Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Husna Juma Sekiboko (2 total)

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza nikupongeze sana kwa Serikali kukamilisha mchakato huu na leo kutuletea rasmi kwamba nchi yetu inakwenda kutekeleza Sera na Mtaala Mpya, lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu katika maelezo yako umeeleza kwamba Mtaala huu unakwenda kujikita katika Elimu ya Ujuzi. Hata hivyo, tuna upungufu mkubwa wa vifaa vya kufundishia katika level zote primary, secondary na Elimu ya kati kwa maana ya vyuo vya kati.

Je, Serikali inajipanga vipi kwenda kuhakikisha kwamba tunapata Makarakana na vifaa vya kufundishia vya kutosha ili kuweza kutekeleza mtaala huu?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Husna, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tumeeleza kwamba elimu sasa isiwe ya kitaaluma pekee bali iingize masuala ya ujuzi kwa lengo la wanaomaliza elimu ya msingi hii ambayo imeenda mpaka kwenye sekondari ngazi ya chini, wanapomaliza wawe wana ujuzi ambao wanaweza wakaanza pia kuingia kwenye ujasiriamali moja kwa moja. Sasa Serikali imejipangje kupata vifaa vya kufundishia, tumeeleza kwenye Sera na kwa kuwa Sera itatekelezeka mwaka 2027, bado Serikali itaendelea kutafuta uwezo wa kuanza kununua vifaa na kupeleka kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, sisi sasa tumeanza ujenzi wa VETA, Vyuo vya Ufundi, lakini pia tuna Vyuo vya Wananchi (FDCs) ambavyo pia vyenyewe vinatoa elimu ya ujuzi. Kwa hiyo kwa kipindi hiki cha mpito tunaanza kuimarisha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi, Vyuo vyetu vya VETA ambavyo wanajenga kila Wilaya kwa lengo la kuanza kutoa ujuzi huku tukijipanga kutafuta vifaa na kupeleka kwenye shule zetu za sekondari. Kama Sera inavyosema mafunzo ya mali na ufundi tutaanza na kidato cha kwanza. Kwa hiyo tuta-concentrate, tutaongeza nguvu katika kutoa vifaa na hasa katika kuongeza bajeti na tutaleta maombi yetu hapa kwenu Waheshimiwa Wabunge, naomba mridhie bajeti zetu ili tuweze kununua vifaa tupeleke sekondari na tutafanya hivyo awamu kwa awamu ili tufikie malengo ambayo tunayakusudia. Hii ndio namna ambayo tunakusudia kuitekeleza ili tuweze kufikia mafanikio, ahsante sana. (Makofi)
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu, elimu, hasa kwa upande wa mtaala mpya kwa maana ya amali, ni jambo mtambuka. Baada ya utekelezaji wa mtaala, wanafunzi watakaohitimu watahitaji kuwezeshwa kwenye sekta nyingine, kwenye maeneo kama TAMISEMI, kilimo, afya na maeneo mengine hasa ya ufundi: Ni kwa vipi Serikali inajiandaa kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya watoto watakaohitimu upande huo wa amali?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sekiboko, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo hili, kwanza nataka kutoa uelewa kwamba tunapotekeleza Sera yetu mpya ya Mitaala, hatuendi moja kwa moja na madarasa yote, tunaanza na makundi machache. Wanaoanza kufundishwa mwaka huu wa 2024 kama tulivyosema tunaanza mwezi Januari, ni darasa la awali, darasa la kwanza na darasa la tatu. Kwa sababu kwenye Elimu ya Msingi tuna makundi matatu; tuna awali, halafu darasa la kwanza na la pili; kundi la tatu, ni darasa la tatu na darasa la sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wanaoanza kufundishwa mtaala mpya ni awali, darasa la kwanza na darasa la tatu. Tunaanza nao mwaka huu. Hiyo ni kwa Shule za Msingi. Kwa upande wa Sekondari, tunaanza na Kidato cha Kwanza. Pia kwa Sekondari, tunajua tuna elimu jumla na kuna zile shule za ufundi. Kwa hiyo, tumechagua Shule za Ufundi, siyo zote, chache ambazo tayari zina miundombinu na walimu wa kuanzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utaratibu huu, utawezesha sasa Serikali kujipanga kupitia Bajeti yetu kuweza kumudu kuongeza pia hata idada ya walimu, kununua vifaa ili kufanya utekelezaji huu wa sera kuwa endelevu. Mwaka huu tunapoanza na awali na darasa la kwanza, darasa la pili hawahudhurii, wanaanza darasa la tatu, tunamfanya kijana wa awali anapohitimu, anapokwenda darasa la kwanza, anaendelezwa. Darasa la pili hapati, lakini anaanzia darasa la tatu, huyu wa darasa la kwanza anakuwa darasa la pili. Kwa hiyo, utakuta awali mpaka darasa la pili itakuwa endelevu kuanzia mwakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kila mwaka tutakuwa tunaenda hivyo. Yule wa darasa la tatu anaenda la nne, la tano, mpaka la sita, mwisho wa Elimu ya Msingi. Utakuta sasa tunaweza ku-cover maeneo yote, kila mwanafunzi anapata elimu hiyo vizuri. Wizara ya Elimu sasa itajitahidi, itapangilia mtihani kulingana na muda waliosoma masomo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunawezaje kuimarisha eneo hili? Ni pale ambapo bajeti sasa tutakuwa tunaiimarisha, kwanza kuongeza miundombinu ya majengo ya kusomea, vifaa vinavyohitajika, na walimu wenye uwezo wa fani hizo. Kwa hiyo, kila mwaka tutakuwa tunaongeza uwezo wetu. Serikali tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba tunaweza kufanikiwa hayo ili sera hii mpya iweze kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, huo ndiyo mpango wa Serikali uliopo. (Makofi)