Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Salim Alaudin Hasham (3 total)

MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, je, Waziri yupo tayari kutembelea baadhi ya zahanati, vituo vya afya pamoja hospitali ya wilaya ili kujionea changamoto hizo?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili, kwa kuwa upungufu wa watumishi katika jimbo langu umefikia asilimia 67, je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza watumishi wa afya katika Jimbo la Ulanga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya Mheshimiwa Salim Alaudin Hasham, Mbunge wa Jimbo la Ulanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni kama ombi, je, tupo tayari kutembelea jimbo lake na kujionea changamoto hizo zinazolikabili. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge tupo tayari mimi na mwenzangu Naibu Waziri wa TAMISEMI anayeshughulikia masuala ya afya Mheshimiwa Dkt. Dugange na tutafika katika eneo lake na kushuhudia haya ambayo ameyazungumza na tutachukua hatua za kimsingi kuwasaidia wananchi wa jimbo lake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili, ameuliza kama tupo tayari kuongeza watumishi. Niseme tu kwa kadri tutakapokuwa tunaendelea kupata kibali cha kuajiri kutoka Ofisi ya Rais – Utumishi tutaendelea kuajiri na kuongeza watumishi. Kwa hiyo, katika nafasi chache tunazozipata kama ambazo tunakwenda kuziajiri nafikiri kabla ya mwisho wa mwezi huu tutakuwa na watumishi kwenye kada ya afya karibu 2,700. Kwa hiyo, miongoni mwa watumishi hao wengine tutawaleta katika jimbo lako ili waweze kusaidia kuongeza ile ikama ya watumishi wa kada ya afya. Ahsante.
MHE. ALAUDIN H. SALIM : Mhesnimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kwamba Wilaya ya Ulanga ni kitovu cha uchimbaji wa madini, lakini pia kuna miradi mikubwa ambayo inaenda kuanza ya madini ya kinywa ambayo ina manufaa makubwa kwa nchi lakini pi kwa uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Ulanga. Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kujenga barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 67 kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Tarafa ya Mwaya ni tarafa inayoongoza kwa kilimo cha pamba pamoja na ufuta.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami ili wanachi hawa waweze kufikisha mazao yao sokoni kwa urahisi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika,naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Alaudini Hasham Salimu Mbunge wa ulanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali ni kujenga barabara kwa kiwango cha lami. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa barabara ambazo zinarudiwa na TANROAD kutoka Mpilo – Mahenge iko kwenye mpango wa EPC+F na tayari Wakandarasi wameshapita na barabara aliyoitaja ya pili Serikali inaendelea kutafuta fedha ili iweze kuijenga kwa kiwango cha lami ili kurahisisha usafiri na kuwafanya wananchi wa Ulanga waweze kufanya biashara zao kwa urahisi. Ahsante.
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Serikali imeliongezea Bonde la Mto Kilombero kwa maslahi mapana ya Taifa letu, kwa hiyo wananchi wa maeneo hayo wamekosa maeneo kwa ajili ya kilimo.

Je, ni lini Serikali itaenda kujenga mradi mkubwa, ili kutoa fursa kwa wananchi wa Jimbo la Ulanga, hususan kwenye Kata za Kichangani, Milola na Minepa, ili kupata sehemu ya uhakika ya uzalishaji mali?

Swali la pili, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kuboresha na kuuendeleza Mradi wa Skimu ya Umwagiliaji ya Minepa yenye ukubwa wa zaidi ya hekta 1,800 ili kutoa fursa kwa wananchi wa vijiji hivyo kupata sehemu kubwa ya uzalishaji mali? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza kama nilivyojibu katika swali langu la msingi kwamba, Skimu ya Minepa tunafanya upembuzi yakinifu na tunajua umuhimu wa skimu hiyo kwa sababu ina hekta karibu 1,800. Kwa hiyo, wakishamaliza watu wetu sisi jukumu letu ni kutafuta fedha na tutaanza ujenzi mara moja kwa sababu ya umuhimu huo.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu hii ya kwenye swali lake la kwanza vilevile alipouliza kuhusu eneo la Bonde la Kilombero na zile Kata za Kichangani, Milola na Minepa, wananchi bado wanauhitaji. Kwa hiyo, sisi bado tuko huko tunafanya upembuzi yakinifu, tukishakamilisha tu tutatoa taarifa hata kwa Mbunge mwenyewe na Wilaya yake, lvilevile tutatafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo, ahsante sana.