Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Cosato David Chumi (78 total)

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa hali iliyoko katika Mji wa Mombo inafanana kabisa na hali katika Mji wa Mafinga ambao unakua kwa kasi na kwa kuwa Mamlaka yetu ya Maji ya Mji wa Mafinga ni ile ambayo ni ya class C, kwa hiyo haijaweza kuwa na uwezo wa kuhudumia maeneo makubwa ya mji. Je, Serikali iko tayari kutusaidia watu wa Mafinga hasa katika Kata za Bumilayinga, Isalavanu na Lungemba japo kuchimbiwa visima?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Chumi, Mbunge wa Mafinga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikupongeze Mheshimiwa Chumi kwa sababu mara nyingi umekuwa unawasiliana na Ofisi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kuhusu kuwapatia maji wananchi wa Mji wa Mafinga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba category ya Mamlaka ya Maji ya Mafinga ni C ambayo inahitaji kupewa msaada na Wizara. Nikiri kabisa kwamba tayari kuna deni la shilingi milioni 150 kwa ajili ya kulipia TANESCO ili umeme uendelee ku-pump maji kupeleka kwa wananchi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Chumi kwamba Wizara ya Fedha kwa sasa imeweka utaratibu, itakuwa inalipa madeni hayo ya maji moja kwa moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu hoja ya pili ya kuchimba visima tuko tayari, Mheshimiwa Mbunge tushirikiane. Kuna hela tuliyokutengea kama itakuwa haitoshi basi ulete taarifa ili tuweze kutenga hela nyingine tuhakikishe hivyo vijiji ambavyo havijapata visima viweze kupata visima.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, TAMISEMI, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, jana wakati Wizara ya Afya ina wind-up, wameendelea kusisitiza kwamba Serikali itaajiri watumishi wa kada za afya wanaozidi 10,000 lakini katika jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri katika uhaba wa watumishi 95 anasema tutapewa watumishi 18. Haoni umuhimu wa kuongeza idadi hiyo ikafika angalau watumishi 50 kwa sababu tutaajiri watumishi 10,000?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kutarajia michango kutoka CHF ni jambo zuri lakini wote tumeona Wabunge hapa katika michango yao mbalimbali wameelezea ambavyo jambo hili linaendelea kuwa gumu kwa sababu ya kipato duni, lakini pia kutokana na ukosefu wa elimu ya uhamasishaji. Sasa kutarajia fedha kutoka CHF ni kama vile tunaota tu ndoto ambayo inaweza isiwe ya kweli. Kwa hali hiyo, kutokana na mazingira ya hospitali hiyo ambayo nimeshayaeleza, hii fedha iliyotengwa shilingi milioni 90, haitoshi hata on call allowance kwa muda wa miezi mitatu, je, Serikali haioni sababu kwa mazingira hayo ambayo nimeelezea kwamba, Hospitali ya Mafinga iko along the highway, ikaongeza kiwango hicho japo hata theluthi moja ya fedha hizo? Ahsante
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba yetu ya jana Mheshimiwa Waziri wangu wa Afya na Waziri wa Utumishi walielezea suala hili la watumishi ambapo taarifa inaonesha watumishi takribani 10,000 wataajiriwa na maombi ya awali ya kibali kutoka Mafinga yalikuwa yanahitaji watumishi 18. Kwa hiyo, katika mgawanyo wa watumishi hawa 10,000 Halmashauri hii ilikuwa na watumishi 18. Hata hivyo kwa sababu mahitaji ni makubwa tutaangalia tutafanya vipi ili kuondoa matatizo ya wananchi katika sekta ya afya. Kwa hiyo, concern kwamba watumishi 18 watakuwa ni wachache hili tutaliangalia, lakini hayo ndiyo maombi ambayo yametoka katika Halmashauri ya Mafinga.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la ukosefu wa uhamasishaji na kwamba hizi fedha ni ndogo, naomba niwaambie ndugu zangu katika maelekezo yetu mbalimbali tulisema sasa hivi jambo muhimu katika sekta ya afya, ukiachia CHF na mifumo mingine, ni ukusanyaji wa mapato. Nimesema tulivyofanya mazoezi ya kukusanya mapato kwa njia ya electronic mapato yamebadilika sana na jana Waziri wa Afya alikuwa akitoa mifano katika Hospitali ya Mbeya badala ya kukusanya shilingi milioni 70 kwa mwezi sasa inakusanya mpaka shilingi milioni 500. Hospitali ya Sekou Toure pale Mwanza badala ya kukusanya shilingi milioni 150,000 mpaka milioni 200,000 kwa mwezi sasa inakusanya shilingi milioni 3.5 kwa siku. Nenda kule Tumbi badala ya kukusanya shilingi milioni 200,000 kwa siku sasa tunakusanya shilingi milioni nne kwa siku, haya ni mabadiliko makubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili ndiyo maana tunatoa msisitizo kwamba Wabunge tuhakikishe, katika hospitali zote mifumo ya electronic iwe imefungwa ili fedha ziweze kukusanywa na ziende katika mgao sahihi wa kununua vifaa tiba na madawa mwisho wa siku mtaona kila kitu kinaenda vizuri. Tusipozingatia haya, hata tukipeleka fedha bado tutakuwa na matatizo. Kwa hiyo, ajenda yetu kubwa ni kwamba, tutumie mifumo sahihi ya electronic kwa ukusanyaji wa mapato kwa ajili ya huduma ya afya.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa, Mheshimiwa Naibu Waziri anasema ni gharama kubwa na ni kweli ni gharama kubwa kufungua Ubalozi kamili. Na kwa kuwa, katika mahusiano ya kimataifa kuna kitu kinaitwa Honorary Consul, ambayo haina gharama zozote za kiuendeshaji. Je, sasa Serikali iko tayari kufungua Honorary Consul au Ofisi ya Uwakilishi wa Heshima huko Lubumbashi ili kusudi Tanzania iendelee kulinda maslahi yake ya kibiashara? Kwa kuwa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo population kubwa inaishi Eastern Congo na ndio ambayo tunafanya nayo biashara katika Miji ya Lubumbashi, Kalemie, Likasi, Kolwezi, Kisangani mpaka maeneo ya Mbujimai.
Mheshimiwa Naibu Spika, na kutoka Lubumbashi mpaka kufika Kinshasha kupata huduma ni umbali wa kilometa zinazidi 2,300; yaani mtu akitoka Dar-es-Salaam atafika Lubumbashi na aliyetoka Lubumbashi hajafika Kinshasa. Kwa hiyo, hili strategically ni eneo zuri kibiashara.
Je, Serikali iko tayari kufungua Honorary Consul?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama alivyosema kwamba, je, Serikali ya Tanzania iko tayari? Anajua kwamba, kuna gharama kubwa ya kufungua Ubalozi na anashauri kwamba kwa nini tusifungue Honorary Consul.
Mheshimiwa Naibu Spika, labda nimhakikishie tu Mheshimiwa Cosato Chumi, wakati kipindi hiki cha session za Bunge zimeanza wakati huu wa bajeti Wizara yangu pamoja Wizara kama nne hivi tumekaa tukijadili suala la mahusiano yetu kati ya sisi na Congo na Kamati zinaendelea kukaa na hili ni moja ya ufunguzi ambao tumeliwekea mkakati. Kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba, tunajua kwamba Lubumbashi pamoja na Kinshasa ni sehemu mbali tofauti kabisa, lakini tuna wafanyabiashara wengi sana ambao wanakwenda Congo na wanafanya biashara vizuri, ila wanapata tatizo la coordination. Hilo tumeliona na kazi inaendelea kufanyika.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Serikali inawauzia kiwanda cha Mgololo nusu ya bei 14,000 badala ya 28,000; je, Wizara iko tayari sasa kuwauzia pia wavunaji wadogo wadogo wa Mafinga na Wilaya ya Mufindi kwa ujumla nusu ya bei kama inavyouzia MPM?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa kumekuwa na ujanja ujanja mwingi katika suala zima la utoaji vibali na kama nilivyosema jana tuko karibu na waridi lazima tunukie waridi; je, Wizara iko tayari sasa katika kutoa vibali, itoe by name and by location ili kusudi wakazi wanaozunguka msitu waweze pia na wenyewe kunufaika kwa kupata vibali hivyo badala ilivyo sasa orodha inaonesha kuna watu wanapata vibali lakini majina ya watu hao sio wanaozunguka msitu. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza kuhusu nusu bei kwa kiwanda cha Mgololo na uwezekano wa kuuza kwa bei hiyo hiyo bidhaa hiyo kwa wafanyabiashara wadogo wadogo au mwananchi mmoja mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili hoja yake ni miongoni mwa hoja kubwa, nzito zilizotolewa wakati wa mjadala wa bajeti jana na kwa sababu hiyo maandalizi ya majibu ya kina yapo kwenye majawabu ya ufafanuzi wakati Mheshimiwa Waziri atakaposimama na nitakaposimama mimi. Sasa kwa kuokoa muda namwomba Mheshimiwa Mbunge asubiri wakati tutakapokuwa tunahitimisha hotuba jioni. Atapata majibu ya kina kuhusu swali hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili la ujanja ujanja na uwezekano wa kutoa vibali kwa majina na kwa maeneo; jawabu ni kwamba jambo la msingi hapa linalohitajika ni uwazi. Wananchi wangependa kuona uwazi zaidi kuliko ilivyo sasa kwamba tutakapotoa takwimu kwamba watu gani wamepata mgao, basi ni vyema watu hao wakaonekana miongoni mwa jamii wazi wazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nimetembelea kwenye shamba la msitu la Sao Hill moja ya mambo ambayo nilisema ni kwamba, kuanzia baada ya ziara yangu wakati utakapofika licha ya ule utaratibu wa kusubiri kupitia mwongozo mzima, hili moja ni la wazi kabisa kwamba tunakwenda kushirikisha Serikali tangu kwenye ngazi ya vitongoji na vijiji si tu kwamba kumtaja mtu mmoja mmoja lakini Serikali kwa ujumla wake kwa kutumia mfumo wake utashirikishwa katika zoezi zima la ugawaji wa malighafi hizi.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona. Kwa kuwa nguzo nyingi za umeme katika nchi hii zinatoka Sao Hill huko kwetu Mafinga ambako pia kuna Kata ya Sao Hill yenye vijiji vya Sao Hill na Mtula. Je, Serikali iko tayari kuenzi Kijiji cha Sao Hill na maeneo jirani ambayo mpaka leo hakuna umeme kwa kufanya upendeleo maalum wa kupatiwa kwa kuwa huko ndiko zinakotoka nguzo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa eneo la Mafinga linazalisha nguzo nyingi hapa nchini. Wala hakuna haja ya kuwa na upendeleo kwa sababu vijiji vyake vyote vimo kwenye REA Awamu ya III. Eneo la Sao Hill alilosema liko REA Awamu ya Tatu lakini mpaka eneo la Isalanavu pia liko kwenye REA Awamu ya III. Kwa hiyo, maeneo yake yote yatapata umeme kwenye REA Awamu ya III.
MHE. COSATO D. CHUMI: Nashukuru Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuniona, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, na mimi naomba kuuliza swali dogo la nyongeza, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mafinga Mjini.
Katika Jimbo la Mafinga Mjini tuna shule mbili za sekondari za bweni, mojawapo ni shule ya sekondari ya bweni ya Changarawe. Katika kutekeleza majukumu kama wananchi, bodi ya shule kwa kushirikiana na wazazi imeanza na inaendeleza jitihada za kujenga jiko la kudumu na bwalo la chakula kwa ajili ya wanafunzi hao. (Makofi)
Je, Serikali kwa kilio changu kile kwamba hii ni Halmashauri mpya ipo tayari kwa kutuongezea nguvu ili kukamilisha jiko hilo la kudumu na bwalo la chakula kwa ajili ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anasema ujenzi wa bweni pamoja na jiko katika Shule ya Sekondari ya Changarawe, naomba niseme kwamba nimelisikia hili jambo, Mheshimiwa Cosato Chumi tumezungumza mambo mengi, ukiachia miradi yake ya maji iliyokuwa imekwama amepambana, na hili naomba niseme kwa sababu hapa siwezi kusema kuna bajeti special kwa ajili ya bweni hili, lakini katika mchakato wetu, kama tulivyoahidiana kwamba mara baada ya Bunge tutapitia, nitakwenda kukagua Shule ya Sekondari ya Iyunga ambayo ujenzi wa mabweni unaendelea, tutapita kuangalia kwa pamoja, mikakati gani tuifanye ili bweni likikamilika na jiko likikamilika, watoto watakula na kuishi sehemu rafiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hatuoni tatizo katika eneo hilo, lakini ni lazima tushirikishane kwa pamoja tuangalie ni mkakati gani wa haraka utaweza kusaidia katika eneo hili la Shule ya Sekondari ya Changarawe. Mheshimiwa Mbunge, naomba niseme kwamba jambo hili nimelipokea tutakapokuwa pale field tutapanga mikakati ya pamoja lengo ni kuwasaidia vijana wetu.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii, kwa kuwa Halmashauri ya Mji wa Mafinga na maeneo mengi ya mijini kumekuwa na kero kubwa kama hii ambayo imeelezwa kwenye swali la msingi iikiwa ni pamoja na timua timua ya wafanyabiashara ndogo ndogo. Sasa kwa kuwa Halmashauri ya Mji wa Mafinga ni Halmashauri mpya bado haijakuwa na uwezo wa kutenga maeneo kwa maana ya kwamba kifedha, kwa ajili ya wafanyabiashara ndogo ndogo. Je, Serikali iko tayari kutusaidia sisi kama Halmashauri mpya japo kusudi kutuwezesha kutenga maeneo hayo na hivyo wafanyabiashara kuwapunguzia bugudha bugudha wamama wauza vitumbua, wauza matunda, vijana wachoma mahindi na wote wanaofanya shughuli za namna hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, si muda mrefu nilifika pale Mafinga nilifika Jimboni kwake Mheshimiwa na nilienda mpaka katika kituo kile cha watoto walemavu pale, lakini kwa maelekezo ya Mheshimiwa Mbunge mwenyewe. Ni kweli Halmashauri ile ni mpya, naomba niseme sisi tutakupa ushirikiano mkubwa kama Serikali kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Lakini suala zima la utengaji wa eneo naomba niwasihi Waheshimiwa Wabunge jambo hili linaanza kwetu sisi wenyewe, kwa sababu sisi ndio tunajua wapi eneo la wazi lipo nini kifanyike.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile atuelekezi watu waende wakapange biashara katika maeneo ya barabara, hilo jambo halikubaliki. Kwa hiyo, naomba nikusihi Mheshimiwa Mbunge ninyi pale kama Baraza la Madiwani naomba anzeni, kwa sababu mnanza kufanya mambo mazuri zaidi. Na sisi Ofisi ya Rais – TAMISEMI tutashauri vizuri nini kifanyike ili mradi wananchi wa Mafinga pale wapate huduma bora hasa ya suala zima ya ujasiriamali kufanya biashara katika maeneo yao.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri sana, hata hivyo kwa namna kero ya askari hawa mgambo walioajiriwa na mamlaka zetu za Serikali za Mitaa na hasa za Mijini ni kero kubwa na inaleta usumbufu mkubwa na miongoni mwa mambo ambayo husababisha na pengine kupelekea hata Serikali kuchukiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta yetu binafsi nchini haijarasimishwa sana na kwa hivyo wananchi wetu wanahangaika kufanya shughuli mbalimbali ili wapate kipato na kwa hakika ndio wanaojenga uchumi wa nchi yetu. Lazima tuwe na staha katika kushughulika nao, maana hata hivyo hatujaweza kuwatengea maeneo ya kufanyia shughuli zao rasmi lakini hatuna mfumo rasmi sana wa mitaji na kwa hivyo kitendo cha askari mgambo kuvuruga biashara zao, kukamata na kutaifisha mali zao kitendo hiki hakikubaliki na Serikali kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuziomba mamlaka zote na hasa za Mijini zinazounda majeshi haya kwa maana ya mgambo chini ya Sheria ile ya Jeshi la Akiba linalosaidiana na Polisi, kuhakikisha kwamba kila operation wanayoifanya basi inakuwa na makubaliano maalum katika mamlaka husika kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na baada ya pale operation yeyote inayofanyika, lazima isimamiwe vizuri, haiwezekani mgambo wa Jiji wakawa wanakamata pikipiki, wanakamata bodaboda, wanakamata yaani ni vurugu tupu. Kwa hiyo, hili jambo halikubaliki nafahamu na nafikiri iko haja tukafanya mapitio ya Jeshi la Mgambo ambalo linaundwa kwenye hizi Mamlaka za Mijini na kuona kama kuna haja ya kuja na mwongozo na utaratibu mpya pamoja na kwamba tunafahamu kwamba iko sheria hili jambo hili liweze kukomeshwa kwa sababu wanaleta mateso na vilio vingi katika familia ambazo zinataifishiwa mali zao.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa nchi yetu kiutalii na kitakwimu tunaambiwa ni nchi ya pili kwa kuwa na vivutio baada ya Brazil na ili kunufaika zaidi na utalii ambao tunaambiwa pia kitakwimu ndiyo sekta zinazoongoza kwa kuingiza fedha za Kigeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kusudi kuiwezesha Bodi ya Utalii Tanzania kufanya promotion na advertisement kwa kiwango cha kuridhisha na hivyo kuongeza idadi ya watalii; je, Serikali iko tayari sasa kuunda chombo maalum ambacho kitasimamia ile Tourism Development Levy kusudi kuiwezesha TTB kufanya promotion na advertisement kwa kiwango kikubwa ili kuvutia watalii wa kutosha na hivyo kuongeza mapato ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli na nafikiri hapa anatukumbusha tu; kama ambavyo nimesema mara nyingi, nchi yetu ina vivutio vingi vya utalii; na ni ya pili baada tu ya Brazil. Kuhusu suala la Tourism Development Levy (TDL) namna ambavyo inaweza kuchangia zaidi na inavyoweza kusaidia zaidi Bodi ya Utalii, (Tanzania Tourism Board) kufanya majukumu yake vizuri zaidi na wazo la kuanzishwa kwa chombo kingine tena cha kuweza kusimamia TDL, napenda kujibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi, suala la (Tourism Develeopment Levy - TDL) kama lilivyo, halina matatizo yanayohitaji kuanzishwa kwa chombo kingine kusimamia. Tunahitaji kuboresha vizuri zaidi usimamizi kupitia vyombo vilivyopo chini ya Serikali hivi sasa, lakini ni kweli kwamba tunakwenda sasa kujipanga vizuri zaidi ili mapato yanayopatikana kutokana na Tourism Develepment Levy yaweze kusaidia zaidi Bodi ya Utalii kutimiza majukumu yake ambayo kwa kiwango kikubwa ni kutangaza utalii ndani na nje ya mipaka ya nchi hii kwa ajili ya kuboresha mapato ya Taifa kupitia Sekta ya Utalii.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri naomba sasa kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, je, ni lini sasa Serikali itaanza kutekeleza kwa vitendo, Waraka namba tatu (3) wa mwaka 2014 unaoelekeza kwamba kutakuwa na posho ya madaraka kwa ajili ya Walimu Wakuu wa shule za Msingi, Walimu wa Sekondari, Waratibu wa Elimu wa Kata na Wakuu wa Vyuo? Sasa utekelezaji wake utaanza lini maana ni mwaka wa pili sasa unakwenda?
Mheshiminiwa Naibu Spika, swali la pili la nyongeza; kwa kuwa umoja wa Wakuu wa Shule za Sekondari hapa nchini maarufu kwa jina la TAHOSSA ulikuwa ukitumia sehemu za michango, kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo pamoja na kufanyisha mitihani ya mock na ujirani mwema ambao ililenga sana kuimarisha na kuboresha taaluma. Sasa, kwa kuwa tunaenda na mpango wa elimu bila malipo, je, Serikali iko tayari kuisaidia ruzuku TAHOSSA ili iendelee kufanya kazi zake kwa ufanisi?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusu suala la utekelezaji wa waraka namba tatu wa posho ya madaraka. Hili ni swali jipya halina uhusiano na swali la msingi kwa hiyo majibu yake yataandaliwa na kuletwa katika kipindi kingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali la pili la TAHOSSA ambalo linaendana na utekelezaji wa Sera ya Elimu Msingi ya Mwaka 2014, ni kwamba katika mwongozo waraka namba sita umebainisha wazi mgawanyo wa fedha na hivyo basi kama kuna mahitaji yanayohusiana na mitihani, fedha zinazotolewa kwa ajili ya elimu bure kuna kipengele cha mitihani. Kwa hiyo, napenda kuchukua nafasi hii kusisitiza kwamba matumizi ya fedha zinazotolewa kwa ajili ya elimu msingi yazingatie mwongozo uliotolewa.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Pamoja na majibu hayo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, katika Jimbo la Mafinga wananchi wa Kijiji cha Lungemba wamepisha eneo kwa ajili ya upanuzi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Lungemba na uthamini umeshafanyika. Je, ni lini sasa Serikali itawalipa wananchi wale ambao wamejitolea ardhi yao kwa ajili ya upanuzi wa Chuo cha Maendeleo ya Lungemba?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri kabla ya Bunge la bajeti nilifika Jimboni kwa Mheshimiwa Chumi na nafahamu miradi mbalimbali ambayo inatekelezwa pale. Kama kumbukumbu zangu ziko sahihi tayari zimetengwa shilingi milioni 200 kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi wa eneo lile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kulikuwa kuna mgogoro kidogo, kuna baadhi ya wananchi walikubali kuchukua hiyo fidia ambayo walikuwa wanapewa, lakini kuna baadhi ya wananchi hawakukubaliana na fidia ambayo ilikuwa inatolewa na hivyo hawakuzichukua na ulipaji wa fidia ukawa kama umesimama. Hivyo, namsihi Mheshimiwa Mbunge, akishirikiana na viongozi wenzake kwenye Halmashauri, watumie jitihada za kuwashawishi wananchi wakubaliane na fidia ambazo zinatolewa na Serikali ili chuo hicho kiweze kuendelezwa na wananchi waweze kupata huduma inayostahili. Nitoe rai kwa wananchi wa eneo lile kwamba miradi ya maendeleo inapokuja kwenye maeneo yao waikumbatie na badala ya kukwepa fidia washirikiane na Serikali ili kuendeleza miradi husika.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu imeeleza kwamba kufunguliwa kwa Ubalozi kutategemea masuala ya kibajeti; je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kufungua ile tunaita Honorary Consul kwa sababu ile haina gharama zozote ambazo Serikali itaingia zaidi ya kupata tu mtu ambaye ni mwaminifu na mwadilifu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kufungua Honorary Consuel ambapo siyo suala lenye gharama kibajeti kama ambavyo Serikali imejibu katika swali la msingi, ni jambo la msingi kwa sababu litawezesha kufungua fursa zaidi za kiuwekezaji siyo tu katika Sudan ya Kusini, lakini pia katika maeneo mengine ambako Serikali imeshindwa kufungua Balozi kwa sababu ya ukosefu wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kufungua fursa hizi za uwakilishi wa heshima, tunapanua wigo wa kuongeza uwekezaji na biashara na hivyo kuongeza mapato ya Serikali ambayo mwisho wa siku wananchi wa Mafinga na Tanzania kwa ujumla watanufaika katika kuboresha huduma zao za kijamii. (Makofi)
Je, Serikali iko tayari pia sasa kufungua Uwakilishi wa Heshima katika Mji wa Lubumbashi ambako kuna fursa kubwa za kibiashara baina yetu sisi Tanzania na nchi ya Demokrasia ya Kongo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba kufungua Uwakilishi wa Heshima ni njia mojawapo ya kuwa na uwakilishi wa nchi yetu katika nchi nyingine, lakini vilevile kuna utaratibu wa Kikonseli lakini na ule utaratibu wa kawaida wa kufungua Ubalozi wenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizo ni kati ya njia ambazo tungeweza kutumia nchini Sudan Kusini, lakini kwa sasa Wizara inafikiria zaidi kujipanga kufungua Ubalozi kamili badala ya kufungua Consul au kutafuta Uwakilishi wa Heshima. Hii ni kwa sababu nchi ya Sudan Kusini ni moja kati ya wanachama wa Jumuya yetu ya Afrika Mashariki, kwa hiyo, ningependa kuwa na Ubalozi kamili.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wakati bado tunaelekea kule, tunajipanga, nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kitendo cha nchi ya Sudan Kusini kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki inatoa fursa nyingi sana na inarahisisha wananchi kuweza kunufaika na fursa zilizoko kule hata bila kuwepo na Ubalozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki unaruhusu pamoja na mambo mengine urahisi wa kusafirisha bidhaa, lakini vilevile huduma na kazi kwenye hizi ambazo ni wanachama.
Kwa hiyo, tayari kuna mazingira mazuri ambayo yanarahisisha wananchi kuweza kunufaika na hizo fursa hata bila kuwa na uwakilishi wa kiheshima bila kuwa na Consul au kuwa na Ubalozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema Wizara inajipanga, tunatambua umuhimu wa Sudan Kusini kama wanachama wa Afrika ya Mashariki, tunatambua fursa lakini huko ndiyo tunaelekea, lakini tunajipanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Mheshimiwa Mbunge amezungumzia kuhusu kufungua Uwakilishi wa Kiheshima Lubumbashi. Napenda kumjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba, ni kweli kabisa tunatambua fursa zilizopo Lubumbashi, tunafahamu fursa zilizopo katika ukanda huo wa DRC, lakini kwa sasa Serikali na Wizara imejielekeza zaidi katika kuimarisha shughuli za Kibalozi kwa sababu tunafikiri bado inakidhi matakwa hayo ya fursa zilizopo, nashukuru sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Nami ni mdau mkubwa wa michezo na hasa mchezo wa soka. Mchezo wa soka ni mchezo unaopendwa nadhani kuliko mchezo wowote duniani na ni mchezo ambao unaweza kutumika kuwa kiunganishi muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, kulikuwa na tuhuma za rushwa katika suala hili kwa kuwa, mchezo huu ni kipenzi cha watu wengi, je, Waziri anaweza kuliambia Bunge hili kwamba, ni lini sasa uchunguzi huu utafika mwisho na wahusika kuchukuliwa hatua ambazo zinatakiwa kuchukuliwa? Ahsante sana.
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema TAKUKURU wanakamilisha utaratibu. Wakati mwingine uchunguzi wa makosa hasa ya rushwa ambayo kwa namna moja ama nyingine wahusika wa pande mbili wanakuwa wamekubaliana huwa yanaweza yakachukua muda mrefu na wakati mwingine kupata uhalisia wake inakuwa ngumu, lakini habari nilizonazo ni kwamba, TAKUKURU wako hatua za mwisho za kukamilisha uchunguzi huo na baada ya kukamilisha uchunguzi huo, hatua zinazostahiki zitachukuliwa.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kwa niaba ya Mheshimiwa Mahmoud Mgimwa, Mbunge wa Mufindi Kaskazini kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kuna mradi wa densification na underline transformer. Mradi huu unafikisha umeme katika maeneo ambayo REA Awamu ya Pili ulifikisha katika baadhi ya Kata lakini siyo vijiji vyote.
Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusiana na maeneo ambayo Kata zile zimefikiwa na umeme lakini siyo vijiji vyote na chini ya mradi huo wa densification na underline transformer inaeleza kwamba unaweza kufikisha umeme ndani ya umbali wa kilometa 10, nini kauli ya Serikali kwa wananchi wa maeneo hayo?
Swali la pili, Mji wa Mafinga ni kati ya miji michache inayokua kwa kasi hapa nchini na ndiyo kitovu cha shughuli za uchumi za Wilaya ya Mufindi, lakini maeneo mengi hayajafikiwa na umeme kama vile Machinjio Mapya, Makalala, Ihongole, Mwongozo na Lumwago. Je, Serikali iko tayari kujenga sub-station ili kuwezesha wananchi kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa asilimia mia moja?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa mradi wa REA awamu ya tatu kimsingi una sehemu tatu. Sehemu ya kwanza ni kupeleka umeme katika maeneo yote ambapo kuna miundombinu ya awamu ya pili lakini component ya pili na kwa niaba ya Mheshimiwa Chumi na Waheshimiwa wananchi wa kule Mufindi pamoja na Mafinga ni kwamba awamu ya tatu itahusisha sasa kupeleka umeme kwenye vitongoji na vijiji vyote kupitia mradi aliosema densification.
Mradi wa densification unapeleka umeme kutoka kwenye miundombinu mikubwa kwenda kwenye vijiji na vitongoji. Nimhakikishie Mheshimiwa Chumi kwamba, vijiji vyake vyote vya Sao Hill vitapata umeme kupitia mradi huu, hata pale Changarawe atapata umeme. Isalavanu, Itubiravamu na Ibongoboni vyote vitapata umeme kupitia mradi huu. Nimhakikishie hata Kijiji chake cha Mkalala pamoja na Bubirayinga vitapata umeme kupitia mradi huu wa Itubiravamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali lake la pili juu ya maeneo ya Mafinga. Ni kweli kabisa maeneo ya Mafinga sasa yana kazi kubwa. Mafinga sasa inapata umeme kutoka Iringa ambako ni kilometa 70, pia kutoka Mgololo kilometa 60, sasa ipo haja kwa kweli kujenga sub-station. Nimhakikishie tunajenga sub-station mwaka wa fedha unaokuja.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja
na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwanza nieleze masikitiko yangu
kwamba yaani kumbe mpaka leo Bodi haina tovuti, 2017, this is very bad, ni
jambo la kusikitisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niende kwenye swali langu la kwanza la
nyongeza, nimeona muainisho wa hizo gharama, wasanii wanapokwenda
kusajili, pamoja na hizo gharama lakini wanalazimika kwenda kupata huduma hii
Dar es Salaam tu haitolewi katika maeneo mengine. Wakishapata hii huduma ya
kutoka BASATA kusajili COSOTA na Bodi ya Filamu, kuna huduma nyingine
kwenda TRA ili wapate stika ambayo ni mapato na stika zinatolewa tu Makao
Makuu ya TRA Dar es Salaam. Je, Serikali iko tayari kuhakikisha kwamba angalau
Ofisi hizi za BASATA, COSOTA na Bodi ya Filamu zinakuwepo hata katika ngazi ya
mikoa ili kuwarahisishia wasanii na kuwapunguzia gharama? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuna hizi filamu za kutoka nje
maarufu sana kwa jina la mazagazaga kwa sababu unakuta wametandika chini
zimezagaazagaa, gharama yake maximum kwa CD moja ni Sh.1,200 lakini
hazitozwi gharama zozote za usajili wala hakuna mapato yoyote ambayo Serikali
inapata. Kwa kulinda kazi za ndani za wasanii wetu wa filamu wa ndani ambao
CD zao sasa zimeshuka thamani hadi Sh. 2,000 halafu wanashindana na za nje za
Sh.1,200 na Serikali inakosa mapato, je, inasemaji katika kudhibiti filamu hizi za
kutoka nje, imeshindwa kabisa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa
Naibu Spika, swali la kwanza anataka kujua kama kuna utaratibu wowote
ambao Serikali imefanya ili wasanii waweze kupata vibali kutoka mikoani.
Ninachoweza kusemea ni kuhusiana na Bodi ya Filamu, kama nilivyosema awali,
Bodi ya Filamu tayari inazo ofisi katika Wilaya na Mikoa na kule kuna Bodi za
Filamu za Mikoa na Wilaya ambapo RAS kwa upande wa Mkoa ndiye Mwenyekiti
na Afisa Utamaduni ndiye Katibu na kwa upande wa Wilaya DAS ni Mwenyekiti
na Afisa Utamaduni wa Wilaya ni Katibu na kuna wajumbe wengine katika Bodi
hizi. Kwa hiyo, vibali vinatoka pia katika wilaya na mikoa na siyo lazima wafuate
huduma hizi Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa TRA zipo ofisi za mikoa lakini
upande wa COSOTA sina uhakika sana. Hata hivyo, tunafanya mazungumzo na
vyombo vyote hivi ambavyo vinadhibiti wizi wa kazi za wasanii na wajumbe wake
wote ni wajumbe wa Kamati ya Urasimishaji na hivyo basi, tunafanya kila jitihada
ili tuweze kuona tunamkomboa msanii kuanzia ngazi za wilaya, mkoa na hata
makao makuu Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa BASATA, mpaka sasa tunataka
kufanya utaratibu wa usajili kwa njia ya mtandao pamoja na Bodi ya Filamu.
Hivyo, niwahakikishie wasanii kwamba huduma hizi zitafikishwa kwao na
watakuwa hawapati usumbufu sana kufika Dar es Salaam kwa sababu
tunawatakia mafanikio.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa filamu za nje, nadhani wengi
tumekuwa mashahidi kwamba Serikali inafanya kila jitihada. Zoezi la urasimishaji
lilianza tangu mwaka 2009 ambapo kazi za wasanii zilianza kuwekewa ushuru wa
stempu tangu mwaka 2013 kwa Sheria ya Ushuru wa Stempu. Kwa zile kazi
ambazo zinatoka nje na hazifuati utaratibu zimekuwa zikikamatwa na wahusika
kuchukuliwa hatua. Napenda kuwatangazia kwamba zoezi hili ni endelevu,
tumekuwa tukifanya msako au opereshenitangu 2014 hadi 2016 na tunaendelea.
Hivyo, nawaomba wote ambao wanauza kazi za wasanii nje ya utaratibu
wafuate utaratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu
Spika, nakushukuru. Nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini pamoja na
majibu yake mazuri, naomba kuongezea kwenye sehemu ya pili ya swali la
Mheshimiwa Cosota Chumi. Ni kweli tatizo la kazi za sanaa kutoka nje katika nchi
yetu ni kubwa na baya na linaua kwa kiasi kikubwa kazi za sanaa za ndani. Ili
kushughulika na tatizo hili kuna sheria za vyombo zaidi ya vitano zinahusika. Kuna
Sheria za TRA, BASATA, Bodi ya Filamu, COSOTA, ukizijumlisha zote kwa pamoja
ndiyo at least unaweza kushughulika na tatizo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inapitia upya sheria hizi na kuangalia
upungufu uliopo, turekebishe na tuzi-harmonise kwa pamoja ili tuweze kulimaliza
tatizo hili. Kwa sheria zilizopo, namna ya kushughulika na tatizo hili bado ni ngumu
sana. Kwa hiyo, tunachoweza kuahidi hapa ni kwamba tunazipitia na tuko
mahali pazuri na tukilikamilisha zoezi hilo kazi hii itakuwa imekwenda vizuri na kwa
hiyo tutapambana na tatizo hili la piracy kwenye nchi yetu.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, katika sheria hii na kwa mujibu wa watu wa TRA, magari ya ambulance yana-fall katika HS Code 87039010 ambayo kitaalamu kwenye kodi inakuwa zero rated yaani haina kodi isipokuwa inatakiwa kulipiwa kodi ya VAT. Sasa swali langu la kwanza, kwa kuwa kwa mwaka wa pili sasa mfufulizo Serikali haijaweza kutenga fedha za kununua magari ya wagonjwa, inaonaje Wizara ikaanzisha mchakato wa kubadilisha sheria kwa kuileta hapa Bungeni ili magari ya wagonjwa yaingie kwenye item no. 7 kusudi na yenyewe ya-enjoy msamaha wa kutolipa VAT? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali
imekiri kwamba haitaweza kununua magari ya wagonjwa isipokuwa Halmshauri zenyewe zitafute fedha kwa ajili hiyo na Halmashauri nyingi hazijaweza kuwa na uwezo huo wa kununua hayo. Pia Waheshimiwa Wabunge wengi wanaomba misaada kutoka kwa watu mbalimbali jambo ambalo siyo guaranteed kwamba utapata gari. Je, Serikali iko tayari kwa wale Waheshimiwa Wabunge na Halmashauri ambazo zitapata magari ya misaada kuwalipia gharama za VAT?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza, mpaka sasa utaratibu ambao unatumika haujaleta usumbufu wowote ule kama Mbunge ama mwananchi yeyote yule mwenye nia ya kutaka kununua gari la wagonjwa atauelewa na kuufuata kwa kadiri ambavyo umewekwa. Sheria ya Kodi ya mwaka 2014 ambayo inasimamiwa na
wenzetu wa Wizara ya Fedha na Mipango imempa mamlaka Waziri mwenye dhamana ya afya kwa maana hiyo kwa sasa ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kutoa mapendekezo ya msamaha kwa Waziri mwenzake wa Fedha na Mipango kwa magari na vifaa mbalimbali ambavyo vimeainishwa kwenye Jedwali la Saba la sheria hiyo ninayoisema.
Mheshimiwa Spika, hakujawahi kuwa na utata/shida yoyote ile kama mtu atafahamu utaratibu huu na akatoa taarifa kwa Waziri wa Afya kwamba ana malengo ya kuagiza gari la wagonjwa ama vifaa mbalimbaliv ya hospitali na
Waziri wa Afya akiridhia basi atawasiliana na mwenzake Waziri wa Fedha na Mipango na mara nyingi kodi zote huwa zinakuwa waved (zinaondolewa). Kwa maana hiyo, hakuna haja ya kufanya mabadiliko yoyote ya kisheria.
Mheshimiwa Spika, lakini swali lake la pili la nyongeza kwamba Serikali ibadili utaratibu huu kwa sababu imeshindwa kuagiza ambulance, hapana. Kipaumbele cha kununua ambulance kwa kweli kinapaswa kutoka kwenye Halmashauri zenyewe husika na Halmashauri kama mamlaka za Serikali zinazojitegema, zinafahamu zaidi mahitaji yake na kipato chake. Halmashauri zinapaswa tu kuweka kipaumbele kwenye kununua magari ya wagonjwa na wakishirikiana na sisi hakuna kitakachoshindikana watapata magari hayo. Sisi kama Wizara ya Afya tunachokifanya kwa kuwa tuna-access na wadau mbalimbali wa maendeleo tumekuwa tukishirikiana nao kuwaomba watusaidie kununua
magari hayo ambayo mara kwa mara tumekuwa
tukiyatawanya kwenye Halmashauri mbalimbali nchini lakini sio jukumu letu la msingi kufanya hivyo.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na jitihada za Serikali kupeleka fedha za maendeleo, ugatuaji lazima uende sambamba na upelekaji wa resources hususan fedha za OC. Fedha za OC zimekuwa haziendi kwa kiwango kinachokusudiwa matokeo yake imekuwa inaathiri mipango inayopangwa na Halmashauri kwa kutekelezwa kutokana na makusanyo ya ndani. Matokeo yake fedha za makusanyo ya ndani sasa zinatumika kuendeshea ofisi badala ya kuelekezwa kwenye shughuli za maendeleo kama inavyoelekeza ile 50%, ikiwepo 5% ya vijana na wanawake. Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha kwamba inapeleka fedha za OC ipasavyo ili kusudi makusanyo ya ndani yasiathiri utekelezaji wa shughuli za maendeleo, kama ambavyo zimepangwa na Halmashauri zetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli na nakumbuka kwamba tulipokuwa katika kikao chetu cha ALAT kule Musoma, concern kubwa ilikuwa siyo fedha za OC peke yake hata pesa za maendeleo. Waheshimiwa Wenyeviti wa Halmashauri na Wakurugenzi wali-raise jambo hili katika ofisi yetu na ndiyo maana katika kipindi cha katikati baada ya harakati hizi kufanyika mmeona tumepeleka fedha nyingi sana za maendeleo na pesa za OC.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wangu siku zote amekuwa akisema definition ya OC maana yake ni Own Source plus zile fedha nyingine zinazotoka Serikali Kuu. Kwa hiyo, sisi Serikali tutajitahidi kwa kadiri iwezekanavyo OC iweze kwenda, lakini niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge katika maeneo yetu vilevile tuhakikishe makusanyo ya ndani haya yanaimarika kwa kiwango kikubwa kwa sababu tumeshuhudia hivi sasa kuna Halmashauri zingine zimefanya vizuri lakini nyingine zinasuasua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili ni jambo letu sisi sote. Upande wa Serikali tutajitahidi kufanya kila liwezekanalo kuziwezesha Halmashauri zetu ziweze kufanya kazi vizuri kwa sababu bila ya hivyo maana yake utekelezaji wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi utakuwa una matatizo. Kwa hiyo, naomba niwahakikishie kwamba Serikali itafanya kila liwezekanalo, tutakusanya mapato lakini tutayapeleka katika Halmashauri zetu ili miradi iweze kutekelezeka vizuri.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya watumishi ambao fedha zao hazijapelekwa kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ninaomba kuuliza swali moja la nyongeza. Hapa nina barua ya mtumishi ambaye anatarajia kustaafu tarehe 15 Juni; mpaka leo makato yake ya miezi 18 hayajapelekwa jambo ambalo litaathiri pensheni yake.
Je, Serikali haioni haja sasa ya kuwa na takwimu ya watumishi ambao wanatarajia kustaafu ili kusudi makato yao yaweze kupelekwa kwenye mifuko na watakapostaafu wapate kile kinachostahili kwa wakati? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma na matakwa ya Serikali yetu kuhakikisha kwamba watumishi wote ambao wamekuwa wakichangia katika Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kulipwa mafao yao ya pensheni kwa wakati. Hivyo, tumekuwa tukitoa maelekezo na maagizo mbalimbali ili taasisi zote zinazoshughulikia malipo ya pensheni kwa wafanyakazi wa Serikali pia kwa wafanyakazi wa private sector wahakikishe kwamba watumishi wanalipwa mafao yao kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukichua hatua pale mafao ya watumishi yanapochelewesha. Ninamuomba Mheshimiwa Chumi atuletee taarifa za mtumishi huyo ambaye amecheleweshewa nasi tutachukua hatua. Niendelee kuwaagiza wale wote wenye jukumu la kusimamia malipo ya pensheni kwa wastaafu, watekeleze wajibu wao na wastaafu waweze kupata mafao yao kwa wakati unaotakiwa bila kucheleweshwa na tukizingati kwamba hata Mheshimiwa Rais amesisitiza na ameagiza sana suala hilo lisimamiwe vizuri na sisi tutaendelea kulisimamia.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza napenda kuipongeza Serikali kwa kuanza kutekeleza Waraka huo wa kuwalipa Posho ya Madaraka Walimu Wakuu wa Shule pamoja na Waratibu. Hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa posho hii kama ilivyoelezwa katika Waraka ni Posho ya Madaraka. Je, Serikali sasa haioni ni wakati muafaka kuanza kulipa posho hii kwa ajili ya viongozi wengine kama vile Afisa Elimu, Afisa Elimu Taaluma pamoja na Afisa Elimu Takwimu na Vifaa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa kazi ya ualimu ni zaidi ya kufundisha, kuna kufanya maandalio, kufundisha, kusahihisha, kupanga matokeo na mengine mengi tu. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kurejesha ile tulikuwa tunaita Teaching Allowance kwa ajili ya kuwalipa walimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mbunge kwa sababu swali hili ni concern ya walimu wote na hii kwanza mwanzo ilikuwa inajitokeza na Serikali tuliamua kuitekeleza kama tulivyosema hapo awali. Suala la jinsi gani tuangalie Maafisa Elimu Taaluma, Maasifa Elimu Takwimu watapata posho hii, nadhani vyeo hivi ni vya kimuundo ambavyo viko katika Halmashauri zetu maana yake kuna hao vilevile kuna Maafisa Kilimo na Maafisa mbalimbali. Kwa sasa kwanza tuendelee na utaratibu wa sasa na pale itakapoonekana kuna haja ya kuweza kufanya mabadiliko tutafanya hivyo. Lengo letu kubwa ni kupandisha motivation ya wafanyakazi hasa watendaji wetu katika ngazi mbalimbali waweze kufanya kazi kwa ufanisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo lingine la Teaching Allowance, hata Mheshimiwa Masoud alisimama hapa hoja yake ilikuwa ni hiyo hiyo, jambo hili tumelichukua. Bahati nzuri Waziri wetu hapa wa Utumishi kutoka Ofisi ya Rais nakumbuka mwezi Mei, 2017 alifanya mkutano rasmi wa uzinduzi wa Bodi hii. Sasa tunakwenda kuangalia suala zima la wafanyakazi katika mazingira mbalimbali maana hatuzungumzii walimu peke yake, tuna Mabwana Shamba, tuna watu wa kada mbalimbali ambao na wenyewe wako katika mazingira hayo magumu. Ndiyo maana Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Utumishi inashughulikia jambo hili kwa upana wake lengo kubwa ni kuja na ajenda pana ya Kitaifa ni nini tufanye kutatua matatizo ya wafanyakazi walio katika mazingira mbalimbali ya utendaji wa kazi.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja, kwa kuwa Serikai imesema kwamba inafanya tathmini kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote ili kuingiza Vijiji vya Mhezi, Msindo, Mshewa, Vuudee, Tae, Gavao na Saweni lakini mara nyingi imejitokeza kwamba mfuko huu hauna fedha za kutosha kutekeleza miradi. Je, Serikali iko tayari kutafuta namna nyingine ili kuwezesha vijiji hivi vipate mawasiliano? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa tatizo la Same Magharibi linafanana kwa kiasi fulani na maeneo kadhaa ya Jimbo la Mafinga Mjini hasa katika Vijiji vya Kisada, Ulole, Bumilayinga na Maduma. Je, Serikali iko tayari kutia msisitizo ili Kampuni ya Viettel ambayo wanaendesha mtandao wa Halotel wakafunge mitambo ili kuwawezesha wananchi wa maeneo hayo kupata mawasiliano ya uhakika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba vijiji vingi sana bado vinahitaji huduma ya mawasiliano. Takwimu zilizopo ni kwamba tuna jumla ya kata 3,381 na kati ya hizo ni kata 443 ambazo tayari zimekwishafikiwa na mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu unaofanywa kupitia Mfuko wa Mawasiliano ni kuangalia asilimia ngapi eneo husika halina huduma ya mawasiliano kwa kutumia prediction map kutoka makampuni ya simu ambayo yanatoa huduma za mawasiliano. Nimepokea maombi mengi sana kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge mbalimbali ambao wamepita pale ofisini kwa ajili ya kutaka huduma za mawasiliano zifike kwenye maeneo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitambue kupokea maombi kutoka kwa Mheshimiwa Cosato Chumi ambaye alifika sana ofisini kwangu, Mheshimiwa Edwin Sannda, Mheshimiwa Venance Mwamoto wa Kilolo, Mheshimiwa Deo Ngalawa na Mheshimiwa Mwakibete wa Busokelo. Serikali inaendelea kufanya jitihada za kuhakikisha kwamba huduma ya mawasiliano inafika kwenye sehemu zote ambazo zinahitaji huduma ya mawasiliano kwa sababu sasa hivi mawasiliano ni nyenzo muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza litalenga wale waliofanya mitihani kabla ya mwaka 2008 ambao hawapewi cheti mbadala. Kwa mujibu wa majibu ya Serikali badala ya kupewa cheti wanapewa uthibitisho na mara nyingi uthibitisho huu mtu anakuwa ameomba ili uelekezwe ama sehemu anayoomba kazi anayoomba kujiunga na masomo zaidi.
Sasa Serikali haioni umuhimu wa hata hawa ambao walipoteza Cheti ambao walihitimu kabla ya mwaka 2008, kuwafanyia utaratibu wa kuwapa hiyo duplicate?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa mara nyingi watu wanaoomba Baraza la Mitihani liwasilishe hizo taarifa kama vyeti kule walikoomba kazi au masomo, vyeti hivyo mara nyingi uthibitisho upo kwamba, vimekuwa vinachelewa na hivyo kuwasababishia watu hao ama kukosa hizo nafasi za kazi walizoomba au nafasi za masomo.
Je, Serikali haioni haja ya kuwa na mifumo kama ya vyuo vya elimu ya juu ambapo mtu ambaye amepoteza cheti anaweza akapewa nakala hata mbili tatu akazitunza mwenyewe, midhali Serikali na Baraza la Mitihani limejiridhisha kwamba, huyo mtu kweli alihitimu masomo hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wahitimu waliomaliza shule kabla ya mwaka 2008, kwa sasa imekuwa ni vigumu kuwapatia vyeti mbadala kwa sababu wakati huo vyeti havikuwa vinabeba picha za wahitimu. Kwa hiyo tukitaka kubadilisha maana yake ni lazima tutafute picha za wale wote ambao wamemaliza shule kabla ya 2008. Kwa vyovyote vile ni kazi kubwa, hata hivyo, sio jambo ambalo haliwezekani kufanyika kwa hiyo, nalibeba tukajadiliane ndani ya Serikali kama linatekelezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kuhusu kuchelewa kupatiwa nakala au cheti mbadala au uthibitisho kwa wale ambao wanakuwa wamepoteza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyopo ni kwamba, mara nyingi watu wanaenda kuomba vyeti mbadala au uthibitisho pale wanapokuwa na uhitaji. Ushauri wangu kwa Watanzania wote ni kwamba, kila mara unapopoteza cheti usisubiri mpaka uhitaji kutumia cheti hicho ndio ukaanze kutafuta mbadala au uthibitisho. Ukishapoteza anza taratibu za kuanza kutafuta, ili ikitokea kwamba, unahitaji iwe ni rahisi kwa sababu, tayari unakuwanacho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa sasa kwa mwombaji yeyote yule, ukiomba inachukua angalau siku 30, lakini hizo ndiyo siku nyingi ambazo kinaweza kuchukua, ni maximum. Inaweza ikawa chini ya hapo na kwa sasa hivi kwa kweli, Baraza la Mitihani la Taifa ni moja kati ya Taasisi za Serikali zinazofanya kazi kwa ufanisi mkubwa sana kwa hiyo, mara nyingi hazifiki hata hizo siku ukikamilisha taratibu zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu pendekezo lake la kutumia utaratibu unaotumiwa na vyuo vikuu la kutoa nakala, naomba nilibebe, ni wazo zuri, tukaangalie namna ya kutekeleza, ili ikiwezekana tunapotoa cheti tutoe nakala kadhaa ili mtu aweze kutumia pale atakapopoteza. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Mafinga ni kati ya miji inayokuwa kwa kasi sana hapa nchi na hivyo uhitaji wa maji umekuwa ukiongezeka kwa kasi. Kutokana na jitihada mbalimbali ambazo wananchi wa Mafinga wanajituma na uwekezaji katika mazo ya misitu.
Je, Serikali, iko tayari lini kutupa kibali kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa miradi ya mwaka huu wa fedha wa 2017/2018?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, lakini nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu Mheshimiwa Cosato Chumi kwa kazi kubwa anazozifanya na namna anavyofuatatilia ili wananchi wake wapate maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa Wizara imeshatoa kibali kwa mradi wa Mji wa Bumilianga ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Nami naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia Halmashauri mbili za Wilaya ya Mufindi na Mji wa Mafinga. Hata hivyo, katika fedha za Basket Fund, Halmashauri ya Mji wa Mafinga inapokea kiasi kidogo kiasi kwamba inaathiri utendaji wa Hospitali ya Mafinga ambayo inahudumia Halmashauri zote mbili. Je, ni lini Serikali itaongeza fedha za Basket Fund kwa ajili ya Hospitali ya Mji wa Mafinga ambayo inahudumia halmashauri zote mbili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachosema Mheshimiwa Chumi, siyo jambo la uongo. Ni kweli Halmashauri ya Mafinga pale ukiangalia ule Mji, wananchi wa Mufindi wote wanakuja kutibiwa pale Mafinga. Bahati mbaya ukifanya comparison; ulinganifu wa Basket Fund ya Mafinga na Mufindi, Mafinga Basket Fund yao ni ndogo, lakini wagonjwa wote wanakuja kutibiwa Mafinga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, scenario hiyo iko sambamba na kule Tarime, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Halmashauri ya Tarime nanii, kwamba ya Mji ina fedha kidogo, lakini Halmashauri hii ina fedha nyingi lakini ha-top up nanii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, maeneo ambayo Halmashauri haina Hospitali ya Wilaya lakini kuna hospitali mfano ya Taasisi ya Dini, wanatumia kituo kile kama DDH na wanapeleka fedha. Sasa tujiulize, kama watu wa Mufindi hawana hospitali, wanatumia Hospitali ya Mafinga na kama wangekuwa hawana Mafinga, maana yake kungekuwa na hospitali ya private pale ya DDH, wangeitumia kama hivyo na kupeleka fedha. Kwa nini hapa msikae sasa kufanya harmonization ya jambo hilo kulifanya liwe vizuri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuseme kwamba jambo hili tumelichukua na nitalikabidhi katika Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, tutaangalia nini tufanye. Lengo kubwa ni kwamba mwisho wa siku, Halmashauri ya Mafinga na Hospitali ya Mafinga iweze kujiendesha vizuri kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wale. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona, Mji wa Mafinga ni kati ya Miji inayokua kwa kasi na hasa kutokana na shughuli za uzalishaji wa mazao ya misitu na bidii ya kufanya kazi ya wananchi wa Mafinga na hivyo uhitaji wa maji umeongezeka. Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza miradi iliyotengwa kwenye bajeti hii ambayo tunaenda kuimaliza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018, tumetenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya Mafinga, lakini pia tayari kuna mikataba ambayo tumeshaanza kuisaini, tayari tumesaini mkataba wa ujenzi wa tenki la lita 500,000 kwenye Kijiji cha Kinyanambo na tunaendelea kusaini mikataba mingine kama Bumilainga na Muduma pia. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunaendelea na hiyo kazi vizuri kabisa tutahakikisha wananchi wake wanapata maji.
MHE. COSATO DAVID CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwanza nipende kumpongeza Mheshimiwa Mwakyembe nilimuona ameenda kumtembelea yule nahodha wa Serengeti Boys ambaye aliumia wakati wa mashindano ya Gabon. Hilo ni jambo jema maana linawatia moyo sana vijana wetu.
Mheshimiwa Spika, sasa nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, wakati Alphonce Simbu anakwenda kushiriki mashindano kule London Marathon, kati ya magumu aliyokutana nayo ni suala zima la yeye kusaidiwa katika kupata visa. Simbu aliondoka hapa Alhamisi kupitia Afrika Kusini na kwenda kushiriki mashindano siku ya Jumapili, kitu ambacho kilimuathiri sana katika performance yake. Kama angeweza kuondoka mapema maana yake angeweza hata kuwa mshindi kuliko kushika nafasi ya tano. (Makofi)
Swali, je, Serikali iko tayari kuwasaidia wanariadha ambao wame-qualify kwenda kushiriki mashindano makubwa ya Kimataifa katika kuhakikisha kwamba wanapata visa kwa wakati? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama nilivyosema, mchezo wa riadha hasa katika kushiriki mashindano makubwa ya marathon kwa mfano, Tokyo Marathon inavutia watazamaji wa barabarani yaani wakati mbio zinakimbiwa kiasi cha watu milioni 1.7. London Marathon watu 800,000 wanakuwa wanashuhudia barabarani, Boston Marathon watu milioni moja.
Swali, je, Serikali ipo tayari kugharamia maandalizi ya wanariadha wetu ambao wanakuwa wame-qualify kwenda kushiriki mashindano haya makubwa ambayo kwa namna moja au nyingine watasaidia kutangaza Taifa letu katika utalii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nianze kwa kupokea pongezi za Mheshimiwa Waziri wangu Dkt. Harrison Mwakyembe kutoka kwa Mheshimiwa Chumi, nitamfikishia salamu hizi. Vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Chumi, kwa kujali kanuni na kujikita katika maswali ambayo yapo ndani ya swali la msingi, ambayo yanahusu riadha, namshukuru sana na ninampongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Vile vile nimpongeze sana kwa sababu yeye ni mwanariadha wa vitendo, kila siku asubuhi huwa tunakutana naye katika uwanja wa Jamhuri akikimbia. Nina imani kabisa kwamba sasa hivi anaweza akawa anakidhi vigezo vya mashindano ya kimataifa.
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Mheshimiwa Spika, kwanza nikubaliane naye kwamba kweli huyu Alphonce Simbu wakati anakwenda katika mashindano ya London alipata matatizo ya kupata visa. Hata hivyo baadaye alifanikiwa kutokana na Serikali kuingilia kati zoezi hili.
Mheshimwia Spika, sasa niseme tu kwamba, mashindano haya huwa yanasimamiwa na vyombo mbalimbali. Kuna yale mashindano ambayo yanasimamiwa na International Federations lakini yapo mashindano ambayo yanasimamiwa na Olympic Committees. Kwa mfano, yapo mashindano ambayo yanasimamiwa na Shirikisho la Riadha la Taifa, lakini pia mashindano ambayo yanasimamiwa na Tanzania Olympic Committee (TOC). Sasa haya ni yale ya Jumuiya ya Madola na yale ya Olympic. Ukiangalia mwanzoni Simbu hakupata matatizo wakati wanakwenda kwenye mashindano ya Olympic, ni kwa sababu hii TOC ilifanya maandalizi mapema.
Mheshimiwa Spika, sasa haya mashindano yake ya pili ni kwamba alichelewa na kwa maana hiyo, napenda kutoa wito kwa wanariadha wote ambao wanapata sifa au vigezo vya kushiriki mashindano yoyote ya kimataifa au kupata mialiko yoyote ya kushiriki mashindano ya kimataifa, wale mawakala au mameneja wao au mashirikisho au pengine vyama, tunavishauri viwasiliane na Serikali mapema ili kusudi Serikali iweze kufanya mipango na kuwasiliana na maafisa wetu wa Ubalozi na kuondoa usumbufu huu ambao ameusema; kwamba wakati mwingine unasababisha mtu kutokufanya vizuri. Kwa hiyo Serikali tukipata taarifa mapema, tunaweza tukasaidia kwa haraka sana ili kusudi mshindanaji na mchezaji ule aweze kupata visa mapema.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili linauliza kama Serikali ipo tayari kugharamia maandalizi. Maandalizi kimsingi yanafanywa na vyama, vilabu na mashirikisho. Kwa kuzingatia kwamba michezo hii ni mali ya jamii na wanamichezo wenyewe wanatokana na jamii. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nirudie tu kusema kwamba maandalizi yanapofanyika mapema, na hasa ile mipango ya vyama au mashirikisho, inapotufikia Serikalini mapema inakuwa ni rahisi kwetu kujua wale wamekwama wapi, wanamikakati gani na hivyo tunaweza tukasaidia katika maandalizi.
Mheshimiwa Spika, kwa mfano tu niseme kuna wanariadha ambao wanatarajia, wanavigezo vya kwenda kufanya mashindano ya Common Walk Games Australia mwezi wa nne ambapo wako sita. Tumeshaanza kufanya mazungumzo na Serikali ya Ethiopia ili kusudi waweze kuweka kambi ya miezi nane kule Ethiopia na kupata utaalam na kuweza kufanya vizuri katika mashindano hayo. Hata hivyo tuko katika utaratibu wa kutafuta vyanzo endelevu vya mapato ili kuweza kuwasaidia wanamichezo wote siku za baadaye. Ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Kwa kuwa matatizo ya Mbulu yanafanana kabisa na Halmashauri ya Mji wa Mafinga ambao kwa juhudi za wananchi pamoja na Serikali tunatarajia kukamilisha Kituo cha Afya cha Ulole, Kisada na Bumilahinga na pia Kituo cha Afya cha Ihongole kufuatia kupewa fedha shilingi milioni 500 na Serikali; lakini kwa kuzingatia kuwa Hospitali Mafinga iko kandokando ya barabara kuu na kati ya Iringa na Makambako hakuna hospitali hapo katikati.
Je, Serikali iko tayari kutuongezea idadi ya Watumishi ili tutakapofungua Zahanati na Vituo vya Afya hivyo, ufanisi wa kukaribisha huduma za afya kwa wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga uwe wa dhati na wa vitendo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, na wewe ni shududa kwamba wakati tunapitisha bajeti yetu Mheshimiwa Mbunge Cosato Chumi alikiri kabisa kwamba sasa hivi Mafinga ni motomoto kwa sababu kuna upanuzi wa hospitali. Pia hali iliyoko Mafinga ukilinganisha na Mbulu kuna utofauti mkubwa, maana wenzetu wana kituo. Kwanza kuna Chuo ambacho kinafundisha Waganga pale. Kwa hiyo, wakati wa kwenda kufanya practical inakuwa rahisi kwa wao kwenda katika Zahanati na Vituo vya jirani ikiwa ni pamoja Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba Vituo vya Afya vyote na Zahanati zote zinakuwa na wahudumu kwa maana ya Waganga pamoja na Wauguzi ili hicho ambacho kimekusudiwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma kwa wananchi kinakuwa kweli na siyo nadharia.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali kwamba wawekezaji binafsi wafanye jitihada wenyewe za ku-access mikopo, naomba kuuliza ni lini Waziri atatembelea viwanda vya Mafinga ambavyo vimeitikia kwa wingi sana katika suala la uchumi wa viwanda ili kuzungumza na wenye viwanda kuhusu changamoto na fursa mbalimbali za mikopo ya riba nafuu inayopatikana kutoka Benki ya Uwekezaji Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kwenda Mara nitaelekea Mufindi. (Kicheko/Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Serikali imeziagiza halmashauri ziwasilishe miradi viporo ambayo ilihubiriwa na wananchi isiyozidi kiasi cha shilingi bilioni 1 na kwamba fedha hizo zitaletwa katika mwaka huu wa fedha ili kuwapa wananchi nguvu waweze kumalizia miradi ile ambayo waliianzisha kwa nguvu zao. Je, ni lini Serikali sasa inaleta fedha zile kwa sababu umebaki takriban mwezi mmoja mwaka wa fedha kuisha na ni Serikali yenyewe ndiyo ilituambia sisi halmashauri tulete hizo fedha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, pale Mafinga tunakusudia kukamilisha Kituo cha Afya cha Bumilayinga pamoja na zahanati mbili na kujenga nyumba za watumishi kwa maana ya wauguzi watakaoishi katika hizo nyumba kwenye Kituo cha Afya cha Bumilayinga na zahanati mbili za Ulole na Kisada pamoja na ile zahanati ya Sao-Hill. Je, ni lini Serikali inatuletea fedha ili tukamilishe miradi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tulielekeza orodha ya miradi viporo iletwe TAMISEMI lakini hiyo ilikuwa ni kwa ajili ya kujipanga vizuri kuweza kuwasaidia au kuunga mkono nguvu za wananchi. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Chumi na Waheshimiwa Wabunge wote kwenye halmashauri zao wawe na subira wakati Serikali inaendelea kujipanga. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi pamoja na maelezo hayo mazuri na jitihada hizo za Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza ninaona hapa ni mamilioni mengi sana yamekuja katika nchi yetu ninauliza Serikali. Je, ni lini maeneo mahususi kama ya Mufindi, Njombe na Ruvuma ambako wananchi wana mwamko wa hali ya juu katika kupanda miti ambayo inasaidia kwa kiasi kikubwa ku- regulate mambo ya tabianchi. Lini wananchi hawa nao wataanza kunufaika na fedha hizi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili umeeleza kuhusu accreditation, kati ya tatizo kubwa ambalo linasababisha Taasisi zetu hapa nchini hususani za kijamii kama NGO’s kukosa fedha kutoka mifuko hii ni kwa sababu sisi kama Taifa bado hatujafanya accreditation katika huo mfuko ambao umeutaja.
Je, ni lini Serikali itakamilisha utaratibu huo ili pamoja na fedha hizi ambazo Serikali inazipata moja kwa moja taasisi pia za kiraia kama ma NGO’s yanayojishughulisha na mazingira yaweze pia kuanza kunufaika na fedha hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chumi ametaka kujua ni lini fedha hizi zina tutazipata ama tutaweza kuzitumia hasa kwa watu ambao wanawajibika na suala la kutunza mazingira kwa kupanda miti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Chumi kwamba kwa sababu sisi focal point, sisi ndiyo waratibu wa mifuko hii hasa GEF, kwa hiyo wakati wowote tutakapokuwa tumepata fedha hizi hasa GEF7 maana yake tutatangaza ili kuhakikisha kwamba tunaweka vipaumbele kwenye eneo hili la wenzetu ambao wanashughulisha kutusaidia kwa ajili ya kutunza mazingira kwa kupanda miti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kupitia NGO’s na tuliposema kuhusiana accreditation maana yake tunatarajia fedha zitakapokuja tutaweka bayana na NGO’s zote na vikundi vyote ambavyo vimesajiliwa vipata fursa ya kuomba fedha hizo na sisi tutawapa kipaumbele, ahsante sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Wakati katika baadhi ya maeneo kumekuwa na migogoro baina ya Serikali na hayo maeneo ya mbuga za wanyama, lakini kuna maeneo mengi ya utalii kwa mfano maeneo ya kihistoria kama kule Iringa Isimila kuna maeneo yana maporomoko ya maji ambayo pia ni kivutio cha utalii na kuna maeneo yana misitu na ndege wazuri ambapo ni vivutio vya utalii. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuwekeza nguvu kutangaza vivutio hivyo ili walao kupunguza pressure huko kwenye mbuga za wanyama?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa nchi yetu imebahatika kuwa na maeneo mengi ya vivutio vya utalii ikiwemo misitu, malikale, maeneo ya historia na mambo mengine. Hivi sasa Serikali imetengeneza mkakati mkubwa wa kuhakikisha kwamba vivutio vyote vinatangazwa ipasavyo ili kuhakikisha utalii wa ndani na utalii wa nje unaongezeka katika maeneo yote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumechukua hatua kuhakikisha kwamba Mikoa ya Kusini tunapanua utalii ili kupunguza pressure kubwa upande wa Kaskazini. Tunaamini jitihada hizi zitazaa matunda makubwa na kuhakikisha kwamba vivutio vyote vinafahamika na watalii wengi wanaongezeka zaidi nchini.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Serikali imekuwa jitihada kubwa kuboresha huduma za maji katika Jimbo la Mafinga Mjini, hata hivyo hamu ya wananchi ni kuona kuwa jitihada hizo zinasambaa na kufika maeneo mengi.
Je, Serikali iko tayari kutusaidia hasa katika maeneo ya Kisada, Matanana, Itimbo, Ndolezi na Maduma na Ugute walau kupata visima virefu ili wananchi wale nao wapate na kunufaika na huduma za Serikali ya Awamu ya Tano?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mhehimiwa Chumi kwamba katika Halmashauri ambazo zimetekeleza miradi ya maji vizuri ni pamoja na Halmashauri yake. Lakini kufuatiwa huu utaratibu unaokuja, sasa nikuhakikishe Mheshimiwa Chumi kwamba sasa utekelezaji unafanywa moja kwa moja na mimi hebu naomba niombee nipe mwaka mmoja uone shughuli nitakayoifanya. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kabla ya maswali yangu niseme jambo moja, kwanza siyo dhambi huyo mzazi kuwa na watoto zaidi ya mmoja ambao baadaye atapata hii huduma kwa sababu naye katika kuwasomesha ili watumikie Taifa hili bila shaka ametoka jasho. Kwa hiyo, kwenye jibu hilo nimeona ni jibu jepesi kwa Serikali. Sasa naenda kwenye maswali yangu ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, sasa hivi tunaenda kwenye E-government hata malipo mbalimbali kiserikali tunafanya kwa njia ya mitandao, teknolojia ya mawasiliano imeendelea kukua kwa kasi. Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka wa kufanya walau huo utambuzi ili kuwezesha watumishi ambao wanakutana na matatizo kama haya kupata huduma hiyo? Fikiria mtu amefiwa na mzazi Tunduru ampeleke Karagwe na huyu ndiyo mzaa chema mwenyewe!
Mheshimiwa Spika, swali la pili, hiyo nia njema ya Serikali kuruhusu watumishi waweze kuchangiana wakipata matatizo kama hayo ni jambo jema lakini wakati mwingine, mimi nilikuwa mtumishi wa umma mifuko hiyo ina-burst, je, Serikali iko tayari japo kutenga ruzuku ndogo kuisaidia hiyo mifuko ili watumishi wakipata matatizo kama hayo waweze kupata hiyo huduma kwa wepesi zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kama alivyosema kwenye swali lake la kwanza na yeye namuingiza katika Ibara ya 63(2) na (3) ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba Bunge linaweza likaishauri Serikali. Kwa hiyo, kulingana na maendeleo ya TEKNOHAMA na E- government kama unavyosema upo uwezekano mkubwa sana hapo baadaye tukawa na mfumo madhubuti wenye utambuzi kwamba Bwana Joseph Kakunda ana watoto saba wameajiriwa katika sehemu mbalimbali za Serikali, amefariki Joseph Kakunda basi pengine mtoto wake wa kwanza ndiyo atabeba hilo jukumu la kupewa hayo mafao ya mazishi. Kwa hiyo, inawezekana huko baadaye hili likafanyika, tunachukua mchango wake kama maoni kwa mujibu wa Ibara hiyo ya Katiba.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuweka ruzuku kwenye mfuko. Kwanza, napenda nitoe wito kwamba ni vizuri sana kila mahali pa kazi pakawa na mahusiano mazuri, watumishi wenyewe wakawa na mahusiano mazuri wao kwa wao kwanza, kwa sababu katika baadhi ya maeneo ya kazi Mifuko hii ya Rambirambi iko vizuri sana. Hata hapa Bungeni uko Mfuko wa Faraja lakini si Wabunge wote ni wananchama. Kwa hiyo, mimi natoa wito tuanze sisi kwanza kuonesha mfano Bungeni humu Wabunge wote wawe wanachama wa Mfuko wa Faraja. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile mahali pote pa kazi watumishi wajiunge katika Mifuko ya Faraja hii ya Kufa na Kuzikana ambayo ni muhimu sana. Tunauchukua ushauri tena ushauri wake kwamba baadaye tutafikiria kuweka kifungu kidogo kwa ajili ya kuunga mkono uchangishanaji ambao unafanywa na watumishi. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali na pia kwa kukiri kwamba inaufanyia mapitio muundo na kwamba itazingatia mawazo ambayo nimeyatoa kutokana na swali langu, hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, wakati huu ambapo tunaelekea uchumi wa viwanda, ni matarajio kwamba Maafisa Biashara tulionao watakuwa na wajibu zaidi ya wajibu walionao sasa ambao kimsingi umejielekeza zaidi katika kufanya kazi ya kutoa leseni na kukagua leseni. Maafisa hawa wengi wao ni watu ambao wana elimu zao, wamesoma mambo ya international trade, international business na kadhalika, kwa hiyo, tunakuwa kama tuna wa- under utilize. Je, lini mipango hiyo ya kukamilisha muundo itakamilika? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali iko tayari wakati inaendelea kukamilisha suala hilo la muundo kuwa- task na kuwawezesha Maafisa Biashara ili waweze kuwasaidia wajasiriamali wetu kuibua miradi, kuwasaidia kuandika maandiko lakini pia kung’amua fursa mbalimbali za mikopo ya riba nafuu. Kwa mfano, kule kwetu Mafinga kuna wafanyabiashara na wajasiriamali wa mazao ya misitu kama mbao, mirunda na nguzo na majirani zangu Njombe wanalima maparachichi. Je, Serikali wakati inaendelea kukamilisha muundo huo iko tayari kuwa-task na kuwawezesha ili wafanye shughuli hizo za kuibua miradi? (Makofi). Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nirejee katika swali langu la msingi nimemshukuru sana kwa mchango wake. Hata haya maswali yake mawili ya nyongeza bado ameendelea kuweka mchango mzuri wa mawazo ambao utakuja kusaidia sana Serikali. Yeye ana uzoefu mkubwa, amefanya kazi katika Serikali za Mitaa sehemu nyingi sana, kwa hiyo, uzoefu wake tutautumia. Hata baada ya leo hapa namkaribisha ofisini kwangu ili tujadiliane kwa kina zaidi haya masuala ya Serikali za Mitaa kwa sababu wote tuna uzoefu nayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wajibu wa Maafisa Biashara, muundo utakapokamilika wataongezewa wajibu zaidi, kwa sababu sasa kama tunawatoa kwenye ile Idara ya Fedha tunawapeleka kwenye Idara nyingine ambavyo sipendi kuitaja kwa sababu haijawa rasmi watashirikiana huko na Maafisa Maendeleo ya Jamii na Wachumi katika kutekeleza yale ambayo Mheshimiwa Mbunge anayependekeza.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, je, Serikali inajiridhisha vipi kwamba ile fidia ya dola 70,000 inayotolewa inawafikia walengwa hasa watoto au mke wa marehemu ambaye anakuwa amepoteza maisha anapokuwa katika vikosi vyetu vya kulinda amani nchi mbalimbali huko duniani? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni muda mrefu sasa tunaendesha mambo yetu ya ulinzi bila kuwa na sera ya ulinzi, je, ni lini Serikali itakamilisha sera hii ili kusudi pamoja na masuala haya ya ulinzi wa amani sehemu mbalimbali duniani. Sera hiyo iweze kubainisha maeneo mbalimbali ambayo kwa namna moja au nyingine yatafanya vikosi vyetu vinavyoenda kulinda amani huko duniani viweze sio tu kunufaika kwa mujibu wa taratibu za UN, lakini pia kwa mujibu wa taratibu za nchi yetu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA:
Mheshimiwa Spika, fedha zinazotolewa kama fidia zinawafikia wahusika kwa sababu Tanzania tumeshakuwa na uzoefu wa jambo hili, tumeshapoteza askari wetu na kuna walioumia, fedha zilizotolewa familia zinaitwa Makao Makuu ya Jeshi na wanakabidhiwa bila ya tatizo lolote na inapobidi basi msimamizi wa mirathi ndiye ambaye anakabidhiwa akiwa pale Makao Makuu ya Jeshi. Mpaka sasa hivi kwa matukio yote yaliyotukuta hakuna tatizo la mtu kudhulumiwa na hivyo tunaamini kwamba fedha hizo huwa zinawafikia walengwa.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili ya Sera ya Ulinzi, kama tulivyowahi kusema mara kadhaa hapa Bungeni, sera hii rasimu yake ipo tayari, imeshajadiliwa na ngazi zote na kinachosubiriwa ni maoni kutoka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kama mdau ili wakishatoa maoni yao basi hatua zilizobaki za kuikamilisha sera hii ziweze kuchukuliwa.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kabla ya maswali haya mawili ya nyongeza naomba kuitahadharisha Serikali katika jibu la msingi Serikali inasema kwamba watatoa vibali.

Katika suala la vibali bila shaka litaleta mazingira ya rushwa ili watu waweze kupata hivyo vibali na bila shaka litaongeza shida na watu wetu wataendelea kupata tabu sana.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza la kwanza, ikiwa katika majibu ya msingi ya Serikali inakiri kwamba hali imeimarika ya watumishi na mambo ya udhibiti na mambo ya ukaguzi. Je, sasa Serikali haioni ikiwa hali imeimarika ni wakati muafaka wa kuondoa zuio hili ili kusudi mazao ya misitu yapate kusafirishwa muda wowote kadri mtu anavyotaka ku- speed up uchumi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa sababu wakati mwingine Serikali ina shaka sana na mbao pori na bahati nzuri Mheshimiwa Spika wewe ni mhifadhi. Je, Serikali iko tayari kuturuhusu sisi ambao mbao hizi, nguzo, mirunda zinatokana na miti ambayo tumepanda sisi wenyewe na siyo mbao pori. Je, Serikali iko specifically tayari kuruhusu kwa mbao ambazo zinatokana na miti ya kupandwa ziruhusiwe kusafirishwa muda wowote ambao mwananchi au mfanyabiashara anaona kwake ni muafaka ili ku-speed up uchumi kwa sababu Serikali iko kazini 24/7 masaa 24 siku saba, hakuna mahali Serikali imelala na inafanya ikaguzi kuna vituo, magari ya patrol. Je, Serikali iko tayari hasa kwa miti ambayo sisi watu wa Mafinga, Mufindi, Iringa, Njombe, Ruvuma tunapanda kwa nguvu zetu kuruhusu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza nakubaliana kabisa na Mheshimiwa Cosato Chumi kwamba tukiweka mazingira magumu ya upatikanaji wa vibali tutasababisha vibali hivi kutolewa kwa upendeleo na pengine kutasababisha kuchochea rushwa nakubaliana naye. Kutokana na sababu hiyo ndio maana tumesema kwa sasa tumefikia mahali huduma zimeimarika na tutaondoa zuio la usafirishaji wa mazao ya misitu kutokana na misitu ya kupandwa ambayo ilikuwa inasafirishwa mchana peke yake sasa kuanza kusafirishwa kwa masaa 24. Nafikiri hilo tayari katika majibu yangu ya msingi nilisema na tuko kwenye hatua za mwisho za kuondoa zuio hilo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tutaendelea kuwa na zuio kwenye mbao za misitu ya pori na hii ni kwa sababu ya kulinda kwanza misitu yenyewe ambayo inaelekea kutoweka, lakini pili kuendelea kuisimamia vizuri ili kupunguza udanganyifu. Hata hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ruhusa ya usafirishaji wa misitu ya kupanda ambayo nimeizungumzia ikiwa ni pamoja na mirunda na mazao yake tutaitoa hivi karibuni na hapatakuwa na masharti kwa mtu ambaye amekamilisha vibali.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri na yenye kujitosheleza ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba nikupe comfort kwamba suala hili tumeshaanza kulifanyia kazi hata kabla ya kupokea swali la kutoka kwa Mheshimiwa Chumi na tupo katika hatua za mwisho mwisho za kuweka utaratibu kwa ajili ya kufungua usafirishaji usiku wa mbao ambazo ni za kupanda.

Mimi binafsi sio muumini sana wa kuzuia watu wasifanye kazi usiku mara mabasi hayasafiri usiku, mara malori hayasafiri usiku, mbao hazisafiri usiku, tunachelewesha ukuaji wa uchumi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo mtazamo wangu ni kwamba ili kutia chachu ya ukuaji wa uchumi watu ni lazima wafanye kazi mchana na usiku na ndio maana nimetoa agizo ndani ya Wizara kwamba walete ushauri wa kitaalam wa namna ambavyo tutaweka control ili kudhibiti uhalifu na vitu vingine lakini watu waruhusiwe kusafirisha mazao yao usiku.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi. Pamoja na kazi nzuri wanayofanya TARURA Mkoa wa Iringa na katika Mji wa Mafinga, hali ya barabara za Mji wa Mafinga ambao ni kitovu cha shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Mufindi siyo ya kuridhisha, ni asilimia 24 tu ya baraba ambazo zinapitika kwa mwaka, ile tunaita good and fair. Je, Serikali ina mpango gani wa kuangalia Mji wa Mafinga kwa macho mawili ili kuhakikisha kwamba barabara za Mji wa Mafinga zinapitika kwa uzuri kwa mwaka mzima ili kusudi ku-speed up ukuaji wa uchumi ambao ndiyo kitovu cha Wilaya nzima ya Mufindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nimjibu Mheshimiwa Cosato Chimi, Mbunge wa Mafinga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanzo wa kuanzishwa TARURA ilikuwa ni kuondoa kero ambazo Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wanazungumzia. Kwa hiyo, naomba niwaelekeze TARURA nchi nzima, wafanye tathmini ya kero kubwa na za muda mrefu katika maeneo yao. Tunatarajia kwenye bajeti ambayo tunakwenda kuijadili, maeneo haya ambayo yanazungumzwa na Waheshimiwa Wabunge, ndiyo maeneo ambayo yatakuwa yamezingatiwa kuondoa kero katika maeneo hayo kwa pamoja na eneo la Mafinga, TARURA kufanya kazi pale na Mkoa wa Iringa, naomba wataalam wetu, Mainjinia nchi nzima wa TARURA, wafanye tathmini na walete kero mahsusi ambazo Wabunge wamezungumza na Viongozi mbalimbali wamewasilisha ili ziondolewe katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Mji wa Mafinga ulikuwa Mamlaka ya Mji Mdogo kwa miaka tisa na Julai 2015 ikawa Halmashauri kamili ya mji. Je, Serikali inaweza kuwahakikishia wana-Mafinga kwamba kwa kuwa Halmashauri ya Mji kamili na wao wameingia katika Mpango Kabambe wa Maboresho ya Miji? Kwa sababu sasa hivi Mafinga ni Halmashauri ya Mji kamili. Tunataka tu kuhakikishiwa na sisi tunaingia katika awamu ya pili? Kwa sababu ndiyo ukombozi wa barabara zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge alikuwa na Mheshimiwa Rais amekubaliwa mambo yake yote manne leo amelala usingizi mnono kabisa. Katika suala hili, kama nilivyojibu swali la Mheshimiwa Zakharia, Mbunge wa Mbulu Mji, tutakapoanza kufanya mchakato miji mipya yote na huo mji wako utaingizwa katika awamu hiyo.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi. Sera tunayoenda nayo sasa tunaelekea katika uchumi wa viwanda, ili tuweze kuwa na uchumi wa viwanda lazima tuhakikishe viwanda vinapata malighafi ipasavyo. Katika Mji wa Mafinga kuna Kiwanda cha Pareto hata hivyo kumekuwa na walanguzi ambao wananunua maua ya pareto na kuyasafirisha kwenda nje ya nchi hivyo kusababisha kiwanda kukosa malighafi.

Serikali inatuambia nini katika kudhibiti walanguzi ambao wanasabisha Kiwanda cha Pareto Mafinga kukosa maua?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo ameeleza changamoto inayopatikana katika Kiwanda cha Pareto cha Mafinga, changamoto hizo pia zipo katika maeneo mengine ya kuhitaji malighafi nchini kama kwenye maeneo ya ngozi na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo ni kwamba unakuta kiwanda kinahitaji kipate hizo malighafi lakini baadhi ya viwanda utakuta kwamba vinanunua malighafi kwa bei ndogo sana kiasi kwamba mkulima anakuwa ahapendi kupeleka hiyo malighafi katika kiwanda kama hicho. Lakini wakati huo hivyo viwanda vinahitaji malighafi hiyo kwa bei ndogo labda kutokana na uwezo wake mdogo wa kifedha hasa katika hatua za awali za ujenzi wa kiwanda.

Kwa hiyo, sisi tunafikiria kama Serikali tunaowajibu sasa wakuingilia kati kuona kwamba viwanda viweze kupata malighafi hizo kwa kusaidiwa na Serikali lakini wakati huo mkulima na yeye aweze kupata bei inayostahili kutokana na kazi aliyoifanya. Kwa hiyo, tumeanza kufanyia kazi masuala hayo katika baadhi ya viwanda na tunaamini kwamba kuna hatua stahiki zitachukuliwa kwa viwanda maalum ambavyo vinatumia malighafi zinazozalishwa hapa nchini.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na kabla ya swali la nyongeza ningependa kuwasilisha shukrani zangu kwa TARURA Mafinga na TARURA Iringa kwa jinsi ambavyo wanajituma kufanya kazi pamoja na mazingira ya uhaba wa fedha. Pia na Wakala wa Misitu Tanzania kwa maana ya shamba la Sao Hill ambao mara kwa mara tumeshirikiana nao kwa kutusaidia Greda na sisi halmashauri kujaza mafuta kusembua barabara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nina maswali mawili ya nyongeza swali la kwanza kwa mujibu wa mgao wa fedha za mfuko wa barabara kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri mpaka hapa tulipo TARURA inapata asilimia 30 na TANROADS inapata asilimia 70 na wote wanashughulika na barabara ambazo ni za muhimu katika Taifa letu, lakini bado TARURA barabara zao ndiyo zinazobeba mazao zinabeba biodhaa, zinabeba mbolea.
Je, mbali ya hiyo kanuni Serikali iko tayari kutafuta namna nyingine ya kuwa chanzo maalum cha kuiwezesha TARURA ifanye kazi zake kwa ufanisi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili Mji wa Mafinga Mjini unakuwa kwa kasi na ndiyo kitovu cha uchumi wa mazao ya misitu katika Wilaya Mufindi na Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Je, Serikali iko tayari japo kuiangalia Mafinga kwa macho mawili ili kusudi miundombinu yake iweze kuboreshwa na hivyo mchango wake katika uchumi wa Taifa ukaongezeka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na changamoto ya mgao wa fedha na tumepokea pongezi kwa niaba ya Serikali kwa kazi nzuri ambayo inafanyika na TARURA na nchi karibu kila halmashauri. Changamoto kubwa ni ufinyu wa bajeti na upungufu wa fedha ambao upo inapelekea changamoto hizo kuendelea kuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mengine kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge jambo hili la mgao wa fedha linafanyiwa kazi kuna Kamati maalum iliundwa naifanyia kazi na Waheshimiwa Wabunge humu ndani walishatoa maoni mbalimbali kutafuta chanzo mbadala, pia kuangali formula ambayo itatumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pamoja na mambo mengine tutaendelea kufanya pia kazi hiyo huu mchakato tutakamilisha na ikishindikana kupata mgao wa fedha hizi au hata 50 kwa 50 basi tuangalie vyanzo vingine vya kusaidia barabara zetu ziweze kupitika. Ni kweli kwamba barabara hizi ni muhimu sana ndipo walipo wananchi wengi, huduma za kijamii nyingi tunajua zinapitika wakati wote na hasa wakati huu wa mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili Mheshimiwa Mbunge anataka kujua kama Serikali inampango wa kuboresha Mji wa Mafinga. Niseme tu kwamba Serikali ina mpango wa kuboresha maeneo yote ya Miji ikiwepo Mafinga Mjini pindi tukipata uwezo wa fedha wa kutosha na kuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi hiyo itafanyika kwenye eneo lake ili uchumi uweze kukua na huduma iweze kupatikana kwa haraka na kwa gharama nafuu, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kabla ya maswali yangu mawili ya nyongeza, napenda kutoa pongezi kwa Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa barabara kati ya Mafinga na Igawa, ambayo ilikuwa imeharibika na kiasi cha kuwa chanzo cha ajiali nyingi ambazo zilipoteza maisha ya watu wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, barabara zinazopitika mwaka mzima Mafinga ni wastani wa asilimia 24 tu; na Mafinga ni kitovu cha shughuli za kiuchumi za Wilaya ya Mufindi kutokana na mazao ya misitu na hivyo kuwa na mchango mkubwa sana katika uchumi wa Taifa letu. Je, Serikali, iko tayari kuiangalia Mafinga kwa jicho la huruma na kuiongezea fedha TARURA Mafinga ili angalau barabara hizi ziweze kupitika kwa mwaka mzima? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa mujibu wa hotuba ya Waziri ukurasa wa 83, TARURA inasimamia wastani wa barabara zenye urefu wa kilomita 100,000 na zaidi na katika hizo, lami haizidi kilometa 1,500, changarawe haizidi kilometa 24,000, za udongo hazizidi kilometa 85,000, madaraja zaidi ya 2,000 na makalavati zaidi ya 50,000. Je, Serikali iko tayari kuiangalia TARURA na kuiongezea fedha ama kupitia mfuko wa barabara ama kutafuta chanzo chochote? Kwa sababu ndiyo ambayo inasimamia barabara nyingi zinazobeba uchumi mkubwa wa kubeba mazao, malighafi na bidhaa kutoka vijijini kwenda highway?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kumpongeza bwana Chumi kwa sababu amekuwa mpiganaji mkubwa sana wa Mafinga katika kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma bora za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, ukiangalia Mji wa Mafinga sasa unakua na eneo kubwa sana la uchumi. Ndiyo maana katika majibu yangu au majibu yetu, Naibu Waziri alizungumza kwamba Mafinga, Kasulu, Nzega na maeneo mengine ambako ile miji imechipua hivi sasa ambayo haikuwepo katika mpango wa kwanza, tunaliwekea mpango maalum. Kwa hiyo, Mheshimiwa Chumi nikuhakikishie kwamba Serikali itafanya tathmini ya kutosha nini kifanyike kwa Mafinga? Lengo ni kusaidia Mji wa Mafinga unaokua ambao vilevile unachangia uchumi hasa wa Taifa letu hili kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuongeza financing katika suala zima la TARURA, ni kweli. TARURA mwanzo tulifanya tathmini, mtandao wa barabara ulikuwa ni kilomita 108,000 lakini sasa hivi tathmini ya juzi, imefika kilomita 135,000, kwa hiyo, package yake ni kubwa. Kwa kuliona hili, Serikali hivi sasa kupitia Mfuko wa Barabara inaendelea kufanya tathmini, nini kifanyike kwa lengo la kuangalia jinsi gani tuboreshe kwa ajenda kubwa ya kusaidia TARURA iweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tunaendelea kufanya resources mobilization kutafuta vyanzo vingine vya mapato na hasa kupitia wadau wetu wa maendeleo. Hapa niwashukuru DFID pamoja na USAID kwa kazi kubwa tunayoendelea kuifanya hivi sasa. Imani yangu ni kwamba kwa mkakati wa Serikali tunaoenda nao, huko mbele ya safari, tutahakikisha TARURA inafanya kazi vizuri kwa maslahi mapana ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, alipopita pale Mafinga tuli-raise hii concern ya suala la umeme na Mheshimiwa Waziri akaahidi kutupatia transfoma tano ambazozitakwenda kwenye vijiji vya Itimbo, Isalavanu, Matanana na Ndolezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa vijiji hivyo wanasubiri hizo transfoma kwa hamu sana nimeambiwa wanashughulikia. Sasa maswali yangu mawili ya nyongeza kama nilivyosema kwenye swali langu la msingi Mji wa Mafinga unakua kwa kasi kiviwanda na kimakazi kiasi kwamba uhitaji wa umeme ni mkubwa na hata TANESCO hivi sasa inakusanya mapato makubwa kushinda hata baadhi ya mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ninalouliza, je, Serikali iko tayari kujenga kituo cha kupoozea umeme ili wananchi hawa wa Mafinga ambao wanapoteza asilimia 30 ya muda wao wa kuzalisha mali, wapate umeme wa uhakika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ninaomba kuthubutu kusema kwamba, mtu aliyepewa kazi ya ku-survey maeneo ya kupeleka umeme REA Awamu ya III, hakufanya kazi yake kwa weledi na kwa ufanisi. Kwa sababu scope coverage ya maeneo mengi ya vijiji iko chini ya nusu, kiasi kwamba maeneo kama Zanzibar, Bandabichi, Dubai, Ndolezi, Rumwago, Ihongele na Matanana, ambako surveyor alisema kuna kaya 33, lakini kuna kaya 700, Serikali iko tayari kuhakikisha kwamba ile scope coverage katika maeneo yale REA Awamu ya III inatekelezwa, inakwenda kuongezeka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, ni kwamba, Mkoa wa Iringa kwa kubahatika kupitiwa na huu msongo mkuu, yaani backbone ya umeme ya umeme wa KV 400, tunatarajia kuimarisha sana ili uweze kutoa support katika maeneo mengine, hasa inapotokea kuna changamoto ya umeme. Kwa hiyo, tunategemea kwanza kuboresha kwa kuongeza hiki kituo cha umeme ambacho kitakuwa cha msongo wa 220 mpaka 33 kwa kuweka transformer mbili zenye ukubwa wa 60 MVA, kwa hiyo, mara mbili ni 120 pale Mafinga, ili uweze pia kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika katika eneo la Kisada, tunategemea pale kwa ajili ya kupitiwa na hii backbone tuweke pia vituo, kituo ambacho kitakuwa ni cha msongo wa 400 KV kitakachokuwa mpaka 220 na mpaka 33 KV na kitakuwa na transformer mbili zenye saizi ya MVA 200 kila moja. Kwa misingi hiyo tunategemea kwamba eneo hilo litakuwa ni kitovu cha uimarishaji wa umeme katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa upande wa kusambaza umeme, ni kweli katika baadhi ya maeneo ambayo yanazunguka miji, siyo tu kwa Mkoa wa Iringa, yaani Mafinga, lakini pia hata maeneo mengine katika nchi. Tunao mradi wa kuendeleza, kusambaza umeme katika maeneo ya pembezoni mwa miji ambao unafadhiliwa na Benki yetu ya Afrika. Kwa hiyo, tunategemea kwamba kwa Mkoa wetu wa Iringa na maagizo haya ambayo alikuwa ameyatoa Mheshimiwa Rais utafanyiwa kazi na utakuwa mnufaika moja wapo.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Mafinga, nafarijika kwamba katika zile Halmashauri 19 za Miji, Mafinga nayo itakuwemo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na jibu la msingi, naomba Serikali iweze kuwaambia wananchi wa Mafinga, mazungumzo haya na Benki ya Dunia kwa ajili ya kuanza kutekeleza program nyingine ya kuendeleza miundombinu katika hiyo Miji 26 na 18 yatakamilika lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hali ya barabara zetu wakati huu ambapo mvua sasa zimeanza kunyesha kwa wingi, maeneo mengi nchi nzima barabara zimekatika baina ya eneo moja na nyingine: Je, Serikali kupitia TARURA iko tayari kutenga fedha za emergence na fedha hizi zikakaa kule kule Wilayani kuliko ilivyo sasa ambapo Wilaya au Mji kama Mafinga inabidi tuombe Emergence Fundkutoka TARURA Makao Makuu; sasa when it is emergence, imaanishe kweli ni emergence: Je, Serikali iko tayari kutenga Emergence Fundkwa ajili ya barabara ambazo zimeleta matatizo wakati kama huu wa mvua nyingi?
NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafingi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika,ni kweli kwamba mazungumzo kati ya Serikali na Benki ya Dunia kuhusu miradi hii ya kuendeleza Miji inaendelea. Niseme kwamba maongezi haya yanaendelea na tunaamini kwamba mipango iliyoko na mwelekeo wa haya mazungumzo haitachukua muda mrefu kukamilisha mazungumzo haya. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira kwamba Serikali inakwenda kutekeleza suala hili kwa ufanisi iwezekanavyo mara baada ya mazungumzo haya kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusiana na miundombinu ya barabara na je, kama Serikali iko tayari kupeleka fedha za dharura kupitia TARURA katika Wilaya kwa ajili ya kuhudumia barabara zilizoharibika. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kupitia TARURA imejipanga ku-respondkwa wakati kutatua changamoto za miundombinu ambayo itatokana na uharibifu wa mvua ambazo zinaendelea kunyesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mara tu changamoto hizi zitakapoonekana katika maeneo husika, naomba nimhakikishie kwamba Serikali iko tayari na tutahakikisha tunatatua changamoto hizo kwa wakati. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakubaliana kabisa na Serikali kwamba ina wajibu wa kulinda ajira za Watanzania kwanza, ndiyo priority. Hata hivyo, Sheria hii ya Uwekezaji sababu ya kutoa nafasi hizo tano automatic mojawapo ilikuwa ni hiyo trust ambayo mwekezaji anayo kwa wale watu watano bila kujali sifa walizonazo ni adimu au siyo adimu. Kwa mfano, watu wa finance mtu amewekeza mradi wake wa milioni mia moja in any way hata kama huyu mtu hana CPA…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa. Swali la kwanza, ni lini Serikali ita-harmonize hizi sheria mbili ili kutengeneza mazingira bora ya uwekezaji ili kuendana na kasi ya kuvutia wawekezaji nchini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa kwa sasa vibali vile life span yake ni ya muda mfupi mfupi na baadhi ya uwekezaji ni wa muda mrefu, je, Serikali iko tayari kuongeza life span ya vibali vile katika kuvutia wawekezaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza kuhusiana na mabadiliko ya sheria, mabadiliko ya sheria hufanyika pale tija inapoonekana. Katika mazingira ya sasa, Sheria ya Uwekezaji tuliyonayo, Sura 38, inatoa nafasi ya mwekezaji kuweza kupata watu watano kwa maana immigration quota. Watu hao watano wanapewa bila masharti yoyote, yeye ndiye atakayewachagua na hakuna hayo matakwa anayosema yapo kwa maana ya kuangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ni sehemu ya incentive au motisha. Katika kufanya hivyo, mwekezaji baada ya kuwa amekidhi vigezo vyote atakuwa na uhuru wa kuweka watu wake hao watano. Hiyo ni kwa mujibu wa Sheria ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa sheria inayohusiana na kuratibu ajira za wageni, yenyewe pia inatoa tu utaratibu na mwongozo mzuri wa local content katika kulinda uchumi wa nchi yetu lakini pia kulinda ajira za wazawa. Sasa katika mazingira haya ukiacha goli wazi, kwa sehemu kubwa uzoefu unaonyesha kila mwekezaji angependa kufanya kazi na watu ambao ni wa kutoka nje. Tuna taarifa kwamba wapo pia wawekezaji wanapata mikopo kutoka kwenye mabenki mbalimbali na masharti inakuwa ni kuajiri raia wa huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Serikali yetu tunawekeza sana kwenye elimu, tuna mpango wa elimu bila malipo ambapo Serikali inatoa fedha nyingi katika sekondari lakini pia vyuo vikuu tunatoa mikopo, vijana hawa wanapomaliza vyuo na ajira hizo zikichukuliwa na wageni inakuwa ni changamoto kwa nchi. Ndiyo maana kwa ikatungwa sheria hiyo udhibiti ili kuhakikisha kwamba ajira za wazawa zinalindwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake dogo la pili kuhusu life span ya permit, nimweleze tu Mheshimiwa kwamba nalo limezingatiwa vizuri na sheria za sasa zinatosha kabisa katika kuelezea hilo. Mwekezaji nchini mbali na kupewa idadi ya watu watano ambao wanaweza kufanya nao kazi, Sheria ya Uwekezaji inatoa muda wa kipindi cha miaka mitano lakini pia akiombea kupitia TIC anapewa kipindi cha miaka kumi. Katika miaka hii kumi na yule anayepewa miaka mitano imewekwa katika awamu ili kuhakiki na kujiridhisha kwamba kweli bado ajira hiyo ni adimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka miwili anapata permit yake ya kwanza ambapo atahitaji kuwa na succession plan aturidhishe kwamba kuna Mtanzania nyuma anajifunza kazi hiyo ya kitaalamu ili hata baadaye hata akiondoka nchini tuweze kubaki na wataalamu. Atapewa tena awamu ya pili miaka miwili na mwisho atapewa final grant kwa maana ya kufikisha miaka mitano. Mazingira hayo yote yanaangaliwa na wakati mwingine wamekuwa wakikata rufaa ofisi ya Waziri mwenye dhamana na zimekuwa zikitolewa kwa kupima mazingira yalivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mpaka sasa hitaji la kubadilisha sheria halijaonekana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka tu kuongezea kidogo kwenye majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Serikali pia ipo katika mchakato wa kufanyia marekebisho Sheria ya Uwekezaji. Pamoja na mambo mengine tutayaangalia baadhi ya mambo Mheshimiwa Mbunge ameya-raise hapa. Pia Waheshimiwa Wabunge watapata nafasi ya kuipitia sheria hiyo na kama kuna maeneo ya kuimarisha basi itakuwa ni fursa nzuri ya kuweza kurekebisha. Ahsante sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Leo tutajadili hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na sehemu ya hotuba hiyo tutajadili suala la ajira hususan kwa vijana. Nina maswali mawili ya nyongeza kwa Serikali.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali iliruhusu tusafirishe mazao ya misitu kwa saa 24 na hivyo kusisimua na kuchechemua uchumi sio wa Mafinga tu na maeneo mengine. Je, Serikali iko tayari kufanya upendeleo maalum kwa Mji wa Mafinga kutokana na nature yake ya kibiashara kuruhusu baadhi ya maeneo watu kufanya biashara saa 24 na yenyewe ikabaki na suala la ulinzi ambayo ni kazi kuu ya Serikali?

Mheshimiwa Spika, swali pili, katika jibu la msingi Serikali imesema kuna changamoto ya miundombinu muhimu kama vile taa, kamera na kadhalika. Sisi kama Halmashauri tuko tayari kujenga baadhi ya miundombinu lakini je, Serikali iko tayari kutusaidia japo taa za barabara katika maeneo muhimu katika njia panda za Itimbo, Madibila, Mufindi na Sokoni ili kuwawezesha wananchi hawa kuendelea kujiajiri na kujipatia kipato na hivyo kuwa na mchango katika Serikali na mifuko yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Mheshimiwa Mbunge alikuwa anataka upendeleo maalum kwa Mji wa Mafinga ili uweze kufunguliwa. Katika jibu langu msingi nilieleza kabisa moja ya jukumu kubwa la Serikali ambalo tunalifanya sasa ni kuhakikisha tunajenga miundombinu na usalama unakuwepo. Baada ya kutathmini ndipo tunaweza kuruhusu Mji wa Mafinga ili uweze kufanya biashara kwa saa 24.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ambalo ni la msingi kabisa Mheshimiwa Mbunge ameainisha commitment ya Halmashauri yake kwamba wao kama Mafinga Mji wako tayari kujenga baadhi ya miundombinu muhimu na sisi kama Serikali tuweze kusaidia katika kuweka hizo taa za barabarani. Nafikiri wazo hilo ni jema na mimi niungane kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kusema kwamba tunaomba Halmashauri ya Mji Mafinga waanze hiyo hatua ya kutengeneza hiyo miundombinu muhimu na sisi tutatuma wataalam wetu waende kufanya tathmini, ili tuweze kuwaruhusu waweze kufanya hiyo biashara yao kwa saa 24 na sisi tutawasaidia katika hiyo sehemu itakayobakia.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Kwanza kabisa, nakupongeza kwa kurudi kwenye hicho kiti, tuliku-miss sana Mzee wa Jaza Ujazwe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza na msingi wa maswali haya ya nyongeza la kwanza, asilimia thelathini ya muda wa kufanya kazi katika Mji wa Mafinga na maeneo yanayozunguka unapotea kutokana na kukatikakatika kwa umeme. Hii maana yake ni nini? Saa za kufanyakazi katika nchi yetu wastani kwa mujibu wa sheria ni saa nane. Kwa hiyo, kwa siku tunapoteza wastani wa saa mbili au dakika 144, kwa wiki tunapoteza wastani wa saa 16 au dakika 1008, kwa mwezi tunapoteza saa ya kufanya kazi 40 au dakika 2,400. Maana yake ni kwamba tunapoteza kwanza mapato kwa TANESCO yenyewe lakini pia mapato kwa wananchi na kwa Serikali. Swali langu linakuja, kama tuna viwanda vikubwa 80 kwa nini tusiwe na Wilaya ya TANESCO katika Mji wa Mafinga kama ambavyo katika Wilaya ya Ilala, Wilaya ya Temeke, Wilaya ya Kinondoni wana Wilaya za TANESCO zaidi ya moja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, toka asubuhi nimepokea simu na meseji nyingi sana kutoka kwa wananchi wakiuliza kwamba wanashindwa kununua LUKU leo siku ya pili jambo ambalo linakosesha TANESCO mapato lakini pia shughuli za uzalishaji kwa wananchi kukosa umeme zinakuwa zimesimama. Nini kauli ya Serikali kuhusiana na jambo hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la kwanza Mafinga ni mojawapo ya maeneo ambayo TANESCO inafanikiwa kwa asilimia kubwa kupeleka umeme wa uhakika, kwa sababu inayo sub-station ambayo ipo jirani kilometa kama 80 kutoka kwenye huo mji wenyewe eneo la Igowolo na umeme huo unatokea Iringa.

Pia tunayo line nyingine ndogo inayotoka Iringa moja kwa moja kupeleka umeme Mafinga. Kwa hiyo, Mji wa Mafinga unalishwa na line mbili za umeme, ikitoka moja inaunganishwa nyingine, ikitoka nyingine inaunganishwa hiyo moja. Kwa hiyo, nimuombe tu Mheshimiwa Chumi aendelee kutuvumilia katika maboresho tunayoendelea kuyafanya kuhakikisha umeme unakuwa wa uhakika na kama ambavyo tumeshasema mara kwa mara eneo la Iringa, Mafinga, Mbeya na Bukoba tunaathari sana za kupatwa na radi kwa hiyo tunaendelea kurekebisha mifumo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili la LUKU, nikiri kwamba kwa siku mbili na leo itakuwa ni ya tatu tumekuwa tuna tatizo na tumepata shida kubwa sana kwenye mfumo wa kidigitali wa kununua na kuuza LUKU. Tunawahakikishia kwamba tunalishughulikia, tunazo system mbili; system moja imekufa, ilipata hitilafu kidogo na tayari tumeshapata itengenezwe na hiyo system nyingine iliyobakia inabeba mzigo mkubwa sana na hivyo inashindwa kuhudumia wateja wote kwa wakati. Tunaahidiwa na wataalamu wetu kwamba kabla ya siku ya leo haijaisha tatizo hilo litakuwa limekwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge na kupitia forum hii, naomba niwaambie Watanzania wote kwamba ukifika katika ofisi za TANESCO unaweza ukanunua umeme. Shida tunayo kwenye ile data base au mfumo unaouza kupitia kwenye mifumo ya kibenki na mifumo ya simu, ile ndiyo imepata shida kidogo lakini ukifika Ofisi ya TANESCO unaweza ukanunua umeme. Naomba radhi kwa niaba ya wenzangu lakini tunawahakikishia kwamba leo kabla siku haijaisha tutajitahidi kuhakikisha huduma hiyo inarejea ili Watanzania waendelee kupata huduma ya LUKU kama kawaida.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza, nitakuwa tu na swali moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika taarifa za Benki ya Dunia za Easy Way of Doing Business moja wapo ya kikwazo kwa wawekezaji ni uchelewaji wa kupatikana hati kwa wakati na utaratibu uliopo ni kwamba ile Kamati ya Kugawa Ardhi ya Kitaifa inakaa mara nne tu kwa mwaka. Je, Serikali ipo tayari kurahisisha walau hiyo Kamati ikakaa hata kila mwezi ili wawekezaji wapate hati kwa wakati? (Makofi)
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na kwa niaba ya Wizara hiyo, ningependa kujibu swali la Mheshimiwa Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kanuni zilikuwa zinataka Kamati hii ikutane mara nne kwa mwaka na ndivyo walivyokuwa wanafanya lakini kutokana na ripoti hiyo na outcry ya wawekezaji na umuhimu wa kuharakisha uwekezaji, kwa sababu Kamati hii inaundwa na mimi, nimeelekeza sasa Kamati hii ikutane kila mwezi badala ya miezi minne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kuanzia Awamu hii ya Sita wameshaanza kukutana mara moja kila mwezi na mwezi uliopita wamekutana kila wiki na ndio maana imewezesha katika maombi 174 yaliyowasilishwa katika Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Rais Samia, tayari maombi 173 yameshapata vibali na yameshaandikiwa hati za uwekezaji na tayari zimeshakabidhiwa kwa EPZA na TIC kwa ajili ya utekelezaji. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi barabara ya Mafinga Mgololo ambayo ni kiungo muhimu sana cha uchumi katika uchumi wa Mufindi na Iringa imeahidiwa toka ilani ya uchaguzi 2005 ninauliza Serikali. Je, wakati jitihada za kujenga kwa kiwango cha lami zinaendelea Serikali iko tayari kushughulikia na maeneo korofi kama vile Itulavanu, Mtili na pale mlima wa Kalinga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chami Mbunge wa Mafinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupitia Bunge hili nimuagize Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa aende akaangalie maeneo hayo korofi aweze kufanya tathmini ili yale maeneo korofi tuweze kutafuta fedha ili barabara hiyo iweze kutengenezwa maeneo korofi yaweze kupitika muda wote wa mwaka. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza naishukuru Serikali kwa kuifanya Iringa kuwa kitovu cha utalii kusini, lakini mradi huu ambao GN hiyo imetangwazwa Julai, 2021 ulizinduliwa tarehe 12 Februari, 2018 na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassain akiwa Makamu wa Rais. Sasa swali langu ni moja tu kwa Serikali, je, inaridhika na speed ya utekelezaji wa mradi huu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi huu utakamilika kwa wakati. Nasema hivyo kwa sababu mradi huu una-cover maeneo manne ya Kusini mwa Tanzania ambako ndiyo unatekelezwa. Mradi huu kwenye maeneo haya ni pamoja na Hifadhi ya Nyerere, Ruaha, Udzungwa na Mikumi.

Mheshimiwa Spika, eneo analoliongelea Mheshimiwa Chumi ni eneo mojawapo ambalo ni ujenzi wa kituo mahususi kwa ajili ya kutunza information za masuala ya utalii. Hivyo, maeneo mengine mradi huu unaendelea ambapo mitambo mbalimbali imeshanunuliwa, magari lakini pia kuna viwanja vya ndege ndani ya hifadhi vimeendelea kukarabatiwa na miundombinu mingine mingi inaendelea kufanyika. Hivyo, eneo hili lilikuwa linasubiri tu GN iweze kukamilika, lakini wakati huo huo tuna mshauri mwelekezi ambaye tayari ameshaanza zoezi na tumeshaanza kupokea ripoti. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakamilisha mradi huu kwa wakati bila wasiwasi. Ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Mji wa Mafinga nadhani ndiyo hospitali inayohudumia Halmashauri nyingi kuliko hospitali yoyote hapa nchini. Hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia zaidi ya Halmashauri tano ikiwepo ya Mlimba ambayo iko Mkoa wa Morogoro. Sasa kutokana na unyeti huo, na kwamba iko kando ya barabara kuu.

Je, Seikali iko tayari kuleta watumishi katika mpango wa dharura?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Wilaya ya Mafinga ni kweli iko barabarani na inahudumia wananchi wengi; na hospitali zote ambazo ziko kimkakati tunaziainisha na kuziwekea mpango, kwanza wa kupeleka vifaa tiba, lakini pia kuboresha upatikanaji wa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie kwamba tutakwenda kwa utaratibu wa kawaida wa kupata watumishi kwa ajili ya hospitali ile badala ya utaratibu wa dharura, kwa sababu utaratibu wa watumishi unapatikana kupitia vibali maalum; laini tutaaipa kipaumbele Hosptali ya Mji wa Mafinga.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa katika Wilaya ya Mbarali kuna uzalishaji mkubwa wa mpunga na viwanda vingi vya kuchakata mazao ya mpunga, lakini umeme ni hafifu kwa maana ni low voltage.

Je, Serikali iko tayari kufunga transformer kubwa ili kusudi kuwasaidia wananchi wa Mbarali ambao wana bidii katika kuzalisha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kutokana na kwamba Serikali hivi karibuni ilitangaza bei mpya na bei hii ni kwa ajili ya maeneo ya mijini na maeneo ya vijijini bado bei itabaki ile ile ya shilingi 27,000/= kwa umeme unaosambazwa na Wakala wa Umeme Vijijini; hata hivyo, sheria inayotumika kuamua kwamba hili ni eneo la mji, kwa maana ya Sheria ya Urban Planning Act. No. 8 ya Mwaka 2007, inasema kwamba eneo litahesabika kuwa ni mji ikiwa lina maduka kuanzia 20 na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo kama Mafinga Mjini, ambapo maeneo kama Vijiji Ndolezi, Makalala, katika Sheria hii ya Serikali za Mitaa inahesabika kwamba hilo ni eneo la mji, lakini maisha halisi ya wananchi ni ya kijijini. Kwa mfano, hapa Dodoma kuna Kata 41; Kata za mjini ni 15 tu, the rest maisha yao ni ya kijijini kabisa: Je, Serikali ina mpango gani kuangalia maisha halisi ya wananchi ambao pamoja na kuwa inasemekana wapo mjini kutokana sheria hii, lakini maisha yao ni ya kijijini ili nao waweze kulipa shilingi 27,000? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la kwanza, ni kweli tunalo tatizo la voltage katika maeneo mengi hapa nchini na tayari Serikali imechukua jitihada za makusudi kabisa za kufanya kitu kinachoitwa voltage improvement kwa kuongeza vituo vya kupooza umeme na kufunga mitambo inayoitwa Auto Voltage Regulators kwenye maeneo mbalimbali ili kuweza kufikisha umeme mwingi zaidi kwa wanaohitaji. Kwa hiyo, eneo la Mbarali ni mojawapo ambalo lipo katika mpango huo na hiyo kazi itafanyika. Namwomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuvumilia kidogo na huduma nzuri itafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, kama alivyosema yeye mwenyewe, sheria inaeleza kama alivyosema; na sheria tulitunga sisi wenyewe hapa Bungeni; lakini uhalisia ni vyema ukaangaliwa na sisi kama tulivyosema siku zilizopita, jambo hili tumelichukua na tumewakabidhi wenzetu wa TANESCO waangalie upya uhalisia unavyosema ili pamoja na sheria kuwepo, tuone namna ambavyo sheria hii itawatumikia wananchi ambapo ndiyo hasa tuliitengeza ili iwalinde wao na kuwahakikishia huduma nzuri. Nashukuru. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na nichukue nafasi hii kuipongeza Sarikali kwamba imefuata usauri wa wabunge na ushari wa kamati na pia kama Mbunge ni jambo ambalo nimekuwa nikilisema toka mwaka 2016 na hatimae Ubalozi mdogo umefunguliwa katika Jiji la Lubumbashi, kwa hivyo itarahisisha sana utendaji wa kazi na biashara kati ya nchi yetu na nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ninaswali moja tu la nyongeza. Kwa kuwa kwa upande wa Ziwa Tanganyika upande ule wa Kalema tayari Serikali yetu imeshaanza ujenzi wa bandari na inaendelea vizuri, lakini upande wa pili ambao kuna kama mwalo wa moba ambao sio bandari hasa haujawa katika mazingira ambao yanaweza ku-facilitate meli na hivyo sisi kufanya biashara.

Je, Serikali iko tayari kukutana na Serikali ya Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo kupitia tume ya pamoja na hivyo kushirikiana na kuangalia uwezekano wa kuona namna gani watashirikiana katika jambo zima la kujenga miundombinu, ili biashara kati ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo iweze kushamiri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kuimarisha barabara sehemu ya pili ya DRC, na kwa hali hiyo tayari saa hizi mazungumzo yameshaanza kati ya DRC na Tanzania na mazungumzo hayo yataendelezwa pia katika Mkutano wa Pamoja wa Ushirikiano (JPC) ambao unatarajiwa kufanyika mwezi Mei na maandalizi wa mkutano huo unategemewa kuanza mwezi wa Aprili. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali na kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa sekta ya uchukuzi ina mchango mkubwa sana katika uchumi wa nchi yetu na madereva ndio wahusika wakubwa: Je, Serikali haioni umuhimu wa kuleta mabadiliko haya ya sheria ili hili kundi maalum likapata hizo hati za dharura walau kwa muda wa miezi sita hadi mwaka mmoja? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Kwa kuwa kupata Passport ni mchakato unaochukua siku kadhaa; je, Serikali iko tayari kuwa na dawati maalum kwa ajili ya kuwahudumia madereva ambao wako tayari kupata Passport za kudumu wapate huduma kwa haraka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu maswali mawili nya nyongeza ya Mheshimiwa Chumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli upo umuhimu wa hawa madereva kuwa na passport, lakini kwa sababu mchakato wa kutoa Passport kwa maana ya kuongeza muda wa Passport za dharura kuzidi mwezi mmoja uliopo sasa unahitaji mchakato wa mabadiliko ya sheria, ni ushauri wetu; kwa sababu hizi safari wanazifanya mara kwa mara, hakuna sababu za kwa nini wasipate hizi passport. Akiipata Passport kwa miaka 10 watakuwa wanazitumia hizi passport. Kwa hiyo, huenda kukawa na nafuu kuliko kupata Passport za dharura mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kwa sababu ya kujua umuhimu wa madareva na safari zao, Wizara ya Mambo ya Ndani kupitia Idara ya Uhamiaji imeweka dirisha maalum la kuwahudumia madereva hawa ili pindi wafikapo wasikae foleni muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
MHE. DAVID C. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na ninakuomba kwa ridhaa yako kabla ya maswali yangu mawili ya nyongeza nitumie nafasi hii kuwapongeza Serengeti Girls na Tembo Warriors kwa kufika hatua ya robo fainali, lakini pia kuwapongeza Simba Queens ambao leo wanacheza hatua ya nusu fainali na Mamelodi Sundowns na kuwapongeza Simba kuingia hatua ya makundi na kuwaombea Yanga leo dhidi ya Club Africain waweze kushinda na kuingia hatua ya makundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizo nina maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali iko tayari kuona kwamba sehemu ya fedha hizi inatumika pia katika kuboresha mchezo wa riadha ambao unaweza kutusaidia katika kujitangaza kwa umadhubuti katika kushiriki michezo kama vile Tokyo Marathon, New York Marathon, Bostin Marathon na kadhalika?

Swali la pili, kwa muda mrefu mojawapo ya shida katika michezo yetu hasa mchezo wa soka ni kiwango duni cha waamuzi.

Je, Serikali iko tayari kutenga sehemu ya fedha hizi kufanya mafunzo maalum kwa ajili ya waamuzi ili waamuzi wetu kuwajengea uwezo na hivyo kuwawezesha kushiriki katika kuchezesha michezo ya AFCON, World Cup na kadhalika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza Mheshimiwa Chumi amependa kufahamu kama Serikali ipo tayari sasa kutenga sehemu ya fedha hizi kuhakikisha pia wanaweza ku-support riadha. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba sisi kama Wizara tunayo michezo Sita ya kipaumbele ikiwemo riadha. Kwa hiyo, tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ku-support riadha ili iendelee kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, amependa kufahamu kama fedha hizi pia zitatumika katika kuwezesha waamuzi. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu na Watanzania pia kwamba chini ya BMT wameendelea kusimamia kwamba vyama vya michezo waweze kuwaandaa waamuzi. Na niwapongeze TFF wiki hii iliyopita walikuwa na programu ya vijana 30 pale Uwanja wa Taifa wakishirikiana na FIFA kuhakikisha kwamba tunapata waamuzi kwenye michezo hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Mradi wa Miji 45 utakaoboresha miji 45 maarufu kwa jina la TACTIC, sehemu mojawapo ni pamoja na ujenzi wa barabara, lakini pia pamoja na ujenzi wa stendi ambazo zitakuwa chanzo cha mapato cha Halmashauri zetu likiwemo pia Jiji la Mbeya. Je, ni lini mradi huo utaanza ili kuwezesha Halmashauri na Miji hiyo kuwa na stendi za uhakika ambazo zitakuwa pia chanzo cha mapato?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Miradi ya TACTIC imegawanywa katika phases tatu. Tier one, two and three, lakini tier one hatua zinaendelea, tier two na three pia hatua zinaendelea ili kuhakikisha katika kipindi hicho miradi yote hii inatekelezwa kwa kuboresha barabara, masoko lakini pia na stendi katika miji hiyo 45. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Mafinga pia itatekelezewa mradi huo kama ilivyopangwa kwenye mpango wa TACTIC, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na jitihada nzuri za Serikali ambazo wiki iliyopita tuliona imetoa kanuni na miongozo ya namna gani Taifa litanufaika na namna ya kuuza ile hewa ya ukaa, kwa maana ya Carbon emission.

Je, Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira iko tayari kutoa mafunzo kwenye Halmashauri ambazo zimekuwa mstari wa mbele katika kupanda miti kama ilivyo Halmashauri ya Mafinga, Mufindi, Kilolo na Halmashauri katika Mkoa wa Njombe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chungahela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefika wakati tumeona kwamba jambo hili la biashara hii ya hewa ukaa ni jambo ambalo pamoja na kwamba lina umaarufu lakini bado lina ugeni kwa baadhi ya maeneo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kikubwa ambacho tumekifanya kwanza tumeandaa kanuni. Tayari kanuni zipo na katika kanuni zile tayari imeelezwa namna ambavyo tutapita kila kijiji na kila eneo. Hivi tunavyokwambia tayari tumeshashirikiana na Wizara nyingine za kisekta wakiwemo watu wa Halmashauri na Wizara nyingine ili lengo na madhumuni kupitia maeneo yote ya Tanzania hasa kwa upande huo; ili lengo na madhumuni kuwaeleza wananchi fursa na faida zinazopatikana katika biashara ile ikiwa ina mnasaba wa kutunza na kuhifadhi mazingira. Kwa hiyo nimuhakikishie
Mheshimiwa Mbunge katika maeneo aliyoyataja yote tutapita, tutatoa elimu, tutawaelimisha wananchi ili waweze kujua fursa na faida zinazopatikana katika biashara hii ya carbon credit.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya Serikali yanasema kwamba katika mwaka 2020/2021 ni wafungwa 70 tu waliopata msamaha kupitia Bodi za Parole. Sheria ilikuja ili kupunguza mzigo na mrundikano wa wafungwa katika magereza yetu ambapo mpaka sasa takribani wafungwa ni 15,000. Sasa ikiwa kwa mwaka tu bodi inatusaidia kusamehe wafungwa 70. Je, Serikali inaona kweli bodi ziko kazini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili matokeo haya ya kusamehe wafungwa 70 tu inawezekana kabisa ni kutokana na kwamba vikao hivi vya bodi vya kimikoa ambavyo vinakaa mara nne kwa mwaka yawezekana kabisa iko mikoa vikao hivi havikaliwi.

Je, Serikali inatoa kauli gani kuwezesha vikao hivyo viwe vinakaa mara nne kwa mwaka kama sheria inavyoelekeza?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Sheria ya Bodi za Parole iliwekwa ili kusaidia kupunguza msongamano wa wafungwa gerezani kwa kuwapa msamaha wale wanaokidhi vigezo. Nikiri kwamba kwa mwaka uliopita 2020/ 2021 vikao vingi havikukaa kwa sababu bodi ziliisha muda wake na bahati mbaya sana mapendekezo yale yalichelewa kumfikia Waziri wa Mambo ya Ndani. Lakini hivi tunavyozungumza bod izote zimeshaundwa mikoa yote, kwa hivi maelekezo yaliyotoka ni kuhakikisha kwamba vikao vinakaa kwa mujibu wa mwongozo ili wafungwa wanaokidhi vigezo waweze kunufaika na uwepo wa bodi hizi.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Jitihada za Serikali ni pamoja na kuhakikisha kwamba mapato yatokanayo na utalii yanaendelea kuongezeka kwa kuboresha miundombinu na kufanya marketing ya utalii. Je, ni lini Serikali itaanza utekelezaji kikamilifu wa Mradi wa REGROW ambao ulizinduliwa tarehe 12 Februari, 2018 na Mheshimiwa Makamu wa Rais ambaye sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa REGROW ulianza kutekelezwa mwaka 2017, lakini kutokana na changamoto ambazo zilijitokeza, Benki ya Dunia iliweza kuongeza muda mpaka mwaka 2025, ambapo tutamaliza mradi huu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara imeunda Kamati Maalum ambayo itafanya kazi bega kwa bega kuhakikisha eneo hili tunasimamia vizuri kama ambavyo tunasimamia fedha za UVIKO ili kuhakikisha mradi huu unakamilika haraka na kuhamasisha watalii waweze kufika katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mafinga tunaishukuru Serikali kwa kutufikishia umeme katika kila kijiji, hata hivyo vitongoji vingi havina umeme: Je, ni lini vitongoji vitaanza kupata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika swali lililotangulia la Mheshimiwa Kavejuru, Serikali ipo katika mpango mkakati mkubwa sana wa kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote takribani 36,000 ambavyo vimebaki Tanzania Bara ambavyo havijapatiwa umeme kwa mradi utakaogharimu karibia Shilingi 6,500,000,000,000/=. Kwa hiyo, taratibu zitakapokamilika kila eneo linalohitaji umeme litafikishiwa miundombinu ya umeme katika vitongoji vyetu.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; je, Serikali wako tayari kukaa na mimi ili kuweza kufahamu hivyo vitongoji ambavyo vinaweza kunufaika na ujazilizi wa awamu ya pili unaoitwa IIC ni vitongoji gani na vingapi ili tuondoe mchanganyiko kwa sababu kuna wakati mwingine vitongoji vya Mafinga vinasomeka Mufindi na pale kuna Halmashauri ya Mji Mafinga na Halmashauri ya Mufindi. Kwa hiyo je, wako tayari kukaa na mimi ili tujue hivyo vitongoji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; tunaipongeza Serikali kwamba maeneo ya vijijini bado wananchi wataingiza umeme kwa shilingi 27,000, lakini maeneo kama ya Mafinga yako maeneo pamoja na kuwa ni Mafinga Mji, lakini maisha, mazingira na kipato ni kama maisha ya kijijini.

Je, Serikali iko tayari maeneo kama hayo kama vile Ndolezi, Luganga na Ulole na wenyewe kuwapa bei nafuu katika kuingiza umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Chumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wetu wa Densification 2C utakuwa na una takribani vitongoji kama 2,562. Kama alivyoomba, na mimi niko tayari, baada ya hapa nitakaanaye ili nimuoneshe vitongoji ambavyo vitakuwa ni vya eneo lake kwa ajili ya kuhudumia wananchi katika Jimbo lake la Mafinga Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye swali la pili, kama ambavyo tumeeleza siku chache zilizopita, ni kweli Wizara ilituma timu yake kwenda katika majimbo yetu yote Tanzania ili kuhakiki yale maeneo ambayo yapo mijini, lakini yana uso wa vijiji ili kuweza kuwapangia bei ambayo ni stahiki na wanayoweza kulipa. Lakini kwa bahati mbaya taarifa tuliyoipata baada ya kui-verify humu Bungeni, tulibaini kuna Waheshimiwa Wabunge hawakushirikishwa. Kwa hiyo tumeiagiza ile timu irudi tena na kwenda kubaini upya hayo maeneo na ituletee taarifa. Hivyo taarifa hiyo itakapofika tutashirikishana hapa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, tunapanga bei ambayo wananchi wataimudu kwa ajili ya kuweza kuunganisha gharama za umeme.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Barabara ya Mafinga Mgololo inapita katika majimbo matatu, kwa maana ya Mafinga Mjini, Mufindi Kaskazini na Mufindi Kusini. Katika majibu ya Serikali mara zote wanasema kwamba barabara hii iko chini ya utaratibu wa EPC+F, na kwamba Wizara ya Ujenzi wao wameshamaliza kazi suala hili liko hazina. Sasa wananchi wa Wilaya ya Mufindi wanatuuliza sisi Wabunge wao watatu, kwamba;

Je, hawa wa ujenzi hawawezi kwenda huko fedha kuwaambia sasa watoe fedha hii barabara ianzwe kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwakikishie Mheshimiwa Chumi, Mheshimiwa Kihenzile na Mheshimiwa Kigahe, kwamba barabara aliyoitaja ya hawa Wabunge wote ipo na hakuna barabara ambayo imeachwa katika huu mpango wa EPC+F. Kwa kweli taratibu zinakwenda vizuri tupo tunakamilisha taratibu na nadhani kipindi cha bajeti hizi barabara zote nategemea tutaziwakilisha na zianze utekelezaji, ikiwepo na barabara ya Mgololo hadi Mafinga, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na majibu ya Serikali. Naomba kutumia nafasi hii kwanza kuipongeza Serikali, kwa maana ya Wizara ya Kilimo na Wizara ya Wizara ya Mambo ya Nje kwa programu hii ya kuwajengea vijana uwezo na mafunzo ya ziada, na pia kuipongeza Serikali hususan Wizara ya Kilimo kwa kuwajumuisha hawa vijana 79 katika programu ya BBT. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza: Kwa kuwa vijana hawa tayari walishasoma vyuo vikuu na vyuo vya kati na wakapata ujuzi wa ziada huko Israel; je, Serikali kwa maana ya Wizara ya Kilimo iko tayari sasa pamoja na kuwahusisha kwenye BBT kuanzisha hiyo programu ya mashamba makubwa (block farming); na kwa kuwa tayari wenyewe ujuzi wanao; na tayari hawa 79 wanatumika kule lakini hawa waanze kabisa kazi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa sababu Serikali imetenga fedha nyingi na inajenga miradi mingi ya umwagiliaji ambayo bila shaka itahitaji wataalam katika kuiendesha katika kuwasaidia wakulima wetu; je, Serikali iko tayari kuwatumia baadhi ya vijana hawa kwa mfumo hata wa kuwalipa japo posho ya kujikimu ili wawasaidiwe wakulima wetu katika hii miradi mikubwa ambayo imetekelezeka hususan kule Mtura?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza vijana wote ambao wanaenda Israel kwenye sekta ya kilimo mazao, wapo wengine ambao hawaendi kwenye sekta ya kilimo mazao; wengine wanaenda kwenye mifugo na maeneo ya namna hiyo. Kwa hiyo, wale ambao wako kwenye sekta ya kilimo mazao, tumeanza kuwa- incorporate kwenye programu ya BBT kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi. Wapo ambao tayari wanafanya shughuli za kilimo ambapo tumeanza kuwatambua sasa hivi, wanafanya shughuli za uzalishaji katika maeneo yao na tumewaingiza kwenye component ya pili ya programu ya BBT ya kuwapa grants na mikopo nafuu ya asilimia 4.5. Kwa hiyo, tumeshaanza kuwatambua na kuwaangalia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kuwatumia kama extensional officers, nilitaka tu niliambie Bunge lako tukufu kwamba, kuanzia mwaka ujao wa fedha na tutakapoleta mabadiliko ya Sheria ya Umwagiliaji na Ugani hapa ndani ya Bunge lako, tunaangalia namna ya kuwatumia vijana waliopo mashuleni kwenye programu za extension ambao wanafundishwa katika vyuo vyetu vya kilimo. Vile vile vijana ambao wana utaalam wa kilimo ili kuanza kuanzisha kampuni binafsi za extension services kwa wakulima na waweze kutoa huduma za namna hiyo.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Mji wa Mafinga imetenga eneo la ekari 750 kwa ajili ya Industrial Park ili tuweze kuwa soko la kimataifa la mazao ya misitu; je, Serikali iko tayari kushirikiana na sisi kupitia EPZA kufanikisha ndoto hiyo ambayo itakuwa ni chanzo cha mapato na chanzo cha ajira?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Chumi, lakini Halmashauri ya Mafinga kwa kutenga maeneo haya ambayo ni mumhimu sana kwa ajili ya uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tunathamini na tutahakikisha tunapeleka wawekezaji, lakini pia kusajili eneo hili chini ya uwekezaji, EPZA, ili mazao au bidhaa zinazozalishwa pale ziweze kuuzwa nje, lakini na ndani ya nchi katika kujiletea maendeleo katika Halmashauri ya Mafinga, lakini nchi kwa ujumla, nakushukuru sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Mwezi wa Sita tulisaini barabara ya Mafinga – Mgololo kupitia ule utaratibu wa EPC+F. Sasa wananchi wanapata shaka, wanasema mbona hawaoni mkandarasi, naomba Mheshimiwa Naibu Waziri awape comfort wananchi wa Mafinga katika barabara hiyo inayo - cut across Majimbo Matatu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa miradi yote ya EPC+F Wakandarasi walishapatikana na walishasaini mikataba ikiwa ni pamoja na hiyo barabara ya Mafinga kwenda Mgololo. Kinachofanyika sasa hivi ni kwamba Wakandarasi wote wapo wanapita site, moja ikiwa ni kuangalia fidia, kuangalia sehemu watakazopata material, wapi watajenga kambi lakini pia hizi barabara kutokana na ukubwa wake kuzigawa kwenye lot kulingana na mazingira yake watakavyogawa Wakandarasi maana yake atakayejenga siyo Mkandarasi mmoja kulingana na ukubwa wa barabara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuna barabara ambazo zitakuwa na Wakandarasi wawili, hadi wanne kulingana na ukubwa. Kwa hiyo, Wakandarasi wako wanapita na kupitia pia usanifu kwa sababu ni wao pia wanatakiwa wajiridhishe na usanifu uliofanyika kabla ya kuanza ujenzi. Kwa hiyo, niwahakikishie wananchi kwamba mpango huo unaendelea na watu wapo kazini, kitakachofanyika baada ya kukamilisha wataanza kuona mitambo ikiwa inawasili kwenye maeneo yao, ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Mji wa Mafinga imejenga Kituo cha Ifingo na Kituo cha Bumilayinga. Hata hivyo vituo hivi havina huduma kwa ajili ya kulaza akina baba, akina mama na watoto isipokuwa tu kina jengo la mama na mtoto. Je, Serikali iko tayari kutusaidia na kuhakikisha tunapata hizo facilities?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliweka mpango wa kujenga vituo vya afya vya kimkakati kwa awamu, na katika awamu ya kwanza ilitoa shilingi milioni 500. Kipaumbele ilikuwa ni majengo ya OPD, Maabara, Jengo la Mama na Mtoto pamoja na majengo ya upasuaji na kichomea taka. Hata hivyo, vituo vyote hivi ambavyo vimejengwa bado vinakosa huduma ya wodi ya wanaume, wanawake na wodi ya watoto. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba Serikali itaendelea kwa awamu zinazofuata kujenga wodi kwa ajili ya kulaza wanaume, wanawake na watoto ikiwemo katika Kituo hiki cha Ifingo pamoja na Bumilayinga katika jimbo la Mafinga.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mradi huu pamoja na mambo mengine utahusisha ujenzi wa miradi ambayo itakuwa chanzo cha mapato katika hiyo miji 45; na kwa kuwa huu ni mkopo: Je, Serikali haioni umuhimu wa kukaa na Benki ya Dunia ili awamu ya pili na awamu ya tatu zote zikaenda pamoja ili utekelezaji wa mradi huu uanze mapema? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tunalipokea. Tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha ambao ndio wanzungumza na World Bank kuona kama hili linaweza likafanyika, lakini kwa sababu ya ukubwa wa miradi hii ni lazima iende kwa awamu ili kuhakikisha monitoring ya miradi hii inakuwa ni nzuri ili fedha zinazoletwa, kama alivyosema yeye mwenyewe, Mheshimiwa Chumi, kwamba ni mkopo, hivyo basi Watanzania watalipa, zisitumike vibaya. Kwa hiyo, ni vyema tuka-monitor miradi hii kwa awamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Chumi kwamba miradi hii itafika katika maeneo yote ya majiji haya 45 kwa wakati ambao umepangwa.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi, je, ni lini Serikali itajenga wodi za wanaume na wanawake katika Kituo cha Afya cha Ifingo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata ili ifingo waweze kupata fedha hii. Lakini vilevile nichukue nafasi hii kuomba Wakurugenzi wa halmashuri kuwa wanatenga fedha kwa ajili ya ujenzi na umaliziaji wa zahanati na vituo vya afya kwenye halmashauri zao. Serikali Kuu imeshapeleka fedha nyingi sana kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya hivi na zahanati hizi na fedha nyingi ya vifaa tiba na wao wasaidie sasa.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, ili upitishe miundombinu ya mawasiliano kwa kila kilometa moja watu wa mawasiliano wanachajiwa dola 1,000, lakini ukipitisha miundombinu kama ya maji au umeme kando ya barabara kuu za TANROADS au za TARURA, charge yake ni kama dola 50 kwa kilometa moja.

Je, Serikali haioni ni wakati sasa wa kuzungumza ndani kwa ndani ya Serikali ili kupunguza hiyo gharama ya dola 1,000 ili kupunguza hizo gharama za mawasiliano?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; maeneo ya Mtula, Kisada na Kata nzima ya Bumilayinga, kuna masiliano ya kusuasua: -

Je, ni lini Serikali itaboresha na kuimarisha mawasiliano katika kata hizo za Mji wa Mafinga?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweIi kabisa kuna gharama za kupitisha mkongo wa Taifa ambazo ni dola 1,000 ambazo tunaziita right of ways na Mheshimiwa Rais tayari ameshaelekeza tuhakikishe kwamba tunalifanyia kazi kwa sababu gharama hizi mwisho wa siku zinaingia kwenye capex na mwisho wa siku zinaenda kwa mtumiaji wa mwisho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ili tuhakikishe kwamba mtumiaji wa mwisho anapata huduma ya mawasiliano kwa gharama nafuu ni kuhakikisha kwamba gharama ambazo zilizopo katikati hapa ambazo zitamsababishia mtumiaji wa mwisho kuwa na gharama kubwa ya kutumia huduma ya mawasiliano tumeshaanza kazi nzuri ya kushirikiana na wenzetu TANROADS, TARURA na kadhalika ili kuhakikisha kwamba hizi gharama tumezitazama kwa namna ambayo zitasaidia zaidi wananchi badala ya kuwaumiza wananchi, ahsante sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mifuko hii ambayo inatenga fedha kwa ajili ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi iko mingi na Mheshimiwa Rais aliposhiriki mkutano kule Scotland aliwasisitiza Mataifa makubwa waheshimu ahadi zao na kutenga hizo fedha. Tatizo na changamoto imekuwepo katika kukosa utaalam.

Je, Wizara iko tayari kuvishirikisha Vyuo Vikuu, Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, SUA na Chuo Kikuu cha Zanzibar katika kupata ule utaalam wa kuandika hayo maandiko ili tupate hizo fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, takribani miradi mingi tumekuwa tunawashirikisha wataalam hasa wataalam kutoka Vyuo Vikuu. Tumekuwa na miradi mingi na miradi hii mara nyingi kwenye masuala ya utafiti tunawashirikisha wanafunzi na walimu wa vyuo vikuu, hata kwenye masuala ya maandiko ya hii miradi kwa maana ya hizo proposal pia huwa tunawapa nafasi ya kuchukua mawazo yao ili lengo na madhumuni tuweze kupata mawazo ya kitaalam kwenye miradi hii, kwa sababu wenzetu wanapokuja kukagua miradi hii huwa zaidi wanaangalia utaalam ambao tumeutumia na zile pocedure ambazo tumezipitia katika kuimarisha miradi hii. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuko tayari na kwa sababu tumeshaanza hilo jambo. Nakushukuru.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, baadhi ya maeneo ya Kata za Rungemba, Bumilayinga na Isalavanu na Kata ya Sao Hill hazina mawasiliano ya uhakika.

Je, ni lini Serikali itafunga japo mnara mmoja kuzunguka maeneo hayo ili wananchi hawa wapate mawasiliano ya uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nipokee changamoto ya Mheshimiwa Chumi ili Serikali ikafanyie kazi na pale fedha zitakapopatikana tutafikisha huduma ya mawasiliano, ahsante sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa Jiji la Dar es Salaam linauhitaji sana wa bidhaa za mbogamboga, je Serikali iko tayari kuwasaidia vijana wa Jimbo la Ilala kwa Mheshimiwa Bonnah kuwa na kitu kinaitwa urban farming na hivyo kuwawezesha kulima mazao ya mbogamboga ili kuliwezesha Jiji la Dar es Salaam kujitosheleza kwa bidhaa hiyo na wao kujipatia kipato?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa mazingira ya Dar es Salaam hayafanani sana na Jimbo la Mafinga Mjini. Je, Wizara na Serikali iko tayari kuwasaidia vijana wa Jimbo la Mafinga kuwapa mafunzo mahususi kwa ajili ya kutengeneza bidhaa za mazao ya misitu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bonnah Kamoli yaliyoulizwa na Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, kama Serikali tuko tayari kuweza kuwasaidia vijana waweze kuona kwa kushirikiana na Halmashauri tutaangalia kama suala la urban farming linawezekana kulingana na upatikanaji wa eneo kwenye hilo eneo, lakini pia Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia maagizo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ilishaagiza kila Halmashauri iweze kutenga maeneo kwa ajili ya vijana kufanya kilimo. Kwa hiyo tutaliangalia hilo na tunalizingatia ili kuweza kuhakikisha ombi hilo tunaenda kulitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, lakini kabla ya hilo kuna program pia ya Vitalu Nyumba ambayo tumekuwa tukiitekeleza katika Halmashauri zote nchini zaidi ya 180. Tutaangalia na kuweza kuhakiki kama lot ya pili pia tutazidi kwenda kutoa vifaa na mafunzo ili waweze kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ambalo ameliuliza Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na Mafinga. Kwa sura ileile hili tumelichukua na tutalizingatia, tutashirikiana na Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kuona tunatengeneza mazingira mazuri ya vijana wetu kupata ajira,, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Hospitali ya Mji wa Mafinga kutokana na sababu za kijiografia inahudumia zaidi ya halmashauri tano. Je, Serikali iko tayari kutufanyia upendeleo wa kipekee?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema awali kwamba Serikali imeajiri watumishi 8,070 wa kada ya afya kote nchini na muda sio mrefu wametoka kuchukua barua zao katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI na kuweza kuripoti katika maeneo ya kazi waliyopangiwa ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Mafinga. Hivyo basi, ni imani yangu kuwa halmashauri hii imepata watumishi hawa wa kada ya afya. Ni wajibu wa Mkurugenzi kuwapangia kule kwenye upungufu ikiwemo katika hospitali ya wilaya.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nilikuwa naomba kuuliza Serikali, je, iko tayari kuwa na mpango mahsusi wa kuisadia SUMA JKT katika kuhakikisha kwamba tunajitosheleza katika suala zima la chakula na mafuta ya kula? Mipango mahsusi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chumi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo tayari kuangalia vipengele mahsusi vya kusaidia mashirika yake na mashirika mengine, lakini ushauri wake pia tumeuchukua na tunaenda kuufanyia kazi.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais mwaka jana iliahidiwa kujengwa barabara kutoka Mafinga inayokwenda Madibila kupitia Sadani.

Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli swali hili limeulizwa jana na Mheshimiwa nakumbuka wa Mbarali na nilijibu kwamba tutaendelea kulitengeneza, lakini marekebisho tu ni kwamba, kama alivyosema wakati Mheshimiwa Rais ametembelea Mkoa wa Iringa, Wabunge wa Mkoa wa Iringa hasa Wilaya ya Mufindi waliomba barabara hiyo ijengwe kwa kiwango cha lami na Mheshimiwa Rais alitoa ahadi na akatoa maelekezo na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi akiwepo, ameshatoa maelekezo, kwamba ile ahadi ya Rais ianze kutekelezwa mwaka huu. Kwa hiyo, tutaanza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami kama maagizo ya Mheshimiwa Rais yalivyotolewa kuanzia huku Mafinga kwenda Mbarali, ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Halmashauri wa Mji wa Mafinga Kata ya Bumilainga kwa kufuata maelekezo ya Serikali kwamba tutenge fedha za mapato ya ndani kujenga kituo cha afya, tumetekeleza na tuko kwenye hatua za mwisho za kukamilisha Kituo cha Afya cha Bumilainga. Je, Serikali mpo tayari kutuletea vifaa ili kituo hichi cha afya kianze kazi, ambacho kinahudumia pia Halmashauri ya Mufindi anakotoka Mheshimiwa Mwenyekiti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mhheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi Mbunge wa Mafinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu kwamba mara baada ya kituo hicho cha afya kukamilika tupo tayari kupeleka vifaatiba pamoja na Wauguzi ili kiweze kufunguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia zaidi ya halmashauri tano na pia iko kando kando ya barabara kuu ya kwenda Zambia mpaka South Africa. Kutokana na sababu hiyo imekuwa na msongamano mkubwa sana wa wagonjwa katika kutoa huduma.

Je, Serikali iko tayari kupitia basket fund, kuongeza bajeti katika Hospitali hii ya Mafinga ambayo inahudumia halmashauri zaidi ya tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Mji wa Mafinga iko barabara inahudumia wananchi wengi kutoka pia kwenye kata na halmashauri za jirani, na utaratibu wa fedha za basket fund utaendelea kutolewa kulingana na population iliyoko ndani ya halmashauri husika na ndicho kinachofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la msingi nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi sasa Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan inajenga vituo vya afya katika kata zote za kimkakati na hospitali za halmashauri katika halmashauri ambazo hazina hospitali. Kwa hiyo, automatically tutapunguza wagonjwa ambao wengi wanakwenda hospitali ya Mji wa Mafinga.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, lakini pia napenda kuipongeza Serikali kwamba sasa imeanza kutenga fedha za dharura kwa ajili ya barabara zetu za TARURA, naipongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza, barabara ya kutoka Changarawe kwenda Kisada ambayo inapita maeneo ya Matanana na Bumilayinga kutokana na miti ambayo wananchi walipanda kwa wingi na sasa imekomaa, inatumika sasa na malori makubwa.

Je, Serikali iko tayari kuitazama barabara hii kwa macho mawili kwa sababu inaharibika mara kwa mara?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; tunafahamu kwamba na wewe Naibu Spika ni mmoja wa wanufaika wa Mradi wa DMDP kama utakuja kukamilika, na sisi watu wa miji 45 tuna Mradi wa TACTIC. Mimi na wananchi wa Mafinga tunapenda kufahamu, je, katika huu Mradi wa TACTIC ambao utanufaisha kata nyingi za pale Mjini Mafinga, Upendo, Isalavanu, Kinyanambo na kadhalika, je, unaanza lini kwa sisi wa tu wa Mafinga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iko tayari kuiangalia kwa umakini barabara ya Changarawe – Kisada ambayo Mheshimiwa Mbunge ameiainisha hapa ili tuhakikishe kwamba inafanyiwa matengenezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lini Mradi wa TACTIC utaanza. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kuwa Halmashauri ya Mji wa Mafinga Mjini ipo katika awamu ya tatu ya utekelezaji wa mradi huo ambao utaanza katika mwaka wa fedha unaokuja wa 2022/2023. (Makofi)

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi.

Rais Samia Suluhu Hassan ameonesha nia ya kuimarisha na kuboresha kilimo na kiasi kwamba tumeongeza bajeti yetu ya kilimo; je, Serikali iko tayari kwa kushirikiana na Vyuo vya Kilimo kutusaidia sisi wananchi huko vijijini kwa kutuletea wale wanafunzi ambao wanakuwa kwenye mafunzo ya vitendo ili waje kushirikiana na wananchi katika kuimarisha nakuboresha kilimo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na programu hiyo ya kuwahusisha wale vijana ambao wako chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia programu ya uhanagenzi na tutaendelea kuifanya hivyo kuhakikisha kwamba wanafikia maeneo mengi zaidi lengo hapa ni kuhakikisha kwamba wanawafikia wakulima wengi zaidi, na wakulima wanapata elimu ya kilimo bora ili kuongeza tija na kufikia malengo ambayo tumejiwekea ya kukuza Sekta ya Kilimo kwa asilimia 10 ifikapo mwaka 2030.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, barabara ya Mafinga kwende Mgololo eneo la Itulavano, daraja lililopo ni jembamba sana na barabara hii inatumika na malori yanayobeba mazao ya misitu.

Je, Serikali ipo tayari kulirekebisha na kulijenga daraja hili ili liwe pana kumudu magari hayo mazito? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli hii barabara aliyoitaja ndiyo barabara ambayo kwa asilimia kubwa inapitisha mbao sehemu kubwa ambazo tunaziona, lakini barabara aliyoitaja pamoja na daraja iko kwenye mpango wa kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na kulijenga hilo daraja ambalo litaendana na barabara hiyo, ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, Mji wa Mafinga ni miongoni mwa miji 45 itakayonufaika na mradi wa TACTIC ambayo pia Jiji la Mbeya lipo.

Je, Mheshimiwa Waziri, uko tayari kukutana na Wabunge wa miji hiyo 45 ili kutueleza maendeleo ya mradi huo kama tulivyofanya kwenye miji 28 maji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, nitamwambia Waziri wa Nchi na tutakutana na Wabunge wote katika hiyo miji 45 ili kuwaelezea juu ya utekeleza wa mradi huo. (Makofi)