Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 34 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2019-05-23

Name

Mary Pius Chatanda

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Korogwe Mjini

Primary Question

MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kumuuliza Waziri Mkuu, Serikali imekuwa ikipeleka fedha nyingi katika Halmashauri zetu kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji na kukamilisha, lakini miradi hiyo imekuwa haitumiki kama ilivyokusudiwa kutokana na usanifu mbovu wa miradi na kutokamilika kwa miradi hiyo.

Je, Serikali ipo tayari kuchunguza na kuchukua hatua kwa wale wote watakaobainika kwamba, walisababishia hasara Serikali na kuwasabishia Wananchi kutopata huduma ambayo walikuwa wamekusudiwa kupewa na Serikali?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chatanda, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba, miradi yetu mingi ya maji ambayo inatekelezwa kwenye maeneo mbalimbali iko mingine haitekelezwi kwa viwango na kwa hiyo, haina thamani ya fedha kama ambavyo tumekusudia iweze kutekelezwa. Lakini pia kama ambavyo Waziri mwenye dhamana alipokuwa ameleta bajeti yake mbele yetu Wabunge alieleza hatua mbalimbali zilizochukuliwa dhidi ya miradi yote ambayo imetangazwa na haina thamani kama ilivyokusudiwa kwa fedha iliyotolewa. Na moja kati ya hatua ambazo amezifanya, alieleza hapa kwenye hotuba yake na ndio hasa kazi ambayo inafanywa, ameshaunda timu inayopita kukagua miradi yote nchini kwa kujiridhisha miradi hiyo kupitia BOQ zake kuona matengenezo yake na kama inakidhi thamani ya fedha kwa fedha zilizotolewa kwa mradi huo.

Mheshimiwa Spika, na pale ambapo sasa hakuna thamani ya fedha hizo hatua ambazo Mheshimiwa Mbunge anataka kujua zinachukuliwa. Na ninataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tumewasikia ushauri wenu kwenye sekta ya maji ikiwemo na kuchukua hatua kali kwa watendaji wetu ambao wanasimamia miradi ya maji na maji hayapatikani, lakini mradi wenywe haujatengenezwa kwa viwango kwamba, hatua kali zitachukuliwa. Na Wizara sasa imeanza kupitia, Wizara yenyewe pale Makao Makuu, na inashuka ngazi ya Mikoa mpaka Wilayani ili kujiridhisha kwamba, tunakuwa na watumishi wenye weledi wa kutekeleza miradi hiii na kusimamia thamani ya fedha kwa manufaa ya Watanzania, ili huduma ziweze kutolewa kwa Wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea na kazi hiyo na Wizara inaendelea kukagua miradi pamoja na ile tume, itakapokamilisha kazi itakuwa na majibu. Wale wote watakaothibitika hatua kali dhidi yao itachukuliwa. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister