Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Jerry William Silaa (3 total)

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza: -

Je, upi mkakati wa kuwapa Wananchi ardhi mbadala wanapoondolewa kwenye maeneo yao kupisha uhifadhi na miradi ya mkakati?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri, kunakuwepo na ulazima wa wananchi kuachia ardhi pale ardhi inapohitajika kwa matumizi ya umma. Mahitaji hayo ni pamoja na ardhi ya uhifadhi na ardhi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, mfumo wa sheria nchini, umeweka wazi juu ya takwa na haki ya wamiliki wa ardhi kulipwa fidia ya ardhi na maendelezo pale ardhi inapotwaliwa kwa matumizi ya umma. Aidha, sheria inaruhusu fidia hiyo kulipwa kwa fedha taslimu au kupatiwa ardhi mbadala. Pamoja na sheria kuruhusu wananchi kupewa ardhi mbadala pindi ardhi yao inapotwaliwa, wananchi wamekuwa wakipendelea fidia ya fedha badala ya ardhi mbadala ili kuwawezesha kutafuta maeneo mengine wanayoyahitaji. Ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO aliuliza:-

Je, lini Wilaya ya Rungwe italetewa Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuajiri Wenyeviti wa Mabaraza ya Ardhi ili kuongeza kasi ya kusikiliza na kuamua mashauri ya ardhi. Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Wilaya ya Rungwe ameteuliwa na kupangiwa kituo tarehe 18 Septemba, 2023 na tayari ameanza kazi. Nakushukuru.
MHE. DEODATAUS P. MWANYIKA aliuliza: -

Je, kwa nini Sheria za Ardhi zinazokusudiwa kutumika kwenye miji zinatumika maeneo ya vijijini?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa kisheria wa usimamizi wa ardhi nchini umegawa ardhi katika makundi matatu ambayo ni Ardhi ya Kijiji, Ardhi ya Hifadhi na Ardhi ya Jumla. Kwa kuzingatia mgawanyo huo, Ardhi ya Vijiji inasimamiwa na Sheria ya Ardhi ya Vijiji, Sura 114 na maeneo ya miji yanasimamiwa na Sheria ya Ardhi, Sura 113. Hata hivyo, yapo baadhi ya maeneo ndani ya mipaka ya vijiji yanayosimamiwa na Sheria ya Ardhi, Sura 113 kutokana na kumilikishwa kabla ya kuanza kutumika kwa Sheria ya Ardhi ya Vijiji, Sura 114 au kuhawilishwa. Aidha, baadhi ya maeneo ya vijiji yametangazwa kuwa ya kuendelezwa kimji (Planning Area) na kuandaliwa Mpango Kabambe (Master Plan) na hivyo kuyafanya yasimamiwe na Sheria ya Ardhi, Sura 113.