Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Doto Mashaka Biteko (7 total)

MHE. DOTO M. BITEKO aliuliza:-
Je, kwa nini Serikali inachukua muda mrefu sana kurekebisha mishahara ya Walimu baada ya kupandishwa vyeo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, Mbunge wa Bukombe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba miaka ya nyuma kulikuwepo na ucheleweshaji wa kurekebisha mishahara kwa kuwa mfumo wa taarifa za kiutumishi na mishahara wa wakati huo ulimtaka kila Mwajiri kuwasilisha marekebisho ya Watumishi wake Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka 2012 Mfumo huu wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara uliimarishwa kutoka Toleo la 7 kwenda Toleo la 9 la Lawson ambapo mwajiri alisogezewa huduma ya kufanya marekebisho mbalimbali ya kiutumishi yanayotokea katika ofisi yake bila ya kulazimika kusafiri kwenda Dar es Salaam. Utaratibu huu umekuwa na manufaa ambapo kwa sasa mabadiliko mbalimbali ya kiutumishi yanafanywa na mwajiri kwa kuzingatia mzunguko wa malipo ya mishahara kwa kila mwezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na utaratibu huu mzuri, mazingira machache yanayoweza kuchelewesha marekebisho ya mishahara kufanyika kwa wakati, kutokana na kuingizwa kwa taarifa za watumishi kwenye mfumo baada ya orodha ya malipo ya mishahara katika mwezi husika kufungwa, au waajiri kufanya mabadiliko bila ya kuweka taarifa muhimu hususan viambatisho kama vile barua za kupandishwa cheo na taarifa kutumwa, zikiwa na makosa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kupitia Bunge lako Tukufu, kuwataka waajiri wote kufanya marekebisho ya mishahara kwa watumishi wote kwa wakati kama ambavyo imekuwa ikielekezwa na Serikali ili kuepusha ucheleweshaji wa haki za watumishi.
MHE. DOTO M. BITEKO aliuliza:-
Maafisa wa Idara ya Misitu walivamia wananchi wa kitongoji cha Idosero kilichosajiliwa kwa GN na kuchoma nyumba 40 za wananchi na kuharibu mazao yao.
Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Idosero kwa hasara kubwa waliyopata?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, Mbunge wa Jimbo la Bukombe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Idosero limo ndani ya misitu ya Biharamulo na Kahama yenye jumla ya hekta 134,684 iliyoanzishwa kwa sheria, Sura ya 389, Nyongeza ya 59 ya mwaka 1954 na kufanyiwa marekebisho kwa Tangazo la Serikali namba 311 la mwaka 1959. Misitu hii kwa sasa inasimamiwa na Sheria ya Misitu Sura ya 323 Toleo la mwaka 2002.
Mheshimiwa Naibu Spika, mnamo tarehe 07 Novemba, 2015 Maafisa kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe walifanya operesheni ya kuhamisha wavamizi katika misitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakazi wa eneo la Idosero walianza kuingia na kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya misitu hii mwaka 1985 na uvamizi uliongezeka hatua kwa hatua na kukithiri baada ya kutolewa kwa Tangazo la Serikali Namba 221 la tarehe 27 Juni, 2015 lililolipa eneo hilo hadhi ya kitongoji kipya katika kijiji cha Nampalahala, bila kubainisha mipaka ya kitongoji hicho. Tamko hilo lilikizana na matangazo ya Serikali yaliyopita au yaliyotangulia na Sheria ya Misitu Sura ya 323 ya mwaka 2002 yanayotambua kuwa eneo hilo ni hifadhi ya misitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hali hiyo, Kamati ya Ulinzi na Usalama yaWilaya ya Bukombe ilifanya mkutano na wakazi wa eneo la Idosero tarehe 08 Mei, 2015 na kuwataka waondoke kwa hiari yao ifikapo tarehe 08 Julai, 2015. Wakazi hao walikaidi amri hiyo kwa madai kuwa eneo hilo si hifadhi kwa kuwa Tangazo la Serikali Namba 221 limetambua eneo hilo kuwa ni kitongoji cha makazi. Aidha, mnamo tarehe 09 hadi 20 Juni, 2014 Serikali ilifanya sensa ya kuhesabu watu na kubaini kuwepo kwa kaya 309 zenye jumla ya wakazi 2,777 ndani ya eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza Sheria ya Misitu Sura ya 323 ya mwaka 2002, watumishi wa TFS au Mamlaka ya Misitu walifanya zoezi la kuwaondoa wavamizi katika eneo hilo ambalo hata hivyo halifanikiwa na wananchi bado wanaendelea kuhamia na kupanua shughuli za kibinadamu katika misitu hiyo na kuendelea kufanya uharibifu wenye athari kubwa za kimazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyokwishaeleza katika majibu ya msingi na nyongeza yaliyopita kwa maeneo yenye changamoto zinazofanana na hii utatuzi wa mgogoro huu utapatikana wakati wa zoezi la pamoja la utatuzi wa matatizo ya ardhi linalotarajiwa kuanza baada ya kukamilika kwa shughuli za Mkutano wa Tatu wa Bunge la Kumi na Moja.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA (K.n.y MHE. DOTTO M. BITEKO) aliuliza:-
Wakulima wa pamba Wilaya ya Bukombe na Geita kwa jumla katika msimu wa mwaka 2015 walipatiwa mbegu na dawa yasiyokuwa na ubora ambayo hayakuua wadudu.
Je, Serikali inawaambia nini wakulima walioathirika na pembejeo hizo na inachukua hatua gani kuhakikisha jambo hili halijirudii tena?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dotto Mashaka Biteko, Mbunge wa Bukombe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepata taarifa kuhusu tatizo lililowapata wakulima wa pamba katika maeneo mbalimbali ikiwemo wale ikiwemo wale wa Mkoa wa Geita kwa kusambaziwa mbegu ambazo hazikuwa na ubora unaotakiwa. Aidha, katika msimu wa kilimo wa mwaka 2015/2016, viuatilifu vilivyosambazwa kwa wakulima vilishindwa kudhibiti wadudu wa pamba kikamilifu katika maeneo mengi ikiwemo Mkoa wa Geita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ununuzi wa pembejeo za zao la pamba unaratibiwa na Mfuko wa Kuendeleza Zao la Pamba (CDTF), usambazaji wa pembejeo hizo baada ya ununuzi unaishirikisha Bodi ya Pamba. Kufuatia taarifa za uwepo wa pembejeo hafifu hususan viatilifu Serikali iliagiza TPRI kufanya uchunguzi wa malalamiko ya wakulima. Uchunguzi ulibaini kwamba kiuatilifu kinachofahamika kwa jina la Ninja 5EC ndicho kilichokuwa kinalalamikiwa na wakulima kwa utendaji hafifu. Uchunguzi zaidi ulionesha kwamba baadhi ya sumpuli za kiuatilifu hicho zilikuwa na kiwango kidogo cha kiambato amalifu (active ingredient) ya kinachotakiwa, hivyo, kiuatilifu hicho hakingeweza kuua wadudu waliolengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa za uchunguzi uliofanywa na TPRI, Bodi ya Pamba, CDTF, wawakilishi wa wasambazaji, wakulima na wadau wengine zimeonesha kwamba viuatilufu hivyo vya Ninja 5EC (Batch Na 2014102001 na KR4003) vilinunuliwa kutoka Kampuni ya Positive Internatinal Limited na kusambazwa na UMWAPA na kutoka Kampuni ya Mukpar Kagera Limited (Batch Na. KR1400451103) na kusambazwa na Mfuko wa Kuendeleza zao la Pamba. Aidha, uchunguzi unaonesha kwamba kuna batches za viuatilifu za mwaka 2014/2015 zilisambazwa pia, ambazo inawezekana kama hazikutunzwa vema ubora ungeweza kuwa na mashaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kwamba matumizi ya kiutalifu hafifu kwa mujibu wa uchunguzi huu kilikuwa na athari kwa wakulima. Kufuatia taarifa hizo za uchunguzi Serikali inakamilisha taratibu za kuchukua hatua za kisheria kwa wale wote waliyohusika na kadhia hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia changamoto za utoaji wa mbegu za pamba ambazo unatokea, Serikali katika msimu wa mwaka 2016/2017 iliamua kufanya majaribio ya utoaji wa mbegu za pamba ambazo zimekuwa zikisambazwa hapo awali bila kujua ufanisi katika utoaji wake. Matokeo ya majaribio ya utoaji yamewezesha kutoa maelekezo kuhusu batches za mbegu za pamba zenye sifa za msingi kusambazwa kwa wakulima katika msimu wa kilimo wa mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha jambo hili halijirudii tena, Serikali itaanza kuzalisha mbegu bora za pamba za UKM08 katika mashamba maalum ili hatimaye baada misimu miwili ya kilimo wakulima wote waweze kupata mbegu bora za pamba.
MHE. DOTO M. BITEKO aliuliza:-
Wakati wa Kampeni za Mwaka 2015, Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania aliahidi kilometa tano kwenye Mji wa Ushirombo:-
Je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, Mbunge wa Bukombe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za Mji wa Ushirombo zinahudumiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe. Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali imekusanya ahadi zote za viongozi na kuweka utaratibu wa jinsi ya kuzitekeleza, ikiwemo ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara zenye jumla ya urefu wa kilometa tano zilizoahidiwa na Mheshimiwa Rais mwaka 2015, Mjini Ushirombo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msimamo wa Serikali ya Awamu hii ya Tano ni kuhakikisha kuwa inatekeleza ahadi zake zote katika kipindi cha miaka mitano.
MHE. DOTO M. BITEKO aliuliza:-
Wilaya ya Bukombe ina mahitaji ya walimu wa shule za msingi 1,425; waliopo ni walimu 982 na upungufu ni walimu 443:- Je, ni lini Serikali itapeleka walimu wa shule za msingi wa kutosha kuondoa upungufu huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, Mbunge wa Bukombe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua upungufu wa walimu uliopo nchini ambapo mahitaji ya walimu wa shule za msingi ni walimu 235,632; waliopo ni walimu 188,481 na upungufu ni walimu 47,151.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imejipanga kuajiri watumishi wa kada mbalimbali wakiwemo walimu wa shule za msingi ili kupunguza pengo lililopo. Aidha, Serikali inakamilisha mpango wa kuwahamishia shule za msingi walimu wa ziada wa masomo ya sanaa wanaofundisha shule za sekondari. Utaratibu huu utasaidia shule za msingi kupata walimu wa kutosha ili kuboresha taaluma.
MHE. DOTO M. BITEKO aliuliza:-
Askari wa Wilaya ya Bukombe wanazo changamoto nyingi zikiwemo ukosefu wa nyumba za askari.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia nyumba askari hao katika Wilaya ya Bukombe?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu Sali la Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, Mbunge wa Bukombe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli Jeshi la Polisi lina changamoto mbalimbali ikiwemo uchache wa nyumba za kuishi askari. Wilaya ya Bukombe ambayo ina jumla ya maafisa wakaguzi na askari 122 ni miongoni mwa Wilaya zenye changamoto za uhaba wa nyumba za kuishi askari.
Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga nyumba za kuishi askari katika mikao ya wialaya kwa awamu. Katika Wilaya ya Bukombe, Jeshi la Polisi lipo kwenye mazungumzo na Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe ili kupatiwa eneo kwa ajili ya kujenga nyumba za kuishi askari. Baada ya kupatiwa eneo hilo Serikali itajenga nyumba hizo kwa fedha za bajeti kwa kadri fedha zitakavyopatikana kwa jinsi ilivyotengwa pamoja na kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA (K.n.y. MHE. DOTO M. BITEKO) aliuliza:-
Je, ni kwa nini Serikali ilihamisha madaktari saba kwa mara moja kutoka Hospitali ya Wilaya ya Bukombe huku ikijua Wilaya ya Bukombe ina upungufu mkubwa wa madaktari?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilihamisha madaktari sita katika Hospitali ya Wilaya ya Bukombe ikiwa ni utaratibu wa kawaida wa kuimarisha ufanisi katika utoaji wa huduma za afya kwa wagonjwa. Ili kuziba nafasi za waliohamishwa kwa lengo la kutoathiri utoaji wa huduma za afya hospitalini hapo, Halmashauri hiyo ilipelekewa madaktari wapya watano na badaye Serikali ilipeleka madaktari wengine watatu na kufanya jumla ya madaktari waliopelekwa Bukombe kuwa nane. Lengo lilikuwa ni kuboresha utoaji wa huduma katika hospitali hiyo.