri, kwa hiyo, tunashukuru kwa kutusaidia katika kuweka sawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia hapa jambo lingine ambalo ni muhimu sana, ni usafiri kwa Jeshi la Polisi kwa Mkoa wangu wa Mjini Magharibi Unguja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ALI HASSAN KING: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu definition (maelezo), recognition na money measurement kwa item ambayo imo katika Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, Definition Maelezo (Broad or Narrow definition), naishauri Serikali kuwa maelezo au definition ya item ambayo imo ndani ya mpango wa maendeleo wa Taifa iwe inahusiana na sehemu ya jambo ambalo litatekelezwa kwa kipindi hicho kuliko kueleza mradi wote ambao unatekelezwa kwa muda wa miaka mingi ijayo. Mfano, mradi wa Mchuchuma na Liganga, katika miradi hii imeelezwa kwamba itaanza na kumalizika ndani ya muda huo huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, recognition, napendekeza kuwa item ambayo itaingizwa humu kama ni mpango iwe imetimiza kigezo ambacho hatua za utekelezaji zitakuwa karibu na utekelezaji ikiwemo mikataba na muda wa dhamira ya kutekeleza ndani ya muda uliowekwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, measurement, fedha zitakazotajwa kutekeleza jambo hilo ziwe zimezingatia muda wa utekelezaji shughuli zilizoainishwa kutekelezwa na kadhalika. Kwa mfano, miradi ya Mchuchuma na Liganga imepangwa kutumia kwa jumla ya dola za Kimarekani bilioni mbili nukta tisa ambazo takribani ni shilingi trilioni sita za Kitanzania wakati katika kugharamia mpango sekta binafsi inakadiriwa kuchangia kwa shilingi trilioni saba nukta nne za Kitanzania. Miradi ya Mchuchuma na Liganga ni mfano tu lakini kwa maeneo mengi kama vile uanzishwaji wa kituo cha biashara Kurasini, ujenzi wa reli ya kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, wingi wa fedha za maendeleo na ukuaji wa mapato ya ndani. Fedha za maendeleo kwa mwaka 2015/2016 zilikuwa trilioni nne nukta tatu, fedha za maendeleo kwa mwaka 2016/2017 zilikuwa trilioni 11.820 lakini ongezeko la makusanyo ya ndani yanakuwa kidogo. Tumeongeza fedha za maendeleo ili tuongeze uwezo wa mapato ya ndani ili tupunguze kukopa, lakini mikopo nayo inaongezeka badala ya kupungua.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kuangalia kuwa fedha za maendeleo kwanza zilenge kwenye miradi itakayotoa majibu kwa haraka ili ichangie katika kukuza mapato ya ndani.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na kufika hapa katika Bunge lako hili Tukufu. Pili, nakushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii, lakini cha tatu nikupongeze sana kwa umahiri wako, ujasiri wako wa kukalia Kiti hicho. Kwa sababu hawa wenzetu wao mpaka sasa hivi kitu kinachowatoa humu ndani ni wewe siyo kwa sababu labda umewafanyia kitu kibaya ni kwa sababu umefuata kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mshairi mmoja anasema, mpewa hapokonyeki, aliyepewa akapewa. Wewe ukifanya chuki bure unajisumbua. Mola ndiye atoaye, mambo yote kamiliki. Kwa yule amtakaye ambaye humbariki na yule asiyemtaka basi kupata hatodiriki. Kwa hiyo, hawa wao watasema nje lakini wewe hapo umekaa umetulia kama jina lako lilivyo. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Naibu Spika, cheo ni jaha na jaha anayetoa ni Mungu. Jaha mpaji ni Mungu binadamu hana lake. Sasa wao kwa upande wao wanalia na hii jaha ya cheo na jaha hii ambayo mtu akipewa na Mungu, hata shetani alipopewa Nabii Adam, Mwenyezi Mungu anahadithia kwenye vitabu vya dini, anasema kwamba alivyowaambia malaika wamsujudie Adam, walisujudu isipokuwa ibilisi. Ibilisi yeye alikataa halafu akafanya kiburi. Kwa hiyo, wanachofanya hawa ni kiburi tu. Ibilisi akafukuzwa mbinguni akaambiwa toka, akatoa ahadi kwa Mungu nitakwenda huko ardhini kuwaposha waja wako. Hawapo huku, sasa wako Kahama, Mwanza, kwa ile ahadi yao kwamba watakwenda kuwapotosha Watanzania. Watanzania tunawaomba wawaelewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kumaliza uchaguzi tuliambiwa kwamba siasa zimehamia Bungeni kama wanavyozungumza watu wengine lakini sasa tazama, majimbo yale ya Wapinzani kule meupe, wote hawapo humu ndani. Hii ni sawasawa na hadithi moja ambayo niliwahi kuhadithiwa na wazee wangu kule, hadithi hiyo inazungumzia habari ya fensi ya ndoa. Katika fensi ya ndoa kuna bibi harusi huyo akipanda mumewe kitandani anatoka, akiingia mumewe chumbani katoka, kwa sababu anaogopa hajajiandaa na harusi, kwa hiyo watu wawaelewe. Kwa hiyo na hii iliyokuwa humu ni fensi ya ndoa, unapoingia watu wanaondoka, kwamba bibi harusi anamwogopa bwana harusi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni-conclude maneno kuhusu hawa, tusiwasemeseme sana kwa sababu kuna mshairi mmoja wa kiarabu anasema, Al junun funun alwak khalfan waheed. Wenda wazimu una matawi mengi sana na matawi ya wendawazimu hawa wenzetu wameyadandiadandia tumeyaona. Kwa hiyo, haya yote wanayokuja nayo, wameshakuja nayo mengi na hili moja katika matawi ya wendawazimu ambayo wamedandia. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wenzetu ndiyo hatuwaoni humu Bungeni lakini sisi tutajadili kwa niaba yao. Sasa nije katika kuchangia bajeti yetu hii. Matumizi ya Serikali siku zote huwa yanapangwa kwa fedha. Fedha zinazopangwa badala yake huwa tunatazama yale mambo yaliyotarajiwa kwenda kufanyika lakini mambo yanayotarajiwa kwenda kufanyika tunatarajia yatokezee kwa 100%. Inawezekana fedha zikatumwa 100% lakini kazi isifanyike kwa 100% kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa gap hii tutaijua au itazibwa kutokana na ukaguzi unaofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo, kuna kila umuhimu wa kuwa na taasisi hii ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali. Madhara yake kama itakuwa ukaguzi haukutosheleza ina maana kwamba mwaka unaofuata wa fedha tunaweza tukapeleka fedha tena katika miradi ileile na fedha ile isiweze kufanya kazi vizuri kwa sababu haiangaliwi, kwa hiyo, hili ni jambo muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha zilizotengwa katika ofisi hii ni ndogo na nasema ndogo kwa sababu gani? Fedha zilizotengwa mwaka jana katika hizo OC, sizungumzii mishahara na development, nazungumzia OC za kufanyia kazi zilikuwa ni shilingi milioni 49 lakini mpaka kufikia Machi, 2016 fedha zilizotoka ni shilingi milioni 39, lakini fedha zilizotengwa kwa ajili ya mwaka huu wa fedha ambao tunaujadili hapa ni shilingi milioni 18.5 ya Other Charges. Shilingi milioni 44 humo kuna development na P.E. Kwa hiyo, hizi fedha tuna-justify kwamba ni kidogo kwa sababu ni asilimia 37 ya fedha zilizotoka mpaka Machi. Kwa hiyo, ukija kutazama kwamba zinatarajia kufanya kazi kwa mwaka mzima tutakuja kuona upungufu wa fedha hizi ni kiasi gani. Najua Serikali itakuja na mid year review lakini katika mid year review hili nalo tulione kama ahadi ya Serikali ilivyosema. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna kitu kimoja ambacho ni kizuri. Audit inapofanyika ina stage nyingi, kuna stage ya planning. Katika stage hii ya planning auditor anapanga wapi atafanya audit ile, anapanga resources, anapanga expert’s watakaohitajika wa-audit eneo fulani lakini pia anapanga na time consuming ambayo atatumia. Sasa katika hatua hizi za mwanzo auditor anahitaji kufanya hayo mambo kama resources zitakuwa hazitoshi ina maana kwamba ingekuwa ana-audit private office siyo Ofisi ya Serikali asinge-accept hii engagement kwa sababu resources zisingemtosheleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine muhimu katika kufanya audit, auditor wetu ana heshima kubwa sana Kimataifa. Katika kulinda reputation yake Kimataifa ni lazima auditor wetu afanye kazi vizuri na apelekewe fedha za kutosha ili aweze kufanya kazi kwa umakini na umahiri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia bajeti ya maendeleo ni kubwa, imeongezeka kwa asilimia 100. Kwa hiyo, tunatarajia fedha za maendeleo zikakaguliwe kwani zimeongezeka kwa asilimia 100. Kitu kingine Halmashauri zetu zimeongezeka kutoka 100 na zaidi hadi kufika 181. Ina maana kwamba kuongezeka kwa Halmashauri ni indication kwamba hata fedha za audit zingeweza kuongezeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, isitoshe, tumesema kwamba Serikali imeamua kulipa madeni, lakini kabla ya kulipa madeni hayo inayakagua ili kupitisha kwamba deni gani linafaa kulipwa. Kwa hiyo, madeni haya ya Serikali yanayokaguliwa pia nayo yataongeza kazi ya auditor kwa hiyo ilipaswa fedha za auditing ziwe nyingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali imeamua kufuta retention, makampuni ambayo yatafutiwa retention yatakuwa hayako radhi, hayataweza ku-submit kila kitu kikawa kiko safi. Kwa hiyo, Serikali ilipaswa iangalie suala hili ili Auditor General aweze kufanya mambo hayo ya ukaguzi. Pia taasisi kama Mahakama ya Kuzuia Ufisadi, TAKUKURU, Bunge tunategemea taarifa za CAG ili tuweze kufanya kazi. Kwa hiyo, hivi vyombo vinaweza vikakosa taarifa ya thamani katika kufanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kingine nije katika deni la Taifa. Wengi wamezungumzia deni la Taifa lakini deni la Taifa ni himilivu tunakubali lakini tunasema hivi, tukope tufanye zile kazi tulizoziainisha na tumalize kazi zile tulizokopea. Kama hatukumaliza, project zikiganda katikati interest rate inalipwa ina maana kwamba tunalipa fedha zetu au tumelipa fedha zimeganda, wananchi wanalipa interest na miradi inakuwa haijakamilika. Kwa hiyo, naomba suala hili tuweze kuliangalia vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo lingine ambalo naweza kuchangia ni eneo la Bodi ya Taifa ya Ukaguzi ambayo ilitajwa katika Mpango. Bodi hii ya Taifa ya Ukaguzi tukifuata nchi za wenzetu huwa wanazitumia Bodi zao za Wahasibu na Auditors ili kuweza kutoa hata mitaala ya sheria za kodi ambazo zimetoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu ambae ametupa uhai na akatufanya sisi leo kuwa miongoni mwa Wabunge ambao tutachangia maslahi ya nchi hii katika mipango ya kuendesha nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Ni nafasi adhimu ya kuweza kuchangia Mpango wa Maendeleo au Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nizungumze kitu kimoja kidogo ambacho wasemaji wengi sana walikuwa wanakigusagusa ambalo linahusiana na masuala ya bandari.
Kwanza nakwenda huko moja kwa moja masuala ya bandari, ni kweli tumeona kwamba mzigo katika bandari umepungua lakini tunaposhauri tujaribu kuangalia katika maeneo ambayo mzigo maeneo gani yamepungua. Ukitizama katika hizi transit goods ambazo zinakwenda katika nchi jirani basi utagundua kwamba nchi ya Zambia na DRC Congo ndipo mzigo ulikopungua, lakini ukiangalia Uganda na Malawi mzigo haujapungua. Sababu zimeleezwa na wengi pengine labda VAT na pengine labda hiyo single custom territory ambayo imechangia kwa kiasi kikubwa kufanya mizigo katika bandari ipungue.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hili nilikuwa naomba Serikali ijaribu kuangalia hivyo vitu ambavyo vimetajwa hapo kwamba ni sababu na tujielekeze na tubaini kwamba hiyo kweli ni sababu; kwa sababu kuna baadhi ya mambo yalianza kabla ya hapo. Tukija katika hiyo single custom territory kwamba ilikuwa iko toka mwaka 2013 ikaanza kuwa implemented Disemba, 2014 sasa tutizame kitu gani kilichotuathiri. Na ukija kutazama katika mizigo mingine hususani ya mafuta mpaka katika nchi za Rwanda na Burundi kwa mujibu wa takwimu ambazo zimo katika kitabu cha bandari kwamba nayo pia ilipungua. Lakini ukiangalia katika nchi nyingine zimeongezeka sasa hili nilikuwa naomba tutafute sababu hasa ili tunapotibu basi tujue tunatibu kitu gani ambacho mahususi moja kwa moja kitakuwa kinatusaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ninataka kulizungumzia amelizungumzia Mheshimiwa Kingu pale kwamba kuhusiana na fedha ambazo zimo katika uchumi wetu. Tunafahamu Serikali imepanga kukopa ndani, lakini moja katika changamoto ambayo Serikali yenyewe ilieleza kwamba kutoshiriki kwa sekta binafsi katika uchumi imefanya kwamba uchumi kutokukua vizuri au mambo kutokwenda sawa.
Sasa tunapoamua kukopa ndani vilevile tutasababisha hali hiyo hiyo ya kwamba fedha zitakuwa hazipatikani kwa wananchi na baadaye hawa watu binafsi hawataweza kukopa, kwa hiyo na sekta binafsi nayo itarudi katika changamoto yake ile ile ya kwamba itaanguka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naishauri Serikali iharakishe suala la kupata ile dhamana ya Kimataifa kukopa kuweza kufanya sovereign rating kwa haraka ili tuweze kupata mikopo ya nje. Lakini pia si vibaya kwakuwa soko letu la hisa la Dar es Salaam Stock Exchange linakubali kualika foreign investors ambao labda Serikali nayo ijielekeze katika kukopa kwa foreign investors ingawaje changamoto zake zinajulikana kwamba ufanisi katika soko lile pamoja na vitendea kazi siyo vizuri kwa muda huu, lakini tutakapotumia njia hiyo, kwa hiyo, tutaweza kupunguza kukopa ndani na baadaye tutajielekeza katika masuala mengine ambayo ya mikopo mizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ni muhimu sana ambalo wengi walilizungumzia, Serikali ingeweka utaratibu uliowazi kufahamu shughuli zinazofanyika. Wengi wanaozungumza hapa wanalalamikia utaratibu wa Serikali kutofikisha fedha katika masuala ya dawa, katika Halmashauri na sehemu nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa mujibu wa report ya BOT ambayo wameleeza kwamba katika mwezi wa Agost, Serikali ililipa zaidi ya shilingi bilioni 900 ili kulipia Deni la Taifa. Katika mwezi wa nyuma yake Serikali iliipa hizo report zimo katika mawasilisho ambayo yalifanywa na Gavana wa Benki Kuu tarehe 25 Agosti. Kwa hiyo, hii ndiyo imepelekea kwamba Serikali kutopata fedha za kutosha katika kuhudumia masuala mengine sasa hapa ikafikia kipindi ambacho watu wakaanza kuisema Serikali vibaya na hapa na mimi ninaomba kidogo niongee neno moja ingawa kwamba kwa wengine itakuwa siyo zuri lakini neno lenyewe ni muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu ambaye yupo hai akatafuta kurehemewa na maiti. Narudia tena, mtu ambaye yupo hai hawezi kutafuta rehema kwa aliyefariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu hapa alizungumza kwamba hii Serikali imefilisika lakini akasahau Serikali hii ndiyo iliyompa yeye majengo bila kulipa akawa anafanya biashara. Sasa kama mfu ndiyo wewe unamtegemea akurehemu, sasa wewe mwenyewe ni mfu zaidi ikiwa aliyekufadhili amefilisika ina maana kwamba wewe uliyefadhiliwa umefilisika zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna msemo wa kiswahili ambao una lafudhi ya Kiarabu ambao unasema wafadhilaka wasajidaka, man-fadhilaka wasajidaka, aliyekufadhili ni bwana wako na sio pundaka; sio punda wako. Kwa hiyo, Serikali bado atabakia bwana wake huyo ambaye amefadhiliwa na Serikali hii, kwa hiyo, Serikali haijafilisika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ni muhimu nazungumza masuala ya retention ambayo pia yameshazungumzwa. Nakumbuka moja ya hoja ambayo Serikali ikaamua kufuta retention kwa taasisi zile ambazo zimefutiwa retention kwa sababu Serikali ilikuwa ikikopa pesa zake wenyewe. Zile taasisi zilikuwa zikiweka pesa benki baadaye Serikali inapopeleka dhamana zake kuuza katika masoko ya hisa, mabenki haya yananunua ambayo ni fedha za taasisi za hii Serikali, kwa hiyo ikaamua kuzitoa kuziweka huku. Sasa ufanyike utaratibu ambao uko mzuri na muafaka ili iweze kupatikana urahisi zaidi kwa fedha hizi kuingia katika mzunguko au Serikali yenyewe kama iliona taabu kukopeshwa na mabenki katika retention ambayo ziko BOT sasa je, Serikali ina mpango gani kuzitumia hizi? Labda pengine nazo zinaweza zikasaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na suala moja ambalo ni muhimu sana ni lazima tuangalie balance ya monetary policy na fiscal policy tunajua Wizara ya Fedha inashughulikia masuala ya fiscal policy, lakini Benki Kuu inashughulikia monetary policy.
Kwa hiyo, vitu hivi viwili ni lazima viwe balanced ili mambo yaweze kwenda sawa na tuweze kuepukana na mambo ambayo hayaendi vizuri. Kuna watu walisifu hapa kwamba Serikali iliyopita ya Mheshimiwa Mwinyi ilikuwa nzuri, ya Mheshimiwa Mkapa ilikuwa nzuri, ya Mheshimiwa Jakaya ilikuwa nzuri na hii pia ninaamini wataisifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mshairi mmoja anasema mpende bado yuko hai, pendo lako alipokee, ukimpenda yuko kaburini umelitupa pendo lako hewani, hayo mapenzi yenu mliyoyataja hapa mmeyatupa hewani lakini tunaamini kwamba na huyu mtampenda. (Makofi)
Sasa jambo lingine ambalo ni muhimu na kama tutalifanyia kazi itakuwa vizuri. Mheshimiwa Khatib pale alizungumza jana kitu kizuri kidogo hata kile kitu nimekipenda. Anasema kwamba alikiombea dua chama chake na akasema kwamba kuna watu wanakiombea kife, hawakiombei kife, mfano wa mtu ambaye ananyeshewa na mvua, tuseme unanyeshewa na mvua baadaye akatokezea mtu akakwambia njoo ujifiche kwenye jeneza unakufa, unajiua? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo,niongee masuala mawili ambayo muhimu. Katika…
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Awali nitangulize shukrani zangu kwa Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uhai na aliyetufanya tukaja leo hapa katika mazingira ambayo tuko salama.

Mheshimiwa Spika, pili, tutoe pole kwa familia ambazo zimepata msiba kutokana na tukio ambalo limetokea ingawa inajirejea, lakini kipekee nahisi sitaitendea haki nchi yangu bila kutoa pole kwa janga ambalo limetokea.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia suala hili, kwanza nianze na chombo muhimu sana ambacho ni TBC. TBC ukiangalia katika dira yake, kwa mujibu wa kitabu ambacho kimetolewa na Mheshimiwa Waziri hapa, ni kwamba kuwa na Taifa linalohabarishwa vizuri na katika dhima wakaandika kwamba upatikanaji stahiki wa habari; halafu tukija katika slogan yao wanasema, “Ukweli na Uhakika.”

Mheshimiwa Spika, sasa kutokana na dhima hii na dira ambayo imeelezwa ya TBC, moja kwa moja ni kwamba TBC inataka kutuhabarisha Watanzania habari za ukweli na uhakika na ndivyo walivyoji-position. Hapo hapo, habari hizo za ukweli na uhakika bila ya kuwa na miundombinu mizuri, bila hawa TBC kuwezeshwa hatutaweza kupata habari za ukweli na uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukisema habari za ukweli na uhakika, wakati mwingine inawezekana kikatangulia chombo kikatoa habari ambazo siyo za ukweli na siyo za uhakika. Sasa TBC baadaye ndiyo ije ikanushe. Sasa inaweza ikachelewa kutoa habari kutokana na miundombinu ambayo wanayo au mazingira ya kazi ambayo yapo. Sasa ili tuihabarishe vyema jamii yetu, basi hapa tunahitaji tuwekeze katika TBC. Tutakapowekeza katika TBC ina maana tunawekeza katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata Serikali inafanya mambo mengi sana ambayo chombo cha kitaifa kipo cha TBC, kwa hiyo, kinao uwezo wa kuitangaza Serikali kupitia mambo yote ambayo wanayafanya. Kwa hiyo, tunaomba kwa Mheshimiwa Waziri kwamba tuangalie zaidi katika hii televison yetu au chombo hiki ili tuwekeze mtaji wa kutosha ambao naamini utatulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu sana, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Wizara hii ya Habari kwa kuifanya Zanzibar sasa ni mwanachama katika Shirikisho la Soka Afrika. Najua hizi jitihada zilifanywa na TFF. Kwa hiyo, napongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina pongezi nyingine lakini pamoja na ombi, tunajua kuna mchakato pengine kwamba Zanzibar pia iweze kutambuliwa na FIFA. Kwa hiyo, nalo hilo pia tunapongeza kama mchakato huo utakuwa unaendelea, utakuwa unakwenda kwa haraka zaidi. Kwa hiyo, hapo nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kufanya kazi hiyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nakumbuka hapa tumepisha sheria ambayo inahusiana na vyombo vya habari na wanahabari, ukatengwa mfuko wa taaluma kwa ajili ya waandishi wa habari. Kwa hiyo hili Mheshimiwa Waziri lisimamiwe vizuri, kwa sababu lengo la sheria ile moja ni kuwawezesha wanahabari. Kwa hiyo, tutenge fedha za kutosha na tulisimamie ili tuweze kuwa na wanahabari wazuri na waweze kutoa habari zao kwa uhakika.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nije katika soka ambalo linazungumzwa; nazungumzia kuhusiana na habari za academy. Tunajua Wizara ndiyo mlezi wa michezo. Basi Wizara iweke sheria, utaratibu na vivutio ambavyo vitawawesha watu kuweka hizi academy, kwa sababu siyo rahisi academy zote zikawekwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, yakiwekwa mazingira na vivutio, inaweza ikachangia kabisa kuwa na wanamichezo wazuri, siyo kwa soka peke yake katika academy, tunaweza tukawa na academy za mambo mengi kama kuogelea na mambo mengine kadha wa kadha.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ni muhimu, nilisikitika sana hapa kumsikia mtu mmoja anauliza katika kuchangia hotuba hii kwamba Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi yuko wapi, labda anaweza akawa ametekwa. Kwa taarifa tu, kwenda kwa Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi hakuingizi kwenye chama. Katibu Mkuu siyo kazi yake kumwingiza au kupokea mwanachama. Katibu Mkuu kazi yake ni kuongoza chama. Kwa hiyo, nami namshauri Mheshimiwa Lema, kama anataka kuja CCM, apite katika shina lake kule Arusha, apite katika ngazi ya Tawi, atapatiwa kadi na atajiunga na chama chetu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tunajua kwenda kumtembelea Katibu Mkuu siyo kuingia katika chama. Kwa hiyo, uje ufauate taratibu hizi za chama na miongozo ambayo ipo. Kwa nini umshike Katibu Mkuu wetu? Ninyi mmechagua Katibu Mkuu siyo zamani sana, lakini hajulikani. Hilo ndiyo tatizo, kwamba hatambuliwi. Sasa unaanza kuingia kwa Katibu Wakuu wa wenzako. Pilipili iko shamba, inakuwashia nini? Eeh, pilipili iko shamba inakuwashia nini au ndiyo kiherehere? (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili walifahamu vizuri kwamba siyo jambo la kusema unazungumza hivyo.

Mheshimiwa Spika, lingine, nizungumze jambo ambalo limewahi kuzungumzwa na watu wengine katika sanaa. Tumeweka sanaa katika mazingira ambayo wasanii wanaweza wakajiajiri na wasanii wanaweza wakajiajiri kupitia njia mbili; wanapoweza kufanya sanaa zao wakazi- record, lakini pia huwa wanafanya maonesho ya live; tuchukulie mfano kama michezo hii ya kuigiza au muziki. Sasa kumetokea sintofahamu, kitu ambacho hakijulikani kimetokea vipi?

Mheshimiwa Spika, wasanii wameshajiandaa kufanya show, tayari wanavamiwa. Sasa ile ajira ambayo tunasema kwamba itatokana na sanaa, au itapatikana kutokana na sanaa, inakufa. Unapokwenda katika kumbi zile katika michezo hii au katika kumbi za sanaa unaweza ukakuta askari wanavamia. Sasa hili siyo jambo zuri, kwa sababu tunawavunja moyo, kwa sababu wao wanapata mapato yao kwa mujibu wa kuuza kazi zao na kufanya maonesho ya live ambayo watu wanaingia kwa vingiilio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri kwa ushirikiano, kwa sababu inawezakana ikawa Wizara yake imeruhusu, lakini pengine inawezekana kuna muingiliano. Kuna baadhi ya Mikoa mingine wasanii hawana raha; wanaingia kwenye show wanabebwa pamoja na watazamaji. Kwa hiyo, hili naomba lingeangaliwa likafanyiwa utaratibu mzuri ili waweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, lingine katika timu yetu hii ya Serengeti Boys, ni kweli timu yetu inafika mbali, lakini tunahitaji kuwekeza katika soka. Tusiwe na Serengeti Boys hii ambayo kwa mwaka huu imeonesha mfano; na tuliwahi kuwa na timu kama hiyo miaka ya nyuma ya akina Ngasa na wenzake waliokuwa katika timu ile ya Serengeti Boys iliyopita. Inapita miaka mitano halafu ndiyo inakuja kuibuka Serengeti Boys nyingine ambayo inaweza ikatupa matumaini Watanzania. Hili jambo tunaomba liwe endelevu.

Mheshimiwa Spika, kama tunakumbuka katika soka, wachezaji wengi sasa hivi ambao wanamalizia umri wao kucheza, walitoka kwenye Serengeti Boys, lakini toka timu ile ilipokuwa ikifanya vizuri, basi mpaka leo imekuja hii nyingine ndiyo inatufuta machozi.Kwa hiyo, tunakaa sana, miaka 10, 15, ndiyo inatokezea timu nyingine ya vijana, inaundwa inakuwa inafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri, tuliangalie hili, timu zetu hizi ziwe endelevu. Tulishashika usukani katika kuingia mashindano ya Afrika, basi tuwe tunaonekana pale mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tujaribu kufanya kitu kama hicho kingine katika riadha, isiwe mwaka huu, tumeshinda kwenye riadha au tumepata nafasi ya tano kwenye riadha katika mwaka huu, wengine wameshinda China kule, wengine wameshinda India. Sasa isije ikaja ikapotea hii, hizi nguvu ambazo tumezitoa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza naungana na wote waliotoa rambirambi na naungana na wote waliopongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze haraka mambo matatu, katika kifungu ambacho kinahusiana na umeme, mafuta na redio Zanzibar ni tatizo. Fedha zilizotengwa hazitoshi katika Mkoa wa Mjini Magharibi. Mkoa wa Mjini Magharibi una Wilaya tatu na una jumla ya vituo 14, Askari wanachangishana wenyewe katika vituo hivi. Kwa hiyo, hapa namwomba Mheshimiwa Waziri aangalie vizuri.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi ya maendeleo, niliahidiwa ukarabati wa nyumba za Polisi, ukarabati wa Makao Makuu ya Polisi na niliahidiwa uzio pamoja na nyumba mpya za Polisi lakini bado hayajafanyika. Hapa kuna kituo kimoja cha Mkokotoni hicho ambacho kimetajwa.Kwa hiyo, hiyo naomba katika miradi ya maendeleo waje watuangalie vizuri.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo hapa lilizungumzwa naona kwamba bora na mimi nigusie, haiwezekani ugomvi wa nyumbani kwako ukaenda ukamtumpia jirani yako. Wewe umeachia ushuzi katika nyumba yako, harufu ya ushuzi ule unamsingizia jirani, jitazameni ninyi wenyewe, CCM haishiriki katika mgogoro waCUF na ndiyo maana tunasema la kuvunda halina ubani. Hiyo nisakaratul maut, mtu anapokuwa katika sakaratul maut anakuwa mara nyingi hajitambui, kwa hiyo, hiyo mtambue ni sakaratul maut hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni muhimu mlijue kilichowaponza ni tamaa zenu wenyewe.

Mlihisi mnakuja kupokea mapesa kumbe ndiyo mmekwenda kukiua Chama. Kwa hiyo, ni ninyi wenyewe, mgogoro wenu wenyewe kwa tamaa zenu wenyewe, msisingizie Chama cha Mapinduzi hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu jambo lingine ambalo ni muhimu mzingatie kwamba hayo mambo mliaza ninyi wenyewe ukaribishaji, utoaji, kumuingiza huyu kwenye Chama, kumtoa huyu mlifanya wenyewe, CCM imehusika wapi? Mjiangalie vizuri.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika hoja moja ambayo alizungumza hapa mtu haki za binadamu katika Magereza. Haki za binadamu katika Magereza ni lazima ziangaliwe pamoja na usalama ndani ya Magereza. Ndiyo maana hapa ikasemwa kwamba watu wanapekuliwa mabanda ya uwani, mabanda ya uwani lazima watu watapekuliwa, anaweza mtu akaingia na shazia ikahatarisha usalama, akaingia na msumari, anaweza mtu akaingia na silaha yoyote. Kwa hiyo, nimpe pole au kama nimpe hongera Mheshimiwa Lema kama na yeye yalimkuta haya ya kupekuliwa mabanda ya uwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ubaya wenyewe unaweza ukaja ukamkuta mwanaume mwenzako anakuvalia gloves halafu anaanza kusema mashallah, lazima utakuja kusema hivyo hapa...(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili nalizungumza maksudi ili watu waache kuota ndoto za kipuuzi na kutangaza hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, Msajili wa Hazina Fungu Na. 7, kuziongezea uwezo taasisi zilizo chini ya Msajili wa Hazina kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, NARCO, taasisi hii ingeongezewa uwezo wa kuwa na ranchi nyingi katika maeneo ambayo yana mifugo mingi. Pia taasisi iweze kutoa taaluma kwa wafugaji wa wanyama wa asili ili mifugo yao iwe na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Tanzania ni ya pili/ tatu kwa mifugo Barani Afrika lakini pia ni nchi yenye migogoro ya wakulima na wafugaji, hivyo basi tutumie changamoto na uimara huu kupitia ranchi zilizo chini ya NARCO kuweka hali sawa. Pia taasisi hii ingepewa uwezo zaidi wa kuzalisha mitambo ya maziwa

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANAPA; Tanzania ni ya pili duniani kwa kuwa na vivutio vya utalii baada ya Brazil. Hivyo, taasisi hii iwezeshwe zaidi katika mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, iongezewe uwezo wa kujenga miundombinu ili vivutio hivyo viwe vinafikika na watalii wa ndani na nje pia kujenga uwezo wa kuweza kuvitangaza vivutio hivyo ili kupata watalii wengi kwani uchumi tunao lakini tunaukalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, COSTECH; (Taasisi ya Utafiti) kwa uchumi wa viwanda, tuwekeze zaidi katika kufanya utafiti hasa kwa kuwatia moyo wabunifu. Income from Investment pia Serikali iwekeze zaidi katika mashirika yanayofanya vizuri ili tuweze kupata pato kutoka kwenye uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Takwimu; Tunakwenda katika uchumi wa viwanda, lakini mpaka sasa kuna upotoshwaji wa takwimu kama vile sukari inayohitajika kwa matumizi ya ndani ya nchi, hivyo imepelekea kupata upungufu wa sukari na bei ikapanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuhusiana na uamuzi wa kuzidisha mwaka 2016/2017 asilimia 10 kwenye mafuta ghafi hatimaye bei imepanda na tunatumia mafuta hayo kutoka nchi jirani kwa magendo kutokana na kukosa takwimu sahihi. Ofisi ya Takwimu ipo wapi? Kwa nini hatuna takwimu sahihi? Kwa nini tunatumia takwimu za wafanyabiashara badala ya kutumia takwimu toka Ofisi ya Takwimu tukaacha kupotoshwa? Izingatiwe kwamba wafanyabiashara hawa wapo makundi mawili kila kundi linataka kuangusha mwenzake.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza mimi ilikua nianze kwa neno moja ambalo ni maarufu sana ambalo hizi hoja zote zinazozungumzwa zinaingia katika al-jununu fununu (uendawazimu una matawi mengi sana), lakini akili fani yake moja tu; leo wako wengine wanaotaka kupongeza huko, wako wengine hawataki, wako wengine wanasema wasishurutishwe, wako wengine wanatakiwa wasilaumiwe sasa mko wapi wenzetu? Hizo ni fani za wendawazimu zote, lakini CCM ni fani moja tu, sisi tunapongeza kwa Rais kitendo alichokifanya, kwa hiyo, ninyi msipopongeza ni kazi kwenu kwasababu al-jununu fununu (wendawazimu una matawi mengi) kwahiyo gawaneni hayo matawi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo watakaodandia la kupongeza, watakaodandia la kusema kwamba lawama, endeleeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine msiseme uongo, mnasema mnafanya research ninyi? Mnasema kwamba bajeti inatakelezwa kwa asilimia 38, ni bajeti ipi? unaijua bajeti? Kuna bajeti ya maendeleo, kuna bajeti yenyewe kuu mnazungumza nini? mnasema mmefanya research hao waliowafanyieni research ni wakaotaji kuni wa usiku wamewafungieni na nyoka humo humo. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawajui, hakuna jambo la maana ambalo wameeleza. Tazama bajeti pesa zilizotoka, halafu ukaangalie maendeleo...

T A A R I F A .....

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri hafahamu kidogo al jununu maana yake ni uwendawazimu una matawi mengi, kwa hiyo wewe tena utajijua kama upo kama tawi la uwandawazimu utakuwa mwendawazimu. Sasa tunasema hivyo ndivyo bajeti inavyotekelezwa.

Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante nilindie muda wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kimezungumzwa kitu ambacho hakihusiani kabisa, kumezungumziwa uchaguzi wa Zanzibar. Sawa, tarehe 25 Oktoba, kulikuwa na NEC kuna ZEC hata kuku wanataga mayai na mayai mengine yakawa viza. Kwa hiyo, uchaguzi ule kwa Wanzanzibar kule ZEC ulikuwa ni viza, na kitu viza huwa si riziki. Naogopa kusema kwamba na aliochaguliwa labda ilikuwa si riziki maana hakupata. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nizungumzie jambo moja kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kuhusu takwimu za viwanda. Tunaelekea katika nchi ya viwanda lakini bado tunategemea takwimu kutoka katika taasisi binafsi. Takwimu kutoka katika taasisi binafsi haziwezi kutusaidia kwa sababu kila mmoja ana takwimu zake. Tunacho kitengo chetu cha takwimu za Serikali, kwa nini tusitumie katika kufikia katika Fiscal Policy zetu? Tutumie kitengo hicho cha Serikali, namshauri Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na lingine kwa Zanzibar kuna VAT ambayo ilianzishwa mwaka jana ya Section 55(a) ambayo bidhaa za kutoka Bara kwenda Zanzibar na zinazozalishwa Zanzibar kuja Bara zilikuwa zimewekewa zero rated. Lakini zero rated hiyo wako watu ambayo ni registered VAT na wengine hawakuwa registered, hawa ambao hawako registered hawatambuliwi, kwa hiyo, wanalipishwa VAT mbili analipishwa na TRA analipishwa pia na ZRB. Kwa hiyo hapa tuangalie, tusiweke double standard tukiweka double standard tutumie destination principles kwa wote, tuwatambue kwa vitambulisho ambavyo wanavyo ili tuwasaidie wafanyabiashara hawa wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nizungumzie utalii. Ili kuweza kukuza mapato yetu na Pato la Taifa liweze kukua, tuna vivutio vikubwa vya utalii katika Tanzania. Tanzania kwenye dunia ni nchi ya pili kwa kuwa na vivutio vizuri baada ya Brazil. Kwa hiyo, tukitumia vivutio hivi vya utalii tunaweza tukaja tukafikia mahali pazuri ili Tanzania yetu nayo iweze kung’ara na tuweze kupata mapato mazuri katika nchi yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mzungumzaji wa Kambi ya Upinzani katika introduction yake alitaja msemo mmoja ambao aliuzungumza Baba Nelson Mandela. Nelson Mandela amesema no easy walk to freedom kwamba hakuna easy walk katika kuuendea uhuru, lakini wenzetu wanataka uhuru upi? Wale waliofanya hivyo anawatetea ni watovu wa adabu ambao Bunge hili liliwapa adhabu. Sasa wao wanawatetea Waheshimiwa watatu ambao walipewa adhabu hapa kutokana na utovu wa adabu. Kwa hiyo wanawasema hapa kwamba no easy walk to freedom kwamba je wanataka uhuru wa kutukana humu ndani? Wanataka uhuru wa kutovuka adabu humu ndani? Wanataka uhuru wa kutokusikiliza kitu humu ndani? Kwa hiyo, hicho sio kitu kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunazungumzia katika upande huo huo, kuna watu walisema kwamba bajeti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia siku ya leo kuwa hai hapa na tukafika katika Bunge lako Tukufu na kuweza kujadili bajeti hii ya Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nakushukuru wewe kuweza kunipa nafasi hii kuweza kujadili lakini kwanza kabla sijaanza kuchangia kitu ambacho nataka kukisema nina mambo kama nane, jambo moja tu ambalo ni muhimu sana kuzingatia.

Katika kitabu hiki cha rangi ya waridi ambacho walizungumza Kambi ya Upinzani wakasema kwamba wanawashukuru waliofanya utafiti mpaka wakaandika kitabu hiki, lakini hiki kitabu kimeandika Bajeti Kuu, hakijaandika bajeti ya Wizara ya Fedha. Sasa pamoja na reseach hiyo halafu bado watu wako nje ya beat, watu wanaimba nje ya key, sasa sijui haya mambo yataendaje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili linakuja kwa sababu ukiajiandaa sana kukosoa basi mwisho unakosolewa wewe, kwa hiyo ndilo nilitaka nitoe taarifa tu kwamba hiki kitabu kiko nje ya beat tena kiko nje ta key kinazungumzia Bajeti Kuu, ikifika siku hiyo ya Bajeti Kuu sijui kutaelezwa nini, ukikitafuta utakiona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ninalotaka kuchangia la mwanzo, nataka kuchangia katika Fungu Namba 10 la Wizara ya Fedha. Fungu Namba 10 ni Tume ya Fedha ya Pamoja. Katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 40 na ukurasa wa 41 amezungumzia Tume ya Pamoja ya Fedha. Katika Tume hiyo ya Pamoja ya Fedha amesema kwamba imefanya mapitio ya study tofauti za masuala ya kodi. Sasa na mimi nizungumze masuala hayo ya kodi ambayo labda mengine kwa kuwa mambo haya yanapita huko na haya yapite huko. Jambo lenyewe ni hili kama lifuatalo:-

Mheshimiwa Mwneyekiti, tunajua tumepitisha Petroleum Act pia tumepitisha Oil and Gas Revenue Management Act, 2015 ambavyo vimelenga kuifanya kwamba Zanzibar kuwa inashughulika na mafuta na gesi ambayo wanachimba kule na Tanzania Bara watashughulika kwa upande wao, lakini kitu kimoja ambacho ninataka kikaangaliwe katika Tume hii ya Pamoja ya Fedha ni kwamba bado Sheria za Kodi ni za Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yangu ni kwamba pato kubwa linalotokana na mafuta na gesi huwa linatokana na kodi, sasa hizi kodi bado ni za Muungano kwa kuwa hizi kodi bado ni za Muungano, Tume hii nayo basi ikakae na ikatazame kwa sababu watu wanazungumza wataalam zaidi ya asilimia 90 ya mapato ya mafuta na gesi ni kodi lakini kama zikiwa hazikuelezwa kodi hizo kama hazitokuwa za Muungano ina maana kwamba bado patakuwa pana utata. Sasa zikaelezwe hizo kodi ambazo zitatokana na mafura na gesi nazo pia ziwe tofauti na Sheria za Kodi ambazo ni Sheria za Muungano, hilo ni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Tume hii ipo kwa maslahi ya kuangalia study na kuangalia masuala ya kodi na kufanya mapitio kama ilivyoelezwa na Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 41 basi pia tukaangalie Tanzania Bara na Zanzibar ni sehemu ambazo hazijapakana kwa mipaka mikubwa, masafa ni madogo sana. Katika masuala ya bidhaa ambazo zinakwenda Zanzibar kuwekewa zero ratekwa masafa madogo inakuwa haiko vizuri ni bora tukatumia ile compensation arrangement kuliko tukatumia zero based arrangement.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama suala hili litakwenda litaafikiwa na litazungumzwa vizuri kwa sababu masafa yetu madogo, zero based mara nyingi watu wanatumia kwa masafa marefu na zero based ina gharama kubwa ina maana kwamba lazima uanze kuweka mambo ya administration katika customs zote, uanze kufanya masuala hayo, jingine ni magendo yanaweza yakaimarika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili nashauri katika Tume ya Pamoja ya Fedha ijaribu kuangalia hili kwa sababu mara nyingi inakwenda hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Fungu 21 - Hazina; Wabunge wengi sana walisema kwamba fedha hawajaziona lakini ukienda katika Kitabu cha Maendeleo cha bajeti, Fungu 21- Hazina iko pale village empowerment na imewekewa fedha zake shilingi bilioni 60. Tukitazama katika vitabu hivyo tutaona. Sasa mimi nazungumzia katika kitu kimoja. Mwaka huu tumesema kwamba tutafanya pilot study lakini miezi tayari inataradadi nafikiri bado nafikiri bado tutakuwa hatujafanya pilot study.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sisi wengine wenye Majimbo na ambao tumechangamka haraka baada ya kusikia fursa hii kwa wananchi, tulijaribu kwenda kuhamasisha, tulisajili vikundi, tulitoa elimu kwa vikundi tayari tulikwishajipanga. Jang’ombe tayari tulishajipanga. Kama hiyo pilot study inataka kufanyika ghafla basi tuleteeni Jang’ombe kwa sababu tumeshatoa elimu na vikundi viko imara na vikundi vimehamasika na vinafanya kazi yake vizuri, kwa hiyo tutakapokwenda tukafanye hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze jambo moja, hili jambo tulisema kwamba kwapilot study ndiyo shilingi bilioni
59.5 lakini iweje na mwaka unaofuata iwe bilioni 60? Na wakati vijiji vinajulikana au mitaa inajulikana idadi yake kwa fedha hizi ambazo tumezitenga kwa mwaka wa pili ni kidogo na fedha hizi mwaka wa mwanzo hazikutoka hatujui kama tumelishwa samaki wa kuchora au vipi! Kwa sabbau bado hazijatoka. Sasa Je, na hizi za mwaka wa pili zitatoka sambamba? Kwa hiyo, hapo namwomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuja kuangalia suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Fungu la Deni la Taifa, tunakubali Serikali ikope, nchi maskini ili iweze kuendelea ikope na tumefurahi kuona kwamba katika Deni la Taifa tunalipa, tunaishukuru na tunaipongeza sana Serikali yetu. Miradi ambayo inayofanyika tukikopa leo wanakuja kulipa wa kesho na kesho kutwa. Watakuja kulipa watu kwa miaka 20 au 25 mbele ambao hawajatumia, sasa miradi ambayo itakuwa inafanyika kwa kukopa fedha hizi basi at least iwe ina record nzuri, iwe inajulikana katika kila hatua kwa maana gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana umekopa umsomeshe mtu mpaka Chuo Kikuu, lakini kumbe yule mtu akamalizia primary lakini mkopo uliochukua ni wa Chuo Kikuu. Sasa tupate faida ile ya kusoma mtu Chuo Kikuu na huo mradi tunaosema ukubwa wake uwe vilevile ambavyo ulitarajiwa na usije ukawa ni mradi ambao ni mfupi ambao faida yake ni ndogo. Tutakuja kuwalipisha watu deni kubwa kuliko faida ya mradi ambao upo kwa sababu deni tutalipa mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu Msajili wa Hazina Fungu Namba 7. Katika Fungu Namba 7 siku zote Serikali inahangaika kutafuta mapato lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru sana. Naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dokta John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua anazochukua kukabiliana na Upotevu wa Mapato ya Serikali katika Sekta ya Madini
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata fursa hii. Kwa kuwa Azimio limejikita katika kumpongeza Mheshimiwa Rais kutokana na tukio ambalo limetokea na sote tunampongeza kama ilivyofanya hotuba ya Mwenyekiti hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, CCM miaka yote tokea mwaka 1992 ni chama kipevu sana tokea huko nyuma kwa hiyo kilijiwekea miongozo ya kwamba kujikosoa leo kuliko jana na CCM imepanga lazima rasilimali za nchi ziwafaidishe wananchi. Katika kufikia lengo hilo ndiyo maana tukaona kwamba Marais wetu ambao wamepita wote walikuwa wana ripoti zao, Mheshimiwa Mkapa alikuwa ana ripoti, Mheshimiwa Mwinyi alikuwa ana ripoti, Mheshimiwa Dokta Kikwete alikuwa ana ripoti kuhusiana na suala hili la kufaidika na rasilimali za nchi. Hata hivyo, isitoshe tunafanya hivyo kwa lengo la kwamba ni lazima kuweka uwiano mzuri kati ya maslahi ya Taifa kwa wananchi wote pamoja na kuwavutia wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika pongezi zangu kwamba Rais Magufuli amejipambanua kutokana na wengine wote ingawaje kwamba wametokezea watu sasa wanajipaka damu za simba kama wao ndiyo walioua simba lakini simba tayari ameshauliwa sasa wanajitokeza. Hoja hii hata kama kuzungumzwa ilikuwa ikizungumzwa mpaka kwenye vibaraza vya kahawa kwamba vipi watu watafaidika na mchanga au na madini ambayo yapo katika nchi kwa hiyo siyo kwamba ni suala la fulani na fulani. Mimi naeleza hili kwamba Rais Dokta John Pombe Magufuli ni kiumbe na roho yake hawa wengine wote wanaojipakapaka ni midoli tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika Azimio hili tuiombe Serikali kwa upande wake iweze kupitia mikataba na kubaini mianya yote na kuiziba ili rasilimali za Taifa zisaidie Taifa. Pia kwa upande wa Bunge kama ilivyopendekezwa kwamba Serikali italeta marekebisho ya sheria, kwa hiyo, yatakapoletwa marekebisho ya sheria tuweze kuziba mianya yote, sisi ni Watanzania tuzilinde rasilimali zetu. Pamoja na hayo Waziri naye atengeneze taratibu kwa sababu madini haya yanatoka sehemu tofauti tofauti, kwa hiyo, hizo taratibu atakazoziweka ziwe sambamba na maeneo ambayo madini yetu haya yanatoka.
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI NDUGU PROF. MUSSA ASSAD, MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza niungane na Kamati kwamba ni kweli maneno yaliyotumika yalikuwa siyo mazuri. Nitoe tahadhari tu kwa wenzangu wengine, hapa kuna watu walisema Waheshimiwa Wabunge wanasinzia. Tulifurahi Wabunge wote kwa kuletwa mbele ya Kamati mtu aliyesema hivyo. Aliletwa Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa hapa Makonda, alikosea; aliletwa Mheshimiwa Mnyeti hapa kwamba alikosea na sote tulikubali kwamba alifanya jambo siyo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie katika mantiki moja, kwa nini naunga mkono? Bunge jukumu lake ni kusimamia na kuishauri Serikali, lakini CAG ni part ya Bunge, yeye ndiye anayeona vitu, analeta katika Bunge na Bunge tunafanyia kazi. Katika collective responsibility yeye CAG ni part ya Bunge, haiwezekani kwa mtu kama yeye peke yake akasema sisi ni dhaifu halafu na sisi dhaifu bado aendelee kufanya kazi nasi. Hicho kitu hakitawezekana. Siyo kitu kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Profesa Assad yeye ni CAG, tumempa Kamati ya LAAC anafanya kazi, tumempa Kamati ya PAC anafanya nayo kazi; na kama ilikuwa mahali pa kusemea, ni kule. Kwenda kusema udhaifu nje ya sehemu ya mipaka yake ya kazi hapo amedhalilisha. Kuna msemo wa Kiswahili unasema, akutukanaye hakuchagulii tusi. Pia mshairi mwingine anasema kwamba ndugu akufukuzaye, hakwambii kwangu hama. Ukiambiwa dhaifu, ina maana kuna jambo kubwa zaidi unaloambiwa. Viile vile akutukanaye hamtaji mama yako. Kwa hiyo, kudhalilishwa siyo lazima utajiwe kwamba mwana kadha kadha, hata hili ni jambo la kudhalilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Bunge ndio ambao tumeona hicho kitu. Kwa hiyo hicho kitu kinaudhi. Kuna mtu mwingine hapa nimpe tahadhari tu, ukizungumzia haki, uhuru na uwazi wa kutoa taarifa au kufanya mawasiliano, siyo kwamba umdhalilishe mwenzio. Katoe taarifa, unayo haki hiyo. Kafanye mawasiliano. Unayo haki ya kufanya mawasiliano, lakini siyo utoe taarifa za kumkashifu mwenzio. Ukitoa taarifa za kumkashifu mwenzako, ina maana kwamba umemkosea yule mtu, unapomalizia wajibu wako, ndipo haki ya mwenzako inapoanza. Kwa hiyo, nami nazungumzia hili neno udhaifu siyo neno zuri na shahidi amekiri kwamba yeye alilisema hili neno, lakini anajaribu kukengeuka kusema kwamba hiyo siyo tafsiri yake, yeye anatumia tafsiri ya kihisabati. CAG hatujampa kazi ya ku-access Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mheshimiwa mmoja hapa alisema kwamba taaluma yake ndio inayomfanya kwamba yeye aseme hivyo, hakuna taaluma ya kuli-assess Bunge akajua upi udhaifu wa Bunge? Yeye ana taaluma ya ku-assess account akaleta taarifa kwa Bunge katika Report na Bunge ndiyo linafanyia kazi. Sasa yeye sijui ka-assess wapi hilo Bunge akagundua kwamba kuna udhaifu. Hawezi kujua, hana kipimo. Kwa hiyo, hapa amekusudia kulifanyia vibaya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante, kwanza nashukuru Mungu kwa kutujalia uhai na pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii lakini niwashukuru na kuwapongeza Wizara ya Makamu wa Rais inayoshughulikia mambo ya Muungano kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nathamini juhudi zao kubwa ambazo wanazozifanya katika kuzitatua changamoto, siwezi kusema kero ni changamoto na kitu chochote kinachohitajika kuendelea ni lazima kitakuwa kina changamoto zake, sasa nashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri January Makamba kwa hotuba yake nzuri na kwa ziara ambayo aliifanya kule Zanzibar. Sasa Mheshimiwa katika ziara yake alipokwenda kule Zanzibar alilalamikiwa na wafanyabiashara. Namshukuru kwa kukutana na wafanyabishara wale ambao walilalamikia double VAT ambayo wanapata, ile VAT wakati wananunua bidhaa zao Tanzania Bara na pia wanapofika Zanzibar wanapata tatizo lile lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tatizo hilo lilizungumzwa mbele ya Rais wetu Mtukufu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wafanyabiashara kutoka Zanzibar walimlalamikia lakini tukisema kodi tunazungumza kodi gani? Kodi hii iko sehemu gani? Kwa hiyo, kodi hiyo, naitaja, Finance Act ya mwaka 2016 kifungu cha 94 ya mwaka 2016 iliweka kifungu kipya katika VAT cha 55A ambacho kinasema:

“A supply of locally manufactured goods by a local manufacturer shall be zero rated if the goods are supplied to a taxable person registered under the Value Added Tax Law administered in Zanzibar and such goods are removed from Mainland Tanzania without being affectively used or enjoyed in Mmainland Tanzania”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndipo palipoleta tatizo la hiyo kodi ambayo ilikuwa ikizungumzwa na nashukuru Mheshimiwa Waziri kifungu hiki alipoenda kuwauliza mwenyewe wafanyabiashara na kwa bahati aliweka vikao tofauti jinsi ya kuvishughulikia. Sasa tamaa au matumaini yetu kwamba Serikali itakapokuja kwenye Finance Act ina maana kwamba jambo hili ni lazima lishughulikiwe, vinginevyo sisi ni watunga sheria, kama hatujalisema wazi hapa tutaliacha na litakuwa linaendelea kututafuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kitu ambacho kinapatikana kutokana na kifungu hiki, kwamba mtu akinunua bidhaa zake kutoka Tanzania Bara akipeleka Visiwani ikiwa yule mtu hajawa-registered by ZRB ina maana kwamba atachajiwa hapa asilimia 18, akifika Zanzibar atachajiwa na ZRB asilimia 18, kwa maana hiyo atalipa asilimia 36. Kwa hiyo, kwa mfanyabiashara mwenye mfuko mdogo hapa msingi wake unakufa kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hasara nyingine tunayopata ni kwamba watu wako tayari kwenda kununua bidhaa zile Kenya na wakati sisi tumo ndani ya Tanzania hii moja, mtu mmoja analipa asilimia 36 mwingine analipa asilimia 18 ya VAT kutokana na kifungu hiki. Sababu ya kifungu hiki kwamba ametajwa mtu lazima awe ame-register na ZRB kama ni taxable person. Sasa kwa taxable person wengine sio taxable person.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano zipo NGO au mashirika mengine ya kijamii, yanahitaji kujenga shule, kununua saruji, mabati na vitu vingine. Wakija kununua hapa wanaanza kuchajiwa huku mwanzo asilimia 18 na akifika Zanzibar anachajiwa tena asilimia 18. Nashukuru Mheshimiwa Waziri kwa taarifa ambazo zipo kwamba kikao kimefanyika, lakini tunataka utekelezaji wake na utekelezaji wake tunaomba Mheshimiwa Waziri alete hapa sheria tuje tubadilishe ili hii kero/changamoto iondoke. Bila kuondoka changamoto hii ina maana kwamba hatutoweza kufikia mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru Serikali mwanzo ilipoona kuna hili tatizo wakasema wabadilishe sheria. Walibadilisha sheria hii naamini kwa nia nzuri tu, lakini utekelezaji wake baada ya kuingizwa haya mambo mawili kwamba lazima iwe manufacturer na lazima awe taxable person ndipo penye tatizo. Kwa hiyo, hili tatizo litakapoondoshwa, whether tukarudi kulekule mwanzo tukatumia origin principal kwa sababu hapa imepelekwa katika destination principal na ukipeleka kwenye destination principal bila ya kuwa na refund scheme ina maana hicho kitu si rahisi kutekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri nakuomba ulete sheria hiyo hapa tuje tufanye marekebisho katika Finance Act. Bila ya hivyo utekelezaji wa hili tunalosema humu tutakuwa tunapiga kelele na sheria yenyewe ni hiki kifungu 55A kilichoongezwa mwaka 2016.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, napenda kuzungumzia biashara, tumesema Tanzania ya viwanda, hatujasema Zanzibar ya viwanda wala hatukusema Tanzania Bara ya viwanda, tulisema Tanzania ya viwanda. Sasa ninachokiomba katika hili, ikiwa tunasema Tanzania ya viwanda ina maana kwamba hii movement of goods kama mtu akiweka kiwanda chake Zanzibar ina maana kwamba hatopata soko la Bara na ikiwa hatopata soko la Bara ina maana investment itakuwa haiwezi kufanyika Zanzibar kwa sababu bidhaa zake mtu hawezi kuingia kwenye soko la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunachoomba, kwa kuwa soko ni kubwa na mtu anapofanya biashara anatazama location yake kwa mujibu wa soko lilivyo anapima Tanzania, Zanzibar ikiwa location kuna tatizo gani huyu mtu kumpatia ufumbuzi, kuna matatizo gani kuweka soko hili free? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nijulikane wazi sipiganii suala la askari, katika suala la askari niko pamoja na msimamo wa Serikali, lakini bidhaa nyingine, tukisema kwamba kila kinachozalishwa Zanzibar hakiingii Tanzania Bara ina maana kwamba tuna-discourage investment Zanzibar. Hakuna investor atakayekubali kwenda kuwekeza kule ikiwa msimamo kila kinachotoka kule kitakuwa hakifai kuingia huku, mtu anatazama soko kubwa na sisi tuko katika Afrika Mashariki, tunapima soko la SADC, tunatazama na soko la Tanzania. Sasa tukianza kujikataa wenyewe nani atatukubali? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kingine, endapo nitazungumza nje ya miko ya taasisi inayoniongoza kisiasa nitaitwa Msungo na kama atatokezea mtu kwamba hana miko katika kuzungumza na taasisi inayomwongoza jambo la ndani akalitoa nje au jambo la kusema ndani yeye akalifanya nje, mtu yule kisiasa anaitwa msungo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili jambo la usungo linafanyika humu. Inakuwaje mtu jambo kama hili inakuwa mtu unalifanya, kitu ambacho kwamba kinajulikana faida za Muungano au chama fulani ndiyo kina msimamo wa Muungano huu, lakini anatokezea mtu pengine umri mkubwa tu akaja akafanya mambo akacheza shere Muungano. Kwa maana hiyo huyo mtu yeye sasa ndio anabakia anakuwa ndio kero ya Muungano, Muungano hauna kero kama alivyo kero huyo mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, nina wasiwasi huenda ikawa kuna minazi ya mpakani humu la sharikia wala gharibia, maana huo mnazi hauko mashariki, hauko magharibi, hatuujui mnazi wa wapi. Kwa hiyo aseme mtu waziwazi, lakini asifanye usungo wa kisiasa katika Bunge lako hili tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii. Mimi la kwanza kabla sijamshukuru Mungu niseme Subhanallah min-dhalika.

Mwenyezi Mungu ametakasika na yote ambayo yamesemwa na mtu ambaye hajielewi, ametakasika. Mungu hakosolewi kwenye imani yoyote ile. Sasa waone Watanzania jinsi gani kwamba mtu kama huyu ndio awe wanamwamini kwamba kumfuata maneno yake ikiwa kwamba kauli zake ndiyo hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa hii nafasi. Pili, namshukuru Mwenyezi Mungu na naomba Mwenyezi Mungu aniongoze, anitoe kile kitanzi wanachotiwa wenzetu wanapojikakamua sauti kali na halafu haitoki, kile kitanzi Mungu mimi aniondoshee nizungumze hivi taratibu ili message yangu ifike vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wanazungumza matukio lakini wanashindwa kusema sababu. Wanataja kulaumu lakini wanashindwa kutaja sababu zilizowapelekea au zilizowafikisha watu pale wao wanapolaumu. Wanalilaumu Jeshi la Polisi lakini wanasahau kwamba kuna mambo yalifanyika Kibiti wakidhibitiwa, mambo yalifanyika Tanga wakidhibitiwa, mambo yanayohamasisha maandamano, mambo ya watu wanaozungumza tofauti, ni sawasawa na kusema kwamba lawama sasa zinahama kwa mjambaji zinakwenda kwa mtema mate. Hivi ndivyo walivyo wenzetu, lawama zinahama kwa mjambaji sasa zinaenda kwa mtema mate, kwa sababu wahamasishaji wa ubaya ni wao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi niongee ya kwangu kwa Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa masikitiko makubwa sana kusikitikia Wizara hii ya Mambo ya Ndani na huzuni kubwa sana, mwaka wa tatu huu haya ninayoyasema leo nayasema tena. Hakuna hata moja ambalo limefanyika kwangu na mimi sasa nazungumza masikitiko yangu Jeshi la Polisi kwangu mimi natokea Jimbo la Jang’ombe, kuna Ziwani Polisi, Jeshi la Polisi kwangu ni sawasawa na double edged sword, upanga wenye ncha mbili. Ncha ya kwanza ni sehemu ambayo tunapata ulinzi na usalama kwa Tanzania nzima na hiyo tunanufaika katika Jimbo letu, lakini ncha ya pili kwa Jeshi la Polisi kwangu mimi ni wapiga kura wangu Mkoa mzima wa Mjini Magharibi Unguja askari wake wanakaa Ziwani Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefanya ziara tarehe 7 Januari, 2018 kwenda Ziwani Polisi nikakuta pale kuna zile nyumba ambazo za single wanakaa mtu mmoja mmoja kutokana na ukosefu wa nyumba, zile nyumba zinakaa familia, zile nyumba zipo 15 kila nyumba moja ina familia nane kuna familia 120, kule kwetu sisi mashallah watu wanazaa. Tukimpa kila mmoja watoto wanne wanakaa watu wanne ndani basi watu 480 wanakaa, lakini wanatumia choo kimoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili nimeshalisema na lilianza kusemwa na Mbunge aliyepita mwaka 2011 halijafanyiwa kazi. Pale kuna choo kimoja kiliwahi kujengwa na Mheshimiwa Nyanga aliyekuwa Mwakilishi wa Jimbo la Jang’ombe. Nampa tena Mheshimiwa Waziri hii taarifa tena, je, likitokea la kutokea choo kimoja watu 480 wanatumia vipi askari hawa. Masafa ya kufuata choo ni mita 100 mpaka mita 200; kila mmoja anatoka na kopo la maji na ndoo, ukitokea ubakaji pale tutasemaje? Yakitokea maradhi ya mlipuko katika choo kile kimoja tunafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri hili naomba nitekelezewe na nimepeleka kwa DCP Malika, Kamishna wa Ujenzi wa Polisi Makao Makuu nimepeleka mwenyewe kwa mkono. Tunahitaji milioni 50 kujenga vyoo pale vya askari, kama kuna dharura basi tuje tusubiri dharura ya kupata maradhi watu wakafa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nyumba ya Kilimanjaro Ziwani Polisi, hii nyumba imejengwa tokea kwenye miaka hiyo ya 1980, hii nyumba inatakiwa kukarabatiwa, nyumba inakaa 12, tukimpa kila mmoja watoto wanne, nyumba inavuja na inakaribia kuanguka. Hivi leo ndio tunataka mpaka nyumba ianguke askari wafe tulete mfuko wa maafa. Tunahitaji milioni 68 kukarabati kuweka paa ili kudhibiti vitu ambavyo vinatokea pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi mvua za juzi, familia mbili zinazokaa juu kwenye jengo la Kilimanjaro Ziwani Polisi zimehama kwa sababu jengo linavuja, je, tunasubiri lianguke? Kama hiki sio kipaumbele, kipaumbele ni kuzika askari wetu? Kipaumbele ni kwenda kuzika familia askari wetu kama hiki sio kipaumbele. Kwa hiyo, nazungumza leo kwa uchungu kabisa katika Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia katika Vote 28 subvote 2005 ya Zanzibar nimeona kuna fedha pale za maintenance and repair of building kwamba imewekwa ni milioni 22. Fedha hizi haziwezi kutosha kwa kufanya hili jambo. Kwa hiyo, naomba Waziri atakapokuja hapa aje anipe maelezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumetajwa katika ukurasa wa tisa wa hotuba ya Waziri miradi ya ujenzi mpya wa nyumba za polisi. Tuliahidiwa tutajengewa nyumba 423 mwaka juzi kukawekwa na bajeti, mwaka jana hakukuwekwa bajeti, mwaka jana kuliwekwa milioni 200 kukarabati kituo cha Mkokotoni, mwaka huu nimeangalia kwenye development hakuna lakini tunaambiwa kuna bilioni 10 ya Mheshimiwa Rais itatokea kwenye bajeti gani, kwanza nataka niambiwe hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia zitajengwa nyumba 400, tulikuwa tunataka tuambiwe kwa Mjini zitakuja ngapi, kila siku unatajwa ujenzi lakini haziji fedha. Sasa na hili vipi tunataka Mheshimiwa Waziri waje watuambie ukweli wanaposema hapa tunayapeleka majimboni kwetu na mimi naishi na askari kule au hawataki nirudi mwenzao hapa. Hakuna jambo hata moja nililotekelezewa tokea mwaka wa kwanza nakuja hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, Ziwani Polisi kuna hospitali, kwa nini tusiipelekee ambulance kama inavyokuwa kwa majeshi, ikitokea dharura ya kuhamisha mgonjwa pale tunafanya nini? Ziwani Polisi wamejenga kituo cha afya kipo kinaendelea kama hospitali nyingine katika kambi lakini katika kituo hiki cha afya wamejenga maternity pale mradi ule haujaisha. Kwa hiyo, je, hapa tunafanya nini katika kuwa- support kwenye hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie jambo ambalo amelizungumzia Mheshimiwa Khatib, kwa mujibu wa Sheria ya Jumuiya (The Society Ordinance) ya mwaka 1954, Wizara ya Mambo ya Ndani ndiyo ambayo inatakiwa kuwa na usimamizi wa jumuiya hizi za kidini. Sasa hapa kifungu kinataka kuteuliwa kwa Msajili wa Jumuiya, msajili huyu hajateuliwa, watu sasa hivi wanafanya hayo mambo chini ya kitengo cha sheria cha polisi, kwa hiyo kifanyike hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wizara inao uwezo wa kupendekeza hilo jina la Msajili likateuliwa lakini pamoja na kuanzisha Ofisi ya Msajili. Kwa hiyo, hili linatakiwa pia nalo lifanyike. Mheshimiwa Waziri amshauri Mheshimiwa Rais amchague Msajili wa mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ninalotaka kuzungumzia ni kuhusu umeme, askari wanalipa wenyewe umeme. Bajeti iliyopita ya mwaka 2016/2017, ilikuwa actual milioni 74 zilizoenda Zanzibar zimeshushwa sasa hivi milioni 24, je, matumizi ya umeme yamepungua? Mwaka jana zimewekwa milioni 24, mwaka huu milioni 24. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aje aweke sawa katika suala hili, sisi tunapokea malalamiko ya askari polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na nashukuru.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuchagia mjadala huu wa Wizara ya Fedha na Mipango. Lakini cha kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kuja hapa kuchangia hoja hii.

Nipende kutumia neno moja ambalo la msingi sana hili neno ni neno kubwa sana ingawa kwamba limo katika misemo ya kizamani, msemo huu unasema ukiona majuha wanapongezana usifikiri wamefanya la maana. Mheshimiwa Mwenyekiti, asiyojua maana haambiwi maana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kwenye Bunge hili kuna milio ya mbwa sasa hawa mbwa kama tutawatoa itakuwa vizuri, sababu nasikia milio ya mbwa, nasikia milio ya mbwa kama hawa mbwa tukiwatoa itakuwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, ahsante katika kuchangia suala hili nilikuwa niendelee na suala moja hasa hasa katika masuala ya mifuko. Masuala ya mifuko mara nyingi Mheshimiwa Waziri hapa alisema kwenye ukurasa wa 19 na 20 ya kwamba kuna uhakiki wa madeni lakini kwenye mifuko hii fedha zake haziendi kwa utaratibu ambao unaotakiwa. Tukitazama kwenye Mfuko wa Reli, tukitazama REA, barabara, maji, Bodi ya Korosho na mambo mengine kwamba utaratibu unaotakiwa fedha hazijaenda. Sasa pamoja na uhakiki tunaotaka, lakini tujue kwamba tumepanga bajeti ndani ya mwaka ni miezi 12, hii miezi 12 tukisema tunachelewesha kupeleka fedha hizi ndani ya miezi 12 ina maana kwamba uhakiki miezi 13. Lakini tumepanga kutumia matumizi ndani ya miezi 12 ina maana kwamba hatutopata tija na mifuko hii ambayo tumeanzisha.

Mheshimiwa Spika, pia kuna masuala ya property tax ambayo tulipanga. Kwa hiyo, naishauri Serikali kwamba ifanye uhakiki ndani ya miezi 12 pamoja na kulipa madeni hayo. Lakini mifuko hii kwamba imo kwa mujibu wa sheria na imo ndani ya Serikali. Kwa hiyo, Serikali yenyewe kwa wenyewe inakinzana katika kuzitumia pesa hizi za mifuko.

Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba Waziri atueleze bayana mpango wake na mkakati wake wa uhakiki huu kufanyika ndani ya miezi 12 kwa mujibu wa bajeti yetu ya miezi 12 na mifuko hii itumike na fedha zitolewe kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, lingine refund za VAT hazijaenda shilingi bilioni 500 kwa watu wa migodi hazijaenda zinageuka zinakuwa deni, kuna refund nyingine ambazo zina deposit za industrial ya sugar, industrial ya sugar shilingi bilioni 35 hazijatoka fedha hizi zimenasisha mitaji kwa wafanyabiashara hawa. Mitaji hii ikikwama ina maana kwamba uwekezaji unapungua ajira kwa wananchi wetu zinapungua. Lakini hizi Taasisi zinaenda kukopa fedha baada ya hizi fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wanapoenda kukopa fedha hizi inamaana kwamba wanalipa interest, kwa hiyo, wanasababisha kuwa na upungufu wa fedha na wanapunguza wanyakazi. Lakini pia money multiply inapungua, ukiwa umezuia mia katika multiply effect inazuia mara tatu ina maana kwamba kwa hizi shilingi bilioni 500 na hizi shilingi bilioni 35 mara tatu yake ndiyo fedha zimekosa mzunguko ndani ya mwaka.

Kwa hiyo, tunamuomba Mheshimiwa Waziri awe na utaratibu mzuri wa kuweza kufanya mambo haya na hili… (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii adhimu ya kuchangia katika Bunge hili. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri imegusa katika Kiswahili na ili tuweze kuenzi Kiswahili hiki, nakumbushia, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, wajaribu kutazama michezo ambayo inakuza Kiswahili chetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kuna tabia ya michezo kutafsiriwa, sisi tuna mila zetu na tuna Kiswahili chetu, mchezo kama unatafsiriwa Kiswahili bora ukaonyeshwe huko nchi nyingine ili Kiswahili kienee. Siyo mchezo unatafsriwa Kiswahili hapa kwetu, haiwezi kuchangia kitu. Hilo moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, alisimama hapa mtu mmoja akazungumza Mheshimiwa Khatib, Mheshimiwa Khatib, najua amezungumza hivyo ili anichafulie katika uteuzi katika chama changu. Kwa sababu najua yeye hana wasiwasi kwenye uteuzi, kwa sababu Mheshimiwa Khatibu ni pete na Maalim ni chanda. Kwa hiyo, najua tu kwamba yeye atachaguliwa na hilo jambo linajulikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, anasema mimi naimba taarab, ni sawa, na starehe kwa mwenye kuimba, taarab inazungumzia sana mapenzi na mapenzi mara nyingi yanakuwa ni baina ya jinsia mbili, mwanamke na mwanamume, mwenzangu yeye hana hilo, hata mke hana! Sasa siwezi kujua kwamba yeye ana kitu gani maana… (Kicheko)[Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali King, hayo ya kutokuwa na mke mwachie yeye mwenyewe kama anayo. Kwa hiyo, hebu endelea na mchango wako, ondoa hayo maneno ya yeye kutokuwa na mke. (Makelele)

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, na yule aliyesimama namjua vizuri tu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali King, kuna taarifa, Mheshimiwa Juma!

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Ally King ya kistaarabu tu Mheshimiwa ana mke na ana watoto sita, mke wake yuko Tanga, familia yake iko Tanga, kwa hiyo, suala la kwamba Mheshimiwa Khatibu hana mke hili Mheshimiwa Ally King siyo la kweli kabisa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa AlI King, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea hii taarifa, ni sawasawa na mchicha wenye miiba lakini huliwa! (Kicheko/Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ali King hebu ondoa hayo maneno yako ya mwisho hapo. (Kicheko)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, naondoa haya maneno.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye michango ya Bunge hili kama watu watakumbuka hoja ya umeme kwenye VAT, hilo lilizungumzwa, kazungumza Mheshimiwa Saada Mkuya nimezungumza mimi, kule hakujakuwepo mtu hata mchango wake. Hoja ya VAT ya bidhaa zinazokwenda Zanzibar, zinazotengenezwa Zanzibar kuja bara, hakuna mbunge aliyeweza kulizungumza hilo nililolizungumza mimi. Sasa hii kupiga makelele, kujikamua na kujidhihirisha ile tabia yake ambayo anayo, hicho siyo kitu ambacho labda kila mmoja anaweza akafanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nimshauri tu Mheshimiwa Khatibu, sie tushamjua na vijana huko nje wanapata taabu sana, waosha magari, tunajua! (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba ajaribu kueleza vitu ambavyo viko kweli. Kwenye masuala ya Muungano sisi Wabunge wa CCM ndiyo tuliozungumzia sana, nami nina hoja nyingi sana ambazo nikiziweka hapa mezani, watu watajua nini nimechangia katika Bunge hili. Kwa hiyo, Mheshimiwa Khatib mimi namwambia hiki kitu aache, mimi muimbaji taarab sawa, lakini yeye asitumie mic nyingine atumie mic ileile ambayo mimi naimbia taarab. Sasa hii mimi napenda kumwambia kitu hiki. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ninachopenda kuchangia katika Bunge hili, tuanze kuandaa vijana vizuri kwa michezo! Michezo, tukiandaa vijana vizuri, timu zetu zitaenda mbele! Watanzania tutakuwa tuna furaha, tusiwe na programmes hizi za zimamoto. Juzi tulifurahi kidogo tatizo tulifungwa na hata siku ile ambayo Simba amefungwa nne, Yanga walifurahi lakini Simba tulinuna, lakini sasa tukiwa na timu zilizoandaliwa itakuwa ni vizuri, kwa nini tusiwe na academy. Academies zipo lakini za watu binafsi!

Mheshimiwa Naibu Spika, ziko taasisi zinao uwezo wa kuhamasishwa hata hizi nyingine, zikaandaa hizo programmes kwa sababu sasa hivi michezo ni uwekezaji, leo tukiwa tuna wanamichezo 20 wanacheza ligi za nje, watachangia katika mapato ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia kwa mia, Wizara ya Michezo izingatie haya ambayo nimeyazungumza. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu kutusajili siku ya leo kuwa miongoni mwa viumbe ambao wana uhai na wana afya. Pili, nikushukuru kwa kunipa hii nafasi ili niweze kuchangia katika hotuba ya Rais ambayo ameitoa mwezi wa 11 wakati wa kufungua Bunge.

Mheshimiwa Spika, lingine nikishukuru chama changu na wananchi wa Jang’ombe kwa kunijalia kurudi tena hapa Bungeni kwani si kazi ndogo kufikia ukarudi. Kwa hiyo, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuchaguliwa tena kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuendelea kuliongoza Taifa hili hali ya kuwa tuko katika uchumi mzuri na katika utulivu na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu mwanzo nitajikita katika ukuaji wa uchumi. Mheshimiwa Rais ametuongoza katika kukuza uchumi na ameeleza katika ukurasa wa 18 kwamba kila mwaka uchumi wetu ulikuwa ukikua kwa asilimia 7 kutoka 2015 hadi 2019 hata na hii 2020. Imeonyeshwa hapo kutoka shilingi trilioni 94.4 mpaka kufikia shilingi trilioni 140 maana yake ni kwamba katika miaka mitano hii tumeongeza karibu ya one third katika GDP yetu ambayo imeanza tokea miaka ya nyuma. Kwa hiyo, katika kipindi cha miaka mitano tumefikia hivi.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tuko katika uchumi wa kipato cha kati lakini pia Mheshimiwa Rais amesisitiza kwamba tunataka kuendeleza ukuaji wa uchumi na ndipo katika eneo hilo ninapotaka mimi kuchangia. Katika eneo hilo nataka nijikite zaidi katika uvuvi wa bahari kuu. Kuna msemo wa wahenga wanasema mtemewa mate na wengi hulowa, kwamba lilishazungumzwa hili eneo la uchumi wa bahari kuu lakini na mimi nalirejea tena kulizungumza kwa umuhimu wake ili lipate kutiliwa mkazo zaidi.

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa 35, 36 na 37 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais ameelezea kwamba ana azma ya kukuza pato la Taifa kwa kuimarisha uvuvi wa bahari kuu lakini pia ameelezea mapato ambayo tunayapoteza ambayo ni zaidi ya shilingi bilioni 350, lakini pia ameelezea makusanyo ambayo sasa hivi tunapata kupitia uvuvi wa bahari kuu kwa sababu tunafanya katika ufinyu wake tunapata shilingi bilioni
3.3 kila mwaka. Kwa hiyo, tunapoteza shilingi bilioni 352 kila mwaka lakini tunachopata sasa hivi kutokana na ufinyu wa uchumi wa bahari kuu tunavyoutumia ni shilingi bilioni 3.3. Taarifa hizi ni rejea za ripoti ya Bunge la Kumi na Moja, tunakupongeza sana Mheshimiwa Spika kwa kulisimamia hili na data hizi sasa hivi zinatumika huko.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameeleza kuwa miaka hii mitano atasimamia vizuri uchumi huu. Pia katika shughuli hii ya uvuvi wa bahari kuu tayari sheria yake imeshapitishwa na Bunge lako Tukufu lakini pia Rais amepanga kununua meli nne Tanzania bara na meli nne Zanzibar. Pia kujenga bandari moja kubwa ya uvuvi itakayoajiri zaidi ya watu 30,000. Vilevile atahamasisha sekta binafsi kuwekeza katika viwanda vya kuchakata samaki ambapo huko ajira zitazaliwa.

Mheshimiwa Spika, haya ni maelezo ambayo yako katika hotuba ya Mheshimiwa Rais, sasa ushauri wangu. Ili tufaidike kikamilifu katika fursa hii basi ni lazima tuwekeze katika ukamilifu wake, tusipowekeza katika ukamilifu wake zile faida tunazozifikiria kwamba tutazipata hatutoweza kuzipata. Soko la samaki linategemea mazingira ya samaki tokea anavyuliwa, bandari gani amepokelewa, store gani amehifadhiwa na mengine mengi ambayo yako katika facilities katika uvuvi huu wa bahari kuu.

Mheshimiwa Spika, kiufupi facilities zote zipatikane ndiyo tutafikia katika haya maono ambayo Mheshimiwa Rais ameyaona na ndipo tutafikia katika ripoti ambayo imetolewa na Bunge hili kwamba tukiwekeza katika bahari kuu tutafaidika na hayo. Sasa ili tufaidike na uvuvi huu tuangalia resources tutapata wapi? Serikali peke yake haitotosha kutoa resources zake kwa ajili ya kuwekeza katika uvuvi wa bahari kuu. Kwa hiyo, inputs ni lazima tuchanganye kutoka katika sekta ya umma, sekta binafsi, lakini pia katika mchanganyiko wa sekta ya umma na sekta binafsi yaani ubia (PPP). Pia siyo makosa tukawaalika wenzetu wa nje wakaja wakatusaidia katika uwekezaji kwa sababu hii sekta inatakiwa kufanywa katika ukamilifu wake. Pia siyo vibaya kupata uzoefu kutoka katika mataifa mengine wanafanyaje wenzetu mpaka wanafaidika na mambo hayo?

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwa kuwa Rais amesema na kwa kule Zanzibar atanunua meli nne, ina meli nne hazitoweza kufua dafu hizo meli zitavua lakini wapi tunaweza kupeleka itakuwa hakuna kwa kupeleka kwa sababu hakuna bandari na ikiwa hakuna bandari hiyo hata viwanda vya kuchakata havitakuwepo na hivyo kufanya marketing yake samaki hao itakuwa ni vigumu, kwa hiyo, hii fursa tunaweza tukaikosa. Sio vibaya na sisi tukawa na dhana au aspect hii ya uchumi wa blue tukiwa na huo uchumi wa blue nao pia unaweza ukatusaidia.

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili, Mheshimiwa Rais katika ukurasa wa 62 na 63 ametambua shughuli nyingi sasa hivi zinafanywa kwa kutegemea TEHAMA. Kwa hiyo, TEHAMA ameipa kipaumbele na ameeleza katika kurasa hizo kwamba amepanga kuongeza wigo wa matumizi wa mawasiliano ya kasi lakini pia kufikisha miundombinu ya mkongo wa Taifa ameeleza ili iwafikie wananchi wengi wa Tanzania na mambo mengine mengi ameeleza katika kurasa hizo ambayo yanahusiana na mambo ya TEHAMA.

Mheshimiwa Spika, pamoja na haya ambayo Mheshimiwa Rais amesema, nampongeza sana ameweka Wizara inayoshughulikia masuala ya TEHAMA. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuliona hilo.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa kuna dhana ya digital economy, hapo ndiyo kwenye hoja yangu mimi, pamoja na uwekezaji huu hivi sasa kutokana na digital economy transactions nyingi sana zinafanyika online kwa maana hiyo tunakosa kukusanya mapato kikamilifu kutokana na dhana hii. Sasa hivi hapa ukienda katika makampuni mengi unaweza ukaagiza unachotaka, ukalipa na ukaletewa lakini Serikali haipati kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kupitia mfumo huu wa TEHAMA, naomba Serikali ijaribu kuangalia katika eneo la ulinzi na usalama kwanza lakini pia Serikali ikasomeshe vijana hapa tunakosa vitu vingi sana ambavyo vinatokana na tax zinazopatikana kutokana na hizo transactions zinazofanyika off show. Tusiseme watu wasifanye hiyo biashara ya off show lakini mpiganaji mzuri ni yule mtu anayemfuata mtu angani kuliko kusema umpopoe mawe aanguke chini um-charge huku chini. Kwa hiyo, Serikali itafute na isomeshe hao vijana ili tuweze kufaidika na hicho kitu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni la umuhimu sana katika uchumi wetu wa Tanzania ili uweze kukua tumeanzisha hii standard gauge reli na imeanza Dar es Salaam tumekusudia inakwenda mpaka kwenye mipaka yetu, lengo letu tuitumie vizuri bandari yetu ya Dar es Salaam. Kwa hiyo, hoja yangu inaanza kujikita kutokana na ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam na hili amelieza Mheshimiwa Rais na hoja yangu pia inajikita katika utoaji au upatikana wa fedha.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, muda wangu umeishia hapo na nashukuru kupata nafasi hii, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nashukuru sana kwa Mwenyezi Mungu kutupa uhai na uzima, lakini pili, nikishukuru wewe kwa kunipa hii nafasi kuweza kujadili Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda katika maoni yangu kwenye Mpango huu, kuna msemo mmoja wa kiarabu unasema lisanu-l-hali haswa umilisan-l-bakabi; lugha ya hali ilivyo ni fasaha zaidi kuliko lugha ya maneno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo mzungumzaji aliyepita anasema kwamba Serikali hii iliwadanganya watu katika umeme, umeme haukufika vizuri vijijini. Wewe tazama hali ya kura zilizokuwemo humu zilivyoenea, ni fasaha Zaidi, halafu tazama na zile zilizobakia, kwa hiyo hii lugha na hii hali ya humu ndani ni fasaha zaidi kuliko maneno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite moja kwa moja katika kuboresha mapendekezo ya huu Mpango. Wizara ya Fedha imetuletea Mpango. Katika Sura ya Sita, wameeleza ugharamiaji wa Mpango na wamesema kwamba Mpango huu utagharamiwa kwa jumla ya trilioni 114. Wakasema sekta ya umma trilioni 74 na sekta binafsi trilioni 40, lakini tukiangalia Mpango uliopita, Serikali ilisema kwamba sekta ya umma Mpango wote utagharimu trilioni 107, sekta ya umma itatumia trilioni 59 na sekta binafsi trilioni 48. Lakini matokeo baada ya miaka minne, sekta ya umma imetumia trilioni 34.9 ambayo ni sawa na asilimia 77 ya miaka minne; lakini sekta binafsi imetumia trilioni 32.6 ambayo ni sawasawa na asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye sekta binafsi, hizi trilioni 32, ni sawa kwa miaka minne, ina maana kwamba kwa miaka mitano sekta binafsi itafika trilioni 40.75. Sasa tumesema tutafanya maboresho kwenye sekta binafsi, huu Mpango umeeleza mambo ya blue Print, umeeleza mambo ya uwekezaji, umeeleza kuondosha vikwazo vingi. Sasa kwa nini tumeipa sekta binafsi trilioni 40, wakati mwaka huu bila marekebisho yoyote, tunaweza kufika trilioni 40 ndani ya miaka hii mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naiomba Serikali ikafikirie tena katika ugharamiaji wa Mpango huu kuwa sekta binafsi haitoshi kwa trilioni 40, tunao uwezo wa kufika zaidi ya trilioni 40 endapo yale maboresho katika Mpango huu kuhusiana na sekta binafsi yatafanyika. Hilo ndilo pendekezo langu la kwanza, kwa sababu tukifika miaka mitano kamili tutakuwa tumeshapita trilioni 40. Je haya maboresho plus tutapata ngapi? Naomba hilo wakalifanye kazi, watakapokuja na Mpango waje watueleze nini kinaweza kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nizungumzie katika Sekta ya Uvuvi. Tumepanga kukuza pato la Taifa kutoka asilimia 7 kwenda asilimia 8; pato la mtu mmoja mmoja dola 1,080 mpaka dola 3,000. Kwenye Sekta ya Uvuvi tumesema kwamba inachangia katika pato hili la Taifa kwa asilimia 1.8 tunataka ichangie asilimia tatu. Ukuaji wa sekta tutatoka kutoka asilimia 3.7 mpaka asilimia 3.9. Uzalishaji kutoka tani 497,000 mpaka tani 600,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa uvuvi huu wa bahari kuu hiki kiwango tulichokiweka ni kidogo kutokana na activities zinazotakiwa kufanyika katika uvuvi wa bahari kuu. Kwa hiyo, naiomba Serikali ijaribu kuweka tena haya malengo kwa sababu ukuaji wa asilimia 3.9 tunaweza tukazidi endapo tutatumia fursa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja ambalo sikuliona katika Mpango huu. Katika Sura ya Tano Mpango huu umezungumzia mambo mawili; ununuzi wa meli na ujenzi wa Bandari ya Mbegani lakini uvuvi wa Bahari Kuu una mambo mengi ambapo tukitazama hotuba ya Rais imesema kwamba kutakuwepo na viwanda vya uchakataji wa samaki. Hili tungeliona pale katika ile item ya 13, katika lile jedwali ambalo limeeleza flagship project, lakini hapa tumekosea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu; sekta binafsi ili tuweze kuiwezesha kuingia katika uchumi huu wa uvuvi wa Bahari Kuu ina maana kwamba ni lazima tupime tuna samaki wa kiasi gani. Hata gesi, ili uchimbe gesi unatakiwa ujue kwamba ipo gesi kiasi gani. Tuna ukubwa wa bahari na tunajua ukubwa wa bahari, lakini wingi wa samaki tunauelewa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta binafsi wanahitaji kuelewa wingi wa samaki halafu wao watakwenda kukopa. Wakiandika proposals zao za kutaka maombi ya kupewa fedha ni lazima waeleze viability ya mpango. Viability ya mpango, moja, ni lazima waoneshe cash flow ambayo itakuwa inapatikana kutokana na huo uvuvi wa samaki. Kwa hiyo, ni lazima wingi wa samaki nao utajwe ili kuwapa kigezo hawa wenzetu wa sekta binafsi waweze kukopa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imegonga Mheshimiwa.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyetupa uhai, lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi. Ingelikuwa inaruhusiwa katika Bunge lako, ningelisema kwamba kitendawili na halafu wangeliniitikia tega, mtanikumbuka, mtanikumbuka, hicho ndio kitendawili ninachokipiga. Maana yake mtajua thamani yangu wakati mie mwenyewe sipo na mtanikumbuka kwa mazuri hamtanikumbuka kwa mabaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu mwenye kusema maneno hayo huyo ni mtu ambaye anahesabiwa mwenye maono. Je, hivi sasa hivi hatumkumbuki? Tunamkumbuka. Sasa ili tuone kama huyu mtu ana maono tulinganishe katika historia na watu wenye maono duniani ambao waliishi kwa maono na wakafanya maono. Mwenyezi Mungu alimwambia Musa nenda kwa mja wangu ambaye huyu utamkuta nimempa hekima na elimu, fuatana naye umsikilize atakwambiaje. Musa akaenda akamkuta Hidhri, Hidhri akamwambia tutafuatana, lakini naomba nitakachofanya usiniulize mpaka nitakapokuja kukwambia mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hidhri akakuta Jahazi akaitoboa, Musa akalalamika akasema unatoboa jahazi ambayo wenyewe wanafanyia kazi katika bahari zao, akamwambia nilikwambia usiniulize utajua nini maana yake mwisho. Akakuta kijana, Hidhri akamuua, Musa akasema unaua nafsi? Akamwambia nilikwambia usiniulize, nilikwambia huwezi kusubiri kufuatana na mimi. Akafika Hidhri akaomba chakula mahali wakanyimwa, lakini katika mji ule ulikuwa unajengwa ukuta, baada ya kunyimwa chakula na maji Hidhri akamwambia Musa, tujenge ukuta, Nabii Musa akalalamika akasema khaa! hawa watu jambo waliotufanyia sio zuri, ndio wewe unasema kwamba tuwasaidie? Akamwambia hapa ndio mwisho wetu mimi na wewe, hadha firakun baini wabaina, saunabi-ukabitaawil maalam tastatwii alaihi swabra.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nakwambia maono yangu, ile safina au jahazi niliyoitoboa ilikuwa ya maskini, maskini hawa wakifanya kazi kwenye bahari, lakini mbele kule wanakokwenda kuna mfalme kila jahazi mpya anaichukua yeye, tumeitia aibu ili aiache, hilo ono la kwanza. Kijana tuliyemuua wazazi wake walikuwa ni waumini lakini tulikuwa tunahofia atawaingiza katika shirki, watampenda mtoto zaidi kuliko kumpenda Mungu, kwa hiyo tumetaka kufanya hivyo ili kuona hivyo. Mwisho, ukuta tumejenga ni wa mayatima wawili chini yake kumewekwa hazina.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tulinganishe tunaingia katika madaraka, Rais Dkt. John Pombe Magufuli Hayati, alisema nazuia mikutano ya siasa kwa mtu ambaye aliokuwa hajashinda jimbo wala hana nchi, nazuia mikutano watu wakalalamika, lakini je, haya maendeleo ambayo tumeyapata sasa hivi tumeona reli na miradi yote ambayo imefanyika ingelikuwa tunafanya siasa katikati tungefikia maono haya? Mtanikumbuka, huo ni uono wa kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuangalie katika kubadilisha Sheria za Madini, kuna watu walikaa hapa wakasema tutashtakiwa, ndiyo wale waliokuwa wakilalamika kwamba wanataka waambiwe palepale. Je, sasa hivi hatumiliki rasilimali zetu wenyewe? Tunamiliki, sasa haya ni maono, namzungumzia Dkt. John Pombe Magufuli katika maono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije katika jambo moja ambalo niliseme la kumuenzi Hayati. Walikuwa wakifanya uzalendo, uadilifu na uwajibikaji kwa sababu wanamstahi na kumwogopa Dkt. John Pombe Magufuli Hayati, ameshafariki na hayupo, lakini kama wale ambao waliokuwa wanakuwa wazalendo, waadilifu na wanachapa kazi na wawajibikaji kwa sababu ya mama Tanzania, basi bado mama Tanzania ipo, hiyo ndio njia ya kumuenzi Rais wetu Hayati Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli alikuwa ni mja wa Mungu, hivyo kama kuondoka kwake sisi tutarudi tena tuanze kula rushwa, tutakuwa tena wavivu na wazembe? Atakayefanya hivyo hataidhuru nchi yake, atajidhuru yeye mwenyewe. Kwa hiyo, hiyo ndio njia ya kumuenzi Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujaalia neema hii ya uhai siku ya leo tukapata fursa ya kuchangia katika katika Mpango wa Taifa letu ambao utakuwa ni chachu ya maendeleo na kuweka sawa hali za Maisha za wananchi.

Mheshimiwa Spika, nianze na dhana au dhima ya mpango huu ni kuwa na uchumi shindani lakini pia kuangalia na maendeleo ya watu na maana ya kuwa na uchumi shindani maana yake tunawashindani na kwa kuwa tunawashindani kwa maana hiyo tuna watu ambao pia tunawashindania kwamba hawa wawe wetu.

Mheshimiwa Spika, sasa tukiangalia kwenye maana hiyo Taifa letu sasa kwa kuwa tuna ushindani na uchumi wetu uwe shindani siye tuwe juu tunapaswa kuwa na miundombinu mizuri na kuondosha vikwazo ili hao tunaoshindana nao sasa sisi tuibuke kuwa champion. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano katika sekta ya usafirishaji tunajua tunaanza kuanzia bandarini tunashukuru tumejenga bandari zetu vizuri tumeimarisha lakini kama tunahisi tunavikwazo hivi vikwazo ndivyo vya kupambana navyo ili tuondoshe. Kwasababu katika eneo la bandari majirani zetu wa Kenya ndiyo tunashindana nao kwa bandari ya Mombasa, Msumbiji tunashindana nao kwa bandari yao ya Beirra lakini Durban pia tunashindana nao na hakuna bandari nyingine.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo kama mnataka kujenga uchumi shindani katika sekta ya usafirishaji ina maana kwamba sisi tuwe na bandari bora lakini pia tuwe na mambo mazuri ambayo yataondosha vikwazo watu waweze kuraghibika kupita katika bandari zetu wapiti kwenye mabarabara yetu wapite katika railway zetu wapite na maeneo mengine ili ule usafirishaji uende vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tutizame wateja wetu hawa tunaowasafirishia wako wapi na wapi na sasa hivi katika usafiri wa barabara ukiangalia tunaweka maeneo ambayo ya mizani. Pengine linaweza likasababisha pengine sisi ku-slow down watu wakatukimbia wakaenda katika maeneo mengine. Kwa hiyo, tufikirie tuwe na hikma ya kutizama katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine ni kodi ambazo zinahusiana na usafirishaji tukiweza kuondosha kikwazo hicho kwa hiyo, tutaweza kujenga huo uchumi shindani lakini pia tutapata kuwagharamia watu wetu katika maendeleo yao hilo ni moja.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili niende katika sura inayozungumzia ugharamiaji wa mpango tumesema mpango wetu utagharamiwa kwa trilioni 114 tukaweka Serikali itachangia trilioni 74 na sekta binafsi tukasema itachangia trilioni 40.6. Sasa nije katika upande wa Serikali, Serikali tumesema kwamba tutakuwa tuna mapato ya ndani ambayo ni trilioni 62 katika kuchangia mapato ya ndani sasa mapato haya ya ndani yanachangiwa na mapato ya kodi sasa hapa kwenye mapato ya kodi ambayo yanachangia 65% mapato ya kodi tunaweza tukaja tuka tukaona kwamba kumbe tuna vikwazo kwenye mapato haya ya kodi.

Mheshimiwa Spika, vikwazo vyenyewe ni vipi zipo kesi kule TRA katika Bodi na katika Baraza ambazo zina fedha trilioni lakini kesi zile zimesimama hazijaendeshwa au nyingine zimekaa zimedunda ina maana pale pana mapato ya ndani ya kodi lakini tunayakosa, tukiboresha tukienda kwa wakati tukawa na ufanisi katika mashauri haya ya kodi ina maana kwamba tutaongeza mapato ya kodi na tunaweza kufika vizuri katika mpango wetu huu katika utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ripoti ya CAG ya mwaka 2018/2019 ambayo tuliijadili hapa Bungeni imeelezea kesi ambazo zimekwama kwasababu Bodi haitimizi quorum au hilo Baraza halitimizi quorum na halitimizi quorum kuna mtu ana mamlaka ya uteuzi? Hakuteua huyo mtu hao wajumbe hajawateua. Sasa tukiondosha hivi vikwazo ina maana kwamba hizi fedha tuna uwezo wa kuzipata na tukagharamia miradi yetu wka kupitia mapato ya kodi. Kwa hiyo, Serikali tusikilize katika hili kuna nafasi zinahitaji uteuzi kesi haziendi kwa hiyo kama tutafanya hivyo tutaongeza mapato ya ndani.

Mheshimiwa Spika, pia kuna fedha ambazo zipo katika kesi, kesi ambayo anayeshitakiwa anatakiwa alipe 1/ 3 yake fedha zile zikikwama 1/3 ya yule mtu imekaa pale imeganda hawezi kujiendeleza kuajiri wala kufanya jambo jingine. Lakini 2/3 ya Serikali ambayo kama Serikali itashinda ina maana kwamba pia itakuwa imekosekana kwa hiyo, tunaomba Serikali hili ikalifanyie kazi ili katika kugharamia mpango wetu tuende vizuri.

Mheshimiwa Spika, jingine katika sekta binafsi ambayo inagharamia trilioni 40 mpango uliopita sekta binafsi tulilipa trilioni 48 lakini ikafanya vizuri mpaka kufikia miaka minne katika mpango uliopita sekta binafsi ilikuwa tayari washatumia trilioni 32 kati ya trilioni 48. Kwa maana hiyo ukiweka average kwamba kila mwaka sekta binafsi ina uwezo wa kuchangia trilioni 8. Kwa maana hiyo ndani ya mwaka huu sekta binafsi itakuwa tayari inakamilisha trilioni 40 ingawaje zile 8 kwamba zitakuwa hazikuweza kupatikana.

Sasa safari hii tumeweka blue print, tunaondosha vikwazo lakini bado sekta binafsi tuliweka hii trilioni 40 ina maana hapa ni lazima kuna jambo la kufanya kwa sekta binafsi pamoja na kutumia uwezo huo ambao tumeondosha ina maana ilikuwa sekta binafsi hapa ni lazima tuzidi kwasababu tayari watu watakuwa washashawishika katika kuendelea kutu-support katika miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niiombe Serikali izidi kushirikiana na sekta binafsi ili ugharamiaji wa sekta binafsi ukiongezeka itakuwa vizuri kwasababu Serikali haijaipata ki- percentage sekta binafsi. Sekta binafsi ki-percentage iko juu kuliko Serikali, kwahiyo hilo ilikuwa nalo pia nilikuwa naomba tuliangalie.

Mheshimiwa Spika, jingine ni jambo muhimu sana ambalo kamati ya bajeti imeshauri tuwe na sera ya monitoring and evaluation tuwe na sera hiyo tusipokuwa na sera hiyo ina maana hata sisi hapa Wabunge tutakuja kujadili mwezi wa tano lakini bila kuletewa ripoti ya utekelezaji ambayo ipo sahihi. Kwa mfano kama tukiwa na monitoring tu peke yake tutajua base line tutajua kwamba hapa tunaanza kutokea ngapi kwenda ngapi. Tuna set target zetu tutapata kupima target zetu whether tumeshindwa katika kupata input tutajua kwamba tatizo ilikuwa ni input na input hizo zimeshindikana na kitu gani tunaweza tukabadilisha msimamo katikati kabla ya kufika miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spka, lakini tukisubiri miaka mitano ina maana kwamba tutakuja kupima matokeo makubwa tutashindwa kujikosoa katikati na ndiyo maana mfano tuna miradi hiyo ambayo imetajwa na kamati hapa miradi ya Mchuchuma Liganga Magadi soda kule Engaluka kwasababu haiwezi kufanyiwa hivyo kwasababu kila mwaka inapita vilevile na mpaka sasa hivi ukiuliza utaambiwa kwamba iko katika hatua ya kulipiwa fidia mradi wa miaka 20 uko katika hatua ya kulipiwa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ingelikuwa kunafanyika monitoring wapi tunakwamba tungeweza kutatua vikwazo na sisi Wabunge tungeweza kushauri. Niseme hayo ingawaje na wengine watayasema haya haya kwasababu mtemewa mate na wengi hurowa tunapenda ushauri wetu huo uchukuliwe nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu.

Pia napenda kukushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi ambapo Wabunge wengi sana wamezungumza kuonyesha hisia na kuonyesha kushangazwa na vitendo vya Wabunge wenzetu ambavyo vimetokea na zile comedy zote zilizojitokeza. Nafikiri kuna neno moja tu hapa tukisema, tutaliweka sawa hili. Kuna msemo mmoja unasema Khalif Tunraf; wewe ukitaka ujulikane, upate umaarufu, basi wewe nenda kinyume tu.

Mheshimiwa Spika, kule kwetu kuna mtaa mmoja unaitwa Mchambawima; na ni kwa sababu huyo mtu hicho kitendo alikuwa akikifanya wima, kwa hiyo, alikuwa maarufu mpaka jina la mtaa lipo.

MBUNGE FULANI: Mchambawima! (Makofi/Kicheko)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Eeh, kwa hiyo, hapa sasa hivi, kwa hivi tunavyoendelea, kwa watu kutaka umaarufu, tutapata wachambawima wengi tu, kwa sababu mtu ukitaka upate umaarufu, basi nenda kinyume. Ukienda kinyume utapata umaarufu; na ndicho kinachotafutwa hapa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mamlaka yaliyowekwa yanapaswa yaheshimiwe. Kama tutakwenda hivi kuchezeana na tutaachiana kama hivi, tutakuja kufika mahali pabaya. Amezungumza hapa Mufti wa Kigoma, Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda, kwamba mamlaka anatoa Mungu na Mungu ndio anayempa mtu mamlaka na hakuna mamlaka mengine yeyote ambayo hayatoki kwa Mungu. Sasa akitokea mtu akiwa ana dharau mamlaka, hapo moja kwa moja huyo mtu sio wa kumchezea, wala sio mtu wa kucheza naye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Gwajima ameeleza kwamba Serikali au watu ambao wameshughulika na chanjo wamepewa pesa; huu ni uongo unaoidhalilisha Serikali, unachochea Serikali na wananchi; na kwa nafasi yake kama Mbunge ina maana kwamba moja kwa moja analidhalilisha Bunge kwa sababu yeye amezungumza kama Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi sikubaliani naye anaposema kwamba yupo katika mahubiri, alikuwa hayupo katika mahubiri. Ukitazama mtiririko, leo kimesemwa hiki, siku ya pili yeye ndio anajibu. Leo kimefanywa hiki, siku ya pili anajibu, leo kazungumza Waziri wa Afya, anasema pia atamfyatua. Kazungumza Naibu…; alikuwa anajibu hoja kwa matukio ya Serikali siyo mahubiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukipata wahubiri kama hawa, nafikiri kuna kesi moja. Kuna kisa kimoja cha Askofu Kibwetere aliwafungia watu Kanisani akawachoma. Kuna Askofu mwingine aliwapeleka watu pale uwanja wa ndege, aliwaambia watapata visa pale, wakalala wiki mbili pale. Sasa wahubiri kama hawa wakati mwingine lazima tuwatazame. Itakuja mahali, yaani ni timing bomb. Bomb litakuja kulipuka!

Mheshimiwa Spika, leo katika familia huko watu hawataki kuchanja kwa sababu ya maneno ya watu. Watu hawataki kufuata taratibu za nchi kutokana na maneno ya watu. Sasa mimi niseme moja kwa moja, naunga mkono hoja ya Kamati; na zaidi vyombo vya usalama, hili jambo linatuharibia. Vyombo vya usalama navyo vichukue hatua kali zaidi. Chama chetu nacho kiangalie kifanye nini katika hili kwa sababu hawa watu watatuharibia nchi, nasi hatutaki kufikishwa mahali pabaya. Hapa tunapokwenda, tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija katika suala la ndugu yangu Mheshimiwa Jerry Silaa, ni kweli alikuja mbele ya Kamati, lakini mimi mwenyewe nashangaa kwamba kweli tufikie katika hatua hii Wabunge hatujui kama tunakatwa kodi! Au ndiyo tunarudi kule mchambawima! Halafu unakuja mbele ya Kamati, yaani mambo yote yanakuwa ni ya vituko vituko. sasa hii, nahisi adhabu iliyopendekezwa na Kamati naiunga mkono. Pia huku kwenye PAP nako tukutazame, ndiyo mwakilishi wa aina hiyo ndiyo tunampeleka huko. Sasa ni lazima tutazame na lazima tuangalie. Sisi kama Wabunge tukianza kuchafua hali ya hewa tutafika pabaya. Tupunguzeni kutafuta umaarufu jamani! Tupunguzeni kutafuta umaarufu, hili litatuharibia na tutaiharibu nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja ya Kamati, lakini zichukuliwe hatua nyingine zaidi kwa sababu tunakwenda kuharibu usalama wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Na mimi awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kupata uzima katika siku hii ya leo kuja kuchangia kwenye bajeti hii kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kwanza katika mjadala wangu ambao nataka kuchangia ni ukurasa wa 22 ambao Mheshimiwa Khatib amegusia. Lakini nitagusia katika utoaji wa haki, na hasa katika ujenzi wa mahakama ambazo zinajengwa na utaratibu unaotumika sasa hivi ambao unachangia katika utoaji wa haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na ukurasa huo, nitaunganisha na ukurasa wa 74 mpaka 76 wa hotuba ya Waziri ambapo ameelezea utatuzi wa changamoto za Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza mimi niipongeze Serikali katika kutatua zile changamoto tano za Muungano ambazo zimeelezwa pale, zimefanyiwa kazi, na tunaipongeza na kuishukuru sana Serikali yetu kwa kutatua changamoto hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushiriki wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano katika kuondosha umaskini, kuna Mfuko wa TASAF unatumika vizuri; kuna Mfuko wa Mazingira unatumika vizuri katika pande zote mbili za Muungano. Sasa kwa mujibu wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ambayo ukurasa wa 278, katika kifungu 227(c) ambacho kinasema kwamba tutahakikisha masuala muhimu ya Muungano yanaratibiwa kwa faida ya pande zote mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili nirudi katika ile miradi. Kuna miradi ya utoaji wa haki ambayo inafadhiliwa au ni mkopo kutoka World Bank. Miradi hii inafadhiliwa na World Bank katika upatikanaji wa haki kwa Tanzania nzima. Na miradi hii inahusisha mkataba ambao ulisainiwa na Mheshimiwa Rais wa dola milioni 65 ambazo ni sawa na bilioni 135, kwa ajili ya upatikanaji wa haki. Nachozungumzia hapa kwamba mgao wa Zanzibari mpaka hivi sasa hivi tunazungumza haujapatikana katika fungu hili, hicho ndicho ambacho hoja yangu ya kwanza niliyotaka kuizungumza. Kwenye bilioni 135 Zanzibar haijaenda hata elfu mbili,

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ikumbukwe kwamba Zanzibar sio mwananchama wa World Bank, mwanachama wa World Bank ni Tanzania na Zanzibar anakuwa kupitia Tanzania naye ni mwanachama kwa hiyo anastahili kupata mgao wake kupitia fungu hili. Na hili nilizungumze katika majukumu ya Tume ya Pamoja ya Fedha ambayo katika Katiba ibara ya 133 na 34 inazungumzia kwamba itakuwa na kazi ya kuchunguza kwa wakati wote mfumo na shughuli za fedha za Jamhuri ya Muungano na pia uhusiano katika masuala ya kifedha kati ya Serikali mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hapo mimi ndiyo kwenye hoja yangu ambapo nazungumzia kwamba kuna fungu lilipaswa kwenda Zanzibar kwa ajili ya kufuatilia utoaji wa haki. Kwa hiyo naishauri Serikali ilifanyie kazi hili. Katika hotuba ambayo Rais wetu mama Samia alivyokuwa anawahutubia mawaziri wakati anawaapisha na Katibu Mkuu Kiongozi alizungumzia changamoto hiyo, kwa hiyo tulikuwa tunaomba ipatiwe ufafanuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la pili, tunazungumzia masuala ya uhusiano wa kimpira, football kuna TFF, TFF inatuwakilisha Tanzania nzima, TFF anapopata msaada wa fedha au ruzuku ya fedha kutoka FIFA inapaswa pia na Zanzibar nao wapate. FIFA kila mwaka inatoa dola 1,500,000 kwa ajili ya maendeleo ya soka Tanzania lakini kwa miaka mingi hakuna hata senti tano ambayo imekwenda Zanziba.

Mheshimiwa Naibu Spika, na Zanzibar hawezi kuwa mwanachama wa FIFA kwa sababu Zanzibar hawezi kujiunga na shirikisho lile la kimataifa. Au, kama inawezekana basi kama hizi fedha haziwezi kugawiwa iruhusiwe na Zanzibar ijiunge kwenye haya mashirika; na kama haiwezi kujiunga sheria haikubali basi huu mgao ufanyike.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna mkataba umesainiwa na Korea Kusini pamoja na Falme za Kiarabu, lakini TFF amesaini peke yake, Zanzibar haiwezi kwenda kusaini mkataba huo. Kwa kuwa haiwezi kwenda kusaini mkataba huo, ilikuwa tuiombe Serikali sasa iiambie TFF kama wao wanaweza kwenda FIFA basi labda na Zanzibari iruhusiwe kwenda FIFA, hilo nalizungumiza hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, linguine ni kuhusu ushirikishwaji wa Timu ya Taifa. Kuna jambo jana nililisikiliza sana nikasikitika sana, na hili nilikuwa naomba Wabunge wanisikilize vizuri. Nimesikiliza maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Chama kimoja cha upinzani ambayo anasema yeye anawahutubia Watanzania kwamba Watanzania wamsikilize yeye maneno ambayo anayasema.

Nimeisikiliza hotuba yake kuanzia mwanzo hadi mwisho, Lakini kitu, alichokuwa anazungumza ni kana kwamba Watanzania wote wadai haki ya kuchaguliwa kuwa na mamlaka ya kama labda kuwa Rais au kuwa Wabunge. Hakuongea jambo la kijamii hata moja. Sasa Watanzania hawa hawapo kama hivyo, hakuna haki kama hiyo ya kwamba watanzania wote wanahitaji haki moja tu, watanzania wanahitaji haki nyingi. Miongoni mwa haki ambazo Watanzania wanahitaji ni kupata elimu, kupata maji safi na salama, kupata usafiri, maisha yao yawe mazuri, wapate na mambo mengine, sasa haya yote hajagusia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania hawa hivyo leo wanasomeshwa bure hivyo kweli wakatazame haki moja tu? Watanzania wanazunguka kila nchi, watu wa Dar es Salaam pale safari zao wanakwenda vizuri, hivyo kweli ukawashauri Watanzania kwa matakwa yako wewe kwamba wadai haki hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa mfano, mmoja tukienda kule katika Jimbo la Hai kati ya watu 300,000 waliotaka Ubunge ni wawili tu, kwa hiyo wewe uliyekosa usiwashawishi wengine kwamba hii nchi haikutenda haki. Watu hawa wamepatiwa haki katika elimu, afya, usafiri, pamoja na masuala yao chungu nzima ya kijamii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda tuwapeleke darasani, kuna Abraham Maslow’s hierarchy of needs. Katika hierarchy of need cha kwanza ni basic needs, nicho watu wengi wanachohitaji. Hawa wanaohitaji mahitaji mengine ni wachache, kwa hiyo huwezi kuwashawishi Watanzania katika mahitaji haya machache.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye basic needs kuna elimu, chakula na vitu vingine. Watu wamepatiwa umeme pamoja na mahitaji yao muhimu. Hivi hatuoni umuhimu wa kumuheshimu huyu ambaye aliyefanya hizi huduma za jamii na muhimu zikapatikana?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi maoni yangu kwa Watanzania hawa tuwapuuze na tuwapuuze kama ushuzi wa ngomani, maana ushuzi wa ngomani hata mtu hashughuliki na harufu, tuwapuuze kama ushuzi wa ngomani…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana mheshimiwa.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru kupata nafasi hii kwa ajili ya kuchangia katika Wizara yetu hii adhimu ni Wizara moja ambayo ina umuhimu mkubwa sana katika maisha yetu. Muungano wetu ni zaidi ya hapa ambapo kila mmoja wetu ametaja zile sifa.

Mheshimiwa Spika, nataka nimnukuu mwimbaji mmoja wa kizazi kipya anatokea kule Jang’ombe kwa Alinatu ni mtoto wa Khadija Kopa anaitwa Zuchu alisema kwamba “ladha yake msambaa shira ya kizanzibar” maana sasa hivi tayari… (Makofi)

SPIKA: Hebu iweke vizuri unajua Kiswahili huku bara na hasa Dodoma huku, ebu iweke vizuri tena amesemaje?

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, anasema ladha yake msambaa shira ya kizanzibar, sasa maana yake kwamba tayari katika Muungano huu nikijamii zaidi tumeshachanganyika kiasi ambacho hata kubagua huwezi tena ni sawa sawa na mchanga ambao umeuchanganya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza niishukuru Wizara kwa kutaja haya mafanikio ambayo katika ukurasa wa 15 na 16 tulizungumza hapa mwaka juzi na mwaka jana, kwa kutosainiwa Mkataba wa SAUD BADEA ambao ulikuwa unahusisha shilingi za Kitanzania bilioni 26 kwa ajili ya barabara ya Chake Chake – Wete hivi sasa imeshasainiwa. Lakini pia tunashukuru kwa kusainiwa Mkataba pia wa Ukarabati wa Hospitali ya Mnazi Mmoja hilo nalo pia tunashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kupitia wewe kwanza nikushukuru wewe katika Bunge lako la 11 tulizungumzia hapa juu ya kutoa VAT katika umeme ambao TANESCO anauza kwa ZECO na kusamehewa deni la shilingi bilioni 22.9 na tulilizungumza hapa lakini tunashukuru Rais alilisikia na Mheshimiwa Rais Mungu amrehemu ampe mapokezi mema huko alipo, akasema analifuta deni lile na ile VAT imeondolewa, kwa hiyo, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna neno moja ambalo ninataka niseme haya tunayoyasifu yote hapa leo na tunapata nguvu ya kuyasifu, huko nyuma tulikuwa tukiyataja kama ni changamoto na yalipofanyiwa kazi badala yake ndipo yamegeuka sasa yamekuwa ni sifa na yamekuwa ni ufanisi na yamekuwa mazuri na yanasifiwa kila mahali. Kwa hiyo, na haya ambayo tunayoyataja leo kama ni changamoto isionekane labda tunasema vitu vya ajabu, vitakapopatiwa ufumbuzi tutakuja kukaa katika wakati mwingine tutakuja kusifu kama ni mafanikio ambayo yamepatikana na kwasababu mwanzo tuliyataja kama changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba Wizara ituchukuliwe, mimi ninaelezea changamoto moja, changamoto nayoelezea ni kuhusiana na bei ya umeme, lile jambo tulilozungumza kipindi kile lilikuwa lina component mbili; kulikuwa kuna VAT, lakini pia kulikuwa kuna bei ya umeme. Bei ya umeme ambayo TANESCO anaiuza ZECO ni bei ambayo ipo kubwa, bei ambayo inasababisha ZECO katika ku-pack zile bei za umeme aweze kuwafanyia wale wanaofanya biashara au watu wa viwanda apeleke mzigo mkubwa zaidi kwa kuwanusuru mtu mmoja mmoja au individuals ambao ni raia wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, sasa bei ile inachosababisha; kama mtu ana kiwanda kule Zanzibar mfano kiwanda cha Soda Zanzibar Bottlers, na kama mtu ana kiwanda kule cha kukoboa kwa mfano kama vile Zanzibar Milling anaona bora atumie kiwanda kilichopo Tanzania Bara, na kile cha Zanzibar anakiacha kwasababu umeme analipa bei kubwa.

Mheshimiwa Spika sasa hicho ndicho kinachosababisha Zanzibar alikuwa na deni, pale wakati tunazungumza mwaka jana alikuwa na deni la shilingi bilioni 132, lakini deni hilo alilolikubali Zanzibar ni bilioni 65.7 ambapo hili amelipa bilioni 57.9, sasa limebakia takribani deni la bilioni saba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini deni ambalo Zanzibar hajalikubali ni deni linalotokana na kilowatt Amps ambayo per unit TANESCO anaiuzia ZECO shilingi 16,000 lakini bei waliyokubaliana ni shilingi 8,000 ni double mara mbili zaidi. Kwa hiyo, hapo pana deni zaidi ya bilioni 66, sasa nini wazo langu ambalo ninalosema au maoni yangu au ushauri wangu, hili jambo katika ngazi ya watendaji alitujibu Waziri Mheshimiwa Kalemani mwaka jana kwamba tayari Wizara imekutana wameshazungumza wameshakubaliana lakini lipo katika desk la Muungano.

Mheshimiwa Spika, sasa tulikuwa tunaomba hili lifanyiwe kazi, na lifanyiwe kazi kwenye mambo mangapi? Kwenye mambo haya matatu ambayo ninayasema hapa sasa hivi, lifanyiwe kazi moja; hii bei ya kilowatt amperes ya 16,560 ibaki lilipwe lile lililokuwa la 8,647, ili hili lingine tunaomba lisamehewe. jingine bei ambayo imependekezwa sasa hivi na EWURA ya 157 ambayo ipo isitumike tunaomba bei ambayo ZECO wamependekeza ya kwa unit moja ikiwa ni kilowatts per hour 130 ikitumika bei hii itakuwa kutakuwa huko mbele hakuna mgogoro na hakutazalisha deni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi lingine la tatu kusamehewa kwa hizi Bilioni 66.5 kwasababu zimetokana na bei ambayo imekuwa disputed sasa hicho ndicho ambacho tulichokuja nacho, kwa hiyo hii ni changamoto, changamoto hii inafanya kwamba ZECO asiweze kuendelea kuuza umeme tujue maingira ZECO imeme anavyoununua, anavyoupokea, anavyoupoza, alafu anaupeleka kwa wanachi yeye mwenyewe. Ukimuuzia kwa bei hii ambayo inafanana na ile ambayo mtu anapelekewa moja kwa moja nyumbani kwake au kiwandani kwake itakuwa haiwi-fare price na hapo ndipo kwenye mahusiano yetu na kuna kauli mbiu ambayo imesemwa hapa katika sherehe hii ya Miaka 57 ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwamba Muungano wetu ni msingi imara wa mapinduzi ya kiuchumi kama ni msingi imara ya mapinduzi ya kiuchumi uchumi huu utatokana na viwanda vikifungwa viwanda Zanzibar msingi huo utakuwepo?

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, nashukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante awali ya yote kwanza nishukuru kwa kupata hii nafasi nimshukuru mwenyezi mungu na pia niishukuru Serikali hii inavyokwenda vizuri hasa katika mambo ya nje kwa hiyo ni jambo la kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nataka kuzungumzia mambo matatu katika East Africa na nitaanza kwa msemo unaosema ndege wenye bwawa za rangi moja na mlio mmoja siku zote huwa wanaruka pamoja. Na katika nchi zetu hizi za Afrika Mashariki ni sawa na kusema ni ndege wenye bwana za rangi moja na mlio mmoja basi pia kuna stahiki tuwe tunaruka pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inapotokea kwamba mruko wa pamoja hatuupati, basi ujue hapo kuna ndege ameshabadilika mbawa, mlio na ndege huyo wakati mwingine anaweza tukasema anaweza anastahili kutengwa. Sasa jambo la kwanza ambalo linalozungumza kwanza nipongeze Serikali kwa mahusiano haya mazuri tunayoyaendeleza maana sisi Tanzania ni kinara katika kuendeleza masuala haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru Serikali ya kuendeleza masuala haya tunaishukuru Serikali pale Rais alipotoka kwenda Kenya, tukakubaliana masuala ya biashara, tunaishukuru tena Serikali Rais alipokwenda Uganda, tukakubaliana mambo ya biashara, tunaishukuru tena Serikali Rais aliyepita naye pia alipatana sana na Burundi na tukapanga mipango yetu ya maendeleo katika nchi zetu hizi za East Africa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mawaziri nao wa sekta nao tumewaona kwamba nao wamekwenda wameshirikiana na wenzao na hili ndilo jambo linalotakiwa. Sasa kuna kitu ambacho kinaweza kikaondosha mazingira haya ya biashara. Katika protocal yetu ya East Africa kuna ibara ya 24 ambayo katika article hiyo ya 24 inahitaji kuwa na Kamati ya Biashara; kamati hii ya biashara hata panapotokea matatizo inatakiwa watu wakae na waweze ku-solve disputes zote zinazotokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mpaka hivi sasa mwaka wa 16 hii Ibara haijatekelezwa hakuna kamati iliyoundwa ya biashara na ndio maana leo Tanzania utasema fungia mahindi yasiende Kenya, kesho mahindi yanapelekwa Kenya, Kenya wanasema rudisha, leo tumekaa hatuna mapatano mengine ambayo yaliyokuwa sio ya kikodi kwa sababu hii article haijatekelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niiombe Serikali ili hii article iweze kutekelezwa na kwa mujibu wa ile sheria tokea imetungwa wakati nchi hizi za East Africa zipo tatu peke yake. Ilikuwa kuna Uganda Kenya na Tanzania na ndio maana katika hiyo article kilichozungumzwa humo ni wajumbe tisa, watatu kutoka kila nchi. Sasa hilo ndipo tunaiomba Serikali ikae Waziri wetu wa Mambo ya Nje, Mama yetu unayependeza sana na unapendwa na watu pamoja na kijana wako hapo mwende mkaunde hii kamati, hayo matatizo yote ya biashara kwa sababu hii kamati haipo na huku haya yaliyopangwa mengine ya biashara yakija kuvurugika tunakaa kikao gani cha kuyapanga, maana wameenda kukua Marais, hawa wajumbe wengine walikuwa awaendi na walikuwa hawapo kwa hiyo hilo ni moja..

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili ambalo nataka nizungumzie kuhusiana na hao ndege wenye mbawa moja; katika ukurasa 51 paragraph ya 100 ya hotuba ya Waziri ameongea hapa kuhusiana na kwamba nchi hizi wananchama zilikutana na wakasema kwamba mwanachama anaweza kuendelea na mkataba wa ubia wa uchumi wa EPA. Kwa hiyo nchi zinazotaka ziruhusiwe lakini hilo jambo limefanyika Februari, 2021 Kenya alikwisha jiunga mapema, huyu sijui kama ndege ambaye ana rangi za kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa sababu nchi zote tulikuwa tunaogopa kuja kuondoa protocol yetu hii ya customs union, yeye atakapokuwa anapata bidhaa na anafanya biashara na nchi za Jumuiya ya Ulaya ina maana kwamba tayari kuna mambo yetu ambayo tumekubaliana humu ndani yatakuwa hayaendi sambamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa mujibu wa Ibara ya 37.4 ya Itifaki ya Umoja wa Forodha hapa tunatakiwa wote tuwe kitu kimoja na yeyote anayetaka kujiunga huku basi kwanza atizame yale makubaliano yetu kwamba hayawezi kuharibika. Lakini hapa kuna wenzetu wameshajiunga sisi tunasema kwamba tumekubaliana waruhusiwe kumbe tayari wameshajiunga na ndio maana nilianza na msemo ule msemo wa ndege wenye rangi moja huruka pamoja, lakini sasa inaelekea tuna rangi tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja suala lingine ambalo alilizungumza Mheshimiwa Taska kwamba tunawatuma Wabunge wa Afrika Mashariki, lakini hawawajui wanaenda kufanya kitu gani. Mimi ninachoshauri tuwe na sera sisi Tanzania yakuiendea Afrika Mashariki kama hatuna sera ni kweli wale hatukuwa instrument tutakuja kuwauliza nini, tuliwaambia wakafanye nini, sasa inawezekana wakaja wakaunga kipaumbele cha nchi nyingine kwa sababu sisi wenyewe hatuna sera. (Makofi)

Mheshimiwa Naibi Spika, sera tungekuwa na mkakati, mkakati tungekuwa na malengo ambayo tumejiwekea na vipaumbele vyetu. Kwa hiyo, mimi nashauri tuwe na sera yetu ambao vipaumbele vyetu, vitakuwemo kwenye hii sera na hapa ndipo tutakapokwenda vizuri na tutawajua hawa Wabunge kwa sababu watakuwa tayari wana instrument, watakapokuja kuomba kura aliyekuwa ameenda kinyume na sera na lile ambalo tunalolitaka sisi kama Tanzania basi tuna uwezo wa kumlaumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hapa hatuwezi kuwalaumu kwa sababu hakuna hiyo sera ya Tanzania kuendea East Africa kwa hiyo, naliomba hili nimeomba mambo matatu tukafuate kanuni ya 37(4) haidhuru tunasema kwamba mtu anaweza akaruhusiwa, lakini tuangalie athari zitakazokuja kutokezea kiuchumi na kibiashara, kwa sababu tuna makubaliano ya kibiashara na nchi za East Africa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naliomba hili nimeomba mambo matatu tukafuate kanuni ya 37(4) haidhuru tunasema kwamba mtu anaweza akaruhusiwa lakini tuangalie athari zitakazokuja kutokezea kiuchumii na kibiashara kwa sababu tunamakubaliano na biashara na nchi za East Africa. Na lingine nimeomba kuwepo na sera Waziri atakaposimama hapa kwa nini kwanza hii sera haipo, lakini atuambie lini hii sera itakuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na lingine tunazungumzia kamati ya biashara ya East Africa iwepo, haya yote tunayoenda kukubaliana ikatokezea mizozo hatuna mahali pakwenda tukakaa tuka-solve huo mzozo. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri niombe jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine wamenituma wananchi tena hawa ni wa Jang’ombe, wameondoka wameenda Uganda juzi, wamepimwa vipimo vya corona vingi sana, kwa hiyo, mimi kama Mbunge wao nilisikitika sana na kwa sababu hatuaminiani katika Jumuiya hii ya Afrika Mashariki…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Nashukuru kupata nafasi naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uhai na ametufanya leo hapa tumetokea tupo wazima katika kuangalia mustakabali wa Taifa letu, napenda kukushukuru na wewe kwa kunipa nafasi hii nafasi ya kwanza ili kuweza kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, kuna msemo wa Kiswahili unasema kwamba “penye nia pana njia” na msemo huu penye nia pana njia nimeuona kwa macho yangu katika mwaka 1984, mwaka 1984 wakati ule Mzee Mwinyi anakuja kugombea Urais wa Zanzibar, anakuja kutambulishwa kwamba ni Rais wa Zanzibar basi alizungumza neno moja ambalo mpaka leo linatumika na hakuna mtu ambaye anaweza akalisahau. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipindi hicho tukiweka foleni za makopo kwa ajili ya kupanga foleni ya mchele pengine wiki, wiki mbili mwezi lakini alivyokuja yeye akasema kwamba anachotaka mtu ataweka tui jikoni halafu atakwenda dukani kununua mchele ili aje apike wali wake, kwa maana hiyo limekuja limetoka na limekuja likatokezea mtu anakwenda kuchagua mchele kwa kunusa na tui lipo jikoni au maji yapo jikoni unakwenda dukani. Sasa ni sawa kwakuwa kulikuwa na nia na njia ikapatikana na Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amesema kwamba ataendelea na kazi zote ambazo zilizoanza katika Awamu ya Tano na yeye atazikamilisha katika Awamu hii ya Sita.

Mheshimiwa Spika lakini pia amepanga kuboresha mazingira ya biashara na pia ukusanyaji wa Kodi na Watanzania tunatakiwa tuhamasike ili tuweze kulipa kodi na pia tutoe ushirikiano mzuri kwake maana yake penye nia pana njia na hapo pia tunaweza tukaja tukabaini tukapata tena ule wali nazi kama kwa mzee Mwinyi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu leo nitakwenda fungu Na. 10 lakini pia nitagusia Fungu Na. 7 ambapo kuna usimamizi wa TRA kwa msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Spika, Fungu Na. 10 hili ni Tume ya pamoja ya fedha, katika Tume hii ya pamoja ya fedha Kamati wamesema kwamba imepewa majukumu maalum, jukumu moja ni kufungua hiyo akaunti ya pamoja. Lakini jukumu lingine ambalo kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 134(2)(b) inasema kuchunguza kwa wakati wote mfumo wa shughuli za fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na pia uhusiano katika mambo ya kifedha kati ya Serikali mbili.

Mheshimiwa Spika, ninazungumzia huo mfumo wa ushirikiano wa kifedha kati ya Serikali mbili, na mahali ninapoanzia, naanzia na TRA tunafahamu wote kwamba VAT ni asilimia 18 kwa Tanzania Bara, lakini VAT kwa Zanzibar ni asilimia 15 ina maana kwamba kuna tofauti ya asilimia tatu ya VAT. Sasa tunatumia huduma za pamoja kwa mfano ukifanya muamala wa kibenki unakatwa asilimia 18 ukifanyia kule Zanzibar ulipaswa ukatwe asilimia 15 lakini unakatwa asilimia 18 kwa sababu mifumo inayokusanya ni mifumo ya TRA ndio inayokusanya hayo mapato.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kule Zanzibar zina kwenda asilimia 15 lakini huku alizokatwa mteja ni asilimia 18 sasa mimi nilikuwa ninajiuliza hii asilimia tatu huwa inakwenda wapi? Na mifumo hii ya kifedha kama haitokaa sawa ina maana kwamba moja kwa moja inaweza ikaleta matatizo sasa tokea umeanza mwaka wa fedha uliopita ambao huu tunaomalizia ina maana kwamba kule Zanzibar wamekatwa asilimia 18 lakini zilizopelekwa ZRB ni asilimia 15 sasa nilikuwa ninauliza hii asilimia tatu hizi fedha zimekwenda wapi? Kwa hiyo, nilikuwa ninamuuliza Msajili wa Hazina lakini pia na TRA hizi ni fedha ambazo zipo na hili fungu namba 10 ndilo linaloshughulikia mifumo hii ya pamoja ya kifedha kwa hiyo waje watupe majibu ya hili, na kwa sababu hatutaki liendelee kwa mwaka huu tayari tumeshaliacha limeshakuwa ni mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunaenda huko mbele kule Zanzibar VAT asilimia 15 huku asilimia 18 inayokatwa ni asilimia 18 lakini inayopelekwa ZRB na TRA ni asilimia 15 kwa hiyo, kwanza atueleze asilimia hii tatu inakwenda wapi. Na kingine waje watuambie solution katika hili kwa sababu haliwezi kuachwa likaendelea na wao ndio tuliwapa watutafutie ufumbuzi huo.

Mheshimiwa Spika, kuna jambo jingine baada ya mitandao ya simu kuanza kukatwa katika mwaka 2009 mpaka mwaka 2015 zimekatwa fedha za VAT na exercise duty katika miamala ya simu, fedha hizi ni bilioni 14.7, Bilioni14.7 na pia kuna fedha nyingine ambayo minara yake ipo Zanzibar, minara ipo Zanzibar ambayo Kampuni ya HTT company imetoa fedha imelipa kwa TRA bilioni 1.7 lakini fedha hizi bado zipo TRA.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna VAT tangu mwaka 2011 ya bilioni 11.8 ambazo fedha hizo zinafanya ujumla kuwa ni bilioni 28.1 fedha hizi kwa masikitiko makubwa zipo TRA, ZRB hazikupelekwa. TRA alikusanya kwa niaba ya ZRB kwa hiyo hakuzipeleka. Lakini hazina ilichukua juhudi na ikasema kwamba hizi fedha zirudishwe wakati wa Kamishna Charles Kichele na kule Amour Amir walikubaliana kwamba hizi fedha zitapelekwa.

Mheshimiwa Spika, lakini hizi fedha mpaka sasa hivi tunavyozungumza bado hazijapelekwa, sasa nilikuwa ninajiuliza Hazina tayari mmeshasema kwamba hivi fedha zipelekwe, TRA ana mabawa gani ya kuikatalia Hazina kutopelekwa hizi fedha? Kwa hiyo, nilikuwa niiombe Serikali na kwa kuwa Charles Kichele wakati huo ndio yeye alikuwa anajua hili jambo sasa hivi ni CAG lakini Kamishna aliyekuwepo sasa hivi naye pia anafahamu juu ya hizi fedha kwa hiyo ilikuwa tunaomba hizo fedha zipelekwe.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine lalamiko la TRA kutopeleka hizi fedha wanasema wakati huo ilikuwa hakuna sheria ya marejesho lakini pia wakati huo ilikuwa hakuna fedha za kumshikia mwenzako hakuna sheria ya kumshikia mwenzako fedha kwa hiyo nilikuwa niiombe Serikali ijaribu kuliangalia hili suala na tunaeleza hapa katika fungu namba 10 suala hili pengine kama hatutopata majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri au ya Serikali tunataka pia kuzuia shilingi kutokana na suala hili, kwa sababu haiwezekani TRA ikatae jambo la Hazina na kulifanyika reconciliation kumefanyika auditing kila kitu kilifanyika na kikakamilika na walikubaliana lakini mpaka sasa hivi fedha hazijaenda.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kupitia fungu Na. 10 kupitia fungu Na. 7 wakae hili jambo walishughulikie hili jambo liweze kutatuliwa hasa hili la kodi katika miamala VAT asilimia 18 na 15 hapa kama hatutoweka sawa litaendelea na fedha hizo zitaendelea zitakuja kuwa nyingi tutajiuliza je ni za kampuni ya simu ni za wananchi au ni za ZRB hiyo asilimia tatu. Kwa hiyo, patakuja kuleta utata huko mbele na baadaye itaweza ikazusha sito fahamu lakini kutokana na lengo la hili fungu namba 10 Tume ya pamoja wao wanatakiwa wachunguze kwa wakati wote mfumo wa shughuli za fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mahusiano katika mambo ya kifedha kati ya Serikali hizi mbili kwa hiyo kazi hii ni ya Kikatiba na sisi tunawaambia hilo jambo waende wakalifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutupa uhai leo kuwa wazima tukaja tukajadili mambo yenye maslahi na nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nikushukuru kunipa hii nafasi ili na mimi niweze kuchangia. Katika Ushahidi ambao ninao kwenye Bunge lako hili Tukufu, bajeti hii ya mwaka huu ni bajeti ambayo imeongoza kuwa na maoni ya Wabunge wengi. Tumepitisha bajeti nyingi sana, na kila tukipitisha tulikuwa tuna maombi kama Wabunge, lakini safari hii maombi mengi yamesikilizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yamesikilizwa maombi ya Wabunge wa Bunge lililopita na Wabunge wa Bunge hili la Kumi na Mbili. Kwa hiyo tunaipongeza sana hii bajeti na tunamuombea mama yetu azidi kupiga kazi ili kazi hii aifanye iende kwa wepesi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli bajeti hii imetaja wajibu lakini pia imetaja haki za wananchi. Kuna msemo mmoja unasema kwamba paka kama huli panya Samaki hupewi. Sasa humu ndani ametakiwa paka akamate panya kwanza, ndiyo hizi tozo ambazo zipo kwa ajili ya kuja kufanyia haya maendeleo. Sasa tusilalamike sana kwa sababu hizi tozo ni lazima ziwepo ili mambo yetu yaende vizuri. Kwa hiyo, hilo, kwamba paka asiyekula panya Samaki hapewi, tuendelee kuunga mkono jitihada ambazo zimefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni bajeti ya wananchi. Yameguswa makundi ya watu wengi; wameguswa wafanyabiashara, wameguswa wafanyakazi, wameguswa kwenye hii bajeti hata watu wetu wa bodaboda, wameguswa wanafunzi. Kila mmoja unaona kwamba amepata unafuu ndani ya hii bajeti. Kwa hiyo, hii ni bajeti ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema mwanzo, kwamba hii bajeti imetokana na maoni ya Wabunge wengi sana. Sasa niende kuchangia katika jambo ambalo amelisema Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 31 alipotaja VAT ya bidhaa zinazozalishwa Tanzania Bara zikaenda Zanzibar na bidhaa zinazozalishwa Zanzibar zikaja Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niipongeze sana Serikali kwa hatua hii. Ni jambo ambalo tumelipigia kelele kwa siku nyingi sana, na tulilizungumza, lakini bado haukuonekana umuhimu. Sasa nini inakwenda kutokea; zile biashara za wafanyabiashara wadogowadogo wenye mitaji yao ambao wanakuja kuchukua bidhaa Tanzania Bara, sasa biashara zile zitafunguka na mambo yatakwenda yatakuwa mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na taasisi za kijamii zinakuja kufanya shopping Tanzania Bara, pengine vifaa vya ujenzi; misikiti, makanisa, shule na NGOs nyingine tofautitofauti. Hizo zote zilikuwa zinapata hiyo kero kwa sababu walikuwa wakipigwa double VAT. Sasa imeondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ushauri wangu katika hili; ni kweli tunarudi katika mfumo wa marejesho. Lakini kama tunarudi katika mfumo wa marejesho tufanye utaratibu upi; warejesheane TRA na ZRB, isiingie Hazina katikati. Ikiingia Hazina katikati ucheleweshaji wa marejesho utatokea. Sasa hapo ndipo kwenye ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo nikuombe urudi ule utaratibu wa kurejesheana TRA na ZRB. Tukisema tunapitisha Hazina hapo kikwazo kinaweza kikaja kikatokea tena na baadaye tunaweza tukasema turudi tena katika mfumo wa zero rate. Kwa hiyo hilo nitoe ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu hii tumesema ni nchi ya viwanda. Mheshimiwa Waziri, hili naomba ulisikilize vizuri; ni nchi ya viwanda. Kuna viwanda vya dawa ambavyo vinatengeneza dawa ndani ya hii nchi yetu. Na sisi tuna- import dawa, tuki-import VAT ni zero. Sasa viwanda vyetu vinanunua material (malighafi), wananunua malighafi nje, lakini ile malighafi tunaipiga kodi. Ina maana hawa hatuwaweki katika mazingira mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vifaa mfano vifungashio vya kwenye dawa sisi tuna-import, lakini mle mna kodi Mheshimiwa Waziri. Na kodi inasababishwa kwa hila moja tu; kwamba eti ukileta hicho kitu kiwe kimeshachapishwa huko nje jina la dawa. Sasa ukifika hapa ukitaka kuviosha vile vitu unaviosha vipi? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, hili tunalizungumza hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna material ya kutengenezea dripu, nayo pia yanapigwa kodi. Na kiwanda chetu kitakuwa hakiwezi kushindana, na tujue kwamba tumepewa fursa ya soko la SADC kuuza dawa, SMD. Sasa hii fursa tutaipoteza kwa sababu ya hizi kodi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kifuniko kile cha rubber cha kufungia dawa, nacho pia kinatakiwa kiwe kina jina ndiyo kiwe zero, ukikileta hakika jina ina maana kwamba tayari kinapigwa kodi. Kwa hiyo, viwanda vyetu vitashindwa kuja kushindana na dawa za nje. Ijapokuwa kwamba hatutengenezi dawa zote, lakini tuna lengo la viwanda, kwa kuwa tuna lengo la viwanda hiki kitu tukifanye. Vinginevyo tunaweza tukaja tukashindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze hii bajeti, ni bajeti kweli kwamba kazi iendelee. Ni kweli bajeti kazi iendelee; imegusa miradi yote iliyokuwepo mwanzo na imechukua miradi mingine mipya. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa kufanya bajeti ya aina kama hii ambayo ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, na sisi tunasema kazi itaendelea, na sisi tutaendelea kuiunga mkono. Hii ni bajeti ambayo imetokana na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Yale yaliyosemwa katika ilani tumetakuta leo humu ndani ya bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo maana nikasema katika historia yangu ya kuwa Mbunge, hii ni bajeti ya kwanza ambayo imebeba maoni mengi ya Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Awali ya yote, nami namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kupata uhai na uzima wa kuhudhuria Bunge lako hili Tukufu, leo tunajadili Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2022/2023 ambao utakwenda kuwa bajeti huko mbele kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme kitu kimoja; chanda chema huvishwa pete. Chanda chema huvishwa pete. Nakusudia kwamba anayefanya mazuri, basi ni lazima asifiwe kwa mazuri na ndiyo maana ya chanda chema huvishwa pete. Maana yake pete huwa kama ni tunza. Sasa kwa nini tunasitasita kuyasema yale mazuri ambayo yamefanywa na hii Serikali ya Awamu ya Sita? Kwa nini tunasita? Pete ambayo tutamvisha mama, tunasema mama mitano tena 2025 – 2030. Hiyo ni pete. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa haya mazuri ambayo ameyafanya. Nafikiri kwa Majimbo ya Tanzania Bara katika masuala ya TARURA, walipata kila Jimbo shilingi bilioni 1.5, katika shilingi trilioni 1.3 zimekwenda kwenye madarasa. Wengine wana madarasa 270 na wengine wana madarasa 300. Sasa haya ni maendeleo ambayo ndiyo tunayotarajia. Ndiyo maana tukasema, chanda chema huvishwa pete. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati, sisi Watanzania tuna kawaida ya kuwa na mawazo mgando. Mtu mwenye mawazo mgando kule kwetu sisi huwa tunamwita tozobi. Kwa hiyo, wapo matozobi ambao hawatambui lile jema ambalo linafanywa hata kama analiona. Sasa kwa kuwa akili yake imeganda, mtu kama huyu huwa anaitwa tozobi. Huyo hata awe na jina kubwa vipi, lakini huyo ni tozobi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuepukane na kuwafuata matozobi. Nasi wengine tukawa matozobi kwani huoni kinachofanyika? Huna macho? Au ndiyo bwegenazi? Macho matatu, lakini hakuna jicho hata moja linaloona!

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, amewasilisha vizuri sana. Waheshimiwa Wabunge. ripoti ya Kamati ya Bajeti ni ripoti ya Wabunge wote. Kama utakuwa unazo ziada zako, nawe unaweka pale inputs zako. Ripoti ya Kamati ya Bajeti ni ripoti ya Wabunge. Wewe kama ni Mbunge, ina maana hii ni ripoti yako, unaipingaje? Unaipingaje? Kama una yako, weka, lakini hii imefanyiwa kazi kitafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja niwaambieni Waheshimiwa Wabunge, hii ni ripoti yetu sote. Nina usemi mmoja, wanasema kwamba bubu hutaka kusema mambo yanapomzidia. Nami leo mambo yamenizidi, nataka niseme. Nataka kusema kwenye kilimo. Sijawahi kusemea kilimo, lakini leo naona nisemee kilimo. Nasema kwenye kilimo, namuunga mkono Mheshimiwa Spika Job Ndugai, alisema Bunge hili la Kumi na Mbili liwe ni Bunge la Kilimo. Kwa hiyo, naunga mkono mawazo yote ambayo yametolewa na Wajumbe au Wabunge wa Bunge hili kuhusiana na kilimo, yote waliyoyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naongeza kusema usemi ule ule unaosema kwamba mtemewa mate na wengi, hulowa. Mheshimiwa Waziri, uwekezaji katika Kilimo bado haujatosheleza. Kamati ya Bajeti imeshauri tutenge shilingi bilioni 450 kwa sababu kilimo kinachangia kwenye pato la Taifa kwa asilimia 26.6, lakini hiki kilimo kimeajiri Watanzania asilimia 67. Ina maana kwamba kama tuta-invest zaidi kwenye kilimo, impact ya kukua kwa uchumi itaongezeka zaidi kwa Watanzania wengi na kila mahali tutapagusa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tukiwekeza kwenye kilimo, tukija tuki-set inflation, rate ambayo tunaitaka tutaipata kwa sababu tayari mazao ya kilimo yatapanda bei kubwa. Ina maana kwamba inflation itazidi kwa maana kwamba tuki-control tukiwa tume base kwenye kilimo, tutakuwa tuko vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, faida nyingine ukuaji wa uchumi, kwa kuwa inachangia asilimia 26.6, tuki-invest zaidi ina maana kwamba tutapata ukuaji wa uchumi mkubwa zaidi. Hapo hapo katika mauzo ya nje, kama tutakuwa tumeuza mauzo ya nje mengi katika balance of payment tutakuwa tume-improve. Kwa mauzo ya nje hayo hayo, exchange rate yetu itakuwa stable; katika mauzo hayo hayo ya nje pia kutatusaidia katika masuala mengi. Kwa kuwa GDP itaongezeka, hata kile kipimo cha uhimilivu wa deni la Taifa, kwa sababu itakuwa GDP imeongezeka kuwa kubwa zaidi na deni la Taifa litakuwa halijakua sana, ina maana kwamba tutapata zaidi uhimilivu wa deni la Taifa na itakuwa rahisi kwetu sisi kupata mikopo kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, kiwango cha umasikini kitapungua kwa sababu asilimia hiyo ya kilimo itakayokuwa imeongezeka ni kubwa mno na Watanzania wengi watakuwa wamefaidika. Sasa mimi niseme jambo moja katika vihatarishi kwenye Mpango huu. Naomba hili, kwa kuwa haya ni mapendekezo ya Mpango, naomba hili Waziri alichukue. Kihatarishi tulishaambiwa, tutakuwa tuna mvua chini ya wastani. Kwa kuwa tutakuwa tunamvua chini ya wastani na sisi tulisema kwenye Bunge la Kumi na Moja wakati wa Covid-19, Rais alituhamasisha tulime, tukalima tukapata mavuno mengi. Sasa hivi tumelima huko mahindi mpaka yameshuka bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali iongezee mtaji wa NFRA kwa ajili ya kuhifadhi vyakula hivi. Kuhifadhi vyakula hivi, tutanusurika na balaa ambalo linataka kuja, lakini tutapata na mbegu. Ukipita huu muda wa mvua hizi ambazo ziko finyu, ina maana kwamba tutalima tena. Kwa hiyo, ushauri wangu nauweka kwa Serikali kwamba; kwanza, kutoka shilingi bilioni 234.1 tuweke shilingi bilioni 450, Mheshimiwa Waziri tunalisema hilo wazi. Kwa kuziweka hizo, zikafanye kazi gani? Hizi tukapate pembejeo za kutosha, pia muda sahihi na kwa bei nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine katika hicho kilimo, tukatengeneze mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji. Kingine, zile kodi na tozo kwenye mazao ambazo zinakera, tukiziondoa tutaweza kuweka kama ruzuku, kwa maana hiyo, hayo tutayafikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashauri katika kihatarishi. Kwenye kihatarishi, sisi watu tuliosoma soma vitabu, Mashehe kama sisi, huwa tunajua Nabii Yusuf; Mfalme aliota ndoto akasema kwamba raaitu sababa karatul simani yakul huna sabuna hijaf. Nimeota ng’ombe saba walionona wanawala saba waliokonda. Wasabu sumbulat nhudhuri wa bukharu yabisat. Na mashuke saba mabichi na mengine saba makavu. Kwa hiyo, Mfalme akataka taawil, apewe tafsiri ya ndoto. Nabii Yusuf alimjibu kwamba mtalima miaka saba, itakuwa ya neema, lakini itakuja miaka saba ya njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hifadhini chakula kwa ajili chakula na kingine kwa ajili ya mbegu kwa miaka ambayo mvua zitaanza kunyesha tena. Kwa hiyo, nami natoa ushauri huu kwamba kwa kuwa tumeshatabiriwa kwamba mvua zitakuwa finyu, tuweke chakula, tuhifadhi. Kuhifadhi ina maana kwamba, hifadhi ya chakula cha Tanzania ipewe mtaji kwa ajili ya kuhifadhi. Utakapokuja muda wa njaa, watu watatutegemea; na sasa hivi watu wanatutegemea, tulilizungumza hili mwaka jana 2020. Tumelima kwenye Covid, tukapata mazao mengi, faida yake tuje tuipate hapa sasa hivi. Tumeshaambiwa mvua hazitakuwa sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda nichangie mchango huu wa kilimo katika nchi yangu hii na hilo ndiyo maana nikasema kwamba bubu hutaka kusema mambo yanapomzidia. Limenizidi mwenzenu, leo nasimama mbele yenu, kauli yangu kwenu kuitoa. Kwa hiyo, nami hii kauli kwangu ilikuwa siyo ya kawaida kuzungumzia kilimo, lakini leo imenipasa nizungumzie kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashukuru sana. Tunaiomba Serikali, kwa kuwa haya ni mapendekezo, hebu ajaribu kutazama, tuki-invest kwenye kilimo, tutavuka. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nikupongeze kwa kupata uteuzi huo wa Naibu Spika, nakupongeza sana. Pia tunakupongeza kwa kuwa mgeni juzi siku ya Jumapili pale, na tukaona kwamba ile kutoa mkono wako kama Mgeni rasmi ilisaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite katika hoja moja, nayo ni bandari, Kamati ya Bajeti wameizungumzia Bandari, lakini pia Kamati ya Mitaji ya Umma nao wameisemea. Kwa hiyo, nijikite moja kwa moja katika upakuaji wa mafuta bandarini. Tunafahamu mafuta yanapakuliwa pale bandarini na anayeshughulikia hili pale ni TPDC. Lakini pia kuna PURA naye huwa anasaidia. Sasa, tunapakua mafuta kwa ajili ya nchi tofauti. Yako yanayokwenda Rwanda, Burundi, Malawi pamoja na Congo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa bahati mbaya kuna tozo. TPDC na PURA wanaitoza ZPDC na ZURA tozo ambayo hizi nchi nyingine hawatozwi. Sasa hii tozo imegeuka wakati mwingine inaweza kuwa deni; Sasa nielezee nini athari yake? Athari za tozo hizi ni mbili. Moja, ZPDC na ZURA yaani wanakaa kama watalipa hiki kitu, inamaana kwamba kule Zanzibar bei ya mafuta itakuwa imebaki ileile, lakini TPDC yeye ataandika kama ni deni, lakini litakuwa ni deni hewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na athari nyingine, ZPDC na ZURA walikilipa tozo hii moja kwa moja itakuwa kwamba TPDC na PURA wamepata pesa lakini kule Zanzibar bei ya mafuta itaongezeka. Sasa haya yote mawili yanaweza yakatokea. Ninalizungumzia hili katika muktadha kwamba Serikali iliangalie na walete sheria iliyompa mamlaka hayo TPDC kwamba yeye awe anawatoza kodi watu wote. Kwa hiyo kitu hicho angalau kidogo kitakuwa kimekaa vizuri; kwa hiyo walete sheria hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na tukibadilisha sheria hiyo ina maana kwamba ZPDC na ZURA hawatatozwa tozo na TPDC kwa sababu hawatozi tozo Rwanda, Burundi wala Malawi, na haya mafuta yanapita hapa kama ni transit.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna msemo unasema kwmaba ajizi ni nyumba ya njaa, na chelewa chelewa utamkuta mtoto si wako. Tumelizungumzia hili, Tanzania sasa hivi miundombinu ya upakuaji mizigo ni mizuri, lakini kasoro moja iliyopo ni kwamba hatuna mfumo mmoja kwa taasisi zote zinazoshughulika na pale bandarini. Pale pana TPA, TRA, wako na regulators tofauti ambao wanafika mpaka 12. Hawa regulators mpaka wakimaliza documentation ule mzigo kutoka pale unachelewa, na sisi uchumi wetu tunapitia Bandari ya Dar es Salaam. Tukisema kwamba tunachelewa kutoa mzigo ina maana tunaipunguzia ushindani bandari yetu. Kwa sababu tumezungukwa na bandari nyingine za nchi Jirani, kwa hiyo ili bandari yetu iwe competitive ina maana kwamba tuwe na mfumo mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeeleza kwenye Kamati ya Bajeti kwamba tulikwenda kutembelea bandari ambako walisema kwamba wanatengeneza mfumo wa pamoja. Hata hivyo ni mwaka sasa mfumo huu wa pamoja haujafanya, ndipo nikasema kwamba ajizi ni nyumba ya njaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine, kuna kitu kinaitwa TICTS ambao wameingia mkataba na Serikali juu ya kutoa mizigo pale bandarini. Hata hivyo wakati mwingine kila ukiitazama hii TICS tunaona kama vile kuna vituu kidogo havielekei. Tunaiomba Serikali, TICS wana mkataba ambao wana automatic renew. Kwamba watakapokuwa wametekeleza kigezo fulani mkataba ule unajirudia tena. Lakini bandari sasa hivi inaelekea kujitegemea na inafanya mapinduzi makubwa. Kuwa na TICS pale, na hivi vigezo tunavyompa, akifika kwenye asilimia ile ina maana kwamba bandari haweze kumuingilia TICS.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba Serikali huu mkataba utenguliwe, kwa sababu mkataba huu ni kama umewalenga watu kuwa na maisha yao yote pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwenye mambo matatu. Bajeti, kwa utekelezaji wake kwenye makudanyo, kwenye sheria ya fedha kulisikiliza Buunge, lakini pia katika kupeleka fedha kwenye miradi ya maendeleo kwa zaidi ya asilimia 80.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, naunga mkono hoja zote mbili.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii katika dakika hizi za Aziz Ki. Nami moja kwa moja nitafanya lile lengo la kuweka goli katika uchangiaji wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja katika ugharamiaji wa mpango. Katika hili mara nyingi sana huwa zinatajwa fedha ambazo zitakuwepo katika ugharamiaji wa mpango, na wakati mwingine hutaja vyanzo vya ugharamiaji wa mpango, lakini mara nyingi ule ugharamiaji siyo unaokwenda kutumia fedha zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitaeleza, Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake wakati akitaja bajeti ya 2021/2022 alisema kwamba makusanyo yalikuwa ni asilimia 97 ya mapato, lakini fedha za maendeleo, ukitazama taarifa ya Wizara ya Fedha inaonesha kwamba ni zaidi ya asilimia 85. Sasa ukitazama Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022: Je, ulifikiwa kwa asilimia 85? Huwezi kukuta kwamba ulifikiwa kwa asilimia hizo. Sababu zinazopelekea hivyo ni kitu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi miradi inapopelekewa fedha ambazo tumepitisha kwenye mpango na bajeti, fedha zile zinakwenda kwanza kulipa madeni, claims, interest na variations za miradi. Ukitaka kujua hayo, tutazame percentage ya miradi ambayo labda tunaisema kwenye mpango: Je, kweli tunapokuja kwenye utekelezaji na tunapotoa tathmini inakuwa imefikiwa vile? Inakuwa haikufikiwa hivyo. Sababu ya kutofikiwa ni hizi, kwamba hizi fedha zinaenda kulipwa huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano mmoja. Tulijadili sana hapa kuhusiana na barabara katika bajeti ya 2021/2022, tukaja kugundua kwamba fedha nyingi zilizotengwa kwa ajili ya barabara zilikwenda kulipia madeni kuliko kutengeneza zile barabara zilizotajwa. Kwa kuwa yanatokea hayo, japo kuna msemo kwamba “mpango siyo matumizi,” lakini kwa kuwa Mpango huu tunapanga hapa kwenye Bunge hili, nitoe rai moja. Kwanza, Waziri anapoleta gharama za mpango, anapotaja ile source ya fedha labda kwa mradi fulani fedha hii, basi kile kianzio kiwe ringfenced, na kikiwa ringfenced ina maana hakitaweza kuingiliwa kama zilivyo fedha za REA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, Waziri atakapokuwa anawasilisha labda mradi wa maendeleo, mfano Standard Gauge Railway route ya kutoka Dar es Salaam – Morogoro, anataka kufanya percent ngapi? Ataje baseline na malengo yake ili tukija kutathmini mpango, tukute kwamba fedha zilizotengwa kugharamia huu mpango ziwe zimekwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika dhima ya mpango tutasema ni kujenga uchumi shindani. Mimi nasema ushindani katika usafirishaji. Tuna bandari na tunajenga Standard Gauge Railway. Bandari tunajenga, lakini kuna nchi tunazoshindana nazo; kuna Angola, South Africa, Msumbiji na Kenya. Sisi tuna faida ya kijiografia (geographically advantage), kwamba tunaweza tukapeleka kokote, lakini wenzetu wanatumia mbinu nyingine mbadala katika financing ya mradi wa Standard Gauge Railway. Wenzetu wana-finance mradi wote. Tukitazama nchi nyingine Jirani, wamejenga Standard Gauge Railway, baada ya kuona haitoshi, wanatengeneza mikataba na zile nchi ambazo ni masoko. Wanatengeneza mikataba na Kongo, Zambia, ili kuondoa ile geographical advantage ambayo tunayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasi kama tunataka kujenga uchumi shindani, ni lazima na haya tuyaangalie. Mpango huu utoe jawabu kwamba tunataka kufanya ushindani katika usafirishaji na hawa wenzetu. Kwa mfano, kuna nchi moja ina bandari lakini imeenda kuweka bandari kavu katika nchi nyingine, ambapo nasi katika nchi ile ni soko letu, watu wataenda kuchukulia bidhaa pale. Kwa hiyo, tunataka mpango huu katika usafirishaji hasa kupitia bandari na reli itoe jawabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nije kwenye umeme wa REA. Kuna takwimu ambazo bado sijazielewa. Tulisema tunafanya vijiji 12,000. Tukatoa ripoti 2021/2022 kwamba vijiji 10,000 tayari vimeshafanyiwa. Ila kwenye mpango vimeelezwa vijiji 8,000 ndivyo vilivyofanyiwa, siyo 10,000 tena. Maelezo ya Waziri yanasema vijiji 9,000. Je, tushike kauli ipi hapa? Kwa maana hiyo kama vilifanyika vijiji 10,000, leo tumerudi vijiji 8,000, ina maana bado vijiji 4,000, na Waziri amesema vijiji 9,000. Ina maana bado vijiji 3,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaonesha kitu gani? Kitu kinachooneshwa katika tofauti ndani ya Serikali, ina maana kwamba inawezekana vijiji vile tayari vimeshafanyiwa kazi, lakini pengine kwa sisi tunaofikiria kwamba ile gharama yake watu wanataka kuja kuirudisha ipate kutumika visivyo; au kule mwanzo tulipotajiwa vijiji 10,000, ina maana zile fedha hazikutumika kweli kwenye vijiji 10,000 na fedha zile labda badala yake zilifanyiwa vitu ambavyo siyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali itupe takwimu sahihi katika miradi ya REA. Kuna takwimu tatu tofauti; kuna 10,000, 9,000 na 8,000, ni ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nashukuru sana kupata nafasi hii. Nianze na msemo, watu wengi sana huu msemo tulikuwa hatuujui, lakini leo mimi nitautolea maana. Kuna msemo unasema heri ya nusu shari kuliko shari kamili.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa natafakari sana juu ya msemo huu, lakini jana nilipata maana yake na alichonifundisha maana msemo huu ni mzee Msekwa aliposema kumbe kulikuwa kuna changamoto kubwa zaidi ya kiusalama kule Zanzibar baada ya Mapinduzi, kwa maana hiyo kulihofiwa kuja kuvamiwa tena na kupinduliwa kwa sababu ilikuwa haina Jeshi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hii ilikuwa ni shari kamili, lakini nusu shari ndiyo kama haya mambo madogo madogo ambayo tunayazungumza, ni mambo ambayo yanaweza yakarekebishika. Kwa maana hiyo ile shari kamili tumeepukana nayo, lakini sasa hizi nusu shari zinaweza zikaondoka kirahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba Muungano wetu huu ni Muungano mzuri sana kwa sababu katika miungano yote ya katika dunia hawana chombo cha kukaa wakazungumza mambo yao, lakini sisi kwenye Muungano wetu huu tunacho chombo ambacho ndiyo hiki cha Mheshimiwa Jafo hapa tunamwambia ambacho tunakaa tunaeleza matatizo na changamoto ambazo zimo katika Muungano na ndipo zinakuja zinatatuliwa changamoto hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna aya moja inasema kule kwenye Quran kwamba wanasema kulaukana fil-ardhi malaikatu yamshuna mutumainina laa-nazzalna minasamaai malaka rasula. Ingelikuwa malaika ndiyo wanaoishi kwenye ardhi basi na mitume yao ingekuwa ya kimalaika lakini wanaoishi kwenye ardhi ni binadamu na mitume yao itakuwa ni binadamu. Hii Serikali inaongozwa na wanadamu na ni watu na sisi ni wanaadamu, kwa maana hiyo tunapaswa tuiambie Serikali yetu kuwa kile ambacho kinatutaka. Kwa hiyo tuiambie Serikali ili kuondosha zile changamoto isitoshe na sisi wenyewe ni ndugu, kwa kuwa ni ndugu kwa hiyo tutakapoambizana tutasikilizana zaidi.

Mheshimiwa Spika, sasa na mimi Mheshimiwa Jafo nisikilize jambo moja, kuna makampuni ambayo yamesajiliwa Tanzania Bara yanafanya kazi Zanzibar na kuna makampuni yamesajiliwa Zanzibar yanafanya kazi Tanzania Bara, lakini kampuni zile zilizosajiliwa Tanzania Bara zinafanya kazi Zanzibar hazilipi kodi ya mapato yaani (Cooperate Tax) na kwa sababu Companies Act ya Tanzania Bara inataka mtu alipe Tax Headquarter, kwa hiyo zile Cooperate Tax hazilipwi kule na zile kampuni kule zipo ukichukulia kampuni zote za simu ziko kule, ukichukulia kama benki mengi yako kule, ukichukulia makampuni ya ujenzi yako kule, hayalipi na kule wana-operate under certificate of compliance. Sasa ushauri wangu kule alitoka Waziri mmoja wa Zanzibar alisema hivi kwamba kampuni zinazotoka Tanzania Bara zikajisajili tena Zanzibar, hicho kitu ina maana kwamba hawa ndugu zenu wanakuiteni mwingine katika mazungumzo juu ya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaomba na hili jambo la kuhusiana na mambo ya Cooperate Tax, kwa sababu tunajua Ibara ya nne iliyotaja kutakuwa na mambo ya Muungano kwenye nyongeza ya kwanza item (10) imetaja hiyo kodi ya mapato kwa watu binafsi na makampuni. Hata hivyo, kulipita makubaliano kwamba kila mmoja atakuwa anakusanya kodi hiyo ya mapato sehemu yake, lakini makampuni yale yanafanya kazi kule, lakini yanalipa kodi ya mapato Tanzania Bara, kwa maana hiyo Zanzibar pamoja na kuwahudumia wananchi ambao ni wateja wa makapuni yale kwamba inakuwa haipokei kodi kutoka makampuni yale hakuna NMB, hakuna CRDB, hakuna TCB, hakuna NBC, hakuna hizo TIGO, hizo zote hazilipi kodi ya mapato kule Zanzibar na zinafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili tunaliomba hili lifanyike, kikae kikao maalum hili lifanyike na Muungano huu ninavyosema tumeungana sisi ni zaidi ya haya mambo ambayo yameandikwa. Wizara ya Kilimo siyo ya Muungano lakini nenda katazame katika masoko ya Zanzibar, sisi tunaita mbatata hivi viazi mviringo utakuta kule maharage, utakuta kule kila kitu, hutokuta kule mchele labda umeandikwa huu wa Cheju, lakini mchele wa Mbeya kule utaukuta. Kwa maana hiyo tumeungana zaidi na Muungano wetu siyo wa mambo ambayo yako kwenye makaratasi, Muungano wetu ni wa mambo ambayo tumeungana kwa damu na kiudugu zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naunga mkono hoja Mheshimiwa akatutekelezee mambo yetu hayo. Nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru sana kupata nafasi ya kuweza kuchangia na mimi nataka moja kwa moja nijielekeze katika Jimbo langu la Jang’ombe maana nisije nikaja nikageuka Ngariba wa Kilwa kama msemo wa Kiswahili unavyosema. Maana Ngariba wa Kilwa aliwatahiri wenzake wote halafu yeye akajisahau, sasa mimi naanza na Jang’ombe ambapo naanza Ziwani Polisi.

Mheshimiwa Spika, pale Ziwani Polisi tuna Kituo cha Afya kile kituo cha afya, sasa hivi tumefungua maternity lakini tulipata shida moja hapa Mheshimiwa Waziri nisikilize vizuri. Tulipata shida moja ambulance ikawa hakuna lakini kuna ahadi ya mtu wa juu yako ameahidi hii ambulance. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri utakaposimama hapa useme kwamba utanifikishia hizi salamu. Pia kukashindikana generator katika maternity ile kwa sababu sheria ni lazima kwamba uwe na hiyo automatic generator, Mbunge na mwakilishi wa Jimbo hilo la Jang’ombe tumesema hivi asilimia 50 ya generator hiyo bei yake tutatoa sisi, Mheshimiwa Waziri uje unijibu kama utatuambia kwamba na wewe asilimia 50 utatuletea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ziwani polisi kuna Bwalo lile banda la Brass Band lile pale linavuja watu ndiyo wanapofanya mikutano pale, kwa hiyo tulipokwenda kuwatembelea safari hii tulikuta kidogo hakuko vizuri Mbunge na Mwakilishi tutatoa asilimia 50 Mheshimiwa Waziri njoo uniambie na wewe utatoa ngapi ili tuweze kufanya vitu hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Masheha wangu wamenituma nitoe shukrani kwa Jeshi la Polisi, nitoe shukrani kwa jambo moja kwamba tumepelekewa Wakaguzi Wasaidizi ndiyo Maaskari Shehia, pale sasa hivi uhalifu mambo ya udhalilishaji na mambo ya madawa ya kulevya yataondoka kwa haraka kwa sababu tunafahamu Assistant Inspectors wanakuwa na maamuzi. Kwa kuwa wana maamuzi kwa maana hiyo kila kitu kitafanyika kwa haraka, kwa hiyo tunalipongeza sana Jeshi la Polisi kupitia Mkuu wake Kamanda Sirro wamefanya vizuri sana katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtemewa mate na wengi hulowa, wengi wamezungumzia masuala ya Magereza hasa msongamano. Ninazungumzia msongamano huo katika upande mmoja, kwamba tuna wageni tunawapokea tunawaweka, tunawalisha wanamaliza vifungo vyao hatuwatoi, namshukuru ndugu yangu Jumanne Sagini Naibu Waziri, tulilifuatilia hili ili liishe lakini halijamalizika kwa sababu linahusiana na Magereza, linahusiana na Uhamiaji linahusiana na Wizara ya Mambo ya Nje, wako wafungwa kutoka Ethiopia washamaliza vifungo, hawa haina haja ya kubakia hapa tukawahudumia ilitakiwa waondoke. Hili ninalisema kwa sababu mimi mwenyewe ni Mjelajela nimeacha kule nina cheo cha superintendent, sijajitangaza tu huko zamani lakini na mimi mngeniita mstaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili nalisema kwa sababu mimi mwenyewe ni mjela jela nimeacha kule nina cheo cha super intendent, kwa hiyo sijajitangaza tu huko zamani, lakini na mimi mngeniita mstaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hili tunalielewa vizuri, huo msongamano huko unaosemwa, wengine hakuna hata haja ya kubakia ndani ya Magereza, kwa hiyo hili tunaomba lipatiwe ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine maslahi kwa askari wa Polisi. Kilitokea kisa hapa kimoja cha yule kijana Hamza na tuliwaona askari wetu walivyokuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu. Kwa hiyo hii posho ya mazingira magumu Mama atakapotikisha hiki kichupa cha tumbaku, tunaomba awaangalie hawa askari wetu, kwa sababu pale raia wote waliingia mitini, lakini wote tumeona ile video, askari anavyomwinda mhalifu amejitolea, kwa maana hiyo, angeweza kupigwa yeye au akapiga yeye kama alivyopiga. Sasa askari wetu hawa wanafanya kazi katika mazingira magumu, kwa hiyo tunawaombea waongezewe posho ya mazingira magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, awali ya yote kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutujalia leo kuja kukaa hapa kujadili bajeti ya kuendesha nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nakushukuru wewe kwa kunipa nafasi. Kuna mambo hapa yalisemwa na wengi walizungumza toka tumeanza Bunge hili kuhusu Ripoti ya CAG. Sitozungumza, ila nina shairi dogo ambalo lilitungwa na Haji Gora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Haji Gora alisema kwamba;

Kuna la ajabu mno la kushanagaza moyoni,
Kuna wakongwe watano wanashindana kwa fani, Wakata mawe kwa meno na kujaza matumboni, Nasema kinaganaga mengine yasikieni,
Farasi kula mizoga na kufukua mavani?
Kuna kijungu cha kuaga bila moto jikoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye agenda hiyo nimemaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nakuja katika agenda na mchango wangu wa Fungu 65 – Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu. Hapa nazungumzia vijana na ajira. Tatizo la ajira ni kubwa kwa dunia nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa Mwalimu tatizo la ajira lilikuwepo, wakati wa mzee Mwinyi tatizo la ajira lilikuwepo, wakati wa Benjamin Mkapa tatizo la ajira lilikuwepo, wakati wa Jakaya Kikwete tatizo la ajira lilikuwepo, wakati wa Magufuli tatizo la ajira lilikuwepo na sasa wakati wa mama Samia tatizo la ajira bado lipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Serikali yetu tukufu ilifanya utafiti na utafiti huo iliufanya kuangalia nguvukazi ya nchi ambapo tuna nguvukazi ya watu 23,536,000 na zaidi. Lakini ilivyofanya hapo iliangalia hali halisi ya soko la ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti hiyo ilionesha kwamba asilimia takribani 80 ya nguvukazi ya Tanzania ujuzi wao uko chini; asilimia 16.6 ya nguvukazi ya Tanzania ujuzi wao ni wa kiwango cha kati; asilimia 3.6 ujuzi wao ni wa kiwango cha juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi kwa kuwa ni nchi ya kiwango cha kati tulitakiwa asilimia ya kiwango cha juu iwe asilimia 12; asilimia 34 iwe ya kiwango cha kati na asilimia ya kiwango cha chini iwe 54 kwa kuwa tupo katika uchumi wa kiwango cha kati. Hii ilifanya ndiyo chimbuko la kuwa na programu ya kukuza ujuzi kwa ajili ya kupata ajira. Kwa bahati tukaweka hiyo programu, programu hiyo na components zake za kukuza ujuzi zikatajwa na iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walikubaliana sekta binafsi na Serikali kwamba programu hii ambao ni Mradi Namba 6581 itasimamiwa na SDL (Skills Development Levy), kwamba one- third itatoka itakwenda kushughulikia tatizo la kukuza ujuzi kwa vijana. Na kukuza ujuzi kwa vijana maana yake tutapata tija kwenye bidhaa zetu na ajira zitazalishwa kwa wingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Skills Development Levy iliyokusanywa kwa mwaka 2021/2022 ilikuwa bilioni 291, ambayo one-third yake ilikuwa bilioni 97, lakini kwa bahati utekelezaji wa programu hii ulivyokwenda, ilianza kuchangiwa kwa bilioni 15, tukaja bilioni 18 na sasa hivi tumeshuka tuko katika bilioni tisa. Tunajiuliza, je, tatizo la ajira kwa vijana liliisha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilikuwa nataka niseme neno; na ninataka nitoe rai; Mwenyezi Mungu anasema kwenye Quran Tukufu fama amali Musa illa dhuriyya. Musa hajaaminiwa isipokuwa walibakia vijana watupu ndio waliomuamini Musa na niyo waliomfuata Musa. Lakini wazee wote waliogopa kwa sababu ya kumuogopa firauni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hawa vijana ambao sisi tunaanza kuwashushia hata hiyo pesa kwa ajili ya wao kupata ajira na kukuza ujuzi, tutakimbilia wapi? Serikali lazima itazame katika hili. SDL inatakiwa ipelekwe bilioni 97, sasa kama bilioni 97 haikupelekwa, je, hawa vijana tunawapeleka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo langu; SDL kama haijatoka kwa kiwango cha kutosha kama tulivyosema huku katika makubaliano, kwamba one-third ya SDL iende kwa ajili ya ajira na mafunzo kwa vijana ili kukuza ujuzi, hapa nina lengo la kuzuia shilingi kwa sababu vijana ni tatizo kubwa. Leo tutazame matatizo yote lakini bomu kubwa ni vijana. Sasa kama hatujawaangalia vijana tutaangalia kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema kukuza ujuzi kwa vijana, kama hawajakuziwa ujuzi wao ina maana kwamba bidhaa zetu na vijana tatizo hatutoweza kulipatia ufumbuzi. Hii naomba tuweke kwenye Hansard, nakuja kuzuia shilingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumza Mheshimiwa Mwijage kwamba kuna wazee ambao wamestaafu pensheni zao ni ndogo, malalamiko yao ni kwamba ile sheria iliyotungwa haifuatwi. Na maombi yao wanasema Serikali iunde Task Force kwa ajili ya kufuatilia tatizo la pensheni zao. Na wanaomba hii sheria basi, kwa zile changamoto zao, ikifuatwa hii sheria watakuwa wako sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika Jimbo langu la Jong’ombe. Niliahidiwa kupata skuli pale katika Shehia ya Kwalilatu kupitia TASAF. Lakini mpaka sasa hivi tunakwenda kumaliza bajeti hatujaona. Wananchi wamepita wamehojiwa, taratibu zimefanyika. Nilizungumza na Mheshimiwa Jenista wakati ule alisema atakuja yeye mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali katika kipindi hiki ambacho kimebaki kwa kuwa jambo lilikuwepo katika mchakato, tunaomba tumalizie hili jambo ili kuweza kuwa-accommodate na kufanya lile jambo. Na mimi jamani mwenzenu nahitaji kura za kutoka kwa wananchi ili niweze kuja hapa. Kwa hiyo, jambo moja katika jimbo langu ni jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuzungumzia agenda yangu muhimu ile ya kwanza ya vijana. Endapo Serikali haitofanya, haito-ringfence watuambie mbinu gani watatumia, wata-ringfence lakini fedha at least zipatikane bilioni 36, vinginevyo Waheshimiwa Wabunge hakuna mtu ambaye hana tatizo la ajira katika jimbo lake. Tunafuatwa na wananchi. Nitaomba mje mniunge mkono wakati huo kwa sababu ya kuwasemea hawa vijana. Kama siyo hivyo ina maana kwamba tutawatelekeza vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa vijana wakiamua kufuata njia nyingine tutawafanya nini? Na ukimuona kijana kapata kitu sehemu nyingine mtakuja kusema vijana wanaharibika, lakini itakuwa kuharibika kwenu, kwa wenzenu watakuwa wametengemaa maana watakuwa wanawatumia wao. Sasa ili tuwatumie vijana wetu tuwajali katika ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Lakini pamoja na yote nitakuja kuzuia shilingi katika suala hili la SDL. Naunga mkono hoja; nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. ALLY HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutujaalia siku ya leo uzima kuja kujadili mambo yanayohusiana na bajeti ya Wizara hii ambayo inahusika zaidi na watu.

Mheshimiwa Spika, kwanza mimi nilikuwa niwaambie Waheshimiwa Wabunge wenzangu ambao waliotangulia hapa kuzungumza, naona hii group hii ya wanaume imeandamwa sana. Maana katika group hii members wengi kwanza walishame–left, sasa bado inakamatwa kwamba wapewe pombe wazidi kuleftishwa (to left) wengine watabakia wangapi? Members wengi walisha-left katika hili group jamani. Msiwe na wasiwasi sana kuna visukari huko mtaani.

Mheshimiwa Spika, mimi kwanza niipongeze sana Serikali na nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais katika makundi maalumu, hasa kwa kuwajali kundi hili ambalo linaloitwa wamachinga. Tumeanzisha sub vote ya wamachinga kwa ajili ya maendeleo ya wafanya biashara ndogondogo ambao tunaamini kwamba kwenye sub vote hii itakwenda kuwasaidia. Lakini pamoja na pongezi hizi za kuanzisha sub vote hii, mwaka uliopita tumepeleka bilioni 22 kwenye msimu huu ambao tunaumaliza, na safari hii tunapeleka bilioni 20 nyingine kwa ajili ya wamachinga. Kwa hiyo hii mimi ninawapongeza sana Serikali kwa kuliona kundi hili, hapo pokeeni pongezi Serikali.

Mheshimiwa Spika, katika wamachinga Mheshimiwa Waziri alieleza katika hotuba yake, anasema kwamba Wizara inakamilisha utaratibu wa kuzipokea bilioni 22. Sasa mimi najiuliza, kwa nini hapakuwa na uwazi katika fedha hizi za wamachinga, hizi bilioni 22? Mheshimiwa Waziri anajiandaa kuzipokea, fedha ambazo zilivyokuja zilikuja kama mkopo wa ECF. Mheshimiwa Mwigulu alituambia katika hotuba yake ya bajeti ya mwaka 2022/2023, alisema hivi, kwenye paragraph ya 81, kwamba Serikali inatarajia kupokea fedha trilioni 2.5 ambayo kwa miezi 40. Lakini kwa bahati katika paragraph ya 85 ya Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti kuu 2022/2023 alisema kwamba bilioni 45 zitakwenda kuratibu mambo ya machinga pamoja na kupatiwa mikopo wamachinga waliojipanga vizuri.

Mheshimiwa Spika, sasa hotuba hii moja kwa moja ilipofika tarehe 18 Julai 2022, IMF wame-release hizo fedha kuja hapa Tanzania Julai 2022. Bunge lako kupitia Kamati zake likakaa, na lilivyokaa likapokea fedha hizi Kwenda kwenye sekta tofauti tofauti. Zimekwenda kwenye umeme, kilimo, mifugo, TASAF na nyingine hizi bilioni 22 ndizo zilikuwa zinakuja kwa wamachinga.

Mheshimiwa Spika, jambo la kushangaza ni kwamba hizo zote zimeonekana katika kitabu kikubwa hiki cha bajeti katika approved estimate, lakini hizi za wamachinga hazijaonekana. Sasa mimi najiuliza, kwa nini fedha hizi za wamachinga peke yake zisionekane? Fedha hizi bilioni 22 ukiziwekeza katika Benki ya Azania kwenye fixed deposit kwa miezi 11 unapata faida ya bilioni 2.3. Fedha hizi endapo mzingelikopeshwa kwa wakati kwa wamachinga, kwa sababu zinaitwa revolving, kwa hiyo zingelikuwa zinarudishwa anaanza kukopeshwa wengine.

Mheshimiwa Spika, lakini fedha hizi za wamachinga zingekuwa zimetolewa hiyo athari tunayoisikia huko Kariakoo kwamba kuna wamachinga wanachajiwa (be charged) ushuru wa store lengo lake ilikuwa wale wanaopewa bidhaa mkononi ili waweze na wao kwamba ziwe zimeshalipiwa kodi. Hii ni kwa sababu wanafanyabiashara wakubwa wanatumia ujanja kuwapa wale wadogo wadogo ambao wametandika vi-busati pale mbele na wanaokamata mkononi. Kwa hiyo athari hii nayo pia ingepungua.

Mheshimiwa Spika, cha kushangaza fedha hizi ziliingia mapema sio bajeti inayosubiriwa kukusanywa. Na malengo yake yalikuwa ndiyo hayo. Sasa najiuliza kwa nini kwamba sasa hivi ndio unafanyaika utaratibu. Mwezi wa 11 huu ndio unafanyika utaratibu wa kupokea hizo fedha. Utaratibu huo unafanyika sasa hivi, Serikali ilikuwa wapi muda wote huo? Maana ingelikuwa mimi ningeenda kuweka kwenye fixed deposit nikapata faida. Tunaambiwa sasa hivi, lakini fedha hizi zilikuja tokea mwezi wa saba, na kamati zako hizi ndizo zilizohusika kuzipokea fedha hizi za wamachinga.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nilikuwa naiuliza Serikali, kwa nini fedha hizi hapakuwa na uwazi? Kwa nini kwenye REA zimekwenda bilioni 100? Kwa nini TANESCO zimekwenda bilioni 100? Kwa nini kwenye kilimo zimekwenda? Kwa nini kwenye mifugo zimekwenda? Hizi zilikosa nini? Na fedha hizi zilipokelewa milioni 151.7 Dola za Kimarekani, na zilikuja mwezi wa Saba na zilifanyiwa utaratibu zikaenda kwenye vote hizo. Sasa mimi najiuliza hapa Serikali kwa nini wametufanyia kitu cha aina hii?

Mheshimiwa Spika, wanasema kwamba account haijafunguliwa kwa ajili ya kuwakopesha wamachinga, si kweli. Bilioni 6.8 zilikuwa zinahusika na other charges ambazo ni kuratibu, lakini milioni 680 zilikuwa zinahusika na ujenzi wa ofisi za wamachinga kwa kila mkoa ambazo zimo mule; na hizi Mheshimiwa Rais amepita akizisema anapokutana na wananchi, kwamba atajenga ofisi za wamachinga kila mkoa. Sasa huku uratibu gani unaotakiwa? Bilioni 15.5 ndizo zilikuwa ziwe revolving fund, na tarehe 7 Oktoba. Serikali ilileta kwenye Bunge lako hili kwamba tarahe 7 Oktoba, 2022 kwamba imeleta mchanganuo wa fedha hizi jinsi zitakavyotumika, na hiyo barua imekwenda Wizara ya Fedha na Wizara ya Fedha imekuja nayo Pamoja na Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na makundi maalum. Sasa nashangaa fedha hizo zinatafutiwa utaratibu sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, hapa tunachezewa. Bunge hili tulipokea ceiling, Bunge hili tumepitisha bajeti. Ilitakiwa kuwe kuna media report. Media report ilisemaje? Kwa nini fedha hizi zisiingizwe? Media review kwa nini Bunge lako lisielezwe? Yaani tusijue, tunakuja kuja sasa hivi. Hata hiyo randama ambayo iko hapa sasa hivi ni kwa sababu ya mabadiliko, kwamba Serikali inataka kuji-defend. Sasa hizi fedha zimetumika lazima itakuwa ziko pahala ambako zimekaa.

Mheshimiwa Spika, mimi lengo langu, endapo Serikali haitakuwa na maelezo mazuri juu ya uwazi wa fedha hizi kama Bunge linavuyotaka na sheria ya bajeti inavyosema mimi naweza nikaja nikazuia shilingi ili Serikali itueleze tu; kwa sababu Hapana uwazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ambalo nilizungumze, katika makundi maalumu kuna kundi la wazee pale Zanzibar. Wazee ambao hawakuwa katika mfumo rasmi wa ajira wanapata pension, inayoitwa pension kwa wote. Kwa nini kwenye uchumi mkubwa kama huu wa Tanzania hatuwezi kuratibu hicho kitu cha pension kwa wote? Tuweke pension kwa wote. Hawa wazee ndio walioshughulika kututafutia sisi uhuru, lakini wengine kazi yao walikuwa wakulima, wengine wafugaji, lakini walizalisha. Tukumbuke kwenye vita vya Uganda vita vya mpakani vile watu walitoa mali zao ambao walikuwa si waajiriwa hawa na hii nchi imekuwa salama. Sasa niiombe Serikali au niishauri Serikali, tutengeneze huu mfumo wa pension kwa wote tuwasitiri wazee wetu. Hawa wazee wametulea tusiache wakaanza kupita wakaombaomba huko. Wakianza kuomba omba ni aibu na fedheha kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, nitaunga mkono hii hoja Serikali itakapotupa uwazi pamoja na sheria, kwa sababu kifungu namba 65 cha sheria ya bajeti utakapofanya uzembe kama huu kuna vitu pale vimetajwa.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kwanza, namshukuru Mwenyezi Mungu kunipa hii nafasi na uwezo wa kusimama hapa, lakini pamoja na wewe kunipa nafasi hii kusimama hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ilikuwa nizungumze kidogo kwa rafiki yangu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu hapa, naona leo alikuwa yuko doro doro kwa sababu jana Yanga ilitoka draw halafu Simba kashinda saba, ndiyo maana alikuwa yuko mnyonge mnyonge, ule ndio unyonge wake. Lakini sasa mimi nataka nimtoe unyonge na ninataka achangamke kutokana na haya ambayo nayaeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye paragraph ya 36 katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameelezea pale huduma za pensheni na mafao ya watumishi ambapo kwenye randama tumekwenda kuangalia katika Fungu 23 ambayo ni Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye pensheni mimi nina hoja mbili, ya kwanza, wazee ambao walishastaafu wanapata taabu kupata pensheni zao na kupata viinua mgongo vyao, hususan wa kutoka Zanzibar. Hawa wa kutoka Zanzibar ni lazima wafunge safari waje zao Dodoma ili kuja kufwata mafao yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo wanakwenda, wanarudi mafao yale hawayapati, mwisho kinachotokea wanafanya maamuzi ya kusamehe. Kwa maana hiyo naweza nikasema kwamba Wizara ya Fedha inawadhulumu wazee wetu wastaafu wa Jamhuri ya Muungano ambao wanaishi Zanzibar kwa sababu baadaye mwisho wanaamua kusamehe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo majina hapa, na mimi mwenyewe nimeshughulikia kesi hizi moja baada ya nyingine. Kuna jina la mzee Mohamed Seif Maftaha ambaye ni marehemu, urithi wake unashughulikiwa na na Bi. Pili Ramadhani Saidi. Huyu nimekuja mpaka nimegonga mwamba, mpaka leo mafao yake hajapata, pia kuna Bi. Zuleha; hajapata; kuna Bi. Ruzuna. Hawa wote nimewaleta mimi nimewaweka hapa Dodoma, hawakupata. Tatizo liko wapi Mheshimiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, mikoa au kanda zote kuna ofisi ndogo ya Hazina, lakini kwa nini Zanzibar hamuweki ofisi ya Hazina kuondosha huu usumbufu? Ingekuwepo Ofisi ya Hazina hawa watu wangelishughulikia kulekule, ingekuwa ni rahisi. Kwa hiyo tunawatesa wazee na tunawadhulumu fedha zao. Lakini mimi naahidi hapa nitaendelea kuwafuatilia hawa wazee. Na Mheshimiwa angalia sana katika pensheni, angalia sana katika sehemu hiyo, watu wanadhulumiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya pili kwa Mhasibu Mkuu; tulitembelewa hapa na Jumuiya ya Wazee Wastaafu. Jumuiya hii wana malalamiko mengi, yanafika hata 30, lakini kubwa wanalosema ni kwamba pensheni zao wanalipwa siyo kwa mujibu wa sheria, sheria haifuatwi, Sheria ya PSSF haifuatwi, na ile nyongeza iliyotoka Hazina nayo pia haifatwi. Kwa maana hiyo wazee wanadhulumika. Ombi lao wanasema Mheshimiwa Waziri uunde task force uwasikilize malalamiko yao; usipounda task force hawa wazee nao wataendelea kudhulumiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nina mfano mmoja. Kuna mzee mmoja alisema analipwa pensheni ndogo, tukazungumza na maafisa wako, siku ya pili alipewa pensheni anayostahili na akapewa malimbikizo yake. Sasa wazee kama hawa wako wengi. Kwa hiyo tunaomba hawa wazee uwashughulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Fungu Na. 10; kwa mujibu wa Katiba fungu hili linasimamia uhusiano wa kifedha. Uhusiano huu wa kifedha hapa nimekusudia kuzungumzia mikopo ya nje. Mikopo ya nje ambayo inaingia katika nchi hii inastahili kwamba Zanzibar mgao wake ni 4.5.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimefanya tafiti kupitia taasisi hizi zifuatazo; Wizara ya Fedha yenyewe, IMF, World Bank, African Development Bank, Tanzania Coalition on Debt and Development (TCDD) na taasisi nyingine. Nimegundua kwamba hata asilimia mbili Zanzibar katika ile mikopo ya kutoka nje hapati. Na mikopo ya nje ni suala la Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ukitaka kujua kwamba ni suala la Muungano, akikorofisha Zanzibar mkopo unazuiliwa. Kulikuwa kuna mkopo hapa wa NCC ambao ulikuwa unakuja kwenye REA lakini ilivyotokea vurugu kule Zanzibar mkopo huu ulizuiliwa kwa sababu mkopo ni Muungano. Sasa hii asilimia nne utakaposimama Mheshimiwa Waziri, ninaomba utupe majibu ya kutosha hii asilimia nne ipatikane.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, nimefanya utafii kupitia IMF sasa hivi ni kigezo kipi kinatumika katika kupata mikopo Zanzibar. Nimeona document ya Tanzania kwenye IMF kwamba mnatumia financing gap ili ku-finance au kupata mikopo ya nje. Finance gap ya mwaka 2021/22 ilikuwa 866. Sasa je, tunatumia financing gap, hiyo financing gap mnachukua na financing gap ya Zanzibar au mishatumia hiyo financing gap, kwamba mnatafuta 4.5, na hapa tutazame. Hiki kigezo kimewekwa tangu mwaka 1994 wakati wa mzee Malecela katika tume yake, sasa je, bado ni valid ibakie hiyohiyo 4.5? Na sasa hivi kuna variables nyingi sana zimebadilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dk.t. Mwigulu, atakapokuja hapa nataka anipe ufafanuzi katika suala hili la 4.5 katika mambo mawili, je, ilikuwa ikilipwa kwa mikopo yote? Kwa sababu kuna mikopo ya basket fund tunajua haziwezi kuhusika. Lakini cha pili, je, hii rate ya 4.5 ni valid? Mbona mkienda IMF mnatumia financing gap. Ninataka uje utupe ufafanuzi, kama hatukupata ufafanuzi sisi Wabunge ambao tunatoka upande wa pili kule hatuwezi kuomba maji hapa, hatuwezi kuomba elimu hapa, hatuwezi kuomba afya, tunashughulikia huu uhusiano. Kwa hiyo uje utuambie uhusiano huu ukoje na nini kinapatikana katika uhusiano huu, kipi kilistahili kupatikana katika uhisiano huu; lakini je, bado factor hii ipo, na mnatumia sasa variables nyingine kwenda kukopea. Sasa tunataka Mheshimiwa uje utupe ufafanuzi, kama sitaridhishwa na majawabu yako nimekusudia nikamate shilingi. Nitakamata shilingi ili tupate ufafanuzi kwa sababu hakuna uwazi katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mikopo inatoka World Bank ilikuwa inashughulikia masuala ya utoaji wa haki, zikajengwa mahakama Tanzania nzima. Lakini mkopo ule wa World Bank kule Zanzibar haukufika. Kuna mikopo ilikuwa ikishughulikia kutatua msongamano katika miji mikuu, msongamano ule tukajenga madaraja maeneo chungu nzima, mkopo ule kule Zanzibar haukwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika hii REA tunayozungumzia, portion ya REA tunatoa fedha ambazo nyingine unachangia kutokana na tozo ya mafuta, lakini nyingine tunachangia kutokana na mkopo. Sasa huu mkopo unatoka nje na haukuja kwenye basi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele ya pili hiyo.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, nitaunga mkono hoja endapo nitapata ufafanuzi, vinginevyo nitashikilia shilingi. Nashukuru.
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante, awali ya yote kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kutupa uhai na uzima kusimama leo hapa kuja kujadili jambo lenye maslahi na uchumi na jamii katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi kwa sababu kama ulivyosema walioomba kuchangia ni wengi.

Mheshimiwa Spika, mimi nilikuwa nataka niseme msemo mmoja ambao msemo tunautumia; maa filbidhi ilaldaras; kwenye weupe ukisugua utatia doa, kwenye weupe ukisugua utaweka doa. Maana ukisikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambaye leo hajaruhusu kusema kwamba maelezo haya yaende kwenye Hansard. Watanzania huko nje wamemsikia Mheshimiwa Waziri amesema jambo moja baada ya lingine, ametaja maslahi ya Mkataba huu, ametaja chanzo au chimbuko la Mkataba huu, ameusema na Mkataba wenyewe, amechambua, amesema na faida tofauti tofauti. (Makofi)

Kwa hiyo, Watanzania tunawaomba acheni kusikia yale maneno ya watu wengine kule, hebu sikilizeni ile hotuba ambayo imesomwa na Mheshimiwa Waziri hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Mwenyekiti wa Kamati alimaliza ndio maana nikasema kwenye weupe ukisugua utatia doa; amesema kwa niaba ya Bunge lako hili tukufu na ameishauri Serikali na ameunga mkono hili azimio kwa sababu yale aliyoyaeleza sisi sote tunayakubali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi niseme kuna kitu kimoja, kwa nini watu wamezungumza yale huko nje? Kwa sababau kuna mazingira ya ushindani wa bandari yetu na kuna mazingira ya hawa wawekezaji katika bandari. Kuna ushindani wa wawekezaji katika hii bandari, sasa wengine ukisikia wanachangia huko nje wanachangia, lakini akili zao hazijasalimika. Hili neno naomba liwe noted. Kweli wametoa maoni, lakini wametoa wakati akili zao hazijasalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna watu wanatoa maoni haya akili zao ndani kuna vifurushi vya nongwa, wengine wanatoa maoni katika mkataba huu lakini akili zao kuna vifurushi vya tamaa kwamba kwa nini amepata mtu mwingine, wengine wanatoa maoni lakini ndani ya akili zao kuna kifurushi cha ubaguzi. (Makofi)

Sasa huwezi ukawa akili yako haiko salama ukajadili jambo likaenda salama kwa Watanzania. Naomba Watanzania wamesikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kitila Mkumbo alisema nchi hii ina sera, ubinafsishaji umeanzishwa zamani, uwekezaji na sera zake upo toka enzi ya Rais Mkapa umewekwa, lakini Chama cha Mapinduzi tunayo sera hiyo. Kwa hiyo, Rais huyu huyu angetokea sehemu yoyote ya Tanzania hii angefuata sera za uwekezaji angefuata na sera za Chama cha Mapinduzi na ndicho ambacho kinachosema na ndicho kinachoongoza kusema hayo. (Makofi)

Kwa hiyo, hakufanya Rais huyu kwa sababu ya Uzanzibari, hakufanya Waziri, hakusaini kwa sababu ya Utanzania na sera yetu, mageuzi yetu ndio yaliyoturuhusu tufanye haya na tumefanya tumejirekebisha kama walivyozungumza wazungumzaji wengine na ndipo tukafika hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hebu kila mmoja avute akili yake atizame kuna kikatuni kimoja kilikuwa kinaitwa cha nipashe, kinakuwa kina mdomo mrefu na masikio makubwa kinampasha mtu, halafu chukueni ile sura ya kile kikatuni mlinganisheni kuna mtu fulani alikuwa anazungumza maneno hayo utapata. Sasa sisi hatuwezi kusikiliza umbea kama huu ambao wao walikuwa wakiuzungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mwenyekiti wa Kamati ya Pamoja ambayo imeshughulikia alisema haya ni makubaliano na makubaliano haya yanaweka msingi wa kitu kitakachokuja kufanyika, hiyo mikataba itakayokuja kujengwa huko mbele. Huu sio mkataba wameshazungumza watu, huu sio mkataba, tunawatoa hofu Watanzania wayasikilize hayo maelezo vizuri, lakini mikataba itakuja mmoja mmoja katika eneo moja moja.

Mheshimiwa Spika, ukienda katika mkataba huu kuna appendix I ambayo kuna mambo ambayo phase one project zitakazofanyika. Kwa hiyo, ndani ya project zile zitakapofanyika ndipo kutakuwa kuna hiyo mikataba midogo midogo na mimi nilitoe hofu Bunge hili na wananchi wa Tanzania sio kwamba kila kilichotajwa kwamba kitafanyika kwa yote. Ukisikia kutafanyika development, ukisikia kutafanyika improvement ukisikia kutafanyika management, ukisikia kutafanyika operations, kuna miradi au kuna phase au kuna project ziko katika hatua tofauti tofauti. Ziko nyingine tutaanza kweli ku–develop kwa sababu ni kitu kipya, lakini kuna vingine vinatakiwa kufanyiwa management, lakini kuna vingine vitafanyiwa operation. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ukitazama kuanzia hiyo gati zero mpaka gati number seven utakuja kuona kwamba ni kweli, ukiijua ile bandari kwamba kuna maeneo kutafanyika operation na kuna maeneo mengine wao wata-improve lakini wataachiwa bandari wenyewe waendeleze. Sasa na mimi na stick pale pale kwenye ushauri wa Kamati kwamba ni lazima tuhakikishe hiyo mikataba sasa iwe ina tija kwa Watanzania. Tuhakikishe hiyo mikataba wanashirikishwa wadau husika tutakapoingia hiyo mikataba mmoja mmoja, lakini pia mikataba hiyo ni lazima itoe ukomo au itaje ukomo kama wananvyosema wengine na maoni mwengine ambayo Mwenyekiti ameshauri na Wajumbe wengine Wabunge wengine wameshauri.

Mheshimiwa Spika, lakini hofu nyingine kwamba huu mkataba hauna ukomo, mkataba huu unao ukomo nao umetajwa, sisi kama Wabunge wa Bunge lako hili tukufu tumekaa hapa kwamba tunaelewa nini kinaendelea, sasa tuwaombe Watanzania kile kifurushi walichochanganyiwa kule nje sicho, vifurushi vile vinatokana na mambo tofauti tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwenye ajira za Watanzania ndani ya mkataba huu cha kwanza ni kulinda ajira zilizokuwepo, lakini kutokana na faida na utanuzi ina maana zitapatikana na ajira nyingine. Sasa hapa ndipo tutakapojua kwamba tulikuwa tukipotoshwa ajira haziendi kutolewa, haziendi kuondolewa, tunaenda kuongeza ajira katika mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye manufaa tumeambiwa kwamba siku za kuteremsha makasha zitatoka kuanzia 4.5 mpaka siku mbili, ina maana hiyo ni tija, lakini pia meli kutoka siku tano mpaka saa 24 ni tija hiyo, lakini fedha ambazo zitakusanywa kutoka trilioni 7.7 mpaka trilioni 26.7; haya ni maendeleo makubwa kutokana na haya mageuzi. Sasa sisi kama Wabunge ndio tukasema kwamba hili azimio tunaiunga mkono Serikali kwa sababu tuko katika masuala ya kiuchumi na bandari zetu zina ushindani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, DP World yeye ana market nyingi sana, lakini isitoshe anataka kutuunga mkono ili reli yetu ambayo tumeianzisha ya Standard Gauge ipate mzigo, sasa tushaanzisha reli ipate mzigo halafu tuna ufinyu wa kushusha bandarani unafikirri tutaendelea wapi. Reli itakuja kuwa ya abiria... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja nashukuru kwa nafasi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia pumzi pamoja na uzima wa afya, kuja kujadili bajeti hii ambayo tunapanga maendeleo kwa ajili ya Watanzania na cha pili, nashukuru kwako wewe kwa kunipa hii nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anapokuwa ameudhiwa au amepata jambo ambalo linampa maudhi, basi wale wenzake wanaompenda huwa wanamliwaza. Sasa kwa kuwa, mama yetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tunajua alipata maudhi na watu kwa kumsema vibaya hasa kwa kumbagua, kwa hiyo, nataka kumpa kijishairi kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shairi hili linasema, “Sharti uusafi moyo ukitaka kuwa mwema, uwafanyie wenzio kwa kubembeleza wema, watakuendea mbio upate kurudi nyuma. Wema uutekeleze bila ya kuweka tamaa, watu uwasikilize shida zao kusimama, kisha wema ukuponze ubaki unalalama.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunaelewa kwamba Mheshimiwa Rais alifanya wema kumtoa mtu gerezani na akafanya mengine makubwa tu, kumwachia baadhi ya rasilimali zake ambazo zilikuwa pengine zimeshafutwa, lakini bado ule wema umemponza mama, lakini hizi ni kama tasnia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 21 na 22 wa hotuba yake, katika Paragraph ya 146, alieleza pale mabadiliko ya Sheria ya SDL ambapo hii sheria inaitwa Sheria ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Sura ya 82. Mheshimiwa pale amefanya mabadiliko kwa kuweka 1/3 ya fedha zitakazopatikana na Skills Development Levy kwenda katika Wizara inayohusiana na kazi na ajira. Kwa hiyo, katika Wizara hii, kwa sababu kule kuna program ya kukuza ujuzi, program hii ya kukuza ujuzi ilikuwa iko chini, kwa maana hiyo tulikuwa tunashindwa kupata wataalamu. Kutokana na hiyo 1/3 itakuwa kubwa kwa zaidi ya mara 10. Kwa maana hiyo sasa, Wizara ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo inashughulika na ajira na walemavu itapata hilo fungu kwa ajili ya kukuza ujuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali. Nampongeza na ninamshukuru Mheshimiwa Rais, amekwenda kukuza ajira kwa vijana wetu, anakwenda kukuza ujuzi kwa vijana wetu. Kwa nini? Tumetoka Shilingi bilioni tisa, kama tutaangalia katika Volume IV, kitabu kile page ya nne ya Skills Development Levy kutoka Shilingi bilioni tisa na kwenda kukaribia Shilingi bilioni 100 na kitu. Kwa hiyo, hii maana yake ni kwamba tunakwenda kujenga uwezo kwa vijana waweze kujiajiri. Pamoja na mama ametoa ajira, lakini pia vijana wanajengewa uwezo waende wakajiajiri. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali, tunakushukuru sana mama kwa kuwajali vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu. Fedha hizi, kama tunakwenda kukuza ujuzi tutengeneze skilled labors wa kiwango cha juu ili kuweza kumudu sasa kuingia katika Tanzania ya viwanda. Kwa sababu, mwanzo tulinadi Tanzania ya viwanda, lakini hatukuwa na watu waliokuwa na ujuzi katika sekta hizo. Kwa hiyo, tukajaribu kuangalia upande wa kukuza ujuzi ambapo tutavutia viwanda. Duniani hapa watu wote ambao ni wawekezaji wa viwanda wanatazama vitu kama mfano wa availability of raw materials na skilled labor. Sasa tukiwa na skilled labor ina maana tutaweza kutekeleza ile Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa niishauri Serikali, kwa sababu kila sehemu wanakuza ujuzi, kila Wizara; ukitazama Wizara ya Kilimo wanayo hii program ya kukuza ujuzi, lakini pia Wizara ya Mambo ya Ustawi wa Jamii nao wanakuza ujuzi. Sasa tutazame katika instrument, ni nani ataratibu hili? Maana tukitapanya resources tutakuwa hatuna mratibu na tutakuwa hatuna namba ambayo tunataka kuijua kwamba hii sasa tumekua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ambayo ina kipato cha kati ilitakiwa iwe na at least asilimia 12 ya watu ambao wana ujuzi katika kazi, lakini sasa hivi tuko katika asilimia 3.6. Kwa hiyo, tunamshukuru sana mama, amewajali vijana wake. Vijana ajira zinakuja, mama ameweka Shilingi bilioni 112 katika kukuza ujuzi. Tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka niliongelee, Mheshimiwa Waziri amezungumza katika paragraph ya 151 ambayo ipo katika ukurasa wa 154 wa hotuba yake. Pale alizungumzia Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2004. Mheshimiwa amependekeza katika 151 LN, kutoza ushuru wa forodha kwa kiwango cha asilimia 25 badala ya asilimia 10 kwa mwaka mmoja kwenye nyuzi za pamba (cotton) zinazotambulika kwa HS Code 52.05, 52.06, 52.07, anasema lengo ni hatua ya kulinda viwanda vinavyozalisha bidhaa hiyo kwa kuongeza thamani ya zao la pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Waziri hapa, lakini viwanda ambavyo tunavyo hapa Tanzania vinavyotengeneza hizi nyuzi za aina hii tuliyoitaja, wanatengeneza kwa ajili ya matumizi yao wenyewe na hakuna kiwanda kinachotengeneza kwa ajili ya mwenzie. Kwa maana hiyo, wanaonunua kutoka nje, huwa wananunua kwa sababu ndani hizi nyuzi hazipatikani, na viwanda vinavyotengeneza ukiwaambia labda walete quotation, bei yake inakuwa ni kubwa zaidi kuliko ile ya nje. Pia uwezo wa kutengeneza kibiashara, hakuna kiwanda hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ililisikia hili ikajipanga kuwaalika wawekezaji na wawekezaji walikuja, lakini Serikali yenyewe ilishindwa kwa sababu, imeshindwa kutoa incentives. Walitaka incentives, imeshindikana. Kwa hiyo, viwanda hivi vilipokuja, vikakimbilia Uganda. Kule Uganda wananunua umeme kwa senti nne. Sisi senti 10 ya Dola. Sasa ukienda Zimbabwe wananunua kwa senti nne. Hapa ni senti kumi. Uganda wamehakikisha wanawanunulia pamba wanawawekea kwenye maghala. Kwa maana hiyo, availability of raw materials imehakikishwa. Sasa sisi hapa kwetu haiko hivyo. Isitoshe, tukisema kwamba tumekipandishia hiki kiwanda asilimia 25 tunaenda kuua biashara yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Maendeleo na Ustawi wa Jamii tulitembelea kuangalia wafanyakazi. Pana wafanyakazi 8,700, ukisema hiki kiwanda kinashindwa kufanya kazi, umeondoa ajira za watu 8,700. Isitoshe Afrika Mashariki ushuru ni asilimia 10, Kenya Halimi pamba, lakini anatumia hiyo asilimia 10, Uganda asilimia 10. Sasa sisi tunashindwa kuingia katika ushindani. Soko letu tunalotumia, tunauza AGOA, tunauza South Africa na katika nchi nyingine. Wenzetu zinapatikana bidhaa zao kwa bei rahisi na sisi kwetu zinafeli kupatikana hizi bidhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, tujaribu kuangalia kwa sababu siyo kosa la kiwanda, ni kosa la Serikali kuweka incentives, kiwanda kimeshindwa. Tuweke incentives katika umeme, pia tujaribu kuangalia mazingira yote ya hivi viwanda ili vitusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii mia kwa mia. Naomba Mheshimiwa Waziri aje atupe majibu. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante namshukuru Mungu na nashukuru kwa yote na wote waliofanya vizuri. Kule kwetu kulikuwa kuna bomba/mfereji ambao unatoa maji safi. Sasa kuna mtu alienda akafunga koki kwa sababu yeye ana kisima chake huko yale maji ya kisima chake yanazidi kupanda bei. Katika hii kesi ya pesa za machinga huku nje tunasikia kuna kausha damu wanakopesha kwa riba kubwa lakini kwa nini hizi pesa za wamachinga kwa miaka miwili zilipangwa shilingi bilioni 22 hazikutoka na sasa zimepangwa shilingi bilioni 18 hazikutoka au inafanana na hii kesi ya huyu aliyekwenda kulifunga bomba na huku ana kisima chake ili apandishe maji kwenye kisima, tulitizame vizuri sana hili suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa utaratibu wa benki, ni sawa utaratibu wa benki hivi hiyo Serikali imeshindwa kuwasiliana mpaka leo pesa zikafika hapo. Mwenyekiti alitoa hii hoja kwamba hizi fedha zitolewe kwa haraka na riba ipungue lakini na utaratibu wa kupatikana vitambulisho uende vizuri. Kwa hiyo, hii tunahofia katika suala hili kwa sababu ni mwaka wa pili pesa hizi hazijatoka na mna component tatu, kuna other charges hazijatoka pia kuna fedha ambazo zikajenge zile ofisi amabazo amezizungumzia Mheshimiwa Furaha pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine na kwenda katika Wizara ya Kazi na Ajira, huku tumesema kuna programme ya kukuza ujuzi lakini tumepata poromoko tumetoka kutoka watu 42,000 mpaka 12,000, tumeanguka kwa 71%. Isitoshe kuna mpango wetu wa Taifa tumeuweka kwamba kwa miaka mitano tufikie watu 600,000,081 ambapo kila mwaka ni watu 136,000,000. Hivyo, sisi tunakwenda tunapata watu wachache zaidi. Fedha zilizopangwa zilikuwa zitumike kwa mwaka shilingi bilioni 109 lakini tunatumia shilingi bilioni 9, maana yake tunafikia kwa 8% tu peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo je, ipo haja ya kuwa na hii programu? Hii programu ilipaangwa kwa kulenga one third ya skills development levy ndiyo maana ukaja ukaona kwamba hatuendi sanjari. Sasa je, skills development levy hatupeleki kwa one third. Hapa Mheshimiwa Waziri wa Fedha alileta sheria lakini akaja akaiondosha kwamba ku-ring fence ile one third, aliiondosha. Sasa tutizame je, tunaweza kufikia hili lengo, kama hatufikii tunajidanganyia nini? 8% mwanafunzi au mtoto huwezi ukasema umefaulu kwa 8%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine tuna mifuko yetu ya hifadhi ya jamii, hapa Mwenyekiti ametoa hoja kwamba wastaafu wanaomba kuongezewa pensheni zao. Huku Wizara imesema inataka kufanya actuarial study utafanyaje actuarial study wakati Serikali yenyewe ina deni la shilingi trilioni 2.45 la PSSSF. Kule kwenye NSSF pia 1.39 trillion shillings Serikali wanadaiwa Serikali. Ukitaka kufanya actuarial ina maana kwamba ni lazima uingize na uwezkezaji wa hizi taasisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, uwekezaji hizi fedha zitakuwa ziko nje. Sasa tukisema tunafanya actuarial study ina maana hata tukienda tukataka kuwalipa tutawapunja. Kwa hiyo, Serikali ijaribu kuangalia hivi vitu kwa maana hiyo kweli tuongeze lakini tujaribu kuangalia hilo suala. Jingine alizungumza hapa Babu Tale ameondoka na nilimtania pale kidogo kutokana na hii…

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ali Hassan King kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Taletale.

TAARIFA

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa muongeaji kwa neno la Hayyakum dhanna amedhani kama nimeondoka wakati nipo, ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa King endelea na mchango wako.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, alikusudia iyyakum wadhanna (Jiepusheni na kudhani). Mimi sikumuona pale alipo kwa hiyo nilikuwa niko sahihi macho yangu ndiyo yaliyosema hivyo. Babu tale alisema hapa kwamba ingawaje hii sports betting ni haramu lakini kwa nini isitoke? Kule kwetu kuna usemi, Mshairi mmja anaseama “Ingawa haramu, malipo yake ni moto, msaidie mwenzako.” Kwa hiyo, namuunga mkono kwamba hili fungu la sports ambalo tumesema ni 5% liende kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si kweli kwamba Bunge lako hili unajua kwamba pesa za sports betting kwamba hazijulikani, zinajulikana hata na mimi ninazo. Mtu atakayezitaka hizo hata na mimi nnazo naweza nikazileta za mwaka juzi, mwaka jana na mwaka wa leo kwa sababu zipo lakini kwa nini hazitoki? Nashauri tu-ring fence hii 5%, tu-ring fence Serikali iki-fence tu hapa moja kwa moja zinakwenda zake Wizara ya michezo. Kama hatukufanya hivyo bila ku-ring fence ina maana kwamba matumizi yake bado yatabakiwa kuwepo katika Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengi ya kuzungumza, nashukuru sana kwa kupata nafas, naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2016
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, asante kwanza na mimi napenda nimshukuru Mwenyenzi Mungu, ambaye ametujalia uhai na uzima katika siku ya leo kuja kujadili sheria hii ambayo ya mapendekezo iko mbele yetu ya procurement, ambayo imelenga kuokoa gharama na fedha nyingi za Serikali ambazo zinakwenda katika matumizi ya umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumshukuru Waziri wa Fedha na timu yake kwa kuleta muswada huu kwa wakati ili kuokoa fedha hizo, lakini pia napenda kuishukuru Kamati ya Bajeti nayo kwa kufanya uchambuzi na kupendekeza mambo tofauti ambayo yameboresha sheria hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimekusudia kuongea mambo mawili katika kuchangia muswada huu wa sheria, jambo la kwanzani matumizi ya health commodities, au manunuzi ya health commodities, vifaa tiba ambalo aliongelea kwa upana zaidi Mheshimiwa Martha Mlata, ameongelea kiundani zaidi. Sasa mimi mapendekezo yangu yanakuja hapa, kwa sababu hivi vifaa tiba kikawaida vina sifa ya kwamba vinaokoa maisha ya mwanadamu na hasa hasa katika afya za mama na mtoto ndio usiseme. Zitaokoa maisha ya watanzania kwa ujumla, kwa hiyo kuna uharaka wa kufanya jambo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo langu la kwanza, kungekuwepo na kifungu maalum ambacho kinaelezea hivi vifaa tiba. Lakini kama hilo halikuwezekana la kuwa na kifungu maalum cha kuelezea vifaa tiba, katika mapendekezo ya sheria kifungu cha 24 kimeeleza kwamba kitaongeza ibara ya 65A, ambapo hapo kutatajwa specialized goods, zimetajwa all services ambapo labda hapa inawezekana vikaingia hivi vifaa tiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili neno la specialized goods or services kwamba bado halijawa maalum sana au liko general. Kwa hiyo, labda katika uchambuzi wake lingechambuliwa tukaelewa ni vifaa vya aina gani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine katika kifungu hicho hicho ambacho kimeelezea habari hiyo ya specializes goods cha 65A(2) ambacho kimependekezwa kimempa mamlaka Waziri kutunga kanuni, katika kanuni hizo ambazo atataja hivyo vitu kwa undani wake, basi ndani ya hizo kanuni tulikuwa tunamuomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuangalia hizi health commodities au vifaa tiba kwa lugha ya kikwetu, ili viweze kwenda sambamba. Kwa hiyo, vifaa tiba hivi vitakapopatikana vitaweza kutuongezea thamani ya maisha ya wanadamu katika nchi yetu. Lakini pia ili iweze kwenda sambamba na azimio la Wizara ya Afya, sasa hivi katika manunuzi tumewasikia wamejipanga kivingine, kwa hiyo iweze kuboreshwa katika hivyo vifaa tiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, huo mchango ilikuwa ni katika masuala hayo ya vifaa tiba, ambayo pia katika sheria kuna kifungu cha 67 cha sheria mama, ambacho kiongezwe, wafanye marekebisho katika kifungu hicho ili kiweze kukaa sawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikija katika suala lingine, ambalo lilikuwa lina changamoto kubwa ya kutokuwepo kwa vigezo vya mahitaji ya sekta ya umma yaani standards, ilikuwa hakuna standards. Kwa hiyo, sheria iliyoongezwa 65B katika kifungu cha 24 cha mapendekezo ya sheria kimeeleza kwamba zitatumika hizo specialized standards.Kwa hiyo hizo standards zitakazotumika bado haijaelezwa ni za aina gani, bado iko general. Kwa hiyo itolewe ufafanuzi, itakapotolewa ufafanuzi inaweza ikaleta maana zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine ambacho kwa ajili ya kuboresha sheria hii pia Waziri amepewa mamlaka katika kifungu kinachofuata cha 65B(2) Mheshimiwa Waziri amepewa mamlaka tena ya kutunga regulations. Basi atakapotunga regulations kwa sababu unapoweka standards wakati mwingine kuna watu wanaweka standard kwa sababu wameshajua kwamba anaenda kununua kwa nani.
Mheshimiwa Naibu Spika,kwahiyo zinawekwa standard kama zina m-lead yule mnunuzi kwamba aelekee kwenda kununua kwa mtu gani. Kwa hiyo hii nayo itakuwa inafanyika uongo, sasa uongo huu ili uweze kuwa covered. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri katika kanuni ambayo umepewa nguvu na Kifungu hicho cha pili cha 65B basi aweze kuweka kifungu cha adhabu kwa watakaofanya makosa katika kuweka standard. Kwa sababu wengine wanaweza wakaweka standard za makusudi, za uongo ili kuweza kupotosha, kwahiyo naishauri Serikali katika suala hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine mambo niliyokusudia mawili ni haya ambayo nimeongea lakini jingine nikupongeze wewe mwenyewe kwa kusimama madhubuti katika kiti chako na kusimamia kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maana ya kanuni ni sheria na waswahili tunasema sheria ni msumeno, kwa hiyo na msumeno Al Marhumu Issa Matona alisema kwamba; hukata mbele na nyuma msumeno kazi yake. Usiutie lawama ufanyapo kazi yake. Kwa hiyo na wewe unatumia kanuni naamini unakata mbele, unakata nyuma kwa sababu unatumia kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini aliendelea Al Marhumu Issa akasema kwamba, usitumie mkono kutaka kujiharibia, utakutoka mguno tayari umeshaumia, ukileta mabishano bure utakujalia. Kwa hiyo wenzetu wametumia mkono kutaka kujiharibia hizi kanuni na tayari umeshatoka mguno wameshaumia hawamo ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika kukupongeza huku, pongezi ambazo zimewafanya watu wanune wasikae humu ndani, maana yake kwamba, wameambiwa wasikae humu ndani lakini pia wamepewa sharti kwamba wasitusemeshe, wasitusalimie.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilimsamilimia mwanaume mwenzangu akanitikisikia mabega hivi, kanijibu kwa mabega. Kwa hiyo mimisikumfahamu vizuri lakini kule kwetu kuna msemo mmoja au kuna kanuni moja kwamba mtu ambaye anaweza akamwambia bwana usimsemeshe fulani, fulani akikusalimia usimuitikie mara nyingi mume huwa anamuambia mke kwamba akikusalimie fulani usimsemeshe wala usimuitikie. Kwa hiyo na wao hiyo amri sijui wamepewa na nani maana hawatusemeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la kushangaza ambayo misemo yakiswahili ipo, kama mzazi ameenda hospitali kujifungua kwa bahati mbaya mtoto akapita tunasema yule mtoto sio riziki kapita, na pia akiolewa dada yetu yeyote akipata mume lakini mume hatimizi majukumu ya nyumbani watasema kaolewa lakini mume sio riziki. Kwa hiyo na majimbo yale meupe kweli yana Wabunge lakini wale Wabunge sio riziki. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naunga mkono hoja mia kwa mia na tunamuomba Mheshimiwa Waziri achukue marekebisho ambayo tumeyapendekeza, ahsante nashukuru.
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Kwanza sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uhai leo tumesimama hapa kuchangia Muswada huu wa Upatikanaji wa Taarifa ambao utakuwa una maslahi kwa utendaji wa Serikali pamoja na maslahi kwa wananchi wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza nilikuwa napenda tu kuwatanabaisha Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba kupigapiga makelele sana siyo kitu kizuri kwa kuwa sisi ni Wabunge na halafu wengine tuna historia ukizungumza unaanguka. Sasa humu ndani sina uhakika kama watu wa kubeba walioanguka wako karibu maana wengine wakipiga kelele wanaishiwa na nguvu wanaanguka, kwa hiyo, tuongeeni taratibu afya zetu jamani tunazijua. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha pili katika hii introduction yangu, nafahamu wale mashetani Wakindengereko kama hawakupigiwa mbungi hawatulii. Pia mashetani wa Kinyamwezi kama hawakuchezewa maswezi pia nao wanakuwa hawatulii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nichangie kwa upande huu wa muswada, hapa kuna tatizo kubwa sana kwenye kifungu cha 3 ambacho kimetoa tafsiri ya maneno, ndipo hapa wenzetu kutokana na kutofahamu ile tafsiri wakawa wanaogelea katika bahari tofauti ambapo wengine wameongela kitu ambacho sicho kimekusudiwa kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muswada umeelezea pale nini maana ya information, kwa sisi wenye akili zetu tumefahamu, taarifa uliyoikusudia pale sisi tumefahamu. Hata hivyo, kwa kuboresha muswada huu bora na hili neno la habari pale lingeingizwa halafu likaambiwa maana yake kwa sababu hawa wenzetu zaidi wame-base kwenye habari na wameacha taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia hapa kwamba sheria hii italeta mgogoro kwenye vyombo vya habari. Chombo cha habari kinachukua habari na habari ni kitu kipya, lazima tuwafahamishe wenzetu. Kitu ambacho kimetokezea kipya ndiyo kinaitwa habari kwa kiarabu inaitwa khabar. Taarifa maana yake umeiweka katika format au mfumo maalum halafu ndiyo unaitoa hiyo taarifa. Kwa hiyo, kuna tofauti ya habari na taarifa.
Kwa hiyo, hili neno habari, naomba Mheshimiwa Waziri lingeingizwa kwenye sheria hii, wenzetu hawa pengine na watu wa nje wako kama hivi hatufahamu, sasa isije ikaja ikaleta utata. Kwa kuondoa utata haya maneno yote mawili yangeingizwa kwa faida yao na wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine imezungumzwa taarifa na mwandishi wa habari. Mwandishi wa habari siku zote unapompeleka taarifa basi itabidi wewe ununue page ndiyo uweke taarifa yako au utafute kipindi maalum lakini habari anaitafuta mwenyewe. Sasa unapokuwa na taarifa, mara nyingi taarifa zako unapotaka kuzipeleka kwenye chombo cha habari basi wewe ndiyo unatafuta lakini habari anaitafuta mwandishi wa habari. Kwa hiyo, ni vitu viwili tofauti lakini ikiwekwa tafsiri itatusaidia kuboresha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ambacho nahisi ni cha msingi sana, hapo hapo ilielezewa katika sheria hii jinsi ya upatikanaji wa habari, imeambiwa kwamba kuwe na utaratibu wake wa kupata hii habari. Sasa hapa kuna watu wakaona labda ni kikwazo kwa mwandishi wa habari, hiki sio kikwazo kwa mwandishi wa habari hapa kumetajwa taarifa.
Kwa hiyo, upatikanaji wa taarifa, taarifa ina mwenyewe na ametajwa information holder. Kwa hiyo, huyu information holder ndiyo anayo mamlaka ya kukupa wewe lakini kwake yeye ni wajibu kutoa hizi taarifa. Kwa hiyo, taarifa kama hukupewa ina maana wewe umechukua taarifa ya watu kwa nguvu inakuwa ni wizi. Mtu anayechukua taarifa ya watu bila ya idhini ya mwenyewe anaitwa mmbeya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hawa wenzetu labda wamezoea hii kazi na hapa tunapata sign kumbe ile mijizi ya taarifa za Serikali imo humu. Wewe ukitaka kujua, je, hapa pana nyani kajificha au hajajificha tikisa majani, utatizama kama nyani yupo au hayupo. Kama hakutoka hebu rusha jiwe, utamsikia tu anaguna mmh. Kwa hiyo, hiki kitu kimewakaa sasa zile taarifa za umbeya zitakuwa hapa hazipatikani tena. (Makofi/Kicheko)
Kwa hiyo, tutoe maelezo na huu utaratibu mimi nauunga mkono kwamba kila taarifa inakuwa ina mwenyewe kama hamjui lakini habari ndiyo inayotafutwa, ni lazima muelekezwe kama hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 2 kimeeleza application kwamba hii sheria inaenda kutumika wapi, nafikiri kweli sio ma-DC tu wa kupewa semina na Wabunge wapewe semina wafahamishwe mambo yapi ya Muungano na yapi siyo ya Muungano. Mbona kwenye TAMISEMI sheria zake hawasemi kwamba zipelekwe na Zanzibar. Mbona tukizungumza masuala ya kilimo, tukiacha uvuvi wa bahari kuu hawasemi na yote tumepitisha ina maana kwamba hawajui au kama wanajua wanataka kupotosha umma. Kwani nani asiyejua kuna sekta za Muungano na kuna sekta ambazo siyo za Muungano. Sasa kama mtu hufahamu taratibu jamani njooni tuwafahamishe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumzwa...
TAARIFA...
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa yake nimeipokea hata Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo ndani ya Katiba hiyo hiyo aliyoishika. Kwa hiyo, mambo yake tutajadiliana hapa, kuwa na akili kidogo, eeh, naendelea. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naunga mkono kwenye kifungu cha 5 ambacho kimetaja kwamba haki ya mtu kupata taarifa na wajibu wa mtoaji taarifa kutoa taarifa. Naunga mkono hapa pana maana sana, lakini pafafanuliwe na patiliwe msisitizo kwa sababu bila kupata taarifa watu watafanya mambo ambayo hawayajui yatakuja kuwadhuru mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nNatoa mfano, kuna taarifa moja pengine ingetolewa na Shirika la Nyumba juu ya mdaiwa fulani kiongozi anakaa pale Kambi ya Upinzani shilingi bilioni 1.2 na wangetoa taarifa kwamba ile tarehe 1 ilikuwa ndiyo siku ya kwenda kuzuia shughuli anazozifanya katika majengo yale aliyokodi ambayo kwa miaka 20 hajalipa na halafu mtu yule yule akaitumia ile siku watu waandamane kumbe kwa ajili ya kumlinda, taarifa hii ingekuwa wazi basi watu wasingeambizana habari ya kuandamana wala hakuna mtu angejali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa shilingi bilioni 1.2, deni la muda miaka 20 amekaa na pesa za watu hakuzilipa, leo anasema anatetea maslahi ya wananchi, zingekuwa habari au taarifa hizi zinawekwa wazi basi wananchi wasingepata taabu. Kwa sababu watu walisema tarehe mosi watu wanataka kufanya maandamano walikuwa hawajui kumbe wanakwenda kulinda interest ya mtu. Kumbe nchi hii ni rahisi sana kuishi, wewe daiwa halafu kama una mamlaka yako waambie watu waandamane tu ili usahau lile deni. Shirika la Nyumba tarehe ile lilifanya ile kazi yake na taarifa alikuwa ameshapelekewa miazi miwili nyuma ndiyo maana wakapanga tarehe ile, lakini hajanusirika hata hivyo.
TAARIFA...
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea taarifa yake lakini nilikuwa naomba anitajie ajenda ya leo. Basi naendelea kama na yeye haijui. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, laiti watu mambo haya wangekuwa wameyafahamu wasingeweka ule UKUTA ulioparamiwa na kuku ukaanguka wala wasingeunga mkono vitu vile, lakini leo wakakubaliana, wakashawishika kumbe mtu ana deni huku.
UKUTA ule wa Apolo umeparamiwa na kuku umeanguka, halafu watu wanasema kwamba kwa kutanguliza maslahi ya Taifa kwani ulipopanga ulikuwa hujui kama kuna maslahi ya Taifa au kwamba hamuoni mbali, kama hamuoni mbali ndiyo mkajua wakati ule.
Kwa hiyo, upatikanaji wa taarifa kwa mujibu wa kifungu cha 5 ambacho kimetajwa pale wananchi wakapata taarifa hizi wakazitumia, wakawa well informed, wanaweza wakajiepusha na mambo mengi, watu wangeumia kwa sababu ya mtu, kumbe mtu ana deni, usijipange kukopa bila kujua kulipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nizungumze suala moja ambalo wenzetu wanawaambia waandishi wa habari wasiukubali muswada huu, muswada haukubaliwi na waandishi wa habari, huu muswada tutaukubali hapa Bungeni. Huu muswada tunaupitisha sisi Wabunge na huu muswada siyo kwa ajili ya waandishi wa habari ni kwa ajili ya wananchi. Hiyo mnayozungumza ninyi ni hofu yenu, kumbe tumeshakujueni nyaraka za Serikali mlikuwa mkiiiba…
Sasa ikiwa ni hivyo hii mimi naunga mkono mia kwa mia, nashukuru.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili na mimi nichangie Muswada huu wa habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ningependa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuweka hai na leo kuja kushuhudia haya ambayo tunayaona, mengine kusema kweli kwamba ni mambo ya kushangaza kidogo, hata katika nafsi yangu nashangaa sana. Lakini siwezi kushangaa sana, unajua mtu anapokumbwa na sakaratul maut, anapokaribia kufa pale basi chochote kile kinamtoka. Atasema maneno yaliyokuwemo na yasiyokuwemo. Kwa hiyo, na hii ni sakaratul maut imewakuta watu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, alizungumzia hapa Mheshimiwa Khatib, alitaja habari nzuri kidogo. Habari ya wale waliokuwepo kule magereza Zanzibar miaka ya 90 wakati na mimi nilikuwa ni mtumishi kule. Hata hivyo, kitu kimoja tu alikosea, walikuwa rumande, kwa hiyo rumande walikuwa wakiletewa chakula kutoka nyumbani, nacheza na super league wakati huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende katika Muswada. Katika Muswada huu ambao umezungumzia masuala ya kuipa hadhi hii taaluma ya habari, imezungumzia suala la accreditation, wengine walisema humu wanashangaa kwa nini wameikuta humu accreditation au wanaona ajabu kwa nini watu wanajadiliana nayo wakati hiki kitu kilikuwepo tokea mapema. Kusema ukweli, suala la accreditation ni suala muhimu sana kwa waandishi wa habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia hata referee basi pia naye wanafanyiwa mambo haya na wana daraja zao, leo tuje tulikatae katika uandishi wa habari. Yaani tunazungumzia habari hizi kana kwamba hatuoni nini faida yake. Kwa hiyo, hili suala la accreditation kwa waandishi wa habari ni suala muhimu na napendelea hilo suala liwepo. Cha kushangaza kwamba leo tunasema kwamba tunawatetea waandishi wa habari wakati mnawatetea huko mnakuja na nyimbo kwamba mna imani na mtu fulani, sasa mnatetea au nani aliyetetea? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja iko mbele yetu, kama tunawatetea waandishi wa habari basi hebu tujeni na kitu cha kuwatetea hao waandishi wa habari. Tukija na nyimbo hizi ambazo mnazileta humu, mnafanya kitu ambacho hakiwezekani kabisa, sio kitu kizuri kwamba hata hiyo imani yenu na hao waandishi wa habari wanaowasikiliza sijui wanawaweka daraja gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo katika mjadala wetu huu, nimesoma hoja zote; nimesoma hoja ya Waziri, hoja za Kamati na hoja za upande wa Upinzani, pamoja na wengine wenzangu waliochangia, ndiyo tumesikia jinsi gani watu wanavyochangia, lakini nilichobaini kwamba kuna watu wamekuja kutia kidusi tu, kwamba ni kidusi ili bata asilike, lakini tangawizi ya kumuoshea iko, atalika bata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitazama kwenye kitabu hiki cha Kambi ya Upinzani, katika page za mwanzo kama kilipinga lakini page za mwisho, kikaja kikakubali yale ya leseni, baraza huru, hiyo ithibati. Kwa hiyo, utakuja kukuta kwamba ni kakidusi tu, lakini hiki kitu kinakubalika. Sasa hicho kidusi hapa pana tangawizi, pataoshwa na italika! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitazama humu unaweza ukaja ukakuta kwa lugha ya kilingala tunasema “poto poto” kwamba tope tupu. Huku unazungumza hivi, halafu unakuja unajikanyaga. Sasa katika hawa waandishi wa habari kama tunataka haki zao, basi moja ni hiyo accreditation kwa sababu tukitazama katika perspective ya waandishi wenyewe ambao wengi wametazama kule kwenye waandishi, hawakutazama kwa wale walaji wa habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la accreditation ni la muhimu, lakini hapa tukaja tukaleta historia, labda fulani alikuwa akifanya uandishi wa habari bila ya kuwa na taaluma, fulani alifanya uandishi wa habari bila ya kuwa na taaluma fulani. Sasa tusirudi huko, sasa hivi tunataka kwenda mbele, Taifa kama hili sasa hivi mambo mengi yamebadilika. Kuna mshairi mmoja anasema “zama zimebadilika na mambo yamegeuka” sasa zama zimebadilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuwa anauliza hapa Mheshimiwa Tundu Lissu kwamba kwa nini iwe hivi katika masuala ya accreditation? Wa tilkal ayyamu nudawiluha baina nnasi, hizi ni siku ambazo mambo yanageuka, siku hazigandi, watu hawabakii vile vile, we are not static! Siku zote ulimwengu uko dynamic, mambo yako hivyo. Kwa hiyo, ni lazima tutazame jinsi ya kuweza kuwawezesha waandishi wa habari. Suala hili litawawezesha kufanya kazi zao vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni katika masuala ya habari hizi za uchochezi. Kusema ukweli ni muhimu sana kuwa na Sheria hii kwa sababu wengi wanasema daktari awe na taaluma, lakini mwandishi wa habari asiwe na taaluma. Daktari anaweza akamuathiri mtu mmoja katika chumba cha operesheni, lakini mwandishi wa habari anaweza akaathiri jamii nzima, Tanzania nzima, watu milioni 50.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hiyo accreditation ya mwandishi wa habari iwe kubwa zaidi kuliko hata ya daktari, kwa sababu daktari atamhukumu mmoja au atafanikiwa kumwathiri mmoja, lakini je, mwandishi wa habari kwa kalamu yake atawaathiri wangapi? Kuna mifano ya Rwanda 1994, kuna mifano ya Kenya 2006, kuna na mifano mingine chungu nzima ambayo inatumika. Kwa hiyo, ni lazima tutazame kwamba jinsi gani mwandishi wa habari ataweza yeye mwenyewe kupata sifa ya kuwa mwandishi wa habari na pia ile jamii ambayo anaitazama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine muhimu limezungumziwa neno la kashfa, pendekezo langu kwenye neno hili, bora lingetumika neno lingine kwa sababu kashfa ni kuweka wazi kwa maana fupi. Sasa anaweza mtu akaja akaambiwa amekashfu lakini akaweza kujitetea kutokana na asili ya neno lenyewe. Asili ya neno hili maana yake kukashfu ni kuweka wazi, inawezekana mtu kasema ukweli yaani, inawezekana ikaonekana amekashfu, akapata nafasi ya kujitetea kwa sababu hili neno asili yake ni Kiarabu, kashfa maana yake ni kufunua. Hata mtu ambaye anayepita hapa mavazi hayako vizuri inakuwa naye pia amejikashfu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili neno kama tumekusudia kashfa ya kumsema mtu vibaya, kumwelezea mtu katika lugha mbaya ambayo itamharibia image yake, bora tungetafuta neno lingine ili hili neno la kashfa ambalo limezungumzwa humu likapata maana na katika maana hiyo ikaeleza na ikaeleweka ili kuepuka watu kuja kuweza kujitetea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la taaluma ya uandishi wa habari, huko nyuma au mpaka sasa hivi baadhi ya waandishi wa habari sio waandishi wa habari ni wanaharakati. Kwa hiyo, Sheria hii imekuja kuwafanya waandishi wa habari kuwa wanataaluma. Wengine ni wanaharakati na hata jinsi wanavyoongea, utawaona kwamba ni wanaharakati, sasa tuwatoe kwenye uanaharakati, tuwafanye wana taaluma…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.4) wa Mwaka 2016
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na uzima na nikushukuru wewe kutupa nafasi hii kuweza kuchangia hoja hii ambayo iko mbele yetu. Pia kuwapongeza Wabunge wapya wa Chama cha Mapinduzi ambao wamekuja katika Bunge hili, tunaahidi kushirikiana nao kwa hali na mali. Pia ninakipongeza Chama cha Mapinduzi kwa ushindi mkubwa wa kishindo kilioupata katika chaguzi za Madiwani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo na mimi nijikite katika hoja hii ya mkopo na msaada. Kusema kweli, kuna msemo wa kiarabu unasema, “maa-filbidh illa-l-barasi.” Kwenye weupe ukisugua utatia doa. Mheshimiwa Chenge alivyozungumza Mheshimiwa Chenge nafikiri watu wote hapa wameshaelewa kitu gani kinatakiwa. Kwa kuwa niliomba kuzungumza nitarejea baadhi ya maeneo ambayo nitayazungumza kama nilivyoyaelewa mimi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kitu kimoja ambacho ninapenda watu waelewe katika Bunge hili Tukufu, mwanzo nilipoona baadhi ya Wajumbe wanawasilisha ile hoja nikaona labda wanaionea huruma Zanzibar kwenye mikopo, lakini kumbe wanaona itafaidika, wanaona kumbe itafaidika sasa wakaona waeleze wazi. Kwa kushangaa baadhi ya watu wengine wakapanda yule punda wa bao, hawakujua kama wanapandishwa punda wa bao, wakaunga mkono na wao. Sasa kumbe unanyimwa maendeleo katika nchi yako, unanyimwa maendeleo katika eneo ambalo umetoka wewe kwa kukosa mkopo na msaada. Kwa hiyo, sikuelewa pale mwanzo kumbe walikuwa wako dilemma! Sasa hivi tumeshafahamu, nafikiri acha tuendelee mbele kuwajulisha Watanzania dhamana ambayo tumepewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono katika kifungu cha 12 pamoja na marekebisho ya Serikali ambayo wamekujanayo kwa sababu ya kitu kimoja. Zanzibar siyo sovereign state ambayo inaweza ikakopa yenyewe, tunakoelekea sasa hivi tunaenda kukopa mikopo ya kibiashara ni lazima kufanyike sovereign credit rating ambayo itafanyika kwa nchi na hakuna sovereign credit rating ambayo itaweza kufanyika kwa Zanzibar. Kwa hiyo, kukopa kwa Jamhuri ya Muungano ni sawa kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ni muhimu ni kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania watu hawaifahamu. Wanahisi kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kitu mbali kabisa. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Serikali ya Muungano, kama tulivyoseme, kwa hiyo, Zanzibar imo humo humo ndani yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa sheria hii kumetajwa Wizara ya Fedha na Waziri wa Fedha; kwa mujibu wa sheria hii kumetajwa Taasisi ya Benki Kuu na Gavana; kwa mujibu wa sheria hii kumetajwa Kamati ambayo itakuwa inashughulikia masuala ya Mikopo na Deni la Serikali. Sasa hivi vitu vyote ni vyombo vya Muungano, wakati wowote kiongozi wake inawezekana ikawa ni kutoka Zanzibar. Kwa hiyo, kutokana na hayo ina maana kwamba moja kwa moja Zanzibar inaweza ikafaidika na mikopo hiyo kwa kiasi kikubwa na inaweza ikafanya shughuli zake za maendeleo na kuwapatia maendeleo wananchi wa Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzo nilipomsikia mzungumzaji mmoja anazungumza aliposema kwamba Katiba Pendekezwa ilitaka suala hili Zanzibar iwe na uwezo wake wa kukopa, sasa leo unazungumzia Katiba Pendekezwa ambayo siyo Katiba tunayoizungumzia hapa, siyo Katiba iliyopo sasa hivi. Hii ni Serikali ya Chama cha Mapinduzi, ni Serikali inayoongozwa chini ya Serikali mbili, kwa hiyo mipango ambayo imo humu ni chini ya Serikali mbili, siyo kwa mujibu wa Katiba Pendekezwa. Katiba Pendekezwa au Katiba siku zote ni sheria mama kwa hiyo, haiwezekani azaliwe mtoto kwanza kwamba ili Sheria hii tuiweke hivyo kama ilivyo kwenye Katiba Pendekezwa halafu baadaye ndiyo aje azaliwe mama, hicho kitu ni cha ajabu sana! Hicho kitu ni cha ajabu sana na nilishangaa sana kumsikia mtu huyo anazungumza masuala hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine katika masuala hayo ya kuhusiana na mikopo, kuna faida ambayo tunaweza tukaipata. Siku zote unapoenda kukopa yule anayekukopesha anaangalia default risk yako, kwa hiyo, kwa vyovyote vile kwa Zanzibar inapata faida kwa sababu default risk kwa Zanzibar ingekuwa kubwa, sasa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania default risk haiwezekani ikawa kubwa kuliko ambayo ingekuwa kwa Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala la misaada. Ingawa kuna changamoto katika suala hili misaada, lakini sote sisi tunafahamu kwamba kuna kitu kikubwa zaidi ambacho kinaweza kikakingwa kutokana na sheria hii, sote tunafahamu, kuna watu hatujui kama wameoteshwa au waliambiwa mzimuni kwamba, wewe kuna siku utakuwa Rais. Anapokosa tu anazunguka nchi zote kudai kwamba, Zanzibar inyimwe misaada, lakini kwa Tanzania hawezi! Kwa hiyo, faida hiyo ya misaada kwa Jamhuri ya Muungano ikiwepo na Zanzibar ni vizuri ili kuepukana na watu hao vitimbakwiri walioota au waliopata hicho kitu kutoka huko mzimuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, siku zote political risk kwa Zanzibar baada ya chaguzi zetu zinatokea na zinasababisha suala hili kuyumba, kwa hiyo, inapokuwepo katika sheria hii itasaidia. Kwa hiyo, mimi naunga mkono hiyo hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania labda kuzikopesha taasisi mbalimbali. Serikali yenyewe ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania humu sote tunajua sisi ni Wabunge, pengine inakopa NMB, lakini hata humu Wabunge nao wamekopa NMB. Sasa je, wewe mtu binafsi umekopa NMB na Serikali imekopa NMB! Je, hapa kuna kasoro gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ikiwa Halmashauri, ikiwa taasisi yoyote, ikiwa kampuni yoyote, kukopa, mkopeshaji ni hiyari yake mwenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi wa Mwaka 2018
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa kupata nafasi hii kuchangia muswada huu wa marekebisho ya sheria Sura ya 103 ya PPP, pia naipongeza Serikali kwa hatua hii ambayo ni muhimu kwa uchumi wetu na kwa maendeleo ya Taifa letu katika kupokea huduma kwa wananchi wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuipongeza Serikali pale ilipoleta muswada huu, kuanzia sehemu ya pili mpaka ya saba. Kifungu cha pili mpaka cha saba ambacho kimezungumzia kupunguza urasimu, lakini pia kuimarisha mifumo ya kitaasisi na kisheria katika usimamizi wa miradi ya PPP. Naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja ambalo ni muhimu tuliangalie wengi hatujaelewa nini hapa kimekusudiwa na ndiyo maana unaweza ukaja ukakuta wengine wanaona kwamba siku zimeongezeka na siyo kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi utaratibu wa urasimu uliokuwepo mwanzo ulikuwa na hatua nyingi lakini utaratibu wa sasa hivi hauna hatua nyingi, hatua zimepungua, majukumu katika kila eneo yameongezeka kwa maana hiyo ndiyo maana pengine imechangia kuja siku 21.

Mimi nilipata bahati kupitia marekebisho yaliyofanyika mwaka 2014 ambapo kule mradi wowote kutoka PPP Center unachukua siku 82 mpaka kufikia mwisho, lakini huu wa sasa hivi kutoka PPP Center mpaka kufikia mwisho kwa Waziri wa Fedha unachukua siku 63. Kwa hiyo, utaona wazi kwamba siku zile zimepungua ingawa baadhi ya watu wameongea kwamba siku zimeongezeka badala ya kupungua, lakini ukitazama siku hapa zimepungua. Tunalifahamu hilo, sisi ni wanasiasa kuna usemi wa kiarabu unasema khalifu-tuarafu, wewe ukitaka kujulikana sana
nenda kinyumena ilivyo. Ukiambiwa inflation imeshuka, wewe sema imepanda, ukiambiwa uchumi umekua, wewe sema umeshuka. Kwa hiyo, hayo tumeshayazoea ni ya kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashauri wenzangu tukasome katika part ya pili ya marekebisho yaliyopita, establishment and administration of the PPP Center ambapo imeanza kuanzia section ya nne mpaka section ya 7B nafikiri tunaweza tukaenda tukaliona hili ambalo nimelisema hapa. Kwa hiyo, tunaishukuru Serikali kwa kupunguza urasimu, ukipungua urasimu ina maana kwamba mambo yetu yatapata kwenda kwa haraka na zikipungua siku tutafanya kwa haraka tofauti na vile ambavyo tunazungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niiombe Serikali katika usimamizi wa masuala haya, kwa sababu imetajwa hapa Waziri wa Fedha, lakini itakuwepo contracting authority pengine atakuwepo na Waziri wake. Sasa pamoja na vyeo vyao kwamba vimeshakuwa defined kwamba nani atashughulikia, sasa sijui nani ataweza kumfuata mwenzake kwa sababu inawezekana ikawa ni Wizara ya Miundombinu na Wizara ya Fedha au TAMISEMI na Wizara ya Fedha. Kwa hiyo, ingekuwa kuna mtu ambaye amezidi, mkubwa zaidi basi angeweza kufuatwa kuliko ambao wako katika rank moja inaweza ikatokea sintofahamu katika kulitatua jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kichangia na kuipongeza kwanza Serikali ni pale ilipoleta hiki kifungu cha 9 cha muswada ambacho kimekuja kubadilisha 10A(2) ambacho kinataka kituo cha ubia kufungua akaunti katika Benki Kuu, lakini pia katika kifungu cha 12 ambapo kumezungumziwa masuala hayo ya kuleta akaunti au taarifa za utekelezaji za Mradi wa PPP Center, lakini na kile ambacho kinazungumzia kwamba bajeti nayo iwe imekwenda kwa Waziri mhusika. Hapa napongeza kwa sababu ya udhibiti, jambo likiwa tunalitaka ni lazima tuwe na udhibiti nalo na kama hatukuwa na udhibiti nalo ina maana kwamba tunaweza wakati wowote ule kuja kupoteza faida ambayo tuliitarajia kuipata. Kwa hiyo, naipongeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika hili kwa sababu naliona limekaa vizuri sasa katika utekelezaji usemi wa waswahili unasema kwamba ada ya mja kunena muungwana ni kitendo, tuje tutende, haya ni mazuri, lakini tusipokuja kufanya ina maana kwamba hakutokuwa na faida yoyote ile, kwa sababu tumeshayaweka vizuri lakini hatutokuja kutenda itakuwa hayaji kuleta mfano huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni kuweka usimamizi na kuripoti kwa Waziri wa Fedha itatutoa mashaka Wabunge. Amezungumza Mheshimiwa Dau pale, huu mradi wa Dar Express Way mpaka Chalinze ni mradi ambao Wizara moja ya Serikali inasema kwamba huu mradi umekuwa dropped haupo katika PPP, lakini Wizara nyingine inakubali kwamba huu upo na unaendelea. Kama ikiwa kuna mfumo huu wa taarifa wa kupashana habari kuangalia performance inaendaje itaondoa hii. Hivyo, naishukuru sana Serikali kwa kuliona hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika hii unsolicited project ambazo tunasema kwamba zitakuwa na sifa ya kipekee, lakini pia Serikali imeweka masharti. Mimi nakubali Serikali ni lazima iweke masharti kwa sababu mara nyingi sana miradi ya aina hii mtu anapokuja akathibitishiwa kwamba bila masharti yoyote kwamba kila kitu amefanikiwa anaweza akatumia hiyo document/certificate ambayo amepewa kwenda kukopea nje akachukua mkopo mkubwa halafu akaenda akawekeza kwenye mradi mwingine.

Kwa hiyo, mimi hapa naona Serikali kwamba imefanya jambo la maana kabisa kwa sababu italinda zile interest zetu, kama tuna dhahabu zetu haziwezi kuoza chini, zitakuwa zipo bado ni za Tanzania na za Watanzania. Kwa hiyo, naipongeza Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali lakini pamoja na kutoa ushauri katika hizi small scale projects ambazo zimewekewa kiwango maalum cha fedha. Hapa naipongeza Serikali kwa sababu katika Halmashauri inawezekana tukafanya miradi mingine midogo midogo kwa fedha ambazo Watanzania wanaweza, lakini hapo nachukua ushauri wa Kamati ya Bajeti ambao umesema kwamba ni lazima upatikanaji wa fedha kwa sekta binafsi uwe unaweza kupatikana kirahisi vinginevyo itakuwa hakuna sekta inaweza kuingia, kwa sababu tumesema itaweza kufika kwenye shilingi bilioni 46 kwa sababu hazitazidi shilingi milioni 20 na kushuka chini.

Sasa ikiwa ni hivi ina maana kwamba ni lazima hizi taasisi binafsi ziwe zinaweza kupata mikopo na ushauri mwingine ambao wameshauri Kamati ya Bajeti wa kuimarisha Soko la Dhamana na Mitaji, soko letu la fedha likiimarishwa nalo pia linaweza likachangia na hawa wawekezaji wengine au watu wengine binafsi wanaweza wakakopa na kufanya hiyo miradi na kwa sababu wanakuwa tayari wameshatazama ile viability ya hii project na pengine wanaweza wakafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo nitoe pongezi za jumla kwa muswada huu kuletwa, kuondosha vile vikwazo ambavyo mwanzo vimetukwaza na sasa hivi vimekaa sawa kwa hiyo, naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Sheria ya Fedha ya Mwaka 2019
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na kuja kuchangia sheria hii ya masuala ya kodi (Finance Act) kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajikita katika points kama nne; point moja ambayo imezungumzwa na watu wengi, lakini mtemewa mate na wengi huloa, nami nitarejea tena, sanitary pads. Kwanza tunaipongeza sana Serikali kwa kutanua wigo katika kutoa msamaha kwenye makampuni ambayo yapo tokea mapema pamoja na yale makampuni mapya kwa miaka miwilimiwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la kushauri Serikali ingeendelea na ule msamaha ambao ulikuwepo mwaka jana kwa sababu inasemekana kwamba haukusomeka vizuri. Watu wangeuelewa kidogokidogo basi tungefika katika hatua nzuri, lakini kwa kukatiza pale ina maana ile faida haijapatikana kwa sababu wamefaidika watu wachache. Hatua ya kutangaza kwamba watu waelewe kwamba kumetoka msamaha ingefuatwa, basi nahisi tungefikia mahali pazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ninachotaka kuchangia, ni competitiveness ya viwanda vya ndani, kumudu ushindani. Kwanza naipongeza Serikali kwa hatua za kikodi ambazo zimechukuliwa katika hii Finance Bill ambazo zinakwenda kunufaisha viwanda vyetu vya ndani na vitakuwa vinaleta ushindani. Hata hivyo, nataka nitoe angalizo moja au nishauri kwenye sehemu moja, kuna viwanda vya ndani hasa vya nondo kwamba viwanda hivi sheria zake nyingine ili zibadilishike kuna mahusiano ya kikanda kama vile ni SADC. Kwa hiyo, naiomba Serikali ichukue hatua hizi za haraka kwa sababu viwanda hivi vya nondo na tuna miradi mingi ndani inaweza ikatusaidia hata katika kukuza ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ninalotaka kuzungumza ni uhakika wa takwimu zinazohusika katika kutoa maamuzi haya ya kikodi. Maamuzi ya kikodi wakati mwingine tunatoa lakini takwimu tunazotumia siyo sahihi. Tumekaa na wadau wazalishaji wamesema kwamba mahitaji ni tani 570,000 lakini wao wamezalisha tani 210,000, upungufu ulikuwa ni tani 360,000 lakini bado tukaona kwamba tuweke kodi zaidi katika mafuta ambayo yanaingia ndani. Sasa hapa mimi nina wasiwasi kama kuna mchezo mbaya tunachezewa na wenzetu na mchezo huu hakuna anayeucheza ni majirani zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hivyo kwa sababu tani 210,000 hizi 360,000 kwa taarifa ya Waziri tumesema kwamba tumepunguza import ya mafuta ya kula kwa asilimia 94. Sasa kama tumepunguza kwa asilimia 94 hizi 360,000 zimepitia wapi? Wakati wazalishaji wenyewe wanasema kwamba wanahitaji kutumia tani 3,000 kwa kuzalisha lakini wanatumia 2,000 ina maana kwamba bado hatujaweza kumudu. Kwa hiyo, nilikuwa naishauri Serikali ijaribu kutumia takwimu sahihi vinginevyo tutakuja kupata magendo. Magendo yanakuja wala hayalindwi kwa bunduki, magendo tunaweza tukayalinda kwa sera, kwa hiyo tuwe na sera nzuri ambazo tutumie takwimu sahihi ili kupunguza haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naipongeza sana Serikali, hili ndiyo jambo langu la mwisho. Serikali naipongeza kwa kuweka zero rate katika umeme unaotoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar, tunaishukuru sana hapa Serikali, lakini pia Serikali ijaribu kuangalia katika zero rate iliyowekwa katika bidhaa zinazotoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar na zinazotoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara. Naipongeza hatua ile ya kufikiria kwamba tuweke zero rate ni sawa lakini tutizame ilikuwa tunakinga tatizo gani? Pale mwanzo tulikuwa na sheria ambayo inaruhusu marejesho ya mwaka 1997, sheria ile ya marejesho ilikuwa tatizo ni kurejesheana. Sasa tatizo kama ilikuwa ni kurejesheana ilikuwa tuweke sheria ya kurejesheana lakini tukaweka kwenye zero rate.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tulipoweka kwenye zero rate tukaanzisha changamoto nyingine mbili kwamba sheria inavyotaka, sheria inataka kwamba ni lazima bidhaa zitoke kwa manufacturer na siyo rahisi kwamba watu wote wanaweza kwenda kununua kwa manufacturer. Ukisema unanunua kwa manufacturer ina maana wewe ni lazima uwe mfanyabiashara mkubwa sana. Isitoshe sheria ikasema huyu mtu lazima awe VAT registered na ZRB, siyo wote wanaokuwa VAT registered na ZRB. Kwa hiyo, hiyo ni changamoto ya pili ambayo sisi tulifikiri kwamba ingekuwa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mshairi mmoja anasema kwenye msitari mmoja tu anasema dawa imekuwa sumu nimeila midomoni. Ulifikiria ni dawa lakini kumbe sasa dawa imegeuka imekuwa sumu, hii imekuwa sumu; tuelekee wapi? Basi turudi kwenye marejesho kwa sababu kwenye marejesho lile tatizo linarekebishika kirahisi na kwenye marejesho basi tufungue ESCROW Account katika tatizo hili husika ili kusiwe na kigugumizi katika kurejesheana. Hilo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wa pili; basi tuwe na sheria kama ilivyokuwa proposed, lakini tuongeze isiwe kutoka kwa manufacturer peke yake, lakini pia isiwe kwamba mtu lazima awe VAT registered, lakini tukiiweka vizuri na tukaweka kwamba ni lazima kwamba customs entry point zetu ziwepo kwamba ile entry itakuwa inaonekana kote. Ikiwekwa kwenye entry kwa mtu ambaye ananunua ina maana kwamba hapo hataweza mtu kukimbia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba Serikali ijaribu kutathmini, itazame changamoto ile ya mwanzo na iliyopo sasa hivi ipi kubwa. Hivi sasa hivi malori mengi sana utasikia kwamba yamepakia bia zinataka kusafirishwa kupelekwa Zanzibar lakini ukitazama hao wanywaji wa bia huko Zanzibar na hizo tani ambazo zinakuja zikazunguka humuhumu hazifiki kule, lakini tukiweka hii entry, tukiingiza kwenye entry itaonekana kote kwa sababu tunatumia mfumo mmoja.

Kwa hiyo, naishauri Serikali ijaribu kuweka hii custom entry ambayo itakuwa inaonesha bidhaa inapokwenda na zile zilizotoka zote zitakuwa zinaoneshwa, ikiwa pagumu hapo hatuwezi kutoka, turudie ya zamani, hayakuwa mabaya sana kiasi hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu wa Mwaka 2022
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza napenda kutoa shukrani kwa Mungu na kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa ni dakika tano, nina ujumbe mfupi ambao watu wakiusikiliza vizuri nafikiri hata Wizara ya Fedha hiki kitu watakifanya kwa haraka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mshairi alisema: “Nawauliza nisai na rijali mkiweza, mimi mwenzenu nipo hoi moja linanitatiza, kati ya kuku na yai ni kipi kilichoanza?” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maana, leo hapa tupo katika kutunga sheria ili kuweza kudhibiti, lakini hatuna sera. Sasa kati ya Sera na Sheria, ni ipi iliyotakiwa kuanza?

Kwa hiyo, kama Wizara ya Fedha au Serikali italiona hili, basi kuna umuhimu wa kufanya sera kwa haraka sana ili tuweze kwenda vizuri na kuweza kufuzu katika huko kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie katika reporting persons. Hapa pametajwa wauza magari katika maongezo, Mawakala wa Forodha Clearing Agencies na pia Credit Reference Bureau. Katika kiashiria hiki, ukienda kwenye ripoti ya SM (LAAC); kwenye ripoti ni kwamba hapa sisi tumefanya vizuri, lakini pamoja na kufanya vizuri tukasema tuangalie hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe inzari moja tu. Tukisema tumewaweka hawa na wakati tuna uwezo mkubwa sana wa ku-capture taarifa za hawa ma-agent, TRA kwa maana hiyo inakuwa kama labda tunaweza tukasema kwamba tuna-duplicate. Credit Reference Bureau wao wanachukua taarifa zao za msingi kutoka kwenye mabenki. Wao wanakusanya tu, lakini hizi taarifa wahusika ni wa kutoka kwenye mabenki. Kwa maana hiyo tukisema kwamba naye tumemwingiza hapa, napo kidogo nahisi kama tunaweka mtu ambaye kama hausiki kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu jambo lingine ambalo lilizungumzwa na wengi, hakuna kitambulisho kimoja ambacho kinaweza kikatulinda. Tungekuwa na kitambulisho kimoja kwa hizi taasisi zote, tusingekuwa tunataka taarifa ile ile kutoka kila taasisi. Ingelikuwa tunapata taarifa nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulisema la katika Politically Exposed Person, kuingiza family members; na hasa pale walipotajwa watoto, wazee, wakwe, lakini Serikali imekuja na mabadiliko. Tunashukuru sana, maana hapa ilikuwa tayari ishazuka hofu, leo angetoka Mbunge hapa anakwenda kuposa mahali apewe mke; ina maana kwamba wakimhofia Mbunge huyu anaweza akafanya ufisadi huo, ina maana na wale wakwe nao wanaingia katika Politically Exposed Person kama ni family members. Kwa hiyo, hii at least imetuondolea hofu. Kwa hiyo, hapa tunaishukuru sana Serikali kwa kufanya jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la tatu niliseme haraka haraka ni la Customers Due Diligence. Ni suala zuri, lakini lipunguzwe makali yake kwa sababu hiyo due diligence ambayo tulikuwa tumeisema, ingawa neno “ascertaining” limetolewa na likawekwa “obtaining information,” haidhuru kwamba limekaa vizuri, lakini ingewekwa kama “customers monitoring” ingelikaa vizuri zaidi, kwa sababu “due diligence” ni neno pana. Kwa hiyo, tukisema due diligence maana yake ni kwamba huku mwisho kuna adhabu, (administrative measures), kuna mpaka mtu kuwa convicted. Sasa tunaiweka katika extent ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutashindwa hivyo, kwa maana hiyo sisi tutakuwa tunafuata vigezo vya Kimataifa, lakini kimifumo sisi hatuko sawa. Zile facts ambazo wametoa, vigezo viko juu kwa sababu zile nchi zinajiweza katika mifumo yao. Sisi mifumo yetu bado tunatumia cash economy. Hawa wenzetu wako katika cash less economy, kwa maana hiyo tukiweka due diligence kwa mtu kwa huyo reporting person, sometimes tunaweza tukaja tukawa- commit watu vibaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine naomba nitoe ushauri kwa Serikali ambapo Mheshimiwa Waziri ndio ameanza nalo kuhusu Jina la Muswada. Jina la Muswada wanasema kutakasisha. Kitu kutakasa na kutakata au kutakatisha ni vitu viwili tofauti. Kitu cha kutakasa, haidhuru wamesema wamepewa na BAKITA, lakini BAKITA wana dictionary yao, wamesema kutakatisha na kutakasisha, wametoa tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, laundering ni kutakatisha siyo kutakasisha. Sasa tungeweza kwenda kutazama hili neno vizuri kwasababu wakati mwingine kutakasa tunakuja kwenye jambo la kiroho au kwenye nafsi, ndiyo inaingia kutakasa. Tukisema Mungu ametakasika, basi hata na fedha za kuuzia bangi na gongo nazo zimetakasika? Ukizitoa huko unakwenda kuzitakasa? Tungeenda kwenye neno “kutakatisha,” kwa sababu kutakatisha ndiyo kitu ambacho kinaenda kufuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata leo, ukisema kwamba nguo yangu imetakasika, nimeifua, nimeipeleka laundry, imetakasika, haiji; lakini ukisema nguo yangu imetakata au imetakatika baada ya kuipeleka laundry, hicho ndiyo kipo sawa. Tusiwe kama watu ambao tunaiga Kiswahili, sisi ndio wenye Kiswahili chenyewe. Kwa hiyo, tujaribu kutazama. Ipo dictionary imetolewa na BAKITA ambayo imetolewa na authority ya nchi mbili; Tanzania na Kenya, tukatazame. Tusifundishwe Kiswahili ambacho hakipo sawa. Kutakasa sote tunajua na kutakata tunajua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Fedha wa Mwaka 2022
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwanza kwa kutupa uhai na cha pili kutujalia tukaja hapa tukiwa wazima, na kitu kingine nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nianze na pongezi kwa Serikali kwanza kwa kuleta Muswada huu, lakini cha pili niishukuru Serikali kwa kukubali ushauri na kutengeneza schedule of amendments baada ya kupata ushauri wa Kamati katika masuala ambayo yameletwa mbele ya Kamati. Pia naunga mkono hoja zote ambazo zimewasilishwa na Kamati ya Bajeti ambazo zimelenga kuishauri Serikali katika maeneo mbalimbali katika Muswada huu ambao umeletwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiufupi Muswada huu ulikuwa una Sheria nne ambazo zinakwenda kubadilishwa ili ziende sanjari na ile sheria tuliyoipitisha, ambayo inahusiana na strategic investment, ambayo inakwenda sambamba kwenda kurekebisha sheria ya excise duty, road and fuel tolls sheria ya cooperate tax na VAT kwa ajili ya Kwenda sanjari ili kufanya uwekezaji wa kimkakati uweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, sasa pamoja na hayo ninaushauri ufuatao; ushauri wangu wa kwanza, kwenye punguzo ambalo tumetoa, kuna sheria zimelenga kwenye kupunguza, kwa mfano kuna sheria ina punguza royalty, kuna sheria pia inaweka zero rate, lakini pia kuna pendekezo la sheria hapa ya VAT ya kuweka exemption. Kwa hiyo sheria hizi ambazo zitapunguza mimi nilikuwa nataka kusema msemo mmoja. Tunasema aliyeumwa na nyoka akiona unyasi anashtuka, sasa tumewahi kuwa na sheria ambazo tunatoa punguzo, tumewahi kuwa na sheria ambazo tunaweka zero rate na tumewahi kubadilisha sheria tukaweka exemption kwa ajili ya kuwapa nafuu watumiaji ambao ni wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, lakini sheria hiyo baada ya kupitishwa ikifika kwenye kutumika hatuoni ule unafuu unaopatikana. Ninajaribu kutoa mfano wa sheria hizo; tuliweka hapa zero rate kwenye simu zitakazoingizwa (smartphones) na kwenye sanitary pads lakini baadaye hatukuona bei iliyopungua wala unafuu ambao umepatikana. Kwa hiyo niishauri Serikali, kwenye kulifanyia kazi hili Serikali at least iweke mikataba na watu hawa. Wasipokuja na solution ile ambayo tumeikusudia ina maana kwamba lengo la utungaji au kubadilisha sheria hizi hatuwezi kuufikia. Kwa hiyo niwaambie Serikali kwamba tujaribu kuweka measures ambazo zitadhibitisha na kupata ule unafuu tulioulenga, vinginevyo ndio tutaona huyu ndiye nyoka yule yule.kwa hiyo sasa hivi tunaona unyasi hapa atakuja kutugonga tena.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nizungumzie upunguzaji au kusamehe exercise duty kwaajili ya miradi ya kimkakati. Ni kweli tumepanga bidhaa zitakazoingizwa nchini kwaajili ya miradi ya kimkakati tutoe huo msamaha. Sasa, niishauri Serikali kwamba kabla ya kupitisha kwasababu humu ndani tuna viwanda ambavyo vinaweza vikatoa bidhaa ambazo zinaweza zikawa same na zile ambazo tunataka kuzipa msamaha. Kwa maana hiyo katika miradi ile kwanza tujaribu kuangalie, kwamba Baraza la Mawaziri au NIC wajaibu kuangalia, kwamba kabla ya kukubaliana na hicho kitu kupitishwa at least ijulikane kwamba hicho kitu kinazalishwa nchini, kipo na kinapatikana nchini, ili at least kwamba na sisi viwanda vyetu viweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine katika exercise duty, nazungumzia excise duty ambayo inazungumziwa katika mvinyo wa zabibu. Ninaunga mkono wazo la Serikali kuhusu excise duty kwenye mvingo, lakini tumetoa hiyo excise duty kwa ajili ya kufanya zao la zabibu pamoja na bidhaa zake zitumike. Sasa niishauri Serikali, tujaribu kutafuta matumizi, pamoja na hii ambayo ni hatua ya kikodi lakini baada ya hiyo hatua ya kikodi hebu tukaangalie quality. Wanywaji wa mvinyo wanatazama quality, kwa hiyo na sisi katika viwanda vyetu hivyo hebu tukajaribu Kwenda kufanya kitu amacho kita- improve quality. Tuki-improve quality ya wine ambayo inazalishwa ndani kwa kutumia zabibu yetu basi hapo tunaweza tukapata matumizi ya zabibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine, Serikali ijaribu kufikiria mbali zaidi kuanzisha bidhaa nyingi ambazo zitakuwa zinatumiwa na zabibu au kutoa incentives katika viwanda ambavyo vitazalisha bidhaa nyingi ambazo zinatumia zabibu, hapo tutapata kuzifanya zabibu zetu kuwa zinatumika katika maeneo mengi na badala yake tutaondosha zile zabibu ambazo zipo kwa wananchi ambazo tunasema kwamba zinaharibika. Kingine, tujaribu kukuza teknolojia juu ya utumiaji wa zabibu na bidhaa za zabibu. Pengine inawezekana teknolojia yetu ipo chini, kwa hiyo kila tunachokizalisha hapa haidhuru tutaweka excise duty ndogo; sasa je, kama hakuna teknolojia nzuri Je, hiki kitu kitatumika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali kuhusiana na suala hili, kwamba tujaribu kuwaita wawekezaji wakubwa ambao wataweza kutumia zabibu zetu ili; kwakuwa lengo ni kutaka kuwasaidia wauzaji wa zabibu; hizi zabibu ziweze kutumia lakini watengenezaji wetu wa mvinyo wa zabibu hapa huu ambao wengine wanaita mchuzi wengine wanaita togwa, utakuja kukuta kwamba wanau-store katika maeneo ambayo siyo mazuri. Kwa hiyo Serikali ijaribu ku-facilitate hili jambo ili storage katika masuala haya iweze Kwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, lingine, nitoe ushauri wa jumla. Tumesamehe baadhi ya vitu, vitu ambavyo tumesamehe ni kama vile katika mafuta. Kwenye mafuta huu msamaha ambao tutautoa kwa ajili ya wawekezaji tujaribu kuchukua hatua kuhakikisha mafuta haya ambayo yanaingizwa ndani ya nchi hii ambayo yatakuwa yamesamehewa basi at least yaweze kutumika kwa lengo hilo tu. Na ninaishukuru Serikali kwa hatua ambazo zipo katika mikataba ambazo zinaonesha wazi kwamba nini kitafanyika lakini tuzidi kuwa serious, kwasababu tuliwahi kuwamehe mafuta yanayokwenda kutumika migodini. Mafuta yanayokwenda kutumika migodini yalikuwa yanarudi tena. Watu wana visima vya mafuta, mafuta yale hayatumiki tena kule yanarudi mtaani yanauzwa bei ambayo siyo fair price ambayo biashara nyingine zinakuwa zinapata taabu. Kwa hiyo hili tujaribu kuliangalia kwa vizuri zaidi ili tuweze kulimudu na Kwenda nalo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Naipongeza Serikali kwa kuja na mabadiliko haya. Sasa, kila tulicholenga kutoa nafuu basi kibakie palepale, kwamba kinakwenda kutoa nafuu. Tulicholenga kwenda kuzindisha uwekezaji basi kirudi pale pale na tuona kinafanya hivyo na siyo kuja kushusha biashara nyingine kwasababu ya fursa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2023
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante na awali ya yote kwanza shukrani ni kwake Mwenyezi Mungu aliyetupa uhai lakini pia ametupa uzima leo tumekuja hapa.

Mheshimiwa Spika, kingine, nishukuru sana kupata hii nafasi. Tunataka leo tuwawakilishe Watanzania walio wengi katika nchi yetu hii ambao ni vijana. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa sikivu na kuendelea kuwasikiliza wananchi ambao wanawakilishwa na Wabunge wao ambao tupo hapa kuwasilisha mawazo yao na maono yao. Tunaishuru sana Serikali.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake kwenye ile hotuba yake ya mwanzo, ukurasa wa 142 alizungumzia kuhusiana na kufanya mgawanyo wa one third kutoka katika tozo ya skills development levy kwenda katika Wizara unayoshughulikia vijana na ajira. One third iende kule, one third itakwenda katika mfuko wa mikopo ya elimu ya juu na one third itakwenda katika mfuko wa elimu ya ufundi stadi.

Mheshimiwa Spika, sasa alivyozungumza vile alisema kuwa mabadiliko hayo ya Sheria aliyafanya katika Ibara ya 71 ya hii Sheria ya Mabadiliko ya Sheria ya Fedha, kwa hiyo alitaka kubadilisha kifungu cha 15 aliweka. Lile wazo la kubadilisha kifungu kile cha 75 ni wazo ambalo lilitokana na Kamati ya Maendeleo na Ustawi wa Jamii. Na kwa nini tuliona vile? Tuliona vile kwa sababu kuna makubaliano ya hii skilled development levy, one third iende katika Wizara inayoshughulikia ajira na vijana na kwa sababu tumeliona wimbi la vijana la kukosa ajira.

Mheshimiwa Spika, na yote haya yametokana na kwamba ulifanyika utafiti. Utafiti uligundua kwamba tuna nguvu kazi ambayo ni zaidi ya vijana milioni 23. Lakini katika nguvu kazi hii ni asilimia 3.6 pekee ndiyo nguvu kazi ambayo ina kiwango cha juu cha ujuzi. Na kiwango cha juu cha ujuzi kinatakiwa at least kufikia asilimia 12. Na Wizara ambayo ina ratibu nguvu kazi tunajua kwamba ni Wizara hii ya vijana. Kwa hiyo lile wazo la mwanzo la kuleta Sheria ya kwamba one third iende kule lilikuwa ni ombi. Na kwa sababu kule kuna vijana wengi sana wanashindwa ku-cope kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, leo hii tukienda katika SGR utakuta kwamba wafanyakazi wengi ambao wanakiwango cha ujuzi cha juu au kati ni wa kutoka nje wakati vijana wetu wapo. Kama tuungewafunza na tungewasimamia ingekuwa haina haja ya hizo ajira kuchukuliwa na watu wengine. Lakini isitoshe, tukitazame leo, tumekwenda zetu kule Arusha tuliangalia tukakuta kwamba watu wamefundishwa jinsi ya kulima kupitia halmashauri, wanaita green house, lakini ukitizama katika Green House zile imefanyika katika Halmashauri chache sana na sisi tuna halmashauri nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, lakini isitoshe sasa hivi utalii umekuwa ni mkubwa sana. Watalii wengi sana na hatuna watu wa kuweza kwenda kuwahudumia. Kwa hiyo ilikuwa ni muhimu hii one third. Mheshimiwa Waziri angeliacha kule kule. Maelezo ya leo ya Mheshimiwa Waziri, alisema kwamba kifungu hicho kwamba kinaondolewa, kwamba haya mabadiliko ya kwenda kwenye one third yanaondolewa.

Mheshimiwa Spika, mimi pendekezo langu, Waheshimiwa Wabunge, sisi tuna vijana wengi ambao leo tunatamani wawe na ujuzi, ujuzi huo uwasaidie katika kupata ajira. Hawa vijana ndio nguvu kazi yetu sisi. Sisi leo tunakwenda mbele lakini ni kwa sababu ya vijana, matukio yote ni vijana. Sasa hii nguvu kazi ambayo kwamba leo tunakataa kwenda kuisimamia kupata ujuzi kwa ajili ya kujiajiri, tukisema tunaondosha one third tunaiacha vile vile ina maana kwanza hizi fedha hazitawafikia.

Mheshimiwa Spika, niseme neno moja, ilikubalika tangu mapema kwamba one third iende kule kwa sababu two third inakwenda Katika mfuko wa elimu ya juu. Sasa two third kule kupeleka one third ilikuwa haiendi zinakwenda bilioni tisa tu peke yake, sasa zikienda bilioni tisa vijana wanaokwenda kule kupata yale mafunzo wanakuwa ni vijana wachache, ndiyo maana tulipendekeza iwepo hiyo one third. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, mabadiliko ambayo anataka kuyafanya katika kifungu cha 71 cha kwamba bado two third ibakie kule katika elimu ya juu arudishe huku kwa sababu kuna vijana tunawatarajia.

Mheshimiwa Spika, kuna msemo mmoja ambao unasemwa kwamba thamaa amalal mousa ila dhuriyah, hakuna watu waliomwamini Musa isipokuwa vijana. Vijana ndio waliomwamini Musa na vijana ndio waliompa Musa nguvu na sisi tuna vijana. Hawa vijana wakitukimbia sisi tunaelekea wapi? Hawa vijana hii fedha wanapelekewa ikawatengenezee ajira zao wapate ujuzi. Leo zinazalishwa product lakini product ziko finyu, ni kwa sababu vijana hawana ujuzi, sasa leo tumetenga fedha kwa ajili ya kuwapa vijana ujuzi tukaenda tukaiondosha.

Mheshimiwa Waziri naomba uirejeshe, hii schedule of amendment ni sawa utaleta schedule of amendment lakini one third ibakie pale pale, unasema umekubaliana na Kamati ya Bajeti lakini Kamati hii ya Ustawi wa Jamii tumepita maeneo mengi tumeona hawa vijana na mahitaji hayo yapo kwa sababu vijana wapo. Tuna vijana milioni 23, leo waliokuwa skilled ni asilimia tatu tu, tunakwenda katika viwanda hivyo tutaviendeaje kama watu wetu wana ujuzi wa kiwango cha chini? Watu wa kiwango cha chini ujuzi wao ni zaidi ya asilimia 70, leo tunataka kukuza ujuzi kwa vijana, kwamba tunataka kupunguza hiyo fedha.

Mheshimiwa naomba hii fedha uiache kwa vijana, hawa vijana hata mama naye anawategemea, na mimi pia nawategemea hawa vijana na ninyi Majimboni kwenu Waheshimiwa mnawategemea hawa vijana. Mheshimiwa Mwigulu hii one third…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: …ibakishe iende kwa vijana maana tuna tatizo la ajira kwa vijana. Hawa vijana hawawezi wote kwenda Serikalini. Hapa kila mmoja kapigiwa simu ya ajira na vijana, sasa fedha ziko zinaweza zika-mobolize vijana wetu wakapata ajira sasa leo unaziondoshaje? Tunaomba tuachie hii one third ije.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja lakini Mheshimiwa hili lifanye kwa ajili ya vijana wetu. Nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)