Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dunstan Luka Kitandula (44 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DUSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nichangie kwenye Mpango uliowasilishwa na Serikali. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye kwa rehema zake amenipa kibali niwe miongoni mwenu kuwatumikia Watanzania kupitia Bunge hili Tukufu. Vile vile, nitumie fursa hii kuwashukuru sana ndugu zangu wa Mkinga kwa kunipa heshima kwa mara ya pili, kuwa Mbunge wao niweze kuwawakilisha katika Bunge letu ninawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaahidi kuwatumikia kwa uwezo wangu wote kwa maarifa ya hali ya juu, na niimani yangu kwamba, kile tunachokikusudia tutakipata. Nitumie fursa hii vilevile kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo ameanza kushika hatamu za kuliongoza Taifa letu. Watanzania wana imani kubwa na uongozi wake, nimpe maneno ya kumu- encourage kwamba, tupo pamoja naye katika kuwatumikia Watanzania na Watanzania wanaamini kwamba, kasi ya mabadiliko waliokuja nayo itakuwa ni kasi ya ukweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie maneno, niazime maneno ya Rais wa 33 wa Marekani aliyekuwa akiitwa Harry Truman aliandika katika memo yake, Years of Trial and Hope katika ile volume ya pili anasema, „‟Being a President is like riding a tiger, a man has to keep on riding or be swallowed.”
Anaendelea kusema: “A President either is constantly on top of events or if he hesitate events will soon be on top of him.” Mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumwambia Mheshimiwa Rais Watanzania wana imani naye, aendelee na mwendo huo aliouanza nao bila ku-hesitate, tunaiona Tanzania yenye mabadiliko na mafanikio makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sasa nichangie mpango huu ulioko mbele yetu. Nimejaribu kuusoma mpango huu, lakini vilevile nikapata fursa ya kusoma Household Survey Report, lakini vile vile nikasoma report ile Human Development Report nikajaribu ku-combine maudhui tunayoyapata kutokana na taarifa zile. Maudhui ya taarifa zile yanatuambia kwamba tuna namba nzuri sana za mafanikio ya ukuaji wa uchumi. Namba zile zinatofautiana, ukisoma household survey na ile report nyingine zinatofautiana takwimu kidogo lakini bottom line ninachosema ni kwamba, hatujafanya vizuri sana katika maendeleo ya binadamu, maendeleo ya watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi ni viongozi lazima tuwe wakweli kwamba, tuna changamoto kubwa mbele yetu ya ku-translate ukuaji wa uchumi ili uweze kuleta maendeleo ya watu. Ndiyo maana hapa naipongeza Serikali kwa kutuletea Mpango huu wa Pili ambao una vionjo vinavyoonyesha kwamba, tunakwenda sasa kwenye kuunganisha ukuaji wa uchumi lakini vilevile ku-translate ukuaji huo kwenye maendeleo ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia kujenga uchumi wa viwanda ambavyo vitazalisha ajira, viwanda ambavyo vitapelekea kupunguza umasikini, tunaelekea huko. Lakini lazima tujiambie kama viongozi, tuwe wakweli tujiambie kwamba mMango huu tuliouleta ambao tunaenda kuufanyia marekebisho ili baadaye uje upitishwe ndani ya Bunge hili, utekelezaji wa Mpango huo tutakaokuwa tumeuleta, ukiwa chini ya asilimia 70 tutakuwa tumeshindwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima tuwe na mikakati madhubuti ya kuhakikisha hatushindwi. Takwimu zinatuambiaje, takwimu zinatuambia tulilenga kuwa na maeneo ya kilimo cha umwagiliaji hekta 1000 tumetoka kutoka kwenye hekta 345 tumekwenda kwenye hekta 461. Lakini hekta tulizonazo zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji katika nchi yetu tuna hekta milioni 29.1, tulichofanikiwa ni asilimia 0.39.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuje na mikakati ya kuhakikisha tunakwenda mbele. Nimeona hapo ujenzi wa viwanda, ujenzi wa bandari ya uvuvi ni jambo zuri, lakini ili tufanikiwe lazima tuunganishe jambo hili la ujenzi wa bandari ya uvuvi tuliunganishe na jambo la ufugaji wa samaki maana dunia ndiyo inapokwenda huko. Haiwezekani leo hii nusu ya samaki wanaoliwa duniani wanatokana na ufugaji wa samaki halafu sisi tusione umuhimu wa kufuga samaki, lazima tubadilike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari ile itakapojengwa lazima tujenge miundombinu ya ufugaji wa samaki, twende kisasa lazima tuwe na aquaculture industrial zone. Tuunganishe pale, bandari ya uvuvi, viwanda vya kuchakata samaki, viwanda vya kuchakata barafu na kadhalika na kadhalika na ufugaji wa samaki uwe pale pale. Katika maeneo yaliyotajwa katika kujenga bandari. Nilisema kipindi kilichopita iliainishwa bandari ya Dar es Salaam wote tunajua. Bandari ya Dar es Salaam hapafai kuna msongamano mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, Moa kule Mkinga namshukuru Rais maana kila alipokuwa akisimama kutoa hotuba yake anasema ukanda wote wa bahari kutoka Moa kule Tanga mpaka Mtwara hakuna kiwanda cha samaki. Njooni pale Moa wekeni bandari ya uvuvi maana katika maeneo yaliyotajwa matatu Moa ipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu lilitajwa Bagamoyo lakini Kamati iliyopita ilitushauri hapa ndani. Ikasema hivi tunaondoaje Chuo cha Mbegani, twende tukajenge bandari ya uvuvi, ni imani yangu Serikali imesikia njooni Moa tuweke mambo vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa viwanda lazima uzingatie vile vile kuweka mkazo kwenye kujenga.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Muda wako umekwisha.
MHE. DUSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuisimamia Wizara hii, Wizara ambayo kwa muda imekuwa ikikabiliwa na changamoto nyingi sana kiutendaji na kimfumo. Hongera sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utakubaliana na mimi kuwa rasilimali ardhi ina umuhimu wa kipekee kwa uhai na maendeloe ya binadamu. Aidha, kwa uchumi wa Taifa letu ambalo wanancni walio wengi wanategemea sana kilimo, sekta muhimu katika kukidhi mahitaji yao ya kila siku. Ni kutokana na ukweli huu rasilimali ardhi inabeba sifa ya kuwa haki ya kila Mtanzania na kwamba kumnyima Mtanzania yeyote haki ya kumiliki na kuitumia ni uvunjaji wa haki za binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wimbi la kuwepo kwa migogoro ya mipaka na uvamizi wa ardhi katika maeneo ya vijiji limekuwa tatizo kubwa katika nchi yetu. Tatizo hili ni kikwazo kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla. Migogoro hii imeendelea kusababisha upotevu wa mali, vifo na kuendeleza uhasama kati ya jamii na jamii na hivyo kuwafanya wananchi kubaki maskini na kuishi maisha duni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, uwepo wa mashamba makubwa yasiyoendelezwa ni chanzo kingine kikubwa cha migogoro ya ardhi nchini. Kwa muda mrefu, mfumo wetu wa kufuta miliki ya ardhi isiyotumika ipasavyo kwa mujibu wa makusudio ya umiliki wa ardhi husika umetumika kutoa mwanya wa watu wachache kuhodhi ardhi bila kuitumia na kuwaacha wananchi wengi kutaabika kwa kukosa ardhi. Naipongeza sana Serikali kwa jitihada kubwa zinazofanyika sasa kuhakikisha mashamba yaliyotelekezwa yanafutiwa hati za umiliki na hatimaye kugawanywa kwa wananchi. Hongera sana Mheshimiwa Waziri kwa kusimamia vyema jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mkinga ni miongoni mwa Wilaya zinazokabiliwa na migogoro ya umiliki wa ardhi na uwepo wa mashamba yaliyotelekezwa kwa muda mrefu. Kwa nyakati tofauti ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga na mimi binafsi tumewasilisha Wizara ya Ardhi, mapendekezo ya Wilaya kuhusu utatuzi wa migogoro hiyo. Wakati mapendekezo ya ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga yaliwasilishwa Wizara ya Ardhi mapema mwaka 2007, wakati huo Mkinga ikiwa bado ni sehemu ya Wilaya ya Muheza; Ofisi yangu iliwasilisha tena maombi hayo kupitia barua yenye Kumb.MB/MKN/Ardh01/2011 ya tarehe 17 Novemba, 2011.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi chote cha uhai wa Bunge la Kumi mara kwa mara nilikuwa nakumbushia jambo hili kwa michango kwenye hotuba za bajeti za Wizara, na barua. Pamoja na jitihadi hizi bado changamoto hizi hazijapatiwa ufumbuzi. Mheshimwia Waziri nilifarijika sana kupata barua yako iliyotaka Wabunge kuorodhesha migogoro ya ardhi katika Majimbo yetu. Hivyo basi, natumia fursa hii kuikumbushia Wizara juu ya maombi haya ambayo kimsingi yamechukua muda mrefu kupatiwa ufumbuzi:-
(i) Shamba la Kilulu - shamba hili ndipo sehemu ambayo Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga yamejengwa. Shamba hili kwa mara ya kwanza lilimilikishwa kwa Ndugu Van Brandis na Bibi Mary Van Brandis hadi 31/10/1959 ambapo umiliki ulihama kwenda kwa Ndugu Akberali Walli Jiwa. Mmliki huyu hakuendeleza shamba hili lenye ukubwa wa ekari 5,699.9 hadi umiliki wake ukafutwa mwaka 1972. Baada ya kufuta umiliki, Serikali ililipa fidia na shamba likawa chini ya Serikali.
Baadaye Wilaya ya Muheza ilipokea maombi ya kumilikishwa shamba hilo toka Kampuni ya M/S Arusha Farms Ltd. (CHAVDA). Taratibu zote zilifanyika na alimilikishwa ekari 2,699.9 na ekari 3000 walipewa wananchi wa vijiji jirani vya Vuo, Mwachala na Purungu Kasera waliokuwa na shida ya ardhi. M/S Arusha Farms Ltd walipewa barua ya toleo (leter of right of occupancy) ya tarehe 10/05/1991 ambayo ilisajiliwa na Msajili wa Hati tarehe 13/05/1990 kwa Land Office Number 125127.
Mmiliki huyu aliomba mkopo kutoka CRDB kwa kuweka rehani barua ya toleo. Aidha, alishindwa kurejesha mkopo huo na CRDB waliuza shamba kwa M/s Mbegu Technologies Ltd. tarehe 27/03/2004 ambao walilipa mkopo huo, lakini pia hakuweza kuliendeleza shamba hilo. Ndugu Akberali Jiwa licha ya kunyang‟anywa shamba hilo na kulipwa fidia aliwasilisha ombi lake la kurejeshewa umiliki wa shamba hilo. Ombi lake liliwasilishwa katika kikao cha Kamati ya kugawa ardhi tarehe 10/10/1996 na iliazimiwa liwasilishwe katika Kamati ya Ushauri ya Ardhi Mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati hiyo chini ya Uenyekiti wa Mkuu wa Mkoa iliridhia Ndugu Akberali Jiwa apewe shamba hili kwa vile M/s Arusha Farm Ltd. wameshindwa kuliendeleza. Halmashauri ya Muheza ilitoa barua ya toleo kwa miliki ya miaka 99 kuanzia tarehe 1/10/1998 kwa Akberali Jiwa kwa jina la Kampuni ya Kilulu (2000) Ltd. Baada ya tatizo hilo la double allocation kujitokeza, Halmashauri ya Muheza iliandika barua yenye Kumb Na. MUDF/3844/63 ya tarehe 2/4/2007 kwenda kwa Kamishna wa Ardhi kwa ajili ya kuomba kufuta miliki hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taarifa ya Halmashauri hadi leo Halmashauri haijapata majibu yoyote licha ya ufuatiliaji uliofanywa wa mara kwa mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali halisi kwa sasa ni kwamba eneo hili lina michoro ya mipango miji minne, mitatu iliandaliwa na Katibu Tawala wa Mkoa kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Muheza kabla ya kuanzishwa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga na mchoro mwingine umeandaliwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga. Aidha, eneo hili limepimwa jumla ya viwanja 400 kwa matumizi mbalimbali ikiwemo, taasisi, majengo ya Serikali, majengo ya umma, viwanja vya michezo, maeneno ya kuabudia, makazi biashara na maeneo ya wazi. Kwa mara nyingine tena naiomba Serikali ifute milki ya Kilulu Plantation kwa manufaa ya umma.
(ii) Moa Estate - shamba hili lina ukubwa wa ekari 15,739.60 na linamilikiwa na Mkomazi Plantations Ltd. ya S.L.P 2520 Dar es Salaam ambayo baadaye ilibadilisha jina kuwa Mao Plangation and Aquaculture ya S.L.P 364 Dar es Salaam, kwa hati Na. 2468, 9780 na 9781. Halmashauri ya Wilaya ilituma notisi ya kuwafutia hati miliki yao kwa kutelekeza shamba na kulipia kodi. Baada ya hapo Halmashauri ya Wilaya iliwasilisha barua ya mapendekezo kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. MKG/LD/F/2/54 ya tarehe 28/07/2009. Taratibu za ufutaji hati miliki ziliendelea Wizarani lakini Halmashauri ilipokea barua ya mmiliki ikieleza kuwa jina la umiliki lilibadilika na kuwa Moa Plantation and Aquaculture wa S.L.P 364 Dar es Salaam na kwamba wanataka kuendeleza shamba hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ilikwishawasilisha Wizarani barua ya mapendekezo ya kufuta hatimiliki, ililazimika kumwandikia Kamishna wa Ardhi barua yenye Kumb. Na. MKG/LD/F/2/56 ya tarehe 09/06/2001 kumweleza kupokea barua hiyo na kwamba shamba hilo lina vijiji vinne ambavyo vimeanzishwa na kusajiliwa Moa, Ndumbani, Mayomboni na Mahandakini. Aidha, vijiji hivyo tayari vina huduma za jamii kama shule, zahanati, barabara na kadhalika. Katika maeneo hayo hivyo aendelee na taratibu za ufutaji hatimiliki au kama atasitisha ufutaji basi wamiliki wakubali kumega maeneo yanayokaliwa na vijiji na kuendelezwa na wananchi. Kamishna wa Ardhi kwa barua Na. LD/70503/76 ya tarehe 23/11/2011 alisitisha ufutaji huo kwa masharti kwamba walipe kodi ya ardhi kuanzia mwaka 1996 hadi 2011/12 na kumega maeneo ambayo yenye vijiji tajwa. Hata hivyo, hawakutimiza masharti hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia hali hiyo, Halmashauri iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. HW/MKG/LD/F/2/62 ya tarehe 27/07/2012 ili aendelee na taratibu za ufutaji. Kamishna wa Ardhi kupitia barua yenye Kumb. Na. LD/70503/76 ya tarehe 23/11/2011 alisitisha ufutaji huo kwa masharti kwamba walipe kodi ya ardhi kuanzia mwaka 1996 hadi 2011/2012 na kumega maeneo ambayo yenye vijiji tajwa. Hata hivyo hawakutimiza masharti hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia hali hiyo, Halmashauri iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. HW/MKG/LD/F/2/62 ya tarehe 27/07/2012 ili aendelee na taratibu za ufutaji. Kamishna wa Ardhi kupitia barua yake Kumb. Na. LD/70503 ya tarehe 15/01/2013 iliitaka Halmashauri kuwasilisha vielelezo jambo ambalo Halmashauri ilifanya. Aidha, barua ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi yenye Kumb. Na. LD/NZ/12931/18/DW ya tarehe 15/04/2013 kwenda kwa Kaimu Kamishna wa Ardhi nayo inahusika akishauri ufutaji wa hati hizo uendelee. Kwa sasa Halmashauri ya Wilaya inasubiri uamuzi wa Kamishna wa Ardhi.
(iii) Mwele Seed Farm - shamba hili lina ukubwa wa hekta 954, mmiliki ni Wizara ya Kilimo. Wakati ambapo shamba hili lilikusudiwa kuwa shamba la kuzalisha mbegu, hali halisi ni kwamba kwa kipindi cha takribani miaka 15 sasa shamba hili limeshindwa kutumika kama ilivyokusudiwa na sehemu kubwa kubaki kuwa pori. Wananchi wa vijiji vinavyozunguka shamba hili Mbabakofi, Maramba A, Maramba B na Lugongo ndiyo wamekuwa nguvu kazi ya kulifanyia usafi shamba hili pale wanaporuhusiwa kufungua mashamba mapya na kulima mazao ya muda mfupi kila msimu mpya wa kilimo unapowadia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 21/09/2007, Halmashauri ya Wilaya iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na. MUD/ASF/VOL.VI/35 ikipendekeza kumegwa kwa shamba hili na kugawiwa kwa wananchi wa vijiji jirani kutokana na uendelezaji wake kuwa mdogo sana na kodi kutolipwa. Hata hivyo, maombi haya hayakuwahi kupatiwa majibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili linapakana na kijiji cha Mbambakofi chenye takribani kaya 500 zenye jumla ya wananchi wapatao 3,173. Mbambakofi ni kijiji pekee katika Wilaya ya Mkinga ambacho kimekosa hata eneo la kujenga huduma muhimu za kijamii kama shule ya msingi na zahanati. Aidha, shamba hili linapakana na Mji Mdogo wa Maramba ambao unakua kwa kasi kubwa, ukiwa na takribani watu 30,000 na kuzungukwa na mashamba ya Maramba JKT hekta 2445, Lugongo Estate hekta 6040, Kauzeni Estate hekta 189.66, Mtapwa Estate hekta 476.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya kutelekezwa kwa shamba hili imezidi kuwa mbaya sana sasa kuliko ilivyokuwa mwaka 2007, wakati Halmashauri ya Wilaya ilipoomba mara ya kwanza kumegwa kwa shamba hili. Kwa sasa hali imekuwa mbaya kiasi kwamba hata majengo mengi yaliyokuwepo yameanguka na machache yaliyosalia yamekuwa magofu, mashine na mitambo yoyote ya kilimo iliyokuwepo shambani hapo imeharibika na michache iliyosalia imehamishiwa Morogoro. Kwa sasa shamba limebaki na wafanyakazi wasiozidi watano kutoka waliokuwepo miaka ya 1990.
(iv) Shamba la Maramba JKT - ukubwa wake ni hekta 2,445 na linamilikiwa na Jeshi. Eneo kubwa halitumiki na halilipiwi kodi. Barua iliyoandikwa kuhusu Mwele Seed Farm iliunganishwa pia mapendekezo ya kumega shamba hili ili wananchi wa Mji Mdogo wa Maramba waweze kupata eneo la kujenga makazi yao.
(v) Shamba la Segoma - msitu wa Segoma wenye ekari 2,311 upo ndani ya shamba la Sigi Segoma lenye ukubwa wa ekari 2829. Shamba hili lilimilikishwa kwa Shirika la Uchumi la Wilaya ya Muheza (SHUWIMU) kwa hati Na. 7675 ya tarehe 01/04/1990 ya miaka 33. Kutokana na kukosa mtaji na kuzorota kwa SHUWIMU, hati hii ilibadilishwa umiliki kuwa Muheza District Council kuanzia tarehe 16/02/2007.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1992 SHUWIMU kwa kukosa mtaji na utaalam iliingia ubia na M/s Sigi Agricultural Co. Ltd., na SHUWIMU ilipovunjwa shamba lilimilikiwa na Muheza District Council ambayo ilifuta ubia uliokuwepo na kuingia ubia na SWIFTCOM ya Tanga. Hii ilisababisha M/s Sigi Agricultural Co. Ltd. kufungua kesi namba 18 ya 1996 kupiga kupinga kufutwa kwa ubia wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2011 hukumu ya kesi hii ilitolewa na Halmashauri ya Muheza kupewa ushindi. Mwaka 2007 Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ilianzishwa kwa kumegwa toka Muheza. Katika zoezi la kugawana mali, shamba hili liligawiwa kwa Halmashauri ya Mkinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hukumu kutolewa, Halmashauri kwa ufadhili wa Tanzania Forest Conservation Group (TFCG) ilifanya ukaguzi wa uhalisia wa wakati huo na kutoa taarifa katika kikao kilichofanyika tarehe 08/10/2012 kikihusisha viongozi wa kijiji cha Songea, Kata, wataalam wa Halmashauri, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania - Kanda ya Kaskazini na wataalamu wa Mkoa. Aidha, kikao kilitoka na mapendekezo kwa kuwa na kijiji cha Segoma kina tatizo kubwa la uhaba wa ardhi, ekari 518 za shamba zigawanywe kwa wananchi kwa shughuli za kilimo na makazi na ekari 2,311 zitengwe kuwa eneo la hifadhi ya msitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 15/12/2012 kikao cha Baraza la Madiwani kama wamiliki halali wa rasilimali hii kiliridhia mapendekezo haya na kuagiza ekari 518 zigawiwe kwa wananchi wa kijiji cha Segoma kwa shughuli za makazi na kilimo na ekari 231 zimilikishwe kwa kijiji cha Segoma kuwa msitu wa kijiji. Ili kutekeleza agizo la Baraza la Madiwani, Menejimenti iliwasiliana na Meneja wa Kanda wa Wakala wa Huduma za Misitu kwa makabidhiano. Hata hivyo Meneja wa Kanda wa Wakala wa Huduma za Misitu aliomba kuonana na uongozi wa Halmashauri kwa majadiliano juu ya kijiji kumilikishwa misitu. Taarifa ya ombi hilo ilipofikishwa kwenye kikao cha Baraza cha tarehe 16-17/07/2014, Baraza liliagiza kuwa wataalam wa Ardhi na Misitu wa Wilaya watekeleze Azimio la Baraza la tarehe 05/12/2012.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Menejimenti kutekeleza agizo hilo, tarehe 28/11/2014 kwa mshangao mkubwa Halmashauri ilipokea barua kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ikiamuru kusitishwa kugawa ardhi kwa wananchi kwa ajili ya kilimo na makazi na hali kadhalika kukabidhi msitu kuwa wa kijiji cha Segoma. Jambo hili limeleta taharuki kubwa kwa wananchi kiasi kwamba walikuja Dodoma wakati wa vikao vya bajeti kuwasilisha malalamiko yao. Aidha, wakati wa kuhitimisha mjadala wa bajeti nililazimika kuomba ufafanuzi kuhusiana na jambo hili na Naibu Waziri alikiri kuwa wananchi wa Segoma wanayo haki ya kupatiwa ardhi tajwa na kwamba atatembelea Mkinga ili kulipatia ufumbuzi jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tukiendelea kusubiri utekelezwaji wa ahadi ya Naibu Waziri kutembelea Mkinga kuja kuupatia ufumbuzi mgogoro huu, Halmashauri ilipokea barua toka kwa Katibu Tawala wa Mkoa yenye Kumb. Na. BF 174/314/02/35 ya tarehe 02/12/2015 ikiagiza eneo la ekari 518 likabidhiwe rasmi kwa kijiji na eneo la msitu lenye ukubwa wa ekari 2311 kuwa chini ya usimamizi wa Wakala wa Huduma za Misitu hadi hapo uamuzi mwingine utakapotolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi haya ya kuinyang‟anya Halmashauri ya Mkinga rasilimali yake siyo tu kwa nia ya uonevu mkubwa bali pia yanakinzana na Sheria ya Misitu ya mwaka 2002 ambayo inabainisha wazi kuwa jamii inaweza kulinda, kuhifadhi, kusimamia na kutumia kiuendelevu misitu katika ardhi ya kijiji ili kukidhi mahitaji yao ya kimaendeleo ya muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikimbukwe kuwa zaidi ya hekta milioni mbili za misitu hapa nchini zinasimamiwa na Serikali za vijiji zaidi ya 1000. Hivyo kijiji cha Segoma kukabidhiwa kusimamia msitu wao wa asili haitakuwa mara ya kwanza. Tungependa kuona busara iliyotumika mwaka 2015 kuruhusu Kata ya Enguserosambu katika Wilaya ya Ngorogoro kusimamia msitu wa Longido II ikitumika hata kwa msitu wa Segoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kutokana na ukweli kuwa wananchi hawa ndiyo wameutunza msitu wa Segoma na kuwajibika kuhakikisha msitu unabaki salama pasipo kuombwa wala kukukabidhiwa na Serikali. Inasikitisha kuona leo wananchi hawa wakiporwa rasilimali hii kwa mabavu, kejeli na udhalilishwaji kuwa wao ni wavamizi. Halmashauri ya Mkinga na wanakijiji wa Segoma wanataka kunufaika na umiliki wa rasilimali yao kupitia mapato yatokananyo na mavuno ya msitu huu ili kuboresha huduma za kijamii na kuleta maendeleo ya kijiji.
(vi) Kwamtili Estate - shamba hili lina ukubwa wa hekta 1,150 na lina milikiwa na Kwamtili Estate Ltd. yenye certificate of Incorporation No. 2649 iliyosajiliwa tarehe 09/01/1961 ikiwa na wanahisa wafuatao:

S/N JINA LA MWENYE HISA ANAPOISHI MAELEKEZO

1 Dennis Martin Fielder 4 Market Square Tenbury,Wells Worcestershine – UK Amerudi Uingereza
2 National Agriculture &
Food Corporation (NAFCO) Box 903 DSM Shirika limefutwa
3 Handrik Tjails Scheen C1/30 Algami nes Bank, Amsterdam, Netherland Amefariki
4 Louis Van Wagenburg Layscian Ag Vaghel, Holland Amefariki
5 Schoonmarkers Bart
Venderburg De Conqabsen, 163 Schlkher, Holland Amefariki
6 Tracey Elan Allison The Willos Terrigton, Herefordenshire, UK Amefariki
7 Juvent Magoggo 42 Block S. Mikanjuni Box 5855 Tanga Anaishi Tanga
8 W.J. Tame Ltd Box 118 Tanga Amefariki
9 Jacobus Cornelius Logtanburg Vaghel, Holland Amefariki
Josephus Moris


Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili lililopo katika eneo la Kwamtili, Kata ya Bosha, Wilaya ya Mkinga lilitumika kwa kilimo cha kibiashara cha zao Kakau. Hata hivyo kwa muda wa miaka takribani 26 saa shughuli za kilimo cha zao la Kakau zimesimama baada ya aliyokuwa Menejiment ya Kampuni chini ya Ndugu Dennis Fielder kutelekeza shamba. Aidha, baada ya shamba kutelekezwa, mmoja wa wanahisa Ndugu Juvent Magoggo amekuwa akifanya shughuli ndogo ndogo ikiwemo kuvuna miti ndani ya shamba hili kwa lengo la kupata fedha za kufanyia uzalishaji mdogo mdogo; na hali kadhalika kuruhusu wananchi wanaozunguka shamba hilo kulima mazao ambayo siyo ya kudumu. Hata hivyo, kwa sasa ndugu Magoggo ameshindwa kuendelea kufanya shughuli hizo baada ya kunyimwa vibali vya kuvuna miti na kusafirisha magogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kuwepo kwa ombwe la umiliki wa shamba hili yamezuka makundi ya watu yanayodai kuwa na haki ya kumiliki shamba hili na hivyo kuwakodisha wananchi wanaozunguka shamba hili maeneo ya kulima kwa kuwalipisha sehemu ya mavuno yatokanayo na matumizi ya ardhi hiyo. Aidha, kumekuwa na wimbi la kujitokeza raia wa kigeni kwa kutumia kivuli cha aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa shamba na kulitekeleza Ndugu Dennis Fielder kufanya uharibifu wa mali za kampuni, ikiwemo upasuaji wa mbao na kuanzisha michakato ya kujimilikisha ardhi hii. Katika hili, wananchi wanainyooshea kidole ofisi ya Wakala wa Hifadhi ya Misitu - Wilaya ya Mkinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kwamtili na Kata ya Bosha kwa ujumla wamebaki katika umaskini wa kutupa baada ya shughuli za kilimo cha Kakau katika shamba la Kwamtili ambacho kilitoa ajira kwao kusitishwa. Nusura kwa wananchi hawa ni kupatiwa maeneo katika shamba hili ili kwa kutumia utaratibu wa wakulima wadogo waweze kufanya shughuli ya kilimo na hivyo kujikimu kimaisha. Naiomba Serikali ifanye uamuzi wa kufuta hati ya shamba la Kwamtili na kisha kuligawa kwa wananchi kwa ajili ya kilimo, na sehemu nyingine kutengwa kuwa hifadhi ya msitu wa kijiji.
(vii) Mjesani Sisal Estate - shamba hili lenye hati Na. 48108 na ukubwa wa ekari 22,725 lilitelekezwa kwa muda mrefu na hali iliyosababisha ardhi kumegwa na kuanzishwa vijiji vinne ndani ya shamba ambalo ni Kwangena, Mchangani, Bomba Mavengero na Mnyenzani. Aidha, Kampuni ya Mohamed Ltd. ya S.L.P 20600 Dar es Salaam imejitokeza na kuanza kuendeleza baadhi ya maeneo ya shamba hili. Hali hii imeleta changamoto kubwa hasa ikizingatiwa kuwa tayari vijiji vilivyomo ndani ya shamba hili vimepatiwa usajili na TAMISEMI. Mfano kijiji cha Kwangena chenye ukubwa wa hekta 300 kimepewa hati ya kuandikishwa kwa kijiji Na. TA/KIJ/603 ya tarehe 03/01/1997, aidha, upimaji wa vijiji ulifanyika na ramani za upimaji kupata vibali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia mkanganyiko huu wa umiliki wa ardhi katika vijiji tajwa, wananchi wa vijiji husika wamekuwa na kilio cha muda mrefu kuiomba Serikali iingilie kati ili kuondoa utata wa umilikishwaji wa maeneo ya vijiji vyao. Mfano, Mkutano Mkuu wa Kijiji cha Kwangena ulikaa na kuomba kupewa ardhi kwa mujibu wa ramani ya kijiji aliyoidhinishwa. Baraza la Madiwani iliyobariki ombi hilo na Halmashauri kupitia barua yenye Kumb. Na. HW/MKG/D.35/138/5 ya tarehe 17/072012 iliwasilisha ombi hilo kwa Kamishina wa Ardhi, mnamo mwaka 2015 Wizara ilituma wataalam wake kuja kufufua mipaka ya shamba na kwa mshangao mkubwa wananchi wa Kwangena wakamegewa ekari 216 tu. Aidha, ndani ya kipindi kifupi sana ramani ya upimaji ikisajiliwa kwa namba 82741, na wakaandaliwa hati nyingine yenye LONO. 560486 na hati ikasajiliwa tarehe 26/11/2015. Tunaomba Serikali iangalie upya suala hili ili wananchi wa vijiji vya Kwangena, Mchangani, Bamba, Mavengero na Mnyenzani waweze kupatiwa ardhi itakayowawezesha kuishi kwa fahari katika nchi yao huku wakiweza kukidhi mahitaji yao ya kimaisha.
(viii) Mgogoro wa Kijiji cha Mkota na Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi - wananchi wa Kitongoji cha Kimuuni katika Kijiji cha Mkota Kata ya Mwakijembe wamekuwa wakiishi katika eneo hilo tangu kabla ya uhuru. Kitongoji hiki kina takribani kaya 170 na wakazi wapato 530. Wananchi hawa wa muda wote wamekuwa msaada mkubwa kwa ulinzi na rasilimali za nchi yetu hasa ikizingatiwa kuwa eneo hili linapakana na nchi jirani ya Kenya. Wananchi hawa wanalalamika kuwa eneo lao limechukuliwa na hifadhi ya Taifa ya Mkomazi na Pori Tengefu la Umba na kwamba sasa wanatakiwa kuondoka kwenye eneo hilo licha ya kufanya uwekezaji mkubwa kwa kutumia nguvu zao kuchimba mabwawa makubwa ya kunywesha mifugo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro huu nimeufikisha Serikalini na nimelizungumzia jambo hili mara nyingi sana katika Bunge la Kumi, lakini hadi sasa halijapatiwa ufumbuzi. Mheshimiwa Anna Tibaijuka wakati akiwa Waziri wa Ardhi akiongozana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, alifanya ziara katika Wilaya ya Mkinga na kufanya mkutano wa hadhara katika kijiji hiki. Katika mkutano ule, Mheshimiwa Waziri aliwaahidi wananchi kuushughulikia mgogoro huu. Aidha, aliyekuwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Mahmood Mgimwa akiandamana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa naye alifanya ziara katika eneo la mgogoro (Kimuni) na kufanya mkutano wa hadhara ambapo alipokea ombi la wananchi kwa eneo hili kupewa hadhi ya kuwa Wildlife Management Area (WMA) na kuahidi Wizara kuanzisha mchakato wa kulitanga eneo hili kuwa WMA. Tunaamini kuwa suluhisho la mgogoro huu ni Serikali kukamilisha mchakato huu ili wananchi waweze kuishi kwa amani.
(ix) Manza Bay Sisal Estate - ni mkusanyiko wa mashamba manne yenye ukubwa wa jumla ya ekari 2,217.6 shamba na. 273 hati na. 7047 LONO. 124814 ekari 461, shamba Na. 196 hati Na. 14275 LONO. 12621 ekari 498.6, shamba Na. 272 hati Na. 3576 LONO. 642 ekari 507 na shamba hati Na. 14322 ekari 764. Mmiliki wa mashamba haya ni Mbegu Technologies Inc. Ltd. wa S.L.P 173 Moshi. Mashamba haya yote yameingia katika eneo la Mji wa Kasea ambao ndio Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga. Kwa muktadha huu naiomba Serikali ione umuhimu wa kufuta hati hizi ili eneo hili liweze kufanyiwa matumizi ya kuendeleza mji wa Kasera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na migogoro hiyo hapo juu, ipo migogoro mingine iliyoibuka kutokana na zoezi la upimaji wa vijiji mwaka 2007 lililohusisha wataalam wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na wataalam wa Halmashauri ya Mkinga. Kiini cha migogoro hii ni zoezi kufanyika bila kuhakikisha ushiriki wa viongozi wa pande zote za vijiji husika katika kubainisha mipaka, jambao ambalo limepelekea vijiji ambavyo havikuwa na uwakilishi kugomea kutambua mipaka iliyowekwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti orodha ya vijiji vyenye migogoro hii ni kama ifuatavyo:-
(a) Kijiji cha Daluni Kibaoni na Kijiji cha Ng‟ombeni; (b) Kijiji cha Daluni Kibaoni, Kijiji cha Mgambo Shashui na Kijiji cha Movovo;
(c) Kijiji cha Mnyenzani na Kijiji cha Jirihini;
(d) Kijiji cha Magodi na Kijiji cha Mwanyumba;
(e) Kijiji cha Dima na Kijiji cha Mazola Kilifi;
(f) Kijiji cha Doda na Kijiji cha Magaoni;
(g) Kijiji cha Monga Vyeru na Kijiji cha Kichalikani;
(h) Kijiji cha Mwakijembe na Kijiji cha Mkota;
(i) Kijiji cha Msimbazi na Kijiji cha Dima; na
(j) Kijiji cha Bosha na Kijiji cha Churwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kuwa sasa changamoto za muda mrefu za uwepo wa migogoro ya mipaka ya vijiji umiliki wa ardhi na uwepo wa mashamba yaliyotelekezwa kwa muda mrefu katika Wilaya ya Mkinga yatapatiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hoja ya bajeti hii atueleze nini kauli ya Serikali kuhusiana na changamoto hizi, na tunamuomba atoe kipaumbele cha kuitembelea Mkinga ili kuja kutatua migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuunga mkono hoja ya Wizara ya Maliasili na Utalii kuhusiana na Makadirio na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imejaaliwa kwa wingi wa vivutio vya utalii ulimwenguni, vivutio ambavyo kwa bahati mbaya hatujavitumia ipasavyo kutuwezesha kuwa na fursa kubwa ya kiushindani katika sekta ya utalii. Wakati ambapo taarifa mbalimbali zimekuwa zikiisifu Tanzania kwa uwepo wa vivutio hivi, ikizidiwa tu na nchi kama Brazil, kama Taifa tumekuwa na changamoto kubwa ya udhaifu katika mikakati yetu ya kuvitangaza vivutio tulivyonavyo. Ni ukweli uliowazi kuwa endapo vivutio hivi vingetangazwa na kutumika vizuri, mchango wa sekta ya utalii katika uchumi wa nchi yetu ungekuwa mkubwa zaidi kuliko ilivyo sasa. Ni lazima tuwe na mkakati mahsusi wa kutangaza vivutio tulivyonavyo na mkakati huo lazima utengewe fedha za kutosha zitakazowezesha kutumika kwa mashirika makubwa ya utangazaji duniani kutangaza vivutio tulivyonavyo na fursa za uwekezaji katika sekta hii zilizopo hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kusuasua kwa ukuaji wa Dodoma kunasemakana kwa kiasi fulani kunachangiwa na mji huu kukosa bahari na maziwa ambayo husababisha utalii. Kwa kiasi cha maji tunachoona kinapotea kwa wingi kila msimu wa mvua unapofika hapa Dodoma, nani anasema hatuwezi kuanzisha state of the art artificial lake kama walivyofanya Malaysia kwenye mji wao mpya? Nani anasema hatuwezi kuwa na zoo ya kisasa kwenye viunga vya Dodoma? Nani anasema hatuwezi kuanzisha utalii wa zao la zabibiu hasa ikizingatiwa kwama Dodoma inasifika kuwa sehemu pekee ulimwenguni ambapo uzalishaji wa zabibu unafanyika kwa misimu miwili katika mwaka? Au nani anasema hatuwezi kunufaika kwa kuanzisha utalii wa tamaduni za Wagogo na nyumba zao za tembe? Hii ni mifano michache tu ya fursa za uwekezaji na vyanzo vipya vya sekta yetu ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Waziri inaonesha kuwa idadi ya watalii waliotembelea nchini imeshuka kidogo ikilinganishwa na mwaka uliopita. Hali hii inashabihiana na taarifa zilizomo kwenye ripoti ya World Tourism Organisation inayoonesha kumekuwa na kushuka kwa idadi ya watalii waliotembelea Bara la Afrika wakati hali kwa Mabara mengine kama Amerika, Asia na Ulaya ni tofauti kwani Mabara hayo yameshuhudia ongezeko la idadi ya watalii katika maeneo yao. Funzo tunalopata hapa ni kuwa lazima tuwekeze katika ubora wa vivutio tulivyonavyo na huduma tunazotoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kama Taifa lazima tuhakikishe kiwango tulichofikia cha idadi ya watalii wanaotembelea nchi kinalindwa kisishuke na wakati huo huo kuja na mikakati mipya ya kuongeza idadi ya watalii wanaokuja nchini. Ripoti ya World Tourism Oraganisation inaonyesha kuwa kwa mwaka 2015 safari za kiutalii zinazofanywa na Wachina zimeongezeka kufikia safari milioni 120, ukuaji ambao umeizidi Marekani na mataifa mengine ya Ulaya. Ukuaji huu wa safari za kiutalii zinazofanywa na Wachina unamaanisha kuwa kwa kila safari kumi za kiutalii zilizofanyika ulimwenguni, safari moja ilihusisha raia wa China. Ukuaji huu wa safari za kiutalii zinazofanywa na Wachina ni fursa muhimu sana kwetu katika kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Tanzania. Nashauri Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje kuchukua hatua za haraka kuweka mikakati ya pamoja itakayotuwezesha kulikamata soko hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu sasa wadau muhimu katika sekta ya utalii nchini wamelalamikia mfumo mbovu wa utoaji leseni kwa kampuni za wazawa na masharti magumu ya uanzishaji kampuni za kusafirisha watalii ikilinganishwa na zile za kigeni. Lazima tuondokane na urasimu usio wa lazima ili kuwezesha Watanzania wengi zaidi kuwekeza katika sekta ya utalii. Ieleweke kuwa urasimu katika utoaji wa leseni na masharti magumu kuhusiana na viwango vikubwa vya mitaji si tu unazuia uanzishwaji wa makampuni ya utalii bali pia unadumaza ukuaji wa huduma zinazotolewa na sekta nyingine za uchumi kama uzalishaji wa chakula, usafiri, hoteli, wapagazi na watu wengine wanaotegemewa kutoa huduma kwa watalii wawe wa ndani au nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa mbalimbali zinaifananisha Tanzania na nchi kama Australia kwa kuwa na mfumo mbovu wa utoaji leseni, mfumo ambao hautoi mwanya kwa ukuaji wa sekta ya utalii. Aidha, utafiti wa IFC unabainisha kuwepo kwa urasimu mkubwa katika udhibiti wa leseni za utalii na upatikanaji wa mtaji hali ambayo inasababisha ugumu kwa wanaotaka kuingia katika sekta ya utalii hususani wazawa. Kwa kuwa kama Taifa tunakubaliana kimsingi kuwa sekta binafsi ni injini ya kukuza uchumi wa nchi yetu, lazima tuhakikishe tunatoa fursa pana kwa wazawa hususan wale wenye mitaji midogo ili nao waweze kushiriki katika kuwekeza. Lazima tuwaondolee vikwazo vinavyowanyima haki ya kujituma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya utalii ina nafasi kubwa ya kuendelea kuwa mhimili muhimu wa kukuza uchumi wa nchi yetu. Hata hivyo, kufanikiwa kwa hili kunategemea sana kufanyika mambo kadhaa muhimu kama vile kuongeza jitihada katika kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo katika kila kona ya nchi yetu, kuboresha miundombinu muhimu, kuboresha taaluma ya utalii ili kuwa na watu wenye elimu na taaluma stahiki na hali kadhalika kuondoa urasimu katika maeneo mbalimbali yahusuyo sekta ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na jitihada hizo ni muhimu vilevile kuelekeza nguvu zetu katika kukuza utalii wa ndani. Kuna umuhimu sasa wa kuja na mkakati mahsusi wa kukuza utalii wa ndani. Lazima mkakati huo uweke bayana jinsi ambavyo tutaweza kutumia makundi yenye ushawishi hapa nchini kama Wabunge, wasanii na hata timu zetu za mpira wa miguu kwenye ligi kuu kushiriki kwenye kuanzisha utamaduni wa utalii wa ndani hapa nchini. Jambo hili ni muhimu kutokana na ukweli kuwa utalii wa ndani ni uti wa mgongo katika ukuzaji wa sekta ya utalii katika nchi yoyote ile. Ni kutokana na ukweli huu hatuna budi kama Taifa kuelekeza nguvu zetu katika kujenga utamaduni wa wananchi kutembelea vivutio vilivyopo nchini na kuwa na mikakati ya kuhamasisha wanafunzi na vijana kwa ujumla kutembelea mbuga zetu na maeneo ya vivutio katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuwe na mkakati kabambe wa kuongeza jitihada zetu katika kutangaza vivutio tulivyonavyo ikibidi suala la utalii wa ndani liwe sehemu ya mitaala yetu ya kufundishia katika shule zetu, tufanye hivyo. Aidha, wakati umefika wa kuanzisha wiki maalum ya uzinduzi wa utalii wa ndani kila msimu wa utalii unapoanza nchini. Hii ni pamoja na kuhakikisha kuwa jitihada zetu za kukuza na kutangaza utalii zinalenga makundi mbalimali ya watu nchini kwa kuzingatia umri, jinsia na uwezo wa kipato ili kumuwezesha kila Mtanzania kushiriki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ninalotaka kulizungumzia ni eneo la migogoro ya ardhi iliyopo katika Wilaya yangu ya Mkinga, migogoro ambayo kimsingi inaigusa Wizara hii. Migogoro hii imechukua muda mrefu kupatiwa ufumbuzi licha ya jitihada kubwa zilizofanyika kuishauri Serikali kuipatia ufumbuzi. Jambo hili limekuwa chanzo cha manung‟uniko makubwa na wananchi kupoteza imani kwa Serikali yao. Migogoro hii ni kama ifuatavyo hapa chini:-
(i) Mgogoro wa wananchi wa Segoma na TFS. Msitu wa Segoma wenye ekari 2,311 upo ndani ya shamba la Sigi Segoma lenye ukubwa wa ekari 2,829. Shamba hili lilimilikishwa kwa Shirika la Uchumi la Wilaya ya Muheza (SHUWIMU) kwa hati Na. 7675 ya tarehe 01 Aprili, 1990 ya miaka 33. Kutokana na kukosa mtaji na kuzorota kwa SHUWIMU, hati hii ilibadilishwa umiliki kuwa Muheza District Council kuanzia tarehe 16 Februari, 2007.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1992 SHUWIMU kwa kukosa mtaji na utaalam iliingia ubia na M/S Sigi Agricultural Co. Ltd. na SHUWIMU ilipovunjwa shamba lilimilikiwa na Muheza District Council ambayo ilifuta ubia uliokuwepo na kuingia ubia na SWIFTCOM ya Tanga. Hii ilisababisha M/S Sigi Agricultural Co. Ltd. kufungua kesi Na. 18 ya 1996 kupinga kufutwa kwa ubia wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2011 hukumu ya kesi hii ilitolewa na Halmashauri ya Muheza kupewa ushindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2007 Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ilianzishwa kwa kumegwa toka Muheza. Katika zoezi la kugawana mali, shamba hili lilikuwa sehemu ya mali zilizogawiwa kwa Halmashauri ya Mkinga. Hivyo basi, kufuatia kutolewa kwa hukumu iliyohusisha shamba hili, Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga kwa ufadhili wa Tanzania Forest Conservation Group (TFCG) ilifanya ukaguzi wa uhalisia wa shamba kwa wakati huo na kutoa taarifa katika kikao kilichofanyika tarehe 08 Oktoba, 2012 kikihusisha viongozi wa kijiji cha Segoma, Kata, wataalam wa Halmashauri, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania – Kanda ya Kaskazini na wataalam wa Mkoa. Kikao kilitoka na mapendekezo kuwa kwa kuwa kijiji cha Segoma kina tatizo kubwa la uhaba wa ardhi, ekari 518 za shamba zigawanywe kwa wananchi kwa shughuli za kilimo na makazi na ekari 2,311 zitengwe kuwa eneo la hifadhi ya msitu. Mnamo tarehe 05 Disemba, 2012 kikao cha Baraza la Madiwani kama wamiliki halali wa rasilimali hii kiliridhia mapendekezo haya na kuagiza ekari 518 zigawiwe kwa wananchi wa kijiji cha Segoma kwa shughuli za makazi na kilimo na ekari 2,311 zimilikishwe kwa kijiji cha Segoma kuwa msitu wa kijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo Meneja wa Kanda wa Wakala wa Huduma za Misitu aliomba kuonana na uongozi wa Halmashauri kwa majadiliano juu ya kijiji kumilikishwa msitu. Taarifa ya ombi hilo ilipofikishwa kwenye kikao cha Baraza cha tarehe 16 – 17 Julai, 2014, Baraza liliagiza kuwa wataalam wa ardhi na misitu wa Wilaya watekeleze Azimio la Baraza la tarehe 05 Disemba, 2012 bila mabadiliko yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Menejimenti kutekeleza agizo hilo, tarehe 28 Novemba, 2014 kwa mshangao mkubwa Halmashauri ilipokea barua kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ikiamuru kusitishwa kugawa ardhi kwa wananchi kwa ajili ya kilimo na makazi na halikadhalika kukabidhi msitu kuwa wa kijiji cha Segoma. Jambo hili limeleta taharuki kubwa kwa wananchi kiasi kwamba walikuja Dodoma wakati wa vikao vya bajeti kuwasilisha malalamiko yao. Aidha, wakati wa kuhitimisha mjadala wa bajeti nililazimika kuomba ufafanuzi kuhusiana na jambo hili na Naibu Waziri alikiri kuwa wananchi wa Segoma wanayo haki ya kupatiwa ardhi tajwa na kwamba atatembelea Mkinga ili kulipatia ufumbuzi jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tukiendelea kusubiri utekelezwaji wa ahadi ya Naibu Waziri kutembelea Mkinga kuja kuupatia ufumbuzi mgogoro huu, Halmashauri ilipokea barua toka kwa Katibu Tawala wa Mkoa yenye Kumb. Na. BF 174/314/02/35 ya tarehe 02 Disemba, 2015 ikiagiza eneo la ekari 518 likabidhiwe rasmi kwa kijiji na eneo la msitu lenye ukubwa wa ekari 2,311 kuwa chini ya usimamizi wa Wakala wa Huduma za Misitu hadi hapo uamuzi mwingine utakapotolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi haya ya kuinyang‟anya Halmashauri ya Mkinga rasilimali yake siyo tu kuwa ni ya uonevu mkubwa bali pia yanakinzana na Sheria ya Misitu ya mwaka 2002 ambayo inabainisha wazi kuwa jamii inaweza kulinda, kuhifadhi, kusimamia na kutumia kiendelevu misitu katika ardhi ya kijiji ili kukidhi mahitaji yao ya kimaendeleo ya muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kuwa zaidi ya hekta milioni 21.7 sawa na asilimia 45.7 za misitu hapa nchini zinasimamiwa na Serikali za Vijiji zaidi ya 1,000. Aidha, hekta milioni 3.5 sawa na asilimia 7.3 za msitu nchini zinasimamiwa na watu binafsi au vikundi. Hivyo, Kijiji cha Segoma kukabidhiwa kusimamia msitu wao wa asili haitakuwa kioja wala mara ya kwanza kwa kijiji kumiliki msitu. Ni kwa msingi huu tungependa kuona busara iliyotumika kuruhusu vijiji zaidi ya 1,000 hapa nchini kusimamia misitu yao ikitumika hata kwa msitu wa Segoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kutokana na ukweli kuwa wananchi hawa ndiyo wameutunza msitu wa Segoma na kuwajibika kuhakikisha msitu unabaki salama pasipo kuombwa wala kukabidhiwa na Serikali. Inasikitisha kuona leo wananchi hawa wakiporwa rasilimali hii kwa mabavu, kejeli na udhalilishwaji kuwa wao ni wavamizi.
Halmashauri ya Mkinga na wanakijiji wa Segoma wanataka kunufaika na umiliki wa rasilimali yao kupitia mapato yatokanayo na mavuno ya msitu huu ili kuboresha huduma za kijamii na kuleta maendeleo ya kijiji.
(ii) Kwamtili Estate - shamba hili lina ukubwa wa hekta 1,150 na linamilikiwa na Kwamtili Estate Ltd.yenye Certificate of Incorporation Na. 2649 iliyosajiliwa tarehe 09 Januari, 1961 ikiwa na wanahisa wafuatao:

S/N JINA LA MWENYE HISA ANAPOISHI MAELEZO
1. Dennis Martin Fielder 4 Market Square Tenbury, Wells Worcestershire - UK Amerudi Uingereza
2. National Agriculture & Food Corporation (NAFCO) Box 903 DSM Shirika limefutwa
3. Handrik Tjails Scheen C1/30 Algamines Bank, Amsterdam, Netherland Amefariki
4. Louis Van Wagenburg Laycisan Ag Vaghel, Holland Amefariki
5. Schoonmarkers Bart Vanderburg De Congabsen, 163 Schlkher, Holland Amefariki
6. Tracey Elan Allison The Willos Terrigton, Herefordenshire, UK Amefariki
7. Juvent Magoggo 42 Block S. Mikanjuni Box 5855 Tanga Anaishi Tanga
8. W. J. Tame Ltd Box 118 Tanga Amefariki
9. Jacobus Cornelius Josephus Moris Logtanburg Vaghel, Holland Amefariki

Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili lililopo katika eneo la Kwamtili, Kata ya Bosha, Wilaya ya Mkinga lilitumika kwa kilimo cha kibiashara cha zao la kakau. Hata hivyo, kwa muda wa miaka takribani 26 sasa shughuli za kilimo cha zao la kakau zimesimama baada ya iliyokuwa Menejimenti ya Kampuni chini ya Ndugu Dennis Fielder kutelekeza shamba hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, baada ya shamba kutelekezwa, mmoja wa wanahisa Ndugu Juvent Magoggo amekuwa akifanya shughuli ndogo ndogo ikiwemo kuvuna miti ndani ya shamba hili kwa lengo la kupata fedha za kufanyia uzalishaji mdogo mdogo na hali kadhalika kuruhusu wananchi wanaozunguka shamba hilo kulima mazao ambayo si ya kudumu. Hata hivyo, kwa sasa Ndugu Magoggo ameshindwa kuendelea kufanya shughuli hizo baada ya kunyimwa vibali vya kuvuna miti na kusafirisha magogo.
Kutokana na kuwepo kwa ombi la umiliki wa shamba hili, yamezuka makundi ya watu yanayodai kuwa na haki ya kumiliki shamba hili na hivyo kuwakodisha wananchi wanaozunguka shamba hili maeneo ya kulima kwa kuwalipisha sehemu ya mavuno yatokanayo na matumizi ya ardhi hiyo. Aidha, kumekuwa na wimbi la kujitokeza raia wa kigeni kwa kutumia kivuli cha aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa shamba na kulitelekeza Ndugu Dennis Fielder kufanya uharibifu wa mali za kampuni, ikiwemo upasuaji wa mbao na kuanzisha michakato ya kujimilikisha ardhi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili, wananchi wanainyooshea kidole Ofisi ya Wakala wa Hifadhi ya Misitu Wilaya ya Mkinga kutaka kujiingiza katika kufanya udalali wa ardhi hii. Wananchi bado wana kumbukumbu nzuri ya jinsi watumishi hawa wa TFS Wilayani Mkinga walivyotumika kuwezesha mwekezaji wa Kiitaliano aliyejaribu kupatiwa ardhi ya Mkinga takribani hekta 25,000 kinyume na taratibu ili kulima jatropher.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Serikali haijaweza kulipatia ufumbuzi tatizo lingine ambalo kimsingi limeanzishwa na TFS kutaka kupora ardhi ya wananchi katika shamba la Segoma, TFS hiyo hiyo inataka kuzalisha mgogoro mwingine wa kupora ardhi nyingine katika Wilaya ya Mkinga. Hatupo tayari kuona hili likitokea hasa ikizingatiwa kuwa Kwamtili inakabiliwa na tatizo kubwa la ardhi. Tunaiomba Serikali kutumia busara kuacha jambo hili na kuirejesha ardhi hii kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kwamtili na Kata ya Bosha kwa ujumla wamebaki katika umaskini wa kutupwa baada ya shughuli za kilimo cha kakau katika shamba la Kwamtili ambacho ndicho kilitoa ajira kwao kusitishwa. Nusura pekee kwa wananchi hawa ni kupatiwa maeneo katika shamba hili ili kwa kutumia utaratibu wa wakulima wadogo waweze kufanya shughuli ya kilimo na hivyo kujikimu kimaisha. Naiomba Serikali ifanye uamuzi wa kufuta hati ya shamba la Kwamtili na kisha kuligawa kwa wananchi kwa ajili ya kilimo na sehemu nyingine kutengwa kuwa hifadhi ya msitu wa kijiji.
(iii) Mgogoro wa Kijiji cha Mkota na Hifadhi ya Taifa Mkomazi; wananchi wa Kitongoji cha Kimuuni katika Kijiji cha Mkota, Kata ya Mwakijembe wamekuwa wakiishi katika eneo hilo kabla ya uhuru. Kitongoji hiki kina takribani kaya 170 na wakazi wapato 530. Wananchi hawa kwa muda wote wamekuwa msaada mkubwa kwa ulinzi na rasilimali za nchi yetu hasa ikizingatiwa kuwa eneo hili linapakana na nchi jirani ya Kenya. Wananchi hawa wanalalamika kuwa eneo lao ambalo ni sehemu ya kijiji cha Mkota kwa mujibu wa ramani ya kijiji iliyosajiliwa, eneo lao limechukuliwa na Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi na pori tengefu la Umba na kwamba sasa wanatakiwa kuondoka kwenye eneo hilo licha ya kufanya uwekezaji mkubwa kwa kutumia nguvu zao kuchimba mabwawa makubwa ya kunywesha mifugo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro huu nimeufikisha Serikalini na nimelizungumzia jambo hili mara nyingi sana katika Bunge la Kumi lakini hadi sasa halijapatiwa ufumbuzi. Mheshimiwa Profesa Anna Tibaijuka wakati akiwa Waziri wa Ardhi akiongozana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa alifanya ziara katika Wilaya ya Mkinga na kufanya mkutano wa hadhara katika kijiji hiki. Katika mkutano ule, Mheshimiwa Waziri aliwaahidi wananchi kuushughulikia mgogoro huu. Aidha, aliyekuwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utaliii Mheshimiwa Mahmoud Mgimwa akiandamana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa naye alifanya ziara katika eneo la mgogoro (Kimuuni) na kufanya mkutano wa hadhara ambapo alipokea ombi la wananchi kwa eneo hili kupewa hadhi ya kuwa Wildlife Management Area (WMA) na kuahidi Wizara kuanzisha mchakato wa kulitangaza eneo ili kuwa WMA. Tunaamini kuwa suluhisho la mgogoro huu ni Serikali kukamilisha mchakato huu ili wananchi waweze kuishi kwa amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu kuwa sasa changamoto za muda mrefu za uwepo wa migogoro ya mipaka ya vijiji, umiliki wa ardhi na uwepo wa mashamba yaliyotelekezwa kwa muda mrefu katika Wilaya ya Mkinga yatapatiwa ufumbuzi. Namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hoja ya bajeti hii atueleze nini kauli ya Serikali kuhusiana na changamoto hizi na tunamuomba atoe kipaumbele cha kuitembelea Mkinga ili kuja kutatua migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja nikiamini kuwa Wizara itachukua hatua stahiki katika kutatua changamoto nilizoelezea na kuzielekeza taasisi zilizo chini yake kuacha kuwa chanzo cha migogoro na kuwanyima haki wananchi wetu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa jitihada kubwa walizofanya kuleta mabadiliko makubwa ya kiutendaji katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali ardhi ina umuhimu wa kipekee kwa uhai wa maendeleo ya binadamu, wanyama, mimea na viumbe vyote. Kwa uchumi wa Taifa letu ambalo wananchi walio wengi wanategemea sana kilimo kama sekta muhimu katika kukidhi mahitaji yao ya kila siku; rasilimali ardhi inakuwa na umuhimu wa kipekee, kiasi kwamba ni haki ya kila mwananchi kupata, kuimiliki, kuitumia na kuitunza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wimbi la kuwepo kwa migogoro ya mipaka na uvamizi wa ardhi katika maeneo ya vijiji limeendelea kuwa tatizo kubwa katika nchi yetu. Tatizo hili ni kikwazo kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla. Tumeendelea kushuhudia migogoro hii ikisababisha upotevu wa mali za wananchi, vifo na kuendeleza uhasama kati ya jamii na jamii na hivyo kuwafanya wananchi kubaki maskini na kuishi maisha duni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kasi ndogo ya upimaji ardhi imeendelea kuwa donda ndugu, wataalam wa ardhi kutowashirikisha wananchi wakati wa uwekaji wa mipaka; na kutowaelimisha wananchi juu ya mipaka iliyowekwa, kama Taifa hatuwezi kuiacha hali hii iendelee. Wizara ichukue hatua za makusudi kuhakikisha kuwa wataalam wa ardhi wanawashirikisha na kuwaelimisha wananchi wakati wa uwekaji wa mipaka. Wizara iongeze kasi ya upimaji wakati wa uwekaji wa mipaka. Wizara iongeze kasi ya upimaji ardhi ili kuzuia wajanja wachache kuvamia maeneo pasipo viongozi wa vijiji kujua na hatua kali zichukuliwe kwa viongozi wa vijiji wanaogawa ardhi kinyume na taratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya wakulima na wafugaji imeendelea kuwa chanzo cha machafuko na umwagaji damu nchini. Lazima kasi yetu ya kutenga maeneo maalum ya wafugaji na wakulima iandamane na utunzaji wa sheria kali utakaozuia uvamizi wa maeneo unaofanywa na pande hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, bado mashamba makubwa yasiyoendelezwa yameendelea kuwa chanzo kikubwa cha migogoro ya ardhi nchini. Bado mfumo wetu wa kufuta miliki ya ardhi isiyotumika ipasavyo kwa mujibu wa makusudio ya umiliki wa ardhi husika umeendelea kutoa mwanya wa watu wachache kuhodhi ardhi bila kuitumia na kuwaacha wananchi wengi wakitaabika kwa kukosa ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kufanya mapitio ya Sheria ya Umiliki Ardhi na kanuni zake ili tupunguze urasimu katika mfumo wetu ili mashamba yaliyotelekezwa yaweze kufutiwa hati za umiliki mara tu yanapothibitika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine nilete kilio cha muda mrefu cha wananchi wa Wilaya ya Mkinga, ambayo ni miongoni mwa wilaya zinazokabiliwa na migogoro ya umiliki wa ardhi na mashamba yaliyotelekezwa kwa muda mrefu. Licha ya jitihada kadhaa ambazo kwa nyakati tofauti Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga na mimi binafsi tumewasilisha Wizara ya Ardhi mapendekezo ya Wilaya kuhusu utatuzi wa migogoro hiyo; bado utatuzi wa migogoro hii umekwama kupata majawabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mapendekezo ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga yaliwasilishwa Wizara ya Ardhi tangu mapema mwaka 2007 wakati huo Mkinga ikiwa bado ni sehemu ya Wilaya ya Muheza; ofisi yangu iliwasilisha tena maombi hayo kupitia mchango wangu wa maandishi wakati wa Bunge la Bajeti mwaka jana na kufuatiwa na barua kwa Waziri wa Ardhi yenye Kumb. Na. MB/MKN/Ardh 01/2016 ya tarehe 30 Mei, 2016. Napenda kuikumbusha Wizara juu ya maombi haya ambayo kimsingi yamechukua muda mrefu kupatiwa ufumbuzi.

(i) Shamba la Kilulu; shamba hili ndipo palipojengwa Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga. Shamba hili kwa mara ya kwanza lilimilikishwa kwa Bwana Van Brandis na Bibi Mary Van Brandis hadi tarehe 31 Oktoba,1959 ambapo umiliki ulihamia kwenda ama Bwana Akberali Walli Jiwa. Mmiliki huyu hakuendeleza shamba hili lenye ukubwa wa ekari 5,699.9 hadi umiliki wake ukafutwa mwaka 1972. Baada ya kufuta umiliki, Serikali ililipa fidia na shamba likawa chini ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye Wilaya ya Muheza ilipokea maombi ya kumilikishwa shamba hilo toka Kampuni ya M/S Arusha Farms Limited (CHAVDA). Taratibu zote zilizofanyika na alimilikishwa ekari 2,699.9 na ekari 3,000 walipewa wananchi wa vijiji jirani vya Vuo, Mwachala na Parungu Kasera waliokuwa na shida ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, M/S Arusha Farms Limited walipewa barua ya toleo (Letter of Right of Occupancy) ya tarehe 10 Mei, 1991 ambayo ilisajiliwa na Msajili wa hati tarehe 10 Mei, 1991 ambayo ilisajiliwa na Msajili wa hati tarehe 13 Mei, 1990 kwa Land Office Number 125127.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmiliki huyu aliomba mkopo kutoka CRDB Bank kwa kuweka rehani barua ya toleo. Aidha, alishindwa kurejesha mkopo huo na CRDB waliuza shamba kwa M/S Mbegu Technologies Limited tarehe 27 Juni, 2004 ambao walilipa mkopo huo. Hata hivyo, pia hakuweza kuliendeleza shamba hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bwana Akberali Jiwa licha ya kunyang’anywa shamba hilo na kulipwa fidia aliwasilisha ombi lake la kurejeshewa umiliki wa shamba hilo. Ombi lake liliwasilishwa katika Kikao cha Kamati ya Kugawa Ardhi tarehe 10 Oktoba, 1996 na iliazimiwa liwasilishwe katika Kamati ya Ushauri wa Ardhi Mkoa. Kamati hiyo chini ya Uenyeviti wa Mkuu wa Mkoa iliridhia Bwana Akberali Jiwa apewe shamba hilo kwa vile M/S Arusha Farms Limited ameshindwa kuliendeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Muheza ilitoa barua ya toleo kwa miliki ya miaka 99 kuanzia tarehe 1 Oktoba, 1998 kwa Akberali Jiwa kwa jina la Kampuni ya Kilulu (2000) Limited. Baada ya tatizo hilo la double allocation kujitokeza, Halmashauri ya Muheza iliandika barua Kumb. Na. MUDF/3844/63 ya tarehe 2 Aprili, 2007 kwenda kwa Kamishna wa Ardhi kwa ajili ya kuomba kufuta miliki hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, licha ya ufuatiliaji uliofanywa wa mara kwa mara, kwa mujibu wa taarifa ya Halmashauri hadi leo Halmashauri haijapata hati yoyote inayoonesha kufutwa milki ya shamba tajwa. Kikao cha RCC kilichofanyika mwaka jana kiliridhia hati ya shamba tajwa ifutwe; hivyo kuagiza taratibu za kutoa notice zifanyike. Hata hivyo, tangu wakati huo kumekuwa na urasimu mkubwa wa utoaji notice tajwa. Naiomba Wizara ifuatilie jambo hili.

(ii) Shamba la Moa; shamba hili lina ukubwa wa ekari 15,739.60 na linamilikiwa na Mkomazi Plantations Limited wa S.L.P. 2520 Dar es Salaam kwa hati Na. 4268,9780 &9781. Halmashauri ya Wilaya ilituma notisi ya kuwafutia hati miliki yao kwa kutoendeleza na kutolipia kodi. Baada ya hapo Halmashauri ya Wilaya iliwasilisha barua ya Mapendekezo kwa Kamishna wa Ardhi yenye Kumb. Na MKG/LD/F/2/54 ya tarehe 28 Julai, 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taratibu za ufutaji hati miliki ziliendelea Wizarani, lakini Halmashauri ilipokea barua ya mmiliki akieleza kuwa jina la umiliki lilibadilika na kuwa Moa Plantation & Aquaculture wa S.L.P. 364 Dar es Salaam na kwamba wanataka kuendeleza shamba hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ilishawasilisha Wizarani barua ya mapendekezo ya kufuta hati miliki, ililazimika kumwandikia Kamishna wa Ardhi barua yenye Kumb. Na. MKG/LD/F/2/56 ya tarehe 9 Juni, 2011 kumweleza kupokea barua hiyo na kwamba shamba hilo lina vijiji vinne ambavyo vimeanzishwa na kusajiliwa (Moa, Ndumbani, Mayomboni na Mhandakini).

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, vijiji hivyo tayari vina huduma za jamii kama shule, zahanati, barabara na kadhalika katika maeneo hayo; hivyo aendelee na taratibu za ufutaji hati miliki au kama atasitisha ufutaji basi wamiliki wakubali kumega maeneo yanayokaliwa na vijiji na kuendelezwa na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati hali ikiwa hivyo, mwaka 2013 mmiliki wa shamba atengeneze PP na kuomba kubadilisha matumizi ya sehemu ya shamba ili kupima viwanja 450 vya makazi. Hata hivyo, viwanja hivyo havikuwahi kupimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatilia ucheleweshaji usioeleweka wa kufuta hati ya shamba hili, mnamo mwezi Oktoba, 2016 mmiliki wa shamba alitumia mwanya huo kutengeneza PP nyingine ya eneo lote la shamba ili kupima viwanja. Aidha, amekabidhi hati ya shamba tajwa ili ipelekwe kwa Afisa Ardhi Mteule-Moshi ili taratibu zinazokusudiwa ziweze kufanywa. Naiomba Wizara iingilie kati mchakato huu ili ardhi tajwa irejeshwe mikononi mwa Halmashauri ya Wilaya.

(iii) Mwele Seed Farm; shamba hili lina ikubwa wa hekta 954. Mmliki ni Wizara ya Kilimo. Wakati ambapo shamba hili lilikusudiwa kuwa shamba la kuzalisha mbegu, hali halisi ni kwamba kwa kipindi cha takribani miaka 15 sasa shamba hili limeshindwa kutumika kama ilivyokusudiwa na sehemu kubwa kubaki kuwa pori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa vijiji vinavyozunguka shamba hili Mbambakofi, Maramba A, Maramba B na Lugongo ndio wamekuwa nguvukazi ya kulifanyia usafi shamba hili pale wanaporuhusiwa kufungua mashamba mapya na kulima mazao ya muda mfupi kila msimu mpya wa kilimo unapowadia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 21 Septemba, 2007, Halmashauri ya Wilaya iliandika barua kwa Kamishna wa Ardhi Kumb. Na. MUD/ASF/VOL.VI/35 ikipendekeza kumegwa kwa shamba hili na kugawiwa kwa wananchi wa vijiji jirani kutokana na uendelezaji wake kuwa mdogo sana na kodi kutolipwa. Hata hivyo, maombi haya hayakuwahi kupatiwa majibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili lilipakana na Kijiji cha Mbambakofi chenye takriban kaya 500 zenye jumla ya wananchi wapatao 3173. Mbambakofi ni kijiji pekee katika Wilaya ya Mkinga ambacho kimekosa hata eneo la kujenga huduma muhimu za kijamii kama shule ya msingi na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, shamba hili limepakana na Mji Mdogo wa Maramba ambao unakua kwa kasi kubwa, ukiwa na takriban watu 30,000 na kuzungukwa na mashamba makubwa ya Maramba JKT, hekta 2,445; Lugongo Estate, hekta 6,040; Kauzeni Estate, hekta 189.66; na Mtapwa Estate, hekta 476.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya kutekelezwa kwa shamba hili imezidi kuwa mbaya sana sasa kuliko ilivyokuwa mwaka 2007, wakati Halmashauri ya Wilaya ilipoomba kwa mara ya kwanza kumegwa kwa shamba hili. Kwa sasa hali imekuwa mbaya kiasi kwamba hata majengo mengi yaliyokuwepo yameanguka na machache yaliyosalia yamekuwa magofu, mashine na mitambo yote ya kilimo iliyokuwepo shambani hapo imeharibika na michache iliyosalia imehamishiwa Morogoro. Kwa sasa shamba limebaki na wafanyakazi wasiozidi watatu kutoka ishirini na vibarua thelathini waliokuwepo miaka ya 1988 – 1995.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Halmashauri ya Wilaya kusubiri kwa muda mrefu jibu la Kamishna wa Ardhi bila mafanikio, kikao cha RCC kiliiagiza Halmashauri kuandaa maelezo kuhusiana na shamba hili ili Mkuu wa Mkoa aweze kuandikia Wizara husika kuomba rasmi Halmashauri kukabidhiwa eneo tajwa. Tayari Halmashauri imetekeleza maagizo haya. Naiomba Wizara ya Ardhi isaidie katika utatuzi wa kero hii ambayo inawasumbua sana wananchi.

(iv) Kwamtili Estate; shamba hili lina ukubwa wa hekta 1,150 na linamilikiwa na Kwamtili Estate Limited yenye Certificate of Incorporation Na. 2649 iliyosajiliwa tarehe 9 Januari, 1961 ikiwa na wanahisa wafuatao:-

S/N JINA LA MWENYE HISA ANAPOISHI MAELEZO
1 DENNIS Martin Fielder 4 Market Square Tenbery,Wells Worcestershinre –UK Amerudi Uingereza
2 National Aggriculture
& Food Corporation (NAFCO Box 903 Dar es Salaam Shirika limefutwa
3 Handrick Tjails Scheen CI/30 Algamines Bank, Amsterdam, Netherland Amefariki
4 Louis Van Wagenburg Laycsan Ag Vaghel, Holland Amefariki
5 Schoonmarkers Bart Vandrbug De Congqabsen,163 Schikher, Holland Amefariki
6 Tracey Elan Allison The Willos Terrigton, Herefordenshire, UK Amefariki
7 Juvent Magoggo 42 Block S. Mikanjuni Box 5855 Tanga Anaishi Tanga
8 W.J. Tame Ltd Box 118 Tanga Amefariki
9 Jacobus Cornelius Josephus Moris Logtamburg Vaghel Holland Amefariki

Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba hili lililopo katika eneo la Kwamtili, Kata ya Bosha Wilaya ya Mkinga, lilitumika kwa kilimo cha kibiashara cha zao la kakau. Hata hivyo, kwa muda wa miaka takriban 26 sasa shughuli za kilimo cha zao la kakau zimesimama baada ya iliyokuwa Menejimenti ya Kampuni chini ya Ndugu Dennis Fielder kutelekeza shamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, baada ya shamba kutelekezwa, mmoja wa wanahisa Ndugu Juvent Magoggo amekuwa akifanya shughuli ndogo ndogo ikiwemo kuvuna miti ndani ya shamba hili kwa lengo la kupata fedha za kufanyia uzalishaji mdogo mdogo; na hali kadhalika kuruhusu wananchi wanaozunguka shamba hilo kulima mazao ambayo si ya kudumu. Hata hivyo, kwa sasa ndugu Magoggo ameshindwa kuendelea kufanya shughuli hizo baada ya kunyimwa vibali vya kuvuna miti kusafirisha magogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kuwepo kwa ombi la umiliki wa shamba hili, yamezuka makundi ya watu yanayodai kuwa na haki ya kumiliki shamba hili na hivyo kuwakodisha wananchi wanaozunguka shamba hili maeneo ya kulima kwa kuwalipisha sehemu ya mavuno yatokanayo na matumizi ya ardhi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kumekuwa na wimbi la kujitokeza raia wa kigeni kwa kutumia kivuli cha aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa shamba na kulitekeleza Ndugu.Dennis Fielder kufanya uharibifu wa mali za kampuni, ikiwemo upasuaji wa mbao na kuanzishwa michakato ya kujimilikisha ardhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili, wananchi wanainyooshea kidole Ofisi ya Wakala wa Hifadhi ya Misitu, Wilaya ya Mkinga kutaka kujiingiza katika kufanya udalali wa ardhi hii. Wananchi bado wanakumbukumbu nzuri ya jinsi watumishi hawa wa TFC Wilayani Mkinga walivyotumika kuwezesha mwekezaji wa Kiitaliano aliyejaribu kupatiwa ardhi ya Mkinga takriban hekta 25,000 kinyume na taratibu ili kulima Jatropher.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Serikali haijaweza kulipatia ufumbuzi tatizo lingine ambalo kimsingi limeanzishwa na TFC kutaka kupora ardhi ya wananchi katika shamba la Segoma, TFC hiyo hiyo inataka kuzalisha mgogoro mwingine wa kupora ardhi nyingine katika Wilaya ya Mkinga.

Hatupo tayari kuona hili likitokea hasa ikizingatiwa kuwa Kwamtili inakabiliwa na tatizo kubwa la ardhi. Tunaiomba Serikali kutumia busara kuacha jambo hili na kuirejesha ardhi hii kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kwamtili na Kata ya Bosha kwa ujumla wamebaki katika umaskini wa kutupa baada ya shughuli za kilimo cha kakau katika shamba la Kwamtili ambacho ndicho kilitoa ajira kwao kusitishwa. Nusura pekee kwa wananchi hawa ni kupatiwa maeneo katika shamba hili ili kwa kutumia utaratibu wa wakulima wadogo waweze kufanya shughuli ya kilimo na hivyo kujikimu kimaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali ifanye uamuzi wa kufuta hati ya shamba la Kwamtili na kisha kuligawa kwa wananchi kwa ajili ya kilimo na sehemu nyingine kwa wananchi kuwa hifadhi ya msitu wa kijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua changamoto kubwa inayowakabili wananchi wa Kwamtili, RCC iliagiza mmiliki wa shamba hili kupewa notice ili taratibu za kufutiwa hati ziweze kufanyika. Kwa masikitiko makubwa kumekuwa na urasimu mkubwa wa taratibu wa kutolewa notice tajwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya Afisa Ardhi Mteule toka Ofisi ya Kanda-Moshi kuja Mkinga kufanya zoezi la uhakiki mwanzoni mwa mwezi Aprili hadi leo hakuna kinachoendelea licha ya kukumbushwa mara kadhaa kwa simu na Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Mkinga. Naiomba Wizara iingilie kati jambo hili ili ujanja ujanja usitumike kuvuruga mchakato wa kuwapatia haki wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo haya, naunga mkono hoja. Aidha, naomba Wizara ya Ardhi kwa kushirikiana na TAMISEMI itusaidie Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga tuweze kuajiri Afisa Ardhi Mteule ili atusaidie kuondoa migogoro.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili nami nipate wasaa wa kuchangia kwenye Bajeti iliyoko mbele yetu. Namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma kwa kunipa tunu ya uhai. Kwa namna ya kipekee niwashukuru wananchi wa Mkinga kwa heshima waliyonipa ya kuwa mtumishi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kugusia eneo la afya. Mwezi Februari, tulizindua taarifa ya tathmini ya utoaji wa huduma za afya nchini. Taarifa ile ukisoma inakupa matumaini kweli kweli. Ni taarifa inayosema kwenye vituo vya afya vya private sector, huduma za afya za mtoto zinatolewa kwa asilimia 80, lakini kwenye vituo vya Serikali huduma za kisasa za huduma ya mama na mtoto zinatolewa kwa asilimia 97. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali lakini napongeza yale yaliyomo kwenye taarifa ile. Nilipokuwa nikiisoma taarifa ile nikasema hapa barabara, kwenye suala la universal health tunakwenda vizuri; lakini nikapata mashaka makubwa nilipokuja kuiona hotuba. Nilipokwenda ukurasa wa 32, ukajaribu kunionyesha mambo tofauti. Ukurasa ule utuambia katika Halmashauri 181, Halmashauri 84 ndiyo zina hospitali za Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri 97 zinapata kudra ya Mwenyezi Mungu ya huduma kutoka kwa Taasisi za Mashirika ya Dini na kadhalika. Hili likanishtua kwa sababu Mkinga leo hii tunapozungumza, Wilaya iliyoanza mwaka 2005 na kupata hadhi ya kuwa Halmashauri mwaka 2007 mpaka leo hatuna Hospitali ya Wilaya. Tunapata huduma kutoka Tanga kwenye Hospitali ya Bombo, tunapata huduma kwenye Hospitali ya Wilaya ya Muheza. Tumekuwa tukitenga kwenye bajeti fedha kwa ajili ya ujenzi tangu mwaka 2011, fedha haziji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndani utaambiwa kwamba nendeni mkatenge kwenye bajeti. Tunatenga, fedha haziji! Tusaidieni! Tusaidieni ili watu wetu waweze kupata huduma hizi, maana Serikali ina wajibu wa kulinda maisha ya watu wake. Wananchi wametuamini, tuwatendee haki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hotuba hii ukurasa wa 32 ule, unatuonyesha kwamba tunatakiwa kuwa na direction mpya ya kuhudumia mambo. Sweeping statement kwamba tunataka kila kijiji kiwe na zahanati, tunataka kila kata iwe na kituo cha afya, pekee haitoshi tunatakiwa tufanye zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zile ukiziangalia zinaogopesha! Vituo vya afya 484 katika kata 3,506. Maana yake, tumeweza kujenga vituo vya afya 12% tu katika maeneo yetu, hii haikubaliki hata kidogo! Tuna vijiji 12,500 na kitu, vijiji 8,043 havina zahanati. Maana yake nini? Maana yake tumeweza kupeleka huduma hii kwenye vijiji siyo zaidi ya asilimia 36. Lazima tubadilike! Mkakati wetu wa kutufikisha kwenye kutoa huduma hizi una walakini. Mawaziri mliopo kwenye Wizara hizi, tunawaamini, tunaamini mtatoa uongozi utakaotutoa hapa twende mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni uwezeshaji wa wananchi kiuchumi. Nataka ni-declare interest, mimi nimetoka kwenye huduma hizi za fedha. Kumbukumbu zangu zinanionyesha, zimekuwepo jitihada mbalimbali za kupelekea huduma za kifedha kwa wananchi, kuwawezesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbukumbu zangu za haraka haraka zinaniambia tumekuwa na miradi takribani 17 yenye lengo la kutoa huduma za kifedha kwa wananchi. Utazungumzia SELF, utazungumzia PRIDE, utazungumzia mradi wa huduma za kifedha vijijini, utazungumzia miradi ya vijana; miradi karibu 16, yote hii inafanyika kwa lengo zuri la kuwawezesha wananchi, lakini changamoto tuliyonayo, mitaji hiyo haitoshi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja na Shilingi milioni 50 hizi kwa kila kijiji; tusiende kichwa kichwa. Wapo wenzetu walikwenda hivi wakaumia. Uganda walianzisha mradi wa namna hii wakiuita Entandikwa. Mwaka 2000 nilikuwa Uganda nikaenda kuungalia, repayment 0%, hakuna hela ilirudi. Wenzetu wa Thailand walifanya kitu cha namna hii, lakini wao walikuwa makini kidogo, mambo yao yamekwenda vizuri. Tusiwe na haraka ya kutoa fedha hizi bila ya kuwa na utaratibu makini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mifumo yetu ya kifedha, Bunge lililopita tulikuwa tunalalamika hapa, tunasema tupewe mitaji ya kuwezesha kuanzisha community bank. Leo hii community bank ukitaka kuianzisha, unazungumzia shilingi bilioni mbili. Kama tungekuwa makini, tungeweza kujipanga. Mimi nina vijiji 85, ukiniambia unapeleka shilingi milioni 50 kwenye kila kijiji, ni shilingi bilioni nne na kitu. Ningeweza kukwambia peleka Shilingi bilioni mbili ifunguliwe community bank ambayo kila mwananchi katika Wilaya yangu atakuwa na hisa kwenye benki hiyo na hizi fedha nyingine tuweze kuzikopesha. Tungekuwa na uhakika kwamba fedha hizi zitawafikia wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimeambiwa mtakuwa na pilot katika kugawa fedha hizi. Twendeni kwenye hiyo pilot, lakini tuangalie vile vile uwezekano wa kuanzisha community bank kupitia fedha hizi. Wale tutakaoweza kuwa na regional bank, tukikubaliana mimi na Mheshimiwa January na wenzangu wengine wa Tanga tuwe na regional bank katika Mkoa wa Tanga, tukikubali kwamba mafungu yatoke kwenye fedha hizo ambayo inafikia shilingi bilioni tano kwa kuwa na regional bank, mtukubalie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maji. Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga hayana maji. Kuna mradi pale tumebuni chanzo cha Kinyatu, tumeambiwa tutapata ufadhili wa Benki ya Dunia. Tumepeleka maandiko yanayotakiwa tupate mshauri mwelekezi tangu mwaka 2011, hakuna kitu! Tusaidieni watu wa Mkinga tupate huduma ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia bajeti iliyoko mbele yetu. Nitamke bayana kabisa kwamba naunga mkono bajeti hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa karama hii ya uhai na kwamba leo napata fursa ya kuzungumza ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nizungumzie eneo la REA, nitumie fursa hii kupongeza kazi kubwa iliyofanywa na wenzetu wa REA, imefanyika kazi kubwa sana, kazi ambayo ripoti inaonesha kwamba tumefikia kupeleka umeme vijijini sasa kwa asilimia 40, ni jambo zuri. Wakati tumefanya kazi hii vizuri ni ukweli vilevile kwamba zipo changamoto kubwa sana katika utekelezaji wa miradi hii ya REA. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Nishati, kwa hiyo nilipata fursa ya kuzungukia miradi ya REA, vilevile nina hazina ya uzoefu kwa miradi ya REA kule kwenye Jimbo langu. Kubwa tuliloliona ni kwamba kuna changamoto kubwa sana ya kusimamia utekelezaji wa miradi hii. Maeneo mengine yamerukwa kwenye vitongoji, maeneo mengine vijiji vimerukwa bila sababu za msingi na maeneo haya ni maeneo ambayo awali yalikuwemo kwenye mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilayani kwangu vipo vitongoji vimerukwa na bahati mbaya sana vitongoji vilivyorukwa wananchi wamekatiwa mazao yao ili umeme uweze kufika, mimea imekatwa hakuna fidia, lakini mwisho wa siku wanakosa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano na hili Naibu Waziri analijua kwa sababu nililisema tukiwa kweye Kamati, kijiji ninachotoka mimi zimepelekwa nguzo 15, hivi nguzo 15 zinapelekaje umeme kwenye kijiji? Sasa matokeo yake taasisi muhimu kama zahanati, sekondari, shule za msingi zimekosa huduma hii, ukiacha wananchi ambao wamekatiwa mazao yao. Nadhani hii siyo sahihi tujitahidi katika kusimamia ili tuondokane na kero hii ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeliweka tena eneo hili la Kata ya Kigongoi kwa matumaini kwamba linaingia kwenye REA Awamu ya Tatu. Hivyo, naomba miradi hii ya REA tuisimamie iende vizuri, mapungufu yote ambayo yameonekana sasa yasije yakaathiri utekelezaji wa REA Awamu ya Tatu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haingii akilini, kwamba umeme unapelekwa kwenye kijiji lakini wananchi wanaambiwa umeme ulioletwa hauwawezeshi ninyi kuendesha mashine za kusaga unga na mambo kama hayo, tufanye marekebisho, tufanye usimamizi wa karibu ili changamoto hizi ziweze kuondoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine linalokwenda sambamba na hilo ni kukatika umeme katika maeneo ya Mkoa wa Tanga, nilisema hapa eneo la Maramba, mwenzangu Majimarefu akazungumzia kule Korogwe, dada yangu Chatanda akazungumzia Korogwe Mjini na Waziri akatuambia kwamba upo mradi mkubwa wa kuboresha upatikanaji wa umeme, naomba jambo hili lisimamiwe kwa karibu ili tuondokane na tatizo hili.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwenye eneo la uchimbaji wa madini ya graphite. Taarifa zilizopo sasa zinasema Tanzania itakuwa miongoni mwa Mataifa makubwa yanayozalisha graphite, tutakuwa ndani ya nchi kumi zinazozalisha graphite ulimwenguni. Wakati tukielekea huko nataka tujiulize, tumejipanga namna gani kusimamia eneo hili ili yasije yakatukumba kama yaliyotokea malumbano wakati tunaenda kwenye uchimbaji wa dhahabu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwnyekiti, taarifa zilizopo ni kwamba tayari wapo wajanja wachache ambao hawastahili kuajiriwa kwenye sekta hii, makampuni ya nje yamewaajiri watu ambao vibali vyao vinatia mashaka kuajiriwa kwenye sekta hii, taarifa zilizopo zinasema wapo watu wameajiriwa kwa fani ambazo Watanzania wanaweza kuzisimamia. Hivi inakuwaje leo tunaajiri mtu wa sekta ya ununuzi kutoka Australia, kwamba Watanzania hawapo wenye uwezo wa kusimamia mambo haya? Mheshimiwa Waziri naomba tufanye due diligence katika mambo haya ili tusije tukaingia kwenye matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo taarifa kwamba ipo kampuni imepewa leseni, kampuni hiyo tunaambiwa inatoa asilimia tano ya hisa kwa Tanzania, madini yetu tunapewa asilimia tano, mimi sitaki kulikubali hilo, lakini kama ni kweli Mheshimiwa Waziri hebu lifuatilie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni madini ya vito. Tumelizungumza kwenye Kamati tukajielekeza moja kwa moja kwenye Tanzanite, ripoti za kitafiti duniani zinaonesha kwamba madini ya vito asilimia 50 yanazalishwa kwenye ukanda wa Afrika Mashariki. Lakini kwa bahati mbaya sana nchi hizi zimeshindwa kunufaika ipasavyo kwenye madini haya, hapa ndipo linapokuja suala la Tanzanite, tumezungumza kwenye Kamati nini cha kufanya, naiomba Serikali imuelekeze Mkaguzi na Mthibiti Mkuu Hesabu za Serikali aende akafanye ukaguzi maalum kule Tanzanite ili ripoti hiyo ituwezeshe Bunge kuishauri Serikali ipasavyo, hatujanufaika na Tanzanite. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Lema pale anasema, sasa jamaa wameondoka kutoka kununua Arusha, Tanzanite inafungashiwa Mombasa, nataka wakati tukiyasikia haya turudi kwenye tafiti, taarifa ya Umoja wa Mataifa inasema nini, taarifa ya Umoja wa Mataifa inasema madini haya gemstone ndiyo imekuwa kichaka cha magaidi, kujificha kwenye jambo hili. Sishangai kusikia kwamba badala ya watu wale kuwa Nairobi sasa Tanzanite inafungashiwa Mombasa, nikisema hivi nafikiri mnaelewa ninasema nini, tuyasimamie madini yetu vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni EWURA, tulifanya uamuzi wa kuanzisha EWURA na tulipoanzisha work load ya sekta ya nishati haikuwa kubwa sana, kwa hiyo ilikuwa ni sahihi pengine EWURA kusimamiwa na Wizara ya Maji. Sasa workload ya upande wa nishati imepanuka sana, nadhani siyo sahihi kuendelea kuiacha EWURA ikasimamiwa na Wizara ya Maji, nafikiri busara itumike, Mheshimiwa Rais ashauriwe ili ile instrument inayoelekeza EWURA kusimamiwa na Wizara ya Maji sasa ibadilishwe na hata ikibidi EWURA igawanywe, tuwe na kitengo kinachosimamia sekta ya nishati ibaki Wizara ya Nishati, na ile inayoshughulikia sekta ya maji ibaki Wizara ya Maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni matumizi ya gesi, tumekuwa tukijielekeza kwenye matumizi…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye mawasilisho ya bajeti iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze kwa kuipongeza sana Kamati ya Bajeti, imefanya kazi kubwa, na naomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tusome sana hotuba ya Kamati ya Bajeti, wamekuwa wazalendo kweli kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niungane nao kuzungumzia masikitiko yangu kwamba kama kweli Bunge hili linataka kutumika kama rubber stamp Wabunge tukatae kwa nguvu zetu zote. Tulifanya kazi kubwa ya kuja na Budget Act, tukasema ni sheria inayokuja kututoa kwenye kufanya mambo kama business as usual. Ninyi leo mnataka kuturudisha kule?
Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa ya Kamati inalalamika kwamba haikuzingatia maoni ya Kamati, Wabunge tusikubali asilani. Serikali hii ni sikivu, sikieni haya yanayosemwa na Kamati ya Bajeti, sikieni haya yanayosemwa na Wabunge. Nchi hii yetu sote, tukifika mahali kikundi fulani kikajiona chenyewe kinajua zaidi ya Wabunge tuna tatizo kama nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma mpango, Ripoti ya Hali ya Uchumi inatuambia sekta ya ujenzi imeongoza kwa kuchangia kwa asilimia 16.8, sekta ya habari na mawasiliano asilimia 12, sekta ya fedha na bima asilimia 11, sekta ya madini asilimia 9.1; lakini sekta zote hizi zinashughulisha watu wachache. Sekta inayoajiri asilimia 70 ukuaji umeshuka. Sekta ya kilimo ukuaji umeshuka kutoka asilimia 3.4 sasa ni asilimia 2.3 and yet we are happy, hii haikubaliki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nataka nijielekeze kwenye eneo moja, sekta ya uvuvi hivi tunataka tuambiweje ili tuelewe?
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma ripoti ya mwaka 2014 ya state of the fisheries ya Shirika la Chakula Duniani inasema kwamba uzalishaji wa samaki kupitia ufugaji (aquaculture) ulikuwa ni tani milioni 100 ulimwenguni; pasipo kuzungumzia uvuvi bali ufugaji wa samaki; zenye thamani ya bilioni 144.4. Hivi watanzania hatutaki kushiriki kwenye uchumi mkubwa kiasi hiki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika uzalishaji huo Asia imezalisha asilimia 88 ya hizi, Amerika asilimia 4.7, Europe asilimia 4.3, Afrika asilimia 2.2, kwa maana kwamba imezalisha tani milioni 1.4. Lakini angalia kichekesho chake katika tani milioni 1.4. Lakini angalia kichekesho chake, katika tani milioni 1.4 Misri peke yake imezalisha tani milioni 1, nchi nyingine za Afrika ndio tunanyanganyia 0.4. Lakini Misri hii ufugaji huu wa samaki inategemea maji kutoka Mto Nile, Tanzania ikiwa sehemu ya uchangiaji wa maji ya Mto Nile. Sisi tuna ziwa Victoria, Tanganyika, tuna bahari, tuna Ziwa Nyasa tumelala usingizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uchumi mkubwa kama China wanaona umuhimu wa kushiriki kwenye uchumi huu, wanazalisha nusu ya samaki wanaofugwa ulimwenguni. Sisi Watanzania tunaona sekta hii ya kipuuzi, tubadilike. Ni kwa kupuuza vitu kama hivi ndiyo maana leo hii mchango wa sekta ya uvuvi umeshuka, na umekuwa ukishuka tangu mwaka 2007. Mchango wa sekta hii ilikuwa asilimia 1.7, tumeporomoka mpaka asilimia 1.2 mwaka jana, lazima tubadilike. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Kamati kwa kuzungumzia suala la mfuko wa maji, safari hii msitufanyie kiini macho. Mwaka wa jana tulisema fedha zile ziende vijijini mkazipeleka mijini safari hii pelekeni fedha zile vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Bajeti imesema tuweke tozo kwenye mafuta mbona Wakenya wameweka bajeti yao ya juzi? Tuweke tozo kwenye mafuta, twende tukajenge zahanati. Hii ni aibu kwamba tangu mwaka 2000 tunaweka kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kwamba tutapeleka zahanati kwenye kila kijiji tumekwenda kwa asilimia 20 tu. Tutenge bajeti twende tukajenge zahanati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuongeze fedha za maji, wananchi wetu wanataabika vijijini. Pale Mkinga kuna one stop border post, tumeambiwa kimekamilika; kituo kile hakina maji. Mheshimiwa Mpango watu wako watakuwa kwenye ofisi ile haina maji; yatakuwa yanachukuliwa kutoka Kenya. Tuna mradi wa bilioni sita tupeni fedha tukafanye mambo pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nipongeze jitihada zinazofanyika katika kuanzisha Vituo vya Pamoja vya Utoaji Huduma Mipakani (OSBP). Kituo cha Horohoro/Lungalunga ni miongoni mwa vituo vilivyokamilika. Hata hivyo, kituo hiki kinakabiliwa na tatizo kubwa la maji. Kituo hiki kimejengwa upande wa Tanzania eneo ambalo kuna tatizo kubwa la maji kiasi kwamba wananchi wanalazimika kufuata huduma ya maji umbali mrefu upande wa Kenya. Halmashauri ya Mkinga imejitahidi kuibua miradi itakayokuwa suluhisho la tatizo la maji katika eneo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari ripoti ya detailed design imepatikana ikionesha kuwa mradi huu unahitaji kiasi cha takribani shilingi bilioni sita na nusu. Halmashauri ya Mkinga haina uwezo wa kifedha wa kujenga mradi huu. Nashauri Wizara ya Mambo ya Nje ichukue mradi huu kwa kutafuta fedha toka vyanzo vya Jumuiya ya Afrika Mashariki au ufadhili mwingine wowote utakaowezesha kutekelezwa kwa mradi huu. Itakuwa jambo la aibu endapo kituo hiki kitafunguliwa bila ya kuwepo jawabu la utatuzi wa tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni European Union kushinikiza nchi za kiafrika kutia saini mkataba ujulikanao kama Economic Partnership Agreement. Mkataba huu ni mbovu na una madhara makubwa kiuchumi kwa nchi za kiafrika Tanzania ikiwemo. Taifa linapaswa kuwa na tahadhari kubwa na mkataba huu hususan sasa ambapo kama Taifa tumedhamiria nchi yetu kuwa nchi ya uchumi wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iweke wazi ndani ya Bunge hili msimamo wetu kama nchi kuhusiana na jambo hili. Waziri atakapokuwa anafanya
majumuisho alieleze Bunge lako ni kwa vipi nchi yetu itaachana na mkataba huu wa kinyonyaji. Wizara ilishirikishe mapema Bunge katika kufahamu kwa undani suala hili la EPA ili Wabunge wawe na uelewa mpana utakaowawezesha kufanya maamuzi sahihi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja.
Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii. Nimshukuru Mungu sana kwa siku ya leo kufika, kwa sababu ni siku ambayo niliitarajia na niliitegemea sana. Nasema haya kwa sababu nimepata bahati ya kushiriki makongamano ya kitaalam ya jambo hili, mwaka 2013 kule Rwanda na mwaka 2014 kule Brussels, Ubelgiji.
Mheshimiwa Spika, kiufupi mkataba huu ni hovyo! kiufupi wenzetu hawana nia njema kupitia mkataba huu. Mkataba huu umejadiliwa kwa miaka 12, miaka 12 nchi zetu zimekuwa kwenye majadiliano ya mkataba huu and yet tuna mkataba mbovu kiasi hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, huu ni mkataba ambao nchi yetu imeamua kuchukua njia ya kidiplomasia kusema kwamba inajitoa kwa sababu Uingereza inajitoa kwenye European Union, kauli ya kidiplomasia, lakini nchi ya Tanzania tumeheshimika duniani kwa kusimamia tunachoamini, tusijifiche kwenye diplomasia hii, tuwaambie ukweli hawa wenzetu ambao hawana nia njema na sisi. Tuwaambie ukweli kwamba tunathamini Utanzania wetu, tuwaambie ukweli kwamba tunajiheshimu na hatuko tayari kupuuzwa kupitia mkataba huu.
Mheshimiwa Spika, mambo mengi yamesemwa, loss of revenue, kulinda viwanda vya kati na vidogo, yamesemwa kuhusu rendezvous clause, mimi nataka niya-sum up kwa mambo haya machache nitakayouliza.
Mheshimiwa Spika, wakati nikisoma mkataba huu najaribu kujiuliza hivi mkataba huu unakusudia kutuongezea uzalishaji katika nchi zetu? Jibu ni hapana. Hivi mkataba huu unatuhakikishia usalama wa chakula? Jibu ni hapana. Hivi mkataba huu unatuongezea fursa za ajira zenye staha katika nchi zetu? Jibu ni hapana. Hivi mkataba huu unatuwezesha kutoka katika uchumi wa kutegemea natural resources exportation na kwenda kwenye production of sophisticated products? Jibu ni hapana. Lakini kilichowazi ni mkataba wa kutweza utu wetu, tufike mahali tuwaambie mchana kweupe macho makavu, kwamba hatutakubali kudhalilishwa.
Mheshimiwa Spika, tuupinge mkataba huu. Nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja kuhusiana na Bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji katika Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwepo wa miundombinu ya uhakika ya barabara katika maeneo ya vijijini una umuhimu mkubwa katika kufungua fursa za kiuchumi na hivyo kuharakisha maendeleo kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapojiwekea lengo la ujenzi wa barabara za lami kuunganisha Mkoa kwa Mkoa, tuna wajibu vile vile wa kutoa msukumo kwa barabara za aina hiyo zenye umuhimu wa kimkakati katika usalama na kukuza fursa ya kuongeza/kuunganisha vivutio vya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabokweni – Gombero – Maramba – Bombo Mtoni – Kitivo – Mlalo hadi Same ni barabara mbadala ya kuunganisha Mkoa wa Tanga na Mkoa wa Kilimanjaro. Barabara hii inapita kwenye maeneo makuu ya uzalishaji mazao ya chakula na biashara. Ni barabara inayounganisha maeneo haya ya Bandari ya Tanga na nchi jirani ya Kenya. Aidha, kwa upande wa usalama wa nchi, barabara hii ni barabara ambayo ina umuhimu wa kiusalama kwa nchi yetu kutokana na ukweli kuwa inaambaa katika mpaka wetu na nchi ya Kenya. Hivyo, kufanya zoezi la kukagua na kulinda mpaka wetu kuwa na uhakika zaidi kinyume na ilivyo sasa ambavyo tunalazimika maeneo mengi kupitia Kenya ili kuweza kukagua mpaka wetu na Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mabokweni – Maramba – Bomba Mtoni – Mlalo hadi Same ni barabara muhimu kwa kukuza utalii, kwa kuunganisha Mbuga ya Saadani na Mkomazi ambayo inagusa Wilaya ya Mkinga eneo la Mwakijembe ambako yapo maeneo ya asili ya mazalia ya faru. Kwenye Umba Game Reserve, Wilaya ya Lushoto eneo la Mlalo hadi Wilaya ya Same kwenye Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kutaimarisha na kuunganisha Sekta ya Utalii siyo tu kwa Mbuga ya Sadaani na Mkomazi, bali kutaunganisha utalii kwa watalii kutoka Zanzibar kuweza kutembelea vivutio kutoka Saadani, Amani, Nature Reserves, Mapango ya Amboni hadi maeneo ya utalii ya Ngorongoro, Mlima Kilimanjaro na kadhalika. Aidha, barabara hii itavutia watalii toka Mombasa, Kenya; kuvutika kwa urahisi zaidi kuja Tanzania kupitia Horohoro, Mbuga ya Mkomanzi kuanzia Mkinga hadi Kilimanjaro. Naiomba Serikali kuipa kipaumbele barabara hii kwa kuanza kufanya upembuzi yakinifu ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuanza ujenzi wa reli kwa standard gauge. Naishauri Serikali kwamba, umefika wakati sasa tuanze kuweka mfumo wa infrastructure bond katika ujenzi wa reli na barabara zetu. Nashauri tujifunze kwa wenzetu wa Nigeria, India na Israel katika kutumia infrastructure bonds katika kujenga miundombinu muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kutenga shilingi milioni 865 kwa ajili ya fidia kwa wananchi katika barabara ya Tanga - Horohoro. Hata hivyo, naisihi Serikali ihakikishe fedha hizi zinapatikana kwa sababu hii imekuwa kero ya muda mrefu kwa wananchi. Aidha, ni vyema kukawa na ushirikishaji wa karibu kwa uongozi wa eneo husika pindi malipo yatakapokuwa yanafanyika ili kuhakikisha kila anayestahili kuliwa anapata haki yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kutenga fedha, shilingi milioni 120 ku-upgrade Mkinga Township Road kilometa nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nikikumbusha kuwa bado barabara ya TANROADs kuunganisha Maramba na Makao Makuu ya Wilaya katika Mji wa Kasero haijakamilika. Aidha, eneo la Magoli bado ambalo barabara itapita pembeni ya Kijiji halijakamilika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba iliyoko mbele yatu. Nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama mbele ya Bunge letu Tukufu na kuweza kuwasilisha mawazo ya watu wa Mkinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie firsa hii vilevile kuwapa pole ndugu zangu wa Mkinga kwa maafa makubwa waliyoyapata kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika Jimbo letu la Mkinga na kwa Mkoa wa Tanga kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa za Kituo cha Utafiti cha Mlingano zinasema mvua zinazoendelea kunyesha sasa zimefikia milimita 316 katika span ya siku tatu. Kiwango hiki ni kikubwa sana, mvua hizi hazijawahi kuoneka kunyesha kwa miaka 40 iliyopita. Kwa hiyo, tunapozungumzia madhara yaliyotokana na mvua hii tunaiomba Seriakli ilichukulie jambo hili kwa umakini mkubwa. Hivi ninavyozungumza mabwawa yangu saba katika Wilaya ya Mkinga ambayo yanatusaidia kupata maji yamepasuka. Miradi ya maji ambayo mabwawa yamepasuka ni Bwagamacho, Horohoro border, Doda, pamoja na Machimboni na mradi wa maji Maramba mabomba yamesombwa na maji, kwa hiyo, mpaka kwenye hospitali yetu ambayo sasa tunaitumia kama Hospitali ya Wilaya imekosa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, bwawa la maji Mwanyumba ambapo sambamba na hilo kuna daraja kubwa limepsuka na daraja limekatika, kwa hiyo, mawasiliano kati ya Tarafa ya Maramba na Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga yamekatika. Scheme yetu ya umwagiliaji Mwakijembe imesombwa na maji, mitaro imejaa mchanga, hekta karibu 98 za mazao zimesombwa. Athari yake; takribani watu zaidi ya 10,000 hawana maji.

Naiomba Serikali ilichukulie jambo hili kwa uzito mkubwa na kwa uharaka ili huduma ya maji iweze kurejeshwa. Ninawaomba ndugu zangu wa Mkinga waendelee kuwa wavumilivu Serikali ninaamini italifanyia kazi jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo ya utangulizi naomba nianze mchango wangu kwa kunukuu taarifa ya wataalam katika jarida la World Water and Sanitation. Katika mchango wao pale wanasema na ninanukuu:-

“The world does not stand a chance without water, it spread disease, compromise safety, makes education elusive and economic opportunity further out of reach. The lack of access to safe and clean water is deadly, dangerous and major obstacle to people of developing world becoming economically empowered and it is what it is standing between billions of people and their health, safety, opportunity to unlock their potential.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali yangu isikubali ukosefu wa maji ukazuia fursa za maendeleo kwa watu wetu. Naiomba sana Serikali yangu isikubali ukosefu wa maji ukawa chanzo cha vifo vya watu wetu.

Wale tuliokuwemo kwenye Bunge lililopita wanakumbuka, tulijadili mambo kwa kina hapa katika Bunge hili wakati tunazungumzia kuweka tozo kwenye mafuta ya taa ili kupata fedha za kupeleka umeme vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia watakumbuka sentiments zilizokuwepo, hofu ya kuleta mfumuko wa bei na kadhalika, lakini tuliishauri Serikali na hatimae ikakubali, tukaweka tozo kwenye mafuta ya taa na leo kila mtu anashangilia upatikanaji wa umeme vijijini. Wananchi walikubali maumivu yale na leo wanashangilia umeme vijijini. Tusiwe wazito kukubali ushauri wa Bunge hili kuongeza tozo ya mafuta ili tupate fedha za kupeleka maji vijijini, let us unlock the potential of our people, tuwape maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Makao Makuu ya Mkinga hayana maji. Nimelisema hili kwa muda mrefu, nafurahi leo katika hotuba hii nimeona Wizara imetenga fedha kwa ajili ya kutengeneza mradi wa maji pale, lakini fedha zile nimeona zinagusa maeneo mengi, nimeona shilingi bilioni mbili pale; lakini fedha zile zinaigusa Handeni na maeneo kadhaa. Hofu yangu ni kwamba inawezekana fedha zile zisiweze kutosha kukamilisha jambo lile. Shida ya maji kwenye mji wa Kasera ni kubwa mno, naomba twendeni tukatekeleze mradi ule wa kutoa maji Kinyatu ambao utagusa kata za Mkinga, Parungu- Kasera, Boma pamoja na Manza. Tusaidieni tupate maji kwenye Makao yetu makuu ili tuweze kuujenga mji wetu, tuweze kuwahakikishia watu wetu afya bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine nilisema hapa kwenye bajeti iliyopita kwamba mji wa mpakani wa Horohoro ambako tumejenga Kituo cha Biashara ya Pamoja (One Stop Border Post) hauna maji. Tunapata aibu, watu wanakwenda kuchota maji Kenya. Tulikuwa na bwawa dogo pale ambalo lilikuwa linasaidia watu, leo hii ni miongoni mwa maeneo niliyosema hata bwawa hilo limepasuka.

Mhesimiwa Naibu Spika, tunao mradi, tumeshafanya usanifu unaotoa maji Mwakikonge, mradi ule unahitaji shilingi bilioni sita, tutakuwa tumemaliza tatizo lote la maji kwenye eneo lile. Naomba Serikali tusaidieni watu wale wapate maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni yamekuwepo malalamiko ya maji ya mji wa Tanga kuchafuka. Chanzo cha maji yale yanatoka Bosha na Mhinduro…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wale hawana maji, tunaomba muwapatie maji.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuunga mkono hoja ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kuhusiana na makadirio ya matumizi ya fedha ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia inashuhudia mabadiliko makubwa katika mifumo ya maisha na mazingira ya kiusalama yasiyotabirika. Katika mazingira haya, ulinzi wa mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na uhuru wa nchi yetu ni jambo la kufa na kupona linalopaswa kupewa umuhimu mkubwa na wa kipekee sasa kuliko wakati mwingine wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika zama hizi za mabadiliko makubwa ya teknolojia na changamoto za ushindani katika ukuzaji uchumi wa viwanda, kama nchi usalama wetu na uhuru wetu unategemea sana uwepo wa jeshi imara la kisasa lenye weledi, vifaa vya kisasa, uzalendo na nidhamu ya hali ya juu. Hivyo basi ni wajibu wetu kama Taifa kuhakikisha inakuwepo bajeti ya kutosha itakayoliwezesha jeshi letu kukabiliana kikamilifu na changamoto za sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mkinga inapakana na nchi jirani ya Kenya. Katika jitihada za kuimarisha ulinzi Halmashauri ya ilitenga fedha za kujenga daraja ili kuwezesha ulinzi na ukaguzi wa mpaka wetu. Hii ni kutokana na ukweli kuwa kabla ya uwepo wa daraja hilo, ukaguzi wa mpaka wetu ilibidi ufanyike kwa kupitia Kenya. Kazi ya kujenga daraja hilo ilikabidhiwa kwa JWTZ. Natoa pongezi kwa JWTZ kwa kukamilisha kazi ya kujenga daraja hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuiomba Serikali iongeze nguvu katika ulinzi wa mipaka yetu kwa kuweka miundombinu muhimu kama barabara na madaraja yanayokidhi viwango na mahitaji ya kijeshi katika maeneo yote ya Wilaya za mipakani.

Aidha, fedha na jukumu la kujenga miundombinu muhimu katika maeneo haya ya kimkakati, kiulinzi na kiusalama lisiachwe mikononi mwa Halmashauri bali liwe jukumu la moja kwa moja la JWTZ.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Mwakijembe ni miongoni mwa kata 22 za Wilaya ya Mkinga. Kata hii ipo katika mpaka wetu na nchi ya Kenya na kwa miongo kadhaa wananchi hawa wamefanya kazi kubwa ya kuwa walinzi wa mpaka wetu. Naipongeza sana Serikali kwa uamuzi wake wa kuimarisha ulinzi katika Kata ya Mwakijembe kwenye mpaka wetu na nchi ya Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, wakati naipongeza Serikali kwa hatua hii, utekelezaji wake umekuwa na dosari na hivyo kuitia doa Serikali. Doa hili linatokana na JWTZ kutwaa mashamba ya wananchi bila kutoa fidia stahiki kwa wananchi. Inasikitisha kuwa Jeshi lilitumia mabavu kuwapora wananchi ardhi yao tena kwa kufyeka mazao yaliyokuwa mashambani. Hali hii imeleta manung’uniko na wananchi wanaona wamedhulumiwa na Serikali yao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kihistoria eneo hili limekuwa mali ya wananchi kwa miongo na vizazi kadhaa. Hata pale Halmashauri ilipoamua kuanzisha skimu ya umwagiliaji, iliamua kuyajumuisha maeneo haya ya wananchi kwenye skimu lakini ikahakikisha umiliki wa maeneo hayo unaendelea kuwa mikononi mwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ifanye tathmini ya haraka kwa ardhi ya wananchi iliyotwaliwa ili wananchi hawa waweze kulipwa fidia stahiki. Wananchi ambao mashamba yao yametwaliwa ili kuwekwa kambi/ makazi ya jeshi ni Ndugu Benard Kinyili (ekari moja); Ndugu Ngoma Joseph (ekari moja na nusu); Ndugu Hamisi Joseph (ekari moja na nusu); Ndugu Mlewa Malonza (ekari mbili) na Ndugu Mwanza Kiziku (ekari mbili).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja nikiamini kuwa malalamiko ya wananchi wa Mkinga yatapatiwa ufumbuzi wa haraka.
Itifaki ya Nagoya ya Kusimamia Upatikanaji na Mgawanyo Sahihi wa Faida zitokanazo na Matumizi ya Rasilimali za Kijenetiki.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie kwenye itifaki hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema naiunga mkono itifaki hii kwa sababu inazungumzia maisha ya sisi watu wa Pwani na sisi watu wa Pwani bila bahari maisha hayapo. Vilevile niseme kwamba itifaki hii itakuwa na maana tu kama itatuhakikishia watu wa Pwani maisha yetu yataboreka. Kama itifaki hii haitatusaidia maisha yetu kuboreka haina maana, kama itifaki hii haitatuhakikishia kuboreka kwa maisha ya watu wa Pwani basi itifaki hii haina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya kwa sababu mwaka 1996 tulisaini mkataba ule uliokuwa unazungumzia udhibiti wa bahari ukanda wa Afrika Mashariki. Mwaka 2010 tukaiboresha itifaki ile tukasaini. Nataka tu nijiulize hivi tangu 1996 tuliposaini watu wa Pwani maisha yamekuwa bora? Nini kinatuhakikishia leo kwa kusaini itifaki hii kwamba maisha ya Pwani yataboreka? Utafiti umetuonyesha kwamba itifaki hii katika utekelezaji wake tangu mwaka 1996 umekuwa na changamoto kubwa ya kimfumo wa usimamizi wa taasisi za usimamizi, vilevile changamoto kubwa ya kifedha. Tafiti hazifanyiki na zikifanyika zinafanyika kwa ufinyu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka leo watu wa Pwani zana tunazotumia kwenye uvuvi ni zana duni, tumekuwa tukitamani tuyaone yanayofanyika kwenye sekta ya kilimo kupewa pembejeo na vitu vya namna hii, yafanywe kwenye sekta ya uvuvi hayafanyiki. Tumekuwa tukitamani tuyaone yanayofanyika kwenye sekta ya mifugo kwa watu wa sekta ya uvuvi hayafanyiki. Ndiyo maana mnashuhudia watu wale wanaendelea kutumia zana duni za tangu enzi ya Nabii Nuhu. Ndiyo maana mnashuhudia uvuvi wa kutumia mabomu unaendelea, ndiyo maana mnaona mazalia ya samaki yanaendelea kuharibika kwa sababu tumeitupa mkono sekta ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifurahi kwenye Ilani yetu tuliposema kwamba katika kipindi hiki tutaleta meli tano za uvuvi. Nataka tu niikumbushe Serikali yangu, mwaka wa pili huu sasa wa utekelezaji, tumebakia na miaka mitatu tujitahidi ahadi ile itimie. Lakini hata ahadi hiyo ikitimia bado asilimia kubwa ya wavuvi watakuwa hawana zana za kisasa kwenda kuvua, ndiyo maana leo unaona hata kwenye uuzaji wetu wa samaki tunategemea sana samaki wa kutoka Ziwa Victoria, uvuvi kwenye eneo la baharini uko duni. Twendeni tukawekeze kwenye blue economy, twendeni tukahakikishe ufugaji wa samaki unafanyika kwenye ukanda wa Pwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jarida la Sofia la FAO linatuambia hivi takribani watu milioni 57 wana… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami nichangie kwenye hotuba hii ya Wizara ya Viwanda. Namshukuru sana Mungu kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuzungumza katika Bunge lako Tukufu. Nianze kwa kusema naiunga mkono hoja iliyoko mbele yetu, nikiwa na reservation kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuleta hamasa kwa Watanzania kuona umuhimu wa kumiliki viwanda. Amefanya kazi kubwa ya kuwahamasisha Watanzania kubadili mitazamo ya uwekezaji ili wajielekeze kwenye kumiliki viwanda; viwe viwanda vidogo, viwanda vya kati, lakini vile vile viwanda vikubwa. Hongera sana, ameitendea haki taalum yake ya Masoko. Naomba sasa hili lisiwe jukumu lake peke yake, Wizara ilichukue hili kwa ujumla wake. Ongezeni nguvu katika kuhamasisha Watanzania wabadilishe mitazamo katika umiliki wa viwanda katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, nataka nieleze masikitiko yangu; pamoja na nia nzuri ya kuanzisha viwanda, lakini yapo mambo yanakwamisha sana ukuzaji wa viwanda katika nchi yetu. Ukifuatilia mijadala na sisi tunaopitia pitia tafiti zinazofanyika katika nchi hii, moja kubwa ni lack of coordination. Kuna maeneo tunakwenda hatua moja mbele, tunarudi hatua mbili nyuma; na nitatoa mfano.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nataka nizungumzie Sekta ya Maziwa. Utafiti wa wenzetu wa ESRF unaonesha kwamba mwaka 2010 tulikuwa tunaingiza maziwa kutoka nje takriban lita milioni 40 zenye thamani ya dola milioni 20. Ilipofika mwaka 2014 uingizaji wa maziwa ukaongezeka kutoka lita milioni 40 ukapanda mpaka lita milioni 70 zenye thamani ya dola milioni 40. Unaweza kuona ni jinsi gani tunapoteza fedha kwa kuingiza maziwa kutoka nje. Wakati tukiingiza maziwa kwa kiasi hicho, sisi tunazalisha takriban lita bilioni mbili, lakini zinazosindikwa hazifiki lita 150,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 62 ya maziwa tunayoingiza yanatoka Kenya, asilimia 32 yanatoka South Africa, asilimia nne Uganda. Hata haya yanayopitia South Africa, kuna walakini mkubwa. Tunaambiwa ni uchochoro wa kukwepa kodi. Nitayasema baadaye haya. Masikitiko yangu ni yapi? Kiwanda cha Tanga Fresh ambacho ndiyo kinazalisha kwa wingi sasa, kinazalisha lita 50,000 kwa siku. Ni kiwanda ambacho tulitakiwa kukilinda kwa nguvu zetu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda hiki miaka minne iliyopita, walitaka kuongeza uzalishaji kutoka lita 50,000 kwenda lita 120,000 na tulikuwa tumepata grant ya kuweza kufanya jukumu hilo. Wenzetu wa Bodi ya Ushindani wakawapiga faini ya shilingi bilioni nne wakisema walinunua assets kinyume na utaratibu. Assets zilizonunuliwa zilikuwa za kiwanda kilichokufa, kwa hiyo, hoja ya kuua ushindani haipo. Tumeminyana, faini ile imepungua mpaka sasa hivi bado imeng’ang’aniwa shilingi milioni 400. Hiki ni kiwanda ambacho kingeongeza uzalishaji katika nchi yetu. Fedha ile imepotea! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanga Fresh wameamua kukopa sasa. Wanataka kutumia assets zao, majengo yao waende wakakope. TRA wanakuja wanazuia wanasema hawawezi kutumia majengo yale kukopa kwa sababu aliyewauzia hakulipa kodi stahiki. Vitu vya ajabu sana! Yaani aliyekwepa kodi yupo, anajulikana; anaendelea kufanya biashara kwenye nchi hii, TRA, hawaendi kumbana, wanaenda kumbana Tanga Fresh ambaye hahusiki. Mambo ya ovyo sana! Tunashindwa kukuza viwanda vyetu kwa mambo ya ovyo kiasi hiki! Leo hii ninapozungumza, vituo 28 vya kukusanya maziwa kule Morogoro vimefungwa, wananchi hawana sehemu ya kuuzia maziwa yao kwa sababu hayawezi kupokelewa Tanga Fresh. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanga Fresh wananunua maziwa Mkoa mzima wa Tanga; Tanga Fresh wananunua maziwa kutoka kwa wakulima Mkoa wa Pwani; Tanga Fresh wananunua maziwa kutoka Morogoro. Hivi ninavyozungumza, Tanga Fresh wameombwa na wakulima kutoka Mbeya wanunue maziwa yao, wanashindwa! Maziwa yanamwagwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaingiza maziwa ya mabilioni haya kutoka Kenya, halafu tunakuja hapa tunasema tunataka kuendeleza viwanda, hii haiwezi kuwa sawa. Napiga kelele kwa Mheshimiwa Waziri wa Viwanda kwa sababu sera ya ukuzaji wa viwanda iko kwake, lakini najua mchawi wetu hapa ni Wizara ya Fedha. Najua jitihada alizofanya ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage ili jambo hili liishe, lakini barua ile aliyoandika mpaka leo imekaliwa pale Wizara ya Fedha hakuna kinachoendelea. Tutaendelea namna hii namna gani? Lazima tubadilike. Naiomba Serikali yangu jambo hili lishughulikieni, tuondoleeni aibu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kichekesho kingine, tulipitisha hapa Sheria ya VAT kwenye bidhaa za maziwa, tuliingizwa mkenge na wenzetu Kenya lakini Kenya wananchi walipopiga kelele, wenzetu wakafuta kodi ile, sisi tumeendelea nayo. Wabunge tukisimama tukisema hapa, tunaonekana vituko. Tuliyasema hapa kwenye Sekta ya Utalii hatukusikilizwa, Sekta ya Maziwa nayo imeingiliwa, hebu tuwe smart; tunapokubaliana na hawa wenzetu, tukiona wamekiuka makubaliano, mara moja na sisi tugeuke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu korosho; nilikuwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda, kipindi kilichopita, tuliahidiwa viwanda sita vya Korosho, leo hii havipo. Ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage, taarifa za Bodi ya Korosho wanatuambia mwaka huu, tani zilizouzwa korosho ghafi, tani 260,000 tusiendelee kuangalia jambo hili, tutumie Mfuko ule wa Export Levy kujenga viwanda. Nendeni mkafanye utafiti tujue, kama tunataka korosho yetu ibanguliwe hapa, angalau nusu ya tani hizi, tunahitaji viwanda vingapi, tutengeneze Mfuko wa Mikopo kutokana na Export Processing Levy tuitangaze, watu waje wakope fedha zile tujenge viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa pumzi na uhai na kwamba naendelea kuwatumikia wananchi wa Mkinga, lakini vilevile kutoa mchango kwa Taifa langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Kamati inayohusika na Wizara hii. Kamati imefanya kazi kubwa, Kamati imetufumbua macho juu ya hali mbaya iliyopo katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapoambiwa ukuaji wa sekta hii ni 1.7%, lakini unapoambiwa kwamba 65% ya Watanzania nguvu kazi hiyo inafanya kazi kwenye sekta hii halafu unapoambiwa kwamba mikopo inayokwenda kwenye sekta hii is only 2% na unapoambiwa kwamba fedha za maendeleo zilizotoka ni 3% tu, unachanganyikiwa. Kama nchi lazima tujitazame upya, lazima tujitafakari, tukishindwa kufanya hivyo tutaendelea kuwa soko la nchi nyingine.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii usindikaji wa maziwa yetu is only 3% ya tunachozalisha. Tunaagiza 62% ya maziwa kutoka Kenya, tunaagiza twenty something percent kutoka South Africa, tunaagiza 4% ya maziwa kutoka Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa hapa ni mashahidi leo hii Tanzania imekuwa jalala la matunda kutoka South Africa. Tunaagiza apples, machungwa na kadhalika. Hatuwezi kwenda namna hii lazima tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri anapoambiwa kwamba usindikaji wa maziwa katika nchi yake ni 3% tu, hili lazima limuumize kichwa. Nawasihi sana tuongeze nguvu katika kurekebsha mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye korosho halikadhalika. Korosho yetu yote tunaipeleka ikiwa ghafi kwa kiasi kikubwa. Nilisema juzi hapa na wapo baadhi ya Wabunge wenzangu waliniunga mkono kwamba tutumie fedha zile za export levy, twendeni tukajipange tuseme walau tuanze kwa kuhakikisha 50% ya korosho yetu inabanguliwa hapa ndani, tutumie fedha zile kujenga viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Wizara wamekuja na initiative ile ya kugawa bure dawa zile za kunyunyiza. Vilevile mnaangalia uwezekano wa kutoa hata magunia, ni hatua nzuri. Hata hivyo, ili twende haraka zaidi hebu twende kule kwenye kujenga viwanda vya kubangua korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, tuliwahi kuambiwa hapa ndani ya Bunge, wakati watu wa Tanga tunapiga kelele kuhusu viwanda vya matunda, tukaambiwa Tanga machungwa yenu hayafai kwa kutengeneza juice. Sasa Serikali mkishasema hivyo halafu mnaishia hapo, kwa nini hamji na utaratibu wa kuhakikisha mnabadilisha mbegu ile ili tuwe na mbegu zinazofaa kwa wakulima wetu? Kwa nini hatuipi nguvu Mlingano iweze kufanya utafiti au tukaingiza mbegu kutoka nje ili kubadilisha machungwa katika nchi yetu tuwe na machungwa hayo yanayofaa kwa kutengeneza juice? Nawasihi sana liangalieni hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Tanga tunalima mazao ya viungo, Muheza, Korogwe na Mkinga, lakini tuna tatizo kubwa la utafiti wa mbegu bora katika maeneo hayo. Mbegu inayotumika ni ya tangu Adam na Hawa. Tunaomba mfanye kazi katika eneo hilo. Najua huko mbele ya safari mtasema tumieni ASDP na kadhalika lakini toeni maelekezo ili kutumia ASDP II mambo haya yaweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine. Hivi Serikali mmeshindwa kutusaidia watu tunaolima zao la minazi kuweza kuondokana na tatizo lile kwa zaidi ya miaka 20 sasa? Kweli mmeshindwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Philipines walipopata tatizo la janga lile la mafuriko na minazi yao ikaondolewa walikimbilia kwa watu wa FAO, walipata fedha dola milioni 35. Leo hii Philipines imerudi kwenye chart yake ya kuwa nchi ya pili kwa uzalishaji wa zao la nazi duniani. Tunaomba mtusaidie tuondokane na umasikini kwa watu wetu. Zao la minazi ndani yake unapata bidhaa karibu 11 lakini zao la minazi ukilienzi maana yake hata mazingira unayatunza. Hebu tujielekeze kwenye eneo hili tuondoe tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nisipolisema nitakuwa sijatenda haki ni kuhusu uvuvi. Nimekuwa nikisema hapa sekta ya ufugaji wa samaki ndiyo sekta inayokua katika ulimwengu kwa kasi kuliko sekta yoyote ndani ya sekta za kilimo. Hapa nimeona taarifa kwamba kwa mwaka jana mazao ya samaki kutokana na ufugaji wa samaki yameongezeka kutoka tani 3,000 mpaka tani 11,000. Nina uhakika hizi ni jitihada binafsi za watu kwa sababu jedwali hili linatuonesha kwamba hatukuwa na fedha za maendeleo kwa mwaka uliopita lakini hii ni sekta ambayo tukiwekeza tunaweza kuvuna zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Kenya miaka sita iliyopita waliwekeza takribani bilioni 35. Mwaka huu wa fedha wametenga bilioni saba kwa sekta ya ufugaji wa samaki peke yake. Jirani zetu Zambia wameanzisha mradi mkubwa, wamewekeza bilioni 112 kwa ajili ya sekta ya ufugaji wa samaki peke yake, halikadhalika Uganda. Hii maana yake nini? Maana yake wenzetu wameiona hii opportunity wanawekeza, sisi hatuwekezi maana yake tutakuwa soko la samaki watakaowazalisha. Nawasihi sana twendeni tukawezeke kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni bandari ya uvuvi. Hivi tunapata kigugumizi gani kwenye jambo hili? Mimi niliwahi kusema hapa hebu tujiongeze…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia kwenye hotuba mbili hizi za Kamati; Kamati ya Miundombinu lakini vilevile Kamati ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa ya Kamati ya Miundombinu imesisitiza umuhimu wa kuimarisha barabara zetu. Katika ule ukurasa wa 37, anazungumzia umuhimu wa kuunganisha makao makuu ya mikoa kwa mikoa. Vilevile katika ukurasa wa 38, naomba kunukuu kipengele (d), anasema, kuendelea na ujenzi wa barabara za lami hasa maeneo yanayochochea uchumi wa Taifa letu kama vile maeneo yenye vivutio vya utalii, kilimo, viwanda na madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili, napenda niikumbushe Serikali, imekuwa ikitoa ahadi nyingi kwa barabara za namna hii hasa katika Mkoa wa Tanga na upande kwa Kilimanjaro. Ipo barabara inayounganisha Mkoa wa Tanga na Kilimanjaro lakini ni barabara ya kimkakati maana inapita kwenye maeneo muhimu ya ukuzaji wa uchumi, utalii na viwanda. Ni barabara kutoka Tanga – Mabokweni – Maramba - Mtoni Bombo - Mlalo - Same.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili kwanza linagusa usalama wa nchi yetu, maana ni eneo la mpakani lakini vilevile kiutalii ni eneo ambalo ukitokea ukanda wa Tanga mpaka kule Same unazungumzia kuunganisha utalii kutoka Mombasa, Saadani na Mbunga ya Mkomazi ambayo inaanzia upande wa Mkinga inakuja mpaka Mlalo, inakuja mpaka Same tunaelekea Kilimanjaro na maeneo ya namna hiyo.

Kwa hiyo, rai yangu, barabara hii imekuwa ikipewa ahadi kwa muda mrefu, ni wakati sasa upembuzi yakinifu ufanyike barabara hii iwekewe utaratibu wa kuwekewa lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoka kwenye taarifa ya Kamati hiyo, sasa nizungumzie taarifa ya Kamati ya Nishati. Nataka niipongeze Serikali kwa kazi kubwa inayofanya kwa kupeleka umeme vijijini kupitia mradi wa REA. Tulipoanza na REA I tulifanya makosa lakini ilikuwa ni sawasawa tufanye makosa kwa sababu tulikuwa tunajifunza. Tumekwenda REA II hali kadhalika tumefanya makosa, yapo tuliyorekebisha lakini bado kuna makosa tumefanya katika usimamizi wa miradi ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumeingia REA III, hatuna nafasi ya kufanya makosa kwa sababu tulishapata fursa ya kufanya majaribio na ku-test jinsi yakwenda. Tunakwenda kwenye REA III tumekubaliana kwamba kila kijiji kitakachoguswa tuhakikishe hakuna kitongoji kinaachwa. Naisihi sana Serikali tusije tukarudia makosa ya REA I na REA II ya kuacha baadhi ya vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu zipo changamoto tumeanza kuziona. Kule Jimboni kwangu kwenye maeneo ya Kidiboni, Kitongoji cha Chakachani kimesahaulika. Ninayo ahadi kwamba kitafanyiwa kazi naiomba Serikali ilikumbuke hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipofanya REA I tuliacha baadhi ya sekondari, Sekondari za Reanzoni, Duga na Kigongoi. Tunapokwenda sasa kwenye REA III kwa sababu sekondari hizi zipo jirani na maeneo haya basi tuhakikishe tunaziingiza kwenye mpango ili ziweze kupatiwa umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nataka kuzungumzia deni la TANESCO. Ukienda ukurasa wa 23, Kamati inasema, madeni ya TANESCO yanasababisha kuzorota kwa utendaji wa shirika. Aidha, madeni yameendelea kuongezeka na hakuna jitihada zozote za Serikali za kusaidia kumalizika madeni haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii siyo hali nzuri, TANESCO ina madeni makubwa. Ukienda kwenye ukurasa ule inaonesha kwamba deni la TANESCO limefikia bilioni 913 na katika hizo takribani bilioni 200 ni madeni yanayotokana na taasisi za Serikali. Naisihi sana Serikali ije na mkakati maalum wa kuhakikisha deni hili la TANESCO linalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kamati tuliwahi kuletewa taarifa kwamba Serikali ina mpango wa kukopa fedha Benki ya Dunia ili tulipe madeni haya. Naisihi sana Serikali yangu isiende kukopa Benki ya Dunia ili tulipe madeni haya, tutafute njia nyingine za kulipa madeni haya. Wenzetu Afrika Kusini wana mzigo mkubwa sana kutokana na ESKOM inashindwa sasa kufanya kazi, inakuwa mzigo hata kwa nchi zinazopata umeme kutokana na Shirika la Umeme la South Africa. Tusije tukaingia kwenye mtego huo wa kusababisha tukapata umeme kutoka Afrika Kusini ambao bei yake ni ghali. Tuisaidie TANESCO iweze kutupatia umeme kwa bei ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba tujifunze kwa wenzetu wa Ghana. Wenzetu Ghana waliamua kuanzisha energy bond na katika kufanya hivyo wameweza kukusanya dola milioni 750 ambazo zinaelekezwa katika sekta ya umeme. Kama tunataka kuisaidia TANESCO tuangalie option hii, tujifunze wenzetu walifanya nini, tuone kama tunaweza kuleta energy bond, wananchi wanunue bond hizo na tuweze kusaidia Shirika letu la TANESCO liondokane na mzigo wa madeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nataka kuipongeza sana Serikali kwa uamuzi wake thabiti wa kuamua kuja na Mradi wa Umeme wa Mto Rufiji, ni hatua kubwa ya kimapinduzi, tumechelewa. Wenzetu Ethiopia wameamua kuwa energy hub saa hizi wanazungumzia kuzalisha megawatt 10,000 kutokana na chanzo cha Mto Nile. Sisi tutumie mto huu vizuri kuwekeza ili tuweze kupata umeme wa uhakika ili ndoto yetu ya kuwa na uchumi wa viwanda iweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu tuko katika hatua za mwanzo ambazo utekelezaji utaanza hivi karibuni. Naipongeza Serikali kwa kuanza utekelezaji huu kwa kutumia bajeti za Wizara mbalimbali ili hatua za mwanzo ziweze kutekelezwa. Rai yangu, Bunge hili lishirikishwe ipasavyo, Wabunge wa Bunge hili wapate semina ya nguvu ili kujenga uelewa wa pamoja ili tutakapokuja kuleta bajeti ya mradi huu iweze kupita kwa urahisi tukiwa kitu kimoja, tukiwa tunaelewana kwamba jambo hili ni jambo la kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia kwenye mjadala uliopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema na baraka zake ambazo siku zote zimetuwezesha kuwatumikia Watanzania vyema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazochukua katika kuhakikisha maisha ya watu wetu yanaendelea kuboreka siku hadi siku. Tumekuwa na mjadala mrefu juu ya mambo ya makinikia lakini taarifa za hivi punde zinaonesha kwamba tunaelekea kwenye right direction, hongera sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 nilipochangia nilikuwa bitter, nilitumia lugha kali kwa Wizara hii na nilikuwa na sababu ya kufanya hivyo. Nilifanya hivyo kwa sababu Kamati ya Bajeti walikuja hapa wakalalamika kwamba Wizara hii imekuwa na shingo ngumu, ilikuwa haisikilizi ushauri inayopewa na Kamati. Nafurahi mwaka huu mambo yamebadilika. Wizara imekuwa sikivu, hongereni sana. Huo ni mwanzo mzuri, tuendelee kuwa wasikivu, maana wote tunajenga nchi hii kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa mapendekezo ambayo watu wengi humu tumekuwa tukipigia kelele ni kuongeza tozo ya mafuta ili twende kupata huduma za maji vijijini. Serikali imesikia hilo, imeongeza tozo kwenye mafuta. Wenzetu wa Kamati ya Bajeti wanashauri kwamba fedha yote itakayopatikana na ongezeko hili, asilimia 70 tuipeleke kwenye maji vijijini, asilimia 30 iende kwenye maji mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunapiga kelele kuhusu maji vijijini? Kwa nini tunapiga kelele kuhusu huduma ya maji? Takwimu za Wizara ya Maji zinaonesha kwamba tumepeleka maji vijijini kwa asilimia 72 peke yake. Hii maana yake nini? Maana yake ni kwamba takriban Watanzania zaidi ya milioni 10 vijijini hawana maji. Hatuwezi kuiacha hali iendelee kuwa hivi. Lazima tuongeze nguvu kuhakikisha tunapeleka maji vijijini. Ndiyo maana naipongeza Serikali kwa kuwa sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zimekuwepo hisia za hofu kwamba pengine uamuzi huu wa kuweka tozo umekuwa ni blanket, utagusa kila aina ya mafuta. Naiomba Serikali itakapokuja kuhitimisha hapa, itueleze tozo ile imewekwa kwa mafuta ya aina gani? Vilevile, Wizara itakapokuja kuhitimisha hoja ituambie ina mkakati gani wa kuhakikisha tunafuta Railway Development Levy kwa mafuta ya ndege? Kwa sababu jambo hili limetusababishia kukosa biashara ya kuuza mafuta ya ndege kwa sababu kampuni za ndege zinajaza mafuta Kenya kwa sababu wenzetu hawakuweka levy hii. Kwa hiyo, naomba wakija watupe ufafanuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipochangia Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji nilisema mchawi wetu wa Tanga ni Wizara ya Fedha na Mipango. Nilisema hivyo specifically kwa sababu ya Kiwanda cha Tanga Fresh. Tunaingiza maziwa ya dola milioni 40; tuna uzalishaji wa maziwa hapa nchini lita bilioni mbili; lakini usindikaji tunasindika only 1.4 percent. Hii haiwezi kuwa sawa. Tanga Fresh kwa miaka miwili sasa wanahangaika kutaka kuongeza uwezo wa kiwanda chao wanazuiwa na TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanazuiwa na TRA kutumia majengo yao kama dhamana ya kukopea. Kwa sababu gani? Kwa sababu aliyewauzia majengo Tanga Fresh, alikwepa kodi. Mkwepaji kodi huyu anajulikana, anafanya biashara katika nchi hii. TRA wanaacha kwenda kumkamata mkwepa kodi, wanamuadhibu Tanga Fresh. Hii haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanga Fresh wamemwandikia barua Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji; Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji ameandika barua tangu mwanzoni mwa mwezi wa Tatu kuja Wizara ya Fedha na Mipango. Mpaka leo hatuna jibu. Nataka mtakapokuja kuhitimisha mtuambie, nini hatma ya Kiwanda cha Tanga Fresh? Kwa nini wanawaadhibu Tanga Fresh kwa kosa ambalo siyo la kwao? Kwa nini uzembe wa wafanyakazi wao usababishe Tanga Fresh wakose haki yao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, naipongeza Serikali kwa jitihada inazofanya za kuhakikisha suala la lishe linapewa kipaumbele. Tuna watoto milioni 2.7 waliodumaa; tuna watoto 600,000 wenye utapiamlo; hii ni hatari kwa Taifa letu. Naipongeze Serikali kwamba kwa mwaka huu wameonesha commitment ya kutenga shilingi bilioni 11.4 zipelekwe kwenye Halmashauri zetu. Rai yangu ni kwamba tuhakikishe fedha hizi zinakwenda kwa wakati. Ziende zikaondoe baa hili. Pili, mtakapopeleka fedha hizi, mpeleke maagizo maalum kwamba huko kwenye Halmashauri fedha hizi zisibadilishiwe matumizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie sula la huduma za kifedha. Tunayo Taasisi inaitwa SELF Microfinance. Mwaka 2016 walipanga kutoa mikopo ya shilingi bilioni 12, lakini wakatoa shilingi bilioni tisa; mwaka huu 2017, wamepanga kutoa shilingi bilioni 20. Naipongeza sana taasisi hii kwa kazi kubwa inayofanya. Wakati nikiipongeza Serikali, hebu fanyeni mambo pale. Mmeondoa Bodi, haipo in place, wanashindwa kutoa mikopo kwa sababu bodi haipo. Harakisheni mhakikishe bodi inakuwa in place ili SELF iweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni shilingi milioni 50 za kila kijiji. Fedha hizi hebu tuziwekee utaratibu maalum. Tumeshasema hapa kwamba njia nzuri ya fedha hizi kwenda kwa wananchi hebu tuhakikishe mfumo wa benki za jamii (Community Banks) unaimarishwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami nichangie kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa wingi wa baraka zake ambazo amezidi kutukirimia siku hadi siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza na kumshukuru sana Naibu Waziri, ndugu yangu Mheshimiwa Kwandikwa kwa ziara aliyoifanya kule Mkinga. Nashukuru sana kwa sababu ziara ile ilijenga matumaini kwa watu wa Maramba, Gombero, Mtonibombo, Daluni, wakijua kilio chao cha muda mrefu sasa kimepata jibu, lakini nimepitia vitabu hivi, bahati mbaya sana kilio chao hakijasikika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Mabokweni – Maramba – Bombomtoni – Umba – Kisiwani – Same - Mkomazi ni barabara ya kuunganisha Mkoa wa Tanga na Kilimanjaro, ni barabara ya kimkakati, kiuchumi na ni barabara ya ulinzi. Ni barabara ambayo wagombea wetu wote wa urais kila wakati wa kuomba kura wamekuwa wakiipitia barabara hiyo, ni barabara ambayo imepewa ahadi mara nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawa wamekuwa na subira sana kwa barabara hii lakini barabara hii ni kero na imekuwa mateso kwao. Nilikuwa nasoma kitabu hiki nikadhani angalau safari hii tutaona neno feasibility study inafanyika kwa barabara ile lakini hakuna. Ni barabara ambayo nimeisemea sasa kwa miaka saba mfululizo, lakini Serikali haisikii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii mzee wangu Mheshimiwa Kikwete alipopita aliposikia kelele hizi akasema tuiweke kwenye utaratibu wa Performance-Based Management and Maintenance ili angalau iwe inapitika, tukafanya hivyo. Baadaye tukasema iingizwe kwenye mpango maalum kupitia MCC, namshukuru sana dada yangu aliyekuwa Mkuu wa Mkoa, dada Chiku Galawa akapambana tukaleta maombi barabara hii itengenezwe kupitia MCC, lakini haikuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alipokuja kwenye kuomba kura ndugu zetu wa Maramba wakaomba, akasema amesikia. Alipofika Daluni Kibaoni pale wananchi wakamlilia, akatoa ahadi. Tumeisemea barabara hii lakini kwa masikitiko makubwa kilio chetu hakijasikika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kweli barabara inayounganisha Mbuga ya Saadani na Mbuga ya Mkomazi hatuioni umuhimu wake? Hivi kweli barabara inayounganisha Mbuga ya Tsavo na Mbuga ya Mkomazi na Kilimanjaro hatuioni umuhimu wake? Hivi kweli tunashindwa kukamata kundi la watalii kutoka Mombasa ili waje kutembelea eneo la Mto Umba na Mbuga ya Saadani mpaka Kilimanjaro hatuoni umuhimu wake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi barabara inayotupa uhakika wa usalama wa nchi yetu kiulinzi hatuoni umuhimu wake? Hivi barabara inayopita kwenye maeneo ya uzalishaji wa kahawa, chai, mpunga, mkonge hatuoni umuhimu wake? Barabara hii haituweki vizuri kisiasa. Mheshimiwa Waziri alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama chetu, ninaposema barabara hii haituweki vizuri kisiasa, najua anaelewa. Naomba kilio hiki kisikike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni bandari. Pale Mkinga tuna wawekezaji wa Hengya Cement na kampuni ya Sinoma wameamua kuja kuwekeza pale watajenga viwanda kumi. Miongoni mwa viwanda hivyo kutakuwa na kiwanda kimoja cha cement chenye uwezo wa kuzalisha tani milioni saba kwa mwaka. Maana yake unazungumzia kiwanda ambacho production inayofanyika sasa nchini inakuja kufanywa na kiwanda kimoja. Tunazungumzia uwekezaji wa trilioni 7.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameomba pamoja na uwekezaji huo, wapewe ruhusa wajenge gati itakayowawezesha kusafirisha mizigo yao wenyewe. Wanataka kujenga gati ile kwa utaratibu Build Operate and Transfer watumie fedha zao wenyewe. Sasa huko bandarini kuna mtu nasikia ameweka ngumu hataki kutoa kibali. Uwekezaji wa trilioni saba kuna mtu mmoja anakwamisha, hatuwezi kukubali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisipopata majibu ya kuridhisha nakusudia kushika shilingi. Waheshimiwa Wabunge, naomba kwenye hili mniunge mkono. Hatuwezi kuacha uwekezaji mkubwa wa trilioni saba uzuiwe na mtu mmoja. Hatuwezi kukubali ajira ya watu 4,000 izuiwe na mtu mmoja eti ana ndoto ya kutujengea bandari ya Tanga iwe na uwezo wa kuwa valid kwa miaka 200 ijayo, lakini wakati akisema hayo sisi tunazo taarifa watu wa Tanga kwamba tangu mwaka 77 kwenye business plan ya Mamlaka ya Bandari imekuwa ikisema itajenga Bandari ya Mwambani haijatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna mtu ana hela zake anataka ajenge gati ili uwekezaji mkubwa wa namna hii utokee sisi tunaweka ngumu, haiwezekani. Wakati tunaweka ngumu hii ya kuruhusu kujenga gati pale Pangani Mamlaka hiihii ya Bandari imejenga gati, kwa nini Pangani tujenge gati lakini Mkinga iwe nongwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaunga mkono hoja nikipata majibu ya uhakika. Nashukuru.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye hoja zilizoko mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye kwa rehema zake ametuwezesha tumeendelea kuwa wazima na kuwa na afya njema ya kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuchangia kwenye eneo moja ambalo nisipolichangia nitakuwa sijajitendea haki. Hali yetu ya lishe nchini siyo nzuri. Katika bajeti ya mwaka jana, kwenye fedha tulizotenga ziende kwenye halmashauri zetu ilikuwa ni shilingi bilioni 11 lakini tulipeleka asilimia 8 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema haya kwa sababu nataka kama Taifa tulione jambo hili ni tatizo. Takwimu zinatuambia nini juu ya hali yetu? Takwimu zinatuambia kwamba asilimia 34 ya watoto wetu walioko chini ya miaka mitano wamedumaa. Takwimu zinatuambia asilimia 58 ya akina mama waliko kwenye kipindi cha kuweza kuzaa wana upungufu mkubwa wa damu. Hii ndiyo hali ya Taifa letu kwamba tuna changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande mwingine wakati tuna lishe duni lakini tuna tatizo lingine la lishe iliyopitiliza, viriba tumbo. Ttizo hili linatuletea sasa magonjwa yasiyoambukiza mfano BP, kisukari na kadhalika. Kwa hiyo, tuna matatizo ya aina mbili kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Rais wa Benki ya Afrika anatuambiaje? Anasema stunted children today means stunted economy tomorrow. Tukiwa na watoto ambao hali yao ni mbaya leo basi tusitegemee kuwa na uchumi mzuri siku zijazo. Ukiangalia hali ya uchumi takwimu zile zinaonyesha kwamba uchumi wetu unakua lakini kwa taarifa hizi maana yake tunakoelekea ni kubaya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mpango mwaka huu hakikisha fedha hizi tulizotenga kwa ajili ya kupambana na tatizo la utapiamlo tunazipeleka zikafanye kazi. Maana wataalam wa economics wanatuambia stunted children today means stunted economy tomorrow. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye eneo lingine, naipongeza Serikali nimeanza kuona jitihada za kuzigeuza halmashauri zetu kuwa ni center za investment, ni jambo nzuri. Nasema ni jambo nzuri kwa sababu tumeanza kuona trend ya kuzinyang’anya vyanzo vyake vya mapato lakini sasa tunapoziwezesha kuwa na vyanzo vingine mbadala vya kupata mapato hili ni jambo nzuri. Maana tumeanza kushuhudia kupitia TAMISEMI tunashawishi halmashauri zianzishe miradi, vituo vya maegesho, standi za magari na mabasi, masoko na kadhalika. Yawezekana ni jambo nzuri lakini uwekezaji huu usipogusa maisha ya mtu wa chini, mtu wa kawaida yatakuwa hayana faida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ndipo napokuja kwenye lile jambo mahsusi la sisi watu wa Pwani. Tafiti zinaonyesha kwamba we have unattempted potential kwenye bahari na maziwa yetu. Mheshimiwa Dkt. Mpango Tanzania tuna Ukanda wa Pwani kilometa 1,424, tuna EEZ kilomita 220,000 lakini kwenye eneo la maziwa na mito tuna takribani kilomita 64,500 lakini tunatumiaje rasilimali hii. Uzalishaji wetu wa samaki ukoje? Takwimu zinaonyesha kwenye mpango kwamba kwa takribani miaka mingapi hii, tumekuwa tukivua kati ya tani 325,000 na 380,000. Katika hizo, asilimia 85 uvuvi huu umefanyika kwenye maziwa, asilimia 14 tu ndiyo umefanyika kwenye eneo la bahari. Mbaya zaidi, ufugaji wa samaki kwenye nchi hii, katika hizo tani 380,000 its only one percent, hii haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii ambayo ina potential kubwa namna hii, inachangia ajira asilimia 0.7, haikubaliki. Ukisikiliza taarifa ya Kamati wanasema kwamba tuna tatizo kwenye ajira, tuna tatizo kwenye kuagiza zaidi bidhaa kutoka nje kuliko tunavyoweza kuuza nje, lazima tuwekeze.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwaige wenzetu South Africa, wao kwenye kutatua jambo hili la ufugaji wa samaki, walichofanya wameanzisha Aquaculture Investment Zone. Wanachofanya wanaenda kuanzisha zone maalum kwenye maeneo fulani fulani, kule Eastern Cape, wanazo hizi karibu saba na maeneo haya yameweza kuzalisha ajira karibu 150,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uzalishaji kwenye eneo hili leo hii wanazungumzia mapato yanayotokana na sekta ya ufugaji wa samaki ya shilingi bilioni 115, sisi hatuzitaki hizi? Wenyewe wamejipanga ndani ya miaka miwili ijayo waweze kufikia mapato yanayotokana na ufugaji wa samaki yanayofikia shilingi bilioni mita tano, sisi hatuzitaki hizi? Mheshimiwa Dkt. Mpango tusaidieni watu wa Ukanda wa Pwani, hizi jitihada mnazotuambia tuanzishe standi za mabasi, masoko, tuwezesheni sisi kwenye ufugaji wa samaki kuanzisha Aquaculture Special Economic Zone, tuweze kupiga bao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine, Bunge hili liliridhia tuingie kwenye matumizi ya sarafu moja kwa Ukanda wote huu wa Afrika Masharika. Sijaona kwenye bajeti hii tumeelezwa vipi. Nafikiri ni vizuri kila tunavyokwenda tuwe tunapeana taarifa kwamba maandalizi ya kuelekea huko tumefikia wapi tukijipima na wenzetu. Vilevile tuelezane vihatarishi tunavyoviona, maana taarifa zilizopo wenzetu Kenya wameshafikia ukomo wa kukopa nje. Kila wanavyokopa wamekuwa wakiambiana kwamba deni linahimilika, hii iwe changamoto kwetu kwamba tukope vizuri tusifike huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye eneo la umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye hoja zilizoko mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amezidi kutupa baraka zake na hatimaye tunaweza kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza kwenye mambo matatu. Nitajielekeza kwenye suala la elimu, afya na lishe. Nitumie fursa hii kuishukuru sana Serikali kwa kutupatia fedha za kujenga mabweni na madarasa kwa Sekondari zetu mbili za Maramba na Mkinga ambazo zimekuwa high school, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo bado sekondari hizi ambazo zimekuwa high school zina changamoto nyingi kwani kuna uhaba mkubwa wa nyumba za Walimu. Sekondari ya Mkingaleo hakuna nyumba za Walimu na high school ile inachukua wasichana, kwa hiyo, unaweza kuona hatari iliyopo. Nawasihi sana Serikali tuchukue hatua za haraka kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Sekondari ya Maramba, sekondari ile tulipoianzisha tulichukua majengo ya yaliyokuwa mashamba ya mkonge. Kwa hiyo, nyumba wanazotumia Walimu ni nyumba zile za wafanyakazi wa mkonge, za chini kabisa. Kwa hiyo, unaweza kuona picha Walimu wetu tunawaweka katika mazingira gani. Nawasihi sana, tumezipandisha hadhi shule hizi, basi tuziboreshe na kuzipa hadhi inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile shule hizi zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa Walimu, taarifa tumekwishapeleka naomba waziangalie. Pia shule hizi zinakabiliwa na tatizo la maji, naomba waangalie. Wingi ule wa wanafunzi katika shule zile halafu shule hazina maji ni changamoto kubwa kwelikweli. Vilevile lipo lingine, shule hizi hazina usafiri, tumewaweka vijana wetu pale, lakini shule hizi hazina usafiri ni changamoto kubwa kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunayo madai ya Walimu. Tuna Walimu takribani 271 wanadai madai mbalimbali, ukiacha mishahara, wanadai takribani shilingi milioni 312. Hata orodha ile ya malipo ilipotoka kwa Wilaya ya Mkinga walikuwa ni wafanyakazi wawili tu, naomba waliangalie vizuri jambo hili, halitupi hali nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ndugu yangu Mheshimiwa Waziri atakumbuka niliwahi kuja na timu ya Madiwani kutoka Mkinga, wanastahili posho zao baada ya kumaliza muhula uliopita wa Bunge. Mpaka leo madai yao bado hayajatimia, naomba tuwalipe fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni kwenye afya. Hapa naomba vilevile niipongeze na niishukuru sana Serikali, imetupatia shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga kituo cha afya. Kituo kile kimekamilika, tunaomba zile shilingi milioni 200 zilizobaki ili kufika shilingi milioni 700 kwa ajili ya vifaa tiba, naomba watupatie ili tuweze kukamilisha kituo kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado ombi langu liko palepale la kuhakikisha Wilaya ya Mkinga tunapatiwa fedha za kujenga hospitali ya wilaya. Wilaya ile tuna kata 22, sasa hivi tuna vituo vya afya vitatu. Kwa hiyo, unaweza kupata picha kwa wilaya yenye kata 22, haina hospitali ya wilaya ina vituo vya afya vitatu, unaweza kujua ukubwa wa tatizo ni kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikilisema hili muda mrefu, naomba ifike mahali sasa Serikali isikie. Tunawashukuru World Vision kwa kutusaidia kujenga jengo la kisasa la upasuaji katika Kituo cha Afya cha Mkingaleo, tunaomba na wahisani wengine waige mfano huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna upungufu mkubwa kwenye sekta ya afya, tuna mahitaji ya watumishi 395 waliopo ni 183, tuna uhaba wa karibu asilimia 58 ya watumishi. Maombi haya tumekwishayapeleka muda mrefu, tunaomba wayafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nihamie kwenye lishe. Hapa nataka ku-declare interest kwamba mimi ni Mwenyekiti wa Kikundi cha Ma-champion wa Lishe katika Bunge letu. Niishukuru Serikali juzi imetoa commitment ya kutoa semina kwa Wabunge wote juu ya tatizo tulilonalo la lishe katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwamba kwa ukubwa wa tatizo tulilonalo katika nchi yetu ingekuwa busara sana kama Wabunge wote mngeona umuhimu wa kujiunga na kikundi hiki cha lishe. Mwaka jana tulifanya jambo kubwa, tulipitisha hapa shilingi bilioni 11 ziende kwenye halmashauri kwa ajili ya kutatua tatizo la lishe. Lilikuwa ni jambo kubwa kweli kweli lakini cha kushangaza na imenisikitisha kidogo kwamba nimeisikia hotuba ya Waziri Mkuu sikusikia chochote kuhusu lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeisikiliza hotuba ya ndugu yangu Mheshimiwa Jafo hakuna sehemu imetajwa lishe. Ndugu zangu tuna tatizo kubwa kwenye lishe, wala
tusimumunye maneno, tuna tatizo kubwa. Haiwezekani kwamba takribani asilimia 45 ya vifo vya watoto katika nchi hii vinahusishwa na utapiamlo, haiwezekani asilimia 57 ya watoto katika nchi hii wana upungufu wa damu, haiwezekani asilimia 34 ya watoto wetu wamekuwa stunt halafu hotuba zetuhazigusii jambo hili, si sahihi, si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jafo yeye alikuwa miongoni mwa Wabunge tulioanzisha kikundi cha lishe, najua passion yake kwenye jambo hili, Waziri wa Fedha najua passion aliyonayo kwenye jambo hili, hebu tuchukue hatua. Taarifa zilizopo ni kwamba katika shilingi bilioni 11 tulizoidhinisha it’s only eight percent ya fedha hizo ndiyo zimekwenda. Taarifa hii ni ya mwezi wa Pili. Katika shilingi bilioni 11 tumepeleka shilingi milioni 888, hii haiwezi kuwa sawa. Nawasihi sana tuchukue hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua changamoto tuliyonayo ni kwa sababu fedha hizi tunazipitishia kwenye Health Basket Fund, fedha hizi tunataka zitoke kwenye own source, fedha hizi tunataka zitoke kwenye OC. Njia hii haitatufikisha, tuangalie uwezekano wa kutumia njia ya ku- ring-fence fedha hizi, kuzi-page kwenye GDP asilimia fulani ili tuhakikishe fedha hizi zinakwenda moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitumia bajeti za halmashauri kule tukategemea tutaenda kutatua tatizo kubwa kama hili tunajidanganya. Tumekubaliana kwenye vision 2020-2025 kwamba tutaweka kipaumbele kwenye kuboresha human capital na productivity haya hayawezi kupatikana kama hatutahakikisha tunaondokana na tatizo la lishe duni na lishe iliyopitiliza.

