Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Aziza Sleyum Ally (4 total)

MHE. SHALLY J. RAYMOND K.n.y. MHE. AZIZA S. ALLY aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kuanzisha Kombe Maalum la Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa anajitoa sana kwenye Sekta ya Michezo?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, Watanzania wanatambua na kuthamini mchango mkubwa wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika sekta ya michezo nchini. Katika kuenzi mchango huo, tayari tumeelekeza vyama na mashirikisho ya michezo nchini kuona namna bora ya kuwa na kombe maalum la Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ukubwa zaidi kwa michezo wanayoisimamia, lengo likiwa ni kuwa na mashindano makubwa ya Kitaifa yatakayohusisha michezo mbalimbali yatakayofahamika kama Samia Taifa Cup kuanzia ngazi za chini na tayari Wizara imegawa vifaa katika mikoa yote Tanzania Bara na Visiwani.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa wadau tofauti wameanzisha mashindano mbalimbali yanayotumia jina la Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo ni pamoja na Ligi ya Mama Samia Mshikamano Cup (Mbeya Mjini); Dr. Samia Katambi Cup (Shinyanga); Simiyu Samia Marathon; Dkt. Samia Cup (Same); Chato Samia Cup (Chato); na Samia Afya Cup ambayo ni mashindano yanayoandaliwa na Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) na kushirikiana na taasisi mbalimbali za umma na binafsi na mashindano mengine mengi.
MHE. AZIZA S. ALLY aliuliza:-

Je, Vibali vya Ujenzi hutolewa baada ya muda gani tangu mwombaji aombe kupewa kibali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa vibali vya ujenzi unasimamiwa na Mwongozo wa Utoaji wa Vibali vya Ujenzi na Usimamizi wa Ujenzi wa Majengo wa Mwaka 2018. Mwongozo huo umeweka muda na taratibu za utoaji wa vibali kulingana na aina ya jengo linaloombewa kibali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha Mfumo wa Kielektroniki wa Utoaji wa Vibali vya Ujenzi wa TAUSI na umeanza kutumika Julai, 2024 kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, ambapo halmashauri 47 tayari zinatumia katika kutoa vibali vya ujenzi na halmashauri nyingine zitaanza kutumia. Kupitia mfumo huo, muda wa kutoa vibali umepungua, ambapo kwa sasa kibali kinaweza kutolewa ndani ya siku moja.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE K.n.y. MHE. AZIZA S. ALLY aliuliza:-

Je, nini mkakati wa Serikali wa kutafuta soko la asali?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa na mkakati wa kutafuta soko la asali ambao unajumuisha mafunzo ya uzalishaji bora katika mnyororo wa thamani wa asali. Ujenzi wa viwanda vya pamoja (common facilities) vya uchakataji bora wa asali, utangazaji wa bidhaa za asali zinazozalishwa nchini katika maonesho ya ndani, kikanda na kimataifa na kujumuisha fursa ya asali ya Tanzania katika majadiliano ya nchi na nchi, kikanda na Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, hatua hizo zimewezesha kampuni ndogo (SMEs) 46 zinazozalisha asali kuuza tani 337.3 katika masoko ya nje, hususan soko la Ulaya, ambapo nchi zinazonunua kwa wingi ni Ujerumani, Uholanzi na Poland, ikifuatiwa na Soko la Afrika Mashariki (EAC); Kenya, Rwanda na Uganda na katika Soko la SADC, ikiwemo nchi ya Botswana. Jumla ya mauzo katika masoko hayo kwa mwaka 2023 yalikuwa na thamani ya shilingi bilioni 2.0.
MHE. AZIZA S. ALLY aliuliza:-

Je, lini Serikali itarudisha Somo la Domestic Science katika Mtaala wa Elimu ya Shule za Msingi Nchini?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, somo la sayansi kimu (domestic science) lilianzishwa baada ya mitaala kubadilishwa mwaka 1979 kufuatia Azimio la Musoma ikiwa ni kutekeleza kauli mbiu ya siasa ni kilimo na elimu kwa wote. Somo hili la sayansi kimu liliboreshwa zaidi na maudhui yake kuingizwa katika somo jipya la stadi za kazi mwaka 1997.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ilikuwa ni pamoja na kupunguza wingi wa masomo kutoka masomo 13 hadi masomo saba kwa wanafunzi wa shule za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mtaala ulioboreshwa mwaka 2023 maudhui yanayoshabihiana na somo la sayansi kimu yameboreshwa zaidi kwa kuzingatia mahitaji ya jamii, kukua kwa sayansi na teknolojia pamoja na soko la ajira. Hivyo, maudhui hayo kwa ngazi ya elimu ya msingi yapo kwenye somo la sanaa na michezo, ambalo ni somo la lazima na linafundishwa kuanzia darasa la tatu hadi la sita. Aidha, kuanzia kidato cha kwanza mpaka cha nne kuna mkondo maalum unaofundishwa masuala ya chakula na lishe ambao umejikita kuendelea kujenga maarifa katika eneo hili. Ninakushukuru.