Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 9 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2019-02-07

Name

Pascal Yohana Haonga

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Suala la kuongeza mishahara kwa watumishi wa umma siyo suala la utashi wa mtu bali ni suala la kisheria kwa mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma, Na.8 ya mwaka 2002 pamoja na Kanuni zake za 2003. Ni lini sasa Serikali itaacha kukiuka sheria hii kwa kutopandisha mishahara kwa watumishi wa umma na ituambie rasmi ni lini itapandisha mishahara kwa watumishi wa umma?

SPIKA: Hiyo sheria inasomekaje?

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, ni Sheria ya Utumishi wa Na.8 ya mwaka 2002 ambayo inaeleza kupandisha mishahara pamoja na stahiki mbalimbali za watumishi wa umma.

SPIKA: Si ungetusomea basi hiyo sheria inavyosema. Siyo kila mtu ana nakala hata Mheshimiwa Waziri Mkuu hana nakala, hawezi kukariri sheria zote. (Makofi)

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, swali kwa ufupi linahusu kupandisha mishahara watumishi wa umma, ndiyo logic sasa ya swali hili. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Haonga, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali hajakiuka sheria unayoitaja, kama inasema hivyo, kwa kutolipa nyongeza ya mishahara. Serikali lazima iwe na mipango na mipango ile iliyonayo Serikali lazima imnufaishe mtumishi au yeyote ambaye anapata stahiki hiyo. Nia ya Serikali kwa watumishi ni njema bado ya kuhakikisha kwamba wanapata mishahara na stahiki zao na wanalipwa madeni yanayozalishwa kutokana na utendaji kazi wao. Hiyo ndiyo nia njema ya Serikali na tunatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye eneo la mishahara hili Watanzania wote na wafanyakazi mnajua kwamba nchi hii tulikuwa na idadi kubwa ya wafanyakazi na wengine hawakuwa wafanyakazi kwa mujibu wa orodha na wote walikuwa wanalipwa mishahara na posho mbalimbali. Kwa hiyo, ili kutambua nani anastahili kupata mshahara kiasi gani na kwa wakati gani Serikali ilianza na mazoezi makubwa mawili. Moja, tulianza kwanza kuwatambua watumishi halali na hewa. Baada ya kuwa tumekamilisha zoezi hili baadaye tulikuja kutambua watumishi wenye vyeti stahiki vya kufanya kazi hiyo kwa mujibu wa Kanuni za Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa mazoezi yote yamekamilika huku pia tukiendelea kulipa na madeni ya watumishi ambao tumewatambua pia Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameunda Tume ya Mishahara Mishahara na Motisha. Baada ya kuwa tumemaliza kutambua watumishi stahiki sasa Tume ile inafanya mapitio ya kada zote za utumishi wa umma na viwango vya mishahara yao ili kutambua stahiki ya mshahara huo na kada hiyo baada ya kugundua kwamba ziko tofauti kubwa za watu wenye weledi wa aina moja, wamesoma chuo kikuu kimoja, lakini wanapata ajira kwenye sekta mbili mmoja anapata milioni 20 mwingine milioni 5, jambo hili kwenye utumishi halina tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nia ya Mheshimiwa Rais kuunda ile Tume ni kufanya tathimini nzuri ya kutambua weledi wa kazi lakini pia itahusisha na uwajibikaji mahali pa kazi na tija inayopatikana mahali pa kazi ili alipwe mshahara unaostahili. Kwa hiyo, jambo hili inawezekana limechukua muda katika kuhakikisha kwamba tunafikia hatua hiyo, inawezekana Mheshimiwa Mbunge ukasema kwamba Serikali haijatimiza Jukumu lake lakini nataka nikuhakikishie kwamba kwa taratibu hizi tunalenga kuhakikisha kila matumishi anapata mshahara kulingana na weledi wa kazi yake au daraja lake ili kuondoa tofauti ambazo zipo za kiwango cha mishahara ambazo zinapatikana kwenye maeneo haya watu wakiwa na weledi wa aina moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutakapokamilisha kazi hii, kwa bahati nzuri ile Tume tayari imeshawasilisha taarifa Serikali na Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma inaendelea kuipitia, wakati wowote tunaweza kupata taarifa za matokeo ya Tume ile. Kwa hiyo, niwahakikishie watumishi wote nchini kwanza muendelee kuwa watulivu, mbili muendelee kuiamini Serikali yetu na tatu Serikali inayo nia njema ya dhati kabisa kuhakikisha kwamba watumishi wote wanapata haki zao stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri sana Mheshimiwa Rais wetu amekutana na viongozi wa vyama vya wafanyakazi, ameeleza vizuri haya na viongozi wamepata nafasi ya kueleza changamoto zilizopo kwenye sekta ya umma na Serikali tumechukua hizo changamoto zote na tunazifanyia kazi. Kwa bahati nzuri mjadala wetu na vyama vya wafanyakazi unaendelea vizuri. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge ambaye pia umewazungumzia wafanyakazi uendelee kuwa na imani na Serikali, utaratibu wetu ni mzuri na unalenga hasa kuleta tija kwa mfanyakazi ili aweze kufanya kazi yake vizuri. Kwa hiyo, wakati wowote kazi itakapokamilika tutatoa taarifa kwa wafanyakazi. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister