Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 9 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2019-02-07

Name

Edwin Mgante Sannda

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Primary Question

MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii. Mheshimiwa Waziri Mkuu natamani sana kujua mpaka sasa Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha kwamba tunaboresha na kurahisisha mazingira ya kufanya biashara nchini?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sannda, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali lake haliko mbali sana na swali la Mheshimiwa Lucy ambalo alitaka Serikali itoe msimamo wa namna ambavyo inaboresha biashara na kutoa fursa ya uwekezaji kuwekeza hapa nchini. Swali hili la mpango au mkakati wa Serikali wa kuboresha biashara, kama ambavyo nimesema kwenye swali la awali kwamba Serikali imejenga mazingira mazuri ya kuwezesha kufanya biashara.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba wafanyabiashara ndiyo wanaochangia pato la Serikali hapa nchini. Katika kuchangia pato la Serikali lazima tuhakikishe wafanyabiashara wote; wafanyabiashara wakubwa, wa kati, wadogo wakiwemo wamachinga, mamalishe tuwape fursa ya wazi, pana ya kuweza kufanya biashara hiyo kwa sababu wao wanachangia pato hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika uchangiaji wa pato hilo maana yake lazima Serikali sasa tuendelee kuwahamasisha wafanyabiashara, tunaendelea kuhakikisha tunajenga mazingira mazuri ya kufanya biashara maeneo yote. Watanzania wote ni mashahidi, Mheshimiwa Rais wetu pia kama ambavyo nimesema awali mmeona juzi jitihada za kutoa vitambulisho kwa ajili ya kuwatambua wafanyabiashara wadogo ili waweze kuratibiwa maeneo yao na wafanye biashara vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia wafanyabaishara wa kati nao uko mpango unaendelea na Wizara ya Viwanda na Biashara kuhakikisha kwamba wanakutana na Waziri kujua mwenendo wa biashara kwenye maeneo yao na hivyo hivyo kwa wafanyabiashara wakubwa. Wote mnajua kwamba tunalo Baraza la Wafanyabiashara ambalo pia Mwenyekiti ni Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli amekutana na wafanyabiashara mara kadhaa ili kusikiliza matatizo wanayokutana nayo katika uendeshaji wa biashara zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mkakati wa kujenga mazingira mazuri ya kibiashara unaendelea ikiwemo pia na upanuaji wa sekta zinazowasaidia wafanyabiashara kufanya vizuri wka maana ya kujenga miundombinu, barabara zote nchini kama nilivyosema awali zimepanuliwa na zinaunganisha mikoa. Kwa hiyo, mfanyabiashara ana uwezo wa kufanya biashara kutoka Katavi mpaka Dar es Salaam akipita kwenye barabara nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumenunua ndege, wale wote ambao wanataka kufanya biashara za ndege za ndani na mpango wetu kwenda nje wanayo fursa ya kufanya hilo. Pia usafiri majini, Ziwa Tanganyika, Ziwa Victoria tunajenga meli mpya ili ziweze kusafirisha abiria na wafanyabiashara kutoka eneo moja mpaka lingine. Kwa hiyo, jitihada zote hizi lengo letu ni kuhakikisha kwamba wafanyabiashara wanafanya biashara katika mazingira mazuri na huo ndiyo mpango wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie wafanyabiashara kuendelea kupanga mipango mizuri kwenye mpango wa biashara zao, Serikali inaandelea kuwaunga mkono na pale ambapo wanapata matatizo yoyote kwenye biashara tutaendelea kukutana pamoja na Waziri yupo lakini pia Ofisi yangu iko wazi tunawakaribisha kuja kuzungumzia changamoto ambazo zipo. Muhimu ni tufuate kanuni na sheria na taratibu ambazo zinakuruhusu kufanya biashara. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister