Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Nusrat Shaaban Hanje (4 total)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nimuulize Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa kuna ugumu wa kupata ajira kwa vijana hasa waliomaliza darasa la saba kwenye taasisi za Serikali hata kama wamepata mafunzo katika fani mbalimbali kwenye vyuo vyetu vya ufundi hata vinavyotambuliwa na Serikali kwa kigezo cha cheti cha form four. Vyuo hivi vinatambuliwa na NACTE na Serikali kwa ujumla, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba ina-recognize vijana wetu hawa wa standard seven ambao wanaulizwa kigezo cha form four wakati wamepatiwa mafunzo na wana uwezo wa kufanya kazi hizo? Serikali ina mkakati gani kuwatambua na kuhakikisha kwamba inawasaidia?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat, Mbunge kutoka Mkoa wa Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mazingira ya kawaida ni kweli upo ugumu wa upatikanaji ajira na changamoto ya ajira iko duniani kote ikiwemo na hapa kwetu Tanzania lakini kila Serikali inaweka utaratibu mzuri wa kukabiliana na changamoto hii. Kwetu nchini Tanzania kupitia Serikali yetu inayoongozwa na Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imeendeleza mkakati wa Awamu ya Tano wa kupanua wigo ambao unaruhusu Watanzania kupata ajira bila ya kuangalia elimu yao; muhimu ni ujuzi na hasa anapozungumzia wale wamepata ujuzi kwenye vyetu vya ufundi vinavyotambulika na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkakati wa ujenzi wa viwanda ndiyo jibu sahihi la kupunguza changamoto hii ya ajira kwa ngazi zote; uwe umemaliza darasa la saba, kidato cha nne, una degree hata ukiwa Profesa unaweza kufanya kazi kwenye viwanda kwa sababu kazi za kufanya zipo nyingi. Kwa hiyo, mkakati wetu wa ujenzi wa viwanda ni miongoni mwa njia moja muhimu ya kuwezesha kupata ajira watu wa kada zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbili; tunaendelea pia kuimarisha vyuo vyetu vinavyotoa ufundi stadi kwa sababu unaposoma kwenye vyuo vya ufundi stadi unapata ujuzi, ukipata ujuzi unaweza kujiajiri, unaweza pia ukaanzisha taasisi ukawaajiri wenzako na kuajirika pia kwenye sekta nyingine. Nataka niwaongezee kuwajulisha kwamba hata Ofisi ya Waziri Mkuu tunao mkakati wa kutoa mafunzo ya watu wa ngazi zote ili waweze kupata ujuzi huo wapate nafasi ya kujiajiri, kuajiriwa lakini pia na wale wanaopata ujuzi wakaanzisha kampuni yao na kuweza kuwaajiri wengine; kwa utaratibu huu tumefanikiwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika miaka mitatu iliyopita tuliwahi kukusanya vijana wa taaluma mbalimbali zaidi ya 35,000 tukawapeleka kwenye sekta mbalimbali; kilimo, madini lakini pia utoaji huduma na maeneo mengine, tumewapeleka VETA na Chuo cha Don Bosco, tumewapeleka kwenye mahoteli na maeneo mbalimbali ya utoaji huduma. Wanapokuwa kule asilimia 40 ya muda ni nadharia, asilimia 60 ya muda wao unatumika kwa ajili ya vitendo. Wanapokamilisha mafunzo hayo ya miezi sita wanakuwa tayari wana ujuzi na wengi wamepata mafanikio wameajiriwa na wengine wamejiajiri. Kwa hiyo, huo ndiyo mkakati ambao Serikali inautumia ili kuwezesha kila mmoja kwa ngazi yake kuweza kupata ajira.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi nami niweze kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali. Tarehe 10 Julai, Soko la Kariakoo liliungua, ambapo tarehe 11 Julai, wewe mwenyewe ulikwenda Kariakoo kwa ajili ya kuwapa pole wahanga na pia kutoa maelekezo ya Serikali. Mheshimiwa Waziri Mkuu tunashukuru sana Serikali kwa sababu wamechukua jitihada za kujenga upya soko la Kariakoo ambako tarehe 6 Novemba, 2021 Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI alikwenda Kariakoo kwa ajili ya kutoa maelekezo kuhusiana na kujenga Soko la Kariakoo, kulijenga upya.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, ramani mpya ya Soko la Kariakoo jipya ina masoko mawili ambapo kama sasa hivi yako masoko mawili. Ramani inataka na utaratibu wa kujenga unataka soko dogo na kubwa lijengwe kwa pamoja. Mheshimiwa Waziri Mkuu jambo hili linaweza kupelekea ghasia na sintofahamu kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kwa nini sasa Serikali isiweke utaratibu wa kujenga masoko haya kwa awamu ili wafanyabiashara wa soko dogo wabaki pale ili soko kubwa lijengwe halafu baadaye wahamishiwe likamilike kwa pamoja? Nashukuru sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat, Mbunge wa Mkoa wa Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulipata tatizo la soko la Kariakoo kuungua na wote tunajua, lakini Serikali imefanya jitihada kubwa sana. Tulienda kutembelea na kuwapa pole, lakini tulitaka tujiridhishe ajali ile ilitokana na nini? Tukaunda Timu ambayo pia ilifanya kazi yake vizuri na ikatupa mrejesho wa nini kilisababisha soko lile lakini Kamati ile ilienda mbali zaidi na kutuambia madhara ya soko lile yakoje.

Sasa lile soko pale lilipo limezungukwa na nyumba za watu binafsi, lakini pia kuna soko dogo liko karibu kabisa na lile soko, usalama wa soko lile dogo haukuwa mzuri pia nao. Kwa hiyo katika maoni au mapendekezo ambayo waliyatoa ile Tume ni pamoja na kuliondoa lenyewe na kulijenga lingine jipya ambalo pia litafanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Rais, atatutengea shilingi bilioni zisizopungua 32 mpaka 34 ambazo zitajenga masoko yote mawili na tumeona tufanye maboresho makubwa. Hawa walioondolewa kwenye eneo lile, kimsingi hata pale baada ya kuungua, hawa waliokuwa soko dogo walikuwa hawafanyi kazi zao. Nao tuliwasihi wapishe eneo lile, ili eneo lile sasa uchunguzi upite na sasa maandalizi ya ujenzi yaendelee na tumewapeleka Kisutu pamoja na eneo la Machinga Complex na wengine wameenda kwenye masoko jirani.

Mheshimiwa Spika, wale wote wameorodheshwa, wanafahamika nani alikuwa wapi. Malengo yetu, baada ya kukamilisha katika kipindi tulichokubaliana soko likamilike, wale wote waliokuwa soko dogo waliokuwa mle kwenye soko kubwa, tunawarudisha na kuwaweka kwenye nafasi zao. Kwa kuwa sasa soko tumeliboresha, soko dogo sasa tumelijenga kwenye ghorofa, ghorofa mbili mpaka tatu, tumeongeza na wengine waliokuwa wanazagaa kule nje wakakosa mahali, sasa tunawaingiza kwenye lile jengo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yote haya ni maboresho ambayo tumeyafanya ya kuhakikisha kwamba hawa walioko hapa si kwamba wanapata shida kubwa kwa sababu wengine tumewapeleka pale Kisutu wanaendesha biashara zao na wale kwa sababu wana uhakika jengo likijengwa watarudi na watapata nafasi, naamini wanaiamini Serikali yao kwamba tutatenda hivyo na tutasimamia hilo ili kazi hiyo iweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inasimamia kwa karibu na sasa iko kwenye zabuni ili ujenzi uanze katika kipindi kifupi, wafanyabiashara warudi kufanya biashara zao. Ahsanye sana. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, malengo ya kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana mwaka 1993 ilikuwa ni kuhakikisha inawapatia mtaji vijana kwa mikopo ya masharti nafuu ili waweze kujikwamua kiuchumi, lakini kwa muda sasa mfuko huu umekuwa ukitengewa fedha, lakini vijana wanakosa hizo fedha kwa kiasi kwa sababu ya kukosa vigezo, lakini pia tunafahamu zipo halmashauri ambazo zinakosa asilimia 10 zile ambazo ni four, four, two; nne za vijana, nne za wanawake na mbili za walemavu, kwa sababu hazina mapato ya kutosha.

Ni kwa nini sasa Serikali isitumie Mfuko wa Maeneleo ya Vijana kama equalization fund kuziwezesha zile halmashauri amabzo zina mapato machache, mapato kidogo ili na zenyewe ziweze kutoa zile asilimia nne za halmashauri ili vijana waweze kupata mitaji kama ambavyo yalikuwa malengo ya kuanzishwa Mfuko wa Maendeleo Vijana? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hanje, Mbunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotoa majibu ya swali la awali linalohusu vijana kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea kuwawezesha vijana nchini kwa kuwatengea fedha kupitia mfuko, lakini pia kwa kutengeneza vigezo ambavyo vinaweza vikakidhi kwa ajili ya vijana hawa waweze kunufaika na mfuko wao.

Mheshimiwa Spika, eneo hili la kutunisha mfuko nimeeleza kwamba Serikali inajitahidi kila mwaka kutenga fedha kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu. Tulitenga bilioni moja, tukaongeza milioni 800 na bado tutaenedelea kutenga, lakini bado hazitoshi na nimeeleza awali. Kwa kutotosha fedha hizi bado tunaendelea kuhusisha na Wizara nyingine zenye programu za vijana ikiwemo na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo imetenga mfuko na fedha kupitia mapato ya ndani asilimia 10; asilimia nne ni za vijana, lengo ni kutunisha ule mfuko.

Mheshimiwa Spika, sasa na tumefungua milango kwa taasisi binafsi ambazo na zenyewe zinashughulikia vijana na Serikali yetu tuna marafiki wengi ambao pia wanaona jitihada zetu za kuwawezesha vijana, nazo pia zinachangia na ndio kwa sababu tulianzisha mfuko ili kurahisisha pia michango yao kuingia pale, jukumu letu Serkali ni kuusimamia mfuko uweze kuleta manufaa.

Mhehimiwa Spika, lakini la pili hivyo vigezo ambao vijana wengi wanakosa vigezo, tunaposema kukosa vigezo ni pale ambako kijana anakuwa hana anwani maalum, kijana huyu ni mzaliwa wa pale Singida, lakini anakutwa yupo Dar es salaam; kule Dar es Salaam anahitaji pia kuwezeshwa ni lazima tujue huyu hapa Dar es salaam anakaa wapi? Mtaa gani anafahamika na viongozi wa mtaa huo?

Sasa sehemu kubwa ya vijana wetu wanashindwa kukidhi kigezo hicho kwa sababu na wenyewe wako mobile, wanatembea huku, wanaenda huku katika kutafuta manufaa hayo, katika kujiwezesha kiuchumi. Lakini nini tunakifanya sasa, tunaendelea kuwahamasisha vijana kwenye halmashauri zetu na tunawatambua vijana hawa kupitia Idara yetu ya Maendeleo ya Jamii kwenye halmashauri, tunawatambua vijana kwenye vijiji, idadi yao, mahitaji yao ya shughuli za kiuchumi, huku Ofisi ya Waziri Mkuu kama nilivyosema tumeandaa mpango wa mafunzo ya vijana hawa ili kuwawezesha kuwa mafundi, kuwa na uwezo wa kufanya kazi mbalimbali na mafunzo haya yanachukua miezi sita, yanagharamiwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, wanaenda vyuoni wakisoma miezi sita, wanarudi wanakuwa tayari wanakuwa na vigezo vya kupata mikopo kwa sababu tayari tunafahamu anakokaa, ana ujuzi, unajua akichukua fedha anaenda kuitumia kwa ajili ya moja, mbili, tatu. Jitihada hizi zinaendela kupanuliwa wigo ili sasa tuweze kuwafikia vijana wote.

Mheshimiwa Spika, na mwisho niliishia na ushauri kwa vijana wetu, pindi wanapomaliza mafunzo haya, wanapokuwa pamoja kwa maana ya kuunda vikundi wanakuwa vizuri zaidi, huo ni ushauri na wanapofikiwa ni rahisi wao wakiwa kikundi kukopesheka kuliko wakiwa mtu mmoja mmoja.

Kwa hiyo, tunaendelea kufanya maboresho kwenye maeneo yote haya; kwanza kuwa na vigezo, lakini mbili kuweza kuwafikia na kutunisha mfuko ili waweze kunufaika. Jitihada hizi zinaendelea na tunaendelea sasa kukusanya Wizara zote ambazo zinahusika na vijana ikuwemo na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Ofisi ya Waziri Mkuu yenyewe na wadau ambao tunao na jumuiya mbalimbali za dini na vijana zote hizi zinatumika katika kuhakikisha tunakusanya nguvu ya pamoja kuwawezesha vijana ili kuweza kuwawezesha kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, huo ndio utaratibu tunautumia kwa sasa, lakini nikiri kwamba maswali yote mawili yanaweka msisitizo kwa vijana, kwa hiyo Serikali tutapanua wigo wa kutoa huduma kwa vijana zaidi ili malengo ya vijana yaweze kufikiwa, ahsante sana. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na maendeleo makubwa ya kiteknolojia duniani, watoto wetu wamekuwa wakiingia kwenye mitandao na wakitumia vifaa vya ki-electronic kwa ajili ya kujifunza masuala ya TEHAMA na masuala mengine ya kujipa maarifa katika masomo yao. Tunafahamu wanapoingia katika mitandao wanakutana na mambo mengi ambayo yanaweza kupelekea mmomonyoko wa maadili na udhalilishaji wa watoto mitandaoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu mwaka 2014 Umoja wa Mataifa ulielekeza dunia kuweka mikakati madhubuti ya kuwalinda watoto dhidi ya ukatilii wa mitandao. Nchi nyingi zime-adopt, zimeweka sera madhubuti na sheria madhubuti za ulinzi wa watoto mitandaoni. Sasa nchi yetu imekuwa ikiendesha kampeni zisizo rasmi za ulinzi wa watoto mitandaoni, naomba kufahamu Serikali imejipangaje kuhakikisha inatengeneza mazingira bora ya kisera na ya kisheria kuhakikisha kwamba online child protection inapewa nguvu. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Hanje, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, dunia sasa hivi inaendea kwenye maendeleo makubwa ya matumizi ya mifumo yetu mbalimbali ki-electronic. Pia dunia imeanza kuelimisha umma wake kutumia mifumo hii ya ki-electronic kwa urahisi zaidi, sasa mifumo hii imekuja ikiwa na faida lakini pia kuna changamoto zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zilizopo ni miongoni mwa hayo uliyoyaeleza kwamba jamii baadhi yetu tunatumia vibaya matumizi ya TEHAMA, matumizi ya Mifumo hii ya ki-electronic vibaya kwa kukashfu, kutumia mitandao kudhalilisha watu wakiwemo watoto na wanawake, lakini pia hata juzi tulipokuwa tunapitisha Muswada wetu hapa wa Vyama vya Siasa tulilizungumza hili na tumeliwekea mbano kidogo wale ambao watatumia vibaya mitandao kwa ajili ya kudhalilisha kwenye eneo la siasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huu ni mkakati ambao Serikali pia tumekubaliana na tumesaini mikataba ya kimataifa kukabiliana na unyanyasaji, vitendo vya kikatili kwa watoto na wanawake. Sisi kama Serikali tumeweka utaratibu wetu kupitia Wizara yetu ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto ili kukabiliana na wale wote wanaotumia vibaya mifumo hii kwa kudhalilisha watoto, wanawake na makundi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu ambao tumeufanya huku tukiwa tunapeleka pia kwenye Mtaala wetu wa elimu kufundisha kutoka Shule za Msingi, Sekondari, Vyuo mbalimbali mpaka elimu ya juu, elimu hii ya matumizi ya ki-electronic tumeweka pia na Sheria zinazowabana hawa wote wanaotumia vibaya mitandao hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali inaendelea kuwahakikishia Watanzania kwamba, tutaendelea kuimarisha kudhibiti wale wote ambao wanatumia vibaya mitandao hii na tutachukua hatua kali dhidi ya wale wote ambao watatumia vibaya matumizi haya ya TEHEMA kwa kudhalilisha na kukatili wengine wa aina yeyote ile kwao ili itoe mafundisho kwa wengine ambao wanaweza kuungana nao kwenye matumizi mabaya haya. Kwa hiyo, nitaendelea kuwahakikishia ya kwamba matumizi ya TEHAMA tutaendelea kuhamasisha yake lakini hamasa hii ni kwa matumizi sahihi na siyo vingine. ahsante sana. (Makofi)