Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Alfredina Apolinary Kahigi (15 total)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuongea machache. Mimi nitazungumzia kuhusu mambo ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mwenyekiti wangu Profesa Ibrahim Lipumba, mchumi duniani pamoja na baraza lake, naahidi sitamuangusha Mheshimiwa Lipumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu, katika Kamati yetu ambayo tumekaa kuna Wilaya 64 ambazo zinakosa Hospitali za Wilaya, mojawapo ni Wilaya yangu ya Bukoba Vijijini hatuna Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Bukoba hawana hospitali ya wilaya, wanatembea mwendo mrefu au wanalipa gharama za kwenda kutafuta matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo gharama ambazo wanalipa wanakuwa hawakuzipanga kusudi waweze kwenda kutibiwa huko. Kama wangekuwa na hospitali katika wilaya yao wasingepata usumbufu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iwaangalie kwa jicho la huruma iwajengee Hospitali ya Wilaya. (Makofi)



Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Wilaya ya miaka mingi sana. Wilaya ya Bukoba ni Wilaya ya miaka mingi sana, Wilaya zote ambazo ziko katika mkoa wetu zimetokana na Wilaya hiyo, lakini yenyewe haina hospitali. Watu wengine kwa kukosa hela za kwenda kwenye hospitali za private wanakunywa dawa za mitishamba ambazo hazina vipimo vyovyote, wengine wanakufa, naomba Serikali iliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini namshukuru Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, lazima nimseme jina, pamoja na Naibu wake na wataalam wao, ni watu wenye moyo mkunjufu. Hili suala tumeliongelea na wameliona na wameahidi kutusaidia katika bajeti hii ambayo tutakaa waweze kutuweka katika list hiyo, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka huko, kwa kuwa, dakika ni kidogo niizungumzie Ofisi ya Utumishi. Ninamuunga mkono Rais wangu Mheshimiwa Dkt. Magufuli, kazi aliyofanya siidharau ya kutumbua, kazi ya kutumbua na iwe endelevu, ni kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ninawasikitikia madereva ambao walitumbuliwa. Madereva mimi najua ujuzi wao, leseni zao, kama wanajua kusoma na kuandika, hivyo ndivyo vinavyowafanya wawe na kazi lakini maskini ya Mungu wametumbuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara hiyo iwaangalie sana watakaokuwa wanaajriwa wawaangalie wasiwe wanawafukuza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia suala la maji lililopo katika Jimbo langu. Katika Kata ya Kanyangereko, Vijiji vya Butahyaibega, Bulinda wakati wa kiangazi wanapata shida sana mito inakauka. Hivyo akinamama wanapata shida sana na kauli ya Serikali ni kumtua mama ndoo kichwani. Sambamba na Kata ya Bujugo, Rubafu na Maruku, shida ni hiyohiyo ya maji safi na salama. Naomba suala hili la maji litafutiwe ufumbuzi maana ni kila mwaka shida hii inajitokeza, sijui Serikali itawasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu Wizara ya Mifugo na Uvuvi; je, ni lini Serikali itawapiga marufuku wafugaji kulisha mifugo yao barabarani kwa sababu inaweza kusababisha ajali kwa madereva na sehemu zingine imekwisha tokea. Hivyo, naomba lishughulikiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kuuliza, je, ni lini Serikali itakarabati barabara zilizo chini ya kiwango.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana kwa kazi mnazozifanya, tunaziona, kazana sana. Nashauri katika hospitali nyingi za vijijini hazina vitendea kazi vya kutosha, viongezwe; pili, wafanyakazi ni shida, unakuta wako wawili kazi zinawawia nyingi, wanachoka, hivyo basi lifanyie kazi suala hili waajiriwe wafanyakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu dawa, baadhi ya dawa nyingine hatuzipati, hasa zile muhimu; fuatilia suala hili, tunaambiwa hazipo tununue katika maduka ya dawa ya watu binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, wazee sehemu nyingine hawajapatiwa vyeti vya kutibiwa bure, wasaidie wazee; kama Kata ya Kanyangereko, Maruku, Nyakato na nyingine nyingi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami ili kuweza kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyotuletea mbele yetu. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake ambayo imejaa mambo mazuri mengi, inasomeka na inaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja nichangie hoja chache ambazo nimezipangilia. Nianze na upande wa kilimo. Mimi natokea Mkoa wa Kagera. Hatujamaliza mwaka mzima Mheshimiwa Rais amepunguza tozo ambazo zilikuwa zinabambikizwa wakulima wa kahawa lakini nami lazima niungane na Wabunge ambao jana walizungumzia zao la kahawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la kahawa, sijui hao ambao wameleta kilio tena kwa mara nyingine wamepewa mamlaka na nani kushusha bei ya kahawa na kuirudisha kilo moja Sh.1,000. Wakulima wa kahawa sisi tunakaa pembezoni mwa nchi ya Uganda na kahawa nyingi huwa zinaenda sehemu ya Uganda, nina wasiwasi hata kama wakiweka ulinzi wa namna gani kahawa zitavushwa zitaenda Uganda na pato la Taifa litapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hapa Mheshimiwa Waziri Mkuu yupo, Waziri wa Kilimo yupo, naomba hili suala walishughulikie haraka sana iwezekanavyo kabla kahawa hazijavushwa kwenda Uganda. Binadamu ana akili kali sana huwezi kumzuia, hata ukiwa na bunduki atafanya njia zozote zile atavusha hizo kahawa. Toka juzi wamenipigia simu wanaomba hili suala tuliongelee kwenye Bunge. Sasa maadam tuko kwenye Bunge, kilio cha wananchi nimekifikisha, hivyo naomba hatua za haraka zichukuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi upande wa barabara, kuna Wilaya tatu ambazo zina barabara ambayo haina lami lakini barabara ni nzuri. Nashukuru Serikali ya Mheshimiwa John Joseph Magufuli imeshughulikia barabara na nchi yetu ni kubwa. Nishauri kutoka Muleba Kusini kwenda Bukoba Vijijini kwenda Wilaya ya Karagwe tuna barabara ya udongo. Niishauri Serikali kwa kipindi hiki ambacho tunaingia kwenye bajeti, barabara hiyo waitengeneze kwa kiwango cha lami maana ni kilometa 74. Naomba hilo walizingatie kwani barabara hiyo inasaidia Wilaya tatu, kuingiliana ni kitu cha maana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Omurushaka - Murongo katika Wilaya ya Kyerwa, ina kilomita 120 inaungaisha nchi mbili, Tanzania na Uganda.Mheshimiwa Waziri wa Miundombinu, naomba na barabara hiyo waishughulikie. Ukienda upande wa Uganda unakuta wana barabara ya lami, ukija huku ni barabara ya udongo. Mvua zikinyesha magari yanapita kwa shida sana, hivyo, kama wakitengenezewa wakawekewa lami itakuwa ni nzuri zaidi na itadumu kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoke kwenye suala hilo nije kwenye afya. Kikao kile tulichomaliza niliomba Wilaya ya Bukoba Vijijini na sisi tujengewe Hospitali ya Wilaya kwani hatuna Hospitali ya Wilaya. Wilaya zote zina Hospitali za Wilaya, lakini ni Bukoba Vijijini peke yake ndiyo haina Hospitali ya Wilaya. Nina matumaini makubwa na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na Naibu wake waliniahidi kwamba watatujengea na sisi hospitali. Nimesikia wanasema Wilaya 27 watajengewa hospitali, sina uhakika kama na Wilaya yetu wameiweka, kama wameiweka nitashukuru sana na sisi kupatiwa nafasi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina akili timamu, naongea kitu ambacho nakijua na wamekuwa na mazoea nikisimama kuongea wanaanza kubeza, lakini siyo wote ni wale ambao akili zao sijui zikoje. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika bajeti hii kweli waikumbuke Wilaya yangu, watujengee Hospitali ya Wilaya tuachane na kwenda kwenye hospitali za private na sisi tuwe na hospitali yetu ya kujitegemea moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka upande wa afya nakuja kwenye siasa. Sina vya sijui ni ukurasa gani na nini mimi natwanga tu. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika siasa tuna Msajili wa Vyama vya Siasa, nipende kumtia moyo na kumshukuru sana. Ni Jaji mwenye akili nzuri sana, ni mtiifu na nimshukuru Mheshimiwa Rais aliyemteua kumpa nafasi hiyo. Ujumbe nataka ufike kwa Mheshimiwa Rais; huyu baba hapaswi kumtoa katika nafasi hiyo, ni mvumilivu, ni mstahimilivu ametukanwa sana, lakini mimi nimemsikiliza sana ni baba mwenye moyo safi sana, baba anayependa kulea vyama vyetu, Mheshimiwa Rais aendelee kumweka katika nafasi hiyo mpaka tujue ustaarabu ni nini, anatukanwa bure baba wa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili na Mheshimiwa Mutungi alipo ajue kwamba Mama Kahigi nipo pamoja naye, Mheshimiwa Rais namshukuru sana kwa kutupa Msajili mwenye busara kama huyu, anatukanwa bure, Mungu atawaona. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, niende kwenye miundombinu. Kwenye miundombinu naishukuru Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Mkoa wangu wa Kagera tuna uwanja wa lami ni mzuri mno, lakini hatuna taa za kwenye uwanja ndege haiwezi kuteremka usiku. Ni kitu kimoja tu hicho ambacho wanaweza wakatusaidia, wakatuwekea taa za ndege kuweza kushuka usiku vinginevyo uwanja ni mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru Mheshimiwa Waziri Profesa Makame Mbarawa pamoja na Naibu Mawaziri wake wawili, na watendaji wote wa Wizara, kwa kazi zao nzuri tunazifuatilia na tunaziona. Napenda kuwatia moyo Mola awazidishie nguvu mna kazi kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, maoni, katika Mkoa wangu wa Kagera tuna madaraja ambayo ni mabovu naomba na sisi mtutizame, yatengenezwe yawe imara.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja wa ndege, kiwanja ni kizuri sana kina viwango vya kutosha. Tatizo ni taa ndege haziwezi teremka usiku zinaishia Mwanza. Lakini tungekuwa na taa wasafiri wanaotoka Dar es Salaam, Arusha, Mwanza usiku wasilale Mwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu meli, sina shaka swali hili mnashughulikia. Naomba mkazane na ikibidi tuwe wa kwanza kutengenezewa meli wananchi wana shida sana muda umekwenda sana nawaomba sana sana tuwaonee huruma, mazao yetu yanaoza na kipato chetu tunategemea usafiri wa meli. Nawatakia kazi njema. Hapa Kazi Tu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniamsha siku ya leo nikiwa mzima wa afya na kuweza kuchangia hotuba ya Wizara ya Ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru wewe mwenyewe kwa kunipa nafasi ya kuweza kuongea. Namshukuru Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Naibu wake kwa hotuba nzuri ambayo ametusomea hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitachangia mambo machache katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara hii nimeona kuna changamoto ambazo napaswa kuziongelea kama mbili/tatu hivi. Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii, kuna tatizo la upotevu wa watu wazima na watoto wadogo katika nchi yetu. Nchi yetu ilikuwa kweli ni ya amani na utulivu lakini hili janga ambalo limejitokeza kwa sasa hivi linatutia simanzi kubwa sana, linatuaibisha, sijui ni watu gani ambao wanataka kutuchafulia amani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri pamoja na Jeshi lake la Polisi suala hili walifanyie kazi kwa hali ya juu sana maana sasa hivi watu hatuna amani, tuna watoto wakienda shuleni tunakuwa na wasiwasi watatekwa, watauawa kwa sababu ya watu waovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana Serikali yangu maana ndiyo mnaobeba huu msalaba. Kuna watu wengine wanajipenyeza wenye nia mbaya ya kuchafua jina la nchi yetu ili mwonekane ni wabaya kumbe wakati mwingine Serikali haina ubaya wowote. Naomba Waziri alifanyie kazi kweli kweli suala hili. Sina ubaya wowote na Serikali yangu, sina ubaya wowote na maaskari lakini inasikitisha, walifanyie kazi. Hiyo ni namba moja kwa sababu dakika ni kidogo nitaongea kidogo kidogo kusudi niweze kueleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye suala la Polisi. Maaskari sina ugomvi nao, nawapenda sana na wao wanipende sana lakini maaskari jamani wajirekebishe. Kuna matrafiki, huko njiani wanasumbua sana hasa hawa wa PT. Kuna makosa mengine ni madogo madogo mnaweza mkaongea, lakini wanakupiga faini, wanatusumbua yaani sasa vyombo vya moto inaonekana kama hatuna amani navyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba na lenyewe hilo waliangalie, wawaambie hao maaskari waache kusumbua watu, hasa wa bodaboda wanawasumbua sana na wakati mwingine na kuwapiga wanawapiga. Kwa kweli haki za binadamu zinavunjwa na maaskari wakorofi ambao wanafanya vitu ambavyo hawakuagizwa kuvifanya waache. Waheshimiwa Wabunge, wanaviona vitu vingine sisemi kwamba ni mimi hapa mama Kahigi, hapana, wanafanya mambo ya namna hiyo, yanatuudhi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka hapo nakuja upande wa nyumba za maaskari. Nyumba za maaskari zinasikitisha sana kwani zimepitwa na wakati. Nyumba za mabati utadhani maaskari wetu ni bata au kuku kulala kwenye nyumba mbovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tumeambiwa wanajengewa nyumba 400 ni kidogo sana, naomba wakaze buti, wawajengee nyumba, wakae katika nyumba nzuri na wawe na maisha mazuri na familia zao wajisikie kama vile ambavyo sisi tunavyojisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka katika hilo, nafikiri wamenisikia, watawashughulikia, nakuja kwenye maslahi yao. Maaskari wengine wanaongezwa vyeo lakini mshahara hawaongezwi. Naomba na lenyewe hilo waliangalie, wawaongeze mshahara ili wafanye kazi zao wakiwa na mioyo safi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoka hapo nakuja kwenye suala la passport. Kwa kweli passport ni kitu kizuri sana lakini kiasi ambacho wameweka kwa wananchi wetu wa vijijini nina wasiwasi hawataweza kulipia hizo passport. Kulipia Sh.150,000 ni labda kwa Wabunge na watu wenye vyeo vya hali ya juu ndiyo watakaoweza. Naomba wapunguze gharama hiyo ili watu wetu waweze kuwa na passport. Mtu mwingine anapata safari ya kwenda nchi za nje lakini passport inamkwamisha anashindwa kwenda kwa sababu hana hela ya kuweza kulipia hiyo passport. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nako natoka, la mwisho ni kuhusu kesi kukaa muda mrefu. Naomba upelelezi uwe unafanyika haraka sana, wasifanye kukawa na mrundikano wa kesi, wafanye haraka haraka, kesi ziende mahakamani watu waweze kuhukumiwa, mambo yaende sawasawa sio watu kuwazungushazungusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, nashukuru sana kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji, Naibu wake pamoja na watendaji wote wa Wizara. Mungu awabariki sana katika kazi ngumu wanayoifanya. Tunaona wanajitahidi, lakini nina machache ya kushauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba wajitahidi sana pale wanapoona Waheshimiwa Wabunge wanapiga kelele. Ni kweli shida ya maji ni kubwa sana hasa wakati wa kiangazi, ni janga kubwa. Katika Mkoa wangu wa Kagera, Wilaya ya Karagwe ina mradi uliopata ufadhili toka India. Ni Mradi wa Maji ya Rwakajunju wenye zaidi ya miaka kama 20 na zaidi. Je, Serikali ina kauli gani kuhusu mradi huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu aliusemea Mheshimiwa Marehemu Sir George Kahama, Mheshimiwa Gosbert Blandes na mpaka sasa Mheshimiwa Innocent Bashungwa, na mimi nausemea. Tunaomba jibu. Wananchi wa Karagwe wana shida sana ya maji, waonewe huruma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia na baadhi ya Kata za Bukoba Vijijini wana shida ya maji waokolewe na adha hii ya maji.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namkushukuru Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa hotuba yako nzuri, napenda kupongeza Kamati ya Viwanda na Uwekezaji kwa maoni yao, naomba Serikali iyafanyie kazi maoni hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi ushauri wangu katika Wizara hii naomba katika Mkoa wangu wa Kagera tupatiwe viwanda vidogo vidogo, tunalima maparachichi kwa wingi yanaharibika mashambani, nanasi zinastawi sehemu nyingi, hata ndizi zinaweza kukaushwa na kuwa- packed katika mifuko ya plastiki, tukitumia utaalamu tutapata hela za kujikimu shida zetu. Mkoa wa Kagera ni wa mwisho kwa umaskini au ni wa pili kutoka mwisho, Mheshimiwa Waziri ikupendeze utuonee huruma walau tufikirie tuwekwe kwenye list ya watakaofikiriwa kuanzishiwa viwanda vidogo vidogo na vya kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawatakia kazi nzuri na ya mafanikio, Mungu awabariki sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namkushukuru Mheshimiwa Waziri wa Kilimo pamoja na Naibu wako kwa hotuba yenu nzuri, napongeza Kamati ya Kilimo kwa maoni yao. Naomba Serikali iyafanyie kazi maoni haya na ushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mkoa wa Kagera tuna kilio cha mnyauko wa migomba na ni wa miaka mingi sasa. Ni tatizo gani Serikali imeshindwa kumaliza tatizo hili? Naomba itusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa miwa (outgrowers) katika kiwanda cha Kagera Sugar wanauza miwa yao kwa mwekezaji, wanalipwa baada ya miezi mitatu, je, kuna uwezekano wa kumshauri mwenye kiwanda ili awalipe ndani ya wiki mbili ili kunusuru mashamba yao yasiharibike? Mkulima anamkopesha mwekezaji miezi mitatu miwa yake, kumbuka hawekewi riba yoyote, Mheshimiwa Waziri wasaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nawatakia kazi njema Mungu awasaidie katika kazi zenu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na pongezi. Sina budi kuipongeza Wizara ya TAMISEMI, Waziri Jaffo, Naibu Mawaziri wake, Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Kandege pamoja na Makatibu wao wote kwa kazi zao nzuri na usikivu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi, Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini tumepewa milioni 900 za force account na Serikali. Fedha hizi tumezigawa katika kata mbili; Kata ya Katoro milioni 500 na Kata ya Kishage milioni 400. Katika Kata hizo wanajengewa nyumba za mama na mtoto, nyumba za Waganga kila kata nyumba moja moja na mochwari moja moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo, tuna shida ya Wahandisi wa Ujenzi, tunaomba Serikali itusaidie wahandisi hao maana Wahandisi wa kujitegemea gharama zao ni kubwa sana. Tuna Wahandisi wa TARURA tukiwaomba wanasema wao ni wa barabara. Tunaomba sana watuonee huruma katika shida hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru zahanati tunazo, vituo vya afya angalau tunavyo na dawa zipo, shida hatuna Manesi, pia na Waganga ni wachache sana, tunaomba na eneo hilo tusaidiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu; tuna shida sana na Walimu wa shule za msingi na sekondari kwani tuna upungufu sana. Vile vile tusaidiwe nyumba za Walimu ni shida, vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamwomba Mheshimiwa Waziri katika bajeti yake, basi aiangalie Wilaya yetu ya Bukoba Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, nashukuru.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Kamati yangu ya Katiba na Sheria. Naipongeza Kamati yangu ya Katiba na Sheria kwa ushauri wao mzuri walioutoa, naiomba Serikali ipokee mapendekezo yao na iyafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi katika Kamati yangu ya Katiba na Sheria tumeshauri bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria inapotolewa katika Bunge itolewe kwa muda muafaka ili iweze kufanya kazi maana vijijini huko mahakama za wilaya ni chache na mahakama za mwanzo nyingi zimechoka kwa kuwa ni za muda mrefu, zina nyufa. Tunaomba wawe wanapewa hilo fungu ili waweze kujenga mahakama maana wananchi wanatembea mwendo mrefu kwenda kwenye kesi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumeshauri Majaji, Mahakimu wa ngazi za chini waweze kupewa mafunzo, waweze kufanya kazi zao kwa weledi wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ambacho tumeshauri, Mahakama Kuu hawana mashine maalum, watu wakienda pale wanakwenda kwa kupapaswa wakiwa wanaingia ndani, hiyo na yenyewe ni hatari, ni vizuri na wenyewe wawekewe mashine maalum wasiwe wanaingia hivihivi maana kwenye viwanja vya ndege, sehemu zingine hata na makanisani mahali pengine wana mashine za kuangalia wale watu wanaoingia mle ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ambacho tumeshauri kwenye magereza, kuna wafungwa ambao wamekaa muda mrefu ambao wana wenzi wao, kama ni wanaume wameacha wake zao nje, kama ni wanawake wameacha waume zao nje, ni haki yao kutimiza tendo la ndoa. Tumeshauri mkakati ufanyike watengenezewe sehemu wawe wanakutana maana mtu kukaa miaka kama sita, saba mbegu za uzazi zinaweza zikaharibika, lakini kama wakitengenezewa sehemu ni vizuri na wenyewe wakaweza kukutana, tendo la ndoa ni haki yao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ambacho tumeshauri katika Kamati yangu, upande wa mahakama, Majaji na Mawakili wanapaswa wapewe weledi wa hali ya juu sana, wapewe semina ili waweze kufanya kazi zao vizuri, pale Mawakili wanapotetea wateja wao waweze kutetea kwa umahiri sana, bila kuwapa kozi za maana wanaweza wakafanya mambo ndivyo sivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu ni hayo machache, nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Medard Kalemani, Naibu wake, Mheshimiwa Subira Mgallu pamoja na watendaji wote wa Wizara. Mungu awatie nguvu kwa kazi yao hii ngumu, tuonaona wanavyochapa kazi. Maoni yangu ni kwamba katika Wilaya yangu ya Bukoba Vijijini bado kuna kata nyingi ambazo umeme haujafika, ni nyumba chache zimepata umeme, REA I, II ilikuwa unarukaruka nyumba nyingi, nikiwa na maana vitongoji na vijiji.

Mheshimiwa Spika, nashauri Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu tusaidiane ili walau wapate nao mgao huo. Kuna wenye viduka vyao wanahitaji vitu vingine kuweka katika friji lakini wanashindwa, wanatumia jenereta. Mafundi wa magari kuchomelea vyuma umeme ni shida wasaidie wananchi ili kazi zao ziende vizuri.

Mheshimiwa Spika, lingine, katika vijiji hivyo kuna vitongoji ambako kuna zahanati; katika zahanati hizo kuna dawa zinazopaswa kuhifadhiwa katika friji; umeme hawana na hivyo dawa zinaharibika. Niwaombe hilo liangaliwe kwa jicho la huruma, siwezi kutaja ni vijiji vingapi, ni vingi havina umeme.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu najua ninyi ni wasikivu san sana. Maoni yangu msiyatupe katika dustbin tufikirie tupatiwe walau sehemu kubwa, wanufaike na umeme.

Mheshimiwa Spika, mwisho nawatia moyo Mungu awabariki sana, lakini tukumbuke sana Bukoba Vijijini umeme ni shida. Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri na yenye matumani. Nawatia moyo wasikatishwe tama, wakaze moyo ila watende haki na Mungu atakuwa nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri; katika umeme Wilaya ya Bukoba Vijijini kuna maeneo mengi sana hawajapatiwa umeme na Serikali inasema ifikapo mwaka 2020 vijiji vyote vitakuwa vimeingiziwa umeme wa REA III. Kutokana na utekelezaji wa utaratibu kwa mradi inaweza ikamalizika bila umeme kufika, kwa hivyo ni vigumu viwanda kufanya kama wanavyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo; nashauri kuna wakulima wadogo wadogo wa miwa lakini wananung’unika malipo wanayolipwa katika Kiwanda cha Kagera Sugar ni kidogo sana, kuwepo na mfumo maalum wa kuwatetea waweze kulipwa malipo ya haki sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji; Mkoa wa Kagera Ziwa Victoria limechukua sehemu kubwa karibu wilaya zote, lakini ni manispaa pekee ndiyo haina shida ya maji, wilaya zilizobaki maji ya Victoria wanayaona tu, Serikali ijitahidi wilaya zote zisambaziwe maji kwa sababu ziko katika mkoa huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri mwingine; Sheria ya Kodi, Sura 332; kodi ya taulo za kike zitolewe bure kusudi wanafunzi wa shule za msingi na sekondari waweze kujihifadhi pindi wawapo kwenye hedhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nawatakia kazi njema katika kazi zao na Mungu awaongoze tena vizuri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Nianze na Wizara ya Elimu, Wizara ya Elimu mimi nitaanza na Walimu. Walimu ni kioo cha jamii lakini Walimu kuanzia mavazi, kuja maadili, kuja na mahusiano na jamii Walimu wana upungufu. Kwa mfano mavazi, Walimu hapo zamani tulikuwa tunawaona ndiyo watu ambao wanafundisha watoto, kujipenda, kuvaa vizuri, kuwa wasafi lakini Walimu wa sasa hivi wanasikitisha mavazi wanayovaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Walimu wa kike, baadhi siyo wote wanavaa nguo ambazo hazina heshima yoyote, nguo ambazo ni fupi kiasi kwamba wanafunzi hawajifunzi kitu chochote kwa mavazi wanayovaa. Niombe Wizara ya Elimu katika suala hilo la mavazi iliangalie sana iwape mwongozo kusudi wawe wanavaa nguo ambazo wanafunzi wataona kwamba na sisi tujifunze kutoka kwa Walimu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwa watoto wa kiume wanavaa ma-jeans tisheti, jeans hilo akilivaa wala kulinyoosha halinyooshwi utadhani ng’ombe amelitafuna amelitema ndiyo anakuja amelivaa mwanafunzi akiona namna hiyo kwa kweli haileti ustaarabu wa aina yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka katika mambo ya mavazi, nije katika maadili. Sisi ambao tumetoka vijijini Walimu wa vijijini wanasikitisha, baadhi lakini siyo wote. Wanalewa, wanakunywa pombe yaani Mwalimu anakuta wanacheza ngoma na yeye anafunga kanga anacheza ngoma na wanafunzi wanamwona, kwa kweli haileti heshima yoyote. Mwalimu ni kioo kama nilivyosema, hapaswi kunywa pombe akalewa mpaka na wanafunzi wale ambao anawafundisha wakamwona kesho yake akija darasani watajifunza kitu gani, ni aibu tupu. Niombe Wizara ya Elimu, wajaribu kuwakanya, wajaribu kujieshimu ili watoto wetu waweze kuchukua maadili mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye mahusiano ya Walimu na jamii. Kuna baadhi ya Walimu wanajifanya Miungu watu. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri, Profesa Ndalichako na uongozi mzima kwa kitendo ambacho walitufanyia watu wa Kagera kwa mtoto yule aliyepigwa mpaka akauwawa lakini walisuuza nyoyo za Wanakagera au na wazazi wote Tanzania nzima kwa yule Mwalimu aliyempiga na ameadhibiwa kutokana na makosa yake, lakini bado baadhi ya Walimu wana tabia ambayo si nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi juzi niliangalia kwenye WhatsApp, kuna Mwalimu sehemu za Mbeya amepiga mtoto wa miaka nane, alimfunga miguu juu, kichwa chini mtoto wa miaka nane, eti ameshindwa kufanya hesabu, akampiga mpaka akamvunja uti wa mgongo. Mheshimiwa Waziri nitapenda hilo alifuatilie sana, tujue matokeo ya huyo mtoto. Sisemi vitu vya longolongo nasema vitu ambavyo nimeviona, amenisikitisha mno hata angelikuwa ni mtoto wako ungelia, mimi nilisikitika sana sana. Amempiga, wazazi wake wamemshughulikia yule mtoto mpaka hela zimewaishia, sasa hivi wamelipeleka mpaka kwa Mkuu wa Wilaya. Naomba Mheshimiwa Profesa Ndalichako alifuatilie hilo suala awasaidie wale wazazi wana masikitiko makubwa na mtoto wao. Bado kuna Walimu ambao ni wakorofi, wanajifanya ni Miungu watu, huyo Mwalimu nasikia wamemtoa kwenye hiyo Kata ameenda kwenye Kata nyingine aendeleze na ubabe wake huo, naomba afuatiliwe mpaka apatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za msingi ambazo hazina uzio. Mheshimiwa Waziri, niombe Serikali washughulikie kuwajengea walau shule ambazo ziko mijini, uzio siyo wa matofali hata ukiwa wa senyenge kusudi kile kipindi cha break ambacho wanatoka madarasani kwenda nje, wasizurure hovyo hovyo yaani ndiyo kipindi ambacho wanatoroka, wengine wanaenda kuvuta bangi, wengine wanaenda kufanya mambo ambayo ndivyo sivyo. Niombe walau zile shule ambazo ziko mjini, wajaribu kuwawekea uzio wawe wanakaa shuleni hapo wana-discuss na wenzao muda ukifika wa kurudi nyumbani waende nyumbani, siyo kuzurura zurura. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoke huko nije kwenye suala la Mitaala, suala la Mitaala kuna shule Serikali na shule za binafsi. Shule za Serikali wanafunzi kuanzia awali wanajifunza Kiswahili tu, Kiingereza ni kidogo mno mpaka darasa la saba, lakini shule za watu binafsi wanajifunza Kiingereza kuanzia shule za awali mpaka juu. Kwa hiyo tumekuwa na matabaka ya hawa watoto, watoto wa shule za binafsi wanajiona ni bora zaidi kuliko hawa wenzao na hawa watoto wanapenda nao kujifunza Kiingereza lakini wazazi wao hawana fedha za kuwapeleka kwenye shule za Kiingereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiingereza ni muhimu, sisemi Kiswahili siyo muhimu, Kiswahili ni lugha yetu ya Taifa, ni lugha nzuri sana na mimi naipenda lakini na Kiingereza ni lazima na watoto nao wajifunze. Kama ni kusoma lugha zote mbili, Kiingereza na Kiswahili watoto wote wasome lugha hizo kusudi waweze wote kuwa uniform. Naomba Wizara hilo na lenyewe waliangalie na wengine wameshaliongelea zaidi na mimi nimeliongelea hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye motisha; Walimu nawapenda sana, japokuwa wanafanya mambo ya ndivyo sivyo hao ambao nawasema lakini wengi wanajituma wanafanya kazi nzuri. Naomba Serikali iwaangalie, mishahara yao ni midogo sana, kuanzia shule za chekechea mpaka kwenye vyuo. Sijui maprofesa labda wao wanakula mishahara mizuri sana sijui, lakini hawa Walimu wengine wanakula mshahara mdogo sana. Serikali iwaangalie Walimu iwaongezee mshahara, japokuwa wafanyakazi wote wanalia lakini Walimu wanafanya kazi ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani walikuwa wana- teaching allowance sijui zilienda wapi. Naomba Serikali wafanye mpango zirudi kusudi waweze kukimu mahitaji yao angalau madogo madogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mengi ya kusema mengine nitayaandika, lakini yangu ni haya. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Wizara ya Maji, hoja ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea na mchango wangu, namshukuru Mheshimiwa Waziri Mbarawa; Naibu wake, Mheshimiwa Aweso kijana wangu, kwa kazi ambayo wanaifanya, tunaiona. Nisiwe mwizi wa fadhila, wanafanya kazi usiku na mchana, tunaona wanakimbizana, Mungu awabariki sana na Mungu azidi kuwatia nguvu. Ni lazima nimsifie (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge ninayetoka Mkoa wa Kagera, Kanda ya Ziwa. Mkoa wa Kagera tuna Majimbo mengi ambayo yanapakana na Ziwa Victoria. Ziwa Victoria tuna Wilaya nyingi ambazo zina upungufu wa maji. Kwa mfano, Wilaya ya Bukoba Vijijini, Wilaya ya Muleba Kaskazini na Kusini, Wilaya ya Misenyi; kuna baadhi ya kata ambazo zina matatizo ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha kiangazi ambacho tunaelekea mito inakauka, wanawake wanapata shida kubwa sana ya kupata maji. Pamoja na kwamba Ziwa Victoria, liko sehemu nyingi sana limetambaa Mkoa wa Kagera, lakini kijiografia tuko juu ya Ziwa Victoria. Kata nyingine ziko juu ya Victoria. Naiomba Serikali iwasaidie wananchi wa Kagera ambao wako juu ya milima waweze kuwapatia maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, ninaomba Serikali iweke mkazo, wananchi ambao wanalima kwenye vyanzo vya mito, wanaokata miti ovyo ovyo na kuchoma miti, wakatazwe kabisa wasifanye vitu hivyo, ndivyo vinavyopelekea tukakosa maji kwa wingi. Zamani mito ilikuwa inatiririsha maji vizuri, lakini sasa hivi inakauka, ni kwa sababu ya matatizo hayo. Serikali iwekee mkazo jambo hilo kusudi waache kukata miti na kulima kwenye vyanzo vya mito. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, naiomba Serikali, kwa wale ambao wamejaliwa kujenga nyumba ambazo zina mabati, ni vizuri wakavuna maji ya mvua, wajenge matanki ya saruji madogo madogo, kwa watu wale ambao wanajiweza ili maji yale ambayo yanapotea kwenye ardhi yaweze kuwasaidia wakati wa kiangazi, itakuwa ni jambo zuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile na maji yale ambayo yanapotelea kwenye ardhi, kama watu wangekuwa wanayavuna, mito mingine kipindi cha mvua isingekuwa inafurika na madaraja kuvunjika. Huenda ingekuwa inasaidia na yenyewe kwa ajili ya kuyavuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine naomba, kuna mradi wa Wilaya ya Karagwe, huo mradi ulianza mwaka 2005, ndipo ulipozinduliwa, mradi wa Lwakajunju. Mwaka 2010 upembuzi yakinifu ulikamilisha jambo hilo, mwaka 2018, Mheshimiwa Rais alipokuja kufungua barabara ya Kyaka Bugene, alisema kwamba shilingi bilioni 70 tayari zimeshatoka kwa wafadhili, huo mradi unapaswa kuanzishwa. Mpaka leo hii ninaposema, hakuna kitu ambacho kimeshafanyika. Mheshimiwa Waziri ninaongea na wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alisema kwamba huo mradi uanze, maana shilingi bilioni 70 tayari zimeshatoka kwa wafadhili India, lakini mpaka leo hii huo mradi haujaanzishwa na wananchi wa Karagwe, wanapata shida sana ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Karagwe wana milima mirefu, wanawake wanafuata maji kwenye mabonde, wanapata shida sana. Naomba Mheshimiwa Waziri akija ku- wind-up atuambie huo mradi unaanza lini? Maana umekuwa mradi, mradi, ngonjera, ngonjera, wananchi wa Karagwe wanawake wameota vipara wanapata shida. Naomba Mheshimiwa Waziri anipe jibu ambalo liko sahihi, maana wamenituma nije nisemee hilo jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nilitaka kusema, ni kuhusu…, aah, yameniishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)