Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 9 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2019-02-07

Name

Venance Methusalah Mwamoto

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, naomba niulize swali moja. Nchi yetu imepata bahati ya kuandaa Mashindano ya Vijana ya Afrika (AFCON). Kwa sababu kutakuwa na wageni wengi akiwemo Rais wa Mpira wa Dunia na wageni tofauti ambao wanakuja kuangalia wachezaji wa nchi mbalimbali, kwa hiyo, tutakuwa na ugeni wa kutosha, nilitaka kujua tumehusishaje mashindano haya na utalii wa nchi yetu ili kuutangaza na kuwafanya wageni hao wawe mabalozi watakaporudi kwao? Pia mmehusishaje na Wizara ya Mambo ya Ndani kuhakikisha kwamba…

SPIKA: Swali moja tu.

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Kuhakikisha kwamba usalama unakuwepo? Naomba nijibiwe swali hilo.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwamoto, Kocha wa Timu yetu ya Bunge, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, nataka nitumie nafsi hii kuipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Michezo na Sanaa, kwa kazi nzuri waliyofanya ya ushawishi kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani ili kuleta mashindano haya kwetu nchini Tanzania. Pongezi hizi pia zifikie chombo chetu au Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania kwa jitihada zake za kuratibu vizuri jambo hili kutoka tulipopata dhamana hiyo mpaka hatua tuliyoifikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania kupitia Serikali hii ya Awamu ya Tano imeridhia mashindano hayo kufanyika hapa Tanzania na yanafanyika mwaka huu wa 2019. Katika mashindano hayo vijana wetu wanapata fursa ya kushiriki kutoka ngazi ya awali mpaka fainali kama timu zetu zitafika fainali na ndiyo tunaomba taimu yetu ifike fainali ili sisi kama mwenyeji tuweze kufika kwenye fainali na ikiwezekana pia tuchukue kombe la dunia. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali imejiandaa kupokea wageni wote wanaokuja kushiriki mashindano haya hapa nchini na inaendelea na maandalizi hayo kwa kushawishi sekta zote zitakazonufaika na uwepo wa wageni hao kuja hapa nchini kujiandaa. Vikao mbalimbali vinafanywa na Wizara pamoja na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania na wadau mbalimbali wanashirikishwa na Serikali tunajua kazi kubwa inayoendelea kufanywa na tunatambua kwamba tutapokea wageni wengi akiwemo Rais wa FIFA hapa nchini na tunaendelea kujenga mazingira kuwapokea wageni wengi zaidi kadri watakavyopatikana. Huduma tunazo, tunazo hoteli, maeneo ya kutoa vyakula lakini pia usafiri wa ndani tunao, kwa hiyo, ni maeneo ambayo tumeendelea kuimarisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kupitia mashindano haya tumehamasisha mikoa ya jirani na maeneo ambako viwanja vitatumika na tunaambiwa viwanja vitatu vitatumika wakati wote wa mashindano Dar es Salaam na maeneo mengine, Shirikisho la Mpira litatupa taarifa baada ya kuwa wamekamilisha maandalizi, kwa hiyo, pia na mikoa hiyo nayo itaweza kunufaika. Kwa hiyo, maandalizi ya maeneo yote hayo yanaendelea kufanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupitia swali la Mheshimiwa Mbunge niwahakikishie Watanzania kwamba ujio huu kwetu ni muhimu sana. Kwa hiyo, sote tunatakiwa tushirikiane kuhakikisha kwamba tunapata mafanikio kwa wageni hawa kuingia, kuishi hapa na kurudi makwao wakiwa salama. Kwa hiyo, ni jukumu letu kuhakikisha kwamba tuko salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Shirikisho la Soka Tanzania liendelee kuimarisha maandalizi ya timu yetu ambayo itashiriki kwenye mashindano haya ili hatimaye tuweze kuibuka kidedea. Sisi Watanzania wote tunawajibika sasa kuonesha uzalendo kwa timu yetu itakayofanikiwa kuingia ili kuipa moyo. Kwa hiyo, mchango wa kila mmoja wa namna yoyote ile unahitajika katika suala hili. Kwa hiyo, niwahakikishie Watanzania kwamba mashindano tunayapokea, tuko tayari kuwapokea wageni wake na tutaendelea kushindana kwa sababu na sisi tuna timu ambayo itashindana na naamini tutafanikiwa. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister