Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Ng'wasi Damas Kamani (2 total)

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ulio chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ulianzishwa kama namna mojawapo ya kutatua changamoto ya ajira kwa vijana na chanzo kikuu cha mapato katika mfuko huu ni bajeti inayotengwa na Serikali kupitia Bunge hili tukufu na kwa miaka saba mfululizo, mfuko huu umekuwa hautengewi fedha zozote. Mwaka 2022 mfuko huu umetengewa shilingi bilioni moja ambayo inatakiwa kwenda kwa vijana katika Halmashauri zote 185 nchi nzima. Fedha hizi ni ndogo, hazitoshi na hivyo hata impact ya mfuko huu haionekani kwa vijana. Sasa nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba inatafuta vyanzo vingine vya mapato katika mfuko huu ili kuutunisha na kuuongezea tija zaidi? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba tu ridhaa yako nimjibu Mheshimiwa Ng’wasi na nataka nimjibu kwa sababu ameuliza swali ambalo liko ofisini kwangu na nalifahamu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu inayo Wizara inashughulikia vijana na kwenye eneo hili, ziko programu mbalimbali za uwezeshaji kwa vijana wetu na tumeanzisha na mfuko huo wa vijana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amesema kwa miaka 7 haujatengewa fedha, lakini katika kipindi hiki hiki tulishatenga fedha zaidi ya bilioni moja, kumbukumu zangu nilizonazo ofisini zinaonesha mwaka 2017 tulitenga bilioni moja, hazitoshi kwa mahitaji ya vijana nchini, tukaongeza tena bilioni nane, tukawa na bilioni 1.8 na tulishaanza kuzitoa. Tunatoa kwa vijana kwenye halmashauri zetu ambao wanakidhi vigezo na vigezo kukidhi vigezo ni moja kwanza ufahamike na Ofisi ya Halmashauri, uko wapi? Unafanya nini ili unapopata ile fedha, basi Ofisi ya Halmashauri ambayo inaratibu vijana iwe inafahamu huyu kijana yuko wapi na kwa kuwa sehemu kubwa inaweza kuwa ni mikopo au support lakini tujue kwamba kama ni mkopo unaweza kuurejesha.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kinafanyika? Kwanza tumeunda mfuko maalum huu mfuko ambao tumeunda na tunao mwongozo wa kuendesha mfuko huo. Na mfuko huu, mbali ya Serikali lakini pia huwa tunatoa fursa kwa wadau kuuchangia na sasa tumeanza kuona taasisi mbalimbali ambazo zinasaidia Serikali yetu katika kukuza uwezo wa vijana uweze ku-support.

Nini Ofisi ya Waziri Mkuu imefanya, baada ya kuona kwamba kiwango hiki hakitoshi? Kwa kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu inalenga kuwawezesha vijana kumudu, kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi, sisi tumeanzisha programu ya uanangezi, programu ambayo inawachukua vijana na kuwapeleka kwenye vyuo mbalimbali nchini, ili kupata ujuzi ambao utamuwezesha yeye mwenyewe kujiajiri. Tunawapeleka VETA, tunawapeleka vyuo ufundi binafsi, lakini tunawapa pia mafunzo ya huduma, utoaji huduma, kuwapeleka mahotelini namna ya kutoa huduma kwenye hoteli mbalimbali na anapomaliza kozi yake ya miezi sita, ambayo inagharamiwa na Serikali anakuwa tayari anaweza kujiajiri au kuajiriwa na sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, programu hizi zipo nyingi na tunaendelea kuziratibu na nikuhakikishie najua Mheshimiwa Ng’wasi ni Mbunge na unawakilisha vijana tunao mpango wa kuhakikisha vijana hawa wanakuwa na uwezo, lakini wanakidhi vigezo vya kuweza kupata support kupitia mfuko huu.

Mheshimiwa Spika, lakini hatujaishia hapo tu, Serikali tumeendelea pia kutoa maagizo kwa Halmashauri za Wilaya, ule mfuko unaokopesha wa asilimia nne, wenye kipengele cha vijana cha asilimia nne nao pia wananufaika, na sasa nishauri ili waweze kunufaika waunde vikundi kwenye maeneo yao. Mmoja mmoja ni ngumu, unaweza kukosa kufikia vigezo, lakini mkiwa kikundi inakuwa rahisi zaidi mtafanya shughuli ya pamoja. (Makofi)

Kwa hiyo mfuko wa halmashauri wa asilimia nne nayo inasaidia katika halmashauri zote katika kutambua vijana na kuwa-support ili waweze kufanya shughuli zao kwa lengo la kuongezea uchumi wao. Kwa hiyo, programu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, programu iliyoko Ofisi ya Rais, TAMISEMI hizi zote kwa pamoja, lakini pia michango tuliyopata kwa wadau yote hii inaimarisha katika kuwawezesha vijana kufikia katua na malengo waliyojiwekea, ahsante sana. (Makofi)
MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi kwa kupata nafasi kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Natambua kwamba mwaka 2006 Bunge hili lilipitisha Sheria ya Benki ya Tanzania, ambayo chini ya kifungu cha 27(1)(b) inaipa Mamlaka Benki hii ku-design fedha kwa kuweka nembo na material mbalimbali. Pia natambua mwaka 2021 nchi hii imepata Rais wake wa kwanza Mwanamke anaefanya kazi nzuri na anatambulika katika Bara la Afrika na Duniani kama Rais madhubuti na wa mfano. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri Mkuu, natambua pia kwamba Bunge la Marekani sasa lipo katika utaratibu kupitisha sheria ambayo itawezesha Harriet Tabman, mwanamama, mwanaharakati aliyefanya kazi kubwa kwenye vita dhidi ya utumwa, kuwekwa kwenye dola ishirini kama kumbukumbu. Natambua kwamba katika Bara letu la Afrika nchi kama Nigeria, Malawi na Tunisia zimekwishafanya hatua hizi na zimetambuliwa na Benki ya Dunia na IMF kama hii hatua katika uelekeo unaofaa. Je, Serikali haioni sasa kwamba kuna haja ya kuweka kumbukumbu ya kudumu kwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka picha yake katika fedha za nchi hii? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ng’wasi, Mbunge Vijana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameonesha kutambua kazi nzuri, mchango unaotolewa na Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuona kama je, Serikali inaweza kuona umuhimu wa kutumia picha yake kwenye fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uwekekaji wa picha za viongozi mbalimbali ni maamuzi ambayo huko nyuma tulitoa kwa lengo la kukumbuka mchango wa Viongozi hawa kwenye Taifa hili, hasa picha ambazo zinatumika sasa za Baba wa Taifa hili, Mwalimu Julius Nyerere lakini pia na Mheshimiwa Sheikh Abeid Aman Karume Rais wa kwanza wa Zanzibar ili kutambua tu mchango wao walioutoa katika Taifa hili na kwa hiyo picha zao zilitumika kama sehemu ya kumbukumbu zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunazo aina ya fedha noti na hizi sarafu ambazo pia tunatumia kuweka alama za wanyama wetu. Hii ilikuwa ni kuenzi tunu ya Taifa lakini pia kuuboresha hamasa kwenye Utalii. Sasa maamuzi ya kuweka picha kwenye noti mara nyingi yanafanywa na maamuzi ya kiongozi mwenyewe kwa kushauriana na Benki Kuu. Sasa kwa kuwa umelileta hili na sisi tunatambua kuwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa mchango mkubwa kwenye Taifa hili, niseme tu tunapokea ushauri wako na litaingia Serikali litajadiliwa, pale ambako watafanya maamuzi kwa kushauriana na Benki Kuu taarifa zitatolewa rasmi. Ahsante sana. (Makofi)