Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Latifa Khamis Juwakali (3 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. LATIFA KHAMISI JUAKALI: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami naomba niungane na wenzangu kwa kuendelea kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kuwa hai, lakini pia kutujalia sote kuwa wazima.

Mheshimiwa Spika, kwa upekee sana naomba nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi ambacho kinaongozwa na jemedari wetu, jembe, mpambanaji, mtu mahiri sana, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa imani kubwa ambayo wamenionesha mimi kijana wao wa Chama Cha Mapinduzi kurejeshwa jina langu na kuja kuwawakilisha vijana wenzangu wa Chama Cha Mapinduzi, namshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kuwashukuru sana vijana wenzangu wote wa Tanzania nzima, tukianza na vijana wa Mkoa wangu wa Kusini Unguja na vijana wenzangu wote kwa imani ambayo wamenionesha, naomba niwaahidi kupitia kwenye Bunge lako hili tukufu kwamba sitawaangusha, nipo kwa niaba yao na nitafanya kazi kwa niaba yao. (Makofi)

Mwisho naomba niwashukuru wazazi wangu walezi kwa kunilea, kunitunza na kunifanya mpaka leo niko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dakika zenyewe ni chache, naomba na mimi niunge mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo iliwasilishwa hapa katika Bunge lililopita. Sote ni mashahidi, kazi ambayo imefanywa na Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kubwa na sote tunaijua na Watanzania wote waijua, mwenye macho tunasema haambiwi tazama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi binafsi nimetembea katika Tanzania nzima, nimeona miradi mbalimbali iliyofanywa chini ya usimamizi wa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, vituo vya afya, miradi ya maji, miundombinu, barabara, hakuna asiyejua kazi kubwa ambayo imefanyika chini ya usimamizi wa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nataka nichangie katika suala hili la elimu. Wachangiaji waliopita wamesema sana; elimu yetu ya Tanzania haimuandai kijana kuweza kujiajiri mwenyewe ama kuajirika. Naomba sana niishauri Wizara yetu ya Elimu sasa tuweze kubadilisha mitaala ambayo itaweza kumsaidia kijana wetu aweze kuajirika, lakini hiyo mitaala atakayoweza kumsaidia kijana huyu yeye anapomaliza elimu yake ikiwa elimu ya sekondari lakini hata katika elimu ya chuo kikuu aweze kuajirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia naomba sana Wizara yetu ya Elimu tuandae mitaala ambayo itakuwa inaendana na wakati. Sisi vijana tuna msemo wetu tunasema lazima tuwe up to dated. Kwa mfano sasa Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tupo katika uchumi wa kati, kwa hiyo je, sisi Wizara tunajipangaje kuendana na kasi ya uchumi huu wa kati. Kwa hiyo, lazima tuandae mitaala ambayo inaendana na uchumi.

Mheshimiwa Spika, nataka nishauri katika suala hili la mikopo, wenzetu wengi waliopita wamechangia kuwa lengo la mkopo ni kuwasaidia vijana wetu na kama lengo la mkopo ni kuwasaidia vijana wetu sasa ni vyema Bodi yetu ya Mikopo ikapunguza hii asilimia 15. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sote tunafahamu asilimia kubwa ya wanaopata mikopo ni vijana maskini wenzetu. Kwa hiyo, kama ni vijana maskini, leo kijana huyu amekopa mkopo let’s say milioni 10 ama milioni 15, lakini kijana huyu pengine anakaa miaka mitatu hajaajiriwa, baada ya kuajiriwa pengine mshahara wake ni mdogo, pengine analipwa shilingi 300,000, hiyo hiyo shilingi 300,000 Bodi ya Mikopo kuna asilimia 15 ambayo inaihitaji. Je, pengine analipwa shilingi 300,000 maana yake ukiwa unalipwa shilingi 300,000 Bodi ya Mikopo wanakata shilingi 45,000 kwa hiyo shilingi 300,000 toa shilingi 45,000 kuna kiasi kidogo ambacho kinabakia, bado hapa hujakatwa tax na vitu vingine; je hapa bado tutakuwa tumeendelea kuwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. LATIFA KHAMISI JUAKALI: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, (Muungano na Mazingira). Nami niungane na wenzangu kwa kuendelea kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya.

Mheshimiwa Spika, pia naomba nichukuwe nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kusema kwamba ataendelea kuulinda na kuutetea Muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nami nataka niseme nasi vijana tuko nyuma yako mama, tutaendelea kuulinda, kuutetea kuupigania Muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kusema Muungano wetu huu ni tunu na tunasema tunu hulindwa, tunu hutetewa, tunu hupiganiwa; kwa hiyo, nasi kama Watanzania maana yake ni kwamba wajibu wetu ni kuendelea kuulinda kutetea na kupigania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba ninukuu maneno ya Rais wetu kipenzi chetu Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alivyokuja kuliutubia Bunge letu hili la Kumi na Mbili. Alisema; “Muungano wa Tanzania ni Muungano wa hiari na umetokana na mambo makuu manne.” Jambo la kwanza alisema, maono ya waasisi wa Taifa letu, ambaye ni Hayati Abeid Amani Karume pamoja na Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere; jambo la pili, alisema Muungano huu ulisababishwa na utengamano na ukaribu wa kijiografia kwa Tanzania Bara yaani Tanganyika na Tanzania Zanzibar na kwa sasa tunaita Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sipendi sana kuita Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar, napenda nitumie Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

SPIKA: Kazi iendelee. (Kicheko)

MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Spika, jambo la tatu alisema kwamba uhusiano wa kidugu na urafiki baina na wananchi wa Zanzibar na Tanganyika. Sote tunaona, anayeishi Tanzania Bara na anayeishi Tanzania Zanzibar, karibu sote ni ndugu. Kama huna udugu wa kidamu, basi hata udugu wa kuoana.

Waheshimiwa Wabunge, waliotangulia humu, wengi wamejinasibu, wamesema, wapo ambao wanatoka Zanzibar, lakini wana wake Ukerewe, wameoa wengine Kigoma na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la nne lilikuwa ni uhusiano wa kirafiki na ukaribu uliokuwepo...

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, anayeongea sasa hivi, Mheshimiwa Latifa Juwakali ni Mbunge wa Viti Maalum, ambaye ameshawahi kukimbiza Mwenge wa Uhuru. Kwa hiyo, anajua vizuri majimbo yenu yote na hata kule Kongwa alifika. (Makofi)

Endelea kuchangia Mheshimiwa Latifa. Anaelewa maana ya Muungano ni nini?

MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Jambo la nne ni uhusiano wa kirafiki na ukaribu uliopo kati ya vyama vya TANU kwa upande wa Tanganyika na ACP kwa upande wa Zanzibar. Kwa mantiki hiyo, inaonyesha ni jinsi gani huu Muungano ulikuwa ni Muungano wa hiari na Muungano ambao umeweza kuwaunganisha baina ya pande mbili; Zanzibar na Tanzania Bara.

Mheshimiwa Spika, nimeanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jana tulikuwa tuna kongamano pale na kongamano hili lilikuwa ni kuadhimisha miaka 57 ya Muungano, lakini yeye mwenyewe alikuwa ni shahidi, siyo matarajio kwamba wazee ndiyo watatangulia sisi vijana tutabakia, lakini hata hilo linawezekana, wazee wanaweza wakatangulia, vijana tukabakia au vijana tukatangulia na wazee wakabakia.

Mheshimiwa Spika, kuna kitu ambacho kinanisikitisha sana; leo nchi hii vijana wako wengi sana, lakini kama utakwenda katika vijana kumi uwasimamishe vijana watano wakuelezee historia au wakuambie wanaufahamu vipi Muungano, it is so bad, hawawezi kukuelezea historia ya Muungano. Kwa mantiki hii sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Spika, naomba uniongezee dakika moja.

SPIKA: Endelea.

MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Spika, kwa mantiki hii, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, mbali ya kazi nyingi ambazo anaendelea kuzifanya, waandae mpango maalum wa kuweza kuwasaidia vijana wetu ili waweze kuufahamu Muungano vizuri. Waswahili wanasema unachokijua ndicho unachoweza kukifafanua na ndiyo maana minong’ono mingi inakuwa huku, muda mwingine watu wanafuata mkumbo, vijana wanafuata mkumbo, maana yake kuna kero za Muungano, kuna faida za Muungano, hawaelewi. Kero zilikuwepo lakini nyingine zilishachanganuliwa.

Mheshimiwa Spika, hawa watu au vijana kama watakuwa wana uelewa wa kutosha itawasaidia wao sasa kusimama na kuweza kujenga hoja; kweli tuna Muungano, lakini kero zilikuwa hizi na faida ziko hizi. Naomba sana Mheshimiwa Waziri kama vijana wanasimamishwa kule shuleni, tunafanya debates za mada nyingine, hata na hii iwe miongoni mwa ajenda ya kuipeleka katika shule ili iweze kuwasaidia vijana wetu waweze kujua Muungano ni nini na kuweza kuusimamia na kuulinda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Kwanza kabisa, naomba nichukue nafasi hii kuendelea kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kuwa wazima. Kipekee sana, naomba niendelee kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake makubwa na namna alivyojipambanua katika Wizara ya Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema vijana wa Tanzania tunamwelewa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, tunamaanisha, na tunaposema zaidi tunamwelewa katika Wizara ya Elimu, tunamwelewa sana; na tunaposema Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amejipambanua kwenye elimu, tunamaanisha kwamba ameyatafsiri maono yake kwa vitendo, huku akiamini kwamba, ili kuwawezesha vijana wa Tanzania, lazima tuwe tuna human capital na physical capital. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote ni mashahidi, Wabunge wa Majimbo hapa wamejinasibu sana, wamesema, katika maeneo mbalimbali ya majimbo shule nyingi zimejengwa, lakini siyo shule tu, hivi karibuni tumeiona Wizara ya Elimu imeendelea kufanya maboresho mapya ya mtaala wa elimu. Hiyo inaonesha jinsi gani Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sasa anataka Wizara ya Elimu iendelee kuonesha umahiri na ubora wa human capital. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema human capital, majengo yanajengwa, miradi ya elimu inatekelezwa, lakini hatuwezi kuiboresha elimu kama hatuna uwezo wa kuendeleza skills and knowledge kwa wanafunzi wetu wa kitanzania. Kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunawashukuru wenzetu wa Wizara ya Elimu, kwa sababu kwanza wameendelea kuwa wasikivu na pia tunawapongeza sana, wameendelea kutoa ushirikiano mzuri kwetu sisi Wabunge huku wakiamini kwamba sisi kwa pamoja lengo letu ni kuwasaidia vijana wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, pia nataka niseme kwa dhati ya moyo wangu, vijana wa Tanzania wamenituma niseme kwamba wanampongeza na kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Bodi ya Mikopo kwa kutuongezea kiasi kikubwa cha kujikimu kwa Bodi ya Mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais amejipambanua na kuona kwamba sasa elimu yetu sasa ni sayansi na teknolojia. Hivi karibuni tumewaona wenzetu wa Wizara ya Elimu wameenda kutoa vishikwambi nchi nzima, na vishikwambi hivyo vimetolewa Tanzania Bara na Tanzania Visiwani. Tunamshukuru sana na tunampongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja zangu leo zitajikita katika maeneo matatu. Jambo la kwanza nalotaka kulizungumza, Mheshimiwa Waziri sasa hivi tupo katika formulation ya mitaala. Katika mitaala hii, yako mambo mengi yamezungumzwa, lakini nilitamani sana, na ninajua kwamba katika mitaala hiyo kuna vitu vingi ambavyo vinaenda kuonekana kwamba ni maboresho na vitakuwa vipya. Naomba niwazungumzie walimu. Walimu wanatakiwa nao wapate skills na knowledge mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Wizara ya Elimu hapa walituambia, na katika majibu ya msingi walikuwa wanajibu wakisema kwamba, wamepata kibali cha kuajiri walimu wapya. Nilikuwa naomba sana tuwazingatie na hata wale walimu walio katika site, tuwatengee fedha na bajeti ya kutosha ili nao wakapate mafunzo ya ziada waweze kuendana na mahitaji ya walimu ambao tunawataka katika maboresho ya mitaala yetu ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, pia kuna jambo, hili sikuliona sana kwenye Wizara ya Elimu tu, hata katika Wizara nyingine na sekta nyingine. Tunaposema promotion, tunamaanisha kwamba, kuwa- motivate wale ambao wanatoka stage moja kwenda stage nyingine. Kumekuwa na changamoto moja, wenzetu walimu wanapoomba vibali kutoka kwenye Wizara ya Elimu na Wizara nyingine tofauti, pengine mwalimu amemaliza shahada ya kwanza, ameomba kibali anakwenda kufanya shahada yake ya pili, lakini anaporudi kwenye kituo chake cha kazi kumekuwa kuna changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto inayojitokeza, hakuna aina yoyote ya promotion ambayo anaipata. Jambo hili limekuwa ni changamoto na linaweza kuwafanya wanafunzi wetu wengine wasizidi kwenda kujiongeza kwa sababu wanajua, anaporudi kwenye kituo chake cha kazi hakuna chochote kinachoenda kumwongezea yeye, na hakuna tofauti baina yake na yule aliyemwacha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Waziri wa Elimu na Wizara yetu ya Elimu tulichukue hili tulibebe na liwe kama ni promotion kwa wanafunzi wetu au wafanyakazi wetu ambao wanatoka katika maeneo ya kazi wanapoenda kusoma na wakirudi ili waweze kuwa kama wana motivation fulani kwa sababu wanajua, mimi nimemaliza Degree, nikienda kusoma Masters nikirudi, kuna kitu kidogo kinaweza kikawa kimeongezeka na hiyo inaweza ikawasaidia wengine ili kuweza kupata promotions. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikiliza vizuri sana hapa bajeti ambayo ilikuwa inasomwa. Nilitarajia sana, kwa sababu mmoja wa Mbunge ambaye alikuwa anauliza maswali mengi kuhusiana na vyuo vya kati, nilikuwa ni mimi. Nilitarajia sana leo au jana ikisomwa bajeti hapa, tuone walau kuna kiasi cha fedha ambacho kimetengwa kwa ajili ya vijana wa vyuo vya kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza vyuo vya kati, hivi ndiyo vyuo ambavyo vinarejesha kwa haraka mikopo. Simaanishi kwamba vyuo vya juu wakipewa mikopo hawarejeshi kwa haraka, Hapana, lakini kwenye vyuo vya kati return yake inakuwa ni ya haraka, kwa sababu mwanafunzi anachoenda kukisoma ndicho kile anachoenda kukifanyia kazi katika eneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye vyuo vya kati, huku ndiko tunapowapata vijana wanaojifundisha driving, ndiyo tunawapata vijana ambao wanajifundisha masuala mbalimbali, umeme na vitu vingine. Akitoka pale, mwanafunzi yule tunamtarajia aidha kwa kujiajiri mwenyewe au hata kwa kwenda kuajiriwa. Hata kama hakuweza kuajiriwa, atakuwa ana uwezo wa kujiajiri mwenyewe. Akiwa na uwezo wa kujiajiri mwenyewe, maana yake returns ya ule mkopo itakuwa ni ya haraka zaidi kuliko na wale wengine ambao wanasoma kwa ajili ya kuja kurudisha ile return baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, kama Wizara, hili tulichukue kwa uzito wake, na Wabunge bahati nzuri wamelipigia kelele sana humu ndani wakiomba kwamba hili jambo tulibebe na tuweze kuwasaidia wenzetu ili waweze kupata mikopo katika hivi vyuo vya kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nataka nimalizie katika maslahi ya walimu. Maslahi ya Walimu bado hayaridhishi. Tunaomba sana Mheshimiwa Waziri hili mlichukue, na muwe na wivu na watendaji wenu wa Wizara ya Elimu. Hivi leo ikitangazwa kazi ya TRA na kazi ya Ualimu vijana wengi watafukuzia kazi ya TRA. Kwa nini wafukuzie kazi ya TRA wasifukuzie katika Wizara ya Elimu? Maana yake inaonesha bado masilahi ya walimu yapo duni, na yapo chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi walimu tunasema, kazi hii ya ualimu, malipo yake yapo kwa Mungu. Basi tunaomba walau kidogo wale walimu nao wapate moyo wa kuendelea kufundisha vizuri. Muda mwingine hapa unaweza ukasema mwalimu anafundisha shule mbili; leo yupo private, kesho yupo katika shule ya Serikali, ni kwa sababu bado masilahi yao ni madogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nawashukuru sana. (Makofi)