Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2020-02-06

Name

Pauline Philipo Gekul

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kunipa nafasi nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu swali. Ni sera na ni azma ya Serikali yetu kuwapatia wananchi maji salama lakini kwa bei nafuu pia kwa sababu maji ni huduma si biashara. Niipongeze Serikali yetu kwa kufikia azma hiyo hiyo mijini kwa zaidi ya asilimia 80 na vijijini kwa asilimia 70.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana EWURA walipandisha bili za maji kote nchini, jambo ambali limesababisha wananchi wengi kushindwa kulipa bili hizo. Serikali pamoja na wewe Mheshimiwa Waziri Mkuu mlituahidi hapa Bungeni kwamba EWURA wacheki upya mchakato wao ili waona kama hizi bili zinaweza zikashuka ili wananchi waweze kulipia. Naomba nifahamu Mheshimiwa Waziri Mkuu ni lini mchakato wa EWURA utakamilika ili hizi bili zishuke kwa sababu wananchi wengi wameshindwa kulipia; mfano wananchi wa Babati Mjini? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gekul Mbunge wa Babati Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nimewahi kupokea malalamiko haya kutoka hapa Bungeni, kutoka kwenye mikutano ninayoifanya kwenye maeneo mbalimbali nchini juu ya upandaji wa bei za maji holela na kukwaza wananchi kumudu kupata huduma hiyo ya maji. Kwanza nataka niwahakikishie Watanzania kwamba Serikali yetu imejipanga kutoa huduma za maji mpka kuingia vijijini kama ambavyo tumeeleza na kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameeleza. Kwamba tunahitaji sasa angalau kila kijiji kiwe na angalau kiwekwe kisima kama ni kifupi tupate maji ili wananchi wawe na uhakika wapi watapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hiyo inaendelea vizuri na Wizara yetu ya maji inasimamia kuhakikisha kwamba huduma za maji zinapatikana kwa ujenzi wa miradi ya visima vifupi, vya kati lakini pia hata miradi mikubwa ambayo wakati wote tumekuwa tukiieleza. Maji haya Serikali hailengi kufanya biashara kwa wananchi wala hatuhitaji faida kutoka kwa wananchi, muhimu wa utoaji huduma ya maji kwa wananchi ni kufikisha maji kwa wananchi wayapate maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeunda Kamati zinazosimamia maji kwenye maeneo husika; na pia tumeunda mamlaka ya jumla ambayo inasimamia utoaji wa huduma ya maji kwenye ngazi ya Wilaya RUWASA; kwenye ngazi ya Kitaifa tuna zile mamlaka ambazo zinachukua unaweza ukawa ni Mikoa miwili au mitatu au Kanda kusimamia utoaji huduma lakini pia na ujenzi wa miradi mipya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati hizi tumezitaka zifanye mapitio ya huduma ndogondogo zinazohitaji kwa ajili ya ukarabati wa kuendesha mradi huo kwenye maeneo yao; kama vile kununua tap na kufanya mabadiliko ya bomba lililotoboka. Hiyo tumeiachia zile Kamati ziratibu na sasa Kamati hizi zinahitaji angalau wananchi wachangia huduma ya maji kwenye eneo lao. Huduma hii hatutarajii kusikia mwananchi analipa gharama kubwa inayomshinda na lile ndilo tuliloagiza kwa Wizara. Tumeweka utaratibu EWURA wafanye mapitio ya maeneo haya kuona kwamba gharama haziwi zaidi ya mapato ya mwananchi kwenye eneo lake ili kuongoa usumbufu au dhana ya kwamba tunatoa huduma ya maji kama vile biashara, hapana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumeweka utaratibu EWURA wafanye mapitio ya maeneo haya kuona kwamba, gharama haziwi zaidi ya mapato ya mwananchi kwenye eneo lake, ili kuondoa usumbufu au dhana ya kwamba, tunatoa huduma ya maji kama vile biashara, hapana. Agizo limeshatolewa na Wizara ya Maji imeshatekeleza. kwa hiyo nitamuagiza Waziri wa Maji atupe taarifa ya hatua waliyoifikia ili sasa tuone kuwa huduma hii inatolewa huko kwa namna ambazo mwananchi anaweza kupata maji akaendelea kuhudumiwa. Vilevile kama kijiji, kata, waendelee kufanya ukarabati mdogomdogo ili kufanya mradi huo kuendelea kutoa huduma kwa wananchi wake. Asante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister