Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Juma Othman Hija (82 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natoa shukrani zangu za dhati kwa Rais wa Awamu ya Tano Mheshimiwa John Magufuli kwa imani na uwezo mkubwa alionao katika kuendeleza Taifa letu. Pia napenda kuwapongeza Mawaziri wote kwa juhudi wanazoonesha katika kuendesha Wizara zao. Vile vile nachukua nafasi hii kuwashukuru wananchi wote wa Jimbo la Tumbatu kwa imani waliyonipa kwa kunichagua kuwawakilisha katika Bunge lako Tukufu. Naahidi nitaendelea kuwatumikia kwa uwezo wangu wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, napenda kutoa mchango wangu katika sehemu ifuatayo:
Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma; Katika sehemu hii imeelezwa kuwa, Serikali imetoa elimu kwa Viongozi wa Umma wapatao 3,980 katika sehemu tofauti, ikiwemo Walimu kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, mgongano wa maslahi na maadili ya Utumishi wa Umma kupitia semina, midahalo, mafunzo na vikao mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika sehemu hii naiomba Serikali ieleze ni Viongozi wa ngazi gani walipata mafunzo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naanza kwa kumshukuru Mungu aliyeniwezesha kuwa miongoni mwa Wabunge wa Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nawashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Tumbatu kwa imani yao kubwa waliyonipa, kwa kunichagua kuwa Mbunge wao kwa kura nyingi sana. Natambua imani yao kwangu na nawaahidi kuwa sitawaangusha.
Tatu, natoa pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa John Pombe Magufuli, kwa imani na uwezo mkubwa aliouonesha katika kulitumikia Taifa letu. Namwomba Mungu ampe kila jema katika uongozi wake huu.
Nne, napenda kumpongeza Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa pamoja na Baraza lake lote la Mawaziri kwa kuonesha uwezo mkubwa wa uongozi katika sehemu zao za kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naanza kwa kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uwezeshaji wa wavuvi na wakuzaji viumbe kwenye maji; katika sehemu ya ruzuku za zana za uvuvi, Serikali imetenga shilingi milioni 400 ambazo zilitumika kwa ununuzi wa zana za kilimo, zikiwemo mashine za boti. Pesa hizi ni kidogo sana kwa matumizi ya nchi nzima. Ushauri wangu ni kwamba Serikali iongeze kima hiki cha fedha. Aidha, Serikali iongeze mchango wake kutoka asilima 40 angalau kufikia asilimia 50 ambazo zitawawezesha wavuvi kununua zana hizo za uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwenye ukurasa wa 61, imeeleza kwa ufupi sana juu ya elimu ya maradhi ya UKIMWI. Nashauri kwamba elimu hii iongezwe kwa kiwango kikubwa ili kuwapa weledi zaidi wananchi juu ya ujinga na hatimaye kuepuka kabisa maradhi haya thakili.
Mheshimiwa Naibu Spika, nahitimisha mchango kwa kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naanza kuchangia hotuba hii kwa kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwa miongoni mwa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Pili, napenda kuwashukuru wapigakura wangu kwa kuniamini na kunichagua kwa kura nyingi. Natambua imani yao kwangu na nawaahidi kuwatumikia kwa nguvu zangu zote. Tatu, napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Magufuli kwa kuonesha imani na uwezo mkubwa wa kuendesha nchi.
Nne, napenda kumpongeza Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa pamoja na Baraza lote la Mawaziri kwa kuonesha uwezo mkubwa wa kuongoza Wizara zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii ya Elimu, napenda kuchangia maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ada za vyuo binafsi nchini. Serikali imekuwa na nia nzuri ya kuruhusu vyuo binafsi nchini, hili ni jambo zuri na la maana; masikitiko yangu katika hili ni pale inapoonekana baadhi ya vyuo kutoza ada kwa kulipa fedha za kigeni badala ya fedha ya Tanzania. Miongoni mwa vyuo hivyo ni Chuo cha Kampala (Kampala International University) kilichopo Gongo la Mboto Dar es Salaam. Namwomba Mheshimiwa Waziri kuliangalia suala hili na kuweka utaratibu maalum na kuwalazimisha walipishe wanafunzi kwa pesa za Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, usimamizi wa utekelezaji wa programu na miradi. Katika kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 67, 109 imeeleza namna inavyoendeleza kutekeleza Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES II). Huu ni mpango mzuri na napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa jambo hili. Napenda kumshauri Mheshimiwa Waziri, katika kutekeleza ujenzi wa majengo haya ya sekondari na hata yale ya primary ni vyema ikazingatia kujenga majengo hayo kwa kuzingatia kuwepo kwa wanafunzi wenye uhitaji maalum ili na wao waweze kutumia majengo hayo bila ya usumbufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, naanza kuchangia hotuba hii kwa kumshukuru Mungu kwa kunijalia kuwa miongoni mwa Wabunge wa Bunge hili lako Tukufu.
Pili, nachukua fursa hii kwa kuwapongeza wananchi wangu wa Jimbo la Tumbatu kwa kunichagua kwa kura nyingi kuwa Mbunge wa Bunge hili. Natambua imani kubwa waliyonayo kwangu na naahidi sitawaangusha.
Tatu, napenda kumpongea kwa dhati Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli kwa kuonesha imani na uwezo mkubwa wa kuongoza nchi yetu. Aidha, napenda kumpongeza Waziri Mkuu Mheshimiwa Majaliwa pamoja na Baraza lake la Mawaziri kwa uimara wao katika kuongoza Wizara zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tozo la KUA katika Kisiwa cha Zanzibar. Kwanza napenda kutoa masikitiko yangu makubwa kuona kwamba katika hotuba yote ya Mheshimiwa Waziri Zanzibar haikutajwa hata kidogo pamoja na kwamba ni miongoni mwa wateja wakubwa wa TANESCO.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, namwomba Waziri anieleweshe, kwa nini Zanzibar inatozwa bei kubwa ukilinganisha na wateja wengine? Kwa mfano, KUA moja inatozwa sh. 16,550/= kwa Zanzibar lakini kwa wateja wengine KUA moja (KUA) inatozwa sh. 13,200/=.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Serikali kwa juhudi inayochukuwa katika kuwapelekea wananchi huduma hii katika vijiji vyao. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri haikuzungumza vijini na maeneo yaliyosambaziwa umeme. Naomba Mheshimiwa Waziri aoneshe maeneo hayo (locations) na kiwango cha usambazaji (Kms) uliofanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia hali ya ujenzi wa line hizo haioneshi kama zimejengwa kwa wataalam wa mambo ya umeme. Inaonekana kuwa hakuna design yoyote iliyofanyika kabla ya kujengwa line hizo. Ni vyema, Makandarasi kwa usimamizi wa TANESCO wakalazimishwa kuwa na design pamoja na profiles ya kazi hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kawaida lifetime ya nguzo za umeme huwa ni zaidi ya miaka 20 lakini nguzo ambazo zinatumika katika kazi hii hasa za REA hazioneshi umadhubuti halisi kwa kazi hii. Hivyo nakuomba Mheshimiwa Waziri anieleze lifetime ya nguzo hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naanza kuchangia hotuba hii kwa kumshukuru Mungu aliyeniwezesha kuwa miongoni mwa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nachukua fursa hii kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Tumbatu, kwa kunichagua kwa kura nyingi kuwa Mbunge wao, natambua imani kubwa waliyonayo kwangu na naahidi kuwatumikia kwa nguvu zangu zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, napenda kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa kuonesha imani na uwezo mkubwa wa kuiongoza nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, napenda kumpongeza Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa pamoja na Baraza lote la Mawaziri kwa kuonesha umahiri wa kuongoza katika Wizara zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu udhibiti wa migogoro ya ardhi nchini yanaongezeka siku hadi siku. Hii inasababishwa pamoja na mambo mengine, uhaba wa ardhi inayosababishwa na ongezeko la watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la ongezeko la watu namshauri Mheshimiwa Waziri achukue hatua ya kushirikiana na Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani kuangalia kwa makini uingiaji wa wakimbizi ambao nao pia wanasababisha ongezeko la watu nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, teknolojia ya habari katika kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 27 (36) amezungumzia juu ya teknolojia hii, ni teknolojia inayohitaji ujuzi mkubwa. Ushauri wangu ni kwamba kazi hii pamoja na kupewa makandarasi, Wizara ichukue juhudi za makusudi kuwaelimisha wafanyakazi wazalendo ili kwa baadae kuepuka na hasara za kuwapa kazi makandarasi badala yake kazi hizo zifanywe na wafanyakazi wa Wizara hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mipaka ya Kimataifa, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 34 (46) Waziri ameelekeza namna ya juhudi inayochukua juu suala hili la mipaka ya Kimataifa. Mheshimiwa Waziri ameeleza kukwama kwa upimaji wa mipaka kati ya Tanzania na Burundi. Namuomba Mheshimiwa Waziri anieleze ni kiasi gani kazi hiyo imeathiri zoezi hili kutokana na hali aliyoieleza kuwa ni ya kisiasa.
Mheshimwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naanza kutoa mchango wangu kwa kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwa Mbunge wa Bunge hili. Pili nawashukuru wapiga kura wangu kwa kunichagua kwa kura nyingi kuwa Mbunge wao, natambua imani kubwa waliyonayo kwangu na nawaahidi nitawatumikia kwa nguvu zangu zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kuonesha imani na uwezo mkubwa wa kuendesha nchi yetu, Mungu ampe umri na afya njema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nne napenda kumpongeza Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa pamoja na Baraza lake la Mawaziri kwa kuonesha uwezo mkubwa wa kuongoza Wizara zao. Katika kuchangia hotuba ya Waziri napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sekta ndogo ya ufugaji, kumekuwa na migogoro isiyomalizika kati ya sekta ya ufugaji na wakulima. Hili ni tatizo ambalo Wizara hii inapaswa kulishughulikia kwa namna ya pekee. Naomba Wizara ianzishe idara maalum ndani ya Wizara hii ya kushughulikia migogoro hii ili kuondosha kabisa tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sekta ndogo ya utalii, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 15 imeeleza hali ya sekta hii inavyochangia upatikanaji wa fedha. Takwimu zinaonesha kwenye ukurasa huu ni ndogo, hazilingani na namna uingiaji wa watalii katika nchi yetu. Watalii wanaoingia ni wengi sana hivyo nashauri Wizara ichukue mikakati zaidi ya kuziba mianya ya upotevu wa fedha za watalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mamlaka ya usimamizi wa wanyama pori. Nachukua fursa hii kuipongeza Wizara kwa kuanzisha mamlaka hii ni jambo zuri katika kusimamia na kuwalinda wanyama pori wetu. Nashauri Wizara iharakishe kupeleka mamlaka hii katika Wilaya zote za nchi ili huduma hii ipatikane nchi nzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naanza kuchangia hotuba hii kwa kumshukuru Mungu kwa kunijalia kuwa miongoni mwa Wabunge wa Bunge hili. Pili nachukua fursa hii kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuonesha imani na uwezo mkubwa wa kuongoza nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, nawapongeza wapiga kura wangu kwa kunichagua kwa kura nyingi kuwa Mbunge wao. Natambua imani yao kubwa waliyonayo kwangu na nawaahidi sitowaangusha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, sifa na muda wa wafanyakazi wa Ubalozini. Napenda kuipongeza Wizara na Serikali kwa jumla kwa utaratibu mzuri wa kuwapangia na kuwateua wafanyakazi wa Balozi zetu. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri ni sifa gani wanazotumia katika kuwateua wafanyakazi wetu pamoja na Mabalozi katika nchi za nje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Chuo cha Diplomasia. Nachukua nafasi hii kuipongeza Wizara kwa kukiendeleza chuo hiki muhimu katika kuzalisha na kutayarisha wataalam wetu. Chuo hiki kama vilivyo vyuo vingine kinahitaji mahitaji kama vile mikopo na kadhalika. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri kuna mpango gani wa mikopo kwa wanafunzi wanaosoma katika chuo hiki?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jumuiya ya Afrika ya Mashariki. Jumuiya hii ni ya muda mrefu na ina uzoefu mkubwa. Napenda kueleza wasiwasi wangu juu ya ongezeko la nchi wanachama wa jumuiya hii. Nchi hizi zilizo nje ya Afrika Mashariki zina matatizo makubwa katika nchi zao na ndiyo wanaotuongezea watu katika mipaka yetu. Aidha, zimetuongezea uhalifu na ujangili na matatizo mengine. Hivyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hili na wasite kuongeza wanachama walioko nje ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Watendaji wake kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kutengeneza Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia Mpango huu kwenye maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina azma nzuri katika kuelekea katika uchumi wa viwanda. Hili ni jambo jema sana litakaloivusha nchi yetu katika kuelekea kwenye uchumi mzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika miaka ya 1970 tuliweka viwanda vingi sana ambavyo kwa sasa vimepoteza uwezo wake na vingine vimekufa kabisa. Hivyo, kwanza naishauri Serikali iangalie sababu za kuanguka kwa viwanda hivyo. Sababu hizo ndizo zitakazotuongoza kuelekea kwenye azma hii baada ya kuzifufua.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ni vyema Serikali ianze kujiandaa kwa kutayarisha rasilimali ambazo zitaweza kukabiliana na suala hili. Miongoni mwa rasilimali hizi ni rasilimali watu (HR). Serikali ianze kuwasomesha watu wetu badala ya kuja kutegemea wataalam kutoka nje ya nchi kama ilivyo katika sekta nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia kwa maandishi Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim M. Majaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri yenye mwelekeo na dira ya utekelezaji wa maendeleo ya Serikali yetu. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-
Maeneo ya huduma za Kiuchumi; napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kasi kubwa ya maendeleo inayochukua kasi za maendeleo katika maeneo kadhaa kama vile umeme, barabara, reli na usafiri wa anga ni mkubwa na ni wa kutia moyo kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika eneo hili la huduma za kiuchumi ni kwamba, naiomba Serikali kuwa makini kwa kuangalia viwango vya miundombinu hii ili kuepuka hasara za matengenezo ya muda mfupi mara baada ya makabidhiano ya miundombinu hii. Serikali
imekuwa ikitumia fedha nyingi kwa matengenezo ya miundombinu ambayo mara nyingine sio ya lazima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia fursa hii ya kutoa mchango kwa njia ya maandishi. Napenda kumpongeza Waziri wa Katiba na Sheria yeye pamoja na wataalam wake kwa kuandaa hotuba hii yenye kuonesha ubora na utaalam mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, urejeshwaji wa wahalifu na ushirikiano na Mataifa kwenye makosa ya jinai, hili ni jambo zuri ambalo linaongeza ushirikiano na mahusiano mazuri kwa Mataifa ya nje. Uhalifu ni jambo baya ambalo linahitaji kupigwa vita kwa nguvu zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika suala hili, Serikali iwe makini katika utekelezaji wake. Inapotokelezea ulazima wa kuwapeleka wananchi wetu (wahalifu) ni vyema tukaangalia usalama wa nchi tunayotaka kuwapeleka. Kwa mfano; juzi imetokezea wahalifu wa biashara ya unga ambao wanafika kupelekwa Marekani lakini hivi sasa katika nchi ya Marekani kuna vita ya maneno kati ya Marekani na Korea ya Kaskazini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii inatisha na ni vyema tukachukulia tahadhari kubwa. Korea ya Kaskazini wametishia na wanaendeleza vitisho la kuipiga Marekani kwa silaha za nuclear, hii ni hatari kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo ya rasilimali watu, rasilimali watu ni jambo jema katika sehemu zote za maendeleo. Ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba, Serikali ni vyema ikawatayarisha kwa kuwasomesha na kuwapatia elimu juu ya masuala ya kisheria ili kuendeleza ufanisi katika Wizara hii nyeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii kutoa mchango wangu kwa kuandika katika Wizara hii. Pia napenda kuchukua fursa hii kutoa pongezi zangu kwa Serikali yetu namna inavyotekeleza kwa kasi ahadi zake na huduma za jamii. Vile vile, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na Watendaji wake kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali kwa juhudi zake za kujenga barabara na madaraja. Hii ni azma nzuri ya kuwarahisishia wananchi usafiri wa kupeleka mazao yao katika sehemu moja kwenda nyingine. Ushauri wangu katika jambo hili ni kushauri Serikali iwe makini katika kuwasimamia Makandarasi ili kukidhi viwango vya miundombinu hii. Miundombinu hii itakapokidhi viwango, itaiepushia Serikali gharama za ukarabati wa muda mfupi baada ya kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Posta Tanzania (TTCL) ni chombo muhimu katika kila nchi pamoja na Tanzania. Naipongeza Serikali kwa kuonesha nia ya kuliboresha shirika hili. Ushauri wangu katika uimarishaji wa shirika hili ni kwamba Serikali ilipatie shirika vifaa vya kisasa ili kwenda sambamba na ushahidi mkubwa uliopo katika wakati huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kutoa mchango wangu kwa maandishi kuhusiana na hotuba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumpongeza Waziri pamoja Watendaji wake kwa kuandika hotuba hii kwa ufundi na utaalam mkubwa, namwombea kila la kheri katika kuiongoza Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu rasilimali watu katika sekta ya afya. Rasilimali watu ni miongoni mwa jambo muhimu katika nchi hasa katika Wizara kama hii ambayo inahitaji utendaji wa kitaaluma zaidi. Ushauri wangu katika Wizara hii ni kuongeza juhudi ya kuwasomesha Watanzania katika fani zote hasa ya udaktari ili kupunguza pengo kubwa lililopo kati ya Madaktari na wanaohudumiwa. Takwimu zinaonesha kuwa uwiano (ratio) kati ya Madaktari na wagojwa ni mkubwa sana. Hivyo juhudi za makusudi zinahitajika ili kuondoa kabisa tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba kuongelea kuhusu uboreshaji wa huduma za uchunguzi. Uchunguzi wa maradhi ni hatua muhimu sana katika matibabu. Mgonjwa anapochunguzwa na kuonekana kinachomsumbua ni mwanzo mzuri wa matibabu. Ushauri wangu katika jambo hili ni kwa Serikali kuongeza fedha za kutafutia vifaa vya kisasa zaidi vinavyoweza kuchunguza maradhi kwa ubora zaidi. Kuna matukio mengi ambapo wagonjwa wanachunguzwa na kupewa majibu ambayo ni tofauti na maradhi yanayowasumbua. Hii ni kutokana na kutumia vifaa ambavyo havina ubora. Hivyo juhudi za makusudi zinahitajika ili kuondoa tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni kuhusu udhibiti wa UKIMWI. Naipongeza Wizara kwa juhudi kubwa inayochukua kudhibiti na kuwahudumia waathirika wa maradhi ya UKIMWI. Napenda kuishauri Wizara kuongeza juhudi ya kutoa elimu kwa wananchi hasa wa vijijini ili kuelewa zaidi sababu zitakazowafanya wapate maradhi hayo. Inaonekana kuwa elimu ya UKIMWI inatolewa zaidi katika miji na kidogo sana katika vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia kwa maandishi hotuba hii ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika kwa ufanisi hotuba ya Wizara yao. Nawaombea kila la kheri katika majukumu yao.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC); Shirika la habari ni chombo muhimu katika nchi kwa kuelimisha na kupasha habari wananchi wake. Bado kuna matatizo makubwa kwa wananchi wa vijijini ya usikivu usioridhisha. Wananchi wanashindwa kupata matokeo muhimu ambayo ni haki yao. Ushauri wangu katika hili ni kwamba, Serikali kuboresha miundombinu ya TBC kwa kununua vifaa vya kisasa vitakavyoondoa kabisa tatizo hili. Aidha, Serikali iongeze kasi ya kuwapatia mafunzo wafanyakazi wa Shirika hili.

Mheshimiwa Spika, Sekta ya maendeleo ya michezo; michezo ni jambo lenye manufaa makubwa katika nchi. Michezo inajenga afya pia inaleta uhusiano mwema kati ya Mataifa duniani. Taifa letu limekuwa likidorora sana kwenye sekta ya michezo yote hasa ya mpira wa miguu, hii ni kutokana na matayarisho mabovu katika kuwapata wachezaji wa mpira. Ushauri wangu katika hili ni kuwa, ni vyema Serikali ikaweka sera maalum na endelevu ya kuwapata wachezaji. Ni vyema kuwa na timu ya kudumu ya na siyo kuendelea na utaratibu wa sasa ambao wachezaji hukusanywa pale tu wanapohitajika na kuruhusiwa kuondoka baada ya kumaliza mchezo husika, hali hii siyo ya tija hata kidogo.

Mheshimiwa Spika, ushauri wa pili katika kuwapata wachezaji walio bora ni Serikali ingekuwa na utaratibu maalum wa kuweka somo la michezo katika shule maalum ya michezo. Hii ingerahisisha kuwapata wachezaji wenye viwango ambao watakuwa wameandaliwa kuanzia udogoni (watoto wenye umri mdogo).

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukupongeza na kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii kutoa mchango wangu katika Wizara hii. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na watendaji wake wote kwa utayari wa kuiwasilisha hotuba hii kwa umakini mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni Idara ya Utalii. Sekta ya utalii ni sekta muhimu sana ulimwenguni. Azma ya kuendeleza utalii ni jambo jema angalau litatoa ajira za moja kwa moja na zile zisizo za moja kwa moja. Naiomba Serikali ichukue juhudi rasmi za kusimamia idara hii badala ya kuziachia sekta za wananchi jambo ambalo si zuri. Serikali iendelee kuwaelimisha wananchi na kuwahamasisha wajione kuwa ni sekta yenye manufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali iweke ushawishi maalum kuwashauri watalii kutembelea sehemu zote za Muungano. Hivi sasa kumekuwa na mtindo ambao sio mzuri wa watalii ambao wanatembelea maeneo ya Bara kuishia huku tu, jambo ambalo linawanyima fursa Wazanzibar kuonesha vivutio vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni mafunzo kwa Idara za Wizara hii. Wizara hii ina idara nyingi ambazo ni muhimu katika kuiendeleza Wizara. Kumekuwa na mtindo ambao si wa kuridhisha sana juu ya kuwapatia mafunzo wafanyakazi wa idara hizo. Mara nyingi nafasi za kujifunza zinapotoka huwa zinachukuliwa na viongozi na kuwaacha wafanyakazi wa chini ambao wao ndio wazalishaji wakubwa.

Naiomba Wizara kurekebisha mwenendo huu na kuweka mpango maalum (training program) ili wafanyakazi wa ngazi za chini nao wapate mafunzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hotuba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Waziri, pamoja na watendaji wake wote kwa matayarisho mazuri na ya kitaalam ya hotuba ya Wizara hii. Nawaombea Mungu awape uwezo na mashirikiano katika utendaji wa kazi zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii naomba kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu ujenzi wa mabweni nchini. Napenda kupongeza Serikali yetu kwa juhudi kubwa inayofanya katika ujenzi na ukarabati wa mabweni. Juzi tumeshuhudia Mheshimwa Rais akizindua mabweni katika Chuo cha Dar es Salaam. Ushauri wangu katika suala hili ni kwamba mabweni yawe na miundombinu salama ili kuepuka madhara ambayo mara nyingi yamekuwa yakijitokeza. Pia mabweni yawe na milango zaidi ya mmoja ya kutoka na hata milango ya dharura. Vilevile mabweni yawe na vizimia moto ili kudhibiti madhara ya umeme unapoleta hitilafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ni kuhusu Chuo Kikuu cha Dodoma ni miongoni wa vyuo bora katika nchi yetu. Chuo hiki kina eneo kubwa na sekta nyingi lakini bado inaonekana kuwa wanafunzi wanaojiunga katika chuo hiki ni kidogo kutokana na ukubwa na uwezo wa chuo. Hii inatokana na mabweni ambayo hayaridhishi. Hivi sasa competition ya vyuo ni kubwa sana hapa nchini. Vyuo binafsi vinaonekana vina nafasi kubwa ya kupata wanafunzi wa kujiunga na vyuo vyao kuliko chuo chetu cha Dodoma kutokana na mabweni hafifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri, aniambie ni asilimia ngapi ya wanafunzi waliojiunga mpaka kufikia mwaka huu kutokana na mahitaji ya chuo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni kuhusu Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam. Taasisi hii ni taasisi inayofanya kazi zake vizuri na kwa ubora sana. Tunaiomba Wizara izidi kuboresha ili kufikia lengo lililokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taasisi hii inajishughulisha pamoja na mambo mengine kutoa mafunzo katika ngazi tofauti kama vile ufundi sanifu na uhandisi. Namwomba Mheshimiwa Waziri atueleze sifa za kujiunga na mafunzo hayo ambayo hakuyaeleza katika hotuba yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natoa shukurani zangu kwako kwa kunipatia fursa hii ya kuchangia katika hotuba ya Wizara hii ambayo ni miongoni mwa Wizara muhimu katika Taifa letu.

Pili, natoa pongezi kubwa kwa Mheshimiwa Waziri, pamoja na watendaji wake wote kwa matayarisho ya kitaalam ya hotuba ya Wizara hii. Nawaomba wazidi kushirikiana ili kufanikisha malengo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta binafsi ni sekta muhimu katika nchi yetu. Sekta hii inawagusa wananchi wa kipato tofauti wenye azma ya kujiendeleza kiuchumi. Sekta hii inakabiliwa na matatizo kadhaa, kama vile upatikanaji wa maeneo ya uwekezaji ambayo huwa yanawakatisha tamaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iwaondolee urasimu huu ili kuwawekea mazingira rafiki ili iwe kama ni vivutio kwa sekta hii. Aidha, Serikali iwapunguzie tozo ambazo hazina ulazima. Tozo nyingi huwa zinaidaiwa kwa sekta binafsi mapema kabla ya mwekezaji binafsi hajaanza kazi. Ni vyema tozo (tax) zidaiwe baada ya uwekezaji kuimarika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ujenzi wa viwanda nchini; naipongeza Serikali yetu kwa azma nzuri ya kujenga viwanda, ujenzi wa viwanda utaongeza tija katika nchi na kuongeza nafasi za uajiri. Ujenzi wa viwanda unahitaji matayarisho mengi kabla ya kuanza. Kwa mfano, huwezi kujenga kiwanda mahali ambapo hakuna umeme, maji na miundombinu ya barabara. Naiomba Serikali kuchukua juhudi za makusudi kuimarisha miundombinu hii ambayo itawashawishi wawekezaji wa nje na ndani kuwekeza katika Sekta ya Viwanda. Aidha, naomba Serikali ipunguze baadhi ya kodi kwa wawekezaji wakubwa wa nje na ndani ili pia iwe ni kivutio kwa wawekezaji wa aina hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu matayarisho ya rasilimali watu; Serikali ina azma nzuri ya kufikia na kukuza uchumi kwa kupitia Sekta ya Viwanda. Sekta ya Viwanda ni ya kitaalam ambayo inahitaji weledi wa kupanga na kuendesha sekta hii. Naishauri Serikali kuchukua juhudi za makusudi kuanza kuwatayarisha Watanzania kwa kuwapatia mafunzo ya kila ngazi ili kujiweka tayari kuendesha sekta hii. Aidha, ni vyema kuwafundisha na kuwapa kipaumbele wazawa na kuepuka kabisa kutumia wataalam kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hotuba hii. Nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha hotuba hii na kuiwasilisha kwa utaalam mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikopo ya Pembejeo; napenda kuipongeza Serikali yetu kwa kuweka utaratibu mzuri wa kuwapatia mikopo wakulima wetu. Wakulima wetu ni wa kipato cha chini sana (maskini), hivyo ni nyema kuwapatia mikopo hii. Naiomba Serikali izidishe jitihada ya kuwapatia mikopo na kuwawekea mazingira rafiki wakulima wetu ili waweze kufikia malengo waliyojiwekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hali ya Uvuvi; sekta ya uvuvi ni miongoni mwa sekta muhimu sana katika kukuza uchumi wa nchi na wananchi wetu. Hivyo ni vyema Serikali yetu ikachukua juhudi za makusudi katika mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwaendeleza wavuvi wadogo, kuwapatia elimu na kuwapatia vifaa vya kisasa. Serikali ni lazima ichukue na iwe na mpango maalum wa kuwaendeleza na kuwapatia elimu wavuvi wadogo. Wavuvi wetu wanajitahidi sana lakini bado hawana mwelekeo, bado wanafanya kazi ya uvuvi kwa mazoea. Ni vyema Serikali iwapatie elimu na miongozo juu ya kujiendeleza. Aidha, Serikali iwapatie vifaa vya kisasa vya uvuvi. Hivi sasa vifaa ambavyo wavuvi wetu wanavitumia bado ni vya kizamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii muhimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika hotuba hii na kuiwasilisha kwa utaalam mkubwa. Nawaomba waendelee na ari hii ili wafikie lengo tulilojiwekea.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mahitaji ya maji katika nchi yetu ni makubwa sana na yanaongezeka kila siku. Maji haya mbadala ni muhimu katika dunia kwani unapokosa maji na uhai haupo. Naipongeza Serikali kwa juhudi kubwa inayochukua katika kuondoa matatizo ya maji vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa vijijini wanaendelea kujichimbia visima katika maeneo yao. Nashauri Serikali iendelee kuwaunga mkono kwa njia zote, yaani kwa utaalam na kifedha kwa sababu uwezo wao vijijini siyo mkubwa kifedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu inatakiwa kuweka mipango mizuri ili kuweza kujitegemea, tuepuke kuwa wategemezi wa misaada kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka 2016 ilionesha kuwa Serikali ya India imetusaidia fund ya dola milioni 208,033 kwa miji sita katika nchi nzima pamoja na visiwa vya Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi viongozi wa Majimbo tumekuwa tukiwaeleza wapiga kura wetu juu ya fedha hiyo na kuwaomba waendelee kustahimili mambo yatatengemaa. Mpaka sasa baada ya mwaka mmoja kupita hakuna matokeo yoyote mazuri juu ya fedha hii. Hivyo,
namwomba Mheshimiwa Waziri atupe maelezo mazuri ni nini kimesababisha mpaka leo kutopatikana kwa fedha hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, mabadiliko ya hali ya hewa yanaongezeka ulimwenguni. Misimu ya mvua imekuwa haitegemeki kwa kasi za ukulima. Hivyo, ni vyema Serikali ikachukua juhudi zaidi katika kuendeleza Sekta ya Umwagiliaji ili iweze kufikia kiwango kizuri cha mahitaji. Asilimia 24 iliyopo hivi sasa ni ndogo sana kwa sekta hii. Nchi yetu ina vyanzo vingi vya maji ambavyo vikiboreshwa vitaweza kusaidia sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwako kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Fedha. Nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wake, pamoja na Watendaji wake wote kwa kutayarisha hotuba hii na kuiwakilisha kwa ufanisi mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi kirefu sasa, mwenendo wa thamani ya fedha yetu imeendelea kuporomoka. Hii inaleta tabu kwa wafanyabiashara na wananchi. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri, Serikali ina mpango gani kuzuia mporomoko huu? Ni vema Serikali ikachukua hatua za haraka kuzuia jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa letu bado linaendelea kutegemea misaada kutoka nje ya nchi, hilo ni jambo baya na halifai kuendelea kuwepo. Serikali inatakiwa kuweka mipango mizuri ili kuondokana na utegemezi. Serikali yetu ina vyanzo vingi vya kiuchumi ambavyo kama tutavidhibiti, vitaweza kutuongezea pato na kuondokana na utegemezi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya fedha ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika kuendeleza nchi hii. Hivyo namwomba Mheshimiwa Waziri kuendeleza mpango wa mafunzo kwa Wizara (training program) ili kuweka katika hali ya kuwajengea uwezo wafanyakazi wa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukrani zangu za dhati kwako kwa kunipatia fursa hii ya kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Napenda kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, pamoja na watendaji wao wote wa Wizara hii kwa kutayarisha hotuba hii kwa ufanisi na kuweza kuwakilisha kwa umakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii, napenda kugusia maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chuo cha Diplomasia ni chuo chenye walimu hodari katika Idara zake zote. Ni walimu wanaofanya kazi kwa bidii na kizalendo. Napenda kuchukua nafasi hii kupongeza walimu hao na kuwataka waendelee na juhudi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu ya chuo hicho hayaendani na jina la kidiplomasia. Miundombinu ni mibovu kidogo, hivyo naiomba Wizara iboreshe miundombinu hii ili chuo kiwe bora zaidi Kitaifa na Kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha. Neno Kimataifa ni neno lenye hadhi. Unaposema Kituo cha Kimataifa ni lazima uwe katika nafasi fulani ambayo ni kubwa ulimwenguni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Mikutano cha Arusha bado kinahitaji marekebisho ili nacho kiwe cha Kimataifa. Serikali inajitahidi kuanzisha miradi ambapo ni jambo zuri sana, lakini bado jengo haliko safi upande wa vyoo; hakuna vyoo vya watu mashuhuri (VIP), vyoo vilivyopo ni kama vya shule za primary/secondary. Hivyo naomba Wizara nayo irekebishe suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu uvumi wa udhalilishaji wa Watanzania katika nchi za Kiarabu. Kumekuwa na uvumi usiokuwa na uhakika katika mitandao na vyombo vya habari zinazoeleza juu ya uteswaji wa Watanzania huko Arabuni. Hili ni jambo linalotia wasiwasi sana katika jamii ya Watanzania. Hivyo namuomba Mheshimiwa Waziri akija kutoa majumuisho atueleze na atoe tamko la Serikali juu ya jambo hili ili liwaweke Watanzania katika utulivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Ardhi. Pili, nampongeza Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa mashirikiano yao yaliyopelekea kutayarisha hotuba hii na kuiwasilisha kwa utaalam mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Usimamizi wa Ardhi, hivi sasa nchi yetu inakabiliwa na ongezeko kubwa la watu. Watu kutoka nje ya nchi yetu wanafika nchini kuomba umiliki wa ardhi kwa matumizi mbalimbali. Hivyo, Serikali yetu ni lazima iendelee kuweka utaratibu mzuri wa ugawaji wa ardhi ili kuepuka kutoa fursa kwa wageni na kuwanyima wazawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi inaendelea kuongezeka siku hadi siku hasa kati ya wafugaji na wakulima. Hii inatokana na ongezeko kubwa la wafugaji na upungufu wa maeneo. Nashauri Serikali kuweka mpango maalum wa kutofautisha maeneo ya wafugaji na yale ya wakulima ili kuondosha migogoro hii ambayo inaendelea kupelekea watu wa makundi hayo kuuawa. Aidha, Serikali iweke kima maalum cha ufugaji kuwa na kima maalum cha wanyama ili kuepuka matatizo haya.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika mpango huu wa maendeleo. Napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa juhudi kubwa anayochukua katika kuongoza nchi hii. Namuombea Mungu ampe uwezo na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii ya Fedha, Naibu Waziri na watendaji wake wote kwa umakini wa kuandika na kuwasilisha Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia Mpango huu napenda kusisitiza maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu kuongeza uwezo wa kupambana na umaskini kwa wananchi. Miongoni mwa kundi kubwa la wananchi wa Tanzania ni wafanyabiashara na wakulima. Hivyo, ni vyema Serikali kuendelea kuchukua juhudi za makusudi kuwawekea mazingira mazuri ya kufanikisha shughuli zao. Serikali inapaswa kuwawekea utaratibu maalum wa kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu ili waweze kufanya biashara zao kwa utulivu na kuweza kujipatia kipato kuweza kupunguza umaskini, hasa wafanyabiashara walio wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya uvuvi, sekta hii bado haijaonesha mafanikio katika kuwaendeleza na kuwanyanyua wavuvi wa nchi hii. Bado mpaka leo wavuvi wanahangaika kwa kukosa vifaa vya uvuvi vya kisasa. Hivyo, naiomba Serikali ichukue juhudi za makusudi kuwaendeleza wavuvi kwa kuwapatia zana za kisasa. Aidha, Serikali iunde benki ya wavuvi, ili iweze kuwakopesha wavuvi kwa kuweza kumudu kununua vifaa vya kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miradi ya maendeleo, Serikali ina nia nzuri katika kupanga na kutekeleza miradi ya maendeleo, lakini miradi mingi katika nchi yetu inakosa ufanisi kwa sababu kadhaa. Moja kati ya sababu hizo ni upatikanaji wa fedha kwa wakati. Hivyo, naiomba Serikali kupeleka pesa kwa wakati katika taasisi husika ili kuweza kwenda na wakati wa mipango kazi ya miradi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika taarifa ya mwaka ya Kamati hii. Pia napenda kuwapongeza wanakamati wote wa Kamati hii kwa kuandika na kuiwasilisha kwa ufasaha katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia taarifa hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo: Kwanza, Kamati kupewa semina za mafunzo. Kama inavyofahamika kuwa Kamati hii ni mpya hivyo ni vema semina za mafunzo kwa wanakamati zikapewa kipaumbele. Nashauri Serikali ni vizuri Wajumbe wakawa wanapewa semina ya taasisi fulani ambayo wanataka kuichunguza kabla ya kuichunguza ili kupata weledi wa kinachofanyika katika taasisi husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili; utendaji usioridhisha. Kwenye ripoti ya Kamati hii imeonesha kwa kiasi fulani utendaji usioridhisha kwa baadhi ya taasisi hii. Hii imesababishwa na mambo mengi ikiwemo dhamana/ majukumu ya Serikali katika kuchangia taasisi hizi. Hivyo naomba Serikali ikaiangalie taarifa kwa makini na kujirekebisha ili mashirika hayo yaweze kujiendesha shughuli zake kwa manufaa ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika taarifa ya shughuli za Kamati hii. Aidha, napenda kuwapongeza Wajumbe wa Kamati wote kwa kuandaa na kuiwasilisha kwa umakini kabisa taarifa hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia taarifa hii napenda kuchangia yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa usambazaji umeme vijijini; napenda kuwapongeza Serikali yetu kwa hatua na spidi nzuri ya kuwapelekea wananchi wa vijijini huduma hii. Umeme kwa sasa sio tena luxury ila ni kitu muhimu kwa maendeleo ya nchi hii na wananchi. Hata hivyo, bado inaonekana kuwa kasi ya usambazaji umeme haiendi sawa na kasi ya matumizi au uungaji wa huduma hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika suala hili Serikali iendelee kuwaelimisha wananchi wa vijijini umuhimu wa huduma. Ni vyema vikaundwa vikundi vya kitaalam na kuwezeshwa ili waweze kwenda vijijini kuwaelimisha wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ni vyema kukawa na msamaha wa gharama za kuunga umeme kwa wateja wa awali ili kuwahamasisha kujitokeza kwa wingi wananchi wa vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kuipongeza Kamati kwa kuandika kwa umakini na kuiwasilisha taarifa hii kwa ubora na kwa kufahamika vizuri na Wabunge wote. Katika kuchangia taarifa hii napenda kutoa mchango wangu katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi; Serikali imezoea kupima na kuelekeza matumizi ya ardhi katika shughuli za ujenzi, mashamba na mipango miji, lakini kuna tatizo kubwa ambalo linasumbua na kuleta athari kubwa katika maeneo kadhaa ya nchi yetu; tatizo hilo ni tatizo la maeneo ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika suala hili, Serikali ianze mpango maalum wa upimaji wa maeneo hayo na kuyaelekeza kwa jamii hizi mbili za wakulima na wafugaji. Hii itaondosha usumbufu mkubwa kwa watu hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Matumizi ya Ardhi, Kamati katika taarifa yake ukurasa wa 23 imeshauri kuhusishwa kwa kampuni binafsi ya upimaji na upangaji wa matumizi ya ardhi. Mimi binafsi sikubaliani na ushauri huu kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapotumia kampuni binafsi katika kazi hii tunaongeza gharama za uendeshaji (operation coast) ambazo mwisho wake zinaenda kwa mtumiaji wa ardhi ambaye ni mwananchi wa nchi hii. Ushauri wangu katika suala hili ni Serikali kuwatumia vijana wetu
kwa kuwapa mafunzo ya kazi hii na mwisho wake kuwapatia ajira. Hii itakuwa ni moja ya vyanzo vya kuongeza ajira katika nchi (source of job creation).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu kwa kuchangia Taarifa ya Utekelezaji wa Shughuli za Kamati za Kudumu za Kilimo, Mifugo na Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwapongeza Wajumbe wa Kamati wote kwa kuandika na kuichambua na kuiwasilisha kwa umakini mkubwa katika Bunge lako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia taarifa hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Maendeleo ya Kilimo ni miongoni mwa vitu ambavyo ni tegemeo kubwa kwa wakulima hasa wakulima wa kipato cha chini. Hivyo naungana na ushauri wa Kamati juu ya Serikali kuipatia benki hii uwezo wa kila aina ili iweze kuwavusha wakulima katika azma zao za kilimo chenye faida. Aidha, kwa kuwa Serikali yetu inaelekea kwenye uchumi wa viwanda, lazima tujue kwamba msingi mkubwa wa kuendesha uchumi wa viwanda ni kilimo chenye manufaa. Hivyo, kuiwezesha Benki hii kutupeleka huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekta ya Uvuvi ni moja katika sekta muhimu katika nchi yetu na ulimwenguni kwa jumla. Sehemu kubwa ya wananchi wetu ni wavuvi, lakini bado wavuvi wa kipato cha chini hawajaweza kutimiziwa haja zao na Serikali kwa kuwapatia nyenzo za uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika Sekta hii ya Uvuvi ni kwamba Serikali iwapatie zana za uvuvi kama vile mashine na mitego ya kisasa ili waweze nao kuepukana na kuvua kizamani. Aidha, Serikali iendelee kuwaelimisha wavuvi hawa namna bora ya uvuvi ili kuepuka kuvua kwa mazoea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwa maandishi hotuba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri na wafanyakazi wake wote kwa utayarishaji na uwasilishaji mzuri wa hotuba hii katika Bunge hili. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni uboreshwaji wa Hospitali za Rufaa za Mikoa. Takwimu zinaonesha kuwa ajali nyingi za magari zinatokea katika sehemu za mikoani kuliko mijini ambako ziko hospitali nzuri zenye vifaa lakini Hospitali za Rufaa za Mikoa inaonekana zina upungufu wa baadhi ya vifaa vya kukabili ajali hizo zinapotokea na kulazimika wagonjwa kusafirishwa kupelekwa Dar es Salaam. Mfano wa hivi juzi ambao Waheshimiwa Wabunge sita walipata ajali na kukimbizwa katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro ilibidi wasafirishwe kupelekwa Dar es Salaam kwa matibabu zaidi baada ya kukosekana CT Scan ambayo ingeweza kuwachunguza na kuonekana matatizo yao pale Morogoro, hii inawatokezea Waheshimiwa Wabunge, lakini je, ajali hii kama ingekuwa ya wananchi wa kawaida ingekuwaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Wizara na Serikali kuendeleza juhudi za kuziimarisha hospitali hizi kwa kujipatia vitendea kazi vya kisasa ili kuweza kukabili matokeo haya na mengineo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu udhibiti wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza; napenda kuipongeza Wizara hii kwa kuendelea kusambaza elimu juu ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza, Wizara inajitahidi sana kueneza elimu katika mikoa yote ya Tanzania. Ushauri wangu katika suala hili ni kuomba Wizara iongeze ujuzi wa elimu hii katika maeneo ya vijijini ambako hawawezi kupata elimu hii kwa kutumia njia za vyombo vya habari kama vile tv na magazeti. Ni vyema Wizara ikawa na timu maalum ambayo itaweza kwenda moja kwa moja vijijini ambako itaweza kuwaelimisha wanavijiji

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natoa shukrani kwako wewe binafsi kwa kunipatia nafasi hii kutoa mchango wangu wa maandishi katika Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na watendaji wake wote kwa umahiri wao wa kuongoza Wizara hii. Katika kuchangia Wizara hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali yetu kwa namna inavyowekeza miradi mbalimbali katika nchi yetu. Miongoni mwa uwekezaji unaofanyika ni uwekezaji wa simu za mkononi. Hivi sasa simu za mkononi siyo kitu cha fahari (luxury), hata wananchi wa vijijini wanatumia kwa shughuli zao. Imekuwa simu ni kitendea kazi kwa watu wote lakini bado bei za simu hizo ni kubwa sana kiasi ambacho wananchi hasa wa vijijini wanashindwa kumudu gharama hizo. Ushauri wangu kwa Wizara hii ni kwamba waendelee kusimamia bei hizi na kuzifanya ziwe rafiki kwa wananchi wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bodi za Wakurugenzi katika mashirika yetu, ni sehemu muhimu sana katika kusimamia na kuendesha mashirika hayo. Ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba ni vyema Wakurugenzi wanaochaguliwa wawe na ujuzi wa taasisi husika. Siyo vizuri Mkurugenzi wa Bodi ya TTCL awe ana ujuzi wa kilimo au daktari, hii haitaleta ufanisi mzuri. Ni vyema Mkurugenzi wa Bodi ya TTCL awe na ujuzi wa taasisi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushukuru wewe binafsi kwa kunipatia fursa hii ya kuchangia kwa maandishi katika hotuba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na kuiwasilisha kwa umakini wa hali ya juu hotuba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ni Shirika la Utangazaji Tanzania. Napenda kuipongeza Wizara kwa kuendelea kuliboresha Shirika hili la Utangazaji, ni shirika linalopiga hatua katika utangazaji. Ushauri wangu kwa Wizara, iendelee kutoa mafunzo kwa watendaji wa shirika hili ili kwenda na wakati. Bado kuna wafanyakazi hawaoneshi mabadiliko ya kiutendaji kutokana na pengine kukosa elimu na maelekezo ya kikazi. Mfano kwenye mavazi ya mtangazaji baadhi ya watangazaji hawaoneshi kuwa na elimu ya mavazi (dressing code). Aidha, naomba Wizara iboreshe usikivu katika maeneo ya vijijini, bado kuna maeneo ambayo usikivu sio mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, viwanja vya michezo. Bado viwanja vyetu nchini haviko vizuri. Tunaendelea na kuwa na viwanja vya kurithi, vya karne zilizopita. Ushauri wangu kwa Wizara ni kuboresha viwanja vya michezo ili viwe vivutio kwa wachezaji na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa machango wangu katika hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia. Pia napenda kumpongeza kwa dhati Waziri wa Wizara hii pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika vyema hotuba yao na kuiwasilisha kwa ufasaha katika Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni Chuo Kikuu cha Dodoma. Chuo hiki ni miongoni mwa vyuo muhimu sana katika nchi yetu hasa ukizingatia kuwa kiko katika mji mkuu wa nchi yetu. Kinahitaji maboresho ya hali ya juu katika rasilimali watu ili kiende na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefurahi kuona kuwa katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameeleza kuwa amegharamia masomo kwa walimu/wafanyakazi 377 katika nyanja tofauti. Suala langu katika wafanyakazi hao ni kwamba Waziri hajaeleza wafanyakazi 377 aliowapatia mafunzo ni kati ya wangapi yaani ni asilimia ngapi ya 377 waliopata mafunzo hayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ni kuhusu Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi. Naipongeza Wizara ya Elimu kwa kuimarisha mamlaka hii. Hii ni mamlaka inayowagusa wanafunzi wa kipato cha chini na makundi tofauti. Ameeleza namna inavyojitahidi kuongeza vyuo katika maeneo kadhaa nchini. Nashauri katika ujenzi wa vyuo hivyo uzingatie uwepo wa makundi yote. Majengo yawe na facilities kwa ajili ya watu wenye ulemavu ili nao wafaidi matunda ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, natoa shukrani zangu kwako kwa kunipa fursa hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa uongozi wao wa kuongoza Wizara hii nyeti katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia Wizara hii, naomba kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Wizara kwa kuendelea kujenga na kuimarisha vyanzo vya maji nchini, mijini na vijijini na pia kuimarishwa Mamlaka za Maji katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika suala la vyanzo vya maji ni kusimamia na kuchukua hadhari kubwa ya namna ya kuyatunza maji. Siyo sahihi kuona kwamba mahodhi ambayo yanahifadhi maji huwekwa wazi bila ya kufunikwa. Anaweza kutokeza adui akarusha kitu cha kudhuru (sumu) kwenye maji na akasababisha madhara makubwa kwa wananchi. Mfano wa suala hili ni katika Mamlaka ya Maji Mwanza (MWAUWASA). Katika Mamlaka hii hodhi la kuhifadhia maji liko wazi. Kwa hiyo, naiomba Wizara ielekeze mamlaka husika ichukue hadhari/udhibiti wa suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa fursa hii ya kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Pili, nampongeza Waziri na watendaji wake wote kwa kuandika na kuiwakilisha ripoti hii kwa umakini mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali yetu kwa kutangaza na kuweka azma ya kuifanya nchi yetu kuwa nchi ya viwanda. Jambo hili ni jema lakini linahitaji matayarisho makubwa ili kufikia lengo. Lazima tuwe na rasilimali za aina zote hasa rasilimali watu na vifaa (Human Resource and Materials).

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, ushauri wangu kwenye kutayarisha rasilimali watu lazima tuwatayarishe vijana wetu kwa kuwapatia taaluma inayohusu viwanda. Haitakuwa vizuri leo tuna vijana waliomaliza vyuo wengi, tukatumia wataalam wa kigeni badala ya vijana wetu kwa ukosefu wa ujuzi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutayarisha rasilimali vifaa ni lazima Serikali itilie mkazo kwenye sekta ya kilimo. Kilimo ndiyo msingi wa kila jambo pamoja na viwanda. Hivyo, Serikali ni lazima kuiwezesha kwa maeneo yote sekta ya kilimo kwa kuipatia vitendea kazi na ruhusa zote zitakazo fanikisha azma hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Kilimo. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na kuiwakilisha hotuba hii kwa ufanisi mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii ya kilimo, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Wizara kwa juhudi zake inayochukua kuimarisha na kuhamasisha wakulima wa nchi hii. Wakulima wa nchi hii wameendelea kuonesha juhudi zao katika kilimo cha mazao tofauti hasa yale mazao ya biashara. Juhudi hizi zimeonekana kudorora kutokana na upatikanaji wa masoko ya kuuza mazao hayo. Wakulima wamekuwa wakilundika mazao yao katika maghala kwa muda mrefu jambo linalopelekea kuvunja moyo kwa kiasi fulani. Hivyo nachukua fursa hii kuiomba Serikali kupitia Wizara hii kulichukulia suala hili la kuwatafutia masoko ya uhakika wakulima wetu ili wawe na uhakika wa kuuza mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu kupitia Wizara ya Kilimo inachukua juhudi ya kutafuta namna ya kuboresha kilimo kwa kuwatafutia wakulima wetu zana za kilimo. Nachukua nafasi hii kuipongeza Wizara kwa jambo hili zuri. Imeonekana kuwa jambo hili lina tatizo la wakulima wetu kutomudu kununua zana hizo za kilimo hasa matrekta. Hii ni kutokana na bei kubwa ya ununuzi wa matrekta. Wakulima wa nchi hii, idadi kubwa ni wakulima wa kipato cha chini/kati kiasi ambacho uwezo wao ni mdogo sana. Hivyo naiomba Serikali kupitia Wizara ya Kilimo kuangalia utaratibu mzuri wa kuwawezesha wakulima kupata zana hizi kwa kuwapunguzia bei au kuwakopesha kwa masharti nafuu wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa fursa ya kuchangia katika hotuba hii. Pili, nampongeza Waziri pamoja na watendaji wote kwa kuwasilisha hotuba hii kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia kuhusu wavuvi wadogo. Wavuvi wadogo ni sehemu kubwa ya wananchi wa Tanzania. Kundi hili linahitaji kuangaliwa kwa hisia ya pekee.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kuwatengenezea mazingira mazuri kwa kuwatafutia zana za kisasa na kuwapatia elimu juu ya uvuvi ili waweze kufanikiwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii kutoa mchango katika Wizara hii. Aidha, napenda kumpongeza Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na kuiwasilisha hotuba hii kwa ufasaha mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii ya maliasili na Utalii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, nianze na vivutio cha utalii, napenda kuipongeza Serikali pamoja na Wizara hii kwa kuendelea kutilia mkazo namna ya kuboresha vivutio hivi vya utalii. Mazingira ya vivutio vyetu vinaonekana kuimarika na kuvutia watalii. Ushauri wangu katika suala hili kwa Serikali ni Wizara kwa jumla ni kuongeza vivutio hivyo na kuviweka katika hali ya kisasa zaidi. Aidha, ni vyema kuwe na vivutio vya namna tofauti katika maeneo yetu ya vivutio kwa mfano, ikiwa kivutio kingine kiwe na wanyama wa aina nyingine ili kuweka variety ya vivutio. Kutatua migogoro ya mipaka ya Hifadhi za Utalii.

Mheshimiwa Spika, hali ya migogoro katika nchi yetu imezidi kila siku. Naipongeza sana Wizara hii kwa kuchukua juhudi za kulishughulikia suala hili. Utaratibu wa kuwashirikisha wananchi walio katika maeneo husika ni jambo jema sana. Ushauri wangu katika suala hili ni kuzingatia kuwapa kipaumbele wakulima wa maeneo hayo ili kuendeleza kilimo ambacho ni uti wa mgongo wa uchumi wetu hasa tunakoelekea kwenye siasa ya kujenga viwanda. Viwanda vinategemea sana kilimo kama rasilimali kubwa. Hivyo ni vyema Wizara ikazingatia suala la wakulima. Aidha, wananchi wa maeneo husika wewe wanapewa uhuru wa kuzungumza na kutoa maoni yao badala ya kushirikishwa kwenye mahudhurio tu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi ya kutoa mchango wangu katika hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Aidha, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri na watendaji wake wote kwa kutayarisha na kuwasilisha kwa umakini mkubwa hotuba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kutoa mchango wangu katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Uwakilishi wa Tanzania katika Mabunge ya Nje. Napenda kuchukua nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa Waheshimiwa Wabunge wetu waliopata nafasi ya kuteuliwa katika nafasi kwenye Bunge la Afrika. Wabunge hawa wameonesha uwezo mkubwa katika nyanja za kimataifa na kuonesha kuwa Tanzania tunao watu ambao wanaweza katika maeneo ya kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na matokeo hayo ya kihistoria yaliyopatikana bado juhudi za uwakilishi wa nchi yetu katika Mabunge hayaridhishi kidogo. Bado kunakosekana uwakilishi katika Mabunge kadhaa kwenye mikutano ya Mabunge. Najua kuwa hali ya uchumi wa nchi yetu bado haijatengemaa vizuri, lakini naiomba Serikali kulipa umuhimu wa kipekee jambo hili la uwakilishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Utafutaji wa Misaada kwa Ajili ya Miradi ya Maendeleo. Napenda kuipongeza Serikali yetu kupitia Wizara hii kwa namna wanavyochukua juhudi za kutafuta misaada kwa wafadhili kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Jambo la kutafuta misaada ni jambo la kawaida kwa nchi nyingi ulimwenguni.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba, ni vyema Wizara ikawa na wafanyakazi wenye ujuzi wa aina zote hasa za mikataba ya miradi hiyo pamoja na biashara. Hii itatuepusha na ujanja wa mitego ya kisheria za mikataba ambayo mara nyingi baadhi ya wafadhili huwa wanaitumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JUMA OTHMAN HAJI: Mheshimiwa Spika, natoa shukrani zangu kwako kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hotuba hii ambayo ni muhimu katika nchi yetu. Pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na kuwasilisha kwa ufanisi mkubwa katika Bunge hili. Katika kuchangia nafasi hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Msajili wa Hazina ni miongoni mwa ofisi muhimu sana katika nchi hii. Hii ni ofisi inayosimamia mashirika na taasisi zaidi ya 260 katika nchi hii. Hata hivyo inaonekana utendaji wa ofisi hii bado hajazaa matunda.

Mheshimiwa Spika, Msajili wa Hazina inaonekana mamlaka yake katika baadhi ya mashirika au taasisi hayako vizuri. Anashindwa kukosoa na kuelekeza katika mashirika hayo, hana uwezo wa kutoa maelekezo hasa kwenye mikakati ya utendaji wa mashirika hayo. Aidha, msajili hawezi hata kushauri juu ya uongozi wa taasisi hizo, utakuta taasisi fulani ina uongozi wote wanakaimu lakini msajili anashindwa kutoa maelekezo juu ya uongozi ili kuondoa tatizo la kukaimu kwa uongozi wa taasisi fulani.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Wizara hii ni kwamba Wizara ichukue mikakati ya kumuwezesha Msajili kuwa na uwezo wa kurekebisha na kuelekeza mashirika au taasisi hizo ili ziwe za ufanisi zaidi kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukurani zangu za dhati kwako kwa kunipa fursa hii kutoa michango yangu katika Wizara hii kubwa katika nchi yetu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, namshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuonesha uwezo mkubwa wa kuongoza nchi hii na Insha Allah Mwenyezi Mungu ampe kila la kheri katika kufanikisha suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, namshukuru Mheshimiwa Waziri pamoja na Watendaji wake wote kwa umahiri wao mzuri wa kuwasilisha hotuba hii ambayo imebeba mambo mengi katika nchi yetu hii. Nchi yetu hii ni kubwa lakini hotuba yao hii ni fupi sana lakini ime-cover kila kitu katika nchi yetu hii. Kwa hiyo, nawapongeza watu hawa kwa umahiri wao huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, michango yangu itakwenda kwenye kukumbusha masuala ambayo nimekuwa nikiyazungumza mara nyingi kwenye vipindi vyetu vya maswali na majibu. Suala la kwanza ni kuhusu kituo changu cha Mkokotoni, kituo hiki ni miongoni mwa vituo vikongwe sana katika nchi yetu hii. Ni kituo chakavu kabisa, kinahitaji matengenezo ya kweli kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Wizara ilianzisha jengo pale katika kituo hiki, lakini mpaka sasa hivi jengo lile limekwama, hatujui nini kinaendelea. Jengo limebakia kama gofu, hatujui hatima ya jengo lile. Kwa hiyo, nachukua fursa hii kuiomba Wizara ikamilishe jengo lile ili askari wetu pale wapate makazi mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, askari wetu pale wana hali ngumu sana, katika mvua hizi ambazo zimenyesha juzi, askari wetu imebidi wahamie chumba cha mahabusu kufanya kazi, imagine chumba cha mahabusu askari wetu wamehama kwenye Ofisi yao wanatumia chumba cha mahabusu kufanya kazi katika kituo kile. Kwa hiyo, naiomba Wizara ikamilishe masuala yale ili askari wetu wale waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nimekuwa nikizungumza kila siku ni kituo cha Polisi katika Kisiwa cha Tumbatu. Suala hili nimekuwa nikizungumza kila siku kuiomba Wizara kwamba itujengee kituo katika Kisiwa cha Tumbatu. Jiografia ya Kisiwa cha Tumbatu inahitaji huduma zote pamoja na huduma za usalama. Masafa kutoka Mkokotoni mpaka Tumbatu ni almost kilomita mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, linapotokea neno Kisiwa cha Tumbatu inabidi askari watoke Mkokotoni waende Tumbatu, wavuke kwa kutumia bahari. Imagine kama kuna kitu kimetokezea kule hatuombi kitokezee, lakini mpaka wakifika pale Tumbatu basi lililotokezea limeshaathiri sana. Kwa hiyo, naomba suala hili kwa mara nyingine kwamba Wizara itujengee kituo katika Kisiwa cha Tumbatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni vitendea kazi katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Waheshimiwa wengi hapa wamesimama wanazungumzia vitendea kazi wamekuwa wanaomba magari na vifaa vingine, lakini Wizara hii ina tatizo moja kubwa sana la vitendea kazi hasa kwenye stationeries. Mwaka jana nilipata bahati mbaya, niliibiwa simu yangu nyumbani kwangu nika-report polisi Dodoma hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipofika pale kituo cha polisi Dodoma nilitakiwa nichukuliwe maelezo, basi askari pale hata stationery hawana, stationery ya kuandika ile report yangu hawana mwisho niliona kwamba kwa kweli ni kitu cha aibu, askari pale wanatumia order paper hizi zetu za Bunge, ndiyo wanaandikia report zetu. Kwa hiyo, Wizara iwasaidie siyo Dodoma tu lakini nchi nzima kwamba kuna tatizo la stationeries katika vituo vyetu hivi vya Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo leo nataka nichangie ni kwamba utaratibu wa viongozi wetu wa Wizara hii kutembelea katika mikoa. Mheshimiwa Waziri mara baada ya kuchaguliwa alikuwa na utaratibu mzuri wa kutembelea katika mikoa yetu na wilaya zetu. Namwomba Waziri utaratibu wake ule uwe utaratibu wa kudumu aendelee nao katika Wizara yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe binafsi kwa kutupatia fursa hii ya kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa pamoja na Watendaji wote wa Wizara yake kwa kuandaa na kuiwasilisha hotuba yake kwa ufasaha na umakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ni Mfuko wenye madhumuni ya kuwapunguzia wananchi makali ya kiuchumi. Naipongeza Serikali sana kwa mfuko huo na naomba uendelee zaidi. Hata hivyo, imeonekana kuwa bado kuna matatizo katika utambuzi wa kaya zinazohusika, kuna udanganyifu katika kuwatambua walemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika hili, Serikali iwashirikishe Walemavu, Wabunge katika zoezi la kutambua kaya husika ili kuondoa mkanganyiko huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mfuko wa Rais wa Kujitegemea, Mfuko huu ni mzuri sana, nachukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa kuanzisha Mfuko huu. Bado hakuna uwiano wa kiwango cha wahitimu wanaomaliza shule za VETA. Kiwango cha wanaomaliza shule za VETA ambao ni miongoni mwa walemavu ni mkubwa kuliko kiwango cha fedha zinazotolewa kwa mkopo. Ushauri wangu ni kwamba Serikali iongeze kiwango cha fedha za mikopo kwa Mfuko huu ili dhamira ya Mfuko huu iweze kufikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue fursa hii kuchangia katika hotuba ya Waziri wa TAMISEMI. Nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa umahiri wanaoonesha katika kuongoza Wizara hii nyeti katika nchi hii. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Afya ya Jamii; katika ulimwengu wote afya ni jambo muhimu sana kwa mwanadamu. Naipongeza Wizara kwa kuanzisha utaratibu mzuri wa Mfuko wa Afya ya Jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika utaratibu huu ni kuongeza kasi ya kuwapatia kadi za afya wananchi husika. Bado idadi ya wanachama 12,278,406 ni ndogo sana ukilinganisha na idadi ya wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya maendeleo; naipongeza Wizara kwa ubunifu wanaoonesha kuanzisha miradi mbalimbali ya maendeleo lakini bado inaonekana kuna utegemezi mkubwa wa fedha katika utekelezaji wa baadhi ya miradi, bado Serikali inategemea misaada kutoka taasisi za nje. Ushauri wangu ni kwamba Serikali iongeze speed ya kutafuta vyanzo vya mapato ili tuweze kuendesha miradi yetu kwa fedha zetu za ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja zote mbili. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na kuiwasilisha kwa ufasaha hotuba hii. Katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, upimaji wa viwanja na mashamba; napenda kuipongeza Wizara kwa hatua yake ya kuendelea kupima na kuwapatia viwanja vya makazi wanachi wetu ili kuwaondolea matatizo ya uhaba wa viwanja. Makazi ni hitaji muhimu sana katika maisha ya mwanadamu lakini inaonekana kuwa bado bei ya viwanja si rafiki kwa wananchi wa kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei ya viwanja ni kubwa sana kiasi ambacho wananchi wanakata tamaa na na hivyo kusababisha wananchi hao kutafuta njia mbadala ya kujikatia maeneo ya makazi kwenye maeneo yaliyo karibu nao, jambo ambalo linapelekea kuharibu azma na mpango mzuri uliowekwa na Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika jambo hili ni kuiomba Wizara kupunguza bei ya viwanja hasa vya makazi ili kuwawezesha wananchi kumudu gharama hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nachukua nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wake pamoja na Watendaji wake wote wa Wizara hii kwa kuandika na kuwakilisha hotuba hii kwa ufasaha na kwa utaalam.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Wizara kwa hatua inazozichukua juu ya uendelezaji wa wachimbaji wadogo. Kama inavyojulikana kuwa kundi hili la wachimbaji ni kubwa sana katika nchi yetu kuliko kundi la wachimbaji wengine. Kundi hili linaigusa moja kwa moja jamii ya kipato kidogo ambao wanahitaji msukumo wa kipekee ili waweze kumudu maisha yao na kuweza kupunguza umaskini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika hili ni kuwa Wizara iendelee kuwawezesha kwa kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu pamoja na kuwapatia elimu juu ya kazi hii ili waweze kufanya kazi hii kitaalamu badala ya kuendelea kufanya kazi hii kimazoea. Ikiwa Serikali itawasaidia wachimbaji hawa, wanaweza kwa kiasi kikubwa kuchangia Mfuko wa Serikali kwa kumudu kulipa tozo zitakazowekwa kwa mujibu wa utaratibu wa sheria. Pia Serikali kwa kushirikiana na Wizara hii iweke mpango maalum wa malengo ya kuazimia kuwaondoa wachimbaji hawa katika ngazi ya wachimbaji wadogo mpaka kufikia kuwa wachimbaji wakubwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nianze kwa kuishukuru Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Magufuli kwa uimara wake katika kuendesha vyema nchi jambo ambalo limewezesha kuleta matokeo mengi mazuri. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Watendaji wake wote kwa kuweza kuitengeneza na kuiwakilisha hotuba hii kwa ufasaha wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo, kwanza ni kuhusu ziara za viongozi wa Serikal. Napenda kuchukua nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa viongozi wote wa Serikali namna wanavyofanya ziara katika nchi yetu. Hili ni jambo zuri ambalo linaamsha ari kwa sehemu zinazotembelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba naomba ziara za viongozi wa taasisi za Muungano ziendelee kwa pande zote za Muungano. Kwa kuwa ziara hizi pamoja na mambo mengine zinaimarisha Muungano ni vyema zikatiliwa mkazo kwa kuwekewa mpango maalum wenye msisitizo wa kutembelea sehemu hizi za Muungano ili kuimarisha na kuchochea maendeleo katika Jamhuri yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nizungumzie uwekezaji. Naipongeza Serikali yetu kwa juhudi kubwa inayochukua katika kutilia mkazo uwekezaji katika nchi yetu. Uwekezaji ni miongoni mwa vyanzo vikubwa vya uchumi katika nchi. Aidha, uwekezaji unachochea upatikanaji wa ajira kwa watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali kuendelea kuweka mazingira mazuri ambayo yatawavutia wawekezaji wa ndani na wa nje kwa kuweka miundombinu rafiki itakayorahisisha uwekezaji. Aidha, Serikali iweke mazingira bora yatakayoondoa urasimu wa upatikanaji ruhusa ya uwekezaji kwa wageni na wazawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, natoa shukrani zangu za dhati kwako kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Pili, nipende kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake kwa kutayarisha na kuiwasilisha kwa ufasaha na kwa utaalam.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, michezo; napenda kuipongeza Serikali yetu kwa hatua inayochukua katika kuendeleza michezo. Michezo ni miongoni mwa mambo ambayo yanaonesha utambulisho wa nchi. Naipongeza Serikali kwa kuilinda na kuiwezesha timu yetu ya Taifa mpaka kufika katika hatua ya AFCON.

Mheshimiwa Spika, michezo ni hasara, Serikali inabidi iongeze juhudi ya kuisaidia timu yetu bila ya kujali hasara, bila ya kuisaidia hatuwezi kufika hatua ambapo tunaikusudia. Pia naishauri Wizara ichukue hadhari na iwe makini katika uchaguzi/uteuzi wa wachezaji na viongozi wa kuendeleza na kuendesha timu hiyo. Uchaguzi wa sasa hauridhishi hata kidogo kwa kuwa timu hii ni ya Taifa la Tanzania (Jamhuri ya Muungano wa Tanzania) ni vyema uchaguzi wa wachezaji uzingatie pande zote za Muungano.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake wote kwa kutayarisha na kuwakilisha kwa umakini vizuri hotuba hii. Katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, miradi ya ujenzi wa makazi, Ofisi na Vituo vya Polisi; napenda kuipongeza Serikali kwa kutambua na kuthamini uwepo wa upungufu wa makazi na ofisi/vituo vya Polisi katika nchi yetu. Hili ni jambo jema ambalo litasaidia kuwapatia utulivu Askari wetu na kuweza kufanya majukumu yao kwa ufanisi.

Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ametuomba Waheshimiwa Wabunge tushirikiane katika ujenzi wa miradi hii. Ushauri wangu katika suala hili ni kumwomba Mheshimiwa Waziri kututafuta Wabunge katika hatua za awali ili kutambua kwa pamoja maeneo husika. Kwa mfano, katika hotuba yake ukurasa wa 12 ametaja mikoa ambayo itajengwa makazi ya Polisi lakini mkoa ni eneo kubwa ambalo lina majimbo zaidi ya moja. Kwa hivyo, ni vyema Mheshimiwa Waziri angetaja sehemu maalum yanapojengwa ili kutambua ni Mbunge gani anahusika katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, vitendea kazi; napenda kuipongeza Serikali kwa juhudi zake inayochukua kwa kuendelea kuwatafutia vitendea kazi Maaskari wetu. Vitendea kazi ni chachu ya ufanisi mzuri wa kazi zao. Ushauri wangu katika suala hili ni kwamba, Serikali izidi kuwatafutia vifaa vya kisasa kutokana na ukuaji wa matendo ya uhalifu vifaa ambavyo vitawarahisishia Askari wetu kuwatambua wahalifu kwa urahisi zaidi na kwa uhakika bila kubabaisha.

Mheshimiwa Spika, ajira kwa Maaskari; hivi sasa dunia inakabiliwa na tatizo kubwa la ajira kama inavyokabiliwa nchi yetu hivyo ni vyema Jeshi la Polisi likawa ni chanzo cha ajira katika nchi yetu. Ushauri wangu katika suala hili ni kwamba Serikali iwe makini sana katika kuchuja vijana ambao wanaoajiri ili kuepuka kuajiri vijana ambao hawana sifa na ambao huku nje ni wahalifu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukrani zangu kwako kwa kunipatia fursa hii ya kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Watendaji wake wote kwa kutayarisha na kuwasilisha hotuba ya Wizara yao kwa ufasaha zaidi katika Bunge lako hili. Katika kuchangia hotuba hii, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Wizara pamoja na Serikali Kuu kwa kuweka Baraza la Mitihani la Tanzania ambalo ni chombo muhimu sana katika Sekta ya Elimu. Hivi karibuni kumekuwa na matokeo ya mara kwa mara ya uvujaji wa mitihani katika daraja tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika suala hili ni kwamba, Wizara iendelee kuwa na makini mkubwa katika kudhibiti jambo hili. Wizara katika kutatua suala hili inabidi ilitafutie Baraza vitendea kazi kama magari ya kuweza kusafirisha mitihani kutoka Makao Makuu au sehemu moja kwenda nyingine. Tukiwa tunasafirisha mitihani hii kwa magari ambayo hayana uhakika, inatoa mianya ya kuvuja mitihani hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naipongeza Wizara hii kwa kubuni na kuendeleza mradi wa ukarabati wa Vyuo vya Ualimu, mradi ambao ni muhimu kwa kuwatengenezea mazingira bora ya walimu. Walimu ni rasimali kubwa katika jamii, ni watu ambao wanatakiwa wafanye kazi kwa utulivu ili waweze kufundisha vyema kazi zao. Ushauri wangu ni kwamba, Wizara hii iendelee kuongeza ukarabati huu katika maeneo yote ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, kwanza nachukua fursa hii kukushkuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hotuba hii. Pili nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandaa na kuwakilisha hotuba hii kwa umakini mkubwa sana. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, Shirika la Posta (TPC) napenda kuipongeza Serikali yetu kwa kuendeleza juhudi kubwa za kuendeleza na kuiimarisha Shirika hili, shirika hili ni miongoni mwa mashirika makongwe sana katika nchi hii. Shirika hili linajishughulisha na kazi ambazo ni lazima zifuatiliwe ili kufanikisha kazi hizi mfano, kazi ya posta mlangoni hii kazi inahitaji vitendea kazi vya usafiri ili kufika kwenye eneo husika. Ushauri wangu katika jambo hili ni Wizara kuzidisha juhudi ya kuwatafutia usafiri wa uhakika ili kuweza kukabiliana na ushindani mkubwa uliopo nchini.

Mheshimiwa Spika, Shirika la Mawasiliano Tanzania; shirika hili ni miongoni mwa mashirika muhimu sana katika uchumi wa nchi yetu. Nachukua nafasi hii kuipongeza idadi ya wateja (Active customer) wa huduma mbalimbali, hili ni jambo jema kwa sababu wateja ndio watakaowezesha upatikanaji wa faida katika shirika hili.

Mheshimiwa Spika, kazi za mawasiliano kwa sasa zina ushindani mkubwa sana, mashirika mengi ya binafsi yamejitokeza na yanaendelea kujitokeza, hivyo ni vyema shirika likajipanga ili kukabiliana na ushindani huu.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali iliwezeshe shirika hili ili liweze kukabiliana na mashirika binafsi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nachukua nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipatia fursa hii ya kuchangia katika Wizara hii. Pili napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Biashara pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na kuiwasilisha kwa umakini wa ufasaha na hali ya juu. Katika kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Biashara na Viwanda napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Matrekta aina ya Ursus. Napenda kuipongeza Serikali kwa azma yake ya kuendeleza mradi huu wa matrekta, kama inavyojulikana kwa dhana ya kuelekea kwenye sera ya viwanda haiwezi kufanikiwa bila ya kuimarisha kilimo cha kisasa. Vitendea kazi katika kilimo moja katika hivyo ni matrekta. Hata hivyo, ni vyema Serikali ikatilia mkazo mradi huu. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 10 imeeleza idadi ya matrekta na idadi ya hekari zilizokwishalimwa uwiano wake ni heka 214.1 limelimwa kwa kila trekta moja. Hii ni idadi ndogo sana kwa nchi inayoelekea kwenye kuimarisha viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba Serikali ipunguze bei ya matrekta na kuondosha vikwazo vilivopo ili wananchi wengi waweze kumudu kununua matrekta hayo. Inaonekana kuwa bado bei ya matrekta sio rafiki kwa wakulima wetu. Tanzania ya viwanda itawezekana ikiwa miundombinu ya kuboresha kilimo ambayo ni pamoja na kupunguza bei za matrekta ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika Wizara hii. Pili, napenda kuwapongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake wote kwa kuendelea na kuiwasilisha kwa ufasaha mkubwa hotuba hii. Hii ni Wizara muhimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Kwanza ajira katika Jeshi letu, naipongeza Wizara kwa kuendelea kuchukua vijana wa nchi hii kwa mujibu wa uwezo na sheria ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika suala hili ni kuitahadharisha Wizara iendeleze umakini wa kuwapembua na kuwafahamu vyema vijana ambao wanawaajiri. Nchi yetu imezungukwa na nchi jirani ambazo baadhi yao zina matatizo yao na kukimbilia katika nchi yetu, vijana wa nchi hizi wanapokimbilia katika nchi yetu huwa wanajiingiza (wanaweza kujiingiza) katika jamii ya Watanzania na kuweza kujipenyeza kuweza kujiunga na Jeshi letu. Hivyo Wizara naiomba iendelee kuwa makini sana katika kuwachukua vijana na kujiunga jeshini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana ya Jeshi la Wananchi; Jeshi letu limekuwa na kazi ya kulinda na kuhakikisha usalama wa mipaka yetu lakini Jeshi hili pia linapaswa kuangalia maeneo mengine ya kuweza kusaidia wananchi hasa katika nyanja za kiuchumi. Mfano maeneo yafuatayo yanaweza kusaidia kwa kutoa elimu ya kiuchumi kwa wananchi kama Kiwanda cha Ushonaji, Kiwanda cha Samani Chang’ombe ambacho hutengeneza samani, ufugaji wa samaki katika mabwawa na uvuvi. Maeneo hayo niliyoyaorodhesha nashauri Jeshi lipeleke ujuzi wake kwa wananchi ili na wao waweze kutumia ujuzi wa maeneo hayo kuweza kujikwamua kiuchumi .

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe wa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hotuba hii. Pili, napenda kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Waziri wa Kilimo pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na kuwasilisha hotuba hii kwa ufasaha mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kutoa mchango wangu katika hotuba hii, napenda kuchangia kwenye maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, Vyuo na Vituo vya Mafunzo ya Kilimo; naipongeza Serikali kupitia Wizara hii kwa kuweka utaratibu mzuri wa kutoa mafunzo ya kilimo kwa vijana wetu nchini. Hili jambo ni jema ambalo litatupelekea kulima kwa mtindo wa kisasa badala ya ule wa kufanya kazi kwa mazoea.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Wizara ni kwamba, iweze kuwatumia wataalam wanaohitimu kwenye vyuo vyetu ili walete mafanikio. Wataalam hasa Mabwana/ Mabibi Shamba wawezeshwe ili waende vijijini badala ya kukaa mijini/maofisini. Wakulima wetu wa vijijini hasa wale wa kipato cha chini wanahitaji maelekezo ya kitaalam sana ili kufanikisha kazi zao.

Mheshimiwa Spika, pili, pembejeo za kilimo, Serikali yetu inajitahidi sana kutafuta miundombinu ya pembejeo. Kilimo ni uti wa mgongo hasa katika nchi yetu ambayo inaelekea kwenye siasa ya uchumi wa viwanda, bila ya kilimo hakuna viwanda, hivyo ni vyema Serikali ikawawezesha wakulima kwa kuwapatia pembejeo hizo.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika suala la pembejeo kwa Serikali kuweka bei wezefu ambazo wakulima wetu wa chini wataweza kununua/watamudu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, kwanza nachukua fursa hii kwa kukushukuru wewe kwa kunipatia fursa hii ya kuchangia katika hotuba ya Wizara hii. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuitayarisha na kuiwakilisha hotuba hii katika Bunge lako kwa ufasaha mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, Elimu na Mafunzo ya Uvuvi; nachukua nafasi hii kuipongeza Wizara kwa kuweka mpango huu mzuri katika nchi yetu ambao una manufaa kwa wavuvi wetu. Katika Hotuba ya Waziri, Ukurasa wa 89 – 90 imeeleza namna ya FETA kwa kushirikiana na NORGEES VEL ya Norway iliyofadhili kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya pamoja na mambo mengine lakini zaidi kufundisha stadi za ufugaji na biashara katika maeneo kadhaa ya nchi yetu. Hili ni jambo zuri ambalo linapaswa kushukuriwa na kupongezwa. Ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba, Wizara ipanue wigo wa kueneza jambo hili katika maeneo mengi zaidi, hasa yale ya vijijini ambako kuna wavuvi ambao uwezo wao ni mdogo sana.

Mheshimiwa Spika, Migogoro Kati ya Wafugaji na Wakulima; tatizo la migogoro ya ardhi kati ya makundi haya makubwa katika nchi yetu bado ni kubwa. Ni vyema Wizara ikalichukulia jambo hili kwa uzito unaostahili ili kulitafutia ufumbuzi wa kudumu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natoa shukrani zangu kwako kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika Wizara hii. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuwasilisha katika Bunge lako Tukufu hotuba hii kwa ufanisi mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii napenda kutoa mchango katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Idara ya Utalii; napenda kuipongeza Wizara hii kwa mikakati na matayarisho mazuri katika Idara hii ya Utalii. Hii ni Idara muhimu sana katika tasnia ya utalii. Ni idara ambayo inatakiwa iweze kupanga mipango mikakati ya kuongeza watalii nchini. Utalii ni miongoni mwa vyanzo vizuri katika nchi yetu, hivyo idara hii inafanikiwa kujua hilo na kulitafsiri kwa vitendo ili kufikia azma hii ya kuwa chanzo cha nchini katika nchi yetu badala ya kutegemea vyanzo vingine ambavyo havina uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu mwingine katika Idara hii ni kutayarisha mazingira ambayo watalii wanaokuja nchini waweze kufika katika vivutio vyetu vyote hasa vile vya Zanzibar. Zanzibar ni sehemu ambavyo vivutio vyake ni vya bahari na huku bara vivutio vyake vingi ni vya mapori, hivyo ni vizuri kuwaonesha watalii wanaokuja nchini vivutio vya aina tofauti vilivyopo kwenye nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, kwanza natoa shukrani zangu kwake kwa kunipatia fursa hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuandika na hatimaye kuiwakilisha kwa ufasaha wa hali ya juu. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, mchango wa Sekta ya Madini kwenye pato la Taifa; napenda kuipongeza Serikali pamoja na Wizara kwa kuweka mikakati mizuri katika Sekta ya Madini. Sekta hii ni miongoni mwa sekta muhimu sana katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika suala hili, ni kwamba Serikali iendelee kuweka mikakati ya kuimarisha sekta hii ili kuweza kuongeza pato la Taifa, ni vyema Wizara ikaweka wafanyakazi waaminifu katika sekta hii ambao watasimamia vyema mapato kwa uhakika na kwa uaminifu mkubwa. Mikakati hii iwe ya uhakika na kitaalam zaidi.

Mheshimiwa Spika, uendelezaji wa uchimbaji mdogo wa madini, naipongeza Wizara kwa kuendeleza jambo hili katika maeneo husika. Hii ni sehemu moja kubwa ambayo itaweza kuongeza ajira kwa wananchi wa maeneo husika na kuweza kupunguza umaskini.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika suala hili ni kwamba Wizara iendelee kuwasahihisha wananchi kwa kuwapa elimu na vitendea kazi vya kisasa ili waweze kumudu kazi zao na kuleta ufanisi zaidi. Aidha, Wizara iendelee kuwashirikisha wananchi wa maeneo husika kwenye sekta hii ili na wao wajihisi kama ni sehemu ya kuchochea maendeleo katika sekta hii. Wizara itakapowashirikisha kikamilifu wataweza kulinda na kuithamini sekta hii muhimu katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Nishati. Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na kuwasilisha hotuba hii kwa umakini mkubwa. Katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, Bomba la Mafuta Kutoka Uganda – Tanga. Napenda kuipongeza Serikali na Wizara kwa kufuatilia kwa karibu sana juhudi za kufanikisha mradi huu wa bomba la mafuta kutoka Uganda – Tanga, Tanzania. Tuna bahati kubwa kupata fursa hii ya kipekee. Pamoja na vigezo kadhaa vilivyotumika kutupatia mradi huu lakini kigezo cha amani na usalama katika nchi yetu pia kinapaswa kuzingatiwa na Watanzania. Hivyo ni wajibu wetu Watanzania sote kupitia Serikali na Wizara kuilinda amani hii na kuthamini fursa hii tuliyopewa na jirani zetu.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu; katika jambo hili kwa Serikali ni kuendelea kuwashirikisha wananchi wote wa maeneo husika kwa kuwaelimisha faida na hasara zake. Wananchi wa maeneo hayo watakapopata elimu watajiweka katika nafasi ya kujiona kuwa bomba hili ni lao na watachukua hatua za kulilinda na kulienzi.

Mheshimiwa Spika, naunga hoja mkono.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kukushuKuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika Hotuba ya Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka 2019/2020. Pia niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kuandika na hatimaye kuwasilisha kwa ufasaha mkubwa katika Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuunga mkono hoja hii kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Bajeti hii ni bajeti ya matumaini sana kwa wananchi wote wa Tanzania. Bajeti hii inatoa ufafanuzi mzuri juu ya kupunguza umaskini katika nchi yetu. Hii inatokana na kuangalia mahitaji ya raia maskini yamezingatiwa kwa rasilimali za Serikali. Kodi zote zinazoidhinishwa kwenye mpango huu zinawajenga zaidi maskini badala ya kuwalemaza. Wananchi wana matumaini makubwa na bajeti hii kwa kuwa Serikali imeangalia katika maeneo ya biashara na uwekezaji katika kuimarisha nafasi zote zitakazojitokeza. Bajeti hii imeakisi maisha ya kila Mtanzania mwenye ndoto ya kufikia kilele cha mafanikio. Hizo ndio miongoni mwa sababu zinazonisukuma niunge mkono hoja hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushirikishwaji wa wadau katika kuandaa bajeti hii; katika hitimisho lake Mheshimiwa Waziri ametaja wadau ambao amewashirikisha katika kuandaa bajeti hii. Hili ni jambo jema sana. Ushauri wangu katika suala hili ni kuiomba Serikali kwa bajeti zinazofuatana kuwashirikisha Mabalozi wetu wanaotuwakilisha katika nchi za nje. Hili ni kundi muhimu sana katika nchi yetu ambalo lina uelewa mzuri (exposure) katika nchi inazotuwakilisha. Wanaweza kutumia uzoefu wa bajeti za nchi wanazotuwakilisha na kuuleta kwa matumizi ya bajeti ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vyanzo vya mapato; Mheshimiwa Waziri ameeleza vyanzo vingi vya mapato ambavyo miongoni mwao ni tegemezi, lakini tuna vyanzo ndani ya nchi yetu ambavyo kama tukiviboresha vitaweza kutoa mchango mkubwa sana, mfano ni Bandari bubu.

Mheshimiwa Naibu Spika, bandari hizi zinaitwa bubu kwa kukosa huduma muhimu za wafanyakazi. Ikiwa Serikali itaweza kupeleka Maafisa wa Mamlaka ya Bandari na maofisa wa TRA, bandari hizi zitabadilika kuwa bubu na kuwa bandari official na zitaweza kutoa mchango mkubwa katika nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri mkuu.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na watendaji wake wote kwa kuweza kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha kwa makini na kwa ufasaha mkubwa hotuba hii iliyojaa matumaini makubwa kwa wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Kwanza ni kuhusu huduma za jamii; napenda kuchukua fursa hii kuipongeza kwa dhati Serikali yetu ya awamu tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Joseph Magufuli kwa kusimamia vizuri pamoja na mambo mengine kuwa na uendelezaji wa huduma za jamii nchini. Kitendo cha kuweka elimu bila ya ada ni kitendo chema na kinapaswa kupongezwa na jamii yote ya Tanzania. Elimu ndio ufunguo wa maisha, mtu kukosa elimu sio jambo sahihi. Tunaipongeza Serikali yetu kwa jambo hilo.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba Serikali ifuatilie na ielimishe wananchi hasa wa kijijini juu ya kuweka fursa hii. Inawezekana fursa hii ikatumika kwa watu wanaoishi mijini tu na kukosekana kuwafaidisha wananchi wa vijijini kutokana na kutokuwa na fursa hii.

Pili ni TASAF, miongoni mwa mipango bora ya kuwawezesha wananchi kiuchumi na kupunguza umaskini ambazo Serikali yetu imeendelea kufanya ni kupitia mpango huu wa TASAF. Mpango huu ni miongoni mwa mikakati inayopaswa kuendelezwa kwa nguvu zote. Mpango huu umesaidia sana wananchi hasa wale wa kaya maskini, umewainua kiuchumi, kufikra na umewaendeleza katika juhudi zao za kujitafutia kipato.

Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kuipongeza Serikali yetu inayoongozwa kwa umakini kwa hali ya juu na Mheshimiwa Rais wetu mpendwa. Ushauri wangu katika jambo hili kwa watendaji kama alivyoagiza Mheshimiwa Waziri Mkuu kuwa waaminifu katika kutekeleza jambo hili. Bado kuna manung’uniko katika upembuzi usiokuwa sahihi wa kaya husika. Bado kuna kaya ambazo hazina sifa ya kupata fursa hii na zinaachwa zile ambazo zinastaahiki kupata fursa hii.

Mheshimiwa Spika, tatu ni kilimo; kilimo ni uti wa maisha na maendeleo ya nchi. Serikali yetu inaendelea na juhudi za kusimamia kwa ukamilifu kilimo ili kuona tumefikia katika malengo tuliyojiwekea. Miongoni mwa mambo ambayo Serikali inayasimamia ni pembejeo na zana za kilimo. Bila ya pembejeo na zana za kilimo hakuna uwezekano wa kupata mafanikio ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, nashauri sana Serikali kwa kuiwezesha, kuisimamia na kujielekeza Benki ya Kilimo ya TADB kuhusu kuwakopesha wakulima wetu wa chini, lakini bado gharama za matrekta ni kubwa sana. Kikundi cha wakulima ambao nimejipanga kuendeleza kilimo kuwapa mkopo wa shilingi milioni 78, ni kitendo ambacho kinatakiwa kuangaliwa, si rahisi kuweza kumudu kurejesha mkopo wa aina hii kwa wakati. Ushauri wangu katika hili TADB iendelee kutafuta namna nzuri zaidi ya kuweza kuwapunguzia wakulima bei ya trekta ili waweze kumudu kwa wingi kukopa matrekta hayo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, natoa shukurani zangu za dhati kwako kwa kinipatia fursa hii ya kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Pili, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwalisha katika Bunge lako tukufu kwa umakini mkubwa na kwa ufasaha wa hali ya juu kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi katika kutoa mchango wangu kwa Wizara hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; kwanza ni kuhusu Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Kujenga Taifa ni kitengo muhimu sana katka nchi yetu, ni kitengo kinacholea vijana na kuwaelekeza namna bora ya kuishi katika nchi yetu na katika jamii kwa jumla. Jeshi hili ni lina vitengo muhimu sana katika maisha ya kiuchumi na kuwawezesha wananchi kiuchumi, kwa mfano uvuvi, mifugo na kilimo. Jeshi hili lina wataalam wa kutosha katika maeneo hayo. Aidha, maeneo hayo yanahitajika sana na wananchi wa maeneo hayo huku uraiani ili kuweza kujikwamua kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Wizara na Serikali kwa jumla ni kuushusha utaalam huu kwa raia kwa kuwaelimisha namna ya kuendeleza miradi hii.

Kuhusu makazi ya wanajeshi, napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyochukua juhudi kubwa ya kuwawezesha wanajeshi wetu katika maeneo kadhaa ili kuwafanya wanajeshi wetu kuweza kufanya majukumu yao ya kila siku. Lakini wanajeshi wetu bado wanakabiliwa na tatizo dogo la makazi. Wanajeshi wetu kama binadamu wengine wanahitaji mambo yote ya kimsingi (chakula na makazi). Serikali inachukua jitihada kubwa kwa kuwapatia chakula cha kutosha na bora. Lakini bado wanajeshi wetu makazi yao hayaridhishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado katika maeneo kadhaa wanajeshi wetu wanafanyakazi makambini lakini wanalala uraiani. Hii ni hatari kwa usalama wa wanajeshi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali kuendelea kuchukua juhudi za makusudi ili kutatua tatizo hili la makazi kwa wanajeshi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba ya Wizara hii. Hii ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika nchi yetu. Wizara inawahusu wananchi wote wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako Tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; nikianza na mafunzo kwa watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Wizara hii kwa mipango yake madhubuti ya kuiongoza Wizara hii. Kwa kweli wanaendeleza na kuiongoza Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, dunia sasa hivi inaendelea kwa kasi sana kwa nyanja zote za kiuchumi, kisiasa na kitekhnolojia. Hivyo basi ili kuenda sambamba na kasi hiyo hatuna budi kuwapa fursa za masomo watendaji wetu. Lazima tuwasomeshe ili waweze kufanya kazi zao kiutaalam na kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2020 Wizara hii iliahidi kutoa mafunzo kwa watendaji 700. Lakini mpaka hotuba hii inasomwa leo ni asilimia 19.5 tu ya ahadi hiyo ndio ilioweza kutekelezwa; yaani ni watendaji 137 ndio waliopata mafunzo; hii ni idadi ndogo sana. Pamoja na kwamba Wizara haikusema sababu ya kutokifika lengo hilo lakini ukweli unabaki pale pale kuwa hii ni idadi ndogo kabisa.Ushauri wangu kwenye jambo hili kwa Serikali kuweka kipaumbele cha hali ya juu kutoa mafunzo kwa watumishi wa Wizara hii ili kuenda sambamba na kasi ya ukuaji wa kiitaalam duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ni kuhusu utawala na raislimali watu. Rasilimali watu ni kitendea kazi katika Wizara. Ni lazima suala hili lifikiriwe kwa nguvu zote. Upungufu wa wafabyakazi 3,114 katika nchi ambayo kila mwaka inatoa wahitimu wengi, ni kitu ambacho hakipendezi. Ushauri wangu kwa suala hili kwa Serikali ni kutoa fursa za ajira kwa vijana ambao wapo wengi sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, natoa shukurani zangu za dhati kwako kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Wizara ya Kilimo. Wizara hii ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika nchi yetu.

Pili nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwakilisha katika Bunge lako Tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa. Hotuba hii ni imesheheni mambo ambayo kwa sasa yanahitajika katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia maeneo yafuatayo, nikianza na umwagiliaji na ushirika.

Mheshimiwa Spika, napenda kuipongeza kwa dhati Serikali yetu kwa namna inavyochukua jitihada kubwa katika kuboresha kilimo katika nchi yetu. Kama inavyojulikana kuwa kilimo ni uti wa mgongo katika nchi.

Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri imetaja namna inavyoendelea kuchukua juhudi za kutengeneza maeneo ya unwagiliaji katika nchi yetu. Hivyo imeonesha kuwa kuna engezeko la hekta 330 kutoka mwaka 2020 mpaka 2021.

Mheshimiwa Spika, hotuba imeonesha kuwa mwaka 2020 ilikuwa na hekta 694,715 na mwaka 2021 ni hekta 695,045 za umwagiliaji; sawa na ongezekko la hekta 330.

Mheshimiwa Spika, hili ni ongezeko dogo sana ukilinganisha na umuhimu wa kilimo katika nchi yetu. Aidha, ni ongezeko dogo sana ukilinganisha na ukubwa wa eneo la ukubwa wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni kuongeza juhudi kwa kasi ya zaida kuongeza maeneo ya umwagiliaji.

Pili ni upatikanaji wa pembejeo; wananchi wa Tanzania wanajitahidi sana pamoja na watendaji wa Wizara hii ya Kilimo kutaka kufikia malengo yao ya kimaisha kupitia kilimo. Lakini juhudi hizi zinakwama kutokana na matatizo makubwa ya pembejeo na zana za kilimo. Bado kuna ukakasi mkubwa wa upaikanaji wa pembejeo. Wakulima wanapata shida kupata pembejeo katika maeneo yao.

Aidha, wakulima wetu wanapata shida na wanashindwa kumudu kununua zana za kisasa za kilimo. Bado upatikanaji wa zana hizo ni jambo ambalo ni gumu kwa wakulima wa kawaida. Mfano Serikali ina lengo la kuwatoa wakulima kutumia jembe la mkono, lakini mpaka leo bei ya trekta moja ni kubwa sana kiasi ambacho sio rahisi kwa wakulima wa hali ya chini ambao ni kundi kubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali kuhusu jambo hili ni kuangalia namna ya kuboresha upatikanaji wa pembejeo na urahisi wa bei za zana za kilimo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukrani zangu za dhati kwako kwa kunipa fursa hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Wizara ya Viwanda na Biashara. Wizara hii ni miongoni mwa Wizara muhimu katika kuendesha uchumi wa nchi yetu.

Pili, natoa pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha katika Bunge lako Tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia maeneo yafuatayo; kwanza ni kuhusu mazingira ya kibiashara katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa juhudi kubwa inayochukua katika azma yake ya kuelekea kwenye suala la biashara. Ni azma nzuri ambayo itatuvusha katika kuinua uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lolote linahitaji matayarisho ya kufanikisha jambo hili. Matayarisho hayo ni kuliwezesha jambo hilo kufanikiwa. Bado katika nchi yetu hatujaweza kufanikisha kutayarisha mazingira bora ya kibiashara. Wafanyabiashara wengi hasa wawekezaji wanapata usumbufu namna ya kupata hudumu hasa ya usajili wa biashara zao. Bado kuna mzunguko wa kupata ruhusa ya kufanya au kuwekeza biashara zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali ni kuendelea kwa kasi kubwa kutengeneza mazingira yatakayowavutia wawekezaji wa nje na ndani.

Pili ni kuhusu uhusiano kati ya biashara na kilimo; ni jambo muhimu na ni lazima katika kuleta maendeleo ya kiuchumi katika nchi. Viwanda vyovyote haviwezi kutekeleza malengo yake bila ya kilimo. Kilimo ndio kitakachotoa malighafi ya kuendeleza kiwanda.

Ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kutengeneza mazingira ya kupunguza bei za pembejeo za kilimo ili wakulima waweze kuzalisha mazao ambayo yatapelekwa viwandani kuweza kuendesha viwanda kwa kuzalisha mali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. OTHUMAN HIJA JUMA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukuwa fursa hii kutoa shukurani zangu kwako kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022. Hii ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimae kuiwasilisha katika Bunge lako Tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo. Kwanza ni kuhusu sekta ndogo ya umeme na hali ya upatikanaji wa umeme nchini. Napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyofanya jitihada kubwa ya kutafuta vyanzo vya umeme vya kila aina. Vyanzo vyote ni muhimu sana na vitasaidia katika upatikanaji wa umeme.

Mheshimiwa Spika, uchunguzi unaonesha kuwa umeme wa gesi ni rahisi sana ukilinganisha na vyanzo vingine. Hivyo, ushauri wangu kwa Serikali katika suala hili ni kuharakisha matumizi ya chanzo hiki ili kuwarahisishia maisha wananchi wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, lingine ni mradi wa kuzalisha umeme wa Ruhudji. Mradi huu ni mkubwa sana ambao unazalisha MW 358 kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Ruhudji. Mradi utajengewa laini yenye urefu wa kilometa 170 yenye mkondo wa 400kv. Urefu wa kilometa 170 ni mrefu ambao bila ya shaka laini itapita kwenye vijiji kadha katika maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba wapitie shirika letu la TANESCO na kuweka vituo vya kupoza umeme (substations) katika maeneo yatakayopitiwa na line hii ili wananchi wa maeneo hayo yaweze kufaidika na umeme huo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukurani zangu za dhati kwako kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022. Hii ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika nchi yetu kwa uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwakilisha katika Bunge lako Tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza kwa dhati Serikali yetu kwa namna inavyochukua jitihada kubwa ya kuboresha miundombinu katika sehemu za kitalii. Uboreshaji huu utavutia kuja kwa watalii jambo ambalo litaongezea Taifa letu kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utalii umegawanyika katika sehemu mbili; utalii wa ndani na utalii wa nje. Naipongeza Serikali kwa kuboresha utalii wa nje lakini bado utalii wa ndani haujakaa vizuri. Bado bei za kuingilia katika vituo vyetu vya kitalii ni kubwa kwa watalii na wananchi wetu. Wengi wanashindwa kutumia fursa hii ya kuona rasilimali yetu. Ushauri wangu katika suala hili kwa Serikali ni kuweka bei rafiki kwa watalii wetu wa ndani ili nao waweze kufaidi rasilimali za nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyochukuwa jitihada ya upandaji wa miti. Bado juhudi hii haijafika katika kiwango cha kuridhisha. Idadi ya ongezeko la mashamba bado ni dogo. Ongezeko kutoka mashamba 23 mpaka 25 ni dogo mno. Ushauri wangu kwa Serikali ni kuongezwa kwa jitihada za makusudi ya kupanda miti ili kuboresha utalii katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. OTHUMAN HIJA JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba ya Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Mwaka 2021/2022.

Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa namna alivyoanza kuonesha uwezo mkubwa wa kuliongoza Taifa letu. Namuombea kila la kheri katika maisha yake na tatu, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii kwa ufanisi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kuhusu sera na mikakati ya kuongeza mapato; Mheshimiwa Waziri ametaja hatua kadhaa kama nane hivi ambazo kama tukizisimamia zitatuwezesha kufikia malengo ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hatua hizo bado kuna maeneo ambayo kama Serikali ikiziboresha zinaweza kutuongozea mapato ya ndani. Moja katika sehemu hizo ni sehemu ya bandari bubu. Bandar bubu ni moja kati ya sehemu nyeti sana ambazo kama zikiboreshwa zinaweza kutuongozea mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika suali hili ni kuiomba Serikali kuziboresha kwa kuzipelekea wafanyakazi wa Mamlaka za Mapato wenye kutambulika na Serikali na wenye ujuzi wa kufanya kazi za ukusanyaji wa mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili ni kuhusu Jeshi la Polisi; naipongeza sana Serikali kwa kuwaondoshea askari tatizo la ajira. Tatizo hili ni la muda mrefu sana na lilikuwa linawadhalilisha askari wetu. Lakini hatuba hii imeacha kuzungumzia makazi na vitendea kazi kwa askari wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya muda wa zaidi ya miaka hamsini bado kuna maeneo ambayo makazi ya askari wetu hayaridhishi, majengo ni mabovu sana ambayo hayastahili kutumika na askari wetu. Ushauri wangu katika jambo hili ni Serikali kulishughulikia kwa nguvu zake zote suala hili la makazi na vitendeya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu ni kuhusu wakulima wadogo wadogo; lazima tukubali kuwa katika nchi hii wakulima wetu wanafanya kazi kwa bidii kubwa lakini bado wanakwazwa na mambo kadhaa katika maisha yao ya kikazi. Wanakabiliwa na upatikanaji wa pembejeo kwa kiasi kikubwa sana. Bado mazingira ya utendaji wa kazi zao sio rafiki. Aidha, wakulima wetu wanakabiliwa na uwezo mdogo kifedha. Mabenki yanawapatia mikopo yenye riba kubwa sana ambayo yanawapelekea kufilisika kabisa. Ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuwatengenezea mazingira mazuri ya kupata mikopo yenye mashart nafuu ili waweze kujiendeleza na kazi zao hizi. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, napenda kuanza mchango wangu kwa kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoongoza nchi yetu kwa umakini mkubwa. Namuombea kila la kheri katika kazi zake.

Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na wafanyakazi wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwakilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; kwanza ni Benki ya Maendleo ya Kilimo; napenda kutoa shukurani zangu za dhati kuishukuru Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza mpango wa kuipatia fedha benki hii kwa ajili ya mikopo ya wakulima hasa wadogo wadogo. Benki hii ni mategemeo makubwa kwa wakulima wetu katika ukombozi wa kujinasua kiuchumi.

Ushauri wangu katika jambo hili Serikali iendelee kuhakiki aina ya wakulima wanaostahiii kupata mikopo hiyo ili kuepuka kila mwaka kurejea makundi hayo hayo na kuwaacha wengine.

Mheshimiwa Spika, pili ni kuhusu uvuvi; napenda kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa jitihada yake kubwa inayochukua katika kuimarisha sekta hii ya uvuvi. Sekta hii ni miongoni mwa sekta inayowagusa moja kwa moja wananchi wa kipato cha chini. Ushauri wangu kwa Serikali katika sekta hii ya uvuvi ni kuwaendeleza wavuvi hasa wadogo kwa kuwapatia mitaji, aidha kwa njia ya mikopo au kwa ruzuku ili kuweza kujiendeleza na kuweza kujikwamua kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, tatu ni uwekezaji; napenda kuipongeza Serikali yetu kwa mipango yake yenye azma ya kutekeleza na kukuza uchumi wa nchi kwa kuvutia wawekezaji katika nchi yetu. Uwekezaji ni jambo jema, likisimamiwa vizuri kwa kuliwekea mazingira mazuri ambayo yatawavutia wawekezaji wa ndani na nje.

Ushauri wangu kwa Serikali juu ya sekta hii ya uwekezaji ni kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji. Bado mpaka leo kuna manung’uniko yasiyo rasmi kwamba upatikanaji wa maeneo ya uwekezaji sio rafiki. Wawekezaji wanachukua muda mrefu kupata maeneo hayo hasa ardhi. Urasimu bado unawasumbua wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii jioni hii ili nami nitoe mchango wangu katika Kamati hizi tatu za PAC, PIC na LAAC. Aidha, napenda kuwapongeza Wenyeviti wote wa Kamati tatu hizi pamoja na wajumbe wao wote kwa namna walivyotayarisha na hatimaye kuwasilisha ripoti zao katika Bunge lako Tukufu kwa ufasaha wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mengi yamezungumzwa. Mimi katika mchango wangu wa leo nitachangia kuhusu ukiukwaji wa taratibu za uendeshaji kazi katika wizara, idara na mashirika yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli, ni jambo la kusikitisha sana kuona kwamba, baada ya miaka 60 yetu ya uhuru bado kuna idara zetu na mashirika yetu yanafanya kazi kwa kukiuka taratibu. Hasa inasikitisha zaidi unapoona kwamba yanayofanyika na wanaofanya haya ni wale ambao wanatakiwa wasimamie utaratibu ule; ni jambo la kusikitisha sana.

Mheshimiwa Spika, katika Ripoti ya CAG imeonekana kwamba Lindi Regional Police Commander walimkodia OCD wao ofisi kutoka National Housing kwa malipo ya 1,770,000/=. Katika hili polisi walikuwa wanalipa pungufu; 1,770,000/= wao walikuwa wanalipa 1,500,000/=. Kwa hiyo kulikuwa kuna bakaa ya kama 200,000/= kila mwezi. Hii ime-accumulate fedha jumla ya milioni 37 ambazo mpaka sasahivi hawajalipa.

Mheshimiwa Spika, lakini issue si hiyo, issue ni kwamba hakukuwa na mkataba baina ya Polisi na National Housing, mambo yalikuwa yanakwenda kihivihivi tu. Ndipo pale ninaposema kwamba inasikitisha zaidi kuona kwamba wale wasimamizi wa sheria ndio ambao wanavuruga sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili utakwenda kwenye kutekeleza hoja za ukaguzi. Asubuhi hii kuna mjumbe mmoja, Mheshimiwa Tarimba, alisimama akaeleza namna ya dharau watendaji wetu wanavyodharau. Katika Ripoti ya CAG imeonekana kwamba, katika kipindi cha 2019 Jeshi la Polisi walipewa hoja 13 na CAG, lakini mpaka kufikia hii leo hapa tulipo wametekeleza hoja tatu tu. Kwa hiyo, hii ni ile dharau, kwamba wao wanadharau maelekezo hata ya CAG. Wamepewa hoja 13 wametekeleza tatu tu mpaka hii leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu na la mwisho ni kuhusu kutokutekeleza hata ile mipango yao wanayopanga. Katika uchunguzi wa CAG imeonekana kwamba National Housing katika mipango yao ya 2015/2016, katika strategy planning yao, walijipangia wenyewe watengeneze kampuni tanzu ambayo itawasaidia kwenye mambo yao ya uendeshaji, lakini mpaka hii leo tuko hapa kampuni tanzu hii hawajafanya na zoezi hili bado linasuasua.

Mheshimiwa Spika, mimi kwa haya yangu matatu niliyochangia naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Ofisi ya Makamu wa Rais, (Muungano na Mazingira) kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; nikianza na fedha za Mfuko wa Jumbo; napenda kuipongeza na kuishukuru Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka mpango huu wa Mfuko wa Kuchochea Maendeleo katika Majimbo yote nchini.

Mheshimiwa Spika, kama inavyosomeka dhana ya mfuko huu ni kuchochea maendeleo, lakini kwenye baadhi ya majimbo mengine huwa haikidhi dhana hii; kwa mfano katika majimbo ya Zanzibar kama inavyojulikana kuwa mwaka 2015 ulifanyika ukataji mpya wa majimbo, majimbo mengine yameongezeka sana. Miongoni mwa majimbo hayo ni jimbo la Tumbatu.

Mheshimiwa Spika, kiasi ya fedha tunachopata ni kile kile tangu jimbo halijaongezeka, hivyo basi tunaomba Serikali ichukue hatua maalum ya kuongeza fedha katika majimbo hayo yaliyoongezeka.

Mheshimiwa Spika, pili ni kuhusu tathmini iliyofanywa juu ya Taasisi za Muungano; napenda kuipongeza Serikali kwa kufanya zoezi hili. Hili ni jambo muhimu sana ili kujua mahitaji ya taasisi hizi. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema kuwa ni taasisi 20 ndio zilizofanyiwa tathmini, lakini Mheshimiwa Waziri hakuzitaja. Ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuzitaja taasisi hizi ili nasi tuzitambue kwa manufaa ya wananchi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, tatu ni kutoa elimu kwa umma kuhusu Muungano; napenda kutoa pongezi za dhati kwa Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua hii ya kuwaelimisha wananchi wa Tanzania. Ni dhahiri kuwa mpaka hii leo baada ya miaka 58 bado wapo watu hawajui maana ya Muungano.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili haliwezi kufanikiwa kwa asilimia kubwa kutokana na vyombo vinavyotumika kueneza elimu hii. Kwa mfano wananchi wa vijijini hawawezi kuwa na redio, tv, mitandao ya kijamii au majarida yaliyotajwa katika hotuba hii. Hivyo ushauri wangu katika jambo hili ni kutafuta njia sahihi ya kuwafikia wananchi wa vijijini.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba ya makadirio na mapato ya Wizara ya Madini kwa mwaka wa fedha 2022/ 2023.

Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo nikianza na suala la wachimbaji wadogo; napenda kuipongeza Wizara kwa juhudi zake inayozichukua katika kuwaenzi wachimbaji wadogo. Hili ni kundi kubwa na ni muhimu katika nchi yetu. Kundi hili kwa muda mfupi limeonesha maendeleo katika kuchangiya pato la Serikali.

Mheshimiwa Spika, napenda kushauri Serikali mambo mawikli katika kundi hili; kwanza Serikali ioengeze jitihada ya kuwapatia mafunzo zaidi wchimbaji hawa ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi.

Pili, nashauri Serikali iwapate bima za afya wachimbaji hawa ukizingatia kuwa kazi hii ni miongoni mwa kazi ngumu na za hatari. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami nichukue fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ili nitoe mchango wangu katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, lakini pili nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake Waziri kwa namna walivyowasilisha hotuba hii kwa umakini mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ni Wizara muhimu sana inayolinda amani yetu katika nchi yetu. Katika kuchangia hotuba hii mimi nitachangia masuala mawili tu ambayo yamo katika jimbo langu. Jambo la kwanza ni kuhusu ujenzi wa Kituo cha Polisi katika Kisiwa kidogo cha Tumbatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuwa kila ninapopata nafasi ya kusimama kuchangia katika Bunge lako Tukufu nimekuwa nikilizungumza suala hili la kujenga Kituo cha Polisi katika Kisiwa cha Tumbatu. Mara ya mwisho nilipokuwa nalizungumzia suala hili kupitia swali langu namba 36, Mheshimiwa Waziri alinijibu kwamba, Serikali itachukua hatua ya kufanya tathmini ya kitaalamu ili kuona namna ya kujenga Kituo cha Polisi katika Kisiwa cha Tumbatu. Mpaka leo sijajua nini kinaendelea? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine ni kwamba, alinitaka nioneshe initiative ya kujenga Kituo cha Polisi pale kwetu Tumbatu. Mimi nili-provide kiwanja kwa ajili ya kisiwa kile lakini mpaka leo hii kiwanja kile kipo, hakuna kinachoendelea. Kwa hivyo, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kusimama hapa atueleze nini kinaendelea kuhusiana na ujenzi wa Kituo cha Polisi katika Kisiwa cha Tumbatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo langu la pili ni kuhusu Kituo cha Polisi cha Mkokotoni. Mara ya mwisho nilivyokuwa nazungumza kuhusu jengo la Mkokotoni nilieleza masikitiko yangu makubwa kuhusu hali ilivyo pale Mkokotoni. Askari wa pale walikuwa wanaishi katika mazingira magumu, mabovu, walikuwa wanafanya kazi inaponyesha mvua wana-shift kutoka walipo wanafanya kazi katika chumba kidogo cha mahabusu.

Mheshimiwa Spika, lakini leo nasimama hapa kutoa shukrani zangu za dhati kwa Serikali yetu kwa kutujengea kituo chetu kikuu kile. Tunashukuru sana kwa kutujengea kituo kile. Tumeshapata kituo kizuri cha kisasa kabisa. Ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri na kwa Wizara ni kukiboresha kituo kile, kukiboresha kwa maana ya kwamba, kukijengea thamani na kukijengea uzio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi nilipokwenda kukiangalia kile Kituo cha Polisi cha Mkokotoni waliniambia kwamba, wameshaanza kujenga uzio lakini wamesita kutokana na upungufu wa fedha. Kwa hiyo, naomba Wizara itupatie fedha, iwapatie fedha ili wamalize ule ukuta pale Mkokotoni. Aidha, makazi ya maaskari ya pale Mkokotoni ni mabovu sana. Kuna nyumba pale zimejengwa kabla ya uhuru, yaani kabla ya mapinduzi; nyumba ni chakavu, hazistahiki kabisa kuishi maaskari wetu. Kwa hivyo, naomba Wizara ichukue juhudi za makusudi kuwajengea makazi askari wa pale Mkokotoni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hayo yangu mawili ambayo yanahusu jimbo langu naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa spika, nakushuku kwa kinipatia fursa hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Wizara ya Elimiu, Sayansi na Teknolojia kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwakilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; vyuo vya VETA.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kupia Wizara hii kwa kuendeleza utararibu mzuri juu ya uendeshaji wa vyuo hivi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, vyuo vya VETA ni mwanzo mzuri wa kuwanoa na kuwapa matumaini juu ya hatima ya wanafunzi kimaisha. Lakini inaonekana kuwa baadhi ya masomo yanayofundishwa kwenye vyuo hivi hayawapi matumaini hayo wanafunzi. Madhumuni makuu ya kusoma baada ya kusoma ni kuweza kujikimu maisha yake aidha kwa kuajiriwa au kwa kujiajiri mwenyewe. Lakini bado lengo hili hafikiwi kutokana na nature ya course husika.

Ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuweka masomo ambayo yatakuwa rahisi kuwasaidia vijana wetu kupata ajira.

Pili ni kuhusu mikopo ya wanafunzi; napenda kuipongeza Serikali kwa kuweka mpango huu mzuri wa kuwakopesha vijana wetu ili waweze kutimiza ndoto zao za kimaisha.

Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa suala hili napenda kuishauri kwa Serikali mambo yafuatayo: -

(a) Serikali irekebishe vigezo vya kupata mikopo hiyo.

(b) Kuongeza kima cha fedha ili waweze kukopeshwa wanafunzi wengi zaidi.

(c) Wanafunzi wanaosoma elimu ya kati pia nao wapate fursa ya mikopo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Pili, naungana na wezangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimae kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, nianze na hali ya upatikanaji wa maji vijijini; napenda kuipongeza Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mikakati ya kumtua mama ndoo kichwani. Hili ni jambo zuri sana na la kupigiwa mfano katika nchi yetu.

Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeonesha kuwa upatikanaji wa maji vijijini unaongezeka kila mwaka. Mwaka 2021 hali ya maji vijijini ulikuwa asilimia 74.5, mwaka huu imepanda kwa asilimia mbili. Naipongeza Serikali yetu kwa rekodi hii ya manufaa kwa wananchi.

Ushauri wangu katika upatikanaji wa maji vijijini ni kuendelea kuwasogezea vyanzo vya maji karibu na maeneo yao ili kuwapunguzia masafa marefu ya kufuatilia maji kwa matumizi yao.

Mheshimiwa Spika, pili ni kuhusu udhibiti wa uchafuzi wa vyanzo vya maji; vyanzo vyetu vya maji vinahitaji kuhifadhiwa sana. Vyanzo vingi vya maji viko katika hali ya kuweza kuhatarisha maisha ya wananchi. Utakuta chanzo cha maji hakina uzio wa kukihifadhi, wanyama wanaweza kuingia kwenye chanzo cha maji na kuhatarisha maisha. Aidha, kutokana hali ya dunia sasa hivi watu ambao si wazuri wasiopenda maendeleo inakuwa ni rahisi kuweza kufanya uharibifu wa chanzo cha maji.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuendelea kuchukua hadhari ya kuviwekea uzio vyanzo vote vya maji nchini.

Mheshimiwa Spika, kuhusu vibali vya kuchimba maji; naipongeza Wizara ya Maji kwa kuweka utaratibu huu wa kuruhusu wananchi kuchimba visima vyao kwa matumizi yao binafsi. Hili ni jambo zuri sana litaisaidia Wizara kwa sehemu kubwa.

Ushauri wangu katika jambo hili ni kuweka udhibiti kwa kuwapa maelekezo ya kitaalam namna ya kuchimba visima hivyo ili kuepuka hatari ya miripuko ya maradhi yanayotokana na maji yasiokuwa salama.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa pongezi za dhati kwako kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimae kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; nikianza na upungufu wa dawa nchini.

Mheshimiwa Spika, napenda kuipongeza Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoongoza nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, matatizo ya upungufu wa dawa katika nchi yetu ni ya kusikitisha sana. Tatizo hili ni kubwa na linakera sana. Serikali inajitahidi sana kutoa pesa kwa madhumuni ya ununuzi wa dawa lakini bado ufumbuzi wa suala hili ni kubwa. Ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuweka mikakati madhubuti ya kuwadhibiti maafisa wetu wanaohusika na manunuzi ya dawa ili kuwachulia hatua za kinidhamu na kisheria ili kukomesha kabisa suala hili.

Mheshimiwa Spika, pili ni kuhusu chanjo; naipongeza Serikali yetu kwa kuendelea kuratibu upatikanaji wa chanjo pamoja na kuhakikisha chanjo na vifaa vya kutolea chanjo vinapatikana katika mikoa yetu yote. Hili ni jambo zuri sana katika nchi yetu. Naomba Serikali yetu iendeleze suali hili.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kueneza elimu ya faida ya chanjo hizi katika jamii hasa wananchi wa vijijini.

Mheshimiwa Spika, tatu ni upungufu wa wafanyakazi katika vitu vyetu vya afya. Napenda kuipongeza Serikali yetu kwa jitihada kubwa inayochukua kwa kueneza huduma za afya nchini kwa kujenga vituo vya afya maeneo yote nchini. Hudumu ya afya ni miongoni mwa huduma muhimu sana kwa binadamu. Vituo vingi vimejengwa lakini bado inaonekana kuna upungufu wa wafanyakzi katika maeneo kadhaa nchini.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni ujenzi wa vituo hivi ni vema ukaenda sambamba na kuongeza wafanyakazi ili kuboresha huduma hii. Wafanyakazi wa sehemu zote (idara) pamoja na madaktari ni vyema wakawa wa kutosha kabisa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwako kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Pili napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa namna alivyoitayarisha hotuba yake kwa ufasaha na umakini mkubwa sana na kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa utulivu na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo: -

Kwanza ni uvuvi; napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Mama Samia kwa namna inavyochukua jitihada kubwa za kuendeleza uvuvi nchini. Uvuvi ni sekta muhimu sana inayowaletea maendeleo wavuvi wetu. Uvuvi pia ni muhimu sana katika kuongeza ajira za wananchi wetu. Lakini pamoja na juhudi zote hizo za Serikali bado kunahitajika hatua kadhaa ili kuimarisha uvuvi nchini. Bado wavuvi wetu wanafanya kazi hii kwa mazoea. Vifaa wanavyotumia ni vilevile vya zamani, hivyo naiomba Serikali kuwapatia wavuvi vifaa vya kisasa ili kuwa na uhakika na kazi yao. Aidha Serikali yetu iwapatie elimu ya kisasa ili kuwa na ubora wa kazi yao.

Mheshimiwa Spika, pili ni kuhusu kilimo; napenda kuchukua fursa hii kwa kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyojitahidi kuchukua hatua za makusudi ili kuendeleza kilimo nchini. Naiomba Serikali iendelee na juhudi hizi hasa za kuendeleza kilimo nchini kwa kuendelea kuwapatia pembejeo za kilimo ili wakulima wetu wapate kulima kwa wakati na kupata mazao mengi zaidi.

Mheshimiwa Spika, tatu ni kuhusu Muungano wa Tanzania; napenda kumponeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyochukua juhudi za makusudi za kuimarisha Muungano wetu. Hivi sasa wananchi wa sehemu mbili za Jamhuri ya Muungano wanashirikiana katika nyanja nyingi za maendeleo. Aidha, miradi na misaada inayopatikana sasa inaenda katika sehemu zote mbili za nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoongoza nchi yetu kwa umakini mkubwa sana na kuiweka nchi yetu katika hali ya usalama amani na utulivu.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza mheshimiwa waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimae kuiwakilisha hotuba hii katika bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa sana Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kuhusu barabara; napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyochukua jitihada kubwa za kuweka kipaumbele juu ya ujenzi wa barabara zetu. Barabara ni miongoni mwa vichochezi vya maendeleo katika nchi. Barabara zinapokuwa katika hali nzuri itaweza kurahisisha usafirishaji wa mazao ya wananchi wetu wakulima.

Ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba kwanza TARURA ioengezewe fedha ili iweze kutekeleza malengo yake.

Pili, Serikali itilie mkazo barabara zifike vijijini ili kuwawezesha wakulima kusafirisha mazao yao kupeleka sehemu husika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu afya; napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyochukua jitihada kubwa za kujenga zahanati katika maeneo yetu yote katika nchi yetu. Hili ni jambo zuri sana katika nchi. Hivi sasa karibu kila mkoa kuna zahanati za kisasa kabisa ambazo zinaleta matumaini kiafya.

Ushauri wangu katika jambo hili ni kwanza Serikali ihakikishe inaendeleza kupeleka vifaa tiba vya kisasa katika zahanati na hospitali hizo.

Pili bado masafa kati ya zahanati moja na nyingine ni makubwa sana kiasi ambacho bado inawapa shida wananchi kufuata huduma za afya hasa vijijini. Hivyo ni vyema Serikali ikaliangalia suala hili ili kuwawezesha wananchi hasa wa vijijini kufuata huduma hii ya afya katika masafa mafupi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Pili nachukua fursa hii ya kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoongoza nchi yetu kwa umakini mkubwa sana. Nchi imetulia na maendeleo yanaonekana. Namuombea kila la kheri katika uongozi wake huu.

Mheshimiwa Spika, napennda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na wasaidizi wake wote kwa namna walivyotayarisha hotuba hii kwa ubora wa hali ya juu na hatimaye kuiwasilisha katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, nianze na mikopo ya wanafunzi; napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyojitahidi kuwasaidia wanafunzi katika kuwawezesha kuendelea na masomo yao ya juu. Hili ni suala zuri sana hasa ukizingatia kuwa watoto wengi hali zao za kiuchumi ni ndogo. Ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba Serikali izidi kuboresha mfuko huu wa mikopo ili wanafunzi wengi zaidi waweze kunufaika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu vyuo vya VETA nchini; vyuo vya VETA ni vyuo muhimu sana katika kuwawezesha wanafunzi wetu kujijengea uwezo wa kuweza kujitegemea baada ya kumaliza mafunzo. Tatizo la ajira ni kubwa sana sio tu nchini mwetu bali ulimwengu mzima. Vyuo hivi vya VETA vinaweza kuwa ni suluhisho kubwa kwa tatizo la ajira nchini.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuongeza bajeti ya kuviwezesha vyuo hivi kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, Elimu ya Watu Wazima ni jambo zuri sana. Jambo hili lilikuwepo katika miaka ya nyuma lakini hivi sasa inaonekana sasa hivi Serikali yetu imelegeza kidogo kuliendeleza suala hili.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kurejesha elimu ya watu wazima nchini kwa manufaa ya wananchi wetu ambao kwa namna moja au nyingine walikosa fursa ya kuweza kusoma.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa mwaka wa fedha wa 2023/2024, hii ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika nchi yetu na kwa uchumi wa nchi yetu.

Pili, napenda kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoongoza nchi yetu kwa umakini mkubwa sana na kuiweka nchi yetu katika hali ya usalama, amani na utulivu.

Tatu, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa namna walivyotayarisha hotuba hii kwa ubora wa hali ya juu na hatimaye kuiwakilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; kwanza ni kuhusu huduma za ndege.

Mheshimiwa Spika, napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyojitahidi kutaka kurahisisha usafiri wa ndege katika nchi yetu. Huu ni ujasiri mkubwa uliochukuliwa na Serikali yetu ya kuimarisha usafiri wa ndege nchini. Lakini bado bei za ndege za ndani (domestic flights) ni kubwa sana kwa wananchi wetu. Wananchi wanashindwa kumudu bei hizo na kushindwa kufaidi matunda ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuangalia uwezekano wa kupunguza bei za ndege za ndani kwa manufaa ya wananchi wa nchi hii.

Pili ni kuhusu huduma za bandari, napenda kuipongeza Serikali yetu kwa namna inavyoonesha nia ya kutaka kuboresha bandari zetu kwa nia ya kutaka kuongeza uchumi wa nchi hii kupitia bandari. Bandari katika nchi zote duniani inakuwa ni moja kati ya vyanzo vya mapato.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kwenda na azma yake ya kutafuta wawekazaji ambao wataweza kuendesha bandari zetu hasa ile ya Dar es Salaam ambayo iko kiuchumi zaidi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Hii ni Wizara muhimu katika nchi yenye dhamana ya utulivu, amani na usalama.

Pili, napenda kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoongoza nchi yetu kwa umakini mkubwa sana na namuombea kila la kheri katika uongozi wake huu.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na watendaji wake wote kwa namna walivyotayarisha hotuba hii kwa ubora wa hali ya juu na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, mimi katika kuchangia hotuba hii napenda kuchukua nafasi ya kuipongeza Wizara hii kwa kutekeleza kazi zake kwa utararibu mzuri. Wizara inaendelea kuimarisha amani na utulivu katika nchi yetu. Wananchi tunaishi kwa usalama, wananchi wanafanya mambo yao ya kujiletea maendeleo bila ya wasiwasi wala bughudha yoyote.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ni kiungo kikubwa kati ya nchi yetu na nchi jirani. Kazi hii kwa mtazamo wangu wanaifanya vizuri sana, wanaimarisha mipaka ya nchi yetu na nchi jirani. Nawaomba waendelee na kufanya kazi zao kwa mujibu wa utaratibu na sheria za nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mimi leo mchango wangu ni kuipongeza tu Wizara hii kwa utendaji wake mzuri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwako kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, aidha nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; kwanza ni upatikanaji wa pembejeo kwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, kilimo ni uti wa mgongo kuelekea uchumi wa wakulima wetu. Serikali yetu inaendelea kutilia mkazo wananchi kujishughulisha na kilimo. Lakini kilimo chenye tija ni lazima kiandaliwe kwa kuwapatia wakulima wetu pembejeo za kilimo kwa wakati. Mpaka sasa kuna baadhi ya maeneo katika nchi yetu huwa wanasumbuka, aidha kutopata pembejeo kwa wakati au kukosa kabisa kwa baadhi ya miongo.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali katika jambo hili la pembejeo ni kuhakikisha wakulima wetu wanapata pembejeo hizi kwa wakati na kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, pili kuwawezesha wakulima wadogo wadogo; wakulima wetu wengi katika nchi yetu ni wanyonge sana. Uwezo wao wa kujiendesha kiuchumi ni mdogo sana. Wakulima wetu wanashindwa hata kuanza kilimo kwa sababu ya unyonge. Hivyo basi ni lazima Serikali yetu iwaunge mkono katika kilimo chao. Wengi huwa wanakimbilia kwenye mikopo ambayo baadae huwa wanashindwa hata kurejesha mikopo hiyo kutokana na masharti magumu. Riba kwenye mikopo ni miongoni mwa vihatarishi vikubwa kwa wakulima wetu.

Ushauri wangu katika suala hili la riba kwa mikopo ya wakulima ni Serikali kudhibiti kabisa viwango vya riba kwenye mabenki yetu ili kuondoa kabisa vihatarishi vinavyopelekea kufilisiwa kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, tatu ni kuhusu kilimo cha umwagiliaji; mabadiko ya hali ya hewa ulimwenguni yanaathiri mwenendo wa kilimo kwa kutegemea mvua. Nchi nyingi pamoja na Tanzania hivi sasa zinapata mazao hafifu kwa kutegemea mvua. Wengi wanaelekea kwenye matumizi ya kilimo cha umwagiliaji.

Ushauri wangu kwenye jambo hili ni Serikali iendeleze mikakati ya mpango wa kilimo cha umwagiliaji kwa kueneza scheme za kilimo kwenye maeneo yote nchini. Pia Serikali iendeleze zoezi la kuwa elimisha wakulima wetu faida za kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nikushukuru kwa kunipatia nafasi jioni hii ili kutoa mchango wangu katika Wizara hii muhimu katika nchi yetu. Pili, niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu waliompongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna anavyoiongoza nchi yetu kwa umakini na kwa ufasaha zaidi. Mimi pamoja na wapigakura wangu wa Jimbo la Tumbatu, tunamwombea dua Mwenyezi Mungu amjalie afanye kazi zake kwa wepesi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wetu pamoja na Naibu wake kwa namna walivyotayarisha hotuba yao na baadaye kuiwasilisha kwa umakini kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu leo naenda katika michango ifuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, viongozi wetu wa Wizara hii ni miongoni mwa viongozi wasikivu sana, wanasikiliza maoni ya Wabunge tunapokwenda na kutuelekeza. Kinachotakiwa katika hili ni sisi Wabunge kuwa wasitahimilivu tu lakini ukiwa unakwenda unaomba, unakwenda unaomba, unajibiwa vizuri, basi ustahimili tu unaloliomba utalipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 2016 nimekuwa nikisimama hapa kuiomba Wizara hii kujengewa Kituo cha Polisi katika Jimbo langu la Tumbatu. Kwa muda wote wa miaka mitano nimekuwa nikionana na viongozi hawa, majibu yao yalikuwa ni mamoja, nayo ni kuniambia kwamba Mheshimiwa subiri itafika siku Insha Allah na wewe tutakujengea Kituo chako cha Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeweza kustahimili, na nimestahimili nikijua kwamba mahitaji ya nchi hii katika kujenga vituo hivi ni makubwa, siyo kwangu mie tu, lakini katika nchi nzima mahitaji ya kujenga vituo hivi ni makubwa sana. Sasa unapokwenda kuomba kitu kwa mwenzako lakini asikukatalie anakwambia subiri, basi ni vyema ukasubiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima naishukuru Serikali hii kwa kupitia Wizara hii kwamba ombi langu hili limekubaliwa na Kituo cha Polisi katika Jimbo langu la Tumbatu ujenzi umeshaanza. Kwa hiyo nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali yangu inayoongozwa na Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa namna ombi langu hili lilivyokubaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo naomba mambo mawili katika hili, masafa kutoka Mkokotoni mpaka Tumbatu, jiografia yake ni lazima u-cross bahari, sasa basi maaskari wetu pale watakuwa wanakwenda Tumbatu kwa kutumia vidau au viboti vya wananchi. Naiomba Serikali na ni vyema itafutie boti maalum kwa ajili ya maaskari wetu ambao wanakwenda kule Tumbatu, kuwe na boti maalum kwa ajili ya maaskari ambao wanakwenda katika Kituo chetu cha Tumbatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, katika kutatua hili ni vyema pamoja na kituo cha polisi ambacho kitajengwa kule pia tunaomba maaskari wetu kule wajengewe makazi ili waweze kufanya kazi kule kule. Sisi wananchi wa Tumbatu kwa kushirikiana na Ofisi ndogo ya utawala kule Tumbatu tumeshatenga eneo maalum kwa ajili ya kuwapa Serikali wajenge makazi hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la pili ambalo linafanana kabisa na hili ni kuhusu Kituo changu cha Mkokotoni. Mwaka 2018 nilisimama hapa kutoa masikitiko yangu makubwa kwa namna ya kituo kile kilivyokuwa, lakini nashukuru Serikali imechukua juhudi kituo kile sasa hivi kipo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kutoa mfano, niliwahi kusema ule ukweli ulivyo kwamba, kipindi kile maaskari wetu walikuwa wanafanya kazi, inaponesha mvua wana-shift, kutoka ofisini kwao wanafanya kazi katika chumba cha mahabusu lakini alhamdulillah hali ni nzuri, wanafanya kazi vizuri na jengo liko vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililokuwepo pale ni moja ambalo ni kubwa, kuhusu makazi ya maaskari pale Mkokotoni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hija, malizia, muda wako umeisha.

MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. JUMA OTHMANI HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwako kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknnolojia ya Habari kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa. Hii ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; nikianza na usikivu hafifu katika baadhi ya maeneo nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa pongezi zangu za dhati kwa Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi zinazochukuliwa kwenye tasniya hii ya habari, hivi sasa ulimwengu uko kiganjani. Wananchi wote wanahitaji kupata habari ya kila kinachotokea nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado mpaka leo kuna maeneo katika nchi yetu hawapati habari. Bado usikivu wa habari katika maeneo yao si wa kuridhisha. Ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kujitahidi kurekebisha hali hii ili wananchi wa maeneo husika wapate haki ya kujua matokeo yanayotokea katika nchi yao na ulimwenguni kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa redio jamii, naipongeza Serikali yetu kwa kutoa uhuru wa habari. Uhuru huu umewasukuma wananchi katika maeneo kadhaa kufungua redio za kijamii. Redio hizi zinasaidia sana katika maeneo hayo. Lakini bado redio hizi uwezo wake ni mdogo sana, haukidhi matakwa ya redio hizo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali ni kuiomba iweze kuweka mpango maalum wa kuzitambua na kuzisaidia redio hizi ili ziweze kukidhi malengo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya Makadirio na Mapato ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu. Wizara hii ni miongoni mwa Wizara kubwa katika nchi hii lakini hotuba hii ime-cover mambo yote ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; nikianza na Shirika la Ndege ATCL. Napenda kuipongza Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake inayochukua katika kuendeleza kuboresha shirika hili. Hili ni Shirika muhimu katika nchi katika dhana ya kuimarisha huduma nyingi pamoja na za biashara. Miongoni mwa madhumuni ya shirika hili ni huduma kwa wananchi. Lakini bado wananchi wa nchi hii wanashindwa kutumia fursa ya kutumia usafiri huu kutokana na ukubwa wa bei. Bei za ndege zetu katika nchi hii kwa usafiri wa ndani ni kubwa sana kiasi ambacho si rahisi kwa mwananchi wa kawaida kuweza kutumia usafiri huu.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali yetu sikivu ni kuangalia uwezekano wa kupunguza bei za ndege hizi hasa kwa usafiri wa ndani ili wananchi wengi waweze kutumia ndege zao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Chuo cha Usafiri wa Anga; napenda kuipongeza Wizara hii kwa kuweka Chuo cha Usafiri wa Anga. Miongoni mwa kazi za chuo hiki ni kuwafunza vijana wetu kuwa marubani. Hii ni dhana nzuri ya Serikali yetu. Hivi sasa wananchi wengi wanakimbilia nchi za nje kujifunza urubani. Hivyo kuwepo kwa chuo hiki nchini kitawapunguzia gharama zisizokuwa za lazima.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Serikali yetu ni kukiboresha chuo hiki kwa kukiwekea miundombinu bora inayofanana na hadhi ya chuo hiki kama vilivyo vyuo vya wenzetu nchi za nje.

Mheshimiwa Spika, kuhusu udhibiti wa usafiri wa barabara; usafiri wa barabara ni muhimu sana kwa huduma za wananchi. Kutokana na kupanuka kwa huduma wananchi wamekuwa wakisafiri kila wakati kwa kufuatilia huduma za kimaisha. Safari zao zimekuwa za mchana na usiku pia. Lakini kwa sasa Serikali imezuia usafiri wa mabasi usiku. Jambo hili limekuwa likiwasumbua sana wananchi katika kuunganisha safari zao za kutoka mkoa mmoja kwenda kwenda kuwahi muda.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali katika jambo hili ni kuiomba Serikali yetu tukufu kurejesha usafiri wa mabasi ya safari za usiku ili kuwarahisishia wananchi shuhuli zao za kimaisha.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kinipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kuhusu unyanyaswaji wa wavuvi katika baadhi ya bandari; napenda kuchangia hotuba kwa kutoa masikitiko yangu makubwa juu ya namna ya tabia mbovu ya baadhi ya Maafisa wa Uvuvi wanaojuilikana kama watu wa marine. Watu hawa wamekuwa wakiwapa shida kubwa wavuvi hasa wanaotoka upande mmoja wa Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, wavuvi wanaotoka Zanzibar wamekuwa na utaratibu wa asili kuja kuvua huku Bara. Wanapotoka Zanzibar huwa wanakuja na vielelezo vyote vinavyohalalisha kuwepo kwao. Vielelezo hivyo ni pamoja na leseni za uvuvi, barua kutoka maeneo wanayotoka kwenda maeneo wanayofikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachosikitisha ni kwamba wakifika katika maeneo husika huwa wanaambiwa kuwa vielelezo vile havitambuliki na kutakiwa kutafuta vingine kwa bei kubwa sana.

Aidha wanapoenda kuvua huwa wanawavizia na kuwasingizia kuwa wameharibu mazingira, hatua hii huwapelekea kuwanyang’anya leseni zao za uvuvu na kuwapiga faini kubwa sana ambayo kuna wakati huwa wanashindwa kulipa. Wanaposhindwa kulipa huwa wanawanyang’anya mashine zao za uvuvi mpaka watakapokamilisha malipo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya bandari hizo zinazowapa shida wavuvi ni pamoja na Mnyanjani, Mwarongo, Kigombe na Mwarongo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Wizara ni kufuatilia tatizo hili mapema kabla halijageuka kuwa ni kero za Muungano ambazo Serikali yetu inajitahidi sana kuziondoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Pili nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa. Wizara hii ni miongoni mwa Wizara muhimu sana katika nchi yetu inayoonesha sura ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; kwanza ni kuhusu mapato. Wizara hii ni Wizara kama Wizara nyingine, ina malengo na makusudio yake. Moja katika malengo yake ni kujiwekea target ya matumizi na mapato ya Wizara. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wizara ilijiwekea lengo la kukusanya shilingi 2,550,879,000. Lakini hadi kusomwa kwa hotuba hii ni asilimia 33 tu ya lengo ndio iliyokusanywa. Hii ni rekodi isiyoridhisha kwa Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, uchunguzi wangu unaonesha kuwa vyanzo vilivyotarajiwa kutumika haviko imara (not stable), hivyo basi kuna haja ya kuangalia vyanzo vingine zaidi ili kutimiza lengo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika suala hili la makusanyo ya mapato ni kama ifuatavyo; hivi sasa nchi yetu inasifika kwa zoezi zima la Royal Tour. Napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kuanzisha Royal Tour. Nchi nyingi zinapenda kuja kuona vivutio vyetu. Lakini watu wengi katika baadhi ya nchi hawavijui vilipo na hadhi yake. Ofisi zetu za ubalozi za nje zingetengeneza ramani ya nchi yetu huko kwenye ofisi za mabalozi zinazoonesha vivutio vyetu pamoja na hadhi ya vituo hivyo zikawaonesha watu wa nchi hizo kwa gharama ndogo pamoja na vipeperushi vinavyoonesha vivutio vyetu. Lengo ni kuuza ili kuongeza mapato, lakini pia kuwashawishi kuja nchini kuangalia vivutio vyetu. Hii itaongeza mapato kwa Wizara na kwa nchi kwa jumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa elimu kwa umma; hotuba ya Mheshimiwa Waziri imetaja namna ya kuelimisha umma juu ya yanayofanyika nchini mwetu. Hii ni habari nzuri sana kwa umma, lakini kasoro ya zoezi hili ni vyombo vinavyotumika sio sahihi kwa kuwafikia wananchi wa maeneo ya vijijini. Hotuba imetaja vyombo vinavyotumika ni magazine, television, radio na vipeperushi. Vyombo hivi si rahisi sana kuwafikia wananchi wa vijijini ambao ni sehenu kubwa ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika jambo hili kwa Wizara na Serikali kuweka kikosi kazi kwa kutumia usafiri wa magari kwenda vijijini kuwaelimisha wanavijiji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Chuo cha Diplomasia; naipongeza Serikali yetu kwa kuweka chuo hiki, kimekuwa ni miongoni mwa vyuo muhimu sana katika nchi yetu. Serikali inapaswa kuchukua juhudi za makusudi kuboresha chuo hiki kwa kukiwekea mazingira mazuri ya kimataifa. Bado kuna hali isiyoridhisha kwenye miundombinu za chuo hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mitaala ya chuo hiki pia ni vyema ikajielekeza kuwafundisha vijana wetu pamoja na mambo mengine namna ya kuweza kujitegemea wenyewe baada ya kumaliza mafunzo yao. Bado mpaka leo mitaala ya chuo hiki inawatengeneza wahitimu wetu kutegemea ajira za Serikali. Hivyo kuna haja ya kuwatengeneza watu wetu katika hali ya kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya ajira kwa upande wa Serikali nafasi haziwezi kukidhi kuajiri vijana wetu wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hotuba hii ya makadirio na mapato ya Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Pili, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kutayarisha na hatimaye kuiwasilisha hotuba hii katika Bunge lako tukufu kwa ufasaha na umakini mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti katika kuchangia hotuba hii napenda kuchangia katika maeneo yafuatayo; nikianza na usambazaji wa umeme vijijini. Napenda kuipongeza Serikali yetu kwa kuendelea na utararibu wa kusambaza umeme vijijini. Katika nchi yetu ya Tanzania sasa hivi kuna engezeko kubwa la mahitaji ya umeme. Hivyo ni jambo jema sana kuwapelekea nishati hii wananchi wetu. Umeme una matumizi mengi lakini mpaka sasa wananchi wa vijijini wanaelewa kuwa umeme unatumika kwa matumizi ya taa za majumbani mwao tu, hii sio sahihi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika jambo hili kwa Wizara ni kuweka utararibu maalum wa kwenda vijijini kwa lengo la kuwaelimisha matumizi sahihi ya umeme, kama vile kupikia ili kunusuru ukataji wa miti ambao hivi sasa unaendelea kwa kasi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mradi wa gesi asilia; Tanzania tunapaswa kumshukuru Mungu kwa kutujaalia kuwa na gesi asilia katika nchi yetu. Gesi ni nishati muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu. Nchi yetu ilipogundua nishati hii wananchi tulijawa na matumaini makubwa. Tulidhani kuwa usambazaji wa nishati hii tulitegemea kuwa itasambazwa kwa speed ile kama inavyosambazwa nishati ya umeme inavyosambaa, lakini mpaka leo usambazaji wa nishati hii hauridhishi hata kidogo. Bado wananchi wanaotumia nishati hii ni wachache mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika jambo hili kwa Wizara ni kuweka utaratibu maalum wa kuisambaza huduma hii kwa wananchi wa mijini na vijijini ili kukidhi matumaini ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu deni la TANESCO kwa TPDC; TANESCO kwa muda mrefu sasa wamekuwa wa kudaiwa fedha nyingi na TPDC. Deni hili ambalo ni zaidi ya bilioni mia tano ni deni ambalo linaudhi sana kuona kila mwaka linajitokeza kwenye vitabu vya bajeti na wakati mwingine kwenye vitabu vya wakaguzi. Masharika haya mawili yote yako chini ya Wizara moja hivyo ni jambo la aibu kidogo kuona kuwa mpaka sasa halijapatikana ufumbuzi wake.

Ushauri wangu katika jambo hili kwa Wizara ni kuwaelekeza Maafisa Mausuuli wa Mashirika haya mawili kukaa pamoja kutafuta namna ya kulisawazisha deni hili. Matumaini yangu ni kwamba suala hili litapatiwa ufumbuzi muafaka na halitajitokeza tena kwenye vitabu vya ripoti za wakaguzi na ripoti nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa ushirikiano kati ya TANESCO na ZECO; ZECO na TANESCO ni mashirika mawili katika nchi yetu ya Tanzania yanayoshughulika na usambazaji wa umeme. Mashirika haya ni vyema yakaimarisha ushirikiano wao katika nyanja zote. Hivi sasa inaonekana ushirika wao upo kwenye mambo ya kiufundi tu na sio kwenye ngazi za maamuzi. Hapo zamani ushirikano wao ulikuwa mpaka kwenye mambo ya maamuzi. Kwa mfano ulikuwepo ushirikishwaji wa member wa bodi ya mashirika hayo kuhudhuria kwenye vikao vya maamuzi ya mashirika hayo. Kulikuwa na utaratibu wa mjumbe mmoja wa kila upande kuhudhuria kwenye vikao vya maamuzi ya mashirika haya. Ushauri wangu kwa Wizara kuchukua juhudi za makusudi kuurejesha utaratibu huu kwa maslahi ya pande zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwakilisha.