Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Kenneth Ernest Nollo (2 total)

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, nchi nyingi duniani zimerusha satellite angani kwa matumizi mbalimbali ikiwemo kupata takwimu sahihi za hali ya hewa. Katika anga la Afrika kwa sasa tuna satellite 41 na kati ya hizo 41 mbili zinatoka katika mataifa ya Afrika Mashariki. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuanza na programu ya kutengeneza satellite na baadaye tuweze kuirusha katika anga letu?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kenneth Nollo, Mbunge wa Bahi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa anahitaji kujua maendeleo ya teknolojia kwenye mawasiliano. Ameeleza kwamba nchi nyingine tayari zimejitegemea katika kununu mitambo inayowezesha nchi husika kuboresha mawasiliano yake. Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zinaendelea kwa kasi katika maboresho ya TEHAMA, na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kazi moja kubwa aliyoifanya ni kuanzisha Wizara ya Sayansi, Mawasiliano na Teknolojia ambayo pia ina habari mawasiliano na teknolojia ya habari ambayo pia inaendelea kufanya ufuatiliji wa maeneo ambayo tayari tunayo na maeneo ambayo bado hayapo kwa lengo la kufanya maboresho. Na Wizara, kama ambavyo inaendelea kufanya kazi yake na imeshapitishiwa bajeti yake, na Waziri hapa ameeleza maboresho makubwa yaliyofanywa nchini. Lengo hii teknolojia kufikisha kwa Watanzania mpaka vijijini. Tumeanza na teknolojia ambayo inawezesha kufanya mawasiliano maeneo yote, na tunapanua wigo huu mpaka kwenye ngazi za kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nikuhakikishie kwamba maeneo yote ambayo nchini sasa hayapo ambayo yanahitajika katika kuboreshwa mfumo mzima wa mawasiliano Serikali itafanya maboresho kutafuta fedha zaidi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba teknolojia tunaipandisha na teknolojia inawafikia wananchi wote mpaka kule vijiji, ahsante. (Makofi)
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali ya Awamu ya Sita imefanya kazi kubwa ya kujenga madarasa kwenye shule zote za msingi na sekondari na wakati mwingine imejenga shule iliyokamilika, kutokana na kufanya kazi hii tumeongeza wanafunzi wengi na kutokana na kuongezeka kwa wanafunzi tumeongeza upungufu wa walimu.

Mheshimiwa Spika, ziko halmashauri na majiji ambayo yanakusanya fedha nyingi, lakini nao wanasubiri mgao wa ajira hususan kama ya walimu waweze kupata sawa na halmashauri zingine ambazo hazina mapato.

Je, Serikali haioni kama ni busara na ni vyema kwamba halmashauri na majiji ambayo yana uwezo wa kuajiri walimu waweze kuajiri ili inavyokuja ule mgao wa kitaifa hawa wengine ambao hawana tuwe tumewapunguzia mzigo huo na kufanya hivyo ni kwamba maeneo yale tayari tutakuwa tumeondoa tatizo la walimu? Ahsante sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nollo, Mbunge wa Bahi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imesimamia mifumo ya ajira na ajira zote za kudumu ziko chini ya Serikali Kuu ikiwemo na sekta ya elimu kwa walimu. Nikiri kwamba tunao upungufu wa walimu kwenye shule zetu za msingi hata sekondari na upungufu huu unatokana na vipindi vya ajira, lakini hapa katikati kabla ya ajira kunakuwa na vifo kunakuwa na kustaafu lakini pia hata mpango usiokuwa mzuri wa kwenye halmashauri zenyewe kwa sababu walimu wengi wanaonekana wanajaa sana mijini kuliko vijijini, nitalisema baadae.

Mheshimiwa Spika, kwa nini ajira zote zimepelekwa Serikali Kuu? Lengo ni kuwa na mfumo mmoja wa kuajiri na kupata kanzidata yaani takwimu ya idadi ya waliopo kazini wanaoajiriwa, lakini pia kuweza kusambaza kwa usawa kwenye halmashauri zote ili kusiwe na halmashauri moja kuwa na mlundikano mkubwa kwa sababu tu wana uwezo wa wao kuajiri. Kwa hiyo, Serikali Kuu inasimamia kusambaza walimu nchini kote kulingana na mahitaji, kulingana na fani walizosomea, kwa mfano, masomo ya sayansi na masomo ya sanaa hiyo. Kwa hiyo, mahitaji yanakwenda nchini kote.

Mheshimiwa Spika, tunajua ziko halmashauri zenye uwezo, lakini kuna halmashauri ambazo hazina uwezo. Tukiruhusu halmashauri zenye uwezo ziajiri kuna hatari ya halmashauri ambazo zinapata pato chini ya uwezo wake hakutakuwa na walimu hakutakuwa na wafanyakazi na kwa hiyo, hakutakuwa na usawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali hatuwezi kuruhusu hili na ndio sababu ajira zote tumeweka za Serikali Kuu yenyewe inaajiri walimu 4,000 tunawagawa nchi nzima kulingana na idadi, uwiano wa masomo kwa maana ya fani, lakini na mahitaji ya hizo halmashauri. Tutaendelea kufanya hivi inatusaidia pia Serikali katika kulipa stahiki zao pamoja na mafao yao ya mwisho wa kustaafu, lakini pia inatusaidia kuwa na takwimu.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, sasa nitoe agizo kwa Maafisa Elimu na Wakurugenzi wa Halmashauri kufanya mapitio ya ikama zao. Hapa ndipo tatizo lilipo kwamba halmashauri inaruhusu eneo fulani kuwa na walimu wengi halafu kule vijijini hakuna walimu na kusababisha kuwa na upungufu mkubwa wa walimu, kumbe kama wangekuwa wamewasambaza vizuri ingekuwa na walimu wanaotosha kwenye fani zao. Kwa hiyo, wapitie ikama yao ili wajaribu kuona mlundikano wa walimu kwenye maeneo ya miji na barabarani ili wawapeleke pia na vijijini kuwe na utoshelevu halafu ile kanzidata isaidie pia katika kufanya kila shule kuwa na idadi nzuri ya walimu, hizi ndio sababu ambazo zinapelekea Serikali Kuu kuajiri centrally, ahsante sana. (Makofi)