Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Salma Rashid Kikwete (1 total)

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Awali ya yote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima na afya njema.
Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ushahidi wa kutosha kabisa kuhusiana na wizi unaofanyika kwenye biashara yetu ya korosho hasa katika Mikoa ya Mtwara na Lindi kutokana na kazi iliyofanywa na TAKUKURU iliyobainisha kwamba kumekuwa na upotevu wa kiasi kikubwa sana cha fedha ambacho ni takribani shilingi za Kitanzania bilioni 30 kutoka kwenye Bodi ya Korosho. Hata hivyo, mimi binafsi na naamini na wengine hawajasikia tamko lolote juu ya jambo hili kutoka Serikalini. Je, leo Serikali inatuambia nini kuhusu ubadhirifu huu uliotokea hapa nchini kwetu hasa kwa wananchi wa Mikoa ya Mtwara na Lindi kwa sababu jambo hili linaweza kutokea sehemu yoyote ndani ya nchi yetu? Naomba majibu ya Serikali.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Kikwete kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mwenendo wa vyama vyetu vya ushirika nchini umeweza kuanza kuonyesha dalili ambayo si nzuri kwa sababu ya upotevu mkubwa wa mapato ya fedha za ushirika ambayo pia inapelekea kukatisha tamaa wakulima wetu kote nchini. Ni kweli kwamba Serikali imechukua hatua thabiti kufanya mapitio ya vyama vyote vya ushirika kwa mazao yetu makubwa ambayo yanatuingizia pato kubwa nchini na yanaleta manufaa kwa wakulima wetu. Tulianza na zao la korosho baada ya kupata tuhuma hizo tulipeleka wakaguzi COASCO na baadaye tukapeleka TAKUKURU kwa uchunguzi zaidi lakini kupitia vikao mbalimbali vya wadau wa mazao yenyewe huwa wanabainisha kasoro zinazojitokeza kwenye uendeshaji wa mazao hayo.
Mheshimiwa Spika, kwa kumbukumbu zangu na kwa kuwa mimi mwenyewe pia ni mdau wa zao la korosho tulikuwa na kikao Bagamoyo ambacho pia kilitoa taarifa ya ubadhirifu wa shilingi bilioni 30 kwa Bodi yetu ya Korosho Mkoani Mtwara. Serikali iliunda timu maalum pamoja na TAKUKURU kwa ajili ya uchunguzi, lakini baadaye uchunguzi ulibaini kwamba hasara ile ni ya shilingi billioni sita na siyo shilingi bilioni 30 kwa Bodi ya Korosho na hasara ile haikusababishwa na Bodi ilisababishwa na Vyama Vikuu pamoja na Vyama vya Ushirika vilivyoko kwenye ngazi za kijiji na kata. Hatua kadhaa zimechukuliwa kwa watendaji wote ambao wamehusika kwenye ubadhirifu. Vyama vya msingi na vyama vikuu vyote vilifanyiwa uchunguzi na hatua thabiti zimeanza kuchukuliwa na nyingine zitaendelea kuchukuliwa kadiri tunavyoendelea.
Mheshimiwa Spika, lakini nataka niwaambie Watanzania kwamba jambo hili la ushirika haliko kwenye zao la korosho pekee liko pia kwenye mazao kama tumbaku, pamba, kahawa, chai na mazao mengine yote makuu. Tumeanza kufanya mapitio ya kaguzi za kina kwenye ushirika wa mazao haya kubaini ubadhirifu ili tuweze kufanya marekebisho ya namna nzuri ya kuendeleza mazao haya ili wakulima waweze kupata tija. Kwa sasa tunaendelea na zao la tumbaku, ukaguzi unaendelea na tumeanza na chama kikuu sasa tunaenda kwenye AMCOS tukishamaliza tutaenda kwenye mazao mengine yakiwemo pamba, kahawa, chai na yale yote ambayo yameunda ushirika kwa lengo la kuwalinda wakulima, kuhakikisha kwamba fedha za wakulima zinawafikia wakulima wenyewe na hii ni pamoja na kuondoa tozo ambazo zimewekwa na vyama vyenyewe ambavyo pia vinamletea hasara mkulima.
Mheshimiwa Spika, naomba kusisitiza tu kwa Mheshimiwa Mbunge kwamba hatua hizi zinaendelea kuchukuliwa na tutaendelea kuhakikisha kwamba ushirika nchini unaimarika na unaongozwa na watu waaminifu ambao hawatawaletea hasara wakulima wetu, ahsante.