Supplementary Questions from Hon. Aziza Sleyum Ally (6 total)
MHE. AZIZA S. ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu Kiwanda cha Nyuzi Tabora ambacho kwa muda mrefu kimefungwa hakifanyi kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, tunajua tulikuwa tunazungumzia suala la mbolea na Mheshimiwa Mbunge ameuliza kuhusu Kiwanda cha Nyuzi na sisi Wizara ya Kilimo pamoja na Viwanda na Biashara, jambo hili tunalifahamu. Tunafahamu changamoto ambazo zipo katika viwanda vingi vya nyuzi na moja ya mkakati wa Wizara ya Kilimo ambao tuko nao sasa hivi, ni kuhakikisha tunafufua viwanda vingi ili pamba yote inayozalishwa hapa nchini iweze kutumika na hivi viwanda viweze kufanya kazi. Kwa hiyo, mpango tulionao ni huo kwa sasa na tuko serious katika eneo hili, ahsante sana. (Makofi)
MHE. AZIZA S. ALLY: Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali ina mkakati gani wa kuinusuru Barabara ya Itigi – Tabora ambayo imejengwa kwa muda mfupi na imeshaanza kuharibika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokifahamu ni kwamba Barabara ya Itigi – Tabora imejengwa yote kwa kiwango cha lami na kama kuna uharibifu ambao siyo wa kawaida na najua ni barabara ambayo siyo ya muda mrefu, namwomba Mheshimiwa Mbunge aweze kutusaidia ama niwaagize Mameneja wa Mkoa wa Singida na Tabora waweze kupita katika barabara hiyo ili waweze kujiridhizisha.
MHE. AZIZA S. ALLY: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa kuna utaratibu mpya wa kielektroniki wa kupata hivi vibali; je, kibali hicho, kitadumu kwa muda gani tangu kimetolewa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, wameshatoa elimu katika maeneo mbalimbali kwa wananchi ili waweze kujua kama kuna mfumo mpya; wale wananchi wa Mbeya Mjini waweze kufahamu, wananchi wa Tabora na maeneo mengine waweze kufahamu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mfumo wa Utoaji wa Vibali vya Ujenzi siku za nyuma tulikuwa tunatumia mfumo wa kawaida ambapo mwombaji aliwasilisha makabrasha, ramani na viambatisho muhimu kwa ajili ya kupata vibali.
Mheshimiwa Spika, vibali hivyo vinachukua kati ya siku saba hadi 14 kwa majengo ya kawaida na kati ya siku 14 hadi ya 30 kwa majengo ya ghorofa. Hata hivyo, baada ya kuona kuna maeneo vibali hivi vinacheleweshwa, Serikali ikaanzisha Mfumo wa Kielektroniki wa TAUSI ambao mwombaji ana uwezo wa kupata kibali ndani ya siku moja, lakini kibali hicho kitadumu muda wote wa ujenzi wa jengo husika.
Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na elimu, tunaendelea kutoa elimu kwa wananchi, kwanza kutambua kwamba kuna mfumo huu na namna ya kuutumia. Lakini pia wataalam wote katika halmashauri zetu wamepewa maelekezo ya kuendelea kutoa elimu na kuwasaidia wananchi ili waanze kuutumia mfumo huu muhimu. Ahsante sana.
MHE. AZIZA S. ALLY: Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali ina mkakati gani wa kuinusuru Barabara ya Itigi – Tabora ambayo imejengwa kwa muda mfupi na imeshaanza kuharibika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokifahamu ni kwamba Barabara ya Itigi – Tabora imejengwa yote kwa kiwango cha lami na kama kuna uharibifu ambao siyo wa kawaida na najua ni barabara ambayo siyo ya muda mrefu, namwomba Mheshimiwa Mbunge aweze kutusaidia ama niwaagize Mameneja wa Mkoa wa Singida na Tabora waweze kupita katika barabara hiyo ili waweze kujiridhizisha.
MHE. AZIZA S. ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru. Kwa kuwa barabara hizi zinasimamiwa na TARURA. Serikali imeongezea kiwango kikubwa cha pesa TARURA, lakini bado barabara zina shida za kuweza kupitika. Je, Serikali ina mpango gani wa kuangalia Mfuko huu wa TARURA ili barabara hizi ziweze kupitika kwa muda mrefu zaidi kuliko sasa pesa zinakwenda, lakini bado barabara zinakuwa mbovu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, niseme jambo moja muhimu kwamba katika kipindi hiki cha miaka minne Serikali imeongeza sana mtandao wa barabara za TARURA. Kwa hiyo, barabara nyingi mpya zimeendelea kufunguliwa na kujengwa na hiyo imepelekea mahitaji ya fedha za barabara kuendelea kuongezeka na Serikali imeongeza bajeti ya barabara kutoka shilingi bilioni 275 mwaka wa fedha 2021/2022 mpaka shilingi bilioni 870.3 mwaka wa fedha 2024/2025.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ambayo Bunge hili Tukufu imepitisha wiki mbili zilizopita Mheshimiwa Rais ameongeza tena bajeti ya TARURA kutoka shilingi bilioni 870.3 mpaka shilingi trilioni 1.130. Kwa hiyo, jitihada za Serikali zipo wazi za kuongeza fedha na uwezo wa TARURA na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba barabara hizo zinazoathirika zitaendelea kujengwa kwa awamu. (Makofi)
MHE. AZIZA S. ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; ninaomba nichukue nafasi hii kulipongeza sana Azimio la Musoma. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri haoni kama Azimio la Musoma lilikuwa ni zuri sana lenye kuelimisha, wanafunzi walikuwa na uwezo wa kujua kupika, usafi na hata kujishonea nguo zao wenyewe tofauti na sasa hivi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami tuanzishe shamba darasa kwa kuteua shule moja pale Tabora ili kuweka mtaala kama huu wa Azimio la Musoma ili kuwa mfano kwa shule nyingine ili vijana wetu warudi kule tulikotoka sisi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Aziza Sleyum na nitajibu yote kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la masomo pamoja na mitaala ni suala ambalo ni dynamic siyo static kwa maana kwamba ni lazima kufanya maboresho na marekebisho mara kwa mara. Ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maazimio yote au mitaala yote ni bora au mizuri kulingana na muda ambao mitaala hiyo imeweza kutumika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ninamweleza katika mfumo wa sasa ambao tumefanya maboresho ya sera pamoja na mitaala inafanya elimu yetu ya lazima iwe ni ya miaka 10. Miaka sita shule za msingi na miaka minne katika shule za sekondari. Kwa hiyo, katika mfumo wetu huu wa sasa, wanafunzi wote watakaomaliza watapata ujuzi utakaowawezesha kujitegemea. Katika, darasa la kwanza na la pili, watoto watajifunza hayo masuala ya kushona, kufuma pamoja na mitindo na mambo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo la pili alilolizungumza kuhusu Tabora kwamba tutengeneze pilot, ninadhani baada ya maswali tunaweza tukakutana na Mheshimiwa Mbunge, tukaangalia hilo wazo lako na ushauri wako, ni namna gani tunaweza kutekeleza kwa wakati. Ninakushukuru sana.