Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ghati Zephania Chomete (6 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyeweza kunipa uhai leo nimesimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Kipekee zaidi naomba niwashukuru wanawake wa Mkoa wa Mara walioweza kunichagua mimi kuwa mwakilishi wao katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuweza kuniteua mimi kuwa Mbunge. Pia nakushuru wewe kwa kunipa nafasi leo nimesimama kwa mara ya kwanza katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naomba nimpongeze Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2015 – 2020. Mheshimiwa Rais wetu mpendwa amefanya kazi kubwa sana katika nchi yetu. Kikubwa zaidi Mheshimiwa Rais wetu katika Mkoa wangu wa Mara amejikita kufanya mambo mengi makubwa sana ambayo yamesababisha nchi yetu imepiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite katika suala la afya. Mheshimiwa Rais wetu wetu mpendwa katika Mkoa wangu wa Mara amefanya mambo makubwa katika Sekta ya Afya hasa upande wa hospitali, amejenga zahanati takriban 45 mpya, lakini pia vituo vya afya 13 vipya, amejenga hospitali za wilaya saba mpya. Kipekee kabisa Rais wetu ameweza kutupatia takriban zaidi ya bilioni 15 kuhakikisha tunajenga hospitali ya rufaa maarufu kwa jina la Kwangwa iliyokuwa imekaa zaidi ya miaka 40 sasa inafanya kazi katika kitengo cha mama na mtoto. Mheshimiwa Magufuli apewe sifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi naomba niende kuchangia katika hotuba aliyoitoa ya ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili. Mheshimiwa Rais wetu aliongea hotuba ambayo ilisababisha sisi kutupa dira, maono na mikakati mikubwa ya mstakabali wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba Mheshimiwa Rais wetu kwa hotuba hii ambayo Rais aliitoa imegusa kila eneo la Taifa hili ambayo naomba nielekee katika kundi la wanawake, lipewe fursa kubwa kwenye taasisi za kifedha kama mabenki. Nina Imani ili akinamama hao ambao wamekuwa ni sehemu kubwa mama zetu hawa ambao wamekuwa ni sehemu kubwa katika kulijenga Taifa letu waweze kupata fursa kubwa katika kupunguziwa masharti ya kupewa mikopo ya nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa uhakika nilionao niwaombe masuala ya kuhakikisha wanawake wanapata fursa ya kukopeshwa, naamini watakaoweza kukopeshwa wataweza kuonekana katika ujenzi wa Taifa hasa katika suala la Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua mama zangu wana changamoto kubwa hasa katika masuala ya kiafya. Nijikite kwenye kusema kwamba masuala ya tatizo la kiafya hasa ugonjwa wa akinamama wa kansa ya matiti na ya kizazi, hawa akinamama wanapata tabu sana hapo bada ya kuwa wanakosa huduma pale ambapo Madaktari wanakuwa hawapo pale. Sasa naomba niishauri Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sekta ya kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa letu basi Serikali ilipe kipaumbele suala hili la bajeti ili kukidhi mahitaji ya Maafisa Ugani, mbegu, mbolea bora na pembejeo kwa ajili ya kuchochea hali ya wakulima na hivyo kuchochea uzalishaji bora wa mazao ya chakula na biashara.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali izamilie kuwasaidia wakulima wetu kuuza mazao kwa bei yenye tija na kupata masoko ya uhakika hasa kwa mazao ya kahawa, pamba na kadhalika ili kuwezesha mkulima kunufaika ipasavyo na kilimo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na ukosefu wa mbolea umewafanya wakulima wetu hasa waliopo karibu na mipaka mfano Wilaya ya Tarime wakulima wamekuwa wakinunua mbolea Kenya ili kukidhi mahitaji ya kilimo hii pia ni kwa kuwa mbolea yetu haiwafikii kwa wakati lakini pia ikiwepo huuzwa kwa bei ya juu zaidi.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali ifanye haraka upatikanaji wa mbolea katika mipaka hiyo ili pia kuzuia magendo ya mbolea, kwa sababu wakulima wanafuatwa mpaka mashambani na TRA kuwakamatia mbolea hizo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Wizara kwa juhudi kubwa iliyoanza nayo tangu imeanzishwa.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia kwa kuigawa Wizara hii ili kuwafikia wananchi kwa urahisi.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuishauri Serikali katika kundi hili la mabinti walemavu na mabinti walemavu wanaofichwa na wazazi wao kwa kudhania kuwa ulemavu ule hawezi kupata elimu wala kufanya kazi yoyote.

Mheshimiwa Spika, niombe tutoe elimu kwa jamii ili itambue kuwa watoto hao wanaweza kusoma na kuisaidia jamii yao. Lakini pia wanawake walemavu watambuliwe kwa idadi yao kupitia Kata, Wilaya mpaka Mkoa ili wawezeshwe kwa kupatiwa miradi rafiki kwao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ndoa za utotoni, kumekuwa na ndoa za utotoni sana katika jamii yetu, naishauri Serikali itenge fedha kwa ajili ya kutoa elimu inayohusu madhara ya ndoa za utotoni na kushirikiana na mashirika yanayotoa elimu na yanayopinga ndoa za utotoni kwa mfano kule Mkoani Mara Shirika kama Masanga, Hope for Girls yamekuwa ni mashirika yanayotoa elimu inayohusu madhara ya ndoa za utotoni ili Taifa letu liwe na vijana wenye elimu na afya njema.

Mwisho naishauri Serikali kuviboresha Vyuo vya Maendeleo ya Jamii kama vile Chuo cha Buhare kilichopo mkoani Mara na vingine vingi nchini ili viendelee kufanya vizuri zaidi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Maji. Kwanza kabisa nampongeza Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hotuba nzuri aliyoitoa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia ninampongeza kwa juhudi anazoendelea kuzifanya katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali kwa kuhakikisha inaboresha miradi ya maji nchi. Nampongeza sana Waziri wa Maji, Mheshimiwa Jumaa Aweso, nampongeza Naibu Waziri wa Maji Maryprisca kwa kazi nzuri wanazozifanya pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo na wafanyakazi wote wa Wizara hiyo. Wamefanya kazi nzuri katika Manispaa ya Musoma kwani hivi sasa wananchi wanapata maji mazuri ya bomba kwa kiwango cha kuridhisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi hizo, Mkoa wa Mara ambao una wilaya nyingi sasa maji ni pungufu sana.

Naomba mradi wa kutoka Ziwa Victoria, ule ambao unaanzia Wilaya ya Rorya uhakikishe Wilaya ile ya Rorya pamoja na vijiji vyake vinapata maji. Hivyo hivyo, Wilaya ya Tarime pamoja na Vijiji vya Nyamwaga mpaka Nyamongo wahakikishe vinapata maji. Niombe Serikali ihakikishe mradi huo wa kutoka Ziwa Victoria unawasaidia wananchi wa Wilaya ya Tarime kwa sababu mpaka sasa wanateseka sana hawana maji. (Makofi)

Mheshimiiwa Spika, vilevile Musoma Vijijini, Butiama pamoja na vijiji vyote vinavyozunguka zile wilaya havina maji. Bunda kuna miradi ya maji mpaka sasa miradi ile inasuasua, niombe Serikali kupitia Wizara hii ya Maji iangalie miradi yote iliyoko Bunda inatekelezeka. Mfano Mwibara kuna mradi wa maji ulipelekewa shilingi milioni 510 wa kutoka Namuhura kuelekea Kwibara lakini unasuasua. Kuna mradi wa kutoka Buramba, Kibara mpaka Kisorya mpaka sasa miradi ile inasuasau. Niombe Serikali yangu sikivu kupitia Wizara hii ya Maji ihakikishe miradi ile inatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya Serengeti kuna mradi wa chujio la maji katika bwawa Manchira. Mradi ule ukitekelezeka unasaidia sana Mji wa Mugumu pamoja na vijiji vile vinavyozunguka pale ili wananchi wa maeneo yale waweze kuondokana na kero hii ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna sera ya kusema kwamba tunamtua mama ndoo kichwani, niwaombe sana Wizara ya Maji wahakikishe wanatua ndoo kichwani wale wanawake wa Mkoa wa Mara maana wanateseka sana. Akina mama wa Mkoa wa Mara ni wachapa kazi, wanaamka asubuhi kwenda kutafuta maji. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu sikivu iuangalie kwa jicho la pili Mkoa wa Mara ili kusudi tuweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Rorya, Kata ya Komuge kuna mradi wa maji. Mradi ule ulishatengewa shilingi bilioni 1.3 lakini sasa toka umetengewa fedha hiyo ni miaka mitano sasa umepelekewa shilingi milioni 300 tu. Niombe Serikali ihakikishe mradi ule unatekelezeka. Nasisitiza Serikali ihakikishe inapeleka pesa hizi kwa wakati lakini ihakikishe pia inatekeleza miradi yote iliyowekwa katika Mkoa wa Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja, ahsanteni sana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete. Nilikuwa sijamfahamu, sasa sijui ni katika Waanchari au Wanyichoka au Mkurya au Mjaluo au Mngorebe au Msweta au… Kuna makabila bwana. (Kicheko)

MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, mimi ni Mtimbaru. Mkurya Mtimbaru.

SPIKA: Naam.

MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mimi ni Mkurya Mtimbaru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana katika maisha yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika nchi yetu. Pia nampongeza Waziri wa Afya, dada yangu Ummy Mwalimu, Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Godwin Mollel na wafanyakazi wote wa wizara hii kwa jinsi wanavyoendelea kupambana kumsaidia Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza sana Mama Samia Suluhu Hassan kwa juhudi kubwa alizozifanya katika Mkoa wetu wa Mara. Mheshimiwa Rais alikuja mwaka 2022 katika Mkoa wa Mara, tulimwomba CT-Scan, akaahidi atatekeleza. Sasa ametekeleza, ametuletea CT-Scan Machine. Tunamshukuru sana, sana, sana kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Mara na Watanzania wote wanaoishi Mara. Kwa sababu ile mashine ni muda mrefu haikuwa kuwa katika mkoa wetu na wananchi wa Mkoa wa Mara walikuwa wanatoka Mara kwa gharama kubwa kwenda kutafuta huduma hiyo katika Mkoa wa Mwanza katika Hospitali ya Bugando. Hivyo tunamshukuru sana sana Mheshimiwa Rais kwa juhudi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyoko tu pale, kuna miundombinu ambayo haijamalizika, tunamwomba Mheshimiwa Waziri, ile miundombinu imalizike ili kusudi ile mashine iweze kufungwa na wananchi wale waweze kupata huduma hiyo inavyostahili.

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza Rais wetu kwa jinsi alivyoendelea kutujengea vituo vya afya, hospitali, zahanati na hospitali za mkoa. Mkoa wetu wa Mara, vituo vya kutolea huduma ambavyo vimejengwa, tuna vituo 335. Hivyo ni kwa ujumla wa hospitali na vituo vya afya na zahanati. Katika vituo 335 tuna vituo 35 tu ambavyo ndiyo vinakidhi mahitaji ya Wana-Mara ambavyo vinalaza wagonjwa, vinatoa huduma ya damu na upasuaji.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia uwiano, ni mdogo sana. Huo uwiano kwa Mkoa wa Mara, kwa mwaka mzima wanajifungua akina mama 93,339. Unapojifungua, lazima upate huduma inayostahiki. Vile vituo ambavyo vimejengwa, havina sifa, kwa maana ya kwamba havina vifaa tiba, havina madaktari na havina madawa.

Mheshimiwa Spika, nitatolea mfano, Kituo cha Afya cha Mliba, ambacho kilijengwa mwaka 1985, lakini kinahudumia kata saba; Kata ya Nyanungu, Kata ya Golong’a, Kata ya Kwihancha, Kata ya Nyarukoba, na kata nyingine. Siyo kwamba zile kata ziko karibu, umbali ni mrefu. Mgonjwa anatembea kutoka kilometa 50 kuja tu pale kwenye kituo, na kurudi pia ni kilometa 50.

Mheshimiwa Spika, kwa uwiano, ukilinganisha ni kilometa kama 100 mgonjwa anatembea, lakini anapofika pale kwenye kituo anakosa huduma stahiki. Kituo hakina x-ray, hakina ultra-sound, hakina maji, hakina Daktari hata wa Kituo pale hayupo. Mheshimiwa Ummy mimi naamini kazi yako ni nzuri sana, hebu tembelea Mkoa wa Mara ujionee adha wanayoipata pale akina mama wale wa Mkoa wa Mara. Ni mbali sana. Siyo hicho tu, ukienda Wilaya ya Bunda, Kituo cha Bunda Mjini pale hakina uzio, hakina generator, hakina ultra-sound, wala x-ray haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alisimama hapa Mbunge wa Mwibara, akasema kuna fedha zimeletwa shilingi milioni 300 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Kasuguti kule Mwibara, lakini zile shilingi milioni 300 hazijafanya ile kazi iliyopelekewa kujenga jengo la mama na mtoto. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri aje kutueleza kwamba zile shilingi milioni 300 mama alizozitoa zijenge jengo la mama na mtoto, lakini hazikufanya hivyo, sasa sijui atatuletea nyingine au atafuatilia zile ili tujue hasa nini hatma ya wale akina mama wa Mwibara? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamwomba sana, sana, sana Mheshimiwa Waziri atuletee madaktari, hasa madaktari bingwa, hatuna. Pia tunaomba sana tuletewe vifaa tiba katika vituo vyetu vya afya na hospitali. Tunakuomba pia tuletewe magari kule kwenye Mkoa wetu wa Mara. Wana- Mara wanampenda sana mama, wanapenda sana nchi yao, kwa hiyo, tunaomba huduma zile ambazo zinaweza kupatikana kwa wengine zipatikane pia na Mkoa wa Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee jambo lingine ambalo ninaliona kama ni gumu sana. Kwenye wizara hii kuna Sera ya Afya inayosema, matibabu bure kwa watoto chini ya miaka mitano, wazee na wamama wajawazito. Hili jambo halifanyiki hivyo. Mama zetu, watoto wetu na baba zetu wale wazee ambao ni kuanzia miaka 65 na kuendelea wanapoenda kwenye vituo vile vya afya au hospitali hawapewi matibabu bure wanalipa. Sasa naomba hii sera tujue inatekelezwa vipi?

Mheshimiwa Spika, naomba kuishia hapo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika sekta hii ya miundombinu. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na nimesimama katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya katika nchi yetu katika kuwaletea maendeleo Watanzania wote. Kipekee pia niwapongeze sana Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na wewe kwa jinsi mnavyoendesha Bunge letu Tukufu na kuhakikisha Bunge letu linaendelea kuimarika na kuendelea kuwa kidedea; hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niende kuchangia kuhusu Mamlaka ya Viwanja vya Ndege. Nimpongeze sana Waziri mwenye dhamana Mheshimiwa Prof. Makame Mbarawa na Naibu wake Mheshimiwa David Kihenzile na wafanyakazi wa Shirika hilo la Mamlaka ya Viwanja vya Ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba Mamlaka ya Viwanja vya Ndege inamiliki au inahudumu viwanja vya ndege takribani 53. Katika viwanja hivyo 53 vipo viwanja vitano au havifiki vitano ambavyo ndivyo vinavyosimamia au vinavyohudumu vinavyovisaidia vile viwanja vingine ambavyo vinapelekea vile viwanja vya ndege au Mamlaka uchumi wake au jinsi ya uendeshaji unaendela kushuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wamesema changamoto nyingi zilizopo Mamlaka ya Viwanja vya Ndege. Mimi nimeona pia nigusie changamoto moja. Tunatambua kwamba Serikali imeipa Mamlaka hiyo ya Viwanja vya Ndege kukusanya lakini pia na kupeleka gawio Serikalini. Makusanyo yale ya asilimia 70 ambayo Mamlaka ya Viwanja vya Ndege inakusanya, wao kama Mamlaka baada ya kukusanya na kupeleka Serikalini, wao wanarudishiwa asilimia 15. Hii asilimia 15 wanayorudishiwa ni ndogo sana; na baadaye pia wanaweza wasirudishiwe hiyo asilimia 15. Hii inapelekea utendaji wao wa kazi kushuka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ombi langu kwa Serikali, ninaomba Serikali iliangalie hili Mamlaka iweze kuongezewa kutoka asilimia 15 basi ifike hata asilimia 40 ili kusudi Mamlaka iweze kujiendesha vizuri. Sambamba na hilo basi nashauri asilimia hiyo iliyopangwa na Serikali irudi kwenye Mamlaka kwa wakati ili Mamlaka iweze kujiendesha vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba Mheshimiwa Rais amelifungua anga, amewekeza fedha nyingi kwenye anga. Tunapoacha kuboresha viwanja vyetu sisi wenyewe kama Watanzania tunajishushia uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo naomba nichangie upande wa TANROADS; kwanza naomba nimpongeze sana Waziri pia mwenye dhamana Mheshimiwa Innocent Bashungwa na Naibu wake Mheshimiwa Engineer Godfrey Kasekenya; hawa Wamekuwa ni viongozi wazuri wanaomsaidia sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kule kwetu, nitolee mfano kule Mkoa wa Mara; tumepata miradi mingi ya barabara za lami; nampongeza sana sana Meneja wetu wa TANROADS Mkoa wa Mara, amekuwa ni Meneja mzuri anayesimamia miradi ya TANROADS vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua miradi ya barabara iliyoletwa; ulikuwepo Mradi wa Nata mpaka Sanzati kilometa 40; ule mradi ni wa muda mrefu, lakini Mheshimiwa Rais ametuletea fedha na ule mradi unaendelea mpaka sasa; tunamshukuru sana. Changamoto iliyopo pale ni ucheleweshaji wa fedha kwa mkandarasi. Naiomba Serikali ihakikishe inapeleka fedha zile kwa mkandarasi ili kusudi ule mradi uweze kumalizika kwa sababu ni wa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumepata mradi mwingine wa barabara mradi unaounganisha wilaya kwa wilaya lakini mpaka mkoa kwa mkoa; Mradi wa Tarime – Nyamongo mpaka Mugumu Serengeti kilometa 87. Mradi ule unaendelea mpaka sasa na fedha zimekwenda. Isipokuwa, mradi ulitakiwa kumalizika mwaka jana lakini mpaka sasa mradi haujamalizika. Changamoto iliyopo ni kusuasua kulipwa mkandarasi. Naiomba Serikali yangu iliangalie hili. Tunapochelewa kumlipa mkandarasi tunaenda kuongeza madeni zaidi na kuisababishia Serikali hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anaelewa changamoto za wananchi wa Mkoa wa Mara, ameendelea kutupa Barabara. Tunatambua kwamba katika Bajeti ya 2023/2024 ametupa barabara ya Musoma - Busekera kilomita 92 lakini mpaka sasa ule mradi au ile barabara hakuna kinachoendelea mkandarasi hayupo. Kwa hiyo, naiomba TANROADS kupitia Serikali yangu iangalie ni namna gani mradi ule utaenda kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hajaishia hapo ametupa mradi wa Mika, Utegi mpaka Kirongwe kilomita 56, mpaka sasa wananchi wa Wilaya ya Rorya au Jimbo la Rorya wanatamani mradi ule uende kuanza ni kwa namna gani unaanza, wakitambua kwamba mradi ule umewekwa katika bajeti ya 2023/2024. Wananchi wanatamani kula matunda ya Serikali ya Awamu ya Sita, ninaiomba sana Serikali yangu iangalie ni kwa namna gani inaweza ikakamilisha au ikaanza pia na miradi hii ili kusudi sisi sote tuende kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie suala zima la upande wa Shirika la Ndege. Tunatambua kwamba shirika la ndege Mheshimiwa Rais Dkt. Samia amewekeza vizuri katika shirika hili la ndege na ameendelea kununua ndege nyingi katika nchi yetu, tulipokuwa siko tunakoenda, hii imeonesha ni jinsi gani Mama anaendelea kuchapa kazi. Kuna Mikoa ambayo inatamani kuiona ndege Air Tanzania, ndege yetu ya Serikali lakini mpaka sasa Mikoa hiyo ndege haijawahi kufika na wananchi wanasikia kila wakati kwamba Mama amenunua ndege. Wazo langu au ushauri wangu ni nini? Kamati ilitembelea Mkoa wa Mtwara ilikuta Serikali imewekeza pesa nyingi sana pale kwenye uwanja ule lakini ndege ya Air Tanzania haifiki pale, tatizo ni nini? Naiomba Serikali yangu iangalie kwa jicho la pili Mikoa ambayo Air Tanzania inaweza kufika ili kusudi wananchi wote tufaidike na hii keki ya Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)