Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. David Mwakiposa Kihenzile (16 total)

MHE. SALIM MUSSA OMAR aliuliza:-

Je, lini Shirika la Ndege Tanzania litaanza safari za Pemba?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kutujalia afya njema. Pili, kwa sababu ninasimama kwa mara ya kwanza hapa, nitumie nafasi hii kwa unyenyekevu mkubwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Uchukuzi. Kwa unyenyekevu mkubwa nimepokea uteuzi huu na ninaahidi kufanyakazi kwa juhudi, maarifa kwa ajili ya maslahi makubwa ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee ninakushukuru wewe kama mlezi na Kiongozi wangu kwa ushirikiano mkubwa ulionipatia nikiwa Msaidizi wako kwa nafasi ya Mwenyeketi wa Bunge na Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda, Kilimo na Mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, ninaomba sasa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi kujibu swali la Mheshimiwa Salimu Mussa Omar, Mbunge wa Gando, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ATCL itaanza safari za Pemba baada ya kupata ndege za kutosha kuweza kutoa huduma bila kuharibu ratiba za safari za sasa na urukaji kwa wakati. Kwa kuwa mwisho wa Septemba, 2023 ATCL inatarajia kupata ndege mpya moja aina ya Boeing B737-9MAX na ndege ndogo aina ya Dash 8 Q300 matengenezo yake yanatarajiwa kuwa yamekamilika na kurejea katika ratiba zake za utoaji wa huduma. Uwepo wa ndege hizo kutaiwezesha ATCL kuanzisha safari zake katika kituo cha Pemba kwa tija na ufanisi mkubwa.
MHE. OMAR ISSA KOMBO aliuliza:-

Je, lini Serikali itaweka Mdaki katika Bandari ya Dar es Salaam kwa meli za abiria na mizigo za Azam Sea Link ili kuondoa usumbufu na kero kwa abiria?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omar Issa Kombo, Mbunge wa Wingwi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TPA imenunua midaki mitatu kwa ajili ya kuimarisha shughuli za ukaguzi katika eneo la Azam Link na eneo la kuhifadhi mizigo (Baggage room) ambapo midaki miwili imeshafungwa eneo la kuingia na kutoka katika eneo la kuhifadhi mizigo (Baggage room) na mdaki mmoja utafungwa katika eneo la Azam Link. Aidha, kwa mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali kupitIa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), imetenga fedha kwa ajili ya kununua midaki mingine, kwa ajili ya eneo la Lighter Quay na yadi ya magari (RORO Yard), ahsante.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:-

Je, lini Serikali itafanya mapitio ya bei ya nauli za Shirika la Ndege Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kawaida nauli za safari za ndege hupangwa na soko kulingana na aina ya huduma inayotolewa. ATCL kama ilivyo kwa mashirika mengine ya ndege yanayotoa huduma zake kibiashara, nauli zake zinapangwa na soko kwa kuzingatia matakwa ya sheria za ushindani ambapo vigezo vinavyotumika katika kupanga nauli hizo ni pamoja na gharama za uendeshaji ili kuhakikisha kuwa mashirika ya ndege yanahimili ushindani wa soko na kujiendesha kwa tija na ufanisi.
MHE. ASYA SHARIF OMAR K.n.y. MHE. AMINA ALI MZEE aliuliza:-

Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa madarasa na mabweni ya Chuo cha Usafirishaji (NIT) Mabibo?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Ali Mzee, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali kupitia East Africa Skills for Transformation and Regional Integration Project (EASTRIP), mradi unaofadhiliwa na Benki ya Dunia, imeanza ujenzi wa mabweni mawili yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,500. Ujenzi wa mabweni hayo umefikia asilimia 28. Aidha, kupitia mradi huo Serikali inajenga jengo lenye Madarasa ya wanafunzi 1,500 pamoja na maabara na karakana yenye kuchukua wanafunzi 500 kwa wakati mmoja ambapo ujenzi huo umefikia asilimia 30.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Rasilimali Mafunzo (maktaba) chenye madarasa yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,653 kwa wakati mmoja ambapo ujenzi huo kwa sasa upo kwenye asilimia 85.

Aidha, katika mwaka wa fedha 2023/24, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Chuo, itaanza ujenzi wa Jengo la Kitaaluma la ghorofa tano litakalokuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 4,700 kwa siku, mara litakapokamilika.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka alama za kuongoza meli katika eneo la kuegesha meli kwenye Ziwa Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo:-

Mheshimwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA) ina mpango wa kujenga miundombinu ya bandari katika Ziwa Nyasa hususani Bandari ya Mbamba Bay. Ujenzi wa bandari hizi utahusisha pia usimikaji wa vifaa vya kuongozea meli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, TPA ina mpango wa kuweka alama za kuongozea meli katika bandari za maeneo mengine kuanzia mwezi Machi, 2024 kwani kupitia Mradi wa Upanuzi na Maboresho ya Miundombinu ya Bandari ya Dar es Salaam (Dar es Salaam Maritime Gateway Program – DMGP) maboya yaliyopo Bandari ya Dar es Salaam yataondoshwa kwa sababu mradi huo unahusisha pia uwekaji wa maboya mapya katika Bandari ya Dar es Salaam lakini kwa kuwa maboya hayo bado yapo katika matumizi yatasimikwa katika bandari nyingine.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza:-

Je, nini Mkakati wa Serikali wa kuifanya Bandari ya Tanga iwe na ufanisi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwanaisha Ng’anzi Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu sasa Bandari ya Tanga ilikuwa haihudumii meli na shehena ya kutosha kutokana na changamoto ya kasi ndogo ya huduma za meli na shehena hizo ambazo zilipaswa kuhudumiwa nangani umbali wa kilomita 1.7 kutoka gatini. Hali hii ilipunguza kwa kiasi kikubwa uwezo wa Bandari ya Tanga na ushindani wa bandari hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali kupitia TPA, inaendelea na maboresho ya bandari hiyo katika maeneo ya miundombinu, mitambo na vifaa ili kuvutia meli na shehena nyingi zaidi kama mkakati mahsusi wa kuifanya bandari hiyo ifanye kazi kwa ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizo TPA ina mkakati mahsusi wa kimasoko kwa ajili ya Bandari ya Tanga ambao lengo lake ni kuteka soko la kaskazini mwa Tanzania na nchi jirani za Rwanda, Burundi, Uganda na DRC. Mikakati hiyo ni pamoja na kuwashawishi wateja wakubwa kutumia bandari hiyo kwa kutoa punguzo la tozo.
MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI aliuliza: -

Je, lini Serikali itakarabati na kufufua reli kutoka Kilosa hadi Kidatu?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi, Mbunge wa Kilosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa vipindi tofauti imeendelea kuimarisha huduma za usafiri na usafirishaji katika maeneo mbalimbali nchini. Kuhusu ufufuaji wa reli kutoka Kilosa hadi Kidatu, Serikali kupitia TRC katika bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024 imetenga jumla ya shilingi bilioni 3.4 kwa ajili ya kuanza kazi za awali za marekebisho na ufufuaji wa njia katika kipande hiki chenye urefu wa kilomita 108 ambayo imefungwa kwa muda mrefu zaidi. Reli hii inaunganisha Reli ya Kati na TAZARA eneo la Kidatu. Aidha, kwa sasa TRC imekamilisha tathmini ya kihandisi ikiwemo makadirio ya gharama ya mradi (Engineering estimates) na inaendelea na ukamilishaji wa nyaraka za zabuni kwa ajili ya kumwajiri Mkandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia fursa hii kumuomba Mheshimwa Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi - Mbunge, pamoja na wananchi wa Kilosa kuwa na subira wakati Serikali inaendelea na juhudi ya urejeshwaji wa njia hii ambayo ni muhimu kwa ajili ya usafirishaji wa mizigo na abiria. Lengo la Serikali ni kuendelea kufanya maboresho katika maeneo yenye mahitaji ili wananchi waweze kuendelea kupata huduma za usafiri na usafirishaji.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI aliuliza: -

Je, Mkandarasi wa SGR kipande cha Seke-Malampaka hadi Malya ameajiri wananchi wangapi wanaotoka maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Maswa Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TRC imeendelea kumuelekeza mkandarasi wa ujenzi wa reli ya SGR, kuendelea kutoa ajira kwa wananchi wanaopitiwa na mradi, sambamba na kufuata taratibu na sheria za ajira nchini. Aidha, Serikali imeendelea kutekeleza ujenzi wa SGR kipande cha Mwanza - Isaka (kilometa 341), kinachojumuisha kipande cha Seke - Malampaka hadi Malya kama sehemu ya mradi huo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ajira; hadi kufikia mwishoni mwezi Agosti 2023, mkandarasi ameajiri jumla ya wananchi 6,793. Kati ya hao, wananchi 1,639 kutoka Mkoa wa Shinyanga, wananchi 1,973 kutoka Mkoa wa Mwanza, wananchi 525 kutoka Mkoa wa Simiyu, wananchi 352 kutoka mkoa wa Tabora na wanachi 2,304 kutoka mikoa mingine.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kumsimamia Mkandarasi kuhakikisha kuwa anaajiri kwa kutoa kipaumbele kwanza kwa wananchi wa maeneo husika kabla ya kutafuta ujuzi stahiki kutoka maeneo mengine.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka alama za kuongoza meli katika eneo la kuegesha meli kwenye Ziwa Nyasa?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo:-

Mheshimwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA) ina mpango wa kujenga miundombinu ya bandari katika Ziwa Nyasa hususani Bandari ya Mbamba Bay. Ujenzi wa bandari hizi utahusisha pia usimikaji wa vifaa vya kuongozea meli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, TPA ina mpango wa kuweka alama za kuongozea meli katika bandari za maeneo mengine kuanzia mwezi Machi, 2024 kwani kupitia Mradi wa Upanuzi na Maboresho ya Miundombinu ya Bandari ya Dar es Salaam (Dar es Salaam Maritime Gateway Program – DMGP) maboya yaliyopo Bandari ya Dar es Salaam yataondoshwa kwa sababu mradi huo unahusisha pia uwekaji wa maboya mapya katika Bandari ya Dar es Salaam lakini kwa kuwa maboya hayo bado yapo katika matumizi yatasimikwa katika bandari nyingine.
MHE. ALLY M. KASSINGE aliuliza: -

Je, lini Serikali italipa fidia kwa wananchi 438 Waliofanyiwa uthamini kupisha upanuzi wa Kiwanja cha ndege Kilwa – Masoko?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha robo ya mwisho wa mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali ilikamilisha zoezi la Uwekaji Wazi Daftari la Fidia (valuation report disclosure) kwa wananchi 438 waliofanyiwa uthamini ili kupisha upanuzi wa Kiwanja cha Ndege Kilwa Masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hatua hiyo, mnamo mwezi Agosti, 2023 Wizara ya Fedha ikishirikiana na Wizara ya Uchukuzi, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) na Ofisi ya Ardhi Mkoa wa Lindi, walifanya na kukamilisha zoezi la uhakiki wa daftari la fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hatua hizi, zoezi la ulipaji wa fidia litaanza mara baada ya Wizara ya Fedha kukamilisha taratibu zote za kifedha.
MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga Ghati la Kisasa la Abiria kwenye Bandari ya Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. DAVID M. KIHENZILE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ramadhan Suleiman Ramadhan, Mbunge wa Chakechake, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuimarisha huduma kwa wananchi wake katika maeneo mbalimbali ya nchi, likiwemo Jiji la Dar es Salaam. Ili kuendeleza juhudi hizo, Serikali kupitia TPA inakamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya ujenzi wa gati la kisasa kwenye Bandari ya Dar es Salaam, ambao hadi sasa upo katika hatua za mwisho na unatarajia kukamilika mwezi Desemba, 2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Ramadhan Suleimani Ramadhan na Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla kwa kuendelea kufuatilia kero za wananchi katika maeneo yao. Serikali itaendelea kuboresha huduma hizo ili kuwawezesha wananchi kufanya kazi zao bila kikwazo chochote.
MHE. AMINA ALI MZEE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia ajira ya kudumu vijana ambao wanatumika kama vibarua kwenye ujenzi wa Reli nchini?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Ali Mzee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa takwimu inaonyesha kuwa, toka kuanza kwa ujenzi wa mradi wa Standard Gauge mwaka 2017 hadi kufikia Desemba 2023 jumla ya vijana wa Kitanzania 51,153 wameshiriki katika ujenzi wa mradi wa SGR.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ya mwaka 1998, ajira katika Utumishi wa Umma uzingatia sifa na weledi (merits) na hutolewa kwa ushindani wa wazi. Hata hivyo, Serikali inatambua kuwa vijana wanaoshiriki katika mradi wa ujenzi wa SGR wanapata ujuzi mahsusi katika teknolojia ya reli ya kisasa ambayo itahitajika katika kuhakikisha uendelevu wa reli tunayoijenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua fursa hii kumtaarifu Mheshimiwa Amina Ali Mzee, Mbunge, kuwa kwa kuzingatia mahitaji ya uendeshaji wa reli, vijana hawa watapewa kipaumbele kwa kuwa na sifa za ziada (added advantage) zinazohusiana na ujuzi waliopata kwa kushiriki katika ujenzi wa reli pindi ajira hizo zitakapotangazwa.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani kumaliza migogoro kati ya bajaji na daladala katika miji mingi nchini inayotokana na routes kugongana?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Mwita Kembaki, Mbunge wa Tarime Mjini kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajaji ni miongoni mwa vyombo vya kukodi vinavyodhibitiwa na Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) kupitia Kanuni za Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (magari ya kukodi) za mwaka 2020 (TS 78). Daladala ni miongoni mwa vyombo vinavyodhibitiwa na LATRA kupitia Kanuni za Leseni za Usafirishaji (Magari ya Abiria) za Mwaka 2020 (TS 76).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo kwa vyombo vingine vinavyodhibitiwa chini ya Kanuni za magari ya kukodi, bajaji huwa hazipangiwi njia (route) ya kutoa huduma kama daladala. Badala yake, hupangiwa vituo vya maegesho kwa ajili ya kusubiri abiria ili wakodi na kupelekwa maeneo mbalimbali na kurejea kwenye vituo hivyo kusubiri abiria wengine. Aidha, kanuni ya 15 (h) ya Kanuni za magari ya kukodi inakataza vyombo vinavyodhibitiwa chini ya Kanuni za Magari ya Kukodi, kuingilia huduma za daladala au mabasi ya masafa marefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali kupitia LATRA imekuwa ikitoa elimu na kufanya ufuatiliaji kuhakikisha migogoro hii inakoma. Aidha, kwa sasa LATRA inahimiza madereva wa bajaji na pikipiki kuungana kupitia SACCOS kwa lengo la kuongeza elimu na usimamizi wa kundi hili. Tayari SACCOS inayojulikana kama KIBOBAT SACCOS imesajiliwa mkoani Kilimanjaro kwa ajili ya kufanya majiribio ya mpango huu kuanzia mwezi Februari, 2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Bunge lako Tukufu, napenda kuchukua nafasi hii kuiagiza LATRA kuongeza udhibiti wa vyombo hivi kwa kuharakisha jitihada za kuwaunganisha madereva wa pikipiki na bajaji kupitia SACCOS kwa lengo la kuongeza udhibiti wao. Aidha, niwaombe viongozi wa Serikali kwenye maeneo mbalimbali nchini kuungana na LATRA kuhakikisha bajaji zinatoa huduma kwa mujibu wa sheria ili kuepusha madhara ya kiuchumi na kijamii tunayoyashuhudia sasa.
MHE. ALLY M. KASSINGE aliuliza:-

Je, Serikali imefikia hatua gani kuwalipa fidia wananchi 438 waliofanyiwa uthamini ili kupisha upanuzi wa Kiwanja cha Ndege Kilwa Masoko?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kushughulikia na kufuatilia kwa ukaribu suala la ulipaji wa fidia kwa wananchi wanaopisha upanuzi wa Kiwanja cha Ndege, Kilwa Masoko linakamilika. Hatua ya awali ya kutambua wafidiwa na mali zao imekamilika na kuidhinishwa na Mthamini Mkuu wa Serikali. Sambamba na hilo maombi hayo yamewasilishwa Serikalini kwa ajili ya malipo. Hivyo, Serikali itahakikisha kuwa wananchi wote wanaopisha maeneo yao kwa ajili ya upanuzi wa kiwanja hicho wanalipwa fidia zao stahiki.
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR aliuliza: -

Je, lini Serikali itanunua meli za abiria zitakazorahisisha usafiri kwa wananchi kati ya Pemba, Tanga, Mtwara na Unguja?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bakar Hamad Bakar, Mbunge wa Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali kupitia Kampuni ya Huduma za Meli Tanzania (MSCL) imetenga kiasi cha fedha shilingi milioni 500 kwa ajili ya upembuzi yakinifu ili kujua aina ya meli zitakazojengwa kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya wananchi wa mikoa ya Tanga, Mtwara, Lindi, Pemba na Unguja ambapo zitatoa huduma kwa njia ya maji katika mwambao wa Bahari ya Hindi kwa ajili ya kuchochea ukuaji wa uchumi katika ukanda huo. Matokeo ya utafiti huo ndiyo yatakayobainisha aina na ukubwa wa meli itakayojengwa kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya soko Mikoa ya Pemba, Tanga, Mtwara na Unguja.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na mikakati ya Serikali ya kununua meli kwa ajili kutoa huduma katika mwambao wa Bahari ya Hindi, hata hivyo kutokana na fursa za kibiashara zilizopo katika mikoa ya Tanga, Unguja, Mtwara, Lindi na Pemba, Serikali imeendelea kuhamasisha sekta binafsi kutumia fursa hiyo kuwekeza kwa kununua meli za biashara ili kuhudumia hilo soko ambapo kutachochea ukuaji wa uchumi katika mikoa hiyo na kuongeza pato la Taifa kwa ujumla.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuanza ujenzi wa kipande cha Reli ya TAZARA kutoka Tunduma hadi Bandari ya Kasanga?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephat Sinkamba Kandege, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuunganisha reli ya TAZARA na Bandari ya Kasanga ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo katika ukanda huo hususani Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa TAZARA inamilikiwa na Serikali mbili; Tanzania na Zambia, tumeanza mazungumzo na wenzetu Zambia ili kutenga fedha katika bajeti ya TAZARA kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa awali wa reli hiyo kwa lengo la kubaini gharama za ujenzi wake na manufaa yake kiuchumi.