T A A R I F A . . .

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa lakini hali ni mbaya zaidi ya hapo. Tathmini inaonesha kwamba kama hali ikiendelea hivi ikifika mwaka 2025 Taifa litakuwa limepoteza nguvukazi ya shilingi trilioni 28.8, this is very serious. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri atakapokuwa anahitimisha taarifa yake atueleze, tulikubaliana kwamba tutaajiri Maafisa Lishe 600, nini kimetokea mpaka sasa hatujaweza kuajiri? Vilevile mpaka kufikia kipindi hiki ni fedha kiasi gani tunazipeleka kwenye lishe? Nawasihi sana tunapofanya mabadiliko ya miundo katika Wizara tujitahidi Kitengo cha Lishe kisije kikamezwa tukahatarisha jitihada hizi tulizozianza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi nitoe mchango wangu kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ametupa uhai na tunaweza kuwatumikia Watanzania. Namuomba anipe uwezo wa kuchangia vyema, nichangie nikiwa sober katika suala hili muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa ziara yake aliyoifanya Jimboni kwangu Mkinga, kuja kujionea mwenyewe changamoto kubwa ya maji katika Wilaya ya Mkinga. Ulijionea mwenyewe kwamba Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga hatuna maji, lakini uliona vilevile miradi inayoendelea na changamoto zake. Mheshimiwa Waziri nikukumbushe tu ziko hati tatu mezani kwako, Hati ya Mradi wa Doda shilingi milioni 166, hati ya Mradi wa Bwagamacho shilingi milioni 54, Hati ya Mradi wa Mbuta shilingi milioni 227. Tunaomba fedha hizi zilipwe ili kazi ya miradi ya vijijini iendelee. Mheshimiwa Waziri utakumbuka pale Parungu Kasero ulipokuja tulikumbana na changamoto ya kupeleka umeme mwezi wa 11 ulipokuja ukaahidi kutoa shilingi milioni 49 fedha zile hazijafika, tunaomba sana utusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mara kadhaa tumesikia kwamba maji ni uhai, tumekua tukisikia kauli hiyo kwamba maji ni uhai lakini kitabu hiki cha Mheshimiwa Waziri kinatuambia takribani asilimia 41 ya wananchi wakioko vijijini hawapati maji, maana yake hakuna uhai.

Mheshimiwa Spika, Umoja wa Mataifa mwaka 2010 kwa kutambua changamoto hii ikasema maji safi na salama ni haki ya msingi kwa maisha ya binadamu na kwamba ikifika mwaka 2015 tuwe tumetatua tatizo la maji vijijini kwa asilimia 50. Sasa ukiangalia Human Development Report ya recent na ukiangalia machapisho ya wenzentu wa ESRF wanatuambia nguvu yetu kwenda kutatua tatizo la maji inakwenda taratibu mno. Kutoka asilimia 45 mwaka 2004/2005 mpaka leo tunazungumzia asilimia 58 tunakwenda taratibu mno. Wakati hali ikiwa hivyo, leo hii tunazungumzia cases 5,800 za kipindupindu zinaripotiwa kila mwaka nchini. Wakati hali ikiwa hivyo tunapoteza vijana wetu wa chini ya miaka mitano vinapatikana vifo vya watoto 18,500 na katika hao asilimia 90 vinasababishwa na kukosekana kwa maji safi na salama. Kama Taifa tutaendelea kuiachia hali hii mpaka lini? Mpaka lini tutakubali kupoteza nguvu kazi hii.

Mheshimiwa Spika, takwimu hizi zinaonesha kwamba kila mwaka kwa kutopeleka maji safi na salama tunapoteza bilioni 301mpaka lini kama Taifa tutakubali udhaifu huu. Nimesoma ripoti ya Kamati wanasema tumepeleka kwa asilimia 22 tu za fedha zile. Kwenye umwagiliaji ndiyo usiseme, hapa tunasema kilimo kitukwamue kutoka kwenye umaskini wetu, kilimo cha kisasa cha umwagiliaji hatupeleki fedha, tunakusudia nini. Nawasihi sana tupeleke fedha hizi.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana nilisema hapa kwamba tulipoamua kupeleka umeme vijijini tulipoamua kuweka tozo Serikali walikuwa wagumu kukubali tozo ile lakini leo hii tozo ile ndiyo inatusaidia kupeleka umeme vijijini. Nikashauri hapa mwaka jana kwamba hii tozo inayopigiwa kelele na Wabunge kwenye mfuko wa maji tuiongeze tufikie shilingi 100; hatukuongeza. Lakini leo kinachotuondoa aibu ni Mfuko wa Maji kupitia tozo ile. Nawaomba sana Serikali muwe wasikivu tunaposhauri mambo haya tuongeze tozo lile ili twende tukaondoe tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado narudia kusema Makao Makuu ya Mkinga hatuna maji nimeona kwenye vitabu mmetupangia shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuanza usanifu kwa Miji kama mitano hivi ya Mkoa wa Tanga. Nawashukuru kwa gesture hii, lakini nikumbushe tu mwaka jana mlifanya hivi na fedha hazikwenda. Tunaomba safari hii fedha hizi zitoke ili usanifu ule uweze kufanyika.

Mheshimiwa Spika, nimeona mmetupangia shilingi milioni 500 pale Horohoro lakini mkumbuke wakati mkitupa shilingi milioni 500 mradi ule wa kupeleka maji Horohoro lakini mkumbuke wakati mkitupa shilingi milioni 500 mradi ule wa kupeleka maji Horohoro unazungumzia bilioni sita ni mradi unaoenda ku-save kile kituo chetu pale cha one stop boarder center, tuondoleeni aibu ya watu wetu kwenda kuchota maji Kenya. Haipendezi sana kila siku tukisema maneno haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi ule wa kupeleka maji kutoka Mto Zigi ni muhimu sana. Ni mradi ambao utatusaidia kupeleka maji kwenye viwanda vile 10 ambavyo tunakusudia kuvijenga, uwekezaji wa trilioni 7.6 hautaweza kufanikiwa kama hatutapeleka maji kwenye eneo lile, tunawasihi sana muone umuhimu wa kupeleka maji kwenye eneo lile.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami nichangie kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Nataka kuanza kwa kushukuru Chama changu cha Mapinduzi, kwa mara ya kwanza kutambua umuhimu wa barabara ya Mabokweni - Maramba, Mtoni Bombo kuelekea Korongwe halikadhalika kuelekea Umba Junction mpaka Same, kwamba kwa mara ya kwanza barabara hii sasa imeingia kwenye Ilani ya uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, licha ya kuingia kwenye Ilani ya uchaguzi, kwa masikitiko makubwa, bajeti hii imeisahau barabara hii. Barabara hii nimeizungumzia kwa miaka 10 mfululizo tukipewa ahadi barabaraba itajengwa. Tukipewa ahadi kipindi fulani kwamba barabara hii sasa itajengwa kwa kupitia MCC, mpango ule ukayeyuka. Akaja ndugu yangu Mheshimiwa Kwandikwa mwaka 2019 akaahidi kwamba bajeti ijayo tutaiingiza kwenye mpango wa kufanya feasibility study, halikutokea na hata leo halikutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imeahidiwa na Mheshimiwa Benjamini Wiliam Mkapa, Marehemu, haikutokea; barabara hii akaiahidi Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, hakutokea; barabara hii amehiahidi Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli, haipo hata kwenye feasibility study; barabara hii walizungumzia viongozi wetu wa dini wakubwa wa nchi hii; Shehe Mkuu ameizungumzia barabara hii na alipewa ahadi na Mheshimiwa Rais pale Korongwe mwaka 2020, haijatokea; Askofu Mkuu wa Anglikana wa nchi hii ameizungumzia barabara hii, akaahidiwa itajengwa, haijajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mmepuuza maneno ya Kitandula, basi hata ya hawa viongozi mnayapuuza! Hivi mwambiwe na nani ili mwelewe? Sisi watu wa Mkinga tunasikitika sana na jambo hili; na ninataka niweke rekodi sawa hapa, kuna maneno huwa yanasemwa hapa, kwamba watu wa Kaskazini walipendelewa; jamani, Mkinga hatuna barabara, Tanga hatuna barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Mkinga tuna kilometa zisizozidi 25 za lami na hizi zinakwenda kule Horohoro kwenye boarder yetu na Kenya. Hazikwenda kwenye maeneo ya uzalishaji. Hebu tutendeeni haki, njooni mtusaidie kujenga barabara hii ya kutoka Mabokweni – Maramba - Mtoni Bombo - Mashewa kwenda Korongwe, vile vile tuiunganishe na barabara hii ya kwenda Umba Junction mpaka Same. Hivi ni kwa nini kwa upande ule wa Same feasibility study imekamilika, lakini huku kuna kigugumizi? Tunaomba maelezo, Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja hii, atupe maelezo ya kina, vinginevyo hakitaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna barabara iliyoanza kujengwa ya kwenda Makao Makuu ya Wilaya, kichekesho ni kwamba tunajenga mita 200, mita 150; barabara ya kilomita 28 tunajenga mita 200, hivi tutamaliza lini? Naiomba Serikali ifikirie mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuhitimisha hoja yangu. Nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Bunge ambao wamepata fursa ya kuichangia hoja hii na kutoa mchango wa mawazo. Hoja hii imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa Wabunge 27, katika hao Wabunge 25 wamechangia kwa kuzungumza na Waheshimiwa Wabunge wanne wamechangia kwa maandishi. Katika hao wanne waliochangia kwa maandishi lakini vilevile walizungumza, kwa hiyo, tunabaki na Waheshimiwa Wabunge wawili ambao walichangia kwa maandishi. Kwa hiyo jumla ni Waheshimiwa Wabunge 27.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hoja hizi karibu kila Mheshimiwa Mbunge ameunga mkono hoja ya Kamati yetu. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuwashukuru sana kwa kuunga mkono hoja za Kamati hii. Vilevile kwa niaba ya Kamati, nichukue fursa hii kuwashukuru kwa pongezi mlizotoa kwa kazi iliyofanywa na Kamati, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri ambao wamefanya kazi kubwa ya kujibu sehemu kubwa ya hoja zilizokuwa zimetolewa. Zipo hoja ambazo zilikuwa ni nje ya hoja ya Kamati, kwa hiyo, sitarajii kuzijibu lakini tunazichukua kama rejea ya Kamati kwa ajili ya kuzifanyia kazi kwa siku zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitajikata katika maeneo manne yaliyojitokeza kwa upana ambayo Waheshimiwa Wabunge kwa uwingi wao waliyagusia. Eneo ya kwanza ni eneo la REA. Waheshimiwa Wabunge wameonesha kwamba Mradi wa kupeleka Umeme Vijijini ni hitaji la kila Mtanzania na kwamba kama Taifa tuna kila sababu ya kuhakikisha tunafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba tunakamilisha utekelezaji wa miradi hii kwa wakati. Kamati iliainisha changamoto kadhaa ambazo bahati nzuri na Waheshimiwa Wabunge wamezitolea maelezo. Niishukuru Serikali imekubali kufanyia kazi changamoto zote zilizojitokeza upande wa REA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni umeme wa Mto Rufiji. Namshukuru Mheshimiwa Waziri ametoa maelezo ya kina sana katika eneo hili. Mradi huu kama tunavyofahamu utachukua miezi 36 ya utekelezaji. Mradi huu ulitiwa saini Desemba, 2018 na baada ya kutiwa saini miezi sita itakuwa ni kipindi cha mkandarasi kuji-mobilize kabla ya kuanza kuutekeleza mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Kamati tunasema mradi huu ni wetu. Kwa hiyo, kama Taifa kwetu sisi mradi huu ni wa kufa na kupona. Tulipofika sasa siyo sehemu tena ya kuzodoana na kurudishana nyuma, tulikofika sasa ni kusema tunafanya vipi vizuri zaidi ili mradi huu, hiki chetu kiweze kufanikiwa vizuri. Ndiyo maana katika mapendekezo yetu kama Kamati tumeiomba Serikali ihakikishe kwamba tunasimamia vizuri utekelezaji wa mradi huu na kwamba fedha za utekelezaji mradi huu zitolewe kwa wakati ili usiweze kukwama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine linagusa mapendekezo ya wadau wa sekta ya madini. Waheshimiwa Wabunge wengi waliozungumza wameonesha ipo haja kubwa ya kuwawezesha wachimbaji wadogo. Wameonesha nia na matarajio kwamba tukiisimamia vizuri sekta hii basi mchango wake utakuwa mkubwa kwa uchumi wa Taifa letu. Hicho ndicho ambacho sisi katika Kamati tulikiona na ndiyo maana tumependekeza yale mapendekezo yote ya mkutano wa wadau yafanyiwe kazi. Nafurahi kwamba Mheshimiwa Waziri wa sekta husika ameonesha utayari wa kuyafanyia kazi maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo limezungumzwa kwa mapana na kwa hisia tofauti ni mradi wa Songas na mikataba yake. Mazungumzo yalivyoendelea hapa ndani yalijikita zaidi kwenye mradi Songas lakini sisi tuliiangalia sekta nzima ya gesi nchini tukifanya rejea ya Kamati ndogo iliyoundwa na Mheshimiwa Spika ya kuishauri Serikali jinsi Taifa linavyoweza kunufaika na mapato ya gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili tunampongeza sana Mheshimiwa Spika kwa ujasiri na umakini mkubwa alioufanya kwa kuunda Kamati ile. Namshukuru Mungu nilipata fursa ya kupata nafasi ya kuongoza Kamati ile. Ni Kamati iliyokuwa na watu wa makini, ushauri uliotolewa sina hofu na mashaka hata kidogo kwamba ukifanyiwa kazi utatutoa hapa tulipo ili Taifa liweze kunufaika na rasilimali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, rai yetu kama tulivyoonesha kwenye mapendekezo yetu ni kwamba jambo lile lifanyiwe kazi ili tuweze kurekebisha kasoro zilizojitokeza. Nafurahi kusikia kwamba Serikali inasema imeanza kufanyia kazi jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, lipo jambo lilijaribu kusemwa mwanzo hapa kwamba taarifa hii pengine siyo matokeo ya kazi ya Kamati. Napenda niwahakikishie taarifa hii ni matokeo ya mchango wa mawazo ya Kamati. Kamati ilikutana tarehe 24 kujadili rasimu ya kwanza ya taarifa ya Kamati, wakatoa mapendekezo. Kamati ilikutana tarehe 25 kujadili mapendekezo waliokuwa wameyatoa mwanzoni. Kumbukumbu za vikao hivyo ninazo hapa, ukihitaji tutaweza kuziweka Mezani. Ndiyo maana hata mapendekezo yaliyotolewa na wasemaji yalishabihiana moja kwa moja na kile ambacho Kamati ilikipendekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba sasa Bunge lako liridhie na kuidhinisha maoni na mapendekezo ya Kamati ili yawe ni maamuzi ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametuwezesha kuiona siku hii ya leo. Pili, niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara zote zenye hoja hii na kwa bahati nzuri sana wote wamefika Mkinga, wanaifahamu Mkinga, wanajua changamoto za Mkinga, nawapongeza kwa jitihada mnazozifanya za kutusaidia watu wa Mkinga tuweze kupiga hatua, ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuishukuru sana Serikali kwa jitihada ambazo imefanya kuhakikisha kwamba sekta ya afya katika Wilaya yetu inapiga hatua. Mwaka jana tulipata fedha za vituo viwili vya afya takribani Sh.1,100,000,000. Vituo vile vimekamilika na nimepata taarifa tumepata vifaa vya takribani shilingi milioni 300, kwa hiyo, vituo vile vitaanza kufanyakazi haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia bajeti ya mwaka huu unaokuja nimeona kilio chetu kimesikilizwa. Moja ya kilio ambacho nimekuwa nakipigia kelele sana kila mwaka ilikuwa ni ujenzi wa hospitali ya wilaya. Waziri alipokuwa akiniahidi nilikuwa naona kama vile ananidanganya lakini leo nimeona tumetengewa milioni 500 tuanze ujenzi wa hospitali ya wilaya, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba mmeweka benchmark kwenye ujenzi wa hospitali za wilaya, tumezoea tukisikia Sh.1,500,000,000 sasa sisi mmetuanzia na Sh.500,000,000 tunajua hizo bilioni zinafuata. Kwa hiyo, tunaomba muemndele kuweka nguvu ili tuweze kupata fedha hizi. Jambo hili litawasaidia sana watu wa Mkinga lakini litatusaidia vilevile kwenye hospitali yetu ya Mkoa ya Bombo ambayo imekuwa na msongamano mkubwa wa kupata wagonjwa kutoka Mkinga, jambo hili sasa linakwenda kuondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nikipitia hotuba ya Waziri ukurasa wa 32 mpaka 34 nimefarijika kwa sababu mwaka jana kwenye eneo la lishe nilishangaa kwamba hakukuwa na neno lolote kuhusu lishe. Waziri akaniambia ilikuwa ni kupitiwa na kweli kwa sababu mwaka huu naona ameweka page maalum kwa ajili ya lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze dada yangu Mheshimiwa Sakaya amezungumzia jambo hili la lishe. Mimi kama Mwenyekiti wa kikundi cha lishe napokuwa na Wajumbe makini namna hii wanaoweza kuzielezea issue tunazozijadili kwa umahiri nafarijika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tusikilizane kidogo, kama Taifa tuna tatizo kubwa la lishe. Utafiti wa Hali ya Afya Nchini wa mwaka 2015/2016 unatuambia kwamba watoto wetu chini ya miaka mitano asilimia 30 wana udumavu. Hii maana yake ni kwamba watoto milioni 2,700,000 wamedumaa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake nini? Maana yake watoto hawa hawawezi kufundishika vizuri, makuzi yao ni tatizo na fursa huko mbele ya safari za kuijiondoa kwenye umasikini ni giza. Kwa kuwa na watoto hawa ambao wa udumavu maana yake watazalisha vilevile kizazi chenye udumavu, kwa hiyo, hili ni janga kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana Bunge hapa tulipitisha shilingi bilioni 15 kwa ajili ya lishe. Kinachonisikitisha ni kwamba mpaka Desemba, fedha zilizotoka kwa ajili ya jambo hili ni asilimia 40 tu. Takribani Halmashauri 31 zilikuwa hazijatenga fedha kwa ajili ya jambo hili, hii haikubaliki. Najua kazi kubwa mnayoifanya Wizara lakini hebu tuwabane hawa ambao hawaoni kwamba tuna changamoto na tuna janga kubwa kama hili kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Mikoa ambayo utapiamlo ni zaidi ya asilimia 40. Mikoa hiyo ni Dodoma, Ruvuma, Rukwa, Kigoma, Katavi na Geita. Cha kusikitisha katika Mikoa hiyo ni Dodoma peke yake ndiyo ilikuwa imetenga fedha zile na zimetumika, mikoa mingine utumikaji wa fedha zile ni kwa kiasi kidogo sana. Niwaombe Serikali muwabane watendaji katika maeneo haya ili waone umuhimu wa kutenga fedha hizi na kutumika ili tuweze kuondoa tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie elimu. Tunashukuru Serikali kwa kutupatia fedha wka ajili ya ujenzi wa madarasa, mabweni na mabwalo katika shule zetu mbili za Maramba Sekondari na Mkingaleo Sekondari ambazo hivi sasa zinakwenda kuwa za kidato cha tano na cha sita. Mkingaleo tayari imeanza, imani yangu ni kwamba tukikamilisha kutoa fedha za haraka, Maramba Sekondari nayo mwaka huu inaweza kupokea vijana wa kidato cha tano na cha sita. Nawasihi sana tupeleke fedha hizi ili tumalizie ile kazi ndogo iliyobaki pale ili Maramba Sekondari na yenyewe iweze kupokea vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto ya maboma kwenye shule zetu. Tuna maboma karibu 40 ya shule za msingi lakini hatujapata fedha. Tuna upungufu wa walimu ambapo mahitaji yetu ni walimu 883 waliopo ni 481, karibu asilimia 50 upungufu, naomba tulitupie macho jambo hili. Hata kwenye sekondari walimu wa sayansi tuna upungufu karibu walimu 60, walimu 38 kwenye masomo ya baiolojia, fizikia na chemistry lakini walimu 22 kwenye somo la hisabati, tunaomba mtuangalie kwa jicho pekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini maombi mahsusi, shule yetu ya Kigongoi wiki mbili zilizopita tumepata balaa, madarasa matatu yameezuliwa na upepo. Tunaomba jitihada za haraka zifanyike ili tuweze kupata fedha za kurejesha madarasa yale kwenye hali yake ya kawaida ili wanafunzi wasipate shida ambayo inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilizungumzia Shule yetu ya Lanzoni kwamba shule ile ya sekondari hatuna maji. Watoto wanalazimika kwenda kuchota maji mtoni, mto ule umejaa mamba. Hebu tuwaondolee balaa hili ili watoto wale wasije wakajeruhiwa au wakauawa na mamba. Tunahitaji fedha pale karibu shilingi milioni nane ili tuweze kupeleka maji kwenye shule ile, tusaidieni tuondokane na kadhia hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, Mheshimiwa Waziri unajua kwa muda mrefu nimekuwa nikizungumzia suala la upungufu wa fedha za kiinua mgongo cha Madiwani. Shilingi milioni 11 zisisababishe kilio hiki bila sababu. Mheshimiwa Waziri ukiamua najua ndani ya wiki mbili zijazo hili litakuwa limeondoka, tusaidie kelele zimezidi.

Mheshimiwa Mwenyeiiti, baada ya kusema hayo, nawashukuru sana, ahsanteni. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ili nami niweze kuchangia. Nianze kwa kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa inayofanya, tunajuwa wanafanya kazi kubwa lakini vilevile wanafanya kazi hiyo katika mazingira magumu, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nitazungumzia mambo mawili, kwanza nizungumzie hali ya uraia kule Mkinga. Wilaya ya Mkinga ni wilaya inayopakana na nchi jirani ya Kenya na kwa muda mrefu sasa tumekuwa na tatizo ambalo limekuwa ni kero kubwa kwa wananchi wangu, kero ya uraia. Bahati nzuri jambo hili unalifahamu lilifika Mezani kwako ukataka nikupe ufafanuzi tukafanya hivyo lakini jambo hili mpaka leo bado halijapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, ipo changamoto kubwa sana kwa wananchi wangu wa makabila ya Wataita, Wakamba, Waduruma, ambayo haya ni makabila ambayo unayapata vilevile upande wa pili wa nchi jirani ya Kenya. Hili jambo la kuwa na makabila ambayo unayakuta kwenye nchi mbili tofauti si jambo geni. Kwenye maeneo yetu ya mipakani hili ni jambo la kawaida lakini wananchi wangu kule Mwakijembe wanapata usumbufu mkubwa sana kwa kuambiwa siyo raia kwa sababu tu wanaasili ya makabila ya Kenya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili siyo sawa kwa sababu wananchi hawa wamekuwepo kwenye maeneo yetu kabla ya Uhuru. Wamekuwa wakitambulika kama raia wa Tanzania lakini imeingia sasa kadhia tulipoanza kuandikisha raia wetu, wale wananchi wote wanaoonekana wanamajina ya makabila haya moja kwa moja wanaambiwa siyo raia, hii siyo sawa.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri jambo hili nimeshawasiliana na Waziri tangu mwaka jana, nikamuomba ikiwezekana afanye ziara aje aone kadhia hii. Naamini muda bado upo na Waziri atajipanga ili tuje tutatue tatizo hili lakini kwa kweli ni jambo linalowaumiza sana wananchi wangu kwa sababu wananyimwa haki yao ya msingi ya kuchagua na kuchaguliwa kama viongozi lakini vilevile wananyimwa haki ya kushiriki kwenye shughuli nyingine za kimaendeleo kama wananchi halali wa Tanzania. Naiomba Serikali yangu ilifanyie jambo hili uharaka ili wananchi hawa wasione wananyanyasika katika nchi yao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni vitendea kazi. Wilaya yetu ya Mkinga baada ya kuanzishwa, pale Makao Makuu ya Wilaya hatuna kituo cha polisi. Kituo tunachokitumia kama kituo cha polisi kiko takriban kilomita 40 kutoka makao makuu ya wilaya, hili si jambo zuri. Naiomba Serikali ione umuhimu wa kujenga kituo cha polisi kama Makao Makuu yetu ya Polisi katika Wilaya ya Mkinga pale kwenye mji wetu mkuu wa wilaya pale Kasera.

Mheshimiwa Spika, vilevile kwa upande wa Tarafa ya Maramba ambayo hii inajumuisha kata 10 tuna jengo la kituo ambalo limechoka, jengo hili ni condemned lakini ndipo kilipo kituo chetu. Wananchi wamejitahidi kwa nguvu zao kujenga jengo la kisasa. Tunachohitaji ni msaada wa Serikali tuweze kumalizia jengo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali ifahamu kwamba tuna askari wale wanaohudumu katika kata 10 hawana makazi, hii haiwezi kuwa sana. Naiomba Serikali yangu iliangalie jambo hili na iangalie jambo hili ikijua kwamba maeneo haya ni ya mpakani. Sasa unapokuwa na kituo cha polisi kwenye kata kinachohudumia kata 10 lakini kiko kwenye jengo ambalo ni condemned, Mheshimiwa Waziri wewe unajua mambo ya kiusalama silaha na kadhalika, unajua nisiendelee kwa details hapa, lakini tuna changamoto kubwa tunaomba msaada huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vipo vitendea kazi vingine ni changamoto kubwa kwa askari wetu kule Mkinga ambao wanafanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha hali ya ulinzi na usalama katika maeneo ya mpakani inakuwa shwari. Tunawaomba sana muwaangalie kwa jicho la pekee. Gari moja kwa eneo lile halitoshi, lile gari lililoko kwenye Kata ya Maramba ni bovu. Tunaomba msaada wetu tuweze kupata gari ambalo litasaidia kulinda usalama kwenye maeneo yetu ya mipakani.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nawashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA - (MWENYEKTI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru sana kwa kunipa fusrasa hii ya kuja kujibu hoja au kutoa maelezo ya ziada kuhusiana na kazi ya Kamati yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru Waheshimiwa wagunge wote ambao walipata fursa ya kuchangia kwenye hoja yetu, tumepata wachangiaji 10 ambao kwa bahati nzuri wote wameunga mkono taarifa ya kamati na kuipongeza, kwa niaba ya Kamati napenda kuzipokea pongezi hizo nasema ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi hakuna hoja za kujibu kwasababu wajumbe wote waliozungumza wamekubaliana na mambo yaliyosemwa na Kamati, kwamba kama taifa lazima tuhakikishe tunakuwa na utulivu wa uchumi wa nchi yetu na miradi ya umeme ni miradi muhimu kwa ukuaji wa uchumi wetu. Sekta ya mafuta inachango mkubwa katika uchangiaji wa maendeleo ya nchi yetu, kwa hiyo, wote wamejielekeza kwenye maoneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa tunapozuzngumzia sekta ya umeme wote tunakubaliana kwamba tupo nje ya power system master plane yetu, na kwamba lazima tufanye jitihada zote kuhakikisha tunaitekeleza pawer system master plan hii kwa sababu ndio dira yetu inayotuelekeza kwenye ukuzi wa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafurahi kwamba mawaziri wenye dhaman ya kusimamia sekta hizi wameliona hili na wamekubaliana kwamba ipo haja ya kuongeza jitihada za kuhakikisha mambo yanakwenda sawa. Tunajua kazi ambayo Serikali inafanya kwenye mradi wa mwalimu, tunajua mmekanyaga pedo tunaomba muongeze kasi kuhakikisha mradi huu unamalizika. Tunajua jitihada mnazofanya kwa TANESCO ongezeni juhudi ili tuweze kupata mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyelkiti wangu wakati anachangia alizungumzia suala la miradi ya REA na kwenye taarifa yetu tumezungumza kwamba tuhakikishe miradi hii inakamili, na yeye amekuja na aina nyengine ya kusisitiza, amesema miradi hii ya REA ambayo tumekwisha saini hatutegemei utekelezaji wake uwe chini ya kiwango tulichoingia mikataba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maneno mtaani kwamba huenda wakandarasi wakapunguziwa kazi ambazo walikuwa wamekabidhiwa, tunaiomba sana Serikali hilo lisitokee, na kama tetesi hizo ni kweli basi maelezo hayo yaletwe kwenye kamati ili kuweza kushauriana kwa pamoja, baada ya kusema haya naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa mwenekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia uzima na sisi wote leo tuko hapa tukiwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru Wizara kwa kutupatia fedha za maji. Mwaka 2018 tulitengewa shilingi bilioni 1,400, tumepata shilingi milioni 960, tunazungumzia takribani asilimia 67. Nawashukuru sana. Wakati nikishukuru, nikumbushe tu kwamba kuna kiporo cha shilingi milioni 461, tunategemea fedha hizi zitapatikana ndani ya kipindi cha mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nikisema hayo vilevile natambua katika bajeti ya mwaka kesho tumepangiwa shilingi bilioni 1,139 kwa ajili ya miradi ya kule Mbuta, Mwakijembe, miradi miwili ile ambayo ili ikamilike tunahitaji shilingi bilioni 2,300. Hii maana yake nini? Maana yake tuna upungufu wa shilingi bilioni 1,160 ili miradi hiyo iweze kukamilika. Kwa hiyo, naiomba Serikali ifanye kazi kuhakikisha kwamba fedha hizi zinapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nizungumzie tatizo la maji katika nchi yetu kwa ujumla. Nilikuwa nasoma taarifa ya World Bank, inaitwa Reaching for SDG The Untapped Potential of Tanzania Water Supply Sanitation and Hygine Sector ya mwaka 2018. Taarifa inatuambia kwamba takribani Watanzania milioni 20 hawapati maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposikia jambo hili, siyo jambo zuri hata kidogo. Kwa vigezo vyovyote vile, haiwezekani kama nchi tukaona Watanzania milioni 20 hawapati maji safi na salama halafu tukaona ni jambo la kawaida, lazima tuchukue hatua. Hapa ndipo linapokuja suala hili sasa kwamba lazima tutafute maarifa mapya ya kuhakikisha kwamba kama Taifa tunatoka hapa tulipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili liliazimia, moja ya maarifa iliyotumia Bunge ni kuongeza fedha za Mfuko wa Maji. Najua wenzetu wapo wanaosema kwamba tukiongeza kule tunaweza ku-trigger inflation, lakini statistics zinatuonesha kwamba kwa kipindi cha miaka kumi iliyopita tumeweza ku- control inflation. Kwa mwaka huu ndiyo tumeweza kupata kiwango kikubwa sana cha inflation iliyochangiwa na Sekta ya Usafirishaji, maana yake mafuta yako humu. Wakati tumefikiwa kiwango hicho, bado inflation yetu ni asilimia 3.1. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake nini? Hii maana yake tusijifiche kwenye kichaka cha inflation, bado tuna room ambayo tunaweza kufanya tukatumia Sekta hii Mafuta kupata fedha za maji na hatimaye tukaondoa tatizo hili kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili la maji ni kubwa vilevile Mkinga; na hili nimekuwa nikilisema mara kwa mara. Mkinga imegawanyika katika maeneo mawili, kuna eneo la milima na ukanda wa Pwani. Maji yanayotumika katika Mji wa Tanga, chanzo chake ni Mkinga, katika Kata ya Bosha na katika Kata ya Mhinduru. Tangu kuumbwa kwa dunia watu wa Kata hizi mbili hawajawahi kuona maji ya bomba. Hii haiwezi kuwa sawa hata kidogo. Watu wale wamejitahidi kuhakikisha wanalinda vyanzo vya maji. Maji yale yananywewa Tanga Mjini, wao hawana huduma ya maji. Haiwezi kuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikileta maombi, Halmashauri tumekuwa tukileta maombi kwamba tujenge miradi ya maji kwenye maeneo yale, tumekuwa hatupati majibu. Mwaka huu tumeleta maombi, tunahitaji shilingi bilioni nane ili maeneo katika Kata ya Mhinduru, eneo la kwa Mtiri, Churwa, Muheza, Mhinduro, Bamba, Mazengero, Kichangani na Segoma na vile vile maeneo ya Bosha, Kuze, Kibago, Bosha, Kwamtindi na Buzi Kafishe yaweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wapeni maji watu hawa, ndiyo wanaotunza vyanzo vya maji vinapeleka maji Tanga, ndiyo wanaotunza vyanzo vya maji vinavyopeleka maji sasa Muheza wao hawana maji safi na salama, haiwezi kuwa sawa hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo la pili ni ukanda wa Pwani. Ukanda wa Pwani hatuna Mito, tungetegemea tupate maji kwa kuchimba visima, lakini kila visima tunavyochimba, chumvi inakuwa ni nyingi mno, kwa hiyo, maji yale hayafai kwa matumizi ya binadamu. Sasa wakati ikiwa hivyo nataka mwelewe kwamba Watanzania wenzenu wanakunywa maji yasiyo safi na salama kwa sababu tu tumeshindwa kuwapelekea maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuja Mheshimiwa Kamwelwe akawaahidi watu wale kwamba suluhisho la tatizo lile ni kutoa maji Mto Zigi kuyapeleka kule. Maji yale leo hayajapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi ule uliambiwa utengenezwe ili wananchi wa Mkinga wapate maji, nimeambiwa Wizara ilitoa tangazo la mradi ule, amepatikana Mhandisi mwelekezi, lakini mpaka leo hakuna kinachoendelea. Tangu mwezi wa Kumi nasikia Mhandisi amepatikana, lakini kuna majadiliano yasiyoisha juu ya mradi ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana, nimeangalia vitabu hivi vya bajeti, mradi ule haupo. Hivi mnataka watu wa Mkinga tukapate wapi maji? Mheshimiwa Waziri alikuja mpaka Horohoro akaiona kadhia ile, watu wetu wanaenda kuchota maji Kenya. Tuondoleeni aibu ile. Aliwaahidi watu wale kwamba tutapata mradi wa maji wa quick-win. Aliagiza watu wa Tanga, UWASA walete mapendekezo; nimeambiwa mapendekezo yako Wizarani kwake, tunaomba fedha hizo ili tatizo lile liweze kuondolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anajua, amefika Mkinga, Makao Makuu ya Wilaya hayana maji. Hivi tunakuwaje na Wilaya ambayo haina maji? Tuna mradi pale wa ubabaishaji tu, tunatoa maji kutoka kwenye Kijiji jirani ndiyo ki-save Makao Makuu ya Wilaya. Hii haiwezi kuwa sawa. Tusaidieni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikisema jambo hili tangu Mzee Maghembe ni Waziri, ameondoka Mheshimiwa Prof. Maghembe wamekuja wengine, sasa uko wewe, imani ni yangu ni kwamba jambo hili litapatiwa ufumbuzi. Tusaidieni tuweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa ya Mheshimiwa Waziri, Wilaya ya Mkinga ndiyo eneo lenye Ukanda mkubwa wa bahari kuliko Wilaya nyingine zote katika Mkoa wa Tanga. Kwa hiyo, tuna potential ya ujenzi wa mahoteli katika ukanda ule, lakini tunashindwa kujenga mahoteli kwa sababu hatuna maji. Mahoteli yanajengwa upande wa pili wa nchi ya Kenya, upande wa Mombasa, sisi tunaangalia. Nawasihi sana, tusaidieni tupate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakusudia kujenga kiwanda kikubwa kabisa cha uzalishaji wa cement katika nchi hii. Mapato yanayotegemewa pale ni shilingi bilioni 450 kwa mwezi. Kiwanda kile kitafanyaje kazi tusipokuwa na maji? Kiwanda kile kinategemewa kuvutia viwanda vingine 11 pale Mtimbwani, tunajengaje viwanda vile kama hatuna maji?

Mheshimiwa Waziri, tusaidieni, watu wa Mkinga wana shida ya maji, tupeni maji ili tuweze kupiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mungu kwa kutupa uhai na uzima na kwamba tunaendelea kuwatumikia Watanzania. Niendelee kuwashukuru ndugu zangu wa Mkinga kwa jinsi ambavyo wanaendelea kuniunga mkono ninapotimiza majukumu yangu ya kuwatumikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze vilevile kwa kuishukuru Serikali kwa jitihada inazofanya katika kuwezesha miundombinu ya nchi yetu, hususan Bandari ya Tanga tunaiona kazi inayofanyika ya kupanua na kuongeza kina cha bandari ile, tunawashukuru. Tunawashukuru vilevile kwa Barabara ya Tanga – Pangani – Bagamoyo ambayo tunaambiwa muda si mrefu itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami, tunaishukuru Serikali kwa jitihada hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikitoa pongezi hizo, nieleze masikitiko yangu katika maeneo mawili. Kwa muda mrefu sasa tumekuwa tukipigia kelele barabara ya kutoka Mabokweni – Maramba – Bombo Mtoni – Umba Junction – Mkomazi – Same. Barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa Mkoa wa Tanga na ni muhimu sana kwa watu wa Maramba, Mkinga, Korogwe, Lushoto na Same. Ni barabara inayounganisha Mkoa wa Tanga na Mkoa wa Kilimanjaro lakini vilevile na nchi jirani ya Kenya. Ni barabara ya kiusalama kwa sababu ipo kwenye ukanda wa mpakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni barabara ya kiuchumi kwa sababu inaunganisha maeneo ya kiutalii. Unapozungumzia utalii unaofanyika Zanzibar fursa hiyo vilevile inakuja kwa upande wa Tanga, unaiunganisha na eneo lile la Bagamoyo lakini vilevile unaunganisha na Mbuga ya Mkomazi ambayo inaanzia upande huu wa Mkinga eneo la Mwakijembe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa kiutalii lakini uchumi wa kusafirisha mazao, kama walivyosema wenzangu, bidhaa za mazao ya matunda, mbogamboga, karafuu kutoka kule Kigongoi na mazao ya viungo kutoka Muheza na kule Bosha. Kwa hiyo, ni barabara ambayo tukiona kunakuwa na kigugumizi cha kuishughulikia tunapata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba Serikali ihakikishe barabara hii sasa inawekewa fedha ili iweze kufanyiwa usanifu. Barabara hii kwa upande wa Kilimanjaro tayari usanifu umekwishafanyika, tunashangaa kwa nini upande huu wa pili barabara hii haifayiwi usanifu? Tunaomba suala hili liweze kushughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kuna matengenezo yanayoendelea katika barabara hiyo lakini kuna maeneo korofi. Eneo la kwa Mukamba, pale tunahitaji kifereji na kuweka kifusi cha changarawe ili barabara ile iweze kupitika wakati wote. Eneo la Majumba Matatu na lenyewe ni korofi, najua kuna mifereji inaanza kujengwa pale lakini ikamilishwe kwa wakati na iongozewe eneo refu zaidi ili barabara ile iweze kupitika kwa wakati wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni bandari. Mwaka 2014 Kampuni ya Kichina inayojulikana kama Hengia ilionesha nia ya kuja kuwekeza katika nchi yetu kiwanda cha kuzalisha tani milioni 7 kwa mwaka, uwekezaji wa dola bilioni 3, lakini vilevile walisema wataanza na uwekezaji wa bilioni 1, hapa unazungumzia trilioni 2.3 hivi zingeweza kuwekezwa katika kujenga kiwanda kikubwa katika Ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara. Hata hivyo, pamoja na jitihada zao za kuomba vivutio mbalimbali vya uwekezaji bado tangu mwaka 2014 mpaka leo kiwanda hiki kimekwama kupata vibali kianze kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu hawa walitaka sambamba na kujenga kiwanda cha kuzalisha simenti vilevile waweze kupata fursa ya kujenga jet. Tumekuwa na kigugumizi cha kuwapa ruksa ya kujenga jet kwa sababu za kiusalama. Ni jambo ambalo unaweza kulielewa ukielezwa lakini maswali tunayojiuliza hivi sisi tumeshindwa kuvi-engage vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vikasimamia jet ile hata kama wameijenga wao? Tukawaweka watu wetu wa TRA wakasimamia mapato yetu? Tukaweka vyombo vingine vya bandari vika-manage jet ile ili uwekezaji hu mkubwa tusiweze kuupoteza? Watu wa Mkinga tunahitaji kupata majibu ni lini kitendawili hiki kitateguliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapata hofu kwamba tunaenda kupoteza uwekezaji mkubwa huu wa trilioni 6.5 ambazo zingeingia kwenye uchumi wetu. Tunaiomba Serikali ifanye maamuzi ili watu hawa waweze kuanza ujenzi na kuzalisha simenti. Kama tunadhani hatuwezi kuwaruhusu wao kujenga basi twendeni tukajenge sisi jet ile ili uwekezaji huu usiweze kupotea. Naiomba Serikali ifanye maamuzi ya haraka ili jambo hili liweze kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Kamati naomba niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia katika hoja yetu. Katika mjadala huu, Waheshimiwa Wabunge ambao waliochangia Taarifa yetu ni Wabunge 14. Sehemu nyingi ya michango hii ilikuwa ni ushauri, tunaichukua michango ile kama ushauri lakini yako mambo machache ambayo nilidhani ni vizuri tuyatolee ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, Kaka yangu Mwijage amesema hapa kwamba mimi nimepitia kwenye mikono yake, ni kweli. Kipindi kile naanza kufinyangwa katika Utumishi wa Umma nilianzia pale TPDC na miongoni mwa watu waliofanyakazi kubwa ya kutuonyesha sekta ya Nishati iko vipi ni Kaka yangu Mwijage, na siku zote manshukuru sana kwa kazi kubwa aliyoifanya.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mwijage ameibua mambo makubwa katika Taarifa yetu. Kwanza ameonesha hofu kwamba yapo mambo ya msingi hatukuyatendea haki katika taarifa yetu. Jambo kubwa alilolizungumzia ni uwekezaji unaofanywa na TPDC katika suala zima la kutafiti mafuta na gesi. Ukipitia taarifa yetu ni kweli hatulisema kwa undani jambo hili; na tulifanya hivi makusudi kwasababu mbili:-

Mheshimiwa Spika, jambo hili tumekuwa tukilisema mara kwa mara kwenye Taarifa zetu zilizopita; ni jambo ambalo Serikali inalifanyiakazi. Nataka nimtoe hofu; katika Bajeti tuliyopitisha hapa tulitenga fedha kwa ajili ya kazi ya utafiti; ipo kazi inaendelea kufanywa na TPDC. Hata hivyo kama Kamati tuliamua kufanya uamuzi wa makusudi wa kutoliibua sana jambo hili ndani ya nyumba yako hii kwasababu tuna mfano halisi, nchi inapojenga matumaini makubwa kwa wananchi msipoya-manage matumaini hayo mnaweza kuzalisha tatizo ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, kwahiyo kimsingi tuliamua ku-manage expectation kwa taifa letu; na kama kuna jambo ambalo huwa linajenga matumaini makubwa kwa wananchi ni wanaposikia suala la mafuta. Ukiwaambia tu kuna utafiti kesho yake asubuhi wanakwambia nchi yetu ina mafuta. Kwahiyo tulidhani tuwe makini katika kufanya jambo hili. Itoshe kusema, katika bajeti ya mwaka huu tulitenga shilingi bilioni 33.2 kwa ajili ya Kitalu cha Mnazi Bay kule Kaskazini. Ipo kazi inafanywa kule na TPDC, zipo kazi zimeshafanyika, anatafutwa mshauri mwelekezi ili aweze kushauri jinsi ambavyo tunaweza kufanyakazi ya kuchoronga visima kwa ajili ya utafiti wa mafuta.

Mheshimiwa Spika, vilevile kwenye kitalu cha Easi Wembere nako tulitenga bilioni 6.3, ipo kazi inafayika na kazi inakwenda vizuri. Pia lipo eneo la Kitalu Namba Nne kwenye maji ya bahari ya kina kirefu, tulitenga bilioni 22.62, ipo kazi inaendelea. Nataka niliambie Bunge hili kwamba utafiti uliofanya na TPDC ulitumia the best technology in the World katika kufanya utafiti wa kupata mambo haya. Kwahiyo, itoshe kusema kwamba ipo kazi kubwa inafanyika.

Mheshimiwa Spika, lipo jambo lingine kaka yangu Mwijage amelisema. Hili msingi wake ni kazi ambayo Kamati imekuwa ikiifanya kwa muda mrefu. Hoja ya kuwa na hifadhi ya pamoja (Strategic reserve) ya mafuta katika nchi hii ni hoja ambayo Kamati yangu imekuwa ikiishughulikia kwa muda mrefu. Hivi tunavyozungumza, TPDC ina mkakati wa kutumia matenki yaliyopo Kigamboni kufanya ukarabati ili matenki yale yaweze kuhifadhi mafuta. Kama haitoshi, TPDC imeshapata maeneo kule Tanga kwa ajili ya kujenga matenki ya kuhifadhi mafuta.

Mheshimiwa Spika, vilevile yamekuwepo mazungumzo kwamba tunaweza kutumia refinery yetu iliyoko kule Kigamboni ili kuwa na mfumo huu wa uingizaji wa mafuta kwa pamoja. Imekuwa na changamoto zake, wadau wamekuwa wakipishana, na jambo hili alikabidhiwa TR ili kuweza kuja na majibu ya jinsi gani tunatoka hapa. Kuna kazi inaendelea, kwasababu haijafika sehemu nzuri tulidhani tusillibue ndani ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo, wenzetu wa Mamlaka ya Bandari nao huenda wakaingia wkenye kujenga matenki haya ili yaweze kutumika katika uhifadhi wa mafuta. Ninachoweza kukubaliana nae ni kwamba ni kweli, jambo hili ni la msingi sa, pengine tumechelewa kulifanyiakazi, ni vizuri Serikali ikaongeza kasi katika kushughulikia jambo hili.

Mheshimiwa Spika, amezungumzia katika suala la upotevu wa mafuta, amezungumzia suala la flow meter na margin; haya ni mambo ambayo yanajenga ule msingi wa dhamira yetu ya kuwa na hifadhi ya pamoja ya mafuta. Kwahiyo, nimuondoe hofu, mambo haya Kamati inayashughulikia.

Mheshimiwa Maige kuna jamno amelibua la utozaji wa loyalty katika mawe lakini vilevile katika dhahabu. Hili tunalichukua, nikuahidi Kamati itali-persue tuone tunatokaje katika mkwamo huu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja, ahsante sana. (Makofi)

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii, ili niweze kuchangia kwenye hotuba ya Wizara ya TAMISEMI iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ni kwa upendeleo wake tu kwamba tunaendelea kuwa salama, akizidi kutupa baraka zake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili, niipongeze Serikali, kwa hotuba iliyopo mbele yetu, ni hotuba ambayo inatutia matumaini, inatutia matumaini kwenye maeneo mengi. Kwenye eneo la elimu sisi wengine tukisia kwamba zinakwenda kujengwa sekondari za kata, kwenye kata ambazo zilikuwa hazina sekondari kwetu wengine ni faraja kubwa. Hongereni sana Serikali kwenye sekta ya afya mmesema mengi, hongereni. (Makofi)

Mhesimiwa Spika, lakini niseme machache, nianzie TARURA ambayo wenzangu wengi wamesema, wote tunakubaliana kwamba kiasi cha fedha kinachopelekwa TARURA ni kidogo na kwamba lazima tutumie maarifa mapya ili kupata vyanzo vya kuongeza mapato ya kupeleka fedha kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yametoka mawazo mengi, naomba Serikali iwe sikivu, tuongeze fedha hizi twende tukazijenge barabara za vijijini. Maana barabara hizi, zinahusiano wa moja kwa moja na ukuaji wa uchumi lakini vilevile kuondoa umaskini kwa watu wetu. Lakini wakati tukizungumzia eneo la kuongeza fedha, kuna eneo lingine lazima tuliangalie, udhibiti na ufuatiliaji. Ni eneo ambalo naliona kama hatujalizungumzia sana na hapa nitatoa mifano, mifano ambayo inagusa Mkinga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2019, Mkoa wa Tanga ulipata majanga ya mafuriko, miundombinu mingi ikaharika, Wilaya ya Mkinga tulipata bahati mbaya madaraja ya barabara za TARURA lakini hata zile za TANROADS. Barabara za TANROADS zilifanyiwa kazi lakini TARURA kipindi kile ilishindikana, tukaambiwa jambo lile linachukuliwa liingizwe kwenye bajeti ya mwaka 2020 ikaingizwa, Mwezi wa Julai, 27 ikifunguliwa zabuni kwa ajili ya kutengeneza barabara zile na madaraja yaliyokuwa yameharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tarehe 13 Agosti, 2020, Zabuni ile ikafunguliwa lakini Wakandarasi hawakupatikana. Ikatangazwa tena mwezi Novemba, 2020 akapatikana Mkandarasi, tarehe 03 Machi, 2021 wakaingia Mkataba, Mkandarasi akakabidhiwa eneo la kazi, alitakiwa tarehe 15 Aprili, 2021 awe ameanza kazi, mpaka leo hajaanza kazi. Hii ni dalili mbaya, kwamba Mkandarasi huyu anakwenda kushindwa, akishindwa maana yake tutangaze tena apatikane Mkandarasi, hapa imebaki miezi miwili mwaka wa fedha huu uishe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tangu 2019, watu hawa wa Kuze, watu wa Mhiduro, watu wa Bosha, hawawezi kupitisha mazao yao kwenye barabara kwasababu daraja limevunjika, fedha zipo lakini tunashindwa kuhudumia barabara hizi kwasababu ya taratibu za kirasimu za ununuzi niwaombe sana, tufuatilie eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zinaweza kuwa nitaratibu za kimanunuzi lakini vilevile inaweza kuwa ni uchochoro wa fedha zisitumike eneo hili ziende zikatumike eneo lingine, tusaidieni daraja lile la Kauzeni liweze kushughulikiwa. Lakini hata kwenye allocation ya fedha, TARURA wana mpango wa kutoa fedha za maendeleo zinazokuwa nje ya zile za kibajeti kwenye wilaya hizi ili iweze kusaidia miradi ile ambayo inahitaji fedha nyingi iweze kushughulikiwa. Sisi wa Mkinga tangu mwaka 2013 hatujawahi kupata fedha hizi, wilaya hii ina maeneo ya milima, barabara za kwenye milima ni changamoto kwa hiyo, tunashindwa kutengeneza barabara hizi kwasababu kabajeti ketu ni kadogo. Mtendaji Mkuu wa TARURA alikuja kule, akaiona hali akasema watu wa Mkinga mnastahili kupata fedha hizi mpaka leo, tangu mwaka 2013 mpaka leo, hakuna senti tano iliyokwenda. Hii haiwezi kuwa sawa, tunaomba mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Sekta ya Afya, nakwenda kulekule kwenye ufuatiliaji, tunaishukuru Serikali imetupatia fedha kwa ajili ya kujenga hospitali ya wilaya. Tulipata milioni 500 mwaka wa fedha uliokwisha lakini kwasababu zilichelewa kuletwa mwezi wa Juni fedha zile zikarudishwa. Mwaka huu wa fedha Januari tumepata bilioni 1, tunaishukuru Serikali lakini naomba Serikali mfuatilie, ninashida na utekelezaji wa mradi huu, kwa sababu tumepata fedha Januari… (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, mpaka leo.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, mpaka leo, katika bilioni 1 ni milioni 200 tu zimetumika. Kuna Kamati ya Manunuzi kule ya hovyo nendeni mkafumue kamati ile, haiwezekani miaka miwili mfululizo Serikali inatoa fedha halafu ifike mwezi Juni hapa hakutuweza kutumia fedha zile zirudi serikalini, haiwezekani! Sasa Serikali mtusaidie, msingoje ufike mwezi Juni mtuambie Mkinga hamkuweza kutumia fedha. Nendeni sasa mkasimamie jambo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sekondari ya Maramba. Tumekamilisha madarasa pale, ya kuipandisha hadhi sekondari ile iwe na kidato cha tano na cha sita. Tunaishukuru Serikali ilileta milioni 300 pale, wananchi wamechangia, Mbunge wao kupitia Mfuko wa Jimbo nimechangia, tumakamilisha mabweni, tumeweka samani, ilikuwa ianze mwaka jana kukawa na tatizo la kuweka bajeti ya chakula kwa sekondari ile ikashindwa kuanza. Naomba kipindi hiki sekondari ile ianze. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Lazima ianze.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa kutoa kibali cha zahanati zetu karibu tano hivi tulikuwa tumeziombea zipate kibali zianze. Kibali kimetoka tumeziweka zahanati hizi kwenye mpango wa bajeti vifaa tiba viende. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la mwisho na hili Mheshimiwa Waziri wewe unalijua, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara, akaja Maramba, tukampeleka kwenye Kituo cha Afya cha Maramba. Maramba kuna zaidi ya watu 12,000 tumeomba hospitali ile kwasababu ina hudumia kata saba ipewe hadhi ya kufanya kama hospitali ya wilaya ili mzigo ule wa kuhudumia zile kata sana uishe. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia kwenye hotuba iliyoko mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehma ambaye imempendeza kwamba tuendelee kuwa na uhai huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natumia fursa hii kuishukuru sana Serikali na kuipongeza kwa kazi kubwa iliyofanyika ya kuimarisha na kuboresha sekta ya madini nchini. Wote tunafahamu kwamba biashara ya madini sifa yake kubwa kwa kipindi kilichopita ilikuwa ni biashara ya kificho. Ilikuwa inaonekana ni biashara ya ujanja ujanja, biashara ya kupiga dili, biashara ambayo Watanzania walikuwa wanaisikia pembeni pembeni, lakini Serikali iliamua kuleta heshima kwenye matumizi ya rasilimali madini katika nchi hii. Ikaweka mikakati ambayo leo hii Watanzania ni washiriki kwenye biashara hii muhimu. Imeipa heshima biashara hii, kwamba katika Afrika leo nchi za kiafrika zinaiangalia Tanzania jinsi ambavyo imeleta mageuzi ya umiliki wa rasilimali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali. Mkipitia hotuba ya bajeti na taarifa yetu, mtaona jinsi ambavyo mchango wa sekta hii umekuwa ukiongezeka kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Sekta hii inasimamiwa vizuri, hongereni sana Wizara, hongereni sana Serikali. Wakati tukitoa pongezi hizi, tusibweteke, tuongeze jitihada kwa sababu bado nafasi ya sekta hii kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi wetu bado ni kubwa sana. Tufanye zaidi ili sekta hii itusaidie Watanzania kuondokana na umasikini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nitoe rai, Bunge lililopita liliunda tume ambapo jukumu lake lilikuwa ni kuishauri Serikali juu ya jinsi gani nzuri ya kuboresha sekta hii. Mheshimiwa Spika aliunda tume iliyoenda kuchunguza Mererani, vilevile aliunda timu iliyoenda kufuatilia mambo ya almasi. Bado utekelezaji wa mapendekezo ya tume zile haujakwenda kikamilifu. Tuongeze speed Serikali kushughulikia mambo yale ili kuondoa sintofahamu zisizo na msingi ambazo bado ziko kwenye sekta hii. Rai yangu ya kwanza ni hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nataka kuipongeza Serikai kupitia Wizara kwa jinsi ambavyo imelisimamia Shirika letu la STAMICO. Shirika hili ilifika mahali tulikuwa tukizungumza humu ndani ya Bunge tunasema sasa lifutwe, lakini sasa kuna mabadiliko makubwa. Shirika hii linafanya kazi nzuri. Sasa kama tulikuwa na kigugumizi cha kulipa mtaji shirika hili kwa kisingizio kwamba halifanyi vizuri, kisingizio kile sasa kimeondoka. Twendeni tukaliongezee mtaji Shirika hili ili liwe jicho letu na msimamizi wetu na ushiriki wetu kwenye sekta ya madini kiuwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza STAMICO kwa ubunifu ambao umetuwezesha kuwa na refinery yetu kule Mwanza. Muda mrefu tumekuwa tukipiga kelele kwamba ifike mahali Benki Kuu inunue dhahabu, lakini kwa sababu huko nyuma tuliunguzwa vidole, wenzetu wa Benki Kuu wamekuwa na kigugumizi cha kununua dhahabu kupitia STAMICO na Wizara. Tumeondoa kigugumizi kile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna refinery ya kisasa inayotumia teknolojia ya kisasa ulimwenguni, dhahabu itakayosafishwa pale, purity yake ni 99.9, hatuna sababu ya kutonunua dhahabu sasa na kuiweka kwenye reserve zetu za Benki Kuu. Tukifanya hivyo, tunakwenda kuhakikisha sarafu yetu inaimarika. Sasa tusiwe na kigugumizi kwenye kufanya hilo. Tuna refinery ile, twendeni kwa haraka kuanza kununua dhahabu tuiweke kwenye reserve yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo STAMICO bado kuna changamoto. STAMICO na kampuni zake tanzu bado kuna madeni makubwa ya wazabuni waliokuwa wamefanya kazi na STAMICO. Tumefanya kazi ya kupitia, kutathmini madeni hayo kwa muda mrefu. Vyombo vyetu vya kiserikali vimefanya kazi hii, tuache kigugumizi cha kuwalipa wazabuni wale. Tena twende tukawalipe kwa haki, tusitumie ujanja ujanja wa kukwepa madeni yale, twendeni tukawalipe stahili zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo tumelisema kwenye taarifa yetu, Mheshimiwa Rais alipokuja hapa, aliagiza kwamba sasa twende tukachimbe madini yetu kwenye maeneo ya hifadhi. Rai yetu, tunaomba Wizara ije kwa haraka kufanya mapitio ya sheria zote zinazogusa eneo hili; yale yanayoleta ukinzani wa kauli ile (agizo lile la Rais) kufanyika, tuzifute, tuje na sheria mpya zitakazowezesha jambo hilo; na jambo hili tulifanye kwa haraka ili madini yale yaweze kutusaidia ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu Mererani. Tunafanya kazi kubwa lakini bado ina changamoto. Teknolojia tunayotumia au ile mitambo tunayotumia, bado kuna changamoto ambazo tumezisema ndani ya Kamati, twendeni tukatumie teknolojia za kisasa kuhakikisha pale kwenye geti tunadhibiti ipasavyo; na kule kwenye kamera zetu tuhakikishe tunaunganisha mfumo ule na mfumo wa kutunza kumbukumbu wa Taifa ili taarifa zetu zisipotee. Hili tunalisema hata kule Mwanza kwenye refinery, zile kamera zetu zinatunza kwa miezi sita, twendeni tukaunganishe mfumo ule na taasisi yetu ya kumbukumbu ya Taifa ili tusipoteze kumbukumbu zozote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado uwezeshaji wa wachimbaji wadogo tulifikirie zaidi, tuje na maarifa mengine. Najua Wizara imefanya kazi kubwa ya kuzungumza na mabenki, lakini tufanye kazi zaidi ili upataji wa mitaji isiwe kigugumizi, iwe ni jambo rahisi kwa wachimbaji wetu kuweza kupata mitaji ya kuingia kwenye uchimbaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwasilishaji wa taarifa yetu amepongeza tozo ile ya asilimia moja ambayo imefutwa, nami naongeza sauti yangu hapa, tunaipongeza Serikali, lakini kuna kazi ya kufanya. Tulipokwenda field bado wachimbaji na wauzaji wa madini walikuwa hawana taarifa kwamba sheria ile imefutwa, bado kuna watendaji wetu walikuwa wanatumia kodi ya zamani ambayo ilikuwa imefutwa. Twendeni tukalirekebishe jambo hili, na pale ambapo watu walitozwa kodi ambayo tayari ilikuwa imeshafutwa, twendeni tukafanye utaratibu wa watu wale kurudishiwa fedha zao. Maana tulichokusanya ni haramu kwa sheria. Twendeni tukawarejeshee fedha zao lakini tufanye kazi kubwa ya kutoa elimu ili sekta hii iweze kupata mafanikio.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, vibali vya wale masonara kutoka nje bado kuna kigugumizi, twendeni tukaangalie utaratibu mzuri utakaotuwezesha kupata teknolojia ile kwa wepesi ili masonara wale wanapokuja kutoka nje, waweze kurithisha ujuzi ule kwa Watanzania. Baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. DUSTUN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nichangie kwenye mjadala wa hotuba iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uhai na kwamba tunaishi kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja kwa moja, nianze kuishukuru Serikali, kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu ya Wizara ya Maji, kwa hiki ambacho kwa mwaka huu nakiona katika bajeti hii. Nimesema mara nyingi kwamba katika Mkoa wa Tanga kama kuna Wilaya inashida kubwa ya maji ni Mkinga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepiga kelele sana kuzungumzia tatizo la maji Mkinga, tulikuwa hatusikikisikiki hivi lakini hizi dalili zinazoziona kwenye bajeti hii namshukuru sana Mheshimiwa Waziri na timu yake. Kwa mara ya kwanza katika bajeti hii Wilaya ya Mkinga tumetengewa shilingi bilioni 5 za maji. Katika historia ya kuwepo kwa Mkinga hizi ndiyo fedha nyingi kwa mara ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tukisikia wenzetu wana shilingi bilioni 15 au 20, sisi tunashukuru kwamba kwa mara ya kwanza tumepangiwa shilingi bilioni 5. Hatujawaji kuwa na mradi mkubwa wa Kitaifa kwa mara ya kwanza kilio chetu cha kuwekewa maji kutoka kwenye Mto Zigi kimesikika, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia vitabu pale nimeona mmetutengea shilingi bilioni 3, nawashukuru sana. Sasa vijiji vile 32 vya Tarafa ile ya Mkinga vinaenda kupata maji ya uhakika. Nawashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua fedha hizi hazitoshi lakini ule uthubutu tu wa kusema hapana tuanze kwa kupeleka shilingi bilioni 3 mimi nawashukuru sana. Niwaombe wakati tunapoenda ku-design bomba lile tuhakikishe inafanyika kwa full capacity. Kwa nini nasema hivi? Ni kwa sababu Mkinga ukanda ule ndiyo wenye potential kubwa ya uwekezaji wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi Mheshimiwa Rais wameingia Memorandum of Understanding na Rais wa Kenya kwa ajili ya bomba la gesi kutoka upande huu kwenda Kenya. Waziri Mkuu alipokuja alituhakikishia kwamba kituo kikubwa cha kuchakata gesi hiyo kitakuwa Mkinga. Nini maana yake? Maana yake tutavutia ujenzi wa viwanda, kile kilichotokea Mkuranga kinaenda kutokea Mkinga. Sasa tujipange tuhakikishe bomba hili linakuwa na uwezo mkubwa ili tusije kuhangaika wakati ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Miradi ya Mbuta na Mwakijembe, nilikuambia Mheshimiwa Waziri kwamba miradi hii sijui kwa nini imesahaulika kuitwa miradi ya kichefuchefu, kwa sababu tumekwenda mimi na wewe unajua, Naibu Waziri amekwenda, miradi hii tangu mwaka 2019 mpaka leo hakuna kinachoeleweka. Kwa mwaka mzima huu wa bajeti hakuna kazi yoyote iliyofanyika kuendeleza miradi hii miwili, hii haiwezi kuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeambiwa ule mradi wa Mwakijembe arbitration ile imeisha lakini sijui kuna kigugumizi gani. Pale Mbuta tumepata mkandarasi alikuwa anatakiwa aanze kazi mwezi Januari ameshindwa vigezo, tumemtafuta mkandarasi wa pili, majadiliano yanaendelea hii itatupeleka mpaka kuisha mwezi wa sita, mwaka mzima miradi hii itakuwa hiajafanya chochote, haiwezi kuwa sawa. Naomba tuongeze jicho kuangalia jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nakushukuru kwamba kuna miradi kadhaa imetengewa fedha. Mradi wa Kwantili, Churwa, Muheza, Mihunduro, Bangamwevengero, Mchangani tuna shilingi milioni mia moja na kitu. Kuze, Kibago, Bosha kwa Ntindi, Muze, Kafishe tuna shilingi milioni 173. Bantu, Kwa Ngena, Machimboni tuna shilingi milioni 100. Kidundui, Kwekuyu, Bombo Mbuyuni, Mgambo, Shashui, Emsambia mpaka Vuga tuna shilingi milioni 300 na Ng’ombeni tuna shilingi milioni mia mbili na kitu. Kuboresha ule mradi wa Daruni tuna shilingi milioni 300. Gombero, Vunde, Manyinyi, Jirihini, Dima tuna shilingi milioni 123. Mowa, Zingibari, Mayomboni shilingi milioni 82. Nashukuru sana kwa miradi hii lakini wakati nikushukuru kutengwa fedha hapa ni jambo moja, fedha hizi kwenda katika halmashauri ni jambo lingine. Tunaomba fedha hizi zifike ili tuondokane na tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia hoja ya bajeti ya Wizara iliyoko mbele yetu.

Awali ya yote ninataka kuipongeza na kuishukuru Wizara, Mheshimiwa Waziri na timu yako ya Naibu Mawaziri, Naibu Waziri Gekul wakati akiwa Naibu wako na ndugu yangu Mheshimiwa Ulega ambao wamefanya ziara katika Wilaya yetu na kutatua changamoto zilizokuwa zinatukabili, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Ulega ulivyokuja lile ulilolifanya limeleta matumaini makubwa kwa Wana-Mkinga, lakini limeibua mahitaji makubwa sana, tunashukuru wa engine ya boti ile kwa kikundi kile cha ushirika, lakini sasa kuna vikundi kwenye mwambao ule karibu 12 mahitaji ya engine za boti zile kwa ajili ya uvuvi ni makubwa, nitawasilisha Wizarani kwenu kwa maandishi majina ya vikundi vile tunaomba mtusaidie. (Makofi)

Lakini Mheshimiwa Waziri tulifika Wizarani kwako na Madiwani wawili kuzungumzia changamoto ya mnada kwenye mpaka wetu wa Horohoro, nakushukuru sana, mma- act kwa haraka tumefanya jitihada sasa za kuanzisha mnada ule, naomba mwaka wa bajeti huu utakapoanza tukamilishe yale yaliyobaki ili mnada ule uweze kuanza, tuweze kupata mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nijielekeze kwenye eneo la ufugaji wa samaki; ninaiona jitihada inayofanyika hasa hasa kwenye upande wa uzalishaji wa vifaranga, nawapongeza, lakini ninaamini bado tungeweza kufanya vizuri zaidi hasa kwenye ukanda wa Pwani tumeusahau, aidha tumeusahau au tunaogopa gharama za kuwekeza kwenye eneo hili. Ndugu zangu samaki wanaoliwa duniani zaidi ya asilimia 50 wanatokana na samaki wanaofugwa. Kwa hiyo, hatuwezi sisi kuacha kuwekeza kwenye eneo hilo, hatuwezi kuuacha uchumi mkubwa kiasi hicho, kuna kipindi nilisema hapa hivi wenzetu Afrika ya Kusini Western Cape na Eastern Cape wamewezaje kwamba eneo hili la ufugaji wa samaki linawabeba? Kwa nini tusiende kujifunza kule? Hivi kwa nini sisi leo hii tuzidiwe na Zambia kwenye kuzalisha na kuuza samaki? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miaka michache iliyopita tulikuwa tunazungumza na Katibu Mkuu Dkt. Tamatamah tukiona ni jinsi gani ambavyo Wazambia wale wamekwenda kupata fedha kutoka African Development Bank wameanzisha mradi mkubwa wa ufugaji wa samaki na sasa umeanza kutoa matokeo. Kwa nini sisi tusifanya hivyo? Lakini Wizara kwa nini msichukue initiative? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali hii imetoa fursa kwa Halmashauri kuwa na miradi ya kimkakati, watu wengi wanaenda kuwekeza kwenye stand na vitu vya namna hiyo, kwa nini ninyi Wizara msiichukue hii initiative, msichukue opportunity hii, mkatuma wataalam wenu kwenye Wilaya zile zinazopakana na hahari mkasema tunataka kutengeneza pilot district hata tano tu bila kuisahau Mkinga, mkaenda mkafanya study, mkafanya visibility study, tukaja na Mkakati Wilaya hizo badala ya kuwekeza kwenye stand waende wakawekeze kwenye ufugaji wa samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkiweza kufanya hivyo mtaibua ufugaji wa samaki kwenye maeneo haya na shughuli za kiuchumi zitakuwa. Ninawaomba bajeti hii ikipita tumeni wataalam wenu Mkinga, waje tukae, tutengeneze visibililty study, tuweze kufuga samaki kwenye mwambao ule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye mjadala wa bajeti uliopo mbele yetu. Namshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa pumzi na uhai, naomba aendelee kutulinda ili tuweze kuendelea kulitumikia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, msemaji aliyemaliza kusema amezungumzia jambo la nchi yetu kuanzisha refinery ya kusafisha dhahabu hili ni jambo sana, nataka kuipongeza Serikali kwa hatua kubwa hii ambayo inaenda kuongeza thamani ya dhahabu yetu lakini tukipiga hatua zaidi kwa benki kuu kununua dhahabu ile maana yake tunaenda kuifanya sarafu yetu iwe na thamani zaidi, hongereni sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpongeze Mheshimiwa Rais wakati wa uzinduzi kuna jambo aliliona, jambo ambalo limekuwa likipigiwa kelele kwa muda mrefu kuhusiana na kodi ya ongezeko la thamani kwenye sekta hiyo, ametoa maelekezo kwamba kodi ile isiwe kikwazo cha sisi kuweza kupata manufaa zaidi kutokana na sekta hii ya madini. Hapa ndipo ninapotaka kuanzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka miwili iliyopita tulifanya mabadiliko makubwa sana ya kuruhusu wachimbaji wadogo kuingia kwenye sekta hii, tuliondoa kodi zilizokuwa na kero na hali ile ikachangia wachimbaji wadogo wa Kitanzania kuingia kwa nguvu kubwa kwenye uchimbaji, hali ambayo imeifanya sekta ya madini kuwa na mchango mkubwa katika uchumi wetu. Lakini ninapata hofu kwa measures za kikodi zinazopendekezwa na hofu kwamba tunaweze kufifisha jitihada hizi ambazo tumekwishazifanya na zimeleta manufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendelezo yaliyopo hapa yanaenda kubadilisha kumtambua mchimbaji mdogo ni nini, Sheria ya Madini inamtambua mchimbaji mdogo katika kiwango fulani kikubwa mapendekezo yanayokuja hapa yanaenda kumtambua mchimbaji mdogo Katika level ndogo sana, hii inaweza kuleta kikwazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo yanayokuja yanaenda kupandisha kodi kutoka asilimia saba mpaka kwenda asillimia10, sina uhakika kama tumefanya utafiti wa kutosha kwa nchi zinazotuzunguka wao kodi yao iko vipi, hofu yangu hapa ni kwamba tunaweza kuweka kodi hii tukajikuta tunarejesha tatizo la utoroshaji wa madini kwenda nje. Hivyo ile tamaa yetu ya kuona viwanda hivi tulivyovianzisha vina pata malighafi tukajikuta tunajipiga risasi wenyewe kwenye mguu wetu kwa madini haya kusafirishwa kwenda nje; naiomba Serikali iliangalie vizuri suala hili. Nayasema haya kwa sababu wakati tukiongeza hivi tukumbuke kuwa zipo taasisi nyingine na zenyewe zinaweka tozo kwenye sekta hii hii. Leo hii tunapozungumza watu wa mabonde, Bonde la Ziwa Victoria na kwingineko wanamtoza shilingi milioni sita kwa mwaka mchimbaji mdogo. Kwa hiyo tuangalie jambo hili lisije likawa kikwazo kwenye ukuaji wa sekta yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kwenye eneo la kilimo cha alizeti, naipongeza Serikali kwa jitihada hii. Sisi Mkoa wa Tanga tuliwekwa kwenye mazao saba ya kimkakati, kwa maana ya zao la mkonge, lakini Mkoa wa Tanga umebarikiwa, kwamba unapata mvua mara mbili kwa mwaka. Hivi kwa nini tusiitumie fursa hii ya upatikanaji wa mvua mara mbili kwa mwaka tukauingiza Mkoa wa Tanga kuwa miongoni mwa mikoa inayolima zao la alizeti? Kwa sababu kilimo cha mkonge kinachukua miaka mitatu kuanza kuzalisha, sasa katika kipindi cha hapa katikati ardhi ile inaweza kutumika kuzalisha mazao ya mafuta haya. Kwa hiyo naiomba Serikali iangalie eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema haya kwa sababu huko nyuma mzee Kingunge marehemu alipokuja kuwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga alifanya uamuzi wa kuhakikisha mashamba yote ya mkonge yanatumika kulima kilimo cha mazao ya mahindi; na katika kipindi kile Mkoa wa Tanga uliongoza katika Taifa hili kwenye uzalishaji wa mahindi. Tukitumia mtazamo huu tunaweza kusaidia kukuza uzalishaji wa mazao ya mafuta katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni kuhusu mapendekezo ninayoyaona yanakuja hapa ya kikodi kwenye zao la mkonge. Nataka niipongeze Serikali kwamba ilifanya kazi kubwa sana ya kufufua zao hilo la mkonge, hamasa kubwa iliingia na mifumo ya kikodi iliyokuwa imewekwa ilikuwa inamuhakikishia mkulima kuwa na bei inayotabirika na bei nzuri. Mapendekezo haya yanayokuja yanakwenda kuua hamasa ya kulima zao la mkonge yanakwenda kumsababishia mkulima mdogo aweze kupata bei ndogo na hivyo ulimaji au ufufuaji wa zao hili unakwenda kuanguka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iangalie upya jambo hili eneo la produce cess na lile lingine hebu tuangalie vizuri. Yupo mtu tumempa jambo hilo atalizungumzia vizuri ndugu yangu Mnzava, lakini naomba sana Serikali mliangalie kwa umakini eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwa kutanua wigo wa kodi. Ni jambo ambalo tumekuwa tukihangaika nalo kwa muda mrefu, nikupongeze Mheshimiwa Waziri umekuwa na ubunifu mkubwa sana, hongera sana. Lakini yapo maeneo mengine hebu tuyaangalie. Tunapofanya uagizaji wa mafuta kwa pamoja kwa sasa hivi kampuni zinazoagiza mafuta kutoka nje hazijasajiliwa hapa. Kwa hiyo kunakuwa na shida ya ushindani kati ya kampuni za wazawa zilizoko hapa na zile za kutoka nje. Za kutoka nje hazilipi cooperate tax na service levy. Hii inasababisha ushindani kati ya kampuni hizi za nje na hizi za ndani unakuwa si sahihi. Hebu tuangalie eneo hili tuweze kuona kama tunaweza kutumia mwanya huu kuweza kuongeza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya nakushukuru sana, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia kwenye Hotuba ya Waziri Mkuu. Nianze kwa kumshuruku Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema ambaye ameturuzuku uhai na pumzi hii tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue fursa hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa inayofanyika katika nchi yetu. Tumeona kazi kubwa inayofanyika kwenye Sekta ya Afya, tumeona kazi kubwa inayofanyika kwenye Sekta ya Elimu, tunaona kazi kubwa inayofanyika kwenye barabara za vijijini, hongera sana kwa Serikali. Tunaomba kazi hii iendelee ili tuweze kuwaondolea wananchi matatizo yanayowakabili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii vilevile kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara ambayo aliifanya kwenye Jimbo langu la Mkinga, ziara ambayo imeleta chachu ya maendeleo katika Wilaya yetu. Hapa nitazungumzia kiujumla. Kuna kazi kubwa inafanyika kwenye vituo vyetu vya mipakani kwa facilitate biashara na kuingiza mapato kwenye nchi yetu. Kwa kipindi kirefu, border yetu ya Horohoro ilikuwa haifanyi vizuri, lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja, amefanya kazi kubwa, na leo hii tunasimama kifua mbele, border ile inaingiza mapato mengi sana kwa nchi yetu. Tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati naipongeza, yapo mambo ambayo tunayaona Mkinga na tunahisi vilevile kwenye maeneo mengine ya mipakani yapo. Pamoja na kazi kubwa iliyofanyika hii ya kukusanya mapato, lakini kituo chetu kile kina matatizo ya miundombinu ya usafiri. Kuna matatizo makubwa ya vifaa vya usafiri na vile vile kuna tatizo la huduma ya zimamoto. Vituo hivi vinakuwa na shehena kubwa ya mizigo. Naiomba Serikali iangalie uwezekano wa kuwezesha kupata fire equipment katika maeneo ya mipakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Mkinga inapakana na nchi ya Kenya na mpaka wetu kule ni porous, kwa hiyo, tunahitajika kufanya ulinzi wa mara kwa mara; kufanya doria ya mara kwa mara. Tatizo tunaloliona, watu wetu wa vyombo vya usalama wana matatizo makubwa ya vyombo vya usafiri. Sasa naomba Serikali iangalie hili kwa jicho la pekee kwa Mkinga. Ninaposema hivi Serikali mnaelewa, position ya Mkinga tunahitaji kufanya doria ya nguvu, mambo ya uhamiaji haramu mnayajua, tusaidieni watu wetu wa Polisi wapate gari waweze kufanya shughuli zao vizuri.

Mhehsimiwa Naibu Spika, vilevile Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja kwenye ziara yake alitoa maagizo baada ya kusikia wananchi wana matatizo ya ardhi. Naishukuru Serikali inalifanyia kazi jambo hili kupitia kikosi kazi cha timu ya Mawaziri. Rai yangu, kikosi kazi hiki kinapofanya kazi nchi nzima, lazima kioanishe na ahadi walizotoa viongozi wetu. Kikosi kazi hiki kikienda kufanya shughuli kikasahau kutekeleza ahadi za viongozi wetu, tutakuwa tumewadhalilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja Mkinga, alisikia kilio cha wananchi wa Mkinga, pale Maramba hawana ardhi, akaagiza kazi ifanyike ya tathmini ya tatizo lile mwezi wa Pili mwaka 2020. Miezi sita baadaye Waziri Mkuu aliporudi Tanga, akatoa tamko akiwa Lushoto kwamba wanaenda kumega ardhi ya Shamba la Mwele ili wananchi wapate ardhi. Alipokuja Mkinga wiki moja baadaye akatoa agizo kwamba Serikali inaenda kumega sehemu ya shamba ili wananchi wale waweze kupatiwa ardhi. Tunaposema hapa ni kwa sababu ya tatizo kubwa la ardhi kwenye vijiji vile vya Maramba A na Maramba B.

Mheshimiwa Naibu Spika, Maramba A yenye kaya 1,747 umiliki wa ardhi kwa kila mwananchi mmoja, ni asilimia 0.36 ya hekta; Maramba B yenye kaya 725, umiliki wa ardhi ni asilimia 0.6. Huu ni umasikini mkubwa kwa wananchi hawa. Tunampongeza Waziri Mkuu, aliliona hili. Tunaiomba Serikali, ahadi hizi za viongozi wetu wa wakuu ziweze kufanyiwa kazi. Hili linaenda sambamba na kazi kubwa iliyokuwa imefanyika tangu mwaka 2016 na kikosi kazi kilichoundwa na Serikali, kikafanya kazi kubwa ya kuzunguka vijiji vyote vinavyohusisha Pori Tengefu kwenye Wilaya ya Muheza, Wilaya ya Korogwe na Wilaya ya Mkinga. Maagizo yale tuliyokubaliana, tunaomba yahusishwe kwenye shughuli hii inayoendelea sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwenye Huduma ya Afya imetupatia Hospitali ya Wilaya. Naomba sasa hospitali hizi zijengewe wodi ili wananchi waweze kupata huduma za uhakika. Tumeahidiwa kwa kuda mrefu bandari ya Moa, ambazo ni bandari bubu, kwamba sasa inaenda kuwekewa miundombinu ili biashara kati ya Mkinga na Zanzibar, Mkinga na Pemba iweze kuwa facilitated. Tunaomba ahadi hiyo iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru Serikali kwa jitihada za reli zinazofanyika; maendeleo kwenye sekta ya reli, lakini tunachokiona ni kwamba ujenzi wa reli ule hauendi sambamba na reli nyingine. Reli ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha imesahaulika, kazi inayofanyika sivyo kama tulivyokuwa tumeahidiwa mwanzoni. Tunaomba na reli ile iweze kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba ya Wizara ya Maji tunayoijadili. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameturuzuku uhai na ameendelea kutuongoza.

Mheshimiwa Spika, nitangulie kusema naunga mkono hoja hii. Natangulia kuunga mkono hoja hii kwa sababu ya kazi kubwa inayofanyika. Nataka nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa jinsi alivyoonesha nia ya dhati ya kuhakikisha tunaondokana na tatizo la maji kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwapongeze Waziri na timu yake Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya. Tumeanza kuona mabadiliko ya jinsi tunavyoshughulikia sekta yetu ya maji. Miaka miwili mitatu iliyopita tulikuwa tukija hapa tunalalamika jinsi ambavyo fedha zinapotea kwenye miradi ambayo haioneshi manufaa. Kwa kiasi kikubwa hili tumeweza kulidhibiti, hongereni sana Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili niwashukuru Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Watendaji ndani ya Wizara hii kwa jinsi ambavyo mmetukimbilia watu wa Mkinga. Nimekuwa nikipiga kelele katika Bunge hili kwa tatizo la maji katika Wilaya ya Mkinga na kuna wakati nilisema kama kuna Wilaya katika Mkoa wa Tanga yenye tatizo kubwa la maji ni Mkinga, mmeanza kutuelewa tunawashukuru. Watendaji wote wakubwa wa Wizara mmefika Mkinga kuja kuona tatizo na ninyi mnajua kwamba, tatizo Mkinga ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie kwa mwaka huu tatizo limekuwa kubwa zaidi tofauti na mlivyokuwa mnalifahamu. Mabwawa yetu ambayo walao yalikuwa yanatusaidia, mabwawa matano yamekauka, kwa hiyo wananchi wetu wa Kata zile ambazo mlikuja kuzitembelea walikuwa na shida kubwa ya maji kwa sababu mabwawa yalikauka, walikuwa hawana uwezo wa kupata maji tena. Kwa hiyo, tunapoona jitihada hizi za timu yako kuja kwenye Jimbo kuandaa na kutengeneza mradi ule wa kutoka Mto Zigi mpaka kule Horohoro na kwa ahadi ile mliyotupa kwamba, mwezi wa Sita mradi ule unaanza, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba ahadi ile iwe kweli. Mwezi wa sita tuliokubaliana mradi ule uanze. Vijiji vile 24 vitakavyoguswa na mradi huu viweze kupata maji. Tuweze kufungua ukanda ule wa bahari wa Mkinga ili hoteli na shughuli za kiuchumi ziweze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, malengo ya Sustainable Development Goal yanaiweka sekta ya maji kwenye lengo Namba Sita, ambayo tunasema tunajielekeza kwenye upatikanaji wa clean water and sanitation. Na kwa nini tumeweka lengo hili kama dunia? Ni kwa sababu ya changamoto kubwa ya kidunia iliyokuwa inaonekana kwamba watu Bilioni 2.6 walikuwa hawana uhakika wa maji. Watu Milioni 1.63 watoto wenye umri wa miaka mitano wanapoteza maisha kila mwaka kwa sababu ya tatizo hili. Dunia ikaamua kwamba maji sasa iwe ni human right. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiliacha hilo lipo lile la kawaida ambalo kila siku tunaambiana, maji ni uhai. Tumesema hivyo tumezoea-zoea tunaona ni jambo la kawaida tu, lakini vilevile maji ni ulinzi kwa nchi. Tunaziona nchi zinapigana vita kwa sababu ya maji, kwa hiyo sekta hii hatuwezi kuipuuza hata kidogo. Waziri kwenye takwimu zako umetuambia lengo letu ni kufikisha aslimia 85 ya upatikanaji wa maji safi na salama vijijini, ukurasa wa nane. Leo hii tumefikia asilimia 74.5 bado tuna safari. Katika eneo ambalo halipaswi tushindwe kufikia malengo ni kwenye sekta ya maji. Nawaomba Wabunge wenzangu tufanye kila linalowezekana Wizara hii iweze kupata fedha za kutosha tuweze kuondokana na tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri mlipokuja kutembelea miradi yetu Mkinga tulikwenda kule Mwakijembe. Bwawa lile lilishindwa kuendelea, tuliingia kwenye mgogoro na Mkandarasi tukaenda kwenye arbitration. Tangu mwezi Disemba arbitration imeisha, tuna kigugumizi gani cha kuhakikisha tunampata Mkandarasi mwingine wa kuweza kutekeleza mradi ule? Huu ni mradi ambao umesimama kwa miaka mitatu Mheshimiwa Waziri. Ni mradi ambao upo kwenye Kata ambayo haina mradi wowote wa maji ya bomba. Tuna mabwawa mawili kule, tuna bwawa la Mwakijembe ndiyo hoi, tuna Bwawa la Mbuta.

Nimekuja wiki iliyopita tumekaa tumezungumza, tulisema tukamilishe ujenzi, tumefikia hatua nzuri, lakini kuna certificate pale. Umeniahidi kwamba hivi karibuni Milioni 90 zile zitapatikana, naomba zipatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekubaliana kuna kazi ile ya kukamilisha ujenzi wa kuweka zege na kwenye utoro wa maji ili bwawa lile lisije likapasuka tikapoteza fedha zote tulizozifanya. Mvua sasa zimeanza, sio nyingi kihivyo, lakini tukichelewa zikija mvua kubwa Bwawa lile likapasuka kazi yote tuliyoifanya itakuwa haina maana. Naomba tulifanyie kazi jambo hili kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru kwa miradi ya Gombero na Mhinduro. Taarifa nilizonazo ni kwamba, negotiations zimekamilika. Tunaomba tuweze kumuita kwa haraka yule Mkandarasi tuingie mkataba ule ili kazi ile ianze. Ninawashukuru kwa mradi wa mapatano nimeambiwa mradi umeshasainiwa, kuna Saini kama moja tu imebaki, naomba tusaini kwa haraka ili mradi ule nao uweze kufanyiwa kazi, huku kwenye miradi hii ndiko chanzo cha Mto Zigi, wao bado wanayatazama maji yanakwenda kunywewa Tanga. Tunaomba tuwakamilishie miradi hii ili na wao waone thamani ya kulinda vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, nichukue fursa hii kuwashukuru kwa miradi ile ya UVIKO, tunashukuru kazi kubwa imefanyika. Nitumie fursa hii kuwashukuru wenzetu wa Nyota Foundation, tulipopata tatizo kubwa lile la ukame mabwawa kukauka walitukimbilia wakatuchimbia visima vitano. Walituchimbia kisima pale Horohoro kijijini, wametuchimbia kisima Horohoro border, wametuchimbia visima viwili Maforoni, wametuchimbia kisima Mwakikonge na bado wanaonesha nia ya kuendelea kutusaidia. Tunawashukuru sana, nachukua fursa hii kuwashukuru kwa niaba ya wananchi wa Mkinga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wakati nikishukuru kwa ajili ya uchimbaji huu wa visima, nikushukuru kwa nia nzuri mliyoifanya kwenye bajeti ya mwaka huu ya kuidhinisha visima vitatu kwa Kata ya Mwakijembe na kule Horohoro. Masikitiko yangu ni kwamba…

SPIKA: Sekunde 30 malizia, kengele imeshagonga.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, imechukua mwaka mzima kuweza kupata mkandarasi wa kuchimba visima vile. Kama inawezekana twendeni tukawape hawa Nyota Foundation na timu yao visima vile vichimbwe tuweze kuondokana na tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba nijielekeze kwenye kuchangia bajeti ya Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, napenda nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima. Niishukuru sana Serikali kwa kutupatia fedha takribani shilingi bilioni saba hivi kwa ajili ya maendeleo na matumizi mengineyo lakini vile vile kwenye upande wa barabara lakini na pia kwenye miundombinu ya shule zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili la barabara tulipangiwa kupata shilingi bilioni mbili, tuna shilingi bilioni moja na milioni 300. Tunaomba zile fedha nyingine zilizobakia karibu shilingi milioni 700 zipatikane tuweze kukamilisha miradi iliyopo. Vile vile kwenye eneo la miundombinu ya shule tuna shilingi milioni 692, tunaenda kujenga shule mpya ya msingi. Tuna ujenzi wa madarasa na matundu ya vyoo na hizi tunazielekeza kwenye maeneo ya Maramba JKT, Mazola Kilifi, Mtimbwani, Kisiwani A na Perani. Tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la Sekta ya Afya tunaishukuru Serikali kwa kutuanzishia ujenzi wa Hospitali ya Wilaya na hivi ninavyozungumza tumeshaanza kutibu wagonjwa wa nje lakini bado changamoto ni kwenye matibabu ya kibingwa kwenye kuwalaza wagonjwa na kufanya upasuaji ambao bado tunatumia Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga yaani Bombo. Naiomba sana Serikali itupatie fedha tukamilishe ujenzi wa wodi na vifaatiba ili hospitali hii iweze kuwa kwenye full swing.

Mheshimiwa Spika, vile vile tulileta maombi maalum tulipopewa fursa ya kuelezea maeneo ambayo tuna changamoto za sekta ya afya kwenye vituo vya afya. Tunashukuru tulipata Kituo cha Afya kimoja pale Daluni, lakini kuna eneo la kimkakati tulilolielezea ukanda ule wa Mpakani. Tulileta maombi rasmi ya Kata ya Mwakijembe ambayo wananchi wetu wanalazimika kwenda kupata huduma ya afya upande wa pili wa Nchi ya Kenya. Kwa sababu kutoka Mwakijembe mpaka Makao Makuu ya Wilaya ni kilometa 80.

Mheshimiwa Spika, tuna changamoto kubwa tuna aibu pale kwa sababu wananchi wetu hasa akinamama wanalazimika kwenda kujifungua Kenya, kwa hiyo watoto wanaozaliwa wanasajiliwa Kenya, hii siyo sawa. Tunapokuja kuwapa usajili raia wetu tunapata changamoto. Naomba kwa mara nyingine hebu tuweke mkazo kwenye eneo hili ili wananchi wetu wapate huduma stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili niliomba vile vile Zahanati ya Jasini ambayo na yenyewe inapakana na wenzetu wa ukanda wa Kenya na wananchi wetu hawa wanaenda kupata huduma kule. Wananchi wameshaanza ujenzi wa Kituo cha Afya kule Mwakijembe, wamekwishaanza ujenzi wa zahanati. Tunaomba jitihada ya Serikali tuwasaidie wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni eneo la elimu. Tunaishukuru Serikali kwa kazi inayofanya kwenye Sekondari yetu ya kidato cha tano na sita cha Mkingaleo. Tumepata fedha pale za kukamilisha ujenzi wa mabweni. Tunaomba sasa kuna ahadi pale ya Dada yangu Ummy akiwa kwenye Wizara hiyo alituahidi kujenga uzio, Wizara itajenga uzio kwenye shule ile kwa sababu tuna watoto wa kike pale na Walimu wanaishi nje ya shule ile kwa hiyo ni hatari sana kwa malezi ya watoto wetu lakini vile vile tulikuwa tumeahidiwa ujenzi wa nyumba ya Mwalimu. Tunaomba hili na lenyewe lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali baada ya kuona jitihada zetu tulizozifanya kwenye Shule ya Sekondari ya Zingibari ya maandalizi ya kuipandisha hadhi kuwa kidato cha tano na cha sita. Tulipata fedha takribani shilingi milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ambayo yanakamilika. Tumeomba kwamba shule ile sasa mwezi wa saba iweze kupata wanafunzi iweze kuanza. Tunaomba kibali hicho kiweze kupatikana kwa sababu tayari maombi haya tumeshayapeleka, yapo Wizarani. Sambamba na hilo tunaomba tuweze kujengewa bwalo kwenye shule ile ili wanafunzi wale waende kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na Sekondari ya Zingibari tumeomba kibali maalum kwa ajili ya Shule ya Sekondari ya Doda. Tunaomba kibali kile kipatikane ili sekondari ile iweze kuanza.

Mheshimiwa Spika, mwisho, ni eneo hili ambalo linazungumziwa, la watumishi. Wilaya ya Mkinga tuna uhaba wa watumishi takribani 87. Katika hao 87, watumishi 67 ni Walimu wa masomo ya sayansi, 20 ni Walimu wanaokuja kwa ajili ya shule hizi mbili mpya ambazo tumeziombea kibali. Tunaomba sana Serikali itupe jicho la upendeleo kwa ajili ya mahitaji hayo. Mwisho kila mmoja anayesimama hapa anazungumzia jinsi ambavyo kila Mbunge hapa ana maombi ya vijana wetu kwa ajili ya kupata ajira.

Mheshimiwa Spika, unapoona vijana hawa wanaenda kwamba tumaini lao ni Wabunge wawafanyie jitihada za kupata ajira maana yake mifumo yetu inatiliwa mashaka. Naomba tutumie maarifa ya ziada kuhakikisha kwanza tunajenga imani ya vijana wetu, wakiomba kupitia mitandao waamini kwamba watapata hizo ajira. Vile vile tuone jinsi ya ambavyo utaratibu tunaoutumia utamwingiza kila mmoja wetu isionekane kuna upendeleo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, ambaye imempendeza ameturuzuku uhai kwa siku ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kwenye Wizara hii ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu na ni muhimu sana kipekee kwa sisi watu wa Ukanda wa Pwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru Serikali, tulikuwa na kilio cha muda mrefu cha kutokuwa na mnada wa uhakika pale kwenye border yetu ya Horohoro. Mnada ule umekamilika, tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pamoja na kukamilika kwa mnada ule na wananchi wale kufurahia jambo lile, lakini mnada ule umekuwa kero kwa sababu tangu kukamilika kwa mradi ule mwanzoni mwa mwaka huu mpaka leo mnada ule haujafunguliwa. Mheshimiwa Ulega, hili unaliweza, nakuomba sana. Tukimaliza tu Wizara yako, assignment ya kwanza nakuomba ndugu yangu twende tukafungue mnada ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mkandarasi yule anakataa kukabidhi kwa sababu anatudai karibu milioni 100. Hizi tuna uwezo nazo, twendeni tukafungue mnada ule. Tunapoteza fursa ya mapato kwa sababu hali ya upande wa pili kwa wenzetu Kenya ni mbaya kwenye minada yao. Kwa hiyo, tukifungua mnada ule tumepiga bao. Twende tukafanye jambo hili kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana tuliomba majosho kumi tukapata mawili, si haba, tunaishukuru Serikali tulipata jumla ya milioni 46 tukapeleka Kibewani na kule Mkota. Tunaomba yale yaliyobakia mtufikirie.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile pale Duga tuna josho ambalo tulilijenga tangu mwaka 1972; limechakaa. Nakuomba sana josho lile ni muhimu lifanyiwe kazi kwa haraka hususan kwa hili ambalo mmelifanya jambo kubwa la kuleta mnada mkubwa pale Horohoro. Tunaiomba sana Serikali iangalie eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru Serikali na sisi ni wanufaika kwenye maeneo yale ya kupata boti. Pale Zingibari ndugu zangu wamepata maboti, ndugu zangu wa Mwaboza wamepata boti na tunaye mvuvi mmoja mwingine binafsi na yeye amepata boti; tunashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mmekuwa mkitusaidia kutoa mbegu kwa wakulima wetu wa mwani, tunashukuru sana. Lakini tunahitaji kuongeza jitihada. Mwani unazalishwa kwa wingi lakini uongezaji wa thamani ni mtihani. Tunaomba sana Serikali mliangalie eneo hili; kuongeza thamani ya mwani wetu ili wananchi wale waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu, Mheshimiwa Ulega, mlituahidi kwamba mtatujengea kituo cha kutotoa vifaranga. Ahadi hii kama umeisahau vile; nakuomba ikumbuke ahadi hii. Tunashukuru mnatuletea Mradi wa Bahari Mali kwa kushirikiana na wenzetu wa IUCN ambapo vikundi vyetu vitatu vitakuwa sehemu ya mradi ule; tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba – ndugu yangu Waziri unajua, ukipeleka jambo zuri kama hili kwa watu wenye uhitaji ambao ni wengi, jambo lile badala ya kuwa neema linageuka kuwa kero. Ninawasihi sana, sambamba na mradi huu, Serikali angalieni maarifa mengine ya kuongeza ukubwa wa mradi huu ili wananchi wetu wa Ukanda wa Pwani waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nimeisikia bajeti yako, eneo moja limenisikitisha; tumeingiza lita milioni 11.6 za maziwa zenye thamani ya bilioni 22. Hizi ni fedha ambazo tungeweza kuwasaidia wananchi wetu tukazalisha maziwa kwa wingi ndani ya nchi tukaokoa fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesafirisha maziwa kwenda nje lita 278,000. Kwa hiyo, ukiangalia uwiano tumeingiza zaidi kuliko tulivyouza nje. Tuliangalie vizuri eneo hili, hatuna sababu ya kuagiza maziwa nje, tuna uwezo wa kuzalisha maziwa ndani ya nchi yetu tukajitosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia makusanyo ya Wizara, na Kamati imefanya kazi nzuri, imetuonesha; hali hairidhishi. Tulikusudia kukusanya bilioni 80, tumekusanya bilioni 30; only 37 percent; hii haiwezi kuwa sawa. Tuongeze maarifa zaidi tukusanye zaidi, tuna uwezo wa kufanya hivyo. Na hasa kwenye sekta ya uvuvi, tulikusudia kukusanya bilioni 40, tumekusanya bilioni 13; only 33 percent.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage amesema pale; kwenye eneo hili la uvuvi na ufugaji wa samaki hatupaswi kuwa na kiwango hiki. Yaani mchango wa sekta ya uvuvi kuwa asilimia moja haiwezi kuwa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sekta ambayo ulimwenguni uingizaji wake ni mkubwa sana, hatujafanya vizuri, tuongeze bidii kwenye eneo la ufugaji wa samaki ili tuondoe umaskini kwa wananchi wetu, tujihakikishie usalama wa chakula na lishe katika nchi yetu. Sekta hii ina uwezo wa kututoa. Hatuwezi kusifiwa kuwa nchi ya maziwa makuu, hatuwezi kusifiwa kwamba ni nchi yenye ukanda mkubwa wa bahari lakini ufugaji wa samaki haueleweki; hii haiwezi kuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu, Mheshimiwa Ulega na timu yako uliyonayo sasa, najua tukiamua kuweka mkazo kwenye eneo la ufugaji wa samaki tunaweza kupiga bao. Na hiki kigugumizi cha ufugaji wa samaki kwenye Ukanda wa Pwani kinatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ulega, wewe mtu wa pwani, unajua umaskini wetu watu wa pwani wakati tuna rasilimali ya bahari. Twendeni tukafanye kazi ya kuwaondolea wananchi umaskini kupitia ufugaji wa samaki kwenye eneo la ukanda wa bahari.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru; ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nichangie kwenye hoja iliyoko mbele yetu. Nataka nitumie fursa hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayofanya kwenye Wizara hii, tuna imani naye tunachomuomba aendelee kuweka umakini katika kusimamia sekta zilizoko chini ya Wizara hii. Nataka nimpongeze sana ndugu yangu Mnzava ambaye ameeleza vizuri jambo hili kwa maslahi ya watu wa Mkoa wa Tanga na uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa spika sisi watu wa Tanga ni wahanga wa uwekezaji, siye tumegongwa na nyoka kwa hiyo, tukiona unyasi lazima tushtuke. Mwaka 2017 alijitokeza muwekezaji akiitwa Hengia akionesha nia ya kuwekeza kenye sekta ya saruji katika nchi hii na kiwanda kile alikuwa aje akijenge Mkinga. Mwaka 2019 TIC ilimpa leseni aje awekeze, mwaka 2020 akaanza kutoa fidia kwa ardhi aliyoitwaa kule Mkinga wananchi wakaachia maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, tangu wakati huo fidia stahiki haijatolewa, hivi ninavyozungumza wako wananchi 143 wa Mkinga kutoka Kwale na Mtimbwani wanadai Zaidi ya milioni mia tano na sabini na kitu hivi hazijalipwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilituma timu ikaja kukaa na uaongozi wa Mkoa na uongozi wa Wilaya na mwekezaji, wakakubaliana ifanyike kazi ya tathmini isiyo na shaka ili watu hawa walipwe, kazi imekamilika. Mwekezaji huyu wamepelekewa amegoma kulipa viwango stahiki vya kisheria.

Mheshimiwa Spika, hawa ni wananchi wamepoteza ardhi zao, hawana ruhsa ya kuingia kwenye maeneo yale mpaka leo hawalipwi. Kwa nini mwekezaji halipi? Ni kwa sababu ana machungu nilisema hapa kwamba jamani uwekezaji huu wa Hengia ambao wakati ule kama ungefanyika mwekezaji alikuwa anakuja kujenga kiwanda chenye thamani ya trilioni 2.3 uzalishaji wa saruji alikuwa anaenda kuzalisha tani 7,000,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, nimesikia taarifa ya Wizara hapa inazungumzia kwamba leo viwanda 14 tunazalisha tani 10,000,000 tulikuwa na mwekezaji ambaye alikuwa tayari kuja kuwekeza mtaji wa trilioni 2 azalishe tani 7,000,000,000 tuka–frustrate, nilikuja kusema maneno haya hapa nikasema wapo watendaji wetu hawana nia njema wanam–frustrate mwekezaji, wapo watu ndani ya industry ya saruji hawataki mwekezaji huyo awepo kwa sababu ataleta ushindani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunapozungumza tumepoteza uwekezaji ule, watu wa Tanga tuna machungu, tumegongwa na nyoka tukiona unyasi tunashtuka. Naiomba Serikali tathmini hii ilifanywa na timu ya Serikali Mheshimiwa Waziri nakuomba simamia ndugu zetu wale wa Mkinga 143 walipwe stahiki zao.

Mheshimiwa Spika, Sasa kwa muktadha huo huo, linapokuja suala la uuzaji wa hisa za Tanga Cement sisi hatuna hatupingi, lakini tunasema taratibu zifuatwe, watu wa Tanga leo hii pale Tanga tuna viwanda nane, baada ya kubinafsishwa vimegeuka kuwa magodauni vimegeuka kuwa magofu havifanyi kazi. Hatutakuwa tayari kuona Tanga Cement inabinafsishwa inageuka kuwa godauni mtu anakuja kuchukua raw materials Tanga anakwenda kuzalisha Dar es Salaam hilo hatutaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Viwanda vile nane tumehangaika ndani ya Serikali ili wawekezaji wale waheshimu mikataba yao wakati wanauziwa viwanda vile Serikali mmeshindwa kulisukuma hili, hii ndio hofu yetu, watu wa Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaiomba Serikali taratibu zifuatwe uwekezaji ufanyike tujenge confidence ya wawekezaji tunapata shida kwenye sekta ya madini kila mwekezaji anayetaka kuja akija anang’ang’aniza kwamba kukiwa na disputy twende tukaamuliwe mashauri hayo nje ya Tanzania, kwa nini? Kwa sababu wanasema mahakama zetu haziaminiki. Kama kuna jambo lililoamuliwa kisheria tusikiuke maamuzi yale yaliyoamuliwa kisheria.

Mheshimiwa Spika, kila muwekezaji kwenye sekta kule akija anaenda kujificha kwenye maeneo ambayo tuna mikataba ya kimataifa kwa hiyo anaenda kujisajili kampuni kwenye maeneo hayo ili mashauri yake yasiamuliwe Tanzania yaende kule. Tukiendelea kukiuka maamuzi ya vyombo vyetu vya kisheria tunaenda kupeleka ujumbe kwamba tusitumie mahakama zetu za ndani mashauri yote yakaamuliwe nje, hii haiwezi kuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye hoja iliyoko mbele yetu. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kuendelea kutulinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na eneo la mipaka katika eneo letu la bahari, tuna changamoto kule Mkinga kwenye mpaka wetu na Kenya na changamoto hii ni ya miaka mingi. Mheshimiwa Waziri nafurahi uliwahi kuja Mkinga tukatembelea mipaka yetu kwenye ukanda wa ardhi, lakini tukaenda vilevile Kijiji cha Jasini kwenye ukanda ule wa baharini, uliziona changamoto zetu, nakumbuka ulifika kwenye nyumba ile upande mmoja ni Kenya na upande mmoja ni Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto yetu kubwa, hili la watu kujenga mpakani kabisa tunalisema kiutani utani hivi, lakini athari yake ni kubwa. Niliwahi kusema hapa kwamba wenzetu wa vyombo vya ulinzi vya Kenya wanafika mpaka ndani ya maeneo ya kijiji chetu wakiwa na silaha. Nikasema ni hekima tu za viongozi wa Serikali wakati ule vilisaidia tusiingie kwenye mgogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja tena leo kwa unyenyeku mkubwa naiomba Serikali yangu itusikie. Mwaka 1972 kilifanyika kikao cha kujadili jambo hili la mgogoro wa mpaka, tarehe 8 Mei kikao kilifanyika pale Mombasa; tarehe 4 Septemba, 1975 tulifanya kikao Dar es Salaam; tarehe 9 Julai, 1976 Mawaziri wetu wa nchi mbili hizi aliyekuwa Waziri wetu wa Mambo ya Nje, Mheshimiwa Ibrahim Kaduma na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Dkt. Munyua Waiyaki walisaini document ya makubaliano inayoonesha mambo kadhaa na document ile niliwahi kuileta Wizara na leo tena nitaiweka mezani ili iwe rejea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa pamoja na makubaliano yale kupitia document hii bado kumekuwa na chokochoko hizo. Vyombo vya ulinzi vya Kenya vikiingia kwenye eneo letu, wananchi wetu wa Jasini wanapoenda kuvua wakikamatwa baharini wakapelekwa Kenya kwenda kufunguliwa kesi, mali zao zikataifishwa. Sisi kama Taifa lazima jambo hili tulichukulie kwa uzito mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa mwneyekiti, maboya tuliyoweka ya mipaka kule baharini yameharibiwa, sitaki kusema ni makusudi, lakini nasema yameharibiwa. Wakati hali ikiwa hivi nataka niikumbushe tu au niiambie tu Serikali kwamba kwenye ukanda huu tuna leseni ya utafiti wa mafuta, kwenye ukanda huu tuna leseni ya utafiti wa madini, madini ya kimkakati baharini, lakini wakati hali ikiwa hivi kwenye mpaka wa Kenya na Somalia ambapo kuna dalili zote za kupatikana mafuta kuna mgogoro sasa hivi kule, sijui naeleweka? Tusingoje utafiti utuambie tuna mafuta halafu tushindwe kuyachimba. Tusiache kuchukua hatua watu wetu badala ya kwenda kuhukumiwa Kenya ikafika mahali vyombo vyao vikazamishwa baharini tukapoteza maisha ya watu wetu, nawaomba tuchukue hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili Mheshimiwa Waziri ni jambo ambalo nimelizungumza katika kipindi chote cha Ubunge wangu ni shamba la kwa Mtili, zaidi ya miaka kumi nalizungumza jambo hili. Miaka kumi na zaidi nalizungumza jambo hili, kuna shamba pale limetelekezwa na anayejiita mwekezaji, zaidi ya miaka 25 limetelekezwa. Huyo mwekezaji hayupo, wameshafariki, wapo tu watu wanasimamia kiujanja ujanja pale wakiwakodisha wananchi wetu kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ilituagiza mwaka 2012 ikatumwa ilani ya kufuta shamba lile, lakini ikaonekana ina makosa mwaka 2017 ikatumwa ilani nyingine, mlipotupa shamba lile la kule kwenye kata kule ambapo kipo Kijiji cha Jasini, Kata ya Mahemboni kule nikawaambiwa kuna shamba lingine, tunaomba na hili mlishughulikie, aliyekuwa Waziri wakati ule Mheshimiwa Lukuvi akatuma timu kwenda kufanya uhakiki. Ikaonekana ni kweli, imetumwa ilani, baadaye ikaonekana imetumwa kimakosa kwa sababu kalitumwa kaeneo kadogo, ikatumwa timu nyingine kutoka Wizara ikaja kufanya tathmini, mkajiridhisha kwamba shamba lile limetelekezwa. Ikatumwa ilani nyingine, lakini baadaye ikaambiwa eti huyu jamaa miaka ya 1960 alichukua mkopo mahali huko nje, kwa hiyo tukatuma ilani nyingine kwenye hizo benki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilani hizi zimepita zaidi ya miezi saba sasa au nane Waziri unalijua jambo hili,…

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Nimekuja kwako ukaniambia watu wa mkoani wamechelesha, watu wa mkoani wamekamilisha kazi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kitandula naomba upokee taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mnzava.

TAARIFA

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa kaka yangu mzungumzaji anayezungumza, pamoja na mchango wake mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu kumpa taarifa kwamba jambo hili la kupeleka ilani, lakini utekelezaji hauonekani na tunakaa kwa muda mrefu kusubiri sio tu kwa yale mashamba ya Mkinga, hata Korogwe, shamba la Mwakinyumbi zaidi ya miaka saba kila siku ilani zinatengenezwa, utaratibu unakamilika, lakini ufutaji au ubatilishwaji wa miliki mpaka leo haujafanyika. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dunstan Kitandula unapokea taarifa?

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii kwa sababu katika mkoa ambao una changamoto ya ardhi ya mashamba makubwa ya mkonge na mengine yaliyotelekezwa, Korogwe, Mkinga, Muheza tuna changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwneyekiti, ndugu zenu tunapowaambia tusaidieni, kwa hiyo nimeambiwa kwamba taratibu zote zimekamilika jambo hili lipo Wizarani, Wizara naomba mchukue hatua. Wapo watu kule wanazunguka zunguka wanakuja kutafuta fursa tuwaunge mkono kwa sababu yule mmiliki amejua hana ujanja, anataka kuuza eneo lile, tunaomba mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu, ni lile ambalo kila mmoja wetu analisema, nimeisikiliza taarifa ya Kamati, wote tunajua Kamati ndio inafanya kazi kwa niaba ya Bunge. Kamati inaposema kwamba leteni hayo maamuzi kwenye Kamati tuyajadili wanasema kiustarabu tu kwamba hawaridhishwi kuna jambo linakwenda sivyo. (Makofi)

Naomba muisikie Kamati, tulijadili jambo hili, sisi sote ni viongozi tumeaminiwa na wananchi tusikilizane. Tukifanya maamuzi tuyafanye maamuzi kwa manufaa ya Taifa letu. Mheshimiwa Waziri ushirikishwaji unaujua ulivyo na tatizo, unajua timu ile ya Mawaziri ilipokuja Tanga mimi nilishiriki kikao kile kwa namna gani unajua. Sitaki niseme nilivamia, lakini unajua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nasikia kuna timu huko Mkinga inaendelea…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Naomba tuwashirikishe wananchi, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naomba nami nijielekeze kwenye kuchangia hotuba iliyoko mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuturuzuku uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mchengerwa. Nampongeza kwa sababu ameanza vizuri, ameanza kwa usikivu, ameanza kwa kujishusha kwenda kuwatumia Watanzania kwa kuwasikiliza. Mheshimiwa Mchengerwa hongera sana. Endelea kuwa humble katika kuwatumikia Watanzania hawa, endelea kuwa humble katika kumsaidia Mheshimiwa Rais kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo nizungumzie hali yetu kule Mkinga. Tuna changamoto kubwa sana ya uvamizi wa tembo kwenye Wilaya yetu ya Mkinga. Wilaya ya Mkinga ina Kata 22, hivi ninavyozungumza Kata 13 tembo wanavuruga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzoni maeneo yaliyokuwa yanashambuliwa sana ni Daluni, Bwiti, Duga, Gombero na Mwakijembe. Haya ndiyo yalikuwa maeneo yaliyokuwa yanashambuliwa kwa kiasi kikubwa, lakini leo hii tunapozungumza Kata nyingine Barongo Kasera, Mtimbwani, Doda, Moa, Mapatano, Duga Sigaya, nasikia Maramba wamepita na vilevile Mnyenzani wamepita, hali ni mbaya sana. Hali ni mbaya kwa sababu wananchi wanapoteza…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Kuna Taarifa Mheshimiwa Kitandula.

TAARIFA

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba anavyozungumza tembo hali mbaya, kwenye Jimbo la Bunda karibu Kata zote tembo wako barabarani saa hizi, wako makundi 40, 20, 30, Kata zote toka usiku mpaka leo saa hizi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dunstan Kitandula.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge taarifa ni moja.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda huu ni mdogo. Waheshimiwa Wabunge waache wenzao watumie muda waliouomba kuchangia. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa, kuna taarifa nyingine hapa.

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, taarifa inakuwa ni moja. Hajaanza hata kusema taarifa inatoka wapi? Muache aseme kwanza. Mheshimiwa Kitandula naomba uendelee. (Makofi)

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, daah, mambo mengine yanaudhi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mkinga wanataabika, tumeleta maombi baada ya mazao yao kuharibiwa ili waweze kupata fidia, huu ni mwaka wa tatu hakuna kifuta jasho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Kamati ya Siasa ilikuwa inafanya ziara feedback waliyoipata kutoka kwa wananchi, wananchi wamekata tamaa. Wananchi wanasema Serikali inathamini tembo kuliko wananchi, hili si jambo zuri kwa Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi. Twendeni tukawasaidie wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzoni, mazao yaliyokuwa yanaathirika ni mahindi na mikorosho, lakini sasa hali imekuwa mbaya kwenye zao la mkonge. Tembo sasa mkonge ndiyo imekuwa, sijui nisemeje, wanavuruga kwelikweli. Chama cha Wakulima wa Mkonge kule Mkinga kimeleta malalamiko haya nimeyafikisha, hali ni mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Kaka yangu Ngenya tukiwa kwenye bajeti hapa akawa ananitania ananiambia Mheshimiwa Mbunge, naendelea kuwa maskini. Mwaka huu nilikuwa nategemea nianze kuvuna mkonge, tembo wamemaliza shamba zima. Hali, Mheshimiwa Mchengerwa, ni mbaya!

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Naibu Waziri, nilikuja kumueleza mwanzoni mwa mwezi Mei, baada ya siku mbili akaongeza kikosi pale Mkinga. Mheshimiwa Naibu Waziri, tunakushukuru sana, kikosi kile kilienda tarehe 19. Lakini kwa ukubwa wa tatizo hili kikosi kile hakitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tulikuwa tunazungumza asubuhi, tembo wamevamia Mavovo, wamekula mahindi ya wananchi, Kikosi kile kimeitwa kiende Muheza kwenda kufukuza simba, kwa hiyo kule shughuli inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, nakuomba tukimaliza Bunge hili hebu tuende Mkinga ukaone hali. Hali ni mbaya. Mlituahidi kwamba mtakuja kufundisha vijana kumi kwenye kila kijiji, mtawapatia vifaa ili watusaidie tuwe na usimamizi wa karibu, jambo lile halijafanyika, tunaomba fanyeni jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikosi hiki kilichowekwa ni cha muda, tunahitaji kuwa na kikosi pale cha kudumu kwa sababu tatizo ni kubwa. Tunapata tembo kutoka Tsavo - Kenya, tunapata tembo kutoka Mbuga ya Mkomazi. Njooni mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni changamoto ambayo imeletwa na hili tunalolifanya la kutatua migogoro, hatujalifanya vizuri kule Mkinga. Kata ya Mwakijembe kuna kilio, ushirikishaji haukuwa mzuri. Tarehe 30, ilikuja timu kule kwenda kufanya tathmini, timu ile haikushirikisha hata wenyeviti wa vijiji, tunawezaje kufanya mambo haya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wale wanapita wanawaambia wananchi ukifika mwezi Julai mnaondoka. Tunazalisha taharuki bila sababu ya msingi, tunachukua maeneo yao hatuwaambii fidia tunayowapa ni ipi! Mheshimiwa Mchengerwa, nakuomba hebu tuende Mkinga tukaondoe changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulifanya kazi nzuri sana mwaka 2017, tuliwashirikisha wananchi tukapata muafaka wa Kimkoa na Kitaifa, tukasubiri jambo lile sasa tuende tukalifanyie kazi. Kikosi kazi mlichotuma kimekwenda kutupa yale yote tuliyokuwa tumekubaliana, kimekuja na maamuzi yao tofauti ambayo hawakushirikisha wananchi, hatuwezi kufanya hivi! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji kule wanazuiwa, hata sasa wanaambiwa hawatapeleka mifugo yao kwenda kunywa maji kwenye Mto Umba, mto ambao unatiririka kwenda Kenya, wenzetu wananufaika, sisi tunazuia watu wetu. Tunawezaje kufanya mambo haya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, timu ile ya kwanza ilipokuja ilijiridhisha kwamba eneo lile hakuna uwezekano hata wa kuchimba kisima. Kwa hiyo, eneo pekee ni kwenda kunywa maji kwenye Mto Umba. Leo tunawaambia wafugaji wale kwanza tunachukua maeneo yao, hatuwaambii fidia tutakayowapa ni ipi, halafu tunawazuia wasiende kunywesha maji kwenye maeneo yale. This is…

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie kwenye hoja zilizoko mbele yetu. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutupa uhai ili tuweze kulitumikia Taifa letu. Nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja, naunga mkono bajeti yetu. Bajeti nzuri inayoendelea kutoa matumaini kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi anavyoliongoza Taifga letu kuweza kupata maendeleo ya kiuchumi. Wote tunafahamu kwamba bajeti iliyoko mbele yetu, tunazungumzia bajeti ya shilingi trilioni 44.4, ni bnajeti kubwa na ni bajeti inayoenda kugusa maisha ya Watanzania. Lakini kinachofurahisha zaidi ni kwamba takribani shilingi trilioni 30.2 zitatokana na mapato ya ndani ambayo yataweza kusaidia kuendesha bajeti hii, naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile, naipongeza Serikali kwa jitihada inazozifanya katika kuvutia uwekezaji katika nchi yetu. Taarifa zinatuonesha kwamba kuanzia mwezi wa pili mwaka huu TIC imeweza kuidhinisha miradi 162 yenye thamani ya dola milioni 1,833 na miradi hii inakwenda kuzalisha ajira ya takribani 25,900. Hongera sana Serikali kwa jitihada hizi tunazozifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napitia kitabu cha Mpango wa Hali ya Uchumi nikawa naangalia takwimu zilizoko pale ndani; takwimu zile zimenifariji. Wote tunafahamu kwamba ulimwengu sasa unapitia kwenye mdololo wa kiuchumi lakini licha ya kuwepo kwa mdololo wa kiuchumi bado kwenye nchji yetu tumeweza kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwango cha ukuaji wa Pato la Taifa kwa mwaka huu kilikuwa ni asilimia 4.7 ukilinganisha na asilimia 4.9 ya mwaka jana. Sasa unaweza kuona kwamba kuna kushuka kidogo. Lakini tukizingatia athari za kiuchumi zinazotokana na vita ya kule Ukraine na matatizo ya mafuta katika ulimwengu lazima tuseme kama Taifa tumefanya vizuri sana kuhakikisha kwamba tuna-maintain ukuaji wa uchumi wa kiwango hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na jambo linalofurahisha ni jinsi ambavyo Serikali imekuwa na uwekezaji wa kimkakati kwenye miradi ya kimkakati. Wote tumeona uwekezaji mkubwa umefanyika kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, reli, sekta ya maji pamoja na kwenye sekta ya elimu. Uwekezaji huu ndio umetuhakikishia tumekuwa na ukuaji huu unaoridhisha, Serikali hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja tu ambalo tunapaswa kuliangalia kwa umakini ni ukuaji huu wa uchumi. Ukiuangalia kwa kina unaona kwamba sekta zilizochangia ukuaji huu sekta inayoongoza ni sekta ya burudani kwa asilimia 19, sekta inayofuata ni madini kwa asilimia 10.9, sekta nyingine ni bima asilimia 9.2, malazi na chakula asilimia tisa. Lakini sekta inayogusa Watanzania walio wengi, sekta ya kilimo, ukuaji wake umeshuka na hapa kama Taifa lazima tuongeze maarifa tuone tunatokaje kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wa sekta hii umeshuka kutoka asilimia 3.9 ya mwaka 2021 mpaka asilimia 3.3 mwaka 2022. Kitabu cha Hali ya Uchumi kinatuambia, mchango wa sekta hii kwenye GDP umeshuka kutoka asilimia 26.8 mpaka asilimia 26.2. Lakini alarming katika sekta hizi ni kwenye eneo la sekta ya uvuvi, hapa ndipo nilipo na maneno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wa sekta ya uvuvi umeshuka kutoka asilimia 2.6 mwaka 2021 mpaka asilimia 1.9. Lakini mchango wa sekta hii kwenye GDP umedumaa, upo kwenye asilimia 1.8. Hii haiwezi kuwa sawa kwa sababu potential iliyopo kwenye sekta ya uvuvi ni kubwa, sekta hii hatujaitumia ipasavyo. Lazima tuongeze maarifa ya jinsi ambavyo kama Taifa tunaweza kunufaika zaidi na sekta ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia kwenye ufugaji wa samaki, kwa mwaka huu tumevuna tani 25,000 zilizotuingizia bilioni 170. Lakini tunazungumzia mabwawa ya kufuga samaki kwenye nchi hii, na ukubwa wake wote, tuna mabwawa 31,000. Vilevile tuna vizimba 780 vya kufugia samaki. Ongezeko la vizimba 307 kwa mwaka mzima, hii haiwezi kuwa sawa. Mheshimiwa Waziri tuongeze maarifa hatujatumia rasilimali yetu ipasavyo kwenye kufuga samaki kwenye ukanda wa Bahari; ni lazima tuongeze maarifa ili tunufaike. Kama wenzetu wanavyonufaika kama wenzetu wanavyonufaika kwenye blue economy lazima na sisi tujielekeze huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine nililoliangalia ni kiwango cha shughuli za uzalishaji kwenye kiwanda. Ukiangalia takwimu za hali ya uchumi zinaonesha kwamba kiwango kilishuka kutoka asilimia 4.2 ya mwaka 2021, na sababu ziko wazi, Vita ya Ukraine, kuongezeka kwa gharama za mafuta pamoja na kuongezeka kwa pembejeo za uzalishaji mali. Hapa sasa lazima tujiulize, kama uzalishaji wetu kwenye viwanda ulishuka, measures tunazoziweka kwa mwaka huu wa fedha zinatuhakikishia kwamba tutapandisha? au zitasababisha kuwa na ushukaji mkubwa kwenye uzalishaji kwenye viwanda vyetu. Hili lazima tuliangalie kwa umakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge hapa wamekuwa wakipiga kelele kwamba tumeweka tozo kubwa kwenye saruji, viwango vyetu vile vinaonekana ni vikubwa. Sasa tujiulize, kama tumeweka kodi kubwa kwenye saruji, je, wananchi wetu watamudu kutumia saruji zile? Kama hawatamudu, Je, mchango tunaoutegemea kutoka kwenye viwanda hivi kwenye pato letu la Taifa utakuaje? Utaathirika au utabaki vile vile? Maeneo haya ni vizuri tukayaangalia kwa umakini ili tuweze kutoka vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine nawapongeza kwa jinsi ambavyo wamekuwa wasikivu na kadhia ile ya biashara kule Kariakoo na mpaka tunazungumzia kupandisha kiwango cha VAT kwa turn over ile ya kutoka milioni 100 mpaka milioni 200 na kuendelea. Hapa lazima tuwe makini sana. Tumekuwa na ukuaji wa viwanda vidogo vidogo katika nchi hii na vimeleta msisimko kwenye uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, sasa, wawekezaji wengi kwenye viwanda hivi mtaji wao huo unalenga hapo kwenye milioni 100. Sasa tunapowatoa kwenye eneo hilo tunawapeleka kwenye turn over ya milioni 200, lakini tukumbuke kwamba, kwa sababu hawa uwezo wao ni mdogo wamekuwa wakinunua raw materials kwenye viwanda ambavyo vyenyewe viko kwenye mfumo wa VAT. Kwa hiyo, raw materials watakazonunua itakuwa ni ghali, lakini wao hawapo kwenye mfumo wa VAT. Kwa hiyo, hawatakuwa na uwezo wa ku–recover kile kiwango cha VAT walichokitumia kutokana na kununua raw materials. Hapa naona kuna mgogoro, tunaweza kukuta tunaua ukuaji wa hivi viwanda vidogo. Mheshimiwa Waziri waliangalie hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka siku zilizopita kulikuwa na utaratibu wa kuruhusu wafanyabiashara wanaotaka kuingia kwenye mfumo wa VAT, wakaruhusiwa kwa mpango maalum. Wizara waliangalie hili ili hawa wawekezaji kwenye hivi viwanda vidogo vidogo wanaolazimika kununua raw material kwenye viwanda ambavyo viko kwenye mfumo wa kulipia VAT wasije wakaathirika na waweze ku–recover fedha hizi wanazozitumia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia Bajeti ya Wizara iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, ambaye imempendeza ameweza kuendelea kutulinda na kutupa uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa inayofanyika kwenye Bandari ya Tanga. Tunaishukuru Serikali kwa kuboresha bandari ile ya Tanga kwa kuongeza kina cha bandari ile kutoka mita tatu za zamani zifikie sasa mita 13. Ilikuwa ukileta mzigo kwenye Bandari ya Tanga meli ilibidi ifunge gati umbali wa kilomita 1.7. Kwa hiyo, ilikuwa ni gharama kubwa kushusha mzigo kwenye Bandari ya Tanga, lakini kwa hiki kilichofanyika sasa na kinachoendelea kufanyika tunaishukuru sana Serikali. Kazi ile ikikamilika tunategemea kuongeza ukubwa wa mizigo kutoka tani 700,000 za sasa kwenda tani 3,000,000. Ni mabadiliko makubwa, tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tukisema hayo, yapo mambo ambayo nadhani hayako sawa na ni vizuri tukachukua hatua za haraka ili maboresho yaende sambamba ili tutakapokabidhiwa bandari ile shughuli zitakapoanza kusiwe na msongamano.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la sasa la bandari ile ni hekta 17. Kwa ukubwa wa mizigo tunaoutegemea, eneo hili halitoshi kuweka mizigo, lakini bahati nzuri tuna eneo kule Mwambani la hekta karibu 176. Vilevile tuna eneo kule Chongoleani la hekta 207. Tunachokiomba, tufanye kazi haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo yangu ni kwamba tuboreshe kule Mwambani kwa sababu ni umbali wa kilomita sita tu kutoka bandari ya sasa. Tukiweza kufanya maboresho, maana yake mizigo itakuwa ya uhakika kuweza kutunzwa na kupokelewa. Tusianze shughuli za Bandari ya Tanga bila kuwa na uhakika na sehemu ya kuhifadhi mizigo hii kwa sababu tukienda hivyo, halafu wizi ukitokea, maana yake tunaharibu jina zuri la Bandari ya Tanga. Kwa hiyo hilo lilikuwa ni eneo langu la kwanza. Tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tukipongeza haya, nachelea kusema kwamba bajeti hii sitaiunga mkono. Sitaiunga mkono kwa sababu watu wa Mkinga tumekuwa wahanga wa ahadi zisizotekelezwa. Tuliwahi kupata uwekezaji wa takribani bilioni moja US Dollar kwa ajili ya kujenga Kiwanda cha Saruji pale Mtimbwani. Watu wale walitaka kujenga gati kule Kwale, lakini kwa sababu zisizoeleweka, maamuzi ambayo hayakuwa na faida kwa Taifa hili, watu wale walizuiwa kujenga lile gati na matokeo yake sisi watu Mkinga tukapoteza ujenzi wa Kiwanda kikubwa cha Saruji katika Afrika Mashariki. Jambo lile limekuwa na maumivu makubwa sana sisi watu wa Mkinga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema sitaunga mkono kwa sababu kuna dalili nyingine tunazoziona za barabara yetu ya kutoka Mabokweni, Maramba, Mtonibombo, Magoma kwenda mpaka Korogwe. Mwaka 2021 tuliahidiwa hapa kwamba imetengwa shilingi 1,200,000,000 kwa ajili ya kuanza usanifu wa mradi ule. Ninapozungumza hakuna kinachoendelea kwa maana ya usanifu kufanyika. Taarifa nilizonazo mpaka leo ninapozungumza, tupo kwenye hatua ya evaluation ya kumpata Mhandisi Mshauri. Yaani tumetumia mwaka mzima kumpata Mhandisi Mshauri kwa ajili ya kwenda kufanya usanifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii haiwezi kuwa sawa. Nimeangalia vitabu hapa nione kama kuna fedha nyingine imetengwa kwa ajili ya kazi hiyo kwa mwaka ujao wa fedha, sioni. Kwa hiyo, nasema sitaunga mkono bajeti hii mpaka Waziri atakapokuja kutueleza ni lini evaluation ile itakamilika na kazi ya usanifu itaanza kufanyika ili watu wa Mkinga tuwe na matumaini kwamba barabara hii inaenda kufanyiwa kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema tumekuwa wahanga wa ahadi zisizotekelezwa kwenye upande huu wa bandari kwa sababu tuliahidiwa kwamba kule Mkinga kwenye bandari zile bubu tungeweza kurasimishiwa bandari ya Moa iweze kufanya kazi vizuri, tuweze kufanya biashara vizuri na wenzetu wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aliyekuwa Meneja wa Bandari wa Mkoa wa Tanga alikuja kufanya ziara kule Mkinga mwaka 2018 akatuhakikishia kwamba jambo hili sasa linaenda kufanyika; leo ni miaka mitano hakuna a single cent imetolewa kwa ajili ya kuboresha ile bandari bubu. Tunaendelea kupoteza mapato ya nchi hii kwa sababu bandari ile sasa imegeuka kuwa ni uchochoro wa kuingiza bidhaa za magendo na sisi tunaangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hatutaunga mkono bajeti hii mpaka mje mtuambie ni lini mnarasimisha Bandari ya Moa iweze kufanya kazi vizuri na lini shughuli ya usanifu wa barabara ile ya Mabokweni – Maramba - Mtonibombo mpaka kwenda Korogwe itafanyika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi nichangie kwenye hoja iliyopo mezani. Namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye anaendelea kutupa baraka zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa inayofanya, tulizoea huko nyuma, Wizara hii ilikuwa ni Wizara ya migogoro sana, lakini kadri siku zinavyokwenda tunaona mabadiliko makubwa sana, hongereni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri haya nitakayoyasema sio mageni kwa Wizara, ni mambo wanayoyafahamu naomba wayashughulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ni tatizo la mpaka kwenye ukanda wa bahari, Mheshimiwa Waziri ulifika Mkinga tukaenda Jasini unajua kilichotokea, tuliingia kwenye nyumba pale, upande mmoja ni Mkinga upande mmoja ni Kenya. Kwa hiyo, changamoto ile unaifahamu. Katika eneo lile hasa kwenye ukanda wa bahari wavuvi wetu wanapata shida kubwa, kila unapoenda kuvua wanaambiwa wameingia kwenye eneo la Kenya, mali zao zinachukuliwa, boti zao zinachukuliwa, wanapelekwa Kenya wanafunguliwa kesi kule. Hiki kimekuwa ni kilio cha muda mrefu cha watu wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali twendeni tukaweke mipaka twendeni tukaweke maboya yale yaliharibika ili mpaka ule ujulikane kinagaubaga tuondoe tatizo la watu wetu. Pale Jasini askari wa Kenya wanaingia mpaka Tanzania wakikamata watu, hebu tulishughulikie tatizo hili kwa haraka kabla halijaleta madhara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo ni tatizo la migogoro ya vijiji na vijiji katika Wilaya ya Mkinga, hili nimelileta kwa maandishi muda mrefu na chanzo cha migogoro ile ya vijiji na vijiji, ni ramani iliyotolewa mwaka 2007 wakati Mkinga inamegwa kutoka Wilaya ya Muheza. Zoezi lile halikuwa shirikishi, wanakutwa kijiji kimoja kijiji cha upande wa pili uongozi haupo, wananchi hawakushirikishwa, kwa hiyo tumezalisha migogoro karibu kila kata, kata na kata kijiji na Kijiji. Naomba hili lichukulieni kwa umuhimu mkubwa twende tukaondoe tatizo lile, kama ni kutafsiri ramani ile twendeni tukatafsiri kwa wananchi wale tuondokane na migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wamefikia sasa wanashikiana mapanga huko, tusisubiri watoane uhai twendeni tukashughulikie tatizo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni eneo ambao tuliomba shamba la Kwantili ambao limetelekezwa kwa zaidi ya miaka 20, shamba ambalo hata ulipaji wa ada ya kodi pale anayemiliki halipi sawasawa, tumeomba shamba hili lifutiwe hati. Shamba lenye Hati Na. 47 22 lenye ekari 58 na shamba lenye Hati namba 14501 lenye ekari 2,841 tulitoa ilani mwaka jana baada ya kugundua kwamba mwenye shamba huyu alienda kukopa nje ya nchi na hati zile alizigeuza kuweka dhamana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilani ile imetolewa tangu mwaka jana, imeiva mwaka jana mwezi wa tisa mpaka leo hatujui nini kinaendelea! Mheshimiwa Waziri hili unalifahamu tuliteta kule Tanga Kamishna wa Ardhi alisema anakwenda kuliangalia, hatujapata majibu, tunaomba mtusaidie tufute shamba hili ili ardhi ilejeshwe kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni lile linaloshughulikiwa na timu ya Mawaziri mlipokuja kule Tanga tulieleza, eneo la Kimuni mgogoro ule tulikwisha ushughulikia kwa kina mwaka 2016; Wizara ilituma timu kikosi kazi kikafanya kazi ile tukafanya kazi nzuri ya kushiriki, mikutano ya hadhara na wanavijiji tukafika makubaliano, timu ya uongozi wa mkoa iliyohusisha Mkuu wa Mkoa, Wabunge wa Wilaya zinagusa maeneo haya tulikuja Wizara ya Maliasili tukakubaliana. Tunaomba mnapoenda kufanya maamuzi mapendekezo yale yazingatiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa upande wa kule Maramba kuna ahadi ya Waziri Mkuu kwenye shamba la Mwele, Waziri Mkuu alishaahidi wananchi wale watapatiwa ardhi kutokana na changamoto kubwa ya ardhi, tunaomba ahadi ile ya Waziri Mkuu ipewe umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)