Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from hon Hassan Seleman Mtenga (1 total)

MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumwuliza swali Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuwa nchi yetu imeamua kuongeza wigo wa diplomasia wa uchumi kwa kufungua milango ya kibiashara na kimawasiliano: Ni upi mkakati wa Serikali katika kutekeleza miradi ya ujenzi wa madaraja yanayounganisha nchi kuendana na uchumi ambao sasa tunautarajia katika nchi yetu?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mtenga, Mbunge wa Mtwara Manispaa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua mpango wa Serikali wa kuimarisha ujenzi wa madaraja kwa lengo la kuimarisha diplomasia ya kiuchumi na mawasiliano kati ya nchi yetu na nchi jirani. Mkakati wa Serikali katika kuimarisha diplomasia ya kiuchumi na mawasiliano ni mkakati endelevu na hakika kwenye eneo hili lazima nimpongeze kwanza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ameifungua nchi kwa kuimarisha diplomasia ya kiuchumi na mahusiano na mataifa mengi duniani na tumeanza kuona manufaa ya marafiki wengi kuja nchini kuwekeza katika maeneo mbalimbali. Hii inatokana na jitihada hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mpango wa kuendelea kujenga daraja. Najua anachotaka kukiuliza ni nini? Wiki mbili zilizopita nilikuwa Mkoani Mtwara, na moja kati ya jambo ambalo yeye aliliuliza hadharani ni ujenzi wa daraja wanalolihitaji wakazi wa Mkoa wa Mtwara kwenda nchini Msumbiji. Tuna madaraja mengi. Kule Mkoani Mtwara tuna Daraja la Umoja lile linalotoka Wilaya ya Nanyumbu kwenda Msumbiji. Linaitwa Daraja la Umoja, daraja zuri, kubwa, linalounganisha hizi nchi.

Mheshimiwa Spika, pia tuna madaraja mengine; kule Mkoani Mbeya Wilaya ya Kyela tuna daraja pale Kasumulu, linaunganisha na Malawi; Ileje tuna daraja la Mto Songwe linaunganisha na Malawi pia; na kule Ngara tumefanya ziara kwenye mradi mkubwa wa umeme wa Rusumo, tuna daraja kubwa linaungfanisha na Rwanda. Tunatarajia kuimarisha ujenzi wa madaraja haya ikiwemo na Mkoa wa Mtwara.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa za Wizara ya Ujenzi kupitia Meneja wa Mkoa wa Mtwara wa TANROAD alituhakikishia kwamba liko eneo la Mtwara Vijijini ambalo ndiyo karibu zaidi na Msumbiji, karibu zaidi na maeneo ambayo yana huduma nyingi za kibiashara na mkoa mmoja unaitwa Cabo Delgado, moja kati ya mikoa iliyoko nchini Msumbiji kwamba tayari wameshaanza upembuzi yakinifu ili kujenga daraja kwenye eneo la Kikole, Kikombo ambalo pia litakwenda mpaka Msumbiji. Huo ndiyo mkakati wa kuimarisha ile diplomasia ya kiuchumi na Msumbiji na diplomasia ya mawasiliano na msumbiji kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anatoka Mkoa wa Mtwara alisisitiza kwamba Wanamtwara wanahitaji zaidi.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa daraja hili siyo kwa Wanamtwara tu, ni taifa zima, kwa sababu sisi na Msumbiji tuna mahusiano na maeneo yote yanayohitaji kujengwa daraja, maeneo yote ambayo yanahitaji kuimarishwa vivuko, na maeneo yote yanayohitaji kuimarishwa malango ya uhamiaji kwa lengo la kujenga mahusiano rahisi na nchi jirani ili kuimarisha uchumi na mawasiliano kwenye nchi hizi.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imelichukua jambo hili na kuendeleza jitihada hizi ambazo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wetu amezianzisha na tunataka tuone sasa Watanzania wananufaika na diplomasia hii ya kiuchumi na mawasiliano na nchi jirani na nchi zote ambazo zinajenga mahusiano mazuri na Tanzania.

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo mkakati ambao tunao kwa sasa kwenye eneo hili la kuimarisha mahusiano na hasa kwenye maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge anahitaji zaidi Serikali ianze kujenga daraja la kwenda nchini Msumbiji, ahsante sana. (Makofi)