Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Medard Matogolo Kalemani (23 total)

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wenzangu waliotangulia, kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa mara ya kwanza kabisa kuonekana kwenye Bunge lako Tukufu na mimi nikichangia Mpango wa Maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kumshukuru sana Mheshimiwa Rais pamoja na azma ya Serikali ya hapa kazi tu, haijaishia kwenye maneno. Mwanzoni mwa mwezi huu Mheshimiwa Rais alizindua mradi wa kuzalisha umeme wa Kinyerezi Namba II megawatt 240, lakini mwishoni mwa wiki hii pia amezindua pia ujenzi wa flyover katika barabara ya kuelekea uwanja wa ndege na kama haitoshi juzi amezindua pia ukamilishaji wa Daraja la Kigamboni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Watanzania wote, Waheshimiwa Wabunge na sisi wananchi, tufanye kazi moja ya kutwanga maendeleo, hakuna kazi nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze sasa kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha katika mchango huu wa Mpango wa Maendeleo wa Pili. Katika Mpango huu nijielekeze moja kwa moja katika ukurasa wa 10, kadhalika ukurasa wa 28. Ukurasa wa 10 Waheshimiwa Wabunge, suala la nishati limezungumzwa kwa kirefu sana japo kwa maneno machache, nami niongezee sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama mnavyotambua Waheshimiwa Wabunge, Serikali ya Awamu ya Tano, kwa wananchi na Waheshimiwa Wabunge tunasema suala la nishati sasa ni la kufa na kupona. Tutake tusitake tutazalisha umeme wa kutosha kujenga viwanda vyetu. Ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge, kwa ridhaa yako Naibu Spika kwa jinsi ambavyo wanaunga mkono kuelekeza nguvu za wananchi kwenye kuzalisha umeme wa kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa 10 wa Mpango huu umezungumza kwamba mwaka 2016 tungefikisha megawatt 2,780, bado tunatembea 2016 inaendelea, lakini hata hivyo nguvu kubwa sasa inayoonekana niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge na wananchi, sasa hivi megawatt tunazozipata kwenye nishati asilimia kubwa ni kutokana na gesi asilia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaeleze Waheshimiwa Wabunge, kwa sasa hivi Kinyerezi peke yake tuna uwezo wa kupata zaidi ya megawatt 700. Hapo nyuma tulikuwa tunapata megawatt chini ya 300. Lakini kwa sababu tunataka gharama za umeme zishuke na haziwezi kushuka kama hatuzalishi umeme wa gesi na umeme wa maji, niseme tu kwenye upande wa umeme wa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo kina cha maji cha Mtera kinatosha, kinaongezeka, leo tuna milimita 697 kati ya 698 ambalo ni ongezeko kubwa linatupatia uhakika kwamba tutakuwa na umeme wa kutosha tunakoelekea. Kihansi kati milimita 1,190 tuna milimita 1,782, tunapungukiwa kidogo. Kidatu tuna milimita 471 kati ya milimita 478, kwa hiyo tunakwenda vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa ambayo nataka niwaeleze wananchi ni kupungua kwa gharama za umeme. Mwezi huu gharama za umeme zilizokuwa zinakwaza wananchi tumeondoa gharama za maombi ambayo ilikuwa ni shilingi 6,000.00. tumeziondoa, kadhalika tumeondoa gharama za kufanyiwa service (service charge) ambazo pia zilikuwa zinakwaza sana wawekezaji. Lakini wananchi wa vijijini sasa hivi gharama ambayo wanaweza kuwa nayo kimsingi kwa umeme wetu wa REA ni bure isipokuwa VAT ya shilingi 27,000/=.
Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ni juhudi kubwa sana ya Serikali. Na niwahakikishie wananchi kwamba kwa sasa, niongezee japo kidogo jambo ambalo liliulizwa jana kwa Wizara ya Mambo ya Ndani, kwamba wazee wetu sasa hivi inaonekana kuwa wana macho mekundu kwa sababu ya kupuliza kwenye moto. Sasa hivi moto unaokuja sasa siyo wa kupuliza, ni wa umeme wa kukandamiza. (Makofi)
Kwa hiyo, niwahakikishie wananchi kwamba kutakuwa na umeme vijijini, wataweza kujenga viwanda vidogovidogo kama ambavyo wanafanya nchi nyingine za Thailand na China. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba juhudi za maksudi zinaelekezwa kwenye umeme, pia juhudi za maksudi kuendeleza viwanda vidogo vidogo kwa kutumia umeme itaongezeka kwa kiwango kikubwa. Kama mnavyofahamu sasa hivi tunatarajia, kwenye bajeti yetu tutaeleza kwa upana zaidi, tunatarajia kwenye Awamu hii ya Tatu inayokuja tuunganishe umeme zaidi ya vijiji 6,000, ukiunganisha nguvu hiyo kwa wananchi wa vijijini kwa namna yoyote ile mwenye kuweza kusuka nywele kwa kutumia umeme atatumia umeme.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kalemani naomba umalize, muda wako umekwisha.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba pia leo kwa mara ya kwanza kabisa nihutubie Bunge lako Tukufu kwa niaba ya Watanzania wote, nikiwakilisha Jimbo la Chato. Nianze sasa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai mkubwa na kupata fursa ya kuongea na kuunga mkono hoja hii ya Wizara ya Nishati na Madini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa nguvu kubwa kabisa nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa na kuaminika kwa Watanzania wote kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Makamu wa Rais, mama yetu Mheshimiwa Suluhu Hassan, kwa mara ya kwanza kupata Makamu wa Rais kwa akinamama hapa Tanzania. Ni historia kubwa, Watanzania wote tunajivunia na hasa akinamama wenzetu. Tunawapongeza sana akinamama kwa kuwakilishwa na Makamu wa Rais wa akinamama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee pia kumpongeza Waziri Mkuu. Nampongeza Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa kwa kuteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kadhalika kwa aina ya pekee kabisa nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Ally Mohamed Shein kuchaguliwa kuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa aina ya pekee nimpongeze sana Profesa Sospeter Muhongo, Waziri wangu anavyonisimamia na kuniongoza katika kusimamia majukumu makubwa ya Wizara ya nishati na madini. Nawashukuru sasa kwa nafasi ya pekee wananchi wangu wapendwa, wananchi wa Chato walivyonichagua kwa kura nyingi na wananchi wote kuwawakilisha kama Mbunge wao, naamini wataendelea kunirejesha mpaka uzee wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa aina ya pekee sasa, niishukuru sana familia yangu, wazazi wangu walivyovumilia kwa kipindi chote katika kutekeleza majukumu yangu ya Wizara ya Nishati na Madini, nawapongeza sana Mwenyezi Mungu awajaalie uhai na uzima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, sasa nijielekeze kwenye kuunga mkono hoja. Kabla sijasahau, niseme naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, waliochangia ni wengi, zaidi ya Wabunge 109, lakini naweza nisijibu hoja zao zote, nitakachofanya, tuombe sana Bunge lako Tukufu kwa ridhaa ya Kanuni za Bunge, itambue ushiriki wa Waheshimiwa Wabunge hawa 109 kwa sababu sitaweza kuwataja, lakini waingie kwenye Hansard. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nianze sasa na kujielekeza kwenye hoja za msingi. Kambi ya Upinzani Bungeni imetoa hoja za msingi sana katika kuonesha kuwa na wasiwasi kana kwamba tutaweza kupata kweli nishati ya umeme ya kuweza kutufikisha kwenye uchumi wa viwanda? Wamekuwa na wasiwasi kwamba, sasa hivi tuna takriban megawatts wanasema 2,780 ndiyo ilikuwa maximum.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mnyika kwamba hizo megawatts 2,780 ambazo tulikusudia kuzifikisha, sasa nimhakikishie miaka mitano ijayo tutakuwa na zaidi ya megawatts 3,000; lakini kuja kufikia mwaka 2025 tutakuwa na zaidi ya megawatts 10,000. Ili kumthibithishia sasa, nimweleze tu kwa upande wa nishati ya gesi, sasa hivi tuna installed capacity nyingi za kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyofahamu, pale Kinyerezi tuna megawatts 150 ambazo tayari tunazo. Tunaendelea kupanua megawatts 185, tutakuwa nazo; Kinyerezi II pia tutakuwa na megawatts 240, unatambua Mheshimiwa Rais alizindua hivi karibuni. Tunaendelea na kuwekeza kwenye nishati hiyo hiyo; tutaendelea kuwa na Kinyerezi III ambayo itakuwa na megawatts 300; lakini bado upo uwezekano mkubwa kuwa na Kinyerezi IV megawatts 320. Bado tuna Somanga Fungu, tuna megawatts 350; bado tuna Kilwa Energy, megawatts 320 na kadhalika. Huo ni umeme wa gesi na tuna uhakika kwamba umeme utakuwa mwingi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee tu kusema, tutakuwa na umeme mwingi wa uhakika sana hasa kwenye nishati ya maporomoko ya maji. Tunatarajia kuwa na megawatts 80 za kutoka Rusumo ambazo tutazigawanya megawatts 26.7 kila nchi. Hizo ni nguvu kubwa, itasaidia sana kwa wananchi wa Ngara na maeneo ya jirani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bado tuna umeme wa Kakono wa maji, sasa hivi tunatumia umeme wa kutoka Uganda kwa wenzetu wa Kagera. Sasa tutaachana na umeme wa Kagera kwa kutoa Uganda, tutaanza kutengeneza umeme wetu. Pale Kakono tutakuwa na megawatts 87 na tutausafirisha kwa kilomita 38.8 kutoka Kakono mpaka kwenda Kyaka. Huo ni umeme wa uhakika, nataka niwahakikishie wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunazo nguvu nyingi za umeme, tunapozungumza tutaachana na matatizo ya umeme, tuna uhakika na hizo ni takwimu za kisayansi. Niendelee sasa kusema tu, kuwa na nguvu ya umeme na bila kusafirisha bado haisaidii, niwahakikishie sana Watanzania kwamba sasa nguvu kubwa ya umeme tutakayokuwa nayo kama tulivyoeleza kwenye taarifa yetu ya bajeti, tunaanza sasa kuusafirisha umeme huo ambao utatatua tatizo kubwa la kukatika kwa umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tatizo la kukatika kwa umeme wananchi naomba niwaeleze, ni kwa sababu ya mambo yafuatayo: kwanza, umeme tulionao ni kweli una low voltage. Ili kuondokana na low voltage, sasa tunakuja na umeme mkubwa wa Kilovoti 400 na huu umeme utatapakaa nchi nzima. Nianze kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tutakuwa na umeme wa kilovoti 400 tunaosafirisha kutoka Mbeya unapita Sumbawanga, unaenda Kigoma, unaenda Mpanda mpaka Nyakanazi. Huo urefu mkubwa sana, ni kilomita 1,148. Umeme huo huo tutausafirisha kutoka Nyakanazi mpaka Geita, kilomita 133; umeme huo huo tunautoa Nyakanazi na tutautoa Geita mpaka Bulyankhulu, kilomita 50. Ukanda huo utakuwa na umeme wa uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo tutaanza kuzalisha umeme wa Malagarasi. Umeme wa Malagarasi ndiyo utakuwa mkombozi wa umeme mkubwa kwa wananchi wa Kigoma na maeneo ya jirani kama Ngara. Huo umeme tunaanza kuutekeleza kuanzia mwakani na utakamilika 2019. Kwa hiyo, niwahikikishie wananchi wa Kigoma na eneo la jirani kwamba tunapozungumza eneo la umeme, kwa sasa hivi tumejifunga mkanda, ni suala la kufa na kupona, Watanzania wote watapata umeme wa uhakika ifikapo 2025. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuzungumzia suala hilo hilo la umeme. Tutausafirisha umeme mwingine; nataka niwaeleze mwone jinsi Tanzania nzima itapata umeme wa kutosha. Tutakuwa na umeme wa kutoka North East Grid na huo umeme tutaanza sasa kuutoa Kinyerezi kwa upande wa mashariki. Utatoka Kinyerezi utaenda Chalinze, utaenda Tanga mpaka Arusha mpaka Namanga kilomita 664. Kwa hiyo, Watanzania wa maeneo yale watakuwa wana uhakika wa umeme ambao haukatikikatiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la kusafirisha umeme mkubwa ni kuhakikisha kwamba umeme uliopo sasa ni mkubwa, unatosha kwa matumizi ya viwandani, matumizi ya nyumbani na biashara ndogo ndogo pamoja na biashara kubwa. (Makofi)
Waheshimiwa Wananchi na Waheshimiwa Wabunge, nataka tena niwahakikishie, tunao mradi ninaousema wa backbone. Huu mradi ni wa umeme mkubwa. Ni umeme ambao unatoka Iringa unapita Dodoma unakwenda Singida mpaka Shinyanga na unatumika kwa maeneo yote ya Kanda ya Ziwa na ndiyo umeme wa uhakika mkubwa tunaouzungumzia, siyo umeme wa kutakatikakatika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, suala la kukatika kwa umeme, baada ya miradi hii kukamilika mwaka 2018/2019 yatapungua kwa kiasi kikubwa sana. Sasa hivi niseme tu, siyo kwamba sasa hivi tuna mgao wa umeme. Hatuna mgawo, isipokuwa kuna kukatikakatika kwa umeme kutokana na sababu nilizozitaja hapo awali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie hilo kwamba tunaposema kutakuwa na nguvu kubwa ya umeme, ni umeme wa nguvu kubwa utakaofaa viwandani. Naelewa Mheshimiwa Matiko anajua kwamba, kuna mgao wa umeme na dada yangu naomba uridhike kuwa tatizo hilo litapungua sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie REA na ninapokuwa najibu haya, najibu kwa ujumla wake kwa sababu maswali ni mengi sana. Nizungumzie REA. Ni kweli kabisa REA, awamu ya pili imekwenda maeneo yote tuliyopeleka awamu hiyo, lakini umeme unaishia kwenye vituo tu vya vijiji na siyo kwa wananchi. Lengo kubwa la mradi wa REA, awamu ya pili lilikuwa ni kusafirisha miundombinu ya umeme ili kufikisha vituo vikubwa na baadaye usambazaji kwenda kwa wananchi katika vitongoji uendelee.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa awamu inayokuja, wananchi wengi wameuliza, Waheshimiwa Wabunge mmeuliza kwamba umeme unapita kwenye nyuso za watu. Sasa unakuja mradi unaoitwa underground distribution transformer. Mradi huu unaanza kutekelezwa kuanzia Januari mwakani na utakamilika miezi 18 tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la mradi wa distribution hiyo ninayosema ni ya underground, siyo chini ya ardhi Mheshimiwa Matiko kama unavyosema. Lengo lake, ni kupita kila mahali ambapo transformer na miradi mikubwa ya umeme ambapo Kilovoti 33 imepita, itakuwa sasa inatandaza umeme kutoka kwenye vituo hivyo kwenda kwenye miji ya wananchi. Kwa hiyo, umeme huo utafika kwenye kaya za wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie suala kwamba kuna maeneo yameachwa, yatazibwa pengo pamoja na mradi tunaosema wa underground distribution transformer. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi mwingine huo huo ambao sasa utapita kwenye njia zilizopitisha umeme wa kilovoti 33, kutandaza umeme kutoka kwenye vituo hivyo umbali wa kilomita 10. Huo unaitwa European Union Distribution Grid na utasaidia sana kueneza umeme kwenye maeneo yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, huo mradi pia unagharamiwa takriban shilingi bilioni 58.4 na mradi ule utakapokuwa unapita, maeneo yote ambayo hayakufikiwa na umeme kwa umbali wa kilomita 10 kutoka kwenye nguzo kubwa, sasa utapatiwa umeme wa uhakika na baadaye utapitisha umeme huo huo wa kilovoti 400.
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, nilikuwa nataka tu kueleza maelezo ya kina kabisa kabisa kuhakikisha kwamba umeme unaokuja ni mkubwa na utaingia kwenye Vijiji vyetu na wananchi wote watapata umeme wa uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie sasa kuzungumzia kwenye suala la umeme kuhusiana na kuunganisha Vijiji kwa Vijiji. REA awamu ya tatu ni kweli kabisa, kama tunavyosema REA ya awamu ya pili inakamilika mwezi Juni mwaka huu. Tunachofanya sasa hivi ni kukamilisha uhakiki kutambua vijiji ambavyo havijapata umeme hadi leo, lakini vilikuwa kwenye scope ya REA II, lakini kadhalika ni kuainisha vijiji vyote ambavyo havijapata umeme ama vilikuwa kwenye scope ama havikuwepo kwa sababu lengo kubwa ni kupelekea umeme katika vijiji vyote vilivyosalia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge wala wasiwe na wasiwasi kwamba wanahitaji kuona orodha ama kijiji chako kitasahaulika REA ya awamu ya tatu itapeleka umeme kwenye vijiji vyenu vyote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba hili tatizo la akinamama kujifungua kwa kutumia tochi, hili tatizo la akinamama kuonekana na macho mekundu na wakadhaniwa ni wachawi, kwenye hii awamu ya tano miaka mitano hadi kumi ijayo litatokomea kabisa. Tunataka akinamama badala ya kupuliza moto wa mkaa waanze sasa kukandamiza na kuona mwanga mweupe wakati wa usiku. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwa sababu Serikali imejipanga, ina uhakika wa kuwapatia umeme wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie bei ya umeme. Umeme unapokuwa mwingi na umeme unapokuwa wa uhakika, kwa kawaida gharama za umeme zinashuka bei. Kwa sasa kwa sababu tunatumia kwa kiwango kikubwa umeme wa gesi na kiwango kikubwa sana pia umeme wa maji, tunataka sasa kuachana na umeme wa mafuta.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua tulizochukua kuachana na umeme wa mafuta ni kama ifuatavyo:-
Kwanza, mikataba yote iliyokuwa inatumia umeme wa mafuta inapokwisha sasa hatuiendelezi. Huo ni uamuzi wa Serikali. Kwa hiyo, tumeachana na umeme wa Aggreko, tumeachana na umeme wa Symbion kwenye mikataba ya dharura. Sasa hiyo ni kuonesha kwamba Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba umeme tunaoutumia ni wa gharama nafuu na unaondoa gharama kubwa kwa Serikali na wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, gharama za umeme kwa sasa kama mnavyojua, sasa hivi ili uunganishe umeme kwa wananchi wa Vijijini, ni sh. 27,000/=.
Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na hapo, Mheshimiwa Waziri wangu wakati anawasilisha bajeti yake alieleza kwa kina sana, kwanza tumepunguza gharama zote za kuunganisha na kuomba umeme, lakini kadhalika tunatarajia wananchi watakapoanza kutumia umeme mwingi wa gesi, gharama huenda zikapungua zaidi. Kwa sasa tumeanzia kuondoa gharama za umeme wanapoomba leseni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa tumeanzia na kuondoa gharama za umeme wananchi wanapoomba leseni. Kwa hiyo, wananchi wetu sasa hivi, twende tuwaeleze huko kijijini hawatakiwi kuwasilisha ombi kwa kulilipia, anakwenda anajaza fomu, anaipeleka, anapata umeme, kimsingi ni bure, ukiondoa ile gharama ya kodi ya VAT 28,000. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini akiunganishiwa umeme pia, ataendelea kuutumia umeme huo, TANESCO akija kufanya service halipii kitu chochote na penyewe ni bure. Kwa hiyo, tuwatangazie wananchi wajue sera za Serikali, lakini ili kusema kwamba tuna bei ya chini, tunajilinganisha na nani? Sisi tunaeleza mambo ya kisayansi. Kwa sasa hivi sisi tunazalisha Megawatts kwa ujumla wake 1,554.12 kwa sasa kwa ujumla wake. Kwenye taarifa yetu tumesema 1,461 zipo kwenye grid lakini ukijumlisha na ule ambao haupo kwenye grid ni 1,554.12.
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wa Kenya, kwa Afrika Mashariki ndiyo wanaoongoza peke yao wao wana megawatts 2,357, lakini nchi nyingine zote ziko chini yetu. Waganda kwa sasa wana megawatts 849, sasa hivi watu wa Burundi wenyewe wana megawatts 49 na wenzetu wa Rwanda wana megawatts 185.9, kwa hiyo, sisi ukiji-rank bado tupo juu kwa maana ya kuzalisha umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaeleze, maana yake Waheshimiwa Wabunge tunapozungumza masuala ya umeme kwa sababu tunazungumza uchumi lazima tuzungumze kwa takwimu. Sasa tunajilinganisha vipi kwa bei…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri naomba umalizie. Naomba uwe unamalizia, kengele ya pili tayari.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, sijazungumzia madini, nataka nizungumzie kwenye madini, nikimbie basi niende kwenye madini nizungumze kidogo. Pamoja na kwamba nimejieleza sana kwenye masuala ya umeme, lakini pia nizungumze kidogo kwenye tasnia ya madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu kusema, kwa sasa Wizara yetu inatenga maeneo mengi kwa ajili ya kuwagawia wananchi. Tumesema ni kilometa 12,000 tunatenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Maeneo yatakayotengewa sasa leseni na utafiti unaoendelea yako ya Kasubuya hekta 498, Malengwa hekta 682, yako pia ya Geita takribani hekta 2001 na mpaka kule Chato-Msasa hekta 12,28 na kadhalika na kadhalika. Nyamongo tunaendelea kufanya utafiti kugundua maeneo mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba muda umekwisha, napenda sana nipatiwe muda niendelee kusema zaidi kwa sababu ni nafasi ya pekee lakini kwa sababu muda umekwenda sana...
NAIBU SPIKA: Wakati mwingine Mheshimiwa.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. DKT. MEDARD M. KALEMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi ya barabara za Mikoa inayotengenezwa kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018, barabara kwa ajili ya upgrading to DSD Mkuyuni kutoka Chato Mjini, eneo la Mkuyuni imewekwa kilometa nne tu. Ukweli ni kwamba barabara hii ina urefu wa kilometa 18 kutoka Chato Mjini kupitia Mkuyuni, Rubambangwe JCT, Kanyama, Ilemela hadi Busarara. Barabara hii inaunganisha barabara inayotoka Nyamilembe hadi Katoke inayoungana na barabara ya Biharamulo kuelekea Bukoba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa barabara hii ni muhimu katika kuunganisha barabara kuu ya kwenda Biharamulo na Bukoba na kwa kuwa, ilikuwa katika sehemu ya ahadi za Serikali tangu Bunge la Kumi katika miaka ya 2013/2014, naomba sasa ijengwe kama ilivyotarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa 285 katika jedwali la barabara zilizotengewa fedha kwa kiwango cha lami barabara hii inaonekana kuwa kilometa nne tu ndizo zitakazojengwa kwa gharama ya millioni 300 pamoja na kwamba barabara hii haiishii hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa barabara hii ni mwendelezo wa kilometa nne zilizotajwa katika bajeti ya Wizara zinaishia njiani katika JCT ya Rubambungwe na kuiacha sehemu kubwa bila kujengwa kwa kiwango cha lami. Naiomba sasa Wizara ya Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano waingize sehemu nzima ya barabara hii yenye jumla ya kilometa 18 ili ijengwe kwa kiwango cha lami katika mwaka huu wa bajeti 2017/2018, badala ya kujenga kilometa nne tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia wakati Mheshimiwa Waziri anahitimisha hoja asisitize kuwa barabara hii itatekelezwa ili wananchi wa maeneo haya na maeneo jirani wapate unafuu wa kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa kuwa na usafiri rafiki na rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniamini na kuniteua kuwa Waziri kamili wa Nishati, Wizara ambayo ni mpya. Ninapenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote, hata mimi kuwa Waziri wa Nishati nadhani ni kwa sababu ya mikono ya Waheshimiwa Wabunge hawa, kwa jinsi ambavyo tumeshirikiana sana awamu iliyopita katika masuala yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa juhudi ambazo mlikuwa mnatupa na ushirikiano wenu, tunaamini sasa tutashirikiana zaidi katika safari inayofuata. Hongereni sana Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano, Wizara yetu mpya ya Nishati inayo vipaumbele ambavyo ni vya msingi sana katika kujenga uchumi wa viwanda. Tunatambua kama Serikali kwamba uchumi ni nishati, viwanda ni nishati na maendeleo ni nishati, bila nishati hakuna maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya vipaumbele ambavyo kwa kweli vimezungumzwa vizuri sana na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango ambavyo ninapenda kurejea kwenye michango ni pamoja na miradi mikubwa ya kuzalisha umeme. Hivi sasa tuna mkakati mkubwa wa kuzalisha umeme wa kujitosheleza kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa umeme tulionao unatosha kwa mazingira ya sasa, lakini hauwezi kutosheleza kwa mwendo kasi wa kujenga uchumi tunaokwenda nao. Kwa hiyo, juhudi kubwa tumezielekeza katika kuzalisha umeme ili sasa utumike vizuri kwenye kujenga uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi mkubwa wa kuzalisha umeme tulionao kwa sasa ni Mradi wa Kinyerezi Namba Moja na Kinyerezi Namba Mbili. Mradi huu tuna matarajio utakamilika soon, mwezi Agosti, 2018 miradi miwili itakamilika na kutuingizia sasa jumla ya megawati 425. Huu ni umeme mkubwa, kama utaingia kwenye Gridi ya Taifa utachangia sana kwenye kujenga uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuishukuru sana Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Rais na Serikali yetu kwa kupitisha uamuzi wa kujenga umeme wa maji kupitia Stiegler’s Gorge ya Mto Rufiji. Huu ni umeme mkubwa ambao utatuzalishia megawati 2100. Taratibu za kuanza kuujenga mrdai huu zimeshaanza, hivi sasa tumeshatangaza tender na waombaji zaidi ya 80 wamejitokeza, kesho tunaanza kufungua sasa kuanza kufanya evaluation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matayarisho ya ujenzi wa mradi huu yatakamilika mwezi Disemba mwaka huu na mwezi Januari tunaanza kuujenga. Kwa hiyo, kufikia mwaka 2020 tutaingiza kwenye Gridi ya Taifa megawati nyingine 2100. Tujipongeze sana kwa mradi huu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu ulichelewa kidogo kwa sababu kubwa mbili; ya kwanza, kulikuwa na masuala ya mazingira, katika awamu hii sio kwamba tunapuuza mambo ya mazingira, tutaenda nayo lakini huku tukiharakisha ujenzi wake. Jambo la pili, mradi huu huko nyuma uliwekwa chini ya RUBADA, kazi ya RUBADA kimsingi haikuwa kuzalisha umeme, ilikuwa ni ku-reserve mambo ya mazingira na vyanzo vya maji lakini baada ya Serikali kuamua kwamba mradi huu upelekwe kwenye Wizara inayoshughulika na masuala ya nishati, Serikali tumeuchukua na ndiyo maana tutaharakisha ujenzi wake. Kwa hiyo, niwape uhakika wananchi na Waheshimiwa Wabunge kwamba mradi huu utajengwa kuanzia Januari, 2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipaumbele chetu cha pili, pamoja na mambo mengine, ni ukamilishaji wa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima, Uganda kuja Tanga, Tanzania. Kama mnavyokumbuka, niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge, mwezi Septemba 2017 mlipitisha mkataba wa nchi mbili ili uanze kutekelezwa. Tunawashukuru sana kwa sababu baada ya hapo ujenzi umeshaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu kama ambavyo nimeeleza ni mradi mkubwa. Hapa nchini kwetu utahusisha Mikoa minane ambapo utapita katika Mikoa ya Geita, Tabora, Shinyanga, Singida, Dodoma, Manyara na hatimaye Tanga. Kama ambavyo nimekuwa nikieleza mara zote, mradi huu, nasema utakuwa na impact kubwa kwa sababu unapita katika Wilaya nyingi sana, unapita katika Wilaya 24 katika Mikoa niliyoitaja, kadhalika unapita katika vijiji 134 na unapita katika vitongoji 210. Sasa unaweza ukaona manufaa yake itakavyokuwa kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kokote mradi utakapopita utakuwa na fursa kubwa sana za kiuchumi kwa Watanzania na wawekezaji wengine. Kwa hiyo, mradi huu ujenzi wake unaanza pia mwezi Januari utakapokamilika ndani ya miaka mitatu, fursa kubwa sana za kiuchumi zitakuwa zimeongezeka katika nchi yetu. Kwa hiyo, nilitaka kutoa taarifa kwamba haya ni maendeleo mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na juzi tuikuwa Uganda, tumekamilisha uwekaji wa bomba na kwa upande wetu tulishakamilisha, sasa kazi inayofanyika ni kukamilisha majadiliao kati ya Serikali na wawekezaji. Hatua inayofuata ni kuingia mkataba wa ubia na ujenzi kuanza mara moja; huo ulikuwa ni mradi wa pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa tatu ni Mradi wa Uchakataji Gesi (LMG), huu ni mradi muhimu sana kama ambavyo mnausikia. Upo uvumi kwamba inawezekana mradi huu haupo, niseme kwa niaba ya Serikali; msimamo wa Serikali wa kujenga mradi huu uko palepale. Sasa kinachofanyika, pamoja na mambo mengine, tumeshapata eneo, tumeshafanya tathmini ya wale watakaoathirika na kutakiwa kufidiwa, lakini kazi inayofanyika sasa ni kukamilisha majadiliano ya uwekezaji, hatua inayofuata ni kuingia makubaliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi nyingine iliyokamilika ni kupata eneo ambalo kinu kitajengwa kwa ajili ya kuchakata hiyo gesi. Kwa hiyo, hatua zinakwenda vizuri, na kesho nitakutana na wadau wote watakaojenga mradi ule kama Oil4All, Big Shell na makampuni mengine ili taratibu za kuanza kujenga zianze mara moja. Kwa hiyo, ule uvumi wa kwamba mradi huu umetelekezwa, Serikali iko makini sana na mradi huu na lazima utekelezwe kwa nguvu zote. Kama Waziri wa Wizara hii pamoja na Naibu wangu, tutausimamia mradi huu kwa makini sana mpaka utakapokamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya gesi viwandani. Kama mnavyojua imechukua muda mrefu sana, hasa viwanda vya mbolea na vingine vya mkakati kupewa gesi, ninapenda kutoa taarifa kwenye kikao chako kwamba wiki mbili zilizopita tumekamilisha makubaliano kati ya Serikali
na Ferrostaal, sasa wako tayari kuja kuwekeza wamekubaliana na bei ya Serikali. Walichoomba ni kupata unafuu wa masuala machache ya kodi. Sasa tumeshaanza kukamilisha makubaliano nao, tunachofanya ni kupitia maombi yao ili baada ya kukamilika waanze kuwekeza. Kwa hiyo, maeneo ya Kilwa Masoko kutajengwa kiwanda kikubwa cha mbolea chini ya ujenzi wa Ferrostaal kuanzia sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Mtwara bado tunaendelea kuzungumza na HELM na wenyewe wanaonesha nia ya kukubaliana na Serikali ili sasa nao waingie katika utaratibu wa kujenga. Kwa hiyo, viwanda vya kimkakati vitaanza kujengwa sasa kwa sababu tunakwenda kwa kukubaliana pamoja.

Mradi mwingine ni wa usambazaji umeme vijijini wa REA. Tunaposema ujenzi wa viwanda, havijengwi mjini peke yake. Serikali imedhamiria viwanda vianze kujengwa kuanzia vijijini na hakuna njia ya kujenga viwanda vijijini kama hujawapelekea wananchi umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wetu uko palepale, kama ambavyo tumeeleza, majibu mengi yametolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini mimi nifafanue kwa urefu zaidi. Kwamba mradi huu kama ambavyo tumekuwa tukisema tumeanza kuutekeleza. Na nitoe rai na tamko kwa wakandarasi wote, tunataka ifikapo tarehe 20 mwezi huu, wakandarasi wote wa REA wawe wamesharipoti katika maeneo yao na mkandarasi yeyote abaye atakuwa hajafika kwenye eneo lake na kuanza kazi ifikapo tarehe 20 mwezi huu atakumbwa na kimbunga kikali kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kusema kwamba Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano kuwapelekea umeme wananchi kwa ajili ya kujenga uchumi tunakwenda nao vizuri. Vijiji vyote 7,873 vitapatiwa umeme katika awamu hii ya kwanza tunaanza na vijiji 3,359 lakini baadaye tunamalizia na vijiji 4,320, vyote vitapelekewa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo ya mitambo ya maji ambayo tumedhamiria kuyapelekea umeme ili kurahisisha shughuli zao. Kule Karatu tayari vile visima walivyokuwa wameomba tumewapelekea umeme na tunataka kupeleka visima vya maji maeneo ya Mara na mikoa mingine. Lakini maeneo yote ambayo kutakuwa na mitambo ya maji niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge mtupatie orodha ya maeneo hayo ili tuanze kuyapelekea umeme mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu na mradi wa kusambaza gesi majumbani. Huu mradi ulikuwa unafanyiwa tathmini, tathmini imekamilika, hivi karibuni tutatoa tenda kwa ajili ya kuanza ujenzi. Kadhalika tumezungumza na wadau mbalimbali wanaounga mkono juhudi kwa ajili ya kujenga viwanda hivi. Tutaanza na Mkoa wa Dar es Salaam ili kupunguza matumizi ya mkaa. Tutaanza kusambaza Dar es Salaam kwa kaya 3,000 na baadaye tutahamia Mtwara na Lindi na baadaye tutakwenda katika Mikoa ya Dodoma, Morogoro, Singida na hatimaye katika mikoa yote ya Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, itoshe tu kusema naunga mkono hoja, Wizara ya Nishati itapambana kwa niaba ya Serikali kuhakikisha kwamba uchumi wa viwanda unajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na wenzangu kushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini, lakini kwa upande wa Nishati. Kwanza, nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, ameeleza kwa kiasi fulani mipangilio yetu kuhusiana na miradi ya umeme vijijini. Nami nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, naishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano jinsi inavyotoa pesa za kutosha katika kutekeleza miradi ya REA awamu ya tatu. Kwa takwimu tulizonazo katika kipindi kama hiki, mwaka wa fedha 2015/2016, tulipata asilimia 78.8 katika kipindi kama hiki cha miradi ya REA awamu ya tatu. Katika kipindi cha mwaka 2016/2017, tulipokea asilimia 79.3, kwa hiyo, tuliongeza asilimia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe taarifa mbele ya Bunge lako Tukufu katika kipindi hiki cha nusu ya mwaka, tumepokea asilimia 81.3. Kwa niaba tu ya Wizara yangu na wengine, nichukue nafasi hii kuishukuru sana Wizara yetu inavyoshirikiana na Wizara ya Fedha pamoja na Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwape tu uhakika wananchi na Waheshimiwa Wabunge kwamba kwa utaratibu huu, tuna uhakika mkubwa kwamba miradi hii itatekelezwa kwa asilimia mia moja ndani ya muda mliotupatia na sisi tutafanya kazi kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba kazi inakamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetaja mikoa ambayo tumeshaanza kutekeleza, lakini nichukue nafasi hii kuwaeleza wananchi na Waheshimiwa Wabunge, mpaka sasa tumeshawasha umeme vijiji 24 chini ya mpango huu mpya wa REA awamu ya tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Heche. Nitoe tu taarifa kwamba kwenye Jimbo lake tumeshawasha Kijiji cha Nyangere kwenye Jimbo lake. Kwa hiyo, tayari tumeshamwashia umeme kwenye ile awamu ya tatu. Hata kule Butiama tumeshawasha umeme Masusura; kule Mwanza tumeshawasha Ipanga na Nguge; Geita tumeshawasha Nyangomango; kule Mtwara tumewasha Nalingo; kule Arusha tunawasha Didigo; tunakwenda kuwasha kijiji hadi kijiji. Kwa hiyo, nitoe taarifa kwamba tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kidogo kwenye suala la madeni ya TANESCO. Nami nawapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa kuunga mkono kwamba Shirika letu kwa kweli linahitaji kupewa msukumo wa aina yake. Nazipongeza pia Taasisi za Serikali ambazo zilikuwa zinadaiwa kwa kiasi kikubwa, zimeanza kulipa madeni yake. Kwa hiyo, nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge jinsi mnavyosukuma kwenye Halmashauri zenu, kiasi ambacho sasa tumeanza kupata mapato mazuri kutoka kwenye Taasisi za Maji, Jeshi letu, Mambo ya Ndani na Taasisi nyingine za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa deni kidogo limepungua. Lilikuwa shilingi bilioni 297, sasa limebaki shilingi bilioni 277. Kwa hiyo, ni maendeleo makubwa. Nawaomba tu Waheshimiwa Wabunge kupitia kwenye taasisi zetu, basi tuendelee kuliunga mkono Shirika letu ili liweze kuwahudumia vizuri na kwa asilimia ambazo wananchi wetu wana matarajio nalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kidogo kuhusiana na mradi wa Stieglers. Mheshimiwa Heche amezungumza kwamba tumeanza kuutekeleza. Niseme tu, utekelezaji wa mradi wa aina yoyote una hatua zake. Hatua ya kwanza ya kawaida ya kutekeleza mradi ni maandalizi ya mradi. Hatua ya pili ni kufanya matayarisho ya miundombinu wezeshi kutekeleza mradi; na hatua ya tatu ni ya kujenga mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa tunachofanya ni kuandaa na kutayarisha mazingira wezeshi ya kuutekeleza mradi huo kabambe. Ndiyo maana hivi sasa kwa upande wa miundombinu ya umeme tumeanza kujenga miundombinu ya umeme kupitia Shirika letu la TANESCO ambalo bajeti yake ilipita katika mwaka wa fedha huu tunaoendelea nao. Shilingi bilioni 7.7 zilipitishwa kwa ajili ya miradi ya Morogoro; na mradi unaojengwa sasa kwenda kule ni kupitia bajeti ya Serikali kupitia TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo tutafanya utaratibu na tunaendelea na utaratibu sasa wa kutangaza tenda. Tutakapoukamilisha, ndipo sasa tutajua ni kiasi gani na utekelezaji wa mradi huo utaanza na taratibu za kawaida za kibajeti kuja kwenye Bunge lako Tukufu zitafuatwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba bado maandalizi yanaendelea, lakini nawaomba wananchi na Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono juhudi za Serikali za Mheshimiwa Rais za kuujenga mradi huu kwa sababu utatutoa kwenye shida za upungufu wa umeme na kuwa na umeme wa uhakika wa kujenga uchumi wa viwanda tunaotarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, nizungumze kidogo kuhusiana na miradi ya umeme kule Mtwara na Lindi. Nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara na Lindi kwa jinsi ambavyo mwezi Novemba tulikuwa na shida kidogo, lakini tuliungana pamoja, mwezi Novemba Mtwara tulibaki na mashine tatu zinazofanya kazi hadi kufika Novemba, 2017. Hata hivyo, nitoe taarifa kwa Waheshimiwa Wabunge kwamba hivi sasa mashine zinazofanya kazi kwa Mtwara na Lindi, mashine zote sasa tisa sasa zinafanya kazi. Zimekarabatiwa, zinafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Mheshimiwa Mbunge wa Mtwara kwamba mliomba mashine mbili mpya, tumeshazileta na zimeshaanza kufungwa. Ni matarajio yetu ndani ya miezi miwili nazo zitakamilika. Kwa hiyo, Mtwara na Lindi tutaanza kupata umeme wa megawatts nne za ziada. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali yetu na Waheshimiwa Wabunge mnavyotuunga mkono katika jitihada hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda tu niseme; kweli kabisa katika Mikoa ya Ruvuma na Mtwara tuna changamoto ya miundombinu, lakini tunaendelea kukarabati na kujenga miundombinu mingine mipya. Katika Mikoa ya Sumbawanga, Kigoma pamoja na Katavi ni kweli tunatumia mafuta mazito kwa sasa, lakini Serikali Tukufu kupitia Bunge hili katika bajeti ya mwaka huu mlituidhinishia shilingi bilioni 13.2 kwa ajili ya kujenga umeme mkubwa wa kilovolts 400 wa kutoka Sumbawanga kwenda Mpanda, Kigoma, Nyakanazi, Geita mpaka Bulyanhulu. Hivi sasa utekelezaji umeshaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipande cha Geita – Nyakanazi, Mkandarasi yuko site ameshaanza ujenzi; kwa kipande cha Bulyahkhulu kwenda Geita Mkandarasi yuko site, ameshaanza ujenzi na kwa kipande cha kutoka Mbeya kwenda Sumbawanga, Mkandarasi taratibu za kwanza za kufanya survey anakamilisha; na kufika Julai mwaka huu ataanza ujenzi rasmi. Kwa hiyo, upande wa Sumbawanga napo utapata umeme mkubwa wa kilovolts 400 kwa ajili ya ujenzi wa uchumi wa viwanda vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda la mwisho kwa sababu ya muda nizungumze kidogo kuhusiana na suala la bei za umeme wa REA pamoja na TANESCO. Bei ya umeme kijijini ni Sh.27,000/= basi, hakuna bei zaidi ya hapo. Kwa miradi ya TANESCO ambayo iko katika Mitaa na katika Halmashauri za Mijini ni Sh.177,000/= basi. Hizi ni bei ambazo Serikali kwa kiasi kikubwa imechangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nichukue nafasi hii bado kuipongeza Serikali. Hakuna nchi kwa nchi zinazoendelea zenye gharama ya umeme Sh.27,000/= hata vijijini, hakuna. Tanzania ni bei yetu ya kwanza. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa utaratibu huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna mteja anayelipia nguzo. Ni vizuri nikaliweka bayana suala hili. Gharama za umeme wananchi tunachangia. Gharama ya kununua nguzo moja ni Sh.200,000/= hadi Sh.250,000. Sasa kama ingekuwa ni kulipia nguzo ingekuwa gharama kubwa sana. Kinachofanyika ni kutoa huduma kwa umbali wa huduma zinazoweza kupewa kwa mteja, lakini siyo kulipa nguzo. Kwa hiyo, nguzo hazilipiwi, ni kuchangia juhudi za Serikali katika kutandaza umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nimalizie tu na kusema kwamba, kwa vile sasa hivi tunatekeleza miradi ya umeme vijijini, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, lengo letu ni kupeleka umeme kijiji kwa Kijiji, Kitongoji kwa Kitongoji, nyumba kwa nyumba, taasisi kwa taasisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nawaomba Waheshimiwa Wabunge katika Taasisi za Umma muwashawishi na kuwashauri Wenyeviti wa Halmashauri waanze kutenga fedha kidogo ili kuzifikishia taasisi zetu umeme. Haipendezi na siyo matarajio ya mradi, nguzo kuning’inia karibu na Taasisi ya Umma halafu Taasisi ya Umma isipate umeme ndani ya nyumba. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuwaelekeza na kuwashauri Waheshimiwa Wakurugenzi walipo waanze kufanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho nachukua nafasi hii kuwaagiza Wakandarasi popote walipo, tumeshawaelekeza, mwisho wa kuanza kazi ambao hawajaanza ni tarehe 2 Machi, lakini kwa kiasi kikubwa wameshaanza kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kukupongeza kwa kunipa nafasi hii. Ahsante sana. Nashukuru kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, mmi pia nitajielekeza kwenye sayansi na teknolojia, na maelezo yangu ni dakika tano hadi kumi tu kwa sababu ni sayansi na takwimu peke yake. Nimesoma kwa kina sana taarifa ya Mheshimiwa Waziri na nimesikiliza kwa makini sana michango ya Waheshimiwa Wabunge, niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao, ninakiri na kuamini kwamba wasiwasi walionao Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na ushamilifu wa tasnia ya nishati ya miundombinu mingine pamoja na viwanda, inatakiwa iangaliwe kwa umakini mkubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijasahau niunge mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na takwimu za kisayansi. Tunapozungumza viwanda na biashara, tunapozungumza karne ya viwanda vya kati na ikiwezekana vya juu tunamaanisha miundombinu mingi sana na lazima nikubali kuna changamoto, siyo suala la siku moja wala mwaka mmoja. Lakini nishati kwenye viwanda ndiyo uchumi wenyewe, huwezi ukazungumza viwanda, huwezi ukazungumza chochote kama hujazungumza nishati ya umeme, kwa hiyo nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge na wananchi wengine wanaochangia kwa hoja hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nianze kutaja takwimu, Serikali namna ambavyo imejipanga na nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wa Bunge lililopita kwa sababu mlipitisha mipango hii na sasa ni utekelezaji wake. Leo Tanzania tumegundua kiasi kikubwa kweli cha gesi ambacho mnajua sasa ni trilioni cubic feet 57 wote tunajua, ni gesi nyingi kwa Afrika sisi ni wa kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyeki, leo tunapozungumza uwezo wa kuzalisha umeme, Tanzania kwa leo anayetuongoza kwa Afrika Mashariki ni Kenya peke yake mwenye megawatts 2,357, Tanzania ni ya pili. Tanzania tuna megawatts jumla wake 1554.12; Wanyarwanda wana megawatts 49, Waburundi wana megawatt 185; Waganda wana megawatts 185.6; kwa hiyo sisi ni wa pili na tunatembea. Tunakwenda mbali na hapa tunazungumzia umeme utakaozalisha viwanda vidogo vidogo na vya kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumza tuna uhakika wa umeme nimezungumza kwa ujumla wa megawatts nilizotaja, lakini bado tunaendelea na kugundua umeme wa maji, wenzangu wa Kigoma wamezungumza, Kigoma wanatumia umeme wa mafuta ni kweli na wanatumia zaidi ya shilingi milioni sitakwa siku, sasa umeme wa Malagarasi unakuja, tunaanza kujenga Malagarasi kuanzia mwezi wa tisa mwakani na ni ujenzi wa miaka mitatu, 2019/2020 umeme wa maji Kigoma unatembea na tunawatundikia umeme huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kusema umeme wa viwanda ndiyo huo tunaosema umeme unaotabirika. Sasa hivi wananchi wa Kigoma wanatumia takribani megawatts 15, sasa megawatts 44.8 za Malagarasi zinawatosha na maeneo ya jirani watautumia. Kwa hiyo, viwanda vya tumbaku vya Kigoma, viwanda vya samaki vya Kigoma, viwanda vyote vya nguo na kadhalika vitatembea sasa kwa umeme wa maji. Kwa hiyo, nataka kuwaondoa wasiwasi wanachi wa Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili niunge hoja mkono vizuri kwenye hoja ya viwanda nilikuwa nazungumza ugunduzi wa umeme, tunatoka sasa kwenye umeme wa mafuta tunaelekea kwenye umeme wa gesi na maji. Mwaka huu tarehe 1 Aprili, tumeachana na umeme wa mafuta megawatts 70 wa Aggreko, kwa sababu tunataka kutumia umeme wa gesi tunaanza sasa kusafirisha umeme naomba wananchi na Waheshimiwa Wabunge ninapokuwa nataja zile megawatts muwe mnashangilia basi kwa sababu ni juhudi zenu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa na hizi ni juhudi zenu Waheshimiwa Wabunge leo Kinyerezi I tunazalisha megawatts 150 na tunaongeza megawatts 185 extention yake. Kinyerezi II Mheshimiwa Rais amezindua tena megawatts 240, Kinyerezi III megawatts 300, Kinyerezi IV itakuja baada ya miezi miwili megawatts 320, huo ni umeme wa gesi peke yake na bado tunaendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara kuelekea Songea, Symbion na TANESCO wataanza tena megawatts 600. Waheshimiwa Wabunge, suala la umeme, suala la viwanda ni la kufa na kupona, Waheshimiwa Wabunge nizungumzie usafirishaji wa umeme. Tunaanzia Zambia, tunachota umeme Zambia unaoitwa ZTK tunasafirisha kwa kilovolt 400, tunautoa Zambia kuuleta Iringa – Mbeya kilometa 292, tunasafirisha kilowatts 400. Lakini tunautoa huo huo wa megawatts tunaupeleka mpaka Arusha mpaka Namanga, kilometa 412; sasa huu umeme unapita wapi siyo kwa watu na viwanda? Lakini bado tunapeleka umeme North West Grid wenzangu wanajua, umeme huo unatoka Mbeya unapita Sumbawanga, unapita Mpanda, unapita Kigoma mpaka Nyakanazi kilometa 1,284. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo ni kilovolt 400 za umeme na hapa tunataka tuwaeleze wananchi kwamba sasa umeme utakuwa ni uhakika, lakini bado tuna umeme unaotoka North East Grid kutoka Dar es Salaam Kinyerezi unapita kwa mwenzangu Chalinze Mheshimiwa Kikwete unakwenda mpaka Tanga, una kwenda mpaka Arusha kilometa 664 za umeme, zote ni kilovolt 400 lakini bado tunatembeza umeme huo kutoka Makambako kwenda Songea kilovolt 220 na ni kilometa 100 zote hizo tunatembeza umeme, tunatoa umeme kutoka Geita kwenda Nyakanazi kilovolt 220 kilometa 133, huo ni umeme na yote haya yanajenga viwanda vyetu. Waheshimiwa Wabunge naomba tukumbuke sasa tumedhamiria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bei ya umeme, bei ya kuunganisha umeme sasa hivi ukijaza fomu ni bure, ukishaunganishiwa service charges sasa hivi ni bure, sasa tunataka umeme gani wananchi, Waheshimiwa Wabunge tutajenga viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kutaja ndugu zangu juhudi ambazo tumezifanya, sasa hivi tunapozungumza kuhusu ugunduzi pale Madimba - Mtwara leo tunazalisha trilioni themanini cubic feet za gesi na tunaweza tukafikisha 130 tunachohitaji watu wajitokeze kuusomba umeme wa gesi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazalisha umeme mwingi wa gesi kuliko mahitaji pale Mtwara, lakini bado pale Songosongo tuna uwezo wa kuzalisha sasa hivi trilioni cubic feet 130 hadi 200 na hakuna wanaousomba, tunasubiri viwanda. (Makofi)
Waheshimiwa Wabunge, takwimu tunazosema ni za kisayansi na tunataka tujenge viwanda vya kisayansi na siyo maneno. Nilisema nitatumia dakika tano tu kwa sababu nikibaki humu nitawa-bore, lengo langu ni kuwaletea takwimu za kisayansi zilizokusudia kujenga umeme, viwanda pamoja na miundombinu yote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungemze jambo la mwisho ambalo tulieleza kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, kwamba leo Watanzania wanaopata umeme kweli ni wachache asilimia 40 lakini tunakusudia ifikapo mwaka 2025 Watanzania zaidi ya asilimia 75 watakuwa wanatumia umeme wa uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, natamani niendelee lakini nataka wananchi na Wabunge wabaki na kumbukumbu hizi, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwamba sasa Awamu ya Tano inakuja na umeme unaotabirika wenye gharama nafuu na ambao pia sasa hautakuwa unakatika, tukishaunganisha hizi kilovolt 400 leo ni kweli umeme unakatika kwa sababu tunatumia msongo mdogo zaidi 132 na 220, ifikapo mwaka 2019, tutakuwa tumeshaunganisha miundombinu yote ya kilovolt 400 na umeme sasa utakuwa ni wa uhakika ambao utakuwa haukatikikatiki. Tunajipanga kwa hilo ili kusudi viwanda vya sasa viweze kujengwa kwa uhakika na wananchi wafanye biashara zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache maneno mengi sipendi, nataka mtakapokuja hapa kupitisha bajeti yetu tutaendelea kutundika umeme katika viwanda ili vianzwe kujengwa na maendeleo yaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuchangia bajeti ya Wizara hii muhimu. Pamoja na raha sana zilizotolewa na Mheshimiwa aliyemaliza kuzungumza na mimi basi nizungumze machache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kuchangia kidogo tu kuhusiana na mikakati ya Serikali kuhusiana na masuala ambayo yamezungumzwa na wenzetu wa Kambi ya Upinzani. Nikubaliane na taarifa ya Kambi ya Upinzani ukurasa wa nane na tisa kwamba yapo mambo ya msingi katika mgodi wetu wa Nyamongo kwamba wananchi hawahitaji kunyanyaswa, kudhulumiwa na Serikali kufumbia macho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kufafanua kidogo, nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge kwamba zipo sababu za makusudi za Serikali yetu kuchukua hatua dhidi ya unyonyaji unaoweza kujitokeza kwa wananchi wetu. Nikubaliane kwa kusema tu kwamba, Serikali imechukua hatua madhubuti na niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wa Tarime, Mheshimiwa Heche pamoja na Mheshimiwa Matiko wameshirikiana sana na Serikali hii kuhakikisha kwamba migogoro ya North Mara inamalizika mara moja. Hivi karibuni Serikali yetu imechukua hatua ambazo pia ni shirikishi kwa kuwashirikisha viongozi wa vitongoji wa North Mara kadhalika kuwashirikisha Waheshimiwa Wabunge wanaotoka karibu na mgodi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu inawezekana taarifa ya Kambi ya Upinzani ingekuwa nzuri sana kama ingeweza kutambua juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kuondoa matatizo ya Nyamongo kuliko kuacha kama ilivyo. Nitambue tu kwamba Mheshimiwa Heche pamoja na Waheshimiwa Wabunge wameshirikishwa sana kwenye utatuzi wa migogoro hiyo. Wananchi wa Mara wana masuala ya msingi sana, ni kweli kuna masuala ya mazingira, kuna masuala ya mashimo, kuna masuala ya ajira na kadhalika lakini Serikali haijayafumbia macho. Nataka Waheshimiwa Wabunge pamoja na wananchi wajue kwamba Serikali inachukua hatua madhubuti za kuondokana na migogoro ya North Mara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hiyo haitoshi niseme tu kwamba ile timu iliyoundwa na Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini ambayo kwa sasa bado inakamilisha taarifa zake hatua zitakazochukuliwa pia zitakuwa ni shirikishi. Zitashirikisha Waheshimiwa Wabunge, Madiwani pamoja na Wenyeviti wa Vitongoji husika wa North Mara. Kwa hiyo, nilitaka kuliweka vizuri hilo siyo kweli kwamba Serikali imeyafumbia macho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mgogoro wa Bismarck na mgodi wa Acacia. Ni vizuri tukatambua Sera ya Uwekezaji pamoja na Sera zote za Nishati, Madini na za Mazingira zinahamasisha sana uwekezaji wa ndani na nje. Kwa kutambua hilo, nikubaliane kwamba kampuni ya Bismarck ni ya wazalendo na miaka ya 96 ilipewa leseni ya kutafuta madini kule Mgusu, lakini mwaka 2012 yenyewe ikaamua kuachia leseni zile. Hii ni kwa sababu za kiteknolojia za uchimbaji na mambo mengine. Baadaye sasa maeneo yale yakaombwa kumilikishwa na kampuni ya Pangea Minerals ambayo ni subsidiary company ya Barrick ambapo sasa wanaita Acacia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme sasa na ni jambo la msingi sana Waheshimiwa Wabunge tukitambua kuwa Bismarck ambayo pia ni kampuni ya Watanzania waliamua tu kufanya makubaliano ya kwao kabisa kimkataba na kampuni ya Acacia. Baada ya kutofautiana wakaamua kupelekana kwenye mahakama za usuluhishi za nje. Nitake tu kukubaliana na Waheshimiwa na niwaombe kwamba inapotokea mazingira ya namna hiyo watuletee taarifa Serikalini ili Serikali iyafanyie kazi kwa ufasaha. Sasa hivi suala linalozungumzwa la Bismarck na kampuni ya Acacia wala halipo hapa, wamepelekana wao kwenye usuluhishi wa kimataifa nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tungependa sana Waheshimiwa Wabunge tuleteeni taarifa lakini kwa sasa hivi kulizungumza suala hilo lipo kwenye mahakama ya usuluhishi tutakuwa tunaingilia mhimili mwingine. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge niwaombe sana tuvute subira kwenye masuala haya mawili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nichangie kidogo kuhusu ajira. Mheshimiwa aliyemaliza kuzungumza wa upande wa pili amesema kwamba wananchi wanaachiwa mashimo, hakuna ajira na wanaajiriwa kwenye kazi ndogo ndogo. Nitoe mfano kwa kampuni ya North Mara, ajira kwa Watanzania ni 968 ambapo wageni ni 57. Kwenye mgodi wa Bulyanhulu Watanzania walioajiriwa ni 1,755 na wageni wapo 71. Mgodi wa GGM Watanzania walioajiriwa ni 1,568 na wageni 68.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia uwiano ule bado Watanzania tunapata ajira lakini nikubaliane tuna haja ya kuongeza zaidi. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge niseme tu kwamba michango ya wawekezaji wa nje nayo ni mikubwa na inachangia kwenye pato la Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja hii. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niunge
mkono hoja, pia niungane na waliotoa pole kwa wenzetu wana-CCM ambao walipata
majeruhi huko Moshi, tuwaombee ndugu, jamaa na wengine wapate kupumzika salama.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajielekeza kwenye mambo ya msingi na niwapongeze
sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia, kwenye hoja za maandishi pamoja na zile za
maneno. Kwa ujumla tuna hoja 30 za maneno na za maandishi nane, kwa hiyo, zilikuwa ni hoja
nyingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge nianze tu na
kuzungumza kidogo, kuhusiana na masuala ya kazi ya kusambaza umeme, hasa kwa Shirika letu
la TANESCO. Nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge speed kulingana na uharaka wa
utandazaji umeme kwa kweli haulingani na uwezo wa TANESCO kwa sasa, lakini tunachofanya
ili kuendana na changamoto hizo sasa Serikali imeweka mikakati ya kufuata ili kuhakikisha
kwamba wananchi wanapata umeme kwa haraka kutoka katika shirika letu la TANESCO.
La kwanza kabisa, tunawashukuru Bunge lililopita lilitupitishia bajeti ya kuanzisha ofisi 47
kwa ngazi za Wilaya, sasa tunaanza utaratibu wa kuimarisha ofisi na kujenga ofisi nyingine mpya
katika maeneo ambako hakuna ofisi. Hii ni hatua madhubuti sana kuharakisha upatikanaji wa
umeme katika maeneo yale.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo kwa sababu wakati mwingine ni
ufinyu wa bajeti, ili kupambana na hatua hiyo, TANESCO sasa imeanza utaratibu ufuatao:-
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwanza kabisa tulishaagiza
transfoma zote pamoja na nguzo yataanza sasa kununuliwa hapa nchini. Hii itarahisisha sana
usambaziji wa umeme kwa kasi kubwa. Kwa hiyo, tuna imani kwamba kwa hatua hii
itaharakisha sana usambazaji wa umeme mijini na vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya pili, wakati tunajipanga kujenga ofisi, tumeanza sasa
kuanzisha madawati ya huduma kwa wateja mahala ambako kuna wateja wengi, badala ya
kusubiri kujenga ofisi mpya. Hii ni hatua madhubuti itaturahisishia sana kusambaza umeme kwa
wananchi wengi na kwa muda mfupi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine tumeagiza shirika letu, kuanzia Januari mwaka
huu, litaanza sasa kufata wateje walipo badala ya lenyewe kufuatwa na wateja. Hii itasidia
sana, kwa sababu maeneo mengine kwa wananchi hawawezi kufikia ofisi zetu na hata wakifika
inakuwa kwa gharama kubwa na wakati mwingine wanakata tamaa. Kwa hiyo, sasa
wataalamu wa TANESCO wa shirika letu wataanza kufuata wateja walipo ili kuharakisha
huduma hizi mahsusi. Kwa hiyo, tunaamini kwamba utaratibu huu utachangia sana kuharakisha
uzambazaji wa umeme ili kulingana na kasi ya ukuaji wa umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika sambamba na hilo nizungumzie kidogo kukatikakatika kwa
umeme. Ni kweli, hasa maeneo ya Lindi na Mtwara hata kule Geita kwa Mheshimiwa Kanyasu
na maeneo ya Dar es Salaam. Kazi inayofanyika sasa hivi ni pamoja na ukarabati wa
miundombinu ambayo kwa kiasi kikubwa mingi imekuwa ya muda mrefu. Sasa katika kipindi hiki
kifupi, maeneo mengi yataendelea kupata shida kidogo, lakini ni tatizo la muda mfupi, jitihada
madhubuti zinafanyika ili kurekebisha hali hii. Ni matarajio yetu ndani ya miezi hii miwilii ukarabati
wa maeneo mengi utakuwa umekamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la Lindi na Mtwara nielezee kidogo. Lindi na Mtwara
wananchi wa Lindi wanatumia megawati 18. Kwa sasa mashine moja imeharibika, inafanyiwa
ukarabati hasa kuhakikisha kwamba ile mashine iliyoharibika inafanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo ujenzi wa kusafirisha umeme sasa
kutoka Mtwara kwenda Lindi ambako kituo cha kupoza umeme pale Mnazi Mmoja kinajengwa
na kinatarajiwa kukamilika ndani ya miezi miwili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa wananchi wa Mtwara baada ya kituo kile
kukamilika, hasa kile kituo cha substation kutoka kilovolti 33 kwenda kilovolti 130 zitakapokamilika
matatizo ya kukatika umeme kwa wananchi wa Lindi na Mtwara yatatatulika kwa mara moja.
Kwa hiyo ni vizuri tuwaeleze wananchi wa Mtwara, ni kero hata kwetu sisi tunaliona lakini ni
jambo ambalo linafanyiwa kazi kwa kina sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo lilizungumzwa, ni suala la sera ya mafuta
kutafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili. Ni kweli kabisa suala la kutafsiri lugha za kigeni sasa ni muhimu
sana kwa sababu watumiaji wengi ni Watanzania ambao ndio kwa kiasi kikubwa wanatumia
lugha ya Kiswahili. Mkatati umeshaanza, timu ya wataalam imeshaundwa inayojumuisha wizara
yetu pamoja na taasisi zinazojumuisha Wizara yetu; lakini kazi hii itafanyika kwa kushirikiana na
TUKI ambao ni wataalam wa kutafsiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ili kuepika kufanya kazi na TUKI peke yake, na kuna
masuala mengine ya kiteknolojia na ya kitaalam zaidi, lazima timu mbili zifanye kazi kwa
pamoja. Kwa hiyo, utaratibu unaofuata sasa ni kukaa pamoja ili kuanza kazi hiyo mara moja. Ni
matarajio yetu ndani ya miezi miwili/mitatu timu hiyo itakuwa imeshaanza kazi, pamoja na TUKI.
Kwa hiyo, suala la kutafsiri linafanyika na utaratibu tumeshauanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulinda Tanzanite. Kwanza niseme kwamba ni kweli kabisa
madini ya Tanzanite hapa ulimwenguni yanapatikana Tanzania peke yake, hakuna sehemu
nyingine, kwa maana ya yanakochimbwa. Lakini nikiri kwamba, yako matatizo na changamoto
ambazo zimesababisha pia control yake kuwa kidogo. Hata hivyo hatua za Kiserikali ambazo
zimefanyika, ni vizuri kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kwamba hili neneo kuanzia mwaka
2001 lilianza kutengwa kama eneo tengefu ili kuhakikisha kwamba rasilimali ya Tanzanite
haitoroshwi nje bila kuzingatia utaratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni changamoto kidogo, ilikuwa ngumu na ujenzi wa fence
ulifanyika mwaka 2005, lakini kwa bahati mbaya sana wananchi wanaozunguka maeneo yale
waling‟oa fence pamoja na vyuma. Kwa hiyo, mkakati unaofanyika sasa ni kujenga fence ya
mawe pamoja na tofali, tunatafuta fedha kwa ajili ya kujenga fence hiyo. Kwa hiyo, nikushukuru
Mheshimiwa Ndassa yeye alikuwa Mwenyekiti wa Nishati na Madini huko nyuma huko nyuma
kwa kuliona hili, lakini jitihada zinafanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati mingi sana imefanyika katika eneo hili. Pamoja na
kuanzisha Police Post, kimejengwa Kituo mahususi cha polisi pale Mererani ili kuhakikisha
kwamba udhibiti unakuwa imara na ambao kwa kweli ni shirikishi. Tunaamini kwamba hatua hizi
zimechangia kwa kiasi kikubwa kusaidia madini yetu yasiende nje sana. Lakini pia, kuna joint
committee iliyoundwa ikishirikisha taasisi mbalimbali ikiwemo Uhamiaji, TRA na nyingine ili
kudhibiti utoroshaji huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hayo ili kupunguza utoroshaji wa madini
ya Tanzanite, mwaka 2010 Sheria ya Madini Mpya ilivyotungwa ilipunguza kiasi cha mrabaha
kutoka asilimia tano kwa madini yaliyokatwa kurudi asilimia moja ili kuvutia Watanzania wengi
kukata madini ya Tanzanite hapa nchini. Kwa hiyo, hizo ni hatua ambazo Serikali imechukua,
ambazo ni vizuri sana kuwaeleza wananchi, lakini pia, changamoto tunazichukua bado
tutaendelea kuimarisha ulinzi zaidi katika eneo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu REA III nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge wengi,
REA II iliyokamilika hivi sasa kwanza niseme imekamilika kwa asilimia 95.8 na asilimia 4.2 iliyobaki
ni kwa ajili ya kuwaunganishia umeme wateja. Sasa kazi ya kuunganisha umeme inategemea
mambo mawili, la kwanza utayari wa mwenye nyumba, mtaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, basi nijielekeze la
mwisho, nizungumzie kuhusiana na mikakati ya REA III. REA III imeshaanza maeneo ya mikoa sita
kama nilivyotaja juzi, Mkoa wa Pwani, Mara, Arusha, Iringa, Njombe, Mbeya pamoja na
Songwe, kwa hiyo, tumeshaanza na utaratibu utakwenda hivyo kwa nchi nzima, na mpaka
kufikia tarehe 31 Machi nchi nzima sasa wakandarasi watakuwa wameingia kwenye mikoa yote
kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa REA III.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi zitakazofanyika, nisaidie kunipa dakika moja kwenye hili, ni
pamoja na kufikisha umeme kwenye vijiji vyote vilivyosalia ambavyo ni 7,873 pamoja na
vitongoji vyake. Lakini kazi ya pili ni kupeleka umeme kwenye taasisi zote za umma, hapa nina
maana ya hospitali, zahanati, magereza, polisi, shule, masoko pamoja na pampu za maji. Kwa
hiyo, huu ni mradi mkubwa, tunatarajia wananchi wote watapata umeme kwa kupitia mradi
huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia utapeleka umeme kwenye maeneo ambayo yako nje na
gridi, hasa visiwani pamoja na yale ambayo yanapitiwa na Hifadhi za Taifa. Ni mradi wa miaka
minne hadi mitano, kwa hiyo, mwaka wa 2020/2021 tuna matarajio kwamba vijiji vingi vitakuwa
vimepata umeme kupitia mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kusema jambo hili ambalo nadhani ni tamu sana
kwa Waheshimiwa Wabunge. Hatua tunayofanya kwa sasa ni utandazaji wa umeme shirikishi.
Kabla mkandarasi hajaingia kwenye site yoyote ile ataanza kwanza kupiga hodi kwa Mbunge husika. Hii itasaidia sana kupeleka umeme maeneo ambako wananchi mnajua vipaumbele,
lakini pia ataenda hata kwa Mheshimiwa DC na Mkuu wa Mkoa ili kusaidia katika usimamizi
wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo kwa sababu muda ni mfupi,
ningependa niseme mengi sana kuhusu hili, nashukuru sana. Naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia katika mada muhimu ya Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze pia kuwapongeza sana Kamati ya Kudumu kwa mapendekezo waliyoyatoa. Sisi kama Serikali tumeyachukua tutayafanyia kazi na kufanya maboresho zaidi. Kwa hiyo, napenda sana kumshukuru Mwenyekiti pamoja na Wajumbe wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawapongeze sana Waheshimiwa Wabunge, wametoa michango mizuri, mingi na yenye ushauri. Bado naendelea kusema, kama Serikali, tutaichambua tutaifanyia kazi na kufanya maboresho ambapo lazima pafanyike maboresho.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nami basi niseme machache kuhusiana na ajenda ya leo. Kuhusiana na mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa megawatt 2,115, bila shaka Watanzania wote tunashuhudia, ni mara ya kwanza Tanzania kuingia kwenye ulingo wa kidunia kuwa na miradi mikubwa ya kuzalisha umeme. Kwa hiyo, tuipongeze sana Serikali yetu kupitia kwa Mheshimiwa Rais kwa kutekeleza mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe tu Watanzania na wananchi kupitia Waheshimiwa Wabunge; miradi mikubwa duniani inahesabika mnapokuwa na mradi wa kuzalisha umeme wa kuanzia megawatt 2,000. Kwa hiyo, ndiyo maana tumeingia katika miradi mikubwa 70 duniani, nasi ni wa 60 duniani. Kwa hiyo, napenda tuwapigie makofi Watanzania wote walioshiriki katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi, hata Kiafrika tulikuwa hatusomeki kwenye miradi mikubwa ya kuzalisha umeme. Leo tunaongelea Stiegler’s yenye uwezo wa kuzalisha Megawatt 2,115, ni mradi wa nne Afrika kwa ukubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri sana Wakandarasi ambao wanatekeleza mradi huu ambao ni Arab Contractor kutoka Egypt pamoja na El Sewedy wanatoka katika nchi ambazo zipo katika nchi tano za kuzalisha umeme mkubwa duniani. Walioshiriki sana kwenye kuzalisha umeme wa Aswan Dam wa Megawatt 2,100 kule Egypt. Kwa hiyo, hatuna mashaka na Wakandarasi na hatuna mashaka na maamuzi ya Kiserikali yaliyofanyika. Ni matumaini yetu mradi utatekelezeka vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuwaambia Watanzania kwamba utekelezaji wa mradi huu ndiyo unaanza. Tumesaini mikataba mwezi uliopita, kwa hiyo, hatutarajii Mkandarasi kuwa amelipwa hela nyingi kwa sasa kwa sababu ndiyo kazi zinaanza. Kwa hiyo, ni matumaini yetu tunakokwenda tutamlipa Mkandarasi kulingana na kazi zinavyofanyika. Ndiyo maana kwenye taarifa umeona shilingi bilioni 26 tu kati ya shilingi bilioni 700 za utekelezaji wa kazi hii. Kwa hiyo, ni matumaini yetu, wala hatuna mashaka na wenzetu wa Hazina wataendelea kulipa vizuri kadri utekelezaji wa mradi utakavyoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kutaja umuhimu wa mradi huu. Pamoja na kutekeleza miradi mchanganyiko ya kuzalisha umeme, kama ambavyo tunaendelea kuzalisha umeme wa megawatt 300 ambao tumeanza kuutekeleza sasa kule Mtwara kupitia JICA, wenye uwekezaji wa takribani Dola za Marekani milioni 395 ambao ni megawatt 300, mradi huu tunaanza kuutekeleza kuanzia Julai mwaka huu na utakamilika Juni, 2022 ambao utatuzalishia megawatt 300 za gesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo kweli kwamba tumeacha miradi mingine ya kuzalisha umeme. Umeme huo tutausafirisha kwenye gridi ya Taifa kutoka Mtwara, umbali wa kilometa 512 kwa kuingizwa kwenye rridi yetu ya Taifa. Bado tunatekeleza Mradi wa Kinyerezi na mingine. Hii inaonesha kwamba Watanzania tunaamua kwenda na umeme mchanganyiko. Kwa hiyo, kutekeleza Mradi wa Stiegler’s hakuna maana kwamba tunaondoa utekelezaji wa miradi mingine ya kuzalisha umeme. Naomba Watanzania tuendelee kuunga mkono, tushirikiane mradi utekelezeke ili tuondokane na changamoto ya umeme hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, ni kweli kabisa leo tunapoongea hapa, tuna umeme wa ziada megawatt 278, matumizi yetu ya leo ni megawatt 979, lakini haina maana kwamba hatuhitaji kuendelea kuzalisha umeme. Unatutosha leo, lakini kwa kesho haututoshi. Kwa hiyo, hatuna budi kuzalisha umeme mkubwa ili kujihakikishia ujenzi wa uchumi wa viwanda hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu miradi ya REA, kwanza kabisa, napenda naomba niwapongeze Waheshimiwa Wabunge, mnatuunga mkono sana kwenye miradi hii. Tunapokwenda kwenye miradi yenu, huko kwenye Majimbo yenu mnatupa ushirikiano mkubwa. Nitoe rai tu kwa Wakandarasi kwa sababu limesemwa hapa, kwamba utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini ni mradi shirikishi. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuagiza Wakandarasi kwamba popote walipo wasiingie kwenye maeneo ya Wabunge bila kuwashirikisha Wabunge au uongozi ulioko kule ili utekelezaji uwe na tija zaidi. (Makofi)

Leo tunapoongea, tunapeleka umeme vijiji takribani 6,212. Mwaka 2015 tulipeleka umeme vijiji 1,927 tu, kwa hiyo, ni zaidi ya asilimia 300 kwa miaka hii mitatu tumetekeleza mradi huu wa kupeleka umeme vijijini. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge, mwendelee kutuunga mkono ili tufanye kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Heche alivyosema; juzi tu alituomba tumpelekee umeme Susuni, tukapeleka; tumepeleka Kerenge, tumepeleka Nyamwaga, Nyanungu na Nyurito. Ndugu yangu Mheshimiwa Heche anataka nini? (Makofi)

MHE. JOHN W. HECHE: Taarifa.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano inatekeleza miradi kwa ufanisi sana.

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpe taarifa Mheshimiwa Heche na Wabunge wengine, mradi huu ni wa miaka minne iliyobaki, mwaka…

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.


NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, muda wetu umekwenda sana, kwa hiyo, sitaruhusu taarifa kwa sasa. Mheshimiwa Dkt. Kalemani endelea.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Niwape tu taarifa Waheshimiwa Wabunge, tunachukua michango ambayo wamesema kuhusiana na utekelezaji wa miradi hii, lakini tumejipanga vizuri kwa upande wa vifaa, sasa hivi Wakandarasi wameshaanza kupeleka vifaa site. Ni matumaini yetu kuanzia mwezi ujao speed itaongezeka zaidi ili kufikisha umeme kwenye vijiji ambavyo tumepanga kuvitekeleza kwenye mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la mikataba ya Songas; kwanza nikupongeze kupitia Kiti chako kwamba mwaka 2018 kupitia kwa Mheshimiwa Spika wakati ule, Waheshimiwa Wabunge waliunda Kamati Maalum ya kupitia mikataba hii ya kuzalisha gesi, mafuta pamoja na biashara. Kwenye mapendekezo ya Kamati, ilipendekezwa mikataba yote ipitiwe upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ni sikivu sana, imeanza kupitia upya mikataba yote ukiwemo Mkataba wa Songas. Kwa hiyo, suala la kwamba mkataba ufutwe, urekebishwe ufanyiwe maboresho, itatokana na mapendekezo ya Kamati ambayo sasa marekebisho na mapitio ya mikataba hiyo yanafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini yetu matokeo ya kupitia mikataba yatakuja na mapendekezo ya kuboresha ambayo nia ya Watanzania ni kuhakikisha kwamba stahili ya Watanzania kwenye mikataba hii inapatikana. Kwa hiyo, niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba kwa vile mikataba inapitiwa kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ni matumaini yetu mapitio hayo yataboresha zaidi, siyo kwa upande wa mkataba wa Songas tu, lakini mikataba yote ya kuzalisha gesi pamoja na utafiti wa gesi na mafuta hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kusema kuhusiana na Mradi wa Kinyerezi. Tunayo miradi mingi sana. Mradi wa Kinyerezi wa megawatt 185 hivi karibuni utakamilika. Bomba la gesi ambalo Waheshimiwa Wabunge wanataja, ni kweli kabisa huwezi kuona mahitaji makubwa ya gesi kwa sasa kwa sababu viwanda vingi vya gesi vitaendelea kujengwa. Tutakuwa na mradi wa Kinyerezi Na. 1 unaoendelea extension, tutakuwa na Kinyerezi No. 3 wa megawatt 600 pamoja na Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mahitaji na matumizi ya gesi yataongezeka zaidi. Kwa hiyo, uamuzi wa Serikali walivyofanya kujenga bomba kubwa ambalo leo tunaona matumizi yake ni madogo, siyo vibaya kwa sababu tuna miaka mingi, zaidi ya 100, kuendelea kutumia bomba hili. Kwa hiyo, kutumia asilimia ndogo wala isiwatishe, tutaendelea kutumia kwa sababu miradi mikubwa itaendelea kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa LNG ni kati ya miradi mikubwa sana duniani. Mradi huu mnatambua kwamba uwekezaji wake siyo chini ya Dola za Marekani bilioni 35. Hata hivyo, Serikali imeanza kuutekeleza mradi huu. Tunaposema ujenzi wa uchumi wa viwanda, ndiyo viwanda vya LNG tunavyozungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge na nitoe taarifa; mradi huu haujakwama na hautakwama na tumeanza kuutekeleza. Kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamesema, tumeanza majadiliano na mmoja mmoja, tumeanza na Equinor, lakini wadau wote ambao wanashiriki kwenye kuzalisha, tunajadiliana nao na sasa tunaongeza kasi ili maeneo ambayo yameshapitiwa, yakamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge wa eneo anakotoka kule Likong’o kwamba tathmini ya fidia ya wananchi imeshafanywa na imeshakamilika. Kinachofanyika sasa hivi ni kufanya uhakiki. Taratibu za uhakiki zikikamilika, wananchi watalipwa fidia na mradi utaendelea kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana kusema mengi katika miradi hii, lakini jambo la msingi pia ni umeme wa gridi Kigoma pamoja na Katavi. Katika mradi huu tunatekeleza miradi mikubwa miwili; wa kwanza, ni mradi wa kutoka Iringa, Sumbawanga, Mpanda, Kigoma hadi Nyakanazi ambao umeanza kutekelezwa kwa portion ya kuanzia Iringa mpaka Sumbawanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hatua za haraka ili tuwapelekee umeme wa gridi wananchi wa Kigoma pamoja na Katavi, Serikali kuanzia Desemba mwaka 2018 tumeanza kutekeleza mradi wa kusafirisha umeme wa kilovoti 132, umbali wa kilometa 391 kutoka Tabora, Urambo mpaka Kidahwe, Kigoma. Mradi huu tumeshatenga fedha, Dola za Marekani bilioni 81. Mradi utatekelezwa kama tulivyosema na utakamilika Februari, 2020. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, Katavi…

NAIBU SPIKA: Muda umekwisha Mheshimiwa Dkt. Kalemani. Ahsante sana.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa FAO wa Kuzuia Uvuvi Haramu kupitia Bandari za Nchi Wanachama pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kuanzishwa kwa Ushirikiano wa Kimataifa wa Nishati ya Jua (The Framework Agreement on the Establishment of International Solar Alliance)
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nami napenda nitoe shukrani kwako mwenyewe pamoja na Makatibu wanaokusaidia katika meza wakati wa kuliongoza Bunge hili Tukufu wakati wa mawasilisho Azimio hili muhimu. Niendelee kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge na kwa kuanzia Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Nishati ya Madini kwa wasilisho lake nzuri ambalo kimsingi limeunga mkono karibu kwa asilimia mia moja. Pia niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia na kwa kiasi kikubwa wametoa mapendekezo lakini kimsingi wameridhia kwamba Azimio hili liungwe mkono.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache, yako mambo mahususi ambayo yamejitokeza ambayo Waheshimiwa Wabunge wangependa kupata uhakika wa ufafanuzi wa kina. Baadhi ya mambo ambayo ni ya msingi sana ambayo wananchi wangependa kusikia kutoka kwenye Bunge letu Tukufu ni utashi wa Serikali. Napenda niliambie Bunge lako Tukufu kwamba utashi wa Serikali wa kutekeleza Azimio hili ni mkubwa sana na ndiyo maana mmeridhia katika kikao chako hivi leo na sisi kama Serikali baada ya Azimio kuridhiwa na Bunge sisi ni kwenda kutekeleza mara moja. Kwa hiyo utashi wa kiserikali upo, niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wanaotusikiliza.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na matumizi ya solar, baadhi ya vyanzo vya nishati hapa nchini ni pamoja na rasilimali ya solar. Tunavyo vyanzo vingi sana vya kuzalisha umeme, kama ambavyo mnafahamu tuna vyanzo vya rasilimali gesi, tuna vyanzo vya rasilimali maji, makaa ya mawe, upepo na kadhalika, lakini pia solar.

Mheshimiwa Spika, kulingana na tafiti ambazo zimeshafanywa, na nimeshukuru sana baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kutaka kujua mikakati. Mkakati wa kwanza uliokwishafanyika ni kufanya utafiti wa kina na kubaini uwezo uliopo wa kuzalisha nishati ya solar. Tafiti zilizofanywa mpaka kuishia mwaka 2015 zinaonesha Tanzania tunaweza tukazalisha umeme wa solar kufikia mpaka megawati 1,000.

Mheshimiwa Spika, na bahati nzuri sana, Tanzania tuna potential kubwa ya mionzi ya jua. Potential tuliyonayo sisi ni kilowatt-hours 4 mpaka 7 kwa mita za mraba kwa siku ambapo kipimo cha kimataifa ni kilowatt-hours 3.97, kwa hiyo tuko juu sana kwa maana ya rasilimali ya jua tuliyonayo. Lakini katika mwaka pia Tanzania tunaweza tukapata mionzi ya jua mpaka takribani ya saa 2800 mpaka saa 3500 kwa mwaka kwa hiyo vyanzo vya kuzalisha umeme wa solar ni vingi.

Mheshimiwa Spika, nilitaka kutoa taarifa hiyo ili kuwapa uhakika kwamba baada ya azimio hili kupita na matarajio tuliyonayo ni kwamba Serikali tunakwenda kufanikiwa kwa kiasi kikubwa kuwepo na umeme wa solar hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine limeelezwa kwamba pengine ni muhimu kutekeleza mradi huu kuliko Bwawa la Julius Nyerere. Nataka niseme mkakati wa Serikali ni kuzalisha umeme mchanganyiko kwa kutumia rasilimali zote tulizonazo. Ni kweli zipo tofauti kutoka chanzo kimoja kwenda kingine lakini nataka niseme, chanzo cha kwanza kabisa kwa unafuu katika kuzalisha umeme ni umeme wa maji ambao unatumia shilingi 36 kuzalisha uniti moja ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na umeme wa pili unaofuata kwa unafuu ni huu umeme wa solar ambao wenyewe utazalisha uniti moja kwa Shilingi ya Tanzania 103.28, kwa hiyo bado nao ni wa nafuu. Lakini pamoja na hayo bado tunaona ni jambo la busara kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo mchanganyiko ndiyo maana tunaendelea kuzalisha pia vyanzo vingine.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunasema, pamoja na mambo mengine, unapotumia umeme wa solar unakabiliana kwa hatua ya juu sana na uharibifu wa mazingira, lakini pia usimamizi wake nao ni mwepesi na kwa sababu vyanzo tunavyo, rasilimali ya kutosha, na tumejipanga kwa ajili ya kutekeleza jambo hilo tunadhani azimio hili likipitia itachangia kwa kiwango kikubwa sana kuzalisha umeme wa solar na kuingiza kwenye Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, ni kweli kwa sasa katika Gridi ya Taifa hatujaweza kuunganisha umeme wa solar ingawa tunao umeme wa off-grid katika maeneo mtambuka nje na Gridi ya Taifa chini ya megawatt tano. Kwa hiyo mkakati wetu ni kuzalisha walau megawatt 1,000 za umeme wa solar nazo ziingie kwenye Gridi ya Taifa, na ni kupitia azimio hili likipitishwa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, na ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo ni muda mwafaka sana sasa kukubali azimio hili ili tuingize umeme wa solar katika Gridi ya Taifa na kuchangia ipasavyo katika kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge Ruth alisema tulisaini mwaka 2015, ninapenda niweke sahisho dogo tu; sisi tulisaini mwezi Novemba, 2016. Hata hivyo, mikakati ambayo Mheshimiwa Mbunge alipenda kuona tumechukua ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mkakati wa kwanza ni kuweka mpango wa kuzalisha umeme wa solar kwa miaka 30 ijayo ambao tumeweka walau zaidi ya megawati 1,000. Lakini mkakati wa pili ni kuendelea kutafuta fedha; napenda kuishukuru sana Serikali, katika Mwaka wa Fedha 2019/2020 kupitia Mpango wa Umeme Vijijini, Serikali ilitenga shilingi bilioni 38 kwa ajili ya kuwawezesha wazalishaji wadogowadogo kuzalisha umeme wa solar kwa ajili ya kusambaza umeme vijijini. Hii ni hatua kubwa sana kwa Serikali ilichofanya katika hatua za kwanza za mipango mikakati ya kuhakikisha kwamba rasilimali ya jua nayo inatumika kwenye kuunganishia umeme wananchi.

Mheshimiwa Spika, hatua ya pili ni kwamba bado tunaendelea kupata fedha kwenye makampuni na mashirika ya kimataifa. Benki ya Dunia katika mwaka huu wa fedha pia imetoa dola milioni moja kwa ajili ya kusambaza umeme vijijini. Na hii ni hatua kwa ajili ya kuwawezesha Watanzania wadogowadogo kuweza kuzalisha umeme huu wa solar ili nao uweze kutumika katika maeneo ambako Gridi ya Taifa haijafanikiwa kupita; hii ni mikakati ambayo Serikali inaendelea kuifanya.

Mheshimiwa Spika, mikakati mingine ambayo Serikali inafanya katika eneo hili ni kuhakikisha kwamba wazalishaji wadogowadogo wa Tanzania, hasa binafsi nao wanashiriki katika kuzalisha umeme wa aina hii. Mwaka jana mwezi Oktoba tulitangaza kwa wazalishaji wadogowadogo, na hasa Watanzania, ili waanze nao kuzalisha umeme huu wa solar walau kuanzia megawati 50 mpaka megawati 250. Taratibu zinazofanyika sasa ni kukamilisha uchambuzi ili kuwapata wakandarasi wa ndani ili nao waweze kuzalisha umeme huu. Huu ni mkakati muhimu sana shirikishi ambao Watanzania pia tunawashirikisha.

Mheshimiwa Spika, mkakati mwingine mahususi katika eneo hili, kama ambavyo nimeeleza, ni kuhakikisha makampuni ya Kitanzania yanashiriki. Hivi sasa – kwa kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Tibaijuka – yako makampuni zaidi ya saba ya Watanzania; yupo Lex Energy, yupo Enzora, yupo Baraka, yupo ITOZ, yupo ZOTI, yote hayo ni makampuni ya Watanzania wadogowadogo na wanashiriki katika kuzalisha umeme mdogomdogo na kusambaza kwa Watanzania. Kwa hiyo, ushirikishwaji wa Watanzania uko palepale.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, bado kama Serikali tunawahamasisha Watanzania waendelee kushiriki kwa kiwango kikubwa sana katika kuzalisha umeme huu wa solar ili kuweka mchango mkubwa kwa ajili ya matumizi, lakini kujenga sustainability kwa Watanzania hata kwa miaka mingi ijayo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maelezo niliyosema katika eneo hili, lakini ningependa tu kusema kwamba mkakati mwingine tumetenga maeneo. Yapo maeneo mahususi sana ambayo ni muhimu na yanaweza kuzalisha umeme wa jua. Baadhi ya maeneo tunayo hata hapa Dodoma, eneo la Zuzu linaweza kuzalisha megawati 50 mpaka 100; eneo la Kishapu kule Shinyanga, megawati 150 mpaka 250; eneo la Mkwese kule Manyoni, Singida megawati 100 mpaka 250 na eneo la Same kule Kilimanjaro nayo yanaweza kuzalisha umeme. Haya maeneo tumeyaainisha na kuyatenga kwa ajili ya kuzalisha umeme wa solar.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, hii ni baadhi ya mikakati tu tuliyochukua kuhakikisha kwamba umeme huu unanufaisha hasa rasilimali ya ujenzi wa uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa manufaa; pamoja na kwamba kwa sasa tunaomba kuridhiwa, lakini kwa vile tulishasaini mkataba huu yapo manufaa ambayo Serikali ilishaanza kuyapata. Hivi sasa ninapongea wapo Watanzania ambao wameshaenda kupata ufadhili wa ISA ambao wanakwenda kusoma kwa level ya PhD kwa ajili ya masuala hayahaya ya solar ili waweze kutoa mafunzo kwa Watanzania wengine. Na bado kuna nafasi ambazo tutaendelea kuzipata kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa levels za chini, kati na juu ili Watanzania wengi waweze kupata elimu hii na kuweza kuwafundisha Watanzania wengi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaposema tutakuwa na umeme mwingi hapa nchini, umeme mwingine unatakiwa utokanae na huu utaratibu wa solar. Na tuna mpango huo kwa sababu unapokuwa na umeme wa kutosha na mchanganyiko, hata inapotokea dharura katika vyanzo vingine bado unaweza kuendesha nchi bila kuwa na mashaka yoyote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo utaratibu huu wa ISA hadi sasa mwaka jana tulishiriki kwenye mkutano na ISA ime- commit kwa mwaka wa fedha ujao kutoa takribani Dola za Marekani milioni 385 kwa nchi yetu, na nchi yetu imekuwa- committed pesa nyingi kuliko nchi zote duniani ambazo zimeshiriki kwenye hii ISA, kwa hiyo ni mafanikio makubwa endapo Serikali yetu itaridhia.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu yaliyosemwa ni mengi, itoshe tu nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kweli kwa michango yenu mizuri, lakini Serikali imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda kwa kutumia umeme mchanganyiko. Na mikakati na malengo yetu ni kufikisha megawatt 10,000 mwaka 2025 na kuwapelekea Watanzania umeme pote wanapokaa mijini na vijijini kwa zaidi ya asilimia 85 na kupeleka Gridi ya Taifa maeneo yote ya pembe nne za nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia katika sekta yangu ya nishati na nikushukuru sana kwa kunipa hii fursa nikiwa msemaji wa karibu na mwisho.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia ningependa nitoe shukrani kwanza kabisa kwa Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maelekezo na miongozo thabiti katika kutekeleza shughuli za Wizara yetu, hakika tunamwombea kila la heri katika usimamizi wa shughuli zake za kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan anavyotuelekeza kusimamia miradi hii na sughuli mbalimbali za Wizara yetu na niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uongozi wake thabiti, sisi kama Mawaziri kutusimamia kutekeleza majukumu ya Serikali. Niendelee kumshukuru sana Dkt. Ali Mohammed Shein, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kusimamia vyema Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa Serikali ya mapinduzi Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, pia nikushukuru wewe mwenyewe kwa miongozo mahiri sana katika shughuli za Bunge. Nadhani kila mtu ni shahidi, hongera sana Mheshimiwa Spika. Namshukuru sana Mhshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote katika michango yetu tuliyopata, ushauri na maoni mbalimbali. Nikiri kwamba yote tutakwenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru sana Naibu Waziri wangu, Mheshimiwa Subira Mgallu jinsi anavyonisaidia katika shughuli mbalimbali katika Wizara lakini katika kufuatilia mambo ya utekelezaji wa Wizara yetu. Niendelee kuwashukuru sana watendaji wa Wizara yetu na taasisi zake pamoja na bodi zake zikiongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara yetu Dkt. Mwinyimvua.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Chato napenda popote walipo niwashukuru sana kwanza kwa kunifikisha hapa, lakini pia kwa kuniombea kutekeleza majukumu ya Serikali huku na shughuli ya jimbo naendelea nayo. Hongereni sana wananchi wa Chato, tuko pamoja na ninyi, tembeeni kifua mbele.

Mheshimiwa Spika, niipongeze na kuishukuru familia yangu ikiongozwa na mke wangu Violeth Kalemani ambaye ananiwezesha, kuniandaa vyema kusimama mbele ya Bunge lakini hata katika utekelezaji wa majukumu ya Kiserikali, mama Vaileth na watoto wako, watoto wangu pia, hongereni sana na Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache, naomba sasa nirudi kwenye michango ya Waheshimiwa Wabunge. Kwanza tumekiri kupokea mawazo na ushauri juu ya hoja mbalimbali za maandishi takriban 58 na michango mingine ya kuzungumza 52, kwa hiyo tuna jumla ya michango 110, lakini tunatambua bado michango mingine itaendelea kuja na sisi tunasema m bele ya Bunge lako Tukufu tuko tayari kuipokea na kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo machache, naomba nijielekeze kwa jumla jumla haitakuwa rahisi kujibu hoja moja baada ya nyingine. Nitaanza na kuchangia katika mradi muhimu wa kipaumbele katika Taifa letu wa kuzalisha umeme kutokana na maporomoko ya Mto Rufiji, megawatt 2,115.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, hoja hii imejadiliwa sana na bila shaka hakuna Mtanzania hadi sasa asiyejua umuhimu wa mradi huu. Kilichobaki Waheshimiwa Wabunge na Watanzania hebu tuunge mkono juhudi za Mheshimiwa Rais wetu, tuutekeleze mradi huu, tufike tunakokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili nina mambo matatu makubwa, la kwanza ni la ufahamu tu, hivi mradi huu unachukua eneo gani linalosemwa kwamba likiharibika ustawi wa jamii utakosekana? Hifadhi ya Selous ina ukubwa wa kilometa za mraba 50,000, eneo linalochukuliwa na mradi kwa ujumla wake kwa maana ya miundombinu yote ni kilometa za mradi 914.2 sawa na asilimia 1.8 ya eneo lote, hilo ni jambo la kwanza, ni muhimu sana Watanzania tukaelewa. La pili, katika hilo, tuta litakapojengwa eneo lile ni eneo dogo zaidi ukilinganisha na eneo lote la Selous ambalo ni kilometa za mraba 0.025 sawa na asilimia 0.025, eneo dogo sana.

Mheshimiwa Spika, sina sababu ya kuelezea sana katika hilo. La pili, mradi huu utakapokamilika utatupatia megawatts 2,115, uwezo wetu wa sasa wa umeme tulionao tuna jumla ya megawatts 1601.92 haufikii hata umeme tutakaopata kutokana na mradi huu. Kwa hiyo hapa naeleza manufaa ya haraka ya mradi huu.

Mheshimiwa Spika, la pili, suala la uharibifu wa mazingira limetajwa sana. Ni suala la kujiuliza wala halihitaji elimu ya juu sana. Leo hii tunapoongea wananchi wa Dar es Salaam wanatumia mkaa kwa mwezi magunia 5 00,000 ambapo kila gunia lina kilo 100, hapo ni Dar es Salaam peke yake. Wananchi wa miji mingine matumizi yao katika masuala ya nyumbani ni asilimia 68 lakini wananchi wa vijijini matumizi yao ya mkaa ni asilimia 27, lakini matumizi ya kuni ni asilimia 73, hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, la pili, ukijumlisha mkaa unaotumika Dar es Salaam na maeneo mengine, ukajumlisha mkaa unaotumika vijijini na maeneo mengine pamoja na kuni zinazotumika vijijini pamoja na mengine ni sawa na tani moja ya futi za ujazo ya mkaa pamoja na kuni zinazotumika ambayo inaweza ikavunwa katika eneo la hekta za ukubwa wa futi za ujazo 10 mpaka 12. Maana yake ukataji wa mkaa na kuni ni mkubwa zaidi tukiachia kutekeleza mradi huu kwa sababu Watanzania wengi wataendelea kutumia kuni na mkaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hapa hoja ya bure ni hii, hivi tukiacha kutekeleza mradi huu, tukaendelea kukata kuni na mkaa kwa hali hii hivi nani anaharibu mazingira. Tukiutekeleza mradi huu utatuwezesha kusambaza umeme mpaka vijijini. Kusambaza umeme mpaka kwenye miji, kusambazia umeme Jiji la Dar es Salaam linalotumia mkaa mwingi na hivyo kuokoa uharibifu wa mazingira. Kwa hiyo summary yangu katika hilo suala la mazingira, kuutekeleza mradi huu ni kutunza mazingira zaidi kuliko kuacha kuutekeleza mradi huu. Hii ni hoja ya msingi sana, ya bure kabisa na niwaombe Watanzania watusikilize, watufuate, tuutekeleze mradi huu. Tuepuke kuharibu mazingira yetu. Hiyo ni hoja ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili, gharama za mradi; ili uzalishe megawatt moja ya mradi huu, upate unit moja ya umeme utatumia shilingi 36 tu basi. Kwenye vyanzo vingine hali ikoje? Kwenye gesi nianzie hapo na haina maana kwamna naiponda gesi, nitaizungumza vizuri na yenyewe, kwenye gesi tunatumia shilingi 147 kwa unit, moja kwenye solar tunatumia shilingi 103 kwa unit moja, kwenye upepo tunatumia shilingi 103.2 kwa unit moja, kwenye makaa ya mawe shilingi 118 kwa unit moja. Ukienda kwenye nuclear ambayo bado ni 65 ambayo ndiyo inafuatia kwa wepesi pamoja na jotoardhi. Sasa tujiulize tunataka umeme wa ghali au mwepesi, tunataka tuzalishe umeme wa gharama nafuu ili Watanzania wa Maneromango kule waununue wa bei ya chini, hilo ndilo lengo la Serikali. Kwa hiyo gharama ya utengenezaji na uzalishaji wa mradi huu bado ni mwepesi ukilinganisha na miradi mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya tatu, umeme mchanganyiko; Waheshimiwa Wabunge na Watanzania naomba niseme kutekelezwa kwa Mradi wa Rufiji hakumaanishi hata kidogo (kamwe) kutotekeleza kutumia gesi, kutotumia solar na miradi mingine. Tunakwenda na umeme mchanganyiko, Waingereza wanasema energy mix na ndiyo maana leo umeme mkubwa tunaotumia hapa nchini kwa sasa ni umeme wa gesi asilia ambao katika jumla ya megawatts 1601.92 t unatumia gesi yenye umeme wa sasa megawatts 884 sawa na asilimia takriban 60 ya umeme tunaozalisha. Maana yake bado tuna kipaumbele cha kuzalisha umeme kwa kutumia rasilimali ya gesi. Hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Spika, la pili, matumizi ya gesi sio kuzalisha umeme tu, yako matumizi zaidi ya mara tano ya matumizi ya kuzalisha hiyo. Mpango wetu, tumegawanya mpango wa matumizi sahihi na endelevu ya rasilimali ya gesi kwa miaka 30 ijayo ambayo iko subject to review na yenyewe. Kwa sasa tumetenga takriban 8.8 kuzalisha umeme peke yake, lakini bado kwenye gesi hiyo hiyo tuna futi za ujazo 4.3 kwa ajili ya viwanda vitakavyokuja. Tunataka tujenge viwanda vya mbolea na petrochemicals na ni gesi hii hii tutaitumia. Hayo ni matumizi mengine.

Mheshimiwa Spika, pia tunataka tuwasambazie Watanzania gesi hii ili itumike kwenye viwanda vidogo vidogo na viwanda vingine ambapo napo tumetenga takriban futi za ujazo 3.65 ili ziweze kujenga viwanda. Vile vile tunategemea Watanzania baadaye wasiendelee kukata kuni na kutumia mkaa itumike gesi hii kwa matumizi ya nyumbani ambako nako tumetenga futi za ujazi 1.2 kwa ajili ya matumizi ya nyumbani na katika magari.

Mheshimiwa Spika, leo nimeleta gari linalotumia gesi. Kama ingewezekana kukanyaga ukumbini, ningependa sana likanyage mkaliona lakini kwa Waheshimiwa ya Wabunge na kwa ruhusa yako mara baada ya Bunge hili liko pale nje, Wabunge mnaruhusiwa kutazama muangalie miundombinu kwenye gari inavyotumia gesi. Lipo gari tumelileta kama mfano muone yanavyotumia gesi ambapo kwa sasa tuna magari zaidi ya 200 yanayotumia gesi kutoka magari 80 mwaka juzi, napo tunasonga mbele. Najaribu kuonesha matumizi ya rasilimali ya gesi ambayo wengi wanadhani inasahaulika, hata kidogo! Tunakwenda kuitumia kwa usahihi na usawa ule ule.

Mheshimiwa Spika, matumizi mengine katika gesi naendelea kupambanua kidogo kwa ruhusa yako. Gesi hii tunataka tuwe na viwanda vya vyuma, tutakuwa na ujenzi mwingi sana kwenye ujenzi vya uchumi wa viwanda ambavyo tumetenga futi za ujazo trilioni 1.1 kwa ajili ya viwanda special vya vyuma na bado sasa tunataka kujenga LNG. LNG Waheshimiwa Wabunge itatumia gesi kwenye mpango wetu, kila mwaka tumetenga gesi tani milioni 10 kila mwezi kwa ajili ya LNG tunayotaka kuijenga na LNG itahitaji gesi nyingi sana. Maana yake Waheshimiwa Wabunge, matumizi ya gesi bado yako pale pale hayajasahaulika kwenye umeme na kwenye masuala mengine.

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye umeme, bomba la Madimba, bomba hili linaendelea kutumia gesi hii. Limesemwa kwamba uwezo wa bomba ni mkubwa kuliko mahitaji kwa sasa lakini suala jepesi la kujiuliza hata unapotaka kujenga kiwanja cha ndege, hivi unaogopa kujenga kiwanja kikubwa kwa sababu una ndege moja? Ni afadhali ujenge kiwanja kikubwa utakaponunua ndege 100 zitatua pale. Nataka nilieleze Bunge lako Tukufu, bomba hili kwa sasa hivi na nimshukuru Mheshimiwa CAG wakati anakagua mwaka jana alisema matumizi yake ni asilimia sita ya gesi lakini mpaka sasa nataka niwaambie Waheshimiwa kupitia Bunge lako Tukufu mpaka sasa hivi matumizi ya gesi wala sio asilimia sita, imeshavuka! Imeshafika asilimia 16 na bado tunakwenda na hapa tumefungua tu mradi wa Kinyerezi namba II mwaka jana wenye megawatts 248.

Mheshimiwa Spika, tutaongeza megawatts 185 mwezi Agosti mwaka huu tutakapokamilisha Kinyerezi Na.I extension. Tutaongeza gesi nyingine kwenye kutumia, kwa sasa hivi gesi tunayotumia kwa siku ni milioni 120 milioni futi za ujazo kwa siku. Kwa hiyo gesi inaendelea kuingia kwenye kuzalisha umeme. Nataka niwahakikishie Watanzania kwamba pamoja na kutumia Mradi huu wa Mto Rufiji, bado matumizi ya umeme mchanganyiko ikiwemo gesi tunaendelea kuitumia.

Mheshimiwa Spika, tuna miradi mitatu mikubwa ya kuzalisha gesi katika umeme ikiwemo Kinyerezi I, Kinyerezi III yenye jumla ya megawatts 600 lakini tutaanza kwa awamu na megawatts 300 kwa phase one na phase two. Tuna Mradi wa Mtwara ambao tunaanza kuutekeleza mwakani nao wa megawatts 300 wa gesi.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge na ndugu Watanzania, matumizi ya gesi bado yapo pale pale. Nilikuwa najaribu kuwaondoa wasiwasi Watanzania kwamba kutumia maji katika kuzalisha umeme kwamba tunasahau matumizi ya gesi, la hasha hata kidogo, Mheshimiwa Rais yuko makini, Watanzania tuko makini, Waziri anayeongea yuko makini na Wabunge wako makini, tunaomba mtuamini. Hiyo ni hoja ya kwanza ambayo ningependa nichangie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili, umeme wa upepo. Imeelezwa hapa kwamba katika Mabunge yaliyopita tulieleza nia yetu ya kuzalisha umeme wa upepo kwa haraka haraka, lakini nataka niwaeleze wachangiaji, nimeeleza gharama za kuzalisha umeme kwa upepo, solar na kadhalika lakini katika miradi ambayo tulitaka tuitekeleze ukiwemo Mradi wa Singida na Same kupitia Geo Wind na Wind East Africa wazalishaji hawa walitaka tununue umeme kutoka kwao kwa senti za Marekani 13 kwa unit, jambo ambalo tungefanya hivyo tungeingiza mzigo mkubwa sana kwa Watanzania kupitia TANESCO kwa kununua umeme huo.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme kwa niaba ya Watanzania ni afadhali tuchelewe lakini tuhakikishe safari yetu tutafika salama kuliko kuwahi ukaenda kuishia korongoni. Tungetekeleza miradi hiyo tulikuwa tunakwenda kuwaangamiza Watanzania. Tulichofanya kwanza ni kuanza kupitia upya hizo bei za Watanzania kutakiwa TANESCO kununua, EWURA wamekamilisha, tunakwenda sasa kuzalisha umeme huo kwa bei pungufu ili kusudi TANESCO wakiununua Watanzania wanunuaji wasibebeshwe mzigo.

Mheshimiwa Spika, baada ya mapitio hayo ndiyo maana imetuchukua muda, kwa sasa hivi tutakwenda kama mzalishaji yuko tayari ndiyo maana tumetangaza Novemba mwaka uliopita kwamba kama kuna mzalishaji binafsi na tunawataka sana wazalishaji binafsi tunachotaka ni umakini wa masharti aje badala ya kuendelea na kujadiliana, majadiliano yasiyoisha muda wake. Tumeweka viwango kwamba mzalishaji wa umeme wa upepo kama yuko tayari kutuuzia unit moja kwa senti saba za Marekani na kushuka chini, huyo aje! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa makaa ya mawe, kama yuko tayari kutuuzia kwa dola senti sita huyo aje. Kwa solar kama anataka kutuuzia kwa dola senti tano huyo aje ili TANESCO wakiununua umeme huo atakuuzia wewe mlaji kwa bei ya chini. Tungenunua kwa bei ya senti 13 kama baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanashabikia tukimbilie tulikuwa tunakwenda kuishia korongoni. Kwa niaba ya Watanzania, kama Waziri niliyepewa dhamana, tutakuwa makini katika hili ili kutowabebesha mzigo Watanzania ambao ni wapiga kura wetu.

Mheshimiwa Spika, nimelieleza vya kutosha kwa nini hatukukimbia kuutekeleza, lakini tunakwenda kuutekeleza lakini tunakwenda kutekeleza kwa utekelezaji makini kwani Serikali iko makini, tutaifanya hivyo kwa niaba ya manufaa ya Tanzania. Hapo nimejibu suala la upepo kwa nini hatukutaka kufanya hivyo kwa sababu kuna watu walitaka tutoe maelezo.

Mheshimiwa Spika, hasara kwa TANESCO, hivi hasara ni kitu gani? Kwanza TANESCO imepata mizigo mikubwa sana huko nyuma. Kama ni hasara ziko sababu zilizochangia hasara kwa TANESCO. Sababu ya kwanza kubwa tulikuwa na miradi mikubwa ya kukodi mitambo, mitambo ya kukodi ya kuzalisha umeme wa mafuta mazito na ninyi wengi tunaifahamu Waheshimiwa Wabunge. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, Mabunge yaliyopita na Serikali zilizopita kwa kupiga kelele ili Serikali iachane na ununuzi wa mafuta mazito kuzalisha umeme ikiwemo mtambo wa IPTL, Aggreko, Symbion na mitambo mingine, kwa nini nasema hivyo? Tulikuwa tunalipa capacity charges kila mwaka, zaidi ya shilingi bilioni 635 kwa kampuni moja kuilipa kwenye mtambo mmoja. Hili lilikuwa ni zigo kwa TANESCO, hilo tumeachana nalo tangu mwaka juzi, kwa hiyo, hasara zinakwenda zinapungua.

Mheshimiwa Spika, la pili, viko vituo vingi, ukienda Madaba tulikuwa tunatumia mafuta, Ludewa mafuta, Songea mafuta, Mbinga mafuta, Kigoma mafuta, Loliondo mafuta, Mwanza Nyakato mafuta; na mafuta hayo, natoa mfano, Ludewa tu ulikuwa unaweza kununua mafuta ya shilingi bilioni 703, lakini ukiuza umeme unachovuna ni bilioni 331, hiyo ni hasara.

Mheshimiwa Spika, tulichofanya ni kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya kusafirisha umeme mkubwa, ili nchi nzima tuiunganishe kwenye gridi ya taifa tuachana na hiyo mitambo.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, mwezi juzi alizindua mradi mkubwa sana wa Makambako-Songea, ambao umetuokolea takribani shilingi bilioni 9.8 tulizokuwa tunanunua mafuta kwa ajili ya kuzalisha umemem na kuwasambazia Watanzania. Hizi zilikuwa ni hasara kwa TANESCO ndugu zangu, sasa tumeachana nazo. kwa hiyo zilikuwepo na mkakati ndiyo hiyo ninayoisema (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine ndugu zangu, TANESCO ilikuwa inaleta nguzo kutoka South Africa, ilikuwa inanunua luku za mita kutoka China, turansformar kutoka India, nyaya kutoka nje. Mwaka jana tumepambana na hili, tumesema lazima tujenge viwanda vya ndani, na njia pekee kwa vile vifaa vinavyopatikana nchini ni kusitisha uingizwaji wa vifaa hivi na kuliokolea gharama shirika letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge mliounga mkono jambo hili, wapo lililowaumiza, nafahamu, lakini tunasonga mbele kwa kuokoa gharama na hasara kwa shirika letu. Maana yake nini, tulikuwa tunaweza kununua nguzo moja mpaka kwa shilingi laki nne kwa fedha ya Tanzania. Nguzo kuitoa South Africa na inawezakana hiyo hiyo inazunguka inarudi, bado unatakiwa ui-clear bandarini. Suala siyo gharama tu, hata muda. Sasa hivi unaweza ukakimbia hapa Mafinga ukanunua nguzo moja kwa shilingi 80, ni kiasi gani shirika linaokoa gharama hiyo? Hizo zote zilikuwa ni hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa summary yake, mpaka mwaka juzi shirika lilikuwa na hasara ya shilingi bilioni 349, mwaka jana zimepungua, zimekuwabilioni 122, mwaka huu zinakwisha na kupata faida ya bilioni tisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na Waheshimiwa Wabunge nataka kusema, nini faida ya sitisho hilo? Kwanza tumeokoa jumla ya shilingi bilioni 162.34 ambazo tumenunua vifaa hivyo, lakini pili tumetengeneza ajira kwa watanzania zaidi ya 3520 kwa ajili ya viwanda hivyo. Kwa hiyo, tulikuwa tuna viwanda vitatu vya nguzo, sasa hivi tuna viwanda tisa, tulikuwa tuna kiwanda kimoja tu cha transformer, tuna viwanda takribani vitano. Tulikuwa tuna kiwanda kimoja cha waya, tuna viwanda sita, tulikuwa hatuna kiwanda hata kimoja cha luku, sasa hivi tuna viwanda vitatu vya luku, ndugu Watanzania naomba tuelewe hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mahitaji yetu ya ndani ya vifaa vyote kwa ujumla wake ni nusu ya uwezo wa viwanda vya ndani kwa sasa vilivyojengwa ndani ya miezi saba hadi sasa, hayo ni mafanikio makubwa, (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Suala la Madeni ya TANESCO. Mwezi januari mwaka 2018, ni kweli TANESCO ilikuwa na madeni takribani bilioni 990, lakini sasa hivi inavyolipa yamepungua sana, na inaedelea kuyapunguza, na mkakati wa kumaliza madeni yote kwa shirika hili ni ifikapo mwaka 2026, madeni yote TANSECO itakuwa imeyamaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sasa, madeni yake yanapungua limefikia bilioni 957, lakini tumemuomba mhakiki wa Serikali ayahakiki madeni haya. Yako madeni mengine yanabishaniwa na yako madeni mengine wala si halali; ni matumaini yetu yatapungua sana. Katika madeni hayo TPDC kimsingi, ambaye ndiye anayeuza gesi kwa kiasi kikubwa kwa TANESCO ndiye aliyekuwa na madeni makubwa, 480, lakini sasa yameshuka mpaka 340. Kwa sababu sasa hivi TANESCO ina uwezo wa kulipa, badala ya kulipa bilioni saba kwa wiki sasa hivi ina uwezo wa kulipa bilioni tisa kwa wiki, katika madeni ya TPDC.

Nalielezea Shirika la TANESCOkwa ujumla wake jinsi ambavyo sasa hivi limejipambanua. Silitetei kama shirika la umma lakini kwa kwa sababu sasa hivi lina uwezo wa kuwahudumia Watanzania. Zipo changamoto, lakini lina uwezo wa kuwahudumia Watanzania, na tunakokwenda lita- improve zaidi. kwa hiyo nimeona niseme hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa kuhusiana na madeni, kwa vile TANESCO ina uwezo wa kulipa madeni na kwa vile sasa hivi TANESCO haipati ruzuku kutoka Serikalini, tumemwomba Mheshimiwa Rais na ametuelekeza, shirika hili ni kubwa halina haja ya kuombaomba, shida ilikuwa ni usimamizi na sisi tunalisimamia. Kwa hiyo tangu mwaka juzi shirika hili halipati ruzuku kutoka Serikalini, linajiendesha lenyewe. Zaidi ya hapo linapata faida ya ongezeko ya asilimia 1.5 mwaka juzi na mwaka jana ni 7.6. Kama nilivyosema, ni matumaini yetu, kuanzia mwaka huu na miaka inayokuja, shirika la TANESCO litaanza kutoa gawio Serikalini. Hayo ni mafanikio, nilitaka kueleza kwamba pamoja na madeni hayo, lakini jitihada za kuyalipa ni kubwa na ni matumaini yetu yatakwisha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme moja katika suala la umeme vijijini. Ameeleza Mheshimiwa Naibu Waziri; mwaka 2008 tulikuwana vijiji 506 vilivyokuwana umeme, 506, mwaka 2015 tulikuwa na vijiji 2018 vilivyokuwa na umeme. Leo hii tunapoongea umeme vijijini tumeunganisha vijiji 7127, tunapoongea hapa. Mradi unapotekelezwa tunajua kunakuwa na changamoto nyingi sana. Mradi huu utakwisha mwezi juni mwakani, ni matumaini yetu utakapokamilika mwezi juni mwakani, utafikisha vijiji 10,128 vyenye umeme, sawa na asilimia 84 na tutabakiza vijiji 1990 katika ya vijiji 12,268. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Watanzania, sisi kwa sasa ndiyo vinara, ndio tunaoongoza kwa nchi ya Afrika Mashariki kutandaza umeme vijijini kwa asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzetu wakenya pamoja na kuwa na umeme wa MW 2,003, lakini wana asilimia chini ya 43 kupeleka umeme vijijini. Waganda, mpaka wametuomba tupeleke vijiji sita vya mfano nchini kwao ili nao waone umeme vijijini, na tumewapelekea vijiji vya mpakani, vikiwemo Nangoma pamoja na Umurushenya, tutaendelea kuwapelekea. Huu ni mfano kwa nchi yetu inavyopiga hatua.

Mheshimiwa Spika, lakini zipo changamoto katika suala hili; moja ya changamoto katika maeneo haya kwanza ni uelewa, kwamba hauwezi ukawa wa pamoja kwa wakati mfupi. Kazi yetu ni kuendelea kuwaelewesha wananchi na washirika wengine ili kusudi tuutekeleze mradi huu kama ilivyodhamiliwa.

Mheshimiwa Spika, lakini niwapongeze Waheshimiwa Wabunge, mnatupa ushirikiano mkubwa sana katika kupeleka umeme vijijini, nawapongeza sana sana Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mimi napenda niseme shukrani mlizotupa katika kupiga hatua kwenye umeme vijijini naomba ziwarudie Waheshimiwa Wabunge, mmefanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tutaendelea kutoa ushirikiano ili tupeleke umeme katika vijiji vyote. Lipo jambo lilizungumzwa hapa, kwamba viko vijiji 55 kwamba vilikuwa hewa. Nataka niseme, kwenye miradi hii mikubwa changamoto zipo; lakini kubwa, hata Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi, unaweza ukakuta kijiji kina vitongozi saba, lakini kati ya vitongoji saba ni kitongoji kimoja ndicho kimepelekewa umeme. Swali la kujiuliza, vitongoji vingine tuviache kwa sababu tulishapeleka kitongoji kimoja cha kijiji kile? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini unapopelekea umeme, hukiiti kitongoji, unaita kwa jina la kijiji. Kwa hiyo mnakuta majina mengine yamerudiwa hata zaidi ya 100, lakini tunapokwenda kule la kwanza ni kufanya survey ili kuona ni sehemu gani ya kijiji kilichopelekewa umeme, hakina, ndipo eneo hilo lipelekewe umeme. Nimeona nitoe ufafanuzi katika jambo hilo na kama kuna mahala ambapo kuna kuwa na oversight lazima tufanye replacement na tunafanya hivyo kwa kuwashirikisha Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nichukue nafasi hii kusema kwamba utekelezaji wa miradi hii tutaendelea kufanya usanifu ili kuwa na usahihi wa kutosha. Hata hivyo, tuko tayari kupokea mawazo na ushauri wa Wheshimiwa Wabunge ili tuweze kufanya marekebisho ya kuimarisha kazi hii.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili, ningependa sana niseme, nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge na Watanzania; ni kweli tunapopeleka umeme vijijini maeneo ya taasisi yanasahaulika sana, na ni changamoto si tu kwa shirika na kwa mkandarasi hata wasimamizi wa taasisi hizo. Nichukue nafasi hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge watusaidie kupitia wenyeviti wa halamshauri na wakurugenzi, maeneo yote ya taasisi ambayo yako kwenye vijiji vyenye umeme, niombe sana yalipiwe ili taasisi zote za umeme ziendelee kuunganishiwa umeme.

Mheshimiwa Spika, iko changamoto ya Waheshimiwa Wakurugenzi, Wenyeviti wa Halmashauri kuilalamikia Serikali, kwamba Kituo changu cha Afya hakina umeme, Zahanati haina umeme, shule haina umeme, lakini sababu haijalipiwa. Niwaombe sasa tutumie nafasi hii tulalamike tukiwa tumeshafanya malipo. Nami nitumie nafasi hii kuelekeza Shirika la Umeme TANESCO pamoja na wakandarasi popote watakapoona taasisi ya umma, iwe kilomita 100, iwe kilomita tano, ipelekeeni umeme, ili mradi pamelipiwa. Waheshimiwa Wabunge nimeeleza kwa msisitizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nirudie, nitoe maelekezo kwa wakandarasi, Shirika la Umeme TANESCO na wadauwengine wanaosambaza umeme, kwa niaba ya Serikali, popote pale, taasisi ya umme itakapokuwa, kutoka kwenye kijiji chenye umeme au eneo lenye umeme, iwe kilomita 100, iwe kilomita 20, iwe kilomita mbili, pelekeni umeme kwenye taasisi hiyo ili mradi imelipiwa gharama zake, nadhani limekaa sawa, elfu ishirini na saba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali ya awamu ya tano, na mimi nilisema niliposimama kwenye Bunge lako Tukufu, awamu iliyopita mwaka uliopita, nilieleza kwamba tutapeleka umeme mpaka kwenye nyumba za matembe. Watu walikuwa wanadhani tunatania, mpaka kwenye nyumba za makuti, walikuwa wanadhani tunatania, tuko seriousna jambo hili. Nyumba yoyoye ya mtanzania, mtanzania anamuishi, ndimo humo humo tutampelekea umeme, humo humo tutampelekea umeme. Atakapohama nasi tutapeleka umeme atakakoelekea,tunajali maisha ya watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, elfu 27 lengo lake ni kuhakikisha Watanzania wote wanapata umeme. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa maelekezo mazuri, kwa kujali Watanzania wa maisha ya kawaida. Tumefanya maamuzi, kupitia Bodi ya Shirika letu la TANESCO, kwamba umeme unaopelekwa vijijini, uwe wa REA, uwe unaopelekwa na TANESCO, ili mradi unapelekwa vijijini, kuanzia Mei mosi mwaka huu kuunganishwa umeme ni elfu 27 tu, basi. Iwe TANESCO, iwe REA, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, tukatoe elimu hii na mimi nimesimama hapa kupitia Bunge lako Tukufu, Watanzania wote wanisikie, wandarasi wote wanisikie, TANESCO wanisikie, Wabunge mnisikie, na mimi najisikia hivyo, gharama ni elfu ishirini na saba (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, suala secular lilishatoka na Waheshimiwa Wabunge mtapewa.

SPIKA: Hebu liweke vizuri, Mheshimiwa Waziri, hapo kwenye 27 hebu irudia tenaili Wabunge waondoke nayo vizuri. (Makofi)

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba nirudie kwa ruhusa yako. Kuanzia tarehe moja, Mei mwaka huu kupitia Shirika la Umeme Nchini (TANESCO), bodi imepitisha na secular ilishatoka na imeshaanza kufanya kazi, gharama ya kuunganisha umeme katika maeneo yote ya vijijini; iwe unapelekwa na REA, iwe unapelekwa na TANESCO, au yeyote aliyepewa kazi na Serikali, gharama ni elfu ishirini na saba tu basi. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, kwa heshima ya Bunge lako, nitoe maelekezo kwa mameneja wote wa kanda, mikoa, wilaya, wa TANESCO na Makao Makuu, walisimamie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Niendelee, Kukatika kwa Umeme. Katika maeneo ambayo pia tumeimarisha sana ni pamoja na eneo hili. Pamoja na kukatika kwa umeme katika baadhi ya maeneo, Serikali inachukua hatua za maksudi sana kuhakikisha kwamba jambo hili halijitokezi sana. Katika maeneo ya Dar es Salaam, nitoe taarifa kwa wananchi wa Dar es Salaam na Watanzania, shida inayotokea sasa hivi tulipata break-down ya engine moja, lakini Serikalikupitia kwa Mheshimiwa Rais wetu, tumeleta mashine ya MW 240 ambayo inafungwa sasa hivi kwa Dar es Salaam, ambayo ni matumaini yetu, ndani ya mwezi mmoja itakamilika. Kwa hiyo, maeneo yote ya Dar es Salaam na watanzani kwa sababu inajengwa kwenye gridi ya taifa, umeme utakuwa ni wa uhakika zaidi.

Mheshimiwa Spika, niwaombe Watanzania waendelee kuvumilia, kwa sababu ziko changamoto nyingi, lakini matumaini yetu umeme utakwenda kuimarika na kukatika itapungua sana.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu LNG. Mradi wa LNG umeelezwa sana, na mimi ningependa kurudia. Dhamira ya kutekeleza mradi huu iko palepale. Mradi waLNG utatekelezwa, nimetaja gesi tuliyotenga na hatua tuliyofikia sasa hivi. Nimshukuru sana Mheshimiwa Nape na Wabunge wengine wa Lindi, tuliokuwa nao hivi juzi katika semina tuliyoifanya. Tumekutana na wadau, tumekutana na wawekezaji pamoja na Serikali, tumekubaliana, majadiliano yataongeza speed. Ni matumaini yetu watamaliza mapema, ikiwezekana mwakani, ili utekelezaji uanze kufanyika na ujenzi utaanza miaka mitano ijayo na huu mradi utachukua muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumetenga mpaka fedha kwa ajili ya kufidia wananchi ambao wataathirika na mradi huu. Hii ni kuonyesha commitment ya Serikali kwa lengo la kuutekeleza mradi huu. Niseme tu kwamba ndugu zangu wananchi wa Lindi na Watanzania wote mradi hu ni mkubwa, tumeupa kipaumbele na utatekelezwa bila kusuasua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa suala kurudiwa mikataba hapa, Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameeleza. Iko mikataba ya rasilimali ya gesi, nikopongeze Mheshimiwa Spika, mwaka jana uliunda Tume Maalumu, kwa ajili ya kufuatilia na kukagua umuhimu, dosari na changamoto za mikataba hiyo. Nitoe shukurani sana kwako na kamati iliyofanya kazi hiyo; lakini nirudie kusema, Serikali inachukua hatua madhubuti sana.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ameshanza zoezi hili, ni matumaini yetu litakamilika. Lakini lengo letu kubwa, maama liko jambo limezungumzwa, la kutotoa leseni; lengo letu kubwa, ipo hatari ya kutoa leseni kwenye masharti ambayo ni hasi kwa Watanzania. Tunataka tujiridhishe, kuondoa wasiwasi, kwamba masharti yatakayoingiwa yatakuwa ni sahihi na bora kwa Watanzania baada ya mikataba hii kupitiwa vizuri na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, chukua muda kwa umakini, fanya kazi kwa umakini, toa kitu cha makini, tufanye kazi ambayo itakuwa na tija kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Usambazaji wa Gesi Majumbani. Tumeeleza katika taarifa yetu. Bila shaka katika eneo hili, kati ya maeneo ambayo watanzania watakumbuka sana utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ni pamoja na kutekeleza miradi ya kusambaza gesi majumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisirudie hasara ya mkaa pamoja na mambo mengine yanavyofanyika, lakini ni kubebesha mzigo kwa Watanzania. Watanzania wengi kwa sasa hivi, wengine unaweza kukuta wanakula mlo mmoja kwa sababu ya kuogopa gharama ya matumizi ya kupikia. Mradi huu utaokoa gharama kwa kiasi kikubwa. Mradi huu tumeanza kuutekeleza maeneo ya Dar es Salaam, tumeshaunga wateja zaidi ya 200 na yako maeneo mengi kwa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, tutakuwa na mikondo minne, mkondo wa kwanza wa kupeleka gesi ni ule unaotoka Ubungo, kupitia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam- Mlalakua mpaka Tegeta; mkondo wa pili unakwenda mpaka Mikocheni, mkondo wa tatu unakwenda mpaka Keko na mkondo wa nne unakwenda mpaka maeneo ya Chanika. Kwa hiyo ni matumaini yetu baada ya kusambaza vizuri gesi hii Watanzania, hasa wananchi wa Dar es Salaam watatumia gesi hii kupunguza ukakasi wa maisha.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili muhimu, tulichoanza kufanya, gesi kwa sasa hivi, ambayo tumeanza kuisambaza, ina punguzo la asilimia 40 ya gharama ya matumizi ya kawaida ya sasa hivi ya gesi asilia. Kwa sababu mitungi inayokuja kwa sasa wananchi wanalipa zaidi ya shilingi 50 na 57,000, lakini kwa matumizi ya gesi hii wanayounganishiwa, gharama yake itakuwa ni chini kwa asilimia 40 ya bei na gharama hiyo ya mitungi ya sasa.

Mheshimiwa Spika, vilevile wananchi wanatumia mkaa, nimetaja hasa mkaa wa kilo 100, utakuwa na punguzo si chini ya asilimia 35 mpaka 45. Kwa hiyo, utawapunguzia ugumu na ukakasi wa masiha wananchi kwa ajili ya kutumia rasilimali hii.

Mheshimiwa Spika, Umeme wa Grid Kigoma na Katavi. Yako maeneo tunakubali, kwamba Serikali bado inayafanyia kazi. Tumeanza kutekeleza, tuna miradi miwili, mradi wa kwanza ni wa kupeleka umeme mkubwa wa kV 400, kutoka Iringa kupita Mbeya, Tunduma hadi Sumbawanga. Utekelezaji wa mradi huu umeshaanza, umbali wa kilometa 624. Pia tuna eneo la kutoka Sumbawanga - Mpanda - Kigoma hadi Nyakanazi. Utekelezaji wa eneo hili sehemu yake bado na tunaendelea na majadiliano kupata wawekezaji ili tuanze kuutekeleza. Tumeona tuanze kupeleka umeme mwingine kutoka Nyakanazi kupita Kigoma hadi Geita, utekelezaji wake umeanza.

Mheshimiwa Spika, mradi wa kunusuru Kigoma kwa sasa kwa haraka, ni huu mradi wa kuusafirisha umeme wa kV 132 kuutoa Tabora kupitia Urambo kwenda Nguruka hadi Kidahwe, umbali wa kilometa 391, utekelezaji umeanza na matumaini yetu kwamba tunaweza kukamilisha ifikapo juni mwakani. Kwa hiyo, wananchi wa Kigoma, katika eneo hili wawe na matumaini kwamba nao wataacha kutumia mafuta mazito na kuwapunguzia gharama kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Katavi, tutachukua umeme kutoka Tabora vilevile utapita Ipole kwenda Inyonga mpaka Nsimbo umbali wa kilometa 383. Utekelezaji unaenda sambamba na Mradi wa Kigoma. Miradi yote miwili itagharibu takribani dola za Marekani milioni 92.8. Utekelezaji wa miradi hii ni muhimu sana kuutaja ili pembe zote nne za nchi yetu ziweze kupata umeme wa gridi.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Rukwa ni kweli yako maeneo ambayo hayana gridi kwa sasa tunachukua gridi kutoka Zambia takribani megawati nane lakini yako maeneo tutatoa umeme kutoka maeneo ya Kigoma kupeleka Katavi hadi Rukwa wakati tunakamilisha Mradi mkubwa wa Sumbawanga hadi Nyakanazi.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge pamoja na kueleza maeneo hayo, lakini ningependa pia nizungumzie huu Mradi wa Bomba la Mafuta. Hivi sasa tumeanza kutekeleza Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda, tunafahamu kwamba imechukua hatua kufikia hadi sasa, lakini napenda kutoa taarifa tu katika Bunge lako Tukufu kwamba, mradi huu tunaendelea vizuri. Hivi sasa tuko katika hatua za mwisho kabisa za kumaliza majadiliano na majadiliano yakikamilika hatua inayofuata ni kuanza ujenzi. Nimpongeze sana Waziri wa Ardhi, Mheshimiwa Lukuvi wiki iliyopita ameshafanya semina kwa ajili ya tathmini ya wananchi watakaopisha miradi wakati wa ujenzi.

Mheshimiwa Spika, wakati tunafanya majadiliano hatua za awali za ujenzi zimeshaanza, kwa sasa tunachofanya ni kufanya maandalizi ya kupata ardhi kwa ajili ya ujenzi wa bomba, maandalizi ya kulipa fidia na kwa ajili ya kujenga vituo 16 vitakavyopitiwa na mradi huu. Hatua hii ni kubwa, ni sehemu ya utekelezaji wa mradi huu na ningependa nitoe taarifa kwamba utekelezaji wa mradi huu bado uko pale pale na tumepanga utakamilika ifikapo mwaka 2023, kwa sababu kwa sasa umechelewa kidogo, lakini muda wa kuutekeleza ni uleule, miezi 36.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuzungumza hapa, nilizungumza suala la IFAD watekeleze wataalam wetu, Huyo IFAD alikuwa ni Mkandarasi ambaye ni Consultant ambaye alikuwa anasimamia miradi ya ujenzi wa backbone, ilikuwa kuna hoja kwamba amefanyiwa malipo ya ziada ya milioni 97. Napenda kulieza Bunge Tukufu jambo hilo kwanza lishakuwa close na Mheshimiwa CAG na wala siyo jambo la kujadili kwa sababu alishalipa kulingana na makato ambayo yalifanywa kulingana na mkataba wake. Kwa hiyo jambo hili napenda tu nimweleze Mheshimiwa Mbunge aliyekuwa anataka kujua usahihi wa jambo hili kuwa usahihi wenyewe uko katika hali hiyo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuzungumza kwa sasa ambalo ni vema sana niwaambie Watanzania ni makusanyo na mapato ya shirika letu. Si kwamba narudia naeleza eneo dogo na sehemu niliyokwishaeleza kwa sasa Shirika la Umeme (TANESCO) wako wananchi na baadhi ya watu wanasema ligawanywe, ningependa kuchukua nafasi hii kuwaeleza Watanzania kwamba jamani umeme ni usalama, umeme ni biashara, umeme ni uchumi, sipingani na wanaosema shirika ligawanywe, lakini ningependa sana tuwe makini katika kuchukua hatua za kulimega shirika hili kabla hatujafanya hivyo. Kwa nini nasema hivyo? Ukisema uzalishaji ufanywe na mtu binafsi na amiliki mitambo ya kuzalisha maana yake atakuwa na mamlaka ya kusema leo nazima umeme nakarabati nchi nzima, matokeo yake nchi mnaweza mkaingia gizani, hilo ni jambo mahususi Watanzania tulielewe tunaweza tukaligawa lakini lazima tuwe makini katika kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, katika usambazaji, ni matumaini yangu kama tutaipatia shirika na bahati mbaya ikiwa ni shirika binafsi lisambaze umeme mpaka vijijini ni mashirika machache na wengi wameshajaribu na kushindwa, yatakayoweza kufanya hivyo, matokeo yake watapenda kupata faida kubwa na Watanzania wengi uwezo wao ni mdogo jambo la msingi hapa kitakachokuwa Watanzania watashindwa kumudu na hivyo azma ya Serikali ya kupeleka umeme nchi nzima itashindikana. Ningependa kutoa wito Watanzania tutoe maoni namna bora ya kulifanya shirika letu liimarike zaidi badala ya kuligawa vipande vipande. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru ulipokuwa unazungumza umeme mchanganyiko, mtu akasema kuna umeme solar muhimu sana kuweko kwenye gridi ya Taifa, ulimjibu mpaka nikasema kumbe Mheshimiwa Spika ni mwanasayansi. Unaweza ukatumia ukaweka umeme wa upepo kwenye gridi ya Taifa megawati 1,000, umeme wa upepo megawati 1,000, lakini umeme wa solar unategemea jua.

Kwa hiyo siku jua limeshuka utakosa megawati 1,000, siku jua limeshuka na inategemea na mpango mkakati, hili jambo lazima lielezwe kwa sayansi sana, namwona sana Mheshimiwa Heche anataka kuamka lakini ajiandae na ufafanuzi wa kisayansi.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema hapa katika gridi ya Taifa standard katika kataifa yote umeme wa renewable kwenye absorption ya umeme haitakiwi azidi asilimia 15, kwa sababu ya kuogopa risk. Kwa hiyo kama tuna megawati 1,600 tunatakiwa tuingize umeme wa renewable walau asilimia tano mpaka 15 ikizidi hapo unaiweka nchi katika hatari ya kukosa umeme itakapotokea dharura hiyo. Napenda niseme na kupongeza kwa argument hiyo, (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, umeme wa upepo kulingana na stadi tulizonazo speed maana potential tuliyonayo kwenye umeme wa upepo ni speed ya upepo, speed ya upepo tuliyonayo kwa sasa hivi ni speed ya kuanzia 4.5 meter per second mpaka meter 9.0 per second. Kwa hiyo ikipungua speed maana yake unakosa umeme wa upepo vilevile, haya ni masuala ya kisayansi sana, lakini napenda niyaseme kwa maana ya uelewa Waheshimiwa Wabunge. Kubwa unapokuwa na umeme mchanganyiko na hasa unapokuwa na umeme mwingi wa maji gharama yako itakwenda kupungua. Wenzetu wa Misri ambao wana umeme zaidi ya megawati 4,000 wa maji ndiyo maana bei yao iko chini ya dola 4.6 dola za Marekani, sisi yetu iko juu kwa sababu tumetumia pia gharama kubwa kwenye ku- compute gharama za umeme na kwa sababu hatujazalisha umeme mwingi wa maji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo napenda kutumia nafasi hii kurudia tu kusema kutumia umeme wa maji, kutumia umeme wa gesi, kutumia umeme wa makaa ya mawe ni muhimu sana, lakini yako mambo mawili ya kuzingatia kwanza gharama ya kuijenga mtambo huo na ya pili gharama ya kuwauzia wateja walaji wa mwisho utakapokamilika mradi huo. Ndiyo maana tunasema mara baada ya miradi hii kukamilika na masuala mengine yanayoendelea, ni matumaini yetu kwa Serikali yetu makini inakwenda kutazama upya bei kwa gharama za umeme ili kuwapunguzia mzigo Watanzania ambao tunatumia kodi yao kuzalisha umeme huu kwa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliyotaka kueleza ya msingi nimeyaeleza, sasa ningependa nitumie nafasi hii kwa niaba yako na Waheshimiwa Wabunge nishukuru kwa michango yao, kuna mengi ya kusema mengine tutaendelea kuyaeleza na kwa sababu hiyo mengine tutayaeleza kwa maandishi tutaleta ufafanuzi kwenye Bunge lako tukufu na mengi tumeomba yaiingie kwenye Hansard.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika mada hii muhimu ya Mpango uliopo mbele yetu. Kwanza napenda nimpongeze sana Waziri wa Fedha na Mipango kwa kutuletea Mpango huu mzuri sana. Wapo wachangiaji takriban 10 waliochangia eneo hili, lakini kwa sababu ya muda, nitaeleza kwa ufupi maeneo machache sana.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla tumeamua kujenga uchumi wa viwanda. Ili tuelekee kwenye uchumi wa viwanda, jambo muhimu sana ni kuwa na umeme wa kutosha, unaotabirika na wa gharama nafuu. Nimeanza na jambo hili tuone ili tunapoelekea tuko namna gani. Nianze na suala la kuzalisha umeme mchanganyiko ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelizungumza kwa kirefu sana.

Mheshimiwa Spika, hoja iliyoko mbele yetu hapa tunaweka kipaumbele gani. Mpango wa Serikali yetu ni kuzalisha umeme mchanganyiko na ndio mpango tulionao kwa kutumia vyanzo vyote tulivyonavyo ili kujiridhisha tunapata umeme wa kutosha, unaotabirika, wa uhakika na wa gharama nafuu.

Mheshimiwa Spika, tumeanza kuzalisha umeme hapa nchi toka mwaka 1964 katika mtambo uliopo Hale-Tanga wa megawatts 21.5. Tukaja Mradi wa Nyumba ya Mungu, nao bahati nzuri upo Tanga, maporomoko ya maji wa megawatts nane; baadaye tukaja Mtera karibu na hapa Dodoma, megawatts 80 mwaka 1980. Kwa hiyo, toka miaka hiyo, toka ukoloni mpaka mwaka wa 2000 tulikuwa tunatumia umeme wa maji. Baadaye miaka ya 2000 tulianza kutumia umeme wa rasilimali ya gesi asilia. Hapo kwa umeme tulionao hapa nchi ambao ni zaidi ya megawatts zaidi ya 1,601 asilimia 62 ya umeme tulionao kwa sasa unatokana na rasilimali ya gesi. Kwa hiyo tunaitumia gesi kwa sasa kwa kiasi kikubwa kuzalisha umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hoja ya kwamba pengine hatufuati sana vyanzo vingine haipo. Tunazingatia vyanzo vyote kuzalisha umeme ilimradi uwe umeme wa uhakika, unaotabirika na wa gharama nafuu. Kwenye rekodi tulizonazo umeme wa gharama nafuu kabisa kuliko vyote ni wa rasilimali ya maji. Ili uzalishe megawatts moja ya umeme wa maji unahitaji Shilingi 36 tu basi, fedha ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umeme wa pili unaofuata kwa gharama nafuu, ni umeme wa nyuklia Shilingi 65 peke yake unapata unit moja ya umeme. Unaofuata kwa bei ya chini ni umeme wa solar pamoja na upepo unaohitaji Shilingi 103 kuzalisha unit moja. Umeme unaofuata kwa bei ya chini naomba mnifuatilie vizuri unafuata pia umeme makaa ya mawe ambao ni Shilingi 118 kwa unit. Umeme unaofuata ni umeme wa joto ardhi ni Shilingi 119 hadi 120. Umeme unafuata ni Shilingi 147, umeme wa rasilimali ya gesi Shilingi 147 kwa unit; na umeme wa mwisho ni wa mafuta mazito Shilingi 546 kwa unit. Nimalizie kusema, lazima mwisho wa siku umlegezee mzigo mwananchi wa kawaida na huu ni umeme wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nilipongeze Bunge lako Tukufu,mwaka jana, mwaka juzi na mwaka huu kwa kukubali kutekeleza Mradi mkubwa wa Julius Nyerere utakaozalisha megawatts 2,115. Hata hivyo, haina maana kwamba hatuzalishi miradi mingine, tunaendelea kuzalisha umeme wa gesi na hivi sasa tuna mpango wa kuzalisha megawatts 300 kule Mtwara; megawatts 330 kule Somanga Fungu na tunaendelea kuzalisha megawatts 185 Kinyerezi one extension na miradi mingine.

Mheshimiwa Spika, kwa Mradi huu wa Julius Nyerere ambao utatupa megawatts 2,115 ambao kama nilivyoeleza gharama yake ya kuujenga ni nafuu kuliko miradi mingine, maana yake tunakwenda kupunguza gharama ya umeme kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze jambo moja; kwanza napenda nitoe taarifa, mradi unaendelea vizuri na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu juzi aliutembelea, nisingependa kumsemea lakini aliona mradi unakwenda vizuri na sisi tutaendelea kutembelea hadi ukamilike.

Mheshimiwa Spika, China ambayo ndio anaongoza kuwa na mradi wa kuzalisha umeme duniani, kuna mradi mkubwa wa maji unaozalisha megawatts 22,160, mradi mmoja. Kwa hiyo naomba nisisitize kwamba pamoja na mambo mengine, pamoja na kuzingatia umeme mchanganyiko, lakini pia twende kwa vipaumbele vinavyolenga kweli kujenga uchumi wa viwanda wenye gharama nafuu. Bado narudia, tunatumia vyanzo vyote ndio maana nimesema kwamba rasilimali ya gesi tutaendelea kuzalisha miradi mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo matumizi mengine mazuri sana kwa miradi ya gesi pamoja na kuzalisha umeme katika mradi wa gesi, gesi pia inaweza ikatumika kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vingine; kutengeneza mbolea, kujenga viwanda vya Ngozi, viwanda vya vyuma na kadhalika. Kwa hiyo matumizi ya rasilimali ya gesi bado yapo palepale. Sio rasilimali ya gesi tu nimetaja vyanzo vingine ndio maana tunakwenda kuzalisha umeme wa upepo na jua na uko mpango wa kukamilisha mradi huo mwakani Julai utakaozalisha megawatts 1,100 kwa hiyo vyanzo vingine tutaendelea kuvitumia. Langu la msingi hapo kutoa taarifa hii Bungeni, nitaeleza kwenye mpango na bajeti yetu muda utakapofika, lakini leo nimeona niliweke jambo hili sawa ili Watanzania tujue tunakoelekea.

Mheshimiwa Spika, katika miradi hii ambayo nimeitaja hapa, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba, vyanzo vyote ambavyo viko kwenye mpango wetu vinatumika kuzalisha umeme kwa ajili ya kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa, tutakapozalisha mradi huu wa Julius Nyerere tutakuwa na takribani megawatts 4,887 hapo mwakani mwezi Juni. Kwa hiyo umeme utakaobaki mahitaji yetu, mwakani tutahitaji umeme takribani megawatts 2,001. Kwa hiyo umeme utakaobaki takribani 2,102 tutaweza kuwauzia majirani zetu pia na kuingiza fedha nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nitoe taarifa, kwa sababu mradi huu na naomba nisali mbele yako, mradi huu ukamilike na nina uhakika utakamilika. Tarehe 15 Novemba, 2021, kabla ya saa kumi na mbili jioni tunaanza kujaza maji kwenye bwawa letu ili tuanze kupata umeme wa kutosha. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, nimeona nilieleze vile jambo hili.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Nishati, Spika hajakusikia bado umesemaje?

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, Tarehe 15 Novemba, 2021, kabla ya saa kumi na mbili jioni tunaanza kujaza maji kwenye bwawa letu, kuelekea kwenye kupata umeme wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwenye suala hilo. Naomba niishukuru sana Serikali, hadi sasa katika mradi huo tumeshalipa trilioni 2.04, ambayo ni sawa na asilimia mia moja ya mahitaji ya malipo yanayotakiwa kulipwa kwa Mkandarasi. Naipongeza Serikali kwa sababu hatujachelewa kulipa na tunayo matumaini tutaendelea kumlipa fedha ipo na mradi utakamilika kwa wakati. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye suala la matumizi ya gesi Mtwara, jambo ambalo limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge. Kwa kweli napenda kwa hekima ya pekee niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Mtwara na Lindi kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, rasilimali ya gesi tuliyonayo kwa sasa tunazaidi ya trilioni 57.54 na maeneo makubwa sana tunayotumia ni kwenye kuzalisha umeme lakini tumeanza kutumia pia kwa matumizi ya nyumbani. Kwa Mtwara peke yake, kama nilivyowapongeza Waheshimiwa Wabunge, Mtwara tuna mitambo 13 ya kuzalisha umeme wa gesi. Na umeme wa gesi kwa Mtwara ambao ni megawati 30.45 wakati mahitaji yao ni megawati 15, tunayo ziada ya umeme kwa Mtwara na Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara na Lindi kwasababu wametuhamasisha sana kwamba umeme wa gesi unatumika. Lakini gesi hiihii inatumika kwa sababu suala la msingi ni hii gesi inatumikaje kwa Mtwara. Tumeanza kutumia gesi, na mpaka sasa tumetumia trilioni 0.053 kwa ajili ya kuwasambazia gesi nyumbani wnanachi wa Mtwara na maeneo ya Lindi.

SPIKA: Ahsante sana.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wa Mikoa ya Lindi na Mtwara kwamba tutaendelea kutenga gesi kwa ajili ya kutumia nyumbani.

Mheshimiwa Spika, kwasababu ya muda, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuja kuhitimisha hoja. Nianze kukupongeza wewe mwenyewe kwa jinsi ambavyo umeongoza mjadala kwa upeo wa hali ya juu sana, ahsate sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumepata wachangiaji takribani 82 waliochangia kwa maandishi na wengine kwa kuzungumza na wengine kwa namna mbalimbali. Tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza niwahahakishie kwamba michango yenu yote mliyoitoa kwetu, ushauri na mapendekezo na maoni yenu sisi tunachukulia kama maelekezo ya kwenda kufanyia kazi. Tunawashukuru sana kwa michango yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na kuchangia katika maeneo takribani 12, kwa ujumla jumla na machache sana nitagusia kwa kipekee. Nianze kuzungumzia Mpango wa Serikali wa kufikisha megawatt 5000. Tumeeleza kwenye kitabu chetu cha Mpango na Bajeti ya mwaka huu. Tunatekeleza miradi mikubwa mingi lakini mradi ambao kwa kweli Watanzania tungependa wote kujivunia ni Mradi wa Julius Nyerere, tunakwenda vizuri. Tumeeleza kwenye kitabu kwamba tumefikia asilimia 52 lakini ukienda kule site unaweza ukadhani tumefikia asilimia 80 na kitu, kazi inakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie Watanzania na Waheshimiwa Wabunge kupitia Bunge hili Tukufu mradi huo unakwenda kukamilika ndani ya wakati. Nilizungumza siyo siku nyingi zilizopita kwamba hivi karibuni Novemba mwaka huu tunaanza kujaza maji bwawa. Ni kweli kuja kufika tarehe 15 Novemba 2021, tunaanza kulijaza maji bwawa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi siku hiyo wachache wetu itakuwa ni siku ya sherehe. Kwenye mabwawa kama hayo huwa kuna hatua kubwa mbili; ya kwanza, siku ya kujaza bwawa na ya pili ya kuchaji umeme unapokwenda kutumika kwa wananchi.

Niwaondoe wasiwasi ndugu zangu wananchi na Waheshimiwa Wabunge tutalijaza mpaka kufikia tarehe 25 Aprili, 2022 bwawa letu litakuwa limeshajaa maji ya kuanza kuzalisha umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyowahi kusema kuja kufika tarehe 14 Juni 2022 tunaunganisha kwenye Gridi ya Taifa, tunawasha transformer na wananchi wanaanza kupata umeme. Ni jambo ambalo nimeona niliweke wazi leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sina sababu ya kurudia manufaa ya miradi kama hii, lakini jambo la msingi ambalo Waheshimiwa Wabunge mmechangia ni kuwepo umeme mchanganyiko. Ni kweli tumejipanga vizuri sana kusema ukweli kuanza kutekeleza miradi ya kila aina kuhakikisha tunapata megawatt 5,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mradi huu mkubwa wa Julius Nyerere, lakini tuna mipango ya miradi mingine ya gesi asilia ambapo mwakani kuanzia mwezi Septemba tunaanza kutekeleza mradi wa megawatt 300 kule Mtwara ambao utaunganishwa kwenye Gridi ya Taifa baada ya miezi 18. Kwa kueleza michache tu ni kwamba tumejipanga vizuri na Waheshimiwa Wabunge mnatusaidia kupitisha bajeti leo, sisi kazi yetu kubwa ni kwenda kuhakikisha tunapata megawatt 5,000 ndani ya muda mfupi kufika mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi LNG ni muhimu sana na ni wa kimkakati. Ni lazima tukiri kwamba tumepoteza muda mrefu kidogo, lakini lengo ilikuwa ni kujipanga vizuri ili tusiliwe na wawekezaji. Mnafahamu vizuri sana ni kupitia Bunge hili mlishauri kwamba mikataba yote ya rasilimali ya gesi ichambuliwe na kupitiwa vizuri ili iwe na tija na manufaa kwa Watanzania. Naishukuru sana Serikali imeitika wito, imechambua mikataba yote sasa kazi imekamilika na tunaanza majadiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nitoe taarifa mbele yenu Waheshimiwa Wabunge tumeanza majadiliano toka mwezi uliopita na majadiliano yatachukua takribani miezi sita kutoka wakati huo na baada ya hapo utaratibu wa utekelezaji unaendelea. Kwa hiyo, niwape matumaini wananchi wote wa Kusini na Watanzania kwa ujumla mradi wa LNG unaanza sasa kutekelezwa tena kwa speed kubwa. Kwa hiyo, niwaondoe wasiwasi ndugu zangu wananchi katika jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la msingi hapa kuna suala la mgawanyo na matumizi ya gesi. Ni kweli tumegundua gesi nyingi sana takribani futi za ujazo trilioni 57.54 lakini kiwango tunachokitumia kwa sasa pamoja na kutumia kwa kiwango kikubwa katika kuzalisha umeme takribani asilimia 67 ya umeme tunaotumia, pamoja na kupeleka majumbani zaidi ya wananchi 1,000, magari 700 na viwanda 58 na kadhalika bado tumetumia chini ya asilimia moja kwa maana ya trilioni tulizonazo, ni 0.57 tu ya gesi tuliyoitumia, kwa hiyo, bado tuna gesi nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpango wetu ni nini? Kwanza, ni kuhakikisha kwamba mradi huu wa LNG ambao utatumia takribani tani milioni 10 kila mwaka, kwa matumizi ya gesi kwenye kiwanda hiki gesi itatumika kwa kiasi kikubwa sana. Hadi kumaliza mpango wa utekelezaji wa mradi huu, tutakuwa tumetumia trilioni 3.9 kwenye rasilimali ya gesi. Hicho ni chanzo cha kwanza kuanza kuitumia gesi kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunaendelea kuzalisha umeme wa gesi, megawati 300 Mtwara, megawati 330 Somangafungu na Kinyerezi I na Kinyerezi II tumetumia gesi, tunakwenda kuanza tena Kinyerezi III megawati 600 tutatumia rasilimali ya gesi. Matumizi yetu yatapanda, kwa sasa tunatumia takribani futi za ujazo milioni 200 kwa siku lakini matarajio yetu zitapanda maradufu katika miaka miwili ijayo. Kwa hiyo, niwaondoe wasiwasi wananchi kuhusu utumiaji wa rasilimali ya gesi.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la msingi tuna miradi mikubwa ya gesi, mradi wa kwanza tuna bomba la Uganda. Tunataka tutumie Mkuza huu wa bomba la kutoa mafuta Hoima kuja Tanga na sisi tutumie sehemu hiyo hiyo kupitisha gesi yetu kuwauzia majirani zetu Uganda. Vilevile, tunatarajia kujenga bomba lingine la kutoka Dar es Salaam kuelekea Tanga hadi Mombasa litakalotumika kupeleka gesi pia maeneo ya Mombasa nchini Kenya. Kwa hiyo, bado rasilimali yetu itatumika sana katika maeneo yote. Nimeona hili nilifafanue kwamba rasilimali ya gesi haitakaa idle itaendelea kutumika kwa ajili ya manufaa ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ni muhimu sana Watanzania kulielewa, katika mafanikio ambayo Awamu ya Tano na Awamu ya Sita imepata ni huu mradi wa treni ya mwendokasi ya kisasa ya kutumia umeme. Haya ni mafanikio makubwa sana. Nilieleza kwenye bajeti yetu kwamba hadi sasa tumeshajenga kilometa 160 kwa asilimia 100 hata ukitaka ulete leo treni ya mwendokasi ya kisasa ya kutumia umeme kama tunataka iishie Morogoro, inaweza ikaanza kukimbia hata wiki ijayo na ikafika mpaka Morogoro kwa sababu tumeshajenga na tumekamilisha kwa asilimia 100. Haya ni mafanikio makubwa sana, naipongeza sana Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mradi wa EACOP wa kusafirisha mafuta kutoka Hoima. Huu ni mradi wenye manufaa makubwa sana. Tumeeleza hivi karibuni takribani mikoa nane, wilaya 24, kata 134, vijiji 257 na vitongoji 527 vinapitiwa na mradi huu. Maana yake nini? Maeneo yote niliyoyataja yanakwenda kukua kiuchumi. Kwa hiyo, hii ni fursa kubwa sana kwa wananchi wetu kuchangamkia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuwaambia wananchi wote wanaopitiwa na miradi hii, waanze kujiandaa kuchukua fursa hizi ambazo kwa asilimia 80 ziko kwa Watanzania. Zaidi ya asilimia 80 ya mradi huu uko Tanzania maana yake ni kwamba sisi ndiyo wenye fursa ya kupata manufaa makubwa kutokana na mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilieleza vituo vingapi vitajengwa, kwa haraka haraka tutajenga takribani vituo nane kwa ajili ya kusukuma mafuta lakini vituo 6 kati ya 8 vyote viko Tanzania na vitakuwa na makambi ya wafanyakazi. Tutakuwa na maeneo ya kufunga valve kwenye vituo 79 lakini maeneo 53 yako Tanzania, hizo ni fursa. Tutakuwa na maeneo ambako tutachemsha mafuta hayo kwa sababu ni ya kuchemsha, kati ya vituo 29 vituo 22 viko Tanzania, hizo ni fursa kwetu. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Watanzania kutumia fursa hizi ili kuleta manufaa kwao. Mradi umeshaanza kutekelezwa, ni matumaini yetu ndani ya miaka mitatu mradi utakamilika na manufaa tutayaona zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa zaidi katika Mkoa wetu wa Tanga hasa kule Chongeleani, bandari ya Tanga inakwenda kupanuka sana kwa sababu hapo ndiyo mafuta yatakapokwenda kusimama na kutakuwa na uwekezaji mkubwa zaidi ambapo uwekezaji wa nje tunatarajia kwa Serikali yetu kunufaika kwa asilimia takribani 55. Haya ni manufaa makubwa ambayo Watanzania ni vyema kujivunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi wa REA. Pamoja na maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda niwahakikishie Watanzania na Waheshimiwa Wabunge mradi huu wa REA III round II, tunakwenda kumaliza vijiji vyote na huu siyo utani, hii ni dhamira ya Serikali. Tumedhamiria ni lazima tumalize. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge katika hili kwani wametupa ushirikiano wa kutosha katika kila hatua. Niwaombe, kama kuna Kijiji katika eneo lako kimesahaulika, ama kimerukwa kwa namna yoyote ile tukiwa hapa Bungeni tuletee kabla hatujaondoka ili twende tukakijumlishe na kifanyiwe kazi. Suala la umeme kwa sasa ndugu zangu sio la hiari ni jambo la lazima. Ni lazima tuelewane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ameeleza Naibu Waziri, tumejipanga vizuri leo tuko wa kwanza Barani Afrika kupeleka umeme vijijini lakini tunataka tusiishie hapo tuwe wa kwanza kupeleka umeme bora na wa uhakika, ndio lengo letu la msingi. Vijiji vilivyobaki tumepeleka wakandarasi, tumebakiza wakandarasi watano ni matumaini yetu kwamba wiki ijayo nao wanaweza kupatikana ili mikoa na maeneo yote wakandarasi wawe wameshafika site. Nitumie nafasi hii kutoa wito kwa wakandarasi, mkandarasi yeyote atakayelegalega hata kabla hajachelewesha mradi tukimbaini njiani, tunamuacha, tunamtelekeza, tunachukua mkandarasi mwingine, hiyo hatua tunayokwenda kuchukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeeleza Watanzania Mradi wa Umeme Vijijini haubagui nyumba na hili nisisitize kwa watani wangu wa Dodoma. Zile nyumba zetu za tembe zote ni umeme, hatuchagui nyumba. Najua mmeshatoka huko lakini tunataka Watanzania wote waone hii ni fursa. Nazungumza huu si utani, leo nenda Kongwa kwa Mheshimiwa Spika, Bahi, Singida angalieni barabarani, nyumba za aina hiyo tunataka zikue zifanane na magorofa, wananchi wa-enjoy maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika mradi huu tumejipanga vizuri. Katika maeneo ambayo vitongoji vimebaki, tuna mradi wa vitongoji almaarufu densification. Huu mradi ni muhimu sana, tumetenga shilingi bilioni 366 kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote, hiyo ndiyo dhamira ya Serikali. Pia tuna maeneo ambayo kimsingi sio vijiji yanaitwa mitaa lakini ukiyatazama kwa hali halisi na wala si mitaa kwenye macho ya Watanzania. Hasa maeneo katika Majiji, Manispaa, Halmashauri za Miji yako mengi, tumeanza kushughulika nao. Kwa sasa tumebaini maeneo 637, maeneo ya Dar es Salaam, yakiwemo ya huko Chanika, Bombambili, Dondwe, Msongole, Zingiziwa hayo yote tunawapelekea umeme. Hata kule kwa Naibu Spika kule Tonya, Ituhi, Nzoho, tunapeleka umeme kwa bei hiihii. Hata kwako Mheshimiwa Spika ulisema pale Mbande Kati na Mbande Kisimani tunapeleka kwa bei hii hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwahakikishie wananchi wa Majiji ya Mwanza, iwe Nyamanoro, Nyamadoke, Kishiri, Kabaha, Kalemela yote tunapeleka umeme kwa bei hiihii. Arusha, iwe Murieti, Olasiti, Moshono, Terati, bei ni hizi hizi. Dodoma, iwe Ntyuka, Nala, Vikonje tunapeleka kwa bei hiihii. Tumetenga shilingi bilioni 160 kwa ajili ya kupeleka umeme katika maeneo haya ambayo yanatuchanganya ni vijiji ama ni mitaa. Sisi kwenye macho ya Serikali tumedhamiria yote yawe shilingi 27,000. Kwa hiyo, Watanzania wote watapata umeme bila kuchelewa. Kazi hii si ndogo lakini Serikali tumejipanga, Wabunge mmejipanga najua leo mnatupitishia bajeti, mkishamaliza kupitisha bajeti sisi mtatuona vijijini hatutakaa ofisini, lengo tupeleke umeme kwenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikandamizie mbele ya Bunge lako Tukufu, umeme iwe kijijini anapeleka REA au mjini anapeleka TANESCO bei ni shilingi 27,000. Naomba nirudie, bei ya kupeleka umeme ukiondoa City pale Ilala Dar es Salaam ambapo hata kwa sasa hawahitaji wana umeme, maeneo yote nchini ni shilingi 27,000. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan, Oyeee. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Oyeee. (Makofi)

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba niwaelekeze TANESCO, atakayesuasua kutekeleza agizo hili, hajitaki na atakuwa hana kazi. Hayo ndiyo maelekezo ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kuuziwa nguzo, naomba nirudie, Serikali imegharamia nguzo kwa asilimia 100 na nguzo zipo. Mahitaji yetu ya nguzo kwa mwaka ni nguzo milioni 2.8, nguzo tulizonazo ni milioni 4.9, kwa hiyo, nguzo zipo. Naomba nisisitize kwa mara nyingine wakandarasi, Mameneja wa TANESCO, wala msijiingize kwenye mtego wa kusema mwananchi anunue nguzo tutakushughulikia mapema usiku na mchana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jipangeni, haiwezekani Watanzania wote waishi ndani ya mita 30 kutoka kwenye nguzo. Niwaombe sana TANESCO na wakandarasi mjipange katika hilo, lazima muwe wabunifu, mfanye kazi kwa kasi na uweledi wenye uaminifu. Sihitaji kurudia katika hilo, nadhani watendaji wetu wameelewa na hili linatekelezeka wala hatuna mashaka nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna suala la kucheleweshwa wananchi kuunganishiwa umeme. Ameeleza Mheshimiwa Naibu Waziri yako maeneo kuna sababu lakini pamoja na sababu nzuri tulizozitoa, tumeanza kuchukua hatua na tunawapima Mameneja wetu kwa vigezo viwili, ili apande cheo ni vigezo viwili vikubwa. La kwanza, kuunganishia umeme wateja kwa kasi, hilo ndilo lengo tunalowapimia. La pili, anavyohudumia wateja, hivyo ni vigezo vikubwa sana tunavyovizingatia. TANESCO inafanya biashara, kazi yake kubwa ni kuwajali wateja wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimeshaeleza na nimetoa miezi miwili kwa TANESCO Mameneja wote ambao wanadaiwa na wananchi wameshalipa pesa yao, hajawaunganishia umeme wakamilishe kufanya zoezi hilo ndani ya miezi miwili vinginevyo tutachukua hatua kwa Mameneja wanaohusika. Tumeanza kuchukua hatua, sio lengo letu kuwaonea, lakini tunataka wafanye kazi kwa umakini, kwa kasi na kwa kweli kwa ubunifu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi ambalo napenda kuzungumzia ni kuhusu kukatikakatika kwa umeme. Tumeeleza kwa kiasi kidogo, naomba nirudie tu kidogo. Yako kweli mazingira, nchi yetu ndugu zangu ni kubwa, unauzungumzia waya unatoka Mtwara mpaka Kagera, unatoka Mtwara katika Mtaa wa Mkunjanguo unakwenda mpaka Kyaka, mazingira haya ni marefu, yako maeneo kwa kweli hali halisi inatokea waya ukakatika, hilo nalo lipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, lazima tukubali bado tunatumia nguzo za miti kwa kiasi kikubwa, baada ya miaka miwili zinaoza, si kwamba hazina ubora ndiyo nature ya miti yetu haiwezi kukaa miaka mingi, hiyo changamoto nyingine. Sababu nyingine ni matumizi yetu sisi wananchi, mtu anaweza akagonga nguzo, akachoma moto na kadhalika. Hata hivyo, tumeweka bajeti tumeeleza hapa, mwaka huu tumetenga bajeti ya ndani ya TANESCO shilingi bilioni 85.8 kurekebisha dosari hizo ndogo ndogo ili umeme uwe imara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi kabisa tumeeleza, baadhi ya maeneo kwa kweli njia ni ndefu, umeme unafika ukiwa kidogo. Tumetenga fedha nyingi sana mwaka huu zaidi ya shilingi bilioni 150 kwa ajili ya kujenga vituo vya kufua umeme katika maeneo hayo ili kuimarisha upatikanaji wa umeme. Tumefanya hivi Handeni, Kilindi, Simiyu, Ipole, Nguruka, Urambo na maeneo mengine tunaenda kufanya hivyo. Leo tumeanza kutekeleza mpango wa kujenga substation Mkuranga ili Mbagala ijitegemee na Mkuranga ipate umeme wake, lengo ni kuboresha njia hizo za umeme. Hatukusudii kuendelea kuwa na umeme unaokatika, tumejipanga vizuri na Wabunge mnatuunga mkono, ni matumaini yetu hili jambo tumelipa muda mfupi mbele ya safari tutakwenda vizuri. Tukikamilisha Mradi wa Julius Nyerere nataka niwaambie Watanzania hii nchi inakwenda kuwa Ulaya ya Afrika, hizi ni dosari za wakati huu tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na suala la kukatika kwa umeme Serikali inakwenda kupitia upya bei za ankara za umeme kwa Tanzania. Tunakwenda kuangalia bei kulingana na uzalishaji. Tulisema uzalishaji wa mradi huu unachukua mpaka unit 1 Sh.36 ukilinganisha na vyanzo vingine. Sitaki kutaja kila chanzo, lakini ndio chanzo cha gharama ya chini kabisa unapozalisha umeme, kwa hiyo, Serikali tutafikiria pia kufanya mapitio ya bei za ankara kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bei za visiwani, wazalishaji wadogo maeneo mengine wanaitwa Wananzengo wanawauzia wananchi umeme kwa bei kubwa Sh.3,500 wakati unit 1 kwa bei elekezi ya Serikali ni Sh.100 kwa Watanzania wa kawaida. Tulitoa maelekezo mwaka juzi, tumetoa maelekezo mara nne na leo narudia mara ya tano. Niwaombe na kuwaagiza wazalishaji wote wadogo wadogo, bei elekezi ya Serikali ya kuuza umeme kwa Watanzania ni Sh.100 kwa unit na si vinginevyo. Kwa hiyo, wazalishaji walioko visiwani, Mheshimiwa ameeleza hata kule Ukerewe kuna wazalishaji wa namna hiyo, wako Buchosa kule Maisome wanafanya hivyo, wako Nyantakara Biharamulo, wako Mafia, wako Njombe na Makete na maeneo mengine, tulishawapa muda warekebishe dosari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nielekeze viongozi wenzetu wanaosimamia usalama wa wananchi kule, Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa watusaidie, tulishatoa maelekezo na hata kwenye kanuni na mikataba yao hiyo bei haimo wanafanya hivyo kurejesha faida. Hatuwezi tukakubali arejeshe faida kwa maumivu ya Watanzania, bei inaeleweka.

Kwa hiyo, ni marufuku wazalishaji wengine wowote wale, kuzalisha umeme sio shida, wahudumieni wananchi wetu lakini bei ya umeme lazima iwe linganifu shilingi 100 kwa unit na si vinginevyo. Hili narudia leo tusilisikie tena tutachukua hatua kali dhidi ya wazalishaji hao wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na gridi Kigoma, Katavi na maeneo mengine. Kwanza niwapongeze Waheshimiwa Wabunge wote wa Kigoma na Katavi mnajitahidi sana kutupa ushirikiano. Nataka niwahakikishie kwa Kigoma peke yake, kuna njia nne zote zinashambulia kupeleka gridi ya umeme Kigoma. Njia ya kwanza ni ile ya dharura ya kutoka Urambo, tunapitisha substation kutoka Urambo, Nguruka mpaka Kidahwe na mwakani tunakamilisha, hiyo ya kwanza. Ya pili ni kutoka Kigoma hadi Nyakanazi kilometa 283 kutoka Nyakanazi tunapeleka KV 220 Kigoma mpaka Kidahwe, hiyo ni ya pili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaanza kutekeleza Malagarasi, niipongeze sana Serikali wiki iliyopita tumepata dola milioni 140 kwa ajili ya kuanza kutekeleza mradi wa Malagarasi. Napo tunajenga mradi kutoka Malagarasi kilometa 53 mpaka tena Kidahwe, hiyo ni njia ya tatu. Ya nne ni kutoka Sumbawanga hadi Mpanda mpaka tena Kigoma jamani, wananchi wa Kigoma mtafurahi tu muda sio mrefu. Tunashukuru sana kwa ushirikiano wenu lakini Serikali imejipanga vizuri sana katika hilo. Tuvumilieni kidogo lakini Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan amejipanga vizuri, Makamu wa Rais yuko vizuri, Waziri Mkuu ndio usiseme anatuongoza vizuri tutawafikishia umeme wa gridi Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vivyo hivyo hata Mpanda tumeanza kutekeleza mradi mzuri wa kutoka Tabora kupitia Ipole, Inyonga mpaka Mpanda. Juzi akaeleza Mheshimiwa Mbunge mwingine tupitishe mpaka Nsimbo, tutapita Nsimbo kwa sababu gridi inapita maeneo yale yale. Kwa hiyo, tuna matumaini kwamba umeme wa gridi utafika maeneo yote. Kwa wakati huu tuna vifaa ambavyo vitakwenda kurekebisha tatizo kwa muda mfupi lakini suluhisho la muda mrefu kwa wananchi wa maeneo hayo linakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata wananchi wa Simiyu, Simiyu ni Mkoa unaojenga viwanda, tumeanza kujenga gridi ya Taifa kutoka Ibadakule Shinyanga umbali wa kilometa 109 kwa kutumia fedha ya ndani, eneo la Imalilo tumeanza kutengeneza muda si mrefu. Kwa hiyo, ni matumaini yetu tutakamilisha vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, deni la ZECO na TANESCO. Kwanza niishukuru Serikali mwaka juzi kulikuwa na deni la VAT la shilingi bilioni 22. Kwa umakini wa Serikali yetu deni likaondolewa, tunawapongeza sana viongozi wetu. Limebaki deni la KVA charge, nitoe tu mrejesho kwamba linakwenda vizuri, technical team ya masuala ya Muungano, kwa taarifa nilizopewa leo imekaa mwezi uliopita na tarehe 8 na tarehe 9 mwezi huu itakaa kwa ajili ya kufanyia kazi jambo hili kwa sababu liko kwenye Serikali ya Muungano na litakamilishwa muda si mrefu. Kwa hiyo, wenzetu wa Zanzibar mtuvumilie kwa sababu najua kamati ile ya masuala ya Muungano inalifanyia kazi kwa kina sana Inshaalah najua matokeo yake yatakuwa mazuri zaidi kama ambavyo imekuwa siku za nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumze kidogo kuhusiana na vituo vya mafuta vijijini. Tunaposema kupeleka nishati vijijini naomba isitafsirike kwamba ni umeme peke yake. Nishati vijijiji ni pamoja na mafuta vijijini pamoja na gas ya mitungi vijijini. Tumeanza, katika mwaka uliopita tumepeleka takriban vituo vidogo 221 vijijini vya mkono mmoja walau wananchi wanaomiliki bodaboda na taksi waweze kupata mafuta kule vijijini. Hivi viroba vya mafuta kubebwa kwenye bodaboda tunataka yafike mwisho ili wananchi nao wapate huduma hii kulekule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumejipanga vizuri na wenzetu EWURA tuliwaambia wafanye mapitio upya pamoja na taasisi nyingine kuondoa mlolongo na ukiritimba na gharama kubwa ya uanzishwaji wa vituo hivi; ambavyo vinafanya Watanzania washindwe kuviendesha. Kwa hiyo, matumaini yetu tutakwenda vizuri katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imeelezwa vizuri kuhusiana na deni la Mradi wa Bomba la Gesi Madimba. Serikali yetu inalipa na tunakwenda vizuri na mradi hauna mashaka. Deni lilikuwa ni Dola za Marekekani bilioni 1.2 tumeshalipa zaidi ya milioni 221 na tunakwenda kulilipa vizuri. Kwa trend ya kulilipa ni nzuri na wenzetu wa Hazina wanatupa ushirikiano mzuri tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bei ya mafuta ameeleza Mheshimiwa Mwijage ni mtaalam mzuri sana. Mheshimiwa Mwigaje nakupongeza sana kwani umenisaidia sana. Kwa kweli bei hupangwa na soko la dunia. Masuala haya ya mafuta na gesi kuna wakati bei kwenye soko la dunia kwa sababu mbalimbali inaweza ikashuka. Mkiona hapa tumeshusha bei maana yake na kule imeshuka. Sisi huwa tunatangaza bei inayopangwa pia kwenye soko la dunia. Bahati nzuri sana bei inapopanda kwenye soko la dunia na huku ikapanda huwa tunapiga kelele lakini ikishuka kule na huku ikishuka huwa sisikii watu wakipiga kelele. Hiyo ndiyo fluctuation ya soko la dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili lazima tuelezane ukweli. Kwa hiyo, ndugu zangu kazi yetu ni kufuatilia, je, vyanzo vya bei hivi ni halisi? Niwaombe sana wenzetu Wakala wa Mafuta (EWURA) kuanza kufuatilia kisasa bei za soko la dunia katika mafuta ili Watanzania waweze kuelewa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda ambao umenipa, naomba labda nirudie jambo moja tu katika mradi wa EACOP. Watanzania wanataka kujua kuhusu semina kuelezea manufaa ya mradi huu na ule wa LNG. Tumetaka kuwa na semina kwenye maeneo ambako miradi inapita kwa ajili ya kuwajengea uwezo na ufahamu wananchi namna ya kushiriki kwenye miradi hii ya kimkakati. Semina hizi tumezianza katika maeneo ya Nzega lakini Waheshimiwa Wabunge mnaotoka katika maeneo ya miradi ya Kagera, Geita, Shinyanga mpaka kufika Tanga tunategemea kuanzia wiki ijayo tunaanza semina. Tunapenda sana tuwashirikishe Wabunge wawasaidie wananchi ili miradi hii iwe na manufaa na wajiandae. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusiana na kuwashirikisha katika kazi za bomba, tumeandaa kanzidata (database) kwa ajili ya makampuni yote. Makampuni yote ya ndani yameorodheshwa kupitia Kanzidata ya EWURA. Kwa hiyo, niombe kama kuna kampuni ya kizalendo, ya kitanzania na ina uwezo, sifa na nia ya kufanya kazi katika miradi hii ipeleke company profile yake EWURA ili kusudi wakati wa mchujo tuzingatie makampuni ya kitanzania siyo makampuni yaliyosajiliwa Tanzania. Hii ndiyo itakuwa jambo lenye manufaa kwetu kwa ajili ya kunufaika na miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa LNG tumeshalipa fidia ya shilingi bilioni 5.71. Tunachofanya sasa ni kufanya mapitio ya eneo ambako wananchi watanufaika. Yako maeneo ya Likong’o, Mtomkavu na Masasi ya Leo. Maeneo hayo yote tunataka wananchi washiriki ipasavyo katika mradi huu wa kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu leo kazi kubwa ni kuomba fedha na naomba mnitume tukakimbie tuwapelekee umeme kwenye vijiji, nisitumie muda mrefu sana, niwaomba Waheshimiwa Wabunge mtupitishie fedha zetu, sisi tupo tayari kwenda kufanya kazi. Ahsanteni sana kwa ushirikiano wenu na mimi naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. MEDARD M. KALEMANI: Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukrani nyingi sana kwako kwa kunipa heshima kubwa ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika Bajeti Kuu ya Serikali, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema sisi Waheshimiwa Wabunge wa Bunge lako tukufu, lakini kubwa nikupongeze na kukushukuru wewe kwa umahiri wako, uhodari wako, uzoefu wako, kwa kweli unaliongoza Bunge vizuri, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niwapongeze Waheshimiwa Wabunge na tujipongeze Waheshimiwa Wabunge wote tulivyo mpata Mheshimiwa Spika huyu, ahsanteni tujipongeze Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nimpongeze pia Mheshimiwa Naibu Spika kaka yetu Azzan Zungu kwa kazi nzuri anayofanya ya kukusaidia wewe. Kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kuchangia kwa namna hii toka nizaliwe naomba nianze mchango wangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda nikipongeze sana chama chetu Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri kinachofanya kutengeneza Ilani inayotekelezeka kwa mpango wa bajeti tunayokwenda kupitisha leo na kipekee nimpongeze sana Mwenyekiti wa chama chetu Ndugu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kukiongoza vizuri Chama cha Mapinduzi. Lakini kipekee nimpongeze kaka yetu Comrade Abdulrahman Kinana, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi anavyomsaidia Mheshimiwa Mwenyekiti wa chama chetu na nimpongeze Comrade Daniel Chongolo, Mtendaji Mkuu wa Chama cha Mapinduzi kwa jinsi ambavyo anasimamia Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitachangia kwa bajeti kuu ya Serikali kama ambavyo nimeomba, lakini kubwa naomba nianze kwa kweli kumshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuandaa bajeti kubwa na nono ambayo haijawahi kutokea kwa takribani miaka yote toka nchi yetu imeumbwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunakwenda kujadili na kupitisha bajeti hii kubwa ya shilingi trilioni 44.14; ni bajeti kubwa sana inayokwenda kujibu na kutatua kero za Watanzania wanyonge. Hongera sana Mheshimiwa Rais na Serikali kwa kutuleta bajeti hiyo kubwa. Lakini Waheshimiwa Wabunge mnakwenda kuvunja rekodi kuwa Wabunge wa kwanza kupitisha bajeti kubwa ya namna hii, hongereni sana kwa kupitisha bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na bajeti; kwa takribani miaka minne iliyopita bajeti ambayo tumeipitisha katika Bunge hili ukiangalia na ukilinganisha na bajeti ya leo ni kubwa, hii bajeti inakwenda kuisha maradufu kuliko za miaka iliyopita. Mwaka 2019/2020 tulipitisha katika Bunge hili hili takribani shilingi trilioni 29.5 na tukapeleka fedha za maendeleo shilingi trilioni 9.3, mwaka uliofuata mwaka 2020/2021 tukapitisha bajeti katika Bunge hili hili shilingi trilioni 34.8 na tukapeleka kwenye fedha za maendeleo shilingi trilioni 13.3, mwaka 2021/2022 tukapeleka bajeti shilingi trilioni 36.84 na tukapeleka kwenye miradi ya maendeleo shilingi trilioni 13.87. mwaka jana kwa maana mpango unaomalizika tulipitisha trilioni kama mnavyofahamu shilingi trilioni 41.48 na zilizokwenda kwenye miradi ya maendeleo ni shilingi trilioni 15.00.

Mheshimiwa Spika, mwaka huu bajeti hii ikipita ni shilingi trilioni kubwa zaidi ya shilingi trilioni 2.8 zaidi ya bajeti iliyopita ambayo ni takribani asilimia 7.0 ya bajeti zilizopita. Tujipongeze sana Wabunge, tumpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumze sasa kwenye miradi ya kimkakati, tumeona kwenye bajeti nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mwigulu Madelu Nchemba hongera sana kwa kazi kubwa. Wewe na timu yako Mheshimiwa Naibu Waziri na watendaji wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Mwigulu kwa sababu alivyoisoma bajeti ya juzi imetatua na inakwenda kujibu kero za Watanzania wanyonge. Hongera sana kaka yangu Mwigulu Mungu akutangulie, tuna matumaini makubwa bajeti ikitekelezeka maana yake utafanya kazi ya kukumbukwa kwa dunia nzima, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze sasa kwa miradi michache ya kipaumbele. Tumeona Mradi wa SGR, tumeanza kuutekeleza takribani miaka minne iliyopita, lakini kasi tunayokwenda nayo hatuna budi kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa fedha kudhihirisha kwamba utekelezaji wa mradi huo utakamilika kama ulivyotarajiwa na tunaona miradi mikubwa kama ambavyo ameweka dhamira yake wazi kwamba kazi inaendelea tunamhakikishia sisi Waheshimiwa Wabunge na mimi ninasema kwa niaba yangu na wananzengo ambao wanatusikiliza, Mheshimiwa Rais kazi anayoifanya ni ya uzalendo sana. (Makofi)

Ndugu zandu Waheshimiwa Wabunge hii treni ya SGR, ya mwendo kasi ikitekelezwa kama ambavyo tumepanga nimeona kwenye bajeti ilivyosomwa katika nchi za Afrika Mashariki itakuwa ndio treni ya kwanza kutembea kuliko nchi nyingine ambazo zinatuzunguka. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni treni ambayo tumeona bajeti yake ni kubwa, lakini utekelezaji wake unakwenda vizuri. Nimesikiliza vizuri sana bajeti ya Mheshimiwa Mwigulu na Waziri wa Ujenzi kwamba tumeshakamilisha kipande cha kilometa 300 kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro na tunakwenda kukamilisha umbali wa kilometa 822 kutoka Morogoro kwenda Makutopora na kutoka Makutopora kwenda mpaka Tabora takribani kilometa 371 zinakwenda kutekelezweka na itakamilika si muda mrefu, lakini kutoka Isaka kwenda Mwanza kilometa 341 inakwenda kukamilika na kutoka Isaka kwenda Tabora 342 zinakwenda kukamilika, kutoka Tabora mpaka Kigoma kilometa 506 zinakwenda kukamilika. (Makofi)

Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, mnafahamu wenzetu majirani wetu wanajiandaa pia kujenga SGR, lakini nataka niwape taarifa kwamba Rwanda hawajaanza kutumia, Burundi hawajaanza kutumia, Kenya hawajaanza kuitumia, sisi chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan tunakwenda kuwa watu wa kwenza kutumia treni ya mwendokasi ya SGR ni jambo la kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. Lakini hiyo haitoshi na nikapenda niwaambie Watanzania treni hii nadhani tumeshapata taarifa kwamba ina uwezo wa kukimbia umbali wa kilometa 160 kwa saa. Sasa hesabu kutoka Dar es Salaam mpaka Mwanza ambapo ni kilometa 1,112 itakwenda masaa mangapi? Kwa hiyo, ni masaa machache sana. (Makofi)

Kwa hiyo, Watanzania tujiandae kuitumia ili iweze kulrta tija kwenye shughuli zetu za uchumi. Lakini nitoe rai tu kwa wasimamizi kwamba isimamie kwa haraka, ikamilike haraka ili Watanzania waanze kuitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, SGR napenda nizungumze eneo hili kwa upana kidogo, itakuwa inatumia umeme na ni mara ya kwanza sisi hapa Bara la Afrika ukiondoa Ethiopia ambao walianza kuitumia kwa umbali wa kilometa 752. Ukiondoa Ethiopia, Morocco, Afrika ya Kusini na Nigeria nchi inayofuata kwa nchi za Afrika ni Tanzania. (Makofi)

Kwa hiyo, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amedhihirisha kwa nchi za Afrika Mashariki kuwa Rais wa kwanza kuanza kulitembeza na kulikimbiza li-SGR tukiwa sisi Watanzania. Hongera sana Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nizungumze mabehewa yatakayoanza kufanya kazi kwa nilivyosoma katika Taarifa za Serikali. Kutakuwa na mabehewa takribani 400 ya abiria lakini mabehewa 59 yataanza kuingia na mabehewa 14 yameshaanza kuingia. Mheshimiwa Waziri wa ujenzi na wewe hongera sana Kaka Mbarawa kwa kusimamia kwa ubora kabisa kazi hiyo. Lakini hiyo ni kazi ya Mheshimiwa Rais ameifanya na sisi watendaji tumuunge mkono kwa kuharakisha utekelezaji huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mabehewa haya yatakuwa na uwezo wa kutunza umeme kwa masaa manne bila kukatika hata kama umeme utakatika sehemu zingine. Kwa hiyo, ni jambo la kheri ni uhakika kwamba yatafanya kazi lakini mabehewa ya mizigo yatakuwa takribani 1,430. Sasa elewa ni mizigo mingapi ya Watanzania itabebwa katika mabehewa yale kwa muda mfupi. Kwa hiyo, ni kazi nzuri naomba tumuunge mkono Mheshimiwa Rais na Serikali tukamilishe mradi huu na mradi huu ndugu zangu Wakenya wanatengemea kuanza kuujenga mwakani na Burundi na Uganda na sehemu nyingine mwaka 2025. Kwa hiyo, miaka mitatu hii tutakuwa tunaongoza katika ulingo wa kuhudumia hapa Afrika Mashariki, Tanzania tukiongoza kukimbiza na kutembeza li-treni la mwendo kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niende kwa Bwawa la Mwalimu Nyerere; naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais nimeona fedha zilizotolewa kwenda kukamilisha mradi ule kwa mwaka jana takribani shilingi bilioni 869 ambazo tuna matarajio kwa muda uliopangwa mradi huu unakwenda kukamilika. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa dhamira hiyo ya kutoa fedha na wewe Mheshimiwa Mwigulu Nchemba usingekuwa unatoa fedha mradi usingefika kiwango hicho, hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Nishati Kaka yangu January Makamba kwa kusimamia vizuri pamoja na timu yake pamoja na TANESCO wanafanya kazi nzuri ni matumaini yetu kwamba mradi ule unakwenda kufufua uchumi kwa kiwango cha juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania mnaonisikiliza, Mradi huu wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ni mradi mkubwa sana. Kama tulivyo kwenye SGR kwa nchi za Afrika Mashariki ndio bwawa kubwa peke yake hakuna bawawa lingine linalozalisha umeme wa namna hii na kwa nchi za SADC ni bwawa la tatu kwa ukubwa ikiongozwa na Bwawa la Mambilla lililoko Nigeria na Caculo Cabaça la Angola na linafuata la Tanzania. Kwa Afrika nzima ni bwawa la nne ukiondoa la Ethiopia ambalo ni Renaissance, la megawati 6,450 na duniani kote ni bwawa la 60. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tuelewane, sasa elewa dunia kuna nchi ngapi? Kwa hiyo, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa Afrika anaongoza kwa kuwa na bwawa kubwa kwa nchi za Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Rais hongera sana kwa kazi hiyo tunakwenda kufufua uchumi tunakwenda kumaliza changamoto za kinishati tukikamilisha bwawa hili pamoja na miradi mingine itakapo kamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee niwapongeze Serikali na Mheshimiwa Rais na Waheshimiwa Wabunge, na ninyi Waheshimiwa Wabunge mnakwenda kuingia kwenye rekodi ya Bunge Hansard zitaandika kwamba militekeleza miradi hii mikubwa kwa niaba ya Watanzania. Mjipongeze sana kwa kazi nzuri tunayoifanya. Bwawa la Mwalimu Nyerere likikamilika litatuongezea umeme, kwa sasa nimeona kwenye taarifa kwamba tuna takribani megawati 1,872 kwa uwezo wa juu, ingawaje mahitaji yetu nilivyoona kwenye taarifa ni megawati 1,432.05 lakini tukikamilisha tutakuwa na takribani megawati 4,193 ukijumlisha na miradi mingine. Maana yake nini? Mwaka 2025/2026 miaka inayokuja michache mahitaji yetu ya umeme yaweza kufikia megawati 2070 kwa sasa mahitaji yetu ni megawati 1,432.05. Kwa hiyo, tutaweza kujitosheleza kuwa na umeme nchini, lakini na kuwasambazia majirani zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na Waheshimiwa Wabunge leo hii Kenya ana jumla ya megawati 2,722 anahitaji umeme takribani megawati 500; kwa hiyo, tunaweza kumuuzia. Rwanda ana megawati 230, Burundi ana megawati 86, Zambia ana megawati 1,472; sisi tunakwenda kuwa na megawati 4,198 mnasubiri nini kupiga makofi kwa Mheshimiwa Rais wetu, ni kazi kubwa ameifanya. Lakini ni ninye Waheshimiwa Wabunge na Serikali na wananzengo... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, sekunde 30 malizia sentensi yako.

MHE. DKT. MEDARD M. KALEMANI: Mheshimiwa Spika, naomba niongezee dakika mbili. Mradi huu unakwenda kujibu kero za Watanzania, mahala ambapo kuna changamoto za umeme. Tumeelewa bado kuna vitongoji takribani 36,101 lakini mradi unakwenda kukamilisha vitongoji vya Wabunge takribani vyote, hata kwako pale Igomba, Itonya na Itua ambako kuna kero wanakwenda kupelekewa umeme. (Makofi)

Kwa hiyo, ni matumaini yetu kwamba Watanzania wengi watapata umeme, hata Gezaulole kwa Mheshimiwa kule Kigamboni watapata umeme, mpaka kule Itonya na maeneo mengine ambayo nimesema mpaka Katubuka watapata umeme. Kwa hiyo, ni matumaini hata kule Chato kwenye Majangala watapata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu ni mkubwa sana ni mategemeo yetu kwamba utakwenda kujibu kero za Watanzania.

Naomba niombe kidogo kwa sababu hela hizi ni nyingi zinakwenda kwa wananchi takribani kujibu kero za Watanzania wanyonge na wakulima wanyonge. Ninajua mradi huu utakwenda kwa Watanzania milioni 61; utakwenda kwa ng’ombe tulionazo milioni 6.6; kwa mbuzi milioni 21.6; kwa kondoo milioni 92.7; pamoja na nguruwe milioni 3.7; na mifugo mingine, lakini tutatatua kero za wakulima wetu kwa ajili ya kuwapelekea kilimo cha umwagiliaji. Naona Mheshimiwa Bashe umefanya kazi kubwa sana, peleka miradi ya umwagiliaji kule Chato, maeneo ya Makurugusi, Ilyamchele, Nganza, Rubambangwe, Nyambogo, Katende, Mongela pamoja na maeneo mengine ambayo hayajapata mradi wa umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, Mheshimiwa Mbarawa tumepitishia bajeti kubwa sana; kuna barabara ya kero kubwa ya muda mrefu kule Jimbo langu la Chato na wanachato wananisikia, kutoka Nyamirembe - Gatini mpaka Katoke yenye umbali wa kilometa 51.0 inayojengwa kwa kiwango cha lami. Naomba uanze kutekeleza miradi hiyo kwa sababu Mheshimiwa Rais ametoa shilingi bilioni 2.3 na tayari umezipokea. Tangaza tender, peleka ma-bulldozer wananchi wa Ichwankima wanaopitiwa na barabara hiyo, wananchi wa Busarara, wananchi wa Nyambiti, wananchi wa Kalwelezo, wananchi wa Kazunguti, wananchi wa Kasenka mpaka Katoke mradi uweze kukamilika kwa kiwano cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa naomba kipekee, tumpongeze sana Mheshimiwa Rais, tumtakie kila la kheri sisi pamoja na Watanzania wote Kwenda kutekeleza mradi huu muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi, nashukuru sana. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, ahsanteni sana.

MHE. DKT. MEDARD M. KALEMANI: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nichukue nafasi fupi sana kuchangia katika Wizara hii, lakini awali ya yote niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na timu yake ya wataalam. Nawapongeza kwa kazi kubwa waliyofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo nitachangia kwa kiasi kikubwa sana ni matumizi mbadala ya mkaa pamoja na kuni. Kama ambavyo wameeleza wenzetu katika taarifa hii, mkakati waliouweka ni pamoja na kuonyesha kwamba matumizi ya mkaa pamoja na kuni yanapungua kwa kiwango kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo mkakati mkubwa na wenye dhamana kubwa ya kuhakikisha kwamba mkakati wa kuni na mkaa unaisha na kwamba sasa tunatumia nishati mbadala ni Wizara yetu ya Nishati na Madini, kwa hiyo nitajielekeza kwenye hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni tuna mpango wa kimataifa wa matumizi endelevu unaotaka kuhakikisha kuwa matumizi ya mkaa pamoja na kuni yatakomea ifikapo mwaka 2030.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo, kwanza kabisa nitumie nafasi hii kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa ujumla kwamba matumizi ya mkaa katika nchi zinazoendelea hadi sasa yanafikia asilimia 90 ya nishati ya umeme duniani. Hiyo ni takwimu ya Benki ya Dunia. Lakini pamoja na hayo bado kwa nchi zetu zinazoendelea hasa zilizoko chini ya Kusini mwa Afrika, pamoja na maendeleo ya nchi za Afrika tani milioni 2.3 kwa nishati tunayotumia inatokana na kuni pamoja na mkaa. Kwa hiyo, ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama Serikali, mpango madhubuti uliopo ni kwamba, moja, sisi ni wanachama wa kimataifa wa matumizi mbadala ya nishati ya kuni pamoja na mkaa. Mkakati madhubuti ambao Serikali tumechukua, napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, ni kwamba sasa Shirika letu la TPDC kuanzia mwaka 2013/2014 lilianza rasmi kujenga miundombinu ya matumizi ya gesi kuanzia mijini mpaka vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa hatua ya kwanza, tumeanza na Dar es Salaam. Mwaka 2014/2015 tumeshaunganisha wateja 70 ambao tumewaunganishia miundombinu ya gesi katika maeneo ya Mikocheni. Kwa hiyo, ni hatua kubwa, lakini hatua ya pili tumepeleka matumizi hayo hayo ya gesi kwenye magari yetu. Hadi sasa tunapozungumza magari takriban 60 yanatumia gesi, hiyo ni hatua ya kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hatua ya pili ni kupeleka miundombinu ya matumizi ya gesi, na hii gesi ninayoizungumzia ni ya aina hii ya mathane, si ile gesi ambayo tumeizoea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kuna taarifa yetu itakuja hapo baadaye tutaeleza kwa upana zaidi; lakini kwa ufupi tu niseme kwamba kuanzia mwaka 2017/2018 tutaunganisha matumizi ya gesi katika Mikoa ya Mtwara na Lindi pamoja maeneo yote ya Dar es Salaam yakiwemo maeneo ya Mbagala, Kurasini, Buguruni na maeneo mengine ya jiji ya Dar es Salaam. Tunatarajia wananchi 30,000 tunawaunganishia gesi ili matumizi makubwa ya mkaa na kuni yapungue. Asilimia 70 ya mkaa unaotumika hapa nchini unaingia Dar es Salaam, kwa hiyo tukishaunganisha gesi kwa wananchi wa Dar es Salaam tutapunguza kwa kiasi kikubwa uharibifu wa mazingira, hiyo ni hatua ya kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili, kwa sababu muda ni mfupi sana, inahusu usambazaji wa umeme mijini na vijijini. Kama ambavyo mnajua tunapeleka umeme katika mikoa yote katika miji yote na vitongoji vyetu. Tuna mpango wa kendeleza umeme mijini, na mpango huu unaanza mwaka 2017/2018 kwa maeneo ya mjini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. MEDARD M. KALEMANI: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukrani nyingi sana kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi anavyotafuta fedha, kutoa fedha na kuleta maendeleo kwa Watanzania, hongera sana.

Mheshimiwa Spika, tunaona jinsi pesa nyingi za ujenzi wa miradi ya miundombinu ikiwamo barabara, bandari na madaraja zinavyoendelea kumiminika katika maeneo ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, miradi ya barabara zilizokamilika na zinazoendelea kujengwa, zilizoorodheshwa katika taarifa ya Wizara ni kielelezo cha kazi kubwa inayoendelea kufanyika kutokana na juhudi za Mheshimiwa Rais. Nashukuru katika Jimbo la Chato pia pesa nyingi zaidi ya shillingi bilioni 5.7 katika kipindi cha miaka miwili iliyopita zimetolewa. Hii ni hatua ya kupongezwa sana. Naishukuru Serikali kwa niaba ya Wana-Chato kwa kutoa shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya kuanza kujenga barabara kutoka Bandari ya Nyamilembe kuelekea Katoke umbali wa km 50.01, bararara ya SIDO - Ginnery ya Chato na Ginnery hadi Sekondari ya Janet Magufuli. Ombi langu ni kuiomba Wizara kupitia TANROADS kukamilisha haraka taratibu za manunuzi ili ujenzi wa barabara hizi uanze haraka.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wananchi katika eneo hilo hasa katika sehemu ya upanuzi wa eneo la Gati la Nyamilembe wapo wananchi wanadai fidia, naiomba Serikali yetu ikamilishe fidia hiyo ili kundoa kero hiyo kwa wananchi hao.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Jimbo la Chato wamenituma nitoe shukrani kwa Serikali hasa kwa Mheshimiwa Rais kwa kukamilisha ujenzi wa Gati la Bandari ya Nyamilembe, tunaomba bandari hii izinduliwe ikiwezekana na viongozi wa kitaifa ili wananchi wafikishe shukrani na furaha hizo moja kwa moja kwa Serikali yao. Nampongeza Mheshimiwa Waziri na timu nzima ya Wizara na taasisi zake.

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na.3 wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja kama ilivyowasilishwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Napenda kwa hatua ya awali kabisa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan katika kuamua kutekeleza mradi huu tena kwa kasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtakumbuka mradi umeanza takribani miaka mitatu iliyopita, lakini toka ameingia madarakani Mheshimiwa Rais, kazi kubwa pamoja na mambo mengine anayofanya ni kuusukuma na kuuwezesha utekelezaji wa mradi huu kwa kasi kubwa. Kwa hiyo, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo hoja zimeulizwa na Waheshimiwa Wabunge nami napenda nichangie, nitoe ufafanuzi walau kidogo kwa sababu ya muda. Katika kutekeleza mradi huu, jambo la kwanza ambalo litarahisisha sana usimamizi wa mradi huu ni kupitisha Muswada huu wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambao kimsingi ukishapitishwa unarahisisha sana usimamizi wa mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, usimamizi mahususi kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamechangia, mradi huu kimsingi ni wa kimkakati na usimamizi wake ni lazima uwe wa kimkakati, kwa hiyo, hatua ya kwanza ambayo tumeifanya kwa upande wa Serikali, kwanza sisi Serikali kushiriki.

Mheshimiwa Nainu Spika, nirudie kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa sisi Serikali kuwa wadau na wabia wa mradi huu kwa asilimia 15, jambo ambalo linatupa fursa ya kusimamia kwa ukaribu kama sehemu ya utekelezaji wa mradi na pia tukiwa ndani ya Kampuni ya Usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wameuliza Waheshimiwa Wabunge, tumejipanga vipi katika usimamizi? Jambo la kwanza, tumeunda timu mahsusi; na napenda nitoe taarifa mbele ya Bunge lako Tukufu na Waheshimiwa Wabunge kwamba tayari tumeshateua waratibu wa mradi huu ambao ni Watanzania, tena vijana wataalam waliobobea kwenye masuala ya mafuta hapa nchini. Kwa hiyo, tumejipanga vizuri katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee, tunahusisha kila taasisi ya Serikali na sekta ambazo ni muhimu katika kusimamia ambazo zina utaalam uliobobea na wa hali ya juu wa ndani na wa Kimataifa kwa ajili ya kuratibu usimamizi wa mradi huu. Kwa hiyo, tuna timu mahususi ambayo imeundwa na imeshaanza kazi chini ya waratibu ambao tuliwatua miezi miwili iliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sehemu ya Pili ya Usimamizi, tumeunda chombo kinaitwa Government Facilitation Team. Badala ya kusubiri vibali mahali ambapo watahitaji vibali vya wataalam wakati wa utekelezaji wa mradi, tumeweka mamlaka kwa wenye mamlaka vibali kuteua wataalam waandamizi ili kusaidia katika uratibu wa mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mathalani, labda kibali kinahitajika kutoa exemption TRA, tumemtaka na kumwomba Kamishna wa TRA kuteua afisa kama Desk Officer ili jambo likifika lisilale wala kuchelewa. Tumefanya hivyo kwenye sekta zote za Serikali. Hii inasaidia sana kurahisisha usimamizi na utekelezaji wa mradi huu ili tuendane na wakati wa kuukamilisha kwa ajili ya manufaa ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili kimuundo, nitumie nafasi hii pia kuwaomba, kwa umuhimu wa maradi huu; na huu mradi unapita karibu sehemu kubwa sana ya nchi yetu; asilimia 80 ya mradi huu upo kwetu. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge, Viongozi na wananchi kwa ujumla, mahali ambapo bomba litapita, sisi tuwe watu wa kwanza kulinda bomba; na ni sehemu ya usimamizi. Kwa hiyo, nawaomba sana katika eneo hilo, pia sisi kwa ujumla wetu tusaidiane kuusimamia mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mnavyofahamu mradi utapita katika maeneo mengi. Kwa ujumla wake usimamizi wa mradi huu kama nilivyosema, kwa sababu unapita eneo kubwa, utawahusisha sana wananchi. Tumetaka sehemu ya kwanza hasa kwenye ulinzi wa bomba lazima zitumike kampuni za ndani ya nchi yetu kwa ajli ya kulinda usalama wa bomba lenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa wasimamizi, tumepitisha pia utaratibu ambao utapita karibu kila kata ambako mradi unapita. Viongozi wa Kata, viongozi wa Tarafa, Wakuu wa Wilaya na wengine watakuwa ni wasimamizi wa kwanza kuhakikisha vijana wenye uwezo wa kufanya kazi hizo maeneo yale, vijana wa maeneo hayo ndio wanapata ajira kwa fursa ya kwanza. Tumejipanga vizuri kwa upande huo na ninampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kutoa maelekezo ya awali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la local content, napenda nitoe taarifa kidogo, tumefanya maboresho. Siku ya nyuma tulikuwa tunawaruhusu Wakandarasi kutoa tender au matangazo ya kazi za ndani. Kwa hatua ya kwanza mwaka huu tumefanya marekebisho na Mheshimiwa Rais ametuelekeza vizuri sana, kwanza tumeanzisha kanzidata ambayo inasajili makampuni ya ndani ambayo yatafanya kazi zote za supply, ujenzi, kutoa huduma, kwa hiyo, yamesajiliwa EWURA.

Kwa hiyo, kila kampuni ya ndani ambayo itatakiwa kufanya kazi hii badala ya kutoa tangazo, Kampuni ya SINO HYDRO kwa mfano, ambayo ni ya China labda ndio Mkandarasi wa Kimataifa; akitoa tangazo kwa mfumo wa zamani, watu walikuwa wanaomba na wakajionesha kwao ni akina Masanja, akina Lugekingila, lakini ukiingia ndani, ni Wachina wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulichofanya ni kusajili kampuni za ndani. Kwa hiyo, kampuni ikitaka kuajiri kampuni ya ndani tunaiambia lete fursa, tunamkabidhi makampuni ya ndani ambayo yamesajiliwa hapa, anachagua. Kama ni Makampuni mawili, anayachagua kati ya makampuni kumi yote ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni hatua nzuri sana ambayo itasaidia sana kujihakikishia kwamba makampuni yanayofanya kazi za kutoa huduma za kujenga, zote ni za ndani. Kwa hiyo, kuna kila namna ya kuipongeza Serikali yetu kwa hatua hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitoe wito pia kwa wananchi na Waheshimiwa Wabunge, tutakaporudi katika maeneo yetu, tuwaambie wakandarasi wenye uwezo wale wa ndani waendelee kwenda kujisajili EWURA ili waweze kupata fursa ya kufanya kazi hizi wakati wa utekelezaji wa mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili tulilofanya ni kutoa fursa. Nampongeza sana Mheshimiwa Kamani, Mheshimiwa Mbunge kijana kwa niaba ya vijana; na tunasisitiza kweli asilimia kubwa ya kazi hizi zifanywe na vijana. Hatuna maana kwamba wengine wasifanye, lakini wanayo fursa kubwa sana. Mathalani tumetoa maeneo mengi na sasa tunaanza kutoa semina.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa taarifa, tarehe 3 tutakuwa na Semina ya Tanzania Private Sector Foundation. Ile taasisi private tunakaa nayo itupe mkakati na yenyewe wa namna ya kuchukua fursa hii. Tunafanya mkutano wa kwanza mkubwa ambao utakuwa eneo la Chongoleani kule Tanga tarehe 3 mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaomba sana vijana, kupitia Tanzania Private Sector Foundation na taasisi za vijana, mtumie vehicle hizo ili tuone, tuwasajili kwa nafasi mnazoweza kuzifanya, mzifanye wenyewe badala ya kuwapa vijana kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, yapo makampuni ya kigeni ambayo yanaweza kufanya kazi hizi ambazo ni za kitaalam zaidi. Kwa mujibu ya Sheria yetu ya Mafuta, imetoa utaratibu kwamba kampuni za ndani zote ambazo zitafanya kazi katika mradi huu, zitatakiwa kuwashirikisha Watanzania ndani ya makampuni hayo au Makampuni ya Kitanzania ambayo ushiriki wao usipingue asilimia 25 katika makampuni hayo. Huu ni udhibiti ambao utasaidia sana kuratibu Watanzania kupata fursa ya kujenga miradi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, naomba niongelee kidogo kuhusu manufaa ya mradi huu. Manufaa ya mradi huu ni makubwa sana. Tumeeleza na kila mtu anafahamu kwamba ni takribani kilometa 1,145 zipo Tanzania na tunayo makambi 14 yatakayojengwa kwenye bomba hili. Pia kwenye makambi 14 hayo, makambi takribani 11 yapo Tanzania. Vilevile tutakuwa na vituo; kwa sababu bomba hili ni la kupasha joto, kutakuwa na vituo vya kupasha joto bomba 29 na vituo 22 vyote vipo Tanzania. Pia kuna mahali tu pa kufungulia valve ambavyo vipo vituo 76 vya kufungua valve. Vituo 53 vipo Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna vituo sita vingine vya kusukuma na kupunguza mgandamizo na speed ya mafuta, vinne vipo Tanzania. Kutajengwa matenki takribani matano makubwa kule Chongoleani. Nafasi hizi zote ni fursa kwa Watanzania.

Mheshimwia Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kuwaomba sana Watanzania wachangamkie fursa. Ni zaidi ya asilimia 80 ya ajira zinatoka Tanzania. Tunatarajia vijana wetu na wafanyakazi wapatao 15,000 wakati wa ujenzi wa mradi huu wataajiriwa.

Kwa hiyo, nitoe wito kwa Watanzania wenye uwezo kwenda kuchangamkia fursa hizi; iwe mama ntilie, kampuni za ulinzi, iwe kampuni za ku-supply, vyote vitafanywa na Watanzania. Ila msisitizo mkubwa tunauweka zaidi kwamba vifaa vyote vya ujenzi wa bomba, iwe cement, iwe nondo au misumari, ni lazima vitokane na viwanda vyetu vya ndani. Huo ndiyo msisitizo tunaousisitiza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naunga mkono sana hoja hii, tena ikipita leo, haraka sana kwa sababu utekelezaji wa mradi umeshaanza ili iturahisishie kwenda kutekeleza mradi huu kwa kasi zaidi. Nimalizie kwa kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, toka tulipoanza, hata Bunge lililopita kupitisha masuala yote yanayohusu utekelezaji wa bomba hili ili bomba hili likatekelezwe haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimwia Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
NAIBU WAZIRI WA NIASHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Nianze na mimi kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi kubwa waliyofanya, pamoja na Katibu Mkuu. Hata hivyo, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa namna anavyosimamia rasilimali za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mambo ambayo yamezungumzwa kwa wingi sana katika bajeti hii na yanahusu sana kwa kiasi kikubwa Wizara ya Nishati na Madini. Hata hivyo nitajielekeza sana kwenye hoja za nishati kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, suala la LNG, suala la kiwanda cha kusindika gesi; Waheshimiwa Wabunge wameuliza kama mradi upo ama haupo.

Mheshimiwa Spika, nataka nilieleze Bunge lako Tukufu kwamba mradi wa LNG wa Lindi bado upo na wala hautahamishwa, hauendi Msumbiji wala sehemu yoyote. Na hapo tulipofika sasa tuko katika utekelezaji na tarehe 24 mwezi huu watalaam wanaondoka kwenda Trinidad & Tobago kwa ajili ya kukamilisha mazungumzo na wajenzi; na wajenzi watakaojenga ni makampuni makubwa ya ExxonMobil, BG Shell, pamoja na TPDC. Kwa hiyo, mradi huo upo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo suala la ujnzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda hadi Tanga.

Mheshimiwa Spika, nilitaka tu kutoa taarifa kwa sababu ni suala la maendeleo, tunajenga viwanda. Utaratibu wa ujenzi wa bomba hili umeshaanza na sasa nitoe taarifa sahihi kwamba bomba hili litafika katika mikoa minane ya nchi yetu na wilaya 24 na urefu wa kilometa 1,445 kwa kiasi kikubwa katika Tanzania. Hatua inayofuata katikati ya mwezi unaokuja tutasaini, lakini pia tutafanya uzinduzi na ujenzi wa jiwe la msingi huko Tanga katika eneo linaloitwa Chongoleani, Mjini Tanga. Kwa hiyo, ujenzi unaanza na utekelezaji utakamilika mwaka 2025. Kwa hiyo, Ujenzi wa Mradi wa Bomba la Mafuta unaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, mradi wa Makambako Songea; huu ni mradi muhimu sana. Wananchi walio wengi wa maeneo ya Mikoa ya Njombe, Songea na Wilaya zake wanautarajia sana mradi huu, uko katika hatua nzuri. Hata hivyo niseme tu commitment ya Serikali, kwa mwaka huu wa fedha tumetenga bilioni kumi na moja kwa ajili ya kwenye mradi huu, na ujenzi umeshaanza kufika katika hatua nzuri na mwezi Oktoba mwakani utakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niwaambie tu shughuli kubwa zinazofanyika katika mradi huu, ya kwanza kabisa ni ujenzi wa vituo vya kupoza umeme vilivyoko Madaba, Njombe pamoja na Songea Mjini na utakamilika hivi karibuni. Mradi mzima utagharimu Swedish Krona milioni 620, Dola za Marekani milioni 20 na shilingi bilioni 17 za Tanzania. Kwa hiyo, utekelezaji ukwenda vizuri mwezi Agosti mwakani utakamilika.

Mheshimiwa Spika, katika mradi huu kazi zitakazofanyika ni pamoja na kujenga transmission line ya urefu wa kilometa 250 kutoka Njombe hadi Songea, transmission ya kusambaza umeme katika vijiji 120 katika Wilaya nilizozitaja na kuwaunganishia umeme wateja 22,700. Kwa hiyo ni mradi mkubwa na unakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kusambaza Umeme Mijini, maana wako Wabunge wamehoji kwamba tunapeleka umeme vijijini tu lakini mjini hatuendi. Niseme tu kwamba tumepata Dola za Kimarekani milioni 424 kwa ajili ya ujenzi na miundombinu ya mijini ili kuhakikisha kwamba
mijini tunakuwa na umeme wa kutosha ili viwanda vinavyojengwa mijini sasa viwe endelevu na kazi hii inafanyika vizuri. Kazi zitakazofanyika, ili nitumie nafasi hii vizuri, sana sana ni ufungaji wa transfoma kubwa na ndogo zinazoanzia KVA 50, KVA 100, KVA 200 hadi KVA 315. Hii ni katika kuhakikisha kwamba umeme mijini pia unaimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, REA Awamu ya Tatu; ninatambua kwamba muda ni mfupi sana, lakini niwape taarifa Waheshimiwa Wabunge kwamba tarehe 24 Juni (kesho kutwa tu) tunaanza sasa uzinduzi rasmi wa mradi mkubwa wa REA Awamu ya Tatu katika mikoa yote Tanzania Bara. Tunaanza na Mkoa wa Manyara tarehe 24, tarehe 4 hadi 5 tunakwenda Katavi na Rukwa, tukitoka Katavi na Rukwa tunaenda Mtwara na Lindi halafu tunaenda Kigoma. Kwa hiyo, wananchi wa Kagera Nkanda, Kazumulo pamoja na kule Kagera tutaendelea kuzindua hadi mikoa yote ikamilike kwa muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muda ni mfupi, lakini niendelee kuzungumza kidogo suala la usambazaji wa gesi majumbani.

Mheshimiwa Spika,…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzunguzaji)

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunisikiliza.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
NAIBU WAZIRI WA NIASHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Nianze na mimi kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi kubwa waliyofanya, pamoja na Katibu Mkuu. Hata hivyo, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa namna anavyosimamia rasilimali za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mambo ambayo yamezungumzwa kwa wingi sana katika bajeti hii na yanahusu sana kwa kiasi kikubwa Wizara ya Nishati na Madini. Hata hivyo nitajielekeza sana kwenye hoja za nishati kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, suala la LNG, suala la kiwanda cha kusindika gesi; Waheshimiwa Wabunge wameuliza kama mradi upo ama haupo.

Mheshimiwa Spika, nataka nilieleze Bunge lako Tukufu kwamba mradi wa LNG wa Lindi bado upo na wala hautahamishwa, hauendi Msumbiji wala sehemu yoyote. Na hapo tulipofika sasa tuko katika utekelezaji na tarehe 24 mwezi huu watalaam wanaondoka kwenda Trinidad & Tobago kwa ajili ya kukamilisha mazungumzo na wajenzi; na wajenzi watakaojenga ni makampuni makubwa ya ExxonMobil, BG Shell, pamoja na TPDC. Kwa hiyo, mradi huo upo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo suala la ujnzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda hadi Tanga.

Mheshimiwa Spika, nilitaka tu kutoa taarifa kwa sababu ni suala la maendeleo, tunajenga viwanda. Utaratibu wa ujenzi wa bomba hili umeshaanza na sasa nitoe taarifa sahihi kwamba bomba hili litafika katika mikoa minane ya nchi yetu na wilaya 24 na urefu wa kilometa 1,445 kwa kiasi kikubwa katika Tanzania. Hatua inayofuata katikati ya mwezi unaokuja tutasaini, lakini pia tutafanya uzinduzi na ujenzi wa jiwe la msingi huko Tanga katika eneo linaloitwa Chongoleani, Mjini Tanga. Kwa hiyo, ujenzi unaanza na utekelezaji utakamilika mwaka 2025. Kwa hiyo, Ujenzi wa Mradi wa Bomba la Mafuta unaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, mradi wa Makambako Songea; huu ni mradi muhimu sana. Wananchi walio wengi wa maeneo ya Mikoa ya Njombe, Songea na Wilaya zake wanautarajia sana mradi huu, uko katika hatua nzuri. Hata hivyo niseme tu commitment ya Serikali, kwa mwaka huu wa fedha tumetenga bilioni kumi na moja kwa ajili ya kwenye mradi huu, na ujenzi umeshaanza kufika katika hatua nzuri na mwezi Oktoba mwakani utakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niwaambie tu shughuli kubwa zinazofanyika katika mradi huu, ya kwanza kabisa ni ujenzi wa vituo vya kupoza umeme vilivyoko Madaba, Njombe pamoja na Songea Mjini na utakamilika hivi karibuni. Mradi mzima utagharimu Swedish Krona milioni 620, Dola za Marekani milioni 20 na shilingi bilioni 17 za Tanzania. Kwa hiyo, utekelezaji ukwenda vizuri mwezi Agosti mwakani utakamilika.

Mheshimiwa Spika, katika mradi huu kazi zitakazofanyika ni pamoja na kujenga transmission line ya urefu wa kilometa 250 kutoka Njombe hadi Songea, transmission ya kusambaza umeme katika vijiji 120 katika Wilaya nilizozitaja na kuwaunganishia umeme wateja 22,700. Kwa hiyo ni mradi mkubwa na unakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kusambaza Umeme Mijini, maana wako Wabunge wamehoji kwamba tunapeleka umeme vijijini tu lakini mjini hatuendi. Niseme tu kwamba tumepata Dola za Kimarekani milioni 424 kwa ajili ya ujenzi na miundombinu ya mijini ili kuhakikisha kwamba
mijini tunakuwa na umeme wa kutosha ili viwanda vinavyojengwa mijini sasa viwe endelevu na kazi hii inafanyika vizuri. Kazi zitakazofanyika, ili nitumie nafasi hii vizuri, sana sana ni ufungaji wa transfoma kubwa na ndogo zinazoanzia KVA 50, KVA 100, KVA 200 hadi KVA 315. Hii ni katika kuhakikisha kwamba umeme mijini pia unaimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, REA Awamu ya Tatu; ninatambua kwamba muda ni mfupi sana, lakini niwape taarifa Waheshimiwa Wabunge kwamba tarehe 24 Juni (kesho kutwa tu) tunaanza sasa uzinduzi rasmi wa mradi mkubwa wa REA Awamu ya Tatu katika mikoa yote Tanzania Bara. Tunaanza na Mkoa wa Manyara tarehe 24, tarehe 4 hadi 5 tunakwenda Katavi na Rukwa, tukitoka Katavi na Rukwa tunaenda Mtwara na Lindi halafu tunaenda Kigoma. Kwa hiyo, wananchi wa Kagera Nkanda, Kazumulo pamoja na kule Kagera tutaendelea kuzindua hadi mikoa yote ikamilike kwa muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muda ni mfupi, lakini niendelee kuzungumza kidogo suala la usambazaji wa gesi majumbani.

Mheshimiwa Spika,…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzunguzaji)

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangie katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwa heshima ya pekee ningeomba sana kwa idhini yako Wabunge wote tugonge meza zetu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo imesheheni mambo mengi ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hivyo ndivyo basi, naanza kabisa kuunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja ili hata kama nikisahau niwe nishamemaliza kabisa katika suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo ya msingi ambayo yamezunguzwa sana katika hotuba hii kwa upande wa nishati ni mambo matatu. Pamoja na mambo mengine napenda sana nijielekeze zaidi katika hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la vyazo vya kuzalisha umeme kwa upande wa gesi na suala la maji limetajwa kwa kiasi kikubwa. Napenda kuliondoa wasiwasi Bunge lako Tukufu kwamba vyanzo vya kuzalisha umeme kwa njia ya maji havijatajwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi si kweli, Ilani imetaja vyanzo haijabainisha mradi kwa mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Ilani yetu aya ya 43.A imeeleza vyanzo vya msingi ambavyo Serikali itajielekeza katika kuzalisha umeme wa uhakika, unaotabirika na wa gharama nafuu na vyanzo vya maji vikiwemo. Kwa hiyo, napenda sana niondoe wasiwasi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ukurasa wa 81 umetaja bayana vyanzo halali, vyanzo vitakavyotupunguzia bugudha na tofauti ndogo ndogo na migogoro ya upungufu ya umeme ikiwemo vyanzo vya gesi asilia, maji, geothermal, makaa ya mawe pamoja na upepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka kuwaondoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba tunapotaja vyanzo vya kuzalisha umeme kimsingi hatutaji mradi kwa mradi. Mradi kwa mradi utakuja katika mipango yetu ya maendeleo kisekta ambayo tutakuja kuiwasilisha itakapofika wakati wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nieleze kwa nini nasema hivyo. Kwanza kabisa Serikali haijatelekeza kutumia gesi asilia. Hivi sasa Wabunge wote tunatambua tunayo trilioni 57.5 ya gesi asilia na umeme tunaotumia kwa sasa hivi zaidi ya megawatt 787 zinatokana na gesi asilia. Kwa hiyo, si kweli kwamba tumetelekeza kutumia gesi asilia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais tarehe 3 Aprili, 2018 alizindua mradi mkubwa wa kuzalisha megawatt 198 ambao unakwenda kutupatia megawatt 240 mwishoni mwa Juni, 2018. Kama hiyo haitoshi Desemba, 2018 tutaanza tena kutumia nishati nyingine ya gesi asilia ya megawatt 185 kutoka kwenye mradi mwingine wa Kinyerezi II nao unatokana na gesi asilia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwakani tunaanza kujenga mradi mwingine wa gesi asilia kutoka Somanga Fungu wa megawatt 330, nao unatokana na gesi asilia. Mwaka huo huo Julai tutaanza kujenga mradi mwingine wa megawatt 300 unaotokana na gesi asilia huko Mtwara. Kinyerezi peke yake kuja kufika mwaka 2020 tutakuwa na megawatt 1,560 za gesi asilia.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kusisitiza kwamba matumizi ya gesi asilia bado ni mengi sana. Mbali na kuzalisha umeme, gesi asilia itatumika katika masuala mengine yafuatayo:-

Kwanza, jumla ya trilioni 8.8 itatumika kuzalisha umeme; trilioni 4.3 itatumika kwenye viwanda vya mbolea na petrochemicals; trilioni 1.2 itatumika kusambaza gesi majumbani na kwenye magari yetu na trilioni 1.1 itatumika pia kwa ajili ya viwanda vya vyuma. Kwa hiyo, niendelee kusema bado matumizi ya gesi asilia ni makubwa na Serikali inaendelea kuyazingatia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kusema kwenye mradi wetu wa LNG tutatumia tani milioni 10 kila mwaka za gesi asilia. Kwa hiyo, nipende kusema tu kwamba pamoja na vyanzo hivyo tuna maana kwamba bado tunaendelea kutumia kile kinachoitwa energy mix kwa maana ya kutumia vyanzo vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini sasa tunataka kuendeleza Mradi wa Stiegler’s Gorge? Nitumie nafasi hii kusahihisha kidogo, naomba Waheshimiwa Wabunge mradi huu tuuite Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Rufiji badala ya Stiegler’s Gorge. Stiegler’s Gorge ilikuwa ni jina la Mzungu aliyefika maeneo yale na alishaondoka na hayupo. Kwa hiyo, si vema sana kuendelea kumuenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kusema hapa, Mradi huu wa Maporomoko ya Mto Rufiji utakaoweza kuzalisha megawatt 2,100 ni mkubwa sana. Waheshimiwa Wabunge, tutambue kwamba tumekuwa tukitumia miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia maji tangu enzi za ukoloni na miradi hiyo tunaitambua; tuna Mradi wa Kidatu, Mradi wa Kihansi, Mradi wa Mtera na New Pangani Fall. Miradi hii ina uhai wa zaidi ya miaka 40 na imeshaanza kuchoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitumie nafasi kueleza kwamba ni vema sana tukaanza sasa kutumia miradi mikubwa ambayo itatutoa kwenye changamoto za upatikanaji wa umeme. Kuanza kwa mradi huu kutakuwa na manufaa makubwa yafuatayo:-

Tukiingiza megawatt 2,100 kutoka kwenye zile tulizonazo na zingine tukaingiza kwenye vyanzo mbalimbali tuna uwezo sasa wa kujitosheleza hapa ndani na kuwauzia majirani zetu. Kwa hiyo, niombe Bunge lako Tukufu kwa pamoja tumuunge mkono Mheshimiwa Rais wetu kwa kuanzisha mradi huu. Kwa kweli tukifanya hivyo tutajenga sasa uchumi wa viwanda utakaotuondoa kwenye changamoto za umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu ukijengwa pamoja na kupeleka umeme katika gridi ya Taifa lakini utaleta maendeleo makubwa sana. Moja ya maendeleo ni ujenzi wa barabara za viwango vya lami kuelekea kwenye mradi wenyewe. Maendeleo mengine kwa sababu bwawa hili litakalojengwa litakuwa na urefu wa kwenda juu takribani ghorofa zaidi ya 78, itakuwa ni chanzo kikubwa cha kuvutia utalii ambapo utaleta fedha za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile bwawa hili litahifadhi maji ya kutosha hata kwenye kilimo cha umwagiliaji. Niwashawishi Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono juhudi za Serikali ili mradi huu uendelee kutekelezeka sambamba na miradi mingine ya kuzalisha umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye mradi….

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye mradi wa LNG, unaendelea vizuri. Utekelezaji wa miradi unaenda hatua kwa hatua, tulishakamilisha hatua tatu za mradi huu ambapo tulishapata eneo la ukubwa wa hekta 2,071. Tulishafanya tathmini ya fidia ambayo ni takribani bilioni 3.3 na tumeshakamilisha tathmini kwa ajili ya kuanza ujenzi. Kazi zinazoendelea sasa hivi kwenye LNG ni kukamilisha majadiliano ambayo yatakamilika Septemba 2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii nimwombe sana Mheshimiwa Mbunge mwenzangu, Mheshimiwa Nape tuwahamasishe wananchi wa maeneo yote ya Mtwara na Lindi uwekezaji wa LNG bado uko pale pale na mwaka huu wa fedha tumeomba bilioni 6.5 Waheshimiwa Wabunge mkiidhinisha mradi utatekelezeka vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaombe wananchi wa Mtwara na wananchi wengine waendelee kwenda kuwekeza Lindi na Mtwara kwa sababu mradi huu bado uko pale pale na utakamilika ndani ya wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nichukue nafasi hii kusema kwamba mradi huu utaanza kujengwa ndani ya miaka mitano na ukikamilika manufaa yake yataanza …
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nashukuru sana kwa kunipa fursa hii na mimi nitoe mchango katika Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na Watendaji wa Wizara hii kwa hotuba yao mahiri na ni nzuri yenye kueleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nawapongeza sana Serikali kwa kuweka mikakati mizuri ya kutupeleka kwenye kujenga uchumi wa viwanda. Katika Wizara yetu yako mambo mawili ya msingi ambayo nadhani katika Wizara hii ni muhimu sana tukayafafanua vizuri kama mikakati ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti pamoja na Waheshimiwa Wabunge, lipo suala la kuzalisha umeme wa kutosha, wa uhakika na unaotabirika. Njia pekee ni kuwa na umeme mchanganyiko. Kuwa na umeme mchanganyiko maana yake utumie rasilimali zote ulizonazo, ukusanye nguvu zote upate umeme mwingi, wa uhakika na wenye gharama nafuu ili kujenga uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo ya Serikali hadi sasa ni kuzalisha umeme upatao megawati 5,000 ifikapo mwaka 2020 na megawati 10,000 mwaka 2025. Sasa huwezi kuupata umeme huu kwa chanzo kimoja. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kusema kwamba tunayo rasilimali nzuri sana ya gesi asilia kuzalisha umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa katika umeme tulionao, kama malengo yetu ni kupata megawati 5,000 mwaka 2020, hivi sasa tuna jumla ya megawati 1,513. Kwa hiyo, bado safari ni ndefu. Kwa hiyo, lazima tuzalishe umeme wa kutosha ili kujenga uchumi wa viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika umeme huo hadi sasa, tuna takribani megawati 783 zinazotokana na rasilimali ya gesi asilia, lakini umeme wa maji ni megawati 567.7. Kwa hiyo, bado tupo mbali. Umeme wa mwisho wa kuzalishwa katika miradi ya maji ni huu mradi wa Kihansi wa mwaka 2000. Mradi kabla ya hapo ulikuwa ni umeme wa Kidatu wa mwaka 1975 na 1980. Kwa hiyo, ni miaka mingi tangu tumezalisha umeme wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika rasilimali ya gesi mwaka 2008 tulizalisha megawati 102 Ubungo I na mwaka 2012 tulizalisha megawati 129, mwaka 2016 megawati 150 Kinyerezi I na mwezi Aprili tumezalisha megawati 168 za gesi asilia. Kwa hiyo, ni lazima tuendelee kuzalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, katika gesi asilia bado kuna miradi mikubwa mitano ijayo. Mradi wa kwanza ni wa Somanga – Fungu wa megawati 330 tunaoanza kuzalisha na kuujenga mwaka huu wa fedha na mradi mwingine wa Mtwara megawati 300 za gesi asilia. Mradi mwingine utakaoanza mwakani ni mradi wa Kinyerezi III, megawati 300 na Kinyerezi II megawati 300 na hatimaye Kinyerezi IV megawati 330. Hayo malengo lazima tuyatimize. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fursa nyingine ya kutumia rasilimali ya gesi ni pamoja na matumizi ya viwandani. Tuna takribani trilioni 4.6 zitakazotumika kwa ajili ya kutengeneza viwanda vya mbolea na petrochemicals. Kwa hiyo, hayo ni matumizi ya gesi asilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kutumia rasilimali hiyo katika kusambaza mbolea lakini pia kwenye ujenzi wa viwanda vinavyoendelea ambavyo matumizi yake ni trilioni 3.6. Hayo ni matumizi ya gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna mpango wa kusambaza gesi majumbani na katika magari ambayo itatumika trilioni 1.2 kama gesi asilia ya kutumia kwenye matumizi yetu nyumbani na bado trilioni 1.2 itatumika kwa ajili ya viwanda vya vyuma. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kusema kwamba matumizi ya gesi asilia bado ni mengi kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mpango wa kujenga kiwanda kikubwa cha kusindika gesi kwenda kwenye kimiminika na matumizi hayo kila mwaka kiwanda hicho kitatumia tani milioni 10 kwa ajili ya kujenga kiwanda hicho cha gesi asilia. Kwa hiyo, manufaa ya gesi asilia bado ni mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia nafasi hii wananchi wa Mtwara, Lindi na maeneo mengine bado tutanufaika na hii rasilimali ya matumizi ya gesi asilia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, potential tuliyonayo, tunavyo vyanzo vingi. Hivi sasa potential tuliyonayo kwa upande wa kuzalisha umeme wa maji, tukizitumia vizuri, tunayo potential ya kuzalisha megawati 4,700 ya maji ambayo hatujaitumia. Hivi sasa tumetumia asilimia 12 tu. Wakati kwenye gesi, niweke sahihisho kidogo, jana nilisikia imesemwa kwamba ni 5%, siyo kweli, tumeshafika asilimia 10 ya matumizi ya gesi asilia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya gesi ambayo nimeisema, ukiangalia kwenye matumizi ya maji, kati ya megawati 4,700 tumetumia megawati 567 tu. Kwa hiyo, ni lazima tuendelee kuzalisha umeme wa maji ili rasilimali ya maji tuliyonayo ambayo ni kubwa ilete manufaa makubwa kwa ujenzi wa uchumi wa viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kusema mradi wa maporomoko ya maji ya Mto Rufiji na wala siyo Stiegler’s Gorge; maporomoko ya Mto Rufiji ni muhimu sana tukiujenga sasa kuliko kuuacha. Maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama malengo yetu ni kufikia megawati 5,000 mwaka 2020 na 10,000 mwaka 2025, umeme unaokwenda kutukomboa kwa mkupuo, kwa mchapuo, mara moja, ni megawati 2,100 wa maji ya maporomoko ya Mto Rufiji. Kwa hiyo, naomba sana Waheshimiwa Wabunge kwamba tuunge mkono juhudi za Serikali ili kusudi tuweze kupata umeme huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo vyanzo vingine ambavyo nazungumza mbali na kusema Mradi wa Mto Rufiji, ipo miradi ya geothermal na makaa ya mawe. Hivi sasa tuna potential ya makaa ya mawe tani bilioni tano hatujawahi kuzitumia. Tunayotumia sasa ambayo ni proven ni asilimia
25. Kwa hiyo, ni vema sana Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuhamasisha energy mix katika kujenga uchumi wa viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna potential ya geothermal ambayo inafikia pia megawati 5,000, hatujaanza kuitumia. Ni vizuri sana Waheshimiwa Wabunge tukiunga mkono juhudi za Serikali kutumia umeme mchanganyiko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie nafasi hii kusema Mradi wa Maporomoko ya Mto Rufiji ni muhimu sana kwa kuzalisha umeme lakini pia kwa utalii pamoja na shughuli za umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda kulizungumza ni kupata umeme wa uhakika na unaosafirishwa. Ni kweli kabisa tunazungumza hapa suala la umeme kukatika. Kwa sasa umeme tulionao, hali halisi ya umeme inaendelea kuimarika kwa kiasi kikubwa, changamoto tuliyonayo kidogo ni katika miundombinu. Lakini kama Serikali tumejipanga na tuna miradi mahususi ya kufanya ukarabati wa miundombinu ili kuhakikisha umeme tulionao haukatiki. Hiyo inaenda sambamba na kuwa na umeme wa kutosha ikiwemo na miradi mikubwa niliyoitaja.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nziungumze kidogo kuhusu juhudi za Serikali ya kusambaza umeme vijijini kama juhudi za kuunga mkono ujenzi wa viwanda. Ni dhamira ya Serikali kwamba ni lazima sasa viwanda tunavyovizungumza vianze kujengwa kuanzia vijijini na wala siyo mijini tu. Ndiyo maana kama Serikali tunapeleka umeme katika vijiji vyote mwaka 2020/2021. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa katika nchi yetu, kati ya vijiji 12,268 ni takribani vijiji 4,878 vimeshapelekewa umeme na vijiji vingine 500 vipo katika kuunganishwa umeme. Ni matumaini yetu kwamba mara baada ya miradi hii ya umeme vijijini kukamilika viwanda sasa vitarejea kuanzia vijiji. Ni matumaini yetu mihogo inazalishwa vijijini, hivyo tukiwapelekea umeme vijijini wananchi wote, viwanda vya kusaga na kukoboa unga vitaanzia vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naunga mkono juhudi za Mheshimiwa Waziri wa Viwanda kuhamasisha viwanda, uchumi wa kati ili kujenga uchumi wa Taifa letu. Kwa hiyo, nishati ndiyo mhimili pekee tunapokwenda kwenye uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi kwa hatua hii kwa sababu mambo ya msingi ambayo tunatakiwa tuyazungumze leo yana itifaki kubwa sana katika mustakabali wa maendeleo ya uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru wewe kwa kuendesha mjadala huu vizuri, na unaweza ukaona pande zote zinaridhika kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inafanya kazi vizuri sana katika masuala yote ya miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati, kaka yetu Mheshimiwa Kitandula na Makamu Mwenyekiti pamoja na Wajumbe wa Kamati. Lakini kwa aina ya pekee naomba niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa kipindi chote cha miaka minne iliyopita, wamekuwa wakitoa msaada mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unapoona Wabunge wanakuja kwenye kiti chetu hapa si kwamba wanakuja kuomba misaada au miradi ya umeme vijijini kwa upande wao, mara nyingi huja kutoa ushauri. Na kwa kiasi kikubwa tunawashukuru sana, tumezingatia sana ushauri wenu na ndiyo maana tumefika hatua hii. Waheshimiwa Wabunge kwa kweli tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee sasa kuchangia kwenye mada ya leo. Yapo mambo mengi yamezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge, lakini kwa sababu ya muda nitaongea kwa ufupi sana.

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu. Katika awamu hii, yako mambo mengi sana ambapo Tanzania itakumbukwa katika vitabu vya Watanzania kwa historia ya miaka mingi ijayo. Kuna miradi mikubwa sana ya vielelezo ambayo imetekelezwa na kila mtu ni shahidi. Mradi wa kuzalisha umeme wa Mto Rufiji almaarufu Julius Nyerere, kama ambavyo mnafahamu, unaenda kuondoa kero zote zilizokuwepo katika masuala ya undeshaji wa nishati hapa nchini. Kwa hiyo, ni hatua kubwa sana Awamu ya Tano imefanya katika jambo hili.

Mheshimiwa Spika, nami nawashukuru Waheshimiwa Wabunge jambo hili mnalifahamu. Jambo la pili katika hili, tumeingia katika historia ya kidunia. Mradi huu tumekuwa tukisema mara zote na ninapenda nirudie tu, ni mkubwa sana katika mabwawa yote duniani. Kwa mara ya kwanza tunaingia kwenye kitabu cha kidunia cha kutekeleza miradi mikubwa kama hii. Ni jambo la kumpongeza sana Mheshimiwa Rais na Serikali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kabla ya mwaka 2015 tulikuwa na uhaba mkubwa sana wa umeme. Tulikuwa na upungufu wa umeme takribani Megawati 270, ndiyo maana tulikuwa tuna mgao wa umeme, kwa maana ya kugawiana kidogo tulichokuwa nacho. Kwa leo mnaona kuna mabadiliko makubwa sana, tuna zaidi ya Megawati 280 mpaka 320 kwa siku. Hii ni hatua kubwa sna imefanyika kufikia hatua hiyo.

Mheshimiwa Spika, tunatarajia sasa kwenda kwenye jambo kubwa sana la pili la kihistoria kwa nchi yetu; kuendesha treni itakayotumia umeme katika mwendo kasi. Hii ni mara ya kwanza kwa nchi yetu kuanza kutumia umeme, kuendesha treni ya mwendo kasi. Tumetenga takribani ya Megawati 70 na treni kama mnavyojua, itakwenda umbali wa speed kubwa. Huu ni umbali mrefu sana, tunajenga mradi huu kwa umbali wa kilometa 160 na gharama yake ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, napenda niseme tu kwamba haya ni mabadiliko makubwa ambayo hayatasahaulika. Ingawaje halijajadiliwa hapa, lakini niseme, haya masuala mawili katika miaka miwili ijayo mradi mkubwa utakamilika Juni, 2022, na huu mradi wa SGR utakamilika hivi karibuni ikiwezekana mwakani, mtaona matokeo yake jinsi nchi itakavyopaa kiuchumi na tunasema Tanzania inaweza ikawa ni Tanzania ya miaka zaidi 40 kwa mfano wa nchi za Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende sasa kwenye hali ya umeme nchini. Ni kweli hali ya umeme imeendelea kuimarika sana. Nyote ni mashahidi, wote mliokuwa mnapita Kariakoo, mliokuwa mnapita Manzese, mlikuwa hamwezi kupokea sumu kwa wakati huo kwa sababu ya kelele za majenereta. Leo hii Awamu ya Tano imezima majenereta, unaweza ukaongea na simu wakati wowote, maeneo yoyote bila kuwa na wasiwasi. Ni kielelezo rahisi sana lakini ni rahisi kukiona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo la msingi kabisa, toka mwaka 2015 mtandao wa umeme nchini ulikuwa ujafikia asilimia 70, leo tunapoongea hapa katika nchi yetu tumeshatandaza umeme kwa umbali wa kilometa 130,000 nyaya kote nchini zimeshapita, hakuna mahali nyaya ya umeme haijafika kwenye nchi hii. Ni jambo ambalo ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na idadi ya nguzo kwa wakati huo milioni 1.1, leo tuna idadi ya nguzo zilizosimikwa na zenye umeme milioni 3.3, ni jambo kubwa sana. Tulikuwa na transfoma takribani 65,000, leo tuna transfoma 142,000. Ni kazi kubwa sana zimefanyika.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kwa sababu ya muda…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Malizia ya mwisho.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, mambo ya msingi ambayo ningependa nizungumzie hapa ni umeme Vijijini. Mwaka 2005 tulikuwa na umeme katika vijiji 231; mwaka 2008 tulikuwa na umeme katika vijiji 561, mwaka 2015 tulikuwa na umeme katika vijiji 218; leo tunapoongea kwa heshima ya Watanzania wote, tuna vijiji takribani 8,674 vina umeme hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika jambo hili unaweza ukaliona ni jepesi. Kwa Afrika sisi kwa sasa hivi ukiondoa Nigeria ambao wameshafikia asilimia 72 na wanaelekea 75, sisi tunategemea kufikia asilimia 76 mwakani na kuipita Nigeria. Kwa hiyo, tunaweza tukaanza kuongoza katika umeme Vijijini. Jambo hili ni kubwa sana na tunaomba sana tuipongeze sana Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbali na kupeleka umeme katika vijiji nilivyotaja, nchi yetu ina takribani ya Wilaya 180 na kitu; hivi sasa Wilaya 34 tumekamilisha kupeleka umeme katika vijiji vyake vyote. Wilaya hizo tutapeleka umeme kwenye Vitongoji tu, lakini kama Wilaya tumeshakamilisha. Hata kwako, vile Vijiji vya Saigoni, Makutupa pamoja na Soni na Laiboni, tumeshakamilisha na kwa kwako tutapeleka Vitongoji tu. Kwa hiyo, niseme kwa niaba ya Watanzania, nawashukuru sana wananchi kwa kukubali hili. Kazi kubwa imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbali na hilo, umeme tunaopeleka katika Vitongoji kwa kweli ni mara ya kwanza mnashuhudia, hakuna nyumba ya Mtanzania inayoachwa bila kupelekewa umeme. Nyumba za aina zote wananchi wanafurahia; wa maisha ya chini, kati na juu wanafurahia katika mpango huu.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Kalemani.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, la mwisho LNG…

SPIKA: Nakushukuru sana, ahsante sana.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nami nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo kwa kweli inatekelezeka kwa asilimia 100. Hongera sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naungana na Waheshimiwa Wabunge na Mawaziri wengine waliochangia kupongeza kwa kweli taarifa ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa sababu maeneo ambayo nitapita kwa kifupi sana ni matatu. Jambo la kwanza ililionekana ni kuhusiana na suala la LNG na suala la pili ni mradi wa mafuta wa ECOP wa Uganda na Tanzania na eneo la umeme vijijini.

Mheshimiwa Spika, napenda nianze na la mwisho. Katika eneo hili la kupeleka umeme vijijini, napenda niwaeleze Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wanaonisikiliza kwamba jambo hili limetupa sifa sana kidunia, tumefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bila kupoteza muda, labda niwapitishe Waheshimiwa Wabunge kidogo tu. Mwaka 2008 tulipoanza kutekeleza miradi ya kupeleka umeme vijijini tulikuwa kwenye nafasi ya 50 Afrika na tulifikisha asilimia 16.5 lakini Mwaka 2015 tulipofikisha sasa asilimia 39.5 tulikuwa na nafasi ya 25 Afrika. Mwaka 2017 tukiwa tunasogea sasa, wakati tunapelekea umeme vijijini tulifikia asilimia 47 tukiwa kwenye nafasi ya 18. Mwaka 2018 tulifikia nafasi ya nne Afrika tukiwa na asilimia takribani 58. Mwaka 2019 mwezi Desemba tulikuwa nafasi ya tatu, wakitupita Afrika Kusini na Nigeria. Mwaka huu mwezi wa Pili tukashika namba moja. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme tu, mwaka 2019 Afrika Kusini walikuwa na silimia 64 umeme vijijini; Nigeria walikuwa na asilimia 72 kwa umeme vijijini; leo sisi tunapoongea tuna asilimia 75.2 umeme vijijini. Kwa nini nimelazimika kuyasema haya?

Mheshimiwa Spika, kwanza naipongeza Serikali kwa kutoa fedha kwa kipindi chote hiki kuwapelekea umeme Watanzania. Takribani shilingi trilioni 2.8 zimetumika kuwapelekea umeme wananchi kwenye maeneo haya. Hongera sana Mheshimiwa Spika, hongera sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, nampongeza sana Mheshimiwa Rais katika jukumu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huwezi ukazungumza uchumi wa viwanda kama umeme vijijini haupo. Viwanda vinajengwa na raw materials kutoka vijijini, kwa hiyo msitari wa kwanza kupeleka viwanda ni kuanzia vijijini. Serikali yetu imejipambanua vizuri; huwezi leo ukazungumza kujenga kiwanda Dar es Salaam, eneo liko wapi? Huwezi kuzungumza kujenga kiwanda kizuri Dodoma Mjini, eneo liko wapi? Maeneo ya viwanda yako vijijini, ndiyo maana umeme tumepeleka huko. Kwa hiyo, jambo hili tumelitekeleza vizuri sana, naipongeza sana Serikali. Katika hili, nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge. Wametupa ushirikiano mzuri sana katika kufanya kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona niseme machache katika eneo hili kwa sababu ya muda. Najua tutawasilisha taarifa yetu mwezi ujao tarehe 26, nitaeleza kwa upana zaidi katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi, tunapoongea hapa, zipo Wilaya 35 ambazo Kata zake zote zimefikiwa na umeme, vijiji vyake vyote vimefikiwa na umeme. Kwa hiyo, mradi unaokuja hatutapeleka umeme kwenye vijiji, bali kwenye Vitongoji tu. Ni jambo kubwa sana limefanyika kwa mara ya kwanza. Kwa hiyo, katika eneo hilo, ni-reserve muda tu kwa ajili ya taarifa nyingine ambazo nimetakiwa nizieleze mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la mradi wa LNG kumekuwa na concern kubwa sana kwamba inawezekana mradi huu hautekelezeki. Naomba nitoe taarifa mbele ya Bunge lako tukufu; mradi wa LNG uko pale pale. Utatekelezwa na kazi za kufanya zinafanyika na Serikali imetenga fedha na harakati za kutekeleza zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, labda nitoe taarifa kidogo. Ni kweli takriban miaka miwili iliyopita speed imekuwa siyo nzuri na zipo sababu za msingi. Sababu ya kwanza, kwanza nilipongeze Bunge lako, mwaka 2018 uliunda Tume Maalum ya Wabunge Kupitia Mikataba ya Kugawana Mapato. Katika mapendekezo ya Tume ya Wabunge, ilipendekeza mikataba yote 11 (PSA’s) zifanyiwe mapitio na taratibu nyingine ziendelee baada ya mapitio hayo kukamilika. Sasa hili ni letu sisi kama Serikali. Tulifanya hivyo kwa nia njema ili kuhakikisha kwamba tunapokwenda huko mbele ya safari hatuangukii shimoni.

Mheshimiwa Spika, nampongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, baada ya mapendekezo ya Tume ya Bunge, Serikali imefanyia kazi mapendekezo hayo. Pamoja na kazi iliyofanyika ni kufanyia mapitio. Mwanasheria Mkuu wa Serikali amefanya kazi hiyo, nampongeza sana na kazi imekamilika. Hivi karibuni taarifa imewasilishwa Serikalini. Kinachofanyika sasa, Serikali inatafakari taarifa hiyo ili mapendekezo yatakayotokana na mapitio hayo sasa tuendelee na hatua ya utekelezaji wa mradi wa LNG.

Mheshimiwa Spika, kwa hatua tu tuliyofikia, jambo la kwanza tumetenga gesi asilia tani milioni 10 kwa ajili ya kutekeleza mradi huu. Kwa hiyo, commitment ya Serikali iko pale pale. Jambo la pili, tumetenga fedha kuwalipa wafidiwa 693 ambao watafidiwa takribani ekari 2,071; na hivyo pesa zipo. Najua Waziri wa Fedha amejiandaa kuwalipa taratibu zikikamilika, nadhani ni mwisho wa kipindi cha fedha cha mwaka huu. Kwa hiyo, ambao wamepitiwa na mradi huu wawe na imani na Serikali, watalipwa fidia zao ilimradi uhakiki utafanyika. Nimeona nitoe taarifa kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni mradi wa mafuta wa Hoima na Tanzania. Kwanza naipongeza Serikali mradi huu unatekelezwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, nieleze tu kidogo yapo mambo mawili ambayo tumeyafikia kwa sasa. Jambo la kwanza ni wenzetu Waganda walianza majadiliano na wazalishaji wa mafuta kwenye mkondo wa juu, imetuchukuwa muda mrefu lakini napenda kutoa taarifa kwamba wametuletea taarifa majadiliano wamekamilisha kwa hiyo sasa kuanzia hapo tunaweza kuendelea na mradi.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili tumekamilisha kwa upande wetu tadhimini ya watakao fidiwa ambao wanafika watu takribani watu elfu tisa kwa upande wa korido, lakini takribani watu elfu 3,420 kwenye maeneo yatakapo jengwa camp fedha zipo takribani bilioni 50 zimetengwa na Serikali yetu tukufu na Bunge lilipitisha tunashukuru sana kwa kazi hii. Kwa hiyo, niseme tu kwamba miradi itatekelezeka bila wasiwasi wote isipokuwa haya mambo mawili tunayakamilisha.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kwenye mradi huu ni suala la corona tunachofanya kwa sasa kwa sababu wataalam wetu hawawezi kwenda Uganda na waganda kuja Tanzania tunafanya mikutano kwa video conference ili kuonyesha kwamba Serikali tumekusudia kutekeleza mradi huu, kwa sababu ya muda nimeona nichangie haya machache sasa naunga hoja asilimia mia moja.