Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mrisho Mashaka Gambo (18 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi pia nitumie fursa hii kukushukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuweza kuchangia Ofisi ya Rais, Utumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza kwenda kwenye hoja zangu moja kwa moja nakumbuka siku moja hapa Mheshimiwa Spika aliongea kauli ambayo ilinigusa sana, kuna jambo lilitokea Wabunge tukapiga makofi, akasema wakati mwingine Wabunge tunapiga makofi hata hatujui tunapiga makofi kwa jambo gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo jambo linanikumbusha wakati wa kampeni nilivyokuwa Arusha Mjini, nilikwenda kufanya ziara kwenye viwanda viwili, Kiwanda cha A to Z na Kiwanda cha Sunflag. Wafanyakazi wale waliniuliza maswali ambayo kila siku nayakumbuka; kwanza walitaka niwahakikishie kwamba nitakapokwenda Bungeni sitakuwa Mbunge wa makofi na ndio hata kwa mambo ambayo yanaumiza wananchi, la pili wakaniambia je, naweza kutoa hoja zenye maslahi ya wananchi au nitakwenda kuunga kila kitu mkono hata kama kinaumiza wananchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakanikumbusha kwamba wanasema wana hasira sana na hoja ya kikokotoo. Kwa hiyo, na yenyewe pia walisema niiweke kwenye maanani, lakini pia wakataka niweke kichwani kwangu changamoto iliyopo ya kima cha chini cha mshahara kati ya wafanyakazi wa sekta binafsi na wafanyakazi wa sekta ya umma ambapo wafanyakazi wa sekta binafsi wanaohusika na mambo ya kilimo na nguo kwenye viwanda, kima cha chini ni 100,000/= lakini wa Serikali ni 300,000/=. Kwa hiyo, hayo mambo ambayo nimesema leo niwakumbushe kwamba na mimi nayakumbuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajielekeza kwenye mambo mawili; jambo la kwanza nakumbuka Serikali yetu ya Awamu ya Tano ilifanya zoezi moja muhimu sana na zoezi nyeti sana, zoezi la kuhakiki vyeti vya watumishi wetu. Lilikuwa ni zoezi la lazima, lilikuwa ni zoezi ambalo linatusaidia kufanya usafi kwenye sekta nzima ya utumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ninakumbuka tarehe 7 Machi, 2018 ilitoka Taarifa ya mwisho ya Serikali ambayo ilituambia wafanyakazi 511,789 ambao ni sawasawa na asilimia 96.71 walikuwa ni wafanyakazi waliohakikiwa, lakini wafanyakazi 14,409 ambao ni sawasawa na asilimia 2.82 walikuwa ni wafanyakazi ambao walibainika wana vyeti fake na wafanyakazi 1,907 walikuwa ni wafanyakazi ambao walikuwa bado hawajapeleka uthibitisho wa vyeti vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ambayo nataka niijenge hapa, pamoja na kuunga mkono zoezi la Serikali la kuwatambua watumishi wenye vyeti fake na kuchukua hatua stahiki, lakini lazima tukumbuke hawa watumishi walifanya kazi ya kuitumikia nchi hii. Hata masuala ambayo tunajivunia leo wao pia ni sehemu ya kazi ambayo tumeifanya. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kujenga hoja kupitia Wizara yetu hii ya Utumishi ni vizuri sasa wafanyakazi hawa tukaangalia utaratibu wa kuwapatia haki zao kwa sababu, wakati wanafanya kazi waliweza kukatwa fedha ambazo zikaenda NSSF, leo zile fedha zimekwenda kule zinamnufaisha nani?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wafanyakazi hawa wengine walipitisha muda wa kisheria, miaka 15, miaka 20 na kuendelea, walistahili pia kulipwa kiinua mgongo. Kwa hiyo, pamoja na Serikali kuwaondoa kazini nilikuwa naomba Serikali hii ya Awamu ya Sita ikaangalie jambo hili kwa jicho la huruma, ikawaangalie wananchi hawa wananchi 14,409 ambao wana familia zinawategemea wakaweze kupata kiinua mgongo chao wakapate na mafao yao na baada ya hapo tuendelee sasa kuchukua watumishi wenye sifa. Maana sisi kama Serikali pia tulichangia kuingiza watumishi hawa kwa sababu waliingia kwa utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la pili niende kwenye mchakato mzima wa kuwapandisha vyeo watumishi na madaraja na mimi nakiri hotuba ya jana ya Mheshimiwa Rais imetupunguzia maneno kwa sababu watumishi wa umma walikuwa na kilio kikubwa sana. Watumishi wa umma toka mwaka 2015 walikuwa hawajapandishwa mishahara. Watumishi wa umma wamekuwa na matatizo mengi sana kwenye madaraja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala la madaraja sio suala jepesi kama tunavyoliona. Mimi nakumbuka mwaka 2012/2013 wakati nikiwa Mkuu wa Wilaya ya Korogwe kweye bajeti ya mwaka 2012/2013 Mkurugenzi wa Halmashauri ya Korogwe Mji alisahau kuwaingiza watumishi kwenye mchakato wa kupanda vyeo, watumishi ambao waliajiriwa mwaka 2009. Matokeo yake ni kwamba wale TSC au kwa maana ya TSD huko zamani ambao lazima kikao chao kikae kiweze kuwapitisha hakikuweza kukaa eti kwa sababu hakuna posho, watumishi wakakosa haki yao ya msingi ya kupanda madaraja na baadaye wakatakiwa waandike barua ya kuomba kupata daraja la mserereko.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa hoja yangu ni nini; lazima tuangalie vizuri mfumo wetu wa kuwapandisha madaraja watumishi. Kwa sababu nimeambiwa taratibu ambazo zinafuatwa, taratibu ya kwanza tunaangalia bajeti. Mfano mwaka huu tumeajiri watu 800, uwezo wetu wa bajeti wa kupandisha ni watu 300, tunabakisha watu 500 ambao wao watakuja kupanda mwaka mwingine wa fedha. Kumbuka hawa wameanza kazi pamoja, huyu ana TGS D atatoka D atakwenda E, ambaye ameanza naye kazi pamoja atabaki kwenye TDGS D ile ile ambayo italeta manung’uniko na malalamiko makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeambiwa pia wanaangalia tange kwa maana ya seniority list, lakini pia wanaangalia na OPRAS. OPRAS ambayo ina changamoto nyingi inatakiwa kuwe na malengo, lakini pale kuwe na resources. Unakuta malengo yanakuwepo, lakini resources zinakuwa hazipatikani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa nataka niseme kwamba, changamoto ya madaraja ya watumishi ni kubwa tofauti na ambavyo tunaiona. Nilikuwa nataka niishauri Serikali ni vizuri sasa, kwa mapendekezo yangu, tukaunda tume au tukaunda timu maalum ambayo itafanya kazi ya kupitia changamoto za madaraja ya watumishi kwa miaka yote iliyokuwepo. Vinginevyo wale ambao wanaweza wakalalamika watapata solution, wale ambao hawawezi kuwafikia Serikali watabaki wananung’unika na mwisho wa siku tunaanza kuwatupia mzigo Maafisa Utumishi wakati tunafahamu kwamba Afisa Utumishi hawezi kupandisha nje ya bajeti na hawezi kupandisha nje ya utaratibu wa Serikali.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nitumie fursa hii kukushukuru sana kwa nafasi hii ili niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Ardhi. Mimi nina msemo wangu mmoja huwa nasema, mtu ukiwa mnafiki ukiwa kijana, ukizeeka lazima utakuwa mchawi, na mimi kwa sababu sina mpango wa kuwa mchawi kwenye uzee wangu, napenda nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, William Lukuvi; Naibu wake Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Makamishna wote kwa kazi kubwa wanayofanya kwenye Wizara ya Ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa changamoto za Wizara hii ukiona wachangiaji wachache maana yake changamoto nyingi zimefanyiwa kazi, tumebaki na sisi wachache ambao tunadhani pia watatusikiliza, watakwenda kuzimaliza ili huko mbeleni changamoto zisiwepo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakwenda kwenye masuala mahsusi kwa sababu yale maswala ya kijumla jumla sijui kuna mgogoro mpaka kati ya mtaa na mtaa, sijui kata na kata hayo siwezi kuzungumza kwa sababu ule ni mipaka ya kiutawala tu, haikuzuii kununua ardhi mahali popote, haikuzuii kufanya shughuli zako. Kwa hiyo ni masuala ambayo yatamalizwa huko kwenye ngazi ya mitaa, ngazi ya kata, wilaya na mikoa, hapa tunazungumzia masuala mahsusi ambayo tunadhani yanahitaji attention ya Wizara ili mambo yaweze kuwa rahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la kwanza; Arusha tuna mgogoro mkubwa sana wa ardhi ni mgogoro kati ya Jeshi letu la Wananchi na Kata za Mushono, Mlangalini na Nduruma. Ni mgogoro wa miaka mingi sana, lakini mgogoro ambao umeshika kasi mwaka 2012. Tunaishukuru sana Serikali, baada ya changamoto kuwa kubwa, Mheshimiwa Waziri Mkuu kipindi hicho alikuwa ni Mheshimiwa Mizengo Peter Kayanza Pinda, aliitisha kikao tarehe 20 Machi, 2012 kwa ajili ya kujadili mgogoro huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kikao hicho maelekezo yaliyotoka. Katika maelekezo hayo pamoja na kuwa na maagizo kumi, lakini maelekezo ya msingi yalikuwa ni mawili. La kwanza, Jeshi irekebishe mipaka yake upya na kuacha eneo lenye mgogoro kwa wananchi; na la pili, Jeshi wapewe eneo la mlima ambapo wananchi hawana mgogoro nalo eneo hilo wapo tayari kulitoa. Maelezo haya ya Serikali yaliwasilishwa na Naibu Waziri Mheshimiwa Goodluck Ole-Medeye kipindi hicho, aliyafanya kwa wananchi tarehe 28 Machi, 2012.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto iliyojitokeza pale Serikali ilikwenda mwaka 2012, ikabainisha baadhi ya maeneo ambayo wanadhani wanatakiwa waondoe watu wakaenda wakafanya uthamini mwaka 2012, wakaondoka zao. Mwaka 2012, 2013, 2014, 2015 mpaka 2019 na tunafahamu kwa mujibu wa sheria uthamini ukishafanyika ikipita miezi sita kuna interest kidogo inalipwa, ikifika miaka miwili inabidi ule uthamini ufanywe upya, lakini uthamini wa mwaka 2012, Serikali imekuja kurudi mwaka 2019 na kuwalipa watu kwa uthamini wa siku za nyuma ambao hautambuliki kwa mujibu wa sheria kwa sababu miaka miwili tayari ilishapita.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kibaya zaidi mwaka 2015 Serikali ilikwenda pale na Mkuu wa Wilaya wa kipindi hicho na viongozi wengine wakawahakikishia wananchi kwamba, eneo hili Serikali haina interest nalo tena kwa hiyo, wananchi wenye maeneo yao wanao uhuru wa kufanya shughuli zozote. Wale wananchi wakaamua kuyauza yale, maeneo wakawauzia wadau wengine na wakati huo Serikali hiyo hiyo, ilishakwenda kutengeneza mchoro, kuna approved plan pale No. CAO/65/01/6 na wananchi ambao wanataka kujenga walienda kuomba vibali vya ujenzi wakapewa na halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi walikwenda kwenye mitaa na vijiji wakapitishiwa, wamejenga mpaka magorofa, leo Serikali inakuja, inataka kutumia mabavu na kutaka kwenda kuwaondoa wale wananchi. Kosa lililofanyika hapo mara baada ya Serikali kurudi mwaka 2019, ikaja na orodha yao ile ile ya mwaka 2012, wakaanza kutumia nguvu na mabavu wanawarushia watu hela kwenye Mpesa na kwa njia nyingine ili mradi tu zile hela zilizokuja ziweze kwenda.

Mheshimwia Naibu Spika, badala ya kumlipa mwananchi ambaye anaishi pale kwa wakati huo na ambaye amejenga, wamekwenda kumlipa mtu ambaye alishauza na alishaondoka siku nyingi. Nadhani hapa TAKUKURU wana kazi ya kufanya kuwatafuta wale watu waliolipwa, warudishe zile fedha na Serikali ifuate maelekezo haya ya Serikali ambayo yalisimamiwa na Waziri Mkuu wa nchi hii, ili wale wananchi wabaki pale wafanye shughuli zao na kama kuna maelekezo mengine yoyote basi ni vizuri Serikali ikakaa chini na wahanga wale tutafute solution ya kudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwenye jambo hili, kwanza, nimepata taarifa kwamba Mheshimiwa Waziri huenda akawa Arusha kwenye ziara ya kikazi wiki ijayo, tulikuwa tunamwomba Mheshimiwa Waziri akutane na wahanga hawa ili apate picha pana ya jambo hili na mwisho wa siku Serikali ifanye maamuzi kwa maslahi mapana ya wananchi wa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu la pili kwa Mheshimiwa Waziri, namwomba kwamba kama kuna mchakato wowote wa kutoa hati kwa Jeshi la Wananchi usitishwe hadi hapo mgogoro huu utakapohitimishwa na Serikali itakaporidhika na hali halisi ya mchakato mzima kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la pili, shida ya hii nchi kuna double standard, kuna maeneo mengine maamuzi yanafanyika very fast, kuna maeneo mengine maamuzi yanafanyika kuangalia maslahi mapana ya nchi, kuna maeneo mengine kuna ku-delay. Yako mashamba ambayo hayajaendelezwa kwenye nchi hii ambayo Serikali imeyachukua, lakini kwa upande wa Jiji la Arusha kuna kigugumizi kikubwa sana, liko shamba la Bondeni City ambalo kwanza halijaendelezwa na mimi nina ushahidi na Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba halijaendelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi na yeye tuliwahi kuhudhuria kikao kikubwa kabisa kilichoongozwa na Kiongozi Mkuu wa Nchi hii yeye akiwepo, Mheshimiwa Mhagama, Waziri wa TAMISEMI na Makatibu wao Wakuu na mimi nilikuwepo, maelekezo yalishatoka pale lakini kuna kwenda mbele, kuna kurudi nyuma. Ziko baadhi ya hatua zimechukuliwa, kwanza, lilitakiwa lipatikane eneo mahususi kwa ajili ya kujenga stendi, kwenye hili Waziri nampongeza sana kwa sababu, eneo limeshapatikana na Wizara ya TAMISEMI kupitia TACTIC imeji-commit kutoa fedha, pale tutajenga stendi ya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi letu kwa Mheshimiwa Waziri, hili jambo alipe uzito unaostahili, tunaomba hili jambo sasa aende akalihitimishe, tunaomba hili jambo ajiridhishe kwa sababu kwanza taarifa ziko kwamba mmiliki mwenyewe kwanza sio raia wa Tanzania, taarifa zipo pia mmiliki mwenyewe ameshakufa, taarifa zipo kwamba halmashauri waliingia makubaliano ya kiujanjaujanja na yule mwekezaji ya hiyo asilimia tano, eti Jiji asilimia tano yule mhusika asilimia 95.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kupigwa mkwara wakabadilisha, ikawa Jiji asilimia 10 yule asilimia 90. Sasa hivi tena wamepigwa mkwara mwingine tena wanasema Jiji asilimia 50 yule mwingine asilimia 50, huu ni utani, kwa sababu, Jiji la Arusha tuna changamoto kubwa ya ardhi, tumetenga fedha kujenga vituo vya afya, kujenga shule na maeneo mengine ya maendeleo. Tulikuwa tunaomba Serikali ikasimamie jambo hili kwa haki na kwa mujibu wa sheria na ikiwezekana hiyo ardhi irudi Serikalini ili maeneo ambayo hakuna shule tukajenge. Maeneo hakuna vituo vya afya tukajenge na mambo mengine yaweze kuwa mazuri zaidi. Tunamwomba Waziri mwenye dhamana ya ardhi aingilie kati ili mgogoro huu uhitimishwe kwa mujibu wa sheria na tufanye masuala ya maendeleo badala ya kuanza kunung’unika na kuzua masuala mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwangu la tatu ni kuhusu urasimishaji. Tuna dhamira nzuri sana, lakini kama kuna zoezi ni kichefuchefu ni urasimishaji. Tuna Kata pale kama ya Sekei, kuna Kata ya Balaa, Kata ya Lemala na Kata nyingi za Jiji la Arusha ambazo watu wamekwenda kufanya zoezi la kurasimisha, wamechukua fedha za watu na zoezi halijakamilika, zaidi ya mwaka umeshakwenda. mambo haya hayatoi sura nzuri kwa Serikali, Mheshimiwa Waziri Lukuvi ni mtu anayefanya kazi kwa weledi sana, watendaji wake wanaendana na kasi yake vizuri sana, heshima aliyoijenga kwenye nchi hii ni kubwa sana, lakini hili la urasimishaji litampunguzia umaarufu kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ombi langu atakapokuja Arusha tukutane pia na viongozi wanaotoka kwenye Kata zote zinazofanyiwa urasimishaji, ili tumweleze changamoto halisi na yeye kama Waziri mwenye dhamana na timu yake waende wakatutafutie majawabu ya kudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, kwa heshima na taadhima naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, nami naomba nitumie fursa hii kukushukuru sana kwa kupata fursa ya kuweza kuchangia mada iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, mimi nitalenga zaidi kwenye masuala mawili; suala la kwanza, nitazungumzia mfumuko wa bei, hasa kwa bidhaa ambazo zinatokana na kilimo; pili, nitazungumzia kuhusiana na mashamba ya maua ambayo mengi yako kule Mkoani Arusha.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba hali ya kipato cha Mtanzania wa kawaida ni ngumu, tunafahamu kwamba kuna changamoto kubwa sana ya ajira katika nchi yetu, watu wengi wanamaliza vyuo vikuu, wanamaliza shule lakini hawapati ajira kiasi ambacho kinawasababisha kuwa na ugumu kwenye maisha.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba kuna changamoto pia kwenye masuala yanayohusiana na mishahara yetu. Tukiangalia kwa mfano kwenye sekta binafsi mishahara kwa kiwango cha chini imetoka kwenye shilingi 120,000 mpaka shilingi 140,000 kwa maana kuna ongezeka la kama shilingi 20,000; tumeona pia kwenye sekta ya umma tumetoka shilingi 300,000 mpaka shilingi 375,000 kwa maana ya kwamba tumeongezewa kwa shilingi 75,000.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nasema hayo ili nitakapozungumzia mfumuko wa bei tuangalie na athari tulizokuwa nazo kwenye maisha yetu ya kila siku kwenye mishahara pamoja na changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia website ya Wizara ya Kilimo ambayo imetoa data mbalimbali kuhusiana na bei za vyakula nchini, ukiangalia kwenye upande wa mchele inaonekana mwaka 2020 kilo moja ya mchele ilikuwa ni shilingi 1,486 lakini mwaka 2023 kilo moja ya mchele inaonekana ni shilingi 2,888. Hii kwa mujibu wa Wizara ya Kilimo ni bei ya jumla, bei ya sokoni. Kwenye upande wa mahindi imetoka shilingi 570; mwaka 2020 mpaka shilingi 1,160 na mwaka 2023 na upande wa maharage imetoka shilingi 2,040 mpaka shilingi 2,916.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia hapa tu kwa mujibu wa maelezo ya Wizara ya Kilimo ambayo yanasema kwamba mfumuko wa bei umetokana na sababu nne; kwa maana ya UVIKO-19, vita ya Urusi na Ukraine, kupanda kwa bei za mafuta na mabadiliko ya tabianchi. Kwa maoni yangu, sababu zote za UVIKO, mabadiliko ya tabianchi, vita ya Ukraine zimeangaliwa kutoka shambani mpaka walivyosafirisha hadi zikafika sokoni ndiyo maana bei leo imeweza kuwa shilingi 2,888 kwa mchele; shilingi 1,160 kwa mahindi na shilingi 2,916 kwa maharage.

Mheshimiwa Spika, ukiacha hiyo bei ya jumla sasa ukienda kwenye soko lenyewe kwa maana ya bidhaa ya rejareja. Ukitembelea Soko letu la Majengo hapa Dodoma unakuta mchele unauzwa mpaka shilingi 3,400. Ukienda kule Arusha unakuta mchele unauzwa mpaka shilingi 3,500. Sasa ninajiuliza kwamba kutoka shilingi 2,888 kama wastani hadi kufika shilingi 3,500 sasa pale role ya Serikali ni nini?

Mheshimiwa Spika, kwa sababu inavyoonekana sasa hivi wafanyabiashara kama wako huru sana kujiamulia kupanga bei wanavyotaka. Maana kutoka shilingi 2,888 mpaka shilingi 3,500 nadhani difference ni kubwa kwa sababu mzigo mkubwa tayari umeshabebwa; mzigo wa usafirishaji kutoka shambani mpaka kufika sokoni, mzigo wa pembejeo tayari mkulima alishaubeba kule.

Mheshimiwa Spika, huyu anayetoa Soko Kuu la Arusha au anayetoa Soko Kuu la Majengo anakwenda kupeleka dukani kuuza rejareja kwa nini gap limekuwa kubwa. Mimi naona hapa kuna kazi ya Serikali ya kufanya ya kusimamia mfumuko wa bei na siyo kuacha tu bei iwe ni ya kiholela kwenye maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ukiangalia hii taarifa yenyewe ambayo imetolewa kwenye website ya Wizara ya Kilimo unaona kabisa inawatia moyo wafanyabiashara kuendelea kuuza bidhaa kwa bei ya juu. Ukiangalia mfano taarifa yao hii ya tarehe 2 hadi 6 Januari, 2023, kwa upande wa Mkoa wa Dodoma wanatuambia kwamba mchele unauzwa shilingi 3,400 kwa maana ya rejareja lakini mhusika kule amenunua kwa shilingi 2,775, kwa hiyo kuna ongezeko kama la shilingi 625.

Mheshimiwa Spika, upande wa Arusha pia ukiangalia ni shilingi 4,000 lakini yeye amenunua bei ya jumla shilingi 2,900 kwa hiyo kuna ongezeko kama la shilingi 1,100. Lakini kibaya zaidi ukiangalia Mkoa wa Kilimanjaro, Wizara ya Kilimo yenyewe inatuambia kwamba bei ya mchele sasa hivi kwa bei ya jumla ni shilingi 3,500.

Mheshimiwa Spika, sasa nikawa najiuliza, kama pale Arusha naweza nikanunua mchele kwa bei ya jumla ya shilingi 2,775, inakuaje Kilimanjaro nanunua kwa shilingi 3,500? Ni rahisi sana kwa mwananchi kupanda daladala kutoka pale Kilimanjaro akalipa nauli shilingi 5,000 akafika Arusha akanunua mchele akarudi Kilimanjaro akatumia shilingi 10,000. Lakini ukiangalia gharama ambayo imeongezeka hapa siyo chini ya shilingi 500. Kwa hiyo, unaona kabisa kwamba japo kuwa Serikali imejificha kwenye vita vya Ukraine, UVIKO na mabadiliko ya tabianchi lakini bado kuna kazi ya kufanya ili kuondoa mfumuko wa bei kwenye maeneo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ushauri wangu, naomba Serikali yetu iwaangalie wananchi hawa kwa jicho la huruma. Manung’uniko ni mengi, vilio ni vingi.

Mheshimiwa Spika, na kinachonisikitisha hii hela wala hapati mkulima. Kwa sababu kama katika hali ya kawaida nikienda kwenye bei ya jumla ni shilingi 2,950, sasa hebu niambie hii analipwa mfanyabiashara yule wa jumla, je, ndiyo fedha ambayo anapata kweli mkulima wa kawaida?

SPIKA: Mheshimiwa Gambo; Mheshimiwa Waziri amesimama.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ninataka nimpe taarifa kwamba; moja, Serikali haijajificha kwenye anachosema Ukraine wala UVIKO, wala tabianchi. Nimpe taarifa kwamba haya mambo ya Ukraine na UVIKO ni halisia, yaani siyo kisingizio. Haya ni mambo halisia.

Mheshimiwa Spika, na Serikali imechukua hatua ambazo kwa East Africa na SADC hakuna nchi imezichukua, za kutoa shilingi bilioni 100 kila mwezi kwa ajili ya kupunguza gharama. Ndiyo maana unaona hata nchi majirani wanakimbilia kuchukua hivi vitu kutoka katika nchi yetu; shilingi bilioni 100 kila mwezi.

Mheshimiwa Spika, na siyo hapo tu, Serikali ikaondoa kodi na tozo zote kwenye mafuta ya kula, kwenye wheat flour na ikachukua nusu ya bei ya kila mfuko wa mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka kufanya tathmini halisia, ondoa hii gharama ambayo imechangiwa, uone hizi bei zingekuwa wapi. Kwa sababu tusiongelee tu bei iliyopo tukaona hamna kilichofanyika, tunapofanya proximation hizo, weka kama isingekuwepo hiyo bei, uichukulie ile bei ambayo inge-trend. Ndiyo maana bei ya hizi bidhaa ndiyo ziko juu, lakini kwa sababu dunia nzima ziko juu kwa Tanzania iko chini ukilinganisha na nchi za East Africa na za SADC lakini hata maisha hayo fuatilieni kwa nchi zingine za Ulaya na Marekani kote kule kumebadilika kumeenda tofauti.

Mheshimiwa Spika, hivyo, nilitaka nitoe taarifa pamoja na kwamba kuna jitihada zingine tunaendelea kuchukua, ukiona jitihada ambazo zimechukuliwa na Kilimo na zilizochukuliwa na Viwanda na Biashara jitihada zinaendelea lakini lazima tu-recognize jitihada ambazo zimeshafanyika, Serikali iko macho sana kwenye haya mambo na inaendelea kuchukua hatua. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Mrisho Gambo, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, mimi siipokei kwa sababu ni wajibu wake kuitetea Serikali kwa hiyo mimi naomba nisiipokee na nimpongeze kwa kazi yake nzuri ya kuitetea Serikali.

Mheshimiwa Spika, nitampa mfano mmoja tu, mwaka 2022 mwishoni kwa mjibu wa taarifa ya Serikali, ilikuwa inaonekana mchele ni shilingi 2,090 na nikisema shilingi 2,090 sizungumzii shambani, nazungumzia mkulima ameshalima Serikali ime-subsidize mbolea zote zimeshaingizwa, Mkulima ameshauza, dalali amechukua amepeleka sokoni Dar es Salaam, Arusha au Dodoma. Leo mtu ambaye amenunua kwa shilingi 2,090 anakuja kuuza kwa shilingi 3,500 sasa pale UVIKO unaingiaje? Pale vita ya Ukraine inaingiaje?

Mheshimiwa Spika, kuna mahali unaweza ukaona Serikali ime-subsidize ndio maana tukafikia Shilingi 2,090. Tunasema baada ya hapo sasa mbona huku hamuangalii kwa wananchi kunakoendelea, watu wanaamua tu kujiuzia tu wanavyotaka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali, hili jambo la mfumuko wa bei siyo jambo jepesi, sisi wote tunatokana na Serikali hii na Chama chenye Serikali hii, lakini tunao wajibu wa kuwasemea wananchi siyo kutetea kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaomba Wizara ya Kilimo, Wizara ya Fedha na Wizara ya Viwanda na Serikali kwa ujumla watusaidie kwenda kufanya utafiti na kuangalia kama kuna mahali popote wafanyabiashara wanaongeza gharama waende wakasimamie. Tumeona huko siku za nyuma, wafanyabiashara walikuwa wakisikia tu Mwezi Ramadhani unakaribia walikuwa wanapandisha Sukari. Serikali ilikuwa inaingia kila mahali kwenye masoko na maeneo yote, bei ilikuwa inakuwa stable, sasa hivi kigugumizi cha nini? Tunaacha watu wajifanyie wanavyotaka?

SPIKA: Sekunde thelathini, malizia.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia naona muda wa hoja yangu ya pili hautakuwepo lakini ombi langu kwa Serikali tuangalie uwezekano wa kutoa kipaumbele kwenye mfumuko wa bei, hili jambo ni kubwa na lina maslahi mapana kwa nchi yetu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuweza kuchangia kwenye Wizara yetu ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Mimi mchango wangu nitauelekeza kwenye maeneo makubwa mawili. La kwanza ni kwenye mapitio ya bajeti kwa sababu ni utaratibu kabla ya kuchangia bajeti mpya kuangalia bajeti ya mwaka uliopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jiji letu la Arusha tuna changamoto kubwa sana ya ubadhirifu na usimamizi mbovu wa fedha za halmashauri. Hapa nitapenda nitoe mifano michache kabla sijaenda kwenye uhalisia. La kwanza tunajenga jengo la utawala la ghorofa zaidi ya sita, lakini bado wametafuta fundi mjenzi bila kutangaza tender, taratibu za manunuzi hazijafuatwa, wamemtafuta rafiki yao wamweka pale wamesaini mkataba wakampa kazi kwa kiasi cha shilingi 199,750,000. Lakini bado pia wamenunua vifaa vya shilingi 132,000,000, ambavyo havijadhibitika kufika eneo la site. Ukiangalia pia bado wameenda kuongeza nondo ziada ya tani 6.48 yenye thamani ya shilingi 17,000,000 ambazo ni kutokana na uzembe wa wataalamu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameweza pia kuongeza malipo ya 21,000,000 kwa fundi kutokana na uzembe pia wa watalaam wetu. Wameweza pia kuanza ujenzi huo bila kuwa na mtalaam mshauri katika ujenzi huo ambao ninaouzungumzia wa jengo la utawala. Pia bado kumekuwa na malipo fake, kumekuwa na risiti fake za EFD za kiasi cha shilingi 699,945,471, hela zimetoka wamefoji risiti wamepeleka halmashauri na tumekosa kupata huduma. Bado pia wameenda kutengeneza quotation za kughushi za shilingi 580,545,900 kwa kutumia kampuni ya Pedna Limited ambayo ni shilingi 543,000,000 na kampuni ya Arusha Hotel Ltd kiasi cha shilingi 36,000,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado pia wamefanya malipo ya shilingi 36,580,000 kwa wazabuni ambao hawakutoa huduma yoyote katika Jiji la Arusha na Mbunge akizungumza unasema huyu Mbunge anagombana na watu. Kwenye mambo kama haya lazima tugombane mpaka mambo yaweze kueleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kumekuwa na manunuzi ya shilingi 12,822,400 kupitia dokezo ambalo wanasema liliandikwa na mtu anaitwa Optat Ismail; lakini baada ya kuitwa amekana dokezo hilo, kwa hiyo hilo dokezo linaonekana ni fake lakini mchakato uliendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado pia kumekuwa na matumizi ya fedha za masurufu ya kiasi cha shilingi 62,000,000 ambayo yana viashiria vya ubadhirifu na kutokana na matumizi pia mengine ya shilingi 132,000,000 ambazo gharama zake hazina support yoyote ya matumizi. Wanachukua hela wanatumia na wala hawajali kwa sababu wanajua ngazi ya mkoa na wilaya wala hawana cha kuwafanya na pengine inawezekana ikawa ni sehemu ya changamoto hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kumekuwa na matumizi ya fedha taslimu kwa manunuzi ya bidhaa mbalimbali kiasi cha shilingi 2,000,000,000 ambayo hayana udhibitisho na wala matumizi yake hayaelezeki. Sasa haya masuala ni makubwa sana nadhani ni vizuri Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na timu yake wakafanya utaratibu wa kwenda kuweka jicho la ziada kwenye Jiji letu ili mwisho wa siku tuweze kuokoa hizi fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na matumizi pia akaunti ya amana, yaliyokosa udhibitisho ya shilingi 92,692,714. Nimesema nianze na utangulizi huo kwa sababu Jiji letu limekuwa ni shamba la bibi, watu wameungana Serikali Kuu pamoja na Serikali ya Mtaa kuimaliza Halmashauri yetu. Mimi nimejitoa kafara kuhangaika na msuala haya ili kulinda maslahi mapana ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo suala langu la pili, nimesoma Hotuba ya Waziri wa TAMISEMI yenye page zaidi ya 281 lakini sijaona kama wamachinga wamepewa uzito unaostahili. Ukiangalia tu kwenye page ya tisa amezungumzia kwenye (viii) kwamba kuratibu shughuli za wajasiriamali wadogo na wafanyabiashara wadogo basi, ukitoa hapo hakuna sehemu nyingine yeyote ambayo wamachinga wamezungumziwa na wamachinga ni kundi kubwa. Ukiangalia sisi tulitenga fedha mwaka jana kiasi cha 1,000,000,000 kwa ajili ya kuboresha maeneo yao, lakini zile fedha asilimia kubwa zimeliwa, wameenda kujenga eneo moja linaitwa Ulezi, ukiwaambia kule hakuna biashara watu hawawezi kwenda wakapeleka shilingi 86,000,000 baadaye wamebomoa hasara imepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameenda kujenga jengo namba 68 baada ya kujenga bati yenye gauge 28 wametumia bati za gauge 30. Ukienda pale mvua ikinyesha tope tupu wananchi wanapata tabu, hata nia na lengo la Mheshimiwa Rais inakwenda kuwa kero kwa watu wakati dhamira ya Mheshimiwa Rais ilikuwa ni kuwawekea watu mazingira mazuri ili waweze kufanya shughuli zao vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye upande wa machinga sisi pale tuna machinga namba 68, tuna eneo la Machame, tuna eneo la Ulezi na eneo la Mbauda. Ukienda maeneo yote changamoto ni kubwa sana; hakuna mitaro ya kupokelea maji, hakuna mataa ya uhakika. Ukiangalia wenzetu wa Dodoma hapa wamejenga jengo zuri sana ambalo linawapa fursa wafanyabiashara na maeneo mazuri zaidi. Ukienda kule Arusha ni utani na masihara ya hali ya juu. Nikuombe tumwombe na Waziri wetu na timu yake wakaongeze jicho ili wale wamachinga wapate mahali pazuri pa kufanya shughuli zao na mwisho wa siku dhamira na nia njema ya Rais wetu iweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuna changamoto pia ya wenzetu wa mgambo; mgambo wanawasumbua sana wafanyabiashara wanawanyanganya vitu vyao, mama wengine hata wakifunga ushungi wanavuliwa ushungi wao, wanafanyiwa vurugu kila mahali kiasi ambacho inaongeza kero na manung’uniko kwa watu wetu. Mimi niombe mgambo hawa, kwa sababu wao hawana hatia, wao wanatumwa na Serikali katika ngazi ya mkoa na ngazi ya wilaya na wanamshinikiza Mkurugenzi ili kupambana na hawa watu. Naishukuru Halmashauri kwa namna moja au nyingine tukizungumza nao wakati wanapowanyanyasa wale watu wamekuwa wanawarudishia baadhi ya vitu vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe hawa mgambo wawekewe utaratibu maalum, hawa machinga pia wawekewe utaratibu maalum ili pasiwe na sintofahamu na vurugu kwenye jiji letu. Ukienda soko kuu wanaonewa pale, wafanyabiashara wamachinga, ukienda namba 68, ukienda Kilombero, ukienda kila mahali vurugu kila mahali. Kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri pia aongeze jicho kubwa kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulikuwa tuna ushauri, kama kama kuna baadhi ya masoko ya Machinga yanafungwa saa kumi na mbili na yanafungwa saa moja, tutafute baadhi ya barabara jioni ambazo hazitumiki sana na watu tuzifunge zile barabara, wale wafanyabiashara wadogo wadogo kuanzia saa kumi na mbili waruhusiwe kufanya biashara pale wapate riziki zao; maana mgambo wanawanyanganya vitu mpaka saa tano usiku. Hebu mniambie ukimnyanganya mtu muda huo unavipeleka wapi ilhali mtu anatafuta riziki kwenye maeneo yale?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna watu wanahusika na masuala ya parking. Wako wanaofanya biashara ya parking na kila mwananchi analipia parking kila siku, lakini wanashindwa kulipwa mishahara yao mwezi mmoja miezi miwili. Ukiangalia leo tangu Februari na Machi hawajalipwa ilhali ukiangalia fedha imeshaingia Serikalini. Kwa hiyo tuwaombe Serikali mkae na yule mzabuni kila mwisho wa mwezi wale wafanyakazi Watanzania wenzetu wa Arusha maskini wapate haki yao ya ujira wao kama wakati unavyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kumalizia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Gambo, muda wako umeisha.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sekunde chache kumalizia.

MWENYEKITI: Sekunde moja malizia Mheshimiwa Gambo.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwanza wewe binafsi, pia naishukuru Serikali yetu kwa kutenga shilingi 1,000,000,000 kwa ajili ya kukarabati Soko la Samunge, shilingi 1,000,000,000 kukarabati soko kuu na shilingi 1,000,000,000 kukarabati soko letu la Kilombero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana na namtakia Mheshimiwa Waziri…

MWENYEKITI: Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru sana kwa kupata nafasi ili niweze kuchangia Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajielekeza kwenye maeneo mawili; kwenye Bodi ya Mkopo pamoja na Shule yetu pedwa ya St. Jude ambayo ipo pale Mkoani Arusha. Hii ni shule ambayo inasomesha watoto 1,800 bure. Wanatoa chakula bure, usafiri bure, wanalala kwenye mabweni bure na masuala mengine yote. Watoto hawachangii hata shilingi moja. Pia wanasomesha watoto 350 Chuo Kikuu kwa gharama zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, pia wameajiri watu 295. Kati yao, Watanzania ni 286 na wageni wako saba. Cha kushangaza mwaka 2020, mwezi Oktoba, TRA walikwenda kuifunga akaunti ya shule hiyo ambayo ipo kwenye Benki ya NCBA na tarehe 03, Novemba, 2020, walikwenda kuchukua fedha kiasi cha shilingi milioni 500 kutoka kwenye akaunti ya shule hiyo huku wakiwa wamewapa assessment ya shilingi bilioni 5.43.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unajiuliza, hii shule haifanyi biashara, wanaunga mkono juhudi za Serikali za kusomesha bure watoto wa Kitanzania. Mazingira ya shule ni mazuri, lakini bado TRA wanakwenda wanawagawia assessment ya 5.4 billion na wanafunga akaunti yao na wanachukua fedha kiasi cha milioni 500, fedha ambayo ingetumika kwa ajili ya chakula cha watoto, kwa ajili ya uniform za watoto na masuala mazima ya uendeshaji.

Mheshimiwa Spika, nadhani Wizara ya Elimu, mama yangu, Mheshimiwa Prof. Ndalichako, ana kazi kubwa ya kuliangalia suala hili kwa kushirikiana na Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba. Katika hili nitumie fursa hii kumpongeza sana Waziri wa Elimu kwa sababu yeye alimtuma Katibu Mkuu wake akaenda kutembelea shule hii akaona changamoto hizo na wakaahidi kwamba wataongea na Wizara ya Fedha ili changamoto iondoke kwenye shule hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ushauri wangu kwenye eneo hili, kwa sababu shule hii haifanyi biashara, nina mapendekezo mawili. Pendekezo la kwanza shule hii ipate msamaha wa kodi. Pendekezo la pili, kwa sababu tumepata taarifa maana kuna wadau wanasaidia kwenye shule hii na tunaambiwa zaidi ya asilimia 92 ambao wanasaidia shule hii wanatoka Australia na wako wageni ambao wanafanya kazi ya kusaidia kwenye fundraising na wanasaidia kwenye masuala ya marketing, wameomba vibali vya kazi kupitia Idara ya Kazi, wamekosa. Sasa hivi wamekata rufaa kwa Waziri mwenye dhamana, mama yangu, Mheshimiwa Mhagama, mtu ambaye ni mchapakazi, ni mtu ambaye anaendana na falsafa ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yangu kwamba Mheshimiwa Mhagama atakwenda kulipa kipaumbele jambo hili, tuwasaidie watu hawa wawili wapate vibali vya kazi na vibali vya ukaazi ili mwisho wa siku wasaidie kutafuta fedha kwa ajili ya shule ile na watoto wa Kitanzania waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la pili ni kuhusu Bodi ya Mikopo. Katika hili kwa kweli…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gambo, hebu tusaidie jambo moja; katika hiyo shule, umetaja hiyo idadi kubwa ya wanafunzi.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Ndiyo.

NAIBU SPIKA: Hiyo shule ina wanafunzi wanaosomeshwa bure tu au inao na wengine ambao wanasomeshwa kwa kulipa fedha?

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, watoto wote pale wanasoma bure ikiwa ni pamoja na wanafunzi wa kike 600 na pia wameanzisha na shule ya sayansi, wana masomo ya PCB na PCM ili kuunga mkono juhudi za Serikali za kupambana na changamoto ya sayansi na teknolojia. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Haya, endelea na hoja yako.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kuhusiana na Bodi ya Mkopo. Kwanza kabisa nitumie fursa hii kuipongeza sana Serikali Sikivu ya Awamu ya Sita chini ya mama yetu, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Nampongeza pia Waziri wa Elimu kwa sababu nina imani ameshauriana na Mheshimiwa Rais na mwisho wa siku akaweza kufanya maamuzi haya yenye tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata taarifa kwanza siku ya Mei Mosi, Mheshimiwa Rais alitutangazia kwamba asilimia sita ya kulinda thamani ya fedha imeondolewa. Jana pia tumepata taarifa kuwa asilimia 10 ambayo ilikuwa imewekwa kwa wale ambao wanachelewa kulipwa kama penalty na yenyewe pia imeondolewa. Hayo ni mambo makubwa na kama Wabunge tumekuwa tunayapigia kelele kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado kuna changamoto moja kubwa. Tunafahamu kwamba mwaka 2016 Bunge hili lilitunga sheria, lilifanya marekebisho ya Sheria ya Bodi ya Mikopo kutoka asilimia nane kwenda asilimia 15. Changamoto ambayo naiona kwenye hiyo sheria ni kwamba badala ya sheria kuanza kutumika mwaka 2016, imerudi toka watoto walivyaonza kukopeshwa hizo fedha. Matokeo yake, ukiangalia ripoti ya CAG ya mwaka 2016/2017, kwa sababu wao wanafanya sampling, hawakwenda kwa wahusika wote ambao wanatakiwa kulipa. Wanafunzi au wafanyakazi 4,830 wanalipwa mshahara chini ya moja ya tatu, kinyume cha sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria Na. 7 ya mwaka 1970 inasema ni lazima mtumishi yeyote ambaye anafanya kazi, lazima makato yake yasizidi mbili ya tatu ya malipo au pato ghafi ambalo analipwa. Kitendo cha Wizara ya Elimu kushirikiana na Serikali yote kwa ujumla kurudi nyuma zaidi mwaka 2016 imekwenda kuwaathiri wafanyakazi wengi sana. Wapo ambao walikopa kwa sababu wanajua wao wanakatwa asilimia nane, unavyomkata asilimia 15 maana yake ni kwamba unakwenda kuathiri kipato chake na mpango wake mzima wa maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia waraka wa Serikali wa Novemba, 28, 2012, wenye Kumbukumbu Na. CE26/46/01/66 unaelekeza makato ya watumishi yasizidi mbili ya tatu ya mishahara yao ghafi. Kitendo cha Serikali kwenda kuwakata watumishi zaidi ya mwaka ambao sheria imetungwa, kwanza ni kukiuka sheria na kutumia mabavu, kitu ambacho tunadhani siyo sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Rais wetu ni mtu msikivu, ni imani yangu jambo hili litakwenda kupewa kipaumbele na pendekezo langu kwenye jambo hili ni kwamba asilimia 15 ianze kukatwa kuanzia mwaka 2016 na isirudi nyuma ili kuwapa ahueni wafanyakazi wetu. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi naomba nitumie fursa hii kwanza kabisa kushukuru kwa kupata fursa ya kuweza kuchangia Wizara yetu ya Madini. Mimi kwa sababu ya muda nitajielekeza kwenye mambo manne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ni kuhusiana na madini ya tanzanite kuweza kuuzwa kwenye masoko yote ya madini nchini. Hiki kimekuwa ni kilio chetu cha muda mrefu sana. Tunafahamu kwamba tarehe 7 mwezi Julai mwaka 2021 Serikali ilitoa tamko la kuelekeza kuwa madini ya Tanzanite yauzwe kwenye soko moja la Mererani peke yake. Lakini masoko haya ya madini ni masoko ambayo yapo kwa mujibu wa Sheria; na sisi watu wa Arusha tuna bahati moja kubwa sana. Wakati nikiwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha ndugu yangu na rafiki yangu Mheshimiwa Daktari Dotto Biteko alikuja pale Arusha akatuzindulia soko letu la madini, na soko hili limekuwa ni soko lenye mafanikio makubwa sana kwenye nchi hii ya Tanzania lakini cha kushangaza baadaye Serikali hiyo hiyo na chini ya Waziri huyo huyo ikaja na kanuni zilizobadilisha mfumo wa kufanya biashara ya madini hasa biashara ya madini ya tanzanite.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya consultations nyingi na Mheshimiwa Waziri wa Madini kama sekta husika na wadau wote wa masuala ya madini. Kwa pamoja wameona changamoto ambazo zimetokana na matamko hayo ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kimsingi ningependa leo niwape taarifa ifuatayo; kwamba wakati ule Mheshimiwa Waziri alipokuja kuonesha soko la Madini mwaka 2019 kwa mwezi wa saba mpaka wa kumi na mbili 2019 tuliweza kupata madini ya tanzanite yaliyosanifiwa na kung’arishwa karat 76,303 na thamani yake ilikuwa ni bilioni 24. Kodi iliyopatikana Serikalini ilikuwa ni milioni 487. Lakini kwa madini hayo hayo ya tanzanite ambayo yalisanifiwa na kung’arishwa baada ya kuhamishiwa Mererani sasa mwaka 2021kuanzia Januari hadi Disemba tuliweza kuwa na karati 15,820 kutoka karati 76,000. Tuliweza kupata thamani yake ya shilingi bilioni mbili mia sita thelathini na sana kutoka bilioni ishirini na nne, mia tatu na sitini na moja; lakini pia na kodi au ada iliyolipwa ilikuwa milioni 52 kutoka milioni 487.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pia kwenye upande wa madini ya tanzanite ambayo ni ghafi yaliyo chini ya two grams, kwa upande wa soko la Arusha kwa July-December 2019 utakuta karat ambazo zilipatikana zilikuwa ni 7,920,000, thamani yake ilikuwa ni bilioni 12, kodi na ada zilikuwa ni milioni 848, na jumla ya thamani ilikuwa ni bilioni 36 na jumla ya kodi yote ilikuwa ni 1,336,000,000. Kwa upande wa Mererani kuanzia July hadi December 2021 utakuta madini hayo ambayo ni ghafi chini ya gram mbili tulipata shilingi 3,467,000,000 kutoka bilioni 12, lakini pia walipata karat 10,000 kutoka karat 7,920,000,000. Jumla ya mapato yake yalikuja milioni 39 kutoka 1,336,000,000. Tumepata hasara si chini ya asilimia 70. Kwa hiyo vielelezo kama hivi vinaonesha kabisa Serikali inayo sababu, inayo haja na kuna tija kabisa ya kutafakari maamuzi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiacha hasara hiyo bado pia tumeweza kupata hasara kwenye upande wa ajira. Kuna ma-broker pale kati ya 2,500 hadi 3,000 ambao leo wamekosa ajira kwa sababu ya fursa hii ambayo imeondoka kwenda kwenye eneo jingine. Yawezekana Wizara ya Madini kwa data zao ma-broker wakawa ni wachache kwa sababu wengine wengi wameacha kukata leseni kwa sababu mwisho wa siku wameona fursa hiyo imeondoka kwenye eneo hilo. Bado pia kuna majengo ya Serikali ukienda AICC, NSSF, PSSSF nako pia kulikuwa na mashine 437 zimefungwa, ambapo zile mashine leo hazifanyi kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukiangalia na hiyo bado kuna kodi ambayo Serikali ilikuwa inapata kwa kila square meter katika jengo lile. Kwa hiyo, kwa ujumla wake naona maamuzi haya kwa kweli hayana tija na yameitia hasara nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizingatia sizungumziii Arusha tu peke yake, hizi data ni za sehemu moja tu, nenda Mkoa wa Dar es Salaam, nenda Mkoa wa Mwanza, nenda Mbeya, nenda Zanzibar, nenda kwenye masoko ya madini yote nchi nzima utagundua kwamba hasara ni kubwa kupita kiasi na Serikali yetu chini ya Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Serikali ambayo imetoa motisha sana kwa wafanyabiashara. Kwa hiyo ni imani yangu Serikali ya Awamu ya Sita itakwenda kupitia maamuzi haya ili mwisho wa siku tuweze kurejesha furasa hii kwenye masoko yote ya madini nchi nzima ambayo yapo kwa mujibu wa sheria na watu waendelee kunufaika na fursa hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tulikuwa tumeendelea kujenga hoja kwamba siku za nyuma kulikuwa kuna minada ya madini inafanyika, pia kulikuwa kuna maonesho ya madini yalikuwa yanafanyika, hapa katikati yamepotea. Minada ile na maonesho yalikuwa yanasaidia pia kwenye utalii, inaleta wageni wengi kutoka nje ya nchi. Siku za nyuma tulikuwa tunafanyia pale kwenye Hoteli yetu ya Mount Meru, leo kuna hoteli nzuri nyingine ya Melia na Hoteli nyingine nzuri zaidi zimejengwa kwenye mji wetu. Kwa hiyo, fursa ikirudishwa itasaidia kwanza kuleta wageni ambao watalala kwenye mahoteli, watanunua bidhaa mbalimbali na mwisho wa siku fursa zitakuwa ni kubwa zaidi. Kwa hiyo tunaomba Mheshimiwa Waziri wa Madini atusaidie kuhakikisha kwamba maonesho yanarudishwa, minada inarudishwa ili kuongeza fursa mbalimbali katika biashara na maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusiana na changamoto ya wafanyabiashara ya vito, watengenezaji na wauzaji nwa bidhaa za usonara kwa maana ya urembo na dhahabu nchini. Hapa ndio sielewi kabisa, sijui kuna changamoto kubwa kiasi gani. Ukiangalia Sera ya Madini ya mwaka 2009 inasisistiza kuwahamasisha Watanzania na wananchi wote duniani kuweza kuongeza thamani ya madini yetu. Hata hivyo, ukiangalia Sera inavyosema na ukiangalia matakwa ya kisheria yaani ni mbingu na ardhi, ni vitu viwili tofauti kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015, Serikali yetu ilianzisha Mchakato wa Rasimu ya Sheria ya Uongezaji wa Thamani ya Madini, ilikuwa iitwe Mineral Value-Added Act, lakini kabla ya hapo kulikuwa na sheria ambayo Sheria hii kama ingeanzishwa ililenga kufuta ile Sheria ya Gold Smith and Silver Smith Act, CAP 228. Hii Sheria ya nyuma hata sielewi nchi yetu ina changamoto kubwa kiasi gani. Ukiangalia kwenye upande wa biashara ya Usonara. Ili mtu aweze kufanya biashara ya Usonara anahitaji kuwa na leseni tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leseni ya kwanza ni Metallic mineral dealers license, kuna maombi dola 200 na kuna kulipia leseni dola 1000; Kuna Game stone dealers license, kuna maombi dola 200, kulipia leseni dola1000; Kuna Diamond dealers license maombi dola 200, kulipia dealer dola 2000; Gold dealers license maombi dola 200, ada ya leseni dola 1000; na Business license 300,000 unalipia Wizara ya Viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukijumlisha gharama zake zote zinakuja sio chini ya Shilingi Milioni 13. Sasa unajiuliza hivi leseni na yenyewe ni chanzo cha mapato au leseni ni namna ya kumtambua mfanyabiashara aingie kwenye mfumo ili mwisho wa siku sasa Serikali iweze kumtambua, afanye biashara na aweze kulipa kodi. Mwisho wa siku sasa tunajikuta na leseni imekuwa ni chanzo cha mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba ile sheria ambayo ilikuwa inatakiwa kutungwa ya Mineral Value Added Act mchakato wake ambao uliishia mwaka 2016 kwenye kikao cha Makatibu Wakuu, Waziri achukue Sheria hiyo iendelee na mwisho wa siku alete Bungeni hapa tuweze kuhitimisha na Watanzania waweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kumalizia tunalo ombi pia, tunaomba uwepo wa leseni moja ya wafanyabiashara wa madini nchi nzima, ikishindikana kabisa basi watoe angalau kikanda. Leo mtu anaomba leseni akienda Mererani awe na leseni, akienda Arusha aende na leseni, akienda Shinyanga afungue leseni halafu kwenye kila Mkoa TRA wanawaita wale watu kwa ajili ya kuangalia masuala ya kodi na masuala mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbona Mtanzania ana kitambulisho kimoja tu cha NIDA? Kwa nini pia na leseni isiwe moja ila waweke mfumo mzuri kila anapokwenda kufanya biashara kwenye Mkoa fulani aende akaripoti kwa Afisa Madini wa Mkoa huo na mwisho wa siku aweze kuendelea na shughuli zake. Huo urasimu wa kuwa na leseni kila mahali, hauna tija na unawaongezea tu gharama wafanyabiashara lakini pia usumbufu na kuwapa fursa TRA kuendelea kuwachungulia chungulia kwenye masuala mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuhusiana na kodi ya PAYEE na SDL kwa wachimbaji wadogo wa Mererani. Siku za nyuma hili suala lilizungumzwa sana na nadhani lilieleweka, kwa sababu kutokana na nature ya biashara ya madini ukimwambia mchimbaji mdogo wa madini leo alipe PAYEE na SDL …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kwanza kukushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangoia Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapochangia Bajeti ya Serikali, kwanza kabisa huwa tunafanya mapitio ya Bajeti. Vile vile, ukizingatia mwaka wa fedha uliopita tulipitisha Mradi maarufu sana kama Mradi wa TACTIC kwa ajili ya kujenga miradi mbalimbali kwenye miji 12 ambapo Jiji la Arusha ni mji mmojawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikubaliana kwamba tutaanza kujenga Stendi ya Kisasa, eneo la Bondeni City kuanzia Mwezi wa Saba wa mwaka uliopita. Umepita wa saba tumekwenda mpaka Desemba imepita leo tuko mwezi wa Sita tunakaribia kuumaliza, mpaka leo hata tenda haijatangazwa na bado tunazungumzia bajeti ya mwaka unaofuata. Kwa hiyo, ningefurahi kuona majibu ya Serikali kuhusiana na mpango wa ujenzi wa Stendi ya Jiji la Arusha, kitu ambacho Wanaarusha wanakitamani sana kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni kuishulkuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwenye mpango wa kujenga viwanja vya michezo vya Kimataifa kwenye Mikoa miwili, Mkoa wa Dodoma lakini pia na Mkoa wa Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Arusha ni mahali sahihi kwa sababu hii ni sehemu ya kuunga mkono Royal tour lakini pia ni sehemu ya kuchangia kwenye masuala ya Sports tourism. Hii pia ni kazi nzuri ambayo imefanywa na wenzetu wa Wizara ya michezo kupitia Waziri wetu Dkt. Pindi Chana pamoja na Naibu Waziri, Katibu wetu Mkuu Ndugu yangu Yakubu ambao wanafanya kazi kwa ubunifu mkubwa na wa hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumepokea mpango huu katika hali nzuri zaidi na tumekwishatenga ardhi ya kutosha kwenye Kata ya Olmoti, Diwani na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa wa Kata ya Olmoti wako tayari kabisa kwa ajili ya kuupokea mradi huu kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Arusha tuna hoteli nyingi, tuna mazingira mazuri zaidi, hali ya hewa nzuri na nimeambiwa viwanja hivi vitakwenda kujengwa pia maeneo ya basketball, riadha na hasa ukizingatia kwamba Arusha na hasa maeneo ya Karatu ndio wakimbiaji wengi zaidi wanapatikana katika nchi yetu. Kwa hiyo tunaunga mkono jambo hili na ni imani yangu kwamba consultant ambaye nimeambiwa kwamba atapatikana wakati wowote kuanzia mwezi wa Saba kwa maana ya mwaka wa fedha unaoanza mwezi wa Saba, basi kazi hiyo itakwenda kuanza vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kwenye mapitio upande wa madini, tunaishukuru sana Serikali kwa sababu imekubali kurudisha madini ya tanzanite kwenye masoko yote. Tumeambiwa kwamba mpango huo utaanza kuanzia mwaka wa fedha unaokuja mwezi Julai na kuendelea. Vile vile, kuna mawazo hapa ya kuondoa kodi kwenye minada katika maeneo mbalimbali ambayo itafanyika, tunaunga mkono pia jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya salamu hizo za awali, napenda nichangie kwenye masuala yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza, wakati Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan anafanya ziara Mkoa wa Kagera ilikuwa ni tarehe 9/6/2022, alitoa maelekezo kwa TRA kuhakikisha kwamba hawarudi tena kufukunyua masuala ya kodi zaidi ya mwaka mmoja. Tunaona hapa Waziri wa Fedha amekuja na mapendekezo kwenye Finance Bill, lakini suala hili hajalileta kuliingiza kwenye mapendekezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamwomba, ili kumlindia heshima Rais wetu na ili kuendelea kuyatunza maelezo ambayo Mheshimiwa Rais ameyatoa kwenye hadhara, ni vizuri Mheshimiwa Waziri wa Fedha akatuletea hapa kwenye Finance Bill maelekezo haya yakaingia kwenye Sheria ili TRA wasiingie kwenye mtihani wa kuacha kusimamia sheria. Kama ni vizuri zaidi wakaweka utaratibu mzuri zaidi wa kuhakikisha kwamba wanaingiza kwenye sheria hasa kwenye Muswada wa Fedha wa mwaka huu na Wabunge tutawaunga mkono, kwa sababu ni lazima tumuunge mkono Rais wetu anapoonekana kuwajali wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nimefurahi sana kuona Mheshimiwa Waziri amezungumzia kwamba maeneo ya biashara yasifungwe. Nadhani tamko hilo lingeenda mbali zaidi, sio tu maeneo ya wafanyabiashara, lakini pia wanapoacha kufunga biashara wasifunge pia akaunti za wafanyabiashara. Wanapoacha pia kufunga akaunti za wafanyabiashara, waache pia kwenda kuchukua computer za watu, kuchukua simu za watu kwa wafanyabiashara wa maeneo mbalimbali. Watafute mbinu za kisasa za kuweza kukadiria kodi, kukusanya kodi lakini sio kwenda kuwavamia wafanyabiashara kuchukua vifaa vyao kwa kutumia kigezo cha investigation. Kwa hiyo, nadhani hilo nalo Mheshimiwa Waziri wa Fedha atusaidie kulipa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tumeona pia hapa yamekuja mapendekezo ya kuongeza shilingi 100 kwenye mafuta ya petrol na diesel. Hili wazo mimi binafsi sikubaliani nalo, kwa sababu kwanza ukiangalia kwenye mafuta peke yake kuna kodi kama 22. Kuna kodi ya Wharfage, Railway Development levy 1.5 percent ya CIF, Custom Association Fees, Weight and Measure, TBS, TASAC, EWURA, wako wengi na ziko kodi 22.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kwenye hizo kodi 22 bado kuna kodi kiasi cha shilingi 413 tunaita fuel levy. Hii 413 tayari kodi ya barabara imo humu ndani. Ukiangalia kuna 186 kwa ajili ya TANROADS, kuna shilingi 177 kwa ajili ya TARURA, kuna shilingi 50 kwa ajili ya maji. Kwa hiyo, unaona kabisa barabara zimezingatiwa TANROADS, TARURA wamo humu na maji pia yamo. Kuongeza shilingi 100 nyingine ni kuongeza mzigo kwa mwananchi na kumwongezea mzigo Mtanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi, unapoongeza shilingi 100 mfanyabiashara hana shida, yeye anaongeza ule mzigo, halafu anampelekea mwananchi. Daladala zitataka kupanda bei, mabasi yatapandisha bei na gharama nyingine zitaongezeka kwa sababu itakuwa inagusa pia uzalishaji. Ushauri wangu ni kwamba, tutafute eneo lingine, lakini eneo hili ambalo linakwenda kumgusa moja kwa moja mwananchi kama Serikali tuliangalie vizuri zaidi na hasa ukizingatia tuna changamoto kwenye dola yetu, haijawa stable sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mwaka 2018 dola moja ilikuwa ni sawa na Sh.2,276 kwa wastani, leo dola moja ni sawa na Sh.2,398, maana yake ni nini? Mafuta duniani yanauzwa kwa dola na kama yanauzwa kwa dola yanapokuja Tanzania tukiweka kwa shilingi, peak yake kuna ongezeko la Sh.122. Unaona kabisa mzigo wote huu unaokuja anaubeba Mtanzania. Ni vizuri Mheshimiwa Waziri wa Fedha zaidi akaongeza ubunifu zaidi kwenye vyanzo lakini sio vile ambavyo vinakwenda kumuumiza mwananchi na Mtanzania wa kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sambamba pia na kwenye upande wa kupanda kwa bei ya saruji na yenyewe ni vile vile. Tunataka Watanzania wawe na maisha mazuri, tunataka tuondoe nyumba za tembe, lakini mwisho wa siku gharama za ujenzi unaziongeza. Ukiongeza gharama ya cement maana yake umeongeza gharama ya ujenzi na umemnyima uwezo Mtanzania wa kuweza kununua cement nyingi zaidi ili aweze kujenga nyumba nzuri zaidi. Kwa hiyo, ni ushauri wangu kwamba na hili lenyewe kwa sababu linamgusa mwananchi moja kwa moja, Serikali ikalitafakari na itafute ubunifu mwingine kwenye upande wa kodi lakini siyo huu ambao unakwenda moja kwa moja kwa mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kumekuwa na changamoto nyingi sana, Wakandarasi wetu, wazabuni wetu hawalipwi kwa wakati. Leo ukifanya kazi ya Serikali, ukichelewa kumaliza mradi Serikali wanakupiga penalty, lakini Serikali inapompa kazi mzabuni au mkandarasi, ikichelewa kumlipa yenyewe haipigwi penalty. Nafikiri ni vizuri tuweke utaratibu hapa ikiwezekana Serikali pia inapochelewa kumlipa mkandarasi au mzabuni na yenyewe pia iweze kupigwa penalty.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni mbaya zaidi kwa sababu watu wetu hawa wanakopa fedha benki na kule kwenye benki wanapewa riba. Kwa hiyo, kadri wanavyochelewa kulipwa na wao wanachelewa kufanya marejesho, mwisho wa siku wanapata hasara kubwa zaidi. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri atoe tamko kwenye halmashauri zetu, lakini pia na kwenye taasisi zote za umma ambazo zina madeni walipe madeni kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alishasema jambo hili “Mtu yeyote asitangaze tenda kama hana fedha za kulipa”, lakini huko hali ni mbaya. Nenda karibu kila mahali, halmashauri hazilipi, taasisi za umma hazilipi, kuna madeni kila mahali. Tunaomba hili jambo Mheshimiwa Waziri aliweke vizuri kwa sababu tunajua yeye ni Mchumi mbobezi na tunajua kwenye masuala ya uchumi lazima pia uangalie circulation ya watu wako wale ambao wanafanya shughuli mbalimbali za biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwenye upande wa gharama za bando. Bahati nzuri nimesoma computer science undergraduate lakini hata degree yangu ya pili nilisoma masuala ya computer. Katika kitu ambacho tunatakiwa tukiangalie vizuri ni gharama za bando, zimepanda sana. Majibu tunayopewa hayaendani na hali halisi. Unaambiwa sijui zima App hii, unaambiwa fanya hivi, hicho ni kitu kimoja kitakupunguzia matumizi, lakini hapa tunachokisema ukiangalia data zetu sisi kwa wastani, kwa mfano mwaka 2020, ulikuwa ukinunua data za 15,000 kwa wiki, ulikuwa unapata wastani wa GB 10. Leo 15,000 hiyo hiyo kwa upande wa Vodacom unapata GB 7.38, ukienda Tigo unapata GB 7.2, ukienda Airtel unapata GB 7.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa unaona kabisa imetoka kwenye 10, hawajaongeza bei lakini wamepunguza bando, kwa maana nyingine pia wameongeza bei. Kwa maana ya kwamba ukiangalia kipindi hicho GB moja ilikuwa ni wastani wa shilingi 1500 ambapo GB 10 ilikuwa ni shilingi 15,000. Leo hii GB moja kwa upande wa Vodacom peke yao unapata kwa shilingi 2,054 kwa hiyo hapa wameongeza shilingi 554. Ukienda Airtel wameongeza shilingi 583, ukienda Tigo wameongeza shilingi 583. Kwa hiyo, gharama za bando zimeongezeka na ndio maana watoto wetu wakipewa assignment kule mashuleni ukimwekea bundle la 5,000 akitumia kidogo tu limekwisha. Kwa hiyo, linaongeza gharama za maisha, inaongeza gharama za shule na inapunguza pia ubunifu wa watu wetu kuendelea kudadisi masuala mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Waziri na nimwombe kaka yangu Mheshimiwa Nape Nauye, ni vizuri ili suala wakaliangalie vizuri. Nafahamu uzalendo wa Mheshimiwa Waziri, ni vizuri wakakae na wenzetu wa TCRA, mitandao ya simu waangalie namna ya ku–review data hizi na tusiambiwe kwamba mbona kule duniani gharama ni ndogo. Dunia ni dunia na Tanzania ni Tanzania, tuizungumzie Tanzania yetu ambayo ni bora na ya kipekee, haifanani na nchi nyingine yoyote duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nadhani niliseme ni kwenye upande wa kodi ya majengo. Nimeona hapa Mheshimiwa Waziri amekuja na mapendekezo anataka kodi ya majengo turudi tulikotoka. Maana zamani ulikuwa unafanyiwa uthamini inajulikana value ya jengo halafu unalipa. Gharama zilikuwa ni kubwa, rushwa zilikuwa nyingi, Mthamini akija pale jengo la bilioni mbili ukiongea naye vizuri anakwambia milioni 800. Kwa hiyo wanaweka mianya ya rushwa. Baadaye Serikali hii hii ikaja na utaratibu kwamba, badala ya kwenda kwenye masuala ya uthamini, basi tuweke utaratibu wa kuangalia kama ni nyumba ya chini walisema shilingi 10,000. Kama ni ghorofa kila floor walisema ni shilingi 50,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wameona hizo fedha ni ndogo ni bora wakae chini waangalie badala ya shilingi 10,000 iwe angalau ni Sh.15,000 na badala ya shilingi 50,000 kwa kila floor ya ghorofa basi angalau iwe shilingi 80,0000 au shilingi 100,000, lakini wakianza masuala ya evaluation, maana wametuambia kwenye maelezo yao wataanza 2026. Sisi tunafahamu hii Serikali, leo wameanza wamechokoza kidogo, ukienda mbele unasema kuanzia Januari utekelezaji utaanza. Kwa hiyo unakuwa na statement ambazo mwisho wa siku unashindwa kujua uisimamie ipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri, badala ya kuja na mambo ya uthamini, kwanza yatawapa gharama kubwa, wataalam walio nao ni wachache na wataongeza pia mianya ya rushwa. Tutafute namna nyingine kama wanaona hiki ni chanzo kizuri cha mapato, basi tuongeze pale kidogo, lakini tusiende kwenye uthamini kwa sababu watawakatisha Watanzania kujenga nyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu ana nyumba yake ya ghorofa 10 anamkopo wa kulipa miaka 30 au 40 halafu mkopo hajamaliza, bado Serikali inakuja kumwambia kwamba pengine tumefanya uthamini na kodi ya majengo utalipa asilimia fulani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri kwa sababu namfahamu kuwa ni mchumi mbobezi, daktari na amefanya kazi pia BOT, ni mtu ambaye ana uzoefu wa kutosha pamoja na Naibu Waziri wake na Katibu Mkuu watakwenda kuliangalia, kwa sababu hili wameleta kama pendekezo sio sheria wala sio taratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo hili kwa ushauri wangu ni kwamba ni pendekezo ambalo linahitaji kuangaliwa kwa kina…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, muda wako umekwisha.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, uliahidi kuniongeza dakika mbili sijui bado zipo au umeghairi?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, muda wako umekwisha.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru sana kupata nafasi ya kuweza kuchangia kwenye Bajeti Kuu ya Serikali na nitajielekeza kwenye maeneo matatu, kwenye upande wa maduka ya kubadilisha fedha, kubana matumizi ya Serikali na Tanzanite.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, BOT ina double standard, tunafahamu kwamba kwa muda mrefu imekuwa inapuuza maelekezo ya Serikali. Tumemsikia Waziri wa Fedha kupitia Bajeti ya Wizara ya Fedha ameonyesha umuhimu wa maduka haya ya kubadilisha fedha hasa kutokana na kazi nzuri aliyoifanya Rais wetu kwenye sekta ya utalii. Kuna Kampuni inaitwa Kadoo Bureau De Change inafanya kazi zake Dar es Salaam na Arusha imepewa kibali na BOT, pia kampuni nyingine nyingi zenye sifa zilizoko Arusha zimenyimwa leseni na BOT kwa sababu ambazo hazieleweki na vigezo wameshakidhi, inaonekana kwamba huyu mwenye hii Kampuni wa maslahi naye ndiyo maana wamemuachi na kuzuia wengine ili aweze kufanya biashara peke yake. Tunadhani hili jambo siyo sawa na siyo jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Rais ametoa malekezo akiwa Kagera, kwamba wenzetu wa TRA wanapofuatilia kodi wasiende miaka zaidi ya miwili, lakini kwenye hawa wetu Bureau bado wanakwenda kuwauliza taarifa za mwaka 2015 mpaka 2016 ili tu kuwatafutia sababu na mwisho wa siku wawanyime fursa hiyo ya kufanya biashara kama wenzao wanavyofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi utalii umeongezeka hoteli zimejaa mpaka mwezi Desemba na kuendelea, Ndege nyingi zinaingia usiku tunategemea watalii wanapofika wasipate changamoto ya kubadilisha fedha. Kwa sababu ukileta urasimu wa namna hii mnasababisha pia wakati mwingine kuwa na black market katika maeneo mbalimbali, badala ya ku-change fedha kwenye maeneo rasmi wana-change kwenye maeneo binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia changamoto nyingine kubwa katika jambo hili ambalo tunaomba BOT waliangalie ukiritimba nao ni mkubwa sana. Unapokwenda Benki kwenda kubadilisha fedha ni tofauti na kwenye Bureau wanataka wajue je unayo akaunti, je kama hauna akaunti umetoka wapi na maswali mengine mengi, lakini ukienda kwenye Bureau taratibu zinakuwa rahisi zaidi. Tunaomba BOT waache urasimu, kama wana watu wao wanawataka wawape lakini pia na Watanzania wengine wenye sifa wapewe kama watu wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kuhusu kubana matumizi ya Serikali. Kwanza naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na kwa usimamizi wako Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yako yote, kwenye kuhakikisha magari ya Serikali kwa kiwango kikubwa mnakwenda kuyadhibiti kwa sababu ni kweli gharama zimekuwa kubwa. Lakini kuna eneo jingine pia naomba tuliangalie, angalia kwenye Halmashauri zetu, ukienda Halmashauri za Dar es Salaam, Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam mapato yao ya jumla makisio yao ni bilioni 81, lakini mapato yasiyolindwa ni bilioni 62.2 ukichukua asilimia 70 ambayo inatakiwa iende kwenye maendeleo ni sawasawa na bilioni 43.587, lakini other charges, yale matumizi ya kawaida posho, kaweka mafuta kafanya hivi ni Bilioni 18 kwa Halmashauri moja kwa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Halmashauri kama ya Dodoma makisio yao ni Bilioni 55, mapato yasiyolindwa ni bilioni 44, ukichukua asilimia 60 ni bilioni 26, other charges matumizi yale ya kawaida ya kila siku ni kama bilioni 17. Ukichukua Halmashauri ya Kinondoni hivyo hivyo bilioni 57 ya asilimia 46, maendeleo 32, matumizi ya kawaida bilioni 14. Ukienda Jiji la Arusha mapato yetu ni bilioni 30 makisio, mapato yasiyolindwa bilioni 24, asilimia 70 kwenye maendeleo ni bilioni 17, matumizi ya kawaida ni bilioni saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona mfano mmoja Jiji la Arusha kwa mapato haya ya Bilioni Saba tu wameweza kuingiziana fedha kwenye akaunti binafsi, tumeona aliyekuwa Mkurugenzi wakati huo Ndugu John Pima kachukua milioni 103, kamuingizia Mchumi Innocent Maduhu milioni 103 kwenye akaunti yake binafsi. Mchumi kachukua milioni 25 kaenda kununua gari Subaru kwa matumizi yake binafsi na ushahidi upo. Mkurugenzi kachukua fedha kamuingizia kijana anaitwa Ndugu Alex milioni 65, mwingine milioni 65, unaona hizi fedha ambazo mnazijazia hizi Halmashauri na hizi asilimia zenu zinakwenda kunufaisha watu na siyo kunufaisha wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba tunaomba Wizara ya Fedha wakae na TAMISEMI badala ya kusema waangalie asilimia waangalie matumizi halisi. Ukichukua hizi bilioni 18 za Halmashauri ya Dar es Salaam ni sawasawa na ukichukua Halmashauri ndogo 14, ukichukua Halmashauri ya Mbulu, Halmashauri ya Gairo, Halmashauri ya Butiama, Halmashauri ya Rorya, Kigoma, Kakonko, Buhigwe, Nsimbo, Bumbuli, Mbogwe, Mlele, Momba, Madaba na Halmashauri ya Ileje. Halmashauri 14 hizi matumizi yao ya kawaida kwa mwaka mzima ni bilioni 9.9. Matumizi yao ya kawaida kwa miaka miwili ndiyo matumizi ya Jiji la Dar es Salaam ya kuweka mafuta, kulipana posho na masuala mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani hapa kuna haja ya Serikali kwenda kuangalia kazi nzuri kwenye magari lakini turudi pia kwenye matumizi ya kwenye Halmashauri zetu. Rais anafanya kazi kubwa sana, anakwenda kutafuta hela Dunia nzima, anabana matumizi kila mahali, lakini Waziri wa TAMISEMI na Waziri wa Fedha msaidieni Rais kupitia matumizi haya ya Halmashauri zetu ili tuweze mwisho wa siku kupata fedha za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasi Arusha hapa kwa nilivyoangalia wanavyo kulakula hawa wakipewa hata Bilioni Tatu, Nne zinawatosha, hii Bilioni Tatu nyingine au Nne zinazobaki tuende tukajenge barabara kwa sababu changamoto ya barabara ni kubwa sana, tukanunue vifaa kwenye Vituo vya Afya na tukapeleke huduma mbalimbali kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, nilikuwa naomba pia kutoa mchango wa mawazo kwenye eneo hilo na ni imani yangu kwamba wenzetu wa TAMISEMI watatusaidia. Kwa sababu hizi hela zinaliwa sana nikitaka niseme mnyororo mzima hapa wa namna ambavyo hizi hela za Arusha zilivyoliwa na zilivyogawana hapa ndani kuna wengine tutapoteana kwa sababu changamoto ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la tatu ni kuhusiana na Madini ya Tanzanite. Hili jambo nimekuwa nalisema kila siku na kila nikilisema nadhani sieleweki. Watu wa Arusha hatukatai madini ya Tanzanite kuuzwa Mererani kwa sababu Mererani ndiyo yanakochimbwa. Tunachokisema sisi yakishachimbwa yale madini kwa sababu lengo la kujenga ule ukuta ni kuzuia utoroshaji, yakishichimbwa na Serikali iko pale na vyombo vyote viko pale waangalie kodi zote za Serikali ambazo mwekezaji anatakiwa kuzilipa, kwa sababu akishalipa anaruhusiwa kusafirisha haya madini kupeleka kote Duniani. Akitaka kupeleka India anapeleka, akitaka kupeleka Marekani anapeleka na sehemu nyingine zote, lakini eti haruhusiwi akishalipa tozo zote kupeleka Arusha, kupeleka Dar es Salaam, kupeleka Mwanza, kupeleka na Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanachokifanya wafanyabiashara anakwenda pale Mererani anachimba madini yake, anapata vibali vyote, anafungua Ofisi yake Dubai, anafungua Ofisi yake India, anafungua Ofisi yake Kenya, anasafirisha madini anakwenda kuyachakata kule halafu anakuja kwenye border zetu anayapitisha kuja kuyauza Arusha na maeneo mengine. Sasa tunayafanya haya kwa kumunufaisha nani? Sisi hatukatai mambo haya kupelekwa Mererani lakini tuangalie mtu akishalipa kodi kama anaruhusiwa kupeleka India kwa nini haruhusiwi kupeleka Arusha, kupeleka Dar es Salaam, kupeleka Mwanza, Zanzibar na maeneo mengine? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi wakati huu wa utalii, watalii ni wengi sana mtu anakuja amekwenda kuangalia Pundamilia, kaangalia Simba na wanyama wengine, akitaka kurudi nyumbani anataka arudi na zawadi, anakwenda kununua Tanzanite kama zawadi anapeleka kwa ndugu zake kule nchi alikotoka. Leo haruhusiwi kufanya kitu cha namna hiyo! Kwa hiyo, naomba Wizara ya Madini waliangalie jambo hili kwa uzito unaostahili, kwa sababu kwa kweli changamoto hii ni kubwa na mambo haya yanahitaji uzalendo wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa fursa hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nitumie fursa hii kukushukuru sana kwa kunipatia nafasi ili na mimi kama Mbunge niweze kutoa mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, mimi nitajielekeza kwenye mambo mawili. La kwanza tunafahamu kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu leo amewasilisha taarifa yake na kwenye taarifa hiyo ameomba aidhinishiwe fedha kiasi cha Shilingi Bilioni 116,784,244.

Mheshimiwa Spika, tutakumbuka hivi karibuni Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan aliweza kutoa hotuba elekezi wakati anawaapisha Makatibu Wakuu; hotuba ambayo ilikwenda kukonga nyoyo za Watanzania. Hotuba ambayo ilikwenda kutoa matumaini kwa wawekezaji, hotuba ambayo ilitoa matumaini kwa watanzania wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaenda kwenye hoja yangu ya msingi nataka nikumbushe yafuatayo. Tumekuwa na awamu tano na leo tuna awamu ya sita, na utamaduni wetu kama Taifa tumekuwa kila awamu tumeipa nafasi na heshima inayostahili ili iweze kuongoza nchi. Wakati wa Rais Nyerere tulizungumza masuala yanayohusiana na Rais Nyerere wakati wa Rais Mwinyi tulimpa fursa Rais Mwinyi, wakati wa Rais Mkapa, wakati wa Rais Kikwete, wakati wa Hayati Rais Magufuli na sasa tuna awamu ya sita ya Rais Samia Suluhu Hassan lazima tumpe credit anazostahili, lazima tumuunge mkono lazima tutengeneze mambo humu ndani ya kisheria ili yakarahisishe utekelezaji wa mambo kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nilikuwa nataka niweke wazi, kwamba lazima Wabunge tukubali kwamba tupo awamu ya sita, na ni vizuri sasa tukaweka mtiririko wa kujenga hoja zetu za kumsaidia Rais wetu kuongoza Taifa.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili kwenye kipengele hicho; sisi mpinzani wetu si vyama vya siasa, mpinzani wetu ni changamoto za Watanzania. Leo ukizungumza watumishi wanamanung’uniko kuhusu mishahara yao na kupanda madaraja; kwa miaka mitano hawajapanda madaraja. Leo ukizungumza kuhusu bodi ya mkopo unaona sheria ilikuwa inasema asilimia nane baadaye imekwenda asilimia 15 na kibaya zaidi sheria zote zinazotungwa huwa zinaanzia pale. Sheria yetu ilirudi mpaka nyuma. Watumishi kule wanalia, watu waliosoma vyuo wanalia, lakini hayo mambo yamepitishwa ndani ya Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia pia tuna changamoto kwenye bima afya, tuna changamoto pia kwenye ajira, manung’uniko ni makubwa. Kwahiyo, kazi ya Bunge hili ni kurekebisha sheria kutoa mapendekezo na ushauri ambao Serikali ikiufanyia kazi matumaini yataendelea kudumu kule kwa Watanzania. (makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo; mimi naona hotuba ya Rais wetu Samia Suluhu Hassan tukiifanyia kazi itatusaidi sana kuirahisishia kazi Serikali kwenye masuala mbalimbali. Utaona kila Waziri atakayekuja hapa baada ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, wote watasema mambo yao lakini hatimaye wataomba kuidhinishiwa fedha; hizo fedha zinatoka wapi kama hatukutengeneza mazingira mazuri ya kupata fedha hizo?

Mheshimiwa Spika, mimi nitatoa mapendekezo yangu kwenye sheria nne. Tuna Sheria ya Kazi, Sheria ya Uhamiaji Sheria ya Uwekezaji na tuna Sheria ya Kodi; ziko nyingi, lakini kwasababu muda ni mchache mimi nitazungumzia hizo sheria nne.

Mheshimiwa Spika, ukienda kuangalia sheria ya kazi kwenye Kanuni Kifungu 9(d) tunaambiwa the Employer has provided sufficient evidence from recognize job such mechanism that has been unable to fulfill the particular post due to lack of qualified personnel in the Tanzania labour market. Lakini ukiangalia kanuni hiyo hiyo ya tisa kifungu (9)(2)(d) inasema in the event bulk requitement work permit maybe granted at a ratio of ten local employees to one none citizen employee.

Mheshimiwa Spika, lakini ukienda kwenye sheria hiyo hiyo la labour inakwambia kwamba mwekezaji anapokuja kuwekeza Tanzania atapewa kibali kwa miaka mitano, kama mtaji wake una umuhimu na mkubwa anaweza kwenda hata zaidi ya kumi. Sasa unajiuliza huyu mwekezaji unampa kibali cha kazi mwajiri wake ni nani? na mtu amekuja kuwekeza na yeye pia atakuja kuajiri watu?

Mheshimiwa Spika, ukienda Zanzibar tu hapo wanayo sheria hiyo hiyo pia kama ya kwetu, lakini wao mwekezaji anapata Residential Permit hapati work permit, lakini ukija Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kitu ni kingine.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia pia sheria ya uwekezaji kifungu cha 24 (1) tunaambiwa 24_(1). Every business enterprise granted a certificate of incentives under this act shall be in tinted to an initial automatic in may grand quarter of up to five persons during the startup period.

Ukitaka kuanzisha biashara utapewa watu watano lakini ukiangalia pia sheria ya Uhamiaji kifungu cha; 18 (2) nakuambia 18_2 Resident’s permit shall be issued for any period not exceed three years and may be renewed for any period not exceeding two years by any endorsement of renew endorsed on it by the director but so that the total period of the validity of the original permit and its news shall not in any case exit five year.

Mheshimiwa Spika, ukisoma hivi sheria tatu hazizungumzi utafikiri kila sheria ina nchi yake, sheria ya uwekezaji inakwambia sisi tunakupa incentives ukija kuwekeza Tanzania tutakupa wageni watano, ukienda sheria ya kazi inakwambia sisi ukija kuajiri Tanzania kila ukiajiri 10 tutakupa mgeni mmoja, ukiangalia sheria hiyo hiyo pia labour Kamishna anaambiwa huyo mgeni atakubalika kama hakuna Mtanzania mwenye sifa. Ukiangalia hizi sheria kama vile kila sheria na nchi yake, kila sheria ina dini yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia nchi kama Kenya leo ukienda pale na Dola yako 100,000 unaruhusiwa pale kufanya uwekezaji na unapata vibali bila urasimu wa aina yoyote, ukienda nchi kama Dubai same case ukienda nchi kama Canada ukipeleka tu Dola 750,000 unapewa kabisa na unaruhusiwa kabisa kukaa permanently, ukienda Uturuki ukinunua nyumba tu kiasi cha Dola 200,000 unarahisishiwa kazi unafanya shughuli zako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hakuna kazi ngumu kama kufanya biashara katika nchi ya Tanzania. Tumepata bahati, tumepata Rais mwenye maono, tumepata Rais ambaye amekubali kuwa open minded, tumepata Rais ambaye amewapa nafasi Waheshimiwa Mawaziri mlioteuliwa ili muweze kuja hapa na mapendekezo ya kisheria ili tuweze kufanya harmonization ya sheria zetu, tuwe na sheria moja; mwekezaji asizurure.

Mheshimiwa Spika, mtu kama Dangote kwa mfano kawekeza kiwanda kikubwa sana kule kusini leo akitaka kuja mfano Tanzania eti na yeye pia unamwambia aombe work permit, ili iweje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naangalia malalamiko na manung’uniko mengi tunayoyapata nje ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, ninakupa mfano. Mimi nilivyokuwa Mkuu wa Mkoa, na ndiyo maana nikagombea Ubunge, kila kitu ninachokiona nikitaka kuingilia kati wananiambia hapana hiyo ni sheria. Sasa ukishakuwa Mkuu wa Mkoa kazi yako ni kusimamia sheria huna uwezo wa kutoa ushauri ndani ya Bunge ya namna ya kubadili sheria.

Mheshimiwa Spika, nikasema nimepata bahati na fursa ya upendeleo kwa Mwenyezi Mungu ya kuingia humu ndani nitoe mchango wangu na maoni yangu. Niombe Bunge lako Tukufu lichukulie very serious jambo hili ili tuweze kubadilisha na kurekebisha sheria zetu. (makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwanini nimesema hayo, hapa Serikali ilikuja kuahidi hapa kwenye hotuba ya Rais kwamba tutatoa ajira milioni nane. Ukizungumzia kutoa ajira milioni nane maana yake unazungumzia kila mwaka utatoa ajira milioni 1,600,000, Serikali yetu watumishi wake wa Umma toka uhuru mpaka leo hawajawahi kuzidi 600,000 na mishahara wanayolipwa kwa mwezi ni milioni 660 sasa unajiuliza kama toka uhuru kwa miaka zaidi ya 50 tunaajiri watu 600,000 tutafikiaje target hii ya Milioni nane.

Mheshimiwa Spika, kwa maoni yangu ili tufikie target hii lazima tuweke msukumo na nguvu kubwa sana kwenye private sector. Lazima twende tukafanyie kazi changamoto zote ambazo zimesemwa kwenye private sector humu Wabunge kila siku tumekuwa tunalalamika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika zako zimekwisha ninakupa dakika mbili umalizie.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nilikuwa nasisitiza kwamba tunahitaji kuweka nguvu kubwa sana kwenye private sector, tunahitaji kufanya harmonization ya sheria zetu, tunahitaji pia kujiuliza hivi leo kwanini mtu anamaliza degree anaendesha boda boda? Leo tunatakiwa tujiulize kwanini mwekezaji anang’ang’ania kuja na wageni kutoka nje ilhali Watanzania hapa wapo? na akija pale atamlipa fedha nyingi atamlipia vibali pamoja na changamoto zote, lakini kwanini bado anamuhitaji?

Mheshimiwa Spika, hitimisho langu, naomba Watanzania watuelewe, tunaposema wawekezaji wapewe vipaumbele hatuna maana ya kunyima ajira za Watanzania. Tunasema wapewe vipaumbele kwa sababu tunafahamu kama tukisema mwekezaji ratio yetu ni 1:10 basi anapoajiri watu 10 maana yake 9 watakuwa ni Watanzania au anapoajiri mgeni mmoja 10 watakuwa ni Watanzania. Kwa hiyo, tutakuja na mapendekezo ya sheria ambayo yatawalinda Watanzania lakini pia yatampa amani mwekezaji ili ajira ziongezeke na changamoto iweze kuondoka. (Makofi)

Mheshimwia Spika, la mwisho kabisa sababu muda ni mdogo, sisi Arusha pale tuna kiwanda cha General Tyre kwenye jitihada hizi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa
Mzungumzaji)

SPIKA: Bahati mbaya muda hauko upande wako Mheshimiwa.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nijitahidi kuwa very honest. Nawashukuru sana wenzetu wa Wizara ya Ujenzi kwa maana ya Wizara ya Uchukuzi na TANROADS kupitia Engineer Mfugale na Meneja wetu pale wa Mkoa wa Arusha, Eng. Kalupale, wanafanya kazi kubwa na kazi nzuri sana hasa kwenye Jimbo letu la Arusha mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utakumbuka kwamba, Jimbo la Arusha Mjini tulipata bahati ya kuwa na barabara ya mzunguko ile ya Arusha bypass, tunaiita ya kilometa 42.4, lakini pia tulipata barabara ya Sakina - Tengeru ya Kilometa 14.1. Barabara hizi ni nzuri sana kwa sababu kupitia barabara hizi kwa mara ya kwanza ndiyo tumeweza kuwa na barabara za njia nne katika Mji wa Kimataifa wa Arusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto iliyokuwepo, tunajua phase ya kwanza mmejenga barabara lakini mmetoa baadhi ya matoleo ambayo yanachukua maji kutoka Wilaya ya Arumeru yanawapeleka kwa wananchi, kiasi ambacho barabara kila mwaka zinaharibika. Ombi langu ni kwamba, kwa sababu tunayo mito kwenye maeneo hayo; tuna Mto Nduruma, Mto Ngarenaro, Mto Balaa na Mto Naura, tulikuwa tunaomba sasa phase inayofuata, waisaidie TANROADS kuyazuia yale maji na kuyaelekeza kwenye mito ili yasiweze kuharibu barabara za kawaida na kuwapa changamoto kubwa zaidi wenzao wa TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ambazo zinaathirika sana na changamoto hii, tuna Kata 12; Kata ya Sakina, Kata ya Sekei, Kata ya Balaa, Kata ya Levolesi, Kata Kaloleni, Kata ya Ngarenaro, Kata ya Kimandolu, Mushono, Ololien, Sombetini, Osunyai na Unga Limited; karibu nusu ya kata zote za Jiji la Arusha. Ni imani yangu kwamba TANROADS kupitia ujenzi wa barabara mpya ile ya kutoka Arusha Airport na ile barabara ya Arusha Kisongo ambayo na yenyewe ni ya njia nne, watakwenda kujenga mitaro ambayo itaweza kuya- tap yale maji na kuyapeleka kwenye mito ili wananchi wa Kata ya Sombetini Osunyai na Unga Limited wasipate hivyo changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kwenye uwanja wetu wa ndege wa Arusha Airport, pale TANROADS na kushirikiana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, wamefanya kazi kubwa na nzuri sana. Kuna barabara pale za kisasa zimejengwa na mazingira yamekuwa ni mazuri sana. Changamoto kubwa tuliyokuwa nayo sasa hivi ni changamoto ambayo inahusiana na majengo yaliyoko pale; majengo kama ya abiria wale wanaoingia na wanaotoka, restaurant za kisasa, maeneo ya kununua zawadi mbalimbali ili yafanane na mandhari ya Mji wa Arusha na masuala yaweze kuwa vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni Imani yangu kuwa Mheshimiwa Waziri na timu yake watakwenda kwenye phase II kutuwekea utaratibu mzuri zaidi ili maeneo yale yaweze kuwa mazuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la tatu, pale tunao madereva taxi, madereva taxi wale kwao hii ni fursa, wamekuwa pale kwa muda mrefu, wengine wako toka mwaka 1998, lakini ukiangalia lakini ukiangalia sasa hivi wenzetu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege wamekuja na utaratibu wa kusema wanataka kuongeza mapato eti wanataka watangaze tenda ili wawapate watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani badala ya kutangaza tenda wangekaa na wale ambao walikuwa pale kwa muda mrefu kwa sababu ile kwao ni fursa na ni ajira pia ili mwisho wa siku waweze kuangalia utaratibu mzuri zaidi wa kuweka mazingira mazuri zaidi ili walewale waliokuwepo waweze kuendelea. Vinginevyo watakuja watu wengine ambao wana uwezo zaidi, watatenda kwa juu zaidi halafu wale watu ambao wako kwa muda mrefu na ni watu ambao ni wanyonge watakosa hiyo fursa. Ni imani yangu kuwa Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake watakwenda kulipa jambo hili kipaumbele ili Watanzania wanaopata riziki zao pale waweze kuwepo na waweze kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la nne ni kwamba tuna barabara yetu ya Tipekazi - Losinyai ambayo yenyewe imewekwa kwenye mzunguko ule wa kawaida wa barabara ya Arusha – Kibaya - Kongwa ambayo ni ya kilometa 430. Ile barabara ni kubwa sana inawezekana ujenzi wake ukawa ni wa muda mrefu.

Mheshimiwa NaibU Spika, tuna ombi maalum, tunaomba pale kwenye Kata ya Mwishono kuna kipande kidogo sana kilometa ambazo hazizidi saba kutoka kona ya Kiseriani mpaka kwenda kwenye eneo la By pass ambapo barabara hiyo ikijengwa itatusaidia kuondoa msongamano katika Jiji la Arusha lakini pia na watalii wakiingia mjini watakuwa na route nyingi zaidi za kutuletea dola katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu pia tunayo changamoto ya corona katika nchi yetu. Ni imani yangu wale wafanyakazi sasa wa Mamlaka za Viwanja vya Ndege mara baada ya ripoti ya jana, ya timu ambayo imeundwa na Mheshimiwa Rais wataanza kuvaa sasa zile barakoa na vifaa vingine vyote ambavyo vitairejesha dunia kwamba Tanzania tuko makini na jambo hilo, ili watalii waje wengi zaidi tuendelee kupata dola na miradi hii ambayo tunaililia leo hapa iweze kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba nishukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuchangia Wizara ya Maliasili na Utalii na hasa ukizingatia kwamba, utalii upo Kaskazini. Karibu asilimia 80 ya mapato yote ya utalii yanatoka Kanda ya Kaskazini; na huwezi kuzungumza Kaskazini bila kuizungumza Arusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda nitajielekeza kwenye masuala machache. La kwanza, tunafahamu sote kwamba Corona imetuathiri sana kama Tanzania. Nilikuwa nasikia taarifa ya Waziri kwenye ukurasa wake wa saba na wa nane bado anazungumzia kwamba utalii unachangia pato la Taifa kwa asilimia 17 na unachangia fedha za kigeni kwa asilimia 25. Nadhani hizi taarifa ni za zamani sana kwa sababu kwa namna Corona ilivyotuathiri, mapato yetu yameyumba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia taarifa zilizopo, kwa mujibu wa taarifa ya Wizara, TANAPA mpaka kufikia mwezi Februari, walikusanya asilimia 13, Ngorongoro asilimia 21 na TAWA asilimia 38. Ukiangalia pia taarifa ya Mheshimiwa Waziri ya leo kwenye ukurasa wake wa 10 na wa 11 anatuambia hadi kufikia mwezi wa Nne target yetu ilikuwa ni shilingi bilioni 584 na sisi tumekusanya shilingi bilioni 89 ambayo ni sawa sawa na asilimia 15, lakini ukienda kuangalia pia kwenye World Tourism Organization, tunaambiwa kwamba mchango wa utalii kwenye GDP umeshuka kutoka asilimia 17.5 mpaka asilimia 11.7.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kushangaza, bado Wizara ya Utalii wanakwenda kuongeza tozo kwenye maeneo mbalimbali. Tukiangalia nchi zote za Afrika Mashariki; Uganda wamepunguza park fees kwa asilimia 50, Kenya wamepunguza park fees kwa asilimia 47, lakini Tanzania tunaongeza. Vilevile cha kushangaza, ukiangalia dunia nzima sasa hivi inahangaika kwenye kutoa ahueni kwenye sekta ya utalii, lakini Tanzania tunaongeza tozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninalo tangazo hapa la TANAPA ambalo limetokana na GN ya Serikali ya tarehe 29 Juni, 2020 ambalo wanaongeza kipindi cha High Season tozo kutoka dola 60 mpaka dola 70 ambazo bado hazijaanza, wanategemea zianze tarehe mosi mwezi wa Saba, yaani mwaka wa fedha unaokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ukiangalia TANAPA hao hao kuna tozo nyingine ambayo pia wanakuja kuiongeza; ni tozo mpya hii, wanaita Land Base, Land Fee; yaani mtu amewekeza kwenye hifadhi zetu mfano Serengeti au maeneo mengine, analipa Concession Fee, kila mgeni aliyelala pale analipa dola 50. Leo TANAPA wanakuja wanaongeza pia, inabidi mtu anayeweka kule kama ni Seasonal Camp inabidi alipe dola 2,000, kama anaweka Permanent Tented Camp alipe dola 20,000, kama ana lodge yake, alipe dola 50,000. Kwa hiyo, unashindwa kuelewa tatizo letu ni nini? Kila tukikaa tunafikiria kuongeza tozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua tatizo hili lipo TANAPA kwa sababu tunazo hifadhi 22 ambazo ziko chini ya TANAPA. Hifadhi ambazo zina uwezo wa kujiendesha hazizidi tano, hifadhi nyingine zote zinategemea hifadhi tano ziweze kujiendesha. Matokeo yake sasa kila wakilala wakiamka wanaongeza tozo Serengeti, wanaongeza tozo na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa nadhani kwamba ni vizuri Serikali ikaiona changamoto hii ya Corona kwa uzito wake na kuangalia uwezekano wa kukaa vizuri na wenzetu wa TANAPA ili wasiweze kuongeza sana tozo kama ambavyo wanafanya. Mambo unayoyaona haya hayapo maeneo kama NCAA, wao mambo haya ya Land Base hayapo, lakini ukienda TANAPA kule unaweza ukayakuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naona bado tuna kazi ya kufanya, Wizara ya Utalii ipitie hifadhi zote ambazo tunazo. Hifadhi ambazo hazizalishi, mfano mzuri ni Burigi Chato, hebu mtuletee taarifa hapa, ile hifadhi toka imeanzishwa imepokea wageni wangapi? Imeingiza kiasi gani? Mwisho wa siku pia inatumia gharama kiasi gani? Siyo tunaanzisha hifadhi nyingi, tunaajiri watu wengi, tunapeleka gharama nyingi, halafu mwisho wa siku tunakwenda kuumiza utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima mfahamu kwamba hizi gharama mnazoongeza, anayepewa hizi gharama ni mtalii. Ukimpa tour operator, anachokifanya yeye, anaingiza kwenye gharama zake, mtalii anayekuja anaongezewa gharama na kufanya destination inakuwa very expensive, kwa hiyo, nilikuwa nadhani ni vizuri tukaliangalia vizuri suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine pia ambalo nataka nilizungumzie ni kuhusiana na gharama za kupima Corona. Ukienda Kenya kupima Corona ni dola 30 hospitali za Serikali, private dola 50 ukija Tanzania dola 100. Sasa nashindwa kuelewa, hivi hata Corona pia ni fursa kwenye nchi yetu au ni changamoto!

Kwa hiyo, nilikuwa nadhani na lenyewe pia tuliangalie vizuri, kwa sababu Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kafanya kazi kubwa na nzuri sana kuhakikisha kwamba tunakubaliana na dunia kwamba Corona ipo, tutachukua chanjo. Sasa hivi dunia imeanza kuelewa na tunaamini muda siyo mrefu tutaanza kupata wageni wengi zaidi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najiuliza pia, kwa nini Tanzania tuna kituo kimoja tu cha kupimia Corona, pale Dar es Salaam? Ukienda kwenye airport, sawa, wanachukua zile rapid test; ukienda Kenya wana vituo 47. Nadhani ni vizuri mambo haya tukayaangalia vizuri zaidi. Naona muda ni mdogo sana na hizi mada ni very serious…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Imeshagonga kengele ya pili.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia nzima inatafuta ahueni kwenye sekta ya utalii katika kipindi hiki cha Corona, lakini Tanzania tunaongeza tozo mfano kuanzia Julai, 2021 Park Fees zitaongezeka kwa 10 USD kwa Serengeti na Nyerere kipindi cha high season wakati Kenya, Uganda na Rwanda wamepunguza. TANAPA pia pamoja na uwekezaji ndani ya hifadhi kulipiwa Concession fee ya 50 USD bado wanaanzisha Land Base Rent ya 2000 USD kwa Seasonal Camps, Permanent Tented Camps 20,000 USD na Lodges 50,000 USD. Suala hili linaongeza gharama za utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANAPA wana hifadhi 22 ila hifadhi zinazoweza kujiendesha ni hifadhi zisizozidi tano na ndiyo maana kila mara wanaongeza tozo na kuongeza mzigo kwa hifadhi kama Serengeti, Nyerere na KINAPA. Nashauri tozo hizi zisitishwe hadi Julai, 2022 ili kutoa ahueni kwenye sekta ya utalii kipindi cha corona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tozo kama ukikodisha gari ya utalii kwa kampuni nyingine pamoja na kulipa TRA pia inabidi ulipe 50 USD Wizara ya Maliasili na Utalii. Hii ni kuongeza gharama za kufanya biashara Tanzania. Nashauri tozo hii iangaliwe upya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu TDL, fedha hizi nashauri ziwekwe kwenye akaunti maalum na zifanye kazi iliyokusudiwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za kupima Corona ni kubwa nchini Tanzania ambayo ni 100 USD wakati Kenya ni 30 USD Serikalini na 50 USD kwa Hospital binafsi. Gharama hizi ziangaliwe upya. Rapid test kote ni sawa kwa maana ya 25 USD.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Fedha ikae na bank na BOT ili kuangalia uwezekano wa kutoa ahueni kwa wadau wa utalii ambao walikopeshwa magari ya utalii na kushindwa kulipa kwa sababu ya Corona ili deni lao lisogezwe mbele bila penalty kama sehemu ya kutoa ahueni kwenye sekta ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasilisha.
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na wenzangu kwanza kabisa kukupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika, na ninakutakia kila la kheri kwenye kazi zako.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitaongeleza jambo moja tu kwa sababu ya changamoto ya muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba malengo makubwa tuliyo nayo ni kuhakikisha kwamba tunaongeza ajira kutokana na Ilani yetu ya Uchguzi ya CCM; tuliahidi ajira milioni nane mpaka mwaka 2025, lakini pia kuongeza na mapato. Na kwa kupitia Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ndiko kwenye uwezekano mkubwa wa kutoa ajira nyingi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ukiangalia, taarifa yam waka 2019 inaonesha kwamba sekta ya horticulture imeweza kuchangia asilimia 38 ya fedha zote za kigeni ambazo zinatokana na mapato ya kilimo. Ukiangalia kwa mujibu wa data zilizopo pia kwa nchi za Tanzania, Kenya na Ethiopia tunaona kwamba Tanzania tunatumia eka zisizozidi 120 kwa ajili ya horticulture, wenzetu wa Ethiopia eka 1,450 na Kenya 2,800; na ukizingatia kwamba sisi kule Arusha tuna mashamba 11 ambayo yamefungiwa, hayafanyi tena shuhguli zile ambazo zilikuwa zimeusudiwa. Mashamba hayo ni kama vile Kiliflora, Meru Flowers na mashamba mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kufungiwa kwa mashamba haya tumepata changamoto nyingi sana. Changamoto ya kwanza tumepoteza fedha za kigeni kiasi cha dola za Kimarekani 42,450,000, tumepoteza pia ajira kama 4,010, na hizi ni ajira za moja kwa moja, ukiacha nyingine ambazo zinatokana na sekta yenyewe. Tumepoteza pia fursa kutokana na mnyororo wa thamani, kwa sababu kutokana na kilimo kile kuna ambao walikuwa wanauza pembejeo, kuna ambao walikuwa wanafanya biashara za usafiri pamoja na shughuli nyingine. Lakini pia tumeondoa imani kwa wawekezaji, kwa sababu mashamba yale 11 yalikuwa chini ya wawekezaji, kitendo cha kuchukuliwa na Serikali imetoa hofu kwa wawekezaji wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto hizo mimi nilikuwa na mapendekezo yafuatayo.

Kwanza, nilikuwa nashauri kwamba kama wawekezaji waliokuwepo wameshindwa kuwekeza na ushahidi upo kwa sababu alikuwa anadaiwa na Serikali kupitia benki yatu ya TIB, lakini bado dhana na tija ya uwekezaji wa sekta ya bustani (horticulture) kwenye yale maeneo bado iko pale pale. Kwa hiyo tunashauri kwamba Serikali baada ya kuchukua mashamba yale sasa watafutwe wawekezaji wengine wakafanye uwekezaji ili tuweze kupata zile fursa ambazo tunazikosa, kama vile ajira pamoja na fursa ya mapato.

Lakini pia tulikuwa tunashauri kuwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami namshukuru Mungu kwa kupata nafasi niweze kuchangia bajeti hii ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na kazi nzuri sana aliyoifanya hasa kuchukua maoni mengi ya Wabunge na kuyaingiza kwenye Mpango wa Serikali, nampongeza pia Waziri wa Fedha kaka yangu Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu Waziri wa Fedha Mheshimiwa Injinia Masauni kwa kazi kubwa na nzuri sana ambayo wanaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitajikita kwenye mambo mawili la kwanza ni kuhusu utalii. Sekta ya Utalii imesahaulika sana. Bajeti hii imeangalia mambo mengi sana, lakini nataka nikuhakikishie haijatoa ahueni yeyote kabisa kwenye sekta ya utalii. Wizara ya Maliasili na Utalii ni kana kwamba vile haijui dunia imetoka wapi, ipo wapi na inakwenda wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia taarifa zilizopo kutokana na changamoto za Corona duniani tunaambiwa kwamba uchumi umekuwa na mdororo hadi kufikia asilimia 3.3 ambayo ni hasi kutoka asilimia 2.8 ya mwaka 2019. Lakini tunaambiwa kwamba Pato la Taifa limeshuka kutoka asilimia 7 mpaka asilimia 4.8 mwaka 2019/2020. Tunaambiwa pia mchango wa utalii umeshuka kutoka asilimia tuliyoizoea 17.5 mpaka asilimia 10.7 kwenye Pato la Taifa. Tunaambiwa pia mapato yamepungua na taarifa imetolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii kutoka bilioni 584 mpaka bilioni 89 ambayo ni sawasawa na asilimia 15 ya malengo yaliyowekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia mapato ya mwaka 2019/2020 yalikuwa bilioni 252 kipindi kama hiki leo bilioni 44.8 kwa taarifa zao wenyewe Wizara ya Maliasili na Utalii. Tunaambiwa pia idadi ya utalii imepungua kutoka mwaka 2019/2020 walikuwa milioni moja elfu hamsini na mbili mia tisa arobaini na tatu (1,529,443) na sasa hivi ni watalii laki nne na kumi na nne na thelathini (414,030).

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba changamoto kubwa zimejitokeza hasa kwenye ajira, ukienda Arusha hoteli nyingi zimeathirika, Tour Operators wameathirika, waongoza utalii wameathirika, karibu sekta zote madereva, wahudumu wa hoteli, wapagazi wale, wapiga mahema, wapishi, staff wa maofisini wapo hoi kwa sababu hakuna wageni. Tunajua, Waziri anajua, Waziri wa Fedha anajua, Waziri wa Utalii anajua, lakini mambo yanavyokwenda kana kwamba wapo dunia nyingine tofauti na sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachonishangaza pamoja na matatizo yote haya solution waliyokuja nayo Wizara ya Maliasili na Utalii na Serikali yetu hii ni kuongeza tozo. Utaona tumeongeza dola 10 kipindi cha high season kwenye hifadhi ya Serengeti na hifadhi ya Nyerere, lakini tumeleta tozo nyingine mpya inaitwa land base rent kwa watu ambao wanakuwa na seasonal camp dola 2,000, ukiwa na permanent tented camp dola 20,000, ukiwa na lodge dola 50,000 ndani ya hifadhi, Serengeti mle ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mtalii anapokuja Tanzania akifika airport pale analipa VISA, akitoka pale anapanda gari ya utalii anachangia mafuta pamoja na masuala mengine, akienda kwenye hoteli akilala analipa ambapo Serikali inapata fedha, akienda kwenye park analipa park fee, akitoka pale akilala ndani ya hifadhi analipa kitu kinaitwa concession fee ambayo kila siku anayolala ndani ya hifadhi analipa dola 50 bila VAT.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wamekuja wenzetu maliasili na utalii na tozo nyingine, eti ukitengeneza seasonal camp umechukua hema lako umeliweka mle ndani ya hifadhi dola 2000, ukichukua hema lako kama ni kwa muda fulani, permanent dola 20,000, umejenga lodge ume-invest wanakupiga dola 50 hasa ile concession fee ni ya nini? kwa hiyo, unaona kabisa Wizara ya Maliasili na Utalii wasipoangaliwa hawa wanakwenda kuiua kabisa sekta hii wanakuwa ni Corona namba mbili katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina ushauri kwenye jambo hili Serikali ikaliangalie jambo hili vizuri hizi tozo zisitishwe, kwa sababu kwanza hazijaanza kutozwa, zitaanza kutozwa kuanzia tarehe Moja mwezi wa Saba mwaka huu inamaana bajeti hii ikipita. Tunavyozungumza leo hata wakisitisha Serikali haijapata hasara yoyote kwa sababu mambo haya ni mapendekezo yote wamekuja nayo Wizara ya Maliasili na Utalii. Ndiyo maana nilisema kwenye mchango wangu uliopita tunazo hifadhi 22, hifadhi ambazo zinazalisha ni tano peke yake, hifadhi 17 hazina uwezo wa kuzalisha kiasi cha kujiendesha, badala ya Wizara ya Maliasili na Utalii kuja na mpango mbadala kila siku wanafikiria kuongeza tozo Serengeti, kuongeza Nyerere na masuala mengine, ukiwauliza ni kwa sababu gani wanasema tunataka tuzuie congestion! eti tukiongeza tozo watalii wataogopa kwenda hifadhini kwa hiyo hifadhi zitabaki salama, halafu leo wanakuja na maelezo hapa tunataka tuongeze watalii kutoka idadi ya sasa mpaka milioni tano, unashindwa kujua hata haya mambo wanayo yazungumza wanayatoa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili jambo ni very serious naiomba sana Serikali kwa sababu tunaye Rais msikivu, Rais ambaye ameamua kuleta ahueni kwenye sekta binafsi, Rais ambaye anafahamu hawa sekta binafsi, kuna hotel pale Karatu, walikuwa zamani kabla ya utalii hotel ya dola 200 leo mtu ameshusha mpaka dola 100 ili kuweza kuvutia wageni waje, Serikali hii inakwenda kuongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani hili jambo ni vizuri Bunge lako Tukufu na Serikali yetu waende wakaliangalie watu wa Maliasili na Utalii wakumbushwe kwamba kazi yao wao ni kuangalia interest za Serikali pia kuangalia na interest za wawekezaji kwa maana ya sekta binafsi, lakini siyo kuangalia Serikali peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kuhusu wenzetu hawa wa bureau de change, tumepata shida kubwa sana Mkoa wa Arusha, tumeteseka na ma-task force kila siku yanashindana kuja tu pale, baadaye wamekuja na mambo haya ya bureau, na watu wa bureau hawa kuna mchezo wanaucheza ambao sijui hawa watu wa Serikali kuna watu wao wanataka wafanye hii biashara? Maana ukiangalia mwaka 2015 mtaji wa mtu wa bureau ulikuwa milioni 40, wakaja mwaka 2015 hadi kufika mwaka 2017 wakaongeza ikaja milioni 100, kufika 2018 Mei wakapeleka milioni 300, baadaye wakaona sasa kila wakiongeza wale wanafanya biashara, kila wakiongeza wanafanya biashara, baadaye wakaamua kuvamia na kwenda kuwapora! Wakapora pesa zao, wakapora magari yao, wakapora hati zao za nyumba, wakapora viwanja wamewaacha hoi taabani.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mrisho Gambo kengele imegonga.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana lakini ombi letu kwamba warudishiwe leseni, warudishiwe fedha zao, gharama zipungue na assessment za kienyeji zile zifutwe ili watu wafanye biashara Serikali ipate kodi na fedha zake.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na wenzangu kushukuru sana kupata fursa hii adimu niweze kutoa mchango wangu kwenye Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Mwaka 2021 ajenda yangu kubwa ilikuwa utalii; mwaka huu ajenda yangu kubwa itakuwa ni sekta ya madini. Kabla sijaenda kwenye sekta ya madini, naomba nizungumzie changamoto tulizokuwanazo katika uwanda mzima wa biashara sisi kama Watanzania na pia kama Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ukiangalia Sheria yetu ya Mwaka 2007, ukienda ukurasa wa 72 Kifungu cha 31, tunaambiwa kwamba “The Business Licensing Act of 1972 is hereby repealed.” Kwamba sheria hii ya mwaka 1972 ilifutwa, lakini cha kushangaza sheria hii ambayo ilifutwa mwaka 2007 kupitia sheria ya Business License Act ya 2007 Kifungu 31, bado tukaenda kuifanyia marekebisho mwaka 2014, 2015 na 2018. Yaani Bunge lako hili lilifuta sheria ya mwaka 1972, likaanzisha sheria ya mwaka 2007, lakini bado likaenda mwaka 2014 lirekebisha sheria ambayo ilishafutwa tayari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye sheria hii ya mwaka 1972, ukienda kwenye ukurasa wa 9, kuna Act (No. 2) of 2014 Section No. 6; ilifanyia marekebisho ya sheria ambayo imefutwa. Pia ukienda kwenye ukurasa wa 12, mwaka 2015 yalifanyika marekebisho kupitia Sheria ya Fedha kwa kuongeza maneno yafuatayo, pia ilienda ikafuta na jedwali, yaani imekwenda kurekebisha kitu ambacho Bunge tayari ilishafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo uone ni namna gani tulikuwa na changamoto kubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ukienda kwenye Sheria yetu ya Madini, ukiangalia kanuni yetu, tulikuwa na kanuni ya mwaka 2002 ambayo tulikwenda kuifuta mwaka 2019. Mara baada ya kuifuta, tukaja kufanya marekebisho mengine mwaka 2021. Kinachonishangaza, ukiangalia hii Kanuni, inasema imekuwa gazetted tarehe 2/7/2021. Nimekwenda kutafuta gazeti la Serikali la tarehe 2/7/2021, sijaikuta hii kanuni. Ila nimekwenda kuikuta kwenye gazeti la Serikali la tarehe 9/7/2021. Gazeti lenyewe pia ukiangalia bado limeandikwa tarehe 2/7/2021, ukija hapa ni la tarehe 9 Mwezi wa Saba. Kwa hiyo, utajiuliza, ni kweli sisi wote ni vipofu? Yaani Bunge, Wizara ya Madini, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, wote hatuoni?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini yametokea haya? Yametokea haya kwa sababu tunajua Serikali inapotoa maelekezo, inatoa kwa nia njema sana na Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokwenda Mererani tarehe 2/7/2021, alitoa maelekezo kwamba Sheria ya Madini na Kanuni zake viweze kubadilishwa. Tarehe 8 wakabadilisha kanuni, Waziri akasaini, tarehe 9 tukai-gazette. Katika uharaka wa namna hiyo bila kushirikisha wadau, lazima kuwe na changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba sasa niende kwenye hoja ya msingi. Ukienda kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ukurasa wa 37 kipengele cha 67, Mheshimiwa Gwajima alikuwa anashika documents zangu, isije ikawezekana kwamba ameziweka pembeni; inasema kwamba, “Serikali imeendelea kuimarisha usimamizi na kuanzisha masoko mapya ya madini na vituo vya ununuzi nchini kwa lengo la kupata takwimu sahihi za mauzo ya madini, kuongeza ukusanyaji wa maduhuli na kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata soko la uhakika na kupata bei stahiki kwa bidhaa za madini.”

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu sote kwa mwaka, 2019 tulianzisha masoko ya madini. Arusha lilikuwepo, Mererani lilikuwepo na maeneo mengine mbalimbali katika nchi yetu. Kwenye masoko ya madini haya tulikuwa tunaruhusiwa kuuza madini ya aina zote, ukienda pale Arusha leo tuna madini kutoka Kongo DRC, kutoka Msumbiji, kutoka Ethiopia na kutoka Kenya, lakini tanzanite ambayo inapatikana Tanzania hairuhusiwi kwenda kuuzwa kwenye soko la Arusha. Maamuzi ya kubadilisha Kanuni yameipatia Serikali hasara kubwa sana naomba nikupe taarifa ifuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, wakati linaanzishwa soko pale Arusha, nikichukua taarifa ya Julai hadi Disemba, 2019 tulipata carets 76,000 lakini kodi iliyopatikana ya Serikali ilikuwa ni shilingi milioni 487. Ukiangalia kwenye rough tanzanite tulipata kiasi cha kodi shilingi bilioni 1,300,000,000/= na point kadhaa. Ukija mwaka 2020 tuliweza kuwa na caret ya 85,000 tuliweza kupata kodi ya shilingi milioni 332 lakini kwenye rough tanzanite tuliweza kupata kodi ya shilingi bilioni 1.1.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuhamishia Mererani ukiangalia kipindi kile kile cha Julai, 2021 tumeacha Disemba hadi Januari, Serikali imepata kodi kiasi cha shilingi milioni 339 kutoka shilingi bilioni 1.3. Unaangalia kwenye upande wa caret tumeweza kuwa na caret 15,000 kutoka 85,000. Kwa hiyo, unaona kabisa maamuzi haya yamekwenda kuitia hasara Serikali lakini pia, kwa mujibu wa taarifa tulizokuwa nazo pale Arusha idadi ya dealers walikuwa ni 103, leo kuna dealers 48 tu kule Mererani. Kulikuwa kuna mashine za kukatia 427… (Makofi)

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa mtoa hoja taarifa kwamba madini ya tanzanite yapo katika Mkoa wa Manyara na katika takwimu zinaonyesha, Serikali imeweza kuongeza kipato toka soko liliporejeshwa katika Mji wa Mererani ambapo madini ndipo yanapochimbwa. Pia, imeweza kuwarahisishia wafanyabiashara pamoja na wachimbaji wadogo wadogo kuweza kuuza madini, kwa uhakika na usalama uliokamilika na kuendelea kuukuza Mji wa Mererani katika Mkoa wa Manyara. Hivyo, napenda kumpa mtoa mada taarifa kama anatamani madini ya tanzanite basi tunamkaribisha katika Mkoa wa Manyara, tuna maeneo makubwa bado tunahitaji wananchi wa kuja kuwekeza. Kwa hiyo, tunamkaribisha katika Mkoa wa Manyara ili apate madini. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante. Mheshimiwa Gambo taarifa hiyo.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwamba Wabunge watafute hoja za kuchangia sio tunadandia tu mradi tuonekane na wananchi wetu. Hapa tunaongea mambo serious, kwa hiyo sipokei taarifa yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna ajira ambazo zimepotea, ajira zaidi ya 413, kuna ma-broker pale kati ya 2,500 – 3,000 ambao pia wamekosa ajira. Hata hivyo, Serikali ikiwa imepata hasara Soko la Madini la Arusha inahusisha majengo ya AICC, NSSF na PSSSF. Serikali imepata hasara kiasi cha shilingi milioni 128 ambazo zilikuwa zinalipwa na wafanyabiashara wa madini kwenye maeneo hayo. Naomba nitoe mapendekezo na ushauri kwa sababu wote tunajenga nyumba moja. Mapendekezo yangu; la kwanza, tunaomba masoko ya madini ambayo yameanzishwa kwa mujibu wa taratibu za nchi hii, yaruhusiwe kuuza madini ya aina zote, maana inashangaza kuona leo Tanzanite unachukua Mererani… (Makofi/Kicheko)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili hiyo, malizia sekunde mbili, Mheshimiwa Gambo.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, unakwenda kuiuza India na Tanzania haipatikani. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Kengele hiyo ya pili, sekunde mbili malizia.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Kwa hiyo, napendekeza pia Mererani ibaki sehemu ya uzalishaji wa tanzanite na soko la malighafi kwa mfumo wa mnada mara moja au mara mbili kwa wiki. Kwa sababu… (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kushukuru sana kwa kupata fursa ya kuweza kuchangia na kutoa mchango wangu wa mawazo kwenye Wizara hii ya Madini. Nitajielekeza kwenye maeneo matatu; moja, kwenye dhana ya kuhamisha madini ya tanzanite kwenda Mererani; pili, changamoto zake halafu; na tatu, kwenye mapendekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dhana nzima ya kuondoa madini ya tanzanite na kutaka yauzwe Mererani peke yake inahusisha maeneo mawili. Eneo la kwanza, utoroshaji na kwenye utoroshaji wa madini sina mashaka kabisa kwa sababu kwenye eneo la Mererani ambako Serikali imejenga ukuta ndio eneo ambalo kuna ulinzi wa uhakika, kuna vyombo vyote vya ulinzi na usalama, kuna Jeshi la Wananchi, kuna Usalama wa Taifa, kuna TAKUKURU, kuna Polisi na kuna Wizara yenyewe ya Madini. Kwa hiyo, dhana ya utoroshaji na changamoto hiyo kwa muktadha wa Mererani haipo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nasi hatutaki madini haya yauzwe Arusha peke yake, tunataka yauzwe Mererani, Arusha, Mwanza, Zanzibar na kwenye masoko yote ambayo yapo kwa mujibu wa sheria ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa changamoto; tuna changamoto ambazo tumezipata kutokana na maamuzi hayo ya Serikali. Changamoto ya kwanza, mapato ya Serikali yameshuka. Kabla ya maamuzi haya, kipindi kama hiki tulikuwa tunapata kiasi cha Shilingi bilioni 1.3 kwenye Soko la Madini la Arusha. Hiyo ni kwa madini yote, lakini kwa Tanzanite peke yake ilikuwa ni shilingi milioni 800. Leo tumepeleka Mererani kipindi kama hicho tunapata shilingi milioni 339. Kwa hiyo, changamoto ya kwanza Serikali imepata hasara, tumepoteza mapato.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya pili, katika Soko la Madini la Arusha, tuna maeneo kama NSSF, PSSF na AICC ambayo ni majengo ya Serikali. Serikali ilikuwa inapata kodi kupitia wafanyabiashara ya madini, ambapo kwa mwezi tulikuwa tunapata shilingi milioni 128. Hadi kipindi cha sasa tumepotezza kiasi cha shilingi bilioni 1.152 ya pango kwenye taasisi hizi za Serikali. Kwa hiyo, unaona maamuzi haya tuliyoyafanya yametuletea changamoto kubwa ya kukosa mapato kwa pande zote.

Mheshimiwa Spika, pia tuna changamoto kwenye upande wa ajira. Tumekosa ajira 403 kwa wale ambao wote ambao walikuwa wanafanya biashara hizo kwenye masoko yetu ambayo yapo hapa. Tumepata changamoto kwa ma- broker wetu; ma-broker 2,500 mpaka 300 wamepata changamoto kubwa sana kwa sababu asilimia karibu 80 ya madini yanayouzwa kwenye masoko ya Arusha yanatokana na Tanzanite.

Mheshimiwa Spika, pia tulikuwa na mashine 427 kwenye Soko la Madini la Arusha, sasa hivi Mererani zimekwenda mashine 48 tu ambayo ni sawa sawa na asilimia kama 11.24. Kwa hiyo, unaona mashine ambazo zimebaki hazitumiki watu wamekosa ajira kwenye maeneo hayo, lakini pia na changamoto nyingine nyingi kwa mapana yake.

Mheshimiwa Spika, kutaka tu madini ya Tanzanite yauzwe Mererani peke yake, una-monopolize soko lenyewe, inasababisha kushuka kwa thamani, kwa sababu kunakuwa hakuna ushindani. Leo ukiuza madini Mererani, ukiuza Arusha, ukiuza Mwanza, ukiuza Zanzibar na maeneo mengine ya Tanzania, itasaidia sana kwa wafanyabiashara hao kushindana kutafuta wanunuzi nje ya nchi na mwisho wa siku faida itakuwa ni kubwa zaidi na mapato pia yataweza kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, pia kitendo cha kuruhusu wageni kutoka nje ya nchi kwenda moja kwa moja Mererani kununua madini, kwanza ni hatari kwa usalama wa nchi yetu, lakini pia inaondoa fursa kwa watu mbalimbali walio katika nchi ya Tanzania kuweza kunufaika na madini hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baada ya kusema hayo, nilikuwa na mapendekezo yafuatayo kwa Wizara yetu ya Madini na Serikali kwa ujumla. La kwanza, sisi hatuna tatizo kabisa, tunataka Serikali ikusanye kodi na tunataka kodi zote zilipwe pale Mererani; walipe kama ni mrabaha, inspection fee, baada ya kulipa kama ambavyo wanaruhusiwa leo, wakishalipa wapeleke madini yao India, Marekani na maeneo mengine, waruhusiwe pia kupeleka na Tanzania kwa sababu ni sehemu ya dunia ambayo inachanganya Arusha, Mwanza, Zanzibar, na Mererani kwenyewe.

Mheshimiwa Spika, tunao mfano, tuna madini kama haya yanaitwa pink ruby ambayo yanapatikana kule Thailand peke yake. Madini haya yanayopatikana kule pamoja…

(Hapa kengele ililila kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, naamini hiyo ni kengele ya kwanza.

SPIKA: Kengele ni moja tu. Malizia sentensi yako.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, tunaamini kwamba madini haya yakiruhusiwa kuuzwa kwenye masoko mbalimbali itatusaidia sana.

Kwanza yatatoka kwa mchimbaji, yatakwenda kwa broker, baadaye yatakwenda kwa dealer na baada ya hapo yataongeza mzunguko ndani ya nchi yetu na pia yatafika huko duniani.

Mheshimiwa Spika, pia tunaomba…

SPIKA: Ahsante sana. Muda wako umeisha.

MHE. MRISHO M. GAMBO: …tuweze pia kuanzisha maonesho ya madini, ili madini yetu haya ya Tanzanite na madini mengine tuwe na maonesho yake pale Arusha, dunia nzima iweze kuyaona, na mwisho wa siku iweze kutusaidia kuitangaza Tanzania, na kuleta watalii ndani ya nchi yetu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuchangia hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Mchango wangu utajielekeza kwenye maeneo mawili. Upande wa utawala bora na upande wa masilahi ya watumishi.

Mheshimiwa Spika, kwenye utawala bora, nina ushauri mmoja kwa TAKUKURU, kwa sababu kuna masuala mengine yako wazi kabisa lakini michakato yake inachukua muda mrefu sana. Nakumbuka mwaka 2017/2018 kuna mchakato ulianzishwa pale Jijini Arusha, wenzetu wa boda boda wakaweza kuchangisha fedha kiasi cha shilingi milioni 400 ambazo baadaye zilikuja kuibiwa na baadhi ya watu.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ni kwamba, mnamo tarehe 18 Juni, 2021, katika Tawi la NMB Mbagala kuna Mtu anaitwa Maulid, mwingine anaitwa Makongoro, Mwingine anaitwa John F. Fungameza, walikwenda kuchukua fedha kwenye akaunti kiasi cha shilingi 39,500,000. Mnamo tarehe 8 Julai, 2021, kuna mtu mwingine tena ambaye anaitwa John na mwingine anaitwa Edwin, walikwenda kwenye Akaunti na kuchukua fedha kiasi cha shilingi 43,500,000. Mnamo tarehe 31 Agosti, 2021, kwenye Tawi la Kariakoo wakachukua tena Fedha kiasi cha shilingi 43,800,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia tena mnamo tarehe 25 Novemba, 2020, kupitia NIDA namba ya T100027912657 walikwenda kuchukua shilingi 15,000,000. Orodha ndefu na inaendelea. Hoja yangu hapa ni kwamba hawa watu wa bodaboda fedha zao zimeibiwa na walioiba fedha wanajulikana, wameenda benki wamechukua fedha na wametoa vitambulisho vya NIDA na wamechukua kwa majina yako. Hata hivyo, toka mwaka 2020 mpaka leo suala hili halijapelekwa Mahakamani na wahusika hawajakamatwa, badala yake inatolewa fursa kwa baadhi ya watu kuanza kuchafua majina ya watu ambao hwahusiki kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Spika, ombi langu, tuwaombe TAKUKURU, najua wanafanya kazi kubwa na wanafanya kazi nzuri. Kama wezi wanajulikana na ushahidi upo, kigugumizi ni cha nini kuhusu kuwakamata na kuwapeleka mahakamani ili kuweza kuondoa changamoto hii kwenye maeneo mengine?

Mheshimiwa Spika, jambo langu la pili, maana hapa ukiangalia fedha zilizochukuliwa ni kiasi cha shilingi 214,500,000. Hizi ni fedha nyingi sana kama zingepatikana zingewasaidia vijana wa bodaboda kuendelea kukopeshana kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, jambo langu la pili ni kuhusiana na madai ya watumishi. Ukiangalia Jiji la Arusha ulifanyika uhakiki mwaka 2017 wa kuangalia ni watumishi gani ambao walikuwa wanadai masilahi yao. Ukiangalia mfano, kwenye upande shule ya msingi na shule ya sekondari kwenye uhakiki huo, kwenye upande wa likizo kwa upande wa shule za msingi zinadaiwa shilingi 105,000,000; Kwenye upande wa sekondari ni shilingi 94,000,000; jumla ni shilingi milioni 200.141.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa waliokwenda masomoni kwenye shule ya msingi shilingi 2,800,000 na shule za sekondari shilingi 600,000, jumla ni shilingi 3,400,000; Ukienda kwenye matibabu jumla ni shilingi 14,775,000; Ukienda kwenye uhamisho wa watumishi ni shilingi 56,757,000; Ukienda kwenye fedha za kujikimu ni shilingi 2,211,000; Ukienda kwa waliostaafu yaani kuna watu waliostaafu kabla ya mwaka 2017, wamelipwa stahiki zao zote, lakini mpaka leo hawajalipwa fedha za kusafirisha mizigo yao ambazo ni kiasi cha shilingi 26,837,013.94; Kuna ambao walifiwa mpaka leo wanadai shilingi 3,150,000; Kuna ambao wanadai hela zao za mizigo shilingi 12,000,000; Kuna nauli pia kwa ajili ya ajira mpya, mtu ameajiriwa nauli yake ya kumpeleka kituoni hajapewa na asingeenda kituoni pengine angepewa adhabu ya kutokuwa kazini. Wanadai na wenyewe kiasi cha shilingi 998,000 tu; na ukiangalia stahiki za Wakuu wa Idara zenyewe ni shilingi 38,050,000. Kwa hiyo jumla yake ni shilingi 358,420,582.89.

Mheshimiwa Spika, ndio maana tunapoona kwenye Jiji la Arusha kuna ufisadi na wizi tunapiga kelele kwa sababu tunaamini tukidhibiti ule wizi, zile fedha zitakuja kuwasaidia hawa wanyonge ambao wanasaidia kufanya kazi mbalimbali kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni ombi langu, si lazima kila kitu tuchukue fedha kutoka Hazina. Zile halmashauri ambazo zina mapato makubwa kama vile Arusha, Ilala, Mwanza zile za majiji zote, wangepewa maelekezo na utaratibu hela ndogo kama hizi milioni 358 wangezilipa wao wenyewe ili kuwaondolea wananchi wetu kero pamoja na masuala mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia fedha hizi katika ufisadi uliofanyika Arusha zile risiti fake peke yake tu milioni 699 peke yake zingeweza kulipa deni hili na change ingebaki na masuala mengine pia yangeweza kuendelea.

Mheshimiwa Spika, suala lingine pia ambalo ningependa kulizungumzia kuhusiana na watumishi wetu ni kuhusiana na kupanda madaraja kwa watumishi. Kwenye suala la kupanda madaraja, katika hili naomba niipongeze Serikali kwa sababu kwa kweli kuna kazi kubwa imefanyika. Kwa sababu kwanza nafahamu kuna mwongozo wa Serikali ulitoka wa tarehe 27 Machi, 2018 ambao ulielekeza kwamba ukurasa wa pili, kifungu cha 3(b) ulikuwa unasema, kufuta barua za awali za kuwapandisha vyeo na badala yake barua za vyeo hivyo zionyeshe kuwa vyeo vya watumishi hao vinaanza tarehe 1 Aprili, 2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tafsiri yake ni kwamba walikuwa wamenyimwa miaka miwili ya kupandishwa mishahara yao. Hata hivyo, bahati nzuri kwa sababu ya usikivu wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, tumeona mwaka huu 2023 tarehe 23 Desemba, umetoka mwongozo wa Serikali ambao umeelekeza watumishi walioathirika na zoezi la uhakiki katika upandishaji vyeo mwaka 2016 ambao walipandishwa kwa makundi mawili ya mwezi Novemba, 2017 na Mwezi Aprili, 2018 na kupanda vyeo walivyonavyo sasa mwezi Mei, 2022, lengo la hatua hii ni kuwezesha uwepo wa msawazisho wa vyeo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni imani yangu kwamba wenzetu Wizara ya Utumishi watahakikisha kwamba wafanyakazi wote hawa kama Serikali ilivyoelekeza, wanaingizwa kwenye utaratibu na wanapata haki zao kama ambavyo Serikali imeelekeza.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo kulikuwa na changamoto za jumla, Serikali siku za nyuma imekuwa inapandisha mishahara kutokana na uwezo wake wa kibajeti. Kwa hiyo, sisi ombi letu ni kwamba wasiangalie uwezo wa kibajeti, waangalie kama miaka mitatu imefika watumishi wote wajue mwaka huu wanatakiwa wapandishwe, wapandishwe wote. Kwa sababu, mwaka huu ukipandisha nusu halafu mwakani ukapandisha wengine watakuwa wanatofautiana vyeo na mishahara wakati walianza kazi siku moja na sifa kwa ujumla wake zinafanana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MRISHO M. GAMBO. Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, nami nitumie fursa hii kukushukuru sana kwa kupata nafasi hii niweze kutoa mchango wangu kwenye sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nami niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na kazi nzuri sana ambayo ameifanya ya kuutangaza utalii wetu duniani kote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo kwamba napingana na wenzangu, sisi watu wa Arusha ndiyo wanufaika wakuu wa utalii na ndiyo maana utaona leo watu wakizungumza kuhusiana na mateso ya tembo, sisi tunazungumza kuhusiana na ajira ambazo zinameongezeka kwenye mahoteli yetu, tunazungumza mapato ambayo yanapatikana kwenye nchi yetu, tunazungumza faida nyingi, tunazungumza mama ambaye analima mbogamboga anaweza akauza bidhaa zake kwenye hoteli, tunazungumza mfugaji kutoka Ngorongoro ambaye anafuga anaweza akauza maziwa kwenye mahoteli. Kwa hiyo, sisi watu wa Arusha tukiwaambia kwamba ni wanufaika wakubwa wa masuala ya utalii ni vizuri wakatuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kwenye upande wa usalama; tunauza bidhaa nyingi sana, tunauza wanyamapori, tunauza big five na vivutio vingine, lakini lazima tukubali kwamba component ya usalama ni component kubwa sana ndiyo maana sisi katika Jiji la Arusha kwa kushirikiana na Serikali katika ngazi ya Mkoa, kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa usimamizi mzuri wa IGP Simon Sirro pamoja na RPC wa Arusha vimewezwa kujengwa vituo vya kisasa maalum kwa ajili ya kuwahudumia watalii. Tuna kituo kikubwa pale Central, tuna kituo pale Kikatiti kama unatoka airport, tuna kituo kule Engikaret kama unatoka Namanga kwa maana ya Kenya, tuna kituo Makuyuni na tuna kituo Karatu maalum kuhakikisha kwamba watalii hawasumbuliwi barabarani. Wanakuwa na kituo kimoja wanasimama, wanakaguliwa na maisha yanaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwenye hoja hii, tunawaomba wenzetu wa Wizara ya Maliasili na Utalii watusaidie kuwaunga mkono Jeshi la Polisi kwenye masuala ya usalama kwa sababu usalama ndiyo bidhaa namba moja kwenye utalii, kama hakuna usalama hakuna utalii. Wana shida ya magari kwa ajili ya patrol, tunataka wazungu/wageni wakija kwenye nchi yetu wanapokelewa kwa escort kuanzia airport wanapewa red carpet, wanakwenda kwenye mahoteli ili wakirudi wakaongee hadithi nzuri ya namna watu wa Tanzania tulivyo wakarimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunaomba pia Wizara ya Maliasili itusaidie, wenzetu wa TATO hawa wa masuala ya utalii, private sector, wao wamejenga kile kituo kilichopo pale Arumeru, wenzetu wa TATO wamejenga kituo kilichopo pale Central, wametoa gari brand new Land Cruiser na Wizara ya Maliasili kwa sababu wao ndiyo wanufaika wakuu watusaidie kwa kuwaunga mkono kwa kutusaidia hayo magari kwa ajili ya polisi, lakini pia na kuboresha na kituo kilichobaki cha Makuyuni na kile kituo cha Engikaret. Pia niwashukuru wenzetu wa CRDB kwa sababu wameahidi kutuchangia pikipiki kumi kwa ajili ya kuimarisha usalama na kumuunga mkono Mheshimiwa Rais kwenye programu nzima ya Royal Tour. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo langu la tatu; kuna leseni ya biashara kwa ajili ya mountain guide. Kipindi kilichopita tulizungumza kuhusiana na tour guide, hawa tour operators ambao walikuwa hawana kampuni wana gari moja moja walikuwa wanalazimika kujichomeka kwenye makampuni mengine ili wafanye biashara. Serikali ikashauriwa ipunguze tozo ili iweze kuwashawishi watu wengi zaidi kuweza kujisajili na kufanya biashara, wakaweza kupunguza ile TAA license gharama yake kutoka kwenye dola 2,000 hadi kufika dola 500 mpaka ninavyoongea sasa hivi wale wafanyabiashara wadogo wadogo zaidi ya 270 wameweza kujiandikisha na Serikali inaweza kuwatambua, inaweza ikapata mapato na masuala yanaendelea. (Makofi)

Tunaomba pia kwenye jambo kama hilo tulifanye wale mountain guides ambao wanatakiwa walipe dola 2,000 kila mmoja. Hebu niambie mtu leo ametoka pale Mweka kusoma au ametoka chuo chochote cha utalii anataka kuanza kazi ya kupeleka wageni mlimani, anaambiwa bila kuwa na dola 2,000 ya leseni huwezi kuanza kazi, matokeo yake sasa wanatafuta wale wenye biashara za utalii wanawapa dola 10, 10 kwa kila mgeni ili wapate vocha na waweze kupeleka watu kwenye utalii. Ni vizuri Serikali ikaliangalie suala hilo, mkawapa nafasi, mkapunguza angalau kutoka mtu anayepandisha Mtalii mmoja mpaka 100 mkampa dola 500, wanaopandisha watalii 100 na kuendelea mkawapa dola 2,000 na kuendelea na mkifanya hivyo watakuwa wamewatambua wale watu wa wadogo, wameingiza kwenye mfumo rasmi, watafanya shughuli zao, lakini baadae pia itakuwa rahisi kuweza kulipa kodi pamoja na masuala mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna changamoto kwenye upande land base rent. Unajua kule Serengeti kuna tozo nyingi sana, kuna mtu analipa park fee, kuna ambao wanalipa concession fee, mtu akilala tu kwenye hoteli yoyote kwenye park kama siku kama ni high season dola 60, kama ni low season dola 50 bila VAT. Lakini bado hawa Maliasili wamekuja kuleta kitu kinaitwa land base rent. Sisi ushauri wetu kwa sababu ukileta hii tozo inaonekana kwa makadirio watapata dola milioni 3.2, ni bora wangeongeza fee kidogo angalau dola tano au dola 10 ili waweze kupata ile kodi na ni kodi ambayo italipwa na mgeni kutoka nje, haitalipwa na yule mwekezaji itaweza kupunguza changamoto na maisha pale yataweza kuendelea.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kuhusiana na tozo mchanganyiko; ukienda kwenye ma-gate yetu, leo mtalii mfano kutoka Arusha akitaka kwenda Lake Natron anakutana na vijiji kama vitatu kila kijiji analipa dola 10, kingine dola 10, kingine dola 10, baadae anakwenda TAWA analipa dola 25. Sasa unashindwa kuelewa Serikali ni moja kwa nini kila mtu akusanye tozo kana kwamba Serikali hii haina usimamizi? Ni vizuri Serikali iratibu tozo zote, kama zinalipwa TAWA zilipwe TAWA, kama ni Halmashauri walipe Halmashauri, halafu wao ndani ya Serikali watagawana kidogo kidogo ili kuondoa usumbufu na siku hizi fedha zote zinaenda kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali sasa kuna haja gani ya kila mtu kulipa moja moja.

Mimi nilikuwa naomba Serikali yetu izungumze Lugha moja kwa maana ya TAMISEMI, Wizara ya Maliasili na Wizara ya Fedha wakae chini waje na utaratibu mmoja ili kuondoa usumbufu kwa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale Arusha tuna eneo linaitwa Clock Tower; Clock Tower ndiyo center ya Afrika kati ya Cairo kule Misri na Cape Town kule Afrika ya Kusini. Pale Clock Tower tunaambiwa kwa sababu ni center sisi tunataka tuitumie kama kivuko…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 malizia sentesi.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, tunataka tuitumie kama ni kivutio cha utalii. Tumeongea na Balozi wa India yuko tayari kushirikiana na Wizara ya Maliasili pamoja na Serikali ngazi ya Mkoa ili tutengeneze tower pale ambayo mwisho wa siku watalii wakija watafika pale, watapanda kwenye ile tower watalipa tozo, tutaitangaza Arusha yetu, wataangalia Mlima Meru ulioko jirani pale, mapato yatapatikana. (Makofi)