Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 9 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2019-02-07

Name

Lucy Simon Magereli

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCY S. MAGERELI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Siku ya Jumatatu tarehe 4 Februari, 2019, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wakati wa majumuisho ya Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Miundombinu na Kamati ya Viwanda na Biashara alitoa kauli ndani ya Bunge lako iliyomaanisha kusema Serikali imejidhatiti kukuza mitaji yake yenyewe ili kuacha kutegemea mitaji ya uwekezaji na misaada kutoka nje na alitamka akisema wawekezaji wengi ni wezi na wana mikataba ya kinyonyaji. Je, huo ndiyo msimamo wa Serikali kuhusu wafadhili na wawekezaji wa nchi hii?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba sina uhakika kama Naibu Waziri wetu aliwahi kutoa kauli hiyo kwa sababu huo siyo msimamo wa Serikali. Msimamo wa Serikali ni kukaribisha wawekezaji kuwekeza kwenye sekta zote za kibiashara na tunatoa fursa hiyo kwa mwekezaji yeyote wa ndani mwenye uwezo na wale wa nje wanakaribishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali tumefanya kazi kubwa ya kujenga mazingira ya uwekezaji mzuri hapa nchini. Tuna ardhi ya kutosha na tumetoa maelekezo katika Halmashauri zote kutenga ardhi kwa ajili ya kufungua milango ya wawekezaji wanaotaka kuwekeza kwenye sekta ya ardhi lakini pia tuna madini na sekta nyingi ambazo kila moja anayetaka kuwekeza anao uhuru wa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jukumu letu Serikali ni kuhakikisha kwamba tunatengeneza mifumo rahisi ya kumwezesha mwekezaji kuwekeza biashara yake na kufanya biashara yake katika mazingira rahisi. Pia Serikali inajitahidi kukutana na wawekezaji wakati wowote kuzungumza nao ili kusikia changamoto ambazo zinawakabili kwenye uwekezaji wao. Ndiyo sababu Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ameendelea kutoa wito wa ujenzi wa uchumi wa Tanzania kupitia viwanda na sehemu kubwa ya viwanda vinawakaribisha wawekezaji ili waweze kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nitumie nafasi hii kutoa wito kwa wawekezaji wote nchini na wale wa nje kuja Tanzania kuwekeza; sekta za uwekezaji ziko nyingi, Serikali inajenga miundombinu, tumejenga barabara nzuri za kufanya biashara zao, tunaendelea kuboresha reli, Shirika la Ndege na usafiri wa majini, malengo yetu ni kumwezesha mwekezaji na mfanyabiashara huyu kufanya biashara yake katika mazingira rahisi. Kwa hiyo, huo ndiyo msimamo wa Serikali wa kuhamasisha uwekezaji na kwamba tutawalinda wawekezaji wale wanaojenga viwanda vya ndani na tutalinda viwanda vya ndani ili viweze kufanya biashara yake vizuri zaidi. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister