Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Eng. Kundo Andrea Mathew (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nipende kutoa shukrani zangu na pongezi kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa maono yake makubwa katika sekta hii ya mawasiliano kwa kufungua milango ya uwekezaji. Ambapo sisi sekta ya mawasiliano tunaiona na katika kuwekeza, katika miundombinu na mifumo ya mawasiliano na pia kwa utayari wake ili kurejea Sera na Sheria ambazo haziendani na wakati wa sasa, ambapo tuna teknolojia zinazoibukia hivyo basi Mheshimiwa Rais yuko tayari.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuridhia mchakato wa uundwaji wa satellite yetu. Ambapo anaenda kuweka alama kubwa sana katika sekta ya mawasiliano na katika ulinzi wa nchi yetu hivyo tunampongeza sana kwa kutekeleza mfumo wa anuani ya makazi kwa asilimia 100 kabla hata ya kufikia mwaka 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuniamini na kwa kuakikisha kwamba leo hii nasimama katika bajeti ya tatu ya Wizara hii nikiwa namshukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa maelezo yake, kwa ushauri wake wa kuhakikisha kwamba sisi wasaidizi wake tunaendelea kufanya kazi kwa weledi mkubwa. Nimshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Nape Moses Nnauye Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa uongozi wake mzuri, maelekezo yake na kwa malezi yake yenye lengo la kuinua Sekta ya Habari na Mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Katibu Mkuu, Mheshimiwa Mohammed Khamis Abdulla pamoja na Naibu Katibu Mkuu na Wakurugenzi wote wa Taasisi ambazo ziko chini ya Wizara yetu. Niwapongeze na kuwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Bariadi kwa kuendelea kunipatia ushirikiano katika majukumu yangu ndani ya jimbo na wakati napotekeleza majukumu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kutumia fursa hii kumshukuru sana mke wangu Grace ambaye kwa kweli ananipatia utulivu na kuhakikisha kwamba nawajibika vizuri katika majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru wewe pamoja na Mheshimiwa Spika, kwa kuendelea kuongoza Bunge hili kwa viwango vya kimataifa. Baada ya kusema hayo sasa naomba nirejee hoja za Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, kwanza tunaishukuru sana Kamati yetu ya Kudumu ya Miundombinu pamoja na michango yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wamejaribu kugusia. Niseme jambo moja Wizara hii champion wake ni Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania akisaidiwa na kaka yangu, Mheshimiwa Waziri, Nape Moses Nnauye, pamoja na Taasisi zetu ambazo ziko chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tumebaini kuna changamoto katika mgawanyo wa minara ambapo Waheshimiwa Wabunge wamejaribu kugusia na mgawanyo huu tuliangalia kwa kuangalia wilaya kwa wilaya. Lakini baada ya kugawa kwa wilaya tukagundua kwamba kuna majimbo mawili kwenye baadhi ya wilaya hatimaye tukajikuta kwamba kuna baadhi ya majimbo yanapata minara mingi na majimbo mengine yanapata minara michache, hivyo tumeishaliona hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nitumie fursa hii katika Bunge lako tukufu kusema kwamba Mheshimiwa Rais, amesaini mikataba ya kufikisha huduma ya mawasiliano katika Kata 713 kwa ujenzi wa minara 758. Hiyo ni mvua ambayo haijawahi kushuhudiwa sasa tunakuja na mvua nyingine ya kuleta minara 1,600. Ambapo Mheshimiwa Rais tayari ameisharidhia na ameishatafuta fedha na tutaanza na minara 600, ambayo kufikia Desemba nafikiri fedha zitakuwa zimeishapatikana tayari mchakato utakuwa umeishaanza wa kutafuta wakandarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo Waheshimiwa Wabunge niwatoe hofu na Watanzania kwa ujumla mvua hii itakapokatika itaanza mvua nyingine ya minara. Kwa hiyo, tutahakikisha nchi yetu inafikishiwa huduma ya mawasiliano kwa mujibu wa utekelezaji wa Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ambalo Waheshimiwa Wabunge wameligusia kwamba Wizara yetu mpaka sasa tumepokea fedha kidogo katika miradi ya maendeleo. Miradi yetu yetu inatekelezwa kwa ujenzi na wakandarasi, mkandarasi anapopatikana hatuwezi kumlipa fedha zote mpaka pale atakapokuwa anatoa certificate na miradi hii mingine inakamilika kwa miezi sita, mwaka mmoja. Hivyo tunatarajia kila anapokamilisha hatua moja na anapo raise certificate na ndipo tunapoweza kufanya malipo. Kwa hiyo, fedha zipo na tuna uwakikia watakapoleta certificate watalipwa na miradi itakamilika bila kuwa na changamoto yoyote ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna baadhi ya Waheshimiwa wameshauri na kuna baadhi ya changamoto nipende kusema kwamba baadhi ya changamoto zao tumezipokea, ushauri wenu tumeuzingatia, maoni yenu tunayazingatia na tutahakikisha kwamba tunaenda kuyafanyia kazi kwani nyinyi mko hapa kwa niaba ya Watanzania milioni 63 hivyo Serikali hii ya Mama Samia Suluhu Hassan ni sikivu na sisi wasaidizi wake tutahakikisha kwamba tunafanyia kazi mambo yote hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee jambo moja la mkomazi Mheshimiwa Zuena Athumani Mbunge kutoka Kilimanjaro aliongelea kuhusu usikivu wa TBC. Usikivu wa TBC tulikuwa na mtambo wetu pale Rombo Tarakea ule mtambo uko chini na sasa tunaenda kufunga mtambo mwingine pale Rombo DC. Hivyo tutakuwa tumetatua kabisa changamoto ya maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile umeongelea kuhusu hifadhi ya Mkomazi, katika hifadhi hiyo tayari kuna mawasilino tunapeleka katika eneo la Kata ya Kilia, Kwakoa, Toloha pamoja na Mgagawa ambazo ziko pembezoni mwa nchi yetu ambapo baada ya kuweka hiyo minara itaweza kufikisha huduma ya mawasiliano katika lango la hifadhi ya Mkomazi. Kwa suala kama hili naamini kwamba Mheshimiwa Mbunge awe na subira na Serikali iko kazini kuhakikisha kwamba changamoto hii inatatuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nimeshuhudia Waheshimiwa Wabunge wakiishukuru Serikali na sisi hatuta bweteka kwa shukurani zao. Sisi tutaendelea kuhakikisha kwamba katika maeneo ambayo bado hayajafikishiwa huduma na mawasiliano na katika changamoto zile ambazo wamekuja kuzisema kwa niaba ya wananchi wao sisi tunazichukua na tutaenda kuzifanyia kazi kwa weledi, maarifa yote kwani tunazingatia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nikushukuru sana na niombe kusema kwamba niwashawishi Waheshimiwa Wabunge, tuiunge Bajeti yetu hii kwa asilimia mia moja kwani ni bajeti shirikishi na ni bajeti ya wananchi…

NAIBU SPIKA: Ahsante, ahsante kwa mchango mzuri.

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa hii nami nichangie katika mapato na matumizi ya mwaka wa fedha 2022/2023 Wizara ya Habari na Teknolojia ya Habari. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuwa na afya njema, lakini vile vile nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini katika nafasi hii ya Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile nishukuru Bunge lako Tukufu kwa kuendelea kutupatia mchango mawazo maoni ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kuboresha katika utekelezaji wa majukumu yetu. Lakini sambamba na hilo nawapongeza sana na kuwashukuru watendaji wote wa Wizara vile vile wakiongozwa na Mheshimiwa Waziri wangu Mheshimiwa Nape Mose Nnauye lakini vile vile namshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais Dkt. Mpango pamoja na Waziri Mkuu pamoja na Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu lakini pia natambua mchango mzuri sana ambao umetolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wakichangia bajeti yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kabisa kwamba muda hautoshi lakini natambua michango ya Waheshimiwa Wabunge inalenga kwenda kutatua changamoto za wananchi walioko katika Majimbo yao. Lakini tunasema kwamba ili nchi yoyote iweze kuendelea ni lazima kwanza tuwe na huduma bora na za uhakika, lakini kabla ya kuwa na huduma bora za uhakika ni lazima tuwe na miundombinu ambayo inaweza kutoa huduma hizo lakini pia tuwe na sera safi tuwe na utulivu wa kisiasa na sheria nzuri lakini haya yote yanawezekana kutokana na kiongozi mahiri mwenye maono na anayetaka matokeo chanya kwa watanzania ambaye sasa tunaye Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kweli mambo mengi yanafanyika kwa kasi kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu zifuatazo; mwaka huu pekee minara 488 inaenda kufanyiwa upgrading ambayo ni takriban bilioni 9.76 ambayo imeandaliwa. Lakini vilevile tuna dola milioni 150 ambayo inaenda kutekeleza mradi wa Tanzania ki-digital ambapo ukiangalia ni minara 763 inaenda kujenga. Lakini vilevile kuna minara ambayo tayari imeshajenga takriban 161, kuna minara ambayo haijawashwa imeshakamilika 181. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yakishakamilika changamoto zote za Wabunge ambazo leo wameziongea hapa zitakuwa zimeisha kama siyo kupungua kwa kiasi kikubwa sana umeshuhudia Waheshimiwa Wabunge wamesimama hapa wameongelea namna ambavyo tumefika kwenye majimbo yao lakini vile vile maeneo ambayo tumefika katika majimbo yao wamejionea katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri maeneo yao yamejumuishwa katika bajeti yetu. Kwa hiyo, tuwaombe Waheshimiwa Wabunge tuendelee kushirikiana kuhakikisha kwamba tunaendelea kujenga Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa ambacho naweza kuongea hapa ni uelekeo wa Tanzania tunayoenda nayo sasa ni Tanzania ya kidigitali na Tanzania hii inaendana sambamba na ujenzi wa miundombinu ambayo inaenda kutoa huduma hizi. Miundombinu hii ni pamoja na Mkongo wa Taifa, ni ujenzi wa minara kama ambavyo nimetaja, katika zoezi la anuani za makazi na postcode ambalo Mheshimiwa Waziri ameongoza timu yetu ya Wizara kuhakikisha tunafikia kiwango cha asilimia 106.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa majukumu yetu haya ni utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi ukurasa wa 98 Ibara 61(j)na(m) ni katika kuhakikisha tunaweka mawasiliano kwa Watanzania ili waweze kufanya biashara zao, waweze kuwasiliana kwa sababu tafsiri yetu ni kwamba mawasiliano ni uchumi, mawasiliano ni usalama na mawasiliano ni haki ya kila mtanzania kuipata. Na sisi wasaidizi wa Mheshimiwa Rais tunaenda kwa kasi kweli kweli kama ambavyo yeye mwenyewe ametuelekeza tufanye kwa utashi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyagusia naomba niyajibu kwa haraka haraka. Suala la TTCL ambalo limegusiwa na Mheshimiwa Tabasamu TTCL hawajauza minara na kama ambavyo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema kwamba TTCL tunaenda kuiwezesha ili ikasimamie miundombinu yote ya kimkakati ikiwemo na ujenzi wa minara na usimamizi na Mkongo wa Taifa minara yote na miundombinu mingine yote ya kimkakati TTCL inaenda kusimamia. Kwa hiyo, niliomba niweke ufafanuzi kwa namna hiyo katika upande huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile naomba nitolee ufafanuzi jambo moja ambalo liliongelewa na Mheshimiwa Zuena Mheshimiwa Bushiri. Kwenye suala la Mkomazi tayari tumeshaliingiza katika utekelezaji kwa bahati mbaya katika bajeti iliyopita tuliliingiza kwa bahati mbaya watoa huduma hawakuweza kulichagua lakini tumeliingiza kwenye mpango mahsusi wa National Parks ambapo sasa tunaenda kuhakikisha kwamba tunaweza utaratibu maalum ili mtoa huduma lazima apatikane kwa ajili ya kufikisha mawasiliano katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile suala jingine ambalao nimeona Mheshimiwa Condester Sichalwe ameliongelea kwa sababu ameongelea masuala ya teknolojia na sisi tunahakikisha kwanza tunaweka Sera safi ambayo ni wezeshi wawekezaji waweze kuja lakini vile vile katika force industrial Revolution imaging technology hatuwezi kuzikwepa kwa sasa. Imaging technology ni kama vile Artificial Intelligence, Block Chain Technology, Internet of Things haya yote tunaenda kuhakikisha kwamba tunaweka mazingira rafiki ili yote yaweze kufanyika kwa sababu…

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Waziri.

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: …na sisi ndiyo uelekeo wetu wa Tanzania kwenda katika Tanzania ya kidigitali…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, majibu mazuri!

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kuwepo ndani ya Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda niwapongeze Menejimenti ya Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari ikiongozwa na Mheshimiwa Waziri, Dkt. Faustine Ndugulile; Katibu Mkuu, Dkt. Zainab Chaula; na Dkt. Jim Yonazi, kwa ajili ya kazi hii kubwa ambayo imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwapongeze Waheshimiwa Wabunge kwa michango, maoni na ushauri walioutoa, hakika imeonesha namna gani sote tunatembea katika njia moja ya kuhakikisha kwamba sekta yetu na Wizara yetu ya Mawasiliano inazidi kwenda mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite katika baadhi ya maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyagusia. Tukianza na masuala ya minara ambapo baadhi ya Wabunge wameweza kuonesha kwamba katika maeneo yao kuna changamoto ya minara; mingine ambayo haijawaka, pia ambapo inasababisha na wengine wanasema kwamba ndoa zinavunjika na wengine wanatumia miti kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wanapata mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niongelee suala ambalo linahusika na masuala ya mipakani ambapo kuna changamoto ya gharama za mawasiliano kupitia roaming ambayo inafanyika katika mipaka. Naomba nikufahamishe kuwa suala la roaming tayari Serikali kupitia Wizara ya Mawasiliano tumeshalifanyia kazi na tayari tumeshaingia mkataba, Roaming Agreement na wenzetu wa East Africa ili kuhakikisha kwamba gharama za kupiga simu ukiwa katika maeneo ya mipakani zinashuka. Hivyo basi, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wakiwepo katika maeneo hayo, basi hili ndilo ambalo linakwenda kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunafahamu tuna changamoto ya mawasiliano mipakani. Changamoto hii inatokana na mwingiliano wa mawasiliano na kuna maeneo mengine ambayo hakuna kabisa mawasiliano, lakini kupitia Mfuko wa Mawasiliano wa Wote, tumeshafanya tathmini na tunakwenda kuhakikisha kwamba mipaka yetu yote inakwenda kufikishiwa mawasiliano ili kuhakikisha kwamba changamoto hii inaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na mipaka hiyo takribani minara 160 ambayo itajengwa katika kuzunguka nchi yetu yote katika maeneo ya mipaka, tunafahamu pia kuna baadhi ya ofisi za Halmashauri ambazo ni mpya lakini bado zina changamoto ya mawasiliano ikiwepo Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe ambapo tunakwenda kuweka huduma ya mawasiliano; tuna Wilaya ya Tanganyika, Kakonko, Malinyi, Mtwara DC, Msalala DC, Bariadi, Nzega, Kilindi pamoja na Pangani. Maeneo haya tunakwenda kuhakikisha kwamba katika zabuni ya awamu ya sita yanaingizwa na utekelezaji wake utaanza mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kabisa kwamba Waheshimiwa Wabunge wameongelea masuala ya co- location. Nasi tangu tulivyoteuliwa tarehe 5 Desemba, 2020 na kwa maelekezo mahususi kabisa, mimi pamoja na Mheshimiwa Waziri tulitoa maelekezo kwamba kuanzia sasa hatutajenga mnara ambao utakuwa unatoa huduma ya operator mmoja. Kuanzia sasa tutakuwa na cost sharing, maana yake kutakuwa na co-location, mnara mmoja uweze kuhudumia makampuni mawili au matatu kulingana na uhitaji wa eneo husika. Kwa hiyo, hayo tunakwenda kuyafanyia kazi kwa utaratibu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo haya yameendana sambamba na kuhakikisha kwamba tunatoa maelekezo kwa watoa huduma kuhakikisha minara yote ambayo ilijengwa ikiwa inatumia teknolojia ya 2G, yote inakuwa upgraded na inatoa huduma ya 3G na 4G. Pia Serikali bado inaendelea kujiridhisha na uhitaji iwapo tutahitaji 5G na pia soko litaamua ni nani atahitaji kutumia. Serikali kazi yetu ni kuhakikisha kwamba tunaweka miundombinu na sera safi za kuhakikisha kwamba wawekezaji wetu wanaweza kufanya biashara bila kuwa na changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunafahamu kabisa kwamba tuna changamoto; na Waheshimiwa Wabunge wamegusia masuala ya vifurushi. Katika suala la vifurushi Waheshimiwa Wabunge wameuliza kwa nini tuwe na bundles? Kwa nini tusiwe na utaratibu wa kutumia mpaka ukamaliza salio lako wewe mwenyewe? Kwa kutumia nafasi hii, naomba nikufahamishe kwamba suala la bundles ni sawa sawa na gharama au biashara ya jumla, lakini Mtanzania hajalazimishwa kununua vifurushi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna huduma ya aina mbili; pay as you go, maana yake ni kwamba unatumia kwa kadri wewe mwenyewe unavyohitaji, lakini pia tuna huduma ambayo ndiyo ya vifurushi sasa ambapo utaamua kuchagua kifurushi cha siku moja, siku mbili, siku tano, ni wewe mwenyewe. Changamoto ambayo tumeiona, siyo kwamba ni kwa nini tununue vifurushi? Watanzania hawajui matumizi, namna gani yanatumika katika simu zao? Sasa hilo Serikali tumeanza kulifanyia kazi kuhakikisha kwamba Mtanzania awe anajua bundle lake limetumika wapi; na ametumia kiasi gani na kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumekuja na utaratibu ambao tunakwenda kuhakikisha kwamba ukishanunua bundle lako kuna njia mbili za kuhakikisha kwamba halipotei. Iwapo muda wa matumizi, kwa mfano, umenunua bundle la siku saba, lakini inafika siku ya saba umeshatumia GB labda tatu na ulikuwa umenunua GB kumi, utakuwa na fursa mbili; ya kwanza ni ku-top up, maana yake utanunua bundle lile lile ambalo ulikuwa umenunua hapo awali maana yake tuta- carry forward ile balance ya bundle lako la hapo awali, maana yake ni kwamba utalitumia. Kama ulikuwa umebakiza saba, maana yake ni kwamba ukinunua 10 utakuwa na 17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukajua kwamba kuna changamoto nyingine, mwingine atakutwa hana salio la kununua hilo bundle au ku-top up, maana yake ni kwamba utakuwa unaruhusiwa sasa kuhakikisha kwamba unamhamishia rafiki yako ambaye ataweza kuitumia hiyo bundle, nafikiri itakuwa kwa maelewano yenu ninyi binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utakuwa umehakikisha kwamba bundle lako, kama ni 10 GB utakuwa umeweza kuzitumia zote. Kama utashindwa kuzitumia zote, basi rafiki yako. Tutakuwa na utaratibu wa kuhakikisha kwamba kiwango cha chini cha kuhamisha bundle ni MB 250, lakini utakayemhamishia hataruhusiwa yeye kumhamishia mtu mwingine. Utakayemhamishia, yeye ataruhusiwa kuitumia mpaka itakapokwisha. Haya yote tunaendelea kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunafahamu kwamba kuna changamoto ya masuala ya gharama. Serikali ni Sikivu; na hili tunaendelea kulifanyia mchakato, tutakapokuwa tumejiridhisha, kwa sababu biashara hii inahusisha pande tatu; Serikali, watumiaji na watoa huduma, pale ambapo tutaamini sasa kwamba tumefikia maelewano ya kutosha, basi tutakuja na mpango ambao utahakikisha kwamba unawasaidia Watanzania ili waendelee kufanya biashara mtandao na kufanya mambo mengine ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba tunaelekea katika uchumi wa kidigitali. Uchumi huu wa kidigitali tunahitaji kuwa na uwezo wa kufanya biashara mtandao, biashara mtandao hii inatokana na miundombinu ambayo tutakuwa nayo sisi Watanzania, miundombinu ambayo itakuwa wezeshi ambazo ndiyo drivers za kutufikisha sasa kwenye uchumi wa kidigitali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa tuna miundombinu ya aina tofauti; kuna Mkongo wa Taifa ambao mpaka sasa tumeshajenga takribani kilometa 7,910 na tayari kuna zingine tena tunaelekea kujenga kilometa 409. Vilevile katika mwaka fedha huu ambao tunaombea bajeti hii tunaenda kujenga kilometa 1,880. Kadri ambavyo muda unaenda, tutakuwa tunahakikisha kwamba baadhi ya changamoto tunazifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nashukuru Waheshimiwa Wabunge wamegusia suala la National Internet Data Center, kwa kweli Data Center yetu ina uwezo mkubwa ni three tier kama walivyosema ambayo ina interruption ambayo inaenda kwenye 99.82 ambapo kwa kweli hii ni ya kiwango cha juu, kwa sababu kiwango cha juu kabisa katika ubora wa Data Center ni tier four. Sasa tunaamini kabisa kwamba katika Afrika Mashariki na Kati Data Center yetu inatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wakiwa na biashara zao, wakiwa na makampuni yao, Data Center yetu ni sehemu sahihi kwa ajili ya kutunza taarifa zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miundombinu ya anuani za makazi na postikodi; ili tuweze kufanya biashara mtandao kuna mazingira ambayo yatatufanya sasa tuweze kufanya biashara yetu bila kuwa na changamoto yoyote. Wizara yetu tayari imeshatenga bilioni tatu katika mwaka wa fedha 2020/2021, lakini imetengewa kiasi kingine katika bajeti hii inayokuja kwa ajili ya kuhakikisha kwamba anuani za makazi na postikodi zinakuwa vizuri. Hii faida yake ni kwamba; wenzetu wa halmashauri itawasaidia kupanua wigo katika ukusanyaji wa mapato. Pia Mamlaka ya Mapato Tanzania itawasaidia kuwajua walipakodi wao na wafanyabiashara wao ili kuweza kuhakikisha kwamba wanapofikia hatua ya kukusanya kodi, basi watawafikia kiurahisi, kwa sababu hii itaweza kutoa anuani pale ambapo mlipa kodi alipo na nyumba anayokaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumekuja na mfumo wa kuhakikisha kwamba una uwezo wa kumfikia mwenzako pale alipo kwa kutumia application inaitwa NAPA, ambapo sasa badala ya kutumia Google Map, sisi tumejiongeza na kuhakikisha kwamba tunatumia mfumo wetu ambao umejengwa na vijana wa Kitanzania, ambao ni vijana wetu, kwa sababu sisi kama Serikali tumeamua kuhakikisha kwamba tunawekeza zaidi katika local content.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo local content ambayo ni ya watu wa kutoka nje, ni local content ikiwa na maana anayeifanya kazi ni Mtanzania mwenyewe na vilevile anaye- deploy ni Mtanzania mwenyewe. Kwa hiyo tunaamini kabisa iwapo anuani za makazi, mradi huu utakapokamilika na niwaombe Waheshimiwa Wabunge tutakapofika katika halmashauri zao waweze kutupa ushirikiano pale ambapo tutakuwa tunaweka hizi alama na majina ya mitaa, basi tusiwe na changamoto yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu tunautekeleza kwa ushirikiano mzuri sana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI). Pia tunawapongeza sana Wakurugenzi nchini kote wamekuwa wakitoa ushirikiano wa kutosha. Tunaamini kwamba tukishafikia hapa basi tutakuwa tuna uwezo wa kufanya biashara mtandao, tutaweza kuagiza bidhaa yoyote ukiwa umekaa nyumbani na ukaweza kufikishiwa nyumbani bila kuwa na changamoto yoyote. Tunaendelea vile vile kuimarisha mifumo yetu ya kifedha ambayo haitotoa nafasi ya udanganyifu wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kabisa kwamba teknolojia inakimbia kwelikweli lakini na sisi tumejipanga kwelikweli kuhakikisha kwamba iwe kama mwizi na Polisi, kwamba hatutaki kuachwa nyuma, kama itafikia sasa wakati ambapo itabidi tutumie block chain technology huu ndiyo wakati wenyewe. Tutajiridhisha wapi tutumie na tutakapokuwa tayari Waheshimiwa Wabunge, basi tutakuwa tumefikia katika lengo ambalo litakuwa linasaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge pia wameongelea suala la utapeli mtandaoni, hasa tuma pesa kwa fulani, tuma kwenye namba hii. Naomba nikujulishe, tumeunda Kamati, ambapo kikao cha Makatibu Wakuu ambao tunalenga katika hii sekta sana sana katika masuala ya cybercrime, maana kwamba nani hii makosa ya kimtandao, wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia Habari na watu wa Sheria watakaa tarehe 20 kwa ajili ya kujadili namna bora ya kuhakikisha kwamba haya masuala tunayatatua. Ikiendana sambamba na hiyo, tarehe 26 kikao cha Mawaziri pia kitakaa kwa ajili ya ku-finalize na kujua kwamba tufanye jambo gani. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Waziri.

NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa hii nami niweze kuchangia katika hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu ili katika nafasi mbalimbali niweze kutoa ufafanuzi katika maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wameweza kuyagusa katika Wizara yetu ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.

Mheshimiwa Spika, nimepitia hoja ya Mheshimiwa Mhata Mbunge wa Nanyumbu kuhusiana na masuala ya ujenzi wa mkongo wa Taifa ambapo matarajio yake ni kwamba mkongo huu unapokamilika basi alitarajia mabadiliko ya bei yatokee katika Jimbo lake la Nanyumbu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa Serikali ilianza kuwekeza katika ujenzi wa mkongo wa Taifa mwaka 2009 ambapo kufikia mwaka 2021 tayari kilometa 8,319 zilikuwa zimejengwa nchi nzima kwenye Mikoa 25 vilevile Wilaya 43.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako Tukufu lilipitisha bajeti mwaka jana ya ujenzi wa mkongo wa Taifa takribani Bilioni 170 ambazo ni uwekezaji ambao unaenda kukamilika katika mwaka huu wa fedha ambapo takribani kilometa 4,442 zitaweza kukamilika, maana yake itakuwa tumefikia asilimia 85 ya lengo la kufikia kilometa 15,000 ifikapo mwaka 2025.

Mheshimiwa Spika, implication yake nini ni kwamba tunaweza tukaangalia bei ya mawasiliano kuanzia mwaka 2009 na mpaka sasa mwaka 2022 ili kuona nini Mkongo wa Taifa umesaidia. Mwaka 2009 Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote watakumbuka kupiga simu ilikuwa ni Shilingi 147 kutoka mtandao mmoja kwenda mtandao mwingine hiyo ni kwa wastani, lakini kulikuwa na makampuni mengine ambayo ilikuwa zaidi ya hapo. Vile vile kupiga simu kutoka mtandao mmoja wa Vodacom labda kwenda TiGO gharama ilikuwa inaongezeka.

Mheshimiwa Spika, leo hii kutokana na uwekezaji huu wa Serikali kilichofanyika ni mpaka sasa ukipiga simu bila kujiunga na kifurushi chochote kile utaweza kutumia Shilingi 30 peke yake bila kujali unapiga kutoka mtandao wa Vodacom kwenda TiGO, unapiga TiGO kwenda Halotel kwa wastani ni Shilingi 30. Hayo ni mapinduzi makubwa ambayo yametokana na Serikali kuwekeza katika ujenzi wa mkongo wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kwa upande wa Mangaka kwenda Mtambaswala ambapo Serikali imejenga takribani kilometa 72. Lengo kuu la ujenzi wa mkongo ule ni kuhakikisha kwamba tunaenda kutoa huduma katika nchi jirani ya Msumbiji ili tuhakikishe Serikali inajipatia mapato yanayotokana na fedha za kigeni ambapo tukiwa tunatoa huduma ya mkongo wa Taifa, ndiyo maana pale tumeweka POP pale Mtambaswala mpakani.

Mheshimiwa Spika, kuna mambo mengine ambayo yamejitokeza ambayo yamejadiliwa na Waheshimiwa Wabunge, ambayo sana sana ni upatikanaji wa mawasiliano katika maeneo yao. Hili ni takwa la Ilani ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 61 (J) ambapo inahitaji Serikali kuhakikisha kwamba inafikisha mawasiliano kwa wananchi wote vijijini.

Mheshimiwa Spika, kwa Serikali kwa kuona hilo kupitia Sheria Namba 11 ya Mwaka 2006 ambapo mfuko wa mawasiliano kwa wote ulianzishwa mahsusi ili kuondoa pengo lilokuwepo la mawasiliano kati ya Vijijini na Mijini.

Mheshimiwa Spika, Serikali sasa imeshaanza kuwekeza katika maeneo ambayo yameonekana na changamoto ninapenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba Serikali kupitia mradi wa Tanzania kidigitali, ifikapo mwezi wa Tano inaenda kutangaza zabuni ya maeneo 778 ambapo maeneo haya yote yataenda kufikishiwa huduma ya mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo haya ni pamoja na maeneo ambayo Mheshimiwa Shangai Mbunge wa Ngorongoro ambaye alihitaji kutajiwa maeneo ambayo kuna Kata ambazo hazijafikiwa na mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, nikuhakikishie uwekezaji ndani ya Wilaya ya Ngorongoro na Kata ambazo Mheshimiwa Mbunge anazihitaji tuko Tayari kumpatia ili ajiridhishe maeneo yake yanaenda kufikishiwa huduma ya mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa ya kuchangia hotuba ya Bajeti ya Waziri Mkuu. Kwa upekee kabisa niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa namna ambavyo wamegusia katika Sekta yetu ya Maji, nasimama hapa nikiwa naelewa kabisa kwamba Sekta ya Maji, inagusa nyenzo muhimu sana katika uhai wa binadamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia ni zaidi ya sita, lakini wote kwa umoja wao wameonyesha namna ambavyo wanataka kuharakisha miradi ya maji na kuboresha namna ambavyo Wakandarasi wetu wanafanya. Miradi ya maji inayoendelea nchini iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji, lakini vilevile ipo katika hatua ambazo zinaenda kuleta huduma ya maji kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba miradi hii itakamilika kabla ya muda, kwa sababu wiki iliyopita Serikali imetoa fedha bilioni 60 kwa ajili ya kuanza kulipa Wakandarasi ambao wanatekeleza miradi ya maji vijijini. Leo asubuhi nimejulishwa na Katibu Mkuu, Mfuko wetu wa Maji pia tumeweza kupata bilioni 18. Kwa hiyo, kwa ujumla tuna bilioni 78 kwa ajili ya kuhakikisha miradi yetu ya maji huko vijijini inaendelea kutekelezwa na ili iweze kukamilika kwa wakati. Hizi ni dalili tosha kabisa za kuonesha kwamba tunaye Rais, ambaye anajali Watanzania, tuna Rais ambaye amejikita katika utoaji wa huduma za msingi kabisa kwa Watanzania, hivyo tuendelee kumuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika yale ambayo yameongelewa na Waheshimiwa Wabunge, naomba nigusie jambo ambalo ameongea Mheshimiwa Issa, Mbunge wa Kibamba kuhusu bwawa la Kidunda. Napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Mheshimiwa Rais, ametoa fedha takribani bilioni 49 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba bwawa hili ambalo ndilo linaenda kutoa uhakika wa maji katika Mto Ruvu ambao ndiyo chanzo cha maji yanayopatikana katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo ya Mkoa wa Pwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, bwawa hili limefikia katika 20% ya utekelezaji wake na litakapokamilika litaweza kutoa lita bilioni 190 ambapo zitakuwa zina uwezo wa kuhudumia mikoa ya jirani pamoja na Dar es Salaam. Vilevile katika ujenzi wa bwawa hili, kuna ujenzi wa kituo cha kufua umeme ambapo takribani Megawatt 20 zitazalishwa pale. Pia kuna njia kuu ya msongo mkubwa wa umeme kutoka Kidunda mpaka Chalinze takribani kilometa 101. Maana yake ni kwamba tunaenda kuwa na uhakika wa huduma mbalimbali unaotokana na bwawa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kuongelea Bwawa la Farkwa. Mheshimiwa Kunti amejaribu kuligusia katika kuchangia kwake na ameonyesha hofu yake, lakini nimhakikishie kwamba Serikali iliingia makubaliano na Benki ya Maendeleo ya Afrika na takribani dola za Kimarekani 125 zilitolewa. Tunafahamu kabisa kwamba bwawa hili limekuwa na changamoto kidogo kwa sababu ya kubadilika kwa mahitaji ya maji na kubadilika kwa wingi wa watu katika Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumepata mtaalamu mshauri ili aweze kupitia ule usanifu wa bwawa na kuhakikisha kwamba anapitia mpango wa kulinda na kutunza mazingira ambayo ndiyo chanzo cha maji kitakachokuwa kinapeleka katika lile bwawa. Kwa hiyo, tunaamini kwamba akishapitia huu usanifu, maana tumempatia muda mpaka mwezi wa Tisa awe amekamilisha ili ujenzi wa bwawa hili uanze mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba Waheshimiwa Wabunge tunafahamu kwamba miradi ya maji ni miradi muhimu sana. Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imejikita kuhakikisha kwamba miradi hii inakamilika kama ambavyo imepangwa na hili bwawa pamoja na mabwawa mengine, kwa sababu mabwawa yapo mengi ambayo yanaendelea katika hatua mbalimbali. Tuna uhakika kwamba kwa sababu tunaenda kwenye bajeti ijayo, Waheshimiwa Wabunge watatuunga mkono ili tuweze kuhakikisha kwamba miradi hii tunaisimamia ili iweze kukamilika na iweze kutoa huduma ya maji kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba changamoto ya maji katika Jiji la Dodoma inaendelea kuwepo, lakini tuna miradi 15 inayoendelea katika Jiji la Dodoma. Vilevile tuna miradi 78 ambayo inaendelea katika Mkoa wa Dodoma ambapo miradi hiyo ina takribani shilingi bilioni 54 na watu takribani 400,900 wanaenda kunufaika na huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba changamoto ya Dodoma hatuwezi kuitatua kwa mpango wa muda mrefu peke yake. Serikali imejipanga katika mpango wa muda mfupi, muda wa kati na vilevile muda mrefu. Mpango wa muda wa kati kwa Jiji la Dodoma, tayari tuna miradi midogo midogo 15 ambayo inaendelea kujengwa katika maeneo ya Nzuguni, Nala na maeneo mengine ili kuhakikisha angalau wananchi wanaokuja katika Jiji la Dodoma na wananchi wanaoishi katika Jiji la Dodoma hawapati changamoto yoyote ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo tunaomba muwe na subira, pale ambapo kutakuwa na changamoto, tunaamini kwamba kila changamoto tutaichukua kwa uzito wake kwa sababu tunaamini kutatua changamoto na kuhakikisha huduma zinazidi kuimarishwa na kuboreshwa, ndiyo mafanikio ya Taifa letu na ndiyo mafanikio ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu, na Waheshimiwa Wabunge, niwahakikishie kwamba Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Sekta ya Maji ameendelea kufungua kapu lake na ameendelea kuonesha kwamba kumtua ndoo mama kichwani...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, muda wako umekwisha.

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo kipaumbele katika kuhakikisha kwamba...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, mengine yajibu kwa maandishi.

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.

NAIBU SPIKA: Yaliyobakia jibu kwa maandishi.

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia taarifa ya Kamati ya Miundombinu. Naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapinduzi ya sekta ya mawasiliano yanachangiwa kwa kiasi kikubwa sana na Kamati hii ya Miundombinu. Hivyo nawapongeza sana na tunaendelea kuwashukuru sana kama Serikali kwa kuendelea kutushauri na kutusimamia, na pale ambapo tutahitajika tutashirikiana vizuri ili kuhakikisha kwamba Serikali yetu inaendelea kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuongelea maeneo mawili. Eneo la kwanza ni safari ya Tanzania kuelekea kwenye uchumi wa kidijitali. Uchumi huu unahitaji miundombinu ya kidijitali, na miundombinu hii ni pamoja na ujenzi wa mikongo ukianzia mkongo wa baharini, mkongo wa Taifa, last mile connectivity ambayo inahusisha minara pamoja na fiber mlangoni kwako.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya nini? Upande wa Mkongo wa Baharini Serikali inaendelea kuvutia wawekezaji ili tuweze kuwa na mikongo mingi ili kuhakikisha kwamba tunashusha gharama ya matumizi ya internet. La pili, ni ujenzi wa Mkongo wa Taifa, Mheshimiwa Rais alipoingia madarakani alitoa kiasi cha shilingi bilioni 170 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mkongo wa mawasiliano unajengwa na kufika katika Wilaya nyingi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkongo wa Mawasiliano ni moja ya ecosystem katika miundombinu ya mawasiliano. Tunapoanza na mkongo wa baharini, tunakuja mkongo wa Taifa, tunapokuja kwenye last mile connectivity, sasa tunafika kwenye minara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kipindi cha kuanzia 2021 - 2023 imeweza kutoa fedha za ujenzi wa minara 1,070 yenye gharama ya takribani shilingi bilioni 170.978. Minara ambayo bado ipo katika hatua za utekelezaji ni minara 758 ambapo minara 320 inatokana na fedha za ndani na minara 438 inatokana na fedha za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba kuna maeneo ambayo bado yana changamoto na Mheshimiwa Rais anaendelea kutafuta fedha ambazo zitakuja kutatua changamoto katika baadhi ya maeneo. Tayari Mheshimiwa Rais ameshapata fedha kwa ajili ya kuongeza minara mingine 636, lakini katika minara hiyo kuna minara ambayo itaenda kujengwa katika maeneo yenye changamoto ya TBC, minara ambayo ni takribani 15.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maeneo ambayo minara tayari imeshajengwa na Waheshimiwa Wabunge wameonesha changamoto ya minara kuwaka asubuhi na mingine inawaka kwa masaa machache baadaye jioni inakuwa haipatikani.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshatoa maelekezo kuhakikisha kila mtoa huduma anapojenga minara ya mawasiliano cha kwanza ni lazima iwe na huduma ya internet. Jambo la pili, ni kuhakikisha kuwe na source ya power tatu; ya kwanza ikiwa solar, ya pili ikiwa betri na ya tatu ikiwa generator. Tunaamini kwamba kwa kufanya hivyo, hata kama solar itakosa nguvu, basi betri itaweza kusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuongea kidogo kuhusu suala la ujenzi wa Chuo cha ICT. Mheshimiwa Rais tayari ameshaelekeza na Mshauri Elekezi ameshafika kutoka South Korea na kazi ameshaanza tayari toka tarehe 29 Januari. Hivyo tutegemee kwamba ukamilishaji wa chuo hiki kitawasaidia Watanzania kuwajenga katika maarifa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile suala la kuwa na ICT hubs, tayari Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa kiasi cha dola milioni sita kwa ajili ya kujenga ICT hubs katika maeneo ya Dodoma, Dar es Salaam, Tanga, Mbeya, Lindi, Mwanza, Arusha pamoja na Zanzibar. Lengo ni nini? Lengo ni kuandaa vijana wetu wawe tayari kuingia katika soko la kidijitali ili Tanzania yetu ifikie uchumi wa kidijitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuongea kitu kidogo kuhusu suala la teknolojia zinazoibukia. Mheshimiwa Engineer Ulenga ameongelea kuhusu attacks katika critical infrastructure. Ni kweli kabisa, nchi za jirani hivi karibuni wawepambana na changamoto hii, lakini Serikali yetu tayari imeshaanda miongozo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Malizia.

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, tayari Serikali yetu imeshandaa miongozo mitano na tunapitia sera zetu ili kuhakikisha kwamba tunapambana na majanga haya yanayotokea. Mpaka sasa pamoja na kwamba nchi jirani zimeshapambana na haya majanga ya attack, Serikali yetu bado iko salama, mifumo yetu bado iko salama, lakini Serikali haitabweteka, itaendelea kuweka mkakati wa kuhakikisha kwamba mifumo yetu inaendelea kuwa salama zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)