Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Dr. Medard Matogolo Kalemani (113 total)

MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-

Tathmini ya Mgodi wa Nyamongo (ACACIA) kwa wakazi wa Vijiji vya Nyakunguru, Kewanja, Nyangoto, Matongo kupisha upanuzi wa uzalishaji wa mgodi ilifanyika kuanzia mwaka 2012 ambapo wananchi walizuiwa kuendeleza maeneo yao:-

(a) Je, Wananchi hao watapewa lini fidia kutokana na maeneo yao kulingana na bei ya sasa?

(b) Je, fidia hiyo itaendana na usumbuu na hasara waliyoipata hadi sasa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wananchi hawajaanza kulipwa fidia, ukweli ni kwamba fidia imeanza kutolewa na imelipwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kijiji cha Nyakunguru, awamu namba 24, awamu namba 34 na awamu namba 35 kijiji hiki kina ukubwa wa hekta 35. Makadirio ya fidia ilikuwa shilingi bilioni mbili, lakini ziliongezeka hadi kufikia bilioni ishirini na saba kutokana na ujenzi holela na upandaji wa mazao unaofanywa na baadhi ya wananchi wasio waaminifu wakati wa fidia ikifanyika maarufu inaitwa mtegesho.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hiyo, mgodi umeamua kuliacha eneo hilo na kutumia njia ya uchimbaji wa chini ya ardhi yaani underground mining method. Aidha, awamu namba 22 mheshimiwa spika, 23, 25, 28, 29, 33 na 44 yenye ukubwa wa eneo la hekta 90.4 ambao fidia yake ni shilingi bilioni 12 ililipwa kati ya mwaka 2012 na 2014.

Mheshimiwa Spika, kijiji cha Kewanja, awamu namba 30. Ukubwa wa kijiji hiki ni hekta 8.10. Makadirio ya fidia yalikuwa shilingi milioni 250 lakini kwa sababu ile ile ya ujenzi holela na upandaji wa mazao unaofanywa na baadhi ya wananchi wasio waaminifu, fidia pia iliongezeka kutoka shilingi milioni 200 hadi kufikia shilingi bilioni 8.3. Mgodi umeamua kuliacha eneo hilo kwa sababu hauna fedha ya kuwalipa, aidha awamu namba 26, 27 na 31 jumla ya hekta 26.8 zililpwa fidia ya shilingi bilioni 8.8.

Mheshimiwa Spika, kijiji cha Nyangoto, awamu namba 20, namba 36, namba 37, namba 38, namba 40, 41, 42 na 44, kijiji hiki kina ukubwa wa eneo wa hekta 115.79, jumla ya fidia iliyolipwa kwa mgodi huu ilikuwa ni shilingi bilioni 41.14.

Mheshimiwa Spika, ieleweke pia katika awamu ya 20, jumla ya hundi 157 zenye thamani ya shilingi bilioni 3.7 bado hazijachukuliwa na wafidia, baada yao kusingizia kwamba pesa hiyo waliyolipwa ni kidogo mno.

Mheshimiwa Spika, kijiji cha Matongo, awamu namba 39, mgodi ulihitaji eneo kwa ajili ya kinga ya kiusalama tu ambao ni Bufferzone ya mita hasa 200 wakati wa ulipuaji baruti kati ya eneo la mgodi na wananchi, lakini kwa sababu ya tegesha ile ile, mgodi uliamua sasa kuachana na eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, fidia husika hulipwa kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi Na. 4 na Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 zote za mwaka 1999. Fidia hii ni kulingana na thamani ya kipindi ambacho tathmini ilifanyika, lakini pia fidia hizi zilizingatia usumbufu na uharibifu wa mali za wadai husika. Aidha, wananchi wa maeneo hayo wanatakiwa kujua kwamba viwango vya fidia vinavyotolewa na mgodi wa North Mara ni vikubwa zaidi ya viwango vinavyowekwa na Serikali. Kutokana na ukweli huo, wananchi wote wanaotakiwa kuchukua fidia na kupisha shughuli za uchimbaji wanashauriwa sasa wachukue fidia ili kupisha shughuli za uchimbaji.
MHE. LOLESIA J. M. BUKWIMBA aliuliza:-
Je, ni lini miradi ya usambazaji wa umeme katika Kata za Kamena, Nyamalimbe, Busanda, Nyakamwaga, Nyakagomba, Nyaruyeye, Kaseme, Magenge, Nyalwanzaja na Bujula katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita utaanza rasmi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lolesia Jeremiah Maselle Bukwimba, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Kanda za Busanda na Nyakamwaga zinafanyiwa tathmini ya Kampuni ya Ramaya International Tanzania Limited na zimewekwa kwenye Mpango wa Mradi wa Geita – Nyakanazi Transmission Line.
Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye Kata za Busanda na Nyakamwaga, itajulimsha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 23.7; pamoja na ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 wenye urefu wa kilomita 18.5; lakini kadhalika, ufungaji wa transfoma sita ambapo transfoma moja ina ukubwa wa kVA 50; transfoma mbili mbazo zina ukubwa wa kVA 100 na transfoma tatu zenye ukubwa wa kVA 200.
Mheshimiwa Spika, gharama ya kazi hii inakadiriwa kuwa shilingi bilioni 1.6. Kazi inatarajia kuanza mwezi Oktaba mwaka huu wa 2016 na itakamilika mwaka 2018.
Mheshimiwa Spika, Kata za Kamena, Nyamalimbe, Kaseme pamoja na Nyarwanzaga, zimefanyiwa tathmini na kubainika kuwa kazi ya kupeleka umeme kwenye Kata hizo itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme msongo kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 50.8. Kadhalika ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 25, pamoja na ufungaji wa transfoma 11 ambapo transfoma tatu zaina ukubwa wa kVA50; transfoma sita zina ukubwa wa kVA 100 na tranfoma mbili zenye ukubwa wa kVA200. gharama ya kazi hii ni shilingi bilioni 2.87.
Mheshimiwa Spika, Kata hizi zimo pia katika mpango wa awamu ya tatu ya kusambaza umeme vijijini yaani REA - Phase III unaotajariwa kukamilika mwezi Julai, 2016.
Mheshimiwa Spika, tathmini ya mahitaji halisi kwa ajili ya kupeleka umeme katika Kata za Nyaruyeye, Magenge, Nyakagomba na Bujula inafanywa na TANESCO na itakamilika mwezi Machi, mwaka huu ili kujumlishwa katika Mradi wa Awamu ya Tatu wa Kusambaza Umeme Vijijini yaani REA-Phase III unaotarajiwa pia kuanza mwezi Julai, mwaka 2016.
MHE. JAMES F. MBATIA (K.n.y. MHE. JOHN J. MNYIKA) aliuliza:-
Pamoja na kuwa karibu na Makao Makuu ya TANESCO, baadhi ya maeneo ya Jimbo la Kibamba hayana umeme na yale yenye umeme kiwango chake hupungua na kuongezeka (low voltage and fluctuation):-
(a) Je, Serikali inaweza kuwasilisha orodha ya maeneo yasiyo na umeme katika Kata za Saranga, Mbezi, Msigani, Goba , Kwembe na Kibamba, na lini maeneo hayo yatapatiwa umeme; (TANESCO)?
(b) Je, Serikali ina inachukua hatua gani kuondoa tatizo la kupungua na kuongezeka kwa umeme katika Kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Kibamba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, orodha ya maeneo yasiyo na umeme katika Kata ya Saranga, Mbezi, Msigani, Goba, Kwembe pamoja na Kibamba ni kama yafuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Kata ya Saranga ni Saranga Ukombozi na Nzasa na yanatarajiwa kupatiwa umeme mwezi Mei mwaka huu; Kata ya Msigani na Marambamawili inatarajiwa pia kupata huduma za umeme mwezi Aprili, mwaka huu; Kata ya Goba na Kata ya Goba Mpakani inatarajiwa pia kupata umeme mwezi Septemba, mwaka huu; Kata ya Kwemba ni King‟azi „B‟ itakayopatiwa umeme mwezi Septemba, mwaka huu; na Kisokwa ambalo limeombewa fedha kwenye bajeti ya TANESCO mwaka 2016/2017.
Pia Kata ya Mbezi ni Kibesa inayoombewa fedha katika bajeti ya TANESCO ya mwaka 2016/2017; na Msumi ambalo inapatiwa umeme mwezi Mei, mwaka huu; na katika Kata ya Kibamba maeneo yote yamefikiwa na umeme wa huduma iliyopita.
Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na tatizo la kupungua na kuongezeka kwa umeme katika Kata hizo, ukarabati wa miundombinu unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia mwezi Februari, 2016 na pia unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2016.
Kazi zitakazohusishwa na ukarabari huo ni pamoja na kuongeza njia ya umeme toka njia moja hadi njia tatu, yaani (upgrading), lakini kufunga nyaya zenye uwezo mkubwa wa kuondoa tatizo la kupungua kwa umeme chini ya utaratibu unaoitwa re-conductoring. Aidha, kutakuwa na ufungaji wa transfoma kubwa na kuondoa ndogo ili kukidhi mahitaji ya umeme katika maeneo husika.
MHE. UPENDO F. PENEZA aliuliza:-
Wananchi wa Mtaa wa Katoma, Kata ya Kalawala Wilaya ya Geita wameathirika sana na shughuli za Mgodi wa geita Gold Mine (GGM) ambapo nyumba zimepata nyufa na kuanguka kutokana na mitetemo, milipuko ya mara kwa mara inayoletwa na kelele na vumbi linaloathiri afya za wananchi wa mtaa huo pamoja na vyanzo vya maji.
Je, ni lini wananchi hao wa Katoma watapewa fidia za mali zao ili waondoke katika eneo hilo jirani kupisha shughuli za Mgodi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Upendo Furaha Peneza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ili kupata ufumbuzi wa malalamiko ya wananchi wa Mtaa wa Katoma, Wizara imeunda Timu ya Wataalam kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini kama athari zinazodaiwa na wananchi wa Katoma za kusababisha nyufa kwenye nyumba zao zinatokana na shughuli za ulipuaji wa baruti zinazofanywa na Mgodi wa GGM (Geita Gold Mine).
Mheshimiwa Spika, Timu hiyo itakamilisha kazi yake tarehe 25 Februari, mwaka huu na iwapo itabainika kuwa athari zinazolalamikiwa na wananchi wa Katoma zinatokana na shughuli za ulipuaji wa baruti kwenye mgodi huo, basi Serikali itahakikisha kuwa Mgodi wa GGM unalipa fidia stahiki kwa wananchi hao ili wahame na kupisha shughuli za uchimbaji madini kwenye eneo hilo.
MHE. DEO K. SANGA aliuliza:-
Serikali imeshaweka Mkandarasi ambaye kwa sasa yuko site anaendelea na kazi ya Mradi wa umeme katika Vijiji vya Mawande-Utengule, Luhota, Ngamanga, Ikwata, Mlowa, Mkolanga, Ibumila, Mahongole, Manga Usetule, Kifumbe, Mtanga, Kitandililo, Ibatu, Nyamande, Mtulingala na Mbugani;
Je, ni lini mradi huo wa umeme katika vijiji hivyo utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyanda Sanga, Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo:-
Ni kweli kwamba Serikali imeweka Mkandarasi Lucky Exports ambaye kwa sasa anatekeleza mradi wa REA awamu ya pili Mkoani Njombe. Mkandarasi huyo amepewa Vijiji vya Ikwata, Kifumbe, Luhota, Manga, Mlowa, Mwande, Ngamanga, Usetule pamoja na Utengule, ambayo amepatiwa kama kazi ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kazi ya usanifu tayari imekamilika na kwa sasa Mkandarasi anasubiri kusaini Mkataba kati yake na Wakala wa Umeme Vijijini (REA) kabla ya mwezi Machi mwaka huu, ili aanze utekelezaji wa mradi. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi unajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomiti 38.8, lakini pia ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 51, ufungaji wa Transfoma 19 ambapo transforma nne za ukubwa wa kVA 25 na transfoma 15 za ukubwa kwa kVA50. Hii ni pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,875. Kazi hii itachukua miezi sita kukamilika na itagharimu shilingi bilioni 3.3.
Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Mahongole, Manga, Mbugani, Mtanga, Mtulingala, na Nyamande vimewekewa umeme kwenye Mradi wa awamu ya tatu, (REA phase III) inayoanza utekelezwa hivi karibuni. Kazi ya kupeleka umeme kwenye Vijiji hivi inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33, yenye urefu wa kilomita 73, ujenzi wa njia ya umeme wa msongo kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 36, ufungaji wa transfoma 14 ambapo transfoma tano za ukubwa wa kVA 25 na transfoma tisa za ukubwa wa kVA 50. Hii ni pamoja na kuwaunganishia umeme wateja awali 1493. Kazi hii itaanza Julai mwaka huu na itagharimu shilingi bilioni 4.05.
Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Ibatu, Ibumila na Kitandililo tayari vimefanyiwa tathmini ya gharama za kupeleka umeme na kazi inatakiwa kufanyika kwenye kazi za nyongeza lakini kutokana na gharama kuwa kubwa itajumuishwa kwenye mradi wa awamu ya tatu.
Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka kwenye vijiji hivi inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu kilomita 11, ujenzi wa njia ya umeme wa msongo kilovoti o.4 yenye urefu wa kilomita 13 pamoja na ufungaji wa transfoma tano ambapo transfoma ambapo transfoma moja ina ukubwa wa kVA 50 na transfoma Nne za ukubwa kVA 100.
Hii pia itaunganisha pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 589. Kazi hii itaanza Julai, 2016 na itagharimu takribani shilingi milioni 885.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-
Miradi ya umeme ya REA Awamu ya Kwanza na ya Pili inaendelea vizuri.
Je, ni lini miradi ambayo haijakamilika itakamilika hasa ikizingatiwa kuwa Serikali iliahidi kukamilika kwa miradi hiyo kabla ya tarehe 30 Juni, 2015?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilifadhili utekelezaji wa mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini, Awamu ya Kwanza na ya Pili kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini (REA). Miradi ya awamu ya kwanza imeshakamilika kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya fedha iliyotengwa kutekeleza miradi ya REA Awamu ya Pili ni shilingi bilioni 877.3 na hadi sasa Serikali imeishalipa asilimia 75 na inaendelea kutoa fedha ili miradi ikamilike kabla ya mwezi Juni, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Awamu ya Pili, katika Mkoa wa Mwanza ikiwemo Jimbo la Sumve Wilaya ya Kwimba unatekelezwa na Mkandarasi Chico-CCC (BV) JV. Wigo wa kazi wa Mkoa wote kwa Mwanza ni ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 wenye urefu wa kilomita 463. Kadhalika ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 365 na kuunganisha umeme wateja wa awali wapatao 8,990. Utekelezaji wa kazi wa Mkoa wa Mwanza umefikia asilimia 78. Gharama ya Mradi wote wa REA Phase II ni shilingi bilioni 25.36. Mradi unatalajiwa kukamilika kabla ya mwezi Juni mwaka huu.
MHE. JAMES K. MILLYA aliuliza:-
Madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania tu katika Wilaya ya Simanjiro, tofauti na dunia inavyopotosha kuwa madini hayo yanatoka India na Kenya, ambako huenda Serikali hizo huwapa mitaji wafanyabiashara wao:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia Watanzania wanaofanya biashara ya Tanzanite kwa kuwapatia mitaji ili waweze kushindana na wafanyabiashara wa nje?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa James Kinyasi Millya, Mbunge wa Simanjiro, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania tu katika Wilaya ya Simanjiro. Maelezo kwamba yanapatikana sehemu nyingine duniani, ni upotoshwaji mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sina uhakika kwamba Serikali za India na Kenya zinawasaidia wafanyabiashara wa Tanzanite katika nchi zao kwa kuwapa mitaji ili kufanya biashara na ushindani wa nchi za nje. Lakini Serikali ya Tanzania inawasaidia wafanyabiashara wa madini wakiwemo wa Tanzanite kwa kuwawekea mazingira mazuri ya kibiashara kwa kuhakikisha kwamba wanakuwa na leseni halali za brokers au dealers ili wafanye biashara zao kihalali kwa kutumia mitaji yao ya kifedha na pia kwa kuzingatia sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na Kituo cha Arusha International Conference Center ina mpango wa kujenga jengo katika Jiji la Arusha kwa ajili ya biashara ya madini ambalo litakuwa na miundombinu inayotakiwa kwa ajili ya biashara hiyo. Lengo ni kuwahakikishia wafanyabiashara wa madini wanauza madini yao nchini kwa usalama na uhakika zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiandaa maonesho ya madini ya vito nchini maarufu kama Arusha Gem Fair yanayofanyika kila mwaka jijini Arusha. Lengo ni kuwaunganisha wafanyabiashara wa madini nchini pamoja na wale wa Kimataifa ili kujitangaza kibiashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kuwa biashara ya madini inaenda sambamba na shughuli zinazofanywa na wachimbaji wa madini wadogo wadogo. Hivyo, Serikali imekuwa ikiwasaidia wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini kuwapatia ruzuku, ambapo kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara ilitoa ruzuku ya jumla ya shilingi bilioni 7.2 kwa wachimbaji wadogo. Kadhalika ilitoa ruzuku hiyo kwa watoa huduma migodini, wakiwemo wanaofanya biashara ya Tanzanite.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale ambao hawakukidhi vigezo, wamepewa barua kueleza sababu za kutokidhi vigezo hivyo na wanakaribishwa kuomba ruzuku tena mara watakapopata fedha na kutoa tangazo la kibiashara kwa ajili ya ruzuku ya awamu inayofuata.
MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Mgodi wa Stamigold, Biharamulo uko kijijini Mavota katika Wilaya ya Biharamulo na wananchi wa Kijiji cha Mavota kwa sasa hawana fursa hata kidogo ya kufanya uchimbaji mdogo mdogo licha ya kwamba mgodi huo upo kijijini kwao, hali ambayo imekuwa chanzo kikubwa cha migogoro inayosababisha uvunjifu wa amani:-
(a) Je, Serikali iko tayari kuwa na mazungumzo ya kimkakati na wananchi wa Kijiji cha Mavota kupitia Mbuge wao kwa manufaa ya uwekezaji na wanakijiji wa Mavota?
(b) Kama Serikali haiko tayari kufanya mazungumzo hayo, je, ni kwa sababu zipi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ipo tayari kuwa na mazungumzo na wananchi wa Kijiji cha Mavota kwa lengo la kuwawezesha wananchi hao kutumia fursa zilizopo katika Mgodi wa Stamigold karibu na Mavota. Mgodi huo kwa sasa unamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100 kupitia STAMICO ambapo Stamigold kampuni tanzu ya STAMICO ndiyo inayofanya shughuli za uchimbaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo muhimu yatakayozingatiwa ni pamoja na kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji hao wadogo, kuwaelimisha namna ya kupata mitaji ya uchimbaji ikiwa ni pamoja na kutumia fursa za kuomba ruzuku Serikalini. Kadhalika, pamoja na kuwapa elimu na kuwahamasisha kuunda vikundi vya uchimbaji ili waweze kusaidiwa kwa pamoja. Aidha, Mgodi wa Biharamulo utawapatia mafunzo ya utaalamu wa kuchimba madini pamoja na kuwafundisha kanuni za usalama, afya na utunzaji wa mazingira katika migodi yao. Lakini pia watapewa mafunzo kwa vitendo katika mgodi wa Stamigold pale itakapohitajika kufanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, mgodi huo uko tayari na ulishaanza kuwasaidia wananchi wa Kijiji cha Mavota. Kati ya tarehe 26 na 30 Juni, 2015, Mavota Gold Mine Group kilipewa ushauri wa namna bora ya kuendesha shughuli za uchimbaji na utafiti wa dhahabu katika eneo walilomilikishwa leseni. Kikundi hicho kilimilikishwa leseni ya uchimbaji mdogo yenye Namba PL 001493WLZ iliyotolewa tarehe 23 Februari, 2015. Eneo hilo lina ukubwa wa hekta 9.43.
Mheshimiwa Naibu Spika, mgodi umetoa fursa za ajira kwa vijiji vya jirani. Vijana wenye ajira za muda mrefu kutoka vijiji vya jirani ni 15 na wafanyakazi wenye mikataba ya muda mfupi ni 54.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mgodi umetoa fursa za kibiashara kwa vikundi vitatu kutoka vijiji vya Mavota pamoja na Mkukwa ambapo wanavikundi hushirikiana kutafuta mazao ya kuuza mgodini kwa kuwasilisha mazao hayo kila wiki. Mazao hayo ni pamoja na viazi vitamu, mihogo, mboga za majani pamoja na matunda. Kutokana na kufanya biashara na Stamigold kati ya kipindi cha Julai 2014 na Disemba 2015, vikundi vyote vitatu vimeweza kujipatia zaidi ya shilingi milioni 200.
MHE. KISWAGA B. DESTERY aliuliza:-
Serikali imeweka mpango wa umeme vijijini ambapo kwa Jimbo la Magu ni asilimia 20 tu ya vijiji ndivyo vimepata umeme ambalo ni hitaji muhimu kwa kila Mtanzania:-
(a) Je, asilimia 80 ya vijiji vilivyobaki vitapata lini umeme?
(b) Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na tatizo la kukatikakatika kwa umeme nchini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniventura Desdery Kiswaga, Mbunge wa Magu, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kutambua juhudi za Serikali za kusambaza umeme katika Jimbo lake la Magu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji 39 kati ya 142 vilivyoko kwenye Jimbo la Mheshimiwa sawa na 27% tayari vimepatiwa umeme. Hata hivyo, vijiji 18 sawa na 13% viko katika utekelezaji wa awamu ya pili na hivyo kufanya jumla ya vijiji 57% sawa na 40% kuwa vimepatiwa umeme mara baada ya awamu ya pili kukamilika Juni, 2016. Vijiji 34 kati ya 85 vilivyosalia vitajumuishwa kwenye mpango wa usambazaji umeme awamu ya tatu utakaoanza Juni, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la kukatikakatika kwa umeme nchini inatokana na sababu za uchakavu na kuzidiwa kwa miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme na vituo vya kupoza umeme. Sababu nyingine ni pamoja na matukio ya kulipuka kwa transfoma yanayosababishwa na radi hasa kipindi cha mvua pamoja na wizi wa mafuta ya transfoma unaofanywa na wananchi wasiokuwa waaminifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na tatizo la kukatikakatika kwa umeme nchini, TANESCO inachukua hatua za kujenga mifumo ya njia kubwa za umeme wa msongo wa kilovoti 400 za backbone unaoanzia Iringa – Dodoma - Singida - Shinyanga. Kadhalika kuanzisha mradi wa North East Grid unaoanzia Dar es Salaam – Chalinze - Tanga - Arusha. Sambamba na miradi hiyo, upo mradi wa North West Grid unaoanzia Geita – Chalinze – Katavi – Kigoma - Rukwa - Mbeya. Hali kadhalika na mradi wa Makambako - Songea wenye kilovoti 220.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika kwa miradi hii, kutaimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika maeneo mengi nchini. TANESCO inakamilisha upanuzi wa mifumo ya usambazaji wa umeme katika Majiji makubwa ya Arusha, Dar es Salaam pamoja na Mwanza. Kazi zinazohusika ni pamoja na ujenzi wa njia mpya za umeme na kupanua vituo vya kupoza umeme (substations). Kukamilika kwa kituo cha kupoza umeme cha KIA Mkoani Kilimanjaro kutaimarisha sana upatikanaji wa umeme maeneo ya Mererani pamoja na uwanja wa ndege wa KIA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vya kupoza umeme katika Jiji la Dar es Salaam vya Gongolamboto, Kipawa, Mbagala na Kurasini vitaunganishwa kwa njia ya sakiti mizunguko (ring circuits) kutoka Ubungo, Kinyerezi kuanzia Machi, 2016. Kukamilika kwa mradi huu kutaimarisha upatikanaji wa umeme katika maeneo yanayohudumiwa na vituo hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingine ni ule wa ujenzi wa kituo cha kupoza umeme katikati ya Jiji la Dar es Salaam ukijumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 chini ya ardhi kwenda kituo cha Sokoine pamoja Kariakoo. Aidha, ifikapo Machi, 2016, TANESCO itakamilisha ujenzi wa Kituo cha Udhibiti wa Mfumo wa Usambazaji wa Umeme kwa Jiji la Dar es Salaam (Dar es Salaam Distribution Management System).
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo la umeme hasa kuungua kwa transfoma, TANESCO imeendelea kufunga mifumo ya kudhibiti radi (lightning arrestors) nchi nzima na kuachana na transfoma za mafuta hasa maeneo yaliyokithiri kwa wizi wa mafuta.
MHE. ALLY K. MOHAMED (K.n.y. MHE. KABWE Z. R. ZITTO) aliuliza:-
Je, ni lini Mradi wa kuzalisha umeme wa Malagarasi utaanza?
NAIBU WAZIRI NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabwe Ruyagwa Zitto, Mbunge wa Kigoma Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, baada ya tafiti za kimazingira kuonesha kuwa utekelezaji wa miradi wa kuzalisha umeme katika Mto Malagarasi katika maeneo ya Igamba Na. III ungekuwa na athari za kumazingira, Serikali itafute eneo lingine. Eneo la Igamba Na. III, lilipatikana na Mkandarasi Mshauri ESBI alianza kazi ya upembuzi yakinifu mwezi Juni, 2010 kupitia ufadhili wa Mfuko wa Changamoto za Milenia (MCC I). Upembuzi yakinifu na usanifu wa awali (preliminary design) ulikamilika mwaka 2012 na kubainika kuwa maporomoko ya sehemu hiyo yana uwezo wa kuzalisha MW 44.8 na Mkandarasi Mshauri alipewa kazi ya kufanya upembuzi yakinifu na utekelezaji wa miradi kufanywa na Mfadhili mwingine.
Mheshimiwa Spika, hivi sasa TANESCO inaendelea na taratibu za kumpatia Mtaalam Mshauri kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina yaani (detail design) na kutengeneza nyaraka za zabuni (tender document) zitakazotumika kumpata mkandarasi wa ujenzi wa kazi hiyo. Mradi huu unakusudiwa kutekelezwa kwa njia ya EPC (Uhandisi, Manunuzi pamoja na Ujenzi).
Mheshimiwa Spika, taratibu za kumpata Mtaalam Mshauri zitakamilika mwezi Juni, 2016, kazi ya usanifu wa kina pamoja na taratibu za kumpata mkandarasi wa ujenzi itachukua miezi sita. Mkandarasi atakayepatikana ataanza kazi Februari, 2017 na utekelezaji wa mradi utachukua miaka mitatu, fedha zitakazotengwa katika mwaka wa fedha 2016/2017 kwa utekelezaji wa mradi huu ni shilingi bilioni tano.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Wananchi wa Ludewa wamekuwa wakisikiliza mipango ya Serikali juu ya miradi mikubwa ya Makaa ya Mawe, Mchuchuma na Liganga ambapo kumekuwa na mipango mingi ambayo kwa sasa inaonekana kutekelezwa:-
(a) Je, ni lini wananchi walioachia ardhi yao kupisha miradi hiyo watalipwa fidia?
(b) Je, ni lini miradi hiyo inatarajiwa kuanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, miradi ya makaa ya mawe ya Mchuchuma na Liganga inasimamiwa na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji lakini inafanywa hivyo kwa kupita Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC). Miradi hii inaendelezwa kwa pamoja kwa maana ya (Intergrated Projects) kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) lenye asilimia 20 ya hisa na Kampuni ya Sichuan Hongda (Group) Company Limited ya China yenye hisa asilimia 80 kupitia kampuni ya ubia Tanzania China International Mineral Resources Limited (TCIMRL).
Mheshimiwa Spika, Serikali ilitoa leseni za uchimbaji mkubwa SML namba 533/2014 ya tarehe 09/10/2014 katika eneo la Liganga lenye ukubwa wa kilomita za mraba 30.41. Lakini SML ya pili namba 534/2014 ya tarehe 9/10/2014 katika eneo la Mchuchuma lenye ukubwa wa kilomita za mraba 25.46. Leseni hizi zilitolewa kwa kipindi cha miaka 25 na zitaisha muda wake tarehe 08/10/2039.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ilifanya uthamini wa mali za wananchi walioko ndani ya maeneo ya miradi ambao walitakiwa kupisha shughuli za utekelezaji wa miradi mwezi Agosti, 2015 na kuridhiwa na Mthamini Mkuu wa Serikali mwezi Agosti, mwaka huo huo. Mpango wa kulipa fidia unatarajiwa kuanza mwezi Juni, mwaka huu chini ya usimamizi wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
(b) Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mradi unatarajiwa kuanza Machi, 2017 na kukamilika mwezi Julai, 2020 na utafanywa hivyo chini ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI aliuliza:-
Ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Musoma kuwa kwenye hadhi ya Kitaifa kama siyo Kimataifa ni wazo la siku nyingi.
(a) Je, ni lini uwanja huo utajengwa katika hadhi stahiki?
(b) Je, Serikali ina mpango gani mahususi wa kuwa na ndege zake ili Mbuga yetu ya Serengeti iweze kufikiwa na watalii kwa urahisi kutoka nje moja kwa moja kuliko kupokea watalii wanaofikia Kenya na kuishi Kenya?
(c) Je, ni kiasi gani cha fedha tunachopoteza kwa kutokuwa na ndege zetu wenyewe kuleta watalii hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joyce Bitta Sokombi, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikifanya matengenezo ya miundombinu ya Kiwanja cha Ndege cha Musoma ili kiendelee kutoa huduma kama ilivyokusudiwa. Katika mpango wa muda mrefu, Serikali inaendelea na maandalizi ya uboreshaji wa miundombinu ya kiwanja hicho ambapo upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa kutumia fedha za mkopo toka Benki ya Dunia unaendelea.
Mheshimiwa Spika, kazi hii ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina unahusisha pia viwanja vya ndege vya Iringa, Njombe, Songea, Lindi, Kilwa Masoko, Tanga, Moshi, Lake Manyara, Singida na Kiwanja kipya katika Mkoa wa Simiyu ambapo viko katika hatua za mwisho na inatarajiwa kukamilika ndani ya mwaka huu wa 2015/2016.
(b) Mheshimiwa Spika, mpango mahususi wa Serikali kuimarisha Shirika la Ndege la Tanzania yaani ATCL katika siku za hivi karibuni ni kununua ndege mbili mpya zenye uwezo wa kubeba abiria 78 kila moja ili kuimarisha huduma ya usafiri wa ndege hapa nchini hiyo ikiwa ni pamoja na nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Spika, mpango mwingine ni kununua ndege nyingine mbili mpya zenye uwezo wa kubeba abiria 120 na 155 ambazo zinatarajiwa kufika hapa nchini mwanzoni mwa mwaka 2017 na 2018. Ndege hizo zikifika, zitaliwezesha Shirika la Ndege ATCL kurejesha safari zake za Afrika Kusini, Afrika ya Magharibi, Uarabuni pamoja na India. Idadi hii itafuatiwa na ununuzi wa ndege za ziada katika kuimarisha soko hilo. Hatua ya tatu ni kununua ndege ya masafa marefu kuelekea China, Mashariki ya Mbali, Jumuiya ya Ulaya na kadhalika. Hatua hii itakaribisha pia wawekezaji wa ndani na nje.
Mheshimiwa spika, pia kuchukuliwa kwa hatua hizi kutawawezesha watalii wengi kufika Tanzania moja kwa moja kwa kutumia Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) wakiwemo watalii wa Mbuga ya Wanyama ya Serengeti.
(c) Mheshimiwa Spika, ni vigumu sana suala hili kulitolea takwimu sahihi kwakuwa linahitaji kufanyiwa utafiti wa kina zaidi. Aidha, faida ambazo nchi zenye Mashirika ya Ndege ya Taifa yenye nguvu huzipata ni kuimarika kwa uchumi wa Kimataifa pamoja na kuharakisha maendeleo zaidi. Watalii, wawekezaji na watu wa kawaida hupenda kuwa sehemu ya mataifa yenye usafiri wenye hakika wa ndege, hivyo kujengeka kwa uchumi wa nchi hizo.
MHE. KUNTI Y. MAJALA (K.n.y. MHE. PAULINE P. GEKUL) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo la ulipaji wa ushuru wa huduma ambao ni asilimia 0.3 unaotozwa kutoka mitandao ya simu ambao kwa sasa Halmashauri zimeshindwa kukusanya ipasavyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Pauline P. Gekul, Mbunge wa Babati Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, suala la ulipaji wa ushuru wa huduma za mawasiliano ambao ni asilimia 0.3 limekuwa ni tatizo kwa pande zote mbili yaani Halmashauri ambazo ndiyo zinakusanya kwa upande mmoja na kampuni za mawasiliano ambazo anakabiliwa na ugumu wa kuzilipa kwa upande mwingine.
Mheshimiwa Spika, suala hili limejadiliwa na wadau kwa kuongozwa na Wizara yenye dhamana na Mawasiliano na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Mheshimiwa Spika, napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMESEMI), hivi sasa inafanyia marekebisho Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Sura 290 ili kuwezesha kukusanya ushuru wa huduma wa mawasiliano pamoja na maeneo mengine.
Mheshimiwa Spika, hatua hii litasaidia sana kupatia ufumbuzi tatizo lililoelezwa na Mheshimiwa Mbunge kwa mapato kukusanywa sehemu moja na Halmashauri zote kupata mapato stahiki. Rasimu ya Sheria hiyo ikikamilika inatarajiwa kujadiliwa katika kikao cha wadau hivi karibuni
Halmashauri ya Mbeya ina vijiji vingi ambavyo havijapata umeme katika Mpango wa REA na pia utekelezaji wa REA II uko nyuma sana:-
(a) Je, ni vijiji vingapi vya Halmashauri ya Mbeya vimo kwenye REA II na mradi utakamilika lini?
(b) Je, Kwa nini mradi wa REA II haujalenga kupeleka umeme kwenye huduma za kijamii kama vile Shule, Zahanati, Nyumba za ibada na vyuo?
(c) Je, ni lini sasa vijiji vilivyobaki vitapewa umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vya Halmashauri ya Mbeya vilivyomo kwenye REA Awamu ya Pili ni 27, vikiwemo vijiji vya Chang’ombe, Hatwelo, Haporoto, Idimi, Kasele, pamoja kijiji cha Wambishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi unaotekelezwa katika Awamu ya Pili , unafanywa na Mkandarasi SINOTEC ambao umefikia asilimia 54.33 na mradi huu unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2016/2017.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika miradi yote inayotekelezwa na Serikali kupitia Mfuko wa REA Vijijini, kipaumbele kimewekwa kwenye huduma za kijamii kama vile shule, zahanati, vituo vya afya, nyumba za ibada na mashine za kusukuma maji. Katika Mpango wa Awamu ya Pili ya umeme vijijini maeneo ya huduma za jamii ambayo yatafikishwa huduma ya umeme katika Halmashauri ya Mbeya Vijijini ni pamoja na shule za msingi 23, shule za sekondari tano, zahanati 10, kituo cha afya kimoja, pamoja na nyumba za ibada 42.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vingine vya Mbeya Vijijini ambavyo havikupata umeme kwenye Mpango wa REA kabambe Awamu ya Pili, vimewekwa kwenye Awamu ya Tatu unayotarajiwa kutekelezwa mara baada ya bajeti hii ya mwaka 2016 kupitishwa na Waheshimiwa Wabunge. Jumla ya vijiji 111 katika kata 30 za Mbeya Vijijini vimejumuishwa katika REA Awamu ya Tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye maeneo yanayojumuisha ujenzi wa shule za umeme pamoja na zahanati, inafanyika kwa ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 480; ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 530, ufungaji wa transfoma 137 za ukubwa mbalimbali pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 7,465. Gharama ya kazi hii inakadiriwa kufikia shilingi bilioni 51.52
MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza:-
Je, Serikali kupitia REA inachukua hatua gani kwa Mkandarasi CHICCO ambaye ameshindwa kukamilisha utekelezaji wa Mradi wa Kupeleka Umeme Vijijini Awamu ya Pili (REA II) katika vijiji vya Mwangoye, Mbutu na Mambali?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Bukene, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkandarasi CHICCO kutoka China alishinda zabuni ya usambazaji wa umeme vijijini REA Awamu ya Pili katika Mkoa wa Tabora. Ni kweli kwamba mkandarasi huyu alianza kazi kwa kusuasua hali iliyosababisha Wakala wa Nishati Vijijini kuchukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kumwandikia barua ya kutoridhishwa na kazi na kuongeza usimamizi wa kufuatilia utendaji wake. Hatua nyingine iliyochukuliwa ni pamoja na kumtaka mkandarasi huyo kuongeza kampuni nyingine (sub-contractor) ili kuharakisha shughuli za ujenzi wa mradi huo. Utekelezaji wa kazi hiyo wa mkoa mzima unaendelea ambapo kazi imekamilika kwa asilimia 82 na mradi unatarajiwa kukamilika mwishoni wa mwezi Juni, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme vijiji vya Mambali, Mbutu pamoja na Mwangoye inaendelea na imefikia utekelezaji kama ifuatavyo:-
(i) Kijiji cha Mambali kazi ya kupeleka umeme imekamilika kwa asilimia 100 na wateja wapatao 49 wameunganishiwa umeme.
(ii) Kijiji cha Mwangoye kazi ya kujenga njia ya umeme imekamilika. Taratibu za ufungaji wa transfoma zinaendelea na umeme unatarajiwa kuwashwa mara baada ya kukamilika kwa ufungaji wa transfoma hizo.
(iii) Kijiji cha Mbutu hakikuwepo kwenye mradi huu hata hivyo mkandarasi CHICCO alipewa kazi ya ziada na mradi unaendelea. Mkandarasi amemaliza kazi ya upembuzi yakinifu na sasa yupo katika hatua za mwisho za kukamilisha michoro ya kiuhandishi kabla ya kuanza utekelezaji wa mradi wa umeme katika kijiji hiki.
MHE. MARY P. CHATANDA aliuliza:-
Umeme katika Mji wa Korogwe uliingia miaka 50 iliyopita ukitokea kwenye mitambo ya kuzalisha umeme iliyopo Mji wa Hale kilometa 30 toka Mji wa Korogwe. Umeme huo ulikusudiwa kupelekwa kwenye mashamba makubwa ya mkonge na chai na ili kuupata umeme huo kwa Mji huo ilibidi upite kwenye mashamba ya mkonge Magunda, Kwashemshi na kwenda kwenye mashamba ya chai ya Ambangulu na Dindira:-
Je, Serikali haioni ni wakati muafaka Mji wa Korogwe na viunga vyake kuunganishwa na Gridi ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mary Chatanda, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hadi sasa Mji wa Korogwe hupata umeme kutoka kituo cha kuzalisha umeme cha Hale kilichounganishwa katika Gridi ya Taifa. Viunga vya Mji wa Korogwe navyo vimeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa na hivyo vitaendelea kupata umeme kutoka katika vyanzo vya maji vya Hale. Mji wa Korogwe una maeneo ambayo pia bado hayajapata huduma ya umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya ni pamoja na Vitongoji vya Bagamoyo, Habitat, Kilole Sobibo, Kitopeni, Kwandungwe, Makwei, Ruengera Relini, Ruengera Darajani na baadhi ya maeneo ya vitongoji vya Mtonga, Kwamkole pamoja na Kwasemangube. Maeneo haya yataingizwa katika mpango wa utekelezaji wa bajeti ya TANESCO kwa mwaka 2017/2018.
MHE. HASSAN E. MASALA aliuliza:-
Kwa muda mrefu kumekuwa na zoezi la utafiti katika Kata ya Nditi, Wilayani Nachingwea linalofanywa na kampuni tofauti:-
(a) Je, nini hatma ya utafiti huo wa muda mrefu ambao unaleta mashaka kwa wananchi wanaozunguka maeneo hayo?
(b) Je, wananchi wa maeneo jirani wanaweza kuruhusiwa kufanya shughuli za uchimbaji mdogo ili waweze kunufaika badala ya kuwa walinzi na vibarua?
(c) Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta watafiti zaidi katika maeneo mengine ya Wilaya hizo kama Kiegei, Marambo, Nditi na kadhalika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias Masala, Mbunge wa Nachingwea, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa eneo la Nditi lililoko Wilaya ya Nachingwea limefanyiwa utafiti wa madini kwa muda wa zaidi ya miaka minane sasa, hasa madini ya nickel katika eneo la Ntaka Hill. Leseni ya utafutaji ya PL Namba 4422/2007 ilitolewa tarehe 7 Aprili, 2007 kwa kampuni ya Warthog Resources ambayo inatoka Australia ambayo kwa sasa inaitwa Nachingwea Nickel Limited.
Mheshimiwa Naibu Spika, tangu mwaka 2007 hadi mwaka 2014 kampuni hii imetumia zaidi ya dola za Marekani milioni 36 na kugundua mashapo ya madini ya nickel takribani tani 356,000 na ya shaba tani 76,000 na upembuzi yakinifu unaonesha mashapo yanatosha kuchimba kwa mgodi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuendelea kuanguka kwa bei ya nickel kwenye Soko la Dunia kumesababisha kampuni kutoanzisha mgodi wa uchimbaji mapema. Kampuni inakusudia kuanzisha mgodi huo mara baada ya bei ya nickel kuimarika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kifungu Namba 14 cha Sheria ya Madini ya 2010, kinamzuia mtu yeyote asiye na leseni halali ya kuchimba madini, kufanya hivyo. Namuomba Mheshimiwa Mbunge pamoja na Bunge lako Tukufu tushirikiane kuelimisha wananchi ili kutovamia maeneo kuchimba madini kiholela bila kuwa na leseni.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Lindi kuna kampuni 98 zenye jumla ya leseni 213 za utafutaji mkubwa wa madini. Madini yanayofanyiwa utafiti ni pamoja na nickel, dhahabu, graphite, gypsum, manganese pamoja na beach sands.
Sehemu kubwa ya maeneo aliyotaja Mheshimiwa Mbunge, ya Kiegei, Marambo na Nditi ni baadhi ya maeneo ambayo leseni hizi za utafutaji zipo. Tunashauri pia wananchi wa maeneo hayo watumie fursa ya uwepo wa makampuni haya kushirikiana nayo katika shughuli za utafiti. Aidha, Wakala wa Jiologia Tanzania (GST) wanaendelea kufanya utafiti wa madini katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na maeneo ya Nachingwea.
MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-
Mgodi wa North Mara (Acacia Gold Mine) umeanza uchimbaji wa ardhini (underground) sasa yapata mwaka mzima bila kuweka wazi kama kuna mabadiliko ya kimkataba na kitendo hiki ni hatari kwa usalama wa kijiografia kwa wakazi wanaozunguka mgodi huo:-
Je, kwa nini Serikali isizuie zoezi hili mpaka mikataba iridhiwe na Serikali za Kijiji na kuanza upya bila kuwepo makandokando?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba uchimbaji wa madini chini ya ardhi (ungerground mining) katika mgodi wa North Mara (Acacia Gold Mine) ulianza mwaka 2015 katika eneo la Gokona baada ya Tathmini ya Kimazingira kufanyika na kibali kutolewa tarehe 23 Aprili, 2015. Aidha, mgodi haukuwahi kuwa na mkataba wa uchimbaji baina yake na vijijii vinavyozunguka eneo hilo. Kifungu cha 48(1)(a) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 kinamtaka mmiliki wa leseni ya uchimbaji mkubwa (Special Mining Licence) kubadili njia ya uchimbaji madini (mining method) pale inapohitajika kufanya hivyo hasa kwa lengo la kufanya uchimbaji kuwa endelevu kulingana na uwepo wa mashapo na jiografia yake. Mabadiliko hayo ya uchimbaji yalihusisha pia kufanya Tathmini ya Mazingira (Environmental Impact Assessment) zinazoweza kujitokeza wakati wa kutekeleza mabadiliko ya uchimbaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mgodi wa North Mara una mikataba na vijiji saba vinavyozunguka mgodi inayohusu namna ya kunufaika na uwepo wa shughuli za uchimbaji kwenye mgodi huo. Vijiji hivyo ni Kerende, Kewanja, Matongo, Ngenkuru, Nyakunguru, Nyamwanga na Nyangoto. Mikataba hiyo haihusiani kabisa na namna mgodi unavyowajibika katika kutekeleza sheria wakati wa uendeshaji wa shughuli za uchimbaji. Hivyo, mgodi haulazimiki kuomba ridhaa ya Serikali ya Vijiji husika wakati wa kubadili aina ya uchimbaji yaani kutoka mgodi wa wazi kwenda mgodi wa chini ya ardhi. Hata hivyo, pamoja na mgodi kubadilisha aina ya uchimbaji, mikataba yote iliyopo kati ya vijiji hivyo pamoja na wadau wengine itaendelea kuwepo kwa mujibu wa mikataba yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kusimamia uchimbaji huo kwa mujibu wa sheria husika na kuchukua tahadhari ili kuhakikisha kwamba uchimbaji wa madini chini ya ardhi katika mgodi huo hauhatarishi usalama wa wananchi wanaozunguka mgodi huo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. JAMAL KASSIM ALI) aliuliza:-
Serikali katika kipindi hiki imejipanga kufufua viwanda vyetu:-
Je, katika mipango hiyo mizuri, Serikali imejipanga vipi kusaidia wananchi kuweza kuanzisha viwanda hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jamal Kassim Ali, Mbunge wa Magomeni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kufufua viwanda vilivyobinafsishwa ambavyo havifanyi kazi ili kuongeza ajira kwa vijana na pato la Taifa. Kupitia Wizara yangu na kwa kushirikiana na Msajili wa Hazina tunafuatilia mikataba ya viwanda vilivyobinafsishwa ili kuona utekelezaji wa mikataba ya mauzo kama kufanya uperembaji wa kina ili kujiridhisha kabla ya kuvirejesha kwa Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu inaendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji kwa wazawa na tunahimiza Halmashauri za Wilaya zote nchini pamoja na Mamlaka za Mikoa kutenga maeneo katika wilaya, vijiji, kata ili yaweze kutumika kwa ajili ya uwekezaji. Serikali imejipanga kuwezesha upatikanaji wa maeneo ya kujenga viwanda, kuhamasisha uwekezaji katika viwanda, kushauri kuhusu upatikanaji wa mitaji na teknolojia ya kisasa, kuwaibua wanaviwanda, kuwalea na kuwaendeleza kupitia viatamizi (incubators) lakini kadhalika kutoa ushauri wa kitalaam na kujenga miundombinu wezeshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wawekezaji wazawa wanashauriwa kutafuta wabia wenye mitaji au kuungana nao na kuomba mikopo katika benki mbalimbali hususan TIB. Pia, Taasisi za Serikali za TBS, TIC, TIRDO na Benki ya Wakulima, zinaelekezwa kutoa maelekezo na huduma inayotakiwa ili kufanikisha wazalendo kuwekeza katika viwanda.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. SEIF K. S. GULAMALI) aliuliza:-
(a) Je ni lini Serikali itakwenda kuona hali ya Kiwanda cha Manonga na kukifanya kiweze kufanya kazi na kutoa ajira kwa vijana wa Mkoa wa Tabora?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kukiangalia upya Kiwanda cha Nyuzi Tabora ili uzalishaji uweze kuanza?
NAIBU SPIKA: Naibu Waziri wa Nishati na Madini kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Gulamali, Mbunge wa Manonga, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji yupo tayari kwenda Manonga na kutembelea Kiwanda cha Manonga.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kukifufua Kiwanda cha Manonga Ginnery ili kiweze kufanya kazi na kutoa ajira kwa vijana wa Mkoa wa Tabora. Pamoja na jitahadi za Wizara yangu na Msajili wa Hazina, mkakati wa kufufua sekta ya pamba pamoja na nguo (cotton to clothing strategy) utaongeza uzalishaji wa pamba. Chini ya mkakati huo tunalenga sasa kuongeza uzalishaji wa pamba kwa tija lakini wingi wa pamba utapelekea pia kutosheleza mahitaji na matumizi ya ginneries ikiwemo ikiwemo Ginnery ya Manonga.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Tabotex kilichopo Mkoani Tabora kimekuwa kikifanya shughuli za usokotaji nyuzi tangu mwaka 1978 chini ya umiliki wa Serikali. Ilipofika Aprili, 2004, Serikali ilikibinafsisha kiwanda hicho kwa kampuni za Noble Azania Investment Limited na Rajani Industries Limited. Kiwanda hicho hakijafungwa bali kimesimamisha uzalishaji kutokana na changamoto ya soko la nyuzi ndani na nje ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha Tabotex kilisimamisha uzalishaji Mei, 2015 kutokana na kuwa na akiba (stock) kubwa ya nyuzi zilizozalishwa mwaka 2013 ambapo hadi sasa zinaendelea kuuzwa. Soko kubwa la nyuzi za Tabotex ni soko la nje huku kiwango kidogo kikiuzwa katika soko la ndani. Kawaida wanunuzi wakubwa wa nyuzi ni viwanda vinavyofanya shughuli za ufumaji wa vitambaa lakini viwanda vyote vinavyofanya kazi ya ufumaji vitambaa nchini vikiwemo 21st Century, Sunflag Limited, Urafiki, NIDA na Musoma Textile vina mitambo yake ya kusokota nyuzi, hivyo soko la ndani la Tabotex kuachwa kwa wafumaji wadogo wadogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hilo sasa, kiwanda hicho sasa kinatafuta mwekezaji ambaye atakuwa tayari kuingia nacho ubia kwa kupanua wigo wa uzalishaji na kukufua shughuli za ufumaji vitambaa (weaving) hadi ushonaji. Wadau tushirikiane ili tupate mshirika atakayeweza kuboresha shughuli za kiwanda cha Tabotex.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI (K.n.y. MHE. LAMECK O. AIRO) aliuliza:-
Usambazaji wa umeme kupitia REA ulikusudiwa kufikishwa kwenye vijiji na senta 54 kwenye Awamu ya II na ingewezesha upatikanaji wa umeme asilimia 25-30, kwani upatikanaji wa umeme kabla ya mpango huo ulikuwa ni asilimia 5 na kwa kuzingatia mahitaji makubwa ya umeme kwa maendeleo ya wananchi wa Rorya umeme wa asilimia 25 bado ni wa chini na hata hivyo bado mradi unasuasua:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza kasi ya usambazaji umeme katika Wilaya ya Rorya?
(b) Je, ni lini Mpango wa REA II utakamilika na kuanza REA III?
(c) Je, REA III ina vijiji na senta ngapi ndani ya Wilaya ya Rorya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lameck Okambo Airo, Mbunge wa Rorya, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa REA Awamu ya II kwa Wilaya ya Rorya ulitarajia kufikisha huduma ya umeme katika vijiji 44. Mradi huu upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji ambapo ujenzi wa njia kubwa ya umeme msongo wa kilovoti 33 na ufungaji wa transfoma umekamilika kwa asilimia 95 na wateja zaidi ya 300 katika vijiji 16 wameunganishiwa umeme kwa sasa. Ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa muda uliopangwa, Serikali imeongeza kasi ya usimamizi wa karibu pamoja na kumwelekeza Mkandarasi Derm Electric kukamilisha kazi hizo kwa wakati.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa REA, Awamu ya II utakamilika mwishoni mwa Juni, 2016. Vijiji vitakavyobaki katika REA Awamu ya II vitaunganishiwa umeme kupitia REA Awamu ya III itakayoanza Julai, 2016.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Rorya, vijiji vipatavyo 56, sekondari nne na kanisa moja vinatarajiwa kupatiwa umeme katika Mpango wa REA Awamu ya III.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA (K.n.y. MHE. EZEKIEL M. MAIGE) aliuliza:-
Kilio kikubwa cha wananchi waishio jirani na Mgodi wa Bulyankulu ni kunufaika na mgodi huo:-
(a) Je, ni kiasi gani cha pesa Mgodi wa Bulyankulu ulitumia katika miradi ya ujirani mwema?
(b) Je, kwa nini mgodi huo hautekelezi miradi yake kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Msalala ambako kuna wataalam na gharama za utekelezaji miradi ni ndogo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 2015 Mgodi wa Bulyankulu kwa kutumia “Maendeleo Fund” ulitumia takribani dola za Marekani milioni 1.98, sawa na takribani shilingi bilioni 4.4 kwa ajili ya miradi ya ujirani mwema iliyotolewa na Kampuni hiyo ya Bulyankulu.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni za Migodi huwa na utaratibu wa kutekeleza shughuli zake kwa kuajiri wafanyakazi kulingana na mahitaji yao na kwa kuzingatia sheria za nchi. Pamoja na hayo, kampuni hizo huruhusiwa kuajiri wakandarasi wafanyakazi katika taaluma za ujuzi ambao haupo nchini. Hadi sasa kampuni imeajiri wafanyakazi hapa nchini wapatao 1,168, kati yao wafanyakazi 517 wanatoka katika maeneo yanayozunguka mgodi huo. Aidha, miradi husika hutekelezwa kwa kushindanisha wakandarasi na wataalamu kutoka sehemu mbalimbali nchini wakiwemo kutoka Halmashauri husika na hasa ya Msalala.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tutachukua hali hii kama ombi rasmi la Mheshimiwa Mbunge wa Msalala ili kulitafakari na kulifanyia kazi na kukaa na wakandarasi pamoja na mgodi unaomiliki shughuli za Mgodi wa Bulyankulu.
MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Wananchi wa Kijiji cha Busiri, Wilayani Biharamulo ni miongoni mwa Watanzania wanaoendesha maisha yao kwa shughuli za uchimbaji mdogo mdogo ambazo zinahitaji kuungwa mkono na Serikali kimkakati.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwaunga mkono wachimbaji wadogo wadogo wa Busiri?
Je, Serikali iko tayari kuwatembelea wananchi wa Busiri na kuwaelewesha ni namna gani na ni lini itaanza kutekeleza mkakati huo wa kuwaunga mkono wachimbaji wadogo wadogo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya mikakati ambayo Serikali imechukua kwa wachimbaji wadogo wa madini hasa katika eneo la Busiri ni kuwatafutia maeneo ya uchimbaji wa madini. Wizara imetenga eneo lenye ukubwa wa takribani hekta 11,031 lililoko chini ya leseni za utafutaji wa madini namba 3220 ya mwaka 2005 iliyokuwa inamilikiwa na Ndugu Daudi Mbaga. Kadhalika katika eneo hilo la leseni ya utafutaji wa madini namba 5853 ya mwaka 2009 iliyokuwa chini ya kampuni Meru Resource Limited ambazo zote zimemaliza muda wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwisho wa mwezi Machi mwaka jana na mwisho wa mwezi Machi mwaka huu Wizara imegawa kwa wananchi wa Busiri leseni 81 zenye uchimbaji mdogo wa madini ambazo kwa ujumla wake zinachukua hekta 810 kati ya hekta 11,031 za eneo hilo. Aidha, Wizara imegawa leseni nyingine 30 za uchimbaji mdogo katika eneo lililoko katika karibu na eneo hilo takribani kilometa moja tu kutoka eneo la uchimbaji mdogo wa madini la Busiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati mwingine ni kuendelea kulitumia eneo la Shirika la STAMICO kutoa huduma za ugani kwa wachimbaji madini wadogo hasa wa kijiji cha Busiri na maeneo mengine nchini. Mkakati mwingine ni kuwapatia ruzuku pamoja na kuwapatia elimu endelevu itakayoendelea kutolewa pamoja na shirika la STAMICO.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikiwatembelea wachimbaji hawa mara kwa mara hasa kwa kutumia Maafisa na wataalam wa ofisi ya Kanda ya Ziwa Victoria Magharibi na Afisi Madini Mkazi wa ofisi ya Bukoba. Tarehe 11 Machi, 2016 Afisa Madini Mkazi wa Bukoba alifika na kufanya mkutano na kikundi cha Busiri Mining Co-operative Society Limited chenye leseni ya uchimbaji mdogo. Aidha, ili kutekeleza sasa ombi la Mheshimiwa Mbunge Wizara yangu itamtuma tena Afisa Madini kutembelea eneo hilo na kuwaelimisha wananchi juu ya uchimbaji mzuri mdogo wa madini katika eneo hilo.
MHE. COSTANTINE J. KANYASU (K.n.y MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA) aliuliza:-
Mkandarasi wa REA anayefunga umeme katika Jimbo la Geita Vijijini amemaliza tatizo na yule anayeunganisha kutoka Sengerema yupo pole pole sana.
Je, ni lini sasa Serikali itamsimamia kikamilifu mkandarasi huyo ili aweze kumaliza kazi hiyo na umeme uweze kuwashwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Musukuma Joseph Kasheku, Mbunge wa Geita Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa REA Awamu ya II katika Mkoa wa Geita likiwemo Jimbo la Geita Vijijini unatekelezwa na mkandarasi Nakuroi Investiment Company Limited. Kazi ya kupeleka umeme Geita inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 161.5; ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 119.2; ufungaji wa transfoma 49 za ukubwa mbalimbali. Pamoja na hayo pia kuunganisha umeme wateja wa awali 2,560 na kazi za mradi zimekamilika kwa asilimia 94 ambapo ujenzi wa laini kubwa umekamilika kwa asilimia 100 na ujenzi wa laini ndogo umekamilika kwa asilimia 84. Kadhalika ufungaji wa transfoma 29 zimefungwa na wateja 846 wameunganishiwa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, umeme umeshafika Nyamadoke kutoka Sengerema Mkandarasi ameelekezwa sasa kuhakikisha kwamba, kazi zote za kuunganisha zinakamilika ifikapo mwezi June mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, REA pamoja na TANESCO wameongeza kasi sasa ya kumsimamia Mkandarasi huyu ili kuhakikisha kwamba kazi za ujenzi zinakamilika ifikapo Juni mwaka huu.
MHE. FLATEI G. MASSAY (K.n.y MHE. WILLY Q. QAMBALO) aliuliza:-
Pamoja na kuwa katika Kata ya Qurus zipo Ofisi ya Kituo cha TANESCO, Vijiji vingi vya Kata hiyo vikiwemo Gongali, Qurus, Qorongaida, Genda na G/ Lambo havijafikiwa na umeme na vichache vyenye umeme, kwango cha usambazaji ni kidogo sana:-
Je, ni lini Serikali itawapaia wananchi wa Kata hiyo huduma hiyo muhimu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Willy Qulwi Qambalo, Mbunge wa Karatu linaloulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Flatei Massay Mbunge wa Mbulu Vijijini kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, jina la Kata iliyoko Wilayani Karatu ni Qurus yenye vijiji vya Bashay, Doffa G‟Lambo, Gendaa, Gongali, Qorong‟aida na Qurus. Aidha, hakuna Ofisi ya kituo cha TANESCO katika Kata hii. Vijiji vyote 23 vilipangwa kupatiwa umeme katika mradi wa REA awamu ya II Wilaya ya vimewashiwa umeme na hivi sasa Mkandarasi Angelique International Ltd anaendelea na kazi ya kuwaunganishia umeme wateja. Utekelezaji wa mradi huu umefikia asilimia 99 na utakamilika ifikapo tarehe 30 Juni, mwaka huu. Gharama za mradi huu ni shilingi bilioni 53.24.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vilivyotajwa na Mheshimiwa Mbunge G‟lambo, Gongali, Qorong‟aida na Qurus vimewekwa kwenye mpango wa REA awamu ya III unaoanza Julai, 2016. Kazi ya kupeleka umeme katika Vijiji hivi itahusisha pia ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 8, ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 12, ufungaji wa transfoma 5 zenye ukubwa mbalimbali lakini pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 236. Gharama ya kazi hii ni hsilingi milioni 740.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itawapa maeneo ya uchimbaji wachimbaji wadogo wa Kata za Nyarugusu, Nyaruyeye na Kaseme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lolesia Jeremiah Bukwimba, Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2001 Wizara ilitenga eneo lenye ukubwa wa hekta 533.55 kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika eneo la Nyarugusu. Pamoja na hatua hiyo, wachimbaji wadogo wameendelea kuomba kumilikishwa maeneo hasa ya Buziba yanayomilikishwa na Kampuni ya Buckreef Gold Ltd, kupitia leseni namba PL 6545/2010. Leseni hii itaisha muda wake tarehe 11 Julai, 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya Nyaruyeye na Kaseme pia yana leseni hai ya utafutaji wa madini yenye leseni RL 0007/2012 ya Kampuni ya ARL ambayo pia itaisha muda wake tarehe 20 Septemba, 2017. Kwa sasa Serikali inafanya mazungumzo na kampuni hizo ili kuona uwezekano wa kuachia maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea na utaratibu wa kutenga maeneo kwa ajili ya shughuli za wachimbaji wadogo hapa nchini. Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) wanaendelea kutathmini maeneo mbalimbali ili kuona kama maeneo hayo yana mashapo ya kutosha kwa ajili ya wachimbaji wadogo.
Aidha, Serikali itaendelea kujadiliana na kampuni zinazomiliki leseni za madini kwa wachimbaji hapa nchini kwa ajili ya kuwagawia wachimbaji wa maeneo ya Nyarugusu, Nyaruyeye pamoja na Kaseme.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, katika kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo, vigezo vinavyozingatiwa ni pamoja na uwepo wa eneo lililo wazi kwa ajili ya kuwagawia wachimbaji kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 2010.
MHE. JAMAL K. ALI aliuliza:-
Kwa miaka mingi nyuma TANESCO ilikuwa ndicho chombo kilichohusika katika kuuza na kupanga bei za umeme kwa wateja wake katika makundi tofauti ya wateja wake katika nchi yetu mpaka pale EWURA ilipoanzishwa na kuanza kufanya kazi:-
(a) Je, ni vigezo gani ambavyo EWURA inavitumia katika kupanga bei hizo?
(b) Je, kuna unafuu gani wanaopata kwa wateja wanaochukua umeme katika mikondo mikubwa ya KV 11, KV 33 na KV 132?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jamal Kassim Ali, Mbunge wa Magomeni, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, EWURA hupanga bei ya umeme kwa kuzingatia gharama halisi za uendeshaji wa biashara kama ilivyobainishwa kwenye Sheria ya Umeme ya mwaka 2008. Bei hiyo ya umeme hupangwa kulingana na makundi ya watumiaji ili kila kundi libebe gharama zake.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, TANESCO ina wateja mbalimbali ikiwa ni pamoja na wateja wa majumbani ambao ni D1 na T1. Wateja wa viwanda vidogo vidogo ambao pia wanatumia msongo wa volti 400 na matumizi kwa mwezi ni zaidi ya uniti 7,500 ambao ni T2, lakini wateja wakubwa waliounganishwa katika msongo wa kati wa medium voltage yaani T3 na MV na wateja wakubwa waliounganishwa katika msongo mkubwa (high voltage: T3-HV).
Mheshimiwa Naibu Spika, unafuu wanaopata wateja wanaounganishwa katika msongo mkubwa wa umeme ni kuwa na bei ya chini (energy charge) ukilinganishwa na wateja wadogo, hasa majumbani ambao ni T1. Unafuu huo unatokana na ghrama za usambazaji na upotevu wa umeme kuishia kwenye mfumo wa HV na medium V, yaani kilovoti 220, Kilovoto 132, KV 66, KV 33 pamoja na KV 11.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana bei za umeme zilizopo hivi sasa, mteja wa T1 analipa shilingi 292/= kwa unit moja; mteja wa viwanda vidogo vidogo (T2) wanalipa shilingi 195/= kwa unit moja na mteja wa T3-MV analipa shilingi 157/= kwa uniti moja; na mteja wa T3 yaani high voltage ikiwemo migodi mikubwa ya madini kama GGM na mingine, pamoja na ZECO wanalipa shilingi 152/= kwa unit moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, h•Hata hivyo, wateja wadogo wadogo, hasa wa majumbani ambao ni D1 wanaotumia chini ya unit 75 kwa mwezi wanalipa shilingi 100/= kwa unit moja.
MHE. ISSA A. MANGUNGU (K.n.y MHE. LUCY SIMON MAGERELI) aliuliza:-
Machimbo ya Madini ya ujenzi yaliyoko Kigamboni yanatoa malighafi muhimu sana inayosaidia ujenzi katika jiji la Dar es Salaam; machimbo haya yanatoa ajira kwa zaidi ya wakazi 6,000 na ndiyo machimbo yenye mwamba laini kwa Mkoa wa Dar es Salaam ukilinganishwa na madini yanayotoka Goba:-
(a) Je Serikali haioni kuwa utaratibu wa kuratibu zoezi la kufunga machimbo haya utakosesha ajira kwa watu zaidi ya 6,000?
(b) Je, kwa kufunga machimbo hayo, Serikali haioni kuwa inawanyima fursa wananchi wa Dar es Salaam na Pwani kupata madini ya bei nzuri na kuwapunguzia gharama za ujenzi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Simon Magereli, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini hapa nchini hufanyika kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 2010. Sheria hiyo imeweka utaratibu Maalum wa uchimbaji wa madini ikiwemo kuacha umbali wa mita 200 kutoka makazi ya watu yaani bufferzone.
Umbali huo umekadiriwa kitaalam kuzuia madhara yanayoweza kutokea kutokana na shughuli za uchimbaji hasa maeneo ya makazi. Kwa sababu hizo sasa, Wizara ya Nishati na Madini inafanya mipango wa kutathmini namna bora ya kuendelea uchimbaji madini ya ujenzi katika mkoa wa Dar es Salaam hasa bila kuathiri mazingira, afya pamoja na maeneo ya wakazi kama nilivyoeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona umuhimu sasa wa kupanua fursa na kuwezesha wananchi wengi kushiriki katika shughuli za uchimbaji wa madini haya. Hata hivyo Serikali inachukua fursa hii kutoa wito kwa Mheshimiwa Mbunge na wananchi wote kwa wachimbaji wote ili kuzingatia sheria zilizowekwa kwa mujibu wa sheria na kuongeza pato la Taifa.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Katika Halmashauri ya Mbeya kuna mradi wa uchimbaji wa madini unaotarajiwa kuanza kwenye eneo la Mlima Songwe, lakini pia kuna mradi mwingine mkubwa wa joto ardhi kwenye Kata za Swaya, Ijombe na Bonde la Songwe.
(a)Je, kwa nini Serikali Kuu haihusishi Halmashauri ya Mbeya katika mradi hiyo ili elimu iweze kutolewa kwa wananchi?
(b)Je, wananchi wa Jimbo la Mbeya Vijijini watanufaika vipi na miradi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa kifungu Namba 95(1)(b) cha Sheria Sheria ya Madini Namba14 ya 2010, kabla ya kuanza utafutaji na uchimbaji wa madini, mmiliki wa leseni husika hutakiwa kupata kibali cha kumruhusu kuingia na kushughulika na utafutaji na uchimbaji wa madini kutoka kwenye Halmashauri za zilaya pamoja na mkoa. Kampuni za Cradle Resources Ltd/RECB Co. Ltd. ilipewa leseni tatu za uchimbaji wakati wa madini ya niobium. Leseni hizo ni ML 237, 238 na 239 zilitolewa mwaka 2006 zenye jumla ya ukubwa wa eneo la kilometa za mraba 22.06. Kwa sasa kampuni hiyo inakamilisha maandalizi kabla ya kuanza kwa ujenzi wa mgodi huo ifikapo mwaka 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa utafiti wa madini hayo ya niobium kampuni ya Cradle Resources Ltd/RECB Co. Ltd. inayomiliki leseni ilijitambulisha kwa uongozi wa mkoa wa Mbeya ikiwa ni pamoja na Gereza la Songwe ambapo mradi huo upo. Aidha, kampuni hiyo hivi sasa iko kwenye mazungumzo ya Gereza la Songwe pamoja na Wizara ya Mambo ya Ndani kuona namna ya kulihamisha Gereza hilo kabla ya kuanza uchimbaji kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa niobium utakuwa na faida kubwa kwa uchumi wa viwanda ikizingatiwa kwamba Serikali inajikita katika kufufua na kukuza viwanda nchini. Miongoni mwa matumizi ya madini haya ni kutumika kama alloy kwenye chuma kwa kuboresha uimara wake. Vilevile madini hayo hutumika katika kutengeneza mabomba mathalani mabomba ya kusafirisha gesi asilia. Matumizi mengine ya madini haya ni matengenezo ya sumaku pamoja na utengenezaji wa injini za ndege na rocket.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya Tanzania Geothermal Development Company Limited (TGDC) ni kampuni tanzu ya Shirika la Umeme nchini (TANESCO) ambayo imepewa dhamana ya kusimammia miradi ya kufua umeme wa joto ardhi katika Ziwa Ngozi lililopo kati ya Mbeya Vijijini. Mradi huu pia utazalisha umeme wa megawati 20 kwa kuanzia na baadaye utaweza kuzalisha megawati 100. Shughuli za utafiti wa mradi huu zilianza mwaka 2015 na zinatarajiwa kukamilika mwaka 2018 kwa kuzalisha umeme wa megawati 20. Mwezi Agosti 2015, kampuni ya TGDC iliendesha mafunzo kwa viongozi wa Mkoa, Wakuu wa Wilaya, watendaji wa Kata na vijiji wa Mbeya yaliyolenga kuwajengea uelewa wananchi hao. Aidha, mafunzo kama hayo yalitolewa kwa njia ya mihadara kwa wananchi wa Vijiji vya Ijombe, Mwakibete, Nanyara na Swaya vinavyozunguka maeneo yanayofanyiwa utafiti wa joto ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na joto ardhi kutumika kuzalisha umeme manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi wanaozunguka eneo la mradi ni pamoja na kutumia maji ya moto majumbani lakini pia katika vitalu vya kilimo. Kadhalika itatumika katika kufugia samaki, kukausha mazao, kujenga mabwawa ya kuogelea na kwa matumizi mengine ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla miradi ya uwekezaji hunufaisha wananchi wa eneo husika katika ukuaji wa shughuli za kiuchumi na ajira. Miradi hii miwili itakapotekelezwa wananchi wa Halmashauri ya Mbeya Vijijini, Rungwe, Mbeya pamoja na Watanzania wote watanufaika kwa kupata ajira, ushuru pamoja na tozo mbalimbali pamoja na huduma za jamii.
MHE. MOSHI S. KAKOSO aliuliza:-
Vijiji vingi katika Jimbo la Mpanda Vijijini havina huduma ya umeme.
Je, ni lini Serikali itapelekea huduma ya umeme katika vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Mpanda vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Miradi ya REA awamu ya kwanza nay a pili haikuhusisha Jimbo la Mpanda Vijijini. Katika kuhakikisha kwamba wananchi wa Mpanda wanapata umeme wa uhakika Serikali inatarajia sasa kuvipatia umeme vijiji 49 vya Mpanda Vijijini pamoja na Ofisi za Wilaya kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu unaotarajiwa kuanza mwezi Juni, mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika Jimbo la Mpanda Vijijini itahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovolt 0.4 yenye urefu wa kilometa 280. Lakini pia ufungaji wa transfoma 64 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,452. Gharama ya kazi hii ni shilingi bilioni 9.4.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Uholanzi kupitia Mradi wa ORIO itafunga mitambo mipya ya kuzalisha umeme wa megawatts 2.5 katika Mji wa Mpanda itakayowezesha maeneo mengi kupata umeme wa uhakika. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2016 na kukamilika mwezi Julai, 2017.
Kuwawezesha Wananchi Kupata Umeme wa Bei Nafuu
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Licha ya Serikali kupeleka umeme vijijini kwa kasi kupitia mradi wa REA, bado kuna changamoto za kuunganisha umeme kwa wananchi.
(a) Je, Serikali ina mpango gani kuwawezesha wananchi kupata umeme kwa bei nafuu?
(b) Nguzo za umeme zinasimikwa kwenye njia kuu tu; je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha nguzo hizi zinapelekwa kwenye vitongoji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuwezesha wananchi kupata umeme kwa gharama nafuu, Serikali kupitia mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini (REA) inaunganisha umeme kwa gharama ya shilingi 27,000 tu na hii ikiwa ni Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) imepunguza gharama za umeme kwa kuondoa gharama za malipo ya maombi ya kufungiwa umeme yaani shilingi 5,000 pamoja na malipo ya huduma ya kila mwezi (service charge) ambayo ni shilingi 5,520 kwa wateja wote wa majumbani; hatua hii imeanza tangu tarehe 1 Aprili, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kuwekeza zaidi katika uzalishaji wa umeme kwa kutumia vyanzo vya gesi asilia, joto-ardhi, jua, maji na makaa ya mawe pamoja na tungamotaka, ili kupunguza gharama za umeme zaidi.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, nguzo nyingi zimesimikwa kwenye njia kuu, hata hivyo katika Mpango wa REA Awamu ya Tatu utakaoanza bada ya bajeti yetu kupita mwezi Julai mwaka huu, maeneo mengi ya vitongoji yatafikiwa kwa kupewa huduma ya umeme, ili kurahisisha shughuli za uchumi za wananchi wa maeneo ya Kalenga.
MHE. FLATEI G. MASSAY: aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme katika maeneo ya Tarafa za Jimbo la Mbulu za Manetadu, Tumatu Arri, Masieda na Yayeda chini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inagharamia utekelezaji wa mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini (REA), kupitia mpango huu wa REA Vijijini (REF). Mradi huu unatekelezwa katika mikoa yote ya Tanzania Bara ikiwemo Mkoa wa Manyara. Mkandarasi, CC International Nigeria Limited, hivi sasa anaendelea na utekelezaji wa mradi huo katika Wilaya za Mkoa wa Manyara ikiwemo Wilaya ya Mbulu Vijijini. Utekelezaji wa mradi huu umefikia asilimia 84, ambapo tayari transformer zimeshafungwa na pia wateja 354 wameunganishiwa umeme katika Mkoa mzima wa Manyara.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu unategemea pia kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu 2016. Lengo kubwa la mradi huu ni kupeleka huduma za umeme kwa wananchi na hivyo kurahisisha shughuli za kiuchumi pamoja na kijamii. Tarafa za Manetatu, Masieda, Tumatiadi na Yaeda Chini zimejumuishwa katika Mpango wa Usambazaji wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu, utakaoanza mara baada ya bajeti ya mwaka huu 2016/2017.
Umeme ni muhimu sana kwa maisha bora ya wananchi, lakini wananchi wa Songea Mjini hawana uhakika wa umeme kutokana na kutegemea zaidi umeme wa jenereta na ule kidogo unaozalishwa na Shirika la Masista Chipole:-
(a) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa Gridi ya Taifa toka Njombe/Makambako?
(b) Je, Serikali inafahamu kuwa watu wengi wanashindwa kuja kuwekeza Songea kutokana na kukosa umeme wa uhakika?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Leonidas Tutubert Gama, Mbunge wa Songea Mjini, lenye sehemu a na b kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango wa kufikisha umeme wa Gridi ya Taifa mkoani Ruvuma kupitia mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa kilovoti 220 kutoka Makambako hadi Songea. Kazi za mradi huu na utekelezaji wake umeshaanza na zimegawanyika katika sehemu kuu mbili:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya kwanza inajumuisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 yenye urefu wa kilometa 250 kutoka Makambako hadi Songea. Kazi hii pia inahusisha pia upanuzi wa kituo cha kupooza umeme kutoka Makambako, lakini pia ujenzi wa vituo vipya vya kupooza umeme katika Mji wa Madaba pamoja na Mji wa Songea. Kazi hii inatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018 naitagharimu dola za Kimarekani milioni 34.68 lakini pia shilingi bilioni 15.41.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili inahusisha ujenzi wa njia ya kusambaza umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 900. Lakini pia wateja wa awali 22,700 katika vijiji 120 vya Wilaya ya Ludewa, Njombe Mjini, Njombe Vijijini, Wanging‟ombe katika Mkoa wa Njombe wataunganishiwa umeme. Kadhalika kazi hii itajumuisha pia katika wilaya za Mbinga, Namtumbo, Songea Mjini na Songea Vijijini katika Mkoa wa Ruvuma. Kazi hii inatarajiwa kukamilika mwezi Disemba 2017 na itangarimu dola za Marekani milioni 37.63 na shilingi bilioni 6.51.
Mheshimiwa Naibu Spika, upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Ruvuma umeimarika kwa siku za hivi karibuni. Na hii ni kutokana na kufunguliwa kwa vituo mbalimbali vya kuzalisha umeme, ikiwa ni pamoja na vituo vya umeme vya Donya (megawatt 0.5), Mbinga (megawatt 2.5), Namtumbo (megawatt 0.4) Songea (Megawatt 4.5) na Tulila (megawatt 5) vilivyofikisha jumla ya megawatt 12.4.
Mheshimiwa Naibu Spika, mahitaji ya juu ya umeme kwa Mji wa Songea ni megawatt 4.7, na uwezo wa uzalishaji ni megawatt 9.5, hivyo kuwa na ziada ya umeme wa megawatt 4.8. Ni matumaini ya Serikali kuwa kukamilika kwa
mradi wa njia ya kusafirisha umeme ya Makambako kwenda Songea kutamaliza kabisa tatizo la changamoto za umeme na kufufua fursa za uwekezaji katika Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla wake.
MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-
Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Malengo ya Dira ya Taifa 2025, inaeleza kwamba ifikapo mwaka 2025 Tanzania itakuwa na uchumi wa kati unaoongozwa na viwanda.
(a) Je, Serikali imeweka mkakati gani wa kuinua wananchi wa tabaka la kati (middle class) kuweza kujitegemea?
(b) Je, ni kampuni ngapi zilizowekeza nchini na Serikali ina hisa kiasi gani kwenye kampuni hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima, Mbunge wa Singida Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkakati Unganishi wa Maendeleo ya Viwanda yaani Integrated Industrial Development Strategy 2020 unahimiza ushiriki katika ujenzi wa uchumi wa viwanda ambapo malighafi zake zinapatikana hapa nchini. Mikakati mingine ni pamoja na mkakati wa pamba mpaka mavazi, mafuta yatokanayo na alizeti lakini ngozi bidhaa pamoja na ngozi yenyewe pamoja na mkakati wa mazao ya jamii ya kunde.
Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati hiyo ni utekelezaji wa mpango elekezi wa miaka 15 wa Dira ya Taifa ya Maendeleo mwaka 2025 unaolenga kutanzua vikwazo vya uchumi hapa nchini. Mpango wa pili una dhima ya kujenga uchumi wa viwanda ili kuleta mageuzi ya kiuchumi na maendeleo ya watu. Mpango wa tatu unalenga kuimarisha ubunifu na ushindani wa Kimataifa. Msukumo wa mipango hii ni kuhakikisha kuwa na rasilimali za fursa za nchi zinatumika vizuri katika uchumi wa viwanda vya kati hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Taarifa za Ofisi ya Msajili wa Hazina kuna jumla ya makampuni 61 yaliyowekeza katika sekta mbalimbali za uzalishaji na utoaji wa huduma hapa nchini. Ukitoa makampuni 21 ambayo Serikali inamiliki asilimia 100; lakini makampuni mengine manne Serikali inamiliki hisa asilimia 50, na makampuni meninge manne pia asilimia 50 pamoja na makampuni asilimia 32 yanayomilikiwa asilimia 50.
MHE. RIZIKI S. MNGWALI (K.n.y MHE. MAGDALENA H. SAKAYA) aliuliza:-
Wananchi wa Kitongoji cha Twende Pamoja, Kijiji cha Igwisi, Wilaya ya Kaliua wamekuwa wakipata athari kubwa za kiafya kutokana na milipuko ya baruti inayofanywa na Kampuni ya CHIKO, kupasua mawe na kokoto kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Kaliua mpaka Kigoma:-
(a) Kwa nini Serikali isiwalipe Wananchi hao stahiki zao ili waondoke sehemu hiyo na waende kuishi maeneo mengine ambayo ni salama?
(b) Kijiji cha Igwisi kinanufaikaje na Machimbo haya ya Mawe ambayo yapo kwenye eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya CHICO inatekeleza mradi wa ujenzi wa barabara wa kilometa 56 kuanzia Kaliua hadi Kazilambwa. Kipande hiki ni sehemu ya barabara kuu inayounganisha wilaya ya Kaliua, Mkoa wa Tabora pamoja na Mkoa wa Kigoma. Ili kupata madini ya ujenzi wa barabara, Kampuni ya CHICO inachimba mawe na kokoto katika leseni ya uchimbaji mdogo PML namba 001290CWTZ iliyopo katika Kijiji cha Igwisi iliyotolewa na Wizara ya Nishati na Madini tarehe 12 Aprili, 2013 kwa TANROADS Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya uchimbaji wa mawe na kokoto inahusisha ulipuaji wa baruti inayoweza kusababisha madhara katika maeneo ya jirani. Ili kuepusha madhara kwa wananchi wanaoishi maeneo hayo, tathmini hufanyika na kwa sasa tathmini ya wananchi 71 imefanyika na kati ya hao, wananchi 34 ni kwa ajili ya mazao na wananchi 37 ni kwa ajili ya makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya CHICO iliwapa fidia waathirika 71 jumla ya shilingi milioni 473.9 chini ya usimamizi wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia TANROADS.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Igwisi kinanufaika na Mradi huu ambapo kwa sasa eneo lao linapitika kwa kipindi cha muda mrefu bila kuwa na matatizo yoyote. Sababu nyingine ambazo zinachangia ni pamoja na kunufaika na uchimbaji huo kwa wannchi kuweza kufanya biashara katika maeneo hayo, lakini pia kwa Halmashauri kulipa service levy. Hivi sasa TANROADS inakusudia kulipa shilingi milioni 23 inachodaiwa kwa kipindi cha Aprili hadi Desemba, 2014.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza:-
Kampuni ya BG-EXXON MOBIL, OPHIR na washiriki wenzao wako tayari kuanza ujenzi wa LNGPlant.
(a) Je, ni nini kinachokwamisha kuanza kwa utekelezaji wa mpango huo?
(b) Je, ni hatua gani za makusudi zinachukuliwa ili kuharakisha utekelezaji wa mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kusindika Gesi Asilia (Liquefied Natural Gas – LNG) ulibuniwa mwaka 2014 kufuatiwa ugunduzi wa gesi asilia nchini ambao umetoka katika bahari ya kina kirefu. Mradi huo unatekelezwa katika na kampuni za kimataifa ya Statoil ya Norway, BG ya Uingereza, Exxon Mobil ya Marekani pamoja na Ophir ya Uingereza. Kampuni nyingine Pavilion ya nchini Singapore pamoja na shirika la TPDC ambalo ni la Serikali hapa nchini. Kutokana na umuhimu wa wa mradi huo katika kujenga uchumi wa gesi asilia nchini Serikali inachukua hatua za utekelezaji wa mradi kwa awamu tofauti. Lakini Serikali inachukua tahadhari muhimu sana katika kuandaa mradi huu.
Mheshimiwa Spika, napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa utekelezaji wa mradi huo unaendelea vizuri. Hatua zilizofikiwa kwa sasa ni pamoja na kupata eneo la LNG litakalojengwa kwa umbali wa kilometa 2,000 na katika eneo lingine ambalo litakamilika mpaka 2020.
Mradi huu unatekelezwa kama nilivyosema na TPDC ambapo kufikia mwaka 2015 Serikali ilikabidhi TPDC hatimiliki ya eneo ambalo kwa sasa tafiti mbalimbali za kihandisi, kijiolojia, kimazingira na kijamii zinaendelea kufanyika.
Mheshimiwa Spika, maandalizi ya mikataba mbalimbali yameanza baada ya Serikali kukamilisha uundaji wa timu ya kufanya majadiliano (government negotiating team). Majadiliano kati ya government negotiationteam yameanza na yatakamilika mwezi Septemba mwaka huu. Mahojiano hayo pamoja na mambo mengine yanafanya pia ifikapo mwaka 2020 kukamilika kwa ufasaha kabisa. Aidha, Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini hukutana na wawekezaji hao kila baada ya miezi mitatu ili kutathmini maendeleo ya utekelezaji wa mradi huu.
MHE. OMARY A. BADWEL aliuliza:-
Wananchi wanaoishi kwenye maeneo yenye rasilimali mawe, mchanga na maji inapotokea wakandarasi wanachukua rasilimali hizo au mojawapo kwa ajili ya ujenzi huchukua bure au kwa malipo kidogo na hivyo kuwakosesha wananchi haki ya kunufaika na rasilimali hizo; hali hii ni tofauti na maeneo yenye madini ambapo wananchi hunufaika na uwepo wake:-
Je, Serikali haioni haja ya kuweka bei elekezi kwa wakandarasi wanaohitaji mawe, mchanga au maji ili wananchi wanaoishi maeneo yenye rasilimali hizo waweze kunufaika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omary Ahmad Badwel, Mbunge wa Bahi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na kanuni zake inamtaka kila mmiliki wa eneo la kuchimba madini amiliki leseni halali kutoka Wizara ya Nishati na Madini, hata hivyo leseni katika maeneo ya uchimbaji wa madini ya viwanda na ujenzi yanatakiwa pia kupata leseni bila kuchimba kiholela. Wakandarasi wanaofanya kazi ya ujenzi hulazimika pia kupata leseni za kuchimba madini ya ujenzi na kulipa mrabaha pamoja na ada nyingine kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Spika, kwa wakandarasi wasiokuwa na leseni za uchimbaji hununua madini ya ujenzi kwa wananchi wanaochimba na pia kufanya shughuli za ujenzi, pamoja na hayo, Wizara kwa kushirikiana na Wakala wa Ukaguzi wa Madini (TMA) hutoa matangazo kwenye Ofisi za Madini za Kanda na Maafisa Madini Wakazi yakionesha bei ya soko ya ndani ya ujenzi.
Mheshimiwa Spika, wachimbaji wa madini ya ujenzi wanaweza kuwasiliana na ofisi ya madini kupata mwongozo wa bei ya soko kwa sasa ili kupata ufahamu wa bei halisi ya mazao hayo.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE aliuliza:-
Je, ni aina gani ya madini yanapatikana ndani ya Wilaya ya Kalambo kulingana na tafiti ambazo zimekwishafanywa na Serikali?
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Sinkamba Kandege, Mbunge wa Kalambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na tafiti za awali zilizofanywa na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) pamoja na taarifa kutoka kwa wawekezaji wanaomiliki leseni katika maeneo ya Kalambo, madini yanayopatikana ni pamoja na madini ya chuma, dhahabu, galena kwa maana ya lead, shaba pamoja na madini ya ujenzi. Hata hivyo, GST wanaendelea kufanya utafiti katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wilaya ya Kalambo ili kubaini kama kuna madini mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nitumie nafasi hii kuwaomba wananchi wenye nia ya kupata taarifa kuhusu rasilimali za madini yaliyopo katika maeneo hayo, wafike katika ofisi zetu za madini pamoja na Wakala wake. Aidha, taarifa hizo zinapatikana kwenye tovuti ya Wizara, tovuti ya GST pamoja na machapisho mbalimbali ambayo yapo katika Ofisi zetu za madini.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza:-
Dhahabu ni kati ya madini yanayozalishwa na wachimbaji wadogo wadogo Mkoani Katavi; na kumekuwepo na suala la asilimia hafifu ya dhahabu ya Mpanda Kati ya 60% hadi 90%. Uhafifu huu ulitokana na ukweli kwamba sehemu ya asilimia ni madini mengine kama fedha, shaba na kadhalika, lakini katika mauzo wachimbaji wamekuwa wakilipwa thamani ya dhahabu tu.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwawezesha wachimbaji hawa kwa kuwapatia teknolojia sahihi ya kutofautisha dhahabu, shaba na fedha ili kuongeza thamani na pato halisi kwa wachimbaji hao na kuinua Pato la Taifa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa, mbali na dhahabu (gold ore) katika maeneo ya Mpanda huwa na madini mengine kama vile fedha, shaba pamoja na madini ya risasi. Kwa upande wa wachimbaji wadogo wa dhahabu nchini, kiwango cha uchenjuaji wa dhahabu huwezesha kuzalisha dhahabu kwa wastani wa asilimia 60 tu. Sababu kubwa ni pamoja na mitambo duni ya uchenjuaji inayotumika; kuanza uzalishaji kabla ya kufanya utafiti wa kujua aina ya mitambo inayotumika, lakini pia kiwango duni cha usagaji mbale.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona umuhimu sasa wa kuwawezesha wachimbaji wadogo kwa kuwapatia teknolojia sahihi ya kutofautisha dhahabu, shaba na fedha kwa ajili ya mafunzo. Kuanzia mwezi Septemba, 2016, Serikali kupitia Wizara yangu itaanza kujenga vituo vya mfano pamoja na kutoa mafunzo ya uchenjuaji madini hususan dhahabu katika Mikoa ya Geita, Katavi pamoja na Mara.
Kadhalika madini ya chokaa katika Mkoa wa Tanga, madini ya bati katika Mkoa wa Kagera na madini ya chumvi katika Mkoa wa Lindi ikiwa ni pamoja na madini ya vito katika Mkoa wa Ruvuma. Vituo hivi vitasaidia sana kuongeza viwango vya uchenjuaji madini hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sasa pia niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuwashauri wachimbaji wadogo katika maeneo yao kutumia taasisi zetu za Serikali ikiwa ni pamoja na STAMICO ambalo hushughulikia masuala ya wachimbaji wadogo, Chuo cha Madini Dodoma, Vyuo Vikuu vya Dodoma na Dar es Salaam na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) ili kuwafanyia utafiti na kuwashauri mambo yanayofaa kwa ajili ya uchimbaji na uchenjuaji wa tija.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-
Katika Wilaya ya Tunduru iko miradi mingi ya REA ambayo kampuni mbili zimepewa kazi hiyo lakini wakandarasi wanasuasua kukamilisha miradi hiyo na muda wake umeisha kwa kigezo cha kutolipwa:-
Je, ni lini Serikali itatoa pesa kukamilisha miradi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza mradi kabambe wa REA Awamu ya II katika Wilaya ya Tunduru na kazi hii imeshaanza na inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi huu, mwaka 2016. Kazi ya kupeleka umeme katika Wilaya ya Tunduru inaunganisha pia kazi ya ujenzi wa njia ya umeme Msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 293.2, ujenzi wa njia ya umeme Msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 77.1 lakini pia ufungaji wa transfoma 38 zenye ukubwa mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi hizo, kazi nyingine inayofanyika ni kuwaunganishia umeme wateja wa awali 3,330 lakini pia mradi umekamilika kwa asilimia 79 ambapo ujenzi wa laini kubwa umekamilika kwa asilimia 83, laini ndogo asilimia 74, transfoma saba zimeshafungwa na wateja 182 wameshaunganishiwa umeme. Gharama ya mradi wa Mkoa wa Ruvuma ikiwemo Wilaya ya Tunduru ni shilingi bilioni 32.56. Kiasi ambacho mkandarasi hadi sasa ameshalipwa ni shilingi bilioni 27.22 ambayo ni sawa na asilimia 83.6. REA wanasubiri kupata uthibitisho kutoka kwa mkandarasi kuhusu madai ya shilingi bilioni 3.19 ili aweze kulipwa mara tu baada ya uthibitisho huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Tunduru vijiji vinne vya Jimbo la Tunduru Kusini ambavyo ni Azimio, Chiwana, Mbesa na Mkandu, vimeunganishiwa miundombinu ya umeme ambayo inafanyiwa marekebisho na matayarisho kwa ajili ya kuwashwa. Hivi sasa mkandarasi anaendelea kufunga transfoma na mita za Luku katika vijiji vingine 34 ambavyo vimesalia katika Wilaya ya Tunduru ili viweze kupatiwa umeme ifikapo tarehe 30 Juni, 2016.
MHE. CECIL D. MWAMBE (K.n.y. MHE. LATHIFAH H. CHANDE) aliuliza:-
Mji wa Liwale umebakia kuwa ni Wilaya pekee ya Mkoa wa Lindi ambayo haijanufaika na umeme wa uhakika wa gesi asilia. Umeme unaotumika ni wa jenereta mbili za diseli za kW 800:-
Je, ni kwa nini Serikali isitenge fedha ili kuiunganisha Wilaya nzima ya Liwale na umeme wa gesi asilia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lathifah Hassan Chande, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Liwale unapata umeme kutoka Kituo cha Kuzalisha umeme kwa kutumia mafuta kilichopo Liwale. Hata hivyo, gharama za uendeshaji wa mitambo hiyo inayotumia nishati ya mafuta ni kubwa sana. Kutokana na hali hiyo, Serikali imeanza kutekeleza ujenzi wa njia ya umeme itakayounganisha Wilaya ya Liwale na Wilaya ya Nachingwea ambayo kwa sasa inatumia umeme kutoka Kituo cha Kuzalisha umeme cha Gesi Asilia kilichopo Mtwara.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua iliyofikiwa katika mpango huo ni ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 14.5 kutoka Nachingwea hadi Kijiji cha Luponda, ambapo ni kilometa 73 kutoka Liwale hadi Kijiji cha Nangano. Kazi hiyo, ilianza mwezi Agosti mwaka 2014 na inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Septemba mwaka huu. Gharama za mradi huu ni shilingi bilioni 3.5 na kwa kweli, inaendelea vizuri. Hata hivyo, sehemu iliyobaki ya kilometa 45 kati ya Luponda na Nangano inatarajiwa kukamilika kupitia utekelezaji wa Mpango wa REA awamu ya tatu.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:-
Serikali ya Awamu ya Tano inakusudia kuifanya Tanzania kuwa ni nchi yenye uchumi wa viwanda, hivyo inahitaji kuwa na uzalishaji wa umeme wa uhakika. Hata hivyo, umeme unaozalishwa kwa kutumia gesi asilia pale Somanga Fungu unakatika mara kwa mara na kusababisha adha kubwa kwa watumiaji:-
Je, Serikali inaweza kutuambia wananchi kiini hasa cha ukatikaji huo wa kila siku wa umeme unaozalishwa kutokana na gesi ya Songosongo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Somanga Fungu kilianza kuzalisha umeme mwaka 2010. Kituo hicho kina jumla ya mitambo mitatu ya kuzalisha umeme kiasi cha Megawati 7.5 kwa kutumia gesi asilia. Umeme unaofuliwa kutoka Somanga Fungu unatumika katika Wilaya za Kibiti, Kilwa pamoja na Rufiji. Kwa sasa mtambo mmoja wenye uwezo wa kuzalisha umeme Megawati 2.5 pia haufanyi kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kukatika kwa umeme ni kweli kabisa kumekuwa na kukatika kwa umeme katika Wilaya za Kilwa, Kibiti pamoja na Rufiji kunakosababishwa na hitilafu katika mitambo ya kuzalisha umeme pamoja na miundombinu ya kusambaza umeme. Ili kukabiliana na changamoto hiyo tunaimarisha upatikanaji wa umeme katika wilaya hizo na Serikali kupitia TANESCO imeanza ukarabati sasa, ambao ni overhaul kabisa wa mitambo miwili ya uwezo wa kuzalisha umeme wa jumla ya megawati tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunafanya ukarabati na kufunga mtambo mwingine kwenye mtambo unaozalisha megawati mbili na kufanya sasa jumla ya gharama za marekebisho pamoja na kufunga mtambo kufikia bilioni tano. TANESCO inaendelea na ukaguzi, inafanya usafishaji na ukarabati wa mitambo hiyo ili kuwahakikisha wananchi wa maeneo hayo wanapata umeme wa uhakika.
MHE. VICKY P. KAMATA (K.n.y MHE. CONSTATINE J. KANYASU) aliuliza:-
Mgodi wa GGM - Geita umepewa eneo la ukubwa wa kilometa za mraba 192 kwa ajili ya kuchimba dhahabu wakati wananchi wamenyang‘anywa maeneo yao.
Je, ni lini maeneo waliyonyang‘anywa wananchi yatarudishwa kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constatine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini lililoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Vicky Kamata Likwelile, Mbunge wa Geita Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni ya Geita Gold Mine Limited yaani GGM inamiliki leseni ya uchimbaji mkubwa wa madini kupitia leseni namba SML45/99 yenye ukubwa wa kilometa za mraba 196.27 iliyopewa kwa mujibu wa Sheria ya Madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maeneo ambayo mgodi GGM waliyahitaji ndani ya leseni yao kwa ajili ya uchimbaji walifanya mazungumzo na wamiliki wa maeneo hayo na kulipa fidia kwa mujibu wa Sheria Namba Nne ya Madini ya 2010 pamoja na Sheria Namba Tano ya Ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaomiliki ardhi ndani ya leseni ya GGM kwa ajili ya makazi na shughuli mbalimbali ambazo siyo shughuli za uchimbaji wanaendelea na shuhguli zao kama kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo baadhi ya wamiliki wa leseni za uchimbaji mdogo ambao hawakufikia makubaliano na mgodi wa GGM bado wanamiliki leseni zao za uchimbaji mdogo. Baadhi ya wananchi hao ni pamoja na Bwana Jumanne Mtafuni mwenye leseni ya uchimbaji mdogo PML0001044 pamoja na Bwana Leonard John Chipaka mwenye leseni namba PML0001331 wachimbaji wadogo hawa wanaendelea na shughuli za uchimbaji katika maeneo yao kama kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na maelezo haya sasa wananchi ambao wamepisha maeneo baadhi yao walilipwa fidia kwa mujibu wa taratibu za nchi hii.
MHE. DKT. MARY M. NAGU aliuliza:-
Katika Mwaka wa Fedha 2014.15 Serikali iliunganisha umeme kwenye vijiji vinne tu katika Wilaya ya Hanang; hata hivyo, Mwaka 2015/2016, Serikali iliahidi kuunganisha umeme vijiji vingine 19:-
Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi hiyo, ambayo inasubiriwa kwa hamu na wananchi wa Wilaya ya Hanang?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mary Michael Nagu, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi kabambe wa REA awamu ya pili katika Jimbo la Hanang umevipatia umeme vijiji saba na shule za sekondari tatu kati ya Kata 19 zilizokuwa zimeombewa umeme katika awamu ya pili. Hata hivyo, vijiji vilivyobaki Hanang, vyote alivyoomba Mheshimiwa Nagu vitapatiwa umeme kwenye REA awamu ya tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji 44 alivyoomba Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu pamoja na shule za sekondari, vituo vya afya pamoja na zahanati vinatarajiwa kupatiwa umeme kwenye REA awamu ya tatu kama alivyoomba. Kazi ya kupeleka umeme katika maeneo hayo inajumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 262.4, ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 169.8, lakini pia ufungaji wa transformer 54.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi hizo, kazi nyingine itakayofanyika ni kuwaunganishia umeme wateja wa awali wapatao 11,449. Kazi ya kupeleka umeme katika Jimbo la Hanang itagharimu Shilingi bilioni 15.8.
MHE. OMARY T. MGUMBA (K.n.y. MHE. DKT. HADJI H. MPONDA) aliuliza:-
Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini iliahidi kupeleka huduma za umeme katika Hospitali ya Lugala ambayo ni hospitali pekee na tegemezi katika Wilaya nzima ya Malinyi. Katika kutekeleza agizo hili, Oktoba, 2014, TANESCO Mkoa wa Morogoro ilitengewa fedha kwa kuanza ujenzi huo wa 33KV, HT line ya kilometa 3.5 na kuunganisha umeme katika hospitali hiyo na Kijiji cha Lugala lakini hadi leo agizo hilo halijatekelezwa:-
(a) Je, sababu gani zilifanya mradi huo usitekelezeke licha ya kutengewa fedha?
(b) Je, ni lini hospitali hiyo muhimu kwa wakazi wa Wilaya ya Malinyi itapatiwa huduma ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hadji Hussein Mponda, Mbunge wa Malinyi, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa kupeleka umeme katika Hospitali ya Lugala, Wilayani Malinyi haukuweza kutekelezwa kwa sababu fedha iliyotarajiwa kutengwa kutoka kwenye bajeti ya TANESCO ya mwaka 2014/2015 haikutengwa kutokana na ufinyu wa bajeti ya TANESCO. Hata hivyo, Hospitali hiyo pamoja na Kijiji cha Lugala vitapatiwa umeme mwaka huu kupitia bajeti ya TANESCO. Kazi hii itajumuisha sasa ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa tatu, ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa tano pamoja na ufungaji wa transfoma mbili za kVA 100 na kVA 200.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na utekelezaji huo, kazi nyingine itakayofanyika ni kuwaunganishia umeme wateja wapatao 116 katika maeneo hayo. Kazi hii inatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Juni, 2016 na itakamilika mwezi Julai, 2016 kwa gharama ya shilingi milioni 329.27.
MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-
Ileje inatambuliwa kuwa ndiyo inayokalia ardhi inayotoa makaa ya mawe yanayoitwa Kiwira Coal Mine lakini mgodi huu haujawanufaisha wananchi wa Ileje kwa muda wote uliokuwa ukifanya kazi mpaka ulipofungwa:-
(a) Je, ni lini mwekezaji mpya ataanza uzalishaji tena kwenye mgodi?
(b) Je, ni lini tutakaa na mwekezaji huyu kama halmashauri ili kufahamiana?
(c) Je, ni lini tutapata mwekezaji wa kutumia makaa haya kuzalisha umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mbunge wa Ileje, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira (Kiwira Coal Mine) unamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100 na kusimamiwa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO). STAMICO wanamiliki leseni maalum ya uchimbaji mkubwa yenye usajili namba SML.233/2005 itakayodumu kwa miaka 25. STAMICO wanatarajia kuzalisha umeme megawati 200 kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 500.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka huu wa fedha 2015/2016, shirika liliweza kukamilisha Rasimu ya mwisho ya Upembuzi wa Mazingira kwa mradi wa Open Cast, wa kuzalisha megawati 200. Hata hivyo, mradi huo, pia unahusisha usafirishaji wa msongo wa kilovoti 400 yenye urefu wa kilometa 100 kutoka Kiwira hadi Mwakibete, Mbeya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa STAMICO ipo katika hatua za kumtafuta mzabuni kuendeleza mgodi huo lakini taratibu za kumpata mwekezaji zinaendeleza na zinatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2016. Mara tu mwekezaji atakapopatikana, atatambulishwa kwa viongozi wa Halmashauri za Rungwe na Ileje ambazo sehemu ya mradi huu unapatikana.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Mradi wa REA unaendelea kutekelezwa katika vijiji 24 katika Jimbo la Sikonge lakini mradi huo ulisimamia kwa muda mrefu ambapo baadhi ya maeneo nguzo zilizoachwa barabarani zimeanza kufukiwa na mchanga kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha:-
(a) Je, Serikali itakamilisha lini mradi huo kwa Awamu ya Kwanza na Pili?
(b) Je, Awamu ya Tatu ya utekelezaji wa mradi huo itahusisha vijiji gani katika Wilaya ya Sikonge na ni lini utaanza na kukamilika?
(c) Je, Serikali haioni umuhimu wa kufikisha umeme wa REA kwenye mitambo ya kusukuma maji ya Ityatya, Uluwa, Makazi, Igumila, Majojolo na Kiyombo ili kupunguza gharama za dizeli ambazo zimekuwa zikiathiri upatikanaji wa maji kutokana na gharama kubwa za uendeshaji mitambo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Sikonge ilijumuishwa kwenye REA Awamu ya II ambayo inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2016. Kazi ya kupeleka umeme Wilaya ya Sikonge inajumuisha pia ujenzi wa umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 166.44 lakini pia ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 58.06. Kazi hii pia itajumuisha ufungaji wa transfoma 28 za ukubwa mbalimbali pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,704.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huo ambao unatekelezwa kupitia mkandarasi CHICCO umekamilika kwa asilimia 88 hadi sasa. Ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 umekamilika kwa asilimia 86 na ujenzi wa msongo wa kilovoti 0.4 umekamilika kwa asilimia 89.3, lakini pia transfoma 15 zimeshafungwa na wateja 228 wameunganishiwa umeme. Kazi hii imegharimu shilingi bilioni 6.42.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini REA, Awamu ya III, unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2016. Mradi wa REA Awamu ya III unakusudia kupeleka umeme katika vijiji vyote vilivyobaki vya Mheshimiwa Mbunge pamoja na shule, zahanati na vituo vya afya. Kadhalika, kazi hii itajumuisha kupeleka umeme kwa wananchi wapatao 1,510. Kazi hii inagharimu pia jumla ya shilingi milioni 4.33.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye pampu za kusukuma maji alizozitaja Mheshimiwa Mbunge za Ityatya, Makazi na Uluwa itafanywa na REA Awamu ya III. Kazi ya kupeleka umeme kwa vijiji na pampu hizi itahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa tisa, lakini pia ufungaji wa transfoma tatu pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 141. Kazi hii itagharimu shilingi milioni 317.14. Aidha, pampu za maji za Igumumila, Kiyombo na Magolo zitafanyiwa tathmini kubaini mahitaji yake ili na zenyewe ziweze kupatiwa umeme haraka iwezekanavyo.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA aliuliza:-
Mradi wa REA umekuwa ukisuasua katika maeneo ya vijiji vya Rufiji hususan Tarafa ya Mkongo, Kata za Mkongo, Ngorongo, Kipungila na Kata ya Mwaseni na Ngarambe.
Je, ni lini mradi huo utakamilika katika hatua inayofuata?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa REA Awamu ya III ambao utafuata sasa na ambao unatekelezwa baada ya Mradi wa REA Awamu ya II katika Wilaya ya Rufiji unatekelezwa na Mkandarasi MBH Power Ltd. Wigo wa kazi katika Wilaya hii unahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 217.34; ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 04 yenye urefu wa kilometa 64.18; ufungaji wa transfoma 40 na kuwaunganishia umeme wateja wapatao 2,059.
Mradi umekamilika kwa asilimia 76 zikijumuisha ujenzi wa kilometa 201 za msongo wa kilovoti 33; ujenzi wa kilometa 23 za msongo wa kilovoti 0.4; kufunga transfoma 17 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 256. Mradi huu hadi kukamilika utagharimu shilingi bilioni 7.74.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata za Mkongo, Ngorongo, Kipungila, Mwaseni na Ngarambe ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 94 kutoka Ikwiriri hadi Mloka umekamilika kwa asilimia 90. Ujenzi wa njia ya usambazaji umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu kilomita 24.64 imekamilika kwa asilimia 45 na ufungaji wa transfoma 14 unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Septemba 2016. Kazi hizi zinatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Oktoba, 2016. Kazi hii hadi kukamilika itagharimu shilingi bilioni 3.15.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA (K.n.y. MHE. MBARAKA K. DAU) aliuliza:-
Tafiti nyingi za mafuta na gesi zimefanywa na kampuni mbalimbali Kisiwani Mafia.
Je, ni nini matokeo ya tafiti hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau, Mbunge wa Mafia kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni za BP na Maurel Et Prome kwa nyakati tofauti zilifanya tafiti katika eneo la Kisiwa cha Mafia kukusanya takwimu za mitetemo kwa eneo lenye ukubwa wa kilometa za mraba 380 na 3D, lakini pia na katika Mkuza kwa kilometa 205 za 2D kuchimba visima viwili. Kati ya mwaka 1952 na 1956 kampuni ya BP ilichimba kisima cha Mafia -1 na kati ya mwaka 2006 hadi 2010 Kampuni ya Maurel Et Prome ilichimba kisima cha Mafia Deep -1. Baada ya tathmini ya takwimu hizo kufanyika matokeo yalionesha eneo hilo lina viashiria vya uwepo wa mafuta pamoja na gesi asilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa leseni ya kitalu hicho imekwisha muda wake hivyo eneo hilo liko wazi kwa kampuni yoyote kuomba na kuendelea kazi ya uchimbaji mafuta na gesi katika eneo hilo.
MHE. WILLY Q. QAMBALO aliuliza:-
Katika kupunguza tatizo sugu la maji Wilaya ya Karatu baadhi ya vijiji kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wamechimba visima virefu 12 katika maeneo ya Basodawish, Endabash, Rhotia Kainani, Endamarariek, Getamock, Karatu Mjini, Gongali na kadhalika, visima hivyo vinaendeshwa kwa kutumia mashine za dizeli jambo ambalo linasababisha gharama kubwa za uendeshaji.
Je, Serikali itawasidia lini wananchi hao kwa kuwaunganisha na nishati ya umeme katika visima hivyo ili kupunguza gharama za uendeshaji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kabla sijatoa maelezo ya kuhusiana na swali la Mheshimiwa Mbunge niombe kwa ridhaa ya kiti chako Mheshimiwa Naibu Spika pamoja na Waheshimiwa Wabunge nichukue nafasi moja ya kuwapa pole sana wananchi wa Jimbo langu Chato kwa kupata msiba mkubwa ambao umetokea juzi baada mvua kubwa kunyesha kwenye Jimbo la Chato na kusababisha wananchi wawili kupoteza maisha yao na wananchi wengine 17 kujeruhiwa vibaya sana. Kwa heshima ya kiti chako basi kwa niaba ya Waheshimiwa Wabunge tujumuike na wananchi wa Chato katika kuomboleza msiba huo mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sasa kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Willy Qulwi Qambalo, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya kufikisha umeme katika maeneo yote nchini ikiwa ni pamoja na maeneo ya Wilaya ya Karatu. Kipaumbele katika kutekeleza miradi ya umeme ni pamoja na kufikisha umeme katika miundombinu inayotoa huduma za kijamii ikijumuisha visima vya maji, shule, zahanati, makanisa, misikiti na maeneo ya biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vya Basodawish, Endabash, Endamarariek, Getamock pamoja na maeneo ya Karatu Mjini yamefikishiwa huduma ya umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Pili. Hata hivyo huduma ya umeme haijafikishwa katika visima vya maji vilivyopo katika maeneo niliyoyataja. Kazi ya kupeleka umeme katika visima hivyo itahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 12.6 na ufugaji wa transfoma tano za KVA 100 kila moja. Gharama ya kazi hizi ni shilingi milioni 467.16. Visima vyote katika vijiji vilivyotajwa hapo juu vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika kisima kilichopo Karatu Mjini inahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 1.2 na kufunga transfoma ya ukubwa wa KVA100. Gharama ya kazi hii ni shilingi milioni 33.81 kazi imepangwa kutekelezwa kupitia bajeti ya TANESCO ya mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha vijiji vya Gongali, Gyekrum Lambo, Kainam Rhotia na Kambi Faru vitapata umeme kupitia mradi wa REA awamu ya Tatu. Kazi za kuvipatia umeme vijiji hivi itahusisha pia upelekaji umeme kwenye visima vya maji vilivyopo katika vijiji hivyo.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA (K.n.y. MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA) aliuliza:-
Sheria ya madini inawataka wachimbaji wakubwa kama vile GGM - Geita, kila miaka mitano wamege sehemu ya maeneo na kuyarudisha kwa wananchi.
(a) Je, ni lini Serikali itawarudishia wananchi maeneo ya Sami na Nyamatagata yaliyoombwa na wananchi kupitia vikao vyote hadi Mkoani?
(b) Je, ni lini eneo la STAMICO - Nyarugusu litafanywa kuwa la wachimbaji wadogo wadogo kama ambavyo Mheshimiwa Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alivyokwisha tamka mara mbili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, lililoulizwa na Mheshimiwa Bukwimba Mbunge wa Geita Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya maeneo ya Sami pamoja na Nyamatagata yamo ndani ya leseni ya uchimbaji mkubwa wa madini ya dhahabu ya kampuni ya Geita Gold Mine (GGM) kupitia leseni namba SML 45/99. Hata hivyo Serikali inaendelea na mazungumzo na mgodi huo ili kampuni hiyo iweze kuachia baadhi ya maeneo yasiyohitajika kwa ajili ya kuwamilikisha wachimbaji wadogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la STAMICO na Nyarugusu lipo kitongoji za Buziba lina leseni ya utafutaji Na. PL 6545/2010 inayomilikiwa kwa ubia wa asilimia 45 na 55 kati ya STAMICO na kampuni ya TANZAM 2001, eseni hii itaisha muda wake tarehe 11 Julai 2018. Kwa kuwa eneo la Nyarugusu bado linamilikiwa na STAMICO pamoja na mbia wake ambapo Serikali pia ni mmiliki, Serikali inafanya mazungumzo na wamiliki hawa ili eneo hilo liachiwe sasa kwa ajili ya kumilikishwa wachimbaji wadogo wa eneo hilo.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Kata za Mtambula, Idunda, Maduma, Kiyowela na Idete ili wananchi waweze kufaidika na huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ridhaa ya kiti chako, niombe dakika moja niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kabla sijajielekeza kwenye kujibu maswali yaliyoulizwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge jinsi ambavyo walijitoa kwenye msiba mzito wa mama yangu uliotokea wiki tatu zilizopita, nawashukuru sana na ningependa kwa ruhusa yako kwa uwakilishi wa Waheshimiwa Wabunge niwatambue wachache walioweza kufanikiwa kufika Chato kwa ajili ya msiba, lakini nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa ridhaa hiyo. Baada ya kusema hayo Mungu awabariki sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na madini, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya kufikisha umeme nchi nzima ikiwa ni pamoja na maeneo ya vijiji vya Mufindi Kusini. Vijiji vya Kata ya Idete, Idunda, Kiyowela, Maduma pamoja na Mtambula vitapatiwa umeme kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu unaoanza Disemba mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo nilivyovitaja vya Wilaya ya Mufindi itahusisha itahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolt 33 yenye urefu wa kilometa 242, ujenzi wa njia ya msongo wa kilovolt 0.4 yanye urefu wa kilometa 81, ufungaji wa transfomer 24 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 3,533. Kazi inatarajiwa kuanza mwezi huu wa Disemba, 2016 na kukamilika katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 11.92.
MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:-
Serikali imekuwa na ahadi nyingi, nzuri za kutekeleza katika kusambaza umeme kwenye maeneo mengi ya nchi yetu.
(a) Katika Wilaya ya Nyang‟hwale ni vijiji vitatu tu vya Nyang‟hwale, Nyarubele, Busegwa na Makao Makuu ya Wilaya ambavyo vina umeme; je, katika bajeti ijayo ni vijiji vingapi vya Jimbo la Nyang‟hwale vitapatiwa umeme?
(b) Je, kwa nini nguzo haziletwi Kharumwa wakati wateja wengi tayari wamefanya wiring kwenye nyumba zao?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyang‟hwale lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya vijiji 61 katika jimbo la Nyang‟hwale vitapatiwa umeme katika utakekezaji wa mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu. Kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovolt 33 yenye urefu wa kilometa 50, ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovolt 0.4 yenye urefu wa kilometa 372 na ufungaji wa transformer 24 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 3,578. Kazi hizi zitaanza mwezi Disemba mwaka huu na kukamilika mwaka wa fedha 2019/2020. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 6.23.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Kharumwa ambacho ni makao makuu ya Wilaya ya Nyang‟hwale tayari kimepatiwa umeme na kazi ya kupeleka nguzo inaendelea. Hata hivyo TANESCO inakamilisha kazi za kuunganishia umeme wateja wapya wa Kharumwa kadri maombi yatavyofikiwa. Mpaka mwisho wa mwezi wa Disemba mwaka huu vijiji vya Kharumwa vitakuwa vimepata umeme.
MHE. DEVOTHA M. MINJA (K.n.y MHE. RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:-
Tatizo la umeme katika Mkoa wa Katavi hususan Wilaya ya Mpanda Mjini limekuwa kero kwa wananchi; tatizo hili linafanya maendeleo kuwa duni katika Manispaa ya Mpanda:-
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuachana na matumizi ya jenereta ambalo ni bovu linalosababisha ukosefu wa umeme kila mara?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua kero hii ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutekeleza ujenzi wa Mradi wa Umeme wa Gridi ya Taifa inayounganisha Mikoa ya Rukwa, Katavi pamoja na Kigoma. Ujenzi wa mradi huo utasaidia mikoa hiyo kuondokana na matumizi ya mitambo ya mafuta pia na gharama kubwa. Kwa maana hiyo ujenzi huo unahusisha njia ya umeme msongo wa kilovolti 400; ambao pia ambao pia wameanza kuunganisha katika mikoa Mbeya - Sumbawanga - Mpanda - Kigoma hadi Nyakanzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kuhuisha upembuzi yakinifu wa mradi kutoka kilovoti 220 za awali na kuwa kilovolti 400 zinazoendelea hivi sasa inaendelea. Awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi (Mbeya - Sumbawanga) itakamilika mwaka, 2018 na awamu zote tatu za mradi zinatarajiwa kukamilika mwaka 2022; gharama za mradi huu zinakadiriwa kuwa dola za Marekani milioni 664.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu utakapokamilika utaupatia umeme wa uhakika Mji wa Mpanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa ujenzi wa umeme wa Gridi ya Taifa unaendelea, Serikali kupitia TANESCO imeanza ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia jenereta mbili zenye uwezo wa kuzalisha umeme wa megawati 1.25; kila moja katika Mji wa Mpanda kupitia mradi wa ORIO. Mradi huu unafadhiliwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Uholanzi kwa gharama ya shilingi bilioni 12.21. Kazi za ujenzi wa kituo hicho zimeanza mwezi Oktoba, 2016 na zitakamilika mwezi Julai, 2017.
MHE. MARTHA J. UMBULLA aliuliza:-
Pamoja na juhudi za Serikali kupeleka huduma za umeme vijijiji vya Wilaya ya Kiteto hasa Kata za Lengatei, Kijungu, Magungu, Songambele, Ndedo na Makame, hawajafikiwa kabisa na utaratibu huu wa REA.
Je, Serikali itapeleka lini umeme katika vijiji vilivyotajwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vya kata za Lengetai, Kijungu pamoja na Magungu, kama ambavyo amerekebisha Mheshimiwa Mbunge, pamoja na Songambele, Ndedo na Makame vitapatiwa umeme kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu unaoanza kutekelezwa mwezi Disemba, mwaka huu. Ujenzi wa mradi huu utaanza Disemba kama nilivyosema mwaka huu na utakamilika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Aidha, vijiji vya kata za Lengatei vikiwemo Ilala, Kijungu, Lesoit pamoja na kijiji cha Magomeni pia vitapatiwa umeme kupitia mradi huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme kwenye Wilaya ya Kiteto itahusisha ujenzi wa njia ya msongo wa kilovolti 33 yenye urefu wa kilometa 810. Ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovolti 0.4 yenye urefu wa kilometa 1,725 ufungaji wa transfoma 343 za ukubwa mbalimbali, lakini pia kuwaunganishia wateja wa awali umeme 10,800. Kazi hizi zitaanza mwezi Disemba mwaka huu na kukamilika katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 51.
MHE. OMARI M. KIGUA aliuliza:-
Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini kwa kutambua umuhimu wa wachimbaji wadogo wadogo imekuwa ikitoa ruzuku ili kuwawezesha wachimbaji kunufaika na madini yapatikanayo maeneo mbalimbali nchini:-
(a) Je, mpango huo umenufaisha wachimbaji wangapi nchini?
(b) Je, ni Mikoa na Wilaya zipi zinazonufaika na mpango huo?
(c) Je, Serikali ipo tayari kuweka utaratibu wa kuwakopesha wachimbaji wadogo wadogo ili kuwawezesha kuchimba madini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omar Mohamed Kigua, Mbunge wa Kilindi, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mpango wa utoaji wa ruzuku uanze Serikalini mwaka 2013/2014, jumla ya Wachimbaji Wadogo wa madini 118 wamenufaika na mpango huu. Hadi mwaka 2015/2016 jumla ya shilingi bilioni 8.1 zimetumika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ruzuku hutolewa kwa Wachimbaji wadogo wa madini kwa njia ya ushindani na kwa kuzingatia vigezo husika kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010. Wanufaika 118 wa ruzuku walitoka katika mikoa yote 22 na katika wilaya 53 yenye shughuli za madini hapa nchini. Wanufaika sita walitoka katika Mkoa wa Tanga na katika Wilaya za Handeni pamoja na Tanga yenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013/2014 Serikali ilianzisha Mfuko wa kusaidia Wachimbaji Wadogo na kutenga jumla ya shilingi bilioni 2.3 ambazo zilitengwa na kuwekwa katika Benki ya Rasilimali Nchini (TIB) kwa ajili ya mikopo hiyo. Wachimbaji wadogo wengi walishindwa kukidhi vigezo vya mikopo na hapo sasa Serikali iliamua kutoa ruzuku. Kazi inayoendelea sasa ni kuwapa elimu ya namna sasa ya kunufaika na Mifuko hiyo ili kusudi wananchi waweze kupata fedha hizo kwa kupitia mabenki na taasisi za kifedha hapa nchini.
MHE. JESCA D. KISHOA aliuliza:-
Kwa muda mrefu kumekuwa na habari za uamuzi wa Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo kujenga kituo cha kuzalisha umeme wa upepo Mkoa wa Singida:-
Je, ni lini mradi huo utatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na TANESCO imekuwa ikifanya tafiti kwa ajili ya kuzalisha umeme kwa kutumia upepo katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo na maeneo ya Mkoa wa Singida. Kufuatia tafiti hizo, maeneo ya Kititimo pamoja na Kisaki Mkoani Singida yameonekana kuwa na chanzo kizuri cha kuzalisha umeme kwa njia ya upepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni binafsi ikiwemo Kampuni ya Wind East Africa pamoja na Makampuni mengine kama Six Telecoms na mengine yameonesha uwezo huo kutoka UK. Uwezo wa nguvu inaopata ni pamoja na kuzalisha umeme wa Megawatt 100 katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majadiliano kati ya Serikali kupitia TANESCO na Kampuni ya Wind East Africa sasa yanaendelea vizuri na yatakamilika mwezi Desemba mwaka huu, lakini ujenzi wa mradi sasa utaanza mwezi Aprili mwaka ujao, 2016 na utakamilika mwaka 2019. Ujenzi wa mradi huu utagharimu Dola za Marekani milioni 264.77
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni nyingine inayoonesha kuwekeza katika mradi huo ni pamoja na Kampuni ya Geowind ambayo pia itazalisha Megawatt 50 na mradi utagharimu Dola za Kimarekani milioni 136 na utakamilika...
… katika mwaka ujao wa fedha.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-
Kwa kuwa Jimbo la Mbogwe limejaaliwa kuwa na madini ya dhahabu na utafiti umekuwa ukiendelea bila uchimbaji kufanyika katika maeneo ya Nyakafuru, Kenegere na kadhalika.
Je, ni lini Wizara ya Nishati na Madini itayaachia maeneo haya na kuyagawa kwa wachimbaji wadogo wadogo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, eneo la Nyakafuru lenye leseni ya ukubwa wa kilometa za Mraba 17.53 linamilikiwa na kampuni ya Mabangu Mining Limited ambayo ni kampuni tanzu ya Resolute Tanzania Limited kupitia leseni PL 5374 ya 2008, leseni hii imeisha muda wake tarehe 23 mwezi wa 10 mwaka huu na kuombewa extension. Hadi sasa mashapo yamefikia tani milioni 3.36 zenye wakia 203,000 za dhahabu yamegunduliwa, na jumla ya dola za Marekani milioni 1.83 zimetumika kufanya utafiti katika eneo la mradi.
Mheshimiwa Spika, eneo la Kenegere lina leseni ya utafiti PL 4582 ya 2007 ambayo imeombewa pia extension kupitia PL 6748 ya 2010. Lakini kuna PL 8329 ya 2012 zinazomilikiwa na kampuni ya Resolute Tanzania Limited ambapo mradi huo kwenye ukubwa wa kilometa za mraba 13.18 upo katika hatua ya upembuzi yakinifu.
Mheshimiwa Spika, kampuni hiyo imetumia zaidi ya dola za Marekani milioni 23 kufanya utafiti na imeainisha mashapu ya dhahabu tani milioni 13 zenye wakia 545,000.
Mheshimiwa Spika, pia eneo la Kanegele lina lesni ya utafiti wa madini PL 10159 ya 2014 yenye ukubwa wa eneo la kilometa za mraba 6.39 pamoja na leseni ya kuhodhi eneo RL 0014 ya 2014 yenye ukubwa wa kilometa za 2.94, kampuni pia inamiliki na leseni ya kampuni ya Resolute Tanzania Limited kupitia kampuni yake tanzu ya Mabangu. Mipango ya uendelezaji wa mgodi katika eneo hilo inaendelea kwa kuzingatia mwenendo wa bei ya dhahabu katika soko la dunia.
Mheshimiwa Spika, ili kutohodhi shughuli za utafutaji zinazoendelea katika eneo hilo Wizara ilishauriana na uongozi wa Wilaya ya Mbogwe tarehe 20 Aprili, 2015 na kuamua kutenga maeneo ya Shenda kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Aidha, Kampuni ya Resolute Tanzania Limited imeridhia kutoa leseni ndogo tatu katika eneo la Bukandwa.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Wananchi wa Mbinga wanaishukuru Serikali kwa mradi wa kusambaza umeme vijijini kwani wana imani mradi huo utasaidia kuinua hali za maisha. Hata hivyo ni vijiji 34 tu ndiyo vimepatiwa umeme kupitia mpango wa usambazaji umeme unaotekelezwa na REA Awamu ya Pili.
Je, lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 118 vilivyosailia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alezander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali itapeleka umeme katika vijiji 118 vilivyobaki vya Wilaya ya Mbinga kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu. Ujenzi wa mradi huu utaanza mwezi Disemba, 2016 na kukamili katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Hatua iliyofikiwa hivi sasa ni kukamilika kwa taratibu za kuwapata wakandarasi watakaohusika na ujenzi wa mradi huu.
Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolti 0.4 yenye urefu wa kilometa 471, ufungaji wa transfoma 246 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 19,185. Kazi hii itagharimu shilingi bilioni 18.1.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Serikali ilikuja na mpango mzuri wa umeme Vijijini na kupitia mradi wa REA kukawa na REA I, REA II na sasa REA III na Serikali iliahidi kwamba miradi yote ya REA II ambayo haijakamilika hadi kuanzishwa kwa REA III itatekelezwa sambamba na REA III:-
(a) Je, ni lini Serikali itatekeleza miradi yote ya REA II Jimbo la Chilonwa katika Vijiji vinne vya Kata ya Msamalo(Myunga, Msamelo, Mnase na Mlebe) Vijiji viwili vya Kata ya Zajilwa (Zajilwa na Mayungu) na Kijiji cha Kata ya Manchali?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuviingiza vijiji ambavyo havikuwepo kwenye mpango wa REA II katika mpango wa REA III?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za kupeleka umeme katika Vijiji vya Kata za Manchali, Msamalo na Zajilwa kupitia mradi wa REA Awamu ya II zitakamilika mwezi Novemba mwaka huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vyote vya Jimbo la Chilonwa ambavyo havikupata umeme kupitia REA awamu ya II vitapatiwa sasa umeme kupitia REA Awamu ya III. Kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo itahusisha ujenzi wa umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 68, ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 301, pia ufungaji wa transformer 45. Mradi huu pia utapeleka umeme kwa wateja wa awali 11,276. Kazi zitaanza mwezi Desemba mwaka huu na kukamilika mwaka wa fedha 2019. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 12.09
MHE. COSATO D. CHUMI (K.n.y. MHE. MAHMOUD H. MGIMWA) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Kata ya Ikongosi likiwemo na Gereza la Ilupilo, Kata ya Ikweha yenye Vijiji vya Ukelemi, Uyela, Ugenza, Uhambila, Makongomi, Matelefu, Utosi pamoja na Mbugi.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mahmoud Hassan Mgimwa, Mbunge wa Mufindi Kaskazini, lililoulizwa na Mheshimiwa Chumi, Mbunge wa Mafinga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya kufikisha umeme katika maeneo yote nchini ikiwa ni pamoja na maeneo ya Vijiji vya Mufindi Kaskazini. Aidha, Vijiji vya Kata ya Ikongosi likiwemo Gereza la Ilupilo, Kata ya Ikweha, Vijiji vya Ugenza, Makongomi, Matelefu, Mbugi, Uhambila, Ukelemi, Utosi na Uyela vitapatiwa umeme kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu. Ujenzi wa mradi huu utaanza mwezi Desemba, 2016 na kukamilika katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo pamoja na Wilaya nzima ya Mufindi itahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33, yenye urefu wa kilometa 242, ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 81, ufungaji wa transformer 24, pamoja na kuwaunganishia wateja wa awali 3,533. Kazi hizi zitagharimu shilingi bilioni 11.92
MHE. DANIEL E. MTUKA aliuliza:-
Watanzania wengi wanahitaji umeme mjini na vijijini lakini wanashindwa kuvuta umeme kutokana na gharama kubwa ambapo service line ni shilingi 177,000 na zaidi na gharama ya nguzo ni shilingi 337,740 na zaidi:-
(a) Kwa kuwa nguzo ni mali ya TANESCO, je, kwa nini nguzo hizi zisilipiwe na Serikali?
(b) Je, Serikali haioni kuwa sasa ni wakati muafaka wa kupunguza service line costs kuwa shilingi 27,000 kama ilivyo kwa mradi wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Edward Mtuka, Mbunge wa Manyoni Mashariki, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, TANESCO hugharamia miundombinu ya umeme ikiwemo nguzo na vifaa vingine ili kupeleka umeme kwa wateja. Hata hivyo, kutokana na ufinyu wa bajeti si rahisi kupeleka miundombinu ya umeme maeneo yote kwa wakati mmoja. Kwa maeneo ambayo hayajafikiwa na miundombinu ya umeme wananchi kwa hiari ya kuchangia gharama husogeza miundombinu hiyo katika maeneo ili kuharakisha huduma hiyo. Aidha, kulingana na Kanuni za Sheria ya Umeme ya mwaka 2011, wateja wanaruhusiwa kugharamia miundombinu hiyo kisha kukubaliana na TANESCO namna ya kurejeshewa malipo hayo.
Mheshimiwa Spika, kwa maeneo ambayo tayari yamefikiwa na huduma ya umeme, wananchi huchangia kwa kulipia vifaa muhimu ikiwemo nguzo, mita pamoja na gharama nyingine.
Mheshimiwa Spika, Serikali inagharamia Miradi ya Umeme Vijijini (REA) kwa asilimia 100 na kiasi cha shilingi 27,000 wanacholipa wananchi ili kuunganishiwa umeme katika miradi hii ni kwa ajili ya gharama ya VAT tu. Lengo ni kuhamasisha na kuwawezesha wananchi wa vijijini ili wapate huduma hiyo kwa gharama nafuu. Baada ya miradi ya REA kukamilika, wateja huunganishiwa umeme kwa kufuata taratibu za TANESCO ambapo gharama yake ni shilingi 177,000 kwa umbali usiohitaji nguzo.
Mheshimiwa Spika, gharama za kuunganisha umeme kwa wateja wa majumbani maeneo ya mijini ni shilingi 320,960 kwa umbali usiohitaji nguzo ambapo wateja hufungiwa waya na mita. Gharama za maombi ya services charge ziliondolewa tangu tarehe 01 Aprili, 2016 lengo likiwa ni kupunguza gharama kwa wateja.
MHE. EDWARD F. MWALONGO aliuliza:-
Kumekuwa kukitokea taarifa juu ya kuanza kazi ya uchimbaji katika Migodi ya Liganga na Mchuchuma.
(a) Je, ni lini kazi hiyo itaanza?
(b) Je, nini mazao ya migodi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edward Franz Mwalongo, Mbunge wa Njombe Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, miradi unganishi ya Mchuchuma na Liganga inatekelezwa na kampuni ya ubia kati ya NDC na Sichuan Hongda Group Limited ya China inayojulikana kwa jina Tanzania China International Mineral Resources Limited. Kampuni hii imekamilisha uchorongaji na upembuzi yakinifu wa miradi hiyo. Uchorongaji umeonesha kuwepo kwa tani milioni 428 za makaa ya mawe eneo la Mchuchuma na tani milioni 126 za chuma eneo la Liganga. Upembuzi yakinifu umeonesha Mgodi wa Chuma Liganga una uwezo wa kuzalisha tani milioni 2.9 kwa mwaka na Mgodi wa Makaa ya Mawe ulioko Mchuchuma una uwezo wa kuzalisha tani milioni tatu kwa mwaka; lakini pia uwezo wa kufua umeme wa megawati 600.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, gharama za uwekezaji katika miradi hii ni dola za Marekani bilioni tatu ambapo dola bilioni 600 ni mtaji wa mwekezaji na mkopo utakuwa dola bilioni 2.4.
Mheshimiwa Naibu Spika, kampuni imekwishapata leseni maalum za uchimbaji wa chuma na makaa ya mawe kutoka Wizara ya Nishati na Madini pamoja na vibali vya mazingira mbalimbali. Pia imepata maeneo katika eneo la Katewaka pamoja na Mchuchuma na Lupali. Kazi ya uthamini na makazi na mali ya wananchi walio ndani ya maeneo ya miradi wanaotakiwa kupisha shughuli za mradi, zimekamilika na hivi sasa tathmini ya fidia iko kwa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali ipo katika hatua za mwisho za mazungumzo na mwekezaji. Mradi huu utaanza mara baada ya kukamilisha fidia na wananchi waliopisha mradi pia na Government Notice kwa ajili ya incentive za mradi itakapotolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hiyo unganishi itawawezesha kuchimba makaa ya mawe kiasi cha milioni tatu na chuma ghafi tani milioni 2.9 kwa mwaka. Aidha, sehemu ya makaa ya mawe itatumika kuzalisha umeme na nyingine kwa ajili ya matumizi ya viwandani. Vilevile sehemu ya chuma itatumika kwenye Sekta ya Ujenzi, Viwanda, Kilimo, na kadhalika, lakini madini ya vanadium yatatumika kwa ajili ya matumizi kwenye viwanda vya kemikali pamoja na magari, lakini kadhalika madini ya titanium kwa ajili ya matumizi kwenye viwanda, ndege, meli, pamoja na magari.
MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:-
Kwa mujibu wa tafiti, uchimbaji mdogo ndio unaotoa ajira kwa wingi katika sekta ya madini:-
(a) Je, ni lini Serikali itajenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo katika eneo la Nyamongo?
(b) Je, kwa kutokuwatengea vijana maeneo ya uchimbaji, Serikali haioni kuwa inazidisha chuki ya vijana dhidi ya mgodi wa Acacia North Mara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 Serikali ilitenga eneo lenye ukubwa wa hekta 598 katika eneo la Nyamongo, Kitongoji cha Kerende kuwa eneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo; kadhalika katika eneo hilo ilitoa leseni 96 za uchimbaji mdogo kwa wananchi katika mwaka 2014, kadhalika Serikali ilitenga eneo la ukubwa wa hekta 49.18 katika Kijiji cha Nyakunguru linaloweza kutoa leseni tano za uchimbaji ambapo hivi sasa leseni nne zimeshatolewa kwa Kampuni ya Itandura Miners Cooperation Limited ambayo ipo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengine ambayo yametengewa eneo ni pamoja na eneo la Gorong‟a ambayo ilitenga eneo la hekta 82.52 lenye leseni nane za uchimbaji mdogo ambapo leseni tatu kati ya hizo zimetolewa kwa wananchi wa eneo hilo. Katika eneo la Msege, Serikali pia ilitenga leseni tisa za uchimbaji mdogo kwa wananchi wa eneo hilo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa wananchi wanapokosa maeneo ya uchimbaji wanaweza kuwa na chuki na wawekezaji wakubwa. Kwa kutambua hilo basi, Serikali imeendelea kuitekeleza azma hii ya kuwatengea maeneo wananchi ili wananchi wapate mahali pa kufanyia kazi na kuondoa chuki kati yao na wawekezaji wakubwa.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR (K.n.y. MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH) aliuliza:-

Mafuta na gesi ni rasilimali zinazotegemewa kuwa na mchango mkubwa kwa Taifa letu:-
Je, ni aina ngapi za gesi zilizogundulika na faida iliyopatikana tangu ugunduzi huo ulivyotokea?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maida Hamad Abdallah, lililoulizwa na Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar, Mbunge wa Chakechake, Pemba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), lilianza utafiti wa masuala ya mafuta na gesi asilia nchini mwaka 1950 ikihusisha utafiti katika maeneo ya baharini ya kina kirefu, maziwa na nchi kavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gesi asilia iliyogunduliwa katika maeneo ya bahari ya kina kirefu ni futi za ujazo trilioni 47.08 na katika nchi kavu ni futi za ujazo trilioni 10.17, hivyo kuwa na jumla ya futi za ujazo trilioni 57.25 ya gesi asilia nchini. Gesi asilia iliyogunduliwa ni ya aina moja ya sweet gas, yaani gesi ya kiwango cha juu sana ambayo ina kiwango cha chini sana cha sulfur.
Mheshimiwa Mwenyekiti, faida kubwa iliyopatikana kutokana na ugunduzi wa matumizi ya gesi asilia nchini ni uzalishaji wa umeme wa bei nafuu kwa matumizi ya gesi asilia ikilinganishwa na mafuta. Uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi asilia umeongezeka kutoka unit 2,714.25 kwa mwaka 2014 hadi kufikia unit 4,119 mwaka 2016. Hii ni sawa na asilimia 54.66 ya ongezeko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bei ya umeme imeshuka kutoka wastani wa sh. 188.56 kwa unit mwaka 2014 hadi wastani wa sh. 125.85 kwa unit kwa mwaka 2016, sawa na punguzo la asilimia 33.26. Mbali na punguzo kubwa la umeme, gharama za maombi ya service charge ziliondolewa tangu tarehe mosi Aprili, mwaka 2016, lengo likiwa ni kupunguza gharama za umeme kwa wateja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya Helium One imefanya ugunduzi wa gesi ya helium katika maeneo ya Ziwa Rukwa katika bonde la ufa. Kiasi kilichogundulika kinakadiriwa kufikia futi za ujazo bilioni 54. Gesi ya helium hutumika katika matumizi ya mashine za MRI Scanners na vinu vya nuclear katika matumizi ya baluni kwa matumizi ya ndege, hasa kuruka na ndege hewani.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:- Jimbo la Muheza lina kata 37 na vijiji 135, katika Awamu ya Kwanza na ya Pili ya Mradi wa REA ni vijiji vichache tu vilipata umeme. Je, utekelezaji wa REA III ni vijiji vingapi vinategemea kupata umeme ili wananchi wa maeneo haya waweze kujiandaa katika kujiendeleza kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza, kama ifuatavyo:- Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya vijiji 37 ambavyo havijapatiwa umeme katika Jimbo la Muheza na vitongoji 137 vinatarajiwa kupatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu utakaoanza mwezi Machi mwaka huu. Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa Mpango wa Usambazaji Umeme Vijijini kwa nchi nzima unategemewa kufanya katika vipengele vitatu unaojumuisha densification, grid extension, pamoja na off-grid renewable. REA Awamu ya Tatu kwa ujumla wake katika nchi nzima ikiwa ni pamoja na Jimbo la Muheza itaanza mwezi Machi 2017. Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa mradi huu katika Jimbo la Muheza utajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovolti 33 yenye urefu wa kilometa 50; ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolti 0.4 yenye urefu wa kilometa 82; ufungaji wa transfoma 41; pamoja na kuwanganishia umeme wateja 1025. Mradi huu utatekelezwa kwa muda wa miaka mitano. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 3.94.
MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-
Kuna mahitaji makubwa ya umeme katika Jimbo la Singida Mjini hususani katika kata za pembezoni kama vile Kisaki, Mtama, Mtipa, Mwankoko, Uhamaka, Unyambwa, Unyamikombi na Unyianga.
(a) Je, Serikali ina mpango gani kuvipatia umeme vijiji katika mwaka huu wa fedha?
(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutumia rasilimali ya nguvu ya upepo iliyopo Singida ili kuongeza nishati ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhan Sima, Mbunge wa Singida Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Kisaki, Mtama pamoja na Mtipa pamoja na Mwankoko zimejumuishwa katika mradi kabambe wa REA III unaoanza mwezi Machi, 2017. Katika kazi hizi, maeneo haya yatapelekewa mradi kupitia desification, grid extension pamoja na renewable utakaoanza mwezi huo nilioutaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo inajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 105, ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 126.9, ufungaji wa transfoma 31, pamoja na kuwaunganishia wateja wa awali 1,111. Kazi hii itagharimu shilingi bilioni 8.15.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa muda mrefu wa Serikali ni kutumia vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme ikijumuisha upepo uliopo katika eneo la Singida ambapo katika mpango kabambe wa kuendeleza sekta ya umeme wa mwaka 2016, mradi huu umepangwa kuanza kuzalisha megawati 50 za awamu ya kwanza mwaka 2018. Mradi huu unakadiriwa kugharimu dola za Marekani 136 na utatekelezwa katika maeneo ya Kisasida, Ipungi, Mughamo na Unyankhyanya. Kampuni ya Geo Wind pamoja na Acciona wameingia exclusive agreement kwa ajili ya kipindi cha miezi minne ambayo itaishia mwezi Februari mwaka huu kwa ajili ya kujiridhisha kwa wananchi kama watakubaliana na utekelezaji wa mradi huu ili waweze kupata umeme wa uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni mbalimbali binafsi zimeonesha nia ya kuzalisha umeme kwa kutumia upepo katika Mkoa wa Singida ikiwa ni pamoja na Kampuni ya Wind East-Africa iliyojitokeza kuzalisha umeme wa megawati 50 kwa awamu ya kwanza na baadae kufikisha megawati 100. Mradi huu utatekelezwa katika eneo la Kititimo. Gharama ya mradi huu ni dola za Marekani milioni 264.77.
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:-
Maeneo mengi katika Jimbo la Morogoro Mjini bado hawajapata nishati ya umeme kama vile Kata za Mindu, Lugala, Mkundi, Kiegea A na B, Kihonda, Mafisa, Tungi, Kingolwira na Kauzeni A.
Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo hili la muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdul-Aziz Abood, Mbunge wa Morogoro Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Shirika la Umeme (TANESCO) inatekeleza miradi ya kufikisha miundombinu ya umeme maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na Morogoro Mjini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi unaoendelea katika Kata za Mindu, ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 8.973, ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti nne yenye urefu wa kilometa 35.4, lakini ufungaji wa transfoma saba pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 834.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu utafikisha umeme kwenye maeneo ya Mindu, Kasanga na Madanganya ambapo ni transfoma nne zimefungwa tayari na baadhi ya wananchi pia wameshaunganishiwa umeme. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 1.113. Unajumuisha Mindu -Lugala ambao unajumuisha ujenzi wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 8.9, ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa voti 400 yenye urefu wa kilometa 10.7 na ufungaji wa transfoma tatu. Hali kadhalika utaunganishwa umeme kwa wateja 206. Gharama za mradi huu ni milioni 106.784. Utekelezaji wa miradi hii utakamilika mwezi Juni mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yaliyobaki katika Mji wa Morogoro yataendelea kupatiwa umeme kupitia bajeti ya TANESCO zinazopangwa mwaka hadi mwaka.
MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-
Serikali ilituthibitishia kuwa gesi aina ya Helium iligundulika katika Ziwa Rukwa na kwamba gesi hiyo ina thamani kubwa na ni adimu sana duniani:-
Je, ni lini sasa Serikali itaanza kuchimba gesi hiyo ili Watanzania waanze kunufaika na gesi hiyo kabla haijagunduliwa au kuchimbwa mahali pengine duniani?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kampuni ya Helium One Limited imefanya utafiti wa gesi ya Helium katika Bonde la Ziwa Rukwa. Taarifa za awali zinaonesha uwezekano wa kuwepo kwa gesi ya Helium kiasi cha futi za ujazo bilioni 54 katika maeneo ya Ziwa Rukwa. Matokeo haya yanatokana na uchunguzi wa sampuli tano za mavujia ya gesi ya Helium katika maeneo hayo, kiasi ambacho kinakadiriwa kuwa kikubwa zaidi ya mara sita ya mahitaji ya dunia kwa sasa.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Helium One Limited imefanya utafiti huo kupitia kampuni zake tanzu za Gogota (TZ) Limited, Njozi (TZ) Limited na Stahamili (TZ) Limited zinazomiliki leseni za utafutaji wa gesi ya Helium katika Ziwa Rukwa. Kampuni hizi zilipewa leseni za utafutaji wa Helium katika maeneo mbalimbali kuanzia mwaka 2015. Shughuli za utafutaji wa kina wa gesi ya Helium unaendelea kwa kukusanya taarifa zaidi za kijiolojia, kijiokemia, kijiofizikia na 2D ili zitumike kwa ajili ya uchorongaji wa visima vya utafiti wa gesi asilia kilichopo katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, uchimbaji wa gesi ya Helium utaanza mara baada ya kazi ya utafiti wa kina, upembuzi yakinifu na tathimini ya athari za mazingira kukamilika. Baada ya utaratibu kukamilika, uchorongaji katika maeneo ya Ziwa Rukwa unatarajiwa kuanza mwaka 2018.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA Aliuliza:-
Gesi inayochakatwa Mtwara huweza kuzalisha viwanda vidogo vidogo ikiwemo mbolea na kwa miaka mingi wananchi wa Mtwara wamekosa fursa ya ajira ukilinganisha na maeneo mengine ya Tanzania kama vile Arusha, Mwanza, Kilimanjaro na kadhalika.
Je, ni lini Serikali itasitisha usafirishaji wa gesi kutoka Mtwara kwenda Kinyerezi ili wana Mtwara waweze kunufaika na ajira zinazotokana na uchakataji wa gesi hiyo asilia kufanyika Mtwara na Seriakli kujenga viwanda vitokanavyo na gesi Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maftaha Abdallah Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Sera mpya ya Nishati ya mwaka 2015 na Sera ya Gesi Asilia ya mwaka 2013 zinalenga kutoa fursa ya rasilimali ya gesi asilia kuwanufaisha Watanzania wote wakiwemo wananchi inapopatikana rasilimali hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika hadi sasa kuna miradi miwili inayosafirisha gesi asilia kutoka Mtwara na Lindi hadi Dar es Salaam. Miradi hiyo ni mradi wa kusafirisha gesi kutoka Mtwara na Lindi hadi Dar es Salaam uliokamilika mwaka 2015 na mradi wa Songas uliokamilika mwaka 2004. Gesi inayochakatwa inasafirishwa kwa bomba kwa maeneo mbalimbali nchini yakiwemo kwa ajili ya maeneo ya Mtwara, Lindi, Mkuranga na Dar es Salaam. Visima viwili vya gesi asilia katika eneo la Mnazi bay vimetengwa rasmi kwa ajili ya wananchi wa Mkoa wa Lindi na Mtwara.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na gesi asilia kutoka Lindi na Mtwara kutumika kuzalisha umeme kwa asilimia 50 pia gesi hiyo inatumika katika kusambaza gesi majumbani na viwandani katika maeneo mbalimbali. Kwa sasa Serikali kupitia Shirika la Maendeleo la Taifa (TPDC) inatekeleza mradi wa kuunganisha gesi hiyo katika Kiwanda cha Dangote kilichipo Mtwara ambacho kinahitaji futi za ujazo milioni 45. Pia shirika hilo liko kwenye majadiliano na kiwanda cha URANEX kinachotarajia kujengwa Mkoani Lindi ili kuweza kuunganisha gesi asilia hiyo.
MHE. KAPT. (MST.) GEORGE H. MKUCHIKA Aliuliza:-
Serikali iliwaahidi wananchi wa Mikoa ya Mtwara na Lindi umeme wa uhakika na wa kutosha baada ya kugundulika kwa gesi na baada ya neema ya muda mfupi hivi sasa kuna tatizo kubwa la kukatika kwa umeme mara kwa mara katika Mikoa hiyo ikiwemo na Wilaya ya Newala.
Je, tatizo ni nini na Serikali inachukua hatua gani kumaliza kabisa tatizo hili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kepteni Mstaafu George Huruma Mkuchika, Mbunge wa Newala Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya kukatika kwa umeme mara kwa mara katika maeneo ya Mikoa ya Lindi na Mtwara inatokana na ubovu wa jenereta moja kati ya tisa katika kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia kilichoko Mtwara chenye jumla ya MW 18 ambayo imepungua hadi MW 16. Tatizo lingine ni uchakavu na urefu wa njia inayosambaza umeme wa msongo wa kilovoti 33 kutoka Mtwara kuelekea Wilaya za Mtwara – Tandahimba – Newala – Masasi – Nanyumbu- Nachingwea hadi Ruangwa ambao ni umbali wa kilometa 206.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua zinazochukuliwa na Serikali ili kuondoa tatizo hilo ni pamoja na kufanya ukarabati wa mtambo ulioharibika ili kurudisha uwezo wa kituo katika kuzalisha hali yake ya kawaida MW 18. Kazi hii inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Mei, 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango mwingine ni kuongeza mitambo mingine sita yenye uwezo wa kuzalisha umeme wa jumla ya MW 12 kila moja itakayofikisha MW 30 ambao unatosheleza kwa mahitaji ya mikoa hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha hali ya upatikanaji endelevu wa umeme katika Mikoa hiyo, TANESCO inajenga njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 yenye urefu wa kilometa 80 kutoka Mtwara hadi Mnazi Mmoja, Lindi. Kazi hiyo inajumuisha pia ujenzi wa vituo vya kupoza umeme msongo wa kilovoti 132/33 na transfoma za MVA 20 kwa ajili ya kusambaza umeme wa njia tano. Mradi huu unakamilika mwishoni mwa mwezi Mei, mwaka huu na gharama za mradi huu ni shilingi bilioni 16.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:- Wananchi wa Mtaa wa Katoma na Magema katika Kata za Mtakuja na Kalangalula kwa muda mrefu wamezuiwa kuendeleza ardhi zao kwa sababu Mgodi wa GGM ulipima na kuweka vigingi vya mpaka ndani ya makazi yao.
Je, ni lini mgodi huo utawalipa fidia ili kupisha shughuli za mgodi huo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Madini ya mwaka 2010 huwataka wamiliki wa leseni za uchimbaji wa madini kuzingatia umbali uliowekwa kisheria kutoka sehemu ambako shughuli nyingine za kijamii zinaendelea. Kwa kuzingatia sheria hiyo, mgodi hulazimika kuwalipa fidia na kuhamisha wananchi wanaoishi ndani ya umbali wa mita 200 kutoka katika shughuli za uchimbaji ili kuepuka madhara yanayoweza kutokea kutokana na uchimbaji huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mgodi wa GGM mwaka 2007, 2010, 2013 na 2014 ulilipa fidia ya jumla ya shilingi bilioni 9.67 kwa wananchi 733 wanaoishi ndani ya mita 570 katika maeneo ya Katoma na Nyamalembo. Hata hivyo, kwa kuwa mgodi haujaanza kutumia eneo hilo kwa shughuli za uchimbaji, baadhi ya wananchi waliopata fidia pamoja na wengine wapya, wamejenga tena katika maeneo hayo kwa ajili ya kudai fidia nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa eneo la Magema, mgodi hauzuii wananchi kuendesha shughuli za kilimo na kuendesha shughuli za kimaisha kwa sababu eneo hilo halihitajiki na mgodi kwa sasa. Mgodi utalazimika kulipa fidia kwa kuzingatia sheria husika iwapo mgodi utahitaji kuendeleza eneo hilo.
MHE. LUCY F. OWENYA aliuliza:-
Halmashauri ya Manispaa ya Moshi imekuwa na tatizo la kukatika umeme mara kwa mara.
(a) Je, ni sababu zipi zinazosababisha hali hiyo?
(b) Je, ni lini tatizo hili litakwisha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:- Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Fidelis Owenya, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kilimanjaro ni miongoni mwa mikoa inayofaidika na utekelezaji hali ya utekelezaji wa miradi ya TEDAP. Mradi huu unafadhiliwa na Benki ya Dunia na unalenga kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme nchini. Kazi za mradi huu kwa Mkoa wa Kilimanjaro
zinajumuisha kuongeza uwezo wa vituo viwili vya kupoza umeme vya Trade School kutoka MVA 5 hadi MVA 15. Pia kuboresha miundombinu hiyo katika maeneo ya Boma Mbuzi kutoka MVA 10 hadi MVA 15. Hali kadhalika kubadilisha waya katika njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 kutoka milimita 100 hadi milimita 150. Vilevile kuongeza uwezo wa kusafirisha umeme muhimu na bora.
Mheshimiwa Spika, mradi huu ulianza kutekelezwa mwezi Januari, 2014 na umekamilika kwa asilimia 95 ambapo sasa kilometa 50.95 kati ya kilometa 54.63 zimeshajengwa na waya zimeshaunganishwa.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha utekelezaji wa mradi huu kumekuwa na ulazima wa kuzia umeme katika baadhi ya maeneo ili kupisha marekebisho maalum na kwa usalama zaidi. Zoezi hili limekuwa likifanyika kwa kutoa taarifa katika vyombo mbalimbali vya habari. Tatizo la
kukatikakatika kwa umeme katika maeneo ya Halmashauri ya Mji wa Moshi litaisha mara baada ya shughuli za Mradi huu kukamilika mwezi Mei, 2017.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye Kata za Ifumbo, Lualaje, Mafyeko na Kambikatoto katika Wilaya ya Chunya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa, Mbunge wa Lupa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mradi Kabambe wa Usambazaji Umeme Vijijini Awamu ya Tatu umeanza rasmi nchi nzima tangu mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele-mradi vitatu vya densification, grid extension pamoja na off grid renewable ambapo inalenga kuongeza wingi wa usambazaji umeme kwenye vijiji ambavyo vimefikiwa na umeme lakini kwenye vitongoji havijaunganishwa. Kata za Ifumbo, Kambikatoto, Lualaje na Mafyeko zimejumuishwa katika mradi wa REA Awamu ya Tatu wa grid extension ambao utaanza na kukamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika kata hizo itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 20, ujenzi wa njia ya umeme ya msongo ya kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 76, ufungaji wa transfoma kumi pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,145. Gharama ya kazi hii ni shilingi bilioni 3.142.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma una madini ya chokaa, dhahabu,
platinum na kadhalika:-
Je, Serikali imechukua hatua gani kuendeleza utafutaji na uchimbaji wa madini katika mkoa huo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Mkoa wa Kigoma una madini ya aina mbalimbali yakiwemo madini ya chokaa, chuma, cobalt, dhahabu, galena, nickel, shaba na platinum.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) ilifanya utafiti wa awali wa madini nchi nzima na kuandaa ramani za jiolojia nchini. Utafiti huo utasaidia kutangaza fursa za uwepo wa madini yanayogunduliwa ili wawekezaji wa ndani na nje ya nchi waweze kuwekeza katika tafiti za kina na uchimbaji wa madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1959 hadi 2010 Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) walifanya utafiti wa jiolojia katika Mkoa wa Kigoma na kutengeneza ramani za jiolojia 22 kwa nchi nzima na hasa katika Mkoa wa Kigoma. Kati ya mwaka 2013 hadi 2014, GST kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ikiwemo kampuni ya Beak Consultants GmbH ya Ujerumani na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam walifanya utafiti wa awali kubainisha uwepo wa madini mbalimbali Mkoani Kigoma kama ifuatavyo:-
Madini ya tin katika maeneo ya Bwuhinika, Kabogo, Kapalagulu na Lugufu; madini ya shaba katika maeneo ya Gagwe, Kampisa na Nyamori; madini ya barite katika eneo la Ilagala; chumvi katika eneo la Uvinza; dhahabu katika maeneo ya Isabika, Lumbwa, Lusahunga pamoja na Mwiruzi; madini ya agate katika maeno ya Kabingo, Kasulu, Keza na Nkuba; madini ya nickel katika eneo la Kapalagulu na madini ya chokaa katika maeneo ya Lugufu, Makere, Matiaso pamoja na Kasuku. Utafiti wa kina unahitajika ili kubaini kiasi halisi cha mashapo yaliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwezi Machi 2017, Mkoa wa Kigoma ulikuwa na jumla ya leseni 15 za utafutaji wa madini ya dhahabu, leseni 20 za utafutaji wa madini ya shaba na leseni 2 za utafutaji madini ya platinum. Vilevile kuna leseni 25 za uchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu na leseni 118 za uchimbaji mdogo wa madini ya chokaa, kadhalika kuna leseni 716 za uchimbaji mdogo wa madini ya shaba katika maeneo mbalimbali Mkoani Kigoma.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Tagamenda Substation ni kituo kikubwa kati ya vituo vinavyosafirisha umeme wa Gridi ya Taifa kwani kinapokea umeme kutoka Mtera, Kidatu na Kihansi, lakini vijiji vya Tagamenda, Ikuvilo na Wangama vinavyozunguka kituo hicho havina huduma ya umeme ingawa ndivyo vinalinda kituo hicho.
(a) Je, ni kwa nini Serikali inashindwa kutoa huduma
ya umeme katika vijiji vinavyozunguka kituo hicho?
(b) Je, ni sababu gani zinazofanya vijiji hivyo kukosa kupatiwa huduma hata ya umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Kitongoji cha Malulumo
Kijiji cha Tegamenda kiliwekwa katika Mpango wa kupatiwa umeme kupitia Shirika la Umeme TANESCO katika mwaka 2015/2016. Kazi hiyo ilianza Mei, 2016 na inakamilika Juni, 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za kupeleka umeme katika Kitongoji hicho zimejumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa umeme wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa moja; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 1.4; ufungaji wa transfoma moja pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 70. Kazi hii imekamilika kwa asilimia 90 na inagharimu shilingi bilioni 93.1.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa Mradi Kabambe wa Usambazaji Umeme Vijijini Awamu ya Tatu umeanza nchi nzima tangu mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele-mradi vitatu vya densification, grid extension pamoja na off-grid renewable vinavyolenga kuongeza wigo wa umeme katika vijiji vyote nchini, vitongoji vyote vilivyobaki, taasisi za umma na maeneo ya pembezoni ambayo hayajafikiwa na miundombinu ya umeme ikiwa ni pamoja na visiwa. Vijiji vya Ivukilo, Wangama pamoja na maeneo mengine ya kijiji cha Tagamenda vimewekwa katika utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Tatu wa Densification na Grid Extenson utakaokamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 10.3; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 9.7; ufungaji wa transfoma tatu pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 300. Gharama ya kazi hii ni shilingi bilioni 14.45.
MHE. KABWE Z. R. ZITTO (K.n.y MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Hivi sasa yapata miaka 11 utafiti wa mafuta na gesi katika mwambao wa Ziwa Tanganyika kwenye maeneo ya Kigoma, Rukwa na Katavi umefanyika au unaendelea kufanyika.
(a) Je, ni nini hali ya utafiti huo?
(b) Bonde la Mto Malagarasi nalo limefanyiwa utafiti
wa mafuta na gesi; je, hali ya utafiti huo ikoje?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodem Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, lililoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Kabwe Zuberi Zitto, Mbunge wa Kigoma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya Beach Petroleum
ya nchini Australia ilianza kufanya utafiti wa mafuta na gesi Kusini mwa Ziwa Tanzanyika tangu mwaka, 2010. Kampuni hiyo ilifanya utafiti na kukusanya data ambazo kimsingi ziliwezesha kupatikana taarifa za uchunguzi pamoja na utafiti. Kampuni hiyo imeshindwa kuanza kuchimba gesi kwa sababu zifuatazo:-
Kwanza kabisa ni kwa sababu ya kupanda kwa gharama za uwekezaji, lakini pia kupanda na kushuka kwa bei za mafuta duniani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 10 Oktoba, 2016, Serikali za Tanzania na DRC ziliingia makubaliano ya (MoU) ya kufanya utafiti wa mafuta na gesi pamoja katika Ziwa Tanganyika. Maeneo makubwa ambayo yamekubalika kufanyiwa kazi ni pamoja na kutathmini kwa pamoja data za kijiolojia pamoja na kijiofizikia ili kutambua ukubwa wa mashapo ambayo yatavuka mpaka, vilevile kuandaa jinsi zitakavyofanya kazi kwa ushirikiano. Nchi za Burundi na Zambia nazo zimeomba kuingizwa katika makubaliano hayo ili kufanya utafiti katika ziwa lote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya Motherland Industries ya nchini India iliingia ubia na Serikali kupitia TPDC kufanya utafiti wa mafuta na gesi asilia katika eneo la Bonde la Mto Malagarasi mwaka 2012. Kufuatia kushuka kwa bei ya mafuta duniani tangu wakati huo, kampuni imeshindwa kukamilisha majukumu yake ya kazi kama ilivyokubalika kwenye mkataba wa Production Sharing Agreement, kutokana na hatua hiyo, Serikali inakusudia sasa kurudisha eneo hilo kwa ajili ya utangazaji na wawekezaji wengine wapya.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID aliuliza:-
Vijiji 48 vya Jimbo la Same Magharibi vyenye zaidi ya kaya 2,943 havijapatiwa umeme wa REA japokuwa vina mahitaji makubwa ya umeme.
Je, ni ipi ratiba ya kuwasambazia umeme wananchi hawa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi kabambe wa usambazaji umeme vijijini awamu ya tatu umeanza nchi nzima tangu Machi, 2017. Mradi huu unajumuisha vipengele vya miradi vitatu vya Densification, Grid Extension pamoja na Off Grid Renewable.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi zitakazofanyika ni kuongeza wigo wa usambazaji umeme katika vijiji, vitongoji vyote, taasisi za umma na maeneo ya pembezoni ambayo hayajafikiwa na miundombinu ya umeme, ikiwa ni pamoja na visiwa.
Mradi wa REA Awamu ya Tatu utakamilika mwaka 2020/2021. Vijiji vya Jimbo la Same Magharibi vitapatiwa umeme kupitia mradi huu wa REA Awamu ya Tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo itahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 67.81. Ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 261, ufungaji wa transfoma 43 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 2,457.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hii itagharimu shilingi bilioni 10.8.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Serikali inafanya zoezi la kimya kimya la utafutaji wa mafuta na gesi katika Jimbo la Mlimba bila kutoa taarifa rasmi kwa wananchi juu ya zoezi hilo:-
Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya mchakato huo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, utafutaji wa mafuta na gesi asilia katika Kitalu cha Kilosa Kilombero unaofanywa na Kampuni ya Swala Energy ulianza mwezi Februari, 2012. Kampuni hiyo ilianza kufanya utafiti wa awali wa kijiolojia kwa ajili ya kutambua aina na sifa za miamba iliyopo na kutoa taarifa ya mitetemo (seismic data).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na tafiti hizo, kampuni ilionesha uwezekano wa kuwepo kwa mafuta na gesi asilia katika eneo hilo. Eneo lililoainishwa kwa ajili ya uchimbaji wa kisima hicho lipo katika Kijiji cha Ipera Asilia katika Hifadhi Tengefu ya Bonde la Kilombero. Uchimbaji unatarajiwa kuanza mwezi Septemba, mwaka 2017 baada ya utafiti kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Februari, 2017, Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) ilianza kutoa elimu kuhusu utafiti wa mafuta na gesi asilia na fursa zitakazopatikana kwa wananchi wa Mlimba hasa katika maeneo yanayozunguka mradi huo. Elimu hiyo itahusu pia athari za mazingira na ushiriki wa wananchi katika miradi mbalimbali kwa manufaa ya wananchi pamoja na Taifa kwa ujumla.
MHE. WILFRED M. LWAKATARE aliuliza:-
Mji wa Manispaa ya Bukoba una vijiji ambavyo havina umeme kabisa na havikuingizwa katika mpango wa REA wa kusambaza umeme.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuvipatia umeme vijiji vya kata za Nyanga, Ijuganyondo na Kahororo ambavyo mazingira na hali ya kiuchumi haitofautiani na vijiji vilivyosambaziwa umeme katika wilaya nyingine vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Wilfred Muganyizi Lwakatare, Mbunge wa Bukoba Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Mradi Kabambe wa Usambazaji Umeme Vijijini Awamu ya Tatu umeanza rasmi nchi nzima mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele vya mradi vitatu vya Densification, Grid Extension na Off-Grid Renewable. Mradi huu unalenga kusambaza umeme katika vijiji vyote nchi nzima, vitongoji vyote, taasisi zote za umma na maeneo yote ya pembezoni, ikiwa ni pamoja na visiwa. Mradi wa REA Awamu ya Tatu utakamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, TANESCO inaendelea na usambazaji wa umeme katika maeneo ya mijini ambayo hayajapata umeme, vikiwemo vijiji vya Kata za Ijuganyundo, Kahororo, Nyanga pamoja na Jimbo zima la Bukoba Mjini. Kazi hii inafanyika mwaka huu wa fedha 2016/2017 kwa gharama ya shilingi bilioni 22.96.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengine ikiwemo kata ya Nyanga na vijiji vya Hyolo, Kyakailabwa pamoja na Vijiji vingine vya Rubumba, vitapatiwa umeme kupitia umeme wa Urban Electrification Program chini ya TANESCO. Mradi huu unatarajiwa pia kuanza mwaka 2018. Upembuzi yakinifu wa mradi huo umeshakamilika. Mradi utafikisha umeme kwa wateja wote wa awali 469 na utagharimu shilingi bilioni 782.6.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI aliuliza:-
Serikali inapeleka umeme vijijini kupitia mpango wa REA lakini kuna maeneo mengi ambayo hayajafikiwa na huduma hiyo.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme kwenye kijiji cha Mlalo, Bagamoyo, Mngaza na Kieti kwenye kata ya Vugiri?
(b) Je, ni lini Serikali itafikisha umeme kwenye kata mpya ya Mpale?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stephen Ngonyani, almaarufu Maji Marefu, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Mradi Kabambe wa REA katika nchi nzima kama nilivyosema umeanza tangu mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele vya mradi vitatu katika mikoa yote, Grid Densification, Grid Extension na Off-Grid Renewable. Katika eneo la Mheshimiwa vijiji vya Bagamoyo, Kieti, Mlalo na Mganza katika Kata ya Buhuli vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu utakaokamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme maeneo hayo itajumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa umeme wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 6.6; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 19; ufungaji wa transfoma saba pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 350. Gharama ya kazi hiyo ni shilingi bilioni 940.9
MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-
Serikali imefanikiwa kupeleka umeme katika Wilaya ya Mbogwe kupitia Electricity V na REA lakini huduma hii haijawafikia wananchi walio wengi; Je, ni lini Serikali itaongeza usambazaji wa huduma hiyo muhimu kwa wananchi wengi walio tayari kulipia gharama za kufungiwa umeme katika nyumba zao hususan katika Miji ya Masumbwe na Lulembela?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Mradi kabambe wa usambazaji umeme vijijini awamu ya tatu umeanza nchi nzima tangu Mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele-mradi vitatu vya Densification, kwa maana ya vitongoji, Grid Extention kwa maana ya vijiji vyote pamoja na Off- Grid Renewable katika maeneo ya visiwa. Mradi huu unalenga kuongeza wigo wa usambazaji umeme katika vijiji vyote ambavyo havijafikiwa na umeme ikiwa ni pamoja na vitongoji vyote nchi nzima, taasisi zote za umma, mashine za maji pamoja na visiwa vyote nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, Miji ya Lulembela na Masumbwe imewekwa katika utekelezaji wa mradi wa REA awamu ya tatu utakaokamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika Miji ya Masumbwe unaojumuisha vijiji vya Budoda, Ilangale, Masumbwe, Nyakasaluma na Shenda; na katika Lulembela unaojumuisha Vijiji vya Bugomba, Kabanga, Kashelo, Mtakuja, Nyikonga pamoja na maeneo mengine. Ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti utapelekwa kwenye maeneo yote yenye urefu wa kilometa 38.7; ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 110; ufungaji wa transfoma 20; pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wapya 678. Kazi hii itakamilika mwaka 2020/2021 na itagharimu shilingi bilioni 5.18.
MHE. ESTER M. MMASI aliuliza:-
Kupitia fursa ya ujenzi wa bomba la mafuta Mkoani Tanga, ni dhahiri kwamba vijana takribani 15,000 watapata ajira kwenye mradi kwa upande wa Tanzania:-
(a) Je, Serikali imejipangaje kuona kuwa vijana wa Kitanzania wanapata ajira katika soko la Tanzania kupitia fursa hii ya uwekezaji?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuingiza mtaala wa mafuta na gesi katika mitaala ya VETA ili kuwajengea uwezo, maarifa na ujuzi vijana wa Kitanzania katika sekta hiyo muhimu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa ujenzi wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima (Uganda) hadi Bandari ya Tanga (Tanzania) uko katika hatua ya majadiliano ya jinsi mradi huo utakavyotekelezwa. Katika majadiliano hayo, suala la ajira kwa Watanzania litazingatiwa ili Watanzania wanufaike na ajira kupitia ujenzi na uendelezaji wa mradi huo. Mradi unatarajiwa kutoa ajira 10,000 wakati wa ujenzi na ajira kwa watu 1,000 wakati wa uendeshaji.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 na 2013 Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na Kampuni ya Petrobras ya Brazili, iliendesha mafunzo maalum ya ufundi wa plumbing, uchomeaji, upakaji rangi pamoja na mambo mengine katika Chuo cha VETA huko Mtwara na Lindi. Mafunzo hayo yalilenga kuwaongezea weledi wanafunzi wapatao 350 wa VETA ambao wamepatiwa vyeti vya kimataifa na wanaweza kuajiriwa ndani ya nchi na nje ya nchi. Gharama za mafunzo yote ni Dola za Marekani milioni nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Serikali ya Norway, chini ya Mradi wa Mafuta kwa Maendeleo (Oil for Development) imekamilisha taratibu za kuingiza mtaala wa mafuta na gesi katika vyuo vya VETA hapa nchini. Mtaala huu utaanza kutumika katika baadhi ya vyuo vya VETA hapa nchini mwaka 2018. Utekelezaji wa mpango huu utagharimu Dola za Marekani milioni 20.
MHE. PROF. NORMAN A. S. KING aliuliza:-
Utafiti uliofanywa na Serikali unaonesha kuwa Mto Lumakali unaozalisha maji katika Wilaya ya Makete unaweza kuzalisha megawatts 640 za umeme na hasa ikizingatiwa kuwa Wilaya ya Makete inapata mvua kwa miezi nane (8) kwa mwaka:-
Je, ni lini ujenzi wa bwawa ambao ni mpango wa Serikali wa tangu mwaka 2005 utaanza ili kusaidia kujenga uchumi wa kudumu huko Makete, Mkoa wa Njombe na Mbeya kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Norman Adamson Sigalla King, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, upembuzi yakinifu uliofanyika mwaka 2012 kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ulibainisha kuwepo uwezekano wa kuzalisha umeme wa nguvu za maji wa megawati 222 katika eneo la Mwakauta kwenye Maporomoko ya Mto Rumakali. Juhudi mbalimbali zimefanywa na Serikali ikiwemo kuingia mikataba mbalimbali ya Makubaliano ya Awali ya uendelezaji wa Mradi huu kwa kushirikisha Kampuni mbalimbali za nje za JSC ya Urusi pamoja na kampuni ya China. Kampuni hizo hazikuweza kutekeleza mradi huo kutokana na gharama kuwa kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na taratibu za kumpata mshauri mwelekezi kwa ajili ya kuandaa makabrasha ya zabuni kwa ajili ya kumpata mbia wa ujenzi wa mradi huo. Kazi ya kumpata mbia itakamilika mwezi Juni mwaka huu wa 2017 na ujenzi wa mradi unatarajiwa kuanza mwaka 2019 na utakamilika mwaka 2026. Gharama za mradi huu ni Dola za Marekani milioni 936.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA (K.n.y. MHE. SUSANE P. MASELLE) aliuliza:-
Je, kwa nini Serikali imewanyang’anya ajira vijana waliokuwa wamejiajiri kwenye Machimbo ya Ishokelahela na baadaye ikaamua kubadili umiliki wa leseni kwa siri?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Susane Peter Maselle, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, wachimbaji wadogo waliokuwa wanachimba Ishokelahela hawakuwa na leseni ya uchimbaji bali walikuwa wanachimba katika eneo la utafiti la leseni ya Kampuni ya Carlton Kitongo Tanzania Limited.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, mwaka 2014, Serikali ilifanya mazungumzo na kampuni hiyo na kuwapatia wachimbaji wadogo hao leseni mbili za uchimbaji zenye jumla ya hekta 20. Wananchi hao waliweza kuunda kampuni yao inaitwa Isinka Federation Miners Co-operative Limited.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015 kikundi kiliamua kubadilisha leseni zake mbili za uchimbaji mdogo na kuzifanya kuwa leseni moja ya mgodi wa uchimbaji wa kati lakini chini ya Kampuni yao ya Isinka Federation Miners Co-operative Limited. Umiliki wa leseni hizo haujabadilishwa hadi leo upo chini ya umiliki wa wachimbaji hao wadogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia mwezi Machi, 2017, mgodi ulikuwa umeshakusanya tani 35,000 za mbale (ore) kwa njia ya ubia wa Kampuni ya Busolwa Mining pamoja na wachimbaji hao na waliweza kutoa fursa za ajira 164 za moja kwa moja.
MHE. ABDALLAH H. ULEGA (K.n.y. MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA) aliuliza:-
Mheshimiwa Spika, maeneo mengi ya Pwani huwa na madini mbalimbali.
Je, eneo la Rufiji lina madini gani ili wananchi hawa washauriwe ipasavyo kutouza maeneo yao?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa Mbunge wa Rufiji lililo ulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Abdallah Hamis Ulega, Mbunge wa Mkuranga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika ni kweli kwamba katika ukanda wa Pwani ya Tanzania kunapatikana madini ya aina mbalimbali ambayo ni pamoja na Barite, Chokaa, Chumvi, Clay, Dhahabu, Flourite, Jasi, Kaolin, Mchanga, Mercury, Niobium, Ruby, Rutile, Titanium, Zircon pamoja na Gesi Asilia.
Mheshimiwa Spika, Wakala wa Jiolojia Tanzania GST kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Kampuni ya Beak Consultants GmbH ya nchini Ujerumani ilifanya utafiti wa awali wa mwaka 2013 na 2014. Kutokana na utafiti huo madini yaliyobainika katika eneo la Rufiji ni pamoja na madini ya Chokaa na Niobium ambayo hupatikana katika eneo la Milima Luhombero, vilevile kuna viashiria vya uwepo wa madini ya dhahabu, mchanga pamoja na maeneo mengine ambapo kuna madini ya ujenzi pamoja na madini ya gesi asilia. Utafiti wa kina unahitajika ili kubaini kiasi halisi cha mashapo ya madini hayo kabla ya kuanza uchimbaji wake, ingawa machimbo ya mchanga pamoja na madini ya kokoto yanaendelea kuchimbwa.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE aliuliza:-
Wilaya ya Kigamboni ina uwekezaji mkubwa katika sekta ya nyumba na viwanda, mahitaji ya umeme kwa sasa ni zaidi MW 20; lakini ni MW 8 tu zinazopatikana, nao umekuwa ukikatika mara kwa mara kutokana na mahitaji makubwa pamoja na uchakavu wa miundombinu ya umeme.
(a) Je, Serikali ina mikakati gani ya kuhakikisha Kigamboni inapatikana umeme wa uhakika?
(b) Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha kupoozea umeme (substation) katika Wilaya ya Kigamboni kutokana na mahitaji makubwa ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Faustine Engelbert Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) inakamilisha utekelezaji wa mradi wa uboreshaji umeme katika Jiji la Dar es Salaam kupitia mradi wa TEDAP. Mradi huu unahusisha ujenzi wa vituo vya kupooza umeme vya Mbagala na Kurasini. Kazi ya vituo hivyo ni pamoja na kuimarisha upatikanaji wa umeme katika maeneo ya Kigamboni kwa kuwa Kigamboni sasa itakuwa ikipata umeme kutoka katika vituo hivi vya Mbagala na Kurasini badala ya Kipawa na Ilala kama ilipokuwa hapo nyuma. Ujenzi wa mradi huu ulianza mwaka 2012 na utakamilika mwishoni mwa mwezi Septemba, 2017.
(b) Mheshimiwa Spika, ili kulipatia ufubuzi wa kudumu tatizo la upatikanaji wa umeme eneo la Kigamboni, Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) linajenga njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 kutoka Kurasini kwenda Dege – Kigamboni na kujenga kituo cha kupooza umeme chenye uwezo wa kilovoti 132 chenye uwezo wa kufua umeme wa MVA 120 sawa na MW 100. Taratibu za ujenzi zimeanza mwezi Agosti, 2017 na kazi inatarajiwa kukamilika mwezi Machi, 2018. Gharama ya mradi huu inakadiriwa kufikia shilingi bilioni tano.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Wilaya ya Urambo inapokea umeme kutoka kwenye kituo cha kupoozea umeme cha Kaloleni umbali wa kilometa 90 kufika Urambo ambako ndiko kiliko kikata umeme inapokuwa kumetokea tatizo katika njia. Aidha, chanzo hicho cha umeme pia kimetegemewa na Wilaya ya Kaliua, Jimbo la Ulyankulu na vijiji vya Ikomwa, Igange, Tumbi, Ilolangulu hadi Ugoola (Tabora na Uyui); uzoefu unaonyesha kwamba kama kukitokea tatizo la kiufundi katika njia huwa inasababisha kukatika kwa umeme katika njia nzima likiwemo Jimbo la Urambo na kusababisha malalamiko mengi kwa TANESCO.
Je, kwa nini Serikali isijenge kituo cha kupoozea umeme (substation) karibu na Wilaya ya Urambo ili kiweze kutoa umeme wa uhakika katika Wilaya hiyo inayozidi kukua katika mahitaji ya umeme hasa katika kutekeleza sera ya viwanda na katika taasisi zinazotoa huduma za kijamii kama hospitali, shule na kadhalika kwenye Jimbo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inaendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mikoa ya Tabora na Kigoma kwa kujenga njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 133 yenye urefu wa kilometa 372 kutoka Tabora kupitia Urambo, Kaliua, Uvinza na hatimaye Kigoma.
Mheshimiwa Spika, katika mradi huu, kituo cha kupoza umeme (substation) cha kilovoti 132 kitajengwa kati ya Urambo na Kaliua kitakachosafirisha umeme katika Wilaya ya Urambo, Kaliua, Uvinza hadi Kigoma na hivyo kuimarisha miundombinu katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu wa mradi huu ulianza mwezi Juni, 2017 na utakamilika mwezi Septemba, 2017. Ujenzi rasmi wa mradi unatarajiwa kuanzia mwezi Aprili, 2018 na kukamilika mwezi Agosti, 2018. Mradi huu utagharimu shilingi bilioni 179.
MHE. NAPE M. NNAUYE (K.n.y MHE. PROF. NORMAN A. S. KING) aliuliza:-
Pamoja na juhudi nzuri zinazofanywa na Serikali kupeleka umeme vijijini:-
Je, ni lini Vijiji 86 vya Wilaya ya Makete hususani Tarafa ya Ukwama, Lupalilo, Ikuwa, Matamba na Bulogwa watapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Norman Adamson Sigalla King, Mbunge wa Makete, lililoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, Mbunge wa Mtama, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini kupitia REA awamu ya tatu iliyoanza mwezi Machi, 2017. Utekelezaji wa mradi huu utakamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya mradi huu itajumuisha kufikisha umeme katika vijiji vyote vilivyobaki, vitongoji vyote, Taasisi zote za umma na maeneo ya pembezoni. Vijiji 28 kati ya vijiji 86 vya Wilaya ya Makete vilipatiwa umeme kupitia mradi wa REA II uliokamilika mwezi Desemba, 2016. Vijiji 58 na vitongoji vyake ikiwa ni pamoja na Bulongwa, Lupalilo, Matamba, Ikuwa na Ukwama vitapelekewa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu ulioanza mwezi Juni, mwaka huu ambao pia utakamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji 29 vilivyobaki, itajumuisha kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 47.5, ufungaji wa transfoma 18, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,439. Mradi huu utakamilika mwezi Machi, 2019 na utagharimu shilingi bilioni 4.54.
MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza:-
Jimbo la Ukonga lina shida kubwa ya umeme katika Kata zifuatazo; Kata ya Chanika (Ngwale, Nguvu Mpya, Virobo, Kidugalo, Yongwe, Lukooni, Vikongoro na Tungini); Kata ya Zingiziwa (Zogoali, Zingiziwa, Ngasa, Ngobedi, Somelo na Gogo, Lubakaya na Kimwani); Kata ya Majohe (KIvule na Viwege); Kata ya Buyuni (Zavala, Buyuni, Mgeule Juu, Nyeburu, Mgeule Chini, Kigezi, Kigezi Chini na Taliani); Kata ya Pugu Station (Bangulo, Pugu Station na Kichangani); Msongola (Yangeyange, Mbondole, Kidle, Mkera, Sangara, Kiboga, Uwanja wa Nyani, Kitonga, Mvuleni na Mvuti) na Kata ya Kivule (Bombambili). Maeneo hayo yote yanahudumiwa na Wilaya ya Kisarawe kama maeneo ya vijijini. Je, ni lini maeneo hayo yatapata umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swai la Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, maeneo ya Kidole, Bangulo, Kitonga, Mvuti na baadhi ya maeneo mengine pamoja na Msongole yalipatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Pili uliokamilika mwezi Disemba, 2016. Kazi ya kupeleka umeme katika maeneo hayo ilijumuisha pia vijiji vilivyokuwa vinatoka katika Wilaya ya Kisarawe ambapo pamoja na mambo mengine vimefungiwa transfoma 55 za kVA 50, kVA 100 na kVA 200; ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 pia umejengwa kwa urefu wa kilometa 187.22 lakini njia ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 239.7 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja 1,083. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 5.3.
Mheshimiwa Spika, mitaa mingine iliyobaki ya Kata za Chanika, Zingiziwa, Majohe, Buyuni, Pugu Station pamoja na Msongola, zitapatiwa umeme kupitia Mradi wa Urban Electrification chini ya ufadhili wa Maendeleo wa Benki ya Dunia.
Mheshimiwa Spika, kazi hizi zinajumuisha ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 66.3, msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 336.7 pamoja na ufungaji wa transfoma 73 za kVA 200 na kVA 100. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 10.73 na utaunganishia wateja 7,083.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Je, gharama ya ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam ni shilingi ngapi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara na Songo Songo Mkoani Lindi hadi Dar es Salaam ulianza kutekelezwa mwezi Juni, 2013 na kukamilika mwezi Oktoba, 2015. Ujenzi wa mradi huu ulihusisha ujenzi wa mitambo ya kuchakata gesi asilia yaani Madimba (Mtwara) pamoja na Songo Songo (Lindi) kwa gharama ya dola za Marekani milioni 349.51 na pia ujenzi wa bomba la kusafirishia gesi asilia kutoka Mtwara na Songo Songo – Lindi hadi Dar es Salaam kwa gharama ya dola za Marekani milioni 875.72.
Mheshimiwa Spika, jumla ya gharama zote za mradi huu hadi kukamilika ni dola za Marekani milioni 1,225.23.
Mheshimiwa Spika, bomba lina uwezo wa kusafirisha gesi asilia futi za ujazo milioni 784 kwa siku na linaweza kufikia futi za ujazo milioni 1,002 kwa siku. Kwa sasa gesi inayosafirishwa ni futi za ujazo milioni 68.5 kwa siku.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA aliuliza:-
Katika Mradi wa REA II, Jimbo la Bagamoyo lilipewa vijiji 10 tu na bado utekelezaji wake unasuasua na uko nyuma ya ratiba:-
Je, ni lini miradi ya umeme kwa Vijiji vya Kongo, Kondo na nyongeza ya Matimbwa itakamilika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ilikamilisha kupeleka umeme vijijini kupitia Mradi wa REA Awamu ya Pili ikiwemo Wilaya ya Bagamoyo mwezi Desemba, 2016. Kazi ya mradi huo katika Wilaya ya Bagamoyo ilijumuisha ujenzi wa njia kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 80.13, ujenzi wa njia kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 106.67 pamoja na ufungaji wa transfoma 41, kazi nyingine ilikuwa kuwaunganisha wateja wa awali 2,066 na gharama za utekelezaji wa mradi zilikuwa shilingi bilioni 30.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya Kijiji cha Matimbwa iliyobaki kupatiwa umeme pamoja na vijiji vingine ikiwemo Kondo vitafikishiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu iliyoanza mwezi Juni, 2017 utakaokamilika mwaka 2020/2021.
MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-
Mradi wa umeme wa 400KV wa kutoka Kinyerezi hadi Arusha ni muhimu kwa maendeleo ya wananchi na Taifa letu; kuanzia mwaka 2015 wananchi wa maeneo ya Kibaha Mjini ambako mradi huu unapita wamechukuliwa maeneo yao na yalifanyiwa uthamini kwa ajili ya wananchi kulipwa fidia:-
Je, ni lini fidia hii italipwa kwa wananchi walioathirika na mradi huu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) inatekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 kutoka Kinyerezi hadi Arusha. Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 400 yenye urefu wa kilometa 600, pamoja na kilometa 40 kutoka Kibaha hadi Zinga na kilometa 60 kutoka Segera hadi Kange (Tanga).
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu pia unahusisha ujenzi wa vituo vya kupoza umeme katika maeneo ya Chalinze, Segera, Kange, pamoja na Zinga (Bagamoyo).
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 kazi ya uthamini wa mali za wananchi kutoka Kibaha hadi Chalinze ilifanyika kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi watakaopisha mradi. Taratibu za kulipa fidia zimekamilika na jumla ya shilingi bilioni 21.56 zitahitajika kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi 855. Maeneo yatakayofidiwa ni pamoja na Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini, Bagamoyo pamoja na Kisarawe.
Mheshimiwa Naibu Spika, malipo ya fidia yataanza mara tu uhakiki utakapokamilika.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO (K.n.y. MHE. MOHAMED MCHENGERWA) aliuliza:-
Ni takribani miaka miwli sasa Serikali imeshindwa kuwahakikishia wananchi wa Jimbo la Rufiji kuwa na umeme wa uhakika kufuatia hitilafu ya mara kwa mara kwenye mitambo ya umeme unaozalishwa na gesi kutoka Kilwa.
Je, ni lini Serikali itawaunganisha wananchi wa Rufiji, Kibiti na Kilwa kwenye Gridi ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omary Mohamed Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, lililoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Mbunge maarufu sana wa Kihesa Mgagao, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kilwa, Rifiji pamoja na Kibiti zimeunganishwa katika Gridi ya Taifa kupitia utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Somangafungu, Lindi hadi Kinyerezi, Dar es Salaam. Ujenzi wa mradi huu utaanza mwezi Julai, 2018 na utakamilika mwaka 2019/2020.
Mheshimiwa Spika, kazi za ujenzi wa mradi huu zinahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 yenye urefu wa kilometa 198 kutoka Somangafungu, Lindi hadi Kinyerezi, Dar es Salaam. Lakini pia, kujenga Kituo cha Kupoza Umeme, lakini pamoja na mambo mengine mradi huu utaunganisha wateja mbalimbali na kusafirisha umeme utakaozalishwa kutoka Kituo cha Somangafungu chenye uwezo wa kuzalisha megawati 240. Mradi utafadhiliwa na Kampuni ya Sumitomo ya Japan kwa gharama ya dola za Marekani milioni 340.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:-
Mgodi wa GGM - Geita umekuwa ukitumia milipuko mikubwa wakati wa kulipua miamba ya dhahabu na kusababisha madhara makubwa kwa wananchi jirani na maeneo hayo, kama wale wa eneo la Katoma.
• Je, Serikali inafahamu kwamba nyumba za wananchi zinapasuka na baadhi ya watu huzimia kutokana na mshtuko?
• Je, Serikali inalitatua vipi tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tangu shughuli za ulipuaji zianze katika eneo la Katoma tarehe 23 Septemba, 2014 kumekuwepo na malalamiko kutoka kwa wananchi wa kijiji hicho kuwa milipuko inayofanywa na Kampuni ya GGM imekuwa ikisababisha sauti na mitetemo mikubwa na hivyo kuleta usumbufu na athari mbalimbali kwa wananchi na majengo yao.
Mheshimiwa Spika, kufuatia malalamiko hayo, mwaka 2014 Serikali kupitia Idara ya Madini na Halmashauri ya Wilaya ya Geita kwa kushirikiana na wananchi wa Mtaa wa Katoma pamoja Geita GGM, waliunda Kamati shirikishi ya kushughulikia malalamiko ya wananchi hao, ijulikanayo kama Blast Monitoring Committee (BMC). Kazi kubwa ya Kamati hiyo ilikuwa ni kukutana kila siku ya ulipuaji na kupokea malalamiko wakati wa mlipuko.
Mheshimiwa Spika, mwezi Machi, 2016 Wizara ilituma timu ya wataalam kutoka Wakala wa Jiolojia Tanzania – GST kwa ajili ya kufanya tathmini ya kina ya nyufa za nyumba ambazo zimesababishwa na GGM. Timu hiyo ilibaini uwezekano wa milipuko ya mgodi huo katika shimo la Katoma kuchangia nyufa katika nyumba na maeneo mengine ya Katoma pamoja na Nyamalembo Compound.
Mheshimiwa Spika, kutokana na taarifa hiyo ya GST, Wizara iliunda timu ya wataalam iliyojumuisha wawakilishi wa wananchi wa maeneo hayo ili kufanya utambuzi wa nyuma zenye nyufa. Kutokana na utambuzi huo, takribani nyumba 890 katika maeneo hayo zilibainika kuwa na nyufa. Hivi sasa uchambuzi wa kina unafanywa kuhusiana na hatua stahiki za kuchukua uchambuzi huo utatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2017 na taarifa yake itatolewa kwa wananchi.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE aliuliza:-
Jimbo la Kalambo lina kata 23 na vijiji 111; katika awamu ya kwanza na ya pili ya mradi wa REA ni vijiji vichache tu vilipata umeme.
Je, katika utekelezaji wa REA III ni vijiji vingapi vinategemea kupata umeme ili wananchi wa maeneo hayo waweze kujiandaa kujiendeleza kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephat Sinkamba Kandege, Mbunge wa Kalambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mradi kabambe wa usambazaji umeme vijijini awamu ya tatu umeanza rasmi tangu mwezi Machi, 2017. Mradi huu utajumuisha vipengele mradi vitatu vya densification, grid extension pamoja na off- grid renewable vinavyolenga kuongeza wigo wa usambazaji katika vijiji vyote vilivyobaki nchi nzima, vitongoji vyote, taasisi za umma, na maeneo ya pembezoni ambayo hayajafikiwa na miundombinu ya umeme. Mradi wa REA Awamu ya Tatu katika jimbo la Kalambo utajumuisha vijiji 89 kupitia vipengele
- mradi vya densification grid extension, utaokamilika mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye maeneo ya vijiji hivyo itajumuisha ujenzi wa njia ya msongo umeme wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 413.49; ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 745; pamoja na ufungaji wa transfoma 149. Kazi nyingine itakuwa ni kuwaunganishia umeme wateja wa awali 9,816 kazi ya gharama hii ni shilingi bilioni 36.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-
Leseni ya utafiti wa uchimbaji wa dhahabu ya Mabangu imechukua muda mrefu sana katika Kata za Nyakafuru na Bukandwe.
Je, ni lini mgodi wa uchimbaji dhahabu baina ya Mabangu na Resolute utaanza uzalishaji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Nyakafuru (Nyakafuru Gold Mining Project) unahusisha leseni 22 za utafutaji wa Madini zinazomilikiwa na Kampuni ya Mabangu Mining Limited ambayo ni Kampuni tanzu ya Resolute Tanzania Limited. Mashapo (deposit) katika mradi huu yamesambaa katika leseni hizi ambazo maeneo yake yana ukubwa ya kilometa 1.4 hadi 25.17. Mashapo yaliyogunduliwa katika leseni hizi kwa pamoja ndiyo yanaweza kuchimbwa kibiashara. Hata hivyo kati ya leseni 22, leseni tisa kampuni imeamua kuziachia.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Kampuni ya Mabangu Limited ni Kampuni tanzu ya Resolute Tanzania Limited, na kwa kuwa Kampuni ya Resolute Tanzania Limited iliyokuwa inamilikiwa na Golden Pride ya Nzega inadaiwa kodi na TRA, Kampuni ya Mabangu sasa inahusishwa na deni hilo la shilingi bilioni 147.007. Kutokana na Kampuni hiyo kuhusishwa na deni hilo, anayetarajiwa sasa kuwa mbia wa Kampuni ya Manas Resources mwenye jukumu la kufadhili mgodi ameamua sasa kupeleka mbele ufadhali wake.
Mheshimiwa Spika, mpango wa mradi wa Nyakafuru sasa utaanza kuzalishaji dhahabu mwezi Juni, 2019 baada ya masuala ya kodi kukamilika na kupata leseni ya uchimbaji pamoja na mazingira.
MHE. OMARY T. MGUMBA aliuliza:-
Vijiji 17 pekee kati ya vijiji 64 ndivyo vilivyopata umeme katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki na ni vijiji saba tu vya Ludewa, Mtego wa Simba, Kidugaro, Lung’ala, Mangala na Kinonko vilivyo katika orodha ya kupatiwa umeme katika REA III awamu ya kwanza ya mwaka 2017/2018.
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 47 vilivyosalia?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omary Tebweta Mgumba, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa vijiji 17 kati ya vijiji 64 ndio vilipatiwa umeme katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki. Vijiji vingine saba vitapatiwa umeme katika mzunguko wa kwanza wa mpango wa tatu wa REA ulioanza hivi karibuni. Kampuni ya State Grid ya Tanzania ambayo ndio mkandarasi wa eneo hilo tayari ameshaanza kazi katika vijiji hivyo saba ambavyo tumeviongeza. Katika eneo hilo kazi inajumuisha ujenzi wa njia ya kilometa 16.5 ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 pamoja na kilometa 16 za njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4. Kazi nyingine ni ufungaji wa transformer nane pamoja na kuunganisha wateja 256. Gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni 1.2 na unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2019.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vingine vilivyobaki vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa REA Awamu ya Tatu unaoendelea ambapo kwa pamoja utakamilika mwezi Julai, 2019 baada ya mzunguko kukamilika. Mradi huu utakamilika, kama nilivyosema mwaka 2020/2021.
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA aliuliza:-
Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) iliingia mkataba wa utafiti wa uchimbaji wa gesi na mafuta na Kampuni ya Mafuta ya Swala (SOGTP). Katika utekelezaji wa mpango huo wamegundua kuwepo kwa wingi mafuta ya petroli na gesi katika vijiji vya Kipenyo na Mtimbira Wilayani Malinyi katika Mkoa wa Morogoro.
(a) Je, ni lini uchimbaji wa visima na uvunaji wa mafuta utaanza rasmi katika maeneo hayo?
(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwatayarishia wananchi wa maeneo hayo ili kuondoa migogoro inayoweza kujitokeza baina yao na Serikali kama vile gesi ya Mtwara?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hadji Hussein Mponda, Mbunge wa Malinyi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti wa mafuta katika kitalu cha Kilosa – Kilombero unafanywa na Kampuni ya Swala Oil Gas Tanzania ulianza mwezi Februari, 2012. Utafiti huo ulianza baada ya kusainiwa kwa Mkataba wautafutaji kati ya Serikali kupitia TPDC na Swala mwezi Februari, 2012.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ambalo limeainishwa kwa ajili ya uchimbaji wa kisima hicho lipo katika Kijiji cha Ipera Asilia katika Hifadhi Tengefu ya Bonde la Kilombero.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kisima hicho kinatarajiwa kuanza kuchimbwa mwezi Septemba, 2018 kutegemea matokeo ya utafiti huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TPDC imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi wa maeneo kunakofanyika utafiti huo. Tarehe 06 hadi 17 Februari, 2017 TPDC kwa kushirikiana na Kampuni ya Swala ilitoa elimu ya masuala ya gesi na mafuta katika maeneo ya Halmashauri ya Mji huo ikiwa Mji Mkuu wa Mkoa wa Morogoro na Wilaya za Kilombero pamoja na Malinyi. Aidha, wananchi wa Kata ya Mtimbira, Njiwa pamoja na Kitete katika maeneo vijiji vya Mtimbira, Kipenyo, Ipera Asilia na Warama pia walipata elimu ya hifadhi ya mazingira pamoja na manufaa ya mradi huo.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza:-
Mji wa Ruangwa Mkoani Lindi una madini mengi lakini wachimbaji walio wengi wa madini hayo ni wachimbaji wadogo wadogo ambao hawana zana za kisasa za kuchimba madini.
Je, Serikali haioni haja ya kuwasaidia kwa kuwapa mikopo ili waweze kununua zana za kisasa za uchimbaji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Viti Maalaum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini imeweka vipaumbele vya kusaidia wachimbaji wadogo ili kufanya shughuli zao za uchimbaji huo kuwa wa manufaa kwao pamoja na kuongeza pato la Taifa. Vipaumbele hivyo ni pamoja na kuboresha sekta ya uchimbaji madini mdogo kwa kutoa ruzuku kwa wachimbaji hao wadogo ili waweze kuboresha shughuli zao kuwa za kisasa na kuboresha uchenjuaji na shughuli nyingine za uchimbaji. Lakini vipaumbele vingine ni kuwapa ushauri wa kitaalamu, taarifa za upatikanaji wa vifaa vya uchimbaji, mafunzo kwa vitendo pamoja na masoko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mwaka 2010 na 2013 Serikali ilitoa mikopo ya jumla ya shilingi milioni 910.195 kwa kampuni nane za wachimbaji wadogo. Aidha, kati ya mwaka 2013 na 2015 Serikali ilitoa ruzuku ya shilingi bilioni
• kwa wachimbaji 115 kwa ajili ya uchimbaji wao nchi nzima pamoja na Mkoa wa Lindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilianza kutoa ruzuku badala ya mkopo kwa wachimbaji wadogo kutokana na wachimbaji wadogo kushindwa masharti ya mikopo na hivyo kushindwa kurejesha na badala yake sasa wanapewa ruzuku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vipaumbele muhimu vinavyozingatiwa katika kutoa ruzuku hiyo ni pamoja na kumiliki leseni hai na halali ya shughuli za uchimbaji, kuwa na utambulisho wa kodi na mlipa kodi (TIN) na rekodi nzuri ya kulipa mrabaha na mapato mengine ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Jiolojia Tanzania wataendelea kufanya utafiti wa maeneo yote nchini ili wachimbaji wadogo nao sasa waweze kunufaika na rasilimali hii ya Taifa.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza:-
Katika maeneo ya Bugarama, Wilaya Ngara kuna Mgodi wa Kabanga Nickel uliodumu kwa miaka 30 sasa na kampuni mbalimbali zimekuwa zikiendesha shughuli zake kwenye mgodi huo na kuondoka tangu mwaka 1970 wakidai kuwa wanafanya utafiti huku bei ya Nickel katika soko la dunia akishuka.
Je, wananchi wa Ngara hususan maeneo ya Bugarama watanufaika na uwepo wa rasilimali hiyo iliyopo kwenye maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya Kabanga Nickel inamiliki mradi wa utafutaji madini ya Nickel katika eneo la Kabanga chini ya leseni namba moja ya mwaka 2009 iliyotolewa tarehe 02 Mei, 2009. Kampuni hiyo inaendelea kufanya utafiti wa kina ili kubaini kama mradi huo unaweza kuendelezwa kwa faida zaidi. Hivi karibuni bei ya madini ya Nickel ilishuka ghafla kutoka dola za Marekani 11 kwa pound mwaka 2010 hadi dola za Marekani 4 kwa pound kwa mwaka 2014. Kutokana na hali hiyo, kampuni inatarajia kuendeleza shughuli za uchimbaji mara baada ya bei hiyo kuimarika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi tarehe 4 Aprili, 2017 bado bei ya Nickel katika soko la Dunia ilikuwa dola 4.45 kwa pound ikilinganishwa na bei ya dola 11 mwaka 2009 mradi ulipokuwa ukifanyiwa upembuzi yakinifu. Mgodi unatarajiwa kutoa ajira 1,455 wakati ujenzi ukiendelea na wakati wa uzalishaji itaajiri Watanzania 800. Mradi utakapoanza kupata faida mambo yatakayofanya wananchi wanufaike ni pamoja na kulipa service levy, kutoa huduma za Maendeleo pamoja na ajira hapa nchini. Kadhalika tutajenga miundombinu kwa ajili ya kusaidia jamii.
MHE. DKT. MARY MICHAEL NAGU aliuliza:-
Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni mia tatu (300,000,000/=) kwa ajili ya ujenzi wa Mradi wa Maji wa Katesh, hata hivyo mradi huo bado haujaweza kuwanufaisha wananchi kwa sababu ya gharama kubwa za umeme zinazosababisha pampu za maji kufanya kazi kwa muda mfupi tu.
Je, Serikali haioni haja ya kupunguza au kuondoa kabisa tariff zilizopo ili gharama ya umeme iwe chini kidogo na kusaidia kusambaza maji kwa ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mary Michael Nagu, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu inasambaza umeme vijijini kwa kuweka kipaumbele kwenye huduma za jamiii ikiwemo Mradi wa Maji wa Katesh. Lengo la Mradi huu ni kuwezesha huduma hiyo kupatikana kwa urahisi na kwa gharama nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za kuendesha mtambo wa kusukuma maji kwa kutumia umeme ziko chini ukilinganisha na gharama ya kutumia mafuta ya dizeli. Gharama ya kuzalisha unit moja ya umeme ni shilingi 292 wakati gharama za kufua umeme kwa kutumia mafuta shilingi 450 hadi shilingi 800.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, gharama ya kuunganisha umeme kupitia Mradi wa REA ni shilingi 27,000 tu ambayo ni VAT kwa ajili ya Serikali kwa sababu Serikali imegharamia kwa asilimia 100.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa gharama za umeme ni nafuu kuliko gharama za mafuta, tunashauri Halmashauri husika itenge pesa kwa ajili ya kuunganisha umeme katika mitambo ya maji.
MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-
Mradi wa umeme wa 400KV kutoka Kinyerezi hadi Arusha umepita maeneo mengi ya nchi yetu ikiwa ni pamoja na Jimbo la Kibaha Mjini, uthamini wa mali za waathirika ulishafanyika toka mwaka 2015.
Je, Serikali itawalipa lini wananchi hawa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshiiwa Mwenyekityi, Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) inatekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolti 400 kutoka Kinyerezi hadi Arusha. Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolti 400 yenye urefu wa kilometa 664 pamoja na kilometa 40 kutoka Kibaha hadi Zinga na kilometa 60 kutoka Segera hadi Kange - Tanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu pia unahusisha ujenzi wa vituo vya kupoza umeme vya Chalinze, Segera, Kange, Tanga na Zinga Bagamoyo. Mradi huu utejengwa kwa mkopo kutoka Benki ya Exim ya China.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015 kazi ya uthamini wa mali za wananchi kutoka Kibaha hadi Chalinze ilifanyika ili waweze kulipwa fidia na kupisha ujenzi wa mradi. Kazi inayofanyika kwa sasa ni kukamilisha taratibu za maandalizi ya malipo kwa wananchi waliohakikiwa kwa ajili ya malipo ya fidia. Zaidi ya shilingi bilioni 21.56 zimetengwa na Serikali katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi wanaopitiwa na mradi katika maeneo ya Kisarawe, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini na Bagamoyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawa wataanza kulipwa fidia baada ya uhakiki wa madai ya fidia hiyo kukamilika. (Makofi)
MHE. DKT. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:-

Mkoa wa Mtwara una jumla ya Vijiji 869 na Vitongoji 1,826 na jumla ya Vijiji 372 vimethibitishwa kupatiwa umeme ikijumuishwa kufanya Vijiji vitakavyosalia kuwa 497 na hii ni sawa na wastani wa 23.6% ya utekelezaji wa huduma kwa kila Wilaya ndani ya Mkoa.

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kutekeleza miradi ya REA katika mkoa huu?

(b) Kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Mji wa Masasi ilitengewa Vijiji saba tu kati ya Vijiji 31, je, ni lini vijiji vilivyobaki vitapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Masasi, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kusambaza umeme vijijini katika vijiji vyote vya Tanzania Bara. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2021. Mradi wa REA III Mzunguko wa Kwanza unaoendelea unapeleka umeme katika vijiji 167 vya Mkoa wa Mtwara.

(b) Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Mji wa Masasi mradi wa REA III Mzunguko wa Kwanza unatekelezwa katika vijiji saba ambapo hadi kufika Januari, 2020 vijiji vitatu vya Mumbaka, Mlundelunde na Chanikanguo vimewashiwa umeme. Aidha, mkandarasi anaendelea na kazi za mradi katika Vijiji vya Mayula, Minazini, Mtakuja na Nangose A na B. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi zitakamilika mwezi Aprili, 2020. Gharama za kupeleka umeme katika Wilaya ya Masasi ni shilingi milioni 658.

Mheshimiwa Spika, vijiji 20 vilivyobaki katika Wilaya ya Masasi vinatarajia kupelekewa umeme kupitia mradi wa REA III Mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza mwezi Februari, 2020. Mradi huu utakamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. HALIMA A. BULEMBO aliuliza:-

Katika viwango vya kidunia vya umeme vile ambavyo tunavyofuata, kuna mabadiliko ya rangi za nyaya za umeme yaliyotokea tangu mwaka 2004 kwa nchi yetu ya Tanzania:-

Je, mabadiliko hayo yanafahamika kila mahali?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Halima Abdallah Bulembo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mabadiliko ya rangi za nyaya za umeme ni jambo la kawaida katika taaluma ya uhandisi wa umeme, hivyo mitaala yote ya mafunzo ya uhandisi wa umeme yanazingatia mabadiliko haya. Mabadiliko ya rangi za nyaya za umeme yalitokea mwaka 2004 na hivi sasa yanafundishwa nchini kupitia Vyuo vya Ufundi Stadi (VETA), Vyuo vya Ufundi Mchundo na Vyuo Vikuu. Aidha, somo la rangi za nyaya za umeme linafundishwa katika somo la Fizikia katika shule za Sekondari.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa umeme mkubwa kimazoea (high voltage) unakuwa na rangi tatu ambazo ni nyekundu, njano na bluu. Nyaya za rangi hizo huwa ni moto. Vilevile kwa umeme mdogo (low voltage) unaotumia njia tatu (three phase) unakuwa na rangi nne ambazo ni nyekundu, njano, bluu na nyeusi. Kwa upande wa umeme wa njia moja (single phase) unakuwa na rangi mbili nyekundu na nyeusi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na mabadiliko hayo yaliyoanza mwaka 2004 na kukamilishwa mwaka 2006 ya BS 7671 (British Standard) iliyowianishwa rangi mpya kwa umeme mkubwa (High Voltage) ni kahawia, nyeusi na kijivu kwa umeme mdogo (low voltage) three phase, rangi mpya ni kijani yenye mchanganyiko na njano, bluu kwa nyaya za moto ni kahawia nyeusi na kijivu. Kwa upande wa njia moja (single phase) unakuwa na rangi mbili za kahawia na bluu. Serikali itaendelea kutoa elimu kwa watu wote wanaohusika na matumizi ya rangi hizi ikiwemo wakandarasi, wafanyabiashara, wenye viwanda na wananchi kwa ujumla.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha miradi ya umeme Vijijini katika vijiji ambavyo bado havijafikiwa Wilayani Chunya?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa, Mbunge wa Lupa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi kabambe wa kusambaza umeme vijijini ambapo kwa sasa unatekelezwa kupitia Awamu ya III Mzunguko wa Kwanza unaoendelea utakaokamilika mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Chunya ina vijiji 43, kati ya vijiji hivyo, vijiji 37 tayari vimeshapatiwa umeme vikiwemo Vijiji vya Chokaa, Ifumbo, Isewe, Kibaoni, Lola, Kiwanja, Mlimanjiwa pamoja na Lupatingatinga. Utekelezaji wa kazi hii umekamilishwa na Mkandarasi STEG International Services na uligharimu shilingi bilioni 4.2.

Mheshimiwa Spika, vijiji vilivyobaki katika Wilaya ya Chunya vitapelekewa umeme kupitia Mradi wa REA Mzunguko wa Pili pamoja na miradi mingine ya densification kwa maana ya ujazilizi, itakayoanza mwezi Februari, mwaka huu 2020 na kukamilika ifikapo mwezi Juni, mwaka 2021.
MHE. MUSSA BAKARI MBAROUK aliuliza:-

Tanzania ina jumla ya Majiji sita likiwemo Jiji la Tanga; katika Majiji hayo kuna maeneo ambayo yako nje ya Jiji ambayo ni Mitaa, Vitongoji na Vijiji (Perry Urban); Kitengo cha Perry Urban kimekabidhiwa jukumu la kusambaza umeme wa REA III katika Majiji:-

Je, ni lini Perry Urban itaanza kusambaza umeme katika Jiji la Tanga?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea na utekelezaji wa miradi ya umeme iliyopo katika vijiji, vitongoji na maeneo mbalimbali kandokando ya miji na vijiji yaani Perry Urban. Awamu ya kwanza ya utelelezaji wa mradi huu umeanza katika Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa Pwani na kwa upande wa Dar es Salaam katika Wilaya ya Kigamboni. Utekelezaji wa mradi huu utakamilika mwezi Aprili, 2020. Baada ya kukamilika kwa mradi huu, Serikali itaanza kutekeleza mradi huu katika Mikoa yote nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jiji la Tanga Serikali imekamilisha upembuzi yakinifu na kubainisha kuwa miradi wa kupeleka umeme maeneo ambayo yako kandokando ya Jiji la Tanga unahusisha ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 15, ufungaji wa transfoma 15 kati ya hizo transfoma 4 ni za KVA 200, transfoma sita za KVA 100 na 5 za KVA 50.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi ya Perry Urban katika Jiji la Tanga pia utahusisha ujenzi wa njia ya Msongo wa kilovoti 11 yenye urefu wa kilomita 48.8, ufungaji transfoma 35; na kati ya hizo transfoma nane ni za 200KVA, 20 za 100KVA na saba za KVA 50. Kazi nyingine ni kuvuta laini ndogo ya kV 0.4 yenye urefu wa Kilomita 200. Wateja wa awali watakaonufaika na mradi huu katika Jiji la Tanga ni 5,125 ambao wanatarajiwa kupata umeme katika maeneo hayo. Utekelezaji wa mradi huu utaanza mwezi Julai, 2020 na kukamilika mwezi Machi, 2021. Gharama za mradi huo ni shilingi bilioni 7.5.
MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. BENARDETHA K. MUSHASHU) aliuliza:-

Mkoa wa Kagera una vijiji 134 ambavyo havijafikiwa na umeme wa REA; Biharamulo Vijiji 29, Bukoba Vijiji 9, Karagwe Vijiiji 8, Kyerwa Vijiji 31, Misenyi Vijiji 5, Muleba Vijiji 25 na Ngara Vijiji 27:-

(a) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA katika Vijiji hivyo?

(b) Umeme wa REA ulifika kwenye vijiji vingi lakini haukusambazwa: Je, mradi wa ujazilizi utaanza lini Mkoani Kagera ili wananchi waliorukwa wapatiwe umeme?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bernadetha Kasabago Mushashu lililoulizwa na Mheshimiwa Halima Bulembo, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi kabambe wa kupeleka umeme katika vijiji vyote nchini kufikia mwezi Desemba, 2021. Kwa sasa Mkandarasi Nakuroi anaendelea na kazi ambapo kufikia mwezi Oktoba, 2019 vijiji 82 vimewashwa umeme katika Mkoa wa Kagera na kazi ya uunganishaji wa wateja inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote vitakavyosalia katika Mkoa wa Kagera vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya pili, unaozunguka kuanza sasa ambao utakamilika mwezi Januari, 2020. Pia kukamilika kwa mradi huu mwezi Desemba, 2021 kutapeleka umeme katika maeneo yote katika Mkoa wa Kagera pamoja na Vitongoji vyake.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujazilizi awamu ya pili (Densification IIA) utatekelezwa katika Mikoa tisa na utaanza kutekelezwa kuanzia mwezi Novemba, 2019 hadi mwezi Juni, 2020. Mradi wa ujazilizi katika Mkoa wa Kagera utaanza kutekelezwa kupitia mradi wa ujazilizi awamu ya IIB (Densification IIB) utakaoanza kutekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2020 na kukamilika mwezi Machi, 2021. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, Megawati moja ya umeme inazalishwa kwa bei gani na inauzwa kwa bei gani (unit cost)?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini, inagharamia uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme hadi kwa mteja kwa kuweka miundombinu husika ya umeme. Kwa sasa gharama ya kuzalisha uniti moja (Kwh) ya umeme kwa kutumia chanzo cha maji ni shilingi 36 na gharama ya kuzalisha uniti moja ya umeme kwa kutumia gesi asilia ni wastani wa shilingi 150. Gharama ya kuzalisha uniti moja kwa mitambo inayotumia mafuta ya dizeli katika maeneo yaliyopo nje ya Gridi ya Taifa ni shilingi 720 kwa uniti moja yaani Kwh moja.

Mheshimiwa Spika, bei ya kuuza umeme inatokana pia na gharama za kuzalisha, kusafirisha na kusambaza umeme. Kwa sasa bei ya kuuza umeme ni wastani wa shilingi 242 kwa uniti yaani Kwh.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanzisha Wilaya ya TANESCO katika halmashauri ya Mji wa Mafinga ili kukabiliana na kasi ya ukuaji (kiviwanda na kimakazi) wa Mji wa Mafinga?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mufindi ina halmashauri mbili ambazo ni Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Halmashauri ya Mji wa Mafinga. Katika halmashauri ya Mji wa Mafinga tayari ipo ofisi ya wilaya ya TANESCO inayotoa huduma kwa wananchi wa Mji wa Mafinga pamoja na wananchi wa Wilaya ya Mufindi. Kwa sasa, Ofisi ya TANESCO iliyopo Mafinga inakidhi mahitaji ya kutoa huduma kwa wananchi wote wa Mji wa Mafinga. Hata hivyo, Serikali kupitia TANESCO itaendelea kuboresha huduma za ofisi hiyo ili kukidhi ukuaji wa shughuli za biashara za wananchi wa Halmashauri ya Mafinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kusogeza huduma zaidi kwa wananchi, TANESCO ilifungua ofisi ndogo (sub office) katika maeneo ya Igowole, Kibao na Mgololo. Ofisi hizi ni kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha huduma zinatolewa kwa urahisi kwa wananchi wa maeneo husika. Katika hatua za muda mfupi za kukabiliana na kasi ya ukuaji wa viwanda na makazi katika Halmashauri ya Mji wa Mafinga, Serikali kupitia TANESCO imeongeza njia ya pili ya umeme (Ifunda Feeder) ya msongo wa kilovoti 33 kutoka kituo cha kupooza umeme cha Tagamenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua nyingine, TANESCO ina mpango wa kujenga kituo kikubwa cha kupooza umeme (Grid substation) katika Halmashauri ya Mji wa Mafinga na Kazi ya upembuzi yakinifu imekamilika mwezi Januari, 2019 na ujenzi wa kituo unatarajiwa kukamilika Mwaka wa Fedha 2019/2020.
MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-

Ileje ina miradi iliyobuniwa kwa ajili ya kuzalisha umeme wa maji Mradi wa Luswisi na Ibaba, umeme huu ukizalishwa utaiwezesha Ileje kuwa na umeme wa kutosha kwa mahitaji yake yote na ziada na kuuza:-

(a) Je, Serikali itawasaidia vipi wananchi wa Ileje katika kukamilisha miradi hii?; na

(b) Je, Serikali itawasaidia vipi kuhakikisha usambazwaji wa umeme Ileje unaharakishwa?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mbunge wa Ileje, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuzalisha umeme wenye uwezo wa Megawati 4.7 katika eneo la Luswisi Wilayani Ileje. Gharama za mradi ni Shilingi Bilioni 19.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Umeme Ibaba unafadhiliwa na Serikali ya Ujerumani kupitia Kanisa la Moraviani – Tukuyu ambapo mradi huu ulibuniwa kuzalisha umeme kupitia jua na kusambaza kwa wanakijiji. Hata hivyo, utekelezaji wa mradi ulisuasua kutokana na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kupeleka umeme wa grid katika Kijiji hicho mwaka 2017. Kwa sasa mradi huo unasambaza nishati ya umeme katika maeneo ya Shule ya Msingi Ibaba na Kituo cha Afya Ibaba.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kuhakikisha Vijiji vyote vya Wilaya ya Ileje vinapata huduma ya umeme kupitia Miradi ya Wakala wa Umeme Vijijini (REA) awamu ya pili na awamu ya tatu inayoendelea. Utekelezaji wa miradi ya REA awamu ya tatu utakamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. JEROME D. BWANAUSI aliuliza:-

Serikali iliahidi kusambaza umeme katika Vijiji vya Matogolo na Nagaga.

(a) Je, ni lini vijiji hivyo vitasambaziwa umeme?

(b) Je, ni lini umeme jazilizi katika Jimbo la Lulindi utasambazwa?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jerome Dismas Bwanausi Mbunge wa Lulindi lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kusambaza umeme vijiini katika vijiji vyote vya Tanzania Bara. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwenzi Juni, 2021. Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea utapeleka umeme katika vijiji 67 katika Wilaya ya Masasi kupitia Mkandarasi JV Radi Services Ltd., Njarita Contractors Ltd na Anguila Contractors Ltd.

Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vya Matogolo na Nagaga vimeshapatiwa huduma ya umeme kupitia Shirika la Umeme nchini - TANESCO mwezi Februari, 2020. Kazi zinazoendelea kwa sasa ni maandalizi ya kusambaza umeme katika vitongoji vyote vya vijiji hivyo na kuunganishia umeme wateja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Ujazilizi katika Jimbo la Lulindi Mkoani Mtwara utaanza kutekelezwa kupitia Mradi wa Ujazilizi Fungu la Pili (IIB) ambapo jumla ya Mikoa 16 itanufaika ikiwamo Mtwara. Miradi ya Ujazilizi IIB itawezesha kupeleka umeme katika vitongoji 2,400 na kuunganishiwa umeme wateja wa awali 95,000. Gharama na mradi ni Dola za Marekani milioni 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi huu utaanza mwezi Mei, 2020 na kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 9.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza:-

Kijiji cha Segoma Wilayani Mkinga ni miongoni mwa vijiji vitakavyopata umeme wa REA III.

Je, kwa nini Serikali isitumie fursa hiyo kuunganisha umeme katika Sekondari ya Lanzoni iliyopo karibu na Kitongoji cha Darajani?
WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula, Mbunge wa Mkinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) pamoja na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) inatoa kipaumbele kupeleka umeme katika Taasisi za umma na za kijamii ikiwa ni pamoja na Shule za Awali, Msingi na Sekondari, Vyuo vya Ufundi Stadi, Vituo vya Afya, Zahanati, Visima vya Maji na Nyumba za Ibada.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katika Mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali kupitia TANESCO inaendelea na kazi ya kusambaza umeme katika Vijiji vya Mgamboshashui, Kumbamtoni na Mpale. Kazi hiyo inahusisha kupeleka umeme katika Shule za Sekondari Duga na Lanzoni zilizopo katika Jimbo la Mkinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Gharama ya kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo vitatu pamoja na shule hizo za Sekondari ni Shilingi Milioni 91. Utekelezaji wa kazi hiyo ulianza mwezi Machi, 2020 na utakamilika mwezi Mei, 2020. Jumla ya wateja wa awali zaidi ya 175 wataunganishiwa umeme.