Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Martha Nehemia Gwau (1 total)

MHE. MARTHA N. GWAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi uliyonipa na mimi kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na ongezeko kubwa la watu kuhamahama kutoka eneo moja kwenda lingine kwa sababu mbalimbali. Moja ikiwa kutafuta malisho na maji kwa wafugaji lakini pia wakulima kutafuta maeneo ya kilimo na pia kutafuta maisha kwa ujumla. Wanakohamia kunakuwa hakuna huduma muhimu za kijamii. Je, Serikali haioni haja sasa ya kuongeza maeneo ya utawala kama kusajili Vijiji na Kata mpya ili kupeleka huduma za msingi katika maeneo hayo ambayo watu wamehamia? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gwau, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhamahama kwa wananchi, kutafuta maeneo ya kuendesha shughuli za kijamii kwenye maeneo mengi, ndiyo hasa wananchi sasa hivi tumeona wakisambaa maeneo mbalimbali, lakini Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua kama je, Serikali haioni umuhimu kuanzisha maeneo mapya ya utawala?

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mapya ya utawala yanaanzishwa kwa vigezo. Moja, idadi ya watu; pili, uwezo wa mapato wa maeneo hayo ili kuweza kuendesha mamlaka husika; tatu, uwepo wa huduma za jamii; vile vile, uwezo wa Serikali wa kujenga makao makuu ya mamlaka hiyo mpya iliyoko eneo hilo. Mara kadhaa tumepata maswali haya maeneo mengi. Binafsi nilipofanya ziara kwa wananchi, yapo maeneo wameomba kugawanywa ili wapate mamlaka mpya ya halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini msimamo wa Serikali? Ni kwamba tukiwa tunaendelea kupata takwimu mbalimbali za maeneo haya na kuona umuhimu wa kugawa maeneo haya kuwa na utawala mpya, kwa miaka mitano iliyopita Serikali ilitoa mamlaka mpya kwa maeneo mapya ya vijiji, kata, wilaya, halmashauri na hata majimbo kwa upande wetu Wabunge na mikoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo haya bado tunaendelea kuratibu kwa kupeleka miundombinu wezeshi ya utoaji huduma ya wananchi wa eneo hilo kama makao makuu yake. Sasa hivi, tunaendelea na ujenzi wa ofisi, nyumba za kuishi watumishi wa viongozi kwenye maeneo haya na Serikali imeshaweka msimamo wake kwamba tunaendelea na kuimarisha meneo haya. Hatuwezi kuanzisha maeneo mapya huku tukiwa hatujakamilisha kuandaa mazingira mazuri ya maeneo ambayo tayari yametolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pindi itakapokamilika, ujenzi wa miundombinu wezeshi kwenye maeneo haya ili viongozi wa maeneo haya waweze kutoa huduma na wananchi wapate huduma kwenye maeneo hayo, sasa tangazo la Serikali litatoka. Halmashauri, mikoa, wilaya na maeneo mengine yanahitaji kuwa na mamlaka mpya zitaanza mchakato wa kuomba mamlaka hizo kwa kufuata taratibu zilizowekwa hasa zile ambazo zinajumuisha vikao vya wadau wenyewe kuanzia huko huko walipo, wakubaliane kugawana na pia kama kuna jambo lolote ambalo litahusisha mgawanyo huo, basi maamuzi ya vikao hivyo utakuja na baadaye muhtasari utakuja Serikalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais atakapoona sasa tumekamilisha ujenzi wa miundombinu, anaweza kutoa kibali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI ili kutoa mamlaka nyingine mpya. Huo ndiyo utaratibu wa Serikali tulionao kwa sasa. (Makofi)