Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2020-01-30

Name

Pascal Yohana Haonga

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, uchaguzi wa Serikali za Mitaa, mchakato wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa Mwaka 2019 uligubikwa na dosari nyingi sana, ikiwemo wagombea kutoka vyama vya upinzani kunyimwa fomu, ofisi kufungwa kwa muda wote, hivyo kusababisha baadhi ya wagombea, hasa wa upinzani kushindwa kupata fursa kuweza kugombea.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali haioni kwamba ni vema uchaguzi wa wa Serikali za Mitaa uweze kurudiwa sambamba na Uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi Oktoba mwaka huu?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Haonga, Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, chaguzi hizi zote zinasheria zake na kanuni zake; na hata kanuni za Serikali za Mitaa vyama vyote vya siasa vilishirikishwa katika kutengeneza kanuni zao. Moja kati ya kanuni hizo ni pale ambapo inatoa fursa kwa yeyote ambaye hajaridhika huko anakogombea, kwamba anaweza kukata rufaa, na atakapoona rufaa hiyo kwenye ngazi inayofuata haikutendeka haki aende mahakamani. Kwa hiyo kulichukuwa hili kwa ujumla ujumla si sahihi sana kwasababu kila mmoja alipo alikuwa na mamlaka yake inayoratibu na anayo fursa ya kwenda kwenye mamlaka kukatia rufaa pale ambapo hajaridhika na utekelezaji wa jambo hilo. Vyama vyote vilishiriki kwenye hii kanuni ya kukata rufaa, kwa hiyo ni wajibu wa huyo mgombea kwenye eneo hilo kwenda kukata rufaa.

Mheshimiwa Spika, na kama kulikuwa na dosari kama ambavyo nimeeleza bado zilikuwa zinaweza kuelezwa huko huko kwenye ngazi hiyo, kwa hiyo, huna sababu ya kutengua uchaguzi wote wakati mgombea mwenye malalamiko ana fursa huko huko aliko kwa kukata rufaa na hatimaye hukumu itachukuliwa. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister