Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Paschal Katambi Patrobas (8 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini zaidi nami nitumie fursa hii kuwapa pole Watanzania kwa msiba mkubwa uliotufika wa kumpoteza aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Zaidi ya hapo nimpe pole Mheshimiwa Rais, lakini sambamba na hilo nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini tena katika nafasi hii.

Mheshimiwa Spia, kwa sababu ya ufinyu wa muda, niende moja kwa moja na kujielekeza katika wasilisho la bajeti la Mheshimiwa Waziri Mkuu katika ofisi yake hasa kwenye maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge, lakini pia Kamati zimegusia. Nianze katika eneo moja la ajira, mchango wa ajira au nafasi zinazopatikana katika ajira.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2019 kwa maana ya kipindi cha mwaka 2015 - 2020 taarifa na maswali mengi yalikuwa yanaulizwa kuhusiana na ajira millioni nane ni kama hazipo. Sasa niwape taarifa rasmi kwamba, kwa idadi ya ajira zilizopatikana kwa awamu ya kwanza vijana kati ya umri wa miaka 15 hadi 35 ni 11,891,057 ambayo ni sawa na asilimia 52.96.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia upande wa wenye umri zaidi ya miaka 36 kwenda juu ni sawa na 10,560,488 sawa na asilimia 47.4, hii inatokana na ripoti ya taarifa ya mchanganuo wa ajira kwa shughuli na umri ya mwaka 2019 ambapo pia katika upande wa Wizara ya Fedha Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa wakati huo ambaye sasa ni Mheshimiwa Makamu wa Rais wetu, aliziandikia Wizara zote barua kuweza kutoa taarifa za kuhusiana na ajira. Hizi ndio takwimu kama zinavyojionesha hapo, kwa maana hiyo kwa kipindi hicho chote tulifanikiwa kupata ajira ya zile ambazo zilikuwa zimekusudiwa.

Mheshimiwa Spika, taarifa nyingine pia ambayo ni muhimu katika upande wetu maeneo ambayo mengi yameuliziwa zaidi ni kuhusiana na fursa ambazo vijana wetu wamekuwa wakipewa chini ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Katika kipindi hicho tumekuwa tukitoa mafunzo yaani internship kwa graduates zaidi ya 5,975 walikuwa wanufaika, program ya mafunzo ya ufundi stadi zaidi ya wanufaika 28,941 waliweza kupatiwa mafunzo hayo ya kujenga ujuzi na kuongeza stadi za kazi kupitia mafunzo ya uanagenzi. Pia katika program ya urasimishaji ujuzi, zaidi ya wanufaika 19,462 nao pia waliweza kunufaika na mpango huo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni mafunzo ya kilimo cha kisasa, hapa Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ilifanikiwa kupeleka vijana 136 nchi ya Israel kujifunza namna ya kuweza kufanya kilimo cha kisasa. Hao tunakwenda kuwatumia pia kama trainer, training ilikuwa kama training of trainers ambao nao pia tutawatengenezea utaratibu wa kuweza kupata ajira kwa maana ya kujiajiri na kupewa vifaa au mikopo ili waweze kujiendeleza.

Mheshimiwa Spika, vile vile katika mafunzo ya greenhouse nchini kote kati ya mikoa ambayo ilinufaika, mikoa 12 zaidi ya Watanzania vijana 8,980 nao waliweza kupatiwa mafunzo hayo. Program hizi ni endelevu ikiwa sambamba na Mfuko wa Kukuza Ujuzi (skills development) zaidi ya wanufaika 1,550 wamepata mafunzo hayo.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa pili kwa kujali zaidi muda nijielekeze katika eneo hili la fursa ambazo zilipatikana za moja kwa moja. Fursa za moja kwa moja za ajira zilipatikana kwa mujibu wa taarifa iliyotoka Wizara ya Fedha, baada ya kuwasiliana na Wizara zote, ni zaidi ya 11,891,772 ikiwa ni ulinganifu wa fursa za ajira zisizo za moja kwa moja 881,354…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwanza nikupongeze kwa sababu baada ya wewe kuchaguliwa kwa kishindo na Chama cha Mapinduzi, lakini pia kwa kuidhinishwa na Bunge hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja katika eneo la hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge. Nizungumzie kuhusu suala la Kiwanda cha Mbigiri, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba katika uwekezaji ambao unafanywa na Serikali katika mifuko hii kuna sera ambayo inaongoza uwekezaji wa Mifuko lakini pia tunayo sera ya uwekezaji ambayo ndiyo msimamizi mkuu wa Mifuko hii. Miongozo kabla ya uwekezaji ni lazima ipitishwe na Benki Kuu ya Tanzania na taratibu zinaelezwa na nini kinafanyika kabla ya uwekezaji. Mwongozo unaeleza lazima ufanyike utafiti na upembuzi ili kubaini au kugundua kama kuna economic viability yaani kuangalia faida katika uwekezaji huo.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili linaangaliwa ni katika sasa kufanya uamuzi wa kwamba uwekezaji ufanyike au usifanyike na kwa kuzingatia required rate of return ambayo inaelezwa kwenye mwongozo huo na kwa mujibu wa maelekezo mazuri yanayofanyika na Benki Kuu ya Tanzania na kigezo cha kufanya hivyo kama itaonekana kutakuwa na tija ndipo uwekezaji unaweza ukaendelea kwa kuzingatia pia miongozo ambayo inatolewa na Social Security Investment Guidelines.

Mheshimiwa Spika, sasa Social Security Investment Guidelines ndiyo zingatio la usimamizi wa Serikali katika kuhakikisha chochote kinachowekezwa kinachotoka katika Mifuko hii kiende kuleta tija. Kwa kweli niishukuru sana Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, ya Awamu ya Sita, amekuwa akitupa miongozo kwa wakati wote kuweza kuhakikisha kwamba, tunayatekeleza majukumu kama jinsi ambavyo ilikusudiwa. Nini kilitokea katika kiwanda hiki cha Mbigiri? Changamoto zilizojitokeza baada ya tafiti hizo na kuruhusiwa kuanza, kiwanda hiki ndani ya miezi 16 kilikuwa tayari kilishaanza kufanyakazi by mwaka jana mwezi Agosti kingekuwa kimekamilika.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu sote ni jambo la janga la dunia nzima, baada ya kuanza procurement procedures zilifika zikachelewa kwa sababu ya uwepo wa janga la Covid mashine zikachelewa kuingia na kufikia mwezi Agosti na sasa hivi tunavyozungumza tayari mashine zimekwisha kuingia. Kwa hiyo tunasubiri by mwezi Agosti mwaka huu pengine tayari waende kwenye hatua ya mobilization na installation kwenye eneo hilo la kiwanda.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo mkataba huu tumeendelea kuhakikisha kwamba tunasimamia ili uweze kutekelezwa kwa kadri agizo na ni siku tatu zilizopita Mheshimiwa Waziri wangu Profesa Ndalichako alikuwa kwenye kiwanda hicho na kuangalia tija namna gani Serikali itaenda kupata faida zaidi. Kwa hiyo tunalisimamia kwa karibu zaidi.

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili ilikuwa ni kuhusiana na hasara ambayo wakulima waliipata katika kilimo walichokifanya cha miwa. Sambamba na hilo tukumbuke Serikali pia nayo ililima mashamba, miwa hii yote kwa pamoja kwa maelekezo mazuri ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na uongozi wetu katika Wizara na usimamizi wa Mheshimiwa Waziri Mkuu, ilibidi Serikali ifanye uamuzi wa kutafuta soko na kwenda kuuza katika viwanda vingine na miwa hii ilinunuliwa na faida ilipatikana zaidi ya bilioni moja. Kwa hiyo ilikuwa ni katika hatua ya kupunguza hasara ambayo ilijitokeza kutokana na changamoto tulizozipata.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni kuhusu madeni ya Serikali katika Mifuko. Katika hili turudi katika hoja za CAG, tulizichukua hoja 12 za Ofisi ya CAG na tayari Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri Mkuu wamekwisha kuanza utekelezaji wake na moja ya utekelezaji wa hoja hizo 12 za CAG, tayari zaidi ya shilingi trilioni mbili zimelipwa kwenye Mfuko wa PSSSF na Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan katika kupitia hiyo cash bond.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna hoja nyingine kwa kadri ya maelekezo ambayo umetupa kwamba tujielekeze katika hoja. Suala la fedha ambazo Ofisi ya Waziri Mkuu zinazosemekana bilioni 56 zinazodaiwa kwa kile alichokisema Mheshimiwa Mbunge kwamba zinadaiwa. Ni kweli fedha hizo zilichukuliwa kwa utaratibu wa kuokoa hasara ambayo kubwa walikuwa wanaenda kuipata wakulima. Ndipo Serikali ikalazimika kuchukua hatua za makusudi kuweza kuhakikisha wakulima hawa mazao yao hasa yale mahindi yananunuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, utaratibu kama jinsi ambavyo mikopo mingine inalipwa, Serikali inaendelea kulipa deni hili na Mheshimiwa Aida Khenani atakuwa shahidi hata yeye mwenyewe kuna maeneo ambayo pengine atakuwa na mkopo na mkopo unategemeana na masharti na vigezo. Kwa hiyo huwezi ukalipa kwa mkupuo, kwa hiyo hili suala tayari Serikali inalipa na niwaondoe shaka Serikali ya Awamu ya Sita katika kila hoja zinazotolewa na Wabunge na hoja zinazotolewa na Kamati za Bunge, tunazitekeleza usiku na mchana kuhakikisha kwamba maagizo ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan yanatimizwa. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia katika Bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema siku hii ya leo, na pia tangu tulipoanza shughuli hizi za Bunge. Aidha, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan ambaye kwa wakati wote ameendelea kuonesha mfano tangu alipoingia katika madaraka. Katika kipindi cha miaka miwili amefanya kazi kubwa sana ambayo Watanzania wote tunaiona na tunaishuhudia katika maeneo mbalimbali. Hata hivyo miongozo yake, maelezo yake katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwa kweli sisi sote ni mashuhuda kwamba Mheshimiwa Rais amedhamiria kutuletea maendeleo katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wangu Mheshimiwa Joyce Ndalichako na Mheshimiwa Mama Mhagama ambao kwa maelekezo yao wamenisaidia sana katika kutekeleza majukumu yangu pamoja na Katibu Mkuu na Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitakushukuru wewe pamoja na Naibu Spika, Wenyeviti wa Bunge, Wenyeviti wa Kamati za Bunge na Wabunge wote kwa kutusaidia sana katika kutekeleza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, nianze kwanza kwa kusema naunga hoja mkono na vile vile kwa sababu ya muda, katika yale yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wametoa michango, maoni, mapendekezo na ushauri katika maeneo mbalimbali, niombe tu kwamba yaingie katika Kumbukumbu za Bunge (Hansard) katika taarifa yote ambayo nilipaswa kuiwasilisha.

Mheshimiwa Spika, nitaenda kugusia machache. Mengi tunayachukuwa na tunaenda kuyafanyia kazi kadri tulivyoelekezwa na kushauriwa na Waheshimiwa Wabunge. Lipo suala la fedha za ukarabati wa Vyuo vya Watu Wenye Ulemavu na Utangamao. Ofisi ya Waziri Mkuu imefanya jukumu hilo na ilitekeleza na tumeendelea kutekeleza na mpaka sasa tunavyozungumza, kwa mafanikio makubwa Mheshimiwa Rais ametusadia kuweza kufufua vyuo zaidi ya saba ambavyo vilikuwa viko hoi, kwa zaidi ya miaka 10 vilikuwa havifanyi kazi.

Mheshimiwa Spika, tayari Chuo cha Masiwani Tanga kimefunguliwa, kinafanya kazi na wanafunzi ambao ni Wwatu Wenye Ulemavu tayari wameshaanza kupata mafunzo. Chuo cha Luanzari pale Tabora tayari kimeshaanza kufanya kazi, pia Chuo cha Saba Saba Singida, Mtapika Mtwara, na Chuo cha Yombo. Vyote hivi ni kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Rais amefanya kwa ajili ya Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Spika, vile vile, katika maeneo hayo, pia katika hoja nyingi ambazo za Waheshimiwa Wabunge zilizoelekeza kwamba tuangalie katika kutoa unafuu kwa watu wenye ulemavu, nawashukuru sana kwa michango yao, lakini pia Mheshimiwa Rais alitoa fedha zaidi ya Shilingi milioni 60 ambazo zimeendelea kutolewa kwenye mwaka wa fedha kuwasaidia watu wenye ulemavu kupata mafuta yale maalum ya ngozi. Vile vile kana kwamba haitoshi Mheshimiwa Rais kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na kwa maagizo ya Mheshimiwa Rais na maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, tayari tumeshashaandaa mwongozo maalum ambao unawataka kutoa 3% kwa watu wenye ulemavu ya ajira zote ambazo zinatangazwa. Kama mmeona Mheshimiwa Rais ameendelea kutoa ajira na watu wenye ulemavu tumeendelea kuwapa kipaumbele katika kutoa ajira kwa kufuta mwongozo huo unaotutaka katika ajira zote zinazotangazwa 3% angalau iwe ya watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, pia katika upande ya watu wenye ulemavu, kwenye eneo lingine, tumeweza pia kufanikiwa kupitia Mheshimiwa Rais, ameweza kuchukua Shirikisho la Watu Wenye Ulemavu (SHIVIAWATA) na yeye mwenyewe aliwaalika Ikulu ya Chamwino na zaidi ya hapo akatoa ahadi ya kutoa kiwanja kwa ajili ya kujenga Makao Makuu ya Watu Wenye Ulemavu hapa Dodoma. Mheshimiwa Rais ameshaanza kutekeleza, ametoa kiwanja chenye thamani ya Shilingi milioni 37 kwa ajili wa utekelezaji wa shughuli za watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia lilikuwepo suala lingine la kuhusiana Serikali iweke mikakati ya kukusanya maduhuli kufikia lengo ambalo lilikusudiwa. Katika ukusanyaji wa maduhuli, Ofisi ya Waziri Mkuu tunaipata kupitia vibali vya kazi. Hapa tayari mpango umeshafanywa na tumeshaanza mkakati wa kuangalia namna gani tutaongeza ufanisi katika utekelezaji wa jukumu hilo.

Mheshimiwa Spika, tunatarajia kupata magari 17 ambayo yatafanya kazi ya kufanya ukaguzi kwenye maeneo ya kazi ili kuhakikisha kuna kazi za staha, lakini pia kuna afya na usalama mahali pa kazi na hivyo tutaweza kukusanya tozo na ushuru. Sambamba na hilo, katika sheria yetu inayoratibu ajira za wageni ambayo inataka ada zinazotolewa na watu wanaoomba ajira hawa, wamekuwa wakilipa ada na kwa sababu ya uratibu huu, na kwa sababu ya kufungua makampuni na uwekezaji mkubwa kwa Taifa letu, kumepeleka sasa kuweza kusaidia zaidi kwamba tunaweza tukafikia malengo yaliyokusudiwa kwenye kukusanya maduhuli ambayo tunayakusudia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mikakati ambayo imewekwa pia ni pamoja na kuongeza kupitia Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora ni pamoja na kuongezea uwezo OSHA kwa maana ya kutoa ajira. Kibali cha ajira kimetoka kwa wafanyakazi zaidi ya 18 ambao tunatarajia wataajiriwa na kuweza kuongeza fedha katika uratibu wa shughuli za OSHA katika maeneo kuhakikisha kwamba lile jukumu la Ofisi ya Waziri Mkuu la kuhakikisha kuna kazi za staha nchini linatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine kama nilivyoeleza ambazo tutazijibu tu; moja ni hii ya kwamba Serikali iongeze bajeti katika program ya kukuza ujuzi. Lengo la Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2015 kwenda 2025 tunakusudia kutoa mafunzo kwa Watanzania zaidi ya 681, na katika kufanya hivyo itakuwa ni kwa kipindi cha miaka mitano. Tayari Wizara ya Fedha imeji-commit kwamba tutaendelea kupata fedha kwa ajili ya kuhakikisha mafunzo haya yanafanyika. Pia kumekuwa na program mbalimbali za ukuzaji ujuzi ambapo kwa mwaka wa fedha 2021/2022 tulipata zaidi ya Shilingi bilioni tisa ambazo zilienda kuwasaidia vijana wengi wa Kitanzania kuweza kupata mafunzo kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, pia lilikuwepo suala lingine la kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kutoa program hizi za mafunzo. Wapo wadau wa maendeleo ambao tunashirikiana nao; GIZ, International Labour Organization na IOM ili kuona kam tunaweza kushirikiana katika masuala ya kibajeti ili kuweza kuendelea kuboresha na kuhakikisha kwamba tunapata fursa, na pia kuwapa fursa Watanzania wengi katika kupata mafunzo mbalimbali yanayohusiana na kukuza ujuzi na pia kuwaandaa katika kukabiliana na soko la ajira.

Mheshimiwa Spika, pia lipo suala lingine la fursa za ajira nje ya nchi. Hili tumeshaanza kulifanya. Kama tulivyoeleza pia kwenye hoja za Kamati na Waheshimiwa Wabunge kupitia Wakala wa Ajira Nchini (TAESA) ambapo tayari tumeshasajili na kupitia kamishna wa kazi. Tumeshasajili Wakala wa Ajira ambao wanatafuta ajira ndani na nje ya nchi na kwa kufanya hivyo, tayari tumeingia bilateral agreement na nchi zaidi ya nane ambayo tunaingia nao katika majadiliano ili kuweza kuona namna gani tunaweza kupata fursa zaidi za kuwasaidia Watanzania wengi kuajiriwa nje ya nchi na kutengeneza utaratibu maalum wa kuwasajili wale walio nje ya nchi waliopata ajira ili tuweze remittance ambayo ni sehemu ya mapato pia katika Serikali.

Mheshimiwa Spika, pia kwa kumalizia, lipo suala ambalo Waheshimiwa Wabunge walilizungumzia kuhusiana na kuweka kumbukumbu za hawa watu walioajiriwa nje ya nchi. Tayari tumeshaandaa mfumo maalum wa kieletroniki wa wao kuweza kujisajili na pia tunawasajili wale ambao wanatafutiwa na wakala mbalimbali wa ajira ili kuweza kuwa na kanzidata ambayo itatusaidia katika kuwaratibu na pia kusimamia haki zao huko wanapofanya kazi nje ya nchi. Vile vile kazi zote ambazo ni za nje ya nchi tunataka tuziratibu vizuri ili kuepusha Watanzania wengi kwenda kudhalilishwa ama kuumizwa ama kutendewa matendo yasiyofaa wakiwa nje ya nchi. Hilo ni jukumu ambalo tumeshaanza kulifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuhusiana na maendeleo ya vijana; hapa katika kuboresha kulingana na michango ya Waheshimiwa Wabunge na Kamati, tayari tumeshadilisha miongozo. Mwongozo wa utoaji wa mikopo ule wa asilimia 10 katika Halmashauri, sasa kijana mmoja anaweza kupata mkopo na ni kuanzia Shilingi milioni 10 mpaka milioni 50. Vile vile kwa watu wenye ulemavu, mikopo hii nayo pia inatolewa kwa mapato ghafi ya Halmashauri na tayari mabadiliko ambayo tumeshayafanya huko, ni kuhakikisha pia watu wenye ulemavu kulingana na changamoto zao, ilikuwa ngumu kufanya kazi wakiwa watano, lakini sasa tumefanya mabadiliko, hata mtu mmoja pia anaweza kupewa mkopo kwenye ngazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye eneo hilo, Mfuko wa Maendeleo ya Vijana tunazidi kuuboresha sasa tuweze kuona ni namna gani tutawafikia vijana wengi zaidi kuweza kuwasaidia: Kwanza, kuwapa mafunzo kama yale ambayo wanamaliza walio wahitimu wa vyuo vikuu, kuwatambua waliko, kutambua kada mbalimbali ambazo wamezisomea, kuwasajili TAESA na kuwapeleka kwa waajiri ili wakapate mafunzo ya utayari wa kufanya kazi kwa maana ya internship. Tayari tumeshapeleka vijana zaidi ya 6,000 kwenye maeneo mbalimbali na wanachangiwa fedha kidogo na Serikali zaidi ya Shilingi 150,000 kwa mwezi kwa ajili ya kuwaandaa.

Mheshimiwa Spika, lakini vile vile nikimalizia kwa sababu ya muda, mambo ni mengi na kwa sababu hoja hizi tayari ziko hapa ziweze kuingia kwenye Hansard, Mheshimiwa Rais ameendelea kuweka mpango wa kuwaangalia vijana katika maeneo mbalimbali. Fedha za Bodi ya Mikopo, hizo nazo ni fedha ambayo ni sehemu ya kuwasaidia vijana, kuwaratibu. Zaidi ya Shilingi bilioni 570 ziliongezwa, pia fedha za Halmashauri, zote hizi zinawasaidia hao vijana ambao tumekusudia kuwasaidia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya, ahsante sana.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, pamoja na kupeleka mafunzo ya utaifa, uzalendo lakini pia maadili na kuweza kusaidia Taifa kuweza kuwaandaa vijana ambao ni nguvu kazi ya Taifa ya hivi sasa na hata ya baadaye.

Mheshimiwa Spika, ahsante, mengine Waheshimiwa Mawaziri watanisaidia katika kuweza kuyajumuisha.

MHeshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Nami niungane na wenzangu katika kuwapongeza sana Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kufanya kazi nzuri sana, sana, sana ambazo zimekuwa reflected kwenye takwimu na taarifa mbali mbali. Vile vile nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa hali na azma yake kubwa ya kutamani kuona Tanzania ikikua kiuchumi kwa kubadilisha sheria mbalimbali na pia kubadilisha mifumo na kutengeneza mazingira mazuri kwa ajili ya uwekezaji ndani ya nchi yetu. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nampongeza pia hasa kwa kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara miradi ambayo imesajiliwa kwa kipindi hiki tu kifupi; ukiangalia mwezi Julai, 2022 mpaka Machi, ni zaidi ya miradi 240, ambayo thamani yake ni Dola za Kimarekani milioni 438 na hii imesaidia sana katika kukuza uchumi. Sambamba na hilo, kumekuwa na ongezeko la ajira watu zaidi ya 39,245 ambao wamenufaika na ajira katika usajili wa miradi hiyo mipya.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Mheshimiwa Rais pia ameweka mikakati mbalimbali ya kukuza ajira. Moja ya mikakati ni hili la kuweza kukuza viwanda hasa katika suala la kwenye sekta ya uwekezaji. Tumebadilisha sheria, na pia tumerahisisha mazingira ya uwekezaji nchini kuweza kuwa rahisi zaidi ili uwekezaji ukue na kuweza kupata kipato. Nchi nyingi duniani leo zimetoka kwenye masuala ya kufanya biashara kwa maana ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, Serikali sasa imekuwa inatengeneza mazingira wezeshi na kukusanya kodi. Vile vile sehemu kubwa ya biashara, mfano ajira zinatokana zaidi na private sector ambayo sasa hivi Mheshimiwa Rais ameamua kui-enhance kwa sehemu kubwa sana, tunaona kwenye kilimo mapinduzi makubwa; kwenye uwekezaji tunaona mapinduzi makubwa; na kwenye viwanda tunaona uwekezaji mkubwa ambao unafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika upande wa ajira, tunaweza kuona kwa upande wa ajira za kisekta ni maagizo ya Mheshimiwa Rais na maelekezo mahususi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba Wizara zote za kisekta lazima kwenye mwaka wa fedha unazopewa bajeti, zizalishe ajira ili Watanzania waweze kunufaika na ajira hizo katika ngazi mbalimbali. Hilo limekuwa likitekelezwa.

Mheshimiwa Spika, vile vile katika miradi tu ya Wizara za maendeleo, zaidi ya Watanzania 1,226,925 walipata ajira. Sasa kwa muktadha huo huo wa spirit ya Mheshimiwa Rais ya kutaka kuongeza ajira, kukuza uchumi na kutengeneza uchumi jumuishi ili kila mwananchi aweze kunufaika, ni pamoja na kutengeneza mazingira ya kuwasaidia wawekezaji, na pia kusaidia kwenye sekta ya uchumi ya biashara ili iweze kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, nimesikia hili suala la Tanga ambalo limesemwa sana na Waheshimiwa Wabunge hapa. Nimelazima kufuatilia kwa sababu limegusa hasa kwenye sekta na Wizara yetu ya kwenye masuala ya ajira. Ni kweli nimefanya utafiti na nimeangalia kwenye rekodi mbalimbali zilizofanywa ikiwa ni pamoja na hesabu za kihasabu zilizofanywa kwenye Kampuni ya Tanga Cement, inathibisha kwamba Tanga Cement haina uwezo tena wa kujiendesha, ina-run kwa hasara. Zaidi ya hapo, hata fedha zile ambazo inazipata kidogo katika operation, inajikuta inashindwa kulipa kodi; na kwenye eneo la kodi lazima uangalie kama ni faida. Unaangalia faida ghafi ambayo ni jumla ya gross profit, na pia utaangalia net profit baada ya operational cost. Pia utaangalia gharama nyingine ambazo utazipata kama unapata faida baada ya kulipa kodi, na vile vile utaangalia kabla ya kulipa kodi na baada ya kulipa kodi. Hizi zote zinathibitisha kampuni hiyo haina uwezo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, katika maamuzi ambayo yalifanyika, FCC katika malalamiko yaliyopelekwa tarehe 2 Novemba, 2021 FCC iliamua kwa misingi miwili ambayo imeainishwa kwenye Sheria Ushindani ambapo katika Kifungu chake cha 5 (6) (a) na (b) kinatoa masharti kwamba kampuni haipaswi kuwa na nguvu kubwa kwenye soko, lakini pia (yenyewe peke yake) isiwe na uwezo ambao unaweza kuathiri watu wengine kufanya biashara. Katika tafsiri ambazo zilitumika FCC, waliweza kuzingatia matakwa pia ya Sera ya Taifa na pia mwendendo na mtazamo wa Serikali ya Awamu ya Sita, na pia katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi inayotaka kukuza uchumi wa Taifa, uchumi wa Watanzania na mtu mmoja mmoja na pia kukuza uchumi jumuishi na kutengeneza fursa za ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kipengele kilichotumika waliangalia muktadha huo na kuona kwamba katika kipengele cha 5 (a) kinachohitaji nguvu ya soko, ambayo kwa lugha ya kigeni inasema ni sales volume ambayo inahitaji isizidi asilimia 35, ndicho kigezo pekee ambacho kilionekana. Sheria hii katika kipengele cha pili inahitaji pia huyo mtu ili aweze kuonekana ana dominance kwenye soko, ni lazima awe amekidhi vigezo vyote katika kifungu cha 5 hicho, kipengele (a) na (b).

Mheshimiwa Spika, tafsiri iliyofanyika katika Fair Competitions Tribunal, wao walijikita zaidi kwenye kigezo kimoja tu cha installed capacity ambapo waliangalia katika kipengele cha asilimia 35 bila kuangalia kwamba sheria inataka vyote kwa pamoja vitamkwe kama jinsi sheria inavyosema katika kifungu hicho. Kwa hiyo, wakafanya maamuzi ya ku-crash decision ile na kusema kwamba maamuzi ya FCC yaondolewe na muunganiko huo usiwepo.

Mheshimiwa Spika, sheria hiyo hiyo pia katika kifungu chake cha pili inaitaka mamlaka katika kutafsiri sheria; haitafsiri katika mazingira yale, na ni principle ambayo hata kwenye sheria ipo, ya kusema kwamba every case should be judged from its own circumstances, kwamba kila kesi lazima iangaliwe na kutafsiriwa kwa mazingira yake kama jinsi ilivyo. Katika msingi huo huo, hata kwenye Sheria za Kiuchumi pia maamuzi yanaangaliwa kutokana na jinsi ambavyo hali ya kiuchumi, na mazingira yaliyokuwepo kwa wakati huo.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka 2020, maamuzi yaliyofanywa na FTC (Fair Competition Tribunal), wao walifanya uamuzi kwa ku-base zaidi na tafiti ambazo zilifanyika katika kipindi cha mwaka 2020. Hali ya sasa hata ukiiangalia, mwaka 2020 aliyekuwa anaongoza kama kiwanda kwenye kupata mengi na uzalishaji ilikuwa ni Twiga Cement anafuatiwa na Tanga Cement na Dangote. Kwa hali ya 2022 kwa tafiti zilizokuja kufanyika na takwimu kwa mujibu wa data ambazo zipo, inasema anayengoza kwa sasa, siyo kama ilivyokuwa 2020 tena, takwimu zinaonesha sasa Twiga Cement ndiyo anaongoza, anafuata Dangote na kuna kiwanda kingine ambacho hakikikuwepo kabisa kwenye soko, wakati huo kilikuwa hakizalishi, kilikuwa kinaanza, lakini sasa kinazalisha zaidi ya tani 900,000, ambacho ni Kiwanda cha Shuwan Maweni na kiwanda kingine ambacho kinafuata sasa ndiyo Tanga ambacho bado pia kinashuka katika uzalishaji, ambacho ndiyo maana ya maombi haya kuweza kufanya uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, mwekezaji huyu amekuwa anazalisha na anafanya kazi ya kuzalisha cement za Twiga lakini pia anaenda kuingiza capital, ku-inject new capital ya zaidi ya Shilingi trilioni moja ili kuongeza capacity. Katika maamuzi yaliyotolewa awali ya FCC, yalikuwa na masharti. Masharti hayo yalikuwa kumi, kati ya masharti matatu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba dakika moja nimalizie.

SPIKA: Utakuwa unachukua muda wa Waziri hapo. Malizia dakika moja.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, katika masharti hayo yaliweza kukubaliwa pia na hao wadau wa maendeleo. Zaidi nimalizie tu kwa kusema kwamba, hili jambo siyo jipya. Ipo kesi ya Afrika Kusini ya mwaka 2019 na imefanyiwa maamuzi, ambapo kesi hiyo ilikuwa hivyo hivyo kwamba walirudi tena katika kufanya review baada ya maamuzi ya awali. Kwa hiyo, hakuna suala la kudharau Mahakama au maamuzi hapa. Suala lipo, linatoa haki. Sheria hiyo ni kwamba unaweza ukarudi tena kupeleka maombi kulingana na hali iliyopo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, kuna kesi nyingine pia ya Toyota na Sifao Motors, ambayo nayo pia ilifanyiwa maamuzi hivyo hivyo na FCC ikakataa ombi lao, lakini pia ilivyokuja kurudi FCT, nayo pia ilikuja ikabariki maamuzi yaliyofanywa na FCC. Kwa hiyo, jambo hili siyo geni, tunachelewesha uwekezaji, tunachelewesha Watanzania kuweza kupata uchumi, tutaenda kupata hasara ya kupoteza ajira 3,000 za Watanzania, tutaenda kupata hasara za uwekezaji wa kukosa zaidi ya Shilingi trilioni moja kama maamuzi haya tutaenda kuyafanya kishabiki na bila kuangalia maslahi ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono kwamba suala hili la uwekezaji ni muhimu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa nafasi hii, lakini pia nitumie fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujaalia afya njema sisi sote. Pili, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuwa na imani nami ya kumsaidia katika kutekeleza majukumu chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu katika masuala ya Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niwapongeze sana wasaidizi wa Mheshimiwa Rais ambao ni Makamu wa Rais, Mheshimiwa Dkt. Isdor Mpango, Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa na Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko kwa kumsaidia Mheshimiwa Rais na kutusaidia sana sisi katika kutupa miongozo na maelekezo ambayo yanatusaidia kuweza kutekeleza Dira ya Maendeleo na Mpango wa Maendeleo. Pia kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kupitia ofisi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Tulia Akson, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye yeye pia amekuwa akifanya kazi kwa weledi mkubwa kuliongoza Bunge hili pamoja na wewe, lakini pia Katibu wa Bunge pamoja na uongozi wote wa Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie pia fursa hii kumshukuru sana kwa namna ya kipekee Mheshimiwa Waziri wangu Deogratius Ndejembi na kumpongeza pia kwa uteuzi wake kwa nafasi hii waliyoipata pamoja na Katibu Mkuu wangu kuhudumu katika Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba naye, tunaye Mheshimiwa Jenista Mhagama, amefanya kazi kubwa, Chief Whip tunakushukuru sana kwa miongozo na maelekezo yako. Sisi pamoja na Mheshimiwa Ummy kwa kweli tunanufaika kwa kufanya kazi nanyi za kumsaidia Mheshimiwa Rais, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuwashukuru Wenyeviti wa Bunge, lakini pia wa Kamati za Bunge pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa hoja zao ambazo siku zote zimekuwa kiongozi pia kielelezo cha kutusaidia sisi katika kutekeleza majukumu ambayo yamekusudiwa na Serikali kuweza kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze moja kwa moja katika hoja ambazo zimezungumzwa au zilizoelezwa na kutolewa na Waheshimiwa Wabunge katika kutusaidia sisi kutekeleza majukumu yetu. Kwa hoja ambazo zimeelezwa, kwanza nitambue Wabunge ambao wamechangia kwenye ofisi yetu, kwenye maeneo ambayo yametugusa, ni Wabunge zaidi ya 36 na kwa sababu ya muda, naomba uniruhusu kuzieleza hoja hizi kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuunga mkono hoja ya Hotuba ya Waziri Mkuu pamoja na pendekezo hili la bajeti lililoko chini ya ofisi yake. Zaidi niseme maelezo yote, mapendekezo, ushauri na maoni yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge lakini pia na Kamati za Kudumu za Bunge, tunayachukua kwa ajili ya kwenda kuyafanyia kazi ili kuboresha jukumu hili la utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo, lakini pia na Dira ya Maendeleo pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ili wananchi wetu katika makundi hayo ambayo tumepewa fursa ya kuwahudumia, tuhakikishe kwamba tunawahudumia ipasavyo, kwa kuhakikisha tuna mikakati na mipango endelevu ambayo itawasaidia katika kuwahudumia na kufikia azma ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo amejiwekea.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo ambalo naweza kujielekeza na kwa kueleza kwa ujumla ni kwamba, tumeyachukua maoni na mapendekezo. Lipo eneo la watu wenye ulemavu ambalo Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mapenzi ya dhati aliyonayo kwa watu wenye ulemavu, alidhihirisha hilo alivyowaita Ikulu ya Chamwino tarehe 16 Machi, 2022 na akasema kwamba; “Leo sina jambo lolote zaidi ya kuwasikiliza na mnieleze changamoto zote zinazowakabili, ziwe za kisera, kisheria, au changamoto zozote,” ambazo yeye kama Mkuu wa Nchi alitaka kuzipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais aliwasikiliza lakini pia akatoa maagizo mahususi kwamba twende kutekeleza. Mbali na mambo mengine ambayo aliyasikiliza, mojawapo ilikuwa ni changamoto ya mafunzo ya watu wenye ulemavu ambayo Waheshimiwa Wabunge wameeleza kama moja ya changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo taarifa kueleza kwa furaha kabisa kwamba Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa mapenzi ya dhati aliyonayo alitoa fedha zaidi ya shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ukarabati wa vyuo ambavyo zaidi ya miaka kumi vilikuwa havifanyi kazi. Kikiwemo Chuo cha Masiwani Tanga, Sabasaba pale Singida, Lwanzari Tabora na Mtapika kule Masasi Mtwara ambapo tayari vimeshakarabatiwa na vinafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Chuo cha Yombo pale Dar es Salaam vinafanya kazi kwa ajili ya kutoa elimu kwa watu wenye ulemavu ya utengemao na kuhakikisha kwamba hawabaki mitaani bila kupatiwa elimu ili na wao waweze kujitegemea na kuchangia kwenye ujenzi wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais pia alitoa fedha nyingine zaidi ya shilingi bilioni 3.4 kwa ajili ya ujenzi wa vyuo vipya vya watu wenye ulemavu. Hayo ndiyo majibu ya hoja ya Waheshimiwa Wabunge waliyosema kwamba watu wenye ulemavu waangaliwe, sasa hizo ndiyo hatua ambazo Mheshimiwa Rais alizichukua kwa kutoa zaidi ya shilingi bilioni 3.4 ambazo tumejenga na tunaendelea na ujenzi wa chuo pale Ruvuma kwa Dkt. Mama Mheshimiwa Jenista Mhagama. Tumesema Dkt ni sahihi, tumwombee kwa Mwenyezi Mungu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia chuo kingine kinajengwa pale Mwanza ambacho ni mbadala wa Chuo kile tulichokuwa nacho cha Milongo. Tuna chuo kingine ambacho tunakijenga Kasulu - Kigoma kwa Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako ambapo tayari ujenzi unaendelea na hali ni nzuri. Tunajenga Chuo kingine cha Watu Wenye Ulemavu kule Songwe. Lengo la Dkt. Samia Suluhu Hassan ni nini? Lengo ni kuhakikisha watu wenye ulemavu pia tunawajumuisha katika ujenzi wa uchumi wa Taifa hili, tunahakikisha watu wenye ulemavu hawawi barabarani tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akasema asilimia mbili za mapato ghafi ya halmashauri nazo ziende kwa watu wenye ulemavu, zaidi ya asilimia mbili za fedha hizi sasa zinakusanywa, zitatolewa kwa watu wenye ulemavu ili waweze kunufaika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa tena fedha shilingi 1,000,000,000, tumefungua akaunti maalum BOT kwa ajili ya ruzuku ya watu wenye ulemavu ambapo watapata vifaa saidizi vya kuwasaidia na pia vifaatiba, zaidi ya hapo hata kuwasaidia kwenye masuala ya elimu na changamoto walizonazo. Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha cash na sasa hivi tunasubiri shirikisho la vyama vya watu wenye ulemavu na vikao vinavyohusika viweze kuvipangia matumizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye eneo la watu wenye ulemavu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mapenzi ya dhati ameendelea kuangalia katika maeneo ya ajira, tumetunga mwongozo ambao ameuidhinisha na ametoa ruhusa hiyo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, tayari asilimia tatu ya ajira zote zinazotoka nchini iwe kwa watu wenye ulemavu. Kwa hiyo, kama ni watu 20 lazima angalau watu wawili au zaidi waweze kupata nafasi hiyo kulingana na masharti na vigezo ambavyo tumeviweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika eneo hilo la watu wenye ulemavu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amezidi kuwatendea haki. Tumeenda kwenye miongozo ya ujenzi wote unaofanyika nchini uzingatie mahitaji maalum ya watu wenye ulemavu. Ukijenga ghorofa lako lazima uzingatie kuna lift au kuwe na ramp ambayo itawasaidia watu wenye ulemavu ili kuweza kupata huduma katika sehemu wanayohitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ameendelea kuupiga mwingi Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa watu wenye ulemavu, yeye mwenyewe kwa kujua kwamba walikuwa hawana ofisi ya kitaifa ya kupata huduma, alitoa fedha zake mwenyewe zaidi ya shilingi milioni 36.7 kwa ajili ya kupata eneo la ujenzi wa Ofisi ya Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu, ninavyozungumza tayari hati hiyo wameshakabidhiwa watu wenye ulemavu na wanaendelea kwenye hatua ya ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la watu wenye ulemavu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya mengi, pamoja na kuhakikisha kwamba hata kwenye zile kandarasi ambazo zinatolewa kwenye halmashauri na wao waweze kupewa share yao. Tunaendelea kuwaunganisha hata mikopo iliyokuwa ikitoka kwa kikundi cha watu watano, tumebadilisha mwongozo mwaka 2022 na sasa mtu mmoja mmoja mwenye ulemavu anaweza kupata mkopo wa shilingi milioni 10 mpaka shilingi milioni 50. Huyo ni Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utakuwa shahidi pamoja na Waheshimiwa Wabunge, watu wenye ulemavu sasa hivi wamepungua barabarani. Tulikuwa na kesi nyingi za ombaomba na tulikuwa na kesi nyingi za watu wenye ulemavu kudhalilishwa. Sasa hivi mtu mwenye ulemavu ukimkuta barabarani ni amechagua mwenyewe kwa sababu sikio la kufa wakati mwingine halisikii dawa, lakini kwa sehemu kubwa tayari watu wenye ulemavu tumewaweka kwenye utaratibu wa kupewa nafasi hizi, hata maeneo ambayo yanafanyika ujenzi wa masoko tunawapa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Sekta ya Afya pia hata kwenye huduma zinazotolewa hospitali, watu wenye ulemavu wamepewa kipaumbele pamoja na wajawazito, watoto na wazee katika kupewa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan amejipambanua kuwa rafiki mzuri na mwema kabisa kwa watu wenye ulemavu, tuendelee kumwombea Mwenyezi Mungu, aendelee kudumu ili watu wenye ulemavu waendelee kupata manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliona hatua nyingine ya kuhakikisha tunapunguza ulemavu, kwa sababu wapo wanaozaliwa na ulemavu na wapo ambao wanaupata baada ya kuzaliwa. Tumeweka utaratibu na mikataba ya lishe imesainiwa kupitia Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya ili wahakikishe kunakuwa na lishe bora, imekuwa ajenda ya kudumu kwenye Mwenge wa Uhuru ili kuhakikisha watu wakizaliwa wasiwe na ulemavu, hata wale ambao wanapata madhila yanayotokana na kazi katika maeneo mbalimbali na kupata ajali, ameweka Mfuko wa WCF wa fidia kwa mfanyakazi ili kuweza kuhakikisha wanapata huduma pale ambapo wanaweza kupata madhila yanayowapelekea kwenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo lingine ambalo Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya vizuri, kupitia Bunge lako Tukufu, ameendelea kutengeneza utaratibu mzuri wa kufanya kaguzi kwenye maeneo ya kazi kupitia Wakala wa Kazi (OSHA) ili kuhakikisha tunapunguza madhila, tunakuwa na kazi za staha na ajali ambazo zinatokea kwenye viwanda zinazosababisha ulemavu wa kudumu na vifo zinafanyika. Amewezesha OSHA kwanza kwa kupunguza tozo na kuwawezesha, amewapa magari zaidi ya 13 ili waweze kufanya kaguzi kwenye viwanda kwa lengo la kupunguza ulemavu na ajali ambazo zinatokana na kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la maendeleo ya vijana, zipo fedha ambazo zinatolewa kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana za SDL ambapo katika fedha ambazo tumekuwa tukipata ni zaidi ya shilingi bilioni moja. Waheshimiwa Wabunge wamechangia hapa fedha hizo zipatikane, ni kweli tunaendelea na mazungumzo na Serikali na ahadi iliyopo ya Serikali kwa sasa kupitia Wizara ya Fedha ni kwamba, fedha hizi watatupatia, tayari hatua ya awali tumekwishakopesha zaidi ya shilingi bilioni 1.7 ambazo zimeenda kwa vijana kama revolving fund. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaenda kwenye hatua nyingine, katika mikopo hii ambayo imetolewa, miradi zaidi ya 56 ya vijana ilitolewa fedha kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na tayari vijana wanufaika ni 392, walioweza kuunda makampuni kwa ajili ya kuweza kutumia fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia yapo mafunzo ya kukuza ujuzi ambayo fedha hizi za SDL zimekuwa zikisaidia. Pamoja na watumishi wapo vijana ambao wanafanya programu ya uanagenzi, tuliweza kupeleka vijana zaidi ya 9,593 katika mafunzo. mwaka huu wa fedha 2023/2024 ambapo tunaelekea mwaka wa fedha 2024/2025, tayari vijana 6,000 ninavyozungumza wako katika vyuo mbalimbali kwa ajili ya kupata mafunzo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu masuala ya ajira ndani na nje ya nchi; katika kuzingatia hilo na maagizo mahsusi ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na katika utekelezaji wake kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu tumekwishaanza kuingia mikataba na nchi mbalimbali za ughaibuni ikiwemo Saud Arabia na Falme za Kiarabu. Tumekwishaingia memorandum of understanding na tayari tumeshaanza kupeleka wafanyakazi kule, lot ya kwanza tulikuwa tumepata nafasi ya vijana 300 lakini walioenda ni zaidi ya 276. Tutaendelea pia kwenye nchi nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshakaa na Nchi ya Austria tukafanya makubaliano. Kwa sasa tutaendelea kufungua maeneo haya ikiwa ni pamoja na kusajili mawakala wa ajira za nje ya nchi ili nchi yetu iweze kufunguka na tuweze kupata remittance ya fedha ambazo zinakuja ndani ya nchi ili kuongeza pato la Taifa kwa ajili ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado pia katika eneo hilo la ajira tupo kwenye kutekeleza maagizo mahsusi ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara zote za kisekta zimeelekezwa mahsusi ziweze kila mwaka kwa fedha zinazopewa zizalishe ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja. Kwa kufanya hivyo tayari baadhi ya Wizara zimekwishaanza kutekeleza agizo hilo ikiwemo Wizara ya Mifugo ambapo wana BBT Life, ambapo wajibu wao ni kunenepesha mifugo, Mheshimiwa Ulega anafahamu na ameshafanya kazi hiyo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Katambi, kengele ya pili hiyo.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kuwakopesha hawa vijana, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Madini na Wizara nyingine tunategemea kwamba zitafungua fursa zaidi kwa ajili ya kuongeza wigo wa ajira ikiwemo miradi mikubwa ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aliyoyafanya Dkt. Samia Suluhu Hassan ni mengi, muda hautoshi, lakini naendelea kusema kwamba mchango wangu uweze kuingia katika kumbukumbu, naunga mkono hoja, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya makubwa na ndiyo maana maneno yanakuwa mengi kwa sababu mti wenye matunda ndiyo unaopigwa mawe. Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan achape kazi, tupo pamoja naye, maneno siyo kazi, kazi ni vitendo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa George Simbachawene, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya. Mahususi nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kuiongoza nchi kwa kufuata misingi ya utawala bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninasema hivi kwa sababu misingi ya utawala bora imeainishwa kisheria na kikatiba kwa mambo yafuatayo; Kwanza, lazima kuwe na Utawala wa Sheria na ndiyo maana tunaona hatua zinachukuliwa na Mahakama inafanya kazi kwa kuhakikisha kwamba, inatoa hukumu au maamuzi na vyombo vya ulinzi na usalama vinafanya kazi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuna kuheshimu Katiba na tatu, msingi mwingine ni independence of judiciary kwa maana ya kuwa na uhuru wa Mahakama katika kufanya kazi zake bila kuingiliwa. Jambo lingine ni kuwa na heshima au kuheshimu haki za binadamu. Sambamba na hilo kuna suala la kuheshimu maamuzi yanayoamuliwa na Bunge lako Tukufu, hivyo hivyo, kuheshimu misingi ya kidemokrasia kwa mana ya principle of democracy.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yote yamethibitika ndiyo maana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliunda Tume ya Haki Jinai kuhakikisha kwamba kutakuwa na Utawala wa Sheria. Pia aliweka uhuru katika vyombo vya maamuzi ikiwemo PCCB kwa maana ya TAKUKURU kuweza kufanya maamuzi yake pale ambapo hatua zimekuwa zikichukuliwa, na wapo watu wenye kesi Mahakamani, pia wapo ambao wamechukuliwa hatua mbalimbali. Kwa hiyo, kwenye msingi wa Utawala wa Sheria, nchi yetu imekuwa kielelezo na tutaendelea kusimamia hivyo na Katiba yetu tutaendelea kuiheshimu, kuitii na kuilinda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ni muhimu niweze kulizungumzia ni hili la kikokotoo. Kumekuwa na mixed feelings, na ni kweli tunakubali katika upande wa Serikali kwamba suala la kikokotoo kulikuwa na changamoto kubwa. Lazima turudi kwenye historia. Nakumbuka changamoto hii imejitokeza kutokana na historia ya awali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, kupitia Bunge hili Tukufu tulitunga sheria ya kuanzisha Mfuko wa LAPF, tulitunga sheria ya kuanzisha Mfuko wa PSPF, tukatunga sheria ya kuanzisha Mfuko wa PPF, pia tulikuwa na Mfuko wa GEPF na hivyo hivyo tulikuwa na Mfuko wa NSSF katika kipindi cha nyuma. Tusisahau kwamba Bunge hili ndilo lilipitisha sheria hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadaye katika uendeshaji wa mifuko hii zilitokea changamoto mbalimbali zikiwemo za uendeshaji na kuwa mzigo tena katika mfumo, kwa sababu ilikuwa inatengeneza mfumo wa kiushindani. Sasa kwenye masuala ya wafanyakazi, kwa sababu wanachokichangia ni kwa ajili ya maisha yao, ukiweka mfumo wa ushindani, matokeo yake kutakuwa hakuna uwiano wa mafao kwa wafanyakazi ambao walikuwa wakifikia hatua ya kustaafu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika kutengeneza uwiano wa mafao na kupunguza hasara zilizokuwa zikijitokeza kama Operational Cost za uendeshaji wa mifuko, ndiyo yakafanyika maamuzi mwaka 2018 ya kuunganisha mifuko, tukawa na mifuko miwili. Mmoja wa PSSSF kwa ajili ya wafanyakazi wa sekta ya umma, pia kuwa na Mfuko wa NSSF ambao utashughulika na wafanyakazi wasio katika sekta ya umma au sekta rasmi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo haya nini kilichofanyika? Kwanza, tulienda kwenye unafuu. Yapo mafao awali yalikuwa 25%. Katika kuingia kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan tulifanya actuarial evaluation na katika tathmini hiyo ilitupeleka pamoja na kukaa vikao na Vyama vya Wafanyakazi wote nchini, Vyama vya Waajiri wote nchini na upande wa Serikali kuweza kuangalia na kutafuta ule unafuu, tukatoka 25% kwenda 33%.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa ninavyosema, hatua ni nzuri. Mheshimiwa Rais, alishatoa maelekezo zaidi ya mara mbili akiwa amekutana na Jeshi la Polisi Wastaafu, Wakuu wa Jeshi la Polisi, alitoa maagizo kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba, tufanye tathmini na kuangalia upya na kufanya mapitio kuona hiki kikokotoo cha sasa kama tunaweza tukakiboresha zaidi ili wastaafu wetu wasiweze kupata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshaanza kazi hiyo na pia sheria inatutaka tufanye actuarial evaluation kila baada ya miaka mitatu na tayari miaka mitatu imeshafika kuanzia mwaka 2023, na sasa tupo kwenye hatua hiyo. Tumefanya tafiti nchi nyingi, hatuwezi hata siku moja Serikali kufumba macho wala kuziba masikio katika suala ambalo linawahusu Watanzania ambao wamefanya kazi ya heshima kwa ajili ya ujenzi wa Taifa hili. Hatuwezi hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpe pole Mheshimiwa Neema Mwandabila ambaye kimsingi yeye alikuwa anaeleza kwa maana ya jinsi ambavyo tulimwelimisha kupitia mifuko lakini imeonekana kama mashambulizi yamekuwa mengi kwa Waheshimiwa Wabunge ambao wamekuwa wakieleza kulingana na uhalisia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwape pole, lakini tuseme suala hili ni la kisayansi, linahitaji kufanya tafiti za kina ili kuweza kuhakikisha kwanza kunakuwa na uendelevu wa mifuko, na zaidi, katika tija kuangalia wastaafu hawa waweze kupata fedha na wawe na uhakika wa kulipwa mafao yao pale wanapostaafu kuliko vinginevyo ambavyo imekuwa. (Makofi)

Mheshemiwa Naibu Spika, tumefanya utafiti katika nchi za Afrika, tumeona Tanzania tupo tofauti sana katika nchi zote za Afrika katika utoaji wa mafao. Hata nchi za wenzetu kule nje, tena wao hawatoi kabisa ile fedha ya mkupuo. Wakati mwingine kuzitaja hapa inaweza isilete mahusiano mazuri ya kidiplomasia lakini tunafanya tafiti kuweza kuhakikisha watu wetu wanapata mafao.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi mwenyewe nina maslahi, nina wazee wangu watatu sasa hivi wanaelekea kwenye kustaafu. Sasa ingekuwa ni mambo yangu binafsi, pengine au ni jambo la Mheshimiwa Waziri, au ni la mtu mwingine, maana yake angeangalia maslahi na upendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi tunachoangalia ni ile sustainability na nafuu ambayo ataipata mstaafu awaze kupata heshima ya kuwa na fedha nyingi ambazo anazipata baada ya kufanya kazi kwa kutumikia Taifa lake. Pili, ile mifuko iweze kuwaendeleza wale wengine ambao wanachangia. Kwa hiyo, ndiyo maana ilikuwa ni uamuzi wa Serikali kuhakikisha tunakuwa na mifuko miwili sasa, usimamizi wake uweze kuwa mzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia 81% ya wanufaika kwa sasa imeongezeka, ukiacha ya awali 19% peke yake ndio ambao mkupuo umepungua, lakini 81% zimeongezeka hata yale mapato yao ya mwisho wa kila mwezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa sababu jambo hili limeshatolewa maelekezo na Mheshimiwa Rais, Bunge lako Tukufu limetuelekeza, tunalipokea kwa unyenyekevu mkubwa kwenda kulifanyia kazi na pengine tutasikia kauli ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan pale katika viwanja vya Sheikh Amri Abeid, Arusha Tarehe 01 Mei, ambapo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan rafiki wa Wafanyakazi na rafiki wa Waajiri atakutana nao na ataenda kueleza kuhusiana na suala hili. Kwa hiyo, tumelipa uzito unaostahili kuweza kuhakikisha tunaliweka sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala hili la uhamisho. Ni kweli uhamisho kwa mujibu wa sheria, kwanza unaanzia pale ambapo zinatangazwa ajira. Pili,

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja kwa ruhusa yako.

NAIBU SPIKA: Bado unazo dakika tatu.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala hili la uhamisho, Mtanzania yeyote anapoomba ajira hasa hizi za Serikali, kuna kipengele na makubalino kwamba atakuwa tayari kufanya kazi popote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Tanzania Bara au Tanzania Visiwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika kipengele hicho, anapopata ajira, changamoto ambazo tumekuwa tukizipata kwa upande wa Serikali ni pale ambapo anapata ajira, anaenda kufanya kazi na kuna sharti lingine katika sharti lake la ajira kwamba atafanya kazi kuhudumia Tanzania kwa kipindi cha miaka mitatu ili sasa baadaye katika miaka mitatu hiyo ikiisha, ndiyo aweze kuwa na uhuru wa kuweza kuhama kwenda eneo lingine lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, experience inaonesha pale tu ajira zinapotolewa, mtu anakubali popote kwa sababu Serikali inatoa ajira pia kulinga na uhitaji na ikama kuweza ku-balance kwenye maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maeneo ambayo ni ya pembezoni mwa Tanzania, hawapati wafanyakazi na Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakiomba kwamba wakati wao wana upungufu wa Madaktari, Manesi na kadhalika, inapotokea Serikali imetoa ajira kwa ku-balance hiyo ikama na wale waliokubali kwamba wanaweza wakafanya kazi popote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa zaidi ya miaka mitatu bila kuhama, akishapata ajira, hatua ya pili inayofuata ni kuanza kuomba uhamisho. Anaomba uhamisho atoke Kigoma aende Dar es Salaam kwa sababu shangazi ni mgonjwa, mama ni mgonjwa, baba ni mgonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine kuna maeneo utakuta hata vyeti vya forgery; kumekuwa na sababu za kwenda masomoni, na wengine wamekuwa wakiingia hata kwenye ndoa hata zile mkeka wakati mwingine ili tu mwisho wa siku awe na ndoa ya kwenda kuthibitisha kwamba anahitaji kutoka kwenye eneo lile. Sasa hili ni sisi wenyewe katika sababu hizi ambazo zimekuwa zikitolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo sababu nyingine. Hata viongozi tuwe wa kweli kwa ajili ya Tanzania yetu. Hata sisi Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukiombwa uhamisho. Tunakuja tunaandika memo kwamba tunaweza kuwahimisha kutoka kwenye maeneo fulani tunaweka kwa memo kwamba wahamie kwenye Majiji au kwenye Halmashauri za Miji na Mikoa. Lazima tuseme ukweli kwa ajili ya Tanzania yetu. Sasa changamoto inakuja kwamba, mwingine anasema yupo tayari kuhama hata kama bila kupewa hela za uhamisho na hela za mizigo. Akishahama hatujafuta sheria, akirudi anaenda kudai hela yake ya mzigo kwamba hakupewa. Yanarudi malimbikizo tena, huku wakati huo tunahitaji ku-balance ikama ya maeneo ambayo ni remote area na difficult to reach.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna maeneo ambayo mengine kwa kweli hayapo privileged kulingana na ule umbali. Sasa wakishahama wote, tukajaa Dar es Salaam, wote tukajaa Dodoma na wote tukajaa Arusha, mwisho wa siku maeneo ya Tanganyika na maeneo mengine, hawapatikani. Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy anakubali hapa kwamba wapo Madaktari wanataka kuhama, watumishi wanataka kuhama. Lazima tufike sehemu tuitendee haki nchi yetu na tuseme kweli kulingana na changamoto ambazo tunazipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hatujakataa suala la kuhama, ni sahihi na vigezo vilivyowekewa kisheria vitakuwepo, lakini Serikali lazima itafanya uchunguzi na kuangalia na kufanya mapitio ya yule ambaye anastahili kuhama, atahama bila ajizi yoyote na bila mkwamo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni hayo machache, naomba kuunga mkono hoja, lakini nikiendelea kusema kwamba Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan yupo makini katika kuhakikisha nchi yake na Serikali yake inafikia malengo ambayo amewaahidi Watanzania. Mpango wa Maendeleo tutautekeleza, na pia Ilani ya Chama cha Mapinduzi tutaendelea kuitekeleza bila ajizi. Ndiyo maana umeona miradi yote ya maendeleo tumeshafika 90% mpaka 98%, tunamaliza. Hakuna mwananchi au jimbo ambalo halijaweza kupelekewa miradi ya maendeleo na ushahidi huo wewe mwenyewe umezidi kuona.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kama ni taarifa tutaipata baadaye muda wa taarifa ya habari saa mbili asubuhi. (Makofi /Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema, pia nishukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniteua na kuniamini na kunipa dhamana ya kuweza kuwatumikia Watanzania, ninamuahidi yeye pamoja na viongozi wengine Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba nitatekeleza majukumu yangu kwa uaminifu, uadilifu lakini katika kusaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nikupongeze na kukushukuru pia wewe kwa kuendesha Bunge lako vizuri pamoja na uongozi wote wa Bunge aidha niwapongeze pia Watumishi wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu ambao wametusaidia katika majukumu mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, ninaupongeza muhimili wa Mahakama na viongozi wengine pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuendelea kulisimamia Taifa letu kuwa salama.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda nijielekeze katika mambo ambayo yamezungumzwa zaidi au yamechangiwa zaidi na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, nikianza na eneo la ajira. Ofisi ya Waziri Mkuu mbali na majukumu mengi yaliyopo inalo jukumu pia la kuweza kuhakikisha kwamba inasimamia na kuratibu Sera pamoja na sheria zote zinazohusika na masuala ya ajira. Katika msingi huo tunamshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa akituelekeza wakati wote tuweze kuwapokea, kuwasikiliza pia kuwahudumia wale wote ambao wanafika katika ofisi hiyo kwa ajili ya kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, katika study ambazo tumejaribu kuzifanya ili kutafuta ulinganifu na suluhu ya changamoto za masuala ya ajira nchini, Ofisi ya Waziri Mkuu na kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Waziri wangu wa nchi Professor Joyce Ndalichako pamoja na watumishi tumejaribu kufanya study na ulinganifu mbalimbali katika kuangalia changamoto za ajira kwa nchi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tumeweza kufanya utafiti wa kuangalia na kuandaa taarifa ya uchambuzi wa sera, sheria na mikakati ya nchi mbalimbali kuhusu utatuzi wa changamoto za ukosefu wa ajira. Katika maeneo ambayo tumejaribu kuangazia mojawapo ilikuwa ni nchi ya Uganda, Rwanda, Brazil, China Marekani, Tunisia, Uturuki, South Afrika na Kenya.

Mheshimiwa Spika, katika maeneo hayo yote ambayo tumefanyia utafiti wenzetu wamefanana pia maeneo mengi na sisi lakini sisi pia tumeenda hatua ya mbali zaidi. Changamoto kubwa ambazo zinaonekana katika wimbi hili kubwa la ukosefu wa ajira, ambalo sehemu nyingi wanaita kama timing bomb duniani, sababu zinazosababisha ukosefu au changamoto ya ajira nyingine ni chanya na nyingine hasi.

Mheshimiwa Spika, sababu ya kwanza ni ongezeko la taasisi za elimu kwa maana ya uhamasa katika kusoma, kumekuwa na wahitimu wengi katika kada mbalimbali tofauti na uhitaji wa ajira. Sababu ya pili ya kidunia inayoelezwa katika takwimu mbalimbali za International Labour Organization kwa maana ya shirika la kazi duniani, pamoja na taasisi nyingine ni uwepo wa advancement ya teknolojia.

Mheshimiwa Spika, uwepo wa teknolojia umeenda ku-replace human labor, kwa maana ya computer au mashine sasa inaweza ikafanya kazi ya watu zaidi hata ya
100. Sababu nyingine imeelezwa ni masuala ya natural catastrophic na force majeure - acts of God pamoja na masuala kama ya magonjwa kama vile COVID-19 ambayo imesababisha viwanda vingi kufungwa na changamoto nyingine pia makampuni na kadhalika kuweza kufilisika.

Mheshimiwa Spika, sababu nyingine ni masuala ya sasa biashara kiujumla duniani, Serikali zimeacha kufanya shughuli ya biashara na badala yake zinatoa huduma, kwa hiyo biashara imelekezwa katika private sector. Jingine ambalo limeelezwa katika takwimu ni masuala ya viwango vya elimu inayotolewa, mtu apate skill na knowledge competence and performance ya kuweza kufanya kazi. Kwa hiyo, wanapimwa kulingana na ubora na hizo ndio wakati mwingine vimekuwa ni vigezo vya kuweza kusaili watu.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kimefanyika kwenye Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika eneo hili na katika kutafuta njia mbadala sasa za kukabiliana na changamoto hizo. Kwanza katika kufanya hivyo tulifanya pia utafiti wa kuangalia wingi wa vijana wengi ambao wanaingia katika soko la ajira kila mwaka. Katika tafiti tulizozifanya ukiangalia kwa darasa la saba ukiacha kwa sababu ya muda nisianze mwaka 2012 mpaka mwaka 2021 niende kwenye mwaka 2021 peke yake.

Mheshimiwa Spika, wahitimu wa darasa la saba walikuwa milioni moja na laki moja, kidato cha Nne ni Zaidi ya laki nne na themanini na saba elfu, kidato cha sita ni zaidi ya wahitimu elfu themanini, walioweza kufuzu mafunzo ya VETA ni zaidi ya laki mbili na thelathini na sita na FDC Wahitimu Zaidi ya elfu kumi na moja, lakini pia NACTE ni wahitimu elfu themanini na saba. Kwa ujumla ukienda kwenye vyuo vikuu peke yake kwenye soko wanaingia 47 elfu katika soko la ajira.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kwa sababu ukija kuangalia katika ujumla wake tuna watu zaidi ya laki moja wanohitaji ajira katika soko tofauti na hitaji lilivyo.

Mheshimiwa Spika, hatua tulizozichukuwa Ofisi ya Waziri Mkuu ni:

Moja; kuandaa na kutengeneza uwepo wa vyuo vya VETA kama jinsi China walivyofanya vyuo vikuu zaidi ya laki sita wamevibadilisha na kuwa vyuo vya kati kuweza kutoa mafunzo na skills za kazi.

Pili; tumeendelea kutoa fedha za mikopo za kuweza kuwasaidia katika ngazi za Halmashauri na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ili waweze kupata mitaji ya kuweza kufanya shughuli mbalimbali.

Tatu; kumekuwa na mkakati wa kutengeneza mfumo wa ukuzaji wa ujuzi wa vijana ambao wamekuwa wakitoka vyuo vikuu na wale ambao hawajarasilimishiwa ujuzi, tumekuwa tukitoa fedha kwa ajili ya kurasimisha ujuzi na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa mwaka wa jana alitoa zaidi ya bilioni tisa ilinufaisha vijana zaidi ya 14,440 katika mafunzo.

Mheshimiwa Spika, pia kuna mafunzo ya...

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika,
ahsante sana kwa nafasi hii. Ninashukuru sana nami niungane na wenzangu kuwapongeza sana Wizara ya Ulinzi lakini pia nimshukuru na kumpongeza sana Amiri Jeshi Mkuu Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuiongoza Nchi yetu vizuri na mpaka sasa tunaona amani na salama tunayo na tunaendelea kujenga uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru pia wewe kwa kunipa nafasi hii zaidi nichangie tu kidogo kwenye eneo moja, Kwanza niwape confidence ya Serikali kwenye eneo hili, imezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge vizuri sana hapa kuhusiana na hoja mbalimbali wote ni nia njema ya kutaka kuboresha vyombo vyetu hivi vya ulinzi na usalama na hasa Jeshi letu hili.

Mheshimiwa Spika, Vyombo vya Ulinzi na Usalama vinatambulika kwenye Katiba kwa mujibu wa Ibara ya 147 (1) na (2) lakini pia ni jambo ambalo liko kwenye orodha ya Muungano katika orodha namba tatu na sambamba na hilo vyombo hivi vya ulinzi na usalama Amiri wake Mkuu kwa mujibu wa Ibara ya 148 ya Katiba ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na si mwingine ni Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatambua Serikali upande wa umuhimu kubwa wa Jeshi hili la kwetu hapa la ulinzi na usalama, kwa kutambua umuhimu huo kwa sababu jeshi hili limefanya kazi kubwa ya kulinda mipaka ndani na nje ya nchi lakini pia kulinda viongozi wetu, kulinda uchumi wetu ili isitokee wakati wowote hali ambayo itapelekea kupoteza usalama wa Nchi na hivyo kurudi nyuma katika uchumi na hata kupoteza maisha au usalama wa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika suala hilo niweze kueleza tu kwenye maeneo ambayo yamezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge. Kwanza limezungumzwa hapa suala la kuhusiana na kodi. Niwape tu uhakika na kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba michango yote ambayo wameizungumza hasa kwenye maeneo ya kodi kwenye vifaa vya Jeshi lakini pia maslahi megine ya vyombo vyetu hivi vya ulinzi na usalama si yote ambayo tunaweza tukayazungumza hadharani hapa, kwa sababu Bunge lako Tukufu hili linaenda public, lakini kuna mambo niwahakikishie na kuwapa confidence Waheshimiwa Wabunge kwamba kama Serikali tumeyachukua tunaheshimu sana na kupokea mchango wao kwa moyo mkunjufu ili tuweze kufikisha na viongozi hawa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana husika atakutana na Waziri wa Fedha lakini pia wataongozwa na viongozi na timu nzima, kwa ajili ya kuyaangalia pia masuala haya ya kikodi yamekaaje na kuweza kuyaweka sawa sawa ili kuimarisha Jeshi letu ambalo lina heshima kubwa sana ndani na nje ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, mnakumbuka kwenye peace keeping mission mara nyingi Tanzania tumekuwa tukipata record nzuri sana ya kufanya vizuri katika kazi za Kimataifa ambazo zimekuwa zikitokea katika Ukanda wa Afrika hata katika ngazi ya Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunatambua kwenye eneo lingine la masuala ya wastaafu ambao ni Wanajeshi, wanapopumzika sasa tunatambua wanakuwa wamechangia na wamefanya kazi kwa kweli kubwa kwa kuweka mchango wao kwa masuala ya kiusalama lakini pia ujenzi wa Taifa katika suala la uchumi. Mimi pia katika eneo hili nieleze na kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kwa sababu Mawaziri wenye dhamana husika hapa pengine hawapo lakini kwa hatua hii kwa sababu sisi tuko hapa kuwakilisha hili, tunalichukua nalo na tutaenda kufanya kazi ya kufanya mapitio upya ya wastaafu wetu wa vyombo vya ulinzi na usalama ambao bado wana changamoto za kuhusiana na kupata mafao yao au kupewa stahiki zao ili kuweza kuhakikisha kwamba basi tunaona na kuheshimu mchango wao katika kipindi chote ambacho wamefanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia katika maeneo mengine ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na suala la fursa za ajira kwa ajili ya vijana wetu na namna ya kuweza kuunganisha na kutengeneza teamwork pamoja na Jeshi hili kwa maana ya Wizara ya Ulinzi. Hili nalo tunalichukua kwa ajili ya kulifanyia kazi na hivi yote ni kwa sababu ya maslahi mapana ya Taifa letu lakini nizidi kuhakikishia Watanzania wote wanaonisikiliza lakini pia Bunge lako Tukufu. Sisi Serikali tuko imara tukiongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye Amiri Jeshi Mkuu katika vyombo vya ulinzi na usalama wakati wote, tutasikiliza kwa unyenyekevu na tutaenda kutoa huduma inayostahiki kwa mujibu wa mambo yale ambayo yatakuwa yamepangwa ili kuweza kuhakikisha mipango na mikakati inawekwa sawa sawa ili kuweza kuhakikisha Taifa letu linakuwa salama pia tunaendelea kuulinda uchumi wetu wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatutakuwa na uchumi wala hatutakuwa na shughuli kama usalama utakuwa hatarini, kwa hiyo usalama ni kipaumbele namba moja cha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa muda wako, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)