Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Bakar Hamad Bakar (2 total)

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR aliuliza: -

Je, ni kwa kiwango gani bahari zinachangia kukua kwa uchumi kupitia uvuvi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bakar Hamad Bakar, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Uvuvi hutoa mchango katika uchumi wa nchi kupitia uzalishaji wa bidhaa na huduma mbalimbali zinazozalishwa ndani ya sekta. Aidha, baadhi ya bidhaa na huduma zinazozalishwa hutumika kama mali ghafi katika uzalishaji ndani ya sekta nyingine kama vile viwanda na kuwa na mchango mkubwa zaidi katika sekta hizo. Katika mwaka 2022, sekta ya uvuvi ilichangia asilimia 1.8 ya Pato la Taifa huku ikikua kwa asilimia 1.9.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2022/2023, mazao ya uvuvi kutoka baharini yalichangia jumla ya tani 54,823 sawa na asilimia 10.6 ya mazao ya uvuvi ambayo ni tani 513,525. Vilevile, maduhuli ya Serikali ya shilingi bilioni 1.8 yalikusanywa kutoka katika shughuli za uvuvi baharini. Kiasi hicho cha mazao ya uvuvi kilichozalishwa kutoka baharini kilitokana na uvuvi mdogo na kilikuwa na thamani ya shilingi bilioni 356.3. Naomba kuwasilisha.
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR aliuliza: -

Je, lini Serikali itanunua meli za abiria zitakazorahisisha usafiri kwa wananchi kati ya Pemba, Tanga, Mtwara na Unguja?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bakar Hamad Bakar, Mbunge wa Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali kupitia Kampuni ya Huduma za Meli Tanzania (MSCL) imetenga kiasi cha fedha shilingi milioni 500 kwa ajili ya upembuzi yakinifu ili kujua aina ya meli zitakazojengwa kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya wananchi wa mikoa ya Tanga, Mtwara, Lindi, Pemba na Unguja ambapo zitatoa huduma kwa njia ya maji katika mwambao wa Bahari ya Hindi kwa ajili ya kuchochea ukuaji wa uchumi katika ukanda huo. Matokeo ya utafiti huo ndiyo yatakayobainisha aina na ukubwa wa meli itakayojengwa kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya soko Mikoa ya Pemba, Tanga, Mtwara na Unguja.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na mikakati ya Serikali ya kununua meli kwa ajili kutoa huduma katika mwambao wa Bahari ya Hindi, hata hivyo kutokana na fursa za kibiashara zilizopo katika mikoa ya Tanga, Unguja, Mtwara, Lindi na Pemba, Serikali imeendelea kuhamasisha sekta binafsi kutumia fursa hiyo kuwekeza kwa kununua meli za biashara ili kuhudumia hilo soko ambapo kutachochea ukuaji wa uchumi katika mikoa hiyo na kuongeza pato la Taifa kwa ujumla.