Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Charles John Mwijage (131 total)

MHE. DKT. CHRISTINA G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Licha ya hivyo, nina maswali mawili madogo.
Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kuona umeanzishwa Mfuko wa Dhamana wa kuwasaidia akina mama hawa kupata mikopo. Kwa upande mwingine kuna mabenki mengine pamoja na taasisi ambazo bado wanatoa mikopo, lakini yenye riba kubwa.
Je, kwa upande wa Serikali kuna mikakati gani ya kushauri hizi taasisi na mabenki kutoa riba ndogo?
Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa upande wa masoko ya uhakika, kwa upande wa Morogoro, kulikuwepo kiwanda cha matunda kinachotengeneza juice, lakini mpaka sasa hivi hakifanyi kazi. Je, kuna mkakati gani wa Serikali kushauri hiki kiwanda kiweze kufanya kazi au kuwezesha wawezeshaji waweze kujenga kiwanda Mkoani Morogoro kuwasaidia wanawake wanaolima matunda na wananchi wa Mkoa wa Morogoro kupata soko la uhakika pamoja na wajasiriamali? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Christina Ishengoma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kuhusu riba za mabenki na taasisi za fedha, kimsingi siyo rafiki kwa mtu yeyote kuweza kukopa na ukafanya biashara kwa tija. Serikali inapitia upya suala la riba na Mheshimiwa Waziri wa Fedha ikifika wakati, atakuja kutupa mwongozo.
Mheshimiwa Spika, suala la pili; Morogoro kuna mjasiriamali mmoja au mwekezaji alijasiria na kuanzisha kiwanda cha kutengeneza concentrate. Anakusanya matunda, anayakamua, anatengeneza concentrate na anaweza kuuza nchini na nje kwa wale watengeneza juice. Kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, huyo mjasiriamali au mwekezaji, aliaga dunia.
Mheshimiwa Spika, juzi nilipokwenda Morogoro nimemwagiza Mkuu wa Mkoa akae na wanafamilia kusudi wajadiliane namna gani tunaweza kupata mtu wa kuwasaidia watu wao waweze kuendeleza hicho kiwanda cha concentrate.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge, juice nyingi tunazokunywa hapa zenye picha za matunda ya nchi hii hazizalishwi hapa! Kwa hiyo, tunawatia shime wanafamilia wakubaliane na mapendekezo ya Serikali. Hiyo iko kwenye score card yangu; nitakwenda kushirikiana nao kusudi kile kiwanda kifanye kazi.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri. Pamoja na hayo, Serikali imekiri kwamba ni kweli jambo hili limechukua muda mrefu. Zaidi ya miaka 18 watu hawa wanaishi katika mazingira magumu; na baadhi ya wananchi pale sasa vibanda vyao walivyojenga kwa sababu hawaruhusiwi kuongeza, familia zao wamekwenda kuwekeza kwa ndugu zao; wanaishi tofauti na familia zao.
Mheshimiwa Spika, swali; Serikali itakuwa tayari kuwaonea huruma watu hawa na kuwalipa fidia haraka ili waweze kuishi jirani na familia zao?
Mheshimiwa Spika, la pili. Kwa kuwa wananchi hawa wamejichagua na wawakilishi wao watatu, leo wanakuja hapa, yuko tayari sasa kukutana na mimi, Waziri na Waziri Mkuu na Waziri wa Ardhi, ili tukae pamoja tuwape majibu hawa wawakilishi wa wananchi ambao wanakuja? Nakushukuru?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nimekiri kwamba ndiyo, suala limechukua muda mrefu. Ukweli ni kwamba Soko la Makambako lilionekana kwamba ni soko la Mji wa Makambako, kimsingi ni Soko la Kimataifa. Kwa hiyo, pesa zinazotakiwa ku-compensate Halmashauri ya Makambako isingeweza kuzilipa na ikaendelea vizuri na shughuli zake. Zinahitajika Shilingi bilioni 3,400 kuweza kulipa fidia watu 272.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndiyo maana nikafanya maamuzi, nikalichukua hilo kulileta katika Wizara yangu. Nimeiomba Hazina inipe pesa hizo niweke kwenye bajeti. Ningewaachia ninyi Makambako, msingelimudu. hili ni Soko la Kimataifa, ni Soko la Tanzania. Mtakachofaidi nyie ni ushuru na kodi kutokana na soko lile. Kwa hiyo, hili ni suala la haraka na nilizungumze na lenyewe liko kwenye score card yangu.
Mheshimiwa Spika, kuhusu Wawakilishi watatu, Mheshimiwa Sanga, hili suala nalimudu, usiende kwa mkuu wangu wa kazi! Mheshimiwa Waziri Mkuu hahusiki, uliache nilishughulikie mimi. Una uzoefu wa kufanya kazi nami. Usisahau ule wimbo wa “Nyumba ya upanga!” Kwa hiyo, naweza kulimudu, uwalete kwangu na nitawahakikishia; ni watu 272 wanadai Shilingi bilioni 3,400 na nimeshaomba kwa Hazina kusudi pesa zilipwe.
MHE. KABWE Z. R. ZITTO: Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2014 zao la korosho lilivunja rekodi ya uzalishaji mpaka tani laki mbili kwa mwaka, lakini zao la pamba lilishuka uzalishaji wake kwa takribani asilimia 40, na bado nchi yetu inauza korosho nje kama korosho ghafi, ilihali kulikuwa na viwanda vingi ambavyo vilijengwa na Baba wa Taifa takribani viwanda 12, na baadhi ya viwanda sasa hivi vimegeuka kuwa ni ma-godown kwa ajili ya stakabadhi ghalani.
Serikali inachukua hatua gani ya kuhakikisha kwamba korosho zote ambazo zinazalishwa nchini zinabanguliwa kwanza hapahapa nchini kabla ya kupelekwa nje na kutungeneza ajira nje? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba nitoe jibu kwa Mheshimiwa Zitto, Mbunge wa Kigoma Mjini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu viwanda vya korosho vilivyobinafsishwa na kugeuzwa maghala, Treasury Registrar ametoa malekezo na wito wote wajisalimishe kwao waeleze kwa nini wamekiuka misingi ya mauziano. Misingi ya mauziano ilikuwa ni kwamba walipe pesa kidogo kusudi viwanda vile waendelee kuvitumia kwa kubangua korosho na kutoa ajira. Kwa hiyo, tangazo limetolewa na muda wake umeishakwisha kwa hiyo asiyeenda anakiuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ubanguaji wa korosho. Ubanguaji wa korosho ndiyo msimamo wetu na wiki iliyopita niliongea na Balozi wa India anasema wao hawana matatizo. India wamefungua dirisha kwa mazao ya Tanzania yapatayo 480 anasema hana tatizo, na taarifa yako Mheshimiwa Zito na watu wa Kanda ya Korosho, kuna kampuni imeishaanza mchakato wa kujenga viwanda vipya katika ukanda wa korosho na wanasema korosho yote iliyopo haitoshelezi viwanda vyao wakianza kazi, na wameniomba niwape hata kibali cha kuagiza korosho nyingine kutoka nje ya nchi nimesema hapana, wasaidieni wananchi wetu kulima zaidi ili mbangue na muuze huko duniani.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba awe specific kama Serikali ina mkakati wowote kuhakikisha inaijengea SIDO uwezo ili iweze kutoa mafunzo ya biashara pamoja na masoko kwa wafanyabiashara wadogo wadogo ama wajasiriamali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa kuwa wajasiriamali wadogo wadogo waliokuwa wengi, mitaji kwao ni tatizo na kwa kuwa nchi za wenzetu huko nje zina kawaida ya kutoa kipindi fulani kwa wajasiriamali wadogo wadogo ili kuwasamehe kodi waweze kuwa na nguvu ya kimtaji na waendelee zoezi la kulipa kodi. Napenda kujua kama Serikali yetu ya Tanzania ina mkakati wowote wa kutoa grace period kwa hao wajasiriamali wadogo wadogo. Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, SIDO pamoja na kutoa mafunzo kwa wajasiriamali, inao Mfuko Maalum unaohusisha kutoa pesa. Hata hivyo, SIDO kwa kushirikiana na TBS wanakwenda mbali kwa kuwaongoza wajasiriamali namna ya kutengeneza bidhaa zao ziweze kufaa kwenda sokoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ndiyo swali ambalo Waziri wa Fedha ametujibu hivi punde. Si kivutio, si uwezeshaji, ni msamaha wa kodi tu. Mazingira bora ya biashara ni kivutio kikubwa kuliko ile kumpa pesa. Kwa hiyo, Serikali itahakikisha mazingira bora ya biashara yanapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanzisha incubators na Serikali ya India inakuja kutusaidia kuwawezesha wajasiriamali wadogo waweze kumudu shughuli, waweze kufanya packaging, waweze kwenda kwenye masoko na tutaanzisha mitaa huko vijijini, small industries street kusudi muweze kufanya kazi kule badala ya kudondosha pesa au kuwapa msamaha ya kodi. Misamaha ya kodi mwenye pesa ameshasema kwamba haitakuwepo ila tutaboresha mazingira.
MHE. MASOUD ABDALLA SALIM: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru nina maswali mawili ya nyongeza kwa Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko mengi ya muda mrefu kwa wafanyakazi viwandani kupewa mishahara midogo lakini zaidi maneno ya kuudhi kwa wamiliki wa viwanda jambo ambalo halikubaliki.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuunda Tume Teule ya kufuatilia malalamiko ya wafanyakazi hawa?
Swali la pili, katika jibu la Mheshimiwa Waziri amesema kwamba wale wote watakaobainika kukiuka makubaliano yaliyomo katika mikataba ya awali hatua stahiki zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kuvitwaa na kutafuta wawekezaji mahiri wa kuviendeleza hivyo viwanda.
Kwa kuwa viwanda vya korosho vilivyobinafsishwa miaka 1970 na 1980 ambapo Serikali ilikopa kutoka Italia na Japan dola milioni 20 na viwanda hivyo hadi leo haviendelezwi wamiliki wake wanajulikana. Sasa tatizo nini kwa Serikali mnaelewa kila kitu tumekuwa tukisema muda mrefu.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Je, nini mkakati wa ziada wa kuhakikisha kwamba viwanda vya korosho vimebinafsishwa kule Mtwara na Serikali mkatoa kwa vigogo wengine mnaowajua kwa bei chee! Je, viwanda hivyo ni lini vitarudi kwa wananchi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika viwanda kuna malalamiko na kama mnavyojua tunao ndugu zetu wanafanya kazi viwandani, sioni haja ya kuunda Tume, Wizara yetu ikishirikiana na Wizara ya Ajira tumeanza kazi ya kufuatilia masuala haya na Kamishna wa Kazi yuko ana kazi maalum ambapo tutahakikisha kwamba wafanyakazi wetu wanatendewa haki.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaeleze wawekezaji, sisi tunatengeneza viwanda kutengeneza ajira, kuzalisha bidhaa na kuwafanya mlipe kodi hatutengenezi viwanda kusudi waje kuteseka watu katika nchi yao, huo ndiyo msimamo wa Serikali na tunawahakikishia tushirikiane Waheshimiwa Wabunge, ninyi ndiyo macho yetu mtushauri na mtuelekeze. Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kutoa viwanda, viwanda vile viliuzwa kisheria, nimeshasema mara tatu bei waliyolipa ni pamoja na masharti ya kuzalisha bidhaa kwa tija, kutoa ajira na kulipa kodi.
Kwa hiyo, kama ulimuuzia kisheria utamnyang’anya kisheria na niwahakikishie watu wanaotoka kwenye ukanda wa kulima korosho hakuna tatizo viwanda vitafanya kazi. Pamoja na hivyo wako wawekezaji wako tayari kuwekeza kwenye kutengeneza korosho, yaani korosho inatoka pale kiwandani inaingia mikononi mwa mteja tuna-add value, na tutatoka hapa tunakwenda kuuza Ulaya siyo tunatoka hapa tunauza India, India ipeleke Ulaya. Tunakwenda moja kwa moja sokoni na kazi hiyo naiweza tushirikiane. (Makofi)
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru sana kwa kunipa fursa na kwa sababu ni mara yangu ya kwanza nazungumza tangu nichaguliwe tena kuwa Mbunge wa Arumeru Mashariki na mimi niwashukuru Wanameru.
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Naibu Spika, unapoongelea suala la ukuaji wa viwanda huwezi ukaacha kuongelea habari ya viwanda ambayo vilikuwemo lakini leo hii havifanyi kazi. General Tyre Arusha kilikuwa ni kiwanda pekee cha kuzalisha matairi Afrika Mashariki. Mwaka juzi ndani ya Bunge hili nimejibiwa na Mama Nagu hapa kwamba in less than a year kiwanda kingerudi kifanye kazi, mwaka jana nimejibiwa ndani ya Bunge hili na Mheshimiwa Janeth Mbene kwamba kufikia mwezi wa 11 mwaka jana kiwanda cha General Tyre kingerudi kufanya kazi.
Sasa na mimi niiulize Serikali ya hapa kazi tu, kwamba ni lini kiwanda cha General Tyre kitarudi kufanya kazi kwa sababu tumechoshwa na ahadi za muda mrefu ndani ya Bunge hili na wananchi wa Mkoa wa Arusha ambao walikuwa wanapata ajira ndani ya viwanda vile leo wako nyumbani na matairi tunanunua Korea, India na Japan, lini General Tyre litaanza kufanya kazi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, General Tyre kinachoendelea General Tyre ni nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, General Tyre imeshatwaliwa aliyekuwa mbia mwenzetu mwenye asilimia 26 tumemlipa chake kiwanda ni chetu, kinachoendelea ni kurekebisha mitambo yote ya umeme. Lakini mitambo iliyokuwepo kwa ushindani wa sasa ni absolute zimepitwa na wakati. Tulikuwa tunatengeneza tyres zenye tube, sasa hivi soko linakula tubeless kwa hiyo, tunapaswa kuleta mitambo mingine. Lakini tunatafakari tuende vipi tutafute mbia mwingine au tutafute mtu wa kumwajiri afanye kazi. Kwa hiyo, sasa hivi kinachofanyika ikitoka Government Notice NDC itakwenda kupewa pesa bilioni 60 na itafanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Catherine Magige amelifuatilia suala hili tumelizungumza sana, siyo suala la dakika moja naomba Mheshimiwa Mbunge uje au umuone Mheshimiwa Catherine Magige akueleze shule niliyompa masaa matatu kuhusu General Tyre. General Tyre is coming na iko kwenye score board yangu, nitapimwa kwa General Tyre. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi/Kicheko)
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua nafasi hii kumshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo ameyatoa juu ya Mkoa wa Lindi, lakini naomba pia nitumie nafasi hii kuuliza swali moja la nyongeza. Kama ambavyo yeye amekiri, Mkoa wa Lindi kwa ujumla ulikuwa na viwanda vingi ambavyo sasa hivi vyote vimebinafsishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Nachingwea viko viwanda viwili, Kiwanda cha Korosho pamoja na Kiwanda cha Kukamua Mafuta lakini Lindi pia imekuwa na rasilimali ya bahari ambayo tukiitengenezea mazingira bado tunaweza tukatengeneza viwanda vidogo kwa ajili ya usindikaji wa samaki. Pamoja na majibu hayo aliyoyatoa je Mheshimiwa Waziri anatuahidi nini katika mpango huu ambao tunaelekea na tukiangalia Mkoa wa Lindi haujaguswa kwa namna yoyote ile? Asante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali la nyongeza. Kwa ruhusa yako naomba Mheshimiwa Mbunge tusiwahishe shughuli, bajeti yangu inakuja na mambo mazuri kwa ajili ya Mkoa wa Lindi ikiwemo uanzishaji wa kilimo cha muhogo ambako tutakuwa tuki-export nje tani milioni mbili za mhogo nchini China zenye thamani ya dola milioni 300.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa majibu ya namna hiyo kuhusu viwanda vya Moshi yamekuwa yakitolewa mara kwa mara katika Bunge lako Tukufu bila utekelezaji; na kwa kuwa ilikuwa ni moja wapo ya ahadi ya Mheshimiwa Rais kwamba kwa muda mfupi sana viwanda vile vingetwaliwa kwa waliovitumia bila utaratibu.
Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kutoa muda halisi kwa maana ya time frame ya lini viwanda hivyo vitatwaliwa kwa watu ambao wameshindwa kuvifanyia kazi katika malengo halisi yaliyokuwa yametarajiwa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa kuwa majibu ya Serikali hayaakisi ukweli ulivyo kuhusu wafanyakazi, kwa sababu madai yao ni ya msingi na fedha wanazodai siyo za mikataba ya hiari na wamekuwa wakidai fedha hizo tangu mwaka 1998, na kwa kuwa Serikali haijataka kuwa karibu nao…
NAIBU SPIKA: Naomba uulize swali tafadhali!
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Je, ni lini sasa Serikali itakuwa tayari kuanza kufuatilia ukweli wa madai hayo na kuwa karibu na hao wafanyakazi ili waweze kutoa ufafanuzi unaoridhisha wafanyakazi hao kuondoa manung’uniko yao? Ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na (b) suala la maslahi ya wafanyakazi ni lako wewe, ni langu mimi. Wewe kama Mwakilishi wao na mimi kama Kiongozi wa Serikali, mimi na wewe tuwasiliane tutakwenda wote mpaka Moshi tuwaone hao watu tuzungumze nao tutakwenda kwa Msajili wa Hazina, tutaweza kujua mbichi na mbivu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali (a) Mheshimiwa Rais amezungumza bayana, na mimi nimekuwa nikizungumza mara nyingi kuhusu viwanda ambavyo havifanyi kazi. Jambo moja ambalo tunapaswa kulielewa kuna suala la kisheria kuhusu hivi viwanda vilivyobinafsishwa, kwa hiyo, tunajitahidi kufuata hizo sheria kusudi tuvitwae kisheria kusiwepo migongano. Nia yetu nikuona hivyo viwanda vinafanya kazi haraka sana, hatutaki kwenda mahakamani. Kwa hiyo, viwanda hivyo vitatwaliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada za kuvitwaa tunawafuata wale watu ni Watanzania wenzetu tunawauliza kitu gani kilichowasibu? Sababu nyingine zina mantiki na kuna baadhi ya viwanda vimeshaleta proposal namna gani vitaweza kufufuliwa. Tumewapa wataalam watu, wataalam wa Wizara yangu wawasaidie hao waliovichukua, hasa wale Watanzania wazawa tuweze kuona wanatoa bidhaa tulizotegemea.
Moja ya sababu ni kwamba soko tulilokuwemo lilikuwa linaleta bidhaa ambazo lilikuwa linafanya viwanda vyetu nchini visiwe competitive hilo suala ni historia Mheshimiwa Rais na Waziri wa Fedha wamelisulihisha bidhaa zinaingia kwa kulipa kodi na bidhaa standard. Kwa hiyo, viwanda vya Watanzania waliopewa vitafanyakazi na hiyo ni kazi yangu tulishughulikie mnisaidie Waheshimiwa Wabunge.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana pia kuniruhusu na mimi niulize swali la pili la nyongeza.
Mheshimiwa Waziri wa viwanda na Biashara amejibu majibu mazuri sana, kwa ujumla lakini ningependa na mimi kujua kwamba suala la viwanda vilivyobinafsishwa limekikumba kiwanda chetu cha Nyuzi cha Tabora. Ningependa Mheshimiwa Waziri aniambie ana mkakati gani hasa wa Kiwanda cha Nyuzi Tabora ambacho kilikuwa kinasaidia wakulima wote wa Pamba katika Kanda ya Ziwa Magharibi? Ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha Nyuzi Tabora mmiliki wa Kiwanda hicho ameshaitika wito kwa Msajili wa Hazina, madai yake yeye anasema nyuzi zake hazina soko.
Kwa hiyo, tunashirikiana naye ili tuweze kupata soko la nyuzi zake lakini tuweze kuona kiwanda kile kinafanya kazi. Nyuzi zake zilikuwa zinakosa soko, mtu anakuambia kiwanda hiki nyuzi hazina soko na hayo niliyowaeleza bidhaa kutoka nje ndiyo mojawapo ya mambo yaliyokuwa yanatuumiza. Kwa hiyo, tuko nae bega kwa bega, wataalam wanafanyia kazi, na nitakuja kuleta mrejesho kwa watu wa Tabora ili kusudi kiwanda chenu kiweze kufanya kazi vizuri.
MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa swali la Mheshimiwa Raphael Japhary linafanana na hali ilivyo Moshi Vijijini, kuna kiwanda kilifunguliwa mwaka 1975 na Mwalimu Nyerere na kiwanda kile ni cha ngozi hakikupata mwekezaji mpaka leo, na kimepangishwa kwa shilingi 20,000 kwa mwezi. Naomba Waziri aniambie ni lini atakuwa tayari kwenda kuona hiyo hali nakuchukua hiyo hatua zinazoyostahiki?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Antony Komu, Waziri Kivuli wa Viwanda Biashara na Uwekezaji kuhusu kiwanda chake cha mwaka 1975 Moshi ambacho hakukitaja jina. Kwa kweli nitakudanganya nikisema ninakijua kwa sababu hukukitaja jina, niko tayari wewe unipeleke unionyeshe kiwanda tukitafutie majawabu.
MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa Mwanza tuna Kiwanda cha Tanneries ambacho sasa kimegeuzwa kuwa chuo.
Je, Serikali ina mpango gani wa kukirudisha hicho kiwanda ili kiweze kufanya kazi iliyokusudiwa?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Mwanza kuhusu kiwanda cha Mwanza TANNERIES, ambacho kimegeuzwa kuwa chuo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Katibu Mkuu anayeshughulikia Biashara na Uwekezaji Profesa Mkenda, alikuwa Mwanza wiki iliyopita, kile kiwanda kitaendelea kuwa Chuo na tunalenga kuwafundisha wananchi namna ya kutengeneza nguo, ni Technical School ni VETA ambayo itasaidia watu wa nguo, lakini kando na eneo hilo, kuna Kiwanda cha Ngozi, hicho ndicho tatizo mtu aliyepewa amekigeuza hifadhi ya makatapila na matrekta tunataka kifanyekazi. Kwa hiyo, chuo kitaendelea kufanyakazi tunawafundisha vijana, wanakwenda kwenye viwanda vyao vidogo vidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo ni huyo mtu ambaye kiwanda cha Ngozi cha Mwanza amekigeuza hifadhi na kuja Mwanza tarehe 30 na nitakwenda kushughulikia, tarehe 30 mwezi huu.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza napenda kuishukuru Serikali kwa kutambua uwezo wa wajasiriamali wa Mkoa wa Katavi ambao bado wana viwanda vidogovidogo, lakini kwa kuwa, Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi inalenga uchumi wa kati, je, Serikali inasema nini kuwekeza sasa katika viwanda vikubwa kutokana na malighafi zinazopatikana Mkoa wa Katavi ili tuweze kufikia malengo ya uchumi wa kati?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili; kwa kuwa, Mkoa wa Katavi una wanyama wengi wafugwao hususan ng‟ombe. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwekeza kiwanda cha kusindika mazao ya ng‟ombe, hasa katika Jimbo la Kavuu?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu haja ya kujenga Kiwanda cha Nyama Katavi na Sumbawanga kule, Mheshimiwa Mbunge Wataalam wa Wizara yangu leo wako hapa full team, unione na uwasiliane na Mheshimiwa Zungu kuna Mwekezaji anatafuta mahali pa kujenga viwanda vikubwa vya nyama, nikupe offer leo hii tuonane, huyo mwekezaji aende Katavi na Sumbawanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Serikali kujenga viwanda vikubwa. Mheshimiwa Pudenciana Kikwembe, ananishawishi kusoma hotuba yangu kabla ya wakati! Mkakati wetu ni kuhakikisha viwanda vidogo sana tunavipa nguvu viwe viwanda vidogo na viwanda vidogo viwe viwanda vya kati na viwanda vya kati viende viwe vikubwa, tunafanya business graduation. Kwa hiyo, tutawapeleka taratibu hasa wazawa, kusudi twende sambamba tufike kwenye viwanda vikubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la msingi kama kuna malighafi ambayo inatupa faida ya kiulinganisho niko tayari wakati wowote tusaidiane Wabunge na Serikali ya Katavi, mniambie nini kinawapa faida ya kiulinganisho ili kusudi nilete wawekezaji. Wawekezaji wote watakuwa hapa mpaka Jumatatu, kila mtu ajichukulie wa kwake pale nje.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niulize swali fupi. Kwa kuwa, suala la Katavi linafanana sana na la Mkoa wa Kigoma ambao hatuna kiwanda hata kimoja na rasilimali ziko za kutosha, hususan katika Jimbo la Buyungu ambako kuna rasilimali kama mihogo, mpunga na kadhalika. Je, Waziri yuko tayari kuja kujenga viwanda katika Wilaya ya Kakonko? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haijengi viwanda! Serikali inahamasisha Wawekezaji wa ndani na nje ya nchi waje kujenga viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwape habari nzuri Kigoma; kuna kampuni inaitwa Kigoma Sugar, tumewapa hekta 47,000 watajenga Kiwanda cha Sukari kinachozalisha tani 120,000 watakapoanza kazi, nimewaambia ifikapo Septemba matrekta yote yaende kulima kwetu Kigoma ili kusudi tuzalishe sukari. Mambo mazuri yanakuja Kigoma.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa, Wilaya ya Lushoto inafahamika kwamba ni ya kilimo cha matunda na mbogamboga. Je, ni lini Serikali itajenga kiwanda cha matunda na mbogamboga katika Wilaya ya Lushoto, ili mazao yale yasiendelee kuharibika?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wananilazimisha kufungua bajeti yangu kabla ya muda, lakini anayelipa mahari anayo ruhusa ya kumwangalia mwari hata kabla ya siku ya harusi!
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kiwanda kinaitwa Sayona kitawekwa Mkoa wa Pwani, kitakuwa na uwezo wa kusindika tani 25,000 kwa mwaka. Kitachukua matunda yote ya ukanda wa Pwani mpaka ukanda wa Ziwa. Kuna kiwanda kinaitwa Osasuna kitajengwa Handeni kwa Msisi, kitaanza kuchakata Nanasi, kitakuwa na uwezo wa kulima nanasi kwa shamba la mwekezaji hekta 3,000 lakini out growers watapewa hekta 17,000 kumzunguka na yule mwekezaji atawajibika kuwasaidia wananchi wazawa namna ya kulima kisasa. Mwaka 2018 Novemba, tunaanza kutoa juice ya kwanza.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pia namshukuru Mheshimiwa Waziri lakini sijaridhika na majibu yake. Niliuliza ni lini masoko haya yatafufuliwa kwa sababu haya masoko ni muhimu kwa ajili ya wananchi wa Kyerwa na Waziri mwenyewe anajua wananchi wa Kyerwa wanapata shida hawana mahali pa kupeleka mazao yao. Naomba anieleze ni lini masoko haya yatafufuliwa yaanze kujengwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, naomba Naibu Waziri awaeleze wananchi wa Jimbo la Kyerwa na Watanzania ambao wananufaika na masoko haya, je, Serikali imetenga pesa kwenye Bajeti ya mwaka huu wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya masoko haya kukamilika?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Innocent Bilakwate ameuliza nijibu ni lini? Nimemweleza, DASIP I ilikoma, nimewasiliana na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwamba Mpango wa DASIP II haujaanza, utakapoanza tuwaweke watu wa Karagwe na Kyerwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nina maslahi na sehemu hizi, napenda niseme ukweli, msema ukweli ni mpenzi wa Mungu. Katika bajeti sijaweka lolote kwa ajili ya masoko haya ya Nkwenda na Murongo, lakini kwa ajili ya Nkwenda na Murongo tumeandaa utaratibu ambapo wakulima wa mazao wa Karagwe, hasa maharage tutawaunganisha moja kwa moja na wanunuzi wa Oman na Innocent Bashungwa nimemteua aratibu shughuli hiyo.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, Kumbukumbu za Bunge (Hansard) zinaonesha kwamba swali hili liliwahi kuulizwa mara nyingi na Wizara imekuwa ikitoa maelezo tofauti tofauti ikiwapo na kusema kwamba machungwa ya Muheza siyo mazuri wakati machungwa ya Muheza sasa hivi ni mazuri, tunatumia mbegu ya Valencia, Washington na Msasa na kwamba machungwa hayo yanapelekwa Kenya na kutengeneza juice ya Del Monte. Swali langu la kwanza, Mheshimiwa Waziri atanithibitishiaje kwamba hii Kampuni ya SASUMUA HOLDING ni kweli inataka kujenga hicho kiwanda Mkoa wa Tanga? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ninao wawekezaji ambao wanataka kufanya Muheza iwe kituo cha matunda. Mheshimiwa Waziri atanithibitishia kwamba wawekezaji hao hawatapata usumbufu nitakapowaleta kwake? Nashukuru.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, unapoulizwa swali na Mheshimiwa Mbunge ambaye amewahi kuwa Kamanda halafu ni Balozi inakuwa shida kumjibu. Nimezungumza na watu wa TAHA (Tanzania Horticultural Association) kupita Mkurugenzi Mkuu wao Jacqueline na nimezungumza na SASUMUA HOLDING, vifaa vyao kama earth equipment vimeshafika Kwamsisi, nimeviona na wamenihakikishia. Jambo la kukupa amani ya moyo Mheshimiwa Adadi ni kwamba mimi na wewe pamoja na Waziri, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba na Mheshimiwa Mboni, Mbunge wa Handeni tutapanga twende pale tuone shughuli zinazofanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tuna shughuli ya msingi kwamba yule mtu anataka outgrowers hekta 3,000 na yeye mwenyewe hekta 17,000 na anasema atawapa service. Kwa hiyo, ni jukumu lako Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote wa Tanga mkiongozwa na Mheshimiwa Mboni, mimi na Waziri mwenzangu pacha twende pale tuone Kashenamboni, tuamini au tusiamini mimi na wewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ninalolipenda kuliko yote ni hili swali lako la pili kwamba niko tayari. Leo nina shughuli tena shughuli pevu, nakuomba kesho uniache nipumzike Jumatano walete wawekezaji wako, hakikisha Tanga hakuna vikwazo, mimi saini yangu natembea nayo.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuulize Waziri, amesema kuna wawekezaji ambao wanakusudia kuwekeza pale Kwamsisi, natoa pongezi kwa sababu kiwanda kile kinakuja katika Mkoa wetu wa Tanga. Kwa kuwa ndiyo wanatarajia kuanza kulima hayo mazao ambayo yatalisha kiwanda hicho, je, haoni ni wakati muafaka kwa matunda yaliyopo sasa na hasa ikizingatiwa kwamba Serikali imeshasema itafufua kwanza viwanda vilivyokuwepo hasa kiwanda kilichokuwepo pale Korogwe, ni kiwanda kidogo lakini kinaweza kutengeneza juice kikafufuliwa hicho kwanza wakati tunasubiri kiwanda kikubwa?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, waambie wanipige taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mary Chatanda ameuliza maswali mawili katika moja. Ubora wa matunda au matunda tuliyonayo na hii kampuni ya Kwamsisi ambayo itachukua miezi 18 mpaka ianze kutengeneza juice, jibu lake ni hivi, kuna kampuni nyingine inaitwa Sayona inajenga kiwanda sehemu ya Tanga karibu na Chalinze, itachakata tani 25,000 za matunda yoyote, hii itakuwa inakidhi haja wakati sisi tunasubiri hiki kiwanda cha SASUMUA. Kwa nini SASUMUA hawezi kuanza, yeye analenga kuanza na mananasi na wanasema wataalam kwamba nanasi litakapopandwa linahitaji miezi 18 kuweza kukomaa. Kwa hiyo, yeye ana masharti yake na utaalamu wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili la Korogwe kwamba kiwanda kipo na bahati nzuri ameuliza swali siku nzuri, namuagiza Mkurugenzi Mkuu wa SIDO aende Korogwe na mtaalam wa TIRDO watathmini ni kitu gani kinahusika halafu Halmashauri yake ambaye yeye ni Diwani tuje tuangalie ni namna gani ninyi mnaweza kuhamasisha Wanatanga ili muweze kukiendesha, viwanda vingine siyo vya Serikali. Ni nini tatizo, hiyo ni kazi yangu nitabaini, spare atanunua wapi wataalam wangu watamwambia, ni viwanda vya shilingi milioni 60 au 80, halmashauri mnavimudu.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuulize Waziri swali dogo. Ni lini Serikali itaacha kuagiza toothstick maana tuna miti mingi ya kutosha kule Mbeya na sehemu nyingine. Ni lini Serikali itaacha kuagiza toothstick? Ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, katika mambo yanayoninyima raha ni kama kuona watu wanaagiza toothpick. Mimi nimeleta bajeti yangu hapa lakini haina maana hata ningeisoma kwa mbwembwe namna gani kama ninyi msipoikubali. Ninyi Wabunge mniambie kwamba toothpick zisipite Dar es Salaam muone kama zitaingia.
Mheshimiwa Naibu Spika, mtambo wa kutengeza toothpick ni dola 28,000, ni jukumu lako Watanzania kuwekeza. Kuna Mtanzania mmoja, nawaomba asiyetaka kuwekeza kwenye viwanda na nimelisema mara tatu, kuna Wabunge, kuna watu wanakuja kila siku wanataka kuwekeza, Mtanzania anayeagiza toothpick anaagiza container 100 ni mtu wa Makete. Mtambo wa kutengeneza toothpick ni dola 28,000. Kuna Mbunge Mheshimiwa Lema anafuatilia kuleta mtambo wa toothpick kupeleka Kilimanjaro. Watu wanahangaika, msikosoe, msilalamike twende tufanye kazi. Toothpick inatumia mabaki ya miti haitumii ubao, the reject, the unwanted material ndiyo inatumika. Tuchangamke, twende wote kwenye behewa la viwanda msibaki nyuma. Viwanda ni vita Bwana Msigwa twende kwenye viwanda. Toothpick mkiamua zisiagizwe hazitaingia, TBS ni yangu nitazizuia lakini na ninyi muwekeze watu wanapenda toothpick.
MHE. SAVELINA S. MWIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana.
Kwa kuwa, viwanda vilivyopo Mkoa wa Kagera hasa ukiangalia Kiwanda cha TANICA kimejengwa mwaka 1967, kiwanda cha BUCOP 1967 na Kagera Sugar 1990. Viwanda vyote vimekuwa chakavu na viwanda vyote havifanyi kazi vizuri, tukitegemea Serikali au kutegemea wawekezaji ili waweze kuvitengeneza au kuviboresha tutakuwa tunaenda sehemu ambayo siyo nzuri.
Je, ni lini Serikali itaviboresha angalau vikawa viwanda vya kati?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Mkoa wa Kagera tuna wazalishaji wengi wa matunda na wazalishaji wengi wa maziwa, Mkoa wa Kagera hatuna hata SIDO angalau ya kuweza kujumuisha Mkoa mzima, je, ni lini Serikali itaweka viwanda vya kuzalisha matunda na kuweka viwanda vya SIDO ili vijana wapate ajira?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uboreshaji wa viwanda vilivyopo na mfano wake aliotolea ni Kagera Sugar, mmiliki wa Kagera Sugaranawekeza kisasa kutoka tani 60,000 za sukari anazozalisha akilenga tani 120,000. Nimefanikiwa kuongea na Waziri wa Uwekezaji wa Oman ambako kutoka tani 120,000 Kagera Sugar atazalisha tani 180,000 ili kusudi Kagera Sugar izalishe tani 300,000 tutosheleze soko la ndani na kupeleka Oman.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maziwa na matunda, Kagera ni eneo lenye fursa nzuri ya kuwekeza kwenye maziwa. Mkakati tulionao nawasiliana na wajasiriamali wenye Kampuni ya GESAPU Agro Farming ambao watawekeza pesa karibu bilioni 14, watatengeneza mtandao wa kukusanya maziwa kuanzia Chato kwenda Geita mpaka Kagera na wataweka kiwanda Misenyi na mimi niko tayari kupambana nao ili wafanikiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu SIDO Mheshimiwa Mwijage nitahakikisha SIDO inaanzia Kagera na inasambaa nchi nzima kwa nguvu zaidi.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mwanza hapo awali kulikuwa na zaidi vinu 15 vya kuchambulia pamba, kikiwepo na cha Nyambiti Ginnery, Ngasamo. Mheshimiwa Waziri kwa sababu nilishaongea na Mheshimiwa Waziri Marehemu Abdallah Kigoda, pia niliongea na Waziri aliyekuwepo wakati huo Mheshimiwa Mama Nagu; ni lini sasa angalau Nyambiti Ginnery iweze kutengeneza pamba nyuzi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndassa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pamba limekuwa na hoja kubwa kwenye bajeti yangu, majibu niliyotoa ni kwamba tarehe 02 Mei, nilizindua mkakati namna ya kuboresha pamba kusudi iendane na ujenzi wa uchumi wa viwanda. Ijumaa mikoa yote inayolima pamba, tunakutana Mwanza na mimi nitakuwepo niwapitishe kwenye mkakati na nitahakikisha kwamba Kiwanda cha Nyambiti kiweze kuingizwa katika mchakato wa kuchambua pamba na kutengeneza kiwanda ikiwezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo siku ya Ijumaa shughuli nzima inafanyika Mwanza mimi nitakuwepo pale, tuchambue suala la pamba ili ule mkakati wangu wa nguo uweze kutekekezwa.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika jibu lake la msingi Mheshimiwa Waziri amesema kwamba amewashauri walionunua viwanda ambao wameshindwa kuviendeleza chini ya sera ya ubinafsishaji watafute wabia, lakini wote tunakumbuka Serikali hii wakati wa kampeni na hata baada ya kampeni mara kadhaa imetoa matamko kwamba itawapa muda wawekezaji walioshindwa kuviendeleza viwanda wavirudishe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijue Kiwanda cha ZZK Mbeya, Kiwanda cha Chai Katumba na Mbeya Textile, ni lini vitarudishwa kama ambavyo mliahidi kwenye kampeni na baada ya uchaguzi au hizi ndiyo siasa za flip flap?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbilinyi, Chief Lumanyika kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hotuba yangu haya maneno mengine mimi siyo mtu wa rahisi rahisi siwezi kuteka mtu nyara. Kuna mambo mawili, kiwanda ulichopewa natumia lugha viwanda vilivyobinafsishwa havikuuzwa, walipewa. Kwa sababu ile pesa waliolipa ilikuwa na masharti kwamba ukiendeleze kizae bidhaa, uzalishe bidhaa, utoe ajira na ulipe kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la Mheshimiwa Mwijage nimezungumza lazima mtu alipe kodi, sasa habari yenyewe ndiyo hii, tamko la Serikali ni hili. Aliyepewa kiwanda kwa utaratibu huo, ama kiendeshwe ama atapewa mtu mwingine akiendeleze, mambo ya kujadiliana hayo hayapo, na imeandikwa kwenye hotuba yangu. Nimekuwa nikilisema nimeliandika kwenye hotuba yangu nitakuwa kwenye position ya kuwaeleza kabla ya nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha unaoanza kwamba hizi ni mbivu, hizi ni mbichi, lakini lakini viwanda vyote viwe vinafanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaeleze tu kwamba wote waliochukua viwanda wanakuja kwa Msajili wa Hazina na wametoa programu namna ya kutengeneza, programu siyo moja. Hili suala ni la kimakataba, wanamikataba tunahakikisha kwamba tunakwenda kwa mikataba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna viwanda vingine vilishindwa kufanyakazi kwa sababu ya ushindani usio sawa, ndiyo maana tunaweka mazingira wezeshi kwa kuzuia watu waliokuwa wana-dump bidhaa hapa. Ni kama maswali mnayolalamikia kwamba kuna uplifting, uplifting zitaendela ili kuwazuia watu wanao-dump vitu hapa kusudi viwanda vyangu vifanye kazi.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimwia Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri kwanza nimpongeze amekuwa anatoa majibu marefu na mazuri.
Kwa kuwa viwanda vya pamba au vinu vya pamba katika Wilaya ya Busega vingi havifanyi kazi kwa mfano, kule Ngasamo na Nasa; na kwa sababu Waziri amesema kwamba, ana mkakati wa kuvifufua viwanda hivi, Je, kupitia sera hii mpya ya viwanda kwa Serikali ya Awamu ya Tano, viwanda hivi vitakuwa ni sehemu ya mkakati huo?
WAZIRI WAVIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 02 Mei nimezindua mkakati unaitwa C to C (cotton cloth); ukiusoma ule mkakati unaanzia kwa mzalishaji wa pamba, azalishe kwa tija. Pamba ikiwepo ginnery zitafufuka, ginnery zilikufa kwa sababu pamba haikuwepo, kwa hiyo ni mchakato mzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie kama alivyosema hapa Mheshimiwa Ndassa. Ijumaa nitakuwa na wadau wenyewe wa pamba Mwanza ambapo Wakuu wa Mikoa wote watashiriki na Bodi ya Mazao itashiriki, tutayajadili yote hayo. Nipeni information zote zinazotakiwa kwa siku ya leo kesho naanza safari nitakuwa Mwanza yote hayo nitayafanya tu, ningependa viwanda vyote vifanye kazi ikiwemo kile cha Mzee Gulamali cha Manonga.
MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Waziri wa Wiwanda, ninayo maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka ya karibuni viwanda vingi vilibinafsishwa na kuuzwa, vikiwemo viwanda vya mazao ya kilimo na mifugo na kubadilishwa matumizi yake.
Je, Serikali iko tayari kuhakikisha madhumuni ya awali yanatekelezwa kama ilivyoainishwa uko mwanzo?
Swali la pili, kwa vile suala la vipimo vya kienyeji, kama rumbesa na ndoo, maarufu kama Msumbiji limekuwa likilalamikiwa kwa muda mrefu; Je, Serikali haioni kuna haja ya kutoa tamko ni lini hasa wakala wa vipimo na mamlaka za Serikali za Mitaa zitaanzisha hivyo vituo? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, dhana ya kujenga uchumi wa viwanda, inaendana na utaratibu wa kuhakikisha viwanda vyote vile vilivyobinaifishwa vinarudi kufanya kazi. Wale ambao walipewa viwanda hawakuuziwa walipewa, kwa sababu walilipa kishika uchumba tu, hawakulipa fedha kamili ya kununua kiwanda, ni kwamba wanapaswa wavirudishe. Na napenda nitoe taarifa kwa Bunge lako Tukufu kwamba wanaitikia vizuri na wote watakuja kuendesha viwanda kwa misingi ambayo walikusudia. Atakayeshindwa atanyang‟anywa na atapewa Mtanzania mwingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mkapa, alikuwa na dhamira safi ya kuwapa Watanzania ili kusudi watoke, wajijenge kiuchumi lakini dhamira yake watu wakaitumia vibaya ndiyo hayo wakaenda kutumia viwanda ambavyo havikukusudiwa.
Mhesheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, vipimo aina ya rumbesa, Msumbiji, na wengine wanaita badimanyaira. Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, wameshatoa maelekezo na mtakuta hata njiani, mimi napokea simu nyingi, watu wengi wanakamatwa. Uuzaji wa mazao unakuwa na vituo maalum na Maafisa Ugavi na Watendaji wa Kata, ni moja ya jukumu lao kufika maeneo yale na mnunuzi yeyote hakikisha unapima kilo zisizidi 100. Nitafanya jitihada zaidi kuhakikisha kwamba tunawapelekea mizani kadri tutakapopata uwezo wa kuweza kununua mizani hiyo ili kusudi wananchi pamoja na kupima usawa wa gunia lakini wawe na uhakika kwamba ni kilo 100 tu, wasiwanyonye wauzaji.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa Mkoa wa Dodoma una mifugo mingi na kunahitajika kiwanda cha kuchakata mazao ya mifugo; Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kiwanda hicho katika Mkoa wa Dodoma?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Toufiq. Mpango wa Serikali ni kujenga viwanda vya kuchakata nyama, huu ni mkakati pamoja na faida ya zao hili la nyama, tunalenga kutumia njia hii kuwashawishi wafugaji waweze kutoa mifugo yao kwenye sehemu za hifadhi. Kwa hiyo Sekta binafsi inahamasishwa na tuna machinjio hapa, tunategemea kutengeneza Kongwa, Ruvu, na tunaimani kwamba kwa kuwa na Kongwa na machinjio ya Dodoma kiwanda kitaweza kutangamka. Lakini nichukue fursa hii kukuomba Mheshimiwa Mbunge, ukimuona Mwekezaji yeyote mwambie aje awekeze Dodoma, mimi ninazo ekari 200, kama anataka kuwekeza aje tushirikiane nitampa eneo, ajenge sehemu ya kuchakatia, machinjio tunayo ni sehemu ya kuchakatika nyama tu.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii.
Kwa kuwa, ndizi ni kati ya zao ambalo linatumika sana nchini lakini kipimo chake kimekuwa na tatizo na wakulima wa ndizi wanapunjika sana zikiwemo ndizi kama mishale, minyenyele, mlelembo, toke, kitarasa na mtwishe. Mheshimiwa Waziri anatueleza nini kuhusu soko la bidhaa kama hiyo?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ndizi zimenilea, lakini msema kweli ni mpenzi wa Mungu, sijui international standard za kupima ndizi, nitakwenda kuwa task watu wa TBS na watu wa vipimo kusudi tuweze ku-establish kipimo standard cha ndizi. Lakini kitakachoamua bei nzuri kwa mkulima ni soko la ndizi, watu wa (TAHA) Tanzania Horticulture, chini ya ndugu Jacquline wanatafuta soko la ndizi nje ya nchi, na tumeshapata soko ambalo tunahitaji kuuza nje ya nchi tani 50 kwa wiki. Kwa hiyo tunawasiliana na mama Raymond kusudi tuweze kumuunganisha na Jacquline tuone kama Kilimanjaro mnaweza kulima kusudi kupeleka nje ya nchi.
MHE. MUSSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru pia kwa juhudi nzuri za Mheshimiwa Waziri anazozifanya katika kuhakikisha kwamba Mikoa ambayo inalima mazao mbalimbali, inakuwa na uwezekana wa kupata viwanda vya ku-process hayo mazao. Mkoa wetu wa Tabora una zao la tumbaku, na juhudi ambazo anazifanya Mheshimiwa Waziri tunaziona;
Je, Mheshimiwa Waziri anatuelezaje kuhusu uwezekano wa kupata mwekezaji wa kuja kuweka kiwanda katika cha kuchakata kuchakata zao la tumbaku katika Mkoa wetu wa Tabora?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo ninayahangaikia sana ni kuweza kupata viwanda Tabora. Kwa sababu ameniuliza kuhusu tumbaku nitajibu tumbaku lakini siku nyingine nitakueleza na viwanda vingine ambayo viko kwenye pipe line. Tumehangaika, tumewapata Wachina tunawashawishi wakatengeneze kiwanda cha ku-process tumbaku pale, lakini panapo majaliwa ya Mwenyenzi Mungu, huenda mwisho wa mwezi huu au mwezi ujao nikaenda Vietnam, nakwenda mahsusi kutafuta kiwanda cha tumbaku na kukipeleka Tabora, kwa hiyo nahangaika jambo la muhimu watu wa Tabora muiombee Serikali hii ili kusudi tuchape kazi.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Pamoja na majibu mazuri ya Waziri, ninaomba kumuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa kwenye bajeti ya Serikali mwaka huu moja ya vitu vilivyoainishwa mle ni pamoja na kufanya review ya mikataba mingi kwa hawa waliobinafsishiwa viwanda. Sasa ni lini Serikali itafanya review ya kujua uwezo wa huyo mwekezaji kuhusu kuwekeza Tabora Mjini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa kuna tuhuma zinazomuhusu mwekezaji huyo wa kiwanda cha Nyuzi kwamba kuna mashine mbalimbali ambazo aliziuza kama vyuma chakavu, ambazo zilikuwa mle kwenye kiwanda na kwamba kuna mashine nyingine ambazo tayari zilishasafirishwa, hazipo kabisa pale;
Je, ni lini Serikali itafanya ukaguzi ili kujiridhisha kwamba mwekezaji yule kweli hajaziuza mashine hizo au kuzihamisha nje ya nchi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu review, sina sababu ya kukuficha, review ilishaanza kuhusu Tabotex, nimeshakwenda kumuona hata aliyekuwa Meneja, ambaye sasa hivi ni Meneja Mwatex. Aliyekuwa Meneja wa kiwanda hiki sasa yuko Mwatex Mwanza, nimemfuata nikamuhoji. Ngoja nikueleze, kuna mambo mengine anapoteza muda, kuna majibu amenipa anapoteza muda na iko kwa Msajili wa Hazina na atamshughulikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu namba mbili, kwamba kuna mashine zimeuzwa, ile tathmini nzima ndiyo itakuja kuhitimisha kwamba alipotoa mashine hii na kuleta mashine nyingine aliitoa kwa misingi gani. Niwaeleze ukweli ambao nimeushuhudia, mitambo ya viwanda vyetu vya nguo, viwanda vingine vilikuwa na mitambo ya mwaka 1963, kwa hiyo mwekezaji makini anapoingia ile mitambo ya mwaka 1963 ataiondoa. Nimeona mashine moja imeagizwa kutoka Swiss, kwenye kiwanda kimojawapo, mashine moja ina uwezo wa kufanya kazi kuliko mitambo 10 ya zamani ukiunganisha. Kama amefanya kwa nia hiyo tutamhukumu kwa alivyotekeleza, lakini kama nilivyosema maslahi yetu ni kwamba kiwanda kifanye kazi, kitoe ajira, kizalishe bidha na hatimaye alipe kodi, akitimiza hayo sina tatizo naye.
MHE.DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kuniona.
Kwa kuwa, tatizo la Tabora linafanana sana na tatizo la Mbeya, mojawapo ya Sera ya Awamu ya Tano ni kufufua na kuimarisha viwanda vya ndani katika kukuza uchumi wa ndani, lakini vilevile kuongeza soko la ajira.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mbeya tuna kiwanda cha Mbeya Textile ambacho kimetelekezwa kwa muda mrefu sana, ninaomba Mheshimiwa Waziri atuambie nini mkakati wa kiwanda kile cha Mbeyatex ambacho kimetelekezwa kwa miaka mingi sana? Ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kufufua viwanda hasa viwanda vya nguo, siwezi kutoa jibu moja likawaridhisha Watanzania au Waheshimiwa Wabunge, ni mapana ambayo siwezi kuyakumbatia, kufufua viwanda hivi lazima vifufuke. Ukisoma mkakati wa (C to C) Cotton to Clothing, unaelezea tutakavyofanya, inaanzia kwa wananchi kulima na Serikali kuwawezesha wananchi kulima. Lakini unakwenda zaidi mpaka kwa kudhibiti wananchi wanaoagiza nguo kutoka nje ya nchi ambazo ni dhaifu lakini wengine hawalipi ushuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nimeletewa ripoti, TRA kuanzia mwezi Januari mpaka mwezi wa Mei, walikuwa wameshindwa kuwakamata watu waliopitisha nguo ambazo hazikulipa bilioni 133. Natoka hapa nakwenda kuripoti kwa Waziri wa Fedha, bilioni 133, nguo zilikuwa under-valued, nguo moja nimeoneshwa na wataalam, kilo moja ya nguo ilikuwa imeingizwa nchini kwa kadirio la bei ambayo ni ndogo kuliko pamba, finishing cloth, nguo iliyokwisha tengenezwa kilo moja yake ilikuwa imeingizwa nchini kwa thamani ambayo ni ndogo kuliko bei ya pamba ya Mwanza. Sasa mazingira yote kwa ujumla ndiyo yanafanya ufufuaji wa viwanda hivi iwe vigumu, lakini yote hayo tunayamudu, tutayafanyia kazi, Mbeyatex na yenyewe itafanya kazi.
DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Kwa kuwa, Mkoa wa Tabora ni kati ya Mikoa ambayo tunalima pamba sana hususan Wilaya ya Igunga, na kwa kuwa miaka ya nyuma tulikuwa na kiwanda hicho cha nyuzi lakini pia tulikuwa na kiwanda cha kuchambua pamba kule Manonga ginnery katika Jimbo la Manonga.
Je, Serikali ina mpango gani wa kufufua hicho kiwanda ili kiweze kulisha kiwanda cha nyuzi cha Tabora?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mwizikulu, Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda, Uwekezaji na Mazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza kwa Mheshimiwa Mchungaji Manjelwa, ili Manoga ginnery ifanye kazi na Viwanda vya Tabora ni lazima ule mkakati mzima wa kuanzia pamba mpaka nguo upitiwe wote. Kama nilivyoeleza ni pamoja na kuzuia nguo zinazokuja katika ushindani usio sawa. Tukiweza kutekeleza hayo wakulima wakaridhika, hivi viwanda vitafufuka vyenyewe, lakini wale waliokuwa wamepewa na Mheshimiwa Mkapa na awamu zilizopita, wakashindwa kutumia fursa hiyo tutawanyang‟anya viwanda hivyo, tutawapa Watanzania wengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii ninyi ndiyo wawakilishi wangu, nendeni mkawaambie wananchi anayeona upenyo wowote kwamba mtu anazembea aniletee kielelezo na mimi nitatumia mamlaka niliyonayo kwa kufuata Sheria, tumpe yeye na yeye ajasilie.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa mazungumzo na hawa wawekezaji mahiri wa kusindika tumbaku na mambo ya sigara yanaendelea. Je, mazungumzo hayo yakifanikiwa, ana uthibitishia Mkoa wa Tabora kwamba utapata upendeleo kwa kujengwa Kiwanda cha Tumbaku? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Rais ameonesha nia ya Serikali kuwashirikisha mashirika ya kijamii kama NSSF kushiriki kwenye ujenzi wa viwanda na biashara, je, ni lini mazungumzo hayo, Serikali itaanza na haya mashirika ya kijamii?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ujenzi wa Kiwanda cha Tumbaku Tabora ni la wadau wa Tabora ambao walikaa pamoja na ninyi Wabunge. Nimewaeleza kwamba tunahangaika kutafuta wawekezaji, siku ya Jumapili mwekezaji kutoka China atafika Tabora. Kwa hiyo, Wabunge wa Tabora tukimaliza kikao tukutane kusudi ninyi mtangulie kumpokea Jumamosi halafu tujadiliane. Masharti ni yale yale, kama mtatoa eneo bila kuweka vikwazo vya fidia za ajabu mtapata upendeleo, hali ndivyo ilivyo, utakavyotoa vivutio utapata upendeleo. Ujumbe wa China unakwenda Tabora na Precision Jumapili, tangulieni, Jumamosi tukakutane kule tuweze kuwakaribisha wawekezaji. Kwa hiyo, Tabora nimewafanyia kazi, ni jukumu langu pia ni jukumu lenu.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, uwekezaji wa hizi Social Securities, maelekezo ya Mheshimiwa Rais nimeyasikia, nilichofanya nimemwagiza Katibu Mkuu anayeshughulikia biashara na uwekezaji Wizarani kwangu, akutane na Makatibu Wakuu wa Wizara ya Kazi inayosimamia haya mashirika, akutane na Makatibu Wakuu wa Wizara ya Kilimo, wote wakae, wabainishe ni wapi kwenye shughuli zenye tija ambako hizi Social Securities zinaweza kuwekeza na kuweza kurudisha pato lake. Kwa hiyo ,watalaam watafanya kazi hiyo na nimewaambia kabla ya tarehe 26 waniletee orodha na nitaitangaza hapa Bungeni kwako.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika nakushukuru. Naitwa Genzabuke.
Mheshimiwa Spika, ukosefu wa viwanda katika Mkoa wa Tabora ni sawa na ukosefu wa viwanda katika Mkoa wa Kigoma. Kwa muda mrefu sana Mkoa wa Kigoma umekuwa kama uko kisiwani kwa maana ya ukosefu wa miundombinu ya barabara za lami na umeme. Hata hivyo, kwa juhudi zinazofanywa na Serikali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi, mkoa ule umeanza kufunguka na siyo muda mrefu utafunguka kabisa. Je, Waziri yuko tayari sasa kuwahamasisha wawekezaji kuja kuweka viwanda katika Mkoa wa Kigoma?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ni kweli katika maeneo ambayo nimepewa maelekezo mahsusi kushughulikia ni pamoja na Mkoa wa Kigoma. Napenda kutambua mchango wa Wabunge wa Mkoa wa Kigoma kwa ujumla wenu namna mnavyonipa ushirikiano katika kushughulikia suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, miradi iliyoko mbioni kwenda ni Kigoma Sugar, nimemomba Mkurugenzi Mtendaji wa TIC anipe update kama ilivyokuwa jana, Kigoma Sugar tumefikia wapi. Ameniletea taarifa, nimesema arudie anieleze kwa maandishi yule mwekezaji anasema nini nataka update ya jana, Kigoma sugar iko njiani.
Mheshimiwa Spika, simenti watalaam wa cement wamebainisha kwamba, katika Mkoa wa Kigoma ndiko kuna chokaa nyingi. Kwa hiyo, nakwenda kuwashawishi wenye viwanda, wanaotengeneza clinker Dar es Salaam, itengenezwa clinker Dar es Salaam iletwe Kigoma tuweze kutengeneza cement.
Mheshimiwa Spika, suala la tatu mawese; mpango wa kaya moja kulima heka moja, kaya laki moja, tulime heka laki moja tutengeneze shamba kubwa la mawese nalifanyia kazi na mwekezaji ameshakubali na kiwanda kitagharimu bilioni 15, ni kazi yangu, ni kazi yenu. Atakayenichangamkia ndiyo nitakwenda kwake!
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri napenda kumfahamisha kwamba tunakwenda kwenye Tanzania ya viwanda na kule Mlalo tunalima kabichi, karoti, viazi, hoho pamoja na mazao mbalimbali ya mboga mboga. Je, haoni kwa kuwa sisi tutakosa viwanda wakatutafutia soko zuri la kuweza kupata tija kwenye mazao haya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa mazao na bidhaa nyinginezo zinafungwa katika vipimo ambavyo vinaeleweka, haoni sasa ni wakati wa Serikali kuweka mkazo kwamba na mazao ya wakulima nayo yaweze kufungwa katika utaratibu ambao utawaletea tija wakulima? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu soko la mazao, katika maelekezo ambayo Serikali imetoa na Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yake amesisitiza ni kwamba Halmashauri zote kuanzia ngazi ya Kijiji, Kata mpaka Wilaya tunapaswa kutenga maeneo ambayo moja itakuwa sehemu ya kujenga viwanda vidogo, pili itakuwa sehemu ya kujenga hifadhi na tatu itakuwa sehemu ya kufanyia biashara. Kwa kutengeneza zile business centers, wateja wataweza kufika na kuweza kununua mazao yenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao ya wakulima yakifungashwa vizuri yatapata soko, nakubaliana na hilo. Jambo la kufanya ni kwamba tunapohimiza ujengaji wa viwanda huko vijijini vinaongeza thamani na unapoongeza thamani ya bidhaa inahusisha pamoja na ufungaji. Kwa mfano, tungependa watu wa Lushoto na Tanga zile tangawizi na hiliki mkishazichakata kwenye viwanda vidogo pale ndiyo zinaingia kwenye packaging ambayo itakuwa inaeleza kama ni kilo au ni volume gani.
Mheshimiwa Shangazi tutawasiliana zaidi kusudi niweze kukupa maelekezo ya kiutendaji.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa tatizo la lumbesa linasababishwa na viroba ambavyo vina vipimo tofauti tofauti. Kwa kuwa nchi yetu ilikuwa na kiwanda cha magunia ambayo yalikuwa na kipimo na ujazo ulio sawasawa.
Je, Waziri yupo tayari kwenda kukifufua kiwanda kile ili tuweze kuwa na vipimo vinavyolingana kuepuka kuwadhulumu wananchi wetu? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viroba au vifungashio vyenye ukubwa tofauti suluhisho lake ni kuwa na mizani kwenye buying centre ambao utabainisha kilo stahiki, ukubwa wa gunia sio hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda vya magunia, kwa nini viwanda vya mgunia vya Tanzania vilikufa ikiwemo kile cha Kilimanjaro. Magunia yanayotoka nchi za Asia ikiwemo Bangladesh yanapoingia East Africa hayatozwi ushuru, magunia yanayotengenezwa na viwanda vya Tanzania yanatozwa ushuru katika mazingira hayo lazima tuanguke. Kwa hiyo, mapendekezo ni kwamba lazima tuangalie ulinganisho wa ushuru na gharama za bidhaa zinazotoka nje na zinazoingia ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili limeshafikishwa kwa wahusika na tutaweza kulishughulikia namna hiyo. Kwa hiyo, viwanda vya Kilimanjaro, Singida na Tanzania nzima vitaweze kufufuka kwa namna hiyo.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwanza kabisa nimshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri sana. Kwa kuwa vijana ni nguvu kazi ya Taifa, je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha viwanda vidogo vidogo na kuwawezesha vijana wa Mkoa wa Simiyu, wajasiriamali mitaji ya uhakika na kuwatafutia masoko nje ya nchi, ambapo itapunguza ukosefu wa ajira?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu swali la Mheshimiwa Mbunge limekuwa mahususi naomba nitoe maelekezo yafuatayo:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awasiliane na Meneja wa SIDO wa Mkoa wa Simiyu, atambue kikundi cha Vijana ambao wanatabia ya ujasiriamali, wataelekezwa biashara ya kufanya na katika mkopo wa NDF unaokuja watatengewa fedha kusudi tuwalee na kusudi mje mnipime kwa mwaka mmoja ujao.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Mheshimiwa Waziri, akina mama lishe na akina baba lishe pale Temeke wanakaribia kufilisika toka tatizo la bei ya sukari kupanda lilivyoanza! Hawakushawishika kupandisha bei ya vyakula wanavyouza kwa sababu walitegemea tatizo hili la sukari litakuwa ni la muda mfupi, lakini mpaka leo hawajui ni lini tatizo hili litakwisha. Je, Mheshimiwa Waziri haoni kwamba kuna umuhimu wa yeye kila siku kutoa status update ya sukari hapa nchini kila tunapoingia hapa Bungeni?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwashukuru akinamama lishe kwa kuwa watumishi wa Mungu. Hawana hulka ya kutafuta faida wanatoa huduma, watafurahi duniani na mbinguni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la msingi ni kwamba Mwijage nitoe status ya sukari, kila siku nakubali kabla hatujaahirisha mchana huu nitatoa status ya mgao wa sukari kwa nchi nzima.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri, swali la nyongeza. Kwa kuwa Wilaya ya Maswa imekwishatenga eneo zaidi ya heka 110 na tumekwisha kuandika barua kwa EPZA kuja kuwekeza Maswa. Je, Mheshimiwa Waziri ni lini atatusaidia Maswa, EPZA kuja ku-facilitate maeneo ya uwekezaji ili tuweze kukaribisha wawekezaji kwa maana ya kuwekeza viwanda vidogo vidogo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Mbunge wa Maswa kama Wabunge wengine ambao wamejitolea kutoa maeneo yao ili kusudi kujenga viwanda vidogo lakini na Special Economic Zone. Naomba nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi Mkuu wa EPZA watafute hii barua ya Maswa, waende Maswa na Mkurugenzi wa SIDO wabainishe ni kitu gani kinachoweza kufanyika pale na wanipe jibu ili kusudi nimridhishe Mbunge kabla ya Bunge hili kumalizika.
MHE. JAMES K. MILLYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Ni masikitiko makubwa kwamba kwa miaka takribani miwili, shilingi milioni 15 imezuia kuanzishwa kwa EPZ iliyotarajiwa na Serikali. Mwanzoni mwa mwaka huu mwezi wa Pili, kilo mbili za Tanzanite, kilo mbili Waheshimiwa Wabunge ni takribani bilioni mbili, siyo kama gold, zilikuwa zinaibiwa kutoroshwa nje ya nchi…
MHE. JAMES K. MILLYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali mafupi mawili ya nyongeza. Wahindi hawa wanaoshirikiana na baadhi ya Watanzania waliolelewa na Wahindi walikuwa wanatorosha madini ya Tanzanite nje ya nchi, je, ni lini Serikali itatoa tamko rasmi kwamba EPZ hii itaanza kujengwa Simanjiro ili madini yetu yasije yakatoroshwa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la nyongeza, Mheshimiwa Rais wakati akifungua Bunge hili alisisitiza kuhusu madini haya, Mheshimiwa Waziri juzi wakati akihitimisha hoja yake alisema kuna matatizo makubwa ya Tanzanite. Naomba nitoe takwimu, mwaka 2014…
MWENYEKITI: Tafadhali, swali tu, hakuna takwimu. Naomba kama umemaliza Mheshimiwa Waziri ajibu.
MHE. JAMES K. MILLYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali; mwaka 2014, dola za Kimarekani milioni 300 za Tanzanite zilitoroshwa India, Kenya milioni 100, lakini Tanzania ikauza milioni 38, je, ni lini Serikali ya Tanzania itakuwa makini ili kuwasaidia Watanzania kunufaika na madini yao, na wachimbaji wadogo kama akina Chusa, wachimbaji wadogo kama akina Onee watanufaika na rasilimali hii kubwa waliyopewa na Mungu?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali ni kuligeuza eneo la Mererani Special Economic Zone na mojawapo ya kuweka eneo lile huru la kiuchumi ni kudhibiti ile malighafi au maliasili inayozalishwa pale. Sasa ninachofanya kwa mamlaka niliyopewa, natafuta wawekezaji kama nilivyosema, ili waje pale watengeneze eneo ambako madini yale na madini mengine yatakuwa yanauzwa pale. Tayari ninao wawekezaji watakaobadilisha Mji ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimweleze Mheshimiwa Mbunge kwamba, wamenipa hekta 500, nataka hekta 1000 nyingine zaidi zifike hekta 1,500. Nitatengeneza Special Economic Zone, namwagiza Katibu Mkuu anayeshughulikia uwekezaji wale wawekezaji ambao wanataka kuwekeza Arusha waje Bungeni wafanye demonstration yao ili watu wa Kanda ya Kaskazini muweze kuona wenyewe, niwaachie mzigo ninyi mshindwe kutoa ardhi inayotakiwa.
MHE. JOSEPHINE T. CHAGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Namshukuru sana Waziri kwa majibu yake mazuri na ya kututia moyo wananchi wa Mkoa wa Geita. Nina swali moja tu la kumuuliza. Kwa kuwa vijana wetu wangependa sana kujiajiri au kuajiriwa, lakini hawana ujuzi; je, Serikali iko tayari kuwapa ujuzi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni kwa Waheshimiwa Wabunge wote na Watanzania wote. Katika kila Mkoa kuna Ofisi ya SIDO. Mojawapo ya kazi ya SIDO ambayo analipwa pesa na Serikali ni kutoa elimu ya ujasiriamali kwa watu wote. Semina na mafunzo yale yanatolewa bila gharama.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Chagula, awasiliane na Meneja wa Geita, aandae vijana wake waende wapate elimu hiyo, halafu kuanzia hapo tuone watajiendeleza namna gani.


WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwanza kabisa naomba nikubaliane na sekta ambayo inaongozwa na Waziri mwenye dhamana ya Viwanda na Biashara kupitia SIDO ili kutengeneza ujuzi na kuajiri vijana wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Kitengo kinachoshughulikia Kazi, Vijana na Ajira katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Serikali imetenga fedha ambazo zitatumika kwa makusudi mazima kuongeza ujuzi kwa vijana mbalimbali walioko katika nchi ya Tanzania na ili kuwafanya vijana hao; kwanza, waweze kujiajiri wao wenyewe, lakini vilevile waweze kuajiriwa katika viwanda vilivyopo na vitakavyoanzishwa katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunawahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba, shilingi bilioni 15 zilizotengwa zinaweza kutoa msaada mkubwa sana wa kuongeza ujuzi kwa vijana wa Tanzania na kukabiliana na tatizo hili la ukosefu wa ajira.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nina swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mpango wa REA umesaidia sana kusambaza umeme katika vijiji vyetu, je, SIDO haiwezi kuwasaidia vijana wetu vijijini kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya kukamua karanga, ufuta ili tuweze kupata mafuta kwa ajili ya kuwauzia wananchi wetu likiwemo Jimbo la Mpwapwa
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ya Serikali ni kwamba, kupitia kata na wilaya watenge maeneo ambapo miundombinu wezeshi ya umeme na maji itapelekwa pale. Pia Mamlaka ya Wilaya ibuni ni kiwanda gani kitengenezwe kwa kuangalia malighafi, nguvukazi, soko na teknolojia rahisi. Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji itawapa elimu na utaalam na inapobidi Ofisi ya Waziri Mkuu inayohusika na Uwezeshaji itaweza kuwawezesha.
Mheshimiwa Naibu Spika, niongezee majibu ya swali la Mheshimiwa Mchafu. Mkoa wa Pwani kuna viwanda vikubwa vingi vitajengwa, hilo sina tatizo nalo. Kuna viwanda vikubwa vitajengwa Mkuranga mfano kiwanda cha kutengeneza tires na vigae, hiyo sina shida nayo. Kama nilivyomjibu Mheshimiwa Lubeleje, mtengeneze maeneo kwenye kata, muangalie rasilimali zinazopatikana, tuwapelekee umeme, tuwapelekee maji halafu wataalam watawaonesha kitu gani mtafanya kulingana na hulka zenu na ubunifu mlio nao.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri lakini nilitaka kwanza afanye marekebisho ya jina, naitwa Hawa na siyo Awa. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, napenda kujua huo mwaliko wa HELM umetumwa lini ili tuweze kufuatilia?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mheshimiwa Waziri amekuwa akituhamasisha sana Wabunge kuwahamasisha wawekezaji katika mikoa yetu. Napenda kufahamu ni vivutio gani anavyo ambavyo angependa pale tunapohamasisha tuviseme ili tusikwame kama ambavyo viongozi wa Mkoa wa Mtwara walivyokwama katika suala hili la kiwanda cha HELM?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa. Nahitaji kutoa maelezo kidogo kwa lile la kwanza hata home boy wangu amuita hivyo hivyo. Lile jina ambalo siwezi kulisema hata home boy wangu huwa anamwita hivyo hivyo. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni kwamba kampuni ya HELM imealikwa na TPDC siku 10 zilizopita. Mimi pamoja na yeye Mheshimiwa tutawasiliana na TPDC na kwa kauli yangu nawaagiza TPDC wawasiliana na huyo mwekezaji na watoe taarifa wakati tukiwa hapa Dodoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie vivutio wanavyovizungumzia, tatizo hasa siyo vivutio ni ucheleweshaji wa mradi walioupata watu wa Mtwara. Kilichopelekea ucheleweshwaji wa mradi ni taarifa za kisayansi. Wakati tukiwa na TCF 2 Mtwara tulikuwa hatuna uhakika kama gesi ile ingeweza kutosha mahitaji yetu hasa mahitaji ya umeme. Uvumbuzi wa gesi TCF 2.17 za Ruvu, zimetupa kiburi na kujidai kwamba tunaweza kuwasha mitambo. Ndiyo maana tarehe 10 Julai, kuna mwekezaji nakwenda kuzindua mtambo wake wa megawati 400 pale Bagamoyo. Kwa hiyo, hayo yaliyopita yamekwisha, ukitaka vivutio vinapatikana kwenye Investment Policy, viko wazi na vingine nitaandika kwenye jedwali. Ninyi njooni mnione mimi, mwekezaji akikwama mje mnione, ikikwamishwa na Wizara yoyote njooni mnione mimi. Mimi ndiyo receptionist, nitaweza ku-clear matatizo yanayokwamisha uwekezaji.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kiwanda cha Chai cha Mponde kimefungwa takribani miaka mitatu sasa na Msajili wa Hazina alivyokuja alitamka kuwa zimetengwa shilingi bilioni 4 na kwenye bajeti ya mwaka huu hazipo. Je, Serikali ina mpango gani wa kufungua Kiwanda cha Chai Mponde ili wakulima wale wasiendelee kupata adha ile?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Mponde, shilingi bilioni 4, usitegemee pesa ya kuingia kwenye viwanda uione kwenye bajeti yangu, tunawasiliana na watu wenye pesa watawekeza pale. Nimekwenda mbele zaidi, nafanya mazungumzo na Serikali ya Misri kusudi chai ya Kagera - Maruku na chai ya Mponde - Tanga iuzwe moja kwa moja Misri. Mimi nina maslahi na kiwanda cha Mponde.
MHE. STEPEN J. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda hiki kina umri wa miaka 42 zaidi hata ya umri wangu na tangu kimejengwa hakijawahi kufanya kazi. Nataka majibu ya uhakika kwamba ni lini kiwanda hiki kitafanya kazi na Serikali imetoa muda gani kwa mwekezaji huyu kuhakikisha kiwanda hiki kinafanya kazi?
Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda hiki kimechukua maeneo na mashamba ya wananchi wa Kata za Chibe, Old Shinyanga pamoja Ndembezi. Je, Serikali iko tayari kuruhusu vijana kutumia maeneo hayo kwa kilimo cha bustani ili wajipatie kipato na ajira wakati tathmini hiyo inaendelea kwa miaka 42 ambayo wamesubiri?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naelewa concern ya Mheshimiwa Mbunge anataka ajira kwa ajili ya wananchi wa Shinyanga, lakini anataka soko la uhakika kwa mifugo yote ya Kanda ya Ziwa. Katika miradi inayonipa shida ni pamoja na kiwanda hiki, huyu mwekezaji hakufanya vizuri. Katika watu ambao katika utendaji wangu wa kazi nakuwa mwangalifu nao ni mwekezaji huyu, siyo mwekezaji mzuri, nimemkabidhi kwa Treasurer Registrar anamfuatilia, kuna masuala ya kisheria. Huyu mtu ametumia kiwanda kile akakopa pesa, sasa anategea tumnyang‟anye kiwanda kile kusudi governments guarantee na pesa aliyokopa iishe, siyo mtu mzuri. Mjomba uniache nimfuatilie kwa uangalifu ili tutakapomkamata tumalize kitu once and for all.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kutumia maeneo, huyu mtu yuko under surveillance na nimekwambia siyo mtu mzuri. Kwa hiyo, maeneo yake msiyaguse asije akasema alishindwa kuendeleza kwa sababu tuligusa maeneo yake. Hata hivyo, ni katika maeneo ambayo nataka nitoe majibu yake haraka sana. Nikueleze, hata tajiri namba moja anafuatilia suala hili.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kibiti ni mojawapo ya Wilaya inayolima mihogo kwa wingi lakini ina tatizo la soko ambapo mihogo mingi hutegemewa kuuzwa kwenye Mwezi wa Ramadhani. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kupeleka kiwanda cha kuchakata mihogo katika Wilaya mpya ya Kibiti?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha mihogo, nakuomba Mheshimiwa Ungando uje unione nitakuelekeza kwa Meneja wa SIDO. Pia nitakwenda nawe bega kwa bega tuangalie fursa ya malighafi iliyopo na kiwanda cha namna gani kinaweza kuanzishwa katika mipango hii. Nitafanya kazi na wewe.
MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza; kumekuwa na taarifa kwamba asali yetu ya Tabora ina chembechembe za sumu, lakini je, Serikali imewahi kufanya utafiti wa kisayansi na kuja na majibu ambayo yataleta ukweli wa jambo hili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali sasa iko tayari kuwasaidia wanaoshughulika na zao la asali kuwapatia masoko yenye uhakika, kwa sababu mara nyingi wanakuja watu kutoka nchi za Uarabuni na kununua asali katika njia za panya.
Je, sasa Serikali inao mkakati gani mahususi kuwasaidia wananchi hawa ili asali yao iweze kupata soko la uhakika bila kunyonywa?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, asali ya Tabora na asali ya Tanzania haina chembechembe yoyote ya sumu, ni asali safi na world demand (mahitaji ya dunia) kwa asali ya Tanzania ni tani 5,000 kwa wiki, tani 260,000 kwa mwaka, kiasi kinachoweza kuingiza trilioni nane kwa asali ni kwamba sisi tumebaki kuchangamka. Kwa hiyo, wanaosema ina sumu hawatutakii mema tuliyonayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu masoko ya uhakika kwa kushirikiana na UNDP, TAN TRADE na Wizara yangu tunaandaa mfumo wa soko na mfumo wa soko unaanza kwa kuchakata asali. Nilijibu swali la kwanza la msingi, kimsingi ni-declare interest, kuna mwenzetu tunahangaika kupeleka kiwanda cha kwanza cha asali Tabora. Kiwanda cha asali ni dola 50,000 kwa hiyo, wenzetu wanaotupiga madongo toka nchi jirani wamekuwa wakichukua ile raw honey ambayo haijachakatwa na kuchakata nchini kwao na ku-pack kupeleka. TANTRADE na Wizara yangu, tunalishughulikia na nichukue fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge, tuelekezane, nunua viwanda, mtaweza kuona faida, faida iko kwenye asali. Trilioni nane ni mara mbili ya pesa tunazotumia kununua mafuta jamii ya petroli ambayo inatu-cost trilioni nne kwa mwaka.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Singida pamoja na Mkoa wa Dodoma ni miongoni mwa mikoa masikini ambayo inahitaji usaidizi wa Serikali. Sasa Mheshimiwa Waziri yuko tayari kusaidia wananchi wa mikoa hii ya Dodoma na Singida kwa ushawishi wake mkubwa na weledi wake kufanya basi angalau kiwanda kimoja kiwekezwe katika Mkoa wa Singida, hususan katika Jimbo la Manyoni Magharibi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kutembelea wananchi wa Itigi ili kujionea fursa zilizopo ili kushawishi wawekezaji waweke kiwanda katika eneo la Itigi? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kama niko tiyari kuwekeza Singida na Dodoma? Niko tiyari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili ni kutembelea Itigi.Ninapaswa kutembelea Singida kwenye Jimbo la Mheshimiwa Kingu, kuna mradi wa maziwa, tutapanga twende wote.
Lakini nichukue fursa hii kuwaeleza kwamba ukanda huu una fursa ya maziwa, una fursa ya viwanda vya mafuta jamiii ya alizeti na una fursa ya sekta ya ngozi. Hapa Dodoma Wizara yangu imetengewa ekari 200 na ninayo pesa tayari ya kutengeneza cluster ya ngozi.
Kwa hiyo, hii ni sehemu ambayo ni potential na kwa kutumia ngozi tutatoka; mnajua idadi ya ng‟ombe tulio nao. Kwa hiyo, Dodoma tunaweza kutengeneza viatu tukavika Afrika.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Ikizingatiwa azma ya kujenga Tanzania ya viwanda, ni lini Serikali itajenga viwanda hivi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa nini Serikali isiwekeze kwenye kujenga viwanda vidogo vya drip kwenye hospitali za Rufaa za Mikoa nchini ili ku-supply drip kwenye hospitali husika kama ilivyokuwa zamani badala ya kuagiza drip hizo nje ya nchi jambo ambalo ni aibu kwa Taifa letu? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tunajenga viwanda na niwatoe wasiwasi Wabunge wenzangu kuna kampuni mbili za media zimekubali kunisaidia kujibu maswali ya Wabunge kuanzia kesho. Wataonesha vipindi vyote, kiwanda hiki Mwijage naonyesha, hiki kinajengwa hiki kinajengwa. Hata hivyo, kwenye swali langu la msingi nimeorodhesha makampuni ambayo nimehamasisha, nimepiga sound, wakaja kuomba kuwekeza. Kwa hiyo kazi yangu ndiyo hiyo, nimeeleza viwanda vyote hivi wamekuja kuwekeza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa nini hospitali ndogo zisitengeneze drip. Nimshukuru Mheshimiwa Khadija, hospitali za kwetu nchini ukienda Tabora, Kagondo, Bugando wanatengeneza drip. Nitumie fursa hii kama kuna hospitali yoyote ambayo inataka kwenda kupata ile mitambo ya kutengeneza drip iwasiliane na Wizara ya Afya tuna utaratibu maalum. Viwanda vya kutengeneza drip siyo pesa za ajabu, ndiyo vile viwanda wanavyosema Mwijage anatembea navyo mfukoni, kweli ninavyo.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa, umuhimu wa kiwanda hiki cha matairi unajulikana na uwepo wa kiwanda hiki kufufuliwa katika Mkoa wa Arusha utaongeza ajira, lakini katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga shilingi bilioni 60, mpaka tunapoongea imetolewa shilingi bilioni mbili tu. Je, kwa Serikali hii ambayo imefilisika kuna dhamira ya kweli kufufua kiwanda hiki?
Swali la pili; kuna wafanyakazi ambao bado wanakidai kiwanda hiki na madai yao wameshayafikisha Hazina, lakini mpaka leo hawajalipwa. Je, ni lini sasa madai haya ya wafanyakazi yatalipwa?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na lile gumu la madai ya wafanyakazi. Mheshimiwa Mbunge naomba nakala ya madai iliyopelekwa kwa Treasury Registrar, nipewe nakala hiyo, mimi nitafuatilia. Naomba Mheshimiwa Mbunge anifuatilie mimi na mimi nimfuatilie Treasury Registrar.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza juu ya dhamira ya kweli, Serikali hii ina dhamira ya kweli na nitumie fursa hii, kwamba Tanzania kuna soko la matairi siyo habari mpya, kwamba sisi ni sehemu ya Afrika Mashariki, it is not the news, kwamba sisi tuko SADC siyo tatizo, tumeelekezwa katika Ilani ya Chama chetu na Mpango wa Pili wa Miaka Mitano General Tyre ifufuke.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kama kuna mtu yeyote ana mwekezaji, anataka kujenga kiwanda mimi nitahakikisha nitajenga kiwanda, Mheshimiwa Rajab Adadi na Mheshimiwa Stephen Ngonyani (Majimarefu) wamekuwa wakinifuatilia, fursa ipo, sisi kazi yetu ni kuweka mazingira wezeshi, kupiga sound ili kusudi wawekezaji waje wawekeze, Serikali haitajenga kiwanda inatengeneza mazingira wezeshi.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza kabisa napenda niishukuru Serikali kwa kukiri udhaifu mbalimbali ambao unaweza kuwa unasababishwa na ajali zinazoweza kuwa zinatokea ambazo zimeelekezwa kwenye swali la msingi ikiwemo ni pamoja na uzoefu na uchakavu wa miundombinu. Swali langu la nyongeza ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba wote tunafahamu Tanzania na China ni nchi marafiki na bidhaa nyingi za biashara karibu asilimia 95 zikiwemo pikipiki za bodaboda zimekuwa zikitoka China.
Swali langu, je, ni kwa nini Serikali sasa isione namna ambayo inaweza ikafanya mazungumzo na Serikali ya China kwa kuangalia bidhaa ambazo zinaingizwa zikiwemo za bodaboda na vitu vinginevyo ili Serikali ya China ama kupitia makampuni yanayoagiza hizi pikipiki kuweza kuchangia katika zahanati zetu kama vile ambavyo wawekezaji wengine wanavyofanya katika kutoa huduma za jamii? Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Spika, lakini la pili, pamoja na kuanzishwa na kuletwa hiyo Sheria ya Bima, je, Serikali haioni pamoja na hayo yote, kuiomba na kufanya mazungumzo na Serikali ya China pia katika kusaidia kuongeza vifaa tiba? Kwa sababu bima peke yake haimsaidii mwananchi aliyekatika miguu miwili ama mmoja kuweza kutibiwa na bima, bado atahitaji kununua mguu wa bandia na vitu vinginevyo na hospitali za Serikali yetu bado hazina uwezo katika wa kuwa na vifaa kama hivyo. Je, hawewezi wakafanya mazungumzo ili kuweza kupatiwa huduma hasa za afya ambazo zinaweza zikaenda moja kwa moja vijijini kwa wananchi wetu? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru. Watengenezaji wa pikipiki na magari yao yanakidhi viwango na TBS inathibitisha. Tatizo kubwa la ajali za bodaboda au hizi gari aina ya Noah ni kwa ajili yetu sisi watumiaji. Watu wanaendesha bodaboda wakiwa wamelewa, wanapakiana watano mpaka sita, huwezi kumlaumu mtengenezaji. Hata chakula, ukila kilo 10 za pilau zitakudhuru. Kwa hiyo ni juu yetu sisi Watanzania tufuate masharti ya kutumia hivyo vifaa sio tatizo la Mchina.

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kitaalamu ajali inaweza ikasababishwa na matatizo yanayoweza kujitokeza katika ngazi nne tofauti. Katika ngazi ya mtumiaji, katika ngazi ya chombo, lakini pia katika mazingira ambapo ajali imetokea kwa maana ya design of the road na vitu kama hivyo.
Sasa matatizo yote haya imeonekana kwa kipindi kirefu yanasababisha ajali za barabarani ambazo zinasababisha maumivu kwa watumiaji ama muda mwingine zinasababisha vifo. Yote haya ambayo ni madhara yanayotokana na ajali za barabarani mwisho wa siku yanakwenda ku-impact mfumo wa afya, yanaenda kuongeza mzigo wa gharama kwenye kutoa huduma za afya. Ndiyo maana Serikali sasa inakuja na mkakati wa kufikiria namna ya ku-charge gharama fulani kwenye kila chombo cha moto ambacho kitaingia barabarani kabla hakijaingia barabarani. Tozo hiyo itakuwa inatozwa kila mwaka, lakini bado tuna mazungumzo ndani ya Serikali kuona kama jambo hili litakubalika ili tuweze kulileta sambamba na mapendekezo mengine kwenye Sheria ya Single National Health Insurance ambayo tunatarajia kuileta hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, malengo yetu ni kwamba wote wanaopata ajali wawe na bima za afya ili waweze kupatiwa huduma pale ambapo inajitokeza wamepata matatizo yoyote ya kiafya. Lakini hatuwezi kuchukua mzigo wa magonjwa ya watu wetu tukaurundika kwa Wachina eti kwa sababu wanaunda vifaa vya moto, hapana. Jukumu la kutoa huduma za afya zilizo bora kwa Watanzania ni la Serikali yao na hatujalishindwa bado.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, wakulima wa Tanzania wanaelekea sasa kwenye msimu mwingine wa kilimo ikiwa mazao yao bado wanayo manyumbani hawajauza. Tuliona wakulima wa nyanya, mbaazi, mahindi na mazao mengine, na Serikali ilitoa kauli katika Bunge hili kwamba wanatafuta masoko nje ya nchi nilijibiwa na Naibu Waziri wa Kilimo. Naomba nifahamu mchakato huo umefikia hatua gani maana wakulima mpaka sasa wana mazao yao?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, majibu ya Waziri ni kwamba, wanaanzisha viwanda vidogo vidogo vya kuchakata mazao ili mazao haya yapate soko na mtawezesha sekta binafsi na Serikali haitoi moja kwa moja fedha kwa ajili ya viwanda hivyo watu binafsi waanzishe. Wakulima wa Tanzania wasubiri kwa muda gani mpaka hivyo viwanda vianzishwe ili mazao yao yapate soko?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nianze na hili ambalo ni rahisi. Wananchi wasubiri kwa muda gani kuanzisha hivyo viwanda?
Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunajenga viwanda. Lengo la kujenga viwanda ni kuongeza thamani na kupunguza uharibifu wa mazao (post-harvest loss). Jambo la kufanya Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote na Watanzania nendeni SIDO, na nimekuwa nikilisema, kusudi waweze kutambua na Naibu Waziri wa Ajira alizungumza hapa, kuna kitu kinaitwa ODOP (One District One Product) inalenga kuangalia katika eneo lenu tatizo ni nini, fursa ni ipi.
Mheshimiwa Spika, sasa watakuongoza wale na watakuvuta mpaka uje ufikie kwangu tuweze kupatia suluhisho lakini mimi nina imani na Watanzania wakielekezwa, wakiongozwa wanauwezo wa kuwekeza. Kwa hiyo suluhisho ni tutaanza lini, tumeshaanza sasa hivi tunajenga viwanda. (Makofi)
Tatizo lake Mheshimiwa Mbunge nenda kamuone Meneja wa SIDO kama ukiwa na wepesi njoo unione mimi nitaweza kukupatia suluhisho.
Mheshimiwa Spika, swali la pili; tatizo la nyanya na tatizo la mbaazi. Tanzania kama Taifa tumepata tatizo kubwa la bei ya mbaazi na ndiyo maana wananchi unao wazungumzia wameweka mbaazi zao. Mwaka jana kilo ya mbaazi ilikwenda mpaka shilingi 2,000 lakini bei ya soko la mbaazi imeshuka mpaka shilingi 500 tatizo tunalijua.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje, tunawasiliana na Serikali ya India ili tuwe na makubaliano ya moja kwa moja kuuza mazao hayo ya mbaazi kwa kushirikiana na Serikali ya India. Tanzania tulikuwa tunauza tani laki moja ya mbaazi, Mheshimiwa Mo ametupa order ya tani milioni mbili nina uhakika tutafanikiwa kuwapa majibu Watanzania.
MHE.GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je, Serikali ipo tayari kufanya utafiti ili kubaini faidi na vitu muhimu vinavyohitajiaka katika suala zima la pombe hii?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa vile Tanzania inahitaji uchumi wa viwanda Serikali ipo tayari kuwapeleka wajasiriamali hawa China, Japan na Afrika Kusini ili kujifunza zaidi na waweze kutengeneza kitaalam zaidi kama ilivyo pombe ya konyagi? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, faida za kinywaji hiki gongo zinafahamika. Wataalam wangu wana uwezo na faida za kinywaji hiki, tatizo letu ni usalama. Kwa hiyo, mimi nitawaelekeza wataalam wangu waje kwenye jimbo lako Mheshimiwa Mbunge kusudi wahakikishe kwamba kile kinywaji kama kinatengenezwa kitengenezwe salama.
Lakini kwenye jibu langu nilikuambia watu wengi wanaokunywa gongo hawapendi gongo wanapenda ile ladha yake. Sasa tutatafuta ladha tuwatengenezee kinywaji salama chenye radha ya gongo. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, kuhusu kuwapeleka Watanzania kwenda China, nikimjibu Mheshimiwa Dotto napenda nitoe taarifa kwa Bunge lako Tukufu tarehe 7 mpaka 11 Disemba, 2016 nimewaalika watengeneza viwanda wote na wenye viwanda kwenye uwanja wa Sabasaba kusudi wawaoneshe Watanzania mitambo mbalimbali ambayo ni viwanda na namna ya kuitumia.
Kwa hiyo, badala ya kuwapeleka China, na Watanzania ni milioni 53 sina nauli ya kuwapeleka, njooni Sabasaba kila mtu uangalie kiwanda anachopenda, korosho, kahawa na kila kitu kitakuwa pale.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana lakini napenda kukuthibitishia kwamba niko sawa sawa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, kila kabila hapa nchini lina aina fulani ya pombe ya asili ambayo inapendwa. Kule kwetu Rombo viwanda vidogo vidogo kwa ajili ya pombe za aina mbalimbali viko vingi tu. Niliwahi kuomba hapa Bungeni; ni lini Serikali badala ya kupiga vita viwanda hivi ikatuma wataalam wake wa TBS na TFDA wakafanya ukaguzi na wakapima aina ya pombe ambazo zinapatikana huko; na kwa sababu sasa hivi tunajenga Taifa la viwanda tukawa na viwanda ambavyo vinaweza vika-improve zile pombe za asili kwa faida ya watu wetu na kwa ajili ya kuongeza mapato na ajira ya maeneo husika?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imegawana mikoa yote ya nchi hii katika makundi manane, na nitawaagiza timu itakayokwenda Mkoa wa Kilimanjaro kwenye Jimbo la Rombo kwamba wafuatilie suala hilo namna gani tunaweza kutengeneza viwanda vya kuzalisha ile pombe wanayoipenda wananchi kwa kuzingatia ubora na afya; nitazingatia.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, kuna jambo moja nataka tuliweke kwenye rekodi lakini pia swali langu kwa Mheshimiwa Waziri; kwa sababu kwa muda mrefu Serikali ilikuwa ikitangaza kwamba gongo ni pombe haramu kama ambavyo umeona watu wengi swali hili wakiliuliza, lakini kuna pombe mbalimbali zinazotengenezwa kutokana na mazao.
Mheshimiwa Spika, kule kwetu kuna pombe inatengenezwa nipa ndiyo hiyo hiyo gongo inatokana na mabibo makavu lakini pia ni sehemu ya kuongezea wakulima kipato.
Je, Serikali haioni sasa kama hawataki wakulima wale wapike gongo kwa kutumia zile malighafi zao ambao ni sehemu ya korosho kwa nini sasa isinunue wakaenda kufanya hata chakula cha mifugo kwa nia ya kuwaongezea wakulima kipato?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyozungumza kwenye suala la Mheshimiwa Selasini, suala linalotukwamisha, na ndiyo maana watu wengine kwa kutokujua wanaichukia TFDA, hoja ni kwamba kinywaji kile kinatengenezwa vipi? Kinakuwa packed vipi? Na kinapimwa kuthibitisha huo ubora, na nimeshaahidi, na niwaeleze wataalam wangu watakao kwenda Mikoa ya Lindi kafuatilie kinywaji hicho.
Mheshimiwa Spika, lakini nikutake wewe Mheshimiwa Mbunge rafiki yangu Bwana Mwambe na wewe ni rafiki yangu na unajua. Njoo unieleze wazo hilo tutumie wawekezaji wa ndani hata wa nje tuweze kutengeneza kinywaji kizuri hicho tuweze kuuza Tanzania na masoko ya nje.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nasikitika kwamba Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara wamemuongopea kabisa. Kwa sababu suala la EPZ nilianza ku-deal nalo tangu nikiwa Mbunge wa Viti Malaam na mpaka Mbunge wa Jimbo, hiyo Kata ndiyo Kata yenye wapiga kura wengi na ndiyo waliyonipa kura nyingi kwa sababu ya hiki kitu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pesa zilizotumika kulipa EPZ ni shilingi 1, 240, 000, 000, hakuna ukaguzi wowote ambao umefanyika, wala uchunguzi wowote mpaka hivi sasa tunavyoongea. Kilichotokea, Mkaguzi wa Ndani alitoa ripoti kwa Mkuu wa Mkoa ambaye naye katumbuliwa kuhusiana na hili na Mkuu wa Wilaya aliyeshiriki na ubadhirifu huu ametumbuliwa kwa ajili ya udanganyifu wa suala hili.
Swali la kwanza, je, uko tayari sasa kuagiza TAKUKURU na CAG kufanya uchunguzi ili watu waliokuwa wakilindwa na Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wiliya washughulikiwe?
Swali la pili, nini hatma ya wananchi wa eneo hili ambao waliahidiwa watapelekwa katika eneo mbadala ili kupisha mradi wa EPZ na wala hawana tatizo nalo?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kwa masikitiko makubwa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Ester Bulaya.
Mheshimiwa Spika, taarifa nilizopewa na watendaji wangu wanasema wamelipa bilioni 2.3, yeye alizopata ni bilioni moja, hapa kuna tatizo na hili ni tatizo la kipolisi. Mimi pamoja na CAG pamoja na TAKUKURU, nitamuomba Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi anisaidie. Hili siyo suala la TAKUKURU siyo suala la Polisi, tofauti ya bilioni moja ni pesa kubwa sana wala haihitaji uchuguzi, ni kupiga foleni watu, aliyelipwa akae huku, ambaye hakulipwa akae huku watu wanakwenda selo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, niko tayari na nitaomba Mheshimiwa Mwigulu anisaidie na Mheshimiwa Simbachawene, kwa sababu wanaotuhumiwa ni watu wa TAMISEMI. Hili siyo langu, hivi siyo viwanda hivi, hili siyo eneo langu ni la Mheshimiwa Simbachawene na Mheshimiwa Mwigulu. Wizi siyo viwanda.
Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Bulaya nashukuru, Serikali itakwenda kulishughulikia tunapokwenda Mawaziri watatu kukamata panya hao, tutahakikisha wananchi wanapewa maeneo mazuri. Zaidi niwaambie watu wa Mara, jambo la muhimu linaloniuma ni kuhakikisha watu Mara tunatafuta wawekezaji ili EPZA iweze kutengeneza sehemu ya uwekezaji kwa ajili ya maendeleo ya ukanda ule.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nimesikia na tutalishughulikia!
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru
sana. Kwa kuwa, ulevi wa pombe hizi za kienyeji sasa hivi kumekuwa na
ongezeko la matumizi makubwa sana ya pombe aina ya viroba ambavyo
vifungashio vyake na bei yake imekuwa ni nafuu sana ambapo imepelekea hata
watoto wa shule wanaweza kumudu kati ya shilingi 300 mpaka 500 kuzinunua.
Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kupiga marufuku pombe za viroba ili
kunusuru Taifa hili?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika,
kinachofanyika sasa ni utaratibu, lakini ukweli ulio wazi ni kwamba viroba
vitapigwa marufuku na tutaanzisha packaging ya pombe kali kwenye ujazo
ambao itakuwa ni vigumu kwa mtu kuficha. Watoto wa shule kwa sababu ni
rahisi wanaweza kuficha. Tutaweka kwenye chupa ya glass, ujazo utakuwa
mkubwa kiasi kwamba mtoto ashindwe kununua lakini hata dereva wa daladala
ashindwe kuficha. Ni suala la muda na Waziri wa Mambo ya Mazingira
alizungumzia jana.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona.
Sehemu ya swali langu imeshajibiwa lakini naomba niulize. Kwa kuwa sasa hizi
pombe zinatumiwa sana na watu wengi, ni kwa nini Serikali sasa isifikirie kujenga
kiwanda cha kuzisafisha na kuziwekea viwango kama Uganda wanavyofanya
na kile kinywaji cha „Uganda Waragi‟?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya
Serikali ni kuweka mazingira ya uwezeshaji, wanaowekeza ni Sekta Binafsi.
Nichukue fursa hii shangazi, tujasirie kusudi tuweze kukusanya ile konyagi ya
nyumbani, tuiweke kwenye ubora tuweze kuuza. Kila mtu atafute fursa kwake
kusudi aweze kuboresha vile vinywaji ambavyo havina viwango viingie kwenye
viwango, tupate pesa, tutengeneze ajira lakini mwisho wa siku tulipe kodi.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nataka kufahamu kwamba kwa muda mrefu Serikali kupitia Mfuko wa Wakfu wa kuendeleza zao la korosho umekuwa ukiruhusu pesa kwa ajili ya kufanya tafiti mbalimbali kwenye kuongeza thamani ya mazao ya wakulima ikiwemo mabibo kwa ajili ya kupata juice ambayo inaonekana ina uwezo mara tano zaidi wa kupata vitamin c kuliko ilivyo kwenye machungwa. Pia mabaki ya korosho kavu ambayo ni kochoko na yenyewe kuna uwezekano mkubwa sana wa kuweza kupata gin. Baada ya tafiti hizi kukamilika ni muda mrefu sana umepita, je, Serikali iko tayari kuanzisha viwanda kwa ajili ya kutengeneza juice pamoja na gin ili kuweza kuongezea wakulima hawa kipato kwa sababu mabibo pamoja na kochoko sasa vitakuwa rasmi na vitaweza kununuliwa na Serikali?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilijibu swali la Mheshimiwa Conchesta na naomba nirudie kwa maslahi ya Wabunge wote na Watanzania. Serikali kazi yake ni kuweka mazingira bora ya wawekezaji. Mheshimiwa Mbunge, nakuomba uje tukae wote kusudi hizo taarifa ulizonazo za fursa ya uwekezaji tuweze kuziweka pamoja kwenye andiko zuri, tutangaze ili tuweze kupata wabia wa kuweza kuwekeza kwenye kiwanda hicho. Hata hivyo, mwekezaji mzuri ni Mtanzania, ni mwananchi wa Jimbo lako, ni wewe mwenyewe Mheshimiwa Mbunge. Kwa hiyo na sisi tutafute rasilimali tuweze kujenga viwanda sisi wenyewe.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa bidhaa nyingi zinazoonekana nchini kuwa ni feki kwa asilimia kubwa zinatoka nchi ya China na kupitia Bandari ya Dar es Salaam; mpaka sasa Serikali imewachukulia hatua gani TBS, FCC, pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama vinavyosababisha bidhaa hizi kupita na baadaye kuwaathiri wananchi wasiojua chochote kinachoendelea? (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, hivi karibuni Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano alitangaza kuzima simu ambazo zilionekana ni fake, wakati zinaingia nchini zililipa kodi na zikaonekana ni sahihi mpaka kuingizwa kwenye maduka na baadaye wananchi wakazinunua. Lakini baadae Serikali hii hii ya Chama cha Mapinduzi ikaona hazifai na zikazimwa, badala yake wananchi ndio wakapata gharama ya kuingia tena kununua simu nyingine. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia au kuwalipa gharama wananchi kwa kuwa uzembe huu ulifanyika na Serikali yenyewe ya Chama cha Mapinduzi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aida, na nianze na hili la pili ambalo ni rahisi. Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya mambo yanayotusaidia ni Wanasayansi wa Wizara ya Mawasiliano kwa kugundua njia rahisi ya kuweza kugundua kitu feki. Kwa kufanya hivyo wametusaidia kwa sababu simu zile zina madhara. Bidhaa imeingia, umeinunua, umelipa kodi; si busara kukuacha uendelee kuitumia ikuumize kwa sababu ulilipa kodi; nichukue fursa hii kuwashukuru wataalamu wetu waliogundua njia hiyo. Mheshimiwa Mwenyekiti, nitawasaidiaje; tunalenga kutengeneza kiwanda cha kutengeneza simu ambazo zitawafaa wale wananchi ambao wanashawishika kununua simu za bei rahisi. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, namba (a) hatua gani tumechukua kwa TBS na FCC. Mheshimiwa Mwenyekiti, bidhaa bandia zinaingiaje nchini, tuna matatizo. Mipaka yetu ni porous,lakini katika jibu langu la msingi nimesema kuna wananchi wema wanatusaidia. Kwa hiyo, nchi yetu kwa sababu mpaka ni mkubwa na ni porous,kuna wimbi kubwa la bidhaa zinazoingia humu kimagendo na ndiyo maana kikwazo kimojawapo cha kufufua baadhi ya viwanda, hasa vya nguo ni kwa sababu, kuna bidhaa zinaingia kimagendo kutoka nchi jirani na kutoka hizo nchi zijazo. Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kwamba bidhaa yote bandia inatika China, sina uhakika wa suala hilo.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa naamini kabisa wapo watu kutoka EPZ ambao walikuwa wanafuatilia jambo hili na kwa mara ya mwisho shamba hili lilifutwa miaka mitano iliyopita, kwa hiyo jambo hili lilikufa. Lakini kutokana na jitihada za Mkuu wetu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya pamoja na Mkurugenzi limefufuliwa. Sasa Mheshimiwa huoni kuna haja sasa ya wewe mwenyewe kufika na kujionea; kwasababu, katika Mkoa wa Iringa sehemu pekee ambayo tumeitenga ni sehemu ambayo wananchi waliitoa au tulinyang‟anya mashamba kutoka kwa watu wengine ambao kwa muda mrefu wamekuwa hawayatumii. Sasa huoni kuna haja yaw ewe Mheshimiwa Waziri, na kwa kuwa, umesoma Tosa Maganga, ukafika ukaona hili jambo? Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa, kiashiria kimojawapo cha ujio wa viwanda ni pamoja na EPZ na mambo mengine, na ili viwanda viendelee, ili upate viwanda ambavyo unaimba kila siku na kuvizungumzia vizuri unahitaji uwe na miundombinu ya barabara, maji na umeme; na ukichukulia kwamba katika Mkoa wa Iringa sehemu pekee ni Kilolo ambayo ina sifa hizo, lakini haina miundombinu ya barabara, maji wala haina umeme wa kutosha. Sasa je, huoni kuna haja ya wewe na Mawaziri wenzio mkakaa mkaangalia uwezekano wa kuboresha miundombinu, hasa katika Wilaya ya Kilolo katika barabara za Rang‟ang‟ange, Kidabaga, Mwatasi na sehemu nyingine?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niko tayari na nilishazungumza hata Mheshimiwa Ritta, kuna viwanda vya maji vinatengenezwa. Niko tayari sana, nakwenda, na nimeeleza kwenye jibu la msingi kwamba, inatengenezwa master plan ambayo itaonesha miundombinu wezeshi na miundombinu saidizi. Miundombinu wezeshi na saidizi ndio inawahusu Mawaziri wengine. Ngoja mimi nisafishe njia, Mawaziri wengine watakuja, nakwenda Kilolo.
MHE. GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, wakati Serikali inahamasisha wadau na jamii kujenga viwanda hivi, je, Serikali inatoa kauli gani kwa viwanda ambavyo ilivianzisha na imevitekeleza, kama vile kiwanda cha Nasal Ginnery, Ngasamwa Ginnery, Rugulu Ginnery, Malampaka Ginnery na Solwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kukosekana kwa bei nzuri ya ng’ombe na wananchi wa Mkoa wa Simiyu kulazimika kusafirisha ng’ombe wao kupeleka Jiji la Dar es Salaam, je, Serikali inatoa kauli gani na mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba wanajenga viwanda vya nyama kama alivyojibu kwenye swali lake la msingi, kwamba watajenga Bariadi na Itilima. Ni lini mkakati wa makusudi wa kuharakisha kujenga viwanda hivyo?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hili la pili, sehemu ya Mkoa wa Simiyu ni maarufu kwa ufugaji wa ng’ombe na zao la pamba. Juzi Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Anthony Mtaka alikutana na wataalam wangu wa uwekezaji katika jitihada za kusaidiana kutafuta wawekezaji. Wawekezaji wanatafutwa, kwa hiyo, tunachofanya ni sekta binafsi itakayowekezwa kwa hiyo tunatafuta wawekezaji waje wawekeze.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali langu la pili nilikuomba Mheshimiwa Mbunge na wewe uingie kwenye boti hiyo hiyo ya kuwatafuta wawekezaji. Tunatafuta wawekezaji ili wawekeze, ndiyo namna ya kupata wawekezaji. Nitumie fursa hii, kuwashukuru Wabunge ambao mmekwenda maili moja zaidi na kuwatafuta wawekezaji, ambapo mimi kazi yangu ni kuwaondolea vikwazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la kwanza, kwamba vipo viwanda ambavyo vilibinafsishwa, vipo viwanda ambavyo vimekwama, kauli ya Serikali ni kwamba wale waliokuwa na viwanda vile, walio vinunua au vya kwao wavirudishe katika shughuli vifanye kazi. Tunachofanya sasa chini ya Treasure Registrar Wizara yangu na Wizara za kisekta zinazohusika tunawafuata wale kuwashawishi kutumia nguvu zote ili warudi katika shughuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu viwanda vya pamba naomba niwatoe hofu watu wanaolima pamba, chini ya mkakati wa pamba mpaka mavazi tuna imani kwamba uzalishaji wa pamba kwa tija utalazimisha viwanda vile vifufuke kwa sababu the supply itakuwa nyingi na viwanda vitafanya kazi, tuwe na subira.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nimuulize Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Maswa imekwisha kutenga eneo kwa ajili ya uwekezaji (EPZA) zaidi ya heka 110, na Mheshimiwa Waziri tulishakuja kuleta barua na EPZA walishakubali kuwekeza hapo, lakini mpaka sasa hivi hakuna mkakati wowote unaoendelea. Naomba kauli yako na commitment ya Serikali, je, ni lini Serikali sasa au EPZA watakaa na Halmashauri ya Maswa na kuweza kuanzisha mradi huu katika maeneo haya? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimjibu Mheshimiwa Nyongo kuhusu eneo la uwekezaji la Maswa na tunashukuru tumelipata eneo la Maswa na Mheshimiwa Nyongo nimshukuru ni miongoni mwa Wabunge ambao wamejasiria kutafuta maeneo ya uwekezaji bila vikwazo. Kuna wengine maeneo yao yanakuwa na vikwazo vikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kitakachofuata, kama nilivyofanya kwa Bunda, Bunda nimeishaitangaza kuwa special economic zone; nitaitangaza Maswa halafu sasa tutaanza kutafuta wawekezaji.
Nirudie Waheshimiwa Wabunge Wawekezaji wanatafutwa dunia nzima na Tanzania si destnation peke yake, wana-move kutoka Asia kuja Afrika, Afrika si Tanzania peke yake. Kwa hiyo, tuweke mazingira wezeshi tuwe wakalimu waje kusudi tutengeneze ajira.
MHE. HALIMA ALI MOHAMMED Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, Serikali ina mkakati gani mahsusi wa kuhakikisha kwamba Sera ya Tanzania ya viwanda inamkomboa kweli mwanamke wa Kitanzania?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia uwekezaji katika viwanda unazungumzia akina mama; na nguvu kubwa ya ujenzi wa uchumi wa viwanda, viwanda ambavyo ni sustainable, viwanda ambavyo ni darasa, ni viwanda vidogo sana, viwanda vidogo na vya kati. Katika shughuli za kuhamasisha viwanda hivi mimi ninaokutana nao watupu ni akina mama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shirika la akina mama la Food Processing liko Dar es Salaam, Binti Nasibu ndiye Mwenyekiti wake. Tunawatafuta akina mama tunawahamasisha kusudi muanze viwanda vidogo na vya kati ili kusudi mkue mfundishe na wazazi wenu. Mama akipata kiwanda na wajukuu wanapata kiwanda, na mama zao wanapata viwanda nchi yote inakuwa ya viwanda.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na heshima kubwa ninayompa Mheshimiwa Mwijage, lakini nasikitika kwa majibu yake mepesi kiasi hiki na hii ndiyo inayothibitisha mawazo ya baadhi ya watu ambao wanafikiria kwamba mradi huu ukitekelezwa basi utakuwa umeathiri zoezi zima la kujenga viwanda katika nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, fidia ambayo Mheshimiwa Waziri anaizungumza hapa ililipwa zaidi ya miaka saba nyuma na mpaka leo bado eneo hilo liko wazi, hakuna hatua yoyote nyingine iliyopigwa baada ya ulipaji wa fidia.
Sasa swali la kwanza, kwa kuwa bado kuna malalamiko makubwa kwa waliohamishwa katika eneo hilo kwamba hii fedha shilingi bilioni 101 inayotajwa hapa inawezekana kabisa haikuwafikia waliostahili kufikiwa kwa maana ya waliohamishwa katika eneo lile na bado wanalalamika mpaka leo, je, Mheshimwa Waziri atakuwa tayari sasa kufungua milango ya majadiliano na wanaodai fedha hizi ili aweze kuona wapi zilipopotelea? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa sababu ni kwa muda mrefu Wizara imeshindwa kumpata mbia wa kuendeleza eneo hilo labda kwa sababu ya urasimu ambao upo kwenye Wizara, je, atakuwa tayari sasa kuwakabidhi Halmashauri ya Temeke ambayo iko aggressive zaidi kuona ule mradi unatekelezwa watafute mbia na waweze kuendeleza eneo hilo?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo fidia imelipwa siku nyingi na watu wote wamelipwa, ambao hawajalipwa ni watu watatu kwa sababu mtathmini hakufanya hakufanya kazi hiyo. Kazi niliyofanya, nimemuagiza DG wa EPZA aende kwa Mkuu wa Wilaya na Mamlaka ya Kata kusudi wakae na watu wao waweze kufidiwa. Wale watu hawakufidiwa kwa sababu mthamini hakuwathamini. Mimi nimeona busara hiyo na watu wamezungumza na mimi nimeagiza kwamba wafidiwe. Kwa hiyo, eneo lile liko tayari kwa ajili ya uwekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja kwamba eneo limekaa siku nyingi, inanirudisha kwenye historia, kazi ninayofanya ndiyo muhimu kwako kukueleza kwamba sasa kazi ninayofanya, eneo limetangazwa, wawekezaji wako tayari na ili uweze kujenga pale unafuata sheria za manunuzi na ndizo tunazozifuata. Hata Halmashauri yako ikija kujenga itafuata sheria za manunuzi. Lakini nikupe imani kwamba Kurasini ambalo ni eneo lako la Jimbo itakuwa sehemu nzuri ya viwanda lakini la muhimu kwa wale wenye mashaka na mimi ni kwamba bidhaa zitakazozalishwa pale zitauzwa kwa jumla, hazitauzwa Kariakoo wala Temeke. Lazima eneo lile litoe ajira na mafunzo kwa vijana wako wa Temeke na Tanzania kwa ujumla. Hayo ndio maslahi yako, maslahi yako ya viwanda iwe ajira mengine yatafuata baadaye.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na juhudi za Serikali na Wabunge wote tuliokuwepo katika Bunge lililopita katika kuhakikisha mradi huu wa Kurasini unatekelezeka; na kwa kuwa Serikali imetumia gharama kubwa katika kuwekeza mradi wa Kurasini Logistic Center; na kwa kuwa wananchi wa Temeke na Dar es Salaam kwa ujumla hususan wanawake na vijana tunatarajia kupata fursa kubwa sana za ajira katika eneo hilo la Kurasini Logistic Center; na kwa kuwa mimi kama Mjumbe wa PIC …
Je, ni lini sasa Serikali itaanza kutekeleza mradi ule? Nataka commitment ya Serikali.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ni bora nilieleze, mimi katika ofisi yangu katika Wizara ninayoiongoza, nimeanzisha mkakati unaoitwa fast-tracking of industrialization in Tanzania. Kuna mambo yanaendelea mimi sifurahishwi nayo, ukifuata sheria za manunuzi na mchakato wake ambazo Bunge tulipitisha shughuli hizi haziwezi kuanza. Mimi ningependa kuanza leo, wawekezaji ninao, nawajua lakini lazima nifuate sheria. Kwa hiyo, nitafuata fast-tracking na nimeamua sasa kwenda kwenye Baraza la Mawaziri, wakiniruhusu nianze kesho, nawahakikishia kabla ya mwezi wa tano nitakuwa nimeanza. Kwa hiyo, ni fast-tracking, mimi nakwenda kwa wakubwa zangu, Mawaziri wako hapa, waniruhusu naanza.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na kwamba demand ya Soko la Dunia ni ufuta mweupe, lakini Tanzania tumekuwa tukilima ufuta wa brown ambao bei yake inakuwa haina thamani kubwa kama ilivyo ufuta mweupe: Je, Serikali ina mpango gani wa kuweza kuwasaidia wakulima wa ufuta nao waweze kuanza kulima ufuta mweupe ili kuweza kuongeza kipato? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, ni juu ya Kiwanda cha Korosho kilichopo Lindi, Kiwanda cha TANITA ambacho kilikuwa kinaendeshwa na Serikali na kiliweza kuwapatia ajira wananchi wengi. Sasa hiki Kiwanda cha Korosho, TANITA, kimebinafsishwa ambapo hamna shughuli yoyote inayoendelea baada ya ubinafsishwaji huu na kupelekea wananchi kukosa ajira. Je, Serikali ina mpango gani juu ya kukifufua kiwanda hiki kutokana na kwamba Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano ni Tanzania ya viwanda? Ina mpango gani juu ya kufufua hiki kiwanda na viwanda vingine vingi vilivyoko Mkoani Lindi? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lathifah ameuliza swali lake la kwanza wakati muafaka; bajeti ya Wizara ya Kilimo inafuata nami nitamhimiza Waziri wa Kilimo kwamba tulete mbegu zinazozalisha ufuta mweupe ambao una soko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kiwanda cha korosho, Serikali ina mpango gani? Mpango wetu ni kuhakikisha kwamba viwanda vyote vilivyobinafsishwa vinafanya kazi. Hatuendi kwa kasi inayotakiwa kama nitakavyoeleza kwenye bajeti yangu kesho kutwa, ni kwa sababu viwanda vingine vina matatizo ya mikataba ya kisheria, lakini dhamira yetu ni hiyo na tutahakikisha viwanda vyote vinafanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na viwanda hivi, wako wawekezaji wanakuja na nitahakikisha Mheshimiwa Mbunge tunashirikiana kwamba Waheshimiwa Wabunge wanaokuja waende Lindi na nimeshazungumza hata na ndugu yangu, viwanda vingi vitakwenda vitaanzishwa ikiwemo na kufufua vile vya zamani.
MHE. ZAYNABU M. VULU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Swali langu ni kwamba, kwa kuwa Mkoa wa Pwani wanalima sana matunda ya aina mbalimbali na kwa kuwa kiwanda kipo eneo moja tu Mkuranga ambacho sasa hivi kinazalishana kiwanda kingine kinajengwa Chalinze. Je, ni lini Serikali itawashawishi wenye Kiwanda hicho kuhakikisha wanakuwa na maeneo maalum ya kuwasaidia wakulima kwenda kupeleka mazao yao na kuuza badala ya kutafuta magari na kupeleka mpaka kwenye kiwanda? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kiwanda cha Evelyne kinachokausha matunda asilia na Kiwanda cha Sayona kitakachochakata matunda ya aina zote, mara wanapoanza uzalishaji wataweka collection point. Evelyne wakati wowote atazinduliwa na kuanza kazi, mboga tunategemea aanze mwezi wa Tisa. (Makofi)
MHE. KHADIJA N. ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Serikali imekuwa ikiagiza tani laki nne za mafuta kila mwaka, wakati tuna malighafi za kutosha hapa nchini. Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia mazao hayo ipasavyo ili kuweza kuokoa fedha za kigeni zinazopotea kwenye kuagiza mafuta hayo nje ya nchi? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tunatumia mafuta tani laki nne kwa mwaka na 70 percent inaagizwa kutoka nje. Tunahamasisha ulimaji wa alizeti; tuna mpango wa kulima migaze au michikichi Kigoma na Pwani; pindi tutakapokuwa tumejitosheleza, tutaweza kuzuia mafuta kutoka nje. Hatuwezi kufanya makosa ya kuzuia mafuta kutoka nje, matokeo yake ni kwamba mafuta yatapanda bei.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kigoma wakiwa tayari, Pwani wakawa tayari na alizeti zikawa za kutosha, hatutazuia ugavi kutoka nje. Ugavi kutoka ndani utazuia mafuta yasije. Sisi ni member wa WTO na katika mpango wa WTO, bei ni nguvu ya soko inayomzuia mshindani asiingie kwenye soko letu.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa nchi za Uturuki, Ujerumani na Italy wanakunywa sana chai ya Tanzania. Je, ni lini Serikali itapeleka Kiwanda katika Wilaya ya Rungwe kwa ajili ya wakulima wa chai ili waweze kuuza chai yao ambayo ni nyingi ikaweza kusaidia katika hizo nchi nyingine?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo tulilonalo ni nguvu ya soko. Mheshimiwa Sophia tumeshazungumza kwenda kwenye maonesho ya Kimataifa kwenda kutafuta hayo masoko. Leta hizo order zako kusudi demand pool iwashawishi watu wachakate chai. Kuna watu wana chai hawana soko, sasa wewe nimeshakuruhusu uende kwenye maonesho. Nenda basi ulete hizo order. (Kicheko/Makofi)
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, namwomba Mheshimiwa Waziri awahakikishie wananchi wa Jimbo la Singida Mjini kwamba miradi hiyo aliyoitaja, miradi 33 iliyosajiliwa yenye kutoa ajira zaidi ya 4,000 itaanza lini?(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa Serikali imehamia Dodoma na yako Mashirika ndani ya Wizara, Ofisi za Kanda zipo Dodoma: Je, Mheshimiwa Waziri, sasa upo tayari Mashirika hayo kwa mfano TFDA, TBS na mengine kuanzisha Ofisi za Kanda Singida Mjini ili kuweka ufanisi wa kazi hiyo? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ile miradi 33 niliyoisema, nimesema kuanzia mwaka 1996 mpaka Aprili, 2017, miongoni mwa viwanda hivyo ni kiwanda cha mafuta cha Mount Meru, kimeshaanza kazi. Viwanda hivyo vimeshaanza kazi; na mojawapo ya viwanda hivyo ni Kiwanda cha Maziwa anachokijasiria Mheshimiwa Kingu. Tumeshaanza kazi. Tanzania sasa tunajenga viwanda. Sasa labda anieleze wapi anataka mimi nisukume kwa nguvu kusudi mambo ya nchi yetu yaendelee vizuri na yeye yamnyookee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuanzisha kanda za TBS na TIRDO, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba hakuna tija kuwa Dodoma ukaanzisha Branch Singida, kwa sababu unaweza kuondoka asubuhi ukafanya kazi Singida, ukarudi hapa, ukarudi tena, ukarudi tena. Kwa hiyo, itabaki Dodoma na itakuwa rahisi hata Mheshimiwa Waziri kwenda na Mheshimiwa, rafiki yake wakaweza kuhamasisha shughuli za viwanda.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuelekea kwenye nchi za viwanda; na ninavyofahamu mimi ili twende huko, lengo kubwa ni kuchakata mazao yanayolimwa hapa nchini; lakini kama ambavyo swali namba 206 lilivyojibiwa, sijaona mkakati unaowekwa kwenye zao la ufuta. Ni namna gani Serikali imejipanga kutangaza ili tupate wawekezaji kwenye kusindika mazao ya ufuta?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua haya maneno ya mkakati na vipaumbele yanaleta shida. Nilivyosema kwenye swali la msingi Na. 206 nimesema, viwanda vidogo na viwanda vya kati ni viwanda tunavyoweza kuvimudu. Nikaenda zaidi nikasema sisi Waheshimiwa Wabunge tuwe wa kwanza, kwa sababu sisi ni watu ambao tunafuatwa na watu, ni influential, ukianzisha kiwanda wewe cha shilingi milioni 200, watu wa kwenu wote wakianzisha viwanda, viwanda vitatekelezwa. Ndivyo hivyo nilivyosema.
MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa Mkoa wa Tanga ni miongoni mwa Mikoa ambayo imetenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji. Je, Serikali ina mkakati gani ya kufufua na kuwekeza viwanda vipya? Ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningekuwa na uwezo hili swali nisingelijibu, kwa sababu Mheshimiwa Mbunge ananilazimisha nisome hotuba ya bajeti yangu kabla ya muda na shughuli ni kesho kutwa. Nimejipanga kwa ajili ya Tanga na Jumatano nitawaonesha. (Makofi)
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Waziri, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Mheshimiwa Waziri pale manonga tuna Kiwanda cha kuchambua pamba cha siku nyingi ambacho kina utata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuja tukaongea na Mheshimiwa Waziri, akatuahidi kumwita Rajan na Igembensabo ili kuja kutatua tatizo hili na hatimaye kiwanda hicho kiweze kufanya kazi ili wananchi wa Igunda waweze kupata ajira na sehemu rahisi ya kuuza pamba zao. Je, Mheshimiwa Waziri amefikia wapi kuwaita watu hao ambao alituahidi kuwaita hapa Dodoma ili kuja kupatanao mwongozo ili tuweze kujua tunaanzaje kuhusu kiwanda kile cha Manonga Ginnery? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Mkoa
wa Tabora umekuwa na adha kubwa ya ukosefu wa viwanda; na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara alituahidi kwamba amepata mwekezaji Mchina wa kiwanda cha kujenga Tumbaku Tabora; na lilitokea tatizo pale Airport hatimaye yule mwekezaji hakuweza kuja Tabora kuongea na sisi ili kuweza kujenga Kiwanda hicho cha Tumbaku. Je, Mheshimiwa Waziri, mpaka sasa status ya mwekezaji huyo ambaye alikuwa anakuja Tabora akapata matatizo Airport imefikia wapi? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kujadiliana na Rajan juu ya Manonga Ginnery. Tatizo ninalolipata kuhusu Rajan, aliyerithi kiwanda yuko nje ya nchi. Kwa hiyo, nawasiliana naye kupitia mtu wa kati, lakini naomba mwendelee kunikumbusha, mwendelee kunishinikiza kusudi tuweze kufikia suluhu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaonekana hawa Rajan hawana interest tena na kiwanda na hawako tayari kununua na mwendelee kuwapa shime watu wa Igembensabo waendelee na nia hiyo, tutafikia muafaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la tumbaku; sina mpango tena na yule Mchina ila natafuta wawekezaji wengine wa kuweza kuwekeza kwenye zao la Tumbaku kwa kujenga Kiwanda. (Makofi)
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, suala la zao la pamba na usindikaji wake au kuongeza thamani ni suala la msingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Busega kuna vinu ambavyo ni vya viwanda vya Pamba kama cha Ngasamo na Sir Ginnery. Maeneo yote haya yamekuwa na viwanda ambavyo vimesimama, havifanyi kazi na hivyo kupelekea wananchi wengi na wakulima wa pamba kushindwa kuuza pamba yao kwa bei yenye kuongeza thamani. Je, Mheshimiwa Waziri ana mkakati gani? Pamoja na suala la Manonga na kwingineko ambako kuna viwanda ambavyo havifanyi kazi vizuri, kama Serikali kuna namna gani ya kuweza kuboresha viwanda hivi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, chanda chema huvikwa pete. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wanaotoka kwenye eneo la pamba, nenda kwenye mkakati wa pamba mpaka mavazi, ukurasa wa 91 majibu yote yako pale. Tutaweza kufaidika na pamba kama zamani, soko litakapokuwa linaweza kuvuta (the demand pull) na mojawapo ya mambo ya kufanya ni kuongeza ufanisi katika zao la pamba. Mwaka 2016 kwa kutumia ways and measures baada ya ku-control watu wasichafue pamba, nyie ni mashuhuda bei imepanda kidogo, tutaendelea na nikuahidi Mheshimiwa Mbunge tukitoka hapa nitakupa huo ukurasa namba 91 nilikuja nao nilijua itajitokea uone mambo mazuri. The productivity, pamba ina tatizo kwa sababu hakuna tija katika uzalishaji.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa mikoa ambayo ilikuwa na viwanda vingi sana. Baada ya ubinafsishaji, viwanda vingi vimekufa na vingine vimegeuka kuwa ma-godown. Je, Serikali ina mpango gani wa uhakikisha inafufua viwanda hivi viweze kutoa ajira kwa wakati wa Mkoa wa Morogoro? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Devotha nawe umewahisha shughuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, isionekane mimi ni bingwa wa kukwepa maswali, Mheshimiwa Devotha hakuna kiwanda kitabaki godown Morogoro. Tajiri namba moja alisimama Morogoro na microphone, akasema kama ningekuwa na Waziri wa Viwanda, Viwanda vya Morogoro vingefanya kazi, alikuwa ananisema mimi. Viwanda vyote unavyovisema, vinafanya kazi sasa. Kiwanda cha Canvas kitaanza ku-role Kiwanda cha MOPROCO kitaanza kutengeneza mafuta nami mambo yataendelea kuninyookea. (Kicheko/Makofi)
MHE. SAADA SALUM MKUYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa maelezo yake, lakini Mheshimiwa Waziri najua kwamba karafuu ya Zanzibar ndiyo Karafuu ambayo ni quality duniani kote. Je, Wizara ya Biashara na Viwanda ya Tanzania ina mkakati gani kushirikiana na Wizara ya Biashara na Viwanda ya Zanzibar kuhakikisha kwamba tunajenga kiwanda ambacho kita-absolve karafuu ya Zanzibar kwa ajili ya kutengeneza products, kusafirisha nje lakini vile vile kupatia vijana ajira kama ambavyo tunaelezwa na ndiyo mategemeo yetu?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu Zanzibar ilikuwa ni kwamba Makatibu Wakuu wa Wizara ya Viwanda Zanzibar na wale wa Tanzania kwa upande wa Bara wakutane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda nitoe maelekezo kwamba wanapokutana sasa, kwa sababu najua wananisikiliza; na suala la Karafuu na Kiwanda na lenyewe waliunganishe walete majibu hapa tuweze kupata suluhu ya kutengeneza Kiwanda Zanzibar. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu yaliyo chini ya kiwango ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Saed Kubenea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza liliuliza kwamba mpaka sasa kasi ya kufufua viwanda imefikia wapi?Kwa hiyo, kwa majibu hayo inahitaji tujue kwamba Waziri yuko tayari kukiri kwamba kiwanda hiki hana mpango wa kukifufua kwa maelezo aliyotoa hapa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mpaka sasa anaamini kwamba kauli mbiu ya Serikali ni kuinua viwanda au kuua viwanda? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya Serikali iliyofanyika imeandikwa kwenye jibu langu ni kufanya utafiti; na mwaka jana nilipewa shilingi milioni 150 kwa ajili kufanya utafiti na umakamilika kwa hiyo kazi niliyopewa nimemaliza. Kazi ya Serikali ni kujenga viwanda na viwanda vitaendeshwa na Sekta binafsi, mwaka unaokuja 2017/2018 nimeomba pesa shilingi milioni 70 tu nitangaze tender sekta binafsi ifanye kazi.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Naomba kwanza nitambue jitihada ambazo Serikali imefanya kwa kuona umuhimu wa kufufua viwanda hivi Naomba niulize maswali yafuatayo.
Mheshimiwa Spika, mkataba umesainiwa Machi, 2017 na tunategemea kufanya uzalishaji mwezi Septemba mwaka huu, takribani itakuwa miezi tisa. Naomba nifahamu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, mpaka sasa hivi taarifa nilizonazo ndani ya kiwanda kile kuna mashine zisizopungua 30 zimeshawekwa na mashine hizi ni za manual (za mikono). Sasa nataka nijue mashine hizi ni hii Kampuni ya Sunshine ambayo imeingia mkataba au ni watu wengine ambao wamezileta hizi mashine? Muhimu nilikuwa nataka nijue ambao watu wa Nachingwea wanaufanya.
Mheshimiwa Spika, lakini swali lingine sambamba na hilo, nataka nipate majibu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, majengo ya kiwanda kile cha korosho mpaka sasa hivi yako chini ya Lindi Pharmacy na yanatumika kama maghala ya kuhifadhia korosho. Je, kiwanda hiki ambacho Wachina wamefanya mkataba nacho ni kiwanda gani ambacho kinaenda kujengwa na kinaenda kujengwa maeneo gani?Au ni majengo yale yale yatatumika?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, napenda nikiri, maswali aliyoniuliza ni undani wa MOU na mimi sijaisoma. Kwa hiyo, nitakwenda kwenye MOU niweze kujua undani wa nani anamiliki nini na nani atapata nini.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa madini haya ya jasi
(gypsum) yako mengi sana katika nchi hii hasa Itigi, Msagali maeneo ya Mpwapwa na maeneo mengine. Baadhi ya nchi ambazo zinatuzunguka hazina madini haya ya jasi ikiwemo Congo, Rwanda na Burundi. Je, Serikali itasaidiana na wajasiriamali na wachimbaji wadogo hawa wa jasi kuwapatia masoko katika nchi hizi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa viwanda vya cement vinatumia malighafi hii ya jasi kutengenezea cement lakini sasa kuna baadhi ya viwanda ambavyo vimewekezwa nchi hii vinaagiza clinker moja kwa moja kutoka nchi za Ulaya na Asia. Je, Serikali sasa iko tayari kuhakikisha viwanda vya cement ambayo vitawekwa baadaye vinafanya processing hapa hapa nchini ikiwemo kujenga matanuru ambayo jasi itatumika? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kuhusu kusaidia wawekezaji waweze kutosheleza viwanda vya ndani na ku-export jasi hiyo ni sehemu ya shughuli yangu. Mheshimiwa Mbunge tutakutana tuwa-organize vijana tuweze kuwaongoza kwenda sokoni. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu kuagiza clinker kutoka nje napenda niliambie Bunge lako Tukufu kwamba, uwezo uliosimikwa wa viwanda vya Tanzania vyenye uwezo wa kuzalisha cement tani milioni kumi na laki nane kwa mwaka tuna uwezo wa kujitosheleza clinker. Hata hivyo, jambo moja la kufurahisha, wenye viwanda vyote 11 walikutana Dar es Salaam chini ya Uenyekiti wa Dkt. Meru, Katibu Mkuu wangu na wakakubaliana wao kwamba watapeana clinker yenye viwango na yenye bei nzuri. Hakuna haja ya kuagiza nje wakati clinker inapatikana hapa.
MHE. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Spika, namshukuru Waziri kwa majibu aliyoyatoa. Majibu ambayo mimi na wananchi wa Newala wanaomsikiliza, yametukatisha tamaa kwa sababu swali la msingi halijajibiwa.
Mheshimiwa Spika, swali langu nimeuliza, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha viwanda hivi vinafanya kazi? Ndiyo swali la msingi, lakini majibu ya Mheshimiwa Waziri yanaeleza, mwekezaji atafanya hiki, atafanya hiki. Tangu miaka 14 huko nyuma; tumesubiri miaka 14, bado Serikali inaridhika na maelezo yake, atafanya hiki, atafanya hiki, atafanya hiki.
Mheshimiwa Spika, nataka nikwambieni Serikalini, hawa watu waliochukua viwanda vya Newala walivigeuza kuwa warehouse stores wakavikodisha. Hiyo shilingi milioni 75 waliyolipa imerudi siku nyingi.
Mheshimiwa Spika, sasa swali langu la kwanza, Mheshimiwa Waziri: kwa kuwa, huyu mtu ameshindwa kutekeleza mkataba baina yake na Serikali kwa zaidi ya miaka 10; na kwa kuwa kuna watu wengi waliokuja Newala kuomba wanunue kiwanda hiki. Je, sasa Serikali iko tayari kumnyang’anya kiwanda hiki na kuwauzia watu ambao wakipewa leo leo wanaanza kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kile Kiwanda cha Newala II ni kweli kinafanya kazi na tunamshukuru kwa hapo alipofika, lakini kiwanda kile nimekitembelea, kuna matatizo makubwa mawili; moja maslahi ya wale akinamama wanaobangua korosho pale; pili, hawana hata gloves, zile zana za kufanyia kazi ya kubangua korosho. Je, Serikali iko tayari kumtuma wiki hii Mkaguzi wa Viwanda aende Newala akakague mazingira wanayofanya kazi akinamama wa Newala wanaobangua korosho? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, nianze na swali la pili ambalo ni rahisi. Nachukua fursa hii kutoa maelekezo kwa Maofisa wa Serikali wanaohusika na usalama viwandani watembelee viwanda vyote, siyo vya korosho tu, ili wahakikishe kwamba mazingira ya kufanya kazi ni salama na kazi zile ni za staha, ndiyo maelekezo ya Serikali. Kwa hiyo, fanyeni kazi OSHA, wote mnaohusika, fanyeni kazi na mtoe ripoti watu wafanye kazi za staha.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, maagizo ya Serikali kupitia Mpango wa Miaka Mitano ni kwamba viwanda vyote lazima vifanye kazi. Katika operation ambayo nimeiandika humu, viwanda vyote viko chini yangu sasa. Kwa hiyo, tunahakikisha kila kiwanda kinafanya kazi. Watu wa Newala wanaotaka viwanda vya korosho, waende kwa Msajili wa Hazina kama ni kutaka viwanda.
Mheshimiwa Spika, niwahakikishie, mwaka huu viwanda vyote vinafanya kazi. Nimweleze Mheshimiwa, wamekuja watu wengi waliokuwa na viwanda kueleza kwa nini hawafanyi kazi na nimewapa maelekezo. Mnihurumie, mnipe miezi miwili nifanye kazi iliyoshindikana miaka 14.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ufufuaji wa viwanda vya korosho kwa Ukanda wa Kusini ni ukombozi mkubwa kama ufufuaji huo utafanyika kama ulivyokusudiwa. Kama lilivyoulizwa swali la msingi, ufufuaji huo hasa kwa wale wawekezaji waliopewa viwanda hivi, tunadhani wanafanya chini ya kiwango.
Mheshimiwa Spika, mfano mzuri ni kiwanda cha Kubangua Korosho cha Mtama. Sisi Wanamtama haturidhiki na mwekezaji alivyowekeza na kukiendesha kile kiwanda. Tunaamini anafanya chini ya kiwango ambacho alitakiwa kufanya. Sasa Serikali iko tayari kwenda kufanya ukaguzi kujiridhisha kama uwekezaji ule ndiyo waliokubaliana naye?
Kama siyo, wako tayari kuvunja na kumpa mtu mwingine ili tufaidike na uwekezaji wa viwanda vya korosho na hasa kiwanda chetu cha korosho cha Mtama?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge na Wadau wote wa korosho katika mikoa 11 inayolima korosho. Korosho imewekwa katika mazao ya kipaumbele matano ya kimkakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo maelekezo kutoka kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu; mimi na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo tunafuatilia. Navijua viwanda vyote kwenye ncha ya vidole, najua tasnia nzima ya korosho; nimezunguka dunia nzima natafuta masoko ya korosho. Siyo viwanda tu, najua tatizo la industry. Wataalam wangu wako site kwenye viwanda vyote 10 tunafuatilia. Nina mawasiliano ya mtu mmoja mmoja.
Mheshimiwa Spika, kwa mamlaka niliyonayo, watu wa Treasury Registrar, mtuletee majibu nije nikae na watu wa Newala na watu wa Lindi, nije niwaeleze kwa nini kiwanda hiki kinakwama? Suala siyo kiwanda kuanza, suala ni kiwanda kuwa endelevu. Kuna mambo zaidi katika tasnia ya korosho na ndiyo tunayahangaikia.
Mheshimiwa Spika, mojawapo ya mambo ya msingi nimezungumza. Nimezungumza mambo ya branding humu, tunapigana kutengeneza brand ya korosho ya Tanzania. Brand ya korosho huwezi kuitengeneza mpaka uzalishe wewe mwenyewe. Tunafanya kazi, lakini kwa Newala na Lindi nimewaagiza wataalam.
Mheshimiwa Spika, kwanza mwekezaji aliyechukua Kiwanda cha Mtama nimweleze Mheshimiwa Mbunge, yuko tayari kukiachia yeye mwenyewe. Kwa hiyo, nawaagiza wataalam wangu waje Jumanne watueleze. Yule mwekezaji, yeye si anataka kukiachia, tumemwambia aje akiachie, tusaidiane na Mheshimiwa Mbunge ili tutafute mwekezaji mwingine.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa SIDO ndiyo mlezi wa viwanda vidogo vidogo pamoja na vya kati ambapo tunatarajia viwanda hivi viweze kuelekea katika kuwa viwanda vikubwa na hivyo kuweza kuwezesha uchumi wa viwanda kuendelea hapa nchini Tanzania na Waziri amekiri kabisa kwamba Serikali inalitambua hilo na imekuwa ikitenga fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, utakubaliana na mimi kutenga fedha na kupeleka fedha ni kitu kingine. Kwa taarifa nilizonazo kabisa ni kwamba Serikali kwa mwaka 2015/2016 ilitenga shilingi milioni 500; mwaka 2016/2017 Serikali ilitenga shilingi bilioni 2.4; na kwa mwaka 2017/2018 kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, Serikali imetenga shilingi bilioni 7.14.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pamoja na kutenga fedha hizi zimekuwa haziendi. Kwa maana hiyo, tunategemea nini?
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kauli mbiu ya viwanda ambayo tumeona Mheshimiwa Rais amekuwa akiisema kweli itaweza kutimia kwa mwenendo huu wa kutokupeleka fedha? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wanawake wa Mkoa wa Mwanza wamekuwa wakijishughulisha na shughuli za viwanda vidogo vidogo, lakini changamoto kubwa waliyokuwanayo ni kukosekana kwa vifungashio ambavyo wanavipata kwa gharama za juu sana na hivyo kushindwa kujiendeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua kwamba Serikali inawezaje kuwasaidia wanawake wa Mkoa wa Mwanza ili waweze kupata kiwanda cha vifungashio ili waweze kujikwamua kiuchumi? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nikiri na ninakubaliana naye. Ujenzi wa uchumi wa viwanda endelevu unatokana na viwanda vinayoitwa LGI (Local Grown Industries) siyo hizi FDI. Hawa wanatafuta green pasture, wataondoka na Serikali inalitambua hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 tulipaswa kupewa shilingi bilioni 2.4, hatukupewa. Tumeiomba Serikali tupewe shilingi bilioni 7.04; nina imani Serikali itatoa pesa hizo na ninazifuatilia. Napenda niishie hapo na Kamati yangu imefanyia kazi na tusipotoa pesa hizo, hivi viwanda tunavyoita FDI, hao ni kware. Huwezi kulisha kware ukawaacha watoto wa kuku. Naomba niishie hapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la vifungashio ni tatizo kwa wajasiriamali wadogo wote. SIDO tumeamua kuwekeza katika kiwanda cha vifungashio na hicho kitatoa vifungashio kwa akina mama wote na wajasiriamali wadogo. Nachukua firsa hii kuwahimiza wajasiriamali wanaoweza kuwekeza kwenye biashara hii wawekeze katika vifungashio. Tunatumia pesa nyingi za kigeni kuagiza vifungashio kutoka nje ya nchi.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshmiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa masoko ya nje yanatawaliwa sana na ubora wa mazao na kwa kuwa wanunuzi wa tangawizi kule nje wanapenda sana organic ginger. Sasa Serikali ina mpango gani wa kupeleka elimu kwenye zile sehemu ambazo zinalima sana tangawizi kama vile Mkoa wa Kilimanjaro, Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Ruvuma?
Mheshimiwa Spika swali la pili, kwa kuwa Kiwanda cha Tangawizi cha Mamba Miamba kilichopo Wilayani Same kinategemea kuanza kusindika tangawizi ya kupeleka nje ya nchi katikati ya mwaka 2018.
Je, Serikali itatumia njia gani kuwafanya wananchi ambao wamekata tamaa kulima tangawizi kutokana na bei kushuka sana ili waendelee kulima tangawizi kwa sababu kiwanda hiki cha Mamba Miamba kitahitaji malighafi kwa wingi? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, kwa idhini yako napenda nichukue fursa hii kumtambua Mama Malecela kama Malkia wa Tangawizi. Suala la tangawizi amelifanyia kazi sana. Nichukue fursa hii kushukuru Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambayo ameshughulikia pacha wangu, zimetengwa pesa nzuri zaidi ya shilingi bilioni
• kusudi hicho kiwanda kiwe na hadhi ya Kimataifa, kizingatie ubora kama nilivyoeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu maswali mawili uliyoniuliza, moja la ubora, Wizara yangu inayosimamia SIDO kwa kutambua suala la viwango, maeneo yote ninaojenga sasa katika mikoa yote mipya tunajenga ofisi za SIDO, sheli, maabara, mahali pa kuchakatia chakula kwa viwango vitakuwa ni kipaumbele; Katavi, Rukwa, Geita, Simiyu ndiyo nakwenda kuanza nalo na pesa tayari ninazo kama nilivyoeleza juzi. Kwa hiyo, nitawafundisha wananchi hasa akina mama kuzalisha vyakula kwa viwango vya kuuza Kimataifa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa suala la pili kwamba tutafanyaje, ndiyo tangawizi ilikuwa inauzwa Sh.3,500 najua leo bei imeshuka, sawa sababu mojawapo ni muanguko wa bei za bidhaa, commodity price duniani zote zime-dive. Tutafanya nini?
Kazi ninayofanya sasa ni kutafuta masoko makubwa, masoko mengi ya Kimataifa ile demand pool iwawezeshe wananchi wetu waweze kuuza zaidi lakini zaidi kupitia ESDP II tutaongeza tija (productivity) katika uzalishaji kusudi watu walime sehemu kubwa kwa gharama ndogo ile productivity iweze kupeleka hiyo tangawizi. Kwa sababu kiwanda chako hakina mfano, tangawizi yote itakwenda Mamba, ichakatwe, tupeleke Bandari ya Tanga iende duniani kuuzwa.
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tatizo la Mheshimiwa Mama Kilango linafanana na tatizo lilipo kwangu kuhusiana na mbaazi ambapo wananchi wengi wamelima mbaazi kwa wingi na walihamasishwa kwamba kuna soko kubwa kule India.
Naomba Serikali itoe tamko ni lini mbaazi zile ambazo wananchi wanazo kwa wingi zitaanza kununuliwa?
WAZIRI WA VIWANDA, BISHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, ningekuwa na uwezo hili ndiyo swali ambalo ningependa nisiulizwe leo. Tunalo tatizo la mbaazi, Mheshimiwa Modi, Waziri Mkuu wa India alikuja hapa na akatuhakikishia soko la mbaazi nchini kwake, wananchi walisikia na mimi siwezi kukana nilikuwa mojawapo ya watu waliowahamasisha wananchi walime mbaazi na wamelima. Kilichotokea kwa maandishi, Serikali ya India imetuandikia barua kwamba haitanunua mbaazi zetu.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais akanituma India, nimekwenda India na vielelezo kwamba kulingana na mkataba wa tarehe 14 Januari 2000, Tanzania na India tulikubaliana kwenye suala hili mnapaswa mnunue mbaazi zetu. Tukazungumza vizuri na Serikali ya India wakapitia makabrasha yao wakaona kweli kuna haja ya kununua mbaazi zetu. Wakatuuliza takwimu tunazopaswa kupeleka kule, nikaangalia takwimu mara ya mwisho tulikuwa tumepeleka tani 280, tukakisia kwamba tutawaletea tani 300, nikatoka na bashasha na nderemo narudi nyumbani.
Mheshimiwa Spika, baada ya kufika hapa yule Waziri wa Biashara akapandishwa cheo na kuwa Waziri wa Ulinzi ikabidi nifanye kazi sasa ya kuanza kujenga urafiki na Waziri mpya kumueleza katika makabidhiano waweke suala langu. Hapa nilipo kila siku nimeweka Afisa Mkurugenzi anayewasiliana na India kuangalia kitu gani kinachoendelea.
Mheshimiwa Sapika, katika nchi nyingine, watu wako sensitive na watu wao, kilichotokea India walikuwa wana deficit ya tani milioni tano za mbaazi sasa wananchi wao wamelima wame-bridge ile gap na wananchi wa India Serikali haifanyi lolote mpaka iwafikirie wao. Mimi sifanyi protectionism, lakini na mimi nataka kuangalia watu wangu, masoko yangu yanakuwaje ndiyo maana naweza nikafanya mambo mengine mtu anasema Mwijage unakurupuka, hapana, naagalia maslahi ya wakulima wangu na ndiyo maana mimi naonekana kama mtu wa korosho na mimi naangalia korosho zangu ziende namna gani.
Mheshimiwa Spika, hili ndiyo tatizo lililotupata kwenye mbaazi na nalifuatilia na napozungumza Bwana Gugu, Mkurugenzi wa Biashara ya Kimataifa kabla ya saa 6.00 unieleze huyo mhindi ameshasema kitu gani. (Makofi/Kicheko)
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa jibu la Mheshimiwa Waziri lakini halijanipa faraja hata kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ina fursa nyingi, kuwa mazao mengine sasa hivi hayajajitosheleza, ni kwasababu hakuna masoko, lakini fursa zipo. Sasa hivi hayo maeneo tuliyotenga, nilimuita Meneja wa SIDO Mbeya, alikuwa hajawahi kufika Ileje hata siku moja. Amekuja pale akatuambia tengeni eneo, hakutupa viwango, tutenge eneo kiasi gani? Hakutupa maelekezo yoyote. Miaka miwili imepita, wala hajarudi tena kuangalia kitu gani kinaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna fursa kubwa sana ya viwanda vidogo vya usindikaji wa nafaka. Tunalima mahindi mengi, karanga nyingi na ulezi mwingi. Hivyo ni vitu ambavyo tunaweza kuanzia kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnaposema sisi tutayarishe miundombinu yote wezeshi, kwa uwezo gani wa Halmashauri zetu masikini watu wa pembezoni kama sisi? Nini maana ya ile Sera ya Kuendeleza Viwanda ya 1996 mpaka 2020 inayosema mtapeleka viwanda nchi nzima na mtakwenda mpaka maeneo ya pembezoni? Sisi ndio watu wenyewe wa pembezoni, mnakuja lini kutusaidia kuweka viwanda? Msituachie huo mzigo wa kutengeneza miundombinu, hatuna uwezo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, lini Mawaziri watakuja Ileje? Naomba Mheshimiwa Waziri wa Afya, Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo waje Ileje. Mkija mkajionea wenyewe hali halisi ndiyo mtajua majibu ya kutupa humu ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, naelewa na ninaweza kusikia uchungu alionao Mheshimiwa Mbunge kuhusu Wilaya yake na hasa kuhusu maeneo ya pembezoni. Nianze na lile swali ambalo ni rahisi. Nimeshapata mwaliko kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Katavi na Rukwa. Tarehe 6 Agosti, nitakwenda kutembelea mikoa hiyo tukiwa pamoja na shughuli za Nane Nane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sera ya Viwanda (Sustainable Industrial Development Strategy) ya mwaka 1991 – 2020 katika jibu langu nimeeleza, tumegundua mwendo usio sawa katika viwanda vinavyoenea Wilayani. Kutokana na hiyo na kwenye jibu langu nimeeleza na kwenye bajeti yangu nimeeleza, ndiyo maana tunatengeneza mwongozo. Huo mwongozo utaweza kuwasukuma Watendaji wetu wafuate kama mwongozo unavyosema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge, nikuhakikishie nitafanya kazi na wewe na kuhusu suala la tangawizi tuanze shughuli hapa. Nenda kamfuate Mheshimiwa Mama Kilango akueleze alifanyaje kufufua Kiwanda cha Tangawizi na amepata wapi zile pesa shilingi bilioni 1.7 za kuendesha kiwanda cha Same? Akuelekeze, tuanzie hapo. (Makofi)
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami napenda kuuliza swali moja la nyongeza kwa Mheshimiwa Mwijage. Mkoa wa Mtwara na hasa Manispaa ya Mtwara na Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara tayari tumeshatengeneza Master Plan na tumeshatenga maeneo kwa ajili ya viwanda. Tunayo EPZA, lakini tunayo maeneo ambayo hayahitaji fidia wala nini. Wizara yake inasaidiaje huo mkoa kuhakikisha kwamba na wenyewe unakuwa wa viwanda kwa sababu fursa zote zipo? Gesi, bandari, mazao kama korosho yapo. Je, Wizara yake ina mkakati gani wa kusaidia Mkoa wa Mtwara? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo. Nina taarifa kwamba tarehe 2 Mei, 2017 Master Plan ya Mtwara ilikamilika. Kilichobaki au jukumu nililonalo na Wizara yangu ni kuendelea na jitihada za uhamasishaji. Nimeshaanza uhamasishaji Mheshimiwa Mbunge, juhudi zako za kunipa kwanja cha bure kwa ajili ya kujenga Kiwanda cha Sulphur siyo kwamba nimenyamaza, tunapambana kuweza kuwaleta hao wawekezaji. Niseme kilichobaki ni uhamasishaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara naendelea kuhamasisha, iko kwenye ramani yangu, ni eneo ambalo liko tayari kwa ajili ya uwekezaji. Wawekezaji watakuja Mtwara.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wapogoro tunajulikana dunia nzima kuwa chakula chetu kikubwa ni wali na kambale, kwa kuwa Ulanga tunalima sana mpunga.
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kujenga kiwanda ili sasa wakulima wasiuze mpunga wauze mchele ili kuwaongezea kipato? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vya kukoboa mpunga ni viwanda vidogo na viwanda vya kati. Ni viwanda vyenye thamani kati ya shilingi milioni tano mpaka shilingi milioni 200.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakachofanya kwa ajili ya wajomba zangu, ni kuwahamasisha wananchi. Matajiri wa shilingi milioni 200 tunao, badala ya kuwekeza kwenye malori, ni kununua dryer. Nitoe taarifa, kwa nini mchele wetu wa Tanzania unakataliwa nje? Ni kwamba tunashindwa ku- control moisture content. Nimeshamweleza hata rafiki yangu pale Mheshimiwa anayependa kula sana pepeta, nimeshamweleza kwamba control moisture content. Kwa hiyo, moisture content inauzwa dola 50,000, kinu kinauzwa dola 100,000. Tunaweza kufanya hivyo.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nitasaidiana na wewe na tulishafika pazuri, sitaki kukurudisha kwenye historia; tutaweza kuhamasishana. Hivi viwanda vya shilingi milioni 200, shilingi milioni 300 au shilingi bilioni moja, msitafute wageni, tunavimudu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amezungumza hapa, ziko benki, tunavimudu na tutawasimamia. Ndio nyie wenye kuwekeza. Wale wengine watakuja baadaye, lakini watu wa kuwekeza ni sisi. (Makofi)
MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri swali la nyongeza.
Katika bajeti iliyopita Mheshimiwa Waziri alituahidi wananchi wa Jimbo la Handeni Vijijini kuweza kupata Kiwanda cha Matunda katika Kata ya Kwamsisi na mpaka hivi leo bado wananchi wa Jimbo la Handeni Vijijini wana matumaini makubwa na hakuna ambalo limefanyika. (Makofi)
Je, Mheshimiwa Waziri mko katika hatua gani ili kuweza kuwawezesha wananchi wa Jimbo la Handeni Vijijini kupata kile kiwanda ambacho mlituahidi? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo, Mradi wa Kiwanda cha Matunda Handeni bado upo. Mwekezaji ambaye anawekeza kiwanda, anayelima Bwana Roy Nightingale ameshaanza kuzalisha ndizi kwa ajili ya kiwanda hicho. Sasa ndizi zake zinauzwa kwenye Kiwanda cha Elven.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nisamehe kitu kimoja, niwaelezee kiwanda cha Elven. Kiko kiwanda kinakausha matunda na matunda hayo yanauzwa Ulaya, kiko sehemu ya Bagamoyo juzi nimekikagua pamoja na Mkuu wangu wa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania mpaka ninapozungumza hatuwezi kutosheleza kiwanda hicho kwa matunda. Kwa hiyo, wakati matunda yenu mtayauza Bagamoyo, Kiwanda chenu cha Nightingale, mwekezaji binafsi kinaendelea. Ni matatizo ya kifedha lakini nitaendelea kusimamia na wewe tushirikiane, kiwanda hicho ningependa kuona kinajengwa na kufanya kazi. (Makofi)
MHE. SAVELINA S. MWIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa Mkoa wa Kagera una ardhi kubwa ambayo inatumika hata kwa kuingiza wafugaji haramu na majambazi na kwa kuwa wewe Mheshimiwa Waziri ni mzaliwa wa Mkoa wa Kagera.
Ni lini utaiona Kagera kuweka viwanda angalau vya kuchakata kahawa, majani na vyakula mbalimbali ili tukajivunia kwamba tumekuwa na Waziri wa Viwanda na Masoko? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unitendee haki. Naulizwa mara ya pili swali hili. Mimi ni muumini wa Muammar Gaddafi, alianza kujenga mbali na kwao, akamalizia kwao.
Kuhusu Kagera, mapping ya viwanda Kagera, naomba nitoe jibu. Kagera ina fursa ya kujenga viwanda vya maziwa. Kinachofanyika sasa, tunatafuta mwekezaji wa kuweka Kiwanda cha Maziwa ili sasa soko lije livute uzalishaji. Tulikuwa na ufugaji wa ng’ombe, hatukufanya vizuri, sasa tunatafuta wawekezaji waweke viwanda vikubwa vya maziwa, ni rahisi kwa uoto wa Kagera kuweza kufuga ng’ombe wa maziwa, mkapata maziwa na by product.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikueleze, wapo vijana wajasiriamali na tumeshawaelekeza mahali pa kwenda kusudi waweze kujasiria. Shangazi usiwe na wasiwasi siwezi kuwa ngariba wa Kilwa. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mkoa wa Rukwa tunalima sana mazao ya chakula na sasa ni msimu wa mavuno… (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mkoa wa Rukwa tunalima sana mazao ya chakula na sasa ni msimu wa mavuno, lakini wananchi wa Mkoa wa Rukwa mpaka sasa hawajapata soko la uhakika la kuuza mazao yao wala kiwanda hakipo. Ni lini kiwanda kikubwa kitajengwa Mkoa wa Rukwa ili kiwanufaishe wakulima hao?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili swali limejirudia. Viwanda anavyovizungumza, Viwanda vya Asali, vya Ulezi, vya Mahindi ni viwanda vidogo, vya kati na viwanda vikubwa. Kiwanda alichokijenga Mheshimiwa Aeshi chenye thamani ya dola milioni za Kimarekani, ni kiwanda kikubwa.
Kwa hiyo, ninachokwambia, tuhamasishane sisi tujenge viwanda. Msitafute mtu kutoka nje aje achume sisi tumeshahangaika. Viwanda hivi vya shilingi milioni 400 au shilingi milioni 500 tunavimudu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaeleze, itafika wakati tutaweza kulazimishana mtu asitoe mahindi Rukwa kuyapeleka Dar es Salaam, tengeneza product, zi-brand; regional branding. Brand unga wako kule upeleke mjini chakula, msipeleke ajira mjini. Ndivyo nilivyozungumza kwenye bajeti yangu na tukubaliane tuanze, hatujachelewa.
Mheshimiwa Aida, kiwanda kidogo cha shilingi milioni 500 unakimudu. Kama hujui fursa uliyonayo, njoo nikuelekeze namna ya kuzipata.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wilaya ya Mbulu ni miongoni mwa Wilaya kongwe hapa nchini. Wilaya hiyo kongwe huko mbele ilikuwa na kiwanda cha kutengeneza vigae vya kuezeka maghorofa na pia kulikuwa na kiwanda kilichokuwa kinamilikiwa cha kutengeneza chokaa na gypsum powder. Hivi sasa hivyo viwanda havifanyi kazi.
Je, ni lini Wizara itaenda Mbulu ili ikae na Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu na Halmashauri ya Vijijini waweze kufufua viwanda hivi ambayo vilianzishwa na wenzetu huko awali?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Issaay, kuhusu vifaa vya madini ya ujenzi, kwa mamlaka niliyonayo namuagiza Mkurugenzi anayeshughulikia viwanda aandae safari ya wataalam kwenda kuangalia fursa zilizoko kule na awapeleke wawekezaji kule Mbulu kusudi mimi nikienda, niende kufungua na kuzindua kiwanda hicho.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ninakushukuru. Katika Wilaya ya Mbeya tumekuwa na viwanda vingi sana kama Kiwanda cha Mbeya Textile, Hill Soap, Tanganyika Packers, Zana za Kilimo na kadhalika na viwanda hivi ni vya muda mrefu sana vimekufa. Namuomba Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na Msajili wa Hazina, anieleze ni lini na nini mkakati wa Serikali katika ufufuaji wa viwanda? Siyo ujenzi wa viwanda. Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio. Natambua na kumbukumbu zinaonesha kwamba viwanda vingi vilivyopo Mbeya vilikufa na vilipokufa vilibinafsishwa na kupeleka miliki kwa watu wengine, watu binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa taarifa ya awali kwamba Treasury Registrar kwa kushirikiana na Wizara za kisekta wanafuatilia ikihusisha uhamishaji wa miliki ambayo ni masuala ya kisheria kusudi waweze kuvirudisha hivyo viwanda kwenye wamiliki wapya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niwaeleze Waheshimiwa Wabunge, mtu aliyeuziwa kitu kwa mkataba huwezi kumnyang’anya hivi hivi, labda tubadilishe matumzi ya sheria, siyo kitu rahisi.
Ningependa tuwanyang’anye mara moja, lakini siyo kitu rahisi. Tunachofanya zaidi pamoja na kuwanyang’anya, tunajaribu kuangalia namna gani rasilimali zile zinaweza kutumika kuzalisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, kwa uelewa zaidi, someni vision 2025 mjue kwa nini viwanda vilikufa? Vingine vilikufa kwa sababu pale vilipojengwa, havikustahili kujengwa.
MHE. ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mheshimiwa Waziri kwa sababu nchi hii ina tatizo kubwa sana la sukari na katika Mkoa wa Kagera umesema tuanzishe viwanda vya maziwa, ukitoka pale Bulembo kwenda Busheregenyi, kwenda Msira kwenda Rugongo, kwenda sehemu za huko kama unaenda Kasharu; maeneo yale ni maeneo ya tingatinga kuweza kulima mashamba ya miwa na watu wajasiliamali wadogo wakaanzisha viwanda vidogo vidogo.
Ni lini unaenda Misenyi kukaa na wananchi? Ofisi yako ikawaambie kwa sababu uwezekano wa kupatikana miwa upo ili waweze kuanzisha viwanda vidogo vidogo?(Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, namsukuru Mheshimiwa Bulembo. Hilo la kwenda Busheregenyi kwa bibi zangu halina mjadala, lakini napenda nikueleze kwamba ninaye mwekezaji sasa katika maeneo hayo ambaye anataka kuingia ubia na Jeshi la Magereza sehemu Kitengule, kushirikiana na Jeshi la Magereza kutumia uoto ule kuweza kulima miwa ya kuzalisha sukari. Kwa hiyo, tutalijadili mimi na pacha wangu, yule mwekezaji yupo serious anataka kuwekeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatafuta wawekezaji lakini Waheshimiwa Wabunge muelewe, mwekezaji humleti leo akaanza leo. Mkijua huo mchakato wa kuweza kuchukua ardhi mpaka kuzalisha, ndiyo maana nikaanzisha ule utafiti wa wepesi wa kufanya biashara. Ndiyo mambo ambayo tunayarekebisha na tutayarekebisha kusudi angalau wawekezaji wachukue muda kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala na Mheshimiwa Bulembo ni kwamba Busheregenyi mnaweza kupata huduma Kagera Sugar na mkapata huduma Magereza watakapokuwa wameanzisha kiwanda wale wawekezaji.
MHE. JAMAL KASSIM ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza, Mheshimiwa Waziri katika jibu lake la msingi amekiri kwamba moja ya mambo muhimu kabisa ya Watanzania hawa kwenda kuwekeza kwenye viwanda ni pamoja na kuwa na mitaji. Watanzania hawa wamefanya biashara kubwa sana na Serikali na wana madeni makubwa ambayo wanaidai Serikali.
Je, Serikali haioni ipo haja sasa madeni haya ambayo wamekuwa wakidaiwa kwa muda mrefu kuyalipa kwa haraka ili Watanzania hawa nao sasa wapate fursa ya kwenda kushiriki katika uchumi wa viwanda ambao Mheshimiwa Waziri ameeleza? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kuja na sera maalum ambayo itatoa special incentive package kwa wawekezaji wazawa Watanzania ili nao waweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa viwanda kutokana na kuwa nyuma kiteknolojia, kifedha na mambo mengine ambayo ukiwaweka na wenzetu wa mataifa mengine Watanzania hawa hawawezi ku-compete? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo wapo wafanyabiashara, wakandarasi ambao wamefanya kazi na Serikali na wanadai stahiki yao, Serikali itawalipa. Utaratibu wa Serikali unapitiwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha amekuwa akilisema mara kwa mara kwamba jambo kubwa ni kufanya uhakiki na kadri uhakiki unapofanyika hao watu wanalipwa na niwahakikishie kwamba Serikali itawalipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na vivutio, sasa hivi kuna vivutio, suala la muhimu kwa wafanyabiashara wa Tanzania au kwa Watanzania ambao wangependa kupewa vivutio maalum waone hivi vivutio vilivyopo watuambie ni wapi sio vizuri. Hatuwezi kubadilisha vivutio, kwanza anza utuambie hiki siyo kizuri hiki ndiyo kizuri ndiyo tutabadilisha.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona, naomba niulize swali la nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kuna mfuko wa NEDF ambao Mheshimiwa Waziri ameutaja yaani National Entrepreneur Development Fund, kwa mwaka huu pesa hizo hazijatoka. Napenda kupata kauli ya Serikali, je, ni lini hizo shilingi bilioni 2.5 zitatolewa ili ziweze kuwawezesha Watanzania wanaotaka kufungua biashara ndogondogo au kufungua viwanda vidogo vidogo waweze kuwezeshwa na kufanya hivyo? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa NEDF kama mlivyoona taarifa ambayo imekuja pekee ni mfuko ambao unawachangamsha wawekezaji ukitoa mikopo mbalimbali. Katika mwaka wa fedha tunaomaliza tulitengewa shilingi bilioni 2.4, pesa hizo hazijatoka, lakini mwaka huu haujaisha. Nina imani hizo pesa zitakuja katika mwaka huu wa fedha na nimemkumbusha Waziri wa Fedha kwamba fedha hizo Wabunge wanazihitaji haraka wazipeleke Majimbo. Nina imani kabla jua halijazama pesa hizo zitapatikana.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa sababu tunataka tuingie kwenye Tanzania ya viwanda na Tanzania ya viwanda ni lazima iende sambamba na uwekezaji kwenye ardhi lakini uwekezaji kwenye ardhi unakumbwa na matatizo makubwa. Tatizo la kwanza vijiji vyetu vingi havijaingia kwenye matumizi bora ya ardhi, matokeo yake mwekezaji anakosa nafasi na hata pale ambapo vijiji vimeshaingia kwenye matumizi bora ya ardhi kuna tatizo kwenye Makamishna wa Kanda katika upatikanaji wa ardhi lakini sio hivyo tu, hata kwenye Ofisi ya Rais ambapo nako kuna matatizo...
Je, nini kauli ya Serikali kwa wawekezaji wanaohangaika kutafuta ardhi ya kufanya uwekezaji katika kilimo? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa rafiki yangu Alhaj ametaka kujua kauli ya Serikali. Tunalitambua tatizo la upatikanaji wa ardhi, ndiyo maana si mara moja Mheshimiwa Waziri Mkuu na Ofisi ya TAMISEMI wametoa maelekezo kwa mamlaka za Mikoa na Wilaya, watenge maeneo kwa wale walio tayari waweze kuwekeza mara moja. Nirudie, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, tengeni maeneo yule anayetaka kuwekeza msimsubirishe.
MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza na nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa Serikali ilitembelea katika kiwanda hicho na kujionea migogoro katika kiwanda hicho na waliahidi kusaidia kutatua tatizo la migogoro hiyo haraka iwezekanavyo, je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo?
Swali la pili, kwa kuwa moja ya tatizo katika kiwanda kile ni kutokuwa na Bodi yenye uwiano kati ya mwekezaji na MUVYULU, je, Serikali itawasaidiaje wananchi wale kuhakikisha kunakuwa na uwiano wa bodi ili waweze kupata gawio na kuweza kuwaendeleza wale wakulima? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushirikiano, vile vyama vyenu vya MUVYULU vimekwenda mahakamani. Kwa sababu kesi iko mahakamani, suala lako (a) na (b) mimi mikono yangu inakuwa nje, siwezi kuliingilia. (Makofi)
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na changamoto za upungufu wa viwanda katika Mkoa wa Katavi, lakini pia kuna tatizo kubwa linawasumbua wakazi wa Manispaa ya Mpanda.
Je, Serikali iko tayari kufuatialia mashine ya kukoboa na kusaga iliyonunuliwa na Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda ambayo pia iligharimu pesa nyingi mno, mpaka sasa wananchi hawaelewi kwamba mashine hii iko wapi? Sehemu ambayo ilitakiwa kujengwa kwa ajili ya kuiweka ile mashine ili ifanye kazi mpaka sasa lile eneo ni gofu. Wananchi hawaelewi, nini mkakati wa Serikali kusaidia na kuokoa fedha hizi ili wananchi wapate ajira katika Manispaa ya Mpanda?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge ameuliza swali lake ili kuweka msisitizo. Tumeshakubaliana kwamba tutakwenda kwenye Jimbo lako tuweze kuona hilo suala tulishughulikie. Kwa hiyo, hakuna tatizo Katavi na Rukwa, nimeshazungumza, mikoa yote miwili nitakwenda pamoja na ule mwongozo niliowatolea. Kwa hiyo, masuala yenu nitayashughulikia, tutajipanga upya.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa msiba uliopo huko Lupembe wa kiwanda kufungwa ni sawa kabisa na msiba ulioko kule Bumbuli Kiwanda cha Mponde sasa ni miaka mitano chai inashindwa kuzalishwa na wananchi hawa wanapata hasara.
Je, Serakali inatoa tamko gani kuhusu msiba huo wa watu wa Bumbuli?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, aya ya mwisho katika swali nililolijibu nilisema Serikali inafuatilia hizi changamoto au migogoro kwenye viwanda vya chai. Sitaki kusema zaidi, lakini yule aliyeleta mgogoro, aliyehusika kwenye mgogoro wa Lupembe ndiyo yule anayehusika na kwenye mgogoro wa Mponde. Sasa sijui kuna nini! Niko chini yangu na juzi nilikuwa Tanga, nimewaeleza kwamba tutalifuatilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa Mheshimiwa Shangazi kwamba katika Wilaya yake, Halmashauri sasa inakwenda njia ya pili kuanzisha kiwanda. Nimewaelekeza waende TIRDO wawaongoze namna ya kutengeneza kiwanda kingine, lakini Serikali inafuatilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, jambo la kusikitisha, anayelalamikiwa Kusini, ndiye anayelalamikiwa Mashariki.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, tarehe 19 Aprili, 2016 niliuliza swali hili hili katika Bunge hili hili. Bunge lilielezwa kwamba fidia ingeweza kulipwa Juni, 2016 na mradi kuanza Machi, 2017. Je, tushike kauli ipi kati ya haya majibu mawili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa mwekezaji tayari anayo hela, yuko tayari kulipa, kwa nini Serikali isichukue jukumu la kulipa fidia ili wale wananchi wale waendelee na shughuli zao nyingine za kiuchumi halafu mwisho Serikali itakapokuwa tayari ije ichukue kwa mwekezaji hiyo hela ambayo tayari anayo sasa hivi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ametaka kujua achukue kauli ipi ya Serikali kati ya jibu nililompa tarehe 19 Aprili na hili ninalompa leo. Katika jibu langu nimeeleza kwamba Serikali imechukua hatua ya kupitia makubaliano na mwekezaji ili kuhakikisha kwamba uwekezaji unaowekezwa unakuwa na manufaa kwa Watanzania na kwa mwekezaji. Mheshimiwa Ngalawa huo ndiyo mchezo wa siku hizi, Serikali itahakiki kuhakikisha uwekezaji unaowekezwa unaleta tija kwa mwekezaji na kwa Watanzania. Naogopa usije ukanirudia mwaka 2030 nikiwa Mbunge niko hapa Waziri ukaniuliza mbona mmeacha mashimo Ludewa, nitashindwa kukujibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kulipa fidia Serikali, nina imani hii timu yangu inayofanya kazi, nayoisimamia mimi mwenyewe, hatuondoki hapa Bungeni bila kukubaliana. Wawekezaji wako Dodoma, watendaji wangu wote wako Dodoma, mimi nawasimamia mwenyewe lazima tukubaliane Mchuchuma na Liganga ianze.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize maswali madogo ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Wilaya ya Uyui tayari ina eneo kubwa ambalo wawekezaji wanaweza wakalitumia. Je, Serikali iko tayari sasa kuwapeleka wataalam kuhakikisha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa wawekezaji wengi hapa nchini hukiuka maandiko au mikataba wanayoingia na Serikali. Je, Serikali iko tayari sasa kuipitia upya ile mikataba na kuivunja kabisa mikataba ambayo wameingia hapa nchini kwa mfano Kiwanda cha Manonga na Kiwanda cha Nyuzi? Je, Serikali inasema nini? Je, Waziri yuko tayari sasa kwenda kuviona viwanda hivyo jinsi walivyoviharibu? Naomba majibu. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Uyui, kwenye kongamano nililolisema ambalo analisimamia Mkuu wa Mkoa na Meneja wa Tan Trade na mimi nitakuwepo. Kwa hiyo, nitakwenda Uyui na wataalam tutaangalia hali itakavyokuwa na tutaweza kuwashauri namna ya kufanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, si wawekezaji wote wanakiuka, mmoja anayekiuka umlete tutamshughulikia, ni case by case. Wawekezaji si wabaya, wawekezaji ni wazuri lakini yule anayekiuka tutamshughulikia kulingana na tukio lenyewe.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa TIC ndiyo lango kuu la uwekezaji nchini, je, TIC inaisaidiaje EPZ kwenye kutekeleza majukumu yake vizuri? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, taasisi zote hizi mbili ziko chini yangu, kwa Kiswahili cha kawaida TIC ni receptionist, EPZ ndiyo anaandaa kama ni ubwabwa kwenye meza. Kwa hiyo wote wanashirikiana, ni mkono na mdomo. TIC ni receptionist, ni mpiga sound anakaribisha watu, EPZA anaweza kuwatendea inavyobidi. (Kicheko/Makofi)
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri katika majibu yake ameeleza kwamba uwekezaji ni lazima uende pamoja na manufaa kwa wananchi waliopo katika eneo ambalo uwekezaji umefanyika. Katika Jimbo la Ubungo kuna maeneo ya EPZ yaliyopo eneo la Ubungo External na kuna Kiwanda cha Urafiki ambacho Serikali imekibinafsisha kwa mwekezaji wa nje. Maeneo hayo mawili hayana manufaa yoyote kwa wananchi wa Ubungo na eneo la EPZ lina migogoro mikubwa, wafanyakazi wanalipwa mishahara midogo…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini Serikali itatatua matatizo ya EPZ yaliyoko katika Jimbo la Ubungo?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna msemo kwetu unasema mwenye shibe hamjui mwenye njaa. EPZA kuna viwanda vinaajiri vijana zaidi 3,000, mimi naomba kama kiwanda hicho kingehamia kwetu nikaajiri vijana 3,000. Urafiki inatoa ajira, inaweza kuwa na upungufu yale specific uyalete kwangu niyashughulikie. Wawekezaji wote ni wazuri yule aliye mbaya mumlete kwangu, lakini hao 1,800 na Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu upande wa Ajira wanaajiri vijana 400 kila baada ya miezi minne. Narudia tena na sifichi ningeomba hao watu wangekuwa kwenye Jimbo langu naajiri vijana wangu 400 kila mwezi, usikufuru Mheshimiwa Kubenea.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwanza jina langu ni Saed Kubenea tofauti na Mheshimiwa Waziri alivyolitaja.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kiwanda cha Urafiki kinaendeshwa kwa hasara kuanzia mwaka 1998 na kusababisha malimbikizo ya hasara yanayofikia shilingi bilioni
18.04 hadi tarehe 30 Juni, 2011. Na kwa kuwa mwekezaji aliyepita kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Hodhi la Taifa alichukua mkopo kwenye Benki ya Exim ya China unaofikia shilingi bilioni 56.1 na riba ya shilingi bilioni 4.04; na kwa kuwa Serikali imeamua kuwanyang’anya wafanyabiashara wazawa viwanda ambavyo walivinunua kutoka Serikalini kwa kushindwa kuviendesha. Je, Serikali iko tayari kumnyang’anya mbia huyu Kiwanda cha Nguo cha Urafiki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali ya Tanzania ilituma ujumbe China ambao uliongozwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Viwanda na Biashara, Shirika la Hodhi la Taifa na FTC kati ya tarehe 17 na
23 Desemba, 2011; na kwa kuwa ujumbe huu ndio uliopendekeza mwekezaji mpya kupewa kiwanda na kuhamisha hisa za Serikali kutoka asilimia 49 ambazo ilikuwa inamiliki. Je, Serikali iko tayari kuwawajibisha wafanyakazi hao wa umma waliotuletea mwekezaji fake? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, hatunyang’anyi watu viwanda, hakuna mtu aliyebinafsishwa kiwanda atanyang’anywa, ila kama kiwanda kikikushinda nakushauri na nakuambia umpe jirani yako. Nimekuwa nikilisema ni kama tulivyolelewa sisi na nyanya zetu, ukiwa na nguo ikikubana usiichane, mpe mwenzio avae na viwanda hivi vitafanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Kiwanda cha Urafiki nimesema ni kiwanda cha kihistoria, tulipobinafsisha viwanda, viwanda viwili vilikuwa na maneno na Mwalimu alivisemea, Mwalimu alipinga kubinafsisha Kiwanda cha Bora akasema gharama ya kubinafsisha Bora inazidiwa hata na bei ya plot pale Pugu Road wakampa majibu yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, alipokuja kwa Urafiki akasema mwende kwa Wachina na katika jibu langu nimeeleza mlolongo tunaoufuata kupata partner mpya. Partner mpya sitaki kuendelea zaidi kwa sababu sasa tuna- negotiate na chini ya uongozi wa Kamati yangu ya Biashara unakwenda kupata deal nzuri, Kamati ya Viwanda na Biashara tumiliki zaidi na Mchina amekubali kutupa percent kubwa karibu 75 percent. Kwa hiyo, tutakuwa na umiliki tutaweza kuamua kiwanda kiwanda kiende vipi, tutakujengea Urafiki nzuri Mheshimiwa Kubenea, nataka kuona watu 8,000 wanafanya kazi pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa suala la waliokwenda, hili suala limetolewa maamuzi na CAG. CAG aliyoyaona ukiyaona utalia Kubenea. Kwa hiyo, kila mtu ambaye alihusika katika kutuingiza kwenye dhahama hii rungu litamshukia kama mwewe. (Makofi)
MHE. KHADIJA NASSIR ALI:Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kumekuwa na malalamiko mengi juu ya mlolongo mrefu ambao hauna ulazima kwenye mchakato mzima wa uwekezaji ambao huwakatisha tamaa wawekezaji wengi nchini. Je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza kero hii kwa wawekezaji wetu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anasema yalikuwepo malalamiko; yalikuwepo malalamiko wakati ule sasa hayapo. Yeyote anayetaka kuwekeza anione mimi, kama upo mkoani muone Mkuu wa Mkoa, kama uko Dar es Salaam nenda Ofisi yangu ya Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa amepewa mamlaka ya kukaribisha wawekezaji na Mheshimiwa Rais amesema mwekezaji atakayekwamishwa mkuu wa mamlaka awe Wilaya au Mkoa ajione hayupo salama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ulivyosema Mheshimiwa Mbunge yalikuwepo, sasa yamekwisha. (Makofi)
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Mwezi Septemba, 2015 Serikali iliwalipa fidia wananchi wanaopisha mradi wa bandari katika Vijiji vya Pande na Mlingotini. Miongoni mwao wananchi 687 walibainika kwamba walipunjwa fidia zao; kwa hivyo Serikali iliwafanyia uhakiki mwezi wa kwanza mwaka jana ili kubaini fidia stahiki za wananchi hao. Je, ni lini wananchi hawa watalipwa fidia zao stahiki?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, tarehe 22 Mwezi wa sita mwaka jana wakati anazindua kiwanda cha Elvin katika Kata ya Mapinga, Mheshimiwa Rais aliwatangazia wananchi wanaopisha mradi wa EPZ Bagamoyo kwamba wale wote ambao hawajalipwa fidia zao wanaweza wakarudi sasa katika maeneo yao wayaendeleze maeneo yao. Je, ni lini EPZA na Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo itawaruhusu wananchi hao kumiliki maeneo yao kama ilivyoelekezwa na Mheshimiwa Rais?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipende kumshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa jinsi anavyofuatilia suala hili; lakini na yeye amekiri kwamba uhakiki ulifanyika kufuatilia wale waliopunjwa. Hapa tatizo kama nilivyosema kwenye suala la msingi ni ukosefu wa pesa za kutosha kutoka kwenye Bajeti ya Serikali kufidia maeneo ya kiuwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu Serikali imeshapata njia hii ya pili ya wabia watatu kutafuta pesa, nimshauri Mheshimiwa Mbunge tuendelee kushirikiana kusudi tupate fedha za kuweza kuwafidia kila mtu aridhike kusudi mradi wetu uweze kufanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili kuhusu tamko la Mheshimiwa Rais. Tamko la Mheshimiwa Rais ni maelekezo, watu wa EPZA, watu wa halmashauri na hapa kunapashwa kuingia wananchi, watakaa kusudi watekeleze tamko la Mheshimiwa Rais. Jambo ambalo ningependa Watanzania walielewe lile eneo limeamuliwa kwamba ni Export Processing Zone. Sasa kuna mchakato unapaswa ufanyike kusudi wewe ukawekeze vinginevyo; lakini kwa mamlaka niliyonayo EPZ na halmashauri na wananchi na wewe Mbunge tutakaa chini tuangalie namna ya kuwekeza kwa manufaa ya watu wote.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Ripoti ya CAG inaonesha kwamba mdaiwa mkubwa wa viwanda vyetu vya ndani ni Serikali hususan halmashauri zetu. Je, Serikali ina mkakati gani madhubuti ya kuanza kulipa madeni hayo ili kunusuru anguko la viwanda vyetu ambavyo tunavianzisha kwa nia njema? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo, Serikali inadaiwa na Serikali sasa tunaongeza jitihada za kuhakikisha kwamba kila stahili ya Serikali inakusanywa na kile kitakachokusanywa ndicho kitawalipa wale. Hatujawalipa wale kwa sababu na sisi hatujalipwa kuna watu hawapendi kulipa kodi, hata ukisoma easy of doing business Tanzania tunafanya vibaya kwa sababu watu hawataki kulipa kodi, lakini katika nchi nyingine huwezi kupewa haki nyingine hata kwenda kuchumbia kama huwezi kuonesha tax clearance.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pia naipongeza Serikali kwa juhudi kubwa ambayo inaendelea kuwafanyia wakulima wetu. Nitakuwa na swali ndogo la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri.
Kwa kuwa wakulima wetu wengi especially Mkoa wangu wa Iringa wamekosa mwongozo na baadhi hawana uelewa ni kitu gani wanatakiwa kufanya ili bidhaa zao ziweze kufika kwenye Soko la Kimataifa, sasa Serikali iko tayari kuwa na Kitengo Maalum ambacho kitakuwa kinafanya kazi usiku na mchana, siyo tu kwa kutafuta masoko, bali kwa kutoa taarifa kwenye mikoa yetu juu ya hali ya masoko ya bidhaa ambazo wanazalisha? Nashukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Tweve kwa swali zuri.
Kuanzia mwaka 2017 maelekezo ya Serikali ni kwamba Shirika la TanTrade lina jukumu la kuhakikisha kwamba linatafuta masoko ya mazao na bidhaa zote za Tanzania na lina wajibu wa kuhakikisha linatengeneza mtandao kupitia Halmashauri za Wilaya kwamba waweze ku-identify wakulima wana nini na masoko yako wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu tulionao sasa ni kwamba Wizara yangu kwa kushirkiana na Wizara ya Kilimo na Mamlaka za Serikali za Mitaa, Maafisa Biashara ngazi ya Wilaya watakuwa waki-link na TanTrade na hizi Wizara za kisekta katika kuhakikisha kwamba wakulima wanapata masoko ya mazao yao. (Makofi)
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante viwanda vyote ambavyo vilibinafsishwa kwa maana viendelee kubangua korosho sasa hivi vimegeuka maghala tofauti na mikataba iliyoingiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni juhudi gani Serikali hasa Wizara ya Viwanda na Biashara inasimamia kuhakikisha kwamba vinaendelea kuwa viwanda na sio maghala ya korosho kwa sababu vibali vya kufanya maghala vinatolewa na Wizara ya Viwanda na Biashara. Lini wataacha kuwapa vibali ya kufanya maghala na wafanye viwanda?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Ghasia kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni juhudi gani, kama swali la msingi ilivyoelezwa Kiwanda hiki cha Masasi kimekwama kwa sababu ya shauri lililopo mahakamani. Lakini katika mfumo huo kuna viwanda vingine vipo mahakamani, katika sekta ya korosho ninavyo viwanda ambavyo nimehakikisha mwenyewe wamiliki wake wameshaanza kutengeneza mipango ya kuviendeleza ikiwemo kuleta mitambo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mitambo nimeiona mwenyewe kuanzia hivi vya Kibaha mpaka vya Liwale one, kwa hiyo juhudi zinafanyika kuendelea kuwafuatilia hawa wawekezaji ili waweze kuvirudisha katika njia ya kufanya kazi viwanda hivi, ikiwa ni pamoja na kutafuta mitaji, kwa hiyo, juhudi hizi za kuhakikisha vinafanya kazi tutahakikisha zinaendelea.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, napenda kufahamu kuanzia mwaka 2009 mpaka sasa ina maana Serikali ilikuwa inawekeza katika kiwanda cha General Tyre bila andiko la kitaalam? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama kiwanda kitaendeshwa bila kuwa na ruzuku ya Serikali, je, maslahi ya wananchi wa Mkoa wa Arusha yatalindwa vipi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ni kwamba tumekuwa tukiwekeza bila kuwa na andiko la kitaalam, hapana, lilikuwepo, lakini hii ni biashara, biashara siyo static. Kilichobadilika ni kwamba huwezi kuendesha kiwanda kile kwa kutegemea ruzuku. Ule mradi ni bankable, ni rahisi ukaelezea kwamba una kiwanda kile, Tanzania kuna soko la matairi 44,000,000 kwa span ya miaka mitatu, soko lenye uwezo wa trilioni 1.18.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunataka andiko, TIB ihusishwe, pesa zikopwe kwenye benki za nje zinazotoa riba ndogo, twende kwa mtazamo huo. Ndiyo maana nataka kuitoa kwenye ruzuku, huwezi kuendesha kiwanda kwa ruzuku. Amezungumza Mheshimiwa Bashe jana hapa, ruzuku ya Serikali iende kwenye mambo ya jamii.
Mheshimiwa Spika, namba mbili, maslahi ya watu wa Arusha. Maslahi ya Watanzania wote yatazingatiwa. Maslahi yanakuja wapi, kiwanda kikishatengenezwa kwa menejimenti ni mali ya Serikali. Tunakolenga maslahi ya Watanzania wote yatapatikana, moja kwa ajira lakini pili kiwanda kile kinaweza kuuza hisa Watanzania mkaki-own kama mnavyo-own TBL, mnavyo-own cement.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba Mkoa wa Arusha una kiwanda hicho ambacho kinafahamika zaidi cha General Tyre lakini ni ukweli kwamba Mkoa wa Arusha pia una viwanda vingine vingi ambavyo vimebinafsishwa ikiwemo Kiwanda cha Maziwa, Kiwanda cha Phillips, Kiwanda kilichokuwa cha Nguo. Je, Serikali ina mpango gani wa kufufua viwanda vyote vilivyopo katika Mkoa wa Arusha?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Paresso. Napenda niseme ukweli, sipo hapa kudanganya watu. Sina kumbukumbu kwamba Kiwanda cha Phillips kilikuwa cha Serikali lakini hoja ya Mheshimiwa Mbunge ni kuona Arusha inapata viwanda.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anawahisha shughuli, nimekuwa Arusha mara tano tangu niwe Waziri, nimeupendelea Mkoa wa Arusha. Napenda kusema kwamba viwanda vitaanzishwa na vitaanzishwa kwa Watanzania kuhamasishwa kushiriki katika viwanda.
Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Maziwa ni kiwanda kidogo na tunao mkakati wa kuanzisha Viwanda vya Maziwa, Viwanda vya Ngozi na Viwanda vya Viatu. Kwa hiyo, wakati utakapofika kila mkoa utapata dozi yake na viwanda vitaanzishwa kiuchumi. Bahati mbaya kuna watu hawataki viwanda, hatutapeleka viwanda pale wasipovitaka.
Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru Mheshimiwa Waziri alivyonijibu vizuri na kwa ufasaha swali langu, lakini nitakuwa na maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Waziri, je, kwa nini Serikali haioni
umuhimu wa kuwepo vyombo vya awali vya kuhakiki aina au bidhaa mbalimbali ya vyuma chakavu kabla havijafika sokoni?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa nini usiwepo
utaratibu wa kutofautisha biashara ya vyuma chakavu kabla ya kuharibu miundombinu ya Serikali ambayo sasa hivi imeenea nchi nzima kila mahali vinang’olewa? Kungekuwa na uhakiki kabla ya hivyo vyuma chakavu kuweza kufika
sokoni na kuweza kuuzwa? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ile dhana ya kutumia vyuma chakavu ambavyo kimsingi vinakuwa havitakiwi kwenda kuviyeyusha na kutengeneza chuma ni wazo zuri. Tatizo lililopo ni kwamba watu wenye tamaa, wahalifu ndiyo wanaharibu ile dhana nzuri, hawa ni wahalifu kama wahalifu
wengine. Sasa chombo cha awali cha kuweza kuzuia watu hawa ni wananchi, kama inavyosema Katiba ya nchi yetu, ulinzi wan chi hii ni jukumu la wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwenye ile
miundombinu mikubwa kama ile ya TANESCO nilivyosema, TANESCO anaweka ulinzi akisaidiana na wananchi walio wema. Nina imani huo ndio mfumo mzuri wa kuweza kulinda miundombinu yetu Tanzania nzima, Wizara yangu au Serikali
haiwezi kutengeneza polisi wa kulinda vyuma kuanzia vile vya taasisi mpaka vyetu binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa kutofautisha, kama ilivyo kwa wale wanaoharibu miundombinu kwenda kujipatia pesa wapo hata wenye viwanda ambao wanapokea vyuma ambavyo wazi kabisa vinaonekana vimetoka kwenye miundombinu ya Serikali au ya watu, hao
mimi ndio nakula nao sahani moja. Ma-inspector wangu wanatembelea viwanda hivyo na ni vichache vinajulikana na naendelea kuwapa elimu, atakayebainika atajuta kwanini alifanya hivyo.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Suala la biashara ya vyuma chakavu inaonesha ni wazi kuna soko zuri la chuma nchini na nje ya nchi. Sasa kifupi tu, sijui mradi wa chuma Liganga na Mchuchuma umefikia wapi ili nchi ifaidike na soko hilo? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Mchuchuma na Liganga; katika mpango wa Serikali wa miaka mitano wa ujenzi wa uchumi wa viwanda, mchuma na Liganga ipo. Nilipofikia mimi; hili suala liko mezani kwangu. Nimepitia vivutio vyote vya mwekezaji alivyoweka, nimevikamilisha, vinakwenda kwenye mamlaka kusudi waweke sahihi, mwekezaji yuko tayari kuweka fidia na kuweza kuanza. Nikipata sahihi ya mamlaka tunaanza kazi.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa hii biashara ya vyuma chakavu inavikumba pia viwanda vilivyobinafsishwa kwa muda mrefu sasa kikiwemo Kiwanda cha Nyuzi Tabora, na kwa kuwa kuna taarifa kwamba mashine nyingi mle ndani zimeuzwa kama chuma chakavu na kimefungwa kile kiwanda, je, Mheshimiwa Waziri, kwa sababu nimewahi kulalamika hapa Bungeni na kutoa taarifa kuhusu kufanyika kwa vyuma
chakavu, ni lini tunaweza tukaenda tukakagua kile kiwanda kwa sababu sasa hivi umetoka kusema utakula nao sahani moja, tuweze kujua kama vile zile mashine hazijauzwa kama vyuma chakavu?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Nyuzi cha Tabora kina mwenye nacho (owner) kwa hiyo, mwenye mali anapoibiwa mimi siwezi kwenda kuangalia mali yake yule, lakini taarifa nilizonazo kutoka kwa mwenye kiwanda ameniambia amepata soko la nyuzi na kiwanda hicho kitaanza kazi. Kwa hiyo, mimi naweza kumbana yule kwa kupitia msajili wa hazina kwamba aanze kazi na ndio wajibu wangu. Sasa kama alizembea, mali ikaibiwa mle hilo nadhani ni suala la kila abiria achunge mzigo wake.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii. Ni takribani miaka kumi sasa toka hili swali linaulizwa. Nakumbuka lile Bunge la Tisa niliuliza hili swali
mwaka 2007 na Bunge la Kumi aliuliza Mheshimiwa Maida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jibu la Serikali siku zote ni kwamba muswada unaandaliwa. Ni lini sasa muswada huo utaletwa hapa Bungeni ili uweze kupitishwa kama sheria?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mbunge najua una imani na mimi. Sasa upele umepata mkunaji, safari hii unaletwa chini ya uongozi wangu.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda. Ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imejikita katika uanzishwaji wa viwanda ili kuzalisha ajira za kutosha kwa vijana, je, Serikali ipo tayari sasa kuupa Mkoa wa Singida kipaumbele cha kwanza?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili. kwa kuwa Tanzania tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda: Je, ni lini sasa
Mfuko huu wa SME Credit Guarantee Scheme utaletwa Singida ili vikundi vya wanawake na vijana viweze kunufaika na mfuko huo? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimjibu Mheshimiwa Aisharose maswali yake mawili ya nyongeza na nianze na hili la pili ambalo ni rahisi. Mfuko wa SME Guarantee Scheme umeshafika Singida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kusema kwa sababu yeye anashughulika na akina mama na vijana,
namuagiza Meneja wa Singida awasiliane na Mheshimiwa Mbunge, halafu namuagiza Mkurugenzi Mkuu wa TEMDO wawasiliane, zile mashine zinazotengenezwa na TEMDO huyu mama ndiye awe mhamasishaji wa kuwaonesha watu namna gani wakope. Tumeshusha riba mpaka 17%. Mashine ya kwanza Singida uanze nayo wewe, utembee kijiji kwa kijiji ukiwalenga vijana na akina mama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye swali langu la msingi ni kwamba Singida tayari wako kwenye
uchumi wa viwanda. Tumeshatenga maeneo ya kujenga viwanda na Mbunge wa Singida, Mheshimiwa Kingu,
anajasiria kupitia e-scheme, mradi wa kiwanda cha maziwa.
Kwa hiyo, Singida viwanda siyo jambo geni, tunahangaika Singida kwenye viwanda kuona ile malighafi ya saruji kama tunaweza kutengeneza kiwanda angalau cha ku-blend saruji kutafuta crinker na kuchanganya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tuwe wote, Singida wako kwenye viwanda.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza
kwa niaba ya wananchi wangu wa Mtama na Mkoa wa Lindi kwa wakulima wa ufuta. Naomba kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ongezeko la uzalishaji wa zao la alizeti kasi yake inafanana sana na
ongezeko la uzalishaji wa ufuta katika Mkoa wa Lindi na hasa katika Jimbo la Mtama na kwa kuwa ubora wa mafuta ya ufuta ni mzuri kuliko yale ya alizeti. Sasa Serikali ina mpango gani wa kusaidia uanzishaji wa viwanda vidogo vidogo vya kukamua mafuta ya ufuta kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wangu wa Mtama na Mkoa wa Lindi ambao wanalima ufuta na kuinua uchumi wao?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jibu langu, napenda niseme mafuta yote ya alizeti na yale ya ufuta yote ni mazuri.
Kwa hiyo, wananchi waende kuyatumia, ilimradi yazalishwe Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu viwanda vidogo vidogo, namshauri Mheshimiwa Mbunge awasiliane na SIDO.
Nina Meneja mzuri wa SIDO, Lindi na kwa sababu hili liko kwenye mamlaka yangu, mradi wa SME Guarantee Scheme unahusisha na Mkoa wa Lindi.
Kwa hiyo, Mkurugenzi wangu anayeshughulikia mpango huu, ahakikishe na Lindi inakwenda kule kwa sababu Tanzania tunaagiza mafuta mengi ya kula. Tunaconsume tani 400,000 kwa mwaka, lakini karibu 70%
tunaagiza nje. Mafuta ya kula ni commodity ambayo inachukua pesa za kigeni ikiwa ni namba mbili baada ya
mafuta jamii ya petroli.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, unalisaidia Taifa lako, tukamue mafuta hapa, tujitosheleze, tuokoe pesa za kigeni.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuuliza swali la
nyongeza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Mara kulikuwa na takribani viwanda saba, lakini sasa hivi viwanda
vyote vimekufa, kimebakia kiwanda kimoja tu cha samaki cha Mara Fish.
Je, ni lini Serikali itafufua viwanda hivyo kwa sababu sasa hivi ni kipindi cha viwanda tu? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya maagizo niliyopewa katika Wizara yangu pamoja na Treasurer Registrar ni
kuhakikisha vile viwanda vilivyobinafsishwa au ambavyo havifanyi kazi vinafanya kazi. Zoezi hilo linaendelea.
Mhesimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba nashindwa kusema ni lini kwa tarehe, napenda nimhamasishe
Mbunge na yeye akimbilie kwenye viwanda vidogo, kwa sababu viwanda vidogo kulingana na taratibu za Bunge,
pesa mnazonipa za NEDF, zinaniwezesha mimi kuweza kutoa vile viwanda vya shilingi milioni 10, shilingi milioni 80 na shilingi milioni 200. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, twende kwenye viwanda vidogo kwa sababu vinaweza kufanya kazi kuanzia ngazi ya familia na vinajenga utamaduni wa Watanzania kumiliki. Hivyo viwanda vingine ni vya watu ambao ni wa kupita.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, yenye data na yamenifurahisha. Pamoja na majibu hayo mazuri nina swali moja la nyongeza na ombi moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ahadi ya Mheshimiwa Rais juu ya kujenga viwanda ili kutoa ajira, kujenga uchumi na kutumia malighafi za eneo husika lilizungumzwa bila ubaguzi wowote na kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri katika majibu yake amesema jukumu la Serikali ni kuhamasisha na kuweka mazingira mazuri ya uwezeshaji na ujenzi ni jukumu la sekta binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi nimekuwa nikisikia Wizara hiyo ikisema hapa na kupiga debe kuhusu ngozi, pamba, matunda, sukari, ndizi, mihogo hadi pilipili sijasikia hata siku moja Wizara hiyo ikizungumza kuhusu mchakato wa karafuu. Ni lini sasa Mheshimiwa Waziri ataanza kuweka hamasa ya kasi ili Zanzibar tupate kiwanda cha kuchakata karafuu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu sasa, kwa kuwa suala la viwanda ni la nchi nzima bila kujali suala la Muungano na kuna vitu ambavyo vimefanyika Zanzibar bila kujali suala la Muungano nikitolea mfano wa barabara iliyojengwa round about ya Amani hadi Mtoni ambayo ilijengwa kwa fedha ya Muungano na kupewa jina la Mkapa Road, kwa nafasi hii kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Kaskazini Unguja naomba tujengewe kiwanda cha karafuu Zanzibar ili vijana wetu wapate ajira. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge lile la kwanza ambalo litajibu na namba mbili, kuhamasisha uchumi wa viwanda nchi nzima ni jukumu la Wizara yangu na nitashirikiana na Mheshimiwa Mbunge twende Zanzibar niweze kuhamasisha kwa nguvu ileile ambapo nimeanzia sehemu nyingine. Katika utaratibu huo nitawahasisha wawekezaji ambao najua wapo kusudi tu- take advantage ya karafuu, mwani na michaichai kusudi tu- take advantage ya viungo hivi na manukato. (Makofi)
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, naishukuru pia Serikali kwa majibu mazuri, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa nini Serikali wasifikirie kutafuta wawekezaji ili wajenge viwanda huko Buhigwe au kiwanda huko Buhigwe cha kuongeza thamani kwenye zao la tangawizi ili wananchi waweze kunufaika zaidi kupata ajira na kadhalika badala ya kufikiria soko la kwenda Ulaya na Marekani peke yake?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, matatizo ya tangawizi Buhigwe yanafanana na matatizo ambayo yanatukumba kule Bukoba kuhusu vanilla. Vanilla ni zao ambalo liliingia Kagera likawa na mafanikio makubwa sana, likastawi vizuri na lilikuwa na bei nzuri sana, lakini hakukuwa na soko la zao hili kwa hiyo wananchi wameacha kulima zao hili. Je, Serikali ina mpango gani kusaidia wananchi hawa ili zao hili lifufuliwe na liongeze kipato kwa wananchi?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inashirikiana na wananchi kutafuta wawekezaji, mamlaka ya Mkoa kwa kushirikiana na SIDO na Tantrade inatafuta wawekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie, wawekezaji wa kiwanda cha tangawizi ni sisi wenyewe, kiwanda cha tangawizi kinahitaji pesa isiyozidi millini 200 au 500, hii watanzania wa kawaida wanaimudu. Kwa hiyo wawekezaji wa viwanda vya tangawizi millioni 200, 300, 400, 800 kiwanda cha kati sisi tunaweza.
Mheshimiwa Naibu Spika, namba mbili ambayo inaendana na namba moja, Mheshimiwa daktari kepteni ni kwamba nawasiliana na Mkuu wa Mkoa wa Kagera kati ya mwezi wa saba mpaka wa nane litaendeshwa kongamano kubwa la wafanyabiashara na wawekezaji. Na mimi ni mdau wa Kagera tutasimama wote nikitoka hapo nakwenda Kigoma nitakayoyasema Kagera nitayasema Kigoma tuchangamke sisi wenyewe tuwekeze.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda kwanza kutambua kazi kubwa inayofanywa na Serikali katika kuelekea katika uchumi wa viwanda, lakini ningependa kuuliza swali moja la nyongeza. Changamoto zinazokabili zao hili la tangawizi ni zilezile ambazo zinakabili zao la mchikichi.
Je, Serikali haioni ni wakati wa kuendelea kuongeza nguvu kuhamasisha wakulima waweze kuongeza uzalishaji wa michikichi na kujengwe kiwanda cha kuchakata na kusindika mawese ili kuweza kuongeza kipato kwa wakulima na kuleta manufaa kwa Taifa hili?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo, mpango wa Serikali kwa Mkoa wa Kigoma ni kuainisha kaya 100,000 ambapo kila kaya itapanda michikichi na tunawasiliana na Wabunge wa Kigoma akiwemo Mzee Nsanzugwanko na Mheshimiwa Peter Serukamba ili tuweze kupata vikonya vya kupandikiza kutoka nchi za Malaysia ambazo zitatumia kituo cha Arusha kuzalisha vikonya zaidi kusudi tuzalishe miche ya michikichi tuwagawie wananchi kwa bei nafuu tofauti na shilingi 5,000 ambazo mnanunua mchikichi, tunakuja Kigoma.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, pia nishukuru kwa kutembelea Singida, tulikuwa pamoja Singida, ninakushukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, zao la vitunguu maji ambalo linapatikana sana katika Mkoa wa Singida na hasa Mkalama nalo lina changamoto hiyo ya soko. Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuratibu uuzaji wa zao hilo la vitunguu ambapo naona sasa wananchi wanahangaika?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ninayoweza kumuahidi ni kwamba tutawafundisha zaidi wafanyabiashara namna ya kutafuta masoko, na watu wa Serikali ya Sudan Kusini wameonesha nia ya kununua bidhaa direct kutoka Tanzania. Vitunguu vyetu vilikuwa vinatoka hapa vinakwenda nchi nyingine, nchi nyingine inauza Sudan, kwa hiyo tutasaidiana kutafuta masoko, humu ndani na nchi kama nilivyoitaja hii ya Sudan.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuratibu hatutaweka mikono kwenye shughuli is a free market tutaliacha soko liende lenyewe lakini mimi na wewe tutawafundisha watu wetu mbinu za kuweza kutafuta masoko ya nje, kuna soko kubwa. Vilevile nichukue muda huu kuwaomba wafanyabiashara wote wa Tanzania, kuna soko la vitunguu na viazi mbatata mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwenye Kisiwa cha Pemba. Wajaze majahazi na vyombo vyote wapeleke, soko liko Pemba kule.
MHE. SAUMU H. SAKALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Pangani na Pwani ya Mkoa wa Tanga tunalima sana mwani. Sasa hivi wakazi wa Pangani wameacha kidogo kulima zao la mwani kutokana na kukosa soko. Sasa Mheshimiwa Waziri unatusaidiaje wakazi wa Pangani na Mkoa wa Tanga kwa ujumla katika zao hili la mwani katika kutuletea wawekezaji na soko pia? Mwani unalimwa baharini, ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia fursa nijibu swali la Hajat Saumu. Ilibidi aweke kiangalizo kunieleza mwani inalimwa wapi, mimi kwetu ni Pemba mama yangu anaitwa Mariam huyu unamfahamu, kwetu ni pemba kwa hiyo na mimi mambo ya mwani nayajua.
Mheshimiwa Mbunge ni kwamba nilikuwa Tanga juzi kwenye maonesho ya Kimataifa. Tija ya mwani ni kutengeneza kiwanda cha kuongeza thamani, na kiwanda cha kuongeza thamani ni kiwanda kidogo ambacho Mheshimiwa Mbunge unakimudu. Ninapoendelea na juhudi za kuhamasisha viwanda vidogo na vile vya kati, tunakwenda Tanga kuhamasisha namna ya kuongeza thamani kwenye mwani, hiliki na mdalasini ili tuweze kupata soko. Soko la bidhaa za wakulima ni kuziongezea thamani.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwa kuwa demand ya zao hili la tangawizi imekuwa kubwa sana, kama Mheshimiwa Waziri alivyokiri hata majirani zetu Njombe wanalima zao hili, sasa ni mkakati gani wa makusudi ambao Serikali imeweka kuhakisha tunawajengea uwezo hawa wakulima wetu ili kilimo chao kiwe na tija? Ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wa Tanzania wana uwezo na wanaelewa, kinachoamua ushindi ni mahitaji ya soko (the market pool). Kwa hiyo tulichofanya, jambo la kwanza; Serikali kwa kushirikiana na Mbunge Mheshimiwa Anne Kilango tunaweka bilioni 1.7 kwenye kiwanda cha Tangawizi cha Same, tuchukue tangawizi yote tuichakate Same, tuweze kwenda kwenye soko. Soko likivuta zaidi wananchi watavutiwa na bei na watazalisha. Watanzania wanajua kinachoamua ni soko, panapokuwa na bei nzuri wananchi watazalisha hawahitaji ruzuku yoyote.
Kwa hiyo tunamuwezesha mama Kilango makusudi, tumempa bilioni 1.7 kiwanda kile cha Same kifanye kazi tutachukua tangawizi yote ikonekana mahitaji zaidi tutaweka Buhigwe, tutakwenda Ileje tutaweka kiwanda basi viwanda vitakuwa vinasababisha wananchi wanalima zaidi.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu yaliyo chini ya kiwango ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Saed Kubenea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza liliuliza kwamba mpaka sasa kasi ya kufufua viwanda imefikia wapi? Kwa hiyo, kwa majibu hayo inahitaji tujue kwamba Waziri yuko tayari kukiri kwamba kiwanda hiki hana mpango wa kukifufua kwa maelezo aliyotoa hapa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mpaka sasa anaamini kwamba kauli mbiu ya Serikali ni kuinua viwanda au kuua viwanda? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya Serikali iliyofanyika imeandikwa kwenye jibu langu ni kufanya utafiti; na mwaka jana nilipewa shilingi milioni 150 kwa ajili kufanya utafiti na umakamilika kwa hiyo kazi niliyopewa nimemaliza. Kazi ya Serikali ni kujenga viwanda na viwanda vitaendeshwa na Sekta binafsi, mwaka unaokuja 2017/2018 nimeomba pesa shilingi milioni 70 tu nitangaze tender sekta binafsi ifanye kazi.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kuwa ya jumla kwa sababu swali nililouliza nilitaka nijue kama Momba kitapatikana kiwanda, kitajengwa au hakitajengwa. Kwa hiyo, jibu ni kwamba wananchi wa Momba huko mnakonisikia hamna kiwanda kitakachojengwa na Serikali ya Awamu ya Tano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu ya Mheshimiwa Waziri yanaainisha kwamba jukumu la ujenzi wa viwanda ni la sekta binafsi, lakini kauli za Serikali na viongozi wa Serikali mitaani huko, kila siku statement ambazo wamekuwa wakizitoa ni kwamba Serikali inajenga viwanda. Ni kwa nini sasa Serikali isibadilishe kauli yake ikawaambia wananchi jukumu la kujenga viwanda sio la Serikali, Serikali kazi yake ni kuwezesha mazingira wezeshi kama ambavyo mmekuwa mkitamka hapa. Ninayasema haya kwa sababu tumekuwa tukisia hapa…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio nataka niulize kabisa kwamba kwa nini sasa wasibadilishe hiyo kaulimbiu kwa sababu mind set ya wananchi ni kwamba Serikali inajenga viwanda wakati ukweli ni kwamba Serikali haijengi viwanda?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali imejinasibu hapa kwamba inaweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi pamoja na wafanya biashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ninachotaka nijue jitihada za Serikali juu ya hawa watu wa sekta binafsi kwa sababu moja kumekuwa na malalamiko, mazingira wezeshi kwa mfano huko Momba barabara mbovu, maji hayapatikana, umeme unayumbayumba, mitaji hakuna, riba zimekuwa zinapitiliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka nijue jitihada za Serikali kukabiliana na changamoto hizi ili hii sera ya viwanda iweze kuwa inatekelezeka.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo linalofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano si la kuamka na kufanya. Tunafuata Dira ya 2025, tunafuata Mpango wa Pili wa Miaka Mitano na tunafuata maelekezo ya Mheshimiwa Rais. Imeandikwa katika Mpango wa Pili wa Miaka Mitano kwamba Serikali jukumu lake ni kuweka mazingira wezeshi na kazi ya sekta binafsi ni kujenga viwanda. Sasa sisi Tanzania sisi Serikali ya Awamu ya Tano tunajenga viwanda sisi sekta binafsi sisi ni Serikali tunakwenda pamoja huwezi kutenganisha sekta binafsi na Serikali. Huyo anatengeneza mazingira wezeshi huyu anajenga. Huyu anachota maji, huyu anasonga ugali wote mnapika chakula. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Silinde rafiki yangu usisahau umeme wa Momba kama si Serikali, kama sio mimi nikiwa Naibu wa Nishati usingefika. Tumefyeka msitu, sasa ushukuru kwa kidogo ulichopata nije nikupatie kingine.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri; ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na taarifa za viwanda tunazozisoma na kuzisikiliza kila siku, kwa jibu ni kuwa Kagera bado tuko nyuma katika viwanda. Sasa nini mpango wa Wizara yako kushirikiana na mimi pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kagera kuhamasisha ujenzi wa viwanda?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wananchi wa Kagera wajasiriamali wadogo wadogo ili waweze kupata mikopo ya riba nafuu ili waweze kufungua viwanda?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, jitihada za uhamasishaji zinaendelea, shughuli zinazofanywa na Wizara ya Mifugo za kuondoa uvuvi haramu zinalenga kuona kwamba katika ziwa letu tunapata samaki wa kutosha ili viwanda vya samaki viweze kujengwa. Lakini yako makampuni ambayo tumeshawasiliana nayo, kiwanda cha kutengeneza maziwa kitajengwa Kagera. Pia kampuni moja kutoka Uganda ya Uvan inataka kujenga kiwanda cha vanilla. Suala la uhamasishaji ni endelevu.
Nipende kukuahidi wewe na Wabunge wenzangu na wananchi katika Mikoa ambayo nataka kufanya kazi nayo ya uhamasishaji ni pamoja na Kagera, Kigoma, Mara, Katavi na Ruvuma. Katika miezi minne ijayo tutafanya kampeni kubwa…
…ya mazao ya shamba ambayo tunataka kuyaimiza yaweze kuzalisha bidhaa za viwandani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuwawezesha wananchi akina mama na akina dada kifedha…

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba tunao mfuko wa NADef. Jambo la muhimu si pesa, jambo la muhimu ni kwenda kupata idea na kupata mawazo SIDO. Mkishapata mawazo kupitia SIDO mtanufaika na mfuko wa NADef lakini iko mifuko mingine ambayo iko chini ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nitakapozindua kitabu cha mwongozo wa kujenga viwanda kwa local government katika bajeti yangu siku ya Alhamisi kitabu hicho kitagawiwa mtaweza kujua pesa zinapatikana wapi.( Makofi)
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Mheshimiwa Waziri ambayo na mimi nakubaliana nayo, lakini mafanikio haya yapo hatarini kupotea kabisa ama wafanyabiashara wasio waaminifu wataendelea kungiza sukari nchini kama wanavyofanya hivi sasa na kufanya repackaging ya sukari hiyo kwenye mifuko wakisingizia kwamba imezalishwa hapa nchini wakati sio. Na hivyo kusababisha viwanda kukosa soko kama ambavyo inatokea kwa Kagera Sugar hivi sasa wamezalisha sukari, imejaa kwenye maghala, hawana sehemu ya kuiuza. Je, Serikali inalitambua hilo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kama Serikali inalitambua hilo ni hatua zipi inazichukua kuhakikisha usemi wa kwamba Tanzania tunajenga Tanzania ya viwanda, tujenge kweli Tanzania ya viwanda kwa kulinda viwanda vyetu, lakini si kusema tunasema tunajenga ya viwanda huku tukiruhusu wafanyabiashara wasio waaminifu wanaingiza sukari ndani ya nchi, na wanafanya repackaging wanaua viwanda vyetu?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tunayo sukari nyingi kwenye viwanda vyetu. Kiwanda cha Kagera Sugar kina sukari na imerundikana nje kama ambavyo mmeona kwenye vyombo vya habari. Hali ni hiyo hiyo Kilombero na TPC. Kwa majibu ya swali la kwanza na la pili Serikali tunatambua na kikosi maalum cha Serikali kinafuatilia na kwa ruhusa yako ningeomba nisiende zaidi kwa sababu katika kinachofanyika kuna jinai ndani yake na vyombo vya dola vinafuatilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwambia wawekezaji wote wa viwanda vyetu Serikali inawafuatilia na itawalinda na wale wanaochezea viwanda vyetu nataka niwahakikishie uchunguzi ukikamilika tutachukua hatua kali. Fair Competition wako kazini, TFDA wako kazi, TAKUKURU wako kazini na watu wa TRA wako kazini. Ni timu makini na niwaeleze kwa utangulizi hili suala lina jinai na anayehusika atakiona cha moto. (Makofi)
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nimuombe tu Mheshimiwa Naibu Waziri anisikilize kwa makini kabisa, ninachokizungumza ni Kiswahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri, Muungano wetu huu tumeungana watu nchi mbili, Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Watu wa Tanganyika ndiyo maana jina likapatikana likaitwa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenkiti, kati ya mambo waliyokubaliana yalikuwa ni biashara na viwanda na swali la msingi linahusu viwanda vilevile. Nataka sababu za msingi nijue Kiwanda cha Sukari cha Mahonda hata Wabunge tungesimama mara nyingi mjue kuwa hili suala limetukwaza ndani ya moyo wetu. Bidhaa zinazotoka Tanzania Bara zinakwenda Zanzibar bila kigugumizi, leo viwanda vya Zanzibar kuzalisha na hii Jamhuri inaitwa Tanzania hebu tuelezeni ukweli Kiswahili tuweze kufahamu kwa nini maziwa ya Bakhresa hayawezi kufika hapa yanakwama na huku tukishuhudia wakati mwingine sukari inatoka nje mnaacha kununua kutoka Zanzibar. sababu gani zinasababisha bishaa hizo kupata kigugumizi. Za Tanzania Bara zinaingia Zanzibar, za Zanzibar kuja huku imekuwa kitendawili? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo Kamati kati ya Waziri wa Biashara wa Tanzania (mimi) na mwenzangu wa Zanzibar. Yamekuwepo malalamiko ya wafanyabiashara na kupitia vikao hivyo tunakaa chini na kujadili suala la Kiwanda cha Maziwa cha Bakhresa kilichopo Zanzibar mimi mwenyewe nimekwenda nikakiangalia. Nikakitembelea kiwanda kile, nikaangalia uzalishaji wao ni mzuri na maziwa yamekuwa yanaingia. Tulichokubaliana ni kwamba mtu anapopata tatizo la kukwazwa na watendaji ilitolewa namba maalum na kikao cha Mawaziri wawili kwamba anayekwamishwa awasiliane na mamlaka. Kama kuna tatizo kuhusu maziwa mnijulishe mimi kusudi mimi niende kuwa-task wale wanaohusika. Lakini hao wawekezaji wenye viwanda napenda nikiri kwamba ninashughulika nao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye Kiwanda cha Sukari cha Mahonda. Serikali imeamua kusimamia Sekta ya Sukari kwa sababu kupitia sukari tunataka kuzalisha ajira. Kwa sababu ya nia ya kuzalisha ajira na kwa sababu ya fursa ya ajira katika sekta ya sukari hii sukari ni classified product na sasa hiyo Tume ninayowaeleza ikimaliza kazi ndiyo mtakuja kujua maana ya classified product kwamba sukari inakuwa classified. Kiwanda cha Mahonda wake wa kuzalisha ni tani 4,000 mahitaji ya Zanzibar ni tani 20,000. Mimi nawasiliana na watu wa Zanzibar, Waziri wa Zanzibar kwamba azalishe 4,000 auze kwao. Ndiyo!
…ninachozungumza ndiyo…, ngoja niwaeleze…
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Waheshimiwa Wabunge wanataka kujua ninachokisema.
Ningeomba muwape fursa wale wanaotaka kunisikiliza niwaeleze suala la Mahonda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niku-address wewe Mahonda inazalisha tani 4,000. Itakapokuwa imezalisha tani 4,000 inataka kuziuza katika soko la Tanzania Bara haitazuiliwa, tutakaa chini tuzungumze, lakini huwezo kuwa unazalisha tani 4,000 lakini wewe soko lako ni tani 20,000 halafu wewe unakwenda kuuza tani 4,000 nje hizi nyingine unazipata wapi? Kwa hiyo, ndiyo utaratibu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa taarifa katika Bunge, tunataka ku-classify sukari. Mafuta ya kula ni classified, sukari itakuwa classified kwa sababu tunataka ajira. Niko tayari kulisimamia hilo mpaka nitakapoambiwa vinginevyo. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, mazao haya ya pareto na vitunguu saumu na hata vitunguu maji ambavyo vinalimwa katika maeneo ya Mbulu na Karatu, wakulima wamekuwa wakiuza kwa vipimo vya debe badala ya kilo, na sheria ya vipimo inataka mazao haya yauzwe kwa kilo. Je, kwa nini Serikali isihakikishe kwamba mazao haya yanauzwa kwa kilo badala ya madebe?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kumekuwa pia kuna changamoto ya wafanyabiashara kufuata mazao haya shambani jambo ambalo linamfanya mkulima ananyonywa na asipate faida ya kile anachokilima, hasa mazao ya vitunguu maji ambayo yanalimwa sana kwenye Tarafa ya Eyasi, Wilayani Karatu, lakini pia maeneo ya Mbulu.
Je, Serikali sasa mna mkakati gani wa kuhakikisha kunakuwa na centeres za uuzaji wa mazao haya ili mkulima aweze kufaidika na mazao anayoyalima? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, kuhusu kutumia ujazo na uzito katika kupima mazao, marekebisho ya Sheria ya Vipimo Namba. 340 iko mezani kwangu na nimekataa kuisaini ilivyoletwa nikitaka twende kwa uzito, tupime kwa uzito. Nakubaliana na wewe na sitasaini mpaka wataalam wangu wakubaliane twende kwa uzito. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu vituo vya kuuzia mazao, napenda nimueleze Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote, wakulima wetu tuwahimize warudi kwenye ushirika, washikamane kuwadhibiti wale wanaokuja kunyemelea mazao. Local Government (TAMISEMI), wameshaanza zoezi la kuwa na centers ambako tutaweka mizani, lakini tukiwa na ushirika hao wanaonyemelea ambao wakulima tutaweza kuwadhibiti. Kwa hiyo, ni jukumu letu muisaidie Serikali sisi ndio Serikali twende pamoja tutaweza kuwasaidia wakulima wetu.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kukiri kuwa Tanzania hakuna uhaba wa sukari katika majibu yake na amesema baada ya miaka mitatu au minne uhaba huu utapungua hiki ni kiswahili alichokiandika.
Mheshimiwa Spika, mara kadhaa tukifika katika mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani pamekuwa na kadhia hii ya upungufu wa sukari. Haioni Serikali imefika wakati ipunguze punguzo hili ili kuwalinda wananchi ukizingatia wananchi ndiyo waliyoweka Serikali hii madarakani na si aibu viongozi wetu Zanzibar hao Marais wetu mara nyingi ikafika mwezi Mtukufu wa Ramadhani huondoa ada hii na Tanzania Bara imeiga mambo mengi kutoka Zanzibar ikiwemo vyama vingi vimeanzia Zanzibar, haki za binadamu zimeanzia Zanzibar, matumizi ya dola yameanzia Zanzibar si aibu kuiga. (Makofi)
Je, haioni imefika wakati kuiga formula hii mara kadhaa unalinda viwanda, viwanda hivyo haviwezi kulindika wakati huu?
Mheshimiwa Spika, la pili tumo kwenye Tume ya Afrika Mashariki, lakini mpaka leo bidhaa za Zanzibar haziwezi kufika kwenye soko hilo mpaka upitie Tanzania Bara. Je, haijafika wakati Tanzania Bara mkatamka kwa Zanzibar sasa hivi isiingie katika soko hili kwa kupitia mgongo huo?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi nimeeleza kwanini, sukari inayozalishwa Tanzania Bara inakuwa na gharama kubwa. Nimesema tumeamua kusimamia viwanda hivi ili tuweze kuzalisha ajira. Sasa kuhusu kupunguza nimeeleza kwamba ushuru kwa makubaliano yetu ya East Africa ni asilimia 100, tumepunguza kutoka asilimia 100 kuja 25 tumeshapunguza kuja asilimia 25. Kuhusu bidhaa ya Zanzibar kama kuna mfanyabiashara ana matatizo awasiliane na Waziri wa Zanzibar ambaye mimi na Sekretarieti inawasiliana naye. Mimi Zanzibar sina matatizo bidhaa zinakuja zinaingia nchini kama mtu hafuati viwango ana matatizo yake. Lakini TBS ya Tanzania Bara na Viwango vya Zanzibar wanawasiliana haya mambo madogo madogo myawasilishwe kwa watendaji kule na watendaji watayashughulikia, ahsante.
MHE. SALIM HASSAN ABDULLAH TURKY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona pamoja na majibu mazuri sana ya Waziri. Lakini katika majibu haya kuna swali la msingi ambalo Waziri naona kalikimbia, nalo ni kwamba Zanzibar kuna kiwanda cha sukari kinazalisha na kinauza sukari ile kwa shilingi 65,000 na hawaagizi sukari kutoka nje wao wamewekeza wanazalisha sukari wanauza shilingi 65,000 kwa wananchi wa Zanzibar.
Mheshimiwa Spika, swali la msingi ni kwamba viwanda vyetu vya Bara kwa nini hawawezi kutushushia bei saa hizi na ushahidi kamili ni huu ambao natoa na Bunge hili lisikie sasa hivi. Ni kwamba sukari sasa hivi katika soko la dunia linauzwa kwa bei ya dola 390, ukilipa kodi ya asilimia 25 na VAT asilimia 18 sukari hiyo inasimama kwa bei shilingi 65,000, leo Watanzania tunalanguliwa kwa kuuziwa sukari hiyo shilingi 110,000 kwa misingi gani? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, na hapa hapa tuliomba cost of production ndani ya Bunge hili wakati Naibu Waziri akiwa Malima toka mwaka ule mpaka leo cost of production ya viwanda hivi hatujaletewa ndani ya Bunge hili jamani. (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, nimejitahidi kulieleza suala hili ila muda wenyewe hautoshi. Ni kwamba gharama za uzalishaji kwa viwanda vya Bara ziko juu kuliko Zanzibar, naomba nimepewa muda, muache niwaeleze.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, Zanzibar sukari haitoshi kwanza.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Spika, naomba niwaeleze hili suala sio rahisi namna hiyo mnavyofikiria, ndiyo siyo suala rahisi, I am very good in talking a can talk, simple rahisi, Mheshimiwa Turky ulipopewa kibali na Serikali kuagiza sukari kwa nini wewe ukuuza bei rahisi? (Kicheko)