Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Rashid Abdallah Shangazi (37 total)

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaharakisha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wakazi wa Kata za Manolo, Shume, Sunga na Mbaru ili kuwaondolea usumbufu Wananchi wa maeneo hayo ikiwemo ushiriki hafifu kwenye shughuli za kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Jimbo la Mlalo linakadiriwa kuwa na wakazi wapatao 196,258 kati yao ni asilimia 69 tu wanaopata huduma ya maji safi na salama. Aidha, kwa kutambua tatizo hilo, Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ina mradi wa maji wa Shume, Madala na Manolo. Mradi huu unatarajiwa kugharimu jumla ya shilingi bilioni 2.96 hadi kukamilika ambapo kampuni ya Orange Contractor Ltd. kwa kushirikiana na Linda Technical Service Ltd. kutoka Mjini Lushoto na tayari mkataba umesainiwa. Hata hivyo, kazi hii inasubiri upatikanaji wa rasilimali fedha. Mradi huu unatarajia kuhudumia wananchi wapatao 33,541 katika Kata hizo. Mradi huu utakuwa na urefu wa kilomita 55, vituo 70 vya kuchotea maji pamoja na matenki matatu ya kuhifadhia maji.
Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Mbaru, Halmashauri kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Kiserikali la CHAMAVITA liliufanyia ukarabati mradi mkubwa wa maji wa Rwangi. Kwa mwaka wa fedha 2013/2014 CHAMAVITA ilitumia shilingi bilioni 96.0 kwa ajili ya kuboresha mradi huo kwa kupanua mfumo huo kutoka Kijiji cha Nkelei hadi Vijiji vya Mamboleo na Kalumele ambavyo vipo Kata ya Mbaru. Wananchi wa Vijiji hivi wanapata maji kutoka kwenye tanki la maji kwa Kwekidevu lenye ujazo wa lita 22,500.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Kata ya Sunga yenye Vijiji vitano vya Sunga, Kwemtindi, Masereka, Nkukai na Mambo inakadiriwa kuwa na wakazi wapatao 12,122. Huduma ya maji kwa Kijiji cha Mambo inapatikana kupitia visima vifupi viwili vyenye pampu ya mkono pamoja na vituo vinne vya kuchotea maji kutoka kwenye Mradi Mdogo na Mserereko ambao hauna tanki la kuhifadhia maji. Mradi huu mdogo ulijengwa na Mwekezaji wa Mambo View Hotel kwa gharama ya shilingi milioni 5.0. Katika mwaka wa fedha 2012/2013. Kwa wastani Kata ya Sunga wananchi wanaopata huduma ya maji safi na salama ni asilimia 16 tu.
Mheshimiwa Spika, vijiji vya Sunga, Kwemtindi, Masereka, Nkukai na Mambo katika Kata ya Sunga vitapewa kipaumbele mara tu baada ya vijiji kumi vya awamu ya kwanza ya programu ya maji kukamilika. Aidha, Serikali itaendelea kuboresha huduma ya maji katika Jimbo la Mlalo na maeneo mengine nchini kadri rasilimali fedha zinavyopatikana.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Kilimo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu na Watanzania zaidi ya 75% wanategemea kilimo kama ajira ya kuendesha maisha yao:-
Je, ni lini Serikali itaanzisha miradi mikubwa ya kuhifadhi maji (water reserves) ili kuwa na scheme itakayowezesha wakazi wa Kata za Mnazi, Lunguza na Mng‟aro kuendesha shughuli zao za kilimo msimu mzima?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendeleza kilimo cha umwagiliaji, Serikali inayo mikakati ya kujenga na kuboresha miundombinu ya umwagiliaji katika maeneo mbalimbali hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyataja, Serikali ilishajenga skimu ya umwagiliaji ya Kitivo yenye eneo la hekta 500 kwenye miaka ya 1990. Vilevile mwaka 2013, Serikali ilijenga banio kwa ajili ya skimu ya Kwemgiriti yenye jumla ya hekta 800 na Kituani Mwezae yenye jumla ya hekta 600.
Mheshimiwa Mwenyekiti, skimu hizi zinanufaisha wananchi wa maeneo ya Kata za Mng‟aro, Lunguza na vijiji vinavyozunguka Kata hizo. Chanzo cha maji ya umwagiliaji katika skimu hizo ni Mto Umba ukiunganishwa na Mto Mninga. Taarifa iliyopo kwa sasa inaonesha kuwa wingi wa maji katika Mto Umba umepungua kutokana na shughuli za kibinadamu zinazoendelea katika maeneo ya vyanzo vya mito pamoja na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Mnazi kuna skimu ya Kwemkazu yenye eneo la hekta 150 ambayo ilifanyiwa maboresho ya miundombinu mbalimbali kati ya mwaka 2009 hadi mwaka 2013. Skimu hii inapata maji kutoka Mto Mbarama. Tatizo ambalo limejitokeza kwa sasa, mto huu unakuja na mchanga mwingi sana unaoathiri ufanisi wa banio. Tatizo hili linasababishwa na shughuli za kibinadamu na uharibifu wa mazingira kwenye vyanzo vya mto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha wingi wa maji katika skimu zilizotajwa hapo juu, Serikali itafanya uchunguzi wa awali katika maeneo husika ili kuangalia kama kuna maeneo yanayofaa kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa mapya.
Aidha, namshauri Mheshimiwa Mbunge kushirikiana kwa karibu na Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kuangalia namna bora inayoweza kufanywa kuhifadhi mazingira katika vyanzo vya mito ili kuiwezesha kutiririsha maji vizuri na kupunguza tatizo la mchanga.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itasimamia kwa dhati sheria zake na kuondosha unyonyaji na ukandamizaji unaofanywa na wachuuzi kwa kununua mazao ya wakulima kwa utaratibu wa kufunga lumbesa?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondokana na unyonyaji na ukandamizaji unaofanywa na wachuuzi, Serikali imeamua kufanya mapitio ya Sheria ya Vipimo, Sura ya 340 ili iendane na mazingira ya sasa. Lengo la Serikali ni kumlinda muuzaji kwa kuwadhibiti wanunuzi wanaotumia njia za udanganyifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapitio ya sheria tajwa kwetu ni suala la kipaumbele. Katika kipindi kifupi kadri iwezekanavyo Wizara yangu itawasilisha mabadiliko hayo Bungeni ili Bunge lako Tukufu lifanye marekebisho yanayostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na marekebisho ya Sheria ya Vipimo yaliyotajwa hapo juu, Wakala wa Vipimo imewasilisha kwa Ofisi ya Rais - TAMISEMI, mapendekezo ya kutungwa kwa sheria ndogo (by laws) katika Mamlaka za Serikali za Mitaa zitakazowaongoza wakulima na wafanyabiashara kufungasha mazao kwa mujibu wa Sheria ya Vipimo na Kanuni zake. Ili kurahisisha usimamizi wa matumizi ya vipimo rasmi katika ununuzi wa mazao, Mamlaka za Serikali za Mitaa zitaainisha vituo maalum (buying and selling centre) katika vitongoji nchi nzima na kwa mazao yote na hivyo hakuna mfanyabiashara atakayeruhusiwa kusafirisha mazao ambayo yamefungashwa kinyume na Sheria ya Vipimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wakala wa Vipimo kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa itaanzisha vituo maalumu vya ukaguzi bila kusababisha usumbufu katika ufanyaji biashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia fursa hii kuwatangazia Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuunga mkono juhudi za kupiga vita matumizi ya vipimo batili katika ununuzi wa mazao ya wakulima ikiwa ni pamoja na kutenga na kuyasimamia maeneo maalum ya kuzuia mazao (buying and selling centres). Maafisa Ugani walioko vijijini watumike kusimamia matumizi ya vipimo rasmi katika vituo hivyo na kutoa taarifa zote muhimu kwa Wakala wa Vipimo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itashawishi Benki za Biashara kuwekeza katika Jimbo la Mlalo ambalo mzunguko wa fedha ni mkubwa sana kutokana na magulio ya mboga mboga na matunda?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwepo huduma za kibenki katika sehemu zenye shughuli za kiuchumi kama kilimo cha mboga mboga na matunda kama Jimbo la Mlalo. Kwa sababu hiyo, Serikali imekuwa ikijitahidi kuboresha mazingira ya utoaji huduma za kibenki ikiwa ni pamoja na ujenzi wa barabara na miundombinu ya umeme ili kuchochea zaidi shughuli za uzalishaji na hatimaye kuvutia mabenki kufungua matawi sehemu hizo. Ikumbukwe kuwa uanzishaji wa huduma za kibenki hutegemea upembuzi yakinifu ambao unazingatia uwezo wa kupata faida pande zote mbili yaani benki na wananchi. Hii pia hutegemea na uchumi wa eneo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mabadiliko ya kuendesha mfumo wa kifedha nchini unaotekelezwa kuanzia mwaka 1991, Serikali imekuwa ikitekeleza azma ya kujitoa katika kuhusika moja kwa moja na biashara ya mabenki. Kwa hiyo, Serikali imebaki na jukumu la kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji ili kuiwezesha sekta binafsi kuanzisha benki na kutoa huduma bora za kifedha kwa wananchi wetu, hususan pale ambapo huduma hizo zitaweza kujiendesha. Serikali inaendelea na ushauwishi wake wa Benki za Biashara na taasisi nyingine za fedha kuanzisha huduma za kibenki na kifedha popote ambapo kuna mzunguko mkubwa wa kifedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ushawishi wa Serikali, tunamwomba Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Serikali yetu, kuwashauri wananchi wa Mlalo kujiunga na kuanzisha Benki za Kijamii (Community Banks) na taasisi ndogo za kifedha (Micro Finance Institutions) zinazozingatia mazingira ya mahali husika ili kukidhi mahitaji ya kibenki ya Jimboni Mlalo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Msitu wa Shagayu ndio wenye vyanzo vingi vya mito katika Jimbo la Mlalo, msitu huu uliungua takribani hekari 49 mwaka 2012:-
Je, ni lini Serikali itapanda miti katika eneo lililoungua ili kulinda vyanzo vya maji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa mwaka 2012 Hifadhi ya Msitu wa Shagayu wenye ukubwa wa hekta 8,296.8 iliungua moto ambapo eneo lililoathirika, karibu na Vijiji vya Sunga, Mtae na Mpanga lina ukubwa wa jumla ya hekta 49 sawa na asilimia 0.6 ya msitu wa Shagayu kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jitihada za kurudisha uoto wa asili katika hali yake ya ustawi kama ilivyokuwa kabla ya kuungua na pengine kuwa bora zaidi, Wizara yangu imefanya yafuatayo:-
(a) Kupanda miti rafiki kwa mazingira kama vile ocotea, mibokoboko, minyasa, markamia na mipodo katika eneo la ukubwa wa hekta 11 kati ya 49 zilizoungua, ambalo liliathirika zaidi.
(b) Kuweka mazingira ya kuruhusu kukua kwa uoto wa asili kwa njia asilia katika eneo la hekta 38, njia ambayo kwa kawaida ndiyo mbinu ya kipaumble kutumika katika uboreshaji wa maeneo ya misitu ya asili yaliyoharibika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, kuwa hali ya ulinzi katika eneo la hekta 38 zilizoachwa zikue asilia itaendelea kuimarishwa ili kuliwezesha kukua na kurudi katika ubora wake. Aidha, Mheshimiwa Mbunge, anahamasishwa kushirikiana na Serikali na wadau wengine katika kutoa elimu na kuwashawishi wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya uchomaji moto usio rafiki kwa mazingira na hivyo kuepukana na ajali na athari za moto hususan katika misitu.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Halmashauri ya Lushoto ina mzigo mkubwa wa kulipa mishahara ya watumishi ambapo inatumia zaidi ya shilingi 28,000,000 kila mwezi kulipa mishahara ya watumishi ambao kimsingi mishahara yao ilipaswa kulipwa na Hazina kupitia Utumishi.
Je, ni lini Serikali itawatua wananchi wa Lushoto mzigo huu?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, nakushukuru na napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri za Wilaya wapo watumishi wanaolipwa kutoka Serikali Kuu na wapo watumishi wanaolipwa kutoka katika vyanzo vya mapato ya ndani ya Halmshauri husika (own source). Utaratibu huu ulianzishwa baada ya kuonekana kuwepo kwa mahitaji maalum yanayowasilishwa na waajiri kutaka kuwaajiri watumishi wa ziada tofauti na ukomo wa bajeti ya mishahara ya Serikali.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kuna jumla ya watumishi 116 ambao waliajiriwa katika utaratibu huo wa mapato ya Halmashauri (own source) kwa kuwa Halmashauri hiyo iliona inaweza kumudu gharama za kuwalipa mishahara kutokana na vyanzo vyake vya mapato ya ndani.
Mheshimiwa Spika, napenda kutoa wito kwa Halmashauri zote kuzingatia uwezo wao kabla ya kuamua kuajiri watumishi kwa kutumia vyao vyao vya mapato.
MHE. RADHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Skimu ya Umwagilaji ya Mng’aro imekuwa haina ufanisi mzuri tangu kuanzishwa kwake.
(a) Je, ni lini Serikali itaboresha miundombinu ya skimu hiyo ili kuleta tija?
(b) Je, ni lini skimu hiyo itakaguliwa ili kuondoa malalamiko ya ubadhirifu wa mali za ushirika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Skimu ya Umwagilaji Mng’aro (Kitivo) ipo katika Kijiji cha Mng’aro Wilaya ya Lushoto na iliibuliwa na wananchi miaka ya 1980 kwa ajili ya kuzalisha mazao ya mpunga, mahindi, maharagwe na mboga mboga. Uzalishaji wa mazao katika skimu hiyo haukuwa na tija kwa kuwa wakulima hawakuwa na miundombinu bora ya umwagiliaji ambayo ilikuwa inasababisha upotevu mkubwa wa rasilimali maji na wakati mwingine kukosa kabisa mavuno kutokana na mafuriko au ukame.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hii, Serikali iliboresha skimu hiyo kati ya mwaka 1988 na 1995 kupitia fedha kutoka Mfuko wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa kwa kujenga banio kuu la kuchepusha maji kutoka Mto Umba, kuchimba na kusakafia mifereji mikuu ya kupeleka maji mashambani, kujenga vigawa maji na vivuko vya mifereji, kuchimba mifereji ya matupio ambayo ni mifereji ya kutolea maji ya ziada mashambani na kujenga barabra za kupeleka pembejeo na kutolea mazao mashambani.
Mhesmiwa Spika, katika bajeti ya mwaka 2018/2019 Serikali itaingiza skimu hii kwa lengo la kuboresha miundombinu ya umwagiliaji ili wannachi waendelee kuzalisha kwa tija.
Mheshimiwa Spika, sambamba na juhudi za Serikali, ninawaomba Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla kushirikiana na Serikali kuhamasisha wafaidika wakulima wa skimu hiyo ili waweze kuchangia mfuko wao wa uendeshaji na matengenezo ya miundombinu ya umwagiliaji iliyokwishajengwa na Serikali.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, itatuma wakaguzi kukagua nyaraka mbalimvbali cha Chama cha Ushirika cha Skimu ya Mng’aro (Kitivo) Kijiji cha Mng’aro ili kuona kama kuna ukweli juu ya tuhuma za ubadhirifu wa mali za ushirika na hatua stahiki zitachukuliwa kwa wote watakaobainika kufanya ubadhirifu.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Je, ni lini Wilaya ya Lushoto itaanza tena kupokea matangazo ya Redio ya Taifa (TBC)?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kijiografia Wilaya ya Lushoto katika Mkoa wa Tanga ni kati ya Wilaya ambazo zinazozungukwa na milima, mazingira ambayo huzuia mawimbi ya TBC FM pamoja na TBC Taifa, ambayo hurushwa kutokea mitambo ya FM iliyoko katika eneo la Mnyuzi Wilayani Muheza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua changamoto hii, TBC imeamua sasa mtambo wa kurushia matangazo hayo ujengwe katika Wilaya ya Lushoto ili matangazo ya redio yaweze kufika kwa uhakika katika wilaya hii. Ili kufanikisha kazi hii, TBC imetenga shilingi milioni 50 toka bajeti yake ya ndani kwa ajili ya mnara utakaotumika kuweka mtambo wenye nguvu ya watt 500 na viunganishi vyake kwa ajili ya kupokea matangazo hayo. Mtambo huu utafungwa katika eneo la Kwemashai ambako kuna miundombinu ya kuwezesha zoezi hili kukamika kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha.
MHE: RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Tanzania imeridhia na kuingia mikataba mbalimbali ya kimataifa ikiwemo diplomasia na mahusiano.
Je, ni nchi ngapi na zipi ambazo Watanzania wanaweza kuzitembelea moja kwa moja kwa utaratibu wa visa on entry wakati wa kuingia ukiondoa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa maelezo kwa kuwa visa ni ruhusa inayoambatana na masharti ambayo hutolewa na nchi husika ili kuwaruhusu raia wa kigeni kuingia, kuondoka au kuwepo nchini katika muda maalum. Ruhusa hiyo inapotolewa katika vituo vya kuingilia nchini inajulikana kama visa on arrival.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa utoaji visa on arrival uko katika sura ya makubaliano ama mikataba baina ya nchi na nchi au taratibu zinazotokana na matengamano na ushirikiano wa kimataifa na kikanda. Utaratibu huu unaweza kubadilika kulingana na mahusianao na hali ya usalama kati ya nchi na nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo nchi 16 ambazo Watanzania wanaweza kuzitembelea katika utaratibu wa visa on arrival. Nchi hizo ni Benin, Burkina Faso, Cape Verde, Cote d’voire, Djibout, Gabon, Gambia, Ghana, Guinea, Guinea – Bessau, Liberia, Mali, Mauritania, Niger, Sierra Leone huu wa visa on arrival, pia zipo nchi 67 duniani ambazo Watanzania wanaweza kuzitembelea bila hitajio la visa.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Chuo cha Mahakama Lushoto (IJA) kinatoa taaluma ya Stashahada za Sheria.
(a) Je, ni lini sasa Serikali itaongeza uwezo wa Chuo hicho ili kitoe elimu ya sheria kwa ngazi ya Shahada?
(b) Je, ni kwa nini Serikali sasa isione umuhimu wa kukifanya Chuo hicho kiwe Wakala wa Law School ili mafunzo ya uwakili pia yaweze kutolewa chuoni hapo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, madhumuni ya kuwepo kwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni kutoa elimu endelevu kwa watumishi wa Mahakama na watumishi wa sekta nyingine za umma wakitokea kazini na siyo kutoa elimu ya sheria kwa ngazi ya shahada. Nia na makusudi hayo inalenga katika kuwaimarisha watumishi hao wanapokuwa kazini kwa kuwapatia mbinu na nyenzo muhimu ambazo ni nadra kupatikana wakati wanapokuwa shuleni/vyuoni na hivyo kuwasaidia katika kutekeleza majukumu yao ya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara bado tunaona kuwa kuna umuhimu wa kuendelea kusimamia lengo la kuanzishwa kwa chuo hicho kwani bado ni la msingi katika kuimarisha kitaaluma watumishi wa Mahakama na sekta nyingine nchini. Hata hivyo, kimeunda kikosi kazi cha kutafiti maeneo mapya ya uanzishwaji wa kozi mpya ikiwemo mafunzo ya ngazi ya Shahada ya Sheria katika Uongozi wa Mahakama (Bachelor of Law in Judicial Administration).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kusema, msingi wa kuanzishwa kwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni kutoa elimu kwa wanaotokea kazini ili kuwapatia nyenzo muhimu kuweza kutekeleza majukumu yao vema. Mafunzo yatolewayo na Chuo cha Uanasheria kwa vitendo yanalenga kumuandaa mhitimu wa shahada ya kwanza kutekeleza kazi ya Uwakili ya Uanasheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Chuo cha Lushoto lengo ni kumwongezea mbinu za kutekeleza kazi za kutoa haki yaani Mahakimu na Majaji, mafunzo ambayo yanatolewa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nachukua ushauri wa Mheshimiwa Mbunge ili kuangalia namna njema ya kuoanisha mafunzo yanayotolewa na vyuo hivi viwili.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapitia upya Sera ya Michezo nchini?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, nitoe pole kwa ndugu, jamaa na marafiki wa Watanzania wenzetu 11 waliopoteza maisha na wengine 15 waliojeruhiwa katika ajali nyingine mbaya ya Mlima Igawilo, Mkoani Mbeya, Mungu aziweke roho zao pema peponi.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kufa ni wajibu na maisha lazima yaendelee, niruhusu vilevile nielezee kidogo yaliyotokea Uingereza usiku wa kuamkia jana kwa Mtanzania mwenzetu Hassan Mwakinyo wa Tanga kwa ushindi mnono alioupata huko Birmingham, Uingereza, baada ya kumchakaza mwanamasumbwi nyota wa Uingereza Sam Eggington katika raundi ya pili tu kati ya raundi 10. (Makofi)
Kabla ya pambano hili kufanyika bondia wa Uingereza alikuwa bondia namba nane kwa ubora duniani kati ya Mabondia 1,852 wakati Hassan Mwakinya alikuwa ni Bondia wa 174 na sasa hivi kutokana na matokeo haya Hassan ni wa 16 duniani, ni bondia bora wa kwanza Barani Afrika na bondia wa kwanza Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya haya, naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Sera ya Maendeleo ya Michezo inayotumika sasa hivi ni ya mwaka 1995, ni dhahiri kuwa katika miaka 23 ya sera tuliyonayo sasa tasnia ya michezo imepitia mabadiliko mengi yanayoleta hitaji la mabadiliko kisera kama vile michezo kuwa chanzo kikubwa cha ajira ya uhakika duniani, kuibuka kwa michezo ya kulipwa, ongezeko la mahitaji ya shule na vyuo mahsusi vya michezo mbalimbali kwa lengo la kulea vipaji toka udogoni kwa wavulana na wasichana, ongezeko la hitaji la viwanja vizuri na vya kutosha ngazi za shule za msingi, sekondari, vyuo, sehemu za kazi na makazi kwa lengo la kuibua viipaji na kupunguza gharama za matibabu kwa magonjwa yanayotokana na mwili kukosa mazoezi, ongezeko kubwa la mahitaji ya vifaa mbalimbali vya michezo na umuhimu wa kujenga uwezo wa ndani kuzalisha vifaa hivyo.
Mheshimiwa Spika, ni kutokana na hali hii halisi Wizara ilianzisha mwaka jana zoezi la kuipitia upya Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995, zoezi ambalo limehusisha ukusanyaji wa maoni kutoka kwa wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi. Uandaaji wa rasimu kamili ya Sera mpya ya Maendeleo ya Michezo umefikia hatua za mwisho na ni matarajio ya Wizara kukamilisha zoezi hili ndani ya muda mfupi ujao.
Mheshimiwa Spika, kupatikana kwa sera mpya kutaleta tija na kutuwezesha kuleta mabadiliko chanya katika tasnia ya michezo nchini ikiwa ni pamoja na kutuwezesha kubadili sheria iliyoanzisha Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ili iweze kuleta ufanisi katika uendeshaji wa michezo nchini, ikiwa ni pamoja na kuainisha vyanzo rasmi na endelevu vya mapato katika maendeleo ya michezo nchini.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Gereza la Kilimo la Mng’aro ni miongoni mwa magereza kongwe hapa nchini, lakini gereza hili limekuwa na miundombinu chakavu kutokana na umri wake:-
Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kulifanyia ukarabati mkubwa gereza hili pamoja na kuongeza uwezo wa kuchukua wafungwa wengi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Gereza la Kilimo la Mng’aro miundombinu yake ni chakavu kutokana na gereza hilo kuwa la muda mrefu, tangu mwaka 1977 hali ambayo inasababisha gereza hilo pamoja na miundombinu yake kuwa chakavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto hiyo Serikali linatekeleza mpango wa muda mrefu kwa nchi nzima wa kuboresha majengo hayo kwa kuyafanyia ukarabati mkubwa, ikiwemo Gereza la Mng’aro ili kuimarisha, kuyaboresha na kuyafanyia upanuzi.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Eneo la tambarare la Tarafa ya Umba na Mkomazi hususan Vijiji vya Mkundi - Mbaru, Mkundi - Mtae lina miundombinu ya majosho ya mifugo na malambo ya kunyweshea mifugo iliyo chakavu.
a) Je, ni lini sasa Serikali itaboresha miundombinu hii ili ipunguze adha ya wafugaji kuhangaika?
b) Kwa kuwa eneo hili ni la wafugaji tangu mwaka 1954, je, ni lini sasa Serikali italiwekea mpaka rasmi ili kupunguza migogoro isiyokwisha ya wafugaji na wakulima?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza uniruhusu nikutakie heri ya siku yako ya kuzaliwa hii leo na baada ya kukutakia heri ya siku yako ya kuzaliwa, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa 2016/2017 Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ilijenga birika la maji la kunywea mifugo katika Kijiji cha Kamba kupitia miradi ya maji ya kunywa vijijini. Pia mwaka 2017/2018 Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kwa kushirikiana na wafugaji ilikarabati josho na birika la kunywea mifugo katika Kijiji cha Kivingo kwa gharama ya shilingi milioni 12.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2018/2019 kiasi cha shilingi milioni 4.8 zilimetengwa kwa ajili ya kukarabati majosho mawili katika Vijiji vya Mkundi-Mtae na Kiwanja ili kupunguza adha ya wafugaji kuhangaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto imetenga shilingi milioni kumi kutekeleza mipango ya matumizi bora ya ardhi katika Vijiji vya Mkundi - Mtae, Mkundi - Mbaru na Kivingo. Aidha, utekelezaji wa mipango ya matumizi bora ya ardhi utahusisha uwekaji wa alama za kudumu kwa maana (beacon) pamoja na uendelezaji wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya malisho kwa kuweka miundombinu muhimu ya mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe wito kwa Halmashauri zote nchini kuweka mipango ya matumizi bora ya ardhi ili kupunguza migogoro kati ya wafugaji, wakulima na watumiaji wengine wa ardhi.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga geti la kuingilia Hifadhi ya Mkomazi katika Kijiji cha Kivingo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII aljibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Taifa Mkomazi ipo Wilaya za Same, Mwanga, Lushoto, Korogwe na Mkinga. Kwa sasa wageni wote wanaotembelea hifadhi hii hutumia lango la Zange lililopo katika Wilaya ya Same.

Mheshimiwa Spika, katika mpango na bajeti wa mwaka fedha 2019/2020, Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) limetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa lango la wageni katika eneo la Kamakota, jirani na Kijiji cha Kivingo Wilayani Lushoto. Lango hilo limetengewa kuhudumia wageni wanaotumia barabara ya Tanga – Lushoto - Mlalo - Kihurio na Same.

Mheshimiwa Spika, sanjari na ujenzi wa lango la wageni eneo la Kamakota, Shirika la Hifadhi za Taifa limeweka kwenye mpango wake maeneo yanyotarajiwa kuwekewa malango ambayo ni Njiro (Wilaya ya Same), Ndea (Wilaya ya Mwanga) na Umba (Wilaya ya Mkinga).
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapitia upya Sera ya Elimu kwa lengo la kuongeza tija na kuendana na mahitaji ya sasa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapitio au maboresho ya Sera hufanyika kwa vipindi tofauti kulingana na mahitaji ya wakati. Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 ni matokeo ya mapitio yia Sera ya Elimu ya mwaka 1995.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuanza utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Serikali imebaini changamoto katika baadhi ya maeneo na mengine kuwa na upungufu katika utekelezaji wake. Hivyo, Serikali imeanza mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 kwa kufanya majadiliano na wadau/wataalam mbalimbali kwa lengo la kupata maoni yao na kuhakikisha ushirikishwaji wa makundi yote muhimu unafanyika ili Sera hiyo iweze kuendana na mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato huu wa kupitia upya Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 unaendelea na kwa wakati muafaka tutawashirikisha Waheshimiwa Wabunge.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Mafuriko yaliyotokea Mlalo mwaka 1993 yalisababisha uharibifu mkubwa kwa barabara inayounganisha Tarafa za Umba na Mtae:-

Je, ni lini Serikali itatenga fedha za kukarabati barabara hiyo muhimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara inayounganisha Tarafa za Umba na Mtae yenye urefu wa kilometa 12.7 inajulikana kama barabara ya Mtae – Mtii – Mnazi. TARURA Wilaya ya Lushoto imekamilisha usanifu na tathmini ya kuifanyia matengenezo makubwa, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 2.5 kinahitajika.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kugharamia matengenezo hayo kwa kuwa inatambua umuhimu wa barabara hii.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Lushoto – Mlalo kilomita 45 kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Lushoto – Mlalo yenye urefu wa kilometa 41.93 ni sehemu ya barabara ya Mkoa ya Lushoto – Mlalo – Umba Junction yenye urefu wa kilometa 66.23 inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, ilianza kuijenga kwa kiwango cha lami kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Hadi kufikia Mwaka wa Fedha 2018/2019, jumla ya kilometa 8.6 zimeshakamilika kwa gharama ya Sh.5,263,802,375. Aidha, katika Mwaka wa Fedha 2019/2020, Serikali imeendelea kuitengea fedha barabara hii kwa ajili ya kuendelea na ujenzi. Sehemu iliyobaki yenye urefu wa kilometa 33 itaendelea kujengwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Serikali ya Awamu ya Kwanza ilikuwa na mazao ya kimkakati ya biashara kama Kahawa, Pamba, 9 Pareto na Katani ili kuwa chachu ya kukuza Viwanda:-

Je, Serikali ya Awamu ya Tano ina mkakati gani mahsusi wa kuanzisha uzalishaji wa mazao na kaulimbiu ya Tanzania ya Viwanda?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano ni mwendelezo wa Serikali za Awamu ya Kwanza, Pili, Tatu na Nne, ambapo Sekta ya Kilimo ya kama ilivyokuwa katika awamu zilizopita, imeendelea kuwa uti wa mgongo kwa uchumi wa Taifa.

Mheshimiwa Spika, kutoka Serikali za awamu zilizopita hadi sasa vipaumbele vya mazao vimekuwa vikibadilika kulingana na mahitaji na watu na wakati. Aidha, mazao ya kibiashara yameendelea kuwa kipaumbele kwa Serikali za awamu zote. Hata hivyo, fursa za mazao mengine kulingana na mahitaji ya watu zimeendelea kupewa kipaumbele katika kupanga mipango na mikakati ya Sekta ya Kilimo katika Serikali ya Awamu ya Tano. Ongezeko la watu limesababisha mazao ya chakula na mazao ya bustani (horticulture) kuendelea kuwa sehemu muhimu ya mazao ya kibiashara.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuendeleza mipango ya Serikali za Awamu zilizopita, sera mpya ya kilimo ya mwaka 2019 inatarajia kutoa vipaumbele vya Sekta ya Kilimo katika maeneo makuu manne ambayo ni mazao ya mkakati ambayo ni Pamba, Katani, Chai, Korosho na Kahawa, kwa ajili ya malighafi za viwanda. Mazao ya horticulture yenye thamani kubwa (high value commodities), uzalishaji wa mbegu ili kuifanya Tanzania kuwa muuzaji wa mbegu nje (major seed exporter) na mazao ya chakula ambapo lengo ni kuzalisha kibiashara.

Mheshimiwa Spika, aidha, takwimu zinaonesha kuwa kufikia mwaka 2050 mahitaji ya chakula duniani yataongezeka kwa zaidi ya asilimia 50 ya sasa na hivyo Tanzania inatarajia kutumia fursa ya kijiografia kuzalisha zaidi mazao ya chakula kwa ajili ya biashara.

Mheshimiwa Spika, pamoja na utekelezaji wa mipango hiyo, utekelezaji wa programu ya kuendeleza Sekta ya Kilimo ASDP-II unatarajiwa kuwa chachu ya kukuza Sekta ya Kilimo hasa kwa kuzingatia maeneo manne ya vipaumbele ya programu hiyo ambayo ni usimamizi endelevu wa matumizi ya ardhi na maji, kuongeza tija na faida katika kilimo, upatikanaji wa masoko na kuongeza thamani na kuiwezesha sekta katika uratibu, ufuatiliaji na utathmini. Mkakati ni pamoja na mkakati wa shirikishi na sekta nyingine, hususan sekta za kibiashara na viwanda kwa kuwa sekta hizo haziwezi kukuwa endepo sekta hii ya kilimo hususan agro-processing haitatimiza wajibu wake ipasavyo.
MHE. MARY P. CHATANDA (K.n.y. MHE. RASHID A. SHANGAZI) aliuliza:-

Mkoa wa Tanga ndiyo Mkoa wenye halmashauri nyingi zaidi kwa sasa ukiwa na jumla ya halmashauri kumi na moja:-

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuugawa mkoa huo ili kurahisisha shughuli za utawala na maendeleo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa Mkoa wa Tanga ndio mkoa wenye halmashauri nyingi zaidi kwa sasa ukiwa na jumla ya halmashauri 11. Hata hivyo, kipaumbele cha Serikali kwa sasa ni kuimarisha maeneo ya utawala yaliyopo yaliyoanzishwa katika miaka ya hivi karibuni kwa miundombinu na huduma mbalimbali ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kabla ya kuanzisha maeneo mengine mapya. Hivyo, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira wakati Serikali ikitekeleza azma ya kuimarisha maeneo yake yaliyopo ambayo yana upungufu wa miundombinu na huduma mbalimbali muhimu kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wetu.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Sekta ya Afya nchini inakabiliwa na uhaba wa Watumishi:-

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuziba pengo hili?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuajiri wataalam wa kada mbalimbali za Sekta ya Afya nchini ambapo kuanzia Mei, 2017 hadi Julai, 2019 jumla ya watumishi 8,994 wameajiriwa na kupangwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya. Aidha, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imepewa kibali cha kuajiri Madaktari 610 ambao watapangwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto.
MHE. RASHID A. SHANGAZI Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kukarabati miundombinu ya Skimu za umwagiliaji za Mnazi – Kwemkwazu na Mng’aro – Kitivo ambazo zimeharibiwa kabisa na mvua?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua athari zilizosababishwa na mvua zilizonyesha msimu 2019/2020 na kusababisha uharibifu wa miundombinu ya umwagiliaji na baadhi ya mito kuhama ambapo takriban skimu 70 za umwagiliaji nchini ziliathirika zikiwemo skimu za Kwemkwazu – Mnazi na Kitivo - Mng’aro katika Jimbo la Mlalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha miundombinu ya umwagiliaji inarejea katika hali ya kawaida, Serikali imeanza kukarabati miundombinu hiyo katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo eneo la Ruaha Mbuyuni, Mlenge na Magozi Iringa Vijijini. Aidha, Serikali itaendelea kukarabati miundombinu ya skimu nyingine kwa haraka zikiwemo skimu za Mnazi na Kitivo, Mng’aro katika Jimbo la Mlalo na zitapewa kipaumbele ili kuhakikisha zinakamilika na kurudi katika hali yake ya kawaida na hivyo kuwahudumia wakulima wa maeneo hayo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI Aliuliza:-

Je, ni lini ahadi ya Serikali ya kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Lushoto – Muyanta hadi Mlalo itaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Lushoto – Mlalo yenye urefu wa kilometa 41.93 ni sehemu ya Barabara ya Lushoto – Mlalo – Umba junction yenye urefu wa kilometa 66.23 ambapo kati ya hizo, kilometa tisa ni za lami na kilometa 32.93 ni za changarawe. Katika mwaka wa fedha wa 2020/ 2021 kiasi cha milioni 420 zimetengwa kutoka Bodi ya Mfuko wa Barabara kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa mita 400 za barabara hii kwa kiwango cha lami. Ujenzi kwa kiwango cha lami kwa sehemu zilizobaki utaendelea kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Barabara ya Lushoto – Mlalo – Umba Junction kiuchumi, kiulinzi na kiutalii na hivyo wakati ujenzi kwa kiwango cha lami kwa awamu ukiendelea, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya matengenezo mbalimbali kila mwaka. Katika mwaka wa fedha wa 2020/2021 jumla ya Shilingi milioni 475.5 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ili kuhakikisha kuwa barabara hiyo inapitika majira yote ya mwaka.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO K.n.y. MHE. RASHID A. SHANGAZI Aliuliza:-

Je, ni vigezo gani hutumika kushindanisha ufaulu kwa shule za msingi na sekondari kwa Halmashauri na Mikoa hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kwa vile na mimi ni mara yangu kwanza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu toka uteuzi ulipofanyika, basi nichukue fursa hii adhimu na adimu kwanza kabisa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mungu ambaye ametuumba na akatujalia uhai, lakini shukrani ya pili kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutuamini katika Wizara hii kuendelea kuhudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kigezo kinachotumika katika kuzipanga shule kwa ubora wa ufaulu katika Halmashauri na Mikoa kwenye mitihani ya kitaifa ni wastani wa alama kwa shule za msingi na ufaulu wa watahiniwa kimadaraja na kimasomo kwa shule za sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mpangilio wa ubora wa ufaulu kwa Halmashauri na Mikoa hutegemea wastani wa ufaulu wa shule zilizopo katika Halmashauri au Mkoa husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, shule za msingi hupangwa katika mpangilio wa ubora wa ufaulu kwa kuzingatia kigezo cha wastani wa alama walizozipata watahiniwa wote wa shule husika katika masomo yote waliyoyafanya. Wastani huo hupatikana kwa kufuata hatua zifuatazo; kukokotoa jumla ya alama walizopata watahiniwa wote wa shule husika kwenye masomo yote waliyoyafanywa; na kukokotoa wastani wa alama wa shule kwa kugawanya jumla ya alama walizopata watahiniwa wote wa shule kwa idadi ya watahiniwa wa shule husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa shule za sekondari mpangilio wa ubora wa ufaulu huzingatia kigezo cha wastani wa ufaulu (Grade Point Average-GPA) wa watahiniwa kimadaraja na kimasomo. Wastani huo hupatikana kwa kukokotoa wastani wa ufaulu wa watahiniwa wa shule husika kimadaraja na kimasomo. Jumla ya wastani huo wa ufaulu wa shule wa kimasomo na kimadaraja hukokotolewa tena ili kupata ubora wa ufaulu kwa kila shule. Ahsante!
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Vitendo vya rushwa vimekithiri sana katika mchezo wa soka hapa nchini: -

Je, ni kwa kiasi gani Serikali inakabiliana na kudhibiti hali hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwepo kwa vitendo vya rushwa katika sekta ya michezo hususan mchezo wa soka hali inayoathiri maendeleo ya mchezo huu kwa ujumla, lakini pia kuikosesha Serikali mapato.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TAKUKURU imekuwa ikikabiliana na vitendo vya rushwa kwenye mchezo wa soka kwa kufanya uchambuzi wa mfumo wa ukusanyaji wa mapato ya viingilio katika mechi za mpira wa miguu. Matokeo ya uchambuzi huo yaliwezesha kubaini kwamba kuna mianya ya rushwa kwenye eneo hili ambapo baada ya kubana mianya hiyo mapato yaliongezeka hadi kufikia shilingi milioni 206 kwa watu 50,233 waliokata tiketi katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa mwezi Machi, 2019 ukilinganisha na mapato ya shilingi milioni 122 kwa watu 47,499 waliokata tiketi kwa mechi iliyochezwa Januari, 2019 kwenye uwanja huo.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa sekta ya michezo nchini, mwaka 2016 TAKUKURU iliunda Timu Maalum ya Uchunguzi kufuatilia na kuchunguza vitendo vya rushwa katika michezo ambapo kesi tatu zimefunguliwa mahakamani na tuhuma saba zinaendelea kuchunguzwa. Aidha, semina zimetolewa kwa makundi mbalimbali ikiwemo Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu (TAFCA), Waamuzi na Makamisaa wanaotumika katika michezo ya Ligi Kuu na Ligi Daraja la Kwanza pamoja na kufanya vikao na viongozi wa Chama cha Mpira wa Miguu (TFF) kuhusu kuweka mikakati ya pamoja kuelimisha umma kupitia soka.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kuwataka TFF, wasimamizi wa soka na viwanja vya michezo waruhusu na kushirikiana na TAKUKURU kuweka matangazo ya kukemea rushwa kwenye soka na michezo kwa ujumla.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Halmasauri ya Wilaya ya Lushoto ina upungufu wa walimu wa shule za msingi takribani 1,270 kwa mujibu wa ikama: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka walimu katika Halmashauri hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, – TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017 hadi 2019/2020 Serikali imeajiri na kuwapanga walimu 148 wa shule za msingi na walimu 118 wa shule za sekondari katika Halmashauri ya Lushoto kati ya walimu 26,181 wa shule za msingi na sekondari walioajiriwa katika kipindi hicho. Aidha, Serikali inaendelea kuratibu zoezi la kuajiri walimu 6,949 kwa nafasi za ajira zilizotangazwa mwezi Mei, 2021 ambao watapangwa kwenye shule mbalimbali zikiwemo za Wilaya ya Lushoto, ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Hifadhi ya Taifa Mkomazi imebana sana maeneo ya wananchi na kusababisha kazi za kijamii katika Kata za Lunguza, Mng’aro na Mnazi kushindwa kufanyika: -

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kupunguza sehemu ya Hifadhi ya Mkomazi na kugawa kwa Serikali za Vijiji?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Taifa Mkomazi imetokana na kupandishwa hadhi kwa lililokuwa Pori la Akiba la Mkomazi kupitia Tangazo la Serikali Namba 27 la mwaka 2008.

Mheshimiwa Naibu Spika, hifadhi hii ni sehemu ya mfumo wa ikolojia wa Tsavo-Mkomazi wenye wanyamapori wengi. Vilevile, ni maeneo ya mtawanyiko na shoroba za wanyamapori na tayari kumekuwa na changamoto nyingi za shughuli za binadamu katika maeneo hayo ambazo zimesababisha kuwepo na migongano kati ya wanyamapori wakali na waharibifu yaani tembo na wananchi wanaozunguka maeneo hayo ya hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Serikali haina mpango wa kumega eneo hilo kwani kuendelea kumega eneo hilo ni kuendeleza migongano kati ya binadamu na wanyamapori waharibifu kama tembo. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Tanzania ina idadi ya watu takribani milioni hamsini na tano wenye madaraja tofauti ya uchumi: -

Je, katika idadi hiyo Tanzania ina mabilionea wangapi?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia utafiti uliofanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania kwenye mwaka wa fedha 2014/2015 na baadaye kurejewa mwaka 2019/2020, unaonesha kuwa idadi ya mabilionea duniani inakadiriwa kufikia watu milioni kumi na nne. Kwa mujibu wa Ripoti ya Capgemini and RBC Wealth Management, July 2019. Bara la Afrika pekee lina mabilionea 140,000 sawa na asilimia moja ya mabilionea wote wa dunia nzima. Kati ya idadi ya mabilionea waliopo Barani Afrika, mabilionea 5,740 wanatoka Tanzania ambao wanamiliki asilimia 4.2 ya utajiri katika kundi la mabilionea wa Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha miongoni mwa mabilionea 5,740 waliopo Tanzania, mabilionea 115 sawa na asilimia mbili ya utajiri wa zaidi ya dola milioni 30 wanaomiliki zaidi ya asilimia 28 ya utajiri wote wa mabilionea wanaotoka Tanzania. Kati ya hawa mabilionea waliopo Tanzania wengi wamesajiliwa na Mamlaka ya Mapato yaani TRA na wanalipa kodi zao katika Idara ya Walipa kodi Wakubwa na wamewekeza katika Sekta za Viwanda, Nishati na Madini ikiwemo pia Sekta ya Fedha, Mawasiliano pamoja na Uchukuzi, Utalii na Makazi.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italeta Muswada Bungeni ili kuboresha Sheria ya Usalama Barabarani ya mwaka 1973 kutokana na Sheria hiyo kupitwa na wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kupitia na kuboresha Sheria ya Usalama Barabarani ya mwaka 1973. Maboresho ya sheria hiyo yamefanyika ambapo muswada wenye marekebisho hayo ulisomwa kwa mara ya kwanza katika Mkutano wa Tatu wa Bunge la Kumi na Mbili, tarehe 30 Juni, 2021. Muswada huo uliwasilishwa kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama tarehe 17 Agosti, 2021 ambapo ushauri na maoni ya Kamati yalizingatiwa. Hatua inayofuata ni kufikishwa Bungeni ili kusomwa kwa mara ya pili na tatu hatimaye kuridhiwa.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, ni lini Sheria ya Manunuzi na Ukandarasi kupitia Public Private Partnership itaanza kutumika?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura 410 ipo na inatumika, sambamba na Sheria ya PPP, Sura 210, ambapo mchakato wa zabuni za miradi ya PPP unazingatia sheria zote mbili. Pamoja na sheria hizo kutumika kama rejea wakati wa ununuzi wa miradi ya ubia, Serikali inaendelea na utaratibu wa kupokea maoni na mapendekezo kutoka kwa wadau ili kurekebisha vifungu vyenye changamoto katika utekelezaji wake. Ni matarajio yetu kwamba, marekebisho ya sheria zote mbili yatakamilika katika mwaka 2022/2023. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, ni lini utekelezaji wa Mkataba wa kibiashara kati ya Serikali na Kampuni ya Dubai World utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwezi Februari 2022 Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), ilisaini Hati ya Makubaliano (MoU) na Kampuni ya Dubai Port World (DP-World) ya Umoja wa Falme za Kiarabu, kuhusu uwekezaji katika maeneo ya bandari nchini. Aidha, tarehe 25 Oktoba, 2022 Serikali ilisaini makubaliano na Serikali ya Dubai (Inter-Governmental Agreement - IGA).

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mkataba wa kibiashara unakwenda katika hatua mbalimbali. Hatua ya kwanza ni mkataba kati ya nchi na nchi (Intergovernmental Agreement - IGA) ambao tayari umesainiwa. Mkataba huo unaweka msingi wa Serikali za pande mbili kuanza majadiliano kuhusu maeneo ya uwekezaji. Baada ya kusainiwa kwa mkataba huo, majadiliano yataendelea kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi ili kuhakikisha kwamba uwekezaji huo unakuwa na tija kwa nchi. Matarajio ya Serikali ni kuwa majadiliano hayo yatafikia tamati mwishoni mwa mwezi Desemba, 2022.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaziba nakisi ya uagizaji mafuta ya kula kwa kuruhusu uwekezaji mkubwa katika Bonde la Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mikakati mbalimbali ya kuendeleza sekta ya mafuta ya kula nchini ikiwa ni pamoja na eneo la Bonde la Ziwa Tanganyika katika Mikoa ya Kigoma, Katavi na Rukwa ili kukabiliana na uhaba uliopo. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na uanzishwaji wa mashamba makubwa ikiwemo mashamba ya alizeti na michikichi, kuielekeza Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) kuongeza utafiti na kuhamasisha sekta binafsi kuzalisha mbegu bora za mafuta katika mazao ya karanga, ufuta, alizeti na michikichi na kuhamasisha ushiriki wa taasisi za umma katika uzalishaji wa michikichi kwa ajili ya usindikaji wa mafuta ya kula katika Mkoa wa Kigoma.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaugawa Mkoa wa Tanga ili kuongeza ufanisi katika eneo la Utawala Bora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi Mbunge wa Jimbo la Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kuanzisha Mkoa, Wilaya na Tarafa mpya umebainishwa kupitia Sheria ya Uanzishwaji wa Mikoa na Wilaya Sura ya 397 (The Regions and Districts Establishment Procedure) Act, 2020) na Mwongozo wa vigezo vya Maeneo Mapya ya Utawala wa mwaka 2014.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria hii, hatua ya awali inahusisha kupata ridhaa ya Vijiji, Kamati za Maendeleo za Kata, Mabaraza ya Madiwani ya Halmashauri zilizomo katika Mkoa, Kamati za Ushauri za Wilaya, na Kamati ya Ushauri ya Mkoa Mama. Baada ya hatua hiyo, maombi hayo yanawasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya uhakiki na tathmini na baadaye kuwasilishwa kwa Mamlaka husika kwa maamuzi kadri itakavyoona inafaa.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais TAMISEMI, haijapokea wasilisho la mapendekezo ya kugawa Mkoa wa Tanga. Hivyo, nashauri taratibu za uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala zifuatwe. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafufua upya Tume ya Taifa ya Mipango?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu swali namba 138 lililoulizwa na Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo katika hatua za mwisho za maandalizi ya Muswada wa Sheria kuanzisha Tume ya Mipango. Muswada huu unatarajiwa kuwasilishwa Bungeni katika Mkutano huu wa Kumi na Moja wa Bunge lako unaoendelea sasa. Muswada wa Sheria ukipitishwa Bungeni, Tume ya Mipango inatarajiwa kuanza shughuli zake katika mwaka wa fedha 2023/2024 yaani tarehe 1 Julai, 2023.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, Wamachinga wangapi wamefuzu kuwa Wafanyabiashara rasmi kwa kipindi cha kuanzia 2016 hadi 2021?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA, alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia Machi, 2023 kuna jumla ya Machinga 1,987,361 nchini. Aidha, kwa sasa Serikali inaanda utaratibu wa kuwatambua Wamachinga waliofuzu kuwa wafanyabiashara mara baada ya kurasimisha biashara zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuhamasisha urasimishaji wa biashara nchini kupitia njia mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya faida za urasimishaji biashara kupitia mafunzo mbalimbali ya biashara ya ujasiriamali. Mikakati iliyopo kwa sasa ni uanzishwaji wa vituo jumuishi vya urasimishaji wa biashara na uandaaji wa mwongozo wa taratibu za kurasimisha biashara nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, kuna mkakati gani wa kufufua zao la kahawa nchini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatekeleza mikakati mbalimbali ya kufufua zao la kahawa hususan katika maeneo yenye mibuni iliyozeeka, mashamba yaliyotelekezwa na kuanzisha kilimo cha kahawa katika maeneo mapya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati hiyo inajumuisha uzalishaji na usambazaji wa miche bora ya kahawa; kuimarisha maabara za kuzalisha miche kwa njia ya chupa ili kudhibiti magonjwa na kuongeza kasi ya uzalishaji wa miche bora; kuboresha mifumo ya masoko ya kahawa ili kumlinda mkulima; kuwezesha matumizi ya teknolojia za umwagiliaji kwenye mashamba ya kahawa na kuimarisha utafiti na maendeleo kupitia Kituo cha Utafiti wa Kahawa Tanzania (TaCRI).

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu wa mwaka 2022/2023 jumla ya miche 8,784,146 ilizalishwa na kusambazwa kwa wakulima. Kati ya kiasi hicho, miche 5,458,123 ni aina ya arabika na miche 3,326,023 ni aina ya robusta. Aidha, katika mwaka 2023/2024 Serikali imepanga kuanzisha mashamba 40 ya mfano katika wilaya 20, kuratibu uzalishaji na usambazaji wa miche bora 20,000,000 katika wilaya 52 na kufufua mashamba 150 yenye jumla ya hekta 400.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali italishughulikia tatizo la maji kwa vijiji zaidi ya 14 vya Tarafa ya Mtae?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, na kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Tarafa ya Mtae ina jumla ya vijiji 20 ambapo vijiji 16 vinapata huduma ya maji kupitia visima vifupi na mito. Katika kuboresha huduma hiyo, kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imekamilisha ujenzi na ukarabati wa miradi ya maji ya Bokoboko, Shaghayu na Rangwi inayonufaisha vijiji sita vya Masereka, Mamboleo, Kwemtindi, Tema, Mpondekaya na Kweshindo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, kuna mpango gani wa kuongeza mnyororo wa thamani wa zao la Kahawa ikiwa ni miongoni mwa mikakati ya kukuza soko la Kahawa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Tasnia ya Kahawa inatekeleza mkakati wa miaka mitano wa Maendeleo ya Tasnia ya Kahawa (2021 - 2025). Moja ya malengo ya mkakati huo ni kuongeza thamani ya kahawa kutoka 7% za sasa mpaka 15% ya kahawa yote inayozalishwa nchini.

Mheshimiwa Spika, katika kupunguza utegemezi wa soko la nje, Serikali imeweka mazingira mazuri ya kuvutia uwekezaji kwenye viwanda vya kuongeza thamani ya kahawa kwa ngazi ya tatu na ngazi ya nne (tertiary processing).

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Bodi ya Kahawa kwa kushirikiana na Sekta Binafsi iliweka lengo la kuzalisha miche bora ya kahawa milioni 20. Hadi kufikia Juni, 2023 miche 17,866,980 ya kahawa sawa na 89% ya lengo ilizalishwa. Miche hiyo imeanza kusambazwa kwa ajili ya wakulima katika maeneo yanayopata mvua za vuli.