Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2017-11-09

Name

Abdallah Ally Mtolea

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Temeke

Primary Question

MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nimuulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika Serikali ya Awamu ya Nne nchi hii ilitumia mabilioni ya fedha kuzunguka nchi nzima kwa ajili ya kukusanya maoni ili kuandaa Katiba Mpya na hii ilikuja baada ya kugundua kwamba Taifa hili linahitaji Katiba Mpya ili kutibu changamoto nyingi ambazo zinaikabili katika maeneo mbalimbali ikiwemo kulinda rasilimali, uwajibikaji, haki za binadamu, tunu za Taifa na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, tunaipongeza Serikali ya Awamu ya Nne kwa kuanzisha mchakato ule, pamoja na changamoto ambazo zilijitokeza baadaye.

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali ya Awamu ya Tano toka imeingia madarakani, leo miaka miwili tayari imepita haijafanya jambo lolote la kuendeleza mchakato ule ili zile ndoto za Watanzania za kupata Katiba Mpya ziweze kutimia. Zaidi tumekuwa tukisikiliza kauli mbalimbali za kwenu viongozi na za viongozi wa Chama chenu cha Mapinduzi ambazo hazioneshi nia ya kukamilisha mchakato huo wa Katiba Mpya.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba awaambie Watanzania leo, nini mpango wa Serikali ya Awamu ya Tano katika kutimiza ndoto za Watanzania kupata Katiba Mpya?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mtolea, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali ya Awamu ya Nne ilianza mchakato wa Katiba Mpya na kupitia hatua zote za kuunda Tume, ikapita kukusanya maoni na sisi kama Waheshimiwa Wabunge tulikuwa miongoni mwa Wajumbe ambao tulishiriki katika kuweka misingi ya Katiba hiyo. Suala la Katiba Mpya linahitaji gharama kubwa ya fedha na zinatokana na mapato yanayokusanywa ndani ya nchi lakini kila mwaka wa fedha una vipaumbele vyake na sisi tumejikita katika kutoa huduma za jamii kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukishuhudia Watanzania wanahitaji maji kwenye vijiji, kumekuwa na mahitaji ya huduma za afya, tunahitaji kuimarisha elimu, miundombinu, ili kuwawezesha Watanzania kuendelea na maisha yao. Katiba ni mwongozo ambao unaelekeza mambo kadhaa. Sasa hivi tunayo Katiba ambayo pia ina miongozo ile ile ingawa tumekusudia kuibadilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tunayo Katiba inaendelea na miongozo ipo, na haya ni mapendekezo ya kufanya marekebisho ya maeneo kadhaa; lakini mchakato wake kwa sababu unahitaji gharama kubwa na kipaumbele cha Serikali ni kutoa huduma ya jamii kwa Watanzania; kwanza tumeanza kuimarisha makusanyo ya ndani ili tuweze kumudu kutoa huduma za wananchi, Watanzania. Pale ambapo tutafikia hatua nzuri ya mapato huku tukiendelea kutoa huduma hiyo na matatizo haya yakipungua kwa kiasi kikubwa, tutakuja kuendesha mchakato huo pale ambapo inaonekana tunaweza tukaufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niendelee kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua hayo yote lakini pia tumeona muhimu zaidi tuanze na huduma za jamii ili Watanzania waendelee kufanya kazi zao za kuboresha uchumi wao ili wapate nafasi ya utulivu waje waangalie jambo lingine, kwa sasa tutatumia Katiba iliyopo. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister