Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2017-11-16

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Gender

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Waziri Mkuu nchi yetu imekuwa inakumbwa na majanga mbalimbali kutokana na mabadiliko ya tabianchi. Tumeshuhudia watu wengi wakipoteza maisha, lakini miundombinu ikiharibika, lakini pia hata hali halisi ya mvua zimekuwa hazinyeshi kwa ukamilifu kutokana na kwamba, kuna mabadiliko ya tabianchi ambayo ni suala la kidunia. Mheshimiwa Waziri Mkuu Serikali yetu imejipanga vipi kimkakati kupambana na janga hili la tabianchi katika nchi yetu?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sakaya, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mabadiliko ya tabianchi yaliyoikumba dunia yote, Tanzania ikiwemo, tunaendelea pia kukabili changamoto hiyo huku tukiwa tunaweka mipango mbalimbali ya kuhakikisha kwamba, tunakabiliana nayo mabadiliko hayo. Moja tumejiimarisha kwa sheria zinazohifadhi mazingira yetu, ili kuhakikisha kwamba, mazingira yanabaki yanasaidia pia, kufanya mabadiliko ya hali ya hewa ndani ya nchi yanabaki kuwa ya kawaida yanayowezesha binadamu au Watanzania walioko huku ndani au viumbe hai vyote kufanya kazi zao vizuri na kupata mahitaji vizuri.

Mheshimiwa Spika, pia, Serikali tumeendelea kusimamia Sheria za Mazingira ambazo pia zinakinga maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na misitu, mito na maeneo mengine yote ili kuhakikisha kwamba tunakabiliana na hili. Pia, Serikali tunaendelea kuweka utaratibu wa kutoa elimu kwa jamii kuwaelimisha Watanzania umuhimu wa kuhifadhi mazingira yetu kwa ujumla, lakini pia hata Taasisi za Kimataifa nazo zimeshiriki kikamilifu na Mataifa makubwa nayo yameshiriki kikamilifu katika kupambana na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naamini kwamba, kadri ambavyo dunia na nchi zote duniani zinakabiliwa na jambo hili na Serikali yetu nchini pia, tumeshiriki katika kuhifadhi mazingira huku ndani hiyo ikiwa ni moja ya mapambano ya mabadiliko ya tabianchi duniani. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Watanzania kwamba, mabadiliko ya tabianchi kama tutaendelea kuharibu misitu yetu, kuharibu vyanzo vyetu, tunaweza kukosa huduma za jamii ambazo zinatokana na mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni muhimu sana tukashirikiana kwa pamoja kupitia wataalam ambao wanatoa elimu na wananchi na kila mmoja ambaye ana dhamana kwenye eneo lake, ili tuweze kushiriki kwa pamoja kuhifadhi mazingira yetu, ikiwa ni moja kati ya mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister