Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 9 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2019-02-07

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na songombingo iliyoipelekea zao la korosho kwa msimu uliopita ambao sasa hivi tunaendelea nao kukosa soko jambo lililopelekea Serikali kuingilia kati na kutangaza kwamba inakwenda kununua korosho za wakulima. Hata hivyo, hadi leo wakulima walio wengi hawajapata fedha zao wakati korosho tayari zimeshachukuliwa na Serikali. Siyo hivyo tu, kuna baadhi ya wakulima wameanza kulipwa kidogo kidogo lakini kinachoshangaza wakulima wengi wanalipwa Sh. 2,600 kwa kilo kinyume na Mheshimiwa Rais alivyotangaza kwamba korosho anakwenda kuzinunua kwa Sh. 3,300 kwa kilo.

Mheshimiwa Spika, nini kauli ya Serikali kulingana na hii sarakasi inayoendelea sasa hivi kwenye zao hili la korosho? Kwa sababu sasa hivi msimu wenyewe unakwenda kuisha lakini wakulima malalamiko ni makubwa sana? Nini kauli ya Serikali? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshiiwa Spika, katika kipindi hiki cha Bunge cha wiki mbili hizi suala la korosho limezungumzwa sana na Wizara kwa maana Serikali imetoa ufafanuzi sana namna ambavyo tunaendelea kufanya malipo ya zao la korosho kwa wakulima wanaolima zao hili walioko kwenye mikoa hii mitano ya Ruvuma, Mtwara, Lindi, Pwani na Tanga ambako sasa wako kwenye masoko. Tunachosema zao la korosho siyo kwamba lilikosa soko bali lilikosa bei nzuri, wanunuzi wapo lakini lilikosa bei nzuri. Pale ambapo wanunuzi walikuwa wananua kwa bei ya chini sana kuliko hata ile bei ya kwenye soko la dunia na ilikuwa haimletei faida mkulima. Kwa nia nzuri ya Mheshimiwa Rais akaamua korosho hizi sasa tutanunua kwa Sh.3,300 bila makato yoyote yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alipotoa kauli sasa Bodi ya Mazao Mchanganyiko yenye dhamana kisheria ya kununua mazao na kutafuta masoko popote pale na hasa kwa mazao ambayo yanaonekana yanasuasua kupata masoko ilianza kazi yake. Imetafuta fedha, baada ya kufanya tathmini ilishajua kiwango cha korosho kitakachozalishwa na gharama zake, wana uwezo nalo, wameanza kazi hiyo na sasa wanaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tamko la Mheshimiwa Rais kununua kwa Sh.3,300 kwa kilo maana yake anazungumzia standard grade ile bei kwa korosho ya daraja la kwanza. Zao la korosho lina grade I, II, iko sheria inayoongoza Bodi ya Korosho kwamba korosho za daraja la II zitauzwa asilimia 80 ya bei ya daraja la I. Kwa hiyo, bei iliyotamkwa ni ya daraja la I, unapokuwa na korosho daraja la II maana yake sasa unarudi kwenye sheria yetu mkulima huyu atalipwa kwa bei ya daraja la II ile asilimia 80 ya bei ya daraja la I. Kwa hiyo, ndicho ambacho kinafanyika, hiyo Sh.2,600 ni calculation ya asilimia 80 ya bei ya daraja la I. (Makofi)

Mheshimiwa Spoika, lakini malipo haya yanaendelea vizuri na kama vile tulijua swali litakuja tena na wakati wote kwa kuwa timu iliyoko kule Mtwara inaendelea kutoa taarifa mpaka jana tumewaongezea tena shilingi bilioni 100 na sasa inafanya zaidi ya shilingi bilioni 500 kulipa na mahitaji yetu sisi ni shilingi bilioni 700. Kwa hiyo, wakishamaliza tunaongeza na kuhakikisha tunamaliza na kama ambavyo unajua niliingilia kati mchakato mzima na kuwapa tarehe ya mwisho ya kulipa wakulima ambayo ni tarehe 15, tuna uhakika kufikia siku hiyo tutakuwa tumefikia kiasi kikubwa cha malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka niwahakikishie wakulima kwamba malipo yanaendelea na sehemu kubwa ya wakulima tumeendelea kuwalipa na hasa wale walioko chini ya kilo 1,500 lakini sehemu kubwa ya malipo ambayo yanakuja sasa ni wale wa zaidi ya kilo 1,500, uhakiki umeshafanyika na wanatambulika na sasa utaratibu wa kulipa ambao unaendelea ndiyo ambao utawafanya wakulima sasa kila mmoja aweze kupata fedha yake. Nataka niwahakikishie wanunuzi wa korosho na wakulima wa korosho kwamba korosho zote kama ambavyo tumetamka mara zote kwamba tutazinunua kama ambavyo imekubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini taratibu zinazoendelea ni ili tujue kwa uhakika zaidi mkulima anayelipwa kuwa ndiye mwenye mali na ndiyo anayelipwa, huo ndiyo mkakati ambao unaendelea kwa sasa. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wenzangu na hasa mnaotoka kwenye maeneo ya korosho muwe na amani kabisa, Serikali inaendelea na utaratibu wa kulipa na tutawalipa wakulima wote kwenye maeneo yote. Wakulima wenyewe wawe na imani na Serikali yao na mpango ambao unaendelea kwamba kila mkulima aliyepima korosho zake atafikiwa na atapata malipo yake. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister