Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Amina Ali Mzee (2 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. AMINA ALI MZEE: Mheshimiwa Spika, naomba Serikali iwatumie wanafunzi wa Kitivo cha Kilimo SUA kufanya tafiti mbalimbali za kilimo.

Kwa nini tunakuwa watumwa wa sayansi? Ikiwa wataalamu waliosomea sayansi hawawezi kuitumia sayansi kubadilisha mwelekeo wa idara wanazozifanyia kazi basi wanasayansi hao hawasaidii Serikali na inabidi Serikali ichue hatua.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali iwaandae vijana kuweza kuwaendeleza kwenye kilimo kwa kupatiwa elimu, mikopo na masoko kuweza kujikwamua kiuchumi na kuzalisha ajira nyingi nchi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. AMINA ALI MZEE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nami sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia taarifa ya Kamati hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina budi kumshukuru Mwenyezi Allah Subhana Wa Ta’ala, lakini nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika bajeti ya Wizara hii ilitutengea jumla ya bilioni moja katika sekta ya uchukuzi katika ununuzi wa mitambo ndani ya Chuo cha DMI. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru Mama yetu Kipenzi, Mama Samia Suluhu Hassan ndani ya chuo hichi mtambo huu wa scanner umefika ndani ya chuo na tayari wanafunzi wanaendelea kufaidika na mtambo huu kwa ajili ya kujisomea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite katika mchango wa kamati, changamoto ya kamati yetu zinaonyesha suala la madeni ndani ya taasisi za Serikali. Taasisi nyingi za Serikali zinaonyesha bado zina madeni. TBA inadai madeni mengi katika taasisi za Serikali, kupitia Wakala wa Madeni tuliweza kukusanya jumla ya trilioni saba kwa ajili ya ulipaji wa madeni. Jumla tulikuwa tuna deni la bilioni 25. Tuipongeze TBA kwa kuhakikisha kuendelea kulipa madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tutoe wito kwa Serikali kwa kupitia taasisi zake, Wizara mbalimbali za Serikali zinadaiwa na TBA. Kama sera yetu ya mashirika inavyosema tuhakikishe mashirika yanaendelea kujitegemea kiuchumi na kujiendesha kibiashara na faida. Taasisi za Serikali zijitahidi kulipa madeni ili kuhakikisha Shirika letu la TBA linaendelea kunyanyuka na kuendeleza biashara zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto pia iliyoelezwa suala la upungufu wa watumishi; ndani ya sekta yetu ya uchukuzi tuna takribani upungufu wa watumishi 18,000 lakini mpaka sasa Serikali imeendelea kuajiri watumishi 12,000, tuna upungufu wa watumishi 6,000. Serikali yetu tukufu inayoongozwa na Mama yetu mpendwa, tunaiomba Serikali yetu upungufu wa watumishi 6,000 kuhakikisha kuziba gap ili watumishi wengi wazidi kupata nafasi. Sekta ya uchukuzi tunafahamu, tuna vyuo, tuna bandari, sekta tofauti tofauti lakini upungufu huu unasababisha kuzorotesha kazi zetu ndani ya sekta yetu ya uchukuzi. Tunaiomba sana Serikali iweze kupunguza upungufu huo wa watumishi ili tupate watumishi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)