Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Innocent Edward Kalogeris (10 total)

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na idadi kubwa ya vifo ya karibu watu 60 ndani ya mwaka mmoja na watu 30 kupata vilema vya kudumu, Serikali inakuja na majibu ya kusema kwamba inafanya tathmini. Ni tathmini gani ambayo inataka kuifanya ili kujiridhisha ili waende wakavune na ni lini watakamilisha hiyo tathmini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, ni lini Serikali itatoa kifuta machozi kwa watu ambao ndugu zao wamefiwa au wameliwa na mamba na wengine wamepata majeruhi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ufafanuzi katika eneo la kufanya tathmini. Maeneo ambayo anayaongelea Mheshimiwa Mbunge ni maeneo ambayo kiuhalisia, ni maeneo ya Mito na maeneo mengi ya Mito mamba wengi wanapenda kuishi maeneo hayo. Sekta ya Maliasili na Utalii tunahifadhi maeneo mbalimbali ambayo yanakuwa yamehifadhiwa. Lakini maeneo ya Mito ni maeneo ya mtiririko ambapo ukiangalia Mto kutoka eneo moja kwenda lingine ni eneo refu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunafanya tathmini kuangalia namna ya hawa mamba wanavyoishi majini kwa sababu, wanasafiri wanatoka njia moja kwenda njia nyingine. Unaweza ukamuona mamba yuko Morogoro lakini baada ya muda fulani ukamkuta yuko Pwani au yuko Mkoa wa Dar es Salaam. Kwa hiyo, tunafanya tathmini kuangalia hii namba ya hawa mamba ni kubwa kiasi gani. Kwa sababu, nao wana umuhimu fulani ambao katika maeneo hayo wanapaswa kuwepo sio kuwaondoa kabisa, kwa sababu vile vile, hiyo tunatambua kwamba ni moja ya maliasili ambayo inapaswa kuhifadhiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo, tukishakamilisha tathmini tutaangalia kama idadi ni kubwa basi tutawavuna. Swali la kwamba ni lini ni pale ambapo tutakamilisha tathmini ambayo sasa hivi mchakato wake tumeshaanza na kama ambavyo nimesema ni Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Katavi na Rukwa ambako ndio inasemekana kuna mamba ambao wanasumbua sana. Ikishakamilika tu ndani ya mwaka huu wa fedha tutawavuna ama kuwapunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine ameongelea kuhusu kifuta machozi nimtoe wasiwasi tu Mbunge kwamba, suala la kulipa kifuta machozi tumelianza toka mwaka wa fedha ulioisha na sasa hivi kuna maeneo yanaendelea kulipwa. Kwa hiyo, hata kwenye eneo lake kama wananchi hawajapata kifuta machozi basi ninawaelekeza Idara ya Wanyama Pori, wataenda katika eneo hili na wataenda kulipa wale wananchi ambao wameathirika na tatizo hili. Ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiofichika kwamba ujenzi wa uwanja wa kisasa wa michezo na shughuli za Serikali kwa Makao Makuu ya Dodoma haukwepeki. (Makofi)

Je, Serikali pamoja na majibu ya kusema kutafuta wabia, wadau mbalimbali wa michezo, kwa nini Serikali isiwe na commitment kwamba mwakani katika bajeti tunatenga fedha ili ujenzi huo uanze, ukitilia maanani uwanja hauwezi kujengwa kwa mwaka mmoja?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Innocent kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwisha kujipanga na ndio maana tumeshafanya upembuzi yakinifu kujua kwamba huu uwanja tunaujenga wapi, lakini kwa gharama gani. Huu uwanja unahitaji zaidi ya shilingi bilioni 420 na Serikali tuko kwenye hizo hatua pamoja na maongezi yanayoendelea lakini ndani ya Serikali tunaendelea kutafuta fedha.

Mheshimiwa Spika, nihakikishie Bunge hili tukufu huu uwanja pia ni ahadi ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 na lazima tutaujenga.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri sana ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

La kwanza; uhitaji wa vyumba vya madarasa na mabweni katika shule za sekondari ambazo ziko pembezoni katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini ni mkubwa kama vile Shule ya Sekondari Kasanga, Bwakila Juu na Singisa.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi wa Morogoro Vijijini katika kata tajwa katika ujenzi wa vyumba vya madarasa na mabweni ili kuwaondolea wanafunzi adha ya kutembea mwendo mrefu, lakini vilevile msongamano darasani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuona ni kuamini; je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kuongozana na mimi kwenda katika kata tajwa ili kujionea kwa uhalisi tatizo kubwa tulilokuwa nalo na kuweza kutusaidia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango wa Serikali ni kuhakikisha kata zote za pembezoni tunazifikia kwa kujenga shule, lakini vilevile kwa kuongeza madarasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba kata hizo tutazifikia, na mimi niseme tu kwamba nitakwenda na nitaongozana naye kwenda kushuhudia katika hayo maeneo. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kiuhalisia, ongezeko la Mawakala wa Bima linatokana na vijana wengi waliomaliza elimu ya fani ya bima nchini kuamua kujiajiri wenyewe baada ya kukosa kazi Serikalini: -

Mheshimiwa Spika, je, ni utafiti gani wa kina ambao umefanyika na Serikali hadi kujua kwamba ongezeko hilo linatokana na mfumo wa biashara ya bima kukua?

Mheshimiwa Spika, je, ni utafiti gani ambao mmeufanya katika kujua mawakala vijana ambao wamefunga biashara baada ya kushindwa biashara kutokana na ushindani mkubwa wa biashara ya bima ambao umevamiwa na benki pamoja na kampuni za simu? (Makofi)
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa maswali mazuri. Moja, hivi tunavyoongea mpaka sasa, upande wa masuala haya ya bima hapa nchini ziko takribani asilimia 16 tu, ndiyo tunapata ushiriki wa vijana ambao wako chini ya umri wa miaka 18 na utafiti huo uliofanywa na Finscope ulionesha hivyo. Sasa katika nchi ambazo zimeendelea na kule tunakoelekea tunatamani angalau tufike asilimia 84 au zaidi ya hapo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu utafiti wa mawakala, taarifa ambazo zilikusanywa kwa miaka kadhaa kama nilivyotoa pale mwanzo, zinaonesha kwa mwaka 2020 walikuwa zaidi ya 700, lakini kwa sasa tumeshazidi 930. Kama tumeshazidi 930 hii inaonesha kwamba bado pana fursa ambapo vijana wote wanaweza wakashiriki na bado mafanikio yakapatikana bila wao kuzuiliwa kwa sababu ya uwepo wa BenkiWakala.

Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo, TIRA ilishatoa mwongozo ambao unaweka mipaka ambayo inaonesha ni namna gani italinda BenkiWakala zisilete athari kwa Mawakala hawa wa kawaida ambao wanaendesha shughuli hizo. Tunaamini kwamba biashara hiyo itaendelea kusambaa zaidi kwa wananchi walio wengi zaidi. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali pamoja na kupeleka fedha ile shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni na kazi inaendelea bado kuna uhitaji wa walimu pindi kazi itakapokuwa imekamilika. Vilevile kuna uhitaji wa uzio ili kuweza kuweka usalama kwa watoto hao wenye mahitaji maalum. Je Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha hizo na walimu pindi kazi itakapokamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Mheshimiwa Naibu Waziri uko tayari kufanya ziara katika Jimbo la Morogoro Kusini na kuandamana na mimi ili kwenda kuangalia mahitaji mengine ya elimu na afya katika halmashauri yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu maswali yake haya mawili kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge Mheshimiwa Kalogeris kwa sababu jambo hili ni wiki iliyopita tu alikuja kulifatilia pale ofisini kuhakikisha kwamba wanapata walimu. Nimuhakikishie mbele ya Bunge lako Tukufu nikijibu swali lake la kwanza kwamba katika ajira hizi ambazo zimetolewa kibali na Mheshimiwa Rais kuweza kuajiri tutahakikisha shule hii kwa sababu ni watoto wenye mahitaji maalum wanapata walimu wa kuweza kuwafundisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili nipo tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge mpaka kwenda Jimbo Lake la Morogoro Kusini kwenda kuitembelea shule hii na tuone ni nini kinaweza kikafanyika na Serikali kwa ajili ya kujenga uzio ambao ameuzungumzia Mheshimiwa Mbunge pale.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali, pamoja na Serikali kuendelea kutenga fedha nyingi kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini, bado kuna uhitaji mkubwa wa fedha ambazo ningependa Serikali itenge.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kwenda na mimi akaangalie mazingira ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini ili iwe rahisi kwa Serikali kuendelea kutenga fedha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua kwamba Jimbo la Morogoro Kusini linahitaji fedha zaidi kwa ajili ya utekelezaji wa barabara hizi. Ndiyo maana katika kipindi cha miaka ya fedha mitatu mfululizo, Serikali imeendelea kuongeza bajeti ya barabara katika jimbo hili lakini pia katika majimbo yote.

Mheshimiwa Spika, namhakikishia kwamba nipo tayari kuambatana naye kwenda katika Jimbo la Morogoro Kusini. Tutakubaliana baada ya maswali haya ili tupange, baada ya Bunge tuweze kwenda na kuona hali ilivyo, lakini pia kushirikiana katika kuboresha huduma hiyo, ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itapeleka pesa kukamilisha mradi wa Lubasazi Kata ya Kolelo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema ninayo orodha ya miradi mingi ambayo tunaitekeleza hivi sasa inawezekana nitashindwa kumpa moja kwa moja mradi wake katika hatua iliyofikia lakini mimi nitakaa naye ili tuangalie katika jedwali letu tuone kama mradi huo haupo basi tuweke katika vipaumbele vyetu.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza utalii ukanda wa kusini, Kata ya Kisaki kuna eneo linaloitwa Kisaki Majimoto ambapo kuna chemchemi inayochemsha maji kiasi hata cha kuweza kulifanya yai likaiva, je, Wizara ina mpango gani wa kutambua eneo hilo na kuliingiza katika kivutio cha utalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mkakati wa Wizara ni kuhakikisha maeneo yote ambayo yana vivutio vya kihistoria ikiwemo Majimoto; tuna maeneo mengi ambayo yana majimoto na eneo ambalo anatoka Mheshimiwa Mbunge, lakini tuna maeneo mengine mengi ambayo yana vivutio ambavyo bado hatujaviibua. Tunataka kila Mkoa, kila wilaya angalau mtalii yoyote anayefika katika eneo hilo, basi aweze kuona kivutio kilichopo katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mkakati tulionao ni mkubwa, tunachotafuta sasa hivi ni fedha ya kutosha ili mambo yasonge mbele.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, nini mpango wa Serikali katika kupeleka umeme katika Shule ya Sekondari ya Tawa katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Kalogeris, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tayari tuna miradi ambayo inaendelea kwenye kila Mkoa kuhusiana na kupeleka umeme. Nitafuatilia kuona kama Shule ya Sekondari Tawa ipo katika mipango ambayo tunayo, na kama hamna, basi tutafanya jitihada za ziada, ili kuhakikisha Shule ya Sekondari Tawa inapatiwa umeme, ahsante.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali na hasa, sasa tunakwenda kujenga Mahakama katika Tarafa ya Bwakira Kata ya Bwakira Chini. Naipongeza Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Tarafa ya Bwakira Chini kuna hakimu ambaye anaitwa Deogratius Amatungiro, ni Hakimu ambaye amegeuza Mahakama kama duka la kuuza haki kwa wananchi kiasi ambacho wananchi wa Tarafa ya Bwakira Chini wamemchoka: Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari kwenda nami katika Kata ya Bwakira Chini, Kata ya Kisaki na Kata ya Mngazi ambayo ndiyo Tarafa ya Bwakira, ukasikilize malalamiko ya wananchi? Kwa sababu viongozi mbalimbali wamepita lakini hakuna hatua yeyote ambayo imechukuliwa ili yeye kama msimamizi au ndiyo msimamizi katika Mahakama na Wizara ya Sheria uondoke naye huyo hakimu kwa sababu tumemchoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini tunatarajia kwamba hiyo Mahakama ya Bwakira Chini itaanza kujengwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru, naomba sasa nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameuliza ni lini Mahakama hii katika Kata ya Bwakara Chini itajengwa? Nilijibu katika majibu yangu ya msingi kwamba mwaka huu wa fedha mhimili wetu wa Mahakama imetenga kujenga Mahakama za Mwanzo zaidi ya 60 na tuna zaidi ya shilingi bilioni 88 ambazo Bunge hili wametupititishia. Kwa hiyo, Mheshimiwa Innocent Mahakama hii tunajenga mwaka huu na ndiyo maana nimesema Mkandarasi sasa anatafutwa ili kazi hii ianze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, amemlalamikia Mheshimiwa Hakimu katika Mahakama hii ya Bwakira ambayo tunakwenda kujenga, japo inaendelea katika eneo la godauni. Naomba nimwelekeze Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wenzangu kwamba tuna Kamati zetu za Maadili kwa Maafisa wa Mahakama na Wenyeviti wa Kamati hizi ni Ma-DC wetu katika Wilaya zetu lakini na Waheshimiwa Ma-RC. Kwa hiyo, Mheshimiwa Innocent kwa kuwa kanuni zetu zinatuhitaji, kama kuna malalamiko yoyote kwa Maafisa wetu wa Mahakama, tunapaswa kuandika kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge aandike kwa maandishi ampelekee Mheshimiwa DC wa Morogoro ili Kamati ya Maadili ya Maafisa wa Mahakama katika Wilaya yake sasa waanze uchunguzi, na kama kuna tuhuma zitakuwa zimethibitika, basi hatua zitachukuliwa, ahsante.