Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Jerry William Silaa (16 total)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Je, ni lini Wizara ya Ardhi itaingilia kati kutusaidia kutatua migogoro iliyopo ndani Kata ya Kapele kwa kuwafuatilia watu wote ambao wamehodhi na kupora maeneo ya wananchi kinyume na utaratibu bila kuwa hati na wengine kuwa na hati za uwongo kwa kigezo na kusingizia wametumwa na wakubwa huko juu? Ni lini Wizara ya Ardhi mtatusaidia kutatua jambo hili?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Nina nyongeza ndogo kwenye majibu hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa kuzungumza, naomba dakika moja kutoa shukrani. Kwanza, namshukuru sana Mwenyezi Mungu ambae amenipa kibali kuhudumu kwenye Wizara hii ya Ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuniteua kuhudumu na kumsaidia kama Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Ninachoweza kumuahidi ni utumishi uliotukuka wa uadilifu. Nitatumikia kwa nguvu zangu na akili zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaliomba Bunge lako tukufu ushirikiano na wakati wote nitakuwa tayari kwa ajili ya kufanya kazi hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa nyongeza ndogo ya majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Serikali imejipanga na lipo suala la migogoro ya ardhi. Serikali kupitia Kamati ya Mawaziri Nane ilishafanya utatuzi wa migogoro ya ardhi kwenye vijiji 975.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutumia fursa hii kuwakumbusha Wakuu wa Mikoa 26 yote ya nchi nzima, kuendelea na utekelezaji wa maagizo ya Baraza la Mawaziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwaahidi Waheshimiwa Wabunge ambao wengi tumekutana na wameelezea kero zao akiwemo Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Momba, Mheshimiwa Condester. Baada tu ya Bunge hili kuna mkutano wa Kimataifa Arusha na unaisha Alhamisi, tutajipanga kuanza ziara nchi nzima kutekeleza maagizo ya Baraza la Mawaziri kwenye vijiji 975. Vilevile, kutatua migogoro yote ambayo inajitokeza kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ushirikiano. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa tena nafasi niulize swali la nyongeza, kwanza nitoe shukurani nyingi kwa majibu mazuri ya Serikali kupitia kwa Waziri wa Ardhi, Mheshimiwa Jerry Silaa ambaye alikuwa Mwenyekiti wangu Kamati ya PIC, nimpongeze kwa kuwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu majibu yake yapo sawasawa lakini watendaji wakati wa kutekeleza huwa hawaweki bayana sheria inasemaje badala yake wanakuja wanakuambia jamani hili eneo linachukuliwa kwa ajili yakazi hii na hii ya Serikali ninyi mnatakiwa muondoke, mtapata fidia kwa maendelezo ambayo mlikuwa mmefanya.

Je, Serikali haioni sasa kwamba ni muhimu wakati wa kuhamisha wananchi kwenye maeneo yao watoe maelekezo kwamba watapata nini na nini kulingana na eneo ambalo linachukuliwa either kwa uhifadhi au utekelezaji wa miradi?

Pili, swali langu ni je, Waziri utakuwa tayari kuambatana na mimi tuende tukafanye mkutano uwaeleze wananchi maeneo ya Momela pamoja na KIA ambao wanatakiwa wahame?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa majibu kwa maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa John Danielson Pallangyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, naomba kutumia Bunge lako tukufu kuagiza Wathamini wote na Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali kuhakikisha inatoa elimu stahiki kwa wananchi pindi ambapo maeneo yao yanatwaliwa kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo. Wananchi waelezwe wazi takwa la sheria kwa wale wanaotaka kuchukua fedha taslimu kwa niaba ya ardhi yao na kwa wale ambao wanataka kutafutiwa ardhi mbadala.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, pamoja na kwamba niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Dkt. John Pallangyo lakini eneo la KIA na eneo la Momela ni maeneo ambayo yanaangukia kwenye vile vijiji 975 ambapo wananchi walikuwa wameingia kwenye maeneo ya hifadhi na wengine wameingia kwenye eneo la Uwanja wa Ndege wa KIA. Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan iliona ni busara kuwafidia kwa yale maendelezo waliyoyafanya, maeneo haya fidia yao wanayolipwa haihusishi ardhi ambayo wamekuwa wakiikalia. Baada ya Bunge hili Mheshimiwa Dkt. Palangyo tutaongozana pamoja kwenda kutoa elimu kwa wananchi wa Jimbo lako, ahsante. (Makofi)
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ninaipongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba ni sikivu sana, kwa sababu niliuliza hili swali la imelitekeleza. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuyaelimisha Mabaraza ya Kata ili yasitoe hukumu kwenye mashauri ya ardhi?
Swali langu la pili, katika Wilaya ya Chunya hakuna kabisa Baraza la Ardhi, ukizingatia wananchi wa Chunya wanatoka Kambikatoto, Kipambawe, Mafieko, Bintimanyanga, Matwiga, Luhanga, Ifumbo na Shoga wanakwenda kushtaki mashauri yao kwenye Jiji la Mbeya.

Je, ni lini Serikali itawaepushia shida hiyo wananchi wa Wilaya ya Chunya?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Mabaraza ya Ardhi ya Kata yameanzishwa chini ya Sheria Sura ya 206 na kupitia Bunge lako Tukufu kwenye Marekebisho ya Sheria Namba 3 ya Mwaka 2021 Mabaraza haya yalipunguziwa nguvu ya kimaamuzi na yanapaswa kufanya usuluhishi ndani ya siku 30 baada ya shauri kufikishwa.

Mheshimiwa Spika, tuliongea na Waandishi wa Habari lakini naomba kutumia Bunge lako Tukufu kuwatangazia wananchi wote kwamba Mabaraza ya Ardhi ya Kata nguvu yake ya kisheria ni kufanya usuluhishi ndani ya siku 30 tokea shauri lifikishwe mbele yake. Baada ya hapo kama usuluhishi utashindwa kufanyika mashauri yawasilishwe kwenye Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya. Ninaomba tena kupitia Bunge lako, Wakurugenzi wa Halmashauri maana Mabaraza ya Ardhi ya Kata yanasimamiwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Wakurugenzi wa Halmashauri wanasimamia kwa niaba yake, Waendelee kusimamia mabaraza haya ili wananchi waendelee kupata haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kweli kati ya Mabaraza ya Wilaya zote 139 ni Mabaraza 94 tu ndiyo yenye Wenyeviti wa Baraza la Wilaya. Tayari ofisi yangu imeendelea kufanya mawasiliano ya kuomba vibali vya ajiri kwa ajili ya kupata ajira ya kuajiri Wenyeviti wengine 45, lakini kwenye maeneo yote ikiwemo Wilaya ya Chunya kwenye maeneo aliyotaja Mheshimiwa Mbunge ikiwemo Maeneo ya Bintimanyanga na maeneo ya Shoga tunaendelea kutoa maelezo kwa Msajaili wa Baraza la Ardhi la Wilaya kutumia Wenyeviti wa Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya ya jirani kwenda kwenye mabaraza haya kwenda kusikilza mashauri mpaka pale Serikali itakapokamilisha Wenyeviti kwenye Mabaraza ya Wilaya zote, ninakushukuru. (Makofi)
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa ya swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika Bunge la Bajeti lililopita Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata aliuliza swali juu ya mgogoro huu na ulitoa maelekezo kwamba Waziri afanye utaratibu wa kuja kuangalia mgogoro huu na umalizike. Hata hivyo, nashukuru Naibu Waziri alikuja, jambo lililofanyika ni kutoa maelekezo kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wahakikishe wanashughulikia tatizo hili. Mheshimiwa Naibu Waziri hakupata fursa ya kwenda field kuona tatizo na uhalisia wake.

Mheshimiwa Spika, naomba tena nirudie, naomba tena kupitia Bunge lako, niombe Waziri aje Mkoa wa Rukwa, aende akafuatilie aone uhalisia wa tatizo hili kwa sababu suala la kumuachia Mkuu wa Mkoa limekuwepo tangu miaka 13 iliyopita ambapo Mkuu wa Mkoa, mama yangu Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya analijua vizuri. Ninataka Waziri aje na timu ya wataalam wajifunze vizuri kuliko haya majibu ambayo yanaweza yakachochea hasira na mgogoro zaidi, nakushukuru. (Makofi)
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini niungane na Mheshimiwa Mbunge kwa concern yake ya kupambania wananchi wake.

Naomba nimuahidi tarehe 17 Novemba, baada tu ya Bunge hili nitafika jimboni kwake, nikiambatana na timu ambayo tumeunda task force ya wataalam kwa ajili ya kutatua migogoro mikubwa kama hii, kwenda uwandani kuona hali halisi na kutatua tatizo hili mara moja, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mheshimiwa Waziri, nakushukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Hata hivyo, uhalisia uliopo ni kwamba, kuna mkanganyiko mkubwa sana kwenye halmashauri za miji ambazo zina vijiji. Sasa, Waziri atakubaliana nami kwamba, ni wakati sasa wa kutoa maelekezo kwa sababu sheria inataka utayari wa eneo kabla halijawa declared planning area. Maeneo mengi yamekwenda kuwa declared planning area kabla hayajawa tayari na ni maeneo ya vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa yuko tayari kutoa maelekezo ili kufanyike marekebisho ya kutangaza upya maeneo ya vijiji yasitawaliwe na Sheria za Miji? Ahsante.
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, kwa kuendelea kufuatilia maslahi ya wananchi wake wa Jimbo la Njombe Mjini. Ni kweli Sheria ya Mipango Miji, Sura ya 355 kifungu cha 77(1)(b) kinampa mamlaka Waziri mwenye dhamana ya Ardhi, kutoa Kanuni zinazoongoza upangaji wa miji (Planning Space Standard). Vilevile mwaka 2018 Kanuni hiyo ilitolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilithibitishie Bunge lako kwamba Kanuni hii tumeisimamisha na tumetoa maelekezo kwa wataalam wa ardhi wa Wizara ya Ardhi, kuipitia upya na kutoa Kanuni ambayo itaendana na hali halisi ya maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kanuni hii ndiyo inayohusika kwenye ujenzi wa vituo vya mafuta vile vyenye ardhi ndogo, inahusika kwenye mashamba ya mijini ya ekari tatu na ukiangalia hali halisi ya Mji wa Njombe kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni mji wa kilimo. Pia kilimo kinacholimwa pale ni kilimo cha parachichi na sisi Wizara ya Ardhi hatuwezi kuwa kikwazo cha kuendeleza zao la parachichi ambalo linalimwa kwenye Wilaya ya Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kuirejea Kanuni hiyo na tutamshirikisha Mheshimiwa Mbunge wa Njombe na Wabunge wengine wenye maeneo ya vijiji ambayo na sura ya kijiji, ili Kanuni itakayotoka iweze kuendana na mazingira ya wananchi hao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza swali lingine la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, eneo hili lilipimwa zaidi ya miaka mitano iliyopita na mahitaji ya ardhi kwa uwekezaji katika Wilaya ya Kigamboni ni kubwa sana.

Je, ni ipi mikakati ya Serikali ya kulitangaza eneo hili kwa ajili ya uwekezaji?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kushukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika jitihada zake anazofanya katika kukuza uwekezaji na tumeanza kupata maombi ya uwekezaji katika eneo hili. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge na yeye kwa kutumia influence yake na Bunge lako Tukufu kuendelea kuwatangazia wawekezaji wote wenye nia ya kujenga viwanda kuweza kuwasilisha maombi yao. Ahsante.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Je, ni ipi kauli ya Wizara ya Ardhi kuwasaidia wananchi ambao maeneo yote yaliyokuwa yametengwa ya kutumika ya umma yakaporwa na watu ambao wanajiita ni wawekezaji; kwa mfano, Kijiji cha Msungwe, ata ya Kapele yuko mwekezaji ambaye amepora ardhi ya kijiji yenye zaidi ya ekari 1000; ni upi msaada kutoka kwenye Wizara hii?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, maeneo ya ardhi za vijiji kikiwemo Kijiji cha Msungwe kwenye Jimbo la Momba yanaongozwa na Sheria Na. 5 ya Ardhi ya mwaka 1999 ambayo inatoa mamlaka ya wananchi kusimamia ardhi yao na kutoa kiasi cha ardhi kinachogaiwa kwenye kila ngazi kutoka kijiji, wilaya na mpaka Kamati ya Uwekezaji ya Taifa. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge awasilishe malalamiko ya wananchi wao na tutaishughulikia na tutatoa majibu na haki ya wananchi itapatikana. (Makofi)
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza Serikali kwamba, miji midogo ambayo inachipukia kwa kasi kama Dumila ambao una wakazi zaidi ya 47,000;

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kwenda kupima, kupanga na kumilikisha maeneo hayo?

(b) Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuungana nasi baada ya Bunge kuja Wilaya ya Kilosa, kwa maana ya Jimbo la Kilosa na Mikumi, kwa ajili ya kuangalia migogoro ya ardhi ambayo inapelekea migogoro ya wakulima na wafugaji?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaelekeza maeneo yote siyo tu yanayokua kimiji kupangwa na kupimwa ili kuyatengenezea matumizi bora ya ardhi. Niungane mkono na Mheshimiwa Mbunge kwamba mji mdogo alioutaja unapaswa kufanyiwa mipango ya matumizi bora ya ardhi. Nimuombe tushirikiane katika kuangalia kama halmashauri yake imetenga fedha na pale Wizarani kama tuna uwezo kupitia Mradi wa KKK tuweze kufanya jambo hilo kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, swali la pili baada tu ya Bunge hili la mwezi Februari ninayo ziara ya Jimbo la Kilombero kwa Mheshimiwa Asenga, uko mgogoro kule wa Baba Askofu, nikifanya ziara hiyo namuomba Mheshimiwa Mbunge mara baada ya kikao hiki tukutane tupange ratiba; tutapita na Wilaya ya Kilosa kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kuna mgogoro mkubwa sana kati ya wakulima na wafugaji Mkoa wa Lindi kwenye Wilaya ya Liwale, Kilwa, Nachingwea na Mchinga unaopelekea kuuana na mashamba ya watu kuliwa na mifugo.

Je, Serikali ina mpango gani kabambe kutokomeza suala hili ili wananchi waishi kwa amani?(Makofi)
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna tatizo kubwa la migogoro baina ya wakulima na wafugaji na katika Wilaya alizozitaja Mheshimiwa Mbunge za Liwale na Nachingwea Mkoani Lindi tatizo hili ni kubwa. Vilevile, lilijitokeza kwenye ziara ya Mheshimiwa Rais kwenye Mikoa ya Mtwara na Lindi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujipanga kupitia Wizara husika kwa maana Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Kilimo na Wizara ya TAMISEMI na itakuja na mpango kabambe wa kuhakikisha kadhia hii inaisha na wakulima na wafugaji wanaendelea kufanya shughuli zao katika matumizi bora ya ardhi bila ya kuingiliwa na kuleta machafuko na kuvunja amani.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na migogoro kati ya Kata ya Makanya Ruvu na Makanya Bangalala ya muda mrefu. Je Serikali ina mpango gani wa kumaliza migogoro hii ya ardhi? Ahsante.
SPIKA: Hizo kata ziko wapi Mheshimiwa?

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same, Jimbo la Same Magharibi.
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli wiki iliyopita nilipita Bangalala na Makanya na Mbunge wa Jimbo la Same Magharibi Mheshimiwa David Mathayo. Tayari nimeunda timu ndogo itakwenda Bangalala na Makanya tarehe 07 ya mwezi huu na baada ya kuniletea taarifa nitafika tena kwenda kutoa majibu ya mgogoro huu ambao umekuwa ukiwasumbua wananchi kwenye mipaka yao.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika eneo la Himo, maeneo yale ya Lokolova na mjini ilipokuwa estate ya sisal kuna mgogoro mikubwa na ambayo pia inazuia maendeleo ya pale. Je, Waziri atakubali kuenda na mimi Jimboni baada ya Mkutano huu ili aweze kutatua migogoro hii?(Makofi)
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli mgogoro wa Lokolova pale Himo kwenye Jimbo la Mheshimiwa Dkt. Kimei ni mgogoro mkubwa baina ya Chama cha Ushirika na wakazi ambao wanadai kuwa ni wakazi wa asili wa eneo hilo. Mgogoro huu tayari taarifa yake imeshaandaliwa na tumeshakubaliana na Waziri wa Kilimo mara baada ya Bunge hili tutakwenda kwa pamoja kumaliza mgogoro huu uishe kabisa na usiendelee tena ili wananchi waweze kuendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii.(Makofi)
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kwenye swali hili la msingi.

Swali la kwanza, je, ukiacha hii Sheria ya Milki anayoizungumzia ni lini Serikali kwa ujumla wake kabisa italeta sheria kubwa na pana itakayo govern sekta ya makazi na upangishaji kwa maana ya real estate?

Swali la pili, je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha kanzidata ya nyumba za kupangisha kwenye Majiji, Manispaa na Miji ndani ya nchi yetu?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi tupo katika hatua za ndani za Serikali, kuandaa sheria itakayotoa mwongozo wa jinsi ya kuenenda kwenye soko la nyumba kwa maana ya real estate. Sheria hiyo pamoja na mambo mengine itaunda chombo ambacho kitasimamia mawakala wote wa upangishaji na upangaji wa nyumba.

Mheshimiwa Spika, swali pili Wizara inaendelea na mchakato na iko katika hatua za mwisho kabisa za kutengeneza mfumo mkubwa wa management ya ardhi nchini. Moja kati ya maeneo hayo unapotaja mfumo wa usimamizi wa ardhi, utataja nyumba zilizoko kwenye maeneo yetu vilevile itatoa matumizi ya nyumba ile ikiwa ni pamoja na matumizi ya ardhi ya kiwanja kile.

Mheshimiwa Spika, katika mfumo huo tutazingatia ushauri wa Mbunge kwa kuweka uwezo wa kujua nyumba za upangaji ziko ngapi na kuweza kutoa miongozo na kuweza kuzisimamia ili wananchi wasiweze kupata taabu zilizopo sasa.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni ipi kauli ya Serikali kuhusiana na wananchi wanaoishi katika nyumba za Keko Flats ambao ni takriban miaka saba sasa waliambiwa kuna mwekezaji na wamekataliwa kulipa kodi hawapeleki National Housing, wako katika dilemma. Sasa sijui majibu ya Serikali yakoje, mwekezaji yupo au waendelee kukaa bila kulipa kodi, Je wakija kuwaambia waanze kulipa watadaiwa kuazia hiyo miaka saba iliyopita? Naomba majibu ya Serikali.
SPIKA: Naona maswali yako yamekuwa mengi, uliza moja kati ya hayo.

MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ni upi mkakati wa Serikali kuhusiana na wananchi wanaoishi katika eneo lile la Keko National Housing.
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Kilave ni jirani yangu swali hili nitawasiliana na uongozi wa National Housing na nitampa majibu kwa haraka sana kwa sababu linahitaji details na nitampa majibu yake leo hii.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Wilaya ya Rorya haina Baraza la Ardhi la Wilaya jambo linalosababisha wananchi kusafiri umbali mrefu zaidi ya kilomita 60 mpaka 100 kwenda Tarime kufuata huduma hii, ambapo kwa umbali huo wakati mwingine wananchi hukata tamaa kushughulikia haki zao za kimsingi na za kisheria za utatuzi wa migogoro ya ardhi. Je, Mheshimiwa Waziri haoni sasa kuna umuhimu wa kuanzishwa Baraza la Ardhi la Wilaya ya Rorya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kumekuwa na minong’ono mingi ya wananchi kuhusu kukithiri kwa vitendo vya rushwa kwenye utatuzi wa migogoro kwenye Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya. Nataka kujua mpango mkakati milionao kama Serikali kuhakikisha kwamba vitendo hivi vya rushwa ambavyo vinanyima haki kwa wananchi, Serikali mmejipanga vipi kushughulika navyo ili angalau wananchi waweze kupata haki zao za kimsingi katika maeneo haya? Nashukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nia hasa ya kuanzisha mabaraza haya yalikuja wakati wa ripoti ya Profesa Issa Shivji katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kutatua migogoro ya kisheria katika kipindi ambacho Mahakama zilikuwa hazina ufanisi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi, kwa sasa Mahakama zetu zimeboreshwa sana, zina mifumo ya kisasa na zimesambaa nchi nzima na ndiyo nia ya Serikali kuondoa Mabaraza haya kwenye Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupeleka kwenye Wizara ya Katiba na Sheria chini ya Mhimili wa Mahakama. Katika kufanya hivyo, moja itatatua tatizo ambalo sasa wanalipata wananchi wa Rorya la kusafiri umbali mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kwamba kumekuwa na malalamiko mengi hata kwa Waheshimiwa Wabunge humu ndani kuhusu tuhuma za rushwa kwenye Mabaraza haya. Wizara ilishatoa taarifa kwenye Kamati ya Bunge na ninaomba nitoe taarifa mbele ya Bunge lako Tukufu, pale tutakapopata taarifa mahsusi za Baraza ambalo limefanya shauri kwa kutumia maamuzi ambayo yanaonekana yameshawishiwa na rushwa, tutachukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa nimekubaliana na Mheshimiwa Chege, Wizara inaendelea na taratibu za kuongeza Wenyeviti wa Mabaraza. Mpaka sasa tuna wilaya 36 ambazo zina mabaraza ikiwepo Wilaya ya Rorya, na pale tutakapopata Mwenyekiti wa Baraza, nimwahidi kwamba tutampeleka Mwenyekiti na Baraza litaanzishwa kwenye Wilaya ya Rorya.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Mwaka huu 2024, Januari Mheshimiwa Waziri wa Ardhi alikuja Same kushughulikia matatizo ya ardhi na mipaka katika Kata za Ruvu, Makanya na Bangalala na alituma wataalam wakaangalia matatizo yalivyo. Je, Mheshimiwa Waziri atarudi lini tena Same kwenye Kata za Bangalala, Makanya na Ruvu ili kushughulikia matatizo hayo?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakiri kwamba tarehe 26 Januari, 2024 nilifika Wilaya ya Same kwenye Jimbo la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo. Kweli timu imeshakwenda na taarifa wameshaniwasilishia, na ninamwomba subira Mheshimiwa Dkt. David Mathayo, amekuwa akifuatilia kwa karibu sana, na pia nawaomba subira wananchi wa Jimbo la Same Magharibi, pindi nitakapomaliza bajeti yangu mwisho wa mwezi huu, Juni mwanzoni nitaongozana na Mheshimiwa Mathayo, tutaenda kutoa taarifa hiyo kwa wananchi, naomba wawe wavumilivu. (Makofi)
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mabaraza haya ndiyo yamekuwa chanzo cha kurefusha migogoro ya ardhi nchini. Ni lini sasa mtaleta sheria ili mabaraza haya yaweze kuondolewa na kesi hizi ziweze kuendelea kwenye Mahakama zetu?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, Mbunge kwamba, ni kweli kuna mlolongo mrefu kama alivyosema Mheshimiwa Chege. Mabaraza hayapo wilaya zote, wapo Wenyeviti wanaolazimika kufanya mabaraza zaidi ya wilaya moja na hii inachelewesha haki kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali inamalizia mikakati ya hatua za mwisho za kuhamishia mabaraza haya kwenye mhimili wa Mahakama na pindi itakapokuwa tayari tutaleta sheria Bungeni kwa ajili ya kutekeleza utaratibu huo. (Makofi)