Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Kwagilwa Reuben Nhamanilo (1 total)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kumekuwa na kubadilika badilika kwa wakusanyaji wa kodi ya ardhi ndani nchi yetu kwa maana ya Serikali, kuna wakati kodi ya ardhi imekuwa ikikusanywa na TAMISEMI na kuna wakati kodi ya ardhi imekuwa ikikusanywa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na wakati mwingine kodi hii imekuwa ikikusanywa na TRA.

Mheshimiwa Spika, kubadilika badilika huku kwa wakusanyaji wa kodi kumesababisha kukosa ufanisi kwenye makusanyo ya kodi ndani ya nchi yetu, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali inatoa kauli gani kuhusu jambo hili? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kwagilwa, Mbunge wa Handeni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa sheria tuliyonayo sasa ukusanyaji wa kodi ya ardhi unafanywa na Wizara ya Ardhi yenyewe, Wizara ambayo imepewa mamlaka na Wizara ambayo inafanya kazi ya upimaji wa ardhi, kutoa vibali na inatunza kumbukumbu. Tuliona ni vema na Waheshimiwa Wabunge pia mmechangia pia katika kutunga sheria hii kwamba Wizara ya Ardhi yenyewe ikusanye na sasa tunaona mafanikio ya Wizara hii kukusanya kodi na uelewa wa Watanzania katika kulipa kodi unakuwa mkubwa na kwa hiyo, ukusanyaji unakuwa mzuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, suala la ukusanyaji wa halmashauri na TRA, miaka minne iliyopita hapa tulikutana na Waheshimiwa Wabunge mlitoa ushauri kwa Serikali. haikuwa ni kwa kodi ya ardhi, yalikuwa ni yale malipo ya tozo za nyumba (umiliki wa nyumba) ambayo pia na yenyewe tuliona kuwa ili kupata kodi ya nyumba za ngazi mbalimbali tukabidhi mamlaka iliyoko kule kule ambayo ni halmashauri na TRA iko kule kule kwenye wilaya. Kwa hiyo, hawa wakishirikiana pamoja ni rahisi kuzifikia nyumba zao kuliko Wizara ambayo imeishia tu Wizarani na haina tawi kubwa kule kwenye halmashauri. Hiyo ndiyo ambayo tulikuwa tumeipatia halmashauri na TRA. Hata hivyo, suala la kodi ya ardhi bado liko chini ya Wizara ya Ardhi na tunaona mafanikio makubwa.
Mheshimiwa Spika, mimi nataka nimpongeze Waziri wa Ardhi kwa kuendelea kufanya maboresho kwenye eneo hili la makusanyo ambako sasa watu wanalipa kielektroniki. Sasa tunaona Watanzania wanapata bili zao kupitia simu zao za mkononi na wanalipa kupitia simu zao za mkononi. Kwa hiyo, makusanyo ya kulipa kodi yanakuwa makubwa kuliko sasa kuliko huko awali ambako tulikuwa tunatumia makaratasi zaidi katika kulipa kodi hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na Watanzania na kuwahamasisha Watanzania kulipa kodi, kodi ndiyo msingi wa maendeleo yetu. Tutakapoendelea kulipa kodi ni rahisi sana kwa Wizara kuratibu mipango mbalimbali ya maboresho ya uratibu wa ardhi kama ambavyo sasa tuna Mradi wa Upimaji wa Matumizi Bora ya Ardhi kwenye vijiji ili kila mmoja aweze kutambua eneo lake na anapotaka kulipa kodi ajue kwamba analipa kodi kwa eneo alilopewa na akiwa na hati yake kamili. Iwe ni hati inayotolewa na Wizara yenyewe au hati ya kimila, zote hizi ni sehemu ya vibali vinavyokuruhusu wewe umiliki ardhi na kukutaka sasa ulipe kodi kwa maendeleo ya Taifa letu, ahsante. (Makofi